Waroma
15 Ingawa hivyo, sisi tulio na nguvu twapaswa kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu, na si kuwa tukijipendeza wenyewe. 2 Acheni kila mmoja wetu ampendeze jirani yake katika lililo jema kwa ajili ya kujengwa kwake. 3 Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe; bali kama vile imeandikwa: “Mashutumu ya wale waliokuwa wakikushutumu yameniangukia mimi.” 4 Kwa maana mambo yote yaliyoandikwa wakati wa mbele yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini. 5 Sasa Mungu apaye uvumilivu na faraja na awaruhusu miongoni mwenu wenyewe mwe na mtazamo uleule wa akili aliokuwa nao Kristo Yesu, 6 ili kwa umoja nyinyi mpate kwa kinywa kimoja kumtukuza Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo.
7 Kwa hiyo karibishaneni, kama vile Kristo pia alivyotukaribisha sisi, kwa tazamio la utukufu kwa Mungu. 8 Kwa maana nasema kwamba kwa kweli Kristo alipata kuwa mhudumu wa wale waliotahiriwa kwa ajili ya ukweli wa Mungu, ili kuthibitisha ahadi ambazo Yeye aliwafanyia baba zao wa zamani, 9 na kwamba mataifa yapate kumtukuza Mungu kwa ajili ya rehema yake. Kama vile imeandikwa: “Hiyo ndiyo sababu hakika nitakukiri wewe waziwazi miongoni mwa mataifa na kwa jina lako hakika nitafanya melodia.” 10 Na tena asema: “Iweni na mteremo, nyinyi mataifa, pamoja na watu wake.” 11 Na tena: “Sifuni Yehova, nyinyi mataifa yote, na acheni vikundi vyote vya watu vimsifu yeye.” 12 Na tena Isaya asema: “Kutakuwa na mzizi wa Yese, na kutakuwa na mmoja ambaye anainuka ili kutawala mataifa; juu yake mataifa yataweka tumaini lao.” 13 Mungu atoaye tumaini na awajaze nyinyi shangwe yote na amani kwa kuamini kwenu, ili mpate kuzidi sana katika tumaini kwa nguvu ya roho takatifu.
14 Sasa mimi mwenyewe pia nashawishwa juu yenu, ndugu zangu, kwamba nyinyi wenyewe mmejaa wema pia, kwa kuwa mmejawa na ujuzi wote, na kwamba mwaweza pia kuonyana kwa upole. 15 Hata hivyo, ninawaandikia nyinyi kwa kusema waziwazi zaidi juu ya mambo fulani, kama kwamba ninawakumbusha nyinyi tena, kwa sababu ya fadhili isiyostahiliwa niliyopewa kutoka kwa Mungu 16 ili niwe mtumishi wa watu wote wa Kristo Yesu kwa mataifa, nikifanya kazi takatifu ya habari njema ya Mungu, ili toleo, yaani, mataifa haya, lipate kuthibitika kuwa lenye kukubalika, likiwa latakaswa kwa roho takatifu.
17 Kwa hiyo nina sababu ya kuchachawa katika Kristo Yesu kwa habari ya mambo yanayohusiana na Mungu. 18 Kwa maana hakika sitajasiria kusema jambo moja ikiwa hilo si kati ya mambo yale ambayo Kristo alifanya kupitia mimi ili mataifa yawe yenye utiifu, kwa njia ya neno na kitendo changu, 19 kwa nguvu ya ishara na mambo ya ajabu, kwa nguvu ya roho takatifu; hivi kwamba kutoka Yerusalemu na katika mzunguko hadi Ilirikamu nimehubiri kikamili habari njema juu ya Kristo. 20 Kwa kweli, katika njia hii, nilifanya iwe shabaha yangu kutotangaza habari njema mahali ambapo Kristo tayari alikuwa amekwisha kutajwa jina, ili nisipate kuwa nikijenga juu ya msingi wa mtu mwingine; 21 bali, kama vile imeandikwa: “Wale ambao hawajatangaziwa juu yake wataona, na wale ambao hawajasikia wataelewa.”
22 Kwa hiyo pia nilizuiwa mara nyingi nisiwafikie nyinyi. 23 Lakini sasa kwa kuwa sina tena eneo lisiloguswa katika mikoa hii, na kwa miaka kadhaa nikiwa nimekuwa na hamu sana ya kuwafikia nyinyi 24 wakati wowote ule nikiwa nimeshika njia yangu kwenda Hispania, natumaini, zaidi ya yote, niwapo safarini kuja huko, nipate kuwatazama nyinyi kidogo na kusindikizwa nanyi sehemu fulani ya njia ya kuja huko kwanza mimi nikiwa nimekwisha kutosheka na ushirika wenu kwa kadiri fulani. 25 Lakini sasa nakaribia kufunga safari kwenda Yerusalemu ili kuwahudumia watakatifu. 26 Kwa maana wale walio katika Makedonia na Akaya wamependezwa kushiriki vitu vyao kwa kuwatolea mchango fulani maskini kati ya watakatifu katika Yerusalemu. 27 Kweli, wamependezwa kufanya hivyo, na bado walikuwa wadeni kwao; kwa maana ikiwa mataifa wameshiriki mambo yao ya kiroho, wao pia wawiwa kuwahudumia hadharani kwa vitu ambavyo ni kwa ajili ya mwili wenye nyama. 28 Kwa sababu hiyo nikiisha kumaliza hili na kuwafikishia salama tunda hili, nitaondoka nikipitia kwenu kwenda Hispania. 29 Zaidi ya hayo, najua kwamba nijapo kwenu nitakuja na kipimo kamili cha baraka kutoka kwa Kristo.
30 Sasa nawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, kupitia Bwana wetu Yesu Kristo na kupitia upendo wa roho, kwamba mjikakamue wenyewe pamoja nami katika sala kwa Mungu kwa ajili yangu, 31 ili nipate kukombolewa kutoka kwa wale wasioamini katika Yudea na kwamba huduma yangu ambayo ni kwa ajili ya Yerusalemu ipate kuthibitika kuwa yenye kukubalika kwa watakatifu, 32 ili nifikapo kwenu na shangwe kwa mapenzi ya Mungu nitaburudishwa pamoja nanyi. 33 Mungu apaye amani na awe pamoja nanyi nyote. Ameni.