Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Yona 1:1-4:11
  • Yona

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yona
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Yona

YONA

1 Neno hili la Yehova lilimjia Yona*+ mwana wa Amitai: 2 “Inuka, nenda Ninawi+ lile jiji kubwa, ukatangaze hukumu dhidi ya jiji hilo kwa sababu nimeona uovu wao.”

3 Lakini Yona akainuka na kwenda Tarshishi ili amkimbie Yehova; akashuka kwenda Yopa, akakuta meli inayokwenda Tarshishi. Basi akalipa nauli na kupanda meli ili asafiri nao kwenda Tarshishi, amkimbie Yehova.

4 Ndipo Yehova akavumisha upepo mkali baharini, dhoruba* kali sana ikatokea baharini hivi kwamba meli ikawa karibu kuvunjika-vunjika. 5 Mabaharia wakaogopa sana hivi kwamba kila mmoja wao akaanza kumlilia mungu wake amsaidie. Nao wakaanza kutupa baharini vitu vilivyokuwa melini ili kupunguza uzito wa meli.+ Lakini Yona alikuwa ameshuka chini ndani ya meli,* ambamo alikuwa amelala na kushikwa na usingizi mzito. 6 Nahodha wa meli akamkaribia na kumuuliza: “Kwa nini unalala? Amka, mwombe mungu wako! Huenda Mungu wa kweli atatuhurumia, nasi hatutaangamia.”+

7 Ndipo mabaharia wakaambiana: “Njooni, tupige kura+ ili tujue chanzo cha taabu hii.” Basi wakapiga kura, na kura zikamwangukia Yona.+ 8 Wakamuuliza: “Tafadhali tuambie, ni nani anayetusababishia taabu hii? Unafanya kazi gani, na unatoka wapi? Unatoka nchi gani, na wewe ni mtu wa kabila gani?”

9 Akawajibu: “Mimi ni Mwebrania, nami namwogopa* Yehova Mungu wa mbinguni, Aliyeumba bahari na nchi kavu.”

10 Waliposikia hayo, wanaume hao wakazidi kuogopa, wakamuuliza: “Umefanya nini?” (Watu hao wakagundua kwamba alikuwa akimkimbia Yehova, kwa sababu Yona aliwaambia.) 11 Basi wakamuuliza: “Tukufanye nini ili bahari itulie kwa ajili yetu?” Kwa sababu bahari ilizidi kuchafuka. 12 Akawajibu: “Nibebeni mnitupe baharini, na bahari itatulia kwa ajili yenu; kwa maana najua kwamba dhoruba hii kali imewapata kwa sababu yangu.” 13 Hata hivyo, wanaume hao wakapiga makasia kwa nguvu* ili kuirudisha meli kwenye nchi kavu, lakini wakashindwa kwa sababu dhoruba ilizidi kuwa kali.

14 Kisha wakamlilia Yehova wakisema: “Jamani, sasa, Ee Yehova, tafadhali, tunakusihi usituangamize kwa sababu ya mtu huyu!* Usituadhibu kwa sababu ya damu isiyo na hatia, kwa kuwa umefanya upendavyo, Ee Yehova!” 15 Basi wakambeba Yona na kumtupa baharini; na bahari ikatulia. 16 Kisha wanaume hao wakamwogopa sana Yehova,+ nao wakamtolea Yehova dhabihu na kumwekea nadhiri.

17 Kisha Yehova akamtuma samaki mkubwa ammeze Yona, basi Yona akakaa ndani ya tumbo la samaki huyo kwa siku tatu, mchana na usiku.+

2 Ndipo Yona akiwa ndani ya tumbo la samaki akasali kwa Yehova Mungu wake,+ 2 na kusema:

“Katika taabu yangu nilimlilia Yehova, naye akanijibu.+

Nikiwa ndani ya* Kaburi* nilililia msaada.+

Uliisikia sauti yangu.

 3 Uliponitupa katika vilindi, katikati ya* bahari,

Ndipo mikondo ya maji ikanifunika.+

Mawimbi yako yote makubwa na yale yanayoishia ufuoni yakanifunika.+

 4 Nami nikasema, ‘Nimefukuzwa kutoka mbele za macho yako!

Nitalikaziaje macho tena hekalu lako takatifu?’

 5 Maji yalinifunika na kuhatarisha uhai wangu;*+

Kilindi cha maji kilinizunguka.

Kichwa changu kilisokotwa na magugu maji.

 6 Nilizama sehemu za chini za milima.

Milango ya dunia ilikuwa ikija kunifungia milele.

Lakini uliutoa uhai wangu shimoni, Ee Yehova Mungu wangu.+

 7 Uhai wangu ulipokuwa ukitoka polepole, Yehova Ndiye niliyemkumbuka.+

Ndipo sala yangu ikakufikia, ndani ya hekalu lako takatifu.+

 8 Wale wanaoabudu sanamu ambazo ni ubatili huacha chanzo chao cha upendo mshikamanifu.*

 9 Lakini mimi, kwa sauti ya shukrani nitakutolea dhabihu.

Nadhiri nilizoweka, nitazitimiza.+

Wokovu unatoka kwa Yehova.”+

10 Baadaye Yehova akamwamuru huyo samaki, naye akamtapika Yona kwenye nchi kavu.

3 Ndipo neno la Yehova likamjia Yona mara ya pili likisema:+ 2 “Inuka, nenda Ninawi+ lile jiji kubwa, ukalitangazie ujumbe ninaokuambia.”

3 Basi Yona akatii neno la Yehova,+ akainuka na kwenda Ninawi.+ Sasa Ninawi lilikuwa jiji kubwa sana*—mtu anayetembea kwa miguu angezunguka jiji hilo kwa siku tatu. 4 Ndipo Yona akaingia jijini, akatembea safari ya siku moja akitangaza hivi: “Bado siku 40 tu, jiji la Ninawi litaangamizwa.”

5 Watu wa Ninawi wakamwamini Mungu,+ nao wakatangaza watu wafunge na kuvaa magunia, kuanzia aliye mkubwa zaidi hadi aliye mdogo zaidi. 6 Ujumbe huo ulipomfikia mfalme wa Ninawi, aliinuka kutoka kwenye kiti chake cha ufalme, akavua vazi lake la kifalme, akavaa nguo za magunia, na kuketi katika majivu. 7 Pia, akaamuru tangazo hili litolewe katika jiji lote la Ninawi:

“Kwa agizo la mfalme na wakuu wake: Hakuna mwanadamu yeyote wala mnyama yeyote wa kufugwa anayepaswa kula kitu chochote. Hawapaswi kula chakula wala hawapaswi kunywa maji. 8 Wote wavae magunia, mwanadamu na mnyama; na wamwite Mungu kwa bidii na kuacha njia zao ovu na matendo yao ya ukatili. 9 Ni nani anayejua ikiwa Mungu wa kweli hatafikiria upya* jambo analokusudia kufanya na kuacha hasira yake inayowaka, ili tusiangamie?”

10 Mungu wa kweli alipoona waliyofanya, jinsi walivyoacha njia zao ovu,+ akafikiria upya kuhusu* msiba aliosema kwamba angewaletea, naye hakuuleta.+

4 Lakini jambo hilo lilimchukiza sana Yona, akakasirika sana. 2 Basi akasali hivi kwa Yehova: “Ee Yehova, je, sikujua utafanya jambo hili nilipokuwa katika nchi yangu? Ndiyo sababu tangu awali nilijaribu kukimbilia Tarshishi;+ kwa maana nilijua kwamba wewe ni Mungu mwenye huruma* na rehema, hukasiriki upesi, una upendo mwingi mshikamanifu,+ na unahuzunishwa na msiba. 3 Sasa, Ee Yehova, nakusihi uniue, kwa maana afadhali nife badala ya kuishi.”+

4 Yehova akamuuliza: “Je, una sababu nzuri ya kuwaka hasira?”

5 Ndipo Yona akatoka jijini, akaketi chini upande wa mashariki wa jiji. Akajenga kibanda hapo na kuketi kivulini ili aone jambo litakalolipata jiji hilo.+ 6 Kisha Yehova Mungu akaotesha mmung’unye* ili Yona apate kivuli kwa ajili ya kichwa chake na ili kupunguza taabu yake. Basi Yona akaufurahia sana mmung’unye huo.

7 Lakini siku iliyofuata, wakati wa mapambazuko, Mungu wa kweli akamwamuru kiwavi aushambulie mmung’unye huo, nao ukanyauka. 8 Joto la jua lilipoanza kuongezeka, Mungu akaleta pia upepo wa mashariki wenye joto kali, na jua likamchoma Yona kichwani, karibu azimie. Akaendelea kuomba afe,* na kuendelea kusema: “Afadhali nife badala ya kuishi.”+

9 Mungu akamuuliza Yona: “Je, una sababu nzuri ya kuwaka hasira kwa sababu ya mmung’unye?”+

Ndipo Yona akasema: “Nina sababu nzuri ya kukasirika, nimekasirika sana hivi kwamba natamani kufa.” 10 Lakini Yehova akamwambia: “Uliuhurumia mmung’unye ambao hukuufanyia kazi yoyote wala kuukuza; uliota na kukua usiku mmoja na kunyauka usiku uliofuata. 11 Je, mimi pia sipaswi kulihurumia jiji kubwa la Ninawi,+ ambalo lina watu zaidi ya 120,000 ambao hata hawajui kutofautisha jema na baya,* na kuwahurumia pia wanyama wao wengi?”+

Maana yake “Njiwa.”

Au “tufani.”

Au “chombo chenye sitaha.”

Au “namwabudu.”

Au “wakajitahidi kutafuta njia.”

Au “kwa sababu ya nafsi ya mtu huyu.”

Tnn., “katika tumbo la.”

Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.

Tnn., “katika moyo wa.”

Au “Maji yaliizunguka nafsi yangu.”

Au labda, “cha ushikamanifu.”

Tnn., “jiji kubwa mbele za Mungu.”

Au “hataghairi kuhusu.”

Au “akaghairi kuhusu.”

Au “neema.”

Au labda, “mbarika; mnyoyo; mbono.”

Au “kuomba nafsi yake ife.”

Au “tofauti kati ya mkono wao wa kulia na wa kushoto.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki