Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 1/8 kur. 8-13
  • Mashahidi wa Yehova Katika Ulaya Mashariki

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mashahidi wa Yehova Katika Ulaya Mashariki
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mashahidi wa Yehova Katika Urusi
  • Maendeleo Katika Polandi
  • Uhuru wa Ibada Katika Romania
  • Habari Njema Kutoka Hungari
  • Kusonga Mbele Katika Chekoslovakia
  • Matazamio ya Wakati Ujao
  • Sehemu ya 5—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Ukuzi Wenye Kutazamisha
    Amkeni!—1992
  • ‘Na Ukuta Ukaanguka kwa Kishindo’
    Amkeni!—1992
  • Walishangaa kwa Yale Waliyoona
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 1/8 kur. 8-13

Mashahidi wa Yehova Katika Ulaya Mashariki

WAKATI Ukuta wa Berlin ulipoanguka katika Novemba 1989, gazeti Asiaweek liliripoti kwamba “Wajerumani wa kutoka Mashariki wapatao milioni mbili walimiminika upande wa magharibi katika muda wa siku mbili baada ya Berlin Mashariki kufungua mpaka wa nchi hiyo iliyogawanyika.” Kusudi lao lilikuwa nini?

Kwa walio matajiri zaidi, ulikuwa wakati wa ununuzi mkubwa. Kwa wengine, ulikuwa wakati wa kutazama vilivyo madukani na kuonja uhuru wao mpya uliopatikana. Wengi waliwapata Mashahidi wa Yehova kwenye barabara za Berlin na miji mingine na kukubali vichapo kutoka kwao. Kutoka wakati huo, wengine wameiandikia barua ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Selters, karibu na Frankfurt am Main, wakionyesha miitikio yao yenye kutokeza.

Barua moja ilisema: “Wakati nilipozuru Berlin Magharibi kwa mara ya kwanza maishani mwangu, nilipokea nakala ya Mnara wa Mlinzi ikiwa zawadi kutoka kwa Mashahidi wa Yehova barabarani. Tangu wakati huo, nimeanza kuichunguza Biblia tena, na ingawa nina matatizo mengi kweli kweli, kwa mara nyingine tena kuna mtu ambaye ananipa tumaini na shangwe ya kuishi. Ningefurahi sana kama ningeweza kusoma kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako. Ningependa pia kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova.”

Mgeni mwingine aliandika hivi: “Nilipokuwa nikipita kwenye njia iliyo chini ya ardhi kuelekea stesheni kuu ya Nuremberg, mwanamke mmoja alinipa nakala za Amkeni! na Mnara wa Mlinzi. Nilisisimuka nilipoyasoma. Kwa siku kadhaa nimekuwa nikitumia Biblia kila siku kwa mara nyingine tena.”

Mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova ilifanywa katika miji mikubwa kotekote katika Ulaya Mashariki wakati wa kiangazi cha 1990. Stediamu ya Olympia ambayo kwa wakati huo ilikuwa sehemu ya Berlin Magharibi ilikuwa mahali pamoja palipofanyiwa mkusanyiko mmoja uliohudhuriwa na Mashahidi kutoka mataifa mengi, kutia ndani Ujerumani ya mashariki. Inakadiriwa kwamba kati ya watu 44,532 waliohudhuria, wapatao 30,000 walitoka Ujerumani ya mashariki. Gazeti Berliner Morgenpost liliripoti kwamba Mashahidi wapya 1,017 walibatizwa katika kidimbwi cha kuogelea cha Olympic, wakizamishwa kabisa ndani ya maji, njia ambayo kupitia kwayo “washiriki hushikamana sana na kielelezo cha Wakristo wa kwanza.”

Mambo yamebadilikaje katika Ujerumani ya mashariki? Katika Machi 1990 gazeti la Ujerumani Mashariki lilitangaza kuhalalishwa kwa Mashahidi wa Yehova. Chini ya kichwa “Mashahidi wa Yehova Halali Tena,” gazeti hilo la Ujerumani Mashariki Mitteldeutsche Zeitung lilisema: “Machi 14 ilimaanisha mwisho wa marufuku yaliyodumu kwa muda wa miongo minne. Katika siku hiyo wawakilishi wa Kijerumani wa Mashahidi wa Yehova waliweza kuondoka kwenye makao ya Katibu Mkuu wa Mambo ya Kanisa Katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani wakiwa na hati rasmi mfukoni mwao kuruhusu tena jumuiya yao ya imani kuwa na uhuru wa ibada ya kidini katika enzi ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani.”

Barua moja iliyopokewa masika yaliyopita kutoka kwa Shahidi mmoja katika Leipzig yatoa hadithi hii: “Juma moja lililopita tulikuwa tungali tukiingiza chakula cha kiroho kwa siri kwa kiasi kidogo-kidogo. Sasa [Machi 14, 1990] tumetambuliwa kisheria! Karibuni tutakuwa tukipakua tani nne za fasihi kutoka kwenye lori!” Kwa hakika, lori la kwanza kuingia Ujerumani Mashariki lilikuwa limepakiwa kwa tani 25 za fasihi za Biblia, na kwa muda wa miezi miwili iliyofuata, tani 250 zaidi zilipelekwa. Hiyo ndiyo iliyokuwa njaa ya kiroho ya Mashahidi hao ambao walikuwa wamenyimwa uhuru kwa muda wa miaka 40!

Tunapokumbuka kwamba Unazi (1933-45) na Ukomunisti pia ulijaribu kukomesha kabisa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani, utendaji wao wa wakati uliopita na wa sasa ni ushuhuda mzuri wa uadilifu wao na baraka ya Mungu juu yao.

Mashahidi wa Yehova Katika Urusi

Katika Desemba 1989, Mikhail Gorbachev alikutana na Papa John Paul II katika Vatikani. Gazeti la Urusi Pravda liliripoti Gorbachev akisema hivi kuhusu mazungumzo hayo: “Tulikuwa na mazungumzo yenye kina na yenye maana. . . . Tulizungumza juu ya dini na mambo ya maana yanayoendeshwa katika Ulaya, ulimwengu, na katika Urusi.” Gazeti rasmi la Vatikani, L’Osservatore Romano, liliripoti kwamba Bw. Gorbachev alisema hivi katika mazungumzo yake na papa: “Watu wa imani mbalimbali, kutia ndani Wakristo, Waislamu, Wayahudi, Wabuddha na wengine, wanaishi katika Urusi. Wote wana haki ya kuridhisha mahitaji yao ya kiroho. Karibuni, Sheria juu ya Uhuru wa Dhamiri itatumika katika nchi yetu.”

Kwa kweli kufuatana na neno hilo, katika Septemba 1990 wafanya sheria wa Urusi walikubali sheria inayoruhusu uhuru wa dhamiri. Sehemu ya tatu ya sheria hiyo kama ilivyonakiliwa inasema: “Kupatana na haki ya uhuru wa dhamiri, kila raia anajiamulia mwenyewe uhusiano wake na dini, ana haki ya kuzoea dini yoyote akiwa peke yake au na wengine au kutozoea yoyote ile, kuonyesha na kueneza masadikisho yake kwa kadiri ya uhusiano wake na dini.”

Katika Mikusanyiko ya 1990 yenye kichwa “Lugha Iliyo Safi,” wajumbe zaidi ya 17,000 kutoka Urusi walihudhuria sehemu za Kirusi katika Warsaw kwa kuwakilisha Mashahidi wote waliotawanyika kotekote katika Urusi. Wanatazamia mbele kwenye siku itakapowezekana kuwa na mikusanyiko katika Urusi.

Maendeleo Katika Polandi

Mashahidi wa Yehova waliidhinishwa kisheria katika Polandi katika Mei 1989. Tangu wakati huo ofisi ya tawi imeanzishwa, na makao makubwa zaidi yanajengwa karibu na Warsaw. Hapo mbeleni, mamia ya Mashahidi vijana walitiwa gerezani kwa sababu ya suala la kutokuwamo la Kikristo. Sasa wanaruhusiwa kutotumika katika utumishi wa kijeshi na kutopata adhabu ikiwa wanatoa cheti kinachofaa.

Makusanyiko yaliyofanyiwa Polandi katika 1989 na 1990 yamekuwa kitia moyo kikubwa kwa Mashahidi huko. Ripoti moja inasema kwamba hesabu ya Mashahidi watendaji katika Polandi imekuwa ikipanda kila mwezi mwaka uliopita, kukiwa na kilele kipya cha zaidi ya 97,000. Hakuna shaka kwamba Polandi karibuni itakuwa taifa la 12 lenye Mashahidi zaidi ya 100,000.a Hudhurio la Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika Aprili lilikuwa watu 188,861.

Uhuru wa Ibada Katika Romania

Mashahidi katika Romania walishangilia kusikia kwamba shirika lao limetambuliwa kisheria katika Aprili 1990. (Ona sanduku, ukurasa wa 13) Upesi makusanyiko ya mzunguko yalipangwa kotekote katika taifa, na katika mfululizo mmoja zaidi ya watu 44,000 walikuwapo, ijapokuwa kulikuwako Mashahidi karibu 19,000 tu wakati huo katika nchi hiyo. Kwa kweli watu wengi wa Kiromania wanaitikia ujumbe wa Ufalme.

Mikusanyiko ya wilaya yenye kichwa cha ulimwenguni pote cha 1990 “Lugha Iliyo Safi” ilifanywa katika miji ya Brasov na Cluj-Napoca. Programu ilitolewa katika lugha ya Kiromania na Kihungari. Zaidi ya 36,000 walikuwepo, na 1,445 wakabatizwa.

Kuanzia na toleo la Januari 1, 1991, gazeti Mnara wa Mlinzi katika Kiromania lilianza kuchapishwa sawia na la Kiingereza katika rangi kamili.

Katika Bulgaria iliyo karibu, mahali ambapo dini ya Mashariki ya Orthodoksi ndiyo kubwa zaidi, bado Mashahidi hawajapata utambulisho wa kisheria lakini wanapangisha vyumba ambamo wanafanya mikutano yao ya kundi. Zaidi ya watu mia mbili walisafiri kuelekea Salonika, Ugiriki, kwa Mkusanyiko wa “Lugha Iliyo Safi” uliofanywa katika Kibulgaria na Kigiriki.

Habari Njema Kutoka Hungari

Juni 27, 1989, ilikuwa siku ya kihistoria kwa Mashahidi katika Hungari. Gazeti Magyar Nemzet lilitangaza: “Ofisi ya Kitaifa ya Mambo ya Kanisa ilitangaza shirika la kidini la Mashahidi wa Yehova katika Hungari, kuwa limetambuliwa kisheria kama shirika la kidini, kulingana na sheria inayofuatia uhuru wa kidini.” Habari hiyo ilitangazwa kwenye radio na TV. Wahungaria walijifunza kwamba kazi ya Jehova Tanúi (Mashahidi wa Yehova) hatimaye ilikuwa imetambuliwa kisheria.

Ili kuenea katika sehemu zile kubwa-kubwa za nchi, Makusanyiko ya “Lugha Iliyo Safi” yalifanywa katika Pecs, Miskolc, Debrecen, na Budapest. Watu wapatao 2,000 wanaozungumza Kihungaria walikuja kutoka Chekoslovakia na Urusi. Ili kudhihirisha umoja wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova, kikundi cha wajumbe 700 wenye kuzuru walihudhuria kutoka Finlandi. Jumla ya hudhurio katika Hungari lilikuwa 21,568, kutia ndani zaidi ya wajumbe 2,000 wa Romania.

Tangu Januari 1990, Mashahidi katika Hungari wamekuwa wakipokea magazeti yao yenye rangi kamili kwa ukawaida, yakiwa yametafsiriwa sawia na kurasa za matayarisho ya kwanza kabisa ya gazeti la Kiingereza.

Kusonga Mbele Katika Chekoslovakia

Katika nchi hii maridadi yenye milima ya mawemawe na nyanda zenye rutuba, Mashahidi wa Yehova wana shughuli katika kusaidia majirani wao kujifunza mengi zaidi juu ya Biblia. Ripoti moja juu ya utendaji wao inasema: “Kazi hiyo inaendelezwa waziwazi, na mikutano mikubwa inafanywa.”

Baada ya mabadiliko katika Ujerumani Mashariki katika Novemba 1989, Mashahidi katika Chekoslovakia waliitikia kwa haraka sana na kupanga mfululizo wa makusanyiko ya mzunguko wakati wa miezi ya Aprili hadi Juni 1990. Kama tokeo, kwa mara ya kwanza, kulikuwa na ripoti za magazeti zenye mwelekeo chanya kuhusu Mashahidi. Kwa wakati huu, kuna Mashahidi zaidi ya 21,000 katika Chekoslovakia, na katika 1990 kulikuwa na wahudhuriaji wapatao 40,295 katika Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Zaidi ya nusu ya makundi yamepangia mahali ambamo wanaweza kufanya mikutano, na makundi 12 hata yana Majumba ya Ufalme yao wenyewe.

Mkusanyiko ulifanyiwa Prague katika Agosti 1990, kukiwa na wahudhuriaji 23,876, na wapya 1,824 wakabatizwa. Ili kutayarisha stediamu iwe na sura nzuri kwa mkusanyiko, Mashahidi zaidi ya 9,500 walitumia kwa hiari zaidi ya saa 58,000 katika kusafisha na kupaka rangi. Mwakilishi wa TV ya Chekoslovakia alisema: “Tumezuru mambo mengi ya kijamii lakini tunavutiwa na mpango wenu hapa katika stediamu. Tunaona vigumu kuamini kwamba mnapanga mkusanyiko huo kwa mara ya kwanza.” Mgeni mmoja alisema: “Mimi ninavutiwa na hali ya kiroho, uhusiano mchangamfu, na upendo kati ya ndugu zenu. Nilikuja kama rafiki; ninaondoka nikiwa rafiki mkubwa hata zaidi.”

Magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanachapishwa kwa rangi kamili katika lugha ya Czech na Slovak, na Mnara wa Mlinzi ni sawia na lile la Kiingereza katika lugha zote mbili. Tunapokumbuka ile hali yenye uzuizi ya kidogo tu zaidi ya mwaka mmoja uliopita, haya ni mabadiliko ya ajabu.

Matazamio ya Wakati Ujao

Ni nini yaliyo matazamio ya Mashahidi wanaohubiri katika nchi ambako vizazi vipya zaidi vimelelewa katika imani ya kutokuamini kuna Mungu? Ripoti moja inasema: “Kuna giza jingi juu ya Biblia na Mungu. Hata hivyo, upande ulio mzuri ni kwamba, watu hawajatatanishwa na mafundisho ya dini bandia ambayo lazima yaondolewe. Inaonekana kwamba mavuno yatakuwa mengi.”

Kwa hiyo, ni ujumbe gani ambao Mashahidi wa Yehova wanao kutoka kwenye Biblia kutolea watu wa Ulaya ya Mashariki? Makala inayofuata itajibu.

[Maelezo ya Chini]

a Zile nchi nyingine 11 ni Brazili, Uingereza, Kanada, Ufaransa, Ujerumani, Italia, Japani, Meksiko, Naijeria, Ufilipino, na United States.

[Sanduku katika ukurasa wa 8, 9]

Hatimaye Uhuru wa Ibada!

Yafuatayo ni maelezo ya Mashahidi kutoka ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki waliohudhuria Mkusanyiko wa “Lugha Iliyo Safi” katika Berlin, Julai 1990

“Jina langu ni Lydia. Nina umri wa miaka minane, na ninatoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani. Nina furaha sana kuweza kuhudhuria mkusanyiko huu wa wilaya kwa sababu mwaka mmoja uliopita, mipaka haikuwa imefunguliwa. Ilitubidi tuadhimishe Ukumbusho kwa siri. Wakati huu kwa uhuru! Wakati kila mtu aanzapo kuimba, machozi yanadondoka. Mimi nimesisimuka sana na nitaeleza jambo hilo shuleni!”

“Tumejawa na shukrani na uthamini kwa kuwa wageni wa Yehova hapa katika Berlin kati ya udugu wa kimataifa.”—Bernd.

“Jambo la kwamba hata ndugu wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani walikuwa pia kwenye programu linaonyesha jambo moja la maana: Yehova huwazoeza na kuwastahilisha watu wake hata wanapokuwa chini ya marufuku.”—Gottfried.

“Kupigwa kwa makofi na kuimba kulionyesha kwamba kila mtu alikuwa mwenye furaha. Ilikuwa sauti kubwa iliyotuteremesha kwa ndani. Jinsi lazima iwe Yehova alifurahi!”—Egon.

“Baada ya ubatizo wangu, baadhi ya akina ndugu waliuliza kama maji hayo yalikuwa baridi sana. Ningeweza kujibu tu kwamba sikujua. Baraka ya Yehova ilikuwa yenye joto sana hivi kwamba sikuhisi hali-joto ya maji hayo.”—Heidrun.

“Hali katika mabweni tulikolala haiwezi kuelezeka! Kutoka Denmark, Msumbiji, Uingereza, Kalifornia, Ujerumani ya kusini, Uhispania, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ujerumani—sote tuliimba pamoja, sote tulizungumza ‘lugha iliyo safi.’”—Jutta.

“Wakati wote tulikuwa tunawasimulia watoto wetu yale tuliyokumbuka katika mikusanyiko ya Berlin ya miaka ya 1958 na 1960, ambayo ilikuwa ya mwisho kwetu kuhudhuria. Lakini yale tuliyoona sasa yalizidi kumbukumbu letu na matarajio yetu yote.”—Wolfgang.

“Kile kilichotuvutia zaidi ni wakati maelfu waliposimama kuimba na kumsifu Yehova, hasa wakati wa wimbo wa kufunga pamoja na sala. Hatungeweza tena kuzuia machozi yetu yasitutoke.”—Monika na Reinhard.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

“Ukosefu wa Haki Ulisahihishwa”

Chini ya kichwa hicho, dondoo la habari liliripotiwa katika jarida la Kiromania Tineretul liber (Ujana Huru) la Agosti 11, 1990. Lilisema: “Naam, ukosefu wa haki ulisahihishwa. Shirika la kidini lenye kudhulumiwa sana la ‘Mashahidi wa Yehova,’ ambao wamedumisha ukamilifu wao wakiwa wafuasi wa Kristo kwa miaka 40, wametambuliwa kisheria, wakijipatia cheti cha kuwa shirika la kisheria. Tengenezo hilo huendeleza utendaji walo chini ya usimamizi na mamlaka ya Baraza Linaloongoza, likiwa kama tengenezo la ulimwenguni pote, lenye kutenda katika nchi 210 na maeneo ya visiwa.” Dondoo hilo lilimalizia kwa kutangaza mikusanyiko ya Agosti katika Brasov na Cluj-Napoca.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Utendaji mbalimbali wa Mkusanyiko: (kutoka chini kushoto, kuzunguka kuelekea kulia) kutangazwa kwa broshua mpya katika Warsaw; majukwaa ya Hungari na Romania, Budapest; kuandika mambo makuu, Berlin; kufanyiza sura nzuri katika stediamu kabla ya mkusanyiko, Prague

[Picha katika ukurasa wa 10]

Utendaji mbalimbali wa mkusanyiko: (kutoka kushoto, kuzunguka kuelekea kulia) ubatizo, Romania; stediamu, Prague; familia ikiwa na kitabu “Mankind’s Search for God” katika Berlin; msemaji katika Budapest; kuichunguza Biblia katika Polandi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki