Kampeni Yenye Mafanikio kwa Kutumia Habari za Ufalme
“KWA Nini Maisha Yamejaa Matatizo Sana?—Je, Paradiso Isiyo na Taabu Yawezekana?” Hiki kilikuwa kichwa cha trakti Habari za Ufalme Na. 34, iliyogawanywa ulimwenguni pote katika lugha 139 katika miezi ya Aprili na Mei mwaka uliopita. “Mojawapo mambo makuu ya mwaka” ndivyo Mashahidi katika Jamaika walivyofafanua kampeni hii ya utumishi. “Chanzo kikubwa cha shangwe kwa akina ndugu,” Mashahidi katika Ubelgiji waliita hivyo. Katika Jamhuri ya Cheki hii ilikuwa mara ya kwanza kwa Mashahidi wa Yehova kupata fursa ya kushiriki katika ugawanyaji wa trakti Habari za Ufalme. Tawi laripoti: “Kampeni hiyo ilileta roho ya bidii na idili.” Mambo kama hayo yalisikika kutoka nchi nyingine nyingi.
Trakti Habari za Ufalme Na. 34 ilikuwa na ujumbe wa pekee kwa wale wanaotweta na kuugua kwa sababu ya mapotovu yanayofanywa kwa jina la dini. (Ezekieli 9:4) Ilikuwa na faraja kwa wale ambao wana maisha yenye taabu kwa sababu ya “nyakati za hatari” ambazo hawawezi kuzidhibiti. (2 Timotheo 3:1) Ikielekeza kwenye Biblia, trakti hiyo ilionyesha kwamba matatizo ya maisha yatatatuliwa hivi karibuni. Paradiso isiyo na taabu ni hakika. (Luka 23:43) Wengi waliosoma Habari za Ufalme walivutwa na ujumbe wayo. Mwanamume mmoja katika Togo alimwambia Shahidi hivi: “Mliyoandika hayawezi kubishaniwa.”
Bila shaka, ugawanyaji wa trakti Habari za Ufalme ulivutia uangalifu usio wa kawaida. Katika Denmark mwenye nyumba alimwitikia hivi Shahidi aliyekuwa akitoa trakti: “Nimerudi tu kutoka Marekani. Kabla sijaondoka, mtu fulani alinitolea trakti yenu. Sasa nimefika hapa, na mara trakti hiyohiyo yatolewa kwa lugha ya Kidenmark!”
Uungaji-Mkono Wenye Idili kwa Kampeni
Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kwa idili walijiunga na kazi ya kugawanya ile trakti. Austria, El Salvador, Haiti, Hungaria, Italia, New Caledonia, zilikuwa tu baadhi ya nchi nyingi zilizoripoti vilele vya wakati wote vya wahubiri wakati wa miezi ya ugawanyaji wa trakti Habari za Ufalme.
Katika Zambia mwangalizi wa mzunguko amezoeza binti yake mwenye umri wa miaka mitatu aitwaye Deborah, kutoa fasihi nyumba kwa nyumba. Wakati wa kampeni ya trakti Habari za Ufalme Na. 34, Deborah aliangusha zaidi ya nakala 45 za trakti hiyo. Mama yake alianzisha mafunzo ya Biblia na baadhi ya waliokubali trakti Habari za Ufalme kutoka kwa Deborah.
Katika Afrika Kusini tineja mmoja alimtolea trakti mwanashule mwenzake aitwaye Cashia. Cashia aliisoma trakti na kusema: “Inapendeza sana—kuishi milele katika paradiso duniani! Kwa nini sijaambiwa kuhusu jambo hili mbeleni?” Funzo la Biblia lilianzishwa. Katika juma hilo Cashia alipokea trakti nyingine. Ile ya pili ilitoka kwa rafiki yake wa barua Mkatoliki wa Kiroma, aishiye Saiprasi. Rafiki huyo wa barua alimwelezea Cashia kwa nini mafundisho ya Kanisa Katoliki ya Kiroma ni ya bandia na kumwambia kwamba alikusudia kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Bila shaka, hilo liliimarisha zaidi azimio la Cashia la kuendelea kujifunza.
Mvulana mwenye umri wa miaka kumi katika Uswisi alishiriki pamoja na mama yake kugawanya trakti hiyo. Alimpatia mwanamke mmoja mchanga nakala na kumtia moyo aisome kwa uangalifu. Mwanamke huyo mchanga alimwuliza mvulana yule kama kwa kweli aliamini kilichokuwa kwenye picha ya ukurasa wayo wa juu—uhai usiokoma duniani. Jibu la mvulana lilikuwa nini? “Naam, nina uhakika.” Basi mwanamke huyo akafunua kwamba alikuwa akitafuta imani ya kweli kwa sababu kulikuwa na mapingamizi mengi sana katika dini yake mwenyewe. Kwenye ziara ya kurudia, funzo la Biblia lilianzishwa.
Maitikio ya Mara Moja
Nyakati nyingine trakti Habari za Ufalme ilisababisha itikio la mara moja kwa wale walioisoma. Baada ya kusoma trakti hiyo, msichana mmoja mwenye umri wa miaka 11 katika Ubelgiji alikiri kwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwamba alikuwa akiiba dukani. Mama ya msichana huyo alitaka kuficha jambo hilo, lakini dhamiri ya msichana mchanga ilisukumwa na yale aliyosoma, naye akasisitiza kwenda kumwona meneja wa duka hilo. Mama huyo hatimaye alimruhusu binti yake arudi dukani akiwa na yule Shahidi. Meneja huyo alishangazwa na ungamo lake. Alipojua kwamba ni trakti Habari za Ufalme iliyomchochea atende hivyo, alichukua nakala yake mwenyewe ili aone mambo iliyokuwa nayo yenye nguvu hivyo. Sasa msichana huyo ana funzo la Biblia lenye maendeleo.
Shahidi mmoja katika Kamerun aliyemwachia mwanamume mmoja trakti Habari za Ufalme asimulia: “Tuliporudi, tulipata kwamba alikuwa tayari ameipiga mistari na alikuwa na maswali kadhaa. Baada ya kupata majibu yenye kuridhisha, alitangaza hivi: ‘Ni kweli kabisa kwamba dini imechangia ukosefu wa furaha kwa wanadamu. Trakti yenu imenisaidia kuelewa mengi, lakini ningependa kujua zaidi.’” Sasa yeye ana funzo la Biblia la kawaida.
Shahidi aliyekuwa akienda nyumba kwa nyumba katika Uruguai alimwangushia mwanamume mmoja trakti. Shahidi huyo aliendelea na kazi yake ya kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuhubiri kwenye eneo hilo mpaka akafika mlango wa nyuma wa nyumba ya yule mwanamume. Alishangaa kumpata mwanamume huyo akimngoja, akiwa na trakti mkononi. Alikuwa tayari ameisoma na alitaka habari zaidi. Funzo lilianzishwa mara hiyo.
Umma Wasaidia Ugawanyaji
Katika Japani Shahidi mchanga alimfikia mwanamume aliye katika umri wa miaka ya 50 na kumtolea trakti. Mwanamume huyo aliuliza: “Mnafanyaje na karatasi hiyo mnapokutana na watu wasioona?” Huyo Shahidi akakiri kwamba hajui. Mwanamume huyo akamwambia angoje kidogo naye akarudi nyumbani kwake. Alirudi na nakala ya trakti Habari za Ufalme na kusema: “Tayari nimepokea karatasi hiyo. Niliona kwamba kilikuwa na habari yenye kupendeza sana na yenye maana, kwa hiyo nikaiandika kwa Braille (maandishi ya vipofu). Tafadhali tumia hii kwa watu walio vipofu.” Mwanamume huyo alitumia saa nyingi akinakili trakti Habari za Ufalme katika Braille ili vipofu wasikose kunufaika nayo.
Katika Slovakia mwanamume mmoja aliipenda trakti hiyo sana hivi kwamba akafanyiza nakala 20, na kuzigawanya hizi nakala za rangi nyeusi na nyeupe yeye mwenyewe. Mtangazaji mmoja katika Uswisi aliiachia familia moja trakti Habari za Ufalme naye akaendelea kuhubiri orofa za juu za jengo ambalo familia hiyo ilikuwa ikiishi. Alipofika chini tena, alikutana na mvulana mchanga wa familia hiyo, ambaye alimwomba nakala nyingine 19 za trakti hiyo. Kwenye shule ya mvulana huyo, wanafunzi walikuwa wamepewa mgawo wa kuandika juu ya matatizo na utafutaji wa utatuzi. Yeye alitaka nakala ya trakti Habari za Ufalme kwa kila mwanadarasa mwenzake.
Kila Mtu Aliipata
Wale walioshiriki katika kampeni walijaribu sana kuhakikisha kwamba kila mtu aliipata. Katika New Caledonia Mashahidi wawili walikuwa wakisafiri kwenye eneo la kabila la mbali ili kugawanya trakti Habari za Ufalme. Wakiwa njiani waliona kijia ambacho kilionekana hakijatumiwa, lakini wakaamua kuona kama mtu yeyote alikuwa akiishi mwisho wacho. Wakiacha gari, walitembea kupitia kijia hicho, kupita vijito hadi hatimaye wakapata nyumba moja. Wenzi wa ndoa ambao walikuwa bado hawajasikia juu ya Mashahidi wa Yehova waliishi huko, nao walikubali nakala ya trakti Habari za Ufalme. Baadaye watangazaji hao walifanya ziara ya kurudia na kwa mshangao wao walipata kwamba hao wenzi wa ndoa wametengeneza barabara na madaraja madogo kadhaa ili Mashahidi waweze kuendesha gari lao hadi kwenye nyumba. Funzo la Biblia la kawaida lilianzishwa.
Katika Poland Shahidi alilazimika kupitia mahali pa ujenzi ili amtolee mwenye nyumba nakala ya trakti Habari za Ufalme. Wafanyakazi walimtazama aliporudi kupitia mahali pa ujenzi. Hatimaye, mmoja wa wafanyakazi akamwita, akimwomba asiwasahau. Alipowafikia, walitua na kusikiliza kwa uangalifu utoaji wa trakti. Walikubali nakala za trakti Habari za Ufalme pamoja na magazeti na baadaye, kwenye ziara ya kurudia, vitabu.
Mamia ya mamilioni ya trakti Habari za Ufalme Na. 34 yaligawanywa kwa lugha nyingi. Ujumbe wayo tayari umekuwa na tokeo kubwa. Wengi wamejifunza kwamba ulimwengu usio na taabu wawezekana. Twaomba kwamba watu wenye mioyo yenye uadilifu waendelee kuitikia na hatimaye kuwa miongoni mwa “wenye upole” ‘watakaoirithi nchi, na . . . kujifurahisha kwa wingi wa amani.’—Zaburi 37:11.
[Sanduku katika ukurasa wa 31]
Endelea Kugawanya Magazeti!
Miezi ya Aprili na Mei 1995 ilikuwa na kampeni yenye mafanikio sana ya kugawanya trakti Habari za Ufalme Na. 34. Katika kipindi cha miezi hiyo miwili, pia kulikuwako na ugawanyaji wenye kutokeza wa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa mfano, ndugu mmoja katika Jamhuri ya Cheki, aripoti kwamba katika mwezi wa Aprili aliangusha nakala 250 za trakti Habari za Ufalme na magazeti 750. Katika Guadeloupe, Jumamosi, mwezi wa Aprili 15, ilichaguliwa kuwa siku ya pekee ya magazeti. Karibu kila mhubiri nchini alishiriki katika huduma siku hiyo! Slovakia ilikuwa na kilele kipya katika ugawanyaji wa magazeti mwezi wa Aprili. Ripoti kama hizo zilitoka nchi nyingine nyingi.
Kwa hiyo kwa nini usifanye miezi ya Aprili na Mei 1996 kuwa miezi yenye kutokeza ya ugawanyaji wa magazeti? Makutaniko yanaweza kupanga siku za pekee za magazeti. Watu mmoja-mmoja wanaweza kushiriki katika upainia msaidizi. Kwa njia hii na nyinginezo, ugawanyaji wa magazeti waweza kuchochewa, na ujumbe muhimu uliotangazwa katika trakti Habari za Ufalme Na. 34 utaendelea kuenea. Kisha, kama ilivyotukia mwaka uliopita, hakika Yehova atabariki roho ya bidii tuonyeshayo.—2 Timotheo 4:22.