Dawa za Kienyeji Katika Afrika Je! Zinafaana na Ukristo?
Kwa mamilioni ya Waafrika, waponyaji wa kienyeji ndio chanzo chao pekee cha aina yo yote cha kupatia dawa. Hasa ndivyo ilivyo katika sehemu za mashambani ambako mahospitali ni machache na si rahisi kupata madaktari. Hata hivyo, kwa kawaida dawa za kienyeji zina mizizi yenye nguvu katika ushirikina na kupashana habari na wafu. Imempasa Mkristo afanye nini chini ya hali hizo?
“‘HII “agbo” pengine itamwua na kukomesha kuteseka kwake na kwetu.’ Na hivyo, kwa kudhania kwamba kiponyeshaji hicho kipya kingekuwa na matokeo ya kunikomesha mimi, mchanganyiko huu ulimiminwa ndani ya koo yangu.”
Hiyo iliandikwa na daktari wa tiba katika gazeti moja la Lagos, Naijeria, Sunday Times katika makala yenye kichwa “Usimdharau Mponyaji wa Kienyeji.” Alikuwa akieleza jinsi wazazi wake walikuwa wamekata tumaini juu ya kupona kwake ugonjwa hatari alipokuwa na umri wa mwaka mmoja tu. Dawa hiyo, waliyopelekewa na mponyaji wa kienyeji, ilisifiwa kuwa ndiyo iliyookoa uhai wake.
Waafrika wengi wanaopendelea dawa za kienyeji wanasema juu ya maponyo ya kushangaza yaliyofanywa katika visa ambavyo utibabu wa hospitalini ulikuwa umeshindwa. Wengine wanazilaumu wakisema kuwa zinakosa usafi wa kiafya, ni dawa za uwongo wa ushirikina. Kuna wale wasiopendelea upande huu wala huu wanaotaka kuwe na uchunguzi wa kisayansi katika dawa za miti-shamba ya kienyeji na kutambuliwa na kukubaliwa zaidi kwa waponyaji wa kienyeji. Wengi wangetaka kuona dawa za kienyeji na za kisasa zikichanganywa pamoja, wakitaja kama mfano ule ushirikiano kati ya matabibu wa vikundi vyote viwili katika China na India.
Hata kama wewe huishi katika Afrika, huenda ukapendezwa kujua. kama dawa za kienyeji za Kiafrika zina matokeo na manufaa kweli kweli. Namna gani juu ya ile sehemu ya sherehe iliyo ya kawaida sana miongoni mwa Waafrika? Je! zile nguvu zipitazo uwezo wa asili ni sehemu ya maana au ni sehemu yenye kudhuru ambayo yapasa ikataliwe? Msimamo wa Mkristo kuelekea dawa hizo za kienyeji za Kiafrika wapasa kuwa nini?
Dawa za Miti-shamba
Mimea, bila shaka, ndiyo chanzo kikuu cha vyakula vyetu na ni ya lazima kwa kuwapo kwetu. Pia kuna mimea inayotoa dawa au sumu ambazo zimeangamiza hesabu kubwa za watu ambao wamezitumia vibaya. Lakini je! wewe ulijua kwamba dawa nyingine za hizo zinatumiwa katika matibabu ya kisasa? Wanasayansi walizivumbua nyingine za dawa hizo kwa kuchunguza mimea iliyokuwa ikitumiwa katika utibabu wa kienyeji au katika michanganyiko ya waganga wa kienyeji. Walikusanya violezo, wakavichunguza kwa njia za kemikali, na wakajaribia matokeo yavyo katika miili na katika vijidudu vinavyotokeza magonjwa. Matokeo yamekuwa kutokezwa kwa baadhi ya dawa za kitiba za maana, kama vile kwinini, risepini, digitali, na kodeni.
Watu wa nyakati za kale walivumbua viponyaji vingi vya mitishamba kwa aksidenti, kwa majaribio na makosa, au kwa kuona yaliyowapata wanyama walipokula mimea fulani. Mara nyingi wale waliofanya mavumbuzi hayo na wakawa waponyaji walihifadhi ustadi huo katika jamaa zao. Hivyo maarifa ya mitishamba yakaja kupitishwa kutoka kwa baba kwenda kwa mwana au kwa watu wengine waliochaguliwa kuwa wanafunzi wa ufundi huo. Waponyaji wa kienyeji walio wengi bado wanaelekea kuficha siri sana, mara nyingi wakiwa hawataki hata kidogo kufunua ile mimea ambayo kutoka kwayo wanafanyiza dawa zao. Lakini mengi zaidi ya viponyaji tu vya mitishamba yanahusika katika dawa za kienyeji za Kiafrika.
Ule Uvutano Wenye Nguvu wa Kupashana Habari na Ulimwengu wa Roho
Uponyaji mwingi wa kienyeji wa Kiafrika umeshirikishwa karibu karibu na zile nguvu zipitazo uwezo wa asili. Wengi wanaamini kwamba mimea ina hisia, uwezo wa kupashana habari, na uwezo wa kufahamu mambo upitao ule wa kawaida. Waponyaji fulani hudai kuwa wanafahamu lugha ya mimea na kwamba wanaweza kupashana habari nayo. Wengine hawaoni upashanaji habari kuwa ukitoka kwa mimea, kwa kuwa wanadai kwamba roho zisizoonekana zimewaelekeza kwenye mitishamba iliyo na vitu vya kuponya.
Hivyo upashanaji habari na ulimwengu wa roho umekuwa na daraka lenye nguvu katika dawa za kienyeji katika Afrika. Wanaijeria wengi, kwa mfano, wanaamini kwamba magonjwa na vifo husababishwa ama na miungu iliyokasirishwa (au roho za wazazi waliokufa) au na maadui wanaotumia uchawi. Kwa hiyo dhabihu za kutuliza zinatolewa, na sherehe na njia za upashanaji habari na ulimwengu wa roho hutumiwa.
Asuquo, mponyaji Mnaijeria, ni mmoja aliyeamini sana hivyo. Yeye anasema: “Mimi nilijifunza dawa za mitishamba kutoka kwa baba yangu nami nilizoea kutoa dhabihu kwa miungu na kwa roho za mababu zetu katika kutayarisha michanganyiko yangu. Mimi niliamini kwamba ni wao waliotokeza maponyo na kwamba kukosa kutoa dhabihu kwao kungeleta ugonjwa na kifo.”
Kwa kweli, mara nyingi inatokea katika njia iliyo kinyume. Imani kama hizo zimewatiisha mamilioni ya watu kwenye woga wa ushirikina na utumwa kwa majeshi ya roho wasioonekana. Wengi wameteseka kwa kupagawa na kusumbuliwa na mashetani. Hiyo pekee ni sababu yenye nguvu ya kukataa ponyo lo lote linalotia ndani dhabihu au sherehe nyingine za kupashana habari na roho. Na roho ambazo zingepagaa na kusumbua watu au kuwadanganya kufikiri kwamba mimea inaweza kupashana habari nao au kwamba wazazi wao waliokufa wangali hai kwa wazi ni zenye kudanganya na ni zenye waovu. Biblia inaonya: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani.”—1 Wakorintho 10:20.
Mashetani, malaika wasiotii waliohukumiwa na Mungu waangamizwe wakati ujao, wamejikaza waondoe watu katika kumwabudu yule Mungu wa kweli, Yehova. (2 Petro 2:4; Yuda 6) Wanajifanya katika visa fulani kwamba wao wenyewe ni miungu wenye fadhili. (2 Wakorintho 11:14) Wakizidisha udanganyifu wao, wanajifanya kuwa ndio watu waliokufa na kuongoza watu kufikiri kwamba wazazi wao waliokufa wangali hai katika ulimwengu wa roho. Hata hivyo, Biblia inasema wazi: “Wafu hawajui neno lo lote, . . . kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko [kaburini] uendako wewe.”—Mhubiri 9:5, 10.
Kwa hiyo lingekuwa kosa kwa waabudu wa Mungu wa kweli kukubali kutoka kwa waponyaji wa mitishamba maponyo yanayotia ndani mazoea yanayohusu kupashana habari na roho. Vivyo hivyo, waponyaji wa mitishamba wanaotamani kutoa ibada inayokubalika kwa Mungu lazima waache kuendeleza kila namna ya mazoea yanayohusu kupashana habari na roho. Kweli kweli, wale wanaotumia upashanaji habari na ulimwengu wa roho wanapoteza upendeleo na ulinzi wa Yehova na hawana mahali katika kundi la Kikristo. (Wagalatia 5:19-21; Ufunuo 21:8) Kuna wengi ambao wameukataa upashanaji habari na ulimwengu wa roho, na wamepata kuona kwamba maponyo fulani ya miti-shamba yanaweza kuwa na matokeo kweli kweli bila mazoea yanayohusu kupashana habari na roho.
Lile Badiliko la Kuja Kwenye Ukristo
Akiongea juu ya mambo aliyojionea mwenyewe, Erhabor, tabibu anayetambuliwa rasmi ambaye huendesha hospitali moja ya miti-shamba, anasema: “Mbeleni mimi niliamini kwamba ilikuwa lazima dhabihu zitiwe ndani pamoja na dawa ili kupigana na ile roho iliyokuwa ikileta ugonjwa. Lakini baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kuwa Mkristo, niliweka kando mazoea hayo na sasa napatana na kanuni za Biblia. Nimepata kuona kwamba vitu vyenye kuponya vimo katika mimea yenyewe.”
Hali kadhalika, Asuquo anasema, “Mambo niliyojifunza juu ya Yehova yalileta maana mpya kwa maisha yangu. Hofu yangu juu ya wazazi waliokufa iliondolewa, nami nikapata kumjua Mungu wa kweli. Pia nilipata kuona kwamba dhabihu hazikuwa za lazima na kwamba ni umajimaji katika magamba ya miti na majani unaoponya watu. Watu wengi sasa wanakuja kwangu wapate kutibiwa kwa sababu mimi situmii vibaya ushirikina wao kwa kuwaomba dhabihu. Utibabu wangu hauwagharimu kiasi kikubwa kama vile wakati wanapoendea waponyaji wa juju.”
Kwa sababu Okon, ambaye pia hutumia utabibu wa mitishamba kuponya watu, hatumii maneno ya kiuchawi au dhabihu katika kuponya watu, yeye anashtakiwa na waponyaji wengine wa mitishamba kuwa ‘anaharibu uponyaji wao.’ “Baadhi ya wagonjwa wangu,” asema, “walikuja wakiwa wapelelezi kuthibitisha kwamba mimi ningali natumia dhabihu kwa siri. Baada ya kupewa matibabu kwa kufaulu majuma mawili, wao walikubali kwamba mimi situmii namna yo yote ya juju. Wao walinufaika pia kutokana na mazungumzo ya Kimaandiko niliyozungumza pamoja nao. Nilishangaa kuona wanne wa wale ambao hapo kwanza walikuwa wagonjwa wangu kwenye ‘Upendo wa Kimungu’ Mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova katika Desemba 1980. Walinikumbatia na kusema: ‘Sisi tulikuja kwako kwa ajili ya maponyo ya kimwili. Wewe ulitupa pia maponyo ya kiroho.’”
Wakristo kama hao wamelazimika kupinga wale wanaotamani kwamba wao warudie mazoea yanayohusu kupashana habari na roho. Wao wanajua kwamba ikiwa wangeunganisha njia zao za kuponya pamoja na namna za upashanaji habari na ulimwengu wa roho, hawangefaa tena kubaki katika kundi la Kikristo. Kwa hiyo wao hawatoi dhabihu au kutumia maneno ya kiuchawi. Wao hawafanyi madai ya uwongo kwamba wanaweza kuponya kila aina ya ugonjwa, wala hawajaribu kutoa wazo la kwamba wao wana nguvu za kipekee. Wao wanaepuka hata kutokea kwa upashanaji habari na ulimwengu wa roho.
Uponyaji wa Kweli Kutoka kwa Mungu
Katika mataifa mengi yanayoendelea, walio wengi wa wakaaji wa nchi wanategemea utibabu unaotolewa na waponyaji wa kienyeji, ambao katika hao wengi wanaweka uhakika mkubwa. Zaidi ya hilo, mahospitali na madaktari wa kitiba ni wachache sana kuweza kutosheleza mahitaji ya utibabu. Hivyo, watu walio wengi katika nchi hizo inaelekea wataendelea kuendea waponyaji, wengi wao wakiwa wale wanaotumia njia za kupashana habari na roho. Lakini wewe utafanya nini?
“Hiyo kweli,” akasema Yesu, “itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Akijua kwamba Biblia inalaumu mazoea hayo, Mkristo atakataa kuwa asiye mshikamanifu kwa Mungu kwa kutafuta maarifa ya kimafumbo au kutafuta kutokana na mponyaji wa miti-shamba kiponyo kinachohusiana na uaguzi. (Kumbukumbu 18:10-13; linganisha Hesabu 23:21, 23) Na akiwa mgonjwa, wala halingekuwa jambo la hekima kwa Mkristo kudhani kwamba matatizo hayo yanatokana na ulogi unaohusu roho. Mmoja hana haja ya kuogopa kwamba atafanywa mgonjwa kwa uchawi anapoendelea kubaki akiwa imara upande wa Mungu kwa kukataa cho chote kinachohusiana na upashanaji habari na ulimwengu wa roho. Ikiwa, kwa sababu ya kutokukamilika tuliko nako sisi sote, tunakuwa wagonjwa, basi uamuzi wa kibinafsi lazima ufanywe kuhusiana na namna za utibabu atakazotumia.a
Dhabihu ya ukombozi iliyotolewa na Yesu ndiyo njia ya pekee ya kukombolewa kutokana na dhambi na matokeo yayo ugonjwa na kifo. (Yohana 3:16; Matendo 4:12) Hiyo pekee ndiyo inayofungulia njia kwa watu waaminifu kupata uzima wa milele katika dunia paradiso ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
Mpaka ifikapo siku hiyo yenye furaha, Mungu Mwenye Nguvu Zote anatuhakikishia sisi kwamba yeye atawalinda wote wanaomtumaini. Kwa hiyo Wakristo wote wanahitaji kumtegemea Yehova, wakikaa karibu naye kwa njia ya sala na kuomba kwa kusihi. Hilo litatokeza maisha yenye afya zaidi sasa, na litatuhakikishia sisi kupokea uzima mkamilifu katika Paradiso ya kidunia iliyoahidiwa.—2 Petro 3:10-14; 1 Yohana 2:17.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Juni 15, 1982, kurasa 22-29.