Je, Utanufaika kwa Kuwa na Eneo la Kibinafsi?
1. Eneo la kibinafsi ni nini?
1 Eneo la kibinafsi ni nini? Katika makutaniko yenye maeneo mengi ya kuhubiri, eneo la kibinafsi ni eneo lako mwenyewe la kuhubiri ambalo huenda likawa karibu na mahali unapoishi. Kitabu Tengenezo, ukurasa wa 103, kinaeleza hivi: “Kuwa na eneo lako karibu kutakuwezesha kutumia vizuri wakati wako katika utumishi wa shambani. Unaweza kumwalika mhubiri mwingine aandamane nawe katika eneo lako.”
2. Tunaweza kutumiaje eneo la kibinafsi kuongeza utendaji wetu?
2 Kuongeza Utendaji Wetu: Ukipata eneo la kibinafsi karibu na mahali unapofanya kazi, unaweza kushiriki katika huduma wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana au kabla ya kurudi nyumbani, huenda ukiwa na mhubiri mwingine anayefanya kazi karibu. Ukipata eneo kama hilo karibu na mahali unapoishi, wewe na familia yako mnaweza kuhubiri kwa urahisi eneo hilo jioni. Bila shaka, ikiwa hutahudhuria mkutano wa utumishi wa shambani, inafaa usali ili upate mwongozo wa Yehova kabla ya kuanza kuhubiri. (Flp. 4:6) Kwa kuongezea, unapaswa kuwa na usawaziko kuhusu muda unaotumia kuhubiri katika eneo la kibinafsi na muda unaotumia kuunga mkono mpango wa kutaniko wa kuwa na mahubiri ya vikundi. Hasa mwisho-juma ambapo wengi hukutana kwa ajili ya utumishi wa shambani, kwa kawaida ni bora kuunga mkono kikundi chako cha utumishi wa shambani.
3. Kuna faida gani za kuwa na eneo la kibinafsi?
3 Manufaa: Ikiwa una eneo la kibinafsi, utakuwa na mahali pa kuhubiri wakati wowote ratiba yako inapokuruhusu kufanya hivyo. Unaweza kutumia wakati zaidi kuhubiri na kutumia wakati mchache kusafiri. Jambo hilo huwasaidia wengine kufanya upainia msaidizi au wa kawaida. Kwa kuwa unapata wenye nyumba wanaopendezwa katika eneo moja, ni rahisi zaidi kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia. Wengi wamegundua kwamba kuhubiri katika eneo la kibinafsi huwasaidia kuwajua wenye nyumba na kuwafanya wenye nyumba wawaamini, hasa ikiwa eneo linaweza kuhubiriwa zaidi ya mara moja kabla ya kulirudisha ili wengine waweze kuliomba. Je, kuhubiri katika eneo la kibinafsi kutakusaidia wewe na familia yako kutimiza huduma yenu kikamili zaidi?—2 Tim. 4:5.