-
Mathayo 14:15-21Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
15 Lakini ilipofika jioni, wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Mahali hapa hapana watu na muda umesonga sana; uambie umati uondoke, waende vijijini wakajinunulie chakula.”+ 16 Hata hivyo, Yesu akawaambia: “Si lazima waondoke; ninyi wapeni chakula.” 17 Wakamwambia: “Hatuna kitu hapa isipokuwa mikate mitano na samaki wawili tu.” 18 Akasema: “Nileteeni hapa.” 19 Akauagiza umati uketi kwenye nyasi. Kisha akachukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni, akatoa baraka+ na baada ya kuimega mikate, akawapa wanafunzi, nao wanafunzi wakaugawia umati. 20 Basi wote wakala wakashiba, nao wakakusanya vipande vilivyobaki, wakajaza vikapu 12.+ 21 Sasa wale waliokula walikuwa wanaume karibu 5,000, na pia wanawake na watoto wadogo.+
-
-
Marko 6:35-44Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
35 Ilipokaribia jioni wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Mahali hapa hapana watu, na muda umesonga sana.+ 36 Waambie waondoke, waende wakajinunulie chakula katika maeneo ya mashambani na vijiji vilivyo karibu.”+ 37 Akawajibu: “Ninyi wapeni chakula.” Nao wakamwambia: “Je, twende tukanunue mikate ya dinari* 200 na kuwapa watu wale?”+ 38 Akawaambia: “Mna mikate mingapi? Nendeni mkaangalie!” Baada ya kuhakikisha, wakasema: “Mikate mitano na samaki wawili.”+ 39 Akawaagiza watu wote waketi katika vikundi kwenye nyasi.+ 40 Basi wakaketi katika vikundi vya watu 100 na vya watu 50. 41 Akachukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni akatoa baraka.+ Kisha akaimega mikate na kuanza kuwapa wanafunzi ili wawape watu, naye akawagawanya wale samaki wawili kwa ajili ya watu wote. 42 Basi wote wakala wakashiba, 43 nao wakakusanya vipande vilivyobaki na kujaza vikapu 12, bila kuhesabu samaki.+ 44 Wale waliokula mikate hiyo walikuwa wanaume 5,000.
-
-
Yohana 6:5-13Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
5 Yesu alipoinua macho yake na kuona umati mkubwa ukija, akamuuliza Filipo: “Tutanunua wapi mikate ili watu hawa wale?”+ 6 Hata hivyo, aliuliza swali hilo ili kumjaribu, kwa maana alijua jambo alilokuwa karibu kufanya. 7 Filipo akamjibu: “Mikate ya dinari* 200 haiwezi kutosha hata tukimpa kila mmoja wao kipande kidogo.” 8 Mmoja wa wanafunzi wake aitwaye Andrea, ndugu ya Simoni Petro, akamwambia: 9 “Hapa kuna mvulana mdogo aliye na mikate mitano ya shayiri na samaki wawili wadogo. Je, hivi vitawatosha watu wengi hivi?”+
10 Yesu akasema: “Waambieni watu waketi.” Basi mahali hapo palikuwa na nyasi nyingi, nao watu wakaketi, karibu wanaume 5,000.+ 11 Yesu akaichukua ile mikate, akatoa shukrani, kisha akawagawia wale waliokuwa wameketi hapo; pia akafanya vivyo hivyo na wale samaki wadogo, watu wote wakala na kushiba. 12 Waliposhiba akawaambia wanafunzi wake: “Kusanyeni vipande vilivyobaki, ili chochote kisipotee.” 13 Basi wakakusanya vipande vilivyobaki wakajaza vikapu 12 baada ya watu kula kutokana na ile mikate mitano ya shayiri.
-