Mikutano ya Utumishi wa Shambani Inayotimiza Kusudi Lake
1. Mikutano ya utumishi wa shambani ina kusudi gani?
1 Pindi fulani, Yesu alikutana na wanafunzi wake 70 kabla ya kwenda katika kampeni ya kuhubiri. (Luka 10:1-11) Aliwatia moyo kwa kuwakumbusha kwamba hawatakuwa peke yao, na kwamba wangeongozwa na Yehova “Bwana wa mavuno.” Pia, aliwapa maagizo ambayo yangewatayarisha kufanya kazi hiyo, na kisha kuwapanga “wawili-wawili.” Leo, mikutano tunayofanya kabla ya kwenda utumishi wa shambani ina kusudi kama hilo, yaani, kututia moyo, kututayarisha, na kutusaidia tuwe na utaratibu.
2. Mkutano wa utumishi wa shambani utakuwa na urefu gani?
2 Kwa sasa, mkutano wa utumishi wa shambani unaongozwa kwa dakika 10 hadi 15, mkutano huo unatia ndani kupanga vikundi, kugawa maeneo, na kutoa sala. Sasa kutakuwa na mabadiliko. Kuanzia Aprili, mkutano huo utaongozwa kwa dakika tano hadi saba tu. Hata hivyo, ikiwa mkutano huo utaongozwa baada ya mikutano mingine ya kutaniko unapaswa kuwa mfupi zaidi, kwa kuwa tayari wahubiri wamesikiliza mafundisho mazuri ya kiroho. Kuongoza mkutano huo kwa muda mfupi kutawawezesha wahubiri watumie wakati mwingi zaidi katika utumishi wa shambani. Kwa kuongezea, ikiwa mapainia au wahubiri wameanza kuhubiri kabla ya mkutano wa utumishi wa shambani ni muhimu wakatize utumishi kwa muda mfupi ili wahudhurie mkutano huo.
3. Mikutano ya utumishi wa shambani inaweza kupangwa kwa njia gani ili iwanufaishe wahubiri?
3 Mikutano ya utumishi wa shambani inapaswa kupangwa vizuri ili iwanufaishe wahubiri. Katika makutaniko mengi inafaa zaidi vikundi vya utumishi kukutana sehemu tofauti-tofauti badala ya vikundi vyote kukutana mahali pamoja. Huenda jambo hilo likafanya iwe rahisi kwa wahubiri kufika kwenye mkutano wa utumishi na katika eneo. Pia waangalizi wa vikundi wataweza kuwapanga wahubiri kwa urahisi, na kushughulikia uhitaji wa kila mhubiri katika vikundi vyao. Baraza la wazee linaweza kuzingatia hali za eneo na kufanya uamuzi unaofaa. Kabla ya kumaliza mkutano huo kwa sala fupi, kila mhubiri anapaswa kujulishwa eneo atakalohubiri na yule atakayehubiri naye.
4. Kwa nini mikutano ya utumishi wa shambani ni muhimu kama ilivyo mikutano mingine?
4 Ni Muhimu Kama Ilivyo Mikutano Mingine: Kwa sababu mikutano ya utumishi wa shambani hufanywa kwa manufaa ya wale wanaoenda utumishi, huenda wahubiri wote wasihudhurie. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba mkutano huo hauna manufaa au kwamba si muhimu kama mikutano mingine ya kutaniko. Kama ilivyo mikutano yetu yote, mikutano ya utumishi wa shambani ni uandalizi wa Yehova unaotuwezesha kuchocheana katika upendo na matendo mazuri. (Ebr. 10:24, 25) Kwa hiyo, ndugu anayeongoza mkutano huo anapaswa kujitayarisha vizuri ili mazungumzo hayo yamtukuze Yehova na kuwanufaisha wahubiri. Inapowezekana, wahubiri wanaoenda utumishi wanapaswa kujitahidi kuhudhuria mkutano huo.
Mikutano ya utumishi wa shambani ni muhimu kama ilivyo mikutano mingine ya kutaniko
5. (a) Mwangalizi wa utumishi ana jukumu gani katika kupanga mikutano ya utumishi wa shambani? (b) Dada anapaswa kuongozaje mkutano wa utumishi wa shambani?—Ona sanduku uku. 6.
5 Matayarisho Yanayofanywa na Ndugu Anayeongoza: Ili mtu atayarishe vizuri sehemu yake katika mkutano, anahitaji kupewa mgawo wake mapema. Hivyo ndivyo ilivyo kuhusiana na mikutano ya utumishi wa shambani. Bila shaka, ikiwa vikundi vya utumishi wa shambani vinakutanika mahali tofauti-tofauti, waangalizi wa vikundi au wasaidizi wao wataongoza mkutano kwa ajili ya vikundi vyao. Hata hivyo, ikiwa vikundi vyote vinakutanika mahali pamoja kwa ajili ya mkutano wa utumishi wa shambani, mwangalizi wa utumishi atapanga ndugu atakayeongoza mkutano huo. Baadhi ya waangalizi wa utumishi huwapa ratiba wale watakaoongoza mkutano huo na kuiweka nakala ya ratiba hiyo kwenye ubao wa matangazo. Mwangalizi wa utumishi anapaswa kutumia utambuzi anapopanga ndugu watakaoongoza mkutano huo akikumbuka kwamba, ubora wa mikutano hii unategemea uwezo wa kufundisha na kuratibu mambo wa wale wanaoongoza. Ikiwa hakuna mzee, mtumishi wa huduma, au ndugu mwingine anayestahili kuongoza, mwangalizi wa utumishi anapaswa kupanga dada mwenye uwezo ili aongoze mkutano huo.—Ona makala “Inapokuwa Lazima Dada Aongoze Mkutano.”
6. Kwa nini ni muhimu kwa ndugu anayeongoza kujitayarisha vizuri?
6 Tunapopewa mgawo wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi au Mkutano wa Utumishi, tunauchukua kwa uzito na kujitayarisha vizuri. Huenda wengine wakasubiri mpaka wakati wanapoenda mikutanoni ndipo waanze kufikiria kuhusu jambo watakalosema. Mgawo wa kuongoza mkutano wa utumishi wa shambani unapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Kwa kuwa sasa mkutano huo utakuwa mfupi zaidi, matayarisho mazuri ni muhimu ili mkutano huo uwe wenye kujenga na uishe kwa wakati. Matayarisho mazuri pia hutia ndani kupanga mapema eneo la kuhubiri.
7. Ndugu anayeongoza anaweza kuzungumzia mambo gani?—Ona sanduku uku. 6.
7 Mambo Yatakayozungumziwa: Kwa sababu hali za maeneo hutofautiana, mtumwa mwaminifu hajaandaa mambo hususa kwa ajili ya kila mkutano wa utumishi wa shambani. Sanduku lenye kichwa “Mambo Mnayoweza Kuzungumzia Katika Mkutano wa Utumishi wa Shambani” limeorodhesha baadhi ya mambo hayo. Kwa kawaida mkutano huo hufanywa kwa njia ya mazungumzo. Pindi fulani, huenda ukatia ndani onyesho lililotayarishwa vizuri au video zinazotumiwa katika huduma zinazopatikana kwenye Tovuti ya jw.org/sw. Ndugu anayeongoza mkutano wa utumishi wa shambani anapaswa kutayarisha mambo yatakayo wachochea na kuwatayarisha wale wanaoenda kuhubiri siku hiyo.
Ndugu anayeongoza mkutano wa utumishi wa shambani anapaswa kutayarisha mambo yatakayo wachochea na kuwatayarisha wale wanaoenda kuhubiri siku hiyo
8. Ni mambo gani yanayoweza kufaa kuzungumziwa katika mikutano ya utumishi wa shambani siku za Jumamosi na Jumapili?
8 Kwa mfano, siku za Jumamosi wahubiri wengi hutoa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Wahubiri wengi wanaoshiriki utumishi wa shambani siku za Jumamosi, huenda hawajashiriki katikati ya juma, hivyo inaweza kuwa vigumu kwao kukumbuka mazoezi waliyofanya katika Ibada ya Familia. Kwa hiyo, huenda ikafaa kwa ndugu anayeongoza kurudia moja kati ya mapendekezo kwa ajili ya utumishi yaliyo nyuma ya Huduma Yetu ya Ufalme. Pia mnaweza kuzungumzia jinsi ya kuhusianisha habari, matukio, au sikukuu fulani katika eneo lenu na utangulizi wa kutoa magazeti, au jinsi ya kuweka msingi mzuri kwa ajili ya ziara itakayofuata iwapo tuliwaachia magazeti. Ikiwa baadhi ya wahubiri wamekwisha toa magazeti hayo, ndugu anayeongoza anaweza kuwaomba watoe mapendekezo mafupi au wasimulie mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo. Siku za Jumapili, ndugu anayeongoza anaweza kuamua kutumia njia kama hiyo kuhusiana na toleo la mwezi. Machapisho ya funzo, kama vile broshua Habari Njema na Msikilize Mungu na kitabu Biblia Inafundisha yanaweza kutolewa wakati wowote, kwa hiyo, ndugu anayeongoza anaweza kuzungumzia kwa ufupi jinsi moja kati ya machapisho hayo linavyoweza kutolewa.
9. Ni nini kinachoweza kuzungumziwa katika mkutano wa utumishi mnaposhiriki katika kampeni ya pekee mwishoni mwa juma?
9 Ikiwa kutaniko linashiriki katika kampeni ya pekee mwisho juma, ndugu anayeongoza anaweza kuzungumzia jinsi ya kutoa magazeti ya karibuni pamoja na mialiko au trakti, au anaweza kuzungumzia jinsi ya kufanya tunapokutana na mtu anayeonyesha upendezi. Njia nyingine ni kusimulia mambo yaliyoonwa yanayoonyesha umuhimu wa kampeni hizo.
10, 11. Kwa nini matayarisho ya wahubiri ni muhimu ili kufanikisha mkutano wa utumishi wa shambani?
10 Matayarisho Yanayofanywa na Wahubiri: Pia wahubiri wana sehemu muhimu katika kufanikisha mkutano huo. Wanapojitayarisha mapema kwa ajili ya utumishi, labda hata katika ibada yao ya familia watakuwa na jambo linaloweza kuwajenga wahubiri wengine. Matayarisho mazuri yanatia ndani kuwa na magazeti na machapisho mengine kabla ya kufika kwenye mkutano wa utumishi wa shambani, kufanya hivyo kutasaidia wahubiri wote kuelekea katika eneo mapema.
11 Ni muhimu kupanga kufika mapema kwenye mkutano wa utumishi wa shambani. Bila shaka, tunajitahidi kufika kwa wakati kwenye mikutano yote ya kutaniko. Hata hivyo, tunapochelewa kufika katika mkutano wa utumishi wa shambani jambo hilo linaweza kuwasumbua wengine. Jinsi gani? Ndugu anayeongoza anazingatia mambo mbalimbali kabla ya kupanga kikundi. Iwapo kuna wahubiri wachache, huenda akaamua kuwatuma kila mmoja katika eneo ambalo halijahubiriwa kikamili. Ikiwa baadhi ya wahubiri wanatoka mbali na bado eneo watakalokwenda kuhubiri ni mbali zaidi ndugu anayeongoza anaweza kuwapanga pamoja na wale walio na usafiri. Endapo eneo hilo lina uhalifu mkubwa, anaweza kupanga akina ndugu wahubiri eneo lililo karibu na kikundi cha akina dada. Wahubiri walio na matatizo ya afya wanaweza kupangwa kuhubiri katika mtaa wenye nyumba za kawaida au zisizo na ngazi ndefu. Wahubiri wapya wanaweza kupangwa kuhubiri pamoja na wale walio na uzoefu zaidi. Lakini, ikiwa wahubiri wamechelewa kufika, mara nyingi ndugu anayeongoza hulazimika kubadili mipango. Bila shaka, nyakati fulani huenda tukawa na sababu za msingi za kutofika kwa wakati. Hata hivyo, kama tuna kawaida ya kuchelewa tunaweza kujichunguza ili tuone ikiwa ni kwa sababu ya kukosa kuthamini mikutano hiyo au kutopanga mambo yetu mapema.
12. Ikiwa una kawaida ya kujifanyia mipango ya kuwa na mwandamani wa utumishi, unaweza kufikiri kuhusu jambo gani?
12 Wahubiri wanaweza kufanya mipango yao wenyewe ya kuwa na waandamani kabla ya mkutano kuanza au wanaweza kupewa mwandamani katika mkutano huo. Ikiwa una kawaida ya kufanya mipango yako mwenyewe, je, unaweza ‘kupanuka’ kwa kuhubiri na watu tofauti-tofauti badala ya kwenda na rafiki zako wa karibu mara kwa mara? (2 Kor. 6:11-13) Je, unaweza kupanga kuhubiri pindi kwa pindi na mhubiri mpya ili umsaidie kuboresha uwezo wake wa kufundisha? (1 Kor. 10:24; 1 Tim. 4:13, 15) Sikiliza kwa makini maagizo yote yanayotolewa, kutia ndani maelekezo kuhusu eneo la kuhubiri. Mkutano unapomalizika, epuka kubadili mipango iliyofanywa na uende mara moja katika eneo.
13. Mikutano ya utumishi itatunufaishaje ikiwa kila mmoja atajitahidi kufanya sehemu yake kwa bidii?
13 Baada ya kuhubiri, wale wanafunzi 70 ambao Yesu aliwapanga kwa ajili ya huduma ‘walirudi wakiwa na shangwe.’ (Luka 10:17) Bila shaka, mkutano ambao Yesu alifanya pamoja nao kabla ya kwenda kuhubiri uliwasaidia kupata matokeo mazuri. Leo, mikutano ya utumishi wa shambani inaweza kuwa na manufaa kama hizo. Kila mmoja akijitahidi kwa bidii na kufanya sehemu yake, mikutano ya utumishi wa shambani itatutia moyo, itatutayarisha, na kutusaidia tuwe na utaratibu ili tutimize agizo tulilopewa la kutoa “ushahidi kwa mataifa yote.”—Mt. 24:14.