Uwe Mwenye Nafsi Yote Katika Huduma ya Shambani
Sehemu ya 3: Changia Maendeleo ya Wengine
1 Uhusiano kati ya Paulo ndugu mwenye umri mkubwa zaidi na kijana Timotheo mwenye kujitoa umetajwa mara nyingi kuwa kielelezo chema cha mazoezi katika huduma. (1 Kor. 4:17) Timotheo aliagizwa na Paulo awape wengine maarifa yale yale na mazoezi ambayo yeye alikuwa amepokea. (2 Tim. 2:1, 2) Sisi tutafanya vema kufuata mpangilio uo huo katika kundi leo.
2 Zoeza Wengine: Uhitaji wa kuzoeza unakuwa wazi tujuapo kwamba leo katika Afrika Mashariki kuna wahubiri 4,450 zaidi ya waliokuwako miaka mitatu iliyopita. Yaelekea sana kwamba walio wengi wao wangefaidishwa na mazoezi ambayo wahubiri wenye ujuzi wanaweza kuwapa. Dada mmoja ambaye kwa ukawaida alitumia saa moja au mbili tu kila mwezi katika utumishi wa shambani alijifunza kunena kwa mafanikio milangoni alipopewa msaada na mhubiri mwenye ujuzi zaidi. Kutotaka kushiriki katika huduma alikokuwa nako hapo kwanza kulitoweka, naye akapata kuwa mhubiri mwenye bidii wa habari njema. Sasa akiwa painia stadi, yeye hutazama kwenye wakati uliopita na kusema: “Nililohitaji tu ni kufunzwa mambo ya kusema, kisha nikaanza kuifurahia huduma.”
3 Ikiwa wewe ni mzee, mtumishi wa huduma, painia, au mhubiri mwenye ujuzi, ni jinsi gani unavyoweza kuchangia maendeleo ya wengine? Hatua ya kwanza ingekuwa kumwarifu kiongozi wa Funzo la Kitabu la Kundi lenu kwamba ungependa kusaidia mhubiri mwingine.
4 Uwe na Mpango na Kujitayarisha: Inasaidia kuwa na muadi dhahiri wa kufanya kazi pamoja. Mwanzoni mwenzako aweza kuwa mwenye wasiwasi na asiyejitumaini, lakini atathamini kwamba mtu fulani anafanya kazi pamoja naye ili kumsaidia ikiwa uhitaji unatokea. (Mhu. 4:9) Ikiwezekana, teueni eneo ambalo mwaweza kupata watu ambao watakuwa na nia ya kuzungumza habari ya Biblia. Jambo hilo litamsaidia mpya ajihusishe na hivyo apate uhakika.
5 Ili kuendeleza mazoezi yenye maendeleo, ingefaidi kuzungumza jinsi ya kufanya ziara ya kurudia kupendezwa kulikopatikana. Hilo lahusu kuweka msingi wakati wa ziara ya kwanza kwa kumwacha mwenye nyumba na swali litakalojibiwa mrudipo. Hakikisha umemsaidia mhubiri mwenye ujuzi mchache kutayarisha, kisha uandamane naye kwenda kwenye ziara. Funzo likianzishwa na huyo mhubiri mpya angali bado hana hakika na uwezo wake mwenyewe, mhubiri mwenye ujuzi zaidi aweza kutaka kuongoza funzo hilo mara chache mpaka huyo mpya astahili kuliendeleza.
6 Kukiwa na mmiminiko wa haraka wa wapya katika tengenezo, hekima ya kuandaa elimu kwa juhudi katika huduma ya shambani inajidhihirisha. Msaada wahitajiwa kutoka kwa wale ambao wamesitawisha stadi zao katika utendaji wa kuhubiri. Ikiwa unaweza kusaidia mtu fulani, baada ya wakati yeye vievile atakuwa ‘amestahili vya kutosha kufundisha wengine.’—2 Tim. 2:2.