Sanduku La Swali
◼ Ni wakati gani ambao ungefaa kuanzisha kikundi kingine cha Funzo la Kitabu la Kutaniko?
Itabidi kuanzisha kikundi kingine cha funzo la kitabu ili hudhurio liwe na watu 15 au chini ya hapo katika sehemu zote za funzo la kitabu kutia ndani funzo la Jumba la Ufalme. Kwa nini jambo hilo lapendekezwa?
Vikundi vya Funzo la Kitabu la Kutaniko vinapokuwa vidogo, kiongozi huweza kumpa uangalifu kila anayehudhuria. Kwa kuongezea, wote huwa na fursa nyingi za kutoa maelezo katika mazingira yanayofanya iwe rahisi kutoa tangazo la hadharani la imani yao. (Ebr. 10:23; 13:15) Kuwa na vikundi vidogo katika sehemu mbalimbali kwenye eneo la kutaniko hufanya iwe rahisi kuhudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko na mikutano ya utumishi wa shambani. Makutaniko ambayo yameongeza vikundi vya funzo la kitabu yamekuwa na ongezeko la hudhurio pia.
Huenda kukawa na hali za pekee ambazo zinafanya ifae kuunda kikundi kingine, hata kama kitakuwa kidogo sana. Huenda ikafaa kuanzisha kikundi kingine katika eneo la mbali au mahali ambapo vikundi vya sasa ni vikubwa mno au havina mahali pa kutosha pa kuketi. Ikihitajika, kikundi kingine cha kukutana mchana kinaweza kuanzishwa kwa manufaa ya walio wazee-wazee, wafanyakazi wa usiku, au akina dada walio na waume wasio Mashahidi.
Kila kikundi cha funzo la kitabu chapaswa kuwa na wahubiri kadhaa walio imara kiroho na kiongozi na msomaji anayestahili. Akina ndugu wanapaswa kujitahidi kufikia sifa hizo ili kutimiza mahitaji ya kutaniko.
Wazee wanaweza kusaidia kutaniko lifanye maendeleo kwa kuhakikisha kwamba vikundi vya funzo la kitabu la kutaniko vina ukubwa unaofaa, vinaongozwa vizuri kiroho, na vinakutania mahali pafaapo. Inapofaa, vikundi vipya vyapasa kuanzishwa ili wote waweze kunufaika na mpango huu wa pekee wa kiroho. Je, unaweza kujitolea ili nyumba yako iwe mahali pa funzo la kitabu? Wengi ambao wamefanya hivyo wamefurahia baraka za kiroho.