Mwanzo
25 Kisha, kwa mara nyingine Abrahamu akachukua mke, naye aliitwa jina lake Ketura.+ 2 Baada ya muda akamzalia Zimrani na Yokshani na Medani na Midiani+ na Ishbaki na Shua.+
3 Yokshani akamzaa Sheba+ na Dedani.+
Na wana wa Dedani wakawa Ashurimu na Letushimu na Leumimu.
4 Na wana wa Midiani walikuwa Efa+ na Eferi na Hanoki na Abida na Eldaa.+
Wote hao walikuwa wana wa Ketura.
5 Baadaye Abrahamu alimpa Isaka kila kitu alichokuwa nacho,+ 6 lakini wana wa masuria ambao Abrahamu alikuwa nao Abrahamu aliwapa zawadi.+ Kisha alipokuwa bado hai, akawaagiza waende kutoka kwa Isaka mwana wake,+ upande wa mashariki, kwenye nchi ya Mashariki.+ 7 Na hizi ndizo siku za miaka ya maisha ya Abrahamu alizoishi, miaka 175. 8 Kisha Abrahamu akakata pumzi, akafa katika umri mwema wa uzee, akiwa mzee na mwenye kutosheka, naye akakusanywa kwa watu wake.+ 9 Basi Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango la Makpela katika shamba la Efroni mwana wa Zohari Mhiti lililoko mbele ya Mamre,+ 10 lile shamba ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kutoka kwa wana wa Hethi. Hapo Abrahamu akazikwa, na pia Sara mke wake.+ 11 Ikatokea kwamba baada ya kifo cha Abrahamu, Mungu aliendelea kumbariki Isaka mwana wake,+ naye Isaka alikuwa akikaa karibu na Beer-lahai-roi.+
12 Na hii ndiyo historia ya Ishmaeli+ mwana wa Abrahamu ambaye Hagari Mmisri mjakazi wa Sara alimzalia Abrahamu.+
13 Basi haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kufuatana na majina yao, kulingana na asili za familia zao: Mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli alikuwa Nebayothi+ na Kedari+ na Adbeeli na Mibsamu+ 14 na Mishma na Duma na Masa, 15 Hadadi+ na Tema,+ Yeturi, Nafishi na Kedema.+ 16 Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ndiyo majina yao kufuatana na nyua zao na kufuatana na kambi zao zilizozungushiwa kuta:+ wakuu kumi na wawili kulingana na ukoo wao.+ 17 Na hii ndiyo miaka ya maisha ya Ishmaeli, miaka 137. Kisha akakata pumzi, akafa. Akakusanywa kwa watu wake.+ 18 Nao wakaanza kukaa katika mahema tokea Havila+ karibu na Shuri,+ ambayo iko mbele ya Misri, mpaka Ashuru. Mbele ya ndugu zake wote alikaa.+
19 Na hii ndiyo historia ya Isaka mwana wa Abrahamu.+
Abrahamu akamzaa Isaka. 20 Na Isaka alikuwa na umri wa miaka 40 alipomchukua Rebeka binti ya Bethueli,+ Msiria,+ wa Padan-aramu, dada ya Labani Msiria, awe mke wake. 21 Naye Isaka akaendelea kumsihi Yehova hasa kwa ajili ya mke wake,+ kwa sababu alikuwa tasa;+ kwa hiyo Yehova akakubali kusihiwa kwa ajili yake,+ na Rebeka mke wake akapata mimba. 22 Na wale wana ndani yake wakaanza kupambana,+ hivi kwamba akasema: “Ikiwa hivi ndivyo ilivyo, hasa kwa nini niko hai?” Basi akaenda kumuuliza Yehova.+ 23 Naye Yehova akamwambia: “Mataifa mawili yamo tumboni mwako,+ na vikundi viwili vya mataifa vitatenganishwa kutoka tumboni mwako;+ na kikundi kimoja cha taifa kitakuwa chenye nguvu kuliko kile kingine,+ na mkubwa atamtumikia mdogo.”+
24 Mwishowe siku zake za kuzaa zikatimia, na, tazama! mapacha walikuwa tumboni mwake.+ 25 Kisha yule wa kwanza akatoka mwekundu kila mahali kama vazi rasmi la manyoya;+ kwa hiyo wakamwita jina lake Esau.+ 26 Na baadaye ndugu yake akatoka na mkono wake ulikuwa unashikilia kisigino cha Esau;+ kwa hiyo akaitwa jina lake Yakobo.+ Na Isaka alikuwa na umri wa miaka 60 wakati Rebeka alipowazaa.
27 Na wale wavulana wakawa wakubwa, naye Esau akawa mwanamume anayejua jinsi ya kuwinda,+ mwanamume wa mbugani, bali Yakobo akawa mwanamume asiye na lawama,+ akikaa katika mahema.+ 28 Na Isaka alimpenda Esau, kwa sababu ilimaanisha nyama ya mawindo kinywani mwake, lakini Rebeka alimpenda Yakobo.+ 29 Wakati mmoja Yakobo alikuwa anatokosa mchuzi, Esau alipofika kutoka mbugani naye alikuwa amechoka. 30 Kwa hiyo Esau akamwambia Yakobo: “Haraka, tafadhali, nipe nimeze chekundu—chekundu hicho, kwa maana nimechoka!” Hiyo ndiyo sababu jina lake lilikuwa Edomu.+ 31 Yakobo akajibu akasema: “Niuzie, kwanza kabisa, haki yako ya mzaliwa wa kwanza!”+ 32 Naye Esau akaendelea kusema: “Tazama mimi ninakaribia kufa, nayo haki ya kuzaliwa ina faida gani kwangu?” 33 Naye Yakobo akaongeza hivi: “Niapie kwanza kabisa!”+ Naye akamwapia, akamuuzia Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza.+ 34 Naye Yakobo akampa Esau mkate na mchuzi wa dengu, naye akala na kunywa.+ Kisha akaondoka akaenda zake. Kwa hiyo Esau aliidharau haki ya kuzaliwa.+