-
‘Kufundisha na Kuhubiri Habari Njema’‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sehemu ya 2
‘Kufundisha na Kuhubiri Habari Njema’
Seremala. Mfanya-miujiza. Mponyaji. Yesu alikuwa yote hayo, na mengine mengi. Hata hivyo, watu hawakumwita kwa majina hayo. Walimwita Mwalimu. Ndiyo, kazi yake kuu ilikuwa ‘kufundisha na kuhubiri habari njema.’ (Mathayo 4:23) Tukiwa wafuasi wa Yesu, sisi pia tunapaswa kufanya kazi hiyo. Katika sehemu hii, tutajifunza mfano wake tunaoweza kufuata.
-
-
“Nilitumwa Kufanya Hivyo”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 8
“Nilitumwa Kufanya Hivyo”
1-4. (a) Yesu anamfundisha mwanamke Msamaria kwa ustadi jinsi gani, na anapata matokeo gani? (b) Mitume wake wana maoni gani juu ya jambo hilo?
YESU na mitume wake wamekuwa wakitembea kwa muda fulani. Wanaelekea kaskazini, kutoka Yudea kwenda Galilaya. Njia fupi zaidi, inayochukua siku tatu hivi, inapitia Samaria. Saa sita hivi mchana, wanakaribia jiji dogo linaloitwa Sikari ambapo wanapumzika.
2 Mitume wake wanapoenda kununua chakula, Yesu anapumzika kando ya kisima kilicho nje ya jiji hilo. Mwanamke fulani anakuja kuchota maji. Ikiwa Yesu angetaka, angempuuza kwa kuwa “amechoka kwa sababu ya safari hiyo.” (Yohana 4:6) Ingeeleweka ikiwa Yesu angempuuza mwanamke huyo Msamaria na kuendelea na shughuli zake. Kama tulivyoona katika Sura ya 4 ya kitabu hiki, mwanamke huyo angetazamia mtu yeyote ambaye ni Myahudi ampuuze. Hata hivyo, Yesu anaanzisha mazungumzo pamoja naye.
3 Anaanza kwa mfano unaohusu maisha ya kila siku ya mwanamke huyo. Anazungumzia jambo ambalo mwanamke huyo anafanya sasa hivi. Amekuja kuchota maji, naye Yesu anazungumza kuhusu maji ya uzima yatakayomaliza kiu yake ya kiroho. Mara kwa mara mwanamke huyo anataja mambo yanayoweza kutokeza mabishano.a Kwa busara, Yesu anaepuka mambo hayo na kuzungumzia habari aliyokuwa nayo akilini. Anakazia mambo ya kiroho, yale yanayohusu ibada safi na Yehova Mungu. Maneno yake yana matokeo sana, kwa maana mwanamke huyo anawasimulia watu wa jiji hilo, nao pia wanataka kumsikiliza Yesu.—Yohana 4:3-42.
4 Mitume wanaporudi, wana maoni gani kuhusu ushahidi wa pekee ambao Yesu anatoa? Hawachangamki hata kidogo. Wanashangaa kumwona Yesu akizungumza na mwanamke huyo, na inaonekana kwamba hawaongei na mwanamke huyo hata kidogo. Mwanamke huyo anapoondoka, wanamsihi Yesu tena na tena ale chakula ambacho wameleta. Hata hivyo, Yesu anawaambia: “Nina chakula ambacho hamkijui.” Wanashangaa! Mwanzoni, wanafikiri kwamba Yesu anazungumzia chakula cha kimwili. Kisha, anaeleza hivi: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yohana 4:32, 34) Hivyo, Yesu anawafundisha kwamba anaiona kazi yake kuu maishani kuwa jambo la maana kuliko kula. Anataka wawe na maoni hayohayo kuhusu kazi hiyo. Ni kazi gani hiyo?
5. Ni kazi gani kuu ambayo Yesu alifanya maishani, na tutachunguza nini katika sura hii?
5 Pindi moja Yesu alisema: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Yesu alitumwa kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme wa Mungu.b Wafuasi wa Yesu leo wanafanya kazi hiyohiyo. Basi tuchunguze kwa nini Yesu alihubiri, habari alizohubiri, na jinsi alivyoiona kazi yake.
Kwa Nini Yesu Alihubiri?
6, 7. Yesu alitaka kila “mfundishaji wa watu wote” awe na maoni gani kuhusu kuwaeleza wengine habari njema? Toa mfano.
6 Acheni tuone jinsi Yesu alivyoziona kweli alizofundisha; kisha tutazungumzia maoni yake kuelekea watu aliowafundisha. Yesu alitumia mfano ulio wazi kuonyesha maoni yake kuhusu kueleza wengine kweli ambazo Yehova alimfundisha. Alisema hivi: “Kila mfundishaji wa watu wote, anapofundishwa kuhusiana na ufalme wa mbinguni, ni kama mtu, mwenye nyumba, ambaye hutoa katika hazina yake vitu vipya na vya zamani.” (Mathayo 13:52) Kwa nini mwenye nyumba katika mfano huo anatoa vitu katika hazina yake?
7 Kusudi la mwenye nyumba huyo si kuonyesha tu mali yake kama Mfalme Hezekia wa kale alivyofanya na kujiletea matatizo. (2 Wafalme 20:13-20) Basi, nia yake ni nini? Fikiria mfano huu: Tuseme umeenda kumtembelea mwalimu unayempenda nyumbani kwake. Anafungua kisanduku cha meza na kutoa barua mbili, moja imezeeka na kubadilika rangi, na nyingine ni ya karibuni. Alizipokea kutoka kwa baba yake, moja ilitumwa zamani sana mwalimu huyo alipokuwa kijana mdogo tu, na ile nyingine ilitumwa hivi karibuni. Kwa uchangamfu, anakueleza jinsi anavyothamini barua hizo na jinsi ambavyo mashauri yaliyomo yamebadili maisha yake na kwamba yanaweza kukusaidia. Ni wazi kwamba mwalimu huyo anathamini sana barua hizo. (Luka 6:45) Anakuonyesha barua hizo, si ili kujivuna au kujifaidi kwa njia fulani, bali ili kukufaidi na kukuonyesha kwamba ni zenye thamani.
8. Kwa nini tuna sababu nzuri ya kuziona kweli tunazojifunza katika Neno la Mungu kuwa hazina?
8 Yesu, Mwalimu Mkuu, alikuwa na nia hiyohiyo alipowaeleza wengine kweli kumhusu Mungu. Aliziona kweli hizo kuwa zenye thamani sana. Alizipenda, naye alitamani kuwaambia wengine. Alitaka “kila mfundishaji wa watu wote,” yaani, wafuasi wake wote, wawe na maoni kama yake. Je, tuna maoni kama hayo? Tuna sababu nzuri ya kupenda kila kweli tunayojifunza katika Neno la Mungu. Tunathamini kweli zenye thamani, iwe ni mafundisho ambayo tumeamini kwa muda mrefu au yale yaliyorekebishwa hivi karibuni. Kwa kuzungumza kwa uchangamfu na kuendelea kupenda mambo ambayo Yehova ametufundisha, tunaonyesha upendo huo, kama Yesu.
9. (a) Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu watu aliowafundisha? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kuiga maoni yake kuelekea watu?
9 Kama tutakavyozungumzia kwa undani katika Sehemu ya 3, Yesu aliwapenda pia watu aliowafundisha. Ilitabiriwa kwamba Masihi “atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini.” (Zaburi 72:13) Kwa kweli, Yesu aliwahangaikia watu. Alihangaikia fikira na mitazamo yao; alihangaikia mizigo iliyowalemea na mambo yaliyowazuia wasielewe kweli. (Mathayo 11:28; 16:13; 23:13, 15) Kwa mfano, mkumbuke yule mwanamke Msamaria. Bila shaka, alivutiwa sana kwa kuwa Yesu alipendezwa naye. Utambuzi ambao Yesu alikuwa nao kuhusu maisha ya mwanamke huyo ulimchochea mwanamke huyo kumkubali kuwa nabii na kuwaambia wengine juu ya Yesu. (Yohana 4:16-19, 39) Ni kweli kwamba wafuasi wa Yesu leo hawawezi kusoma mioyo ya watu wanaowahubiria. Hata hivyo, tunaweza kupendezwa na watu kama Yesu alivyofanya; tunaweza kuwaonyesha kwamba tunawahangaikia; na tunaweza kuchagua maneno yatakayofaa mapendezi, matatizo, na mahitaji yao.
Habari Ambayo Yesu Alihubiri
10, 11. (a) Yesu alihubiri nini? (b) Kwa nini Ufalme wa Mungu ulihitajiwa?
10 Yesu alihubiri nini? Ikiwa ungetafuta jibu kwa kuchunguza mafundisho ya dini nyingi zinazodai kuwa za Kikristo, unaweza kukata kauli kwamba alitangaza injili fulani ya kijamii, yaani, kutumia kanuni za Kikristo ili kutatua matatizo ya kibinadamu. Au unaweza kufikiri kwamba aliunga mkono mabadiliko ya kisiasa au alikazia kwamba lazima kila mtu aokoke. Hata hivyo, kama tulivyoona, Yesu alisema hivi waziwazi: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu.” Hilo lilimaanisha nini?
11 Kumbuka, Yesu alikuwa mbinguni wakati Shetani alipotokeza shaka kwa mara ya kwanza kuhusu haki ya Yehova ya kutawala. Haikosi Yesu aliumia sana kumwona Baba yake mwadilifu akichongewa na kushtakiwa kuwa Mtawala asiyetenda kwa haki, ambaye anawanyima viumbe Wake mema! Lazima Mwana wa Mungu alihuzunika sana wakati Adamu na Hawa, waliokuja kuwa wazazi wa wanadamu wote, walipouamini uchongezi wa Shetani! Mwana huyo aliona kwamba familia ya wanadamu imerithi dhambi na kifo kwa sababu ya uasi huo. (Waroma 5:12) Ingawa hivyo, alifurahi kama nini kujua kwamba siku moja Baba yake atanyoosha mambo!
12, 13. Ufalme wa Mungu utaondoa mambo gani yasiyo ya haki, na Yesu alionyesha jinsi gani kwamba Ufalme ndicho kilichokuwa kichwa kikuu cha mahubiri yake?
12 Ni suala gani kuu lililohitaji kutatuliwa? Jina takatifu la Yehova lilihitaji kutakaswa, kuondolewa shutuma zote za Shetani na wote wanaomuunga mkono. Haki ya enzi kuu ya Yehova, njia yake ya kutawala, ilihitaji kutetewa. Yesu alielewa masuala hayo kuliko mwanadamu mwingine yeyote. Katika sala ya mfano, aliwafundisha wafuasi wake waombe kwanza jina la Baba yake litakaswe, kisha Ufalme wa Baba yake uje, halafu mapenzi ya Mungu yatendeke duniani. (Mathayo 6:9, 10) Hivi karibuni Ufalme wa Mungu, Kristo Yesu akiwa Mtawala, utaondolea mbali mfumo mfisadi wa Shetani na kuthibitisha utawala wenye uadilifu wa Yehova.—Danieli 2:44.
13 Ufalme huo ulikuwa kichwa kikuu cha huduma ya Yesu. Maneno yake yote na matendo yake yote yalionyesha wazi maana ya Ufalme huo na jinsi utakavyotimiza kusudi la Yehova. Yesu hakuruhusu jambo lolote limkengeushe aache kazi yake ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wakati huo, kulikuwa na matatizo ya kijamii na ukosefu mwingi wa haki, lakini alikazia fikira habari aliyohubiri na kazi yake. Kwa kuwa Yesu aliendelea kukazia fikira mambo hayo, je, hilo linamaanisha kwamba alikuwa na maoni finyu na kwamba alifundisha kwa njia isiyovutia na yenye kuwachosha watu? Sivyo hata kidogo!
14, 15. (a) Ni kwa njia gani Yesu alikuwa “mkuu kuliko Sulemani”? (b) Tunaweza kumwiga Yesu kwa njia gani tunapohubiri?
14 Kama tutakavyoona katika sehemu hii yote, Yesu alifanya mafundisho yake yavutie na yapendeze. Maneno yake yaligusa mioyo ya watu. Huenda hilo likatukumbusha Mfalme Sulemani mwenye hekima aliyetafuta maneno yenye kupendeza na maneno sahihi ya kweli ili kueleza mambo ambayo Yehova alimwongoza kuyaandika. (Mhubiri 12:10) Yehova alimpa mtu huyo asiye mkamilifu “ukunjufu wa moyo” uliomwezesha kuzungumza kuhusu mambo mengi, kutia ndani ndege, samaki, miti, na wanyama. Watu walitoka mbali kumsikia Sulemani akizungumza. (1 Wafalme 4:29-34) Hata hivyo, Yesu alikuwa “mkuu kuliko Sulemani.” (Mathayo 12:42) Alimzidi Sulemani kwa hekima na “ukunjufu wa moyo.” Yesu alipokuwa akiwafundisha watu, alitumia ujuzi wake mwingi wa Neno la Mungu na vilevile mambo mengi aliyojua kuhusu ndege, wanyama, samaki, ukulima, hali ya hewa, matukio ya karibuni, historia, na hali za kijamii. Lakini Yesu hakutumia ujuzi wake kujionyesha. Ujumbe wake ulikuwa rahisi na wazi. Haishangazi kwamba watu walifurahia kusikia akizungumza!—Marko 12:37; Luka 19:48.
15 Leo, Wakristo wanajaribu kufuata mfano wa Yesu. Hatuna hekima na ujuzi mwingi kama wake, lakini sisi sote tuna kiasi fulani cha ujuzi na uzoefu ambao tunaweza kutumia tunapowafundisha wengine kweli za Neno la Mungu. Kwa mfano, wazazi wanaweza kutumia uzoefu wao wa kuwalea watoto kuonyesha kwamba Yehova anawapenda watoto Wake. Wengine wanaweza kutumia mifano kutokana na kazi yao ya kimwili, shule, au ujuzi wao kuhusu watu na matukio ya karibuni. Wakati huohuo, tunaepuka jambo lolote linaloweza kuwakengeusha watu wasisikilize habari njema ya Ufalme wa Mungu.—1 Timotheo 4:16.
Jinsi Yesu Alivyoiona Huduma Yake
16, 17. (a) Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu huduma yake? (b) Ni kwa njia gani Yesu alionyesha kwamba jambo kuu maishani mwake lilikuwa huduma yake?
16 Yesu aliiona huduma yake kuwa hazina yenye thamani. Alifurahia kuwasaidia watu wamjue Baba yake wa mbinguni vizuri, bila kuwavuruga akili kwa mafundisho na mapokeo ya wanadamu. Yesu alipenda kuwasaidia watu wawe na uhusiano mzuri pamoja na Yehova na wawe na tumaini la uzima wa milele. Alipenda kuwapelekea watu habari njema yenye kufariji na kuchangamsha moyo. Ni nini kinachoonyesha hilo? Ona njia tatu.
17 Kwanza, Yesu alifanya huduma kuwa jambo kuu maishani mwake. Kazi yake kuu maishani ilikuwa kuzungumza kuhusu Ufalme. Hiyo ndiyo sababu Yesu alitenda kwa hekima kwa kuishi maisha rahisi, kama tulivyoona katika Sura ya 5. Kama alivyowashauri wengine, alikazia fikira jambo la maana zaidi. Hakukengeushwa na vitu vingi ambavyo angehitaji kulipia, kutunza, kurekebisha, au kubadili baada ya muda. Aliishi maisha rahisi ili asikengeushwe kutoka kwa huduma yake.—Mathayo 6:22; 8:20.
18. Ni katika njia gani Yesu alijitoa kabisa kutimiza huduma yake?
18 Pili, Yesu alijitoa kabisa kutimiza huduma yake. Alitumia nguvu nyingi katika huduma, akitembea kilomita nyingi nchini Palestina, huku akitafuta watu ambao angeweza kuwahubiria habari njema. Alizungumza nao nyumbani mwao, katika viwanja vya watu wote, sokoni, na mahali palipokuwa na watu wengi. Alizungumza nao hata alipohitaji kupumzika, kula, kunywa maji, au kustarehe pamoja na rafiki zake wa karibu. Hata alipokuwa akifa, aliendelea kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu!—Luka 23:39-43.
19, 20. Ni kwa njia gani Yesu alionyesha kwamba kazi ya kuhubiri inahitaji kufanywa haraka?
19 Tatu, Yesu aliona kwamba huduma yake ilipaswa kufanywa haraka. Kumbuka alipozungumza na yule mwanamke Msamaria kwenye kisima nje ya jiji la Sikari. Inaonekana kwamba mitume wa Yesu hawakuona uharaka wa kuwaeleza wengine habari njema katika pindi hiyo. Yesu aliwaambia hivi: “Je, ninyi hamsemi kwamba bado kuna miezi minne kabla ya mavuno kuja? Tazama! Ninawaambia ninyi: Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.”—Yohana 4:35.
20 Mfano huo wa Yesu ulitegemea majira ya wakati huo. Inaonekana kwamba ulikuwa mwezi wa Kislevu unaolingana na Novemba/Desemba (Mwezi wa 11/Mwezi wa 12). Shayiri ingevunwa miezi minne baadaye, karibu na wakati wa Pasaka, Nisani 14. Kwa hiyo, wakulima hawakuona uharaka wa kuvuna wakati huo. Bado kulikuwa na wakati wa kutosha. Namna gani kukusanywa kwa watu? Wengi walikuwa tayari kusikia, kujifunza, kuwa wanafunzi wa Kristo na kuwa na tumaini zuri ajabu ambalo Yehova aliwaahidi. Ni kana kwamba Yesu alitazama mashamba hayo ya mfano na kuyaona kuwa meupe huku nafaka zilizoiva zikipeperushwa na upepo mwanana, kuonyesha ziko tayari kuvunwa.c Wakati wa mavuno ulikuwa umefika, nayo kazi hiyo ilipaswa kufanywa haraka! Hiyo ndiyo sababu wakati watu wa jiji fulani walipotaka Yesu aendelee kukaa kwao, alisema hivi: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.”—Luka 4:43.
21. Tunaweza kumwiga Yesu kwa njia gani?
21 Tunaweza kumwiga Yesu katika njia zote tatu ambazo tumezungumzia. Tunaweza kufanya huduma ya Kikristo iwe jambo kuu maishani mwetu. Hata ingawa labda tuna madaraka ya familia na shughuli nyinginezo za maisha, tunaweza kuonyesha kwamba tunatanguliza huduma yetu kwa kuifanya kwa bidii na kwa ukawaida kama Yesu. (Mathayo 6:33; 1 Timotheo 5:8) Tunaweza kujitoa kabisa katika huduma, tukitumia wakati, nguvu, na mali yetu ili kuitimiza. (Luka 13:24) Nasi tunaweza kukumbuka sikuzote kwamba kazi yetu inahitaji kufanywa haraka. (2 Timotheo 4:2) Tunahitaji kutumia kila nafasi kuhubiri!
22. Ni nini kitakachozungumziwa katika sura inayofuata?
22 Pia, Yesu alionyesha kwamba anatambua kuwa kazi hiyo inahitaji kufanywa haraka kwa kuhakikisha ingeendelea baada ya kifo chake. Aliwaagiza wafuasi wake wafanye kazi ya kuhubiri na kufundisha. Kazi hiyo itazungumziwa katika sura inayofuata.
a Kwa mfano, mwanamke huyo anapotaka kujua kwa nini Myahudi anazungumza na Msamaria, anataja ugomvi ambao umekuwako kwa karne nyingi kati ya watu wa jamii hizo mbili. (Yohana 4:9) Pia, anakazia kwamba wao ni wazao wa Yakobo, jambo ambalo Wayahudi wa wakati huo wanapinga vikali. (Yohana 4:12) Wayahudi wanawaita Wasamaria, Wakutha, ili kukazia kwamba wametokana na jamii ya kigeni.
b Kuhubiri ni kutangaza au kueneza habari fulani. Kufundisha kuna maana hiyo pia, lakini kunatia ndani kueleza habari kwa mapana na marefu. Kufundisha kuzuri kunahusisha kutafuta njia za kufikia mioyo ili kuwachochea wanafunzi kutenda mambo wanayosikia.
c Kuhusiana na mstari huo, kitabu kimoja kinasema: “Nafaka zinapoiva, rangi yake ya kijani hubadilika kuwa manjano, kuonyesha kwamba ziko tayari kuvunwa.”
-
-
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 9
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”
Mkulima anaweza kufanya nini ikiwa mazao ni mengi sana na hawezi kuyakusanya akiwa peke yake?
1-3. (a) Mkulima anafanya nini mazao yanapokuwa mengi sana hivi kwamba hawezi kuyavuna akiwa peke yake? (b) Yesu anakabili tatizo gani mwaka wa 33 W.K., naye analishughulikia jinsi gani?
MKULIMA ana tatizo kubwa. Miezi michache mapema alilima mashamba yake na kupanda mbegu. Alifurahia kuona mimea ya kwanza ikichipuka, naye akashangilia kuona ikikomaa. Sasa, kazi ngumu aliyofanya inazaa matunda kwa maana wakati wa mavuno umefika. Lakini ana tatizo hili: Mazao ni mengi sana hivi kwamba hawezi kuyavuna akiwa peke yake. Ili kutatua tatizo hilo, kwa hekima anaamua kutafuta wafanyakazi na kuwatuma katika mashamba yake. Ana muda mfupi wa kuvuna mazao yake yenye thamani.
2 Yesu anakabili tatizo kama hilo mwaka wa 33 W.K., baada ya kufufuliwa. Wakati wa huduma yake duniani, alipanda mbegu za ile kweli. Sasa, mavuno yanahitaji kukusanywa, na mazao ni mengi. Watu wengi wanaopendezwa wanahitaji kukusanywa ili wawe wanafunzi. (Yohana 4:35-38) Yesu anashughulikia tatizo hilo jinsi gani? Akiwa mlimani huko Galilaya, muda mfupi kabla ya kwenda mbinguni, Yesu anaamuru wanafunzi wake watafute wanafunzi zaidi, anaposema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20.
3 Kazi hiyo ndilo jambo la msingi linaloonyesha maana ya kuwa mfuasi wa kweli wa Kristo. Hivyo basi, acheni tuchunguze maswali matatu. Kwa nini Yesu aliamuru wafanyakazi zaidi watafutwe? Aliwazoeza wanafunzi wake jinsi gani kuwatafuta? Ni kwa njia gani tunahusika katika kazi hiyo?
Kwa Nini Wafanyakazi Zaidi Walihitajiwa?
4, 5. Kwa nini Yesu hangeweza kumaliza kazi aliyokuwa ameanzisha, na ni nani ambao wangehitaji kuendeleza kazi hiyo baada ya yeye kurudi mbinguni?
4 Yesu alipoanza huduma yake mwaka wa 29 W.K., alijua kwamba anaanzisha kazi ambayo hangeweza kuimaliza mwenyewe. Kwa kuwa muda ambao angekaa duniani ulikuwa mfupi, hangeweza kuhubiri maeneo yote wala kumweleza kila mtu ujumbe wa Ufalme. Ni kweli kwamba aliwahubiria hasa Wayahudi na wageuzwa-imani, “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 15:24) Hata hivyo, ‘kondoo hao waliopotea’ walikuwa wametawanyika kotekote Israeli, nchi yenye ukubwa wa maelfu ya kilomita. Isitoshe, mwishowe habari njema ilipaswa kuhubiriwa katika ulimwengu mzima.—Mathayo 13:38; 24:14.
5 Yesu alitambua kwamba bado kazi kubwa ingehitaji kufanywa baada ya kifo chake. Aliwaambia hivi mitume wake 11 waaminifu: “Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, Yule anayeniamini, huyo pia atafanya kazi ambazo mimi hufanya; naye atafanya kazi kubwa kuliko hizi, kwa sababu ninaenda kwa Baba.” (Yohana 14:12) Kwa kuwa Mwana alikuwa akirudi mbinguni, wafuasi wake—si mitume tu bali pia wale ambao baadaye wangekuwa wanafunzi wake—walipaswa kuendeleza kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Yohana 17:20) Yesu alikubali kwa unyenyekevu kwamba wangefanya kazi “kubwa kuliko” zake. Jinsi gani? Katika njia tatu.
6, 7. (a) Ni katika njia gani wafuasi wa Yesu wangefanya kazi kubwa kuliko zake? (b) Tunaweza kuonyesha namna gani kwamba Yesu hakukosea kwa kuwatumaini wafuasi wake?
6 Kwanza, wafuasi wa Yesu wangehubiri eneo kubwa zaidi. Leo, kazi yao ya kutoa ushahidi imefika miisho ya dunia, mbali na mipaka ya nchi ambayo Yesu alihubiri. Pili, wangewahubiria watu wengi zaidi. Kikundi kidogo cha wanafunzi ambao Yesu aliacha duniani kiliongezeka haraka na kuwa maelfu ya watu. (Matendo 2:41; 4:4) Sasa, wamekuwa mamilioni, na mamia ya maelfu ya wapya wanabatizwa kila mwaka. Tatu, wangehubiri kwa muda mrefu zaidi. Wamehubiri mpaka leo hii, yapata miaka 2,000 tangu huduma ya Yesu ya miaka mitatu na nusu ilipomalizika.
7 Yesu alionyesha kwamba anawatumaini wafuasi wake aliposema kwamba wangefanya “kazi kubwa kuliko hizi.” Aliwapa kazi iliyokuwa ya maana zaidi kwake, kazi ya kuhubiri na kufundisha “habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Aliamini kwamba watatimiza mgawo wao kwa uaminifu. Hilo linamaanisha nini kwetu leo? Tunaposhiriki katika huduma kwa bidii na kwa moyo wote, tunaonyesha kwamba Yesu hakukosea kwa kuwatumaini wafuasi wake. Je, hilo si pendeleo la pekee?—Luka 13:24.
Walizoezwa Kutoa Ushahidi
Upendo unatuchochea kuhubiri popote ambapo watu wanapatikana
8, 9. Yesu alituwekea mfano gani katika huduma, nasi tunaweza kuufuata jinsi gani?
8 Yesu aliwapa wanafunzi wake mazoezi mazuri kwa ajili ya huduma. Isitoshe, aliwawekea mfano mzuri. (Luka 6:40) Katika sura iliyotangulia, tulizungumzia jinsi alivyoiona huduma. Kwa mfano, wafikirie wanafunzi waliokuwa wakitembea pamoja na Yesu katika safari zake za kuhubiri. Waliona kwamba alihubiri popote ambapo watu walipatikana—kando ya maziwa na kwenye milima, katika majiji na masoko, na katika nyumba za watu. (Mathayo 5:1, 2; Luka 5:1-3; 8:1; 19:5, 6) Waliona kwamba alikuwa mwenye bidii, akiamka mapema na kufanya kazi mpaka usiku sana. Hakushiriki katika huduma ili kupisha wakati tu! (Luka 21:37, 38; Yohana 5:17) Haikosi walitambua kwamba alifanya hivyo kwa sababu aliwapenda sana watu. Huenda walipoutazama uso wake waliona huruma aliyokuwa nayo moyoni. (Marko 6:34) Unafikiri mfano wa Yesu uliwasaidia wanafunzi wake kwa njia gani? Mfano huo ungekufaidi wewe kwa njia gani?
9 Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunafuata mfano wake katika huduma yetu. Kwa hiyo, tunafanya kila tuwezalo kutoa “ushahidi kamili.” (Matendo 10:42) Kama alivyofanya Yesu, tunawatembelea watu nyumbani kwao. (Matendo 5:42) Tunabadili mipango yetu, ikihitajika, ili tuwatembelee wakati wanapokuwa nyumbani. Pia, tunawatafuta na kuwahubiria watu kwa busara katika sehemu ambazo watu wanapatikana—barabarani, bustanini, madukani, na kazini. Tunaendelea ‘kufanya kazi kwa bidii na kujikaza wenyewe’ katika huduma, kwa sababu tunachukua kwa uzito kazi hiyo. (1 Timotheo 4:10) Kuwapenda watu sana kutoka moyoni kunatuchochea kuendelea kutafuta nafasi za kuhubiri mahali popote na wakati wowote ambapo watu wanaweza kupatikana.—1 Wathesalonike 2:8.
“Wale 70 wakarudi wakiwa na shangwe”
10-12. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake mambo gani kabla ya kuwatuma kuhubiri?
10 Pia, Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kuwapa maagizo kamili. Kabla ya kuwatuma wale mitume 12 na baadaye wale wanafunzi 70 kwenda kuhubiri, Yesu alitumia pindi mbalimbali kuwazoeza. (Mathayo 10:1-15; Luka 10:1-12) Mazoezi hayo yalikuwa na matokeo mazuri, kwa kuwa andiko la Luka 10:17 linasema: “Wale 70 wakarudi wakiwa na shangwe.” Acheni tuchunguze mambo mawili ya maana ambayo Yesu alifundisha. Tunapofanya hivyo, tusisahau desturi za Wayahudi wa nyakati za Biblia zilizokuwako wakati Yesu alipofundisha mambo hayo.
11 Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kumtegemea Yehova. Aliwaambia: “Msichukue dhahabu wala fedha wala shaba kwa ajili ya mikoba yenu ya mshipi, wala mfuko wa chakula kwa ajili ya safari, wala mavazi mawili ya ndani, wala viatu wala fimbo; kwa maana mfanyakazi anastahili chakula chake.” (Mathayo 10:9, 10) Ilikuwa kawaida kwa wasafiri kuchukua mkoba wa mshipi wa kubebea pesa, mfuko wa chakula, na viatu vya ziada.a Kwa kuwafundisha wanafunzi wake wasihangaikie mambo hayo, ni kana kwamba Yesu aliwaambia: “Mtegemeeni Yehova kabisa, kwa maana atatosheleza mahitaji yenu.” Yehova angefanya hivyo kwa kuwachochea wale ambao wangekubali habari njema waonyeshe ukarimu, kama ilivyokuwa desturi huko Israeli.—Luka 22:35.
12 Pia, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kuepuka mambo yasiyo ya lazima ambayo yangewakengeusha. Alisema hivi: “Msimkumbatie mtu yeyote mkimsalimu barabarani.” (Luka 10:4) Je, Yesu alikuwa akiwaambia wasipendezwe na watu wala kuwa wachangamfu? Hapana! Katika nyakati za Biblia, mara nyingi salamu zilitia ndani mambo mengi. Kwa kawaida, salamu zilitia ndani desturi fulani pamoja na mazungumzo marefu. Mtaalamu mmoja wa Biblia anasema: “Watu wa Mashariki hawakusalimiana kama tunavyofanya, yaani, kwa kuinama kidogo, au kwa kupeana mkono, bali walikumbatiana mara nyingi na kuinamisha kichwa na hata kusujudu. Yote hayo yalihitaji wakati mwingi.” Kwa kuwaambia wanafunzi wake wasisalimiane kulingana na desturi hizo, ni kana kwamba Yesu aliwaambia: “Mnapaswa kutumia wakati wenu vizuri kwa maana ujumbe mlio nao ni wa haraka.”b
13. Tunaweza kuonyesha namna gani kwamba tunatii maagizo ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake wa karne ya kwanza?
13 Tunatii maagizo ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake wa karne ya kwanza. Tunapotimiza huduma yetu, tunamtegemea Yehova kabisa. (Methali 3:5, 6) Tunajua kwamba hatutakosa mambo ya lazima maishani ‘tukiendelea kuutafuta kwanza ufalme.’ (Mathayo 6:33) Ulimwenguni pote, wahubiri wa Ufalme wa wakati wote wamejionea kwamba hata katika hali ngumu, mkono wa Yehova si mfupi. (Zaburi 37:25) Pia, tunatambua kwamba tunahitaji kuepuka mambo yanayoweza kutukengeusha. Tusipokuwa waangalifu, mfumo huu wa mambo unaweza kutukengeusha kwa urahisi. (Luka 21:34-36) Hata hivyo, huu si wakati wa kukengeushwa. Kwa kuwa maisha ya watu yako hatarini, ujumbe wetu ni wa haraka. (Waroma 10:13-15) Tukiendelea kutambua kwamba kazi yetu inahitaji kufanywa haraka, hatutaruhusu mambo ya ulimwengu huu yanayoweza kutukengeusha yachukue wakati na nguvu ambazo tungetumia katika huduma. Kumbuka kwamba wakati unaobaki ni mfupi na mavuno ni mengi.—Mathayo 9:37, 38.
Mgawo Unaotuhusu
14. Ni nini kinachoonyesha kwamba mgawo ulio kwenye Mathayo 28:18-20 unawahusu wafuasi wote wa Kristo? (Ona pia maelezo ya chini.)
14 Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwapa wafuasi wake daraka zito aliposema “Nendeni mkafanye wanafunzi.” Maneno hayo hayakuwahusu tu wanafunzi waliokuwa mlimani huko Galilaya.c Kazi ambayo Yesu aliagiza ifanywe inatia ndani kuwafikia “watu wa mataifa yote,” nayo itaendelea “mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Bila shaka, mgawo huo unawahusu wafuasi wote wa Kristo, kutia ndani sisi leo. Basi acheni tuchunguze maneno ya Yesu kwenye Mathayo 28:18-20.
15. Kwa nini tunapaswa kutii amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi?
15 Kabla ya kuwapa mgawo huo, Yesu anasema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mstari wa 18) Je, kweli Yesu ana mamlaka kubwa hivyo? Bila shaka! Yeye ndiye malaika mkuu, mwenye mamlaka juu ya maelfu mengi ya malaika. (1 Wathesalonike 4:16; Ufunuo 12:7) Akiwa “kichwa cha kutaniko,” ana mamlaka juu ya wafuasi wake walio duniani. (Waefeso 5:23) Tangu mwaka wa 1914, amekuwa akitawala akiwa Mfalme wa Kimasihi mbinguni. (Ufunuo 11:15) Mamlaka yake inafika hata kaburini, kwa kuwa ana uwezo wa kuwafufua wafu. (Yohana 5:26-28) Kwa kutangaza kwanza mamlaka yake kubwa, Yesu anaonyesha kwamba maneno anayosema baadaye katika mstari wa 19 na 20, ni amri lakini si pendekezo. Tunapaswa kumtii, kwa kuwa hakujichukulia mamlaka, bali alipewa na Mungu.—1 Wakorintho 15:27.
16. Anapotuambia “nendeni,” Yesu anatuamuru tufanye nini, nasi tunatimiza sehemu hiyo ya mgawo huo namna gani?
16 Sasa Yesu anataja mgawo wenyewe ambao unaanza kwa neno moja: “Nendeni.” (Mstari wa 19) Hivyo, anatuamuru tuchukue hatua ya kuwaeleza wengine ujumbe wa Ufalme. Ili kutimiza sehemu hiyo ya mgawo huo, tunaweza kutumia njia mbalimbali. Kuhubiri nyumba kwa nyumba ni njia nzuri zaidi ya kuongea na watu binafsi. (Matendo 20:20) Pia, tunatafuta nafasi za kuhubiri hata wakati ambapo hatukupangia; tunapofanya shughuli zetu za kila siku tunajaribu kuanzisha mazungumzo kuhusu habari njema mahali popote inapowezekana. Huenda njia zetu za kuhubiri zikatofautiana, kwa kuwa tunazibadili kulingana na mahitaji na hali za watu wa eneo letu. Hata hivyo, kuna jambo moja lisilobadilika: ‘Tunaenda’ kuwatafuta wanaostahili.—Mathayo 10:11.
17. Tunaweza ‘kufanya wanafunzi’ jinsi gani?
17 Kisha, Yesu anaeleza kusudi la mgawo huo, yaani, ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mstari wa 19) Tunaweza ‘kufanya wanafunzi’ jinsi gani? Kwa kawaida mwanafunzi ni mtu anayejifunza, au anayefundishwa. Hata hivyo, kufanya wanafunzi si kuwaelimisha tu watu. Tunapojifunza Biblia pamoja na watu wanaopendezwa, kusudi letu ni kuwasaidia wawe wafuasi wa Kristo. Wakati wowote inapowezekana, tunakazia mfano wa Yesu ili wanafunzi wetu wajifunze kumwona kuwa Mwalimu wao na Kielelezo chao, wakiishi kama alivyoishi na kufanya kazi aliyoifanya.—Yohana 13:15.
18. Kwa nini ubatizo ndiyo hatua ya maana zaidi katika maisha ya mwanafunzi?
18 Maneno yafuatayo yanaonyesha jambo la maana katika mgawo huo: “Mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mstari wa 19) Ubatizo ndiyo hatua ya maana zaidi katika maisha ya mwanafunzi, kwa kuwa inaonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Mungu kwa moyo wote. Hivyo basi, ubatizo ni hatua ya maana ili kupata wokovu. (1 Petro 3:21) Mwanafunzi aliyebatizwa akiendelea kufanya awezavyo kumtumikia Yehova, anaweza kutazamia kupata baraka milele katika ulimwengu mpya unaokuja. Je, umepata kumsaidia mtu fulani awe mwanafunzi aliyebatizwa wa Kristo? Hakuna jambo lingine katika huduma ya Kikristo linaloleta shangwe nyingi kama hilo.—3 Yohana 4.
19. Sisi tunawafundisha wapya nini, na kwa nini huenda tukahitaji kuendelea kuwafundisha baada ya ubatizo wao?
19 Yesu anaeleza sehemu inayofuata ya mgawo huo, anaposema: “Kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mstari wa 20) Tunawafundisha wapya kutii amri za Yesu, kutia ndani amri ya kumpenda Mungu, kumpenda jirani, na kufanya wanafunzi. (Mathayo 22:37-39) Hatua kwa hatua, tunawafundisha kuwaeleza wengine kweli za Biblia na kutetea imani yao inayoongezeka. Wanapostahili kuhubiri pamoja na kutaniko, tunahubiri pamoja nao na kuwafundisha kwa maneno na mfano wetu jinsi wanavyoweza kupata matokeo katika kazi hiyo. Wanafunzi wapya wanaweza kuendelea kufundishwa hata baada ya kubatizwa. Huenda wale waliobatizwa karibuni wakahitaji kufundishwa zaidi ili wakabiliane na hali ngumu wanazoweza kupata wanapomfuata Kristo.—Luka 9:23, 24.
“Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote”
20, 21. (a) Kwa nini hatupaswi kuogopa tunapotimiza mgawo tuliopewa na Yesu? (b) Kwa nini huu si wakati wa kupunguza mwendo, nasi tunapaswa kuazimia kufanya nini?
20 Maneno haya ya mwisho ya mgawo wa Yesu yanatoa uhakikisho mkubwa: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20) Yesu anatambua kwamba mgawo huo si mchezo. Pia, anajua kwamba nyakati nyingine kuutimiza kutafanya tuchukiwe na wanaotupinga. (Luka 21:12) Hata hivyo, hatupaswi kuogopa. Kiongozi wetu hatazamii tutimize mgawo huo bila msaada au tukiwa peke yetu. Je, haifariji kujua kwamba Yule aliye na “mamlaka yote mbinguni na duniani” yupo pamoja nasi kututegemeza tunapotimiza mgawo huo?
21 Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba atakuwa pamoja nao katika huduma yao sikuzote “mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Kabla ya mwisho kuja, lazima tuendelee kutimiza mgawo tuliopewa na Yesu. Huu si wakati wa kupunguza mwendo. Kazi kubwa ya mavuno ya kiroho inaendelea! Watu wanaopendezwa wanakusanywa kwa wingi. Tukiwa wafuasi wa Kristo, na tuazimie kutimiza mgawo wa maana tuliopewa. Na tuazimie kutumia wakati wetu, nguvu zetu, na mali zetu kutimiza amri hii ya Kristo: “Nendeni mkafanye wanafunzi.”
a Huenda mkoba wa mshipi ulikuwa aina ya mshipi uliotumiwa kubebea sarafu za pesa. Mfuko wa chakula ulikuwa mkubwa zaidi na kwa kawaida ulitengenezwa kwa ngozi, nao ulibebwa begani na ulitumiwa kubebea chakula au vitu vingine vya lazima.
b Wakati fulani, nabii Elisha alitoa maagizo kama hayo. Alipokuwa akimtuma mtumishi wake Gehazi kwenye nyumba ya mwanamke aliyefiwa na mwana wake, Elisha alisema: “Ukikutana na yeyote, usimsalimu.” (2 Wafalme 4:29) Mgawo huo ulihitaji kufanywa haraka, kwa hiyo hakupaswa kupoteza wakati.
c Kwa kuwa wengi wa wafuasi wake walikuwa Galilaya, huenda pindi inayotajwa katika Mathayo 28:16-20 ndiyo ile ambayo Yesu aliwatokea “ndugu zaidi ya mia tano” baada ya kufufuliwa. (1 Wakorintho 15:6) Kwa hiyo, huenda mamia ya watu walikuwapo wakati Yesu alipowapa kazi ya kufanya wanafunzi.
-
-
“Imeandikwa”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 10
“Imeandikwa”
“Leo andiko hili . . . limetimizwa”
1-3. Yesu anawataka watu wa Nazareti watambue jambo gani, naye anatoa uthibitisho gani?
NI MAPEMA katika huduma ya Yesu. Amerudi Nazareti, mji wa nyumbani. Anakusudia kuwasaidia watu watambue jambo hili: Yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa tangu zamani za kale! Anatoa uthibitisho gani?
2 Haikosi wengi wangetazamia afanye muujiza. Wamesikia mambo ya ajabu ambayo Yesu amefanya. Hata hivyo, hatoi ishara yoyote ya aina hiyo. Badala yake, anaingia katika sinagogi kama ilivyo desturi yake. Anasimama ili asome, naye anapewa kitabu cha kukunjwa cha Isaya. Ni kitabu kirefu ambacho inaelekea kimekunjwa katika vijiti viwili, naye Yesu anakikunjua kwa makini kutoka upande mmoja hadi mwingine mpaka anapopata fungu la maneno anayotafuta. Kisha anasoma kwa sauti maneno ambayo sasa yanapatikana katika Isaya 61:1-3.—Luka 4:16-19.
3 Lazima wasikilizaji hao wawe wanayajua maneno hayo. Ni unabii kumhusu Masihi. Kila mtu katika sinagogi anamkazia Yesu macho. Kumetulia tuli. Kisha, Yesu anaanza kufafanua waziwazi: “Leo andiko hili ambalo mmesikia sasa hivi limetimizwa.” Wasikilizaji wanastaajabia maneno yake yenye kuvutia sana, lakini inaonekana kwamba bado wengi wanataka kuona ishara fulani ya pekee. Hata hivyo, kwa uhodari Yesu anatumia mfano wa Kimaandiko kufunua ukosefu wao wa imani. Muda si muda, watu wa Nazareti wanajaribu kumuua!—Luka 4:20-30.
4. Yesu alituwekea mfano gani katika huduma yake, nasi tutachunguza nini katika sura hii?
4 Katika kisa hicho, Yesu alifanya jambo ambalo aliendelea kufanya katika huduma yake yote. Alitegemea sana Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Ni kweli, miujiza yake ilisaidia sana kuthibitisha kwamba roho ya Mungu ilikuwa pamoja naye. Hata hivyo, hakuna chochote machoni pa Yesu kilichokuwa cha maana kuliko Maandiko Matakatifu. Acheni tuchunguze mfano aliotuwekea kuhusu jambo hilo. Tutaona jinsi Bwana wetu alivyonukuu Neno la Mungu, alivyolitetea Neno la Mungu, na kulifafanua Neno la Mungu.
Kunukuu Neno la Mungu
5. Yesu aliazimia kuwajulisha wasikilizaji wake nini, naye alithibitisha ukweli wa maneno yake jinsi gani?
5 Yesu alitaka watu wajue chanzo cha ujumbe wake. Alisema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Pindi nyingine, alisema: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yohana 8:28) Pia, alisema: “Mambo ninayowaambia ninyi sisemi kwa kujitungia mwenyewe; bali Baba ambaye hukaa katika muungano pamoja nami anafanya kazi zake.” (Yohana 14:10) Njia moja ambayo Yesu alithibitisha ukweli wa maneno hayo ni kwa kunukuu tena na tena Neno la Mungu lililoandikwa.
6, 7. (a) Yesu alinukuu Maandiko ya Kiebrania kadiri gani, na kwa nini hilo ni jambo lenye kupendeza? (b) Kuna tofauti gani kati ya njia ya Yesu ya kufundisha na ya waandishi?
6 Kuyachunguza kwa makini maneno ya Yesu yaliyoandikwa kunafunua kwamba alinukuu moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja zaidi ya nusu ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania vinavyokubalika. Huenda hilo lisionekane kuwa jambo la ajabu. Labda unaweza kujiuliza, katika kazi yake ya kufundisha na kuhubiri hadharani, aliyofanya kwa miaka mitatu na nusu, kwa nini hakunukuu vitabu vyote vilivyoongozwa na roho vilivyokuwako? Kwa kweli, huenda alifanya hivyo. Kumbuka kwamba sehemu ndogo tu ya maneno na matendo ya Yesu ndiyo iliyoandikwa. (Yohana 21:25) Hata unaweza kutumia saa chache tu kusoma kwa sauti maneno yote ya Yesu yaliyoandikwa. Sasa, wazia kwamba unazungumza kumhusu Mungu na Ufalme wake kwa saa chache na kwa kipindi hicho kifupi unukuu zaidi ya nusu ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania! Isitoshe, mara nyingi Yesu hakuwa na vitabu vya kukunjwa. Wakati wa Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, alinukuu moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja Maandiko mengi ya Kiebrania kutoka katika kumbukumbu yake!
7 Manukuu ya Yesu yanaonyesha kwamba aliheshimu sana Neno la Mungu. Wasikilizaji wake ‘walistaajabia njia yake ya kufundisha, kwa maana huko alikuwa akiwafundisha kama mwenye mamlaka, na si kama waandishi.’ (Marko 1:22) Waandishi walipofundisha, walipenda kutaja sheria ya mdomo, wakiwanukuu marabi wenye elimu wa nyakati zilizopita. Yesu hakunukuu sheria ya mdomo wala kuwanukuu marabi fulani. Badala yake, aliliona Neno la Mungu kuwa lenye mamlaka kuu. Tena na tena, alitumia usemi, “Imeandikwa,” au maneno mengine kama hayo alipokuwa akiwafundisha wafuasi wake na alipokuwa akisahihisha maoni yasiyofaa.
8, 9. (a) Yesu alitetea jinsi gani mamlaka ya Neno la Mungu aliposafisha hekalu? (b) Ni kwa njia gani viongozi wa dini walilivunjia Neno la Mungu heshima hekaluni?
8 Yesu aliposafisha hekalu huko Yerusalemu, alisema: “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala,’ lakini ninyi mnaifanya kuwa pango la wanyang’anyi.” (Mathayo 21:12, 13; Isaya 56:7; Yeremia 7:11) Siku iliyotangulia alikuwa amefanya kazi nyingi za ajabu humo. Wavulana wachanga waliovutiwa sana walianza kumsifu. Hata hivyo, viongozi wa dini walimuuliza Yesu kwa ghadhabu iwapo amesikia mambo ambayo watoto hao wanasema. Alijibu: “Ndiyo. Je, ninyi hamkusoma hili kamwe, ‘Kutoka katika kinywa cha watoto na wanaonyonya umetoa sifa’?” (Mathayo 21:16; Zaburi 8:2) Yesu alitaka watu hao wajue kwamba jambo lililokuwa likitendeka linapatana na Neno la Mungu.
9 Viongozi hao wa dini baadaye walikutana, kisha wakamkabili Yesu wakiuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani?” (Mathayo 21:23) Yesu alikuwa ametaja wazi kabisa Chanzo cha mamlaka yake. Hakuwa amejitungia wala kubuni mafundisho mapya. Alitumia tu mambo ambayo Neno la Baba yake lililoongozwa na roho linasema. Hivyo basi, makuhani na waandishi hao walikuwa wakimvunjia Yehova heshima na Neno lake. Walistahili kabisa kushutumiwa na Yesu alipofunua nia zao mbovu.—Mathayo 21:23-46.
10. Ni kwa njia gani tunaweza kuiga jinsi Yesu alivyolitumia Neno la Mungu, nasi tuna vifaa gani ambavyo Yesu hakuwa navyo?
10 Kama Yesu, Wakristo wa kweli leo wanalitegemea Neno la Mungu katika huduma. Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa bidii yao ya kuwahubiria wengine ujumbe wa Biblia. Vichapo vyetu vinanukuu na kutaja sana Biblia. Nasi pia tunafanya hivyo katika huduma yetu kwa kuhakikisha kwamba tunayatumia Maandiko kila wakati tunapozungumza na watu. (2 Timotheo 3:16) Tunafurahi kama nini mtu anapoturuhusu tuisome Biblia na kuzungumzia faida na maana ya Neno la Mungu! Ingawa hatuwezi kukumbuka mambo kikamili kama alivyofanya Yesu, tuna vifaa vingi ambavyo Yesu hakuwa navyo. Mbali na Biblia nzima inayoendelea kuchapishwa katika lugha nyingi zaidi, tuna vichapo vingi vya Biblia vinavyotusaidia kupata mstari wowote ambao huenda tukatafuta. Na tuazimie kuendelea kuinukuu Biblia na kuwaelekeza watu katika Biblia nyakati zote!
Kulitetea Neno la Mungu
11. Kwa nini Yesu alihitaji kulitetea Neno la Mungu mara nyingi?
11 Yesu aliona kwamba Neno la Mungu lilishambuliwa mara nyingi, hata hivyo, hilo halikumshangaza. Alipokuwa akisali, Yesu alimwambia hivi Baba yake: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Yesu alijua vizuri kwamba Shetani, “mtawala wa ulimwengu,” ni “mwongo na ndiye baba ya uwongo.” (Yohana 8:44; 14:30) Akivipinga vishawishi vya Shetani, Yesu aliyanukuu Maandiko mara tatu. Shetani alinukuu mstari mmoja kutoka Zaburi, akiupotosha kimakusudi, naye Yesu akamjibu kwa kulitetea Neno la Mungu lisitumiwe vibaya.—Mathayo 4:6, 7.
12-14. (a) Ni kwa njia gani viongozi wa dini walionyesha kwamba hawaiheshimu Sheria ya Musa? (b) Yesu alilitetea Neno la Mungu jinsi gani?
12 Yesu alitetea mara nyingi Maandiko Matakatifu yasitumiwe vibaya au kupotoshwa. Walimu wa dini wa siku zake walilipotosha Neno la Mungu. Walikazia sana kufuata mambo madogo zaidi ya Sheria ya Musa lakini hawakukazia kanuni zilizotegemeza sheria hizo. Kwa kufanya hivyo, ibada ikawa ya kijuujuu tu, na watu wakahangaikia mambo yenye kuonekana na wanadamu badala ya mambo mazito zaidi, kama vile haki, rehema, na uaminifu. (Mathayo 23:23) Yesu aliitetea Sheria ya Mungu jinsi gani?
13 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitumia tena na tena maneno “mlisikia kwamba ilisemwa” kabla ya kutaja amri iliyo katika Sheria ya Musa. Kisha, alikuwa akisema “lakini mimi ninawaambia ninyi” halafu angeeleza kanuni iliyokazia mambo mazito zaidi kuliko tu kushika Sheria kijuujuu. Je, alikuwa akiipinga Sheria? Hapana, alikuwa akiitetea. Kwa mfano, watu waliijua vizuri ile amri “Usiue.” Lakini Yesu aliwaambia kwamba kumchukia mtu ni kuvunja kanuni ya sheria hiyo. Vivyo hivyo, kukuza tamaa kuelekea mtu ambaye si mwenzi wako ni kuvunja kanuni inayotegemeza sheria ya Mungu inayokataza uzinzi.—Mathayo 5:17, 18, 21, 22, 27-39.
14 Mwishowe, Yesu alisema: “Mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Mpende jirani yako na kumchukia adui yako.’ Hata hivyo, mimi ninawaambia ninyi: Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” (Mathayo 5:43, 44) Je, amri inayosema ‘mchukie adui yako’ ilikuwa katika Neno la Mungu? Hapana, hilo lilikuwa fundisho ambalo viongozi wa dini walibuni. Waliidhoofisha Sheria kamilifu ya Mungu kwa mawazo ya wanadamu. Bila woga, Yesu alitetea Neno la Mungu lisiathiriwe na mapokeo ya wanadamu.—Marko 7:9-13.
15. Sheria ya Mungu ilipofanywa ionekane kuwa yenye kudai mno au yenye masharti magumu, Yesu aliitetea jinsi gani?
15 Pia, viongozi wa dini walishambulia Sheria ya Mungu kwa kuifanya ionekane kuwa inadai mno, au ina masharti magumu. Wanafunzi wa Yesu walipong’oa masuke ya nafaka walipokuwa wakipita katikati ya shamba, Mafarisayo fulani walidai kwamba wanafunzi hao wanaivunja sheria ya Sabato. Yesu alitumia mfano wa Kimaandiko kutetea Neno la Mungu dhidi ya maoni hayo yasiyofaa. Alirejelea Andiko moja tu linalozungumzia jinsi mkate wa wonyesho wa hekalu ulivyotumiwa nje ya patakatifu wakati Daudi na wanaume wake wenye njaa walipoula. Yesu aliwaonyesha Mafarisayo hao kwamba walikosa kuelewa kusudi la rehema na huruma za Yehova.—Marko 2:23-27.
16. Viongozi wa dini waliipotosha jinsi gani amri ya Musa kuhusu talaka, naye Yesu alisema nini?
16 Pia, viongozi wa dini walibuni njia za kisheria za kuikwepa Sheria ya Mungu. Kwa mfano, Sheria ilimruhusu mtu kumtaliki mke wake ikiwa angeona “kitu fulani kisichofaa” kwake, pengine tatizo zito lililoiletea aibu nyumba yake. (Kumbukumbu la Torati 24:1) Hata hivyo, kufikia siku za Yesu, viongozi wa dini walitumia sheria hiyo kuwa udhuru wa kumruhusu mwanamume kumtaliki mke wake kwa kila sababu, hata kwa kuunguza chakula!a Yesu alionyesha kwamba walikuwa wamepotosha sana maneno ya Musa yaliyoongozwa na roho. Kisha, akarudisha kiwango cha awali cha ndoa kilichowekwa na Yehova, yaani, kuwa na mke mmoja, na kuonyesha kwamba uzinzi ndio msingi pekee wa talaka.—Mathayo 19:3-12.
17. Wakristo wanaweza kumwiga Yesu jinsi gani wanapolitetea Neno la Mungu leo?
17 Vivyo hivyo, wafuasi wa Kristo leo wanaona ni lazima watetee Maandiko Matakatifu yasishambuliwe. Viongozi wa dini wanapodokeza kwamba viwango vya maadili vya Neno la Mungu vimepitwa na wakati, wanaishambulia Biblia. Pia, Biblia inashambuliwa wakati dini inapofundisha mafundisho ya uwongo na kuyafanya yaonekane kuwa yametoka katika Biblia. Tunaliona kuwa pendeleo kutetea Neno la Mungu la kweli lililo safi, kama vile tunapothibitisha kwamba Mungu si Utatu. (Kumbukumbu la Torati 4:39) Wakati huohuo, tunalitetea kwa busara, tukiwa na upole wa kweli na heshima nyingi.—1 Petro 3:15.
Kufafanua Neno la Mungu
18, 19. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yesu alikuwa na uwezo wa pekee wa kufafanua Neno la Mungu?
18 Yesu alikuwa mbinguni Maandiko ya Kiebrania yalipoandikwa. Haikosi alifurahi sana kupata pendeleo la kuja duniani kuwafundisha watu Neno la Mungu! Kwa mfano, fikiria ile siku isiyosahaulika alipokutana na wanafunzi wake wawili kwenye barabara ya kwenda Emau baada ya ufufuo wake. Kabla ya kumtambua, walimwambia jinsi walivyohuzunika na kuchanganyikiwa kwa sababu ya kifo cha Bwana wao mpendwa. Alifanya nini? “Akaanzia Musa na Manabii wote, akawafasiria mambo yanayomhusu yeye mwenyewe katika Maandiko yote.” Itikio lao lilikuwa nini? Baadaye waliambiana: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia Maandiko?”—Luka 24:15-32.
19 Baadaye siku hiyohiyo, Yesu alikutana na mitume wake na wengine. Ona kile alichowafanyia: “Akafungua akili zao ili kuifahamu maana ya Maandiko.” (Luka 24:45) Hapana shaka tukio hilo lenye kufurahisha liliwakumbusha zile pindi nyingi sana ambazo Yesu aliwafanyia jambo hilohilo, wao na wengine ambao walimsikiliza. Mara nyingi alinukuu maandiko yaliyojulikana sana na kuyaeleza kwa njia ambayo ilichochea sana akili za wasikilizaji wake hivi kwamba wakapata uelewaji mpya na wenye kina wa Neno la Mungu.
20, 21. Yesu alifafanua kwa njia gani maneno ambayo Yehova alimwambia Musa kwenye mti uliokuwa ukiwaka?
20 Pindi moja kama hiyo, Yesu alikuwa akizungumza na kikundi cha Masadukayo. Walikuwa kikundi cha makuhani Wayahudi ambao walijitenga na Dini ya Kiyahudi, nao hawakuamini ufufuo. Yesu aliwaambia: “Kwa habari ya ufufuo wa wafu, je, hamkusoma mliloambiwa na Mungu, akisema, ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo’? Yeye ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai.” (Mathayo 22:31, 32) Hilo ni andiko walilolielewa vizuri sana, ambalo liliandikwa na Musa, mtu ambaye Masadukayo walimheshimu sana. Hata hivyo, je, unaona jinsi maneno ya Yesu yalivyokuwa na matokeo?
21 Musa alizungumza na Yehova wapata mwaka wa 1514 K.W.K., kwenye mti uliokuwa ukiwaka. (Kutoka 3:2, 6) Kufikia wakati huo, miaka 329 ilikuwa imepita tangu Abrahamu afe, 224 tangu Isaka afe, na 197 tangu Yakobo afe. Hata hivyo, Yehova alisema: “Mimi ni” Mungu wao. Masadukayo hao walijua kwamba Yehova si kama mungu fulani wa kipagani wa wafu anayetawala ulimwengu wa wafu. Yeye ni Mungu wa “walio hai,” kama Yesu alivyosema. Hilo linamaanisha nini? Yesu alikata maneno kwa njia hii yenye kusadikisha: “Kwake, hao wote wako hai.” (Luka 20:38) Watumishi wapendwa wa Yehova ambao wamekufa wako salama katika kumbukumbu yake isiyo na mipaka na isiyoweza kufutika. Kusudi la Yehova la kuwafufua watu hao ni hakika sana hivi kwamba inaweza kusemwa wako hai. (Waroma 4:16, 17) Je, huo sio ufafanuzi wenye kupendeza wa Neno la Mungu? Basi, haishangazi kwamba ‘umati ulistaajabishwa’!—Mathayo 22:33.
22, 23. (a) Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani tunapolifafanua Neno la Mungu? (b) Tutachunguza nini katika sura inayofuata?
22 Leo, Wakristo wana pendeleo la kuiga jinsi Yesu alivyofafanua Neno la Mungu. Ingawa hatuna akili kamilifu, mara nyingi tunapata nafasi ya kuwaonyesha wengine andiko ambalo tayari wanalijua na kuwaeleza mambo fulani kulihusu ambayo huenda hata hawakuwa wameyafikiria hata kidogo. Kwa mfano, huenda wamekuwa wakirudia-rudia maneno “Jina lako litukuzwe” na “Ufalme wako uje” maisha yao yote, nao hata hawajui jina la Mungu au Ufalme wake ni nini. (Mathayo 6:9, 10, Union Version) Tunapata pendeleo kubwa kama nini mtu anapoturuhusu kufafanua kweli hizo za Biblia kwa njia rahisi iliyo wazi!
23 Kunukuu Neno la Mungu, kulitetea, na kulifafanua ni kati ya njia kuu za kuiga ufundi wa Yesu wa kuwafundisha wengine kweli. Tutachunguza njia fulani zenye matokeo ambazo Yesu alitumia kufikia mioyo ya wasikilizaji wake alipowafundisha kweli za Biblia.
a Baadaye, mwanahistoria wa karne ya kwanza Yosefo, Farisayo aliyekuwa ametalikiana na mke wake, alidokeza kwamba talaka iliruhusika “kwa sababu yoyote ile (na wanaume wanadai kwamba kuna sababu nyingi).”
-
-
“Mtu Mwingine Hajapata Kamwe Kusema Kama Huyu”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 11
“Mtu Mwingine Hajapata Kamwe Kusema Kama Huyu”
1, 2. (a) Kwa nini maofisa waliotumwa kumkamata Yesu walirudi mikono mitupu? (b) Ni nini kilichomfanya Yesu kuwa mwalimu wa pekee?
MAFARISAYO wamewaka hasira. Yesu yumo hekaluni akifundisha kumhusu Baba yake. Wanaomsikiliza wamegawanyika; wengi wanamwamini Yesu, lakini wengine wanataka akamatwe. Wakiwa wameshindwa kuzuia hasira yao, viongozi wa dini wanawatuma maofisa wakamkamate Yesu. Hata hivyo, maofisa hao wanarudi mikono mitupu. Wakuu wa makuhani na Mafarisayo wanauliza hivi kwa hasira: “Kwa nini hamkumleta?” Maofisa hao wanajibu: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” Walivutiwa sana na mafundisho ya Yesu hivi kwamba hawakuona sababu ya kumkamata.a—Yohana 7:45, 46.
2 Kuna wengine pia waliovutiwa na njia ya Yesu ya kufundisha. Watu walikusanyika kwa wingi kumsikiliza Yesu akifundisha. (Marko 3:7, 9; 4:1; Luka 5:1-3) Ni nini kilichomfanya Yesu kuwa mwalimu wa pekee? Kama tulivyoona katika Sura ya 8, alipenda kweli alizofundisha na aliwapenda watu aliowafundisha. Pia, alikuwa stadi wa kutumia njia mbalimbali za kufundisha. Na tuchunguze njia tatu zenye matokeo alizotumia na jinsi tunavyoweza kumwiga.
Alifundisha kwa Njia Rahisi
3, 4. (a) Kwa nini Yesu alitumia lugha ya kawaida alipofundisha? (b) Mahubiri ya Mlimani yanaonyeshaje jinsi Yesu alivyofundisha kwa njia rahisi?
3 Wazia maneno ambayo Yesu angeweza kutumia! Hata hivyo, alipokuwa akifundisha, hakutumia maneno magumu ambayo wasikilizaji wake hawangeweza kuelewa. Wengi wao walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Matendo 4:13) Kwa kuwa alijua mipaka yao, hakuwalemea kwa habari nyingi sana. (Yohana 16:12) Maneno yake yalikuwa rahisi, hata hivyo, kweli alizofundisha zilikuwa za maana sana.
4 Kwa mfano, fikiria yale Mahubiri ya Mlimani, yaliyo katika Mathayo 5:3–7:27. Mashauri ambayo Yesu anatoa katika mahubiri hayo si ya kijuujuu tu bali yanafikia kiini cha mambo. Hatumii hoja wala sentensi ngumu-ngumu. Ni vigumu kumsikia akitumia hata neno moja ambalo mtoto mdogo hawezi kulielewa kwa urahisi! Basi, si ajabu kwamba Yesu alipomaliza, umati—ambao yaelekea ulitia ndani wakulima, wachungaji, na wavuvi—‘ulishangazwa na njia yake ya kufundisha.’—Mathayo 7:28.
5. Toa mifano ya maneno yaliyosemwa na Yesu ambayo yalikuwa rahisi lakini yaliyojaa maana.
5 Alipofundisha, mara nyingi Yesu alitumia sentensi fupi zinazoeleweka kwa urahisi na kutumia maneno yaliyojaa maana. Nyakati hizo hakukuwa na vitabu vilivyochapishwa. Hivyo, kwa kutumia lugha ya kawaida, Yesu alikazia ujumbe wake katika akili na mioyo yao hivi kwamba hawangeweza kusahau. Fikiria mifano fulani: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe.” “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji.” “Roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”b (Mathayo 7:1; 9:12; 26:41; Marko 12:17; Matendo 20:35) Maneno hayo yangali yanakumbukwa karibu miaka 2,000 baadaye.
6, 7. (a) Ili tufundishe kwa njia rahisi, kwa nini tunapaswa kutumia lugha ya kawaida? (b) Tunaweza kufanya nini ili tusimlemee mwanafunzi wa Biblia kwa habari nyingi mno?
6 Tunaweza kutumia njia gani ili kufundisha kwa njia inayoeleweka kwa urahisi? Njia moja kuu ni kutumia lugha ya kawaida ambayo watu wengi wanaweza kuielewa kwa urahisi. Kweli za msingi za Neno la Mungu si ngumu. Yehova amewafunulia makusudi yake watu walio wanyoofu na wanyenyekevu moyoni. (1 Wakorintho 1:26-28) Maneno rahisi yaliyochaguliwa kwa uangalifu yanaweza kuwa na matokeo yanapotumiwa kujulisha kweli za Neno la Mungu.
Unapofundisha, tumia njia rahisi
7 Ili tufundishe kwa njia rahisi, tunapaswa kuwa waangalifu tusimlemee mwanafunzi wa Biblia kwa habari nyingi mno. Hivyo, tunapoongoza funzo la Biblia, si lazima tueleze kila jambo; wala hakuna haja ya kuzungumzia habari haraka-haraka kana kwamba jambo kuu ni kumaliza idadi fulani ya kurasa. Badala yake, ni jambo la hekima kuongoza funzo kulingana na mahitaji na uwezo wa mwanafunzi. Kusudi letu ni kumsaidia mwanafunzi awe mfuasi wa Kristo na mwabudu wa Yehova. Kwa hiyo, tunahitaji kutumia wakati unaohitajika ili mwanafunzi aelewe vizuri mambo anayojifunza. Kwa kufanya hivyo, ndipo tu kweli za Biblia zitaingia moyoni mwake na kumchochea atumie mambo ambayo amejifunza.—Waroma 12:2.
Kuuliza Maswali Yanayofaa
8, 9. (a) Kwa nini Yesu aliuliza maswali? (b) Yesu alitumia maswali jinsi gani kumsaidia Petro afikie kauli sahihi kuhusu kulipa kodi ya hekalu?
8 Yesu alitumia maswali sana, hata wakati ambapo ingemchukua muda mfupi zaidi kumweleza msikilizaji jambo fulani moja kwa moja. Kwa nini basi alitumia maswali? Nyakati nyingine, aliuliza maswali yenye kupenya ili afichue nia mbovu za waliokuwa wakimpinga na kuwanyamazisha. (Mathayo 21:23-27; 22:41-46) Hata hivyo, mara nyingi alitumia maswali ili wanafunzi wake wafunue mambo yaliyokuwa akilini mwao na ili achochee fikira zao na kuwazoeza kutumia akili zao. Hivyo, aliuliza maswali kama vile, “Mnaonaje?” na “Je, unaamini hilo?” (Mathayo 18:12; Yohana 11:26) Maswali ya Yesu yalifikia na kugusa mioyo ya wanafunzi wake. Fikiria mfano huu.
9 Wakati mmoja, wakusanya-kodi walimuuliza Petro ikiwa Yesu analipa kodi ya hekalu.c Bila kusita Petro alijibu, “Analipa.” Baadaye, Yesu alimuuliza: “Unaonaje, Simoni? Wafalme wa dunia hupokea ushuru au kodi ya kichwa kutoka kwa nani? Kutoka kwa wana wao au kutoka kwa wageni?” Petro akajibu: “Kutoka kwa wageni.” Kisha Yesu akasema: “Basi, kwa kweli wana hawalipi kodi.” (Mathayo 17:24-27) Bila shaka, Petro alitambua kusudi la maswali hayo, kwa kuwa watu wa familia za wafalme hawakulipa kodi. Hivyo basi, kwa sababu Yesu ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mfalme wa mbinguni aliyekuwa akiabudiwa hekaluni, hakuhitaji kulipa kodi. Ona kwamba badala ya kumwambia Petro jibu moja kwa moja, Yesu alitumia maswali kwa busara kumsaidia Petro afikie kauli sahihi na kuona uhitaji wa kufikiri kwa uangalifu kabla ya kujibu endapo hali kama hiyo itatokea tena.
Uliza maswali yanayopatana na hali za mwenye nyumba
10. Ni kwa njia gani tunaweza kutumia maswali kwa ustadi tunapohubiri nyumba kwa nyumba?
10 Ni kwa njia gani tunaweza kutumia maswali kwa ustadi katika huduma yetu? Tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kutumia maswali yanayoamsha upendezi ambayo huenda yakatufungulia njia ya kuhubiri habari njema. Kwa mfano, tukimkuta mzee tunapohubiri, tunaweza kumuuliza hivi kwa heshima, “Umeona mabadiliko gani ulimwenguni?” Baada ya kumruhusu ajibu, unaweza kumuuliza, “Unafikiri ni nini kinachoweza kufanya maisha yawe mazuri zaidi ulimwenguni?” (Mathayo 6:9, 10) Tukimkuta mama mwenye watoto wadogo, tunaweza kumuuliza, “Unafikiri ulimwengu huu utakuwa namna gani watoto wako watakapokuwa watu wazima?” (Zaburi 37:10, 11) Kuwa watambuzi tunapohubiri kutatuwezesha kuchagua swali linalopatana na hali za mwenye nyumba.
11. Ni kwa njia gani tunaweza kutumia maswali kwa ustadi tunapoongoza funzo la Biblia?
11 Ni kwa njia gani tunaweza kutumia maswali kwa ustadi tunapoongoza funzo la Biblia? Maswali yaliyochaguliwa vizuri yanaweza kutusaidia kutambua mambo yaliyo katika moyo wa mwanafunzi. (Methali 20:5) Kwa mfano, tuseme tunajifunza sura yenye kichwa “Kuishi Maisha Yanayompendeza Mungu” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?d Sura hiyo inazungumzia maoni ya Mungu kuhusu mambo kama vile uasherati, ulevi, na kusema uwongo. Huenda majibu ya mwanafunzi yakaonyesha kwamba anaelewa mambo ambayo Biblia inafundisha, lakini je, anakubaliana nayo? Tunaweza kumuuliza, “Je, unafikiri maoni ya Mungu kuhusu mambo hayo yanafaa?” Pia, tunaweza kumuuliza, “Unaweza kutumia habari hii maishani mwako jinsi gani?” Unapofanya hivyo, kumbuka kuwa mwenye busara na kumheshimu mwanafunzi. Hatungependa kuuliza maswali yanayoweza kumwaibisha.—Methali 12:18.
Kutoa Hoja Zenye Kusadikisha
12-14. (a) Yesu alitumia jinsi gani uwezo wake wa kutoa hoja zenye kusadikisha? (b) Yesu alitoa hoja gani yenye kusadikisha Mafarisayo walipodai kwamba anatumia nguvu za Shetani?
12 Akiwa na akili kamilifu, Yesu alikuwa stadi wa kutoa hoja zenye kusadikisha. Nyakati nyingine alitoa hoja zenye kusadikisha kukanusha mashtaka ya uwongo ya wale waliokuwa wakimpinga. Mara nyingi, alitumia hoja zenye kushawishi kuwafundisha wafuasi wake mafundisho ya maana. Acheni tuchunguze mifano fulani.
13 Baada ya Yesu kumponya mtu mwenye roho mwovu aliyekuwa kipofu na asiyeweza kuzungumza, Mafarisayo walimshutumu hivi: “Mtu huyu hatoi roho waovu ila kwa nguvu za Beelzebuli [Shetani], mtawala wa roho waovu.” Maneno yao yalionyesha walitambua kwamba nguvu zisizo za kawaida zilihitajiwa kuwatoa roho hao. Hata hivyo, walidai kwamba nguvu za Yesu zilitokana na Shetani. Shtaka hilo lilikuwa la uwongo na lisilopatana na akili. Akifunua maoni yao yenye kosa, Yesu alijibu: “Kila ufalme uliogawanyika na kupingana wenyewe unaangamia, na kila jiji au nyumba iliyogawanyika na kupingana yenyewe haitasimama. Vivyo hivyo, ikiwa Shetani anamfukuza Shetani, amegawanyika na kujipinga mwenyewe; basi, ufalme wake utasimamaje?” (Mathayo 12:22-26) Ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema: “Ikiwa ninamwakilisha Shetani, na ninaharibu kazi zake, basi Shetani anajipinga mwenyewe na muda si muda atashindwa.” Je, kweli wangeweza kukanusha hoja yenye kusadikisha kama hiyo?
14 Bado Yesu hakuwa amemaliza hoja zake. Akijua kwamba baadhi ya wanafunzi wa Mafarisayo hao walikuwa wamewatoa roho waovu, aliuliza swali rahisi lakini lenye kuchochea fikira: “Ikiwa mimi ninawafukuza roho waovu kwa nguvu za Beelzebuli, wana [au, wanafunzi] wenu wanawafukuza kwa nguvu za nani?” (Mathayo 12:27) Ni kana kwamba Yesu alikuwa akisema: “Ikiwa mimi ninawatoa roho waovu kwa nguvu za Shetani, basi wanafunzi wenu wanatumia nguvu hizohizo.” Mafarisayo hawakuwa na la kusema. Hawangeweza kukubali kwamba wanafunzi wao wanatumia nguvu za Shetani. Basi, Yesu alitumia mawazo yao yaliyopotoka ili wao wenyewe wakubali jambo ambalo hawakutaka. Je, haisisimui kusoma jinsi Yesu alivyowapa sababu zenye kusadikisha? Basi wazia jinsi umati uliomsikiliza Yesu moja kwa moja ulivyohisi, kwa kuwa sauti yake na kuwapo kwake kuliongeza uzito wa maneno yake.
15-17. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yesu alivyotumia maneno “hata zaidi” alipokuwa akifundisha kweli zenye kuchochea mioyo kumhusu Baba yake.
15 Pia, Yesu alitumia hoja zenye kusadikisha na zinazopatana na akili alipokuwa akifundisha kweli zenye kuchochea mioyo kumhusu Baba yake. Mara nyingi alifanya hivyo kwa kutumia maneno “hata zaidi” kuwasaidia wasikilizaji wake wasadiki zaidi kweli wanayoifahamu. Njia hiyo ya kutoa hoja kwa kulinganisha mambo inaweza kuchochea sana. Acheni tuchunguze mifano miwili tu.
16 Alipokuwa akijibu ombi la wanafunzi wake la kuwafundisha kusali, Yesu alieleza jinsi wazazi wa kibinadamu wasio wakamilifu wanavyowapa watoto wao “zawadi zilizo njema.” Kisha akasema: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:1-13) Yesu alitoa hoja yake kwa kulinganisha mambo. Ikiwa wazazi wenye dhambi wanawatimizia watoto wao mahitaji yao, Baba yetu wa mbinguni ambaye ni mkamilifu na mwadilifu katika mambo yote atawapa hata zaidi roho takatifu waabudu wake washikamanifu wanaomwomba kwa unyenyekevu!
17 Yesu alitumia njia kama hiyo alipotoa mashauri yenye hekima kuhusu jinsi ya kushughulika na mahangaiko. Alisema: “Kunguru hawapandi mbegu wala hawavuni, nao hawana bohari wala ghala, na bado Mungu huwalisha. Ninyi ni wenye thamani kama nini kuliko ndege? Angalieni jinsi mayungiyungi hukua; hayo hayafanyi kazi wala hayasokoti . . . Ikiwa, basi, Mungu huvika hivyo mimea iliyo shambani ambayo leo ipo na kesho hutupwa ndani ya jiko, basi atawavika ninyi hata zaidi, ninyi wenye imani kidogo!” (Luka 12:24, 27, 28) Ikiwa Yehova anatunza ndege na maua, atawatunza hata zaidi wanadamu wanaompenda na kumwabudu! Bila shaka, kwa kutumia njia hiyo yenye kuchochea fikira, Yesu alifikia mioyo ya wasikilizaji wake.
18, 19. Tunapozungumza na mtu anayedai kwamba hamwamini Mungu asiyeweza kumwona, tunaweza kutoa hoja zenye kumsadikisha jinsi gani?
18 Katika huduma yetu, tungependa kutumia hoja zenye kusadikisha kukanusha mafundisho ya uwongo na pia tunapofundisha kweli kumhusu Yehova. (Matendo 19:8; 28:23, 24) Je, tunahitaji kujifunza kutumia hoja ngumu? Sivyo hata kidogo. Jambo tunalojifunza kutoka kwa Yesu ni kwamba hoja zinazopatana na akili ambazo zinatolewa kwa njia rahisi zina matokeo zaidi.
19 Kwa mfano, tunaweza kumjibu namna gani mtu anayesema kwamba hamwamini Mungu asiyeweza kuonekana? Tunaweza kujadiliana naye kwa kutumia sheria ya asili ya kwamba kila tokeo lina kisababishi. Tunapoona tokeo, tunajua kwamba lazima kuwe na kisababishi. Tunaweza kusema: “Ikiwa ungekuwa jangwani nawe uone nyumba ambayo imejengwa vizuri yenye chakula tele (tokeo), je, hungekubali kwamba lazima kuna mtu (kisababishi) aliyeijenga? Hivyo basi, tunapoona maumbile na chakula tele kilicho duniani (tokeo), je, haipatani na akili kukata kauli kwamba Mtu Fulani (Kisababishi) ndiye aliyeumba vyote hivyo? Biblia yenyewe inasema hivi: ‘Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.’” (Waebrania 3:4) Ni kweli kwamba, hata tukitoa hoja zenye kusadikisha namna gani, si kila mtu atakayeukubali ujumbe wetu.—2 Wathesalonike 3:2.
Toa hoja zitakazofikia moyo
20, 21. (a) Tunaweza kutumia jinsi gani maneno “hata zaidi” ili kukazia sifa na njia za Yehova? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?
20 Tunapofundisha, iwe katika huduma ya shambani au kutanikoni, sisi pia tunaweza kulinganisha mambo kwa kutumia maneno “hata zaidi” ili kukazia sifa na njia za Yehova. Kwa mfano, tunapoonyesha kwamba fundisho la moto wa mateso linamvunjia Yehova heshima, tunaweza kusema: “Ni baba gani mwenye upendo anayeweza kumwadhibu mtoto wake kwa kuushika mkono wa mtoto wake na kuuweka motoni? Basi, wazo la moto wa mateso linamchukiza hata zaidi Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo!” (Yeremia 7:31) Ili tumhakikishie mwamini mwenzetu aliyeshuka moyo kwamba Yehova anampenda, tunaweza kusema: “Ikiwa Yehova anamwona shomoro mdogo kuwa mwenye thamani, basi anamjali na kumpenda hata zaidi kila mmoja wa waabudu wake walio duniani, kutia ndani wewe!” (Mathayo 10:29-31) Hoja kama hizo zinaweza kutusaidia kufikia mioyo ya wengine.
21 Baada ya kuchanganua njia tatu tu ambazo Yesu alitumia kufundisha, tunaweza kuona kwa urahisi kwamba maofisa hao walioshindwa kumkamata hawakuwa wakitia chumvi waliposema: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” Katika sura inayofuata, tutazungumzia njia ambayo Yesu alitumia sana kufundisha, yaani, kutumia mifano.
a Huenda maofisa hao walikuwa watumishi wa Sanhedrini waliokuwa chini ya mamlaka ya wakuu wa makuhani.
b Maneno hayo ya mwisho yanayopatikana kwenye Matendo 20:35 yananukuliwa na mtume Paulo tu. Huenda alisimuliwa maneno hayo (na mtu aliyemsikia Yesu akiyasema au alisimuliwa na Yesu aliyefufuliwa) au aliyapokea kupitia ufunuo kutoka kwa Mungu.
c Kila mwaka, Wayahudi walipaswa kulipa kodi ya hekalu ya drakma mbili, zinazolingana na malipo ya kazi ya siku mbili. Kitabu kimoja kinasema: “Kodi hiyo ilitumiwa kulipia gharama za toleo la kuteketezwa la kila siku na za dhabihu zote zilizotolewa kwa ajili ya watu.”
d Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-
-
“Hakuwa Akisema Nao Bila Mfano”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 12
“Hakuwa Akisema Nao Bila Mfano”
1-3. (a) Wanafunzi wanaosafiri na Yesu wana pendeleo gani la pekee, naye anafanya nini ili iwe rahisi kwao kukumbuka mambo anayofundisha? (b) Kwa nini mifano yenye matokeo inakumbukwa kwa urahisi?
WANAFUNZI wanaosafiri pamoja na Yesu wana pendeleo la pekee. Wanajifunza moja kwa moja kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Wanaisikia sauti yake huku akiwaeleza Neno la Mungu na kuwafundisha kweli zenye kusisimua. Kwa sasa, lazima wahifadhi maneno hayo yenye thamani katika akili na mioyo yao kwa sababu bado wakati haujafika kwa maneno yake kuhifadhiwa katika vitabu.a Hata hivyo, Yesu anafanya iwe rahisi kwao kukumbuka mambo anayofundisha. Jinsi gani? Kupitia njia yake ya kufundisha, na hasa ustadi wake wa kutumia mifano.
2 Kwa kweli, mifano yenye matokeo haisahauliki upesi. Mwandikaji mmoja alisema kwamba mifano “hugeuza masikio kuwa macho” na kwamba “huwawezesha wasikilizaji kupiga picha akilini.” Kwa kuwa tunafahamu mambo vizuri zaidi tunapopiga picha akilini, mifano inaweza kufanya iwe rahisi zaidi kuelewa hata mambo yasiyoonekana kwa macho. Mifano inaweza kutusaidia kuwazia kinachozungumziwa na kufanya mafundisho yadumu akilini.
3 Hakuna mwalimu yeyote duniani ambaye amewahi kutumia mifano kwa ustadi kuliko Yesu Kristo. Mpaka leo, mifano yake inakumbukwa kwa urahisi. Kwa nini Yesu alitumia sana njia hiyo ya kufundisha? Ni nini kilichofanya mifano yake iwe na matokeo? Tunaweza kujifunzaje kutumia njia hiyo ya kufundisha?
Kwa Nini Yesu Alitumia Mifano?
4, 5. Kwa nini Yesu alitumia mifano?
4 Biblia inaonyesha sababu mbili kuu zilizomfanya Yesu atumie mifano. Kwanza, kwa kufanya hivyo alitimiza unabii. Tunasoma hivi katika Mathayo 13:34, 35: “Yesu aliuambia umati mambo yote hayo kwa mifano. Kwa kweli, hakuwa akisema nao bila mfano; ili litimizwe lililosemwa kupitia nabii aliyesema: ‘Nitakifungua kinywa changu kwa mifano.’” Nabii aliyetajwa na Mathayo ni mwandikaji wa Zaburi 78:2. Mtunga-zaburi huyo aliandika maneno hayo kwa kuongozwa na roho ya Mungu mamia ya miaka kabla ya Yesu kuzaliwa. Fikiria jambo hilo. Miaka mingi mapema, Yehova alitabiri kwamba Masihi angefundisha kwa mifano. Hivyo basi, haikosi Yehova anathamini njia hii ya kufundisha.
5 Pili, Yesu alisema kwamba alitumia mifano kutenganisha watu ambao moyo wao “umekuwa mgumu.” (Mathayo 13:10-15; Isaya 6:9, 10) Mifano ya Yesu ilifunua nia za watu jinsi gani? Katika visa fulani, alitaka wasikilizaji wake wamwombe awafafanulie mifano ili waelewe maana kamili ya maneno yake. Watu wanyenyekevu walikuwa tayari kuuliza maswali lakini wenye kiburi au wasiopendezwa hawakutaka. (Mathayo 13:36; Marko 4:34) Basi, mifano ya Yesu iliwafunulia kweli wale ambao walitamani kutoka moyoni kuzijua; na wakati huohuo mifano yake iliwaficha wenye kiburi ile kweli.
6. Mifano ya Yesu ilitimiza makusudi gani yenye faida?
6 Mifano ya Yesu ilitimiza makusudi mengine yenye faida. Iliamsha upendezi kwa kuwachochea watu kusikiliza. Iliwawezesha kupiga picha akilini na kuzielewa kwa urahisi. Kama ilivyotajwa mwanzoni, mifano ya Yesu iliwasaidia wasikilizaji wake kukumbuka maneno yake. Mahubiri ya Mlimani, yaliyo katika Mathayo 5:3–7:27, ni mfano mzuri unaoonyesha jinsi Yesu alivyotumia mifano mingi. Hesabu moja ilionyesha kwamba kuna mifano zaidi ya 50 katika mahubiri hayo. Kumbuka kwamba mahubiri hayo yanaweza kusomwa kwa sauti kwa dakika 20 hivi. Hivyo, kwa wastani, mfano unatajwa karibu kila sekunde 20! Ni wazi kwamba Yesu aliona faida ya kutokeza picha akilini!
7. Kwa nini tuige jinsi Yesu alivyotumia mifano?
7 Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunataka kuiga njia yake ya kufundisha, kutia ndani kutumia mifano. Kama vile viungo vinavyoongeza ladha ya chakula, mifano yenye matokeo inaweza kufanya ufundishaji wetu uvutie zaidi. Pia, mifano iliyofikiriwa vizuri inaweza kufanya kweli nzito zieleweke kwa urahisi. Acheni sasa tuchunguze mambo fulani yaliyofanya mifano ya Yesu iwe na matokeo sana. Kisha tutaona jinsi tunavyoweza kutumia inavyofaa njia hiyo nzuri ya kufundisha.
Kulinganisha Mambo kwa Njia Rahisi
Ni kwa njia gani Yesu alitumia ndege na maua kuonyesha kwamba Mungu anatujali?
8, 9. Yesu alilinganishaje mambo kwa njia rahisi, na ni nini kilichofanya ulinganifu aliotoa uwe na matokeo sana?
8 Alipofundisha, mara nyingi Yesu alilinganisha mambo kwa njia rahisi akitumia maneno machache tu. Hata hivyo, maneno hayo rahisi yaliwawezesha watu kuona mambo waziwazi na yalifundisha kweli za kiroho zenye maana kubwa. Kwa mfano, alipowahimiza wanafunzi wake wasihangaikie mahitaji yao ya kila siku, alilinganisha hali yao na “ndege wa mbinguni” na “mayungiyungi ya shamba.” Ndege hawapandi wala kuvuna, na mayungiyungi hayasokoti wala kufuma. Lakini Mungu anawatunza ndege hao na maua. Ni rahisi kuelewa jambo kuu, kwamba, ikiwa Mungu anatunza ndege na maua, bila shaka atawatunza wanadamu ‘wanaoendelea kuutafuta kwanza ufalme.’—Mathayo 6:26, 28-33.
9 Yesu pia alitumia sana sitiari, ambayo ni njia ya kulinganisha mambo iliyo na matokeo hata zaidi. Sitiari huzungumzia kitu fulani kana kwamba ni kingine. Alipotumia sitiari, Yesu alilinganisha mambo kwa njia rahisi. Pindi moja aliwaambia wanafunzi wake: “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu.” Haikuwa vigumu kwa wanafunzi kuelewa waziwazi maana ya sitiari hiyo, kwamba, kupitia maneno na matendo yao, wangeangaza nuru ya kweli ya kiroho na kuwasaidia wengine wamtukuze Mungu. (Mathayo 5:14-16) Ona sitiari nyingine ambazo Yesu alitumia: “Ninyi ndio chumvi ya dunia” na “Mimi ndiye mzabibu, ninyi ndio matawi.” (Mathayo 5:13; Yohana 15:5) Mifano hiyo ina matokeo sana na ni rahisi kueleweka.
10. Taja vielelezo fulani vinavyoonyesha jinsi unavyoweza kutumia mifano unapofundisha.
10 Unaweza kutumia mifano kwa njia gani unapofundisha? Si lazima utunge hadithi ndefu zenye mambo mengi. Jaribu tu kufikiria mambo yanayoweza kueleweka kwa urahisi yanapolinganishwa. Wazia unazungumzia ufufuo na unataka kutoa mfano unaoonyesha kwamba si vigumu kwa Yehova kuwafufua wafu. Utatumia ulinganifu gani? Biblia inalinganisha kifo na usingizi. Unaweza kusema, “Mungu anaweza kuwafufua wafu kwa urahisi kama vile tunavyoweza kumwamsha mtu anayelala usingizi.” (Yohana 11:11-14) Tuseme unatoa mfano kuonyesha kwamba watoto wanahitaji kupendwa ili wakue vizuri. Unaweza kutumia mfano gani? Biblia inatumia ulinganifu huu: Watoto ni “kama miche [machipukizi] ya mizeituni.” (Zaburi 128:3) Unaweza kusema, “Mtoto anahitaji upendo kama vile mti unavyohitaji mwangaza wa jua na maji.” Kadiri ulinganifu ulivyo rahisi, ndivyo wasikilizaji wako watakavyoelewa kwa urahisi zaidi mambo unayozungumzia.
Mifano Inayohusu Mambo ya Kawaida Maishani
11. Toa vielelezo kuonyesha jinsi mifano ya Yesu ilivyohusu vitu ambavyo alijionea alipokuwa akikua huko Galilaya.
11 Yesu alikuwa stadi wa kutumia mifano iliyohusu maisha ya watu. Mifano yake mingi ilihusu hali ambazo yaelekea aliziona alipokuwa akikua huko Galilaya. Fikiria maisha yake ya utotoni. Ni mara ngapi alimwona mama yake akisaga nafaka ziwe unga, akiongeza chachu kwenye unga uliokandwa, akiwasha taa, au kufagia nyumba? (Mathayo 13:33; 24:41; Luka 15:8) Ni mara ngapi aliwaona wavuvi wakishusha nyavu zao katika Bahari ya Galilaya? (Mathayo 13:47) Ni mara ngapi aliwaona watoto wakicheza sokoni? (Mathayo 11:16) Bila shaka, Yesu aliona vitu vingine vya kawaida na kuvitumia katika mifano yake, kama vile mbegu zikipandwa, sherehe za ndoa zenye furaha, na mashamba yenye nafaka zilizokomaa.—Mathayo 13:3-8; 25:1-12; Marko 4:26-29.
12, 13. Katika mfano wa Msamaria mwema, kwa nini Yesu alizungumzia barabara ‘inayotoka Yerusalemu kwenda Yeriko’ ili kukazia hoja yake?
12 Katika mifano yake, Yesu alitaja mambo ambayo wasikilizaji wake waliyajua vizuri. Kwa mfano, alianza hadithi ya Msamaria mwema kwa kusema: “Mtu fulani alikuwa akishuka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akaanguka katikati ya wanyang’anyi, ambao walimvua nguo na pia kumpiga, . . . wakamwacha karibu kufa.” (Luka 10:30) Yesu alitaja barabara ‘inayotoka Yerusalemu kwenda Yeriko’ alipokuwa akikazia hoja yake. Yesu alisimulia mfano huo akiwa Yudea, karibu na Yerusalemu; kwa hiyo yaelekea wasikilizaji wake walijua barabara hiyo. Barabara hiyo ilikuwa hatari hasa kwa mtu aliyekuwa peke yake. Kwa kuwa haikupitiwa na watu wengi na ilijipinda-pinda, kulikuwa na sehemu nyingi ambazo wanyang’anyi wangejificha.
13 Yesu alitaja mambo mengine yanayojulikana kuhusu barabara ‘inayotoka Yerusalemu kwenda Yeriko.’ Kulingana na mfano huo, kuhani ndiye aliyepita kwanza katika barabara hiyo kisha akafuatwa na Mlawi, ijapokuwa hakuna yeyote kati yao aliyesimama kumsaidia mtu aliyejeruhiwa. (Luka 10:31, 32) Makuhani walitumikia hekaluni huko Yerusalemu, nao walisaidiwa na Walawi. Makuhani na Walawi wengi walikaa Yeriko wakati ambapo hawakuwa wakifanya kazi hekaluni, kwa kuwa Yeriko lilikuwa umbali wa kilometa 23 tu kutoka Yerusalemu. Kwa hiyo, walipitia barabara hiyo. Pia, ona kwamba Yesu alisema msafiri huyo alikuwa “akishuka,” bali hakuwa akipanda, barabara ‘inayotoka Yerusalemu.’ Wasikilizaji wake walielewa jambo hilo. Yerusalemu lilikuwa juu kuliko Yeriko. Basi, safari ya “kutoka Yerusalemu” ilikuwa ya ‘kushuka.’b Ni wazi kwamba Yesu aliwafikiria wasikilizaji wake.
14. Tunapotumia mifano, tunaweza kuwafikiria wasikilizaji wetu kwa njia gani?
14 Tunapotumia mifano, sisi pia tunahitaji kuwafikiria wasikilizaji wetu. Ni mambo gani kuhusu wasikilizaji wetu yanayoweza kutusaidia kuamua mifano tutakayotumia? Huenda ni umri, utamaduni, malezi, na kazi. Kwa mfano, mifano inayohusu ukulima inaweza kueleweka vizuri zaidi katika eneo la kilimo kuliko katika jiji kubwa. Mambo yanayohusu maisha na shughuli za kila siku za wasikilizaji wetu—watoto wao, nyumba zao, mapendezi yao, na chakula chao—yanaweza pia kutumiwa katika mifano inayofaa.
Mifano Inayohusu Uumbaji
15. Kwa nini haishangazi kwamba Yesu alifahamu uumbaji vizuri?
15 Mifano mingi ya Yesu inaonyesha kwamba alijua mambo ya asili, kutia ndani mimea, wanyama, na hali ya hewa. (Mathayo 16:2, 3; Luka 12:24, 27) Alipata wapi ujuzi huo? Alipokuwa akikua huko Galilaya, haikosi alipata wakati wa kutosha kuchunguza uumbaji. Isitoshe, Yesu ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” na Yehova alipoumba vitu vyote, alimtumia akiwa “stadi wa kazi.” (Wakolosai 1:15, 16; Methali 8:30, 31) Basi, haishangazi kwamba Yesu alifahamu uumbaji vizuri. Na tuone jinsi alivyotumia ujuzi huo kwa ustadi.
16, 17. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alijua vizuri tabia za kondoo? (b) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba kwa kweli kondoo wanasikiliza sauti ya mchungaji wao?
16 Kumbuka kwamba Yesu alijiita “mchungaji mwema” na kuwaita wafuasi wake “kondoo.” Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba alijua vizuri tabia za kondoo. Alijua kwamba kuna uhusiano wa pekee kati ya wachungaji na kondoo wao. Alitambua kwamba kwa kawaida kondoo wanakubali kuongozwa, nao wanamfuata mchungaji wao kwa uaminifu. Kwa nini kondoo wanamfuata mchungaji wao? Yesu alisema ni “kwa sababu wanaijua sauti yake.” (Yohana 10:2-4, 11) Je, kweli kondoo wanaijua sauti ya mchungaji wao?
17 Kutokana na mambo aliyojionea, George A. Smith aliandika hivi katika kitabu chake The Historical Geography of the Holy Land: “Mara kwa mara tulifurahia kupumzika mchana kando ya mojawapo ya visima vya Yudea, ambapo wachungaji watatu au wanne walileta kondoo zao. Kondoo hao walichanganyikana, nasi tukajiuliza jinsi ambavyo kila mchungaji angetambua kondoo wake. Lakini baada ya kondoo hao kumaliza kunywa maji na kucheza, kila mchungaji alielekea upande tofauti wa bonde hilo, na kila mmoja akaitana kwa sauti ambayo ingetambuliwa na kondoo wake; nao kondoo wa kila mchungaji walijitenga na hao kondoo wengine na kufuata mchungaji wao kwa utaratibu kama vile walivyokuja.” Yesu alichagua mfano unaofaa zaidi kukazia hoja yake ya kwamba tukitambua na kutii mafundisho yake na kufuata mwongozo wake, tutatunzwa na “mchungaji mwema.”
18. Tutapata wapi habari kuhusu uumbaji wa Yehova?
18 Tunaweza kujifunza jinsi gani kutumia mifano inayohusu uumbaji? Tunaweza kutumia tabia za pekee za wanyama kulinganisha mambo kwa njia rahisi na yenye matokeo. Tutapata wapi habari kuhusu uumbaji wa Yehova? Biblia ina habari tele kuhusu aina mbalimbali za wanyama, na nyakati nyingine inatumia mifano inayohusu tabia za wanyama. Biblia inataja mwendo wa swala au wepesi wa chui, kujihadhari kama nyoka, na kutokuwa na hatia kama njiwa.c (1 Mambo ya Nyakati 12:8; Habakuki 1:8; Mathayo 10:16) Habari nyingine nyingi ziko katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na vichapo vingine vinavyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Unaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza jinsi vichapo hivyo vinavyolinganisha mambo kwa njia rahisi kwa kutumia mifano inayohusu maajabu ya uumbaji mwingi wa Yehova.
Mifano Inayohusu Mambo Ambayo Wasikilizaji Wanajua
19, 20. (a) Eleza jinsi Yesu alivyotumia kwa matokeo tukio la karibuni kukanusha fundisho la uwongo. (b) Tunaweza kutumia jinsi gani visa na matukio halisi tunapofundisha?
19 Mifano yenye matokeo inaweza kutia ndani visa halisi. Pindi moja, Yesu alitumia tukio la karibuni kukanusha fundisho lisilo la kweli la kwamba msiba unawapata watu wanaoustahili. Alisema: “Wale kumi na wanane ambao mnara katika Siloamu uliwaangukia, na kuwaua, je, mnafikiri kwamba walikuwa na deni [wenye dhambi] kubwa zaidi kuliko watu wengine wote waliokuwa wakikaa Yerusalemu?” (Luka 13:4) Kwa kweli, watu hao 18 hawakufa kwa sababu ya kutenda dhambi fulani iliyomkasirisha Mungu. Badala yake, walipatwa na msiba huo kwa sababu ya “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11) Kwa hiyo, Yesu alikanusha fundisho la uwongo kwa kutaja kisa ambacho wasikilizaji wake walikijua vizuri.
20 Tunaweza kutumia jinsi gani visa na matukio halisi tunapofundisha? Tuseme unazungumzia utimizo wa unabii wa Yesu kuhusu ishara ya kuwapo kwake. (Mathayo 24:3-14) Unaweza kutaja habari za karibuni kuhusu vita, njaa, au matetemeko ya nchi kuonyesha kwamba mambo hususa yanayotajwa katika ishara hiyo yanatimia. Au wazia unataka kutumia jambo lililoonwa kuonyesha mabadiliko yanayohusika katika kuvaa utu mpya. (Waefeso 4:20-24) Unaweza kupata wapi jambo lililoonwa? Unaweza kufikiria malezi mbalimbali ya waamini wenzako, au unaweza kutumia jambo lililoonwa ambalo limechapishwa katika kichapo fulani cha Mashahidi wa Yehova.
21. Ni thawabu gani zinazotokana na kuwa mwalimu mwenye matokeo wa Neno la Mungu?
21 Bila shaka, Yesu alikuwa Mwalimu Mkuu! Kama vile tumeona katika sehemu hii, kazi yake kuu maishani ilikuwa ‘kufundisha na kuhubiri habari njema.’ (Mathayo 4:23) Hiyo ndiyo kazi yetu kuu pia. Thawabu za kuwa mwalimu mwenye matokeo ni kubwa. Kuwafundisha wengine ni njia moja ya kutoa, na tunapotoa kwa njia hiyo tunapata furaha. (Matendo 20:35) Furaha hiyo ni shangwe ya kujua kwamba tunawapa wengine kitu chema na chenye kudumu, yaani, kweli kumhusu Yehova. Tunaweza pia kuridhika kwa kujua kwamba tunafuata mfano wa Yesu, Mwalimu mkuu zaidi aliyepata kuishi duniani.
-