Makusanyiko Yetu ya Wilaya—Ushuhuda Wenye Nguvu wa Ile Kweli
1. Sherehe za majira ziliwapa Waisraeli fursa ya kutafakari na kuzungumzia kweli gani muhimu za kiroho?
1 Waisraeli wa kale walikusanyika mara tatu kwa mwaka kwa ajili ya sherehe za majira. Ingawa ni wanaume pekee waliopaswa kuhudhuria, mara nyingi familia nzima-nzima zilisafiri hadi Yerusalemu kusherehekea makusanyiko hayo yenye furaha. (Kum. 16:15, 16) Matukio kama hayo yalikuwa fursa nzuri ya kutafakari na kuzungumzia kweli muhimu za kiroho. Ni nini baadhi ya kweli hizo? Moja ni kwamba Yehova ni Mwandalizi mkarimu, na mwenye upendo. (Kum. 15:4, 5) Nyingine ni kwamba tunaweza kumtegemea atupatie mwongozo na ulinzi. (Kum. 32:9, 10) Waisraeli pia wangetafakari kwamba kwa kuwa waliitwa kwa jina la Yehova, ni lazima waonyeshe uadilifu wake katika maisha yao. (Kum. 7:6, 11) Leo, makusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka yanatunufaisha vivyo hivyo.
2. Programu ya kusanyiko la wilaya itaangazia kweli katika njia gani?
2 Programu Huiangazia Kweli: Katika makusanyiko ya wilaya, sisi hufurahia hotuba, drama, maonyesho, na mahojiano ambayo hutusaidia kuelewa na kutumia kweli za Biblia vizuri zaidi. (Yoh. 17:17) Tayari, matayarisho mengi yamefanywa kwa ajili ya kusanyiko la mwaka huu. Tengenezo la Yehova linatayarisha programu ambayo imekusudiwa hasa kushughulikia mahitaji ya sasa ya ulimwenguni pote. (Mt. 24:45-47) Je, una hamu ya kuona na kusikia mambo ambayo yameandaliwa?
3. Ili tunufaike na programu, ni lazima tufanye nini?
3 Kwa kweli, tutanufaika kikamili ikiwa tutahudhuria siku zote tatu na kukaza kabisa fikira zetu kwenye programu. Ikiwa bado hujaomba ruhusa kazini, zungumza na mwajiri wako kuhusu jambo hilo. Hakikisha umepumzika vya kutosha kila usiku ili uwe macho wakati wa programu. Wengi wameona kwamba kumtazama msemaji na kuandika mambo makuu huwasaidia kukaza fikira. Usiruhusu simu au peja yako ikukengeushe au iwakengeushe wengine. Programu inapoendelea, epuka kula, au kunywa isipokuwa kwa sababu za kiafya au hali mbaya ya hewa. Ni vizuri pia kuepuka kuzungumza, au kuandika ujumbe kupitia simu.
4. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wafaidike na programu ya kusanyiko?
4 Katika miaka ya Sabato, familia za Waisraeli zilipokusanyika wakati wa Sherehe ya Mabanda ili kusikia Sheria ikisomwa, ‘watoto wao wadogo’ pia walikuwa pamoja nao “ili wasikilize na ili wajifunze.” (Kum. 31:12) Inafurahisha kama nini kuona familia zikiketi pamoja wakati wa kusanyiko na watoto wadogo wakikaa macho na kukaza fikira! Kila jioni, mnaweza kupitia pamoja mambo mliyoandika ambayo yaliyowafurahisha. Kwa kuwa “ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana,” inafaa wazazi wawachunge watoto wao, kutia ndani wale ambao ni vijana, wakati wa mapumziko ya mchana na wanapokuwa hotelini, badala ya ‘kuwaachilia.’—Met. 22:15; 29:15.
5. Mwenendo wetu mzuri tunapokuwa hotelini huipamba kweli katika njia gani?
5 Mwenendo Wetu Mzuri Huipamba Kweli: Mwenendo wetu mzuri tunapokuwa katika mji wa kusanyiko huipamba kweli. (Tito 2:10) Wafanyakazi wa hoteli hutambua wakati ambapo kikundi fulani cha watu kinafuata sheria za hoteli na kuwaonyesha subira na neema. (Kol. 4:6) Mwaka uliopita, wawakilishi wa ofisi ya tawi walipokuwa wakijadiliana na wasimamizi wa hoteli moja, mkurugenzi wa mauzo aliwaambia: “Tunapenda kuwa na watu wenu hotelini mwetu kwa sababu wao ni watu wazuri. Ni wenye adabu na fadhili, na siku zote wanaheshimu wafanyakazi wetu na mahali petu.”
6. Tunaweza kuipamba kweli jinsi gani kupitia mavazi yetu tunapokuwa katika mji wa kusanyiko?
6 Tunapovaa beji zetu za kusanyiko, tunatangaza tukio hilo, tunawawezesha wahudhuriaji wengine kututambua, na vilevile tunatoa ushahidi mzuri kwa wanaotutazama. Watu katika mji wa kusanyiko wataona kwamba wale waliovalia beji ya kusanyiko wamevalia mavazi nadhifu na yenye kiasi, na si yale yanayopendwa na ulimwengu huu ambayo ni ya kizembe na yenye kuwavutia watu kingono au kuudhi. (1 Tim. 2:9, 10) Hivyo basi, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mavazi na kujipamba kwetu tunapokuwa katika mji wa kusanyiko kutia ndani wakati tutakapowasili hotelini. Halingekuwa jambo linalofaa kufika hotelini huku tumevalia kaptura na T-shati. Hata kama kusanyiko linafanywa katika uwanja ulio wazi, mavazi yetu yanapaswa kuwa yenye heshima na nadhifu. Ikiwa tutabadili nguo zetu baada ya programu na kwenda kwenye mkahawa, tunapaswa kukumbuka kwamba sisi bado ni wahudhuriaji wa kusanyiko na hivyo hatupaswi kuvalia kizembe.
7. Njia moja ya kufurahia umoja wetu wa Kikristo ni ipi?
7 Katika sherehe za majira, Waisraeli walifurahia ushirika wenye kujenga pamoja na waabudu wenzao kutoka katika sehemu mbalimbali za taifa lao na za ulimwengu, na hilo lilichochea umoja. (Mdo. 2:1, 5) Wakati wa makusanyiko ya wilaya, undugu wetu wa Kikristo ambao ni wa pekee huonekana wazi kabisa. Kwa kawaida, undugu huo wenye kupendeza ambao ni sehemu ya paradiso yetu ya kiroho huwavutia watu wanaotutazama. (Zab. 133:1) Badala ya kuondoka kwenye eneo la kusanyiko wakati wa pumziko la mchana na kwenda kununua chakula, litakuwa jambo bora zaidi kujibebea chakula chepesi ili tuwe na fursa ya kufahamiana na kuzungumza na ndugu na dada walioketi karibu nasi.
8. Tuna sababu gani za kujitolea kufanya kazi ikiwa hali zetu zinaturuhusu?
8 Mara nyingi, watazamaji huvutiwa na makusanyiko yetu ambayo yamepangwa vizuri na yenye utaratibu, na hasa wanapojua kwamba kazi yote hufanywa na wajitoleaji. Je, unaweza ‘kujitoa kwa hiari’ kufanya kazi kusanyikoni? (Zab. 110:3) Mara nyingi, familia nzima-nzima hujitolea kufanya kazi kama njia ya kuwazoeza watoto wao wawe wakijitoa kuwasaidia wengine. Ikiwa wewe ni mwenye haya, kufanya kazi kusanyikoni ni njia nzuri ya kufahamiana na wahudhuriaji wengine. Dada mmoja alisema: “Isipokuwa familia yangu na marafiki wachache, sikuwafahamu watu wengi kusanyikoni. Lakini niliposaidia katika kufanya usafi, nilifahamiana na ndugu na dada wengi sana. Nilifurahia sana!” Tunapata shangwe tunapojitolea kufanya kazi kusanyikoni, kwa kuwa tunapanuka na kupata marafiki wengi zaidi. (2 Kor. 6:12, 13) Ikiwa hujawahi kujitolea, waombe wazee wakueleze jinsi unavyoweza kustahili kusaidia.
9. Tutawaalikaje wengine wahudhurie kusanyiko?
9 Waalike Wengine Waisikilize Kweli: Majuma matatu kabla ya kusanyiko letu kuanza, tutashiriki katika kampeni ya kuwaalika watu kwenye kusanyiko kama tulivyofanya miaka iliyotangulia. Makutaniko yatajitahidi kugawa mialiko katika sehemu kubwa iwezekanavyo ya eneo lao. (Ona sanduku “Tutaisambazaje Mialiko?”) Mialiko yoyote inayosalia inapaswa kuletwa kusanyikoni. Itatumiwa na wahudhuriaji wanapohubiri isivyo rasmi katika mji wa kusanyiko.
10. Simulia mambo yaliyoonwa yanayothibitisha kwamba kampeni ya kila mwaka ya kuwaalika watu kwenye kusanyiko huwa na matokeo.
10 Je, watu huhudhuria makusanyiko wanapoalikwa? Katika kusanyiko moja, mkaribishaji mmoja aliwasaidia wenzi fulani wa ndoa kupata mahali pa kuketi. Walimweleza kwamba walikuwa wameupokea mwaliko na “wakadhani kwamba tukio hilo litakuwa lenye kupendeza.” Ili kuhudhuria kusanyiko hilo, waliendesha gari kwa umbali wa zaidi ya kilometa 320! Katika kisa kingine, dada fulani aliyekuwa akiwapa watu mialiko nyumba kwa nyumba alimpata mwanamume fulani ambaye alitaka kujua mengi kuhusu kusanyiko hilo. Hivyo, akazungumza naye kuhusu mwaliko huo. Akiwa kusanyikoni siku chache baadaye, dada huyo alimwona yule mwanamume pamoja na rafiki yake, na walikuwa wamebeba mojawapo ya matoleo mapya!
11. Kwa nini ni muhimu kuhudhuria makusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka?
11 Sherehe za majira zilikuwa uandalizi wenye upendo kutoka kwa Yehova ili kuwasaidia Waisraeli ‘wamtumikie kwa njia isiyo na kosa na katika kweli.’ (Yos. 24:14) Vivyo hivyo, kuhudhuria makusanyiko ya wilaya ya kila mwaka hutusaidia ‘kuendelea kutembea katika kweli,’ na ni sehemu muhimu sana ya ibada yetu. (3 Yoh. 3) Yehova na awabariki wote wanaopenda kweli wanapofanya mipango ya kuhudhuria na kufaidika kikamili!
[Blabu katika ukurasa wa 3]
Mwenendo wetu mzuri tunapokuwa katika mji wa kusanyiko huipamba kweli
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Majuma matatu kabla ya kusanyiko letu kuanza, tutashiriki katika kampeni ya kuwaalika watu kwenye kusanyiko
[Sanduku katika kurasa za 3-6]
Vikumbusho vya Kusanyiko la Wilaya—2012
◼ Saa za Programu: Siku zote tatu, programu itaanza saa 3:20 asubuhi. Muziki unaotangulia kila sehemu ya programu unapotangazwa, sote tunapaswa kuketi ili programu ianze kwa utaratibu na heshima. Programu itaisha saa 10:55 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 9:40 jioni siku ya Jumapili.
◼ Maegesho: Katika sehemu zote za makusanyiko ambapo tumeruhusiwa kuegesha magari, sehemu za kuegesha zitapatikana bila malipo, wale watakaofika kwanza ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza.
◼ Viti: Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili ya wale tu unaoishi nao, au unaosafiri nao katika gari moja au watu unaojifunza Biblia pamoja nao.—1 Kor. 13:5
◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa pumziko ili kwenda kutafuta chakula. Mfuko au sanduku maalumu la kubebea chakula ambalo linaweza kuwekwa chini ya kiti linaweza kutumiwa. Mifuko au masanduku makubwa ya kubebea chakula na pia vyombo vya glasi haviruhusiwi kusanyikoni.
◼ Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kusanyikoni kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Cheki au hundi zozote zinazotolewa zinapaswa kuandikwa “International Bible Students Association.” Au jina la shirika la kisheria linalotumiwa nchini kwenu.
◼ Aksidenti na Hali za Dharura: Hali ya dharura ya kimatibabu ikitokea kusanyikoni, tafadhali wasiliana na mkaribishaji aliye karibu, ambaye ataijulisha mara moja Idara ya Huduma ya Kwanza ili mtu anayestahili kutoa huduma ya kwanza achunguze hali hiyo na kutoa msaada unaohitajika. Ikihitajika, ndugu katika idara hiyo watatafuta gari la kubebea wagonjwa. Jambo hili litapunguza idadi ya simu zinazopokewa na kitengo cha huduma za dharura.
◼ Dawa: Ikiwa unatumia dawa ulizoagizwa na daktari, tafadhali hakikisha umebeba za kutosha, kwa kuwa hazitapatikana kusanyikoni. Bomba za sindano au sirinji na sindano zinazotumiwa na wagonjwa wa kisukari hazipaswi kutupwa ovyo kwani ni takataka hatari, wala zisitupwe pamoja na takataka zilizo katika eneo la kusanyiko au hotelini.
◼ Viatu: Kila mwaka watu kadhaa hujeruhiwa kwa sababu ya viatu. Kwa hiyo, ni vizuri kuvaa viatu vya kawaida, vinavyokutoshea vizuri na vinavyokuwezesha kutembea kwa usalama kwenye sehemu zilizoinuka, kwenye ngazi, kwenye viunzi vya chuma na sehemu nyinginezo.
◼ Marashi: Makusanyiko mengine hufanyiwa ndani ya majumba ambayo hutumia mitambo maalumu ya kuingizia hewa. Kwa hiyo, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
◼ Fomu za Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43): Fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi inapaswa kutumiwa kutoa habari kuhusu mtu yeyote mwenye kupendezwa ambaye ulimpata ulipokuwa ukihubiri isivyo rasmi wakati wa kusanyiko. Wahubiri wanapaswa kubeba fomu moja au mbili wanapoenda kusanyikoni. Fomu zilizojazwa zinaweza kuachwa kwenye idara ya vitabu au unaweza kumpa mwandishi wa kutaniko lenu unaporudi.—Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Mei 2011, ukurasa wa 3.
◼ Mikahawa: Liheshimu jina la Yehova kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Toa bakshishi ikiwa ni kawaida katika eneo lenu.
◼ Hoteli:
(1) Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kisikaliwe na watu wanaozidi idadi ya watu inayoruhusiwa.
(2) Usifute hifadhi ya chumba isipokuwa hali ya dharura itokee, na unapaswa kuwajulisha wasimamizi wa hoteli mara moja unapogundua kwamba hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa.—Mt. 5:37.
(3) Tafadhali zingatia kwamba ikiwa utatumia kadi kulipia gharama unapojiandikisha kwenye hoteli, ni zoea la kawaida kwa hoteli “kuweka kando” kiasi fulani cha pesa zako ambazo zinatosha kulipia gharama zako zote na uharibifu au matukio yasiyotazamiwa unapokuwa hotelini. Baada ya kuondoka hotelini, hutaweza kutumia pesa hizo zilizowekwa kando mpaka siku kadhaa za kushughulikia akaunti yako zipite.
(4) Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati tu unapokuwa tayari kukitumia, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia.
(5) Wape bakshishi wafanyakazi wa hoteli wanapokubebea mizigo, na pia yule anayekusafishia chumba.
(6) Pika tu katika vyumba ambavyo upishi umeruhusiwa.
(7) Fuata vizuri utaratibu uliowekwa hotelini kuhusu kiamsha-kinywa, kahawa, au barafu ambazo huandaliwa kwa ajili ya wageni.
(8) Onyesha tunda la roho unaposhughulika na wafanyakazi wa hoteli. Wanawahudumia watu wengi, wanathamini tunapokuwa wenye fadhili, subira, na kiasi.
(9) Wazazi wanapaswa kuwasimamia watoto wao nyakati zote wanapokuwa kwenye hoteli, kutia ndani kidimbwi cha kuogelea, sebuleni, chumba cha mazoezi, na kadhalika.
(10) Kukiwa na shida kuhusiana na chumba chako hotelini, julisha Idara ya Mahali pa Kulala ukiwa ungali kusanyikoni ili ndugu waweze kukusaidia.
◼ Kazi ya Kujitolea: Yeyote ambaye angependa kujitolea anapaswa kwenda kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kusanyikoni. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kufanya kazi, lakini wafanye hivyo chini ya usimamizi wa mzazi au mtunzaji wao. Pia, wanaweza kufanya kazi chini ya usimamizi wa mtu mzima ambaye amekabidhiwa daraka hilo na mzazi au mtunzaji wao.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Tutaisambazaje Mialiko?
Ili tuweze kusambaza mialiko katika eneo lote, huenda itatubidi kusema kifupi. Labda tunaweza kusema hivi: “Habari. Tunashiriki katika kampeni ya ulimwenguni pote ya kusambaza mwaliko huu. Hii ni nakala yako. Habari zaidi zinapatikana katika mwaliko.” Uwe mchangamfu. Inapofaa, unapaswa kuambatanisha magazeti yetu na mialiko hiyo katika siku za Jumamosi na Jumapili.