-
Marko 3:1-6Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
3 Yesu akaingia tena ndani ya sinagogi, na palikuwa na mtu aliyepooza mkono.+ 2 Basi walikuwa wakimwangalia sana waone kama atamponya mtu huyo siku ya Sabato, ili wamshtaki. 3 Akamwambia yule mtu aliyepooza mkono: “Simama uje hapa katikati.” 4 Kisha akawauliza: “Je, ni halali kufanya mema au kufanya mabaya siku ya Sabato, kuokoa uhai* au kuua?”+ Lakini wakanyamaza. 5 Akawatazama kwa hasira na kuhuzunika sana kwa sababu mioyo yao ilikuwa migumu,+ akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha mkono wake, nao ukapona. 6 Ndipo Mafarisayo wakaenda nje na mara moja wakafanya mkutano pamoja na wafuasi wa chama cha Herode+ ili wamuue Yesu.
-
-
Luka 6:6-11Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
6 Siku nyingine ya Sabato+ aliingia katika sinagogi, akaanza kufundisha. Kulikuwa na mtu aliyepooza mkono wa kulia.+ 7 Waandishi na Mafarisayo walikuwa wakimwangalia Yesu kwa makini ili waone kama angeponya katika siku ya Sabato, ili wapate sababu ya kumshtaki. 8 Hata hivyo, alijua mawazo yao,+ basi akamwambia yule mtu aliyepooza mkono: “Inuka usimame hapa katikati.” Naye akainuka na kusimama hapo. 9 Kisha Yesu akawauliza: “Je, ni halali kufanya mema au kufanya mabaya siku ya Sabato, kuokoa uhai* au kuuangamiza?”+ 10 Baada ya kuwatazama wote waliokuwapo, Yesu akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha, nao ukapona. 11 Lakini wakakasirika sana, wakaanza kushauriana kuhusu jambo ambalo wangemtendea Yesu.
-