Usisite
1. Ni nini kinachohitaji ujasiri, na kwa nini?
1 Je, umewahi kusita kutoa ushahidi shuleni kwa sababu unaogopa kudhihakiwa? Kwa kweli unahitaji kuwa na ujasiri ili uweze kueleza wengine imani yako, hasa ikiwa wewe ni mwenye haya. Ni nini kitakachokusaidia?
2. Kwa nini tunahitaji utambuzi tunapohubiri shuleni?
2 Tumia Utambuzi: Ingawa shule inaweza kuonwa kwa kufaa kuwa eneo lako la kibinafsi, kumbuka kwamba si lazima uanzishe mazungumzo ya Biblia na kila mtu kama vile ambavyo ungefanya unapohubiri nyumba kwa nyumba. Tumia utambuzi ili ujue wakati wa kuzungumza. (Mhu. 3:1, 7) Kichwa cha mazungumzo darasani au mgawo wa shule unaweza kukupa fursa ya kueleza imani yako. Au mwanafunzi mwenzako anaweza kukuuliza kwa nini hushiriki katika mambo fulani. Wakristo wengine wamewaeleza walimu wao mwanzoni mwa mwaka wa shule kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova na kuwapa machapisho yanayoeleza imani yetu. Wengine wameacha machapisho juu ya dawati ili kuwachochea wanafunzi wenzao waulize maswali.
3. Unaweza kujitayarisha jinsi gani kutoa ushahidi shuleni?
3 Jitayarishe: Ukijitayarisha, utakuwa na uhakika zaidi. (1 Pet. 3:15) Kwa hiyo jaribu kuwazia kimbele maswali ambayo huenda yakazuka, na ufikirie jinsi ungejibu. (Met. 15:28) Ikiwezekana, beba Biblia yako na machapisho kadhaa, kama vile kitabu Kutoa Sababu,vitabu vya Vijana Huuliza na machapisho kuhusu uumbaji, ili uweze kuvirejelea inapohitajika. Uliza wazazi wako watie ndani vipindi vya mazoezi wakati wa ibada ya familia.
4. Kwa nini uendelee kutoa ushahidi shuleni?
4 Uwe na maoni yanayofaa: Usidhani kwamba nyakati zote wanafunzi wenzako watakudhihaki unapowahubiria. Yaelekea wengine watapendezwa na ujasiri wako na huenda hata wakusikilize. Lakini usivunjike moyo ikiwa hakuna atakayesikiliza. Yehova anapendezwa kwa sababu ulijaribu. (Ebr. 13:15, 16) Endelea kumwomba akusaidie ‘uendelee kusema kwa ujasiri wote.’ (Mdo. 4:29; 2 Tim. 1:7, 8) Hebu wazia furaha utakayopata ikiwa mtu fulani atasikiliza. Hatimaye, huenda mtu huyo akajiunga nawe katika kumtumikia Yehova!