28 “Kwa kweli, kuna mahali pa kupata fedha
Na mahali pa dhahabu ambayo wanasafisha;+
2 Chuma hutolewa katika mavumbi+
Na shaba humwagwa kutoka katika mawe.
3 Ameweka mwisho wa giza;
Naye hutafuta mipaka yote+
Jiwe katika giza na kivuli kizito.
4 Amechimba shimo mbali sana na mahali ambapo watu hukaa ugenini,+
Mahali paliposahauliwa, mbali na mguu;
Baadhi ya wanadamu wanaoweza kufa wameshuka chini, wamening’inia.
5 Kwa habari ya dunia, chakula hutoka humo;+
Lakini chini yake, imepinduliwa kana kwamba ni kwa moto.
6 Mawe yake ni mahali pa yakuti,+
Nayo ina vumbi la dhahabu.
7 Njia—hakuna ndege mwenye kuwinda+ ambaye ameijua,
Wala jicho la mwewe mweusi+ halikuiona.
8 Wanyama wa mwituni wenye fahari hawajaikanyaga ikawa ngumu;
Mwana-simba hakutembea juu yake.
9 Ametia mkono wake juu ya jiwe gumu;
Ameipindua milima kutoka katika mizizi yake;
10 Amechimba ndani ya miamba mifereji iliyojaa maji,+
Na jicho lake limeona vitu vyote vyenye thamani.
11 Ametengeneza bwawa mahali ambapo mito ilitiririka,+
Naye hukileta katika nuru kitu kilichofichwa.
12 Lakini hekima—inaweza kupatikana wapi,+
Na sasa, pako wapi mahali pa uelewaji?
13 Mwanadamu anayeweza kufa hajajua thamani yake,+
Nayo haipatikani katika nchi ya walio hai.
14 Kilindi cha maji kimesema,
‘Haimo ndani yangu!’
Bahari pia imesema, ‘Haipo pamoja nami!’+
15 Dhahabu safi haiwezi kubadilishwa nayo,+
Wala fedha haiwezi kupimwa kuwa bei yake.
16 Haiwezi kulipiwa kwa dhahabu ya Ofiri,+
Wala kwa jiwe la shohamu lisilopatikana kwa urahisi wala yakuti.
17 Dhahabu na kioo haviwezi kulinganishwa nayo,
Wala chombo chochote cha dhahabu safi hakiwezi kubadilishwa nayo.
18 Marijani+ na fuwele ya mawe havitatajwa,
Bali mfuko uliojaa hekima ni wenye thamani kuliko ule uliojaa lulu.+
19 Topazi+ ya Kushi haiwezi kulinganishwa nayo;
Haiwezi kulipiwa hata kwa dhahabu safi.
20 Lakini hekima—hiyo inatoka wapi,+
Na sasa, pako wapi mahali pa uelewaji?
21 Imefichwa kutoka machoni pa kila mtu aliye hai,+
Nayo imefichwa kutoka kwa viumbe vinavyoruka vya mbinguni.
22 Maangamizi na kifo zimesema,
‘Tumesikia habari zake kwa masikio yetu.’
23 Mungu, Yeye ndiye ameelewa njia yake,+
Naye mwenyewe amejua mahali pake,
24 Kwa maana yeye anatazama mpaka miisho ya dunia;+
Anaona chini ya mbingu zote,
25 Ili kuupima upepo,+
Naye ameyapima maji kwa kipimo;+
26 Alipofanyiza sharti kwa ajili ya mvua,+
Na njia kwa ajili ya wingu la dhoruba lenye kunguruma,
27 Ndipo alipoiona hekima kisha akasema habari zake;
Aliitayarisha na pia akaichunguza kabisa.
28 Naye akamwambia mwanadamu,
‘Tazama! Kumwogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima,+
Na kuacha ubaya ni uelewaji.’”+