-
Gabrieli Anamtembelea MariaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 69
Gabrieli Amtembelea Maria
Elisabeti alikuwa na mtu wa ukoo kijana aliyeitwa Maria, ambaye aliishi katika mji wa Nazareti huko Galilaya. Maria alikuwa mchumba wa Yosefu, aliyekuwa seremala. Elisabeti alipokuwa na mimba ya miezi sita, malaika Gabrieli alimtokea Maria. Akamwambia hivi: ‘Siku njema, Maria. Yehova amekupendelea sana.’ Maria hakuelewa kile ambacho Gabrieli alimaanisha. Kisha akamwambia hivi: ‘Utapata mimba na kuzaa mwana, nawe utamwita Yesu. Atatawala akiwa Mfalme. Ufalme wake hautakuwa na mwisho.’
Maria akamwambia: ‘Lakini mimi ni bikira. Ninawezaje kuwa na mtoto?’ Gabrieli akajibu: ‘Hakuna lolote lisilowezekana kwa Yehova. Roho takatifu itakuja juu yako, nawe utapata mwana. Elisabeti mtu wako wa ukoo ana mimba.’ Kisha Maria akasema: ‘Mimi ni kijakazi wa Yehova. Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.’
Maria akaenda kumtembelea Elisabeti kwenye jiji lenye milima. Maria alipomsalimu, Elisabeti alihisi mtoto aliyekuwa tumboni mwake akiruka. Akiwa amejawa na roho takatifu, akasema hivi: ‘Maria, Yehova amekubariki. Ni pendeleo kuwa na mama ya Bwana wangu nyumbani kwangu.’ Maria akajibu hivi: ‘Nafsi yangu yote inamtukuza Yehova.’ Maria akaishi na Elisabeti kwa miezi mitatu, kisha akarudi nyumbani kwake Nazareti.
Yosefu alipogundua kwamba Maria alikuwa na mimba, alitaka kumtaliki. Lakini malaika akamtokea katika ndoto na kumwambia hivi: ‘Usiogope kumchukua awe mke wako. Hajafanya kosa lolote.’ Hivyo, Yosefu akamchukua Maria awe mke wake na akaenda naye nyumbani kwake.
“Yehova hufanya kila jambo apendalo mbinguni na duniani.”—Zaburi 135:6
-
-
Malaika Watangaza Kuzaliwa kwa YesuMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 70
Malaika Watangaza Kuzaliwa kwa Yesu
Mtawala wa Milki ya Roma, Kaisari Augusto, alitoa amri kwamba Wayahudi wote warudi kwenye majiji yao ili wakaandikishwe. Kwa hiyo, Yosefu na Maria wakasafiri kwenda Bethlehemu, ambako familia ya Yosefu ilitokea. Kwa wakati huo, Maria alikuwa karibu kuzaa.
Walipofika Bethlehemu, mahali pekee walipopata ili kupumzika palikuwa zizini. Hapo ndipo Maria alipomzaa Yesu mwana wake. Akamfunga kwa vitambaa na kumlaza kwa wororo katika hori.
Karibu na Bethlehemu, wachungaji fulani walikuwa nje wakati wa usiku, wakichunga makundi yao ya mifugo. Ghafla, malaika akasimama kando yao na utukufu wa Yehova ukamulika pande zote. Wachungaji hao wakaogopa, lakini malaika akawaambia hivi: ‘Msiogope, nina habari zenye kusisimua. Leo, Masihi amezaliwa Bethlehemu.’ Wakati huohuo, malaika wengi wakatokea katika mbingu, wakisema: ‘Utukufu juu kwa Mungu, na amani juu ya dunia.’ Kisha malaika hao wakatoweka. Wachungaji hao walitendaje?
Wachungaji hao wakaambiana hivi: ‘Twendeni moja kwa moja hadi Bethlehemu.’ Nao wakaenda haraka na kuwakuta Yosefu na Maria katika hori wakiwa na mtoto wao mchanga.
Wote waliosikia juu ya mambo ambayo malaika aliwaambia wachungaji hao walistaajabu. Maria alifikiria sana kuhusu maneno ya yule malaika na hakuyasahau kamwe. Basi wachungaji wakarudi kwenye makundi yao ya mifugo, wakimshukuru Yehova kwa ajili ya mambo yote waliyosikia na kuona.
“Nilitoka kwa Mungu nami nipo hapa. Sikuja kwa uamuzi wangu mwenyewe, bali Yeye ndiye aliyenituma.”—Yohana 8:42
-
-
Yehova Alimlinda YesuMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 71
Yehova Alimlinda Yesu
Katika nchi fulani iliyo upande wa mashariki mwa Israeli, kulikuwa na watu walioamini kwamba nyota zingeweza kuwaongoza. Pindi moja wakati wa usiku, wanaume fulani kutoka sehemu za mashariki waliona kitu kilichoonekana kama nyota yenye kung’aa ikisonga angani, na wakaifuata. “Nyota” hiyo ikawaongoza hadi Yerusalemu. Wanaume hao wakaanza kuwauliza watu hivi: ‘Yuko wapi yule mtoto ambaye atakuwa mfalme wa Wayahudi? Tumekuja kumsujudia.’
Herode, mfalme wa Yerusalemu, aliposikia kuhusu mfalme mpya, akawa na wasiwasi sana. Akawauliza wakuu wa makuhani hivi: ‘Mfalme huyo alipaswa kuzaliwa wapi?’ Wakamwambia hivi: ‘Manabii walisema kwamba angezaliwa Bethlehemu.’ Kwa hiyo, Herode akawaita wale wanaume kutoka mashariki na kuwaambia hivi: ‘Nendeni Bethlehemu mkamtafute mtoto huyo. Kisha, mrudi na kunieleza yuko wapi. Mimi pia ninataka kumsujudia.’ Lakini alikuwa akisema uwongo.
“Nyota” ile ikaanza kusonga tena. Wanaume hao wakaifuata hadi Bethlehemu. “Nyota” ile ikatua juu ya nyumba fulani na wanaume hao wakaingia ndani ya nyumba hiyo. Wakampata Yesu akiwa na Maria mama yake. Wakamsujudia mtoto huyo na kumpa zawadi za dhahabu, ubani, na manemane. Je, kweli Yehova alikuwa amewatuma wanaume hao wamtafute Yesu? Hapana.
Usiku huo, Yehova akamwambia hivi Yosefu kupitia ndoto: ‘Herode anataka kumwangamiza Yesu. Mchukue mke na mwana wako na mkimbilie Misri. Kaeni huko hadi nitakapowaambia kwamba ni salama kwenu kurudi.’ Mara moja, Yosefu na familia yake wakaenda Misri.
Yehova alikuwa amewaambia wanaume waliotoka mashariki kwamba wasirudi kwa Herode. Herode alipotambua kwamba wanaume hao hawatarudi, alikasirika sana. Kwa kuwa hangeweza kumpata Yesu, aliagiza wavulana wote waliokuwa na umri kama wa Yesu walioko Bethlehemu wauawe. Lakini Yesu alikuwa salama katika nchi ya mbali ya Misri.
Baada ya muda, Herode akafa. Yehova akamwambia Yosefu hivi: ‘Sasa ni salama kwako kurudi.’ Yosefu, Maria, na Yesu wakarudi Israeli, na kuishi katika jiji la Nazareti.
“Hivyo ndivyo neno langu linalotoka katika kinywa changu litakavyokuwa . . . , na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.”—Isaya 55:11
-
-
Yesu Akiwa KijanaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 72
Yesu Akiwa Kijana
Yosefu na Maria waliishi Nazareti pamoja na Yesu na wana na binti zao wengine. Yosefu aliitegemeza familia yake kwa kufanya kazi ya useremala, na aliwafundisha kumhusu Yehova na Sheria yake. Familia hiyo ilienda katika sinagogi kwa ukawaida ili kuabudu, na pia jijini Yerusalemu kila mwaka ili kusherehekea Pasaka.
Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, kama ilivyokuwa kawaida yao, familia yao ilifunga safari ndefu kuelekea Yerusalemu. Jiji hilo lilikuwa limejaa watu waliokuwa wamekuja kusherehekea Pasaka. Baadaye, Yosefu na Maria wakaanza safari ya kurudi nyumbani, wakifikiri kwamba Yesu alikuwa akisafiri katika kikundi chao. Lakini walipomtafuta kati ya watu wao wa ukoo, hawakumpata.
Wakarudi Yerusalemu na kumtafuta mwana wao kwa siku tatu. Hatimaye, wakaenda hekaluni. Wakampata hekaluni, akiwa ameketi katikati ya walimu, akiwasikiliza kwa makini na kuwauliza maswali. Walimu hao walipendezwa sana na Yesu hivi kwamba wakaanza kumuuliza maswali. Nao walishangazwa na majibu yake. Waliona kwamba alielewa Sheria ya Yehova.
Yosefu na Maria walipatwa na wasiwasi sana. Maria akasema hivi: ‘Mwanangu, tumekuwa tukikutafuta kila mahali! Ulikuwa wapi?’ Yesu akajibu hivi: ‘Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe hapa katika nyumba ya Baba yangu?’
Yesu akaenda nyumbani Nazareti pamoja na wazazi wake. Yosefu alimfundisha Yesu kazi ya useremala. Unafikiri Yesu alikuwa mtu wa aina gani alipokuwa kijana? Alipoendelea kukua, Yesu alifanya maendeleo katika hekima akizidi kupata kibali kwa Mungu na wanadamu.
“Ee Mungu wangu, ninafurahia kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu kabisa.”—Zaburi 40:8
-
-
Yohana Atayarisha NjiaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 73
Yohana Atayarisha Njia
Yohana, mwana wa Zekaria na Elisabeti, alikuwa nabii alipokuwa mtu mzima. Yehova alimtumia Yohana kuwafundisha watu kwamba Masihi angekuja. Lakini badala ya kufundisha katika masinagogi au katika miji, Yohana alihubiri nyikani. Watu walitoka Yerusalemu na sehemu zote za Yudea ili wafundishwe na Yohana. Aliwafundisha kwamba ili wampendeze Mungu, walihitaji kuacha kufanya mambo mabaya. Baada ya kumsikiliza Yohana, wengi walitubu dhambi zao, na Yohana akawabatiza katika Mto Yordani.
Yohana aliishi maisha rahisi. Alivaa mavazi yaliyotengenezwa kwa manyoya ya ngamia na alikula nzige na asali ya mwituni. Watu walishangazwa na Yohana. Hata Mafarisayo na Masadukayo wenye kiburi walikuja kumwona. Yohana aliwaambia hivi: ‘Mnahitaji kubadili njia zenu na kutubu. Au je, mnafikiri kwamba ninyi ni watu wa pekee kwa sababu tu mnasema ninyi ni watoto wa Abrahamu? Hilo halimaanishi kwamba ninyi ni watoto wa Mungu.’
Watu wengi walimwendea Yohana na kumuuliza: ‘Tunapaswa kufanya nini ili tumpendeze Mungu?’ Yohana akawaambia Wayahudi: ‘Ikiwa una mavazi mawili, mpe moja yule aliye na uhitaji.’ Unajua kwa nini alisema hivyo? Alitaka wanafunzi wake wajifunze kwamba ili wampendeze Mungu, ni lazima wawapende watu.
Yohana aliwaambia hivi wakusanya-kodi: ‘Iweni wanyoofu na msimdanganye mtu yeyote.’ Aliwaambia wanajeshi hivi: ‘Msichukue rushwa wala kusema uwongo.’
Makuhani na Walawi walimwendea Yohana na kumuuliza: ‘Kila mtu anataka kujua, wewe ni nani?’ Yohana akawaambia: ‘Mimi ni sauti nyikani inayowaongoza watu kwa Yehova, kama tu Isaya alivyotabiri.’
Watu walipenda sana mambo ambayo Yohana alikuwa akiwafundisha. Wengi walijiuliza ikiwa Yohana ndiye Masihi. Lakini aliwaambia: ‘Kuna mtu mwenye nguvu kuliko mimi anayekuja. Sistahili hata kufungua kamba za viatu vyake. Mimi ninawabatiza kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa roho takatifu.’
“Mtu huyo alikuja akiwa shahidi, ili atoe ushahidi kuhusu nuru, ili watu wa namna zote waamini kupitia kwake.”—Yohana 1:7
-
-
Yesu Anakuwa MasihiMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 74
Yesu Anakuwa Masihi
Yohana alihubiri hivi: ‘Kuna mtu mwenye nguvu kuliko mimi anayekuja.’ Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi, alitoka Galilaya na kwenda kwenye Mto Yordani ambapo Yohana alikuwa akiwabatiza watu. Yesu alitaka Yohana ambatize, lakini Yohana akasema: ‘Sipaswi kukubatiza. Wewe ndiye unayepaswa kunibatiza.’ Yesu akamwambia Yohana hivi: ‘Yehova anataka wewe unibatize.’ Kwa hiyo, wakaingia ndani ya Mto Yordani, na Yohana akamzamisha Yesu ndani ya maji.
Baada ya Yesu kubatizwa, alisali. Wakati huohuo, mbingu zikafunguliwa, na roho ya Mungu ikashuka juu yake kama njiwa. Kisha Yehova akasema kutoka mbinguni: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali.”
Roho ya Yehova iliposhuka juu ya Yesu, akawa Kristo, au Masihi. Sasa angeanza kufanya kazi ambayo Yehova alimtuma afanye duniani.
Mara tu baada ya ubatizo wake, Yesu akaingia nyikani na kukaa huko kwa siku 40. Aliporudi, akaenda kumwona Yohana. Yesu alipomkaribia, Yohana akasema: ‘Huyu ndiye Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.’ Kwa kusema hivyo, Yohana alikuwa akiwajulisha kwamba Yesu ndiye Masihi. Je, unajua kilichompata Yesu alipokuwa nyikani? Acheni tuone.
“Sauti ikasikika kutoka mbinguni ikisema: ‘Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali.’”—Marko 1:11
-
-
Ibilisi Anamjaribu YesuMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 75
TIbilisi Anamjaribu Yesu
Baada ya Yesu kubatizwa, roho takatifu ilimwongoza aingie nyikani. Hakula kitu chochote kwa siku 40, naye akawa na njaa sana. Kisha Ibilisi akaja kumjaribu Yesu na kumwambia hivi: ‘Ikiwa kweli wewe ni Mwana wa Mungu, yaambie mawe haya yawe mkate.’ Lakini Yesu akajibu kwa kunukuu Maandiko akisema: ‘Imeandikwa kwamba mtu anahitaji mengi zaidi ya chakula ili aendelee kuishi. Anahitaji kusikiliza kila neno ambalo Yehova anasema.’
Kisha, Ibilisi akamjaribu Yesu na kumwambia: ‘Ikiwa kweli wewe ni Mwana wa Mungu, jitupe kutoka kwenye sehemu ya juu zaidi ya hekalu. Imeandikwa kwamba Mungu atawatuma malaika zake wakubebe mikononi mwao.’ Lakini kwa mara nyingine Yesu akanukuu Maandiko na kusema: ‘Imeandikwa kwamba hupaswi kumjaribu Yehova.’
Kisha, Shetani akamwonyesha Yesu falme zote za ulimwengu, utajiri wake, na utukufu wake naye akasema: ‘Nitakupa falme hizi zote na utukufu wake ikiwa utaniabudu mara moja tu.’ Lakini Yesu akajibu hivi: ‘Nenda zako, Shetani! Imeandikwa kwamba unapaswa kumwabudu Yehova peke yake.’
Kisha Ibilisi akaondoka, na malaika wakaja na kumpa Yesu chakula. Kuanzia wakati huo na kuendelea, Yesu akahubiri habari njema ya Ufalme. Hiyo ndiyo kazi aliyotumwa kufanya duniani. Watu walipenda sana mambo ambayo Yesu aliwafundisha, nao wakamfuata kila mahali alipoenda.
“[Ibilisi] anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.”—Yohana 8:44
-
-
Yesu Analisafisha HekaluMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 76
Yesu Analisafisha Hekalu
Katika majira ya kuchipua ya mwaka wa 30 W.K., Yesu alienda Yerusalemu. Watu wengi walienda jijini humo ili kusherehekea Pasaka. Sherehe hiyo ilitia ndani kutoa dhabihu za wanyama hekaluni. Watu fulani walikuja na wanyama wao, lakini wengine waliwanunua huko Yerusalemu.
Yesu alipoenda hekaluni, aliwaona watu wakiuza wanyama ndani ya hekalu. Walikuwa wakijipatia pesa ndani ya nyumba ya ibada ya Yehova! Yesu alitendaje? Alitengeneza mjeledi wa kamba naye akawafukuza kondoo na ng’ombe kutoka hekaluni. Akapindua meza za watu waliokuwa wakibadili pesa na kumwaga sarafu zao chini. Yesu akawaambia wale waliokuwa wakiuza njiwa: ‘Ondoeni vitu hivi hapa! Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!’
Watu waliokuwa hekaluni walishangazwa na jambo ambalo Yesu alifanya. Wanafunzi wake wakakumbuka unabii huu uliomhusu Masihi: ‘Nitakuwa na bidii nyingi kwa ajili ya nyumba ya Yehova.’
Baadaye, katika mwaka wa 33 W.K., Yesu alisafisha hekalu kwa mara ya pili. Hangemruhusu mtu yeyote aishushie heshima nyumba ya Baba yake.
“Hamwezi kuwa watumwa wa Mungu na wa Utajiri.”—Luka 16:13
-
-
Mwanamke KisimaniMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 77
Mwanamke Kisimani
Baada ya Pasaka, Yesu na wanafunzi wake wakasafiri kupitia Samaria walipokuwa wakirudi Galilaya. Yesu akafika katika sehemu iliyoitwa kisima cha Yakobo, karibu na jiji la Sikari. Alipokuwa akipumzika, wanafunzi wake wakaenda jijini kununua chakula.
Mwanamke mmoja akaja kwenye kisima hicho kuteka maji. Yesu akamwambia: “Naomba maji ninywe.” Mwanamke huyo akasema: ‘Kwa nini unazungumza nami? Mimi ni mwanamke Msamaria. Wayahudi hawazungumzi na Wasamaria.’ Yesu akamwambia: ‘Ikiwa ungejua mimi ni nani, ungeniomba nikupe maji yaliyo hai.’ Mwanamke huyo akamuuliza, ‘unamaanisha nini? Huna hata ndoo.’ Yesu akasema: ‘Kila mtu anayekunywa maji ninayompa hatapatwa na kiu tena.’ Mwanamke huyo akasema: “Bwana, nipe maji hayo.”
Yesu akamwambia: ‘Nenda, ukamwite mume wako mje hapa kisimani.’ Mwanamke huyo akasema: ‘Sina mume.’ Yesu akamwambia: ‘Umesema kweli. Wewe umeolewa mara tano, na sasa unaishi na mwanamume ambaye si mume wako.’ Mwanamke huyo akasema: ‘Ninaona kwamba wewe ni nabii. Watu wetu wanaamini kwamba tunaweza kumwabudu Mungu katika mlima huu, lakini Wayahudi wanasema tunapaswa tu kuabudu kule Yerusalemu. Mimi ninaamini kwamba Masihi atakapokuja, yeye atatufundisha jinsi ya kuabudu.’ Kisha Yesu akamwambia jambo ambalo hakuwa amemwambia mtu mwingine yeyote: ‘Mimi ndiye Masihi.’
Mwanamke huyo akaenda upesi kwenye jiji la nyumbani kwake na kuwaambia Wasamaria hivi: ‘Nafikiri nimempata Masihi. Anajua kila kitu kunihusu. Njooni mwone!’ Wakamfuata hadi kisimani na kumsikiliza Yesu akifundisha.
Wasamaria walimkaribisha Yesu akae katika jiji lao. Kwa siku mbili, alifundisha katika jiji hilo, na watu wengi wakamwamini. Wakamwambia huyo mwanamke Msamaria hivi: ‘Baada ya kumsikiliza mwanamume huyu, tunajua kwamba kwa kweli yeye ndiye mwokozi wa ulimwengu.’
“‘Njoo!’ na yeyote aliye na kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:17
-
-
Yesu Anahubiri Ujumbe wa UfalmeMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 78
Yesu Anahubiri Ujumbe wa Ufalme
Muda mfupi baada ya ubatizo wake, Yesu alianza kuhubiri: ‘Ufalme wa Mungu umekaribia.’ Wanafunzi walimfuata alipokuwa akisafiri katika eneo la Galilaya na Yudea. Yesu aliporudi katika eneo la nyumbani la Nazareti, alienda kwenye sinagogi, akafungua kitabu cha kukunjwa cha Isaya, na kusoma kwa sauti: ‘Yehova amenipa roho takatifu ili nihubiri habari njema.’ Maneno hayo yalimaanisha nini? Yalimaanisha kwamba ingawa watu walitaka kumwona Yesu akifanya miujiza, sababu kuu ya kupokea roho takatifu ilikuwa ni kuhubiri habari njema. Aliwaambia hivi wasikilizaji wake: ‘Leo unabii huu umetimizwa.’
Kisha Yesu akaenda kwenye Bahari ya Galilaya, ambapo alikutana na wanafunzi wake wanne, ambao walikuwa wavuvi. Yesu akawaambia hivi: ‘Nifuateni, nami nitawafanya muwe wavuvi wa watu.’ Wanafunzi hao walikuwa Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana. Mara moja wakaacha biashara yao ya uvuvi na kumfuata. Walienda katika sehemu zote za Galilaya, wakihubiri kuhusu Ufalme wa Yehova. Walihubiri katika masinagogi, sokoni, na barabarani. Umati mkubwa uliwafuata kila mahali walipoenda. Habari kumhusu Yesu zilienea kila mahali, hata kufikia Siria.
Baada ya muda, Yesu aliwapa baadhi ya wafuasi wake nguvu za kuponya watu na kufukuza roho waovu. Wengine waliandamana naye alipokuwa akihubiri kutoka jiji hadi jiji na kutoka kijiji hadi kijiji. Wanawake fulani waaminifu, kutia ndani Maria Magdalene, Yoana, Susana, na wengine walikuwa wakimhudumia Yesu na wafuasi wake.
Baada ya kuwazoeza wanafunzi wake, Yesu aliwatuma wakahubiri. Walipokuwa wakisafiri kotekote katika Galilaya, wengine wengi wakawa wanafunzi na kubatizwa. Watu wengi sana walitaka kuwa wanafunzi hivi kwamba Yesu akawalinganisha na shamba ambalo liko tayari kuvunwa. Alisema hivi: ‘Mwombeni Yehova awatume wafanyakazi wengi zaidi katika mavuno.’ Baadaye alichagua wanafunzi wengine 70 na akawatuma wakiwa wawili-wawili wakahubiri katika maeneo yote kuzunguka Yudea. Waliwafundisha watu wote kuhusu Ufalme. Wanafunzi waliporudi, walikuwa na hamu sana ya kumwambia Yesu kilichotukia. Hakuna kitu ambacho Ibilisi angefanya ili kuzuia kazi ya kuhubiri.
Yesu alihakikisha kwamba wanafunzi wake wangeendelea kufanya kazi hiyo muhimu baada ya yeye kurudi mbinguni. Aliwaambia hivi: ‘Hubirini habari njema duniani pote. Wafundisheni watu Neno la Mungu na kuwabatiza.’
“Ni lazima pia nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu katika majiji mengine, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.”—Luka 4:43
-
-
Yesu Anafanya Miujiza MingiMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 79
Yesu Anafanya Miujiza Mingi
Yesu alikuja duniani kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Ili kuonyesha mambo ambayo Yesu atatimiza akiwa Mfalme, Yehova alimpa roho takatifu ili afanye miujiza. Angeweza kuponya ugonjwa wowote. Popote alipoenda wagonjwa walimwendea ili awasaidie, naye akawaponya wote. Vipofu waliona, viziwi wakasikia, vilema wakatembea, na wale waliosumbuliwa na roho waovu wakawekwa huru. Waliponywa hata walipogusa tu upindo wa vazi lake. Watu walimfuata Yesu popote alipoenda. Hata alipotaka kuwa peke yake, kamwe Yesu hakumfukuza mtu yeyote.
Pindi moja, watu walimleta mwanamume aliyekuwa amepooza katika nyumba ambayo Yesu alikuwa akiishi. Lakini nyumba hiyo ilikuwa imejaa sana hivi kwamba hawangeweza kumwingiza ndani. Kwa hiyo, wakatoboa tundu kwenye paa na kumshusha mwanamume huyo kwa Yesu. Kisha Yesu akamwambia mwanamume huyo: ‘Simama utembee.’ Aliposimama, watu walishangaa sana.
Pindi nyingine, Yesu alipokuwa akiingia katika kijiji fulani, wanaume kumi waliokuwa na ukoma walisimama mbali na kumwambia Yesu kwa sauti kubwa: ‘Yesu, tusaidie!’ Katika siku hizo, watu wenye ukoma hawakuruhusiwa kuwakaribia watu wengine. Yesu akawaambia wanaume hao waende hekaluni, kama Sheria ya Yehova ilivyosema kwamba watu wenye ukoma wanapaswa kwenda hekaluni baada ya kuponywa. Walipokuwa njiani, wakaponywa. Mmoja wao alipotambua kwamba ameponywa, alirudi kumshukuru Yesu na kumsifu Mungu. Kati ya wanaume wote kumi, ni huyo mmoja tu aliyemshukuru Yesu.
Mwanamke ambaye alikuwa mgonjwa kwa miaka 12 alitamani sana kuponywa. Alikuja nyuma ya Yesu akiwa katikati ya umati na kugusa upindo wa vazi lake la nje. Mara moja, akaponywa. Hilo lilipotukia, Yesu akauliza: “Ni nani aliyenigusa?” Ingawa mwanamke huyo aliogopa sana, alijitokeza na kumwambia ukweli. Yesu alimfariji kwa kumwambia: ‘Binti yangu, nenda kwa amani.’
Ofisa anayeitwa Yairo alimsihi Yesu hivi: ‘Njoo nyumbani kwangu! Binti yangu ni mgonjwa sana.’ Lakini kabla ya Yesu kufika nyumbani kwa Yairo, yule msichana akafa. Yesu alipofika, aliona watu wengi waliokuja kuomboleza na familia hiyo. Yesu akawaambia: ‘Msilie; msichana huyu amelala tu.’ Kisha akamshika msichana huyo mkono na kusema: “Msichana, inuka!” Yule msichana akainuka mara moja, na Yesu akawaambia wazazi wake wampe chakula. Hebu wazia jinsi wazazi hao walivyohisi!
“Mungu [alimtia] mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi, kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.”—Matendo 10:38
-
-
Yesu Anachagua Mitume Kumi na WawiliMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 80
Yesu Anachagua Mitume Kumi na Wawili
Baada ya Yesu kuhubiri kwa karibu mwaka mmoja na nusu, alihitaji kufanya uamuzi muhimu. Angewachagua nani wafanye kazi kwa ukaribu pamoja naye? Angewazoeza nani ili waongoze katika kutaniko la Kikristo? Ili afanye maamuzi hayo, Yesu alihitaji mwongozo wa Yehova. Kwa hiyo, akaenda kwenye mlima ambapo angekuwa peke yake, naye akasali usiku wote. Asubuhi ilipofika, Yesu akawaita baadhi ya wanafunzi wake kisha akachagua mitume 12. Unakumbuka majina yao? Walikuwa Petro, Andrea, Yakobo, Yohana, Filipo, Bartholomayo, Tomasi, Mathayo, Yakobo mwana wa Alfayo, Thadayo, Simoni, na Yuda Iskariote.
Andrea, Petro, Filipo, Yakobo
Mitume hao kumi na wawili wangesafiri na kuhubiri pamoja na Yesu. Baada ya kuwazoeza, Yesu aliwatuma wakahubiri peke yao. Yehova aliwapa mamlaka ya kufukuza roho waovu na kuponya wagonjwa.
Yohana, Mathayo, Bartholomayo, Tomasi
Yesu aliwaita Mitume hao kumi na wawili rafiki zake, na aliwaamini. Mafarisayo walifikiri kwamba mitume walikuwa watu wasio na elimu na wa kawaida tu. Lakini Yesu aliwazoeza kwa ajili ya kazi yao. Wangekuwa pamoja na Yesu pindi muhimu zaidi maishani mwake, kama vile kabla ya kifo chake na baada ya ufufuo wake. Kama Yesu, wengi kati ya wale Mitume kumi na wawili walitoka Galilaya. Baadhi yao walikuwa wameoa.
Yakobo mwana wa Alfayo, Yuda Iskariote, Thadayo, Simoni
Mitume walikuwa wanaume wasio wakamilifu ambao walifanya makosa. Nyakati nyingine, walizungumza bila kufikiri na wakafanya maamuzi mabaya. Nyakati nyingine, walikosa subira. Hata walibishana kuhusu ni nani aliyekuwa mtu mkuu zaidi kati yao. Lakini walikuwa watu wema ambao walimpenda Yehova. Wao ndio wangefanyiza msingi wa kutaniko la Kikristo baada ya Yesu kuondoka.
“Nimewaita rafiki, kwa sababu nimewajulisha mambo yote niliyosikia kutoka kwa Baba yangu.”—Yohana 15:15
-
-
Mahubiri ya MlimaniMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 81
Mahubiri ya Mlimani
Baada ya kuwachagua mitume wake 12, Yesu alishuka kutoka mlimani na kukuta umati wa watu ukiwa umekusanyika. Watu hao walitoka Galilaya, Yudea, Tiro, Sidoni, Siria, na ng’ambo ya Yordani. Waliwaleta wagonjwa na watu waliokuwa wakiteswa na roho waovu. Yesu akawaponya wote, kisha akaketi kando ya mlima, na kuanza kufundisha. Alieleza mambo tunayopaswa kufanya ikiwa tunataka kuwa rafiki za Mungu. Ni lazima tujifunze kumpenda Yehova na kutambua kwamba yeye ni muhimu katika maisha yetu. Lakini hatuwezi kumpenda Mungu ikiwa hatuwapendi wanadamu wenzetu. Tunapaswa kuwa wema na wenye fadhili kwa kila mtu kutia ndani adui zetu.
Yesu alisema: ‘Haitoshi tu kuwapenda rafiki zako. Unapaswa pia kuwapenda adui zako na kuwasamehe wengine kutoka moyoni. Ikiwa umekosana na mtu fulani, nenda umwombe msamaha. Watendee wengine katika njia ambayo wewe ungependa kutendewa.’
Pia, Yesu aliwapa watu ushauri mzuri kuhusu vitu vya kimwili. Alisema hivi: ‘Ni muhimu zaidi kuwa rafiki ya Yehova kuliko kuwa na pesa nyingi. Mwizi anaweza kukuibia pesa, lakini hakuna mtu anayeweza kuiba urafiki wako pamoja na Yehova. Usihangaike kuhusu kile utakachokula, utakachokunywa, au kile utakachovaa. Waangalie ndege wa angani. Wakati wote Mungu anahakikisha kwamba wanapata chakula cha kutosha. Kuhangaika hakutakusaidia kuongeza siku za kuishi. Kumbuka kwamba Yehova anajua vitu unavyohitaji.’
Umati haukuwahi kumsikia mtu mwingine akifundisha kama Yesu. Viongozi wao wa kidini hawakuwa wamewafundisha mambo hayo. Ni nini kilimchofanya Yesu awe mwalimu mkuu? Kwa sababu yale aliyofundisha yalitoka kwa Yehova.
“Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.”—Mathayo 11:29
-
-
Yesu Anawafundisha Wanafunzi Wake Jinsi ya KusaliMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 82
Yesu Awafundisha Wanafunzi Wake Jinsi ya Kusali
Mafarisayo walifanya mambo mengi ili tu waonekane na watu. Kwa mfano, waliwatendea wengine kwa fadhili ili kujionyesha. Walisali kwenye maeneo yenye watu wengi ili kila mtu awaone. Pia, walikariri sala ndefu na kuzirudia-rudia walipokuwa wanasali kwenye masinagogi au kwenye njia panda ili wengine wawasikie. Kwa hiyo, watu walishangaa Yesu alipowaambia hivi: ‘Msisali kama Mafarisayo. Wao hufikiri kwamba Mungu atafurahishwa na maneno yao mengi, lakini sivyo ilivyo. Sala ni kati yako wewe na Yehova. Msiseme mambo yaleyale tena na tena. Yehova anataka umwambie jinsi unavyohisi kikweli.
‘Mnapaswa kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”’ Pia, Yesu aliwaambia kwamba wanapaswa kusali kuhusu mahitaji ya chakula cha siku hiyo, kuomba msamaha wa makosa yao, na kuhusu mambo mengine ya kibinafsi.
Yesu alisema hivi: ‘Msiache kamwe kusali. Endeleeni kumwomba Baba yenu, Yehova, mambo mazuri. Kila mzazi hupenda kumpa mtoto wake vitu vizuri. Ikiwa mtoto wako ataomba mkate, je, utampa jiwe? Akiomba samaki, je, utampa nyoka?’
Kisha, Yesu akafafanua somo la mfano huo: ‘Ikiwa ninyi mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba yenu, Yehova, hatawapa ninyi roho takatifu? Mnachopaswa kufanya ni kuomba.’ Je, unafuata ushauri wa Yesu? Wewe huwa unasali kuhusu mambo gani?
“Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.”—Mathayo 7:7
-
-
Yesu Analisha Maelfu ya WatuMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 83
Yesu Analisha Maelfu ya Watu
Muda mfupi tu kabla ya Pasaka ya mwaka wa 32 W.K., mitume walikuwa wametoka kwenye kampeni ya kuhubiri. Kwa kuwa walikuwa wamechoka, Yesu na mitume wake walipanda mashua kuelekea Bethsaida ili wakapumzike. Lakini mashua ilipokaribia ufuoni, Yesu akaona maelfu ya watu wakiwa wanamsubiri. Ingawa Yesu alitaka yeye na mitume wake wapate nafasi ya kuwa peke yao, aliwakaribisha watu hao kwa fadhili. Aliwaponya wagonjwa wao, na kisha akaanza kuwafundisha. Siku nzima, Yesu aliwafundisha kuhusu Ufalme wa Mungu. Ilipofika jioni, mitume wakamwambia hivi: ‘Bila shaka, watu wana njaa. Waache waende zao ili wakatafute chakula.’
Yesu akasema: ‘Si lazima waondoke. Ninyi wapeni chakula.’ Mitume wakauliza: ‘Unataka tukawanunulie mikate?’ Filipo, ambaye alikuwa mmoja wa mitume akasema hivi: ‘Hata ikiwa tungekuwa na pesa nyingi hatungeweza kununua mikate kwa ajili ya watu wote hawa.’
Yesu akauliza: ‘Tuna chakula kiasi gani?’ Andrea akamjibu: ‘Tuna mikate mitano na samaki wawili wadogo. Lakini kwa kweli chakula hicho hakitoshi.’ Yesu akasema: ‘Leteni hapa mikate hiyo na samaki.’ Kisha, akauambia umati uketi kwenye vikundi vya watu 50 na 100. Yesu akachukua mikate na samaki, akatazama juu mbinguni, na kusali. Kisha, akawapatia mitume, nao wakawagawia watu. Wanaume 5,000 pamoja na wanawake na watoto waliokuwepo, wakala mpaka wakashiba. Baada ya hapo, mitume wakakusanya chakula kilichokuwa kimebaki, kwa hiyo hakuna chochote kilichotupwa. Wakajaza vikapu 12! Huo ulikuwa muujiza wa kustaajabisha, sivyo?
Watu walifurahi sana hivi kwamba wakataka kumfanya Yesu awe mfalme wao. Lakini Yesu alijua kwamba wakati wa Yehova kumweka awe mfalme haukuwa umefika. Kwa hiyo, akawaruhusu watu waondoke na kuwaagiza mitume waende upande ule mwingine wa Bahari ya Galilaya. Mitume walipanda mashua, lakini Yesu akaenda mlimani akiwa peke yake. Kwa nini? Kwa sababu alitaka kusali kwa Baba yake. Hata alipokuwa na mambo mengi sana, sikuzote Yesu alitenga wakati wa kusali.
“Msifanye kazi kwa ajili ya chakula kinachoharibika, bali kwa ajili ya chakula kinachodumu kufikia uzima wa milele, ambacho Mwana wa binadamu atawapa ninyi.”—Yohana 6:27
-
-
Yesu Anatembea Juu ya MajiMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 84
Yesu Anatembea Juu ya Maji
Zaidi ya kuwaponya wagonjwa na kuwafufua wafu, Yesu alikuwa na uwezo wa kudhibiti dhoruba na mvua. Baada ya kusali pale mlimani, Yesu aliona dhoruba kwenye Bahari ya Galilaya. Mitume wake walikuwa kwenye mashua wakijitahidi kupiga makasia licha ya dhoruba kali. Yesu alishuka kutoka mlimani na kuanza kutembea juu ya maji akielekea kwenye mashua yao. Mitume walipomwona mtu akitembea juu ya maji, waliogopa sana. Lakini Yesu akawaambia hivi: ‘Ni mimi, msiogope.’
Petro akasema: ‘Bwana, ikiwa kweli ni wewe, niamuru nije kwako.’ Yesu akamwambia Petro: ‘Njoo.’ Kwa hiyo, dhoruba ilipokuwa ikiendelea, Petro akatoka kwenye mashua na kuanza kutembea juu ya maji kumwelekea Yesu. Lakini, alipomkaribia Yesu, Petro akaitazama ile dhoruba, akaogopa na kuanza kuzama. Petro akapaza sauti: ‘Bwana, niokoe!’ Yesu akamshika mkono, na kumuuliza: ‘Kwa nini umeingiwa na shaka? Imani yako iko wapi?’
Yesu na Petro wakaingia kwenye mashua, na mara moja ile dhoruba ikatulia. Wazia jinsi mitume walivyohisi! Walisema hivi: “Kwa kweli wewe ni Mwana wa Mungu.”
Huu haukuwa wakati pekee ambao Yesu alidhibiti hali ya hewa. Wakati fulani Yesu alipokuwa pamoja na mitume wake wakivuka kuelekea upande ule mwingine wa bahari, Yesu alilala usingizi kwenye mashua. Alipokuwa amelala, dhoruba kali ikatokea. Mawimbi yakaipiga mashua, nayo ikajaa maji. Mitume wakamwamsha Yesu wakisema hivi kwa sauti kubwa: ‘Mwalimu, tunakaribia kufa! Tusaidie!’ Yesu akaamka na kuiambia hivi bahari: “Nyamaza!” Mara moja, upepo ukaacha kuvuma na bahari ikatulia. Yesu akawauliza hivi mitume: ‘Imani yenu iko wapi?’ Wakaanza kuzungumza wenyewe kwa wenyewe wakisema: “[Hata] upepo na bahari vinamtii.” Mitume walijifunza kwamba ikiwa watamtegemea Yesu kikamili, hawatahitaji kuogopa kitu chochote.
“Ningekuwa wapi ikiwa singekuwa na imani kwamba nitauona wema wa Yehova katika nchi ya walio hai?”—Zaburi 27:13
-
-
Yesu Aponya Siku ya SabatoMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 85
Yesu Aponya Siku ya Sabato
Mafarisayo walimchukia Yesu, na walitafuta sababu za kumkamata. Walidai kwamba hakupaswa kuponya wagonjwa siku ya Sabato. Katika siku fulani ya Sabato, Yesu alikutana na mwanamume kipofu akiombaomba barabarani. Yesu akawaambia wanafunzi wake: ‘Oneni jinsi nguvu za Mungu zitakavyomponya mwanamume huyu.’ Yesu akatema mate kwenye udongo akatengeneza tope, kisha, akapaka kwenye macho ya yule mwanamume. Halafu akamwambia: “Nenda ukanawe katika dimbwi la Siloamu.” Mwanamume huyo akafanya kama alivyoagizwa, na kwa mara ya kwanza maishani akaanza kuona.
Watu walishangaa sana. Wakawa wakiulizana hivi: ‘Je, huyu ni yule aliyekuwa akiketi na kuombaomba au ni mtu mwingine anayefanana naye?’ Mwanamume huyo akawajibu: ‘Ni mimi niliyezaliwa kipofu!’ Nao wakamuuliza: ‘Macho yako yalifunguliwaje?’ Alipowasimulia jambo lililotokea, wakampeleka kwa Mafarisayo.
Mwanamume huyo akawaambia Mafarisayo hivi: ‘Yesu alinipaka tope katika macho, kisha, akaniambia niende nikanawe. Nilifanya hivyo, na sasa ninaona.’ Mafarisayo wakasema: ‘Ikiwa Yesu anaponya siku ya Sabato, basi nguvu zake hazitoki kwa Mungu.’ Wengine wakasema: ‘Ikiwa nguvu zake hazitoki kwa Mungu, asingeweza kuponya.’
Mafarisayo wakawaita wazazi wa mtu huyo na kuwauliza: ‘Ni nini kilichofanya mtoto wenu aanze kuona?’ Wazazi waliogopa kwa sababu Mafarisayo walikuwa wamesema kwamba ikiwa mtu yeyote angemwamini Yesu angefukuzwa katika sinagogi. Kwa hiyo, wakajibu hivi: ‘Hatujui. Muulizeni mwenyewe.’ Mafarisayo wakaendelea kumuuliza maswali yule mwanamume, hatimaye akasema: ‘Nimewaambia kila kitu. Kwa nini mnaendelea kuniuliza?’ Mafarisayo wakakasirika na kuamua kumfukuza.
Yesu akamtafuta mwanamume huyo na alipompata akamuuliza hivi: ‘Je, unamwamini Masihi?’ Mtu huyo akamjibu: ‘Ikiwa ningemjua ningemwamini.’ Yesu akamwambia: ‘Mimi ndiye Masihi.’ Kwa kweli, Yesu alimtendea mtu huyo kwa fadhili, sivyo? Hakumponya tu mwanamume huyo bali alimsaidia pia kuwa na imani.
“Ninyi mmekosea, kwa sababu hamjui Maandiko wala nguvu za Mungu.”—Mathayo 22:29
-
-
Yesu Amfufua LazaroMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 86
Yesu Amfufua Lazaro
Yesu alikuwa na marafiki watatu wa karibu sana ambao waliishi Bethania. Marafiki hao walikuwa Lazaro na dada zake wawili, Maria na Martha. Siku moja, Yesu alipokuwa ng’ambo ya Yordani, Maria na Martha walimtumia ujumbe huu wa dharura: ‘Lazaro ni mgonjwa sana. Tafadhali, njoo upesi!’ Hata hivyo, Yesu hakwenda mara moja. Alisubiri kwa siku mbili zaidi, kisha, akawaambia wanafunzi wake: ‘Twendeni Bethania. Lazaro amelala, nami ninaenda kumwamsha.’ Mitume wakamwambia hivi: ‘Ikiwa Lazaro amelala, hiyo itamsaidia kupata nafuu.’ Kwa hiyo, Yesu akawaambia hivi waziwazi: ‘Lazaro amekufa.’
Yesu alipofika Bethania, siku nne zilikuwa zimepita tangu Lazaro alipozikwa. Umati mkubwa wa watu ulikuwa umekuja kuwafariji Martha na Maria. Baada ya Martha kusikia kwamba Yesu amekuja, alikimbia ili akampokee. Akamwambia hivi: “Bwana, kama ungekuwa hapa ndugu yangu hangekufa.” Yesu akamwambia: ‘Ndugu yako atafufuka. Martha, unaamini jambo hilo?’ Akajibu: ‘Ninaamini kwamba atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.’ Yesu akamwambia: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.”
Kisha, Martha akaenda kwa Maria na kumwambia: ‘Yesu amekuja.’ Maria akatoka na kumkimbilia Yesu, nao umati ukamfuata. Alipofika, akaanguka miguuni pake huku akibubujikwa na machozi. Akamwambia Yesu: ‘Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yetu hangekufa.’ Yesu alipoona jinsi Maria alivyohuzunika, yeye pia akatokwa na machozi. Umati ulipomwona akilia, wakasema: ‘Ona, jinsi Yesu alivyompenda Lazaro.’ Lakini wengine wakawa wakiuliza: ‘Kwa nini hakuzuia rafiki yake asife?’ Yesu angefanya nini?
Yesu alienda kwenye kaburi ambalo lilikuwa limefunikwa kwa jiwe kubwa. Akawaamuru na kusema: “Liondoeni jiwe.” Martha akajibu: ‘Lakini siku nne zimepita! Mwili wake utakuwa unanuka.’ Hata hivyo, wakaliondoa jiwe, naye Yesu akasali na kusema: ‘Baba, ninakushukuru kwamba umenisikia. Ninajua kwamba sikuzote wewe hunisikia; lakini ninasema kwa sauti ili watu hawa waamini kwamba umenituma.’ Kisha, akaita kwa sauti kubwa: “Lazaro, njoo huku nje!” Jambo la kushangaza likatokea: Lazaro akatoka kaburini, akiwa bado amefungwa kwa vitambaa. Yesu akawaambia: ‘Mfungueni, mwacheni aende.’
Wengi walioshuhudia ufufuo huo wakaanza kumwamini Yesu. Lakini wengine wakaenda na kuwaambia Mafarisayo. Tangu siku hiyo, Mafarisayo wakapanga njama ya kumuua Lazaro na Yesu. Yuda Iskariote, mmoja wa wale mitume 12, akaenda kisiri kwa Mafarisayo na kuwauliza: ‘Mtanipa nini nikiwasaidia kumkamata Yesu?’ Wakakubaliana kumlipa vipande 30 vya fedha, hivyo, Yuda akawa akitafuta nafasi ya kumsaliti Yesu kwa Mafarisayo.
“Kwetu, Mungu wa kweli ni Mungu anayeokoa; Na Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu huokoa kutoka katika kifo.”—Zaburi 68:20
-
-
Mlo wa Mwisho wa Jioni wa YesuMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 87
Mlo wa Mwisho wa Yesu
Wayahudi walisherehekea Pasaka kila mwaka katika siku ya 14 ya mwezi wa Nisani. Hilo liliwakumbusha jinsi Yehova alivyowakomboa kutoka katika utumwa nchini Misri na kuwaleta kwenye Nchi ya Ahadi. Katika mwaka wa 33 W.K., Yesu na mitume wake walisherehekea Pasaka katika chumba cha juu jijini Yerusalemu. Mwishoni mwa mlo huo, Yesu alisema hivi: ‘Mmoja wenu atanisaliti.’ Mitume walishtuka na kumuuliza Yesu: ‘Ni nani huyo?’ Yesu alijibu: ‘Ni mtu ambaye nitampa mkate huu.’ Kisha, akampa mkate Yuda Iskariote. Mara moja, Yuda akaondoka katika chumba hicho.
Baada ya hapo, Yesu akasali, akaumega mkate vipande-vipande, na kuwagawia mitume waliokuwepo. Akasema hivi: ‘Kuleni mkate huu, unawakilisha mwili wangu, ambao nitautoa kwa ajili yenu.’ Halafu, akasali kwa ajili ya divai na kuwapa mitume wake. Akasema: ‘Kunyweni divai hii, inawakilisha damu yangu, ambayo nitaitoa ili msamehewe dhambi zenu. Ninawaahidi kwamba mtakuwa wafalme pamoja nami mbinguni. Fanyeni hivi kila mwaka, ili kunikumbuka.’ Wafuasi wa Yesu hukutana jioni ya Nisani 14 kila mwaka. Mkutano huo unaitwa Mlo wa Jioni wa Bwana.
Baada ya mlo huo, mitume wakaanza kubishana kuhusu ni nani aliye mkuu kati yao. Lakini Yesu akawaambia: ‘Yule aliye mkuu kati yenu ni yule ambaye anajiona kuwa mdogo zaidi.
‘Ninyi ni rafiki zangu. Ninawaambia kila kitu ambacho Baba anataka niwaambie. Baada ya muda mfupi nitaenda kwa Baba yangu aliye mbinguni. Nitawaacha ninyi, na watu watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu mkiwa na upendo kati yenu wenyewe. Mnapaswa kupendana kama vile mimi nilivyowapenda.’
Mwishowe, Yesu alisali akimwomba Yehova awalinde wanafunzi wake wote. Alimwomba Yehova awasaidie wanafunzi wake wafanye kazi kwa amani. Alisali ili jina la Yehova litakaswe. Kisha, Yesu na mitume wake waliimba nyimbo za kumsifu Yehova na kuondoka. Wakati wa Yesu kukamatwa ulikuwa umekaribia.
“Msiogope, ninyi kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa Ufalme.”—Luka 12:32
-
-
Yesu AkamatwaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 88
Yesu Akamatwa
Yesu na mitume wake walitembea katika Bonde la Kidroni wakienda kwenye Mlima wa Mizeituni. Ilikuwa ni usiku na mwezi ulikuwa mpevu kabisa. Walipofika katika bustani ya Gethsemane, Yesu aliwaambia hivi: “Kaeni hapa na mwendelee kukesha.” Kisha, akaenda mbele kidogo katika bustani na kupiga magoti. Akiwa na uchungu mwingi alisali hivi kwa Yehova: “Acha mapenzi yako yatendeke.” Kisha, Yehova akamtuma malaika ili amwimarishe Yesu. Yesu aliporudi kwa mitume, alikuta watatu kati yao wakiwa wamelala. Akawaambia hivi: ‘Amkeni! Huu si wakati wa ninyi kulala! Saa imefika ya mimi kutiwa katika mikono ya adui zangu.’
Muda mfupi baadaye, Yuda alikuja akiwa na kundi kubwa la watu wenye mapanga na marungu. Alikuwa anajua mahali ambapo Yesu anaweza kupatikana kwa sababu walizoea kuja naye katika bustani hiyo mara kwa mara. Yuda alikuwa amewaambia askari kwamba atawaonyesha Yesu. Hivyo, alienda moja kwa moja kwa Yesu na kusema: ‘Habari, Mwalimu,’ na kisha, akambusu. Yesu akamuuliza: ‘Yuda unanisaliti kwa kunibusu?’
Yesu akasogea mbele na kuuliza umati huo hivi: “Mnamtafuta nani?” Wakasema: “Yesu Mnazareti.” Akawajibu: “Mimi ndiye,” na mara moja wanaume hao wakarudi nyuma na kuanguka chini. Kwa mara nyingine Yesu akawauliza: “Mnamtafuta nani?” Wakamjibu: “Yesu Mnazareti.” Yesu akawajibu: ‘Nimewaambia mimi ndiye. Waacheni hawa waende zao.’
Petro alipoona kile kilichokuwa kikiendelea, alichomoa upanga wake na kukata sikio la Malko, mtumishi wa kuhani mkuu. Lakini Yesu akagusa sikio la mwanamume huyo na kumponya. Kisha, akamwambia Petro hivi: ‘Rudisha upanga wako mahali pake. Ukipigana kwa upanga, utakufa kwa upanga.’ Askari wakamkamata Yesu na kumfunga mikono, lakini mitume wakakimbia. Kisha, umati ukampeleka Yesu kwa Anasi. Anasi alimhoji Yesu, halafu akamtuma kwa Kayafa aliyekuwa Kuhani Mkuu mwaka huo. Lakini ni nini kilichotokea kwa mitume?
“Ulimwenguni mtapata dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 16:33
-
-
Petro Anamkana YesuMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 89
Petro Anamkana Yesu
Yesu alipokuwa na mitume wake katika chumba cha juu, aliwaambia hivi: ‘Usiku wa leo, ninyi nyote mtanikimbia.’ Petro akasema: ‘Sitakuacha! Hata ikiwa wengine wote watakuacha, mimi sitakuacha.’ Lakini Yesu akamwambia hivi: ‘Kabla ya jogoo kuwika, utanikana mara tatu.’
Askari walipomchukua Yesu na kumpeleka kwa Kayafa, wengi kati ya mitume walikimbia. Hata hivyo, mitume wawili waliufuata umati kwa nyuma. Mmoja kati yao alikuwa Petro. Aliingia katika ua wa nyumba ya Kayafa na kuanza kuota moto. Kwa sababu ya mwanga wa moto, kijakazi mmoja alimwona Petro na kumwambia: ‘Ninakujua! Wewe ulikuwa pamoja na Yesu!’
Petro akamjibu: “Simjui wala sielewi unachosema.” Kisha, akatoka na kuelekea nje ya ua. Lakini baada ya muda kijakazi mwingine akamwona na kuuambia umati wa watu hivi: ‘Mtu huyu alikuwa pamoja na Yesu!’ Petro akajibu: ‘Mimi hata simjui Yesu!’ Mwanamume mwingine akasema: ‘Wewe ulikuwa pamoja naye! Njia yako ya kuzungumza inaonyesha kwamba wewe ni Mgalilaya, kama Yesu.’ Lakini Petro akaapa na kusema: ‘Simjui mtu huyo!’
Wakati huohuo, jogoo akawika. Petro akamwona Yesu akigeuka na kumtazama. Akayakumbuka maneno ya Yesu, halafu akatoka nje na kulia kwa uchungu.
Mambo hayo yalipokuwa yakiendelea, Sanhedrini iliamua kusikiliza kesi ya Yesu katika nyumba ya Kayafa. Walikuwa wameamua kwamba watamuua Yesu, sasa walikuwa wanamtafutia kosa. Hata hivyo, hawakupata kosa lolote dhidi yake. Mwishowe, Kayafa akamuuliza Yesu hivi moja kwa moja: ‘Je, wewe ni Mwana wa Mungu?’ Yesu akajibu: ‘Ndiyo.’ Kayafa akasema: ‘Amekufuru! Hatuhitaji ushahidi wa ziada.’ Kisha, wote wakakubaliana kwamba, ‘mtu huyu anastahili kufa.’ Wakampiga makofi, wakamtemea mate, na kumfunika usoni wakisema: ‘Ikiwa wewe ni nabii, tuambie ni nani aliyekupiga!’
Kulipopambazuka, walimchukua Yesu na kumpeleka katika Sanhedrini, kisha wakamuuliza hivi: ‘Je, wewe ni Mwana wa Mungu?’ Yesu akawajibu: ‘Ninyi mnasema kwamba mimi ndiye.’ Wakamhukumu kuwa na hatia ya kukufuru na baadaye wakampeleka kwa Pontio Pilato, Gavana wa Roma. Ni nini kilichotukia baada ya hapo? Acha tuone.
“Saa inakuja . . . wakati kila mmoja wenu atatawanyika na kwenda nyumbani kwake, nanyi mtaniacha peke yangu. Lakini siko peke yangu, kwa sababu Baba yuko pamoja nami.”—Yohana 16:32
-
-
Yesu Afa Huko GolgothaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 90
Yesu Afa Huko Golgotha
Wakuu wa makuhani wakamchukua Yesu na kumpeleka kwenye jumba la gavana. Pilato akawauliza hivi: ‘Mna mashtaka gani dhidi ya mwanamume huyu?’ Wakasema hivi: ‘Anadai kwamba yeye ni mfalme!’ Pilato akamuuliza Yesu, “Je, wewe ndiye mfalme wa Wayahudi?” Yesu akajibu: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.”
Kisha Pilato akamtuma Yesu kwa Herode, mtawala wa Galilaya, aone ikiwa angepata kosa lolote juu yake. Herode hakuweza kupata jambo lolote la kumshtaki Yesu na hivyo akamtuma tena kwa Pilato. Kisha Pilato akawaambia watu hivi: ‘Mimi wala Herode hatujapata kosa lolote dhidi ya mwanamume huyu. Nitamwachilia huru.’ Umati ukapiga kelele na kusema: ‘Muue! Muue!’ Askari wakampiga Yesu kwa mjeledi, wakamtemea mate, na kumpiga ngumi. Wakamvisha taji la miiba juu ya kichwa chake na kumdhihaki wakisema: ‘Siku njema, ewe Mfalme wa Wayahudi.’ Kwa mara nyingine Pilato akawaambia watu: ‘Sijaona kosa lolote juu ya mtu huyu.’ Lakini wakapiga kelele na kusema: “Atundikwe mtini!” Hivyo, Pilato akamtoa ili akauawe.
Wakampeleka Yesu mahali panapoitwa Golgotha, wakampigilia misumari kwenye mti na kisha wakainua mti huo. Yesu akasali hivi: ‘Baba, wasamehe kwa kuwa hawajui wanachokifanya.’ Watu wakamdhihaki Yesu wakisema: ‘Ikiwa wewe ni Mwana wa Mungu, shuka kutoka kwenye mti! Jiokoe.’
Mhalifu mmoja aliyekuwa ametundikwa kando yake akasema hivi: “Unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu akamwahidi hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” Ilipofika mchana, kukawa na giza juu ya nchi kwa saa tatu. Baadhi ya wanafunzi walisimama karibu na mti huo, kutia ndani Maria, mama ya Yesu. Yesu akamwambia Yohana amtunze Maria kama ambavyo angemtunza mama yake mzazi.
Mwishowe, Yesu akasema: “Imetimizwa!” Akainamisha kichwa chake na kukata pumzi. Wakati huohuo, tetemeko kubwa la ardhi likatokea. Ndani ya hekalu, lile pazia zito lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi likararuka katikati. Ofisa mmoja wa jeshi akasema: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”
“Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa ‘ndiyo’ kupitia yeye.”—2 Wakorintho 1:20
-
-
Yesu AfufuliwaMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 91
Yesu Afufuliwa
Baada ya Yesu kufa, mwanamume fulani tajiri, aliyeitwa Yosefu, alimwomba Pilato amruhusu autoe mwili wa Yesu kutoka mtini. Yosefu akaufunga mwili wa Yesu kwa kitani bora na kuupaka manukato na kisha kuulaza ndani ya kaburi jipya. Pia akaviringisha jiwe kubwa kwenye mwingilio. Wakuu wa makuhani wakamwambia hivi Pilato: ‘Tunahofia kwamba baadhi ya wanafunzi wa Yesu watachukua mwili wake na baadaye watasema kwamba amefufuliwa.’ Hivyo Pilato akawaambia: ‘Funikeni mwingilio wa kaburi na mweke walinzi.’
Siku tatu baadaye, asubuhi na mapema, baadhi ya wanawake wakaenda kwenye kaburi na kupata kwamba jiwe lilikuwa limeondolewa. Ndani ya kaburi kulikuwa na malaika aliyewaambia hivi wanawake hao: ‘Msiogope. Yesu amefufuliwa. Nendeni mkawaambie wanafunzi wake wakakutane naye huko Galilaya.’
Maria Magdalene akaondoka haraka kwenda kuwatafuta Petro na Yohana. Akawaambia hivi: ‘Mtu fulani ameuchukua mwili wa Yesu!’ Petro na Yohana wakakimbia kwenda kaburini. Walipoona kwamba kaburi lilikuwa tupu, wakarudi nyumbani.
Maria aliporudi kaburini, aliona malaika wawili ndani na kuwaambia hivi: ‘Sijui walipompeleka Bwana wangu.’ Kisha akamwona mwanamume fulani, na akifikiri kwamba alikuwa mtunza-bustani, akasema: ‘Bwana, tafadhali niambie ulipomlaza.’ Lakini mwanamume huyo aliposema, “Maria!” akatambua kwamba alikuwa Yesu. Akalia na kusema: “Mwalimu!” na kumng’ang’ania. Yesu akamwambia hivi: ‘Nenda kwa ndugu zangu nawe uwaambie kwamba umeniona.’ Mara moja, Maria akakimbia kwa wanafunzi na kuwaambia kwamba amemwona Yesu.
Baadaye siku hiyo, wanafunzi wawili walikuwa wakitembea kutoka Yerusalemu kwenda Emau. Mwanamume fulani akajiunga nao na kuwauliza walikuwa wakizungumza kuhusu nini. Wakasema: ‘Je, hujasikia? Siku tatu zilizopita wakuu wa makuhani walimuua Yesu. Sasa wanawake fulani wanasema kwamba yuko hai!’ Mwanamume huyo akauliza hivi: ‘Je, hamuwaamini manabii? Walisema kwamba Kristo atakufa na kufufuliwa.’ Na akaendelea kuwaeleza maana ya Maandiko. Walipofika Emau, wanafunzi wakamwomba ajiunge nao. Wakati wa mlo wa jioni baada ya kusali kwa ajili ya mkate, wakatambua kwamba alikuwa Yesu. Kisha akatoweka.
Wanafunzi hao wawili wakafanya haraka kwenda Yerusalemu kwenye nyumba ambayo mitume walikuwa wamekutanika na wakawaambia kilichotokea. Walipokuwa kwenye nyumba hiyo, Yesu akatokea mbele yao wote. Mwanzoni mitume hawakuamini kwamba alikuwa Yesu. Kisha akasema hivi: ‘Tazameni mikono yangu; niguseni. Iliandikwa kwamba Kristo angefufuka kutoka kwa wafu.’
“Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.”—Yohana 14:6
-
-
Yesu Awatokea WavuviMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 92
Yesu Awatokea Wavuvi
Muda fulani baada ya Yesu kuwatokea mitume, Petro aliamua kwenda kuvua samaki katika Bahari ya Galilaya. Tomasi, Yakobo, Yohana, na baadhi ya wanafunzi wengine wakaenda pamoja naye. Walijaribu kuvua samaki usiku kucha lakini hawakupata chochote.
Mapema asubuhi iliyofuata, walimwona mwanamume akiwa amesimama ufuoni. Akawauliza hivi akiwa ufuoni: ‘Je, mmepata samaki wowote?’ Wakamwambia, “Hapana!” Mwanamume huyo akasema, “Utupeni wavu upande wa kulia wa mashua.” Walipofanya hivyo, wavu ukajaa samaki wengi sana hivi kwamba hawakuweza kuuvuta. Mara moja Yohana akatambua kwamba mwanamume huyo alikuwa Yesu, naye akasema: “Ni Bwana!” Papo hapo, Petro akajitumbukiza ndani ya maji na kuogelea hadi ufuoni. Wanafunzi wengine wakamfuata kwa mashua.
Walipofika ufuoni, wakaona mkate na samaki vikipikwa juu ya moto. Yesu akawaambia walete baadhi ya samaki waliowavua wawaongezee kwenye mlo wao. Kisha akawaambia hivi: “Njooni, mpate kiamshakinywa.”
Baada ya kula kiamshakinywa, Yesu akamuuliza hivi Petro: ‘Je, unanipenda kuliko unavyopenda kuvua samaki?’ Petro akasema, “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.” Yesu akamwambia, ‘Basi walishe wanakondoo wangu.’ Yesu akamuuliza tena: ‘Petro, unanipenda?’ Petro akasema, ‘Bwana, unajua ninakupenda.’ Yesu akamwambia, “Chunga kondoo wangu wadogo.” Yesu akauliza mara ya tatu. Petro akahuzunika sana. Akasema, “Bwana, wewe unajua mambo yote; unajua kwamba ninakupenda.” Yesu akasema, “Lisha kondoo wangu wadogo.” Kisha akamwambia Petro hivi: “Endelea kunifuata.”
“[Yesu] akawaambia: ‘Nifuateni, nami nitawafanya muwe wavuvi wa watu.’ Mara moja wakaziacha nyavu zao na kumfuata.”—Mathayo 4:19, 20
-
-
Yesu Arudi MbinguniMasomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
-
-
SOMO LA 93
Yesu Arudi Mbinguni
Alipokuwa Galilaya, Yesu alikutana na wafuasi wake. Aliwapa amri hii muhimu sana: ‘Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. Wafundisheni mambo niliyowafundisha, na kuwabatiza.’ Kisha akawaahidi hivi: ‘Kumbukeni, nitakuwa pamoja nanyi sikuzote.’
Kwa siku 40 hivi baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea mamia ya wanafunzi wake huko Galilaya na Yerusalemu. Aliwafundisha mambo muhimu na kufanya miujiza mingi. Kisha Yesu akakutana na mitume wake kwa mara ya mwisho kwenye Mlima wa Mizeituni. Akasema hivi: ‘Msiondoke Yerusalemu. Endeleeni kusubiri kile ambacho Baba aliwaahidi.’
Mitume wake hawakuelewa alichokuwa akimaanisha. Wakamwuliza hivi: ‘Sasa utakuwa Mfalme wa Israeli?’ Yesu akasema, ‘Wakati wa Yehova wa kuniweka niwe Mfalme haujafika. Hivi karibuni mtapokea nguvu kupitia roho takatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu. Nendeni mkahubiri katika Yerusalemu, Yudea, Samaria, na mpaka sehemu za mbali zaidi za dunia.’
Kisha Yesu akainuliwa juu angani na wingu likamfunika. Wanafunzi wake wakaendelea kutazama angani, lakini hakuwapo tena.
Wanafunzi wakaondoka kwenye Mlima wa Mizeituni na kwenda Yerusalemu. Wakawa wakikutana pamoja kwa ukawaida katika chumba cha juu na kusali. Walikuwa wakimsubiri Yesu awape maagizo zaidi.
“Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14
-