Kuanzisha Mazungumuzo kwa Njia Inayoamusha Kupendezwa
1. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Wakristo wa kwanza walivyopatanisha mazungumuzo na hali ya wasikilizaji?
1 Wakristo wa kwanza walihubiria watu wa desturi mbalimbali na wa dini tofautitofauti habari njema. (Kol. 1:23) Walikuwa na ujumbe uleule, ni kusema, Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, walipatanisha mazungumuzo na hali ya wasikilizaji. Kwa mufano, mutume Petro alipozungumuza na Wayahudi ambao waliheshimu sana Maandiko, alitaja maneno ya nabii Yoeli ili kuanza kuzungumuza nao. (Mdo. 2:14-17) Kwa upande mwengine, ona njia ambayo mutume Paulo alitumia ili kuzungumuza na Wagiriki, kama inavyoonyeshwa katika andiko la Matendo 17:22-31. Leo, katika maeneo fulani watu wanaheshimu Biblia, kwa hiyo bila kusita tunaweza kuitumia tunapohubiri nyumba kwa nyumba. Lakini, labda itatuomba kutumia busara kabisa tunapozungumuza na wale wasiopendezwa na Biblia ao na mambo ya dini, ao wale walio katika dini isiyo ya Kikristo.
2. Namna gani tunaweza kutumia vichapo vya kutolea watu katika mwezi ili kuwasaidia wale wanaopendezwa na Biblia na wale wasiopendezwa nayo?
2 Tumia Vizuri Zaidi Vitabu vya Kuwatolea Watu Katika Mwezi: Katika mwaka huu wa utumishi, kisha kila miezi miwili, vitabu vya kuwatolea watu katika mwezi vitabadilishwa; tutatumia hasa magazeti, trakti, na broshua. Hata ikiwa labda watu wengi katika eneo letu hawapendezwe na Biblia, tunaweza kuzungumuzia habari fulani kutoka katika magazeti, trakti, na broshua, ambayo inaweza kuwapendeza. Labda tunapomuhubiria mutu kwa mara ya kwanza haitakuwa lazima kusoma Biblia ao kutaja Biblia. Lakini ikiwa mutu anapendezwa, tunaweza kumurudilia tukiwa na kusudi la kumusaidia awe na imani katika Muumba na katika Neno lake lililoongozwa na roho. Kwa upande mwengine, ikiwa tunahubiri katika eneo ambamo watu wanapendezwa na Biblia, tunaweza kutumia vichapo vyetu na kuanzisha mazungumuzo katika vichapo hivyo. Kwa hiyo, wakati wowote tunaweza kuwatolea kitabu Biblia Inafundisha ao broshua Umusikilize Mungu ao Umusikilize Mungu ili Uishi Milele, hata ikiwa vichapo hivyo si vya kutolea watu katika mwezi. Jambo la lazima ni kuanzisha mazungumuzo na kufundisha kwa njia inayoamusha kupendezwa.
3. Ni katika njia gani mioyo ya watu wa eneo letu inalingana na udongo?
3 Tayarisha Udongo: Moyo wa mutu unalingana sana na udongo. (Lu. 8:15) Inaomba kutayarisha kabisa aina fulani za udongo ili mbegu za kweli ya Biblia ziweze kuwa na mizizi na kukomaa vizuri. Watangazaji wa habari njema wa wakati wa mitume walipanda mbegu za kweli katika kila aina ya udongo, na walipata matokeo mazuri. Hilo liliwaletea furaha kabisa. (Mdo. 13:48, 52) Sisi pia tunaweza kupata matokeo mazuri kwa kufikiria sana namna tunavyoanzisha mazungumuzo.