-
“Mungu Ni Upendo”Mkaribie Yehova
-
-
Sehemu ya 4
“Mungu Ni Upendo”
Upendo ndiyo sifa kuu zaidi ya Mungu. Pia ndiyo sifa inayovutia zaidi. Tunapochunguza baadhi ya mambo yenye kupendeza ya sifa hii bora, tutaelewa kwa nini Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
-
-
“Alitupenda Sisi Kwanza”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 23
“Alitupenda Sisi Kwanza”
1-3. Ni mambo yapi yaliyofanya kifo cha Yesu kiwe cha pekee sana katika historia yote?
SIKU moja miaka 2,000 hivi iliyopita, mtu fulani asiye na hatia alishtakiwa, akahukumiwa kwa sababu ya uhalifu ambao hakufanya, kisha akateswa hadi akafa. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba yeye ni baadhi tu ya watu ambao wameuawa kikatili katika historia. Lakini kifo chake kilikuwa cha pekee sana.
2 Mtu huyo alipokuwa akiteseka kwa maumivu makali saa chache kabla ya kufa, kulikuwa na ishara mbinguni kuonyesha kwamba hilo lilikuwa tukio muhimu sana. Giza liliifunika dunia yote ghafula yapata saa sita mchana. Mwanahistoria mmoja alisema kwamba “nuru ya jua ilikosekana.” (Luka 23:44, 45) Kisha, kabla tu ya kufa, akasema maneno haya yasiyosahaulika: “Imetimizwa!” Kwa kweli, alitimiza jambo zuri sana alipodhabihu uhai wake. Kwa kudhabihu uhai wake, alionyesha upendo ambao hakuna mwanadamu yeyote amewahi kuonyesha.—Yohana 15:13; 19:30.
3 Mtu huyo alikuwa Yesu Kristo. Mateso na kifo chake katika siku hiyo ya kuhuzunisha, Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., ni mambo yanayojulikana sana. Hata hivyo, jambo fulani muhimu limepuuzwa mara nyingi. Ingawa Yesu aliteseka sana, kuna mwingine aliyeteseka hata zaidi. Kwa kweli, kuna mwingine aliyejidhabihu kwa njia kubwa hata zaidi siku hiyo—alitenda tendo kuu zaidi la upendo ambalo halijawahi kufanywa na yeyote katika ulimwengu mzima. Ni tendo gani hilo? Jibu la swali hilo ni utangulizi ufaao wa habari muhimu zaidi ya habari zote: Upendo wa Yehova.
Tendo Kuu Zaidi la Upendo
4. Askari Mroma alipataje kujua kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida, naye alikata kauli gani?
4 Askari Mroma aliyesimamia mauaji ya Yesu alipigwa na bumbuazi alipoona giza lililotokea kabla ya Yesu kufa na tetemeko kubwa la dunia lililotokea baadaye. Alisema hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mathayo 27:54) Ni wazi kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida. Askari huyo aliunga mkono mauaji ya Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu Mwenyezi! Mwana huyo alipendwa na Baba yake kwa kadiri gani?
5. Ni mfano gani umetolewa ili kutusaidia kuelewa kwamba Yehova na Mwanaye wamekuwa pamoja mbinguni kwa muda mrefu sana?
5 Biblia inamwita Yesu “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Hebu fikiria—Mwana wa Yehova alikuwapo kabla ya ulimwengu kuumbwa. Basi, Mwana huyo alikaa na Baba yake kwa muda gani? Wanasayansi fulani wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo kwa muda wa miaka bilioni 13. Huo ni muda usiowazika, sivyo? Ili kuwasaidia watu waelewe muda ambao wanasayansi wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo, jengo moja lenye mitambo ya kuigiza miendo ya sayari lina chati ya tarehe yenye urefu wa meta 110. Wageni wanapotembea kando ya chati hiyo, kila hatua wanayopiga inawakilisha miaka ipatayo milioni 75 ya muda ambao ulimwengu umekuwapo. Alama ndogo inayolingana na unene wa unywele wa mwanadamu imewekwa mwishoni mwa chati hiyo ili kuwakilisha muda ambao wanadamu wameishi duniani! Lakini, hata ikiwa makisio hayo ni sahihi, urefu wa chati hiyo hauwezi kamwe kuwakilisha umri wa Mwana wa Yehova! Alikuwa akifanya kazi gani wakati huo wote?
6. (a) Mwana wa Yehova alikuwa akifanya nini kabla ya kuwa mwanadamu? (b) Yehova na Mwanaye wanaunganishwa na kifungo cha aina gani?
6 Mwana huyo alifurahi kutumiwa na Baba yake akiwa “stadi wa kazi.” (Mithali 8:30) Biblia inasema hivi: “Na bila yeye [Mwana] hata kitu kimoja hakikuja kuwako.” (Yohana 1:3) Kwa hiyo Yehova na Mwanaye walishirikiana kuumba vitu vingine vyote. Walikuwa na kazi zenye kuvutia na kufurahisha kwelikweli. Watu wengi hukubali kwamba mzazi na mtoto hupendana sana. Na upendo “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Basi, ni nani kati yetu anayeweza kuelewa kwa ukamili nguvu za kifungo ambacho kimekuwapo kwa muda mrefu hivyo? Ni wazi kwamba Yehova Mungu na Mwanaye wameunganishwa na kifungo cha upendo chenye nguvu kuliko kifungo chochote kile.
7. Yesu alipobatizwa, Yehova alionyeshaje hisia zake kumwelekea?
7 Hata hivyo, Baba alimtuma Mwanaye duniani ili azaliwe akiwa mwanadamu. Kwa hivyo, Yehova hakuweza kushirikiana kwa ukaribu na Mwanaye mpendwa huko mbinguni kwa miaka kadhaa. Akiwa mbinguni, Yehova alipendezwa sana kumtazama Yesu akikua hadi akawa mwanamume mkamilifu. Yesu alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi. Tunajua jinsi Yehova Baba yake alivyohisi kumhusu, hata alisema moja kwa moja kutoka mbinguni: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Bila shaka Baba ya Yesu alifurahi sana kumwona akifanya kwa uaminifu yote yaliyotabiriwa, mambo yote ambayo alipaswa kufanya!—Yohana 5:36; 17:4.
8, 9. (a) Yesu alitendewaje Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., na Baba yake wa mbinguni alihisije? (b) Kwa nini Yehova alimruhusu Mwanaye ateseke na kufa?
8 Hata hivyo, Yehova alihisije Nisani 14, mwaka wa 33 W.K.? Alihisije Yesu aliposalitiwa na kukamatwa na umati usiku? Alihisije Yesu alipoachwa na rafiki zake na kushtakiwa isivyo haki? Alihisije Yesu alipodhihakiwa, kutemewa mate, na kupigwa ngumi? Alihisije alipopigwa mijeledi iliyochanachana mgongo wake? Alihisije mikono na miguu yake ilipopigiliwa misumari kwenye mti, kisha akaachwa akiwa amening’inia huku watu wakimtukana? Baba alihisije Mwanaye mpendwa alipokuwa akimlilia kwa maumivu makali? Yehova alihisije Yesu alipokata pumzi, na kwa mara ya kwanza kabisa tangu mwanzo wa uumbaji wote, Mwanaye mpendwa akakoma kuwapo?—Mathayo 26:14-16, 46, 47, 56, 59, 67; 27:38-44, 46; Yohana 19:1.
’Mungu alitoa Mwana wake mzaliwa pekee’
9 Hatuna la kusema. Kwa kuwa Yehova ana hisia, hatuwezi kamwe kueleza uchungu ambao alihisi kwa sababu ya kifo cha Mwanaye. Lakini tunaweza kueleza kusudi la Yehova la kuruhusu jambo hilo litukie. Kwa nini Baba ya Yesu alijiruhusu kupatwa na uchungu huo? Yehova anatueleza jambo la kupendeza katika Yohana 3:16—mstari huu wa Biblia ni muhimu sana hivi kwamba umeitwa Injili ndogo. Andiko hilo lasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” Kwa hiyo, Yehova alifanya hivyo kwa sababu ya upendo. Zawadi ambayo Yehova alitoa—kumtuma Mwanaye ateseke na kufa kwa ajili yetu—ndiyo tendo kuu zaidi la upendo ambalo limewahi kufanywa.
Maana ya Upendo wa Mungu
10. Wanadamu wana uhitaji gani, na kwa nini ni vigumu kuelewa maana ya neno “upendo”?
10 Neno “upendo” lamaanisha nini? Imesemwa kwamba upendo ndio uhitaji mkubwa zaidi wa wanadamu. Tangu wanapozaliwa hadi wanapokufa, watu hutamani sana kupendwa, wanaishi kwa furaha wanapopendwa, na hata wanadhoofika na kufa wasipopendwa. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba si rahisi kueleza maana ya upendo. Bila shaka, watu huongea sana kuhusu upendo. Watu wanaendelea kuandika vitabu, kutunga nyimbo, na mashairi mengi sana kuhusu upendo. Hata hivyo, nyakati nyingine hawafafanui ifaavyo maana ya upendo. Neno hilo limetumiwa sana hivi kwamba inaonekana limepoteza maana.
11, 12. (a) Ni wapi tu tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu upendo, na kwa nini? (b) Kigiriki cha awali kinataja kihususa upendo gani mbalimbali, na ni “upendo” gani unaotajwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? (Ona pia kielezi-chini.) (c) A·gaʹpe ni nini?
11 Hata hivyo, Biblia inafundisha waziwazi kuhusu upendo. Kamusi ya Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words yasema hivi: “Upendo unaweza kuonyeshwa tu kupitia matendo.” Masimulizi ya Biblia kuhusu matendo ya Yehova yanatufundisha mengi kuhusu upendo wake ambao unamchochea kuwatendea viumbe wake kwa fadhili. Kwa mfano, ni jambo gani linaloweza kuonyesha sifa hiyo kwa njia bora kuliko tendo kuu zaidi la upendo wa Yehova tulilozungumzia awali? Tutaona matendo mengi ya Yehova ya upendo katika sura zinazofuata. Zaidi ya hayo, tunaweza kupata ufahamu wa ndani kutokana na maneno ya awali yanayotafsiriwa “upendo” katika Biblia. Kigiriki cha awali kilikuwa na maneno manne yaliyotafsiriwa “upendo.”a Kati ya maneno hayo, a·gaʹpe hutumiwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba hilo “ndilo neno linaloeleza upendo kwa njia nzuri zaidi.” Kwa nini?
12 A·gaʹpe ni upendo unaoongozwa na kanuni. Si hisia tunayokuwa nayo bila kufikiri. Upendo huo unatia ndani mambo mengi, unahusisha fikira na una kusudi fulani. Zaidi ya yote, upendo wa a·gaʹpe hauna ubinafsi. Kwa mfano, soma tena Yohana 3:16. Ni “ulimwengu” upi ambao Mungu aliupenda sana hivi kwamba akamtoa Mwanaye mzaliwa-pekee? Ulimwengu huo ni wanadamu wanaoweza kukombolewa. Unatia ndani watu wengi ambao wanaendelea kutenda dhambi maishani. Je, Yehova anampenda kila mtu kama alivyompenda Abrahamu mwaminifu, aliyekuwa rafiki yake? (Yakobo 2:23) La, lakini kwa upendo, Yehova anawatendea watu wote mema hata kwa hasara yake. Anataka watu wote watubu na kubadili njia zao. (2 Petro 3:9) Wengi hufanya hivyo. Naye hufurahi kuwa rafiki yao.
13, 14. Ni nini kinachoonyesha kwamba mara nyingi a·gaʹpe huhusisha shauku ya kirafiki?
13 Hata hivyo, watu fulani wana maoni yasiyofaa kuhusu a·gaʹpe. Wanafikiri kwamba huo ni upendo usio na hisia, unaoongozwa na akili tu. Ukweli ni kwamba mara nyingi a·gaʹpe huhusisha uhusiano wa karibu wenye upendo. Kwa mfano, Yohana alipoandika, “Baba humpenda Mwana,” alitumia aina fulani ya neno a·gaʹpe. Je, upendo huo hauna shauku ya kirafiki? Ona kwamba Yesu alisema “Baba ana shauku na Mwana,” na hapo anatumia aina fulani ya neno phi·leʹo. (Yohana 3:35; 5:20) Mara nyingi upendo wa Yehova hutia ndani shauku ya moyoni. Lakini, upendo wake hautegemei kamwe hisia. Sikuzote unaongozwa na kanuni zake za hekima na haki.
14 Kama tulivyoona, sifa zote za Yehova ni bora sana, ni kamilifu, na zinavutia. Lakini upendo unavutia kuliko sifa nyingine zote. Hakuna kitu kinachotufanya tumkaribie Yehova kama upendo. Inafurahisha kwamba upendo ndio sifa kuu zaidi ya Yehova. Twajuaje?
“Mungu Ni Upendo”
15. Biblia inasema nini kuhusu sifa ya Yehova ya upendo, na kwa nini usemi huo ni wa pekee sana? (Ona pia kielezi-chini.)
15 Biblia inasema jambo fulani la pekee kuhusu upendo ambalo haisemi kuhusu zile sifa nyingine kuu za Yehova. Maandiko hayasemi kwamba Mungu ni nguvu wala hayasemi kwamba Mungu ni haki au hata Mungu ni hekima. Ana sifa hizo, yeye ndiye chanzo chake, na hana kifani katika sifa hizo tatu. Hata hivyo, kuhusu sifa ya nne, Biblia inasema jambo fulani la pekee sana: “Mungu ni upendo.”b (1 Yohana 4:8) Hilo lamaanisha nini?
16-18. (a) Kwa nini Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo”? (b) Kati ya viumbe wote duniani, kwa nini mwanadamu ni mfano unaofaa wa sifa ya Yehova ya upendo?
16 Usemi “Mungu ni upendo” haulingani na usemi, “Mungu ni sawa na upendo.” Hatuwezi kamwe kugeuza usemi huo na kusema “upendo ni Mungu.” Yehova si sifa fulani tu. Ana utu, na mbali na upendo ana hisia na sifa nyingi mbalimbali. Hata hivyo, Yehova ana upendo mwingi sana. Kichapo kimoja cha marejeo kinasema hivi kuhusu mstari huo: “Upendo ni utu au sifa ya asili ya Mungu.” Kwa ujumla, tunaweza kulifikiria jambo hilo kwa njia hii: Nguvu za Yehova humwezesha kutenda. Haki na hekima yake humwongoza kutenda. Lakini upendo wa Yehova humchochea kutenda. Naye sikuzote hutumia sifa nyingine zote kupatana na upendo wake.
17 Mara nyingi imesemwa kwamba Yehova ni wonyesho halisi wa upendo. Kwa hiyo, tukitaka kujifunza kuhusu upendo unaotegemea kanuni, ni lazima tujifunze kumhusu Yehova. Bila shaka, wanadamu pia wana sifa hiyo yenye kupendeza. Lakini kwa nini wanadamu wana sifa hiyo? Wakati wa uumbaji, Yehova alimwambia hivi Mwanaye: “Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” (Mwanzo 1:26) Kati ya viumbe wote duniani, ni wanaume na wanawake tu wanaoweza kupenda na hivyo kumwiga Baba yao wa mbinguni. Kumbuka kwamba Yehova alitumia viumbe mbalimbali kuwa mifano ya sifa zake kuu. Hata hivyo, Yehova alimtumia mwanadamu—kiumbe bora zaidi duniani—kuwa mfano wa sifa Yake kuu zaidi ya upendo.—Ezekieli 1:10.
18 Tunapowapenda wengine bila ubinafsi kupatana na kanuni, tunaonyesha sifa kuu zaidi ya Yehova. Ni kama mtume Yohana alivyoandika: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Lakini Yehova alitupenda kwanza kwa njia zipi?
Yehova Alitupenda Kwanza
19. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba upendo ndio uliomfanya Yehova aumbe?
19 Upendo si sifa mpya. Ni nini kilichomfanya Yehova aanze kuumba? Si kwa sababu alikuwa mpweke na alihitaji mwandani. Yehova ni kamili, hapungukiwi kwa vyovyote wala hahitaji msaada wa yeyote. Lakini alichochewa na sifa yake ya upendo ambayo inaonyeshwa kwa matendo, awape uhai viumbe wake wenye akili ambao wangeweza kuthamini zawadi hiyo. Mwanaye mzaliwa-pekee alikuwa “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufunuo 3:14) Yehova alimtumia Stadi huyo wa Kazi kuumba vitu vinginevyo vyote, kuanzia malaika. (Ayubu 38:4, 7; Wakolosai 1:16) Wakiwa wamepewa uhuru, akili, na hisia, viumbe hao wa roho wenye nguvu waliweza kuwa na uhusiano wenye upendo—kati yao wenyewe na, zaidi ya yote, pamoja na Yehova Mungu. (2 Wakorintho 3:17) Kwa hiyo, walipendana kwa sababu walipendwa kwanza.
20, 21. Ni mambo gani yaliyoonyesha kwamba Yehova aliwapenda Adamu na Hawa, lakini walitendaje?
20 Ndivyo na wanadamu. Tangu mwanzo, Adamu na Hawa walionyeshwa upendo mwingi sana. Kulikuwa na mambo mengi katika makao yao ya Paradiso ya Edeni yaliyowathibitishia kwamba Baba yao aliwapenda. Angalia jinsi Biblia inavyosema: “BWANA Mungu akapanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya.” (Mwanzo 2:8) Je, umewahi kutembelea bustani maridadi kwelikweli? Ni nini kilichokupendeza zaidi? Je, ni nuru iliyopenya majani ya miti kwenye sehemu ya bustani iliyo kimya na yenye kivuli? Je, ni rangi zenye kuvutia sana za maua? Je, ni sauti ya bubujiko la kijito, ndege wanaoimba, na wadudu wanaovuma? Vipi harufu nzuri ya miti, matunda na maua yaliyochanua? Kwa vyovyote vile, hakuna bustani leo inayoweza kulinganishwa na bustani ya Edeni. Kwa nini?
21 Bustani hiyo ilipandwa na Yehova mwenyewe! Bila shaka ilikuwa maridadi isivyoelezeka. Ilikuwa na kila aina ya mti wenye kuvutia na wenye matunda matamu. Bustani hiyo ilikuwa na maji ya kutosha, ilikuwa kubwa sana, na ilikuwa na wanyama mbalimbali wenye kuvutia. Adamu na Hawa walikuwa na kila kitu walichohitaji ili kuishi maisha yenye furaha na yenye kuridhisha, na walikuwa na kazi yenye kuridhisha na urafiki mkamilifu. Yehova aliwapenda kwanza, na walikuwa na kila sababu ya kumpenda vilevile. Lakini walishindwa kufanya hivyo. Badala ya kumtii Baba yao wa mbinguni kwa upendo, walimwasi kwa sababu ya ubinafsi.—Mwanzo, sura ya 2.
22. Hatua ambayo Yehova alichukua baada ya uasi katika Edeni ilithibitishaje kwamba upendo wake ni mwaminifu?
22 Jambo hilo lilimhuzunisha Yehova sana. Lakini je, uasi huo ulitia uchungu moyo wake wenye upendo? La! “Fadhili zake [au, “upendo-mwaminifu,” NW, kielezi-chini] ni za milele.” (Zaburi 136:1) Kwa hiyo, kwa upendo, alikusudia mara moja kufanya mipango ya kumkomboa mzao yeyote wa Adamu na Hawa ambaye ana mwelekeo unaofaa. Kama tulivyoona, mipango hiyo ilitia ndani dhabihu ya fidia ya Mwanaye mpendwa, ambayo ilimgharimu sana Baba yake.—1 Yohana 4:10.
23. Taja sababu moja inayomfanya Yehova awe “Mungu mwenye furaha,” na sura inayofuata itajibu swali gani muhimu?
23 Naam, tangu mwanzo Yehova amechukua hatua ya kwanza kuwapenda wanadamu. ‘Alitupenda kwanza’ katika njia nyingi sana. Upendo hudumisha amani na shangwe, ndiyo sababu Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Hata hivyo, swali muhimu linazuka. Je, kweli Yehova anampenda kila mmoja wetu? Sura inayofuata itajibu swali hilo.
a Kitenzi phi·leʹo, kinachomaanisha ‘kuwa na shauku, kuthamini, au kupenda (kama mtu anavyompenda rafiki wa karibu au ndugu),” hutumiwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Aina fulani ya neno stor·geʹ, au upendo uliopo kati ya watu wa familia, inatumiwa kwenye 2 Timotheo 3:3 kuonyesha kwamba upendo huo ungekuwa haba katika siku za mwisho. Neno Eʹros, au upendo wa kimahaba kati ya watu wa jinsia tofauti, halitajwi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ijapokuwa upendo huo unazungumziwa katika Biblia.—Mithali 5:15-20.
b Maandiko mengine yanatumia semi kama hizo. Kwa mfano, “Mungu ni nuru” na “Mungu . . . ni moto unaokula kabisa.” (1 Yohana 1:5; Waebrania 12:29) Lakini semi hizo zinapasa kuonwa kuwa milinganisho (sitiari), kwa kuwa zinamlinganisha Yehova na vitu vya asili. Yehova ni kama nuru, kwa kuwa yeye ni mtakatifu na mwadilifu. Hana “giza” wala uchafu wowote. Naye anaweza kulinganishwa na moto kwa sababu ya nguvu zake za kuangamiza.
-
-
Hakuna Kitu Kinachoweza “Kututenga na Upendo wa Mungu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 24
Hakuna Kitu Kinachoweza “Kututenga na Upendo wa Mungu”
1. Watu wengi, kutia ndani Wakristo fulani wa kweli, wana maoni gani yenye kuvunja moyo?
JE, YEHOVA anakupenda? Baadhi ya watu wanakubali kwamba Mungu anawapenda wanadamu kwa ujumla kama andiko la Yohana 3:16 linavyosema. Lakini wanahisi hivi: ‘Mungu hawezi kamwe kunipenda mimi.’ Mara kwa mara, hata Wakristo wa kweli huenda wakawa na shaka kuhusu jambo hilo. Mtu mmoja aliyevunjika moyo alisema: “Siwezi kuamini kwamba Mungu ananijali kwa vyovyote.” Je, unahisi hivyo nyakati nyingine?
2, 3. Ni nani anayetaka tuamini kwamba Yehova hatupendi au hatuthamini, na tunawezaje kupambana na maoni hayo?
2 Shetani anataka sana tuamini kwamba Yehova Mungu hatupendi wala hatuthamini. Ni kweli kwamba mara nyingi Shetani anawashawishi watu kupitia kiburi chao na majivuno yao. (2 Wakorintho 11:3) Lakini anafurahia pia kuwafanya wanyonge wajihisi hawafai kabisa. (Yohana 7:47-49; 8:13, 44) Shetani anafanya hivyo hasa katika hizi “siku za mwisho” zenye hatari. Watu wengi leo hulelewa katika familia ambazo hazina “shauku ya kiasili.” Wengine hukutana kila siku na watu wakali, wenye ubinafsi, na wenye vichwa vigumu. (2 Timotheo 3:1-5) Huenda watu hao wakaona kwamba hawafai au hakuna yeyote anayeweza kuwapenda kwa sababu wametendewa vibaya, kubaguliwa, au kuchukiwa kwa miaka mingi.
3 Ikiwa una hisia hizo zenye kuvunja moyo, usikate tamaa. Mara kwa mara, wengi wetu hujilaumu isivyofaa. Lakini kumbuka kwamba Neno la Mungu linakusudiwa “kunyoosha mambo” na “kupindua mambo yaliyotiwa kwa nguvu sana katika mahandaki.” (2 Timotheo 3:16; 2 Wakorintho 10:4) Biblia inasema hivi: “Tutahakikishia mioyo yetu mbele yake kwa habari ya chochote kile ambacho mioyo yetu huenda ikatulaumu katika hicho, kwa sababu Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu na ajua mambo yote.” (1 Yohana 3:19, 20) Hebu tuchunguze njia nne ambazo Maandiko hutusaidia ‘kuhakikishia mioyo yetu’ kwamba Yehova anatupenda.
Yehova Anakuthamini
4, 5. Mfano wa shore ambao Yesu alitoa unaonyeshaje kwamba tuna thamani machoni pa Yehova?
4 Kwanza, Biblia inafundisha waziwazi kwamba Yehova anamthamini kila mmoja wa watumishi wake. Kwa mfano, Yesu alisema: “Je, shore wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka kwenye ardhi bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiwe na hofu: Nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Mathayo 10:29-31) Maneno hayo yalimaanisha nini kwa wale waliomsikiliza Yesu katika karne ya kwanza?
“Nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi”
5 Huenda tukashangaa ni kwa nini mtu anunue shore? Katika siku za Yesu, shore alikuwa ndege wa bei rahisi sana aliyenunuliwa ili kuliwa. Ona kwamba mtu aliyelipa sarafu moja ya thamani ndogo sana, alipewa shore wawili. Lakini baadaye Yesu alisema kwamba mtu aliyelipa sarafu mbili, alipewa shore watano badala ya shore wanne. Shore mmoja aliongezwa kana kwamba hakuwa na thamani yoyote. Huenda viumbe hao hawakuwa na thamani yoyote machoni pa wanadamu, lakini Muumba aliwaonaje? Yesu alisema: “Hakuna hata mmoja wao [hata yule aliyeongezwa] hupata kusahaulika mbele ya Mungu.” (Luka 12:6, 7) Sasa huenda tumeanza kuelewa alilomaanisha Yesu. Ikiwa Yehova anamthamini sana shore mmoja, vipi mwanadamu? Kama Yesu alivyoeleza, Yehova anatujua vizuri sana. Kwani, hata nywele za kichwa chetu zimehesabiwa zote!
6. Kwa nini tuna hakika kwamba Yesu hakutia chumvi aliposema kwamba nywele za kichwa chetu zimehesabiwa?
6 Je, kweli nywele zetu zimehesabiwa? Huenda wengine wakadhani kwamba Yesu alitia chumvi. Hata hivyo, hebu fikiria tumaini la ufufuo. Ni lazima Yehova awe anatujua vizuri sana ili aweze kutuumba upya! Anatuthamini sana hivi kwamba anakumbuka kila jambo, hata chembe zetu za urithi, kumbukumbu na ujuzi wetu wa maisha yetu yote.a Kichwa cha wastani huwa na nywele 100,000 hivi, kwa hiyo kuhesabu nywele za vichwa vyetu ni jambo rahisi sana ikilinganishwa na kukumbuka mambo hayo yote.
Kwa Nini Yehova Anatuthamini?
7, 8. (a) Yehova hufurahia kuona sifa zipi anapotafuta-tafuta mioyo ya wanadamu? (b) Yehova anathamini kazi gani njema tunazofanya?
7 Pili, Biblia hutufundisha sababu zinazomfanya Yehova awathamini watumishi wake. Kwa ufupi, sifa zetu nzuri na jitihada zetu zinampendeza. Mfalme Daudi alimwambia hivi Solomoni mwanaye: “BWANA hutafuta-tafuta mioyo yote, na kuyatambua mawazo yote ya fikira.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Mungu anapotafuta-tafuta mioyo ya mabilioni ya wanadamu katika ulimwengu huu wenye jeuri na uliojaa chuki, anafurahi sana kumpata mtu mwenye moyo unaopenda amani, kweli, na uadilifu. Mungu hufanya nini anapompata mtu anayempenda kwa moyo wote, anayetaka kujifunza na kuwafundisha wengine kumhusu? Yehova anatuambia kwamba yeye anawaona wale wanaowafundisha wengine kumhusu. Hata ana “kitabu cha ukumbusho” kwa ajili ya wote ‘wanaomcha BWANA, na kulitafakari jina lake.’ (Malaki 3:16) Anathamini sana sifa hizo.
8 Ni baadhi ya kazi gani njema ambazo Yehova anathamini? Bila shaka anathamini jitihada zetu za kumwiga Mwanaye, Yesu Kristo. (1 Petro 2:21) Kazi moja muhimu ambayo Mungu anathamini ni ile ya kueneza habari njema za Ufalme wake. Twasoma hivi kwenye Waroma 10:15: “Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale watangazao habari njema ya mambo mema!” Huenda kwa kawaida tusiione miguu yetu duni kuwa “yenye kupendeza,” au mirembo. Lakini hapa miguu ni mfano wa jitihada za watumishi wa Yehova za kuhubiri habari njema. Jitihada hizo zote ni zenye kupendeza na zenye thamani sana machoni pake.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.
9, 10. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anathamini uvumilivu wetu tunapokabili magumu mbalimbali? (b) Yehova hana maoni gani yasiyofaa kuwahusu watumishi wake waaminifu?
9 Yehova anathamini pia uvumilivu wetu. (Mathayo 24:13) Kumbuka kwamba Shetani anataka umpe Yehova kisogo. Kila siku unayodumu ukiwa mwaminifu kwa Yehova unasaidia kujibu lawama za Shetani. (Mithali 27:11) Nyakati nyingine si rahisi kuvumilia. Matatizo ya afya, matatizo ya kifedha, mifadhaiko, na vipingamizi vingine vinaweza kufanya maisha yawe magumu siku baada ya siku. Tunaweza kuvunjika moyo kwa sababu ya matumaini yasiyotimizwa. (Mithali 13:12) Yehova anathamini hata zaidi uvumilivu wetu tunapokabili majaribu hayo. Ndiyo sababu Mfalme Daudi alimwomba Yehova ahifadhi machozi yake katika “chupa” kisha akasema hivi kwa uhakika: “Je! hayamo katika kitabu chako?” (Zaburi 56:8) Naam, Yehova anathamini na kukumbuka machozi na mateso yote ambayo tunavumilia tunapoendelea kuwa waaminifu kwake. Machozi hayo ni yenye thamani machoni pake kama machozi ya Daudi.
Yehova anathamini uvumilivu wetu tunapokabili majaribu
10 Lakini mtu anayejihukumu moyoni anaweza kupuuza mambo yanayoonyesha kwamba anathaminiwa na Mungu. Huenda akajiambia hivi moyoni: ‘Lakini kuna watu wengine wengi ambao ni bora kuliko mimi. Haikosi Yehova anahuzunika sana anaponilinganisha nao!’ Yehova hawalinganishi watu; wala hashikilii mno maoni yake. (Wagalatia 6:4) Yeye husoma mioyo yetu kwa makini sana, naye huthamini sifa zozote nzuri ambazo tunazo—hata zile ndogo.
Yehova Huchunguza kwa Makini Jema na Baya
11. Tunaweza kujifunza nini kumhusu Yehova kutokana na jinsi alivyoshughulikia kisa cha Abiya?
11 Tatu, Yehova hutuchunguza kwa makini na kutafuta lililo jema. Kwa mfano, Yehova alipoagiza jamaa yote yenye kuasi ya Mfalme Yeroboamu iangamizwe, Aliamuru kwamba Abiya, mmoja wa wana wa mfalme, azikwe kwa heshima. Kwa nini? “Limeonekana ndani yake jambo lililo jema kwa BWANA, Mungu wa Israeli.” (1 Wafalme 14:1, 10-13) Basi Yehova alichunguza kwa makini moyo wa kijana huyo na kupata “jambo lililo jema.” Hata iwe jambo hilo jema lilikuwa dogo kadiri gani, Yehova aliona kwamba linafaa kuandikwa katika Neno lake. Hata alimthawabisha kwa sababu ya jambo hilo. Alimwonyesha rehema kwa kadiri ifaayo mtu huyo wa jamaa yenye kuasi.
12, 13. (a) Kisa cha Mfalme Yehoshafati kinaonyeshaje kwamba Yehova anaona sifa zetu nzuri hata tunapofanya dhambi? (b) Yehova hutendaje kama Baba mwenye upendo anapochunguza kazi na sifa zetu nzuri?
12 Mfano mzuri zaidi unahusiana na Mfalme Yehoshafati aliyekuwa mwema. Mfalme huyo alipotenda jambo la kipumbavu, nabii wa Yehova alimwambia hivi: “Kwa ajili ya hayo ghadhabu i juu yako itokayo kwa BWANA.” Ulikuwa ujumbe wenye kuogofya kama nini! Lakini ujumbe wa Yehova haukukomea hapo. Uliendelea kusema hivi: “Walakini yameonekana mema ndani yako.” (2 Mambo ya Nyakati 19:1-3) Kwa hiyo, Yehova hakupuuza wema wa Yehoshafati kwa sababu ya hasira Yake adilifu. Yeye hakutenda kama wanadamu wasiokamilika. Tunapokasirishwa na wengine, huenda tukapuuza wema wao. Na tunapofanya dhambi, sisi huaibika, hutamauka, na kuhisi hatia hivi kwamba tunapuuza wema wetu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova anatusamehe tunapotubu na kujitahidi kabisa kutorudia dhambi zetu.
13 Yehova anapokuchunguza, anatupilia mbali dhambi hizo, kama vile mchimba-dhahabu anavyotupilia mbali changarawe zisizofaa. Vipi kazi na sifa zako nzuri? Aah, sifa hizo ni “dhahabu” kwake kwa hivyo anazihifadhi! Je, umeona jinsi ambavyo wazazi wenye upendo wanavyotunza sana picha au kazi za shuleni za watoto wao, nyakati nyingine kwa miaka mingi sana baada ya watoto wao kuzisahau? Yehova ni Baba asiye na kifani katika kuwapenda watoto wake. Maadamu tunaendelea kuwa waaminifu kwake, hasahau kamwe kazi na sifa zetu nzuri. Kwa kweli, kwa maoni yake, kusahau kazi hizo kungekuwa kukosa uadilifu, naye hawezi kamwe kukosa uadilifu. (Waebrania 6:10) Yeye pia hutuchunguza kwa njia nyingine.
14, 15. (a) Kwa nini Yehova hapuuzi kamwe sifa zetu nzuri kwa sababu ya kutokamilika kwetu? Toa mfano. (b) Yehova atafanya nini na sifa zetu nzuri, naye anawaonaje watu wake waaminifu?
14 Yehova hazingatii kasoro zetu bali anaona hasa uwezo wetu. Kwa mfano: Watu wanaopenda sanaa hufanya yote wawezayo ili kurekebisha michoro au sanaa zilizoharibika. Mtu fulani alipofyatua risasi na kuharibu mchoro wa msanii Leonardo da Vinci wenye thamani ya dola milioni 30 za Marekani, katika Jumba la Kitaifa la Sanaa huko London, Uingereza, hakuna mtu hata mmoja aliyedokeza kwamba mchoro huo utupwe kwa sababu ulikuwa umeharibika. Kazi ya kurekebisha mchoro huo bora sana uliodumu kwa miaka 500 hivi ilianza mara moja. Kwa nini? Kwa sababu watu wanaopenda sanaa waliuthamini sana. Wewe una thamani kuliko mchoro wa chokaa na makaa sivyo? Bila shaka, una thamani sana machoni pa Mungu—haidhuru hali mbaya ya kutokamilika uliyorithi. (Zaburi 72:12-14) Yehova Mungu, Muumba stadi wa wanadamu, atafanya yote yanayohitajika ili wote wanaokubali utunzaji wake wenye upendo wawe watu wakamilifu hatimaye.—Matendo 3:21; Waroma 8:20-22.
15 Naam, Yehova huona sifa zetu nzuri ambazo huenda tusione. Na tunapomtumikia, atakuza sifa hizo nzuri mpaka hatimaye tuwe wakamilifu. Yehova anawathamini watumishi wake waaminifu na anawaona kuwa wenye kutamanika, bila kujali jinsi ambavyo ulimwengu wa Shetani umetutendea.—Hagai 2:7.
Yehova Anatuthibitishia Upendo Wake
16. Ni uthibitisho gani bora kabisa unaoonyesha kwamba Yehova anatupenda, na twajuaje kwamba zawadi hiyo ilitolewa kwa ajili yetu?
16 Nne, Yehova anajitahidi kututhibitishia kwamba anatupenda. Hapana shaka kwamba dhabihu ya fidia ya Kristo ndiyo njia bora ya kupinga uwongo wa Shetani kwamba hatuthaminiwi wala hakuna yeyote anayeweza kutupenda. Hatupaswi kamwe kusahau kwamba maumivu ambayo Yesu alivumilia kwenye mti wa mateso kabla ya kufa, na maumivu makali zaidi ambayo Yehova alihisi alipomtazama Mwanaye mpendwa akifa ni uthibitisho wa kwamba wanatupenda. Kwa kusikitisha, watu wengi hawaamini kwamba zawadi hiyo ilitolewa kwa ajili yao. Wanajiona hawafai. Lakini, kumbuka kwamba mtume Paulo aliwanyanyasa wafuasi wa Kristo hapo awali. Hata hivyo, aliandika hivi: ‘Mwana wa Mungu alinipenda mimi na akajikabidhi mwenyewe kwa ajili yangu.’—Wagalatia 1:13; 2:20.
17. Yehova anatuvuta kwake na kwa Mwanaye kwa njia zipi?
17 Yehova anatuthibitishia upendo wake kwa kumsaidia kila mmoja wetu kufaidika na dhabihu ya Kristo. Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Ndiyo, Yehova humvuta kila mmoja wetu kwa Mwanaye na kwenye tumaini la uhai udumuo milele. Jinsi gani? Yehova humvuta kila mmoja wetu kupitia kazi ya kuhubiri, na kupitia roho yake takatifu ambayo hutusaidia kuelewa na kufuata kweli za kiroho licha ya udhaifu wetu na kutokamilika kwetu. Kwa hiyo, Yehova anaweza kutuambia kama alivyoliambia taifa la Israeli: “Nimekupenda kwa upendo wa milele, ndiyo maana nimekuvuta kwa fadhili zangu.”—Yeremia 31:3.
18, 19. (a) Yehova anatuonyesha upendo kupitia njia gani ya pekee sana, na tunajuaje kwamba anashughulikia jambo hilo yeye mwenyewe? (b) Neno la Mungu linatuhakikishiaje kwamba Yehova hutusikiliza kwa hisia-mwenzi?
18 Yamkini pendeleo la sala ndiyo njia ya pekee ya kufurahia upendo wa Yehova. Biblia inamsihi kila mmoja wetu ‘asali [kwa Mungu] bila kukoma.’ (1 Wathesalonike 5:17) Yeye husikiliza. Hata anaitwa “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Hajampa mtu mwingine yeyote, hata Mwanaye, mamlaka ya kusikiliza sala kwa niaba yake. Hebu fikiria: Muumba wa ulimwengu wote anatuhimiza tumfikie kwa sala, na kusema naye kwa uhuru. Naye husikilizaje? Je, anasikiliza tu bila hisia wala kujali? La hasha.
19 Yehova ana hisia-mwenzi. Hisia-mwenzi ni nini? Mkristo mmoja mwaminifu ambaye ni mzee kwa umri alisema: “Hisia-mwenzi ni kuhisi uchungu wako moyoni mwangu.” Je, kweli Yehova anaumizwa na uchungu wetu? Twasoma hivi kuhusu mateso ya watu wake wa taifa la Israeli: “Katika mateso yao yote yeye aliteswa.” (Isaya 63:9) Yehova hakuona tu taabu zao; bali alihisi uchungu kwa sababu ya taabu zao. Maneno ambayo Yehova aliwaambia watumishi wake yanaonyesha jinsi anavyohisi: “Anayewagusa nyinyi anagusa mboni ya jicho langu.”b (Zekaria 2:8, BHN) Mtu huhisi maumivu makali sana anapoguswa mboni ya jicho. Ndiyo, Yehova anahisi uchungu kwa ajili yetu. Tunapoteseka, anateseka pia.
20. Tunapaswa kuepuka maoni gani yasiyofaa kupatana na shauri la Waroma 12:3?
20 Mkristo mwenye usawaziko hapaswi kamwe kutumia uthibitisho huo wa upendo na staha ya Mungu kuwa udhuru wa kujivuna au kujiona kuwa bora. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia fadhili isiyostahiliwa niliyopewa naambia kila mtu huko miongoni mwenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali afikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia kipimo cha imani.” (Waroma 12:3) Tafsiri nyingine inasema hivi: “Ninamwambia kila mmoja wenu asijikadirie zaidi kuliko alivyo kikweli, lakini ajikadirie kwa kiasi.” (A Translation in the Language of the People, ya Charles B. Williams) Kwa hiyo, tunapofurahia kabisa upendo mchangamfu wa Baba yetu wa mbinguni, na tuwe wenye kiasi na kukumbuka kwamba hatustahili upendo wa Mungu kwa sababu ya jitihada zetu.—Luka 17:10.
21. Tunapaswa kuendelea kukataa kabisa uwongo gani wa Shetani, na tunahitaji kuendelea kujihakikishia mioyoni mwetu ukweli gani ulio katika Biblia?
21 Kila mmoja wetu na afanye yote awezayo kukataa katakata uwongo wote wa Shetani, hata uwongo kwamba hatufai au hatuwezi kupendwa. Ikiwa hali zilizokupata maishani zimekufunza ujione huwezi kamwe kunufaishwa na upendo mwingi wa Mungu, au kuona kazi zako nzuri kuwa duni mno hivi kwamba Yehova hawezi kuziona, au dhambi zako kuwa nyingi mno zisiweze kufunikwa na kifo cha Mwanaye mpendwa, umefunzwa uwongo mtupu. Kataa katakata uwongo huo kwa moyo wako wote! Na tuendelee kujihakikishia mioyoni mwetu ukweli wa maneno ya Paulo: “Nasadiki kwamba wala kifo wala uhai wala malaika wala serikali wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 8:38, 39.
a Mara nyingi Biblia huhusianisha tumaini la ufufuo na kumbukumbu la Yehova. Yobu aliyekuwa mwaminifu alimwambia Yehova hivi: “Laiti . . . ungeniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka!” (Ayubu 14:13) Yesu alisema kwamba “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho” watafufuliwa. Hilo ni kweli kwa sababu Yehova anawakumbuka kabisa wafu ambao anakusudia kuwafufua.—Yohana 5:28, 29.
b Tafsiri fulani zinadokeza kwamba mtu anayegusa watu wa Mungu hagusi jicho la Mungu, bali anagusa jicho lake mwenyewe au jicho la Israeli. Kosa hilo lilitokana na waandishi fulani ambao walidhani kwamba andiko hilo halimheshimu Mungu na hivyo wakalibadili. Jitihada zao zilizopotoka zilificha wingi wa hisia-mwenzi za Yehova.
-
-
“Huruma Nyororo ya Mungu Wetu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 25
“Huruma Nyororo ya Mungu Wetu”
1, 2. (a) Mama hutendaje mtoto wake mchanga anapolia? (b) Ni hisia gani ambayo ni yenye nguvu zaidi kuliko huruma ya mama?
MTOTO mchanga aanza kulia usiku wa manane. Mama yake anaamka mara moja. Mama halali kwa utulivu tangu alipojifungua mtoto huyo. Amejua kutofautisha vilio mbalimbali vya mtoto wake mchanga. Kwa hiyo, kwa kawaida anaweza kujua iwapo mtoto wake anahitaji kunyonya, kubebwa, au kushughulikiwa kwa njia nyingine. Mama humshughulikia mtoto wake haidhuru sababu inayomfanya alie. Hawezi kupuuza mahitaji ya mtoto wake kwa sababu anampenda sana.
2 Huruma ya mama kwa mtoto wake ni mojawapo ya hisia zenye nguvu sana ambazo wanadamu huonyesha. Hata hivyo, kuna hisia ambayo ni yenye nguvu kupita hisia zote—huruma nyororo ya Mungu wetu Yehova. Tunaweza kumkaribia Yehova zaidi tukichunguza sifa hii yenye kuvutia. Basi na tuzungumzie maana ya huruma na jinsi ambavyo Mungu wetu huonyesha sifa hiyo.
Huruma Ni Nini?
3. Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa “onyesha rehema” au “hurumia” kinamaanisha nini?
3 Katika Biblia, huruma na rehema zinahusiana sana. Maneno kadhaa ya Kiebrania na Kigiriki yanadokeza sifa ya huruma yenye upendo. Kwa mfano, fikiria kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ, ambacho mara nyingi hutafsiriwa “onyesha rehema” au “hurumia.” Kichapo kimoja cha marejeo kinaeleza kwamba kitenzi ra·chamʹ “kinaonyesha huruma nyingi na yenye upendo, kama ile tunayohisi tunapowaona wapendwa wetu au wale wanaohitaji msaada wetu wakiteseka au kuumia.” Neno hilo la Kiebrania, ambalo Yehova anatumia kujihusu, linahusiana na neno linalomaanisha “tumbo la uzazi” nalo linaweza kufasiriwa kuwa “huruma ya mama.”a—Kutoka 33:19; Yeremia 33:26.
“Je, mwanamke aweza kumsahau . . . mwana wa tumbo lake? ”
4, 5. Biblia inatumiaje hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha kuhusu huruma ya Yehova?
4 Biblia inatumia hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha maana ya huruma ya Yehova. Twasoma hivi kwenye Isaya 49:15: “Je! mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie [ra·chamʹ] mwana wa tumbo lake? naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.” Maelezo hayo yenye kugusa moyo yanakazia jinsi Yehova alivyo na huruma nyingi kwa watu wake. Jinsi gani?
5 Ni vigumu kuwazia kwamba mama anaweza kusahau kumnyonyesha na kumtunza mtoto wake mchanga. Kwani, mtoto mchanga ni hoi; anahitaji kupendwa na kutunzwa na mama yake usiku na mchana. Ingawa hivyo, inasikitisha kupata habari kuhusu akina mama wanaowatupa watoto wao, hasa katika ‘nyakati hizi za hatari’ kwa sababu watu hawana “shauku ya kiasili.” (2 Timotheo 3:1, 3) “Lakini mimi sitakusahau wewe,” atangaza Yehova. Yehova hakosi kamwe kuwaonyesha watumishi wake huruma nyororo. Huruma hiyo ni yenye nguvu zaidi ya hisia yenye nguvu tunayoweza kuwazia, yaani, huruma ambayo kwa kawaida mama humwonyesha mtoto wake mchanga. Haishangazi kwamba mtoa-maoni mmoja alisema hivi kuhusu Isaya 49:15: “Hili ni mojawapo, au ndilo neno linalofafanua upendo wa Mungu waziwazi zaidi katika Agano la Kale.”
6. Wanadamu wengi wasiokamilika wamekuwa na maoni gani kuhusu huruma nyororo, lakini Yehova anatuhakikishia nini?
6 Je, kuwa na huruma nyororo ni udhaifu? Wanadamu wengi wasiokamilika wamekuwa na maoni hayo. Kwa mfano, mwanafalsafa Mroma Seneca, msomi maarufu wa Roma ambaye aliishi wakati wa Yesu, alifundisha kwamba “huruma ni udhaifu wa akili.” Seneca aliunga mkono Ustoiki, falsafa inayokazia kuwa na utulivu bila hisia zozote. Mtu mwenye hekima anaweza kuwasaidia wale wanaotaabika, akasema Seneca, lakini hapaswi kuwahurumia kwa sababu atakosa utulivu akifanya hivyo. Maoni hayo ya ubinafsi kuhusu maisha yaliwazuia watu wasionyeshe huruma kutoka moyoni. Lakini sivyo alivyo Yehova! Yehova anatuhakikishia katika Neno lake kwamba yeye “ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema [kihalisi, “mwenye huruma”].” (Yakobo 5:11) Kama tutakavyoona, kuonyesha huruma si udhaifu bali ni sifa muhimu sana yenye nguvu. Hebu tuone jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo kama mzazi mwenye upendo.
Yehova Alipolihurumia Taifa
7, 8. Waisraeli walitesekaje katika Misri ya kale, na Yehova alichukua hatua gani kwa sababu ya mateso yao?
7 Huruma ya Yehova yaonekana wazi kutokana na jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Kufikia mwishoni mwa karne ya 16 K.W.K., mamilioni ya Waisraeli waliteswa sana walipokuwa watumwa katika Misri ya kale. Wamisri ‘walifanya maisha yao kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na ya matofali.’ (Kutoka 1:11, 14) Waisraeli walimlilia Yehova awasaidie walipokuwa wakiteseka. Mungu mwenye huruma nyororo alichukua hatua gani?
8 Yehova aliwahurumia. Akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao.” (Kutoka 3:7) Yehova hakuweza kamwe kutazama watu wake wakiteseka au kusikia vilio vyao na asiwahurumie. Kama tulivyoona katika Sura ya 24 ya kitabu hiki, Yehova ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Na hisia-mwenzi, yaani, sifa ya kuguswa moyo na uchungu wa wengine inahusiana sana na huruma. Lakini Yehova hakuwahurumia tu watu wake; alichochewa kuwasaidia. Andiko la Isaya 63:9 lasema: “Kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe.” Yehova aliwaokoa Waisraeli kutoka Misri kwa “mkono hodari.” (Kumbukumbu la Torati 4:34) Baadaye, aliwalisha kimuujiza na kuwapa nchi yenye rutuba.
9, 10. (a) Kwa nini Yehova aliwakomboa Waisraeli tena na tena baada ya kuingia katika Nchi Iliyoahidiwa? (b) Katika siku za Yeftha, Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka katika mateso gani, ni nini kilichomchochea kufanya hivyo?
9 Huruma ya Yehova haikuishia hapo. Waisraeli walimwasi tena na tena baada ya kuingia katika Nchi Iliyoahidiwa na hivyo wakateseka. Lakini walirudiwa na fahamu na kumlilia Yehova. Aliwakomboa tena na tena. Kwa nini? “Kwa sababu aliwahurumia watu wake.”—2 Mambo ya Nyakati 36:15; Waamuzi 2:11-16.
10 Fikiria mambo yaliyotukia siku za Yeftha. Waisraeli walipoanza kuitumikia miungu ya uwongo, Yehova aliwaacha wateswe na Waamoni kwa miaka 18. Mwishowe, walitubu. Biblia inatuambia hivi: “Nao wakaiondoa hiyo miungu ya kigeni iliyokuwa kati yao, nao wakamtumikia BWANA; na roho yake ilihuzunika kwa sababu ya msiba wa Israeli.”b (Waamuzi 10:6-16) Mara tu baada ya watu wake kutubu kikweli, Yehova hakuweza kuvumilia kuwaona wakiteseka. Kwa hiyo, Mungu mwenye huruma nyororo alimpa Yeftha nguvu ili awakomboe Waisraeli kutoka mikononi mwa adui zao.—Waamuzi 11:30-33.
11. Twajifunza nini kuhusu huruma tunapozingatia jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli?
11 Twajifunza nini kuhusu huruma nyororo ya Yehova tunapozingatia jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli? Jambo moja ambalo tunajifunza ni kwamba hawaonei huruma watu wanaoteseka na kuwaacha tu. Kumbuka yule mama ambaye anachochewa na huruma kumsaidia mtoto wake mchanga anayelia. Vivyo hivyo, Yehova hapuuzi vilio vya watu wake. Huruma yake nyororo humchochea kukomesha mateso yao. Zaidi ya hayo, twajifunza pia kwamba huruma si udhaifu kamwe, kwa sababu sifa hii ya kutoka moyoni ilimchochea achukue hatua madhubuti ya kuwatetea watu wake. Lakini je, Yehova anawahurumia watumishi wake wakiwa kikundi tu?
Yehova Amhurumia Mtu Mmoja-Mmoja
12. Sheria ilionyeshaje huruma ya Yehova kwa mtu mmoja-mmoja?
12 Sheria ambayo Mungu alilipa taifa la Israeli ilionyesha kwamba alimhurumia mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, fikiria jinsi alivyowajali maskini. Yehova alijua kwamba Mwisraeli angeweza kuwa maskini kwa sababu ya hali zisizotazamiwa. Maskini walipaswa kutendewaje? Yehova aliwapa Waisraeli amri hii kali: “Usifanye moyo wako kuwa mgumu, wala usimfumbie mkono wako nduguyo maskini. Mpe kwa kweli, wala moyo wako usisikitike utakapompa; kwa kuwa atakubarikia BWANA, Mungu wako, kwa neno hili katika kazi yako yote.” (Kumbukumbu la Torati 15:7, 10) Yehova pia aliwaagiza Waisraeli wasivune kabisa pembeni mwa mashamba yao au kukusanya masazo. Masazo hayo yaliachwa kwa ajili ya maskini. (Mambo ya Walawi 23:22; Ruthu 2:2-7) Taifa la Israeli lilipotii sheria hiyo, maskini hawakuhitaji kuombaomba chakula. Hilo laonyesha huruma nyororo ya Yehova, sivyo?
13, 14. (a) Maneno ya Daudi yanatuhakikishiaje kwamba Yehova anamjali sana kila mmoja wetu? (b) Toa mfano kuonyesha kwamba Yehova yu karibu na wale “waliovunjika moyo” au “waliopondeka roho.”
13 Leo pia, Mungu wetu mwenye upendo anamjali sana kila mmoja wetu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba anajua kabisa mateso yoyote ambayo huenda yakatupata. Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:15, 18) Mtoa-maoni mmoja wa Biblia aeleza hivi kuhusu wale wanaotajwa na andiko hilo: “Ni watu waliovunjika moyo na wenye majuto, yaani, watu walionyenyekezwa na dhambi, wasiojiheshimu; wanaojiona kuwa duni, na wasiojiamini.” Huenda wakahisi kwamba Yehova yu mbali na wao, na kwamba wao ni duni hivi kwamba hawezi kuwajali. Lakini sivyo ilivyo. Maneno ya Daudi yanatuhakikishia kwamba Yehova hawaachi wale “wanaojiona kuwa duni.” Mungu wetu mwenye huruma anajua kwamba tunahitaji msaada wake sana tunapohisi hivyo, naye yu tayari kutusaidia.
14 Fikiria kisa hiki halisi. Mama mmoja nchini Marekani alimpeleka mwanaye mwenye umri wa miaka miwili hospitalini kwa sababu alikuwa na ugonjwa mbaya wa kifaduro. Baada ya kumchunguza, madaktari walimwambia mama kwamba mwanaye angelazwa hospitalini usiku huo. Mama alikesha wapi usiku huo? Alikesha kwenye kiti humohumo hospitalini, karibu na kitanda cha mwanaye! Mwanaye alikuwa mgonjwa kwa hiyo mama alitaka sana kuwa karibu naye. Bila shaka, tunaweza kumtarajia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo atufanyie mengi zaidi! Kwani, tumeumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Maneno yenye kugusa moyo ya Zaburi 34:18 yanatueleza kwamba ‘tunapovunjika moyo’ au ‘kupondeka roho,’ Yehova, kama baba mwenye upendo, “yu karibu”—sikuzote akiwa mwenye huruma na tayari kutusaidia.
15. Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu?
15 Basi, Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu? Haondoi kisababishi cha mateso yetu sikuzote. Lakini Yehova amewapa maandalizi tele wale wanaomwomba msaada. Neno lake, Biblia, lina mashauri yanayofaa ambayo yanaweza kuboresha hali. Katika kutaniko, Yehova ameweka waangalizi wanaostahili kiroho, ambao wanajitahidi kuwa na huruma kama yeye wanapowasaidia waabudu wenzao. (Yakobo 5:14, 15) Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye huwapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Zaburi 65:2, NW; Luka 11:13) Roho hiyo inaweza kututia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili tuweze kuvumilia hadi Ufalme wa Mungu utakapokomesha matatizo yote yanayofadhaisha. (2 Wakorintho 4:7) Tunamshukuru kwelikweli kwa sababu ya maandalizi hayo yote, sivyo? Tusisahau kwamba maandalizi hayo ni uthibitisho wa huruma nyororo ya Yehova.
16. Yehova alionyesha huruma yake kwa njia gani bora, na inamfaidije kila mmoja wetu?
16 Hapana shaka kwamba Yehova alionyesha huruma yake kwa njia bora zaidi alipomtoa Yule anayempenda sana awe fidia kwa ajili yetu. Yehova alionyesha upendo kwa kutoa dhabihu hiyo ambayo ilitufungulia njia ya kupata wokovu. Kumbuka kwamba fidia hiyo inamfaidi kila mmoja wetu. Ndiyo sababu Zekaria, baba ya Yohana Mbatizaji, alitabiri kwamba zawadi hiyo ilithibitisha “huruma nyororo ya Mungu wetu.”—Luka 1:78.
Huruma ya Yehova Inapofikia Kikomo
17-19. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba huruma ya Yehova ina kikomo? (b) Kwa nini huruma ya Yehova kwa watu wake ilifikia kikomo?
17 Je, tufikiri kwamba huruma nyororo ya Yehova haina kikomo? La hasha, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Yehova hawahurumii watu ambao wanakataa njia zake adilifu. (Waebrania 10:28) Ili kuelewa sababu inayomfanya atende hivyo, kumbuka taifa la Israeli.
18 Ijapokuwa Yehova aliwakomboa tena na tena kutoka kwa maadui wao, mwishowe huruma yake ilifikia kikomo. Watu hao wakaidi waliabudu sanamu, hata walileta sanamu zao zenye kuchukiza ndani ya hekalu la Yehova! (Ezekieli 5:11; 8:17, 18) Zaidi ya hayo, twaambiwa hivi: “Waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.” (2 Mambo ya Nyakati 36:16) Hatimaye Waisraeli walizidi hivi kwamba hakukuwa na msingi wowote ufaao wa kuwahurumia, nao walichochea hasira adilifu ya Yehova. Matokeo yakawa nini?
19 Yehova hakuweza tena kuwahurumia watu wake. Alitangaza hivi: “Sitawahurumia, sitawaachia wala sitawarehemu, bali nitawaangamiza.” (Yeremia 13:14, BHN) Basi, Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa, na Waisraeli wakachukuliwa mateka hadi Babiloni. Matokeo yanakuwa mabaya kama nini wanadamu wenye dhambi wanapoasi sana hivi kwamba huruma ya Mungu inafikia kikomo!—Maombolezo 2:21.
20, 21. (a) Ni nini kitakachotukia huruma ya Mungu itakapofikia kikomo katika siku zetu? (b) Tutazungumzia zawadi gani ya huruma ya Yehova katika sura inayofuata?
20 Vipi leo? Yehova hajabadilika. Kwa sababu ya huruma yake, amewaamuru Mashahidi wake wahubiri ‘habari njema ya ufalme’ katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Watu wenye mioyo minyoofu wanapoitikia, Yehova huwasaidia kuelewa ujumbe wa Ufalme. (Matendo 16:14) Lakini kazi hii haitaendelea milele. Bila shaka ni kinyume cha huruma ya Yehova kuruhusu ulimwengu huu mwovu pamoja na mateso na taabu zake ziendelee milele. Yehova atahukumu mfumo huu wa mambo huruma yake itakapofikia kikomo. Hata wakati huo, atakuwa akionyesha huruma—huruma kwa ajili ya ‘jina lake takatifu’ na kwa ajili ya watumishi wake waaminifu. (Ezekieli 36:20-23) Yehova atakomesha kabisa uovu na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. Yehova atangaza hivi kuhusu waovu: “Jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma; lakini nitaleta njia yao juu ya vichwa vyao.”—Ezekieli 9:10.
21 Kabla ya wakati huo, Yehova anawahurumia watu, hata wale ambao wanakabili uharibifu. Wanadamu wenye dhambi ambao wanatubu kikweli wanaweza kufaidika na mojawapo ya zawadi bora zaidi za huruma ya Yehova, yaani, msamaha. Katika sura inayofuata, tutazungumzia baadhi ya masimulizi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Yehova anavyosamehe kabisa.
a Hata hivyo, kwenye Zaburi 103:13, kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ kinamaanisha rehema, au huruma, ambayo baba huwaonyesha watoto wake.
b Usemi unaotafsiriwa “roho yake ilihuzunika” wamaanisha kihalisi ‘subira yake ilifikia kikomo.’ Biblia Habari Njema yasema: “Hakuweza kuvumilia zaidi kuona taabu za Waisraeli.” Kichapo Tanakh—A New Translation of the Holy Scriptures chasema hivi: “Hakuweza kustahimili kuona Israeli ikitaabika.”
-
-
Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 26
Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”
1-3. (a) Mtunga-zaburi Daudi alilemewa na nini, na alipataje faraja katika fadhaa zake? (b) Huenda tukalemewa na nini tunapofanya dhambi, lakini Yehova anatuhakikishia nini?
“DHAMBI zangu zimenifunikiza kichwa, kama mzigo mzito zimenilemea mno. Nimedhoofika na kuchubuka sana,” akaandika mtunga-zaburi Daudi. (Zaburi 38:4, 8) Daudi alijua jinsi dhamiri yenye hatia inavyolemea sana. Lakini alipata faraja katika fadhaa zake. Alifahamu kwamba Yehova anachukia dhambi, lakini hamchukii mtenda-dhambi ikiwa anatubu kikweli na kuacha mwenendo wake wa dhambi. Daudi alisema hivi akiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova yu tayari kuwasamehe wale wanaotubu: “Wewe, Bwana, . . . umekuwa tayari kusamehe.”—Zaburi 86:5.
2 Tunapofanya dhambi, huenda pia tukalemewa sana na dhamiri inayotuumiza. Kuhisi majuto ni jambo linalonufaisha. Kunaweza kutusukuma tuchukue hatua zinazofaa kusahihisha makosa yetu. Hata hivyo, kuna hatari ya kulemewa sana na hatia. Huenda tukajihukumu daima moyoni kwamba Yehova hatatusamehe hata tukitubu jinsi gani. Endapo ‘tutamezwa’ na hatia, huenda Shetani akajaribu kutuvunja moyo na kutufanya tuhisi kwamba hatuna thamani machoni pa Yehova, na hatufai kumwabudu.—2 Wakorintho 2:5-11.
3 Je, hivyo ndivyo Yehova anavyotuona? La hasha! Msamaha ni sifa ya upendo wa Yehova usio na kifani. Anatuhakikishia katika Neno lake kwamba yuko tayari kutusamehe tukitubu kikweli kutoka moyoni. (Mithali 28:13) Ili tusihisi kwamba Yehova hawezi kamwe kutusamehe, hebu tuone kinachomfanya atusamehe na jinsi anavyosamehe.
Kwa Nini Yehova Yuko “Tayari Kusamehe”?
4. Yehova anakumbuka nini kuhusu hali yetu, na hilo linamfanya ashughulike nasi kwa njia gani?
4 Yehova anajua udhaifu wetu. “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi,” yasema Zaburi 103:14. Hasahau kwamba sisi ni viumbe wa udongo, wenye kasoro, au udhaifu kwa sababu ya kutokamilika. Usemi kwamba anajua “umbo letu” unatukumbusha kuwa Biblia inamlinganisha Yehova na mfinyanzi na inatulinganisha na vyombo vya udongo anavyofinyanga.a (Yeremia 18:2-6) Mfinyanzi huyo Mkuu anashughulika nasi kupatana na hali yetu dhaifu yenye dhambi ikitegemea jinsi tunavyofuata au kutofuata mwongozo wake.
5. Kitabu cha Waroma kinaonyeshaje kwamba dhambi ina nguvu nyingi sana?
5 Yehova anaelewa jinsi dhambi ilivyo na nguvu nyingi. Neno lake hufafanua dhambi kuwa nguvu inayosababisha kifo kwa mwanadamu. Dhambi ina nguvu kadiri gani? Katika kitabu cha Waroma, mtume Paulo aeleza hivi: Tuko “chini ya dhambi,” kama vile wanajeshi walivyo chini ya amiri wao (Waroma 3:9); dhambi ‘imewatawala’ wanadamu wote kama mfalme (Waroma 5:21); ‘inakaa’ ndani yetu (Waroma 7:17, 20); “sheria” yake hufanya kazi ndani yetu daima, ikijaribu kuongoza maisha yetu. (Waroma 7:23, 25) Bila shaka dhambi ina nguvu nyingi sana juu ya mwili wetu usiokamilika.—Waroma 7:21, 24.
6, 7. (a) Yehova anawaonaje wale wanaotafuta rehema yake na kutubu kikweli? (b) Kwa nini hatupaswi kutumia vibaya rehema ya Mungu?
6 Kwa hiyo, Yehova anajua kwamba hatuwezi kumtii kikamili, hata tuwe tunatamani sana kufanya hivyo. Anatuhakikishia kwa upendo kwamba atatusamehe tukitafuta rehema yake na kutubu kikweli. Zaburi 51:17 yasema: “Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.” Yehova hatakataa kamwe, au kuupuuza moyo “uliovunjika na kupondeka” kwa sababu ya kulemewa na hatia.
7 Lakini je, hilo lamaanisha kwamba tunaweza kutumia vibaya rehema ya Mungu na kufanya dhambi huku tukitoa udhuru wa kwamba tumerithi dhambi? La hasha! Yehova haongozwi na hisia tu. Rehema yake ina mipaka. Hawezi kamwe kuwasamehe wale wanaofanya dhambi kimakusudi na kwa moyo mgumu, bila kutubu. (Waebrania 10:26) Kwa upande mwingine, yuko tayari kumsamehe mtu anayetubu kikweli. Hebu tuchunguze maneno yanayotumiwa katika Biblia kufafanua wazi sifa hiyo yenye kuvutia ya upendo wa Yehova.
Je, Yehova Husamehe Kabisa?
8. Yehova hufanya nini anapotusamehe dhambi zetu, na hilo latufanya tuwe na tumaini gani?
8 Daudi mwenye kutubu alisema hivi: “Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu. . . . Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu.” (Zaburi 32:5, italiki ni zetu.) Neno “ukanisamehe” ni tafsiri ya neno la Kiebrania ambalo hasa linamaanisha “inua” au “beba.” Linatumiwa hapa kumaanisha kuondolea mbali “hatia, dhambi, uasi-sheria.” Kwa hiyo, ni kana kwamba Yehova aliziinua dhambi za Daudi na kuziondolea mbali. Hapana shaka kwamba hilo lilipunguza hisia za hatia ambazo Daudi alikuwa nazo. (Zaburi 32:3) Sisi pia tunaweza kumtumaini kabisa Mungu ambaye anaondolea mbali dhambi za wale wanaotafuta msamaha wake kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya fidia ya Yesu.—Mathayo 20:28.
9. Yehova huweka dhambi zetu mbali nasi kadiri gani?
9 Daudi alitumia usemi mwingine ulio wazi zaidi kufafanua msamaha wa Yehova: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi.” (Zaburi 103:12, italiki ni zetu.) Mashariki ni mbali kadiri gani kutoka magharibi? Katika maana fulani, sikuzote mashariki huwa mbali kabisa na magharibi; pande hizo mbili haziwezi kamwe kukutana. Msomi mmoja anasema kwamba usemi huo unamaanisha “mbali iwezekanavyo; mbali kabisa.” Maneno ya Daudi yanatuambia kwamba Yehova anapotusamehe, anaweka dhambi zetu mbali kabisa nasi.
“Dhambi zenu . . . zitakuwa nyeupe kama theluji”
10. Yehova anapotusamehe dhambi zetu, kwa nini hatupaswi kuhisi kwamba tuna hatia ya dhambi hizo maisha yetu yote?
10 Je, umewahi kujaribu kuondoa doa katika nguo nyeupe? Huenda hukufaulu kuondoa doa hilo licha ya jitihada zako zote. Ona jinsi Yehova anavyoeleza msamaha wake: “Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.” (Isaya 1:18, italiki ni zetu.) Usemi “nyekundu sana” waonyesha kwamba rangi hiyo ni nyangavu.b Rangi “nyekundu” ilikuwa mojawapo ya rangi zilizotiwa kwenye nguo. (Nahumu 2:3) Hatuwezi kamwe kuondoa doa la dhambi kwa jitihada zetu. Lakini Yehova anaweza kuondoa dhambi ambazo ni nyekundu sana na kuzifanya nyeupe kama theluji au sufu isiyotiwa rangi. Yehova anapotusamehe dhambi zetu, hatupaswi kuhisi kwamba tuna hatia ya dhambi hizo maisha yetu yote.
11. Yehova anatupa dhambi zetu nyuma yake katika maana gani?
11 Hezekia alimwambia Yehova hivi katika wimbo wa shukrani wenye kugusa moyo ambao alitunga baada ya kuponywa ugonjwa wa kufisha: “Umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako.” (Isaya 38:17, italiki ni zetu.) Ni kana kwamba Yehova anachukua dhambi za mtenda-dhambi mwenye kutubu na kuzitupa nyuma Yake ambako Hawezi tena kuziona wala kuzikazia fikira. Kichapo kimoja kinasema kwamba andiko hilo laweza kuelezwa hivi: ‘Umefanya iwe ni kana kwamba sikufanya dhambi.’ Je, hilo si jambo lenye kutia moyo?
12. Nabii Mika anaonyeshaje kwamba Yehova anapotusamehe Anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu?
12 Katika ahadi ya urudisho, nabii Mika alieleza usadikisho wake kwamba Yehova angewasamehe watu wake wenye kutubu: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye . . . kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? . . . Nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.” (Mika 7:18, 19, italiki ni zetu.) Hebu fikiria maana ya maneno hayo kwa watu walioishi nyakati za Biblia. Hakukuwa na uwezekano wowote wa kupata kitu kilichotupwa “katika vilindi vya bahari.” Kwa hiyo maneno ya Mika yanamaanisha kwamba Yehova anapotusamehe, anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu.
13. Yesu aliposema “Utusamehe madeni yetu,” alimaanisha nini?
13 Yesu alitumia mfano wa wakopeshaji na wadeni ili kuonyesha jinsi Yehova anavyosamehe. Yesu alituhimiza tusali hivi: “Utusamehe madeni yetu.” (Mathayo 6:12) Kwa hiyo, Yesu alilinganisha dhambi na madeni. (Luka 11:4) Tunapofanya dhambi, tunakuwa “wadeni” wa Yehova. Kichapo kimoja cha marejeo kinasema kwamba kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “samehe,” kinamaanisha ‘kuachilia au kufuta deni na kutodai malipo.’ Yehova anapotusamehe ni kana kwamba anafuta deni ambalo tungedaiwa tulipe. Kwa hiyo, jambo hilo linaweza kuwafariji watenda-dhambi wenye kutubu. Yehova hatadai kamwe malipo ya deni ambalo amelifuta!—Zaburi 32:1, 2.
14. Usemi “mpate kufutiwa dhambi zenu” unaleta wazo gani?
14 Andiko la Matendo 3:19 laeleza zaidi jinsi ambavyo Yehova anasamehe: “Kwa hiyo, tubuni na mgeuke kabisa ili mpate kufutiwa dhambi zenu.” Neno “kufutiwa” limetafsiriwa kutokana na kitenzi cha Kigiriki kinachoweza kumaanisha “kupangusa, . . . kufuta au kuharibu.” Wasomi fulani wanasema kwamba maneno hayo yanaleta wazo la kufuta maandishi. Hilo liliwezekanaje? Wino uliotumiwa nyakati za kale ulitengenezwa kwa mchanganyiko wa kaboni, gundi, na maji. Mara tu baada ya kuandika kwa wino huo, mtu aliweza kuchukua sifongo yenye maji na kufuta kabisa maandishi hayo. Jambo hilo latufunza somo zuri sana kuhusu rehema ya Yehova. Anapotusamehe dhambi zetu, ni kana kwamba anachukua sifongo na kuzifuta kabisa.
Yehova anataka tujue kwamba yuko “tayari kusamehe”
15. Yehova anataka tujue nini kumhusu?
15 Tunapotafakari semi hizo mbalimbali za mfano, je, si wazi kwamba Yehova anataka tujue kwamba yuko tayari kutusamehe dhambi zetu maadamu tunatubu kikweli? Hakuna haja ya kuogopa kwamba huenda akatuhukumu kwa sababu ya dhambi hizo wakati ujao. Hilo lakaziwa na jambo jingine ambalo Biblia inasema kuhusu rehema ya Yehova isiyo na kifani: Anaposamehe, anasahau.
“Dhambi Yao Sitaikumbuka Tena”
16, 17. Biblia inamaanisha nini inaposema kwamba Yehova anasahau dhambi zetu, na kwa nini unajibu hivyo?
16 Yehova aliahidi hivi kuhusu wale walio katika agano jipya: “Nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yeremia 31:34) Je, hilo lamaanisha kwamba Yehova anaposamehe hawezi kukumbuka tena dhambi hizo? Bila shaka la. Biblia inatueleza kuhusu dhambi za watu wengi ambao walisamehewa na Yehova, kutia ndani Daudi. (2 Samweli 11:1-17; 12:13) Kwa wazi, Yehova bado anakumbuka makosa waliyofanya. Habari ya dhambi zao, toba yao, na jinsi walivyosamehewa na Mungu, imehifadhiwa kwa faida yetu. (Waroma 15:4) Hivyo basi, Biblia inamaanisha nini inaposema kwamba Yehova ‘hakumbuki’ dhambi za wale ambao anawasamehe?
17 Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa ‘nitakumbuka’ hakimaanishi kukumbuka tu mambo yaliyopita. Kichapo Theological Wordbook of the Old Testament chasema kwamba neno hilo ‘ladokeza pia kuchukua hatua inayofaa.’ Kwa hivyo, ‘kukumbuka’ dhambi kwatia ndani kuwaadhibu watenda-dhambi. (Hosea 9:9) Lakini Mungu anaposema kwamba “dhambi yao sitaikumbuka tena,” anatuhakikishia kwamba akisha samehe watenda-dhambi wenye kutubu, hatawaadhibu wakati ujao kwa sababu ya dhambi hizo. (Ezekieli 18:21, 22) Kwa hiyo, Yehova anasahau katika maana ya kwamba hataji-taji dhambi zetu ili atushtaki au kutuadhibu tena na tena. Inatufariji sana kujua kwamba Mungu wetu anasamehe na kusahau, sivyo?
Vipi Matokeo ya Dhambi?
18. Kwa nini mtenda-dhambi aliyetubu hupatwa na matokeo ya dhambi yake ajaposamehewa?
18 Je, yamaanisha kwamba mtenda-dhambi aliyetubu hatapatwa na matokeo ya dhambi yake kwa sababu amesamehewa? Sivyo hata kidogo. Hatuwezi kufanya dhambi na kufikiri kwamba tutaepuka matokeo yake. Paulo aliandika hivi: “Lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” (Wagalatia 6:7) Huenda tukapata madhara fulani kwa sababu ya dhambi zetu. Hilo halimaanishi kwamba Yehova anatuletea misiba baada ya kutusamehe. Anapopatwa na taabu, Mkristo hapaswi kufikiri kwamba labda Yehova anamwadhibu kwa sababu ya dhambi alizofanya zamani. (Yakobo 1:13) Kwa upande mwingine, Yehova hatukingi tusipatwe na matokeo ya dhambi zetu. Mambo yafuatayo yaweza kuwa matokeo yenye kuhuzunisha na yasiyoepukika ya dhambi—talaka, mimba haramu, ugonjwa unaoambukizwa kingono, kutotumainiwa au kutoheshimiwa. Kumbuka kwamba Daudi alipozini na Bath-sheba na kumwua Uria, Yehova alimsamehe lakini hakumkinga na matokeo mabaya sana ya dhambi zake.—2 Samweli 12:9-12.
19-21. (a) Sheria iliyoandikwa kwenye Mambo ya Walawi 6:1-7 ilimfaidije mkosaji na yule aliyekosewa? (b) Ikiwa dhambi zetu zimewaumiza wengine, Yehova anafurahi tunapochukua hatua gani?
19 Dhambi zetu zinaweza kuwa na matokeo mengine, hasa ikiwa tumewaumiza wengine. Kwa mfano, fikiria simulizi la Mambo ya Walawi sura ya 6. Hapa Sheria ya Musa inashughulikia kisa cha mtu anayefanya dhambi nzito kwa kuchukua bidhaa za Mwisraeli mwenzake kupitia wizi, unyang’anyi, au ulaghai. Kisha mtenda-dhambi huyo anakataa kukubali kosa lake, na kuthubutu kuapa kwa uwongo. Ushuhuda wa mkosaji unapingana na ule wa mtu aliyekosewa. Hata hivyo, baadaye yule mkosaji anasumbuliwa na dhamiri na kuungamana dhambi yake. Mbali na kuungama ni lazima afanye mambo mengine matatu ili Mungu amsamehe: arudishe kitu alichokuwa amechukua, amlipe yule aliyekosewa faini ya jumla ya asilimia 20 ya thamani ya vitu alivyoiba, na atoe kondoo mume kama dhabihu ya hatia. Halafu sheria inasema: “Kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake mbele za BWANA, naye atasamehewa.”—Mambo ya Walawi 6:1-7.
20 Sheria hiyo ilikuwa mpango wenye rehema kutoka kwa Mungu. Sheria hiyo ilimfaidi aliyekosewa, kwa kuwa alirudishiwa mali yake na bila shaka alifurahi sana alipoona mkosaji akikiri dhambi zake. Vilevile, sheria hiyo ilimfaidi yule ambaye alichochewa na dhamiri kukiri kosa lake na kulirekebisha. Kwa kweli, kama angekataa kufanya hivyo, hangesamehewa na Mungu.
21 Ingawa hatuko chini ya Sheria ya Musa, Sheria hiyo inatusaidia kufahamu kindani fikira za Yehova, na maoni yake kuhusu msamaha. (Wakolosai 2:13, 14) Ikiwa dhambi zetu zimewaumiza wengine, Mungu anafurahi tunapofanya yote tuwezayo kurekebisha hali hiyo. (Mathayo 5:23, 24) Huenda tukahitaji kukiri dhambi yetu, kukubali kwamba tumekosea, na hata kumwomba msamaha yule tuliyemkosea. Kisha tunaweza kumwomba Yehova msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. Tukifanya hivyo tutakuwa na hakika kwamba Mungu ametusamehe kikweli.—Waebrania 10:21, 22.
22. Huenda msamaha wa Yehova ukaambatana na nini?
22 Kama mzazi yeyote mwenye upendo, huenda Yehova akatusamehe na kututia pia nidhamu kwa kadiri fulani. (Mithali 3:11, 12) Mkristo aliyetubu huenda akalazimika kuacha pendeleo la kutumikia akiwa mzee, mtumishi wa huduma, au mhubiri wa wakati wote. Huenda akahuzunika sana kwa sababu ya kupoteza kwa muda fulani mapendeleo aliyothamini sana. Hata hivyo, ijapokuwa mtu anatiwa nidhamu hiyo haimaanishi kwamba Yehova hajamsamehe. Ni lazima tukumbuke kwamba Yehova anatutia nidhamu kwa sababu anatupenda. Tutafaidika sana tukikubali na kujifunza kutokana na nidhamu hiyo.—Waebrania 12:5-11.
23. Kwa nini hatupaswi kamwe kufikiri kwamba hatuwezi kusamehewa na Yehova, na kwa nini tunapaswa kumwiga kwa kuwasamehe wengine?
23 Inatia moyo kama nini kujua kwamba Mungu wetu yuko “tayari kusamehe”! Licha ya makosa ambayo huenda tukawa tumefanya, hatupaswi kamwe kufikiri kwamba hatuwezi kusamehewa na Yehova. Tukitubu kikweli, na kuchukua hatua za kurekebisha kosa hilo, na kuomba msamaha kwa bidii kwa msingi wa damu ya Yesu iliyomwagwa, tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba Yehova atatusamehe. (1 Yohana 1:9) Na tumwige Yehova kwa kuwasamehe wengine. Ikiwa Yehova ambaye hafanyi dhambi, anatusamehe kwa upendo sana, je, sisi wanadamu wenye dhambi hatupaswi kufanya yote tuwezayo kusameheana?
a Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “umbo letu” linatumiwa pia kuhusiana na vyombo vya udongo vinavyofinyangwa na mfinyanzi.—Isaya 29:16.
b Msomi mmoja anasema kwamba rangi nyekundu “ilikuwa rangi isiyofifia, rangi ya kudumu. Haingeweza kuondolewa na umande, wala mvua, wala kwa kufuliwa, wala kwa kutumiwa kwa muda mrefu.”
-
-
“Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 27
“Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”
1, 2. Wema wa Mungu ni mwingi kadiri gani, na Biblia inakaziaje sifa hiyo?
KATIKA nuru nyangavu ya machweo, marafiki kadhaa wanafurahia kula chakula pamoja bustanini, wanacheka na kuzungumza huku wakifurahia mandhari. Mbali sana, mkulima anatazama mashamba yake na kutabasamu kwa sababu mawingu meusi yametanda angani na mvua imeanza kunyesha. Kwingineko, mume na mke wanafurahi sana kumwona mtoto wao mchanga akiyumba-yumba anapojaribu kutembea.
2 Iwe wanajua au hawajui, watu hao wote wananufaika na jambo moja—wema wa Yehova Mungu. Wanadini wengi hurudia-rudia maneno haya, “Mungu ni mwema.” Biblia inakazia sifa hiyo hata zaidi. Inasema: “Wema wake, jinsi ulivyo mwingi!” (Zekaria 9:17) Lakini yaonekana kwamba ni watu wachache sana leo wanaojua maana ya maneno hayo. Wema wa Yehova Mungu unahusisha nini, na sifa hiyo inamnufaishaje kila mmoja wetu?
Sifa Muhimu ya Upendo wa Mungu
3, 4. Wema ni nini, na kwa nini inaweza kusemwa kwamba wema wa Yehova ni wonyesho wa upendo wake?
3 Katika lugha nyingi leo, neno “wema” halina maana maalumu. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba wema ni sifa ya pekee sana. Sifa hiyo inamaanisha hasa wema wa kiadili. Kwa hivyo, tunaweza kusema kwamba Yehova ni mwema kabisa. Sifa zake zote, kutia ndani nguvu zake, haki yake, na hekima yake ni njema kabisa. Ingawa hivyo, wema unaweza kutajwa kwa kufaa kuwa wonyesho wa upendo wa Yehova. Kwa nini?
4 Wema ni sifa inayoonyeshwa kwa matendo. Mtume Paulo alisema kwamba mtu mwema huwavutia wengine zaidi kuliko mtu mwadilifu. (Waroma 5:7) Mtu mwadilifu hutii matakwa ya sheria kwa uaminifu, lakini mtu mwema hufanya mengi zaidi. Anachukua hatua na kujitahidi sana kuwasaidia wengine. Kama tutakavyoona, hapana shaka kwamba Yehova ni mwema katika njia hiyo. Kwa wazi, upendo wa Yehova usio na mipaka ndio chanzo cha wema wake.
5-7. Kwa nini Yesu alikataa kuitwa “Mwalimu Mwema,” na hivyo alithibitisha ukweli gani hakika?
5 Yehova ni mwema kwa njia isiyo na kifani. Muda mfupi kabla ya Yesu kufa, mtu fulani alimfikia ili kumwuliza swali na akamwita “Mwalimu Mwema.” Yesu akamjibu: “Kwa nini waniita mwema? Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.” (Marko 10:17, 18) Huenda ukashangazwa na jibu hilo. Mbona Yesu alimkosoa mtu huyo? Je, Yesu hakuwa “Mwalimu Mwema”?
6 Ni wazi kwamba mtu huyo alikuwa akimrairai Yesu kwa kutumia maneno “Mwalimu Mwema” kama cheo. Kwa unyenyekevu, Yesu alielekeza utukufu huo kwa Baba yake wa mbinguni, ambaye ni mwema kwa njia isiyo na kifani. (Mithali 11:2) Lakini Yesu alikuwa akithibitisha pia ukweli huu hakika: Ni Yehova peke yake anayeamua yaliyo mema. Akiwa Mwenye Enzi Kuu, ni yeye peke yake aliye na haki ya kuamua mambo mema na mabaya. Adamu na Hawa walijaribu kujitwalia haki hiyo walipoasi na kula tunda la mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Lakini Yesu kwa unyenyekevu anamwachia Baba yake haki ya kuamua mema na mabaya.
7 Isitoshe, Yesu alijua kwamba Yehova ndiye chanzo cha vitu vyote vyema. Yeye ni Mtoaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Hebu tuone jinsi ambavyo ukarimu wa Yehova unathibitisha wema wake.
Mambo Yanayothibitisha Wema Mwingi wa Yehova
8. Yehova amewaonyeshaje wanadamu wote wema?
8 Kila mtu aliyepata kuishi amenufaishwa na wema wa Yehova. Zaburi 145:9 yasema: “BWANA ni mwema kwa watu wote.” (Italiki ni zetu.) Ni mifano ipi inayoonyesha kwamba wema wake unamnufaisha kila mtu? Biblia inasema hivi: “Hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.” (Matendo 14:17) Je, umewahi kufurahia chakula kitamu? Hakungekuwa na chakula chochote kama Yehova hangekuwa mwema na kubuni mzunguko wa maji safi na “majira yenye kuzaa matunda.” Yehova amewatendea watu wote wema, hata wale wasiompenda. Yesu alisema hivi: “Hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:45.
Yehova ‘anawapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda’
9. Tofaa linaonyeshaje wema wa Yehova?
9 Wengi hupuuza ukarimu mkubwa ambao wanadamu wanaonyeshwa kupitia jua, mvua, na majira ya matunda. Kwa mfano, fikiria tofaa, tunda linalokuzwa sana katika maeneo yenye halijoto ya wastani duniani. Ni tunda tamu sana linalovutia, lina madini muhimu na maji tosha yanayoburudisha. Je, wajua kwamba ulimwenguni pote kuna aina 7,500 hivi za matofaa yenye rangi mbalimbali kama vile nyekundu, rangi ya dhahabu, manjano, na rangi ya kijani-kibichi, na yana ukubwa mbalimbali, mengine ni makubwa kidogo kuliko cheri na mengine ni kama balungi? Tofaa lina mbegu ndogo. Lakini mojawapo ya miti maridadi zaidi hukua kutoka kwa mbegu hiyo ndogo. (Wimbo Ulio Bora 2:3, BHN) Kila mwaka mtofaa huchanua maua mengi yenye kuvutia na kuzaa matunda. Kila mwaka, kwa muda wa miaka 75 hivi, mtofaa wa wastani huzaa katoni 20 za matunda, kila katoni ikiwa na uzito wa kilogramu 19!
Mti unaoweza kulisha na kuwafurahisha watu kwa miaka mingi sana hukua kutoka kwa mbegu hii ndogo
10, 11. Hisi zetu zinathibitishaje wema wa Mungu?
10 Kwa wema wake usio na kikomo, Yehova ametupatia mwili ambao ‘umeumbwa kwa jinsi ya ajabu.’ Tuna hisi ambazo zinakusudiwa kutusaidia kutambua kazi zake na kuzifurahia. (Zaburi 139:14) Hebu fikiria tena mambo yaliyotajwa mwanzoni mwa sura hii. Tunafurahia kuona mambo gani? Uso mwangavu wa mtoto anayeangua kicheko. Mvua kubwa inaponyesha. Machweo ya rangi nyekundu, ya dhahabu, na ya urujuani. Jicho la mwanadamu linaweza kuona zaidi ya rangi 300,000! Na tunaweza kusikia na kutofautisha sauti mbalimbali zinazovutia, kama vile mvumo wa upepo katika miti, na kicheko kichangamfu cha mtoto mchanga. Ni nini kinachotuwezesha kufurahia mambo hayo? Biblia inasema: “Sikio lisikialo, na jicho lionalo, BWANA ndiye aliyeyafanya yote mawili.” (Mithali 20:12) Lakini hizo ni hisi mbili tu.
11 Hisi yetu ya kunusa huthibitisha pia wema wa Yehova. Pua ya mwanadamu inaweza kutofautisha harufu zipatazo 10,000. Baadhi ya harufu hizo ni: harufu nzuri ya chakula upendacho kinapopikwa, harufu nzuri ya maua, ya majani makavu, harufu ya moshi. Na hisi yako ya kugusa inakuwezesha kuhisi upepo unapovuma kwa wanana usoni mwako, kupata utulivu unapokumbatiwa na mpendwa wako, kuhisi tunda lenye ganda laini mkononi mwako. Unapoliuma, hisi yako ya kuonja inaanza kufanya kazi. Unafurahia ladha mbalimbali vionjio vyako vinapoonja kemikali tata za tunda hilo. Naam, tuna kila sababu ya kutangaza hivi kumhusu Yehova: “Jinsi gani ulivyo mwingi wema wako, uliowawekea wale wanaokucha!” (Zaburi 31:19, BHN) Lakini Yehova ‘amewawekeaje’ wema wale ambao wanamhofu?
Wema Unaoleta Faida za Milele
12. Ni maandalizi gani kutoka kwa Yehova yaliyo muhimu zaidi, na kwa nini?
12 Yesu alisema: “Imeandikwa, ‘Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.’” (Mathayo 4:4) Kwa kweli, maandalizi ya kiroho kutoka kwa Yehova yanaweza kutufaidi kuliko maandalizi ya kimwili, kwa kuwa yatatuwezesha kuishi milele. Katika Sura ya 8 ya kitabu hiki, tuliona kwamba katika siku hizi za mwisho, Yehova ametumia uwezo wake wa kurudisha hali mpya kuleta paradiso ya kiroho. Jambo muhimu zaidi ni kwamba paradiso hiyo ina chakula tele cha kiroho.
13, 14. (a) Nabii Ezekieli aliona nini katika ono, nalo linatuhusuje leo? (b) Yehova amewapa watumishi wake waaminifu maandalizi gani ya kiroho kwa ajili ya uhai?
13 Katika mojawapo ya unabii mbalimbali muhimu wa urudisho, nabii Ezekieli alipata ono la hekalu jipya lenye utukufu. Kijito kilichotiririka kutoka hekaluni humo, kilizidi kupanuka na kina chake kuongezeka hatua kwa hatua mpaka kikawa “mto.” Mto huo ulikuwa na matokeo mazuri popote ulipopitia. Miti mingi sana ambayo ilitokeza chakula na maponyo ilisitawi kwenye kingo za mto huo. Na mto huo hata ulileta uhai na ufanisi katika Bahari ya Chumvi isiyo na uhai! (Ezekieli 47:1-12) Lakini ono hilo lilimaanisha nini?
14 Ono hilo lilimaanisha kwamba Yehova angerudisha mpango wake wa ibada safi ambao unawakilishwa na hekalu aliloona Ezekieli. Maandalizi ya Mungu kwa ajili ya uhai yangewamiminikia watu wake kwa wingi zaidi kama ule mto ulio katika ono. Tangu kurudishwa kwa ibada safi mwaka wa 1919, Yehova amewabariki watu wake kwa kuwapa maandalizi ya uhai. Jinsi gani? Biblia, vichapo vya Biblia, mikutano, na makusanyiko yamewasaidia mamilioni ya watu kupata kweli muhimu sana. Kupitia njia hizo, Yehova amewafundisha watu kuhusu mpango muhimu zaidi kwa ajili ya uhai—dhabihu ya fidia ya Kristo. Dhabihu hiyo huwawezesha wote wanaompenda na kumhofu Yehova kikweli wawe na uhusiano mzuri naye na kuwa na tumaini la kuishi milele.a Kwa hiyo, watu wa Yehova wamekuwa wakifurahia karamu ya kiroho katika siku hizi za mwisho, huku ulimwengu ukiteseka kwa sababu ya njaa ya kiroho.—Isaya 65:13.
15. Wema wa Yehova utawanufaishaje wanadamu waaminifu wakati wa Utawala wa Kristo wa miaka elfu moja?
15 Lakini mto alioona Ezekieli hautakoma kutiririka huu mfumo wa kale wa mambo utakapoharibiwa. Kinyume chake, utaendelea kutiririka kwa wingi zaidi wakati wa Utawala wa Kristo wa miaka elfu moja. Wakati huo, kupitia Ufalme wa Kimesiya, Yehova atatumia manufaa kamili ya dhabihu ya Yesu ili wanadamu waaminifu wafikie ukamilifu hatua kwa hatua. Ndipo tutakaposhangilia sana kwa sababu ya wema wa Yehova!
Sifa Nyingine za Wema wa Yehova
16. Biblia inaonyeshaje kwamba wema wa Yehova unatia ndani sifa nyingine? Taja baadhi ya sifa hizo.
16 Wema wa Yehova watia ndani sifa nyingine mbali na ukarimu. Mungu alimwambia Musa hivi: “Nitapitisha wema wangu wote mbele yako, nami nitalitangaza jina la BWANA mbele yako.” Simulizi hilo lasema kwamba baadaye ‘BWANA alipita mbele yake, akatangaza, BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.’ (Kutoka 33:19; 34:6) Kwa hiyo, wema wa Yehova unatia ndani sifa kadhaa zenye kuvutia. Hebu tuchunguze sifa mbili tu kati ya sifa hizo.
17. Fadhili ni nini, na Yehova amewaonyeshaje fadhili wanadamu duni wasiokamilika?
17 “Mwenye fadhili.” Sifa hii inatuonyesha jinsi ambavyo Yehova anashughulika na viumbe wake. Badala ya kuwa mkali sana, na asiyejali, au kuwa katili kama watu wengi wenye mamlaka, Yehova ni mpole na mwenye fadhili. Kwa mfano, Yehova alimwambia hivi Abramu: “Tafadhali inua macho yako ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi.” (Mwanzo 13:14, NW) Tafsiri nyingi hazitaji neno “tafadhali.” Lakini wasomi wa Biblia wanasema kwamba maandishi ya awali ya Kiebrania yana kishirikishi cha neno ambacho kinabadili taarifa hiyo kuwa ombi la heshima badala ya amri. Kuna mifano mingine. (Mwanzo 31:12, NW; Ezekieli 8:5, NW) Hebu wazia, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu anasema “tafadhali” anapoongea na wanadamu duni. Katika ulimwengu ambamo watu wengi ni wakali, wachokozi na wasio na adabu, inatia moyo kutafakari fadhili ya Mungu wetu Yehova.
18. Yehova ni “mwingi wa . . . kweli” katika maana gani, na kwa nini maneno hayo yanatia moyo?
18 “Mwingi wa . . . kweli.” Kusema uwongo ni zoea la kawaida ulimwenguni leo. Lakini Biblia inatukumbusha hivi: “Mungu si mtu, aseme uongo.” (Hesabu 23:19) Isitoshe, andiko la Tito 1:2 linasema kwamba ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ Hawezi kusema uwongo kwa sababu yeye ni mwema sana. Kwa hivyo, ahadi za Yehova zinategemeka kabisa; maneno yake hayawezi kamwe kukosa kutimia. Yehova anaitwa pia “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Mbali na kutosema uwongo, anaeneza ukweli kwa wingi. Yeye hafanyi mambo kwa kujificha au kisirisiri, bali yeye huwafundisha watumishi wake waaminifu hekima yake isiyo na mipaka.b Hata anawafundisha jinsi ya kuishi kupatana na kweli hizo ili ‘waendelee kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 3) Kwa ujumla, kila mmoja wetu anapaswa kuitikiaje wema wa Yehova?
‘Ukimbilieni Wema wa Bwana’
19, 20. (a) Shetani alidhoofishaje tumaini la Hawa katika wema wa Yehova, na matokeo yalikuwa nini? (b) Wema wa Yehova unapaswa kutuchochea tufanye nini, na kwa nini?
19 Shetani alipomshawishi Hawa katika bustani ya Edeni, alianza kwa kudhoofisha kwa hila tumaini lake katika wema wa Yehova. Yehova alikuwa amemwambia Adamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula.” Yehova alimkataza kula matunda ya mti mmoja tu kati ya maelfu ya miti yenye kuvutia iliyokuwa bustanini. Hata hivyo, angalia swali ambalo Shetani alimwuliza Hawa: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?” (Mwanzo 2:9, 16; 3:1) Shetani alipotosha maneno ya Yehova ili amsadikishe Hawa kwamba Yehova alikuwa akimnyima kitu fulani kizuri. Kwa kusikitisha, Hawa alidanganyika. Hawa alianza kutilia shaka wema wa Mungu ambaye alikuwa amempa kila kitu alichokuwa nacho. Wanaume na wanawake wengi walioishi baadaye walifuata mfano wake.
20 Tunajua huzuni na taabu nyingi sana zilizosababishwa na shaka hiyo. Basi na tutii maneno ya Yeremia 31:12: “Wataukimbilia wema wa BWANA.” Bila shaka tunapaswa kuukimbilia wema wa Yehova kwa shangwe. Hatupaswi kamwe kutilia shaka makusudi ya Mungu wetu ambaye ni mwema sana. Tunaweza kumtumaini kabisa kwa sababu anataka wale wanaompenda wawe na maisha bora.
21, 22. (a) Ungependa kuonyesha katika njia zipi kwamba unathamini wema wa Yehova? (b) Tutazungumzia sifa gani katika sura inayofuata, na sifa hiyo inatofautianaje na wema?
21 Zaidi ya hayo, tunafurahi tunapopata nafasi ya kuwaambia wengine kuhusu wema wa Mungu. Zaburi 145:7 yasema hivi kuhusu watu wa Yehova: “Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu.” Kila siku tunafaidika kwa njia fulani na wema wa Yehova. Kwa nini usimshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya jambo hususa linaloonyesha wema wake? Kutafakari na kumshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya wema wake, na kuwaambia wengine kuhusu sifa hiyo kutatusaidia kumwiga Mungu wetu mwema. Tutamkaribia Yehova zaidi tukitafuta njia za kuiga wema wake. Mtume Yohana aliyezeeka aliandika hivi: “Mpendwa, uwe mwigaji, si wa lililo baya, bali wa lililo jema. Yeye ambaye atenda mema hutokana na Mungu.”—3 Yohana 11.
22 Wema wa Yehova unahusiana pia na sifa nyingine. Kwa mfano, Mungu ni “mwingi wa fadhili-upendo,” au upendo mshikamanifu. (Kutoka 34:6, NW) Tofauti na wema, Yehova hawaonyeshi watu wote sifa hiyo bali anawaonyesha hasa watumishi wake waaminifu. Katika sura inayofuata, tutajifunza jinsi anavyofanya hivyo.
a Fidia ndiyo uthibitisho bora zaidi wa wema wa Yehova. Ajapokuwa na mamilioni ya viumbe wa roho, Yehova alimchagua Mwanaye mpendwa aliye mzaliwa-pekee afe kwa ajili yetu.
b Kwa kufaa, Biblia inaonyesha kwamba kweli inahusiana na nuru. Mtunga-zaburi aliimba hivi: ‘Niletee nuru yako na kweli yako.’ (Zaburi 43:3) Yehova anawaangazia nuru nyingi ya kiroho wale walio na nia ya kufundishwa au kuelimishwa naye.—2 Wakorintho 4:6; 1 Yohana 1:5.
-
-
“Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 28
“Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”
1, 2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mfalme Daudi alijua matokeo mabaya ya kukosa uaminifu-mshikamanifu?
MFALME DAUDI alijua matokeo mabaya ya kukosa uaminifu-mshikamanifu. Pindi moja utawala wake wenye misukosuko ulikabili matatizo wakati watu wa taifa lake walipopanga njama ya kumwondoa mamlakani. Isitoshe, Daudi alisalitiwa na baadhi ya watu ambao tungetarajia wawe marafiki wake wa karibu. Fikiria Mikali, mke wa kwanza wa Daudi. Mwanzoni, “alimpenda Daudi” na hapana shaka kwamba alimuunga mkono katika madaraka yake ya kifalme. Hata hivyo, baadaye ‘alimdharau moyoni mwake,’ hata akamwona Daudi kama ‘mmojawapo wa watu baradhuli.’—1 Samweli 18:20; 2 Samweli 6:16, 20.
2 Mwingine alikuwa Ahithofeli, aliyekuwa mshauri wa Daudi. Shauri lake lilithaminiwa sana kana kwamba lilikuwa neno la Yehova mwenyewe. (2 Samweli 16:23) Lakini, mwishowe, mshauri huyo mwenye kutumainiwa alimsaliti Daudi na kujiunga na waasi. Ni nani aliyepanga njama hiyo? Absalomu, mwana wa Daudi! Mhaini huyo mwenye kujitafutia makuu ‘aliwadanganya watu wa Israeli,’ akajitawaza mwenyewe kuwa mfalme mpinzani. Uasi wa Absalomu ulipamba moto sana hivi kwamba Mfalme Daudi alilazimika kukimbia ili kujiokoa.—2 Samweli 15:1-6, 12-17.
3. Daudi alikuwa na uhakika gani?
3 Je, hakukuwa mtu yeyote aliyebaki mwaminifu-mshikamanifu kwa Daudi? Katika shida zake zote, Daudi alikuwa na uhakika kwamba kulikuwa na mmoja aliyekuwa mwaminifu-mshikamanifu kwake. Nani? Yehova Mungu mwenyewe. Daudi alisema hivi kumhusu: “Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu.” (2 Samweli 22:26, BHN) Uaminifu-mshikamanifu ni nini, na Yehova anaonyeshaje sifa hii kwa njia bora zaidi?
Uaminifu-Mshikamanifu Ni Nini?
4, 5. (a) “Uaminifu-mshikamanifu” ni nini? (b) Uaminifu-mshikamanifu unatofautianaje na uaminifu?
4 Kulingana na Maandiko ya Kiebrania, “uaminifu-mshikamanifu” ni fadhili ambayo inashikamana kabisa kwa upendo na kitu fulani hadi kusudi lake kuhusiana na kitu hicho linapotimia. Uaminifu-mshikamanifu unahusisha mambo mengi mbali na uaminifu. Mtu anaweza kuwa mwaminifu kwa sababu tu ya wajibu. Kinyume chake, uaminifu-mshikamanifu unategemea upendo. Isitoshe, neno “-aminifu” linaweza kutumiwa kuhusiana na vitu visivyo hai. Kwa mfano, mtunga-zaburi alisema kwamba mwezi ni “shahidi aliye mbinguni mwaminifu” kwa sababu unaangaza kwa ukawaida wakati wa usiku. (Zaburi 89:37) Lakini hatuwezi kusema kwamba mwezi ni mwaminifu-mshikamanifu. Kwa nini? Kwa sababu uaminifu-mshikamanifu unategemea upendo. Na vitu visivyo hai haviwezi kuonyesha sifa hiyo.
Mwezi unaitwa shahidi mwaminifu, lakini ni viumbe wenye akili tu wanaoweza kuiga uaminifu-mshikamanifu wa Yehova
5 Maandiko yanaonyesha kwamba uaminifu-mshikamanifu hudhihirisha upendo. Ni wazi kwamba kuna uhusiano fulani kati ya mtu anayeonyeshwa sifa hiyo na yule anayeionyesha. Uaminifu-mshikamanifu hauna kigeugeu. Si kama mawimbi ya bahari yanayopeperushwa huku na huku. Kinyume chake, sifa ya uaminifu-mshikamanifu, au upendo-mwaminifu inaweza kushinda hali ngumu sana.
6. (a) Uaminifu-mshikamanifu ni haba kadiri gani miongoni mwa wanadamu, na Biblia inathibitishaje jambo hilo? (b) Njia bora ya kujifunza kuhusu uaminifu-mshikamanifu ni ipi, na kwa nini?
6 Ni kweli kwamba uaminifu-mshikamanifu ni haba sana leo. Mara nyingi, marafiki wa karibu ‘huangamizana.’ Tunasikia visa vingi sana vya watu wanaowaacha wenzi wao wa ndoa. (Mithali 18:24; Malaki 2:14-16) Matendo ya hiana ni mengi sana hivi kwamba tunaweza kurudia maneno ya nabii Mika: “Mtu mwaminifu-mshikamanifu ametoweka duniani.” (Mika 7:2, NW) Mara nyingi wanadamu hushindwa kuonyesha uaminifu-mshikamanifu, lakini Yehova huonyesha sifa hiyo kwa njia ya pekee sana. Njia bora ya kujifunza kuhusu uaminifu-mshikamanifu ni kwa kuchunguza jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hii kuu ya upendo wake.
Uaminifu-Mshikamanifu wa Yehova Usio na Kifani
7, 8. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mwaminifu-mshikamanifu?
7 Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Wewe peke yako ni mwaminifu-mshikamanifu.” (Ufunuo 15:4) Kwa nini Biblia inasema hivyo, hali wanadamu na malaika wameonyesha uaminifu-mshikamanifu wa pekee pindi kwa pindi? (Ayubu 1:1; Ufunuo 4:8) Vipi Yesu Kristo? Yeye ndiye mtu “mwaminifu-mshikamanifu” zaidi mbele za Mungu. (Zaburi 16:10, NW) Basi, kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mwaminifu-mshikamanifu?
8 Kwanza, kumbuka kwamba uaminifu-mshikamanifu ni sifa ya upendo. Hakuna mtu awaye yote anayeweza kuwa mwaminifu-mshikamanifu kikamili zaidi kuliko Yehova, kwa sababu “Mungu ni upendo,” yaani, yeye ni wonyesho halisi wa upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa kweli, malaika na wanadamu wanaweza kuiga tu sifa za Mungu, lakini hawawezi kuwa na uaminifu-mshikamanifu wa hali ya juu sana kama yeye. Amekuwa akionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa muda mrefu kuliko kiumbe yeyote duniani au mbinguni, kwa sababu Yeye ni “mzee wa siku.” (Danieli 7:9) Kwa hiyo, Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa kadiri kubwa sana. Yehova anaonyesha sifa hiyo kwa njia isiyo na kifani. Fikiria mifano kadhaa.
9. Yehova ni “mwaminifu-mshikamanifu juu ya kazi zake zote” kwa njia gani?
9 Yehova ni “mwenye fadhili [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW] juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:17) Jinsi gani? Zaburi 136 inajibu swali hilo. Andiko hilo linataja matendo kadhaa ya Yehova ya kuokoa, kutia ndani alipowaokoa Waisraeli kwa njia ya kustaajabisha katika Bahari Nyekundu. Jambo la kutokeza ni kwamba kila mstari wa zaburi hiyo unakaziwa na usemi: “Kwa maana fadhili [au, uaminifu-mshikamanifu] zake ni za milele.” Zaburi hiyo imetajwa katika Maswali ya Kutafakari kwenye ukurasa wa 289. Unaposoma mistari hiyo, utavutiwa sana kuona jinsi Yehova alivyoonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watu wake kwa njia mbalimbali. Naam, Yehova huwa mwaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake waaminifu kwa kusikia vilio vyao vya kuomba msaada na kwa kuchukua hatua kwa wakati wake. (Zaburi 34:6) Yehova huendelea kuwaonyesha watumishi wake upendo-mshikamanifu maadamu wanaendelea kuwa waaminifu kwake.
10. Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kuhusiana na kanuni zake jinsi gani?
10 Zaidi ya hayo, Yehova huwaonyesha watumishi wake uaminifu-mshikamanifu kwa kushikilia kabisa kanuni zake. Yehova si kama wanadamu wasiotegemeka au wasio na msimamo ambao wanafuata tu hisia zao, maoni yake kuhusu mema na mabaya hayabadiliki. Miaka nenda miaka rudi, Yehova hajabadili kamwe maoni yake kuhusu uwasiliani-roho, ibada ya sanamu, na kuua. Alisema hivi kupitia nabii wake Isaya, “Mimi ni yuleyule hata katika uzee wenu.” (Isaya 46:4, BHN) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutafaidika tukifuata mwongozo wa kiadili unaoelezwa waziwazi katika Neno la Mungu.—Isaya 48:17-19.
11. Taja mifano inayoonyesha kwamba Yehova hutimiza ahadi zake kwa uaminifu-mshikamanifu.
11 Yehova huonyesha pia uaminifu-mshikamanifu kwa kutimiza ahadi zake. Kila jambo analotabiri linatimia. Yehova alisema hivi: “Neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isaya 55:11) Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watu wake kwa kutimiza ahadi zake. Yeye hawaahidi mambo ambayo hatatimiza. Yehova amethibitisha kabisa kwamba anatimiza ahadi zake hivi kwamba mtumishi wake Yoshua aliweza kusema: “Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo BWANA alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.” (Yoshua 21:45) Hivyo basi, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatatukatisha tamaa kwa kukosa kutimiza ahadi zake.—Isaya 49:23; Waroma 5:5.
12, 13. Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova “ni wa milele” katika maana gani?
12 Kama tulivyoona hapo awali, Biblia inatuambia kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova “ni wa milele.” (Zaburi 136:1, NW) Jinsi gani? Kwanza, Yehova husamehe kabisa dhambi. Kama Sura ya 26 ilivyoonyesha, Yehova hakumbuki na kumhukumu mtu kwa sababu ya dhambi ambazo tayari amesamehewa. Kila mmoja wetu anapaswa kushukuru kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ni wa milele kwa sababu ‘sote tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’—Waroma 3:23.
13 Lakini uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ni wa milele katika maana nyingine pia. Neno lake linasema kwamba mtu mwadilifu “atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:3) Hebu wazia mti mkubwa sana ambao majani yake hayanyauki! Vivyo hivyo, tukipendezwa kikweli na Neno la Mungu, tutaishi muda mrefu, tutakuwa na amani, na kufanikiwa. Yehova awaahidi watumishi wake waaminifu baraka za milele. Kwa kweli, katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ambao Yehova ataleta, wanadamu watiifu watafurahia uaminifu-mshikamanifu wake milele.—Ufunuo 21:3, 4.
Yehova ‘Hatawaacha Waaminifu Wake’
14. Yehova anaonyeshaje kwamba anathamini uaminifu wa watumishi wake?
14 Yehova ameonyesha uaminifu-mshikamanifu tena na tena. Kwa sababu Yehova hana kigeugeu kamwe, yeye huwaonyesha watumishi wake uaminifu-mshikamanifu wa kudumu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nilikuwa kijana na sasa ni mzee; kamwe sijaona mwadilifu ameachwa na Mungu, au: watoto wake wakiombaomba chakula. Maana Mwenyezi-Mungu hupenda uadilifu, wala hawaachi waaminifu wake.” (Zaburi 37:25, 28, BHN) Ni kweli kwamba Yehova anastahili ibada yetu kwa sababu yeye ni Muumba. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, Yehova anathamini sana uaminifu wetu kwa sababu yeye ni mwaminifu-mshikamanifu.—Malaki 3:16, 17.
15. Eleza jinsi Yehova alivyoonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Israeli.
15 Kwa uaminifu-mshikamanifu, sikuzote Yehova huwasaidia watu wake wanapokumbwa na matatizo. Mtunga-zaburi anatuambia hivi: “Huwalinda nafsi zao watauwa wake, na kuwaokoa na mkono wa wasio haki.” (Zaburi 97:10) Fikiria jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Baada ya kuokolewa kimuujiza katika Bahari Nyekundu, Waisraeli walitangaza hivi katika wimbo waliomwimbia Yehova: “Wewe kwa fadhili-upendo zako [au, “upendo-mshikamanifu,” kielezi-chini] umewaongoza watu uliowakomboa.” (Kutoka 15:13, NW) Hapana shaka kwamba Yehova alionyesha upendo-mshikamanifu alipowaokoa katika Bahari Nyekundu. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “BWANA hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; bali kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu BWANA akawatoa kwa mkono wa nguvu, akawakomboa katika nyumba ya utumwa, katika mkono wa Farao, mfalme wa Misri.”—Kumbukumbu la Torati 7:7, 8.
16, 17. (a) Waisraeli walikosa kabisa kuthamini nini, lakini Yehova aliwaonyeshaje rehema? (b) Waisraeli wengi walionyeshaje kwamba ‘hawangeweza kuponywa,’ na hilo linatupatia onyo gani?
16 Bila shaka, taifa la Israeli halikuthamini uaminifu-mshikamanifu wa Yehova. Baada ya kukombolewa, ‘walizidi kumtenda dhambi [Yehova], walipomwasi Aliye Juu.’ (Zaburi 78:17) Kadiri miaka ilivyopita, waliasi tena na tena, walimwacha Yehova na kugeukia miungu ya uwongo na mazoea ya kipagani ambayo yaliwatia unajisi. Hata hivyo, Yehova hakuvunja agano lake. Badala yake, Yehova aliwasihi hivi watu wake kupitia nabii Yeremia: “Rudi, Ee Israeli mwenye kuasi . . . Sitakutazama kwa hasira; maana mimi ni mwenye rehema [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW].” (Yeremia 3:12) Lakini, kama Sura ya 25 ilivyoonyesha, Waisraeli wengi walikataa kubadilika. Hata, “waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake.” Matokeo yalikuwa nini? Mwishowe, ‘ghadhabu ya BWANA ilizidi juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponywa.’—2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16.
17 Twajifunza nini kutokana na mambo hayo? Twajifunza kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova haudanganyiki wala si wa kijinga. Ni kweli kwamba Yehova ni ‘mwingi wa rehema’ naye hupenda kuonyesha rehema kunapokuwa na msingi wa kufanya hivyo. Lakini Yehova huchukua hatua gani mtu mwovu anapokuwa sugu? Inapokuwa hivyo, Yehova hushikamana na kanuni zake adilifu naye humhukumu mtu mwovu. Musa aliambiwa kwamba Yehova “si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.”—Kutoka 34:6, 7.
18, 19. (a) Yehova anaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaadhibu waovu? (b) Yehova ataonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa?
18 Mungu huonyesha pia uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaadhibu waovu. Vipi? Amri ambazo Yehova anawapa wale malaika saba katika kitabu cha Ufunuo zaonyesha jambo hilo: “Nendeni mkamwage mabakuli saba ya hasira ya Mungu ndani ya dunia.” Malaika wa tatu anapomwaga bakuli lake “ndani ya mito na mabubujiko ya maji,” yanakuwa damu. Kisha malaika huyo anamwambia Yehova hivi: “Wewe, Uliyeko na uliyekuwako, Mwaminifu-Mshikamanifu, ni mwadilifu, kwa sababu umetoa maamuzi haya, kwa sababu walimwaga damu ya watakatifu na ya manabii, nawe umewapa damu wanywe. Wao wastahili hilo.”—Ufunuo 16:1-6.
Yehova atawakumbuka na kuwafufua kwa uaminifu wale ambao wamedumu wakiwa waaminifu-washikamanifu hadi kifo
19 Ona kwamba malaika huyo anapotangaza ujumbe huo wa hukumu anasema kwamba Yehova ni “Mwaminifu-Mshikamanifu.” Kwa nini? Kwa sababu anapowaangamiza waovu, Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa. Kwa uaminifu-mshikamanifu, Yehova anawakumbuka vizuri watumishi hao. Anatamani kuwaona tena waaminifu hao waliokufa, na Biblia inaonyesha waziwazi kwamba anakusudia kuwathawabisha kwa kuwafufua. (Ayubu 14:14, 15) Yehova hawasahau watumishi wake waaminifu eti kwa sababu wamekufa. Badala yake, “kwake, wao wote wako hai.” (Luka 20:37, 38) Kusudi la Yehova la kuwafufua wale walio katika kumbukumbu lake linathibitisha kabisa kwamba yeye ni mwaminifu-mshikamanifu.
Wanazi walimuua Bernard Luimes (kushoto) na Wolfgang Kusserow (katikati)
Kikundi cha kisiasa kilimuua Moses Nyamussua kwa kumchoma mkuki
Upendo-Mshikamanifu wa Yehova Huandaa Njia ya Wokovu
20. “Vyombo vya rehema” ni nani? na Yehova anawaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu?
20 Katika historia yote, Yehova ameonyesha uaminifu-mshikamanifu wa pekee kwa wanadamu. Kwa maelfu ya miaka, Yehova ‘amevumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira ya kisasi vilivyofanywa kufaa kwa ajili ya uharibifu.’ Kwa nini? “Ili apate kujulisha utajiri wa utukufu wake juu ya vyombo vya rehema, alivyotayarisha kimbele kwa ajili ya utukufu.” (Waroma 9:22, 23) “Vyombo vya rehema” ni wale walio na mtazamo ufaao ambao wametiwa mafuta kwa roho takatifu ili wawe warithi pamoja na Kristo katika Ufalme wake. (Mathayo 19:28) Kwa kuandaa njia ya wokovu kwa ajili ya vyombo hivyo vya rehema, Yehova alionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Abrahamu, kwa sababu alikuwa amemwahidi hivi alipofanya agano naye: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.
Watumishi wote waaminifu wa Yehova wana tumaini hakika la wakati ujao kwa sababu yeye ni mwaminifu-mshikamanifu
21. (a) Yehova anaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kubwa”? (b) Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova unakuchochea kufanya nini?
21 Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu pia kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kubwa” na kuishi milele katika paradiso duniani. (Ufunuo 7:9, 10, 14) Kwa uaminifu-mshikamanifu, Yehova anawapa watumishi wake fursa ya kuishi milele katika paradiso duniani ingawa wao si wakamilifu. Jinsi gani? Anawapa fursa hiyo kupitia fidia—wonyesho mkuu zaidi wa uaminifu-mshikamanifu wa Yehova. (Yohana 3:16; Waroma 5:8) Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova unawavuta wale ambao wana njaa ya uadilifu mioyoni mwao. (Yeremia 31:3) Je, huhisi ukiwa karibu zaidi na Yehova kwa sababu ya uaminifu-mshikamanifu wa dhati ambao amekuonyesha na atakuonyesha? Kwa sababu tunatamani kumkaribia Mungu, na tuthamini upendo wake kwa kuimarisha azimio letu la kumtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu.
-
-
“Kuujua Upendo wa Kristo”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 29
“Kuujua Upendo wa Kristo”
1-3. (a) Ni nini kilichomchochea Yesu atake kumwiga Baba yake? (b) Tutachunguza sehemu zipi za upendo wa Yesu?
JE, UMEWAHI kumwona mvulana mdogo akijaribu kumwiga baba yake? Huenda akaiga jinsi baba yake anavyotembea, anavyoongea, au anavyotenda. Muda si muda, huenda mvulana huyo akaanza kufuata maadili na kanuni za kiroho za baba yake. Naam, mvulana huyo hujitahidi kuwa kama baba yake kwa sababu anampenda na kumthamini.
2 Vipi uhusiano wa Yesu na Baba yake wa mbinguni? Yesu alisema hivi pindi moja: “Nampenda Baba.” (Yohana 14:31) Hakuna mtu yeyote anayeweza kumpenda Yehova kama Mwana huyo, ambaye alikaa na Baba yake kwa muda mrefu sana kabla kiumbe yeyote hajaumbwa. Upendo ulimchochea Mwana huyo mwaminifu kutaka kumwiga Baba yake.—Yohana 14:9.
3 Katika sura zilizotangulia za kitabu hiki, tulizungumzia jinsi ambavyo Yesu aliiga kikamili nguvu, haki, na hekima ya Yehova. Lakini Yesu alionyeshaje upendo wa Baba yake? Hebu tuchunguze sehemu tatu za upendo wa Yesu—roho yake ya kujidhabihu, huruma yake nyororo, na utayari wake wa kusamehe.
“Hakuna Aliye na Upendo Mkubwa Zaidi Kuliko Huu”
4. Yesu alionyeshaje mfano bora kabisa wa upendo wa kujidhabihu akiwa binadamu?
4 Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa njia bora sana. Kujidhabihu ni kutanguliza mahitaji na masilahi ya wengine bila ubinafsi. Yesu alionyeshaje upendo huo? Yeye mwenyewe alieleza hivi: “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:13) Yesu alitoa uhai wake mkamilifu kwa hiari kwa ajili yetu. Huo ulikuwa wonyesho mkuu zaidi wa upendo kuwahi kuonyeshwa na mwanadamu yeyote. Lakini Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa njia nyinginezo pia.
5. Kwa nini lile tendo la Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu kuondoka mbinguni lilikuwa kujidhabihu kwa upendo?
5 Kabla ya kuwa mwanadamu, Mwana huyo mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa na cheo cha juu na cha pekee huko mbinguni. Alishirikiana kwa ukaribu sana na Yehova na viumbe wengi wa roho. Licha ya mapendeleo hayo, Mwana huyo mpendwa “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu na kuchukua umbo la mtumwa na kuja kuwa katika ufanani wa wanadamu.” (Wafilipi 2:7) Kwa hiari, alikuja kuishi na wanadamu wenye dhambi katika ulimwengu ambao “unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Bila shaka Mwana wa Mungu alijidhabihu kwa upendo, sivyo?
6, 7. (a) Yesu alijidhabihu kwa upendo katika njia zipi wakati wa huduma yake duniani? (b) Andiko la Yohana 19:25-27 lasimulia jambo gani lenye kugusa moyo kuhusu upendo wa kujidhabihu?
6 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alijidhabihu kwa upendo katika njia mbalimbali. Hakuwa na ubinafsi wowote. Alijishughulisha mno na huduma yake hivi kwamba alijinyima mambo ya kawaida ambayo wanadamu wamezoea. “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Yesu alikuwa seremala stadi sana, kwa hiyo angeweza kujijengea nyumba nzuri sana au angeweza kupata pesa kwa kutengeneza na kuuza fanicha maridadi sana. Lakini hakutumia ustadi wake kupata vitu vya kimwili.
7 Andiko la Yohana 19:25-27 lasimulia jambo lenye kugusa moyo sana kuhusu upendo wa Yesu wa kujidhabihu. Fikiria mambo mengi ambayo yalikuwa katika akili na moyo wa Yesu alasiri ambayo angeuawa. Alipokuwa akiteseka kwenye mti wa mateso, aliwafikiria wanafunzi wake, kazi ya kuhubiri, na hasa uaminifu wake na sifa ambayo angeletea jina la Baba yake. Kwa kweli, wakati ujao wa wanadamu wote ulimtegemea! Hata hivyo, muda mfupi tu kabla ya kufa, Yesu alimhangaikia pia mama yake, Maria, ambaye yaelekea alikuwa mjane wakati huo. Yesu alimwomba mtume Yohana amtunze Maria kama mama yake. Kisha mtume Yohana alimchukua Maria na kwenda naye nyumbani. Kwa njia hiyo, Yesu alifanya mipango ili mama yake atunzwe kimwili na kiroho. Alionyesha upendo ulioje usio na ubinafsi!
‘Alisukumwa na Sikitiko’
8. Neno la Kigiriki ambalo linatumiwa na Biblia kufafanua huruma ya Yesu linamaanisha nini?
8 Yesu alikuwa na huruma kama Baba yake. Maandiko yanaonyesha jinsi ambavyo Yesu alijitahidi kuwasaidia watu waliotaabika kwa sababu aliwahurumia sana. Biblia inafafanua huruma ya Yesu kwa kutumia neno la Kigiriki linalotafsiriwa “sukumwa na sikitiko.” Msomi mmoja anasema hivi: ‘Neno hilo linafafanua hisia ya ndani sana ambayo inamchochea mtu kutoka moyoni. Hakuna neno jingine la Kigiriki linalofafanua hisia ya huruma kwa mkazo sana kama neno hilo.’ Ebu ona pindi fulani-fulani ambapo huruma ilimchochea Yesu kutenda.
9, 10. (a) Ni kwa nini Yesu na mitume wake walitafuta mahali pa faragha? (b) Yesu alihisije umati ulipovuruga faragha yake, na kwa nini?
9 Alichochewa kuwasaidia watu kiroho. Simulizi la Marko 6:30-34 laonyesha sababu iliyomfanya Yesu awasikitikie watu. Wazia hali ilivyokuwa. Mitume walifurahi sana baada ya kuhubiri kotekote. Walirudi kwa Yesu na kumsimulia kwa shauku mambo yote waliyoona na kusikia. Lakini umati mkubwa ukakusanyika, na Yesu na mitume wake wakakosa hata nafasi ya kula. Daima akiwa makini, Yesu akafahamu kwamba mitume wamechoka. Akawaambia: “Njoni, nyinyi wenyewe, kwa faragha mwingie katika mahali pa upweke mpumzike kidogo.” Walipanda mashua na kuvuka upande wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya hadi mahali pa faragha. Lakini umati uliwaona wakienda. Wengine walipata habari hizo pia. Watu hao wote walikimbia kuzunguka ufuko wa kaskazini wa bahari hiyo na kufika ng’ambo nyingine kabla ya ile mashua!
10 Je, Yesu alikasirika kwa sababu watu walivuruga faragha yake? La hasha! Alisikitika sana alipoona umati huo wa maelfu ya watu ukimsubiri. Marko aliandika hivi: “Akaona umati mkubwa, lakini akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” Yesu alitambua kwamba watu hao walikuwa na mahitaji ya kiroho. Walikuwa kama kondoo wanaozurura huku na huku bila mchungaji wa kuwaongoza au kuwalinda. Yesu alijua kwamba watu wa kawaida walipuuzwa na viongozi wa kidini ambao badala ya kuwa wachungaji wenye kujali, waliwatendea bila huruma. (Yohana 7:47-49) Aliwasikitikia sana watu, akaanza kuwafundisha “juu ya ufalme wa Mungu.” (Luka 9:11) Ona kwamba Yesu aliwasikitikia watu hata bila kujua jinsi ambavyo wangeitikia mafundisho yake. Yaani, Yesu hakuwahurumia watu kwa sababu tu walikubali mafundisho yake bali aliwafundisha kwa sababu alichochewa na huruma yake nyororo.
“Akanyoosha mkono wake akamgusa”
11, 12. (a) Wenye ukoma walitendewaje nyakati za Biblia, lakini Yesu alitendaje alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma”? (b) Huenda mtu mwenye ukoma aliyeguswa na Yesu alihisije, na kisa halisi cha daktari mmoja kinathibitishaje jambo hilo?
11 Alichochewa kukomesha mateso. Watu wenye magonjwa mbalimbali walivutiwa na Yesu kwa sababu walijua yeye ni mwenye huruma. Jambo hilo lilionekana wazi wakati Yesu huku akifuatwa na umati alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma.” (Luka 5:11, 12) Katika nyakati za Biblia, wenye ukoma walitengwa ili wasiwaambukize wengine. (Hesabu 5:1-4) Lakini baada ya muda, marabi wasio na huruma walikuwa na maoni mabaya kuhusu ukoma, hivyo wakatunga sheria zao wenyewe zenye kukandamiza.a Ingawa hivyo, hebu ona jinsi Yesu alivyomtendea yule mtu mwenye ukoma: “Huko pia mwenye ukoma akaja kwake, akimsihi sana hata kwa kukunja magoti, akimwambia: ‘Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.’ Ndipo akasukumwa na sikitiko, naye akanyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Mimi nataka. Fanywa safi.’ Na mara hiyo ule ukoma ukamtoka.” (Marko 1:40-42) Yesu alijua kwamba mtu huyo mwenye ukoma hakupaswa kuwa miongoni mwa watu. Hata hivyo, badala ya kumfukuza, Yesu alimsikitikia sana hivi kwamba alifanya jambo la kushangaza. Yesu alimgusa!
12 Wafikiri mtu huyo alihisije alipoguswa na Yesu? Kwa mfano, hebu fikiria kisa hiki halisi. Dakt. Paul Brand, mtaalamu wa ukoma, asimulia kuhusu mtu mmoja mwenye ukoma ambaye alimtibu nchini India. Alipokuwa akimpima, daktari huyo alimshika begani na kumweleza kupitia mkalimani matibabu ambayo angepewa. Mtu huyo alianza kulia ghafula. Daktari akamwuliza, “Nimesema jambo baya?” Mkalimani akamwuliza kijana huyo swali hilo katika lugha yake kisha akajibu: “La, daktari. Anasema analia kwa sababu umemshika begani. Hajapata kamwe kuguswa na yeyote kwa miaka mingi isipokuwa wewe.” Yule mtu mwenye ukoma aliyemfikia Yesu alifaidika hata zaidi alipoguswa naye. Baada ya kuguswa mara moja tu, ugonjwa uliomfanya atengwe na watu ulitoweka kabisa!
13, 14. (a) Yesu alikutana na msafara gani alipokaribia jiji la Naini, na kwa nini kisa hicho kilihuzunisha sana? (b) Yesu alichochewaje na huruma kumsaidia yule mjane wa Naini?
13 Alichochewa kuondoa huzuni. Yesu alisikitishwa sana na huzuni ya wengine. Kwa mfano, fikiria simulizi la Luka 7:11-15. Jambo hilo lilitukia alipokuwa anakaribia kumaliza nusu ya huduma yake duniani. Yesu alikuwa amekaribia jiji la Naini huko Galilaya alipokutana na msafara wa mazishi karibu na lango la jiji hilo. Kilikuwa kisa chenye kuhuzunisha sana. Mwana pekee wa mjane mmoja alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba mjane huyo aliwahi kuwa katika msafara mwingine kama huo wakati wa mazishi ya mume wake. Sasa mwanaye ambaye huenda ndiye tu aliyemruzuku alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba miongoni mwa umati ulioandamana naye mlikuwa na waombolezaji walioimba nyimbo za maombolezo na wanamuziki waliocheza miziki ya maombolezo. (Yeremia 9:17, 18; Mathayo 9:23) Hata hivyo, Yesu alimtazama sana mama huyo aliyekuwa na majonzi tele, ambaye yaelekea alifuata kwa ukaribu jeneza lililobeba maiti ya mwanaye.
14 Yesu ‘alimsikitikia’ mama huyo. Kwa sauti yenye kutia moyo, akamwambia hivi: “Koma kutoa machozi.” Akalikaribia jeneza na kuligusa. Wale waliokuwa wamelibeba—na labda umati wote—wakasimama tuli. Kwa sauti yenye nguvu, Yesu akamwambia hivi yule maiti: “Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!” Halafu ikawaje? “Huyo mfu akaketi na kuanza kusema” kana kwamba ameamshwa kutoka kwa usingizi mzito! Maneno yanayofuata yanagusa moyo sana: “Naye [Yesu] akampa huyo kwa mama yake.”
15. (a) Masimulizi ya Biblia yanayoeleza jinsi Yesu alivyowasikitikia watu, yanaonyesha kuna uhusiano gani kati ya huruma na matendo? (b) Tunawezaje kumwiga Yesu?
15 Twajifunza nini kutokana na visa hivyo? Katika kila kisa, angalia uhusiano uliopo kati ya huruma na matendo. Sikuzote Yesu aliwahurumia watu waliokuwa wakitaabika, na huruma hiyo ilimchochea kutenda. Tunawezaje kuiga mfano wake? Tukiwa Wakristo, tuna wajibu wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Upendo wetu kwa Mungu ndio hasa unaotuchochea. Na tukumbuke kwamba kazi ya kuhubiri ni njia ya kuwaonyesha watu huruma. Tukiwahurumia watu kama alivyofanya Yesu, moyo wetu utatuchochea kujitahidi tuwezavyo kuwahubiria habari njema. (Mathayo 22:37-39) Tutawaonyeshaje huruma waamini wenzetu ambao wanateseka au wamefiwa? Hatuwezi kukomesha mateso yao kimuujiza au kufufua wafu. Lakini, tunaweza kuwahurumia kwa matendo kwa kuwaonyesha kwamba tunawajali au kwa kuwapa msaada wanaohitaji.—Waefeso 4:32.
“Baba, Wasamehe”
16. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa tayari kusamehe hata alipokuwa kwenye mti wa mateso?
16 Yesu aliiga kikamili upendo wa Baba yake katika njia nyingine muhimu—alikuwa “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Jambo hilo lilionekana wazi hata alipokuwa kwenye mti wa mateso. Yesu alisema nini alipokuwa amepigiliwa misumari mikononi na miguuni, kabla ya kufa kifo cha aibu? Je, alimlilia Yehova awaadhibu wale wanaomwua? La hasha! Kati ya maneno ya mwisho ambayo Yesu alisema ni: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui wanalofanya.”—Luka 23:34.b
17-19. Yesu alionyeshaje kwamba alimsamehe mtume Petro ambaye alikuwa amemkana mara tatu?
17 Labda kisa cha mtume Petro kinaonyesha kwa njia yenye kugusa moyo hata zaidi jinsi Yesu alivyokuwa mwenye kusamehe. Hapana shaka kwamba Petro alimpenda mno Yesu. Mnamo Nisani 14, usiku wa mwisho kabla ya Yesu kuuawa, Petro alimwambia hivi: “Bwana, mimi niko tayari kwenda pamoja nawe kuingia gerezani na pia kuingia katika kifo.” Hata hivyo, saa chache tu baadaye, Petro alikana mara tatu kwamba hata hamjui Yesu! Biblia inatueleza jambo lililotukia Petro alipokuwa akimkana mara ya tatu: “Bwana akageuka akamtazama Petro.” Petro alilemewa na majuto kwa sababu ya dhambi yake, hata ‘akaenda nje na kutoa machozi kwa uchungu.’ Yesu alipokufa baadaye siku hiyo, labda mtume huyo alijiuliza hivi: ‘Je, Bwana wangu alinisamehe?’—Luka 22:33, 61, 62.
18 Punde si punde, Petro alipata jibu. Yesu alifufuliwa asubuhi ya Nisani 16, na yaelekea kwamba alimtembelea Petro siku hiyohiyo. (Luka 24:34; 1 Wakorintho 15:4-8) Kwa nini Yesu alimzingatia mtume huyo ambaye alikuwa amemkana kabisa? Huenda Yesu alitaka kumhakikishia Petro aliyetubu kwamba angali anampenda na kumthamini. Lakini Yesu alimhakikishia jambo hilo kwa njia nyingine pia.
19 Pindi fulani baadaye, Yesu aliwatokea wanafunzi katika Bahari ya Galilaya. Wakati huo, Yesu alimwuliza mara tatu Petro (ambaye alikuwa amemkana Bwana wake mara tatu) iwapo anampenda. Baada ya swali la tatu, Petro alijibu: “Bwana, wewe wajua mambo yote; wewe wajua kwamba mimi nina shauku na wewe.” Bila shaka, Yesu, ambaye angeweza kusoma mioyo, alijua vizuri kwamba Petro alimpenda mno. Hata hivyo, Yesu akampa Petro nafasi ya kuthibitisha kwamba anampenda. Isitoshe, Yesu alimwambia Petro ‘alishe’ na ‘kuchunga kondoo Wake wadogo.’ (Yohana 21:15-17) Hapo awali, Petro alikuwa amepewa kazi ya kuhubiri. (Luka 5:10) Lakini sasa, Yesu alionyesha kwamba alimtumaini kabisa kwa kumpa daraka jingine zito—la kutunza wale ambao wangekuwa wafuasi wa Kristo. Muda mfupi baadaye, Yesu alimpa Petro pendeleo la pekee kuhusiana na utendaji wa wanafunzi. (Matendo 2:1-41) Haikosi Petro alifurahi sana alipojua kwamba Yesu alimsamehe na bado anamtumaini.
Je, ‘Wajua Upendo wa Kristo’?
20, 21. Tunawezaje ‘kuujua kikweli upendo wa Kristo’?
20 Neno la Yehova linaeleza kinaganaga juu ya upendo wa Kristo. Lakini tunapaswa kuuonaje upendo wa Yesu? Biblia inatuhimiza ‘tuujue upendo wa Kristo uzidio ujuzi.’ (Waefeso 3:19) Kama tulivyoona, masimulizi ya Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu yanatufundisha mengi kuhusu upendo wa Kristo. Hata hivyo, ili ‘kuujua kikweli upendo wa Kristo’ haitoshi tu kujifunza mambo ambayo Biblia inasema kumhusu.
21 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kujua’ linamaanisha “kujua kupitia matendo, kupitia uzoefu.” Tunaweza kufahamu zaidi hisia za Yesu tunapoiga upendo wake kwa kuwatumikia wengine bila ubinafsi, kuwahurumia na kuwasaidia, na kuwasamehe kutoka moyoni. Hivyo, kupitia uzoefu tunapata “kuujua upendo wa Kristo uzidio ujuzi.” Tusisahau kamwe kwamba kadiri tunavyomwiga Kristo, ndivyo tunavyomkaribia Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, ambaye Yesu alimwiga kikamili.
a Sheria za marabi zilisema kwamba hakuna yeyote aliyeruhusiwa kusimama umbali wa futi 6 hivi kutoka kwa mwenye ukoma. Lakini kukiwa na upepo, mwenye ukoma alisimama umbali wa futi 150 hivi. Kichapo Midrash Rabbah chataja rabi mmoja ambaye alijificha alipoona wenye ukoma, na rabi mwingine ambaye aliwatupia mawe wenye ukoma ili wasimkaribie. Kwa hiyo wenye ukoma walijua uchungu wa kukataliwa, kudharauliwa na kuchukiwa.
b Hati fulani za kale hazina sehemu ya kwanza ya Luka 23:34. Hata hivyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na tafsiri nyingine nyingi zina maneno hayo kwa sababu yanapatikana kwenye hati nyingi mashuhuri. Ni wazi kwamba Yesu alikuwa akizungumza kuhusu askari Waroma ambao walimtundika mtini. Hawakujua walilokuwa wanafanya, kwa sababu hawakujua Yesu ni nani. Bila shaka, viongozi wa kidini ambao walichochea mauaji hayo walikuwa na hatia kubwa zaidi, kwa sababu walifanya hivyo kimakusudi na kwa nia mbaya. Wengi wao hawangeweza kusamehewa.—Yohana 11:45-53.
-
-
“Endeleeni Kutembea Katika Upendo”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 30
“Endeleeni Kutembea Katika Upendo”
1-3. Tunapata nini tunapomwiga Yehova katika kuonyesha upendo?
‘KUNA furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’ (Matendo 20:35) Maneno hayo ya Yesu yanakazia ukweli huu ulio muhimu sana: Upendo usio na ubinafsi unathawabisha. Ingawa kuna furaha nyingi kuonyeshwa upendo, kuna furaha nyingi hata zaidi kuwaonyesha wengine upendo.
2 Hakuna anayeelewa jambo hilo vizuri kama Baba yetu wa mbinguni. Kama tulivyoona katika sura zilizotangulia za sehemu hii, Yehova hana kifani katika kuonyesha upendo. Yehova ameonyesha upendo kwa njia za pekee sana na kwa muda mrefu kuliko mtu yeyote. Ndiyo sababu Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11.
3 Mungu wetu mwenye upendo anataka tujitahidi kumwiga, hasa katika kuonyesha upendo. Andiko la Waefeso 5:1, 2 latuambia hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.” Tunapomwiga Yehova katika kuonyesha upendo, tunapata furaha zaidi ya kutoa. Tunaridhika pia kujua kwamba tunampendeza Yehova, kwa sababu Neno lake linatuhimiza ‘tupendane.’ (Waroma 13:8) Lakini kuna sababu nyingine za kutufanya ‘tuendelee kutembea katika njia ya upendo.’
Kwa Nini Upendo Ni Muhimu?
4, 5. Kwa nini ni muhimu tuwaonyeshe waamini wenzetu upendo wa kujidhabihu?
4 Kwa nini ni muhimu tuwapende waamini wenzetu? Kwa ufupi, upendo ndio msingi wa Ukristo wa kweli. Hatuwezi kuwa na uhusiano mzuri na Wakristo wenzetu iwapo hatuwapendi, na jambo baya hata zaidi ni kwamba bila upendo tunakuwa bure machoni pa Yehova. Fikiria jinsi ambavyo Neno la Mungu linakazia ukweli huo.
5 Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake usiku wa mwisho wa maisha yake duniani: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane. Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Usemi “kama vile nimewapenda nyinyi” unatuamuru tuwe na upendo kama wa Yesu. Katika Sura ya 29, tuliona kwamba Yesu alikuwa mfano bora katika kuonyesha upendo wa kujidhabihu, akitanguliza masilahi ya wengine. Ni lazima pia tupendane bila ubinafsi. Wale ambao si washiriki wa kutaniko la Kikristo wanahitaji kuona kwamba tunapendana kikweli. Kwa kweli, upendo wa kidugu wa kujidhabihu unatutambulisha kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo.
6, 7. (a) Twajuaje kwamba Neno la Yehova linakazia sana umuhimu wa kuonyesha upendo? (b) Maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 13:4-8 yanakazia nini kuhusu upendo?
6 Vipi ikiwa hatuna upendo? Mtume Paulo alisema kwamba ikiwa “sina upendo, nimekuwa kipande cha shaba-nyeupe inayovuma au toazi lenye kulia.” (1 Wakorintho 13:1) Toazi hulia kwa sauti kali sana. Kipande cha shaba-nyeupe huvumaje? Tafsiri nyingine zinasema “sauti ya kengele yenye kelele” au “kengele inayolia-lia.” Mifano hiyo inafaa sana. Mtu asiye na upendo ni kama ala ya muziki inayolia kwa sauti kubwa yenye kuchukiza inayofukuza watu badala ya kuwavutia. Je, mtu kama huyo anaweza kweli kuwa na uhusiano mzuri na wengine? Paulo alisema hivi pia: “Ikiwa nina imani yote ili kung’oa na kuhamisha milima, lakini sina upendo, mimi si kitu.” (1 Wakorintho 13:2) Hebu wazia, mtu asiye na upendo “ni bure kabisa,” hata akifanya nini! (The Amplified Bible) Je, hilo halionyeshi kwamba Neno la Yehova linakazia sana umuhimu wa kuonyesha upendo?
7 Lakini tutaonyeshaje sifa hiyo tunaposhughulika na wengine? Tujibu swali hilo kwa kuchanganua maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 13:4-8. Mistari hii haikazii jinsi Mungu anavyotupenda au jinsi tunavyompenda Mungu. Badala yake, Paulo alikazia jinsi sisi tunavyoweza kupendana. Alieleza mambo fulani kuhusu jinsi upendo ulivyo na jinsi usivyo.
Jinsi Upendo Ulivyo
8. Ustahimilivu unawezaje kutusaidia tunaposhughulika na wengine?
8 “Upendo ni wenye ustahimilivu.” Kustahimili ni kuwavumilia wengine kwa subira. (Wakolosai 3:13) Tunahitaji kuwa na subira, sivyo? Kwa sababu ya kufanya kazi bega kwa bega katika hali yetu ya kutokamilika, ni kawaida kwamba mara kwa mara huenda tukakosewa au tukawakosea ndugu zetu Wakristo. Lakini subira na ustahimilivu unaweza kutusaidia kuvumilia na kutovuruga amani ya kutaniko tunapokosana au kuhitilafiana na wengine kwa sababu ya mambo madogo-madogo.
9. Tunawezaje kuwaonyesha wengine fadhili?
9 ‘Upendo ni wenye fadhili.’ Fadhili huonyeshwa kwa kuwasaidia wengine na kuzungumza nao kwa njia yenye kujali. Upendo hutuchochea kutafuta fursa za kuwaonyesha wengine fadhili, hasa wale wanaohitaji sana msaada. Kwa mfano, huenda mwamini mwenzetu ambaye ni mzee kwa umri ni mpweke na anahitaji kutembelewa na kutiwa moyo. Huenda mama asiye na mume au dada anayeishi katika familia ambayo imegawanyika kidini anahitaji msaada fulani. Huenda mgonjwa fulani au mtu aliyepata msiba anahitaji kutiwa moyo kwa fadhili na rafiki mwaminifu. (Mithali 12:25; 17:17) Tunapochukua hatua ya kuonyesha fadhili kwa njia kama hizo, tunathibitisha kwamba upendo wetu ni halisi.—2 Wakorintho 8:8.
10. Upendo unatusaidiaje kutetea na kusema kweli, hata wakati ambapo si rahisi kufanya hivyo?
10 ‘Upendo hushangilia pamoja na kweli.’ Tafsiri nyingine inasema: “Upendo . . . huunga mkono ukweli kwa shangwe.” Upendo unatuchochea kutetea kweli na ‘kusema kweli na jirani yetu.’ (Zekaria 8:16) Kwa mfano, ikiwa mtu tunayempenda amefanya dhambi nzito, upendo kwa Yehova na kwa yule aliyefanya dhambi, utatusaidia tushikamane na kanuni za Mungu badala ya kujaribu kuficha, kutoa udhuru au hata kusema uwongo kuhusu dhambi yake. Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kukubali amefanya dhambi. Lakini ikiwa tunamjali kikweli mpendwa wetu, tungetaka akubali na kunufaika na nidhamu ya upendo kutoka kwa Mungu. (Mithali 3:11, 12) Tukiwa Wakristo wenye upendo, tunataka pia “kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.
11. Kwa sababu upendo “huhimili mambo yote,” tunapaswa kujitahidi kufanya nini kuhusu kasoro za waamini wenzetu?
11 ‘Upendo huhimili mambo yote.’ Usemi huo unamaanisha kihalisi kwamba upendo “unafunika mambo yote.” (Kingdom Interlinear) Andiko la 1 Petro 4:8 lasema: “Upendo hufunika wingi wa dhambi.” Naam, Mkristo ambaye anaongozwa na upendo hakimbilii kutangaza kasoro na mapungufu ya ndugu zake Wakristo. Mara nyingi, makosa na kasoro za waamini wenzetu huwa ndogo-ndogo mno na zinaweza kufunikwa na upendo.—Mithali 10:12; 17:9.
Upendo hutuchochea tuwaamini ndugu zetu
12. Mtume Paulo alionyeshaje aliamini kwamba Filemoni angetenda ifaavyo, na mfano wa Paulo unatufunza nini?
12 ‘Upendo huamini mambo yote.’ Tafsiri ya Moffat inasema kwamba upendo “sikuzote hujitahidi kuamini mambo mazuri.” Hatuwashuku isivyofaa waamini wenzetu na kutilia shaka kila jambo wanalofanya. Upendo unatusaidia “kuamini mambo mazuri” kuhusu ndugu zetu na kuwatumaini.a Fikiria mfano unaotajwa katika barua ya Paulo kwa Filemoni. Paulo alimwandikia Filemoni ili kumtia moyo amkaribishe kwa fadhili Onesimo yule mtumwa mtoro, ambaye sasa alikuwa Mkristo. Paulo alimsihi Filemoni kwa upendo badala ya kujaribu kumlazimisha. Aliamini kwamba Filemoni angetenda ifaavyo, kwa kusema: “Nikiitibari ukubalifu wako wa kufuata agizo, ninakuandikia wewe, nikijua utafanya hata zaidi ya mambo nisemayo.” (Mstari wa 21) Upendo unapotuchochea kuwaamini ndugu zetu, tunawatia moyo kufanya yote wawezayo.
13. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawatakia ndugu zetu mema?
13 ‘Upendo hutumaini mambo yote.’ Mbali na kuamini, upendo hutumaini mambo yote. Kwa upendo, tunawatakia mema ndugu zetu. Kwa mfano, ndugu ‘akichukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua,’ tunatumaini kwamba atakubali jitihada za upendo za kumrekebisha. (Wagalatia 6:1) Tunatumaini pia kwamba wale walio dhaifu katika imani watapata nguvu tena. Kwa subira, tunawasaidia tuwezavyo wawe na imani yenye nguvu. (Waroma 15:1; 1 Wathesalonike 5:14) Hata mpendwa wetu akiacha njia ya kweli, bado tunatumaini kwamba siku moja atarudiwa na fahamu na kumrudia Yehova, kama yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu.—Luka 15:17, 18.
14. Uvumilivu wetu unaweza kujaribiwa jinsi gani kutanikoni, na upendo utatusaidia tutendeje?
14 ‘Upendo huvumilia mambo yote.’ Uvumilivu hutuwezesha kubaki imara tunapokabili magumu au mambo yanayovunja moyo. Majaribu ya uvumilivu hayatokani tu na mambo yaliyo nje ya kutaniko. Nyakati nyingine, uvumilivu wetu unajaribiwa kutanikoni. Ndugu zetu wanaweza kutuvunja moyo nyakati nyingine kwa sababu ya kutokamilika. Tunaweza kuumizwa na mtu anayenena bila kufikiri. (Mithali 12:18) Labda jambo fulani kutanikoni halishughulikiwi jinsi tunavyotarajia. Ndugu fulani anayeheshimiwa anaweza kutuudhi, na kutufanya tujiulize, ‘Mkristo anawezaje kufanya hivyo?’ Tunapokabili hali kama hizo, je, tutajitenga na kutaniko na kuacha kumtumikia Yehova? Hatuwezi kufanya hivyo ikiwa tuna upendo! Naam, tukiwa na upendo hatuwezi kukazia tu kasoro za ndugu yetu na kukosa kuona sifa yoyote nzuri aliyo nayo au kukosa kuona uzuri wowote wa kutaniko. Upendo unatusaidia kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu na kuunga mkono kutaniko bila kujali mwanadamu mwingine asiyekamilika anasemaje au anatendaje.—Zaburi 119:165.
Jinsi Upendo Usivyo
15. Wivu usiofaa ni nini, na upendo unatusaidiaje kuepuka hisia hii hatari?
15 “Upendo hauna wivu.” Wivu usiofaa unaweza kutufanya tuwaonee wengine kijicho kwa sababu ya vitu walivyo navyo—mali zao, mapendeleo yao, au vipawa vyao. Wivu huo ni hisia hatari sana ya ubinafsi ambayo inaweza kuvuruga amani ya kutaniko isipodhibitiwa. Ni nini kitakachotusaidia tukinze “mwelekeo wa kuhusudu”? (Yakobo 4:5) Ni upendo. Sifa hiyo muhimu sana itatufanya tushangilie pamoja na wale ambao wana mapendeleo fulani ambayo hatuna. (Waroma 12:15) Upendo hutuzuia kukasirika mtu fulani anapopongezwa kwa sababu ya kuwa na kipawa fulani cha pekee au kwa kutimiza jambo fulani kubwa.
16. Ikiwa tunawapenda ndugu zetu kikweli, kwa nini tunapaswa kuepuka kujigamba kwa sababu ya mapendeleo yetu katika utumishi wa Yehova?
16 ‘Upendo haujigambi, haujitutumui.’ Upendo hutuzuia kujigamba kwa sababu ya vipawa vyetu au mafanikio yetu. Ikiwa tunawapenda ndugu zetu kikweli, je, tutajigamba daima kwa sababu ya mafanikio yetu katika huduma au kwa sababu ya mapendeleo yetu kutanikoni? Kujigamba kwa njia hiyo kunaweza kuwavunja wengine moyo, na kuwafanya wajione hawafai. Upendo hutuzuia kujigamba kwa sababu ya mapendeleo ya utumishi ambayo Mungu ametupatia. (1 Wakorintho 3:5-9) Zaidi ya hayo, upendo “haujitutumui,” au kama tafsiri moja inavyosema ‘haujioni kuwa bora.’ Upendo hutuzuia kujiona kuwa bora.—Waroma 12:3.
17. Upendo hutuchochea kuwajali wengine kwa njia gani, na hivyo tutaepuka mwenendo wa aina gani?
17 ‘Upendo haujiendeshi bila adabu.’ Mtu asiye na adabu anatenda kwa njia mbaya sana au yenye kuudhi. Mtu anayejiendesha hivyo hana upendo kwa sababu hajali hisia na hali njema ya wengine. Kinyume chake, upendo ni wenye fadhili na unatuchochea kuwajali wengine. Tukiwa na upendo tutakuwa na adabu, tutajiendesha kwa njia inayompendeza Mungu, na tutawaheshimu waamini wenzetu. Kwa hiyo, tukiwa na upendo tutaepuka “mwenendo wa aibu,” au tabia yoyote ile ambayo itawashtua au kuwaudhi ndugu zetu Wakristo.—Waefeso 5:3, 4.
18. Kwa nini mtu mwenye upendo hasisitizi kila jambo lifanywe jinsi anavyopenda?
18 ‘Upendo hautafuti masilahi yao wenyewe.’ Tafsiri nyingine inasema hivi: “Upendo hausisitizi kufuata njia yake.” Mtu mwenye upendo hasisitizi kila jambo lifanywe jinsi anavyopenda, kana kwamba maoni yake ni sawa sikuzote. Hawashawishi wengine ili kuwashurutisha wenye maoni tofauti wafuate maoni yake. Ukaidi wa aina hiyo unaonyesha kwamba ana kiasi fulani cha kiburi, na Biblia inasema: “Kiburi hutangulia uangamivu.” (Mithali 16:18) Ikiwa tunawapenda kikweli ndugu zetu, tutaheshimu maoni yao, na tutakuwa tayari kuyakubali inapowezekana. Maneno haya ya Paulo yanatutia moyo kuwa na roho hiyo: “Acheni kila mmoja afulize kutafuta sana, si faida yake mwenyewe, bali ya mtu yule mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.
19. Upendo unatusaidia tutendeje tunapokosewa na wengine?
19 ‘Upendo hauchokozeki, hauweki hesabu ya ubaya.’ Upendo haukasirishwi ovyoovyo na mambo ambayo wengine wanasema au kufanya. Ni jambo la kawaida kukasirika tunapokosewa. Lakini hata tukiwa na sababu nzuri ya kukasirika, hatutaendelea kuchokozeka ikiwa tuna upendo. (Waefeso 4:26, 27) Hatutaweka hesabu ya maneno au matendo yenye kuumiza kana kwamba tunayaandika katika kitabu ili tusiyasahau. Badala yake, upendo unatuchochea kumwiga Mungu wetu mwenye upendo. Kama tulivyoona katika Sura ya 26, Yehova husamehe kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Yeye husamehe na kusahau, yaani, hatuadhibu baadaye kwa sababu ya dhambi hizo. Je, hatushukuru kwamba Yehova haweki hesabu ya ubaya?
20. Tunapaswa kuhisije mwamini mwenzetu anapotenda dhambi na kupata madhara?
20 ‘Upendo haushangilii ukosefu wa uadilifu.’ Tafsiri nyingine inasema: “Upendo . . . haushangilii dhambi za wengine.” Tafsiri ya Moffat yasema: “Upendo haufurahii kamwe wengine wanapokosea.” Upendo haufurahii uovu, kwa hiyo tunakataa kabisa ukosefu wowote wa adili. Tunahisije mwamini mwenzetu anapotenda dhambi na kupata madhara? Tukiwa na upendo hatutashangilia kana kwamba tunasema, ‘Shauri yake! Asiyesikia la mkuu huvunjika guu!’ (Mithali 17:5) Hata hivyo, tunashangilia ndugu aliyetenda dhambi anapochukua hatua zifaazo za kujirekebisha na kufanya maendeleo ya kiroho.
“Njia Izidiyo”
21-23. (a) Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba “upendo haushindwi kamwe”? (b) Tutazungumzia nini katika sura ya mwisho?
21 “Upendo haushindwi kamwe.” Paulo alimaanisha nini aliposema hivyo? Muktadha unaonyesha kwamba alikuwa anazungumzia zawadi za roho za Wakristo wa mapema. Zawadi hizo zilithibitisha kwamba Mungu aliunga mkono kutaniko hilo jipya. Lakini si Wakristo wote wangeweza kuponya, kutoa unabii, au kuzungumza kwa lugha mbalimbali. Hata hivyo, hilo halikuwa muhimu; mwishowe zawadi hizo zote zingekoma. Lakini sifa fulani haingekoma, sifa ambayo kila Mkristo angeweza kukuza. Sifa yenye kutokeza sana, na yenye kudumu kuliko zawadi yoyote ya kimuujiza. Paulo aliiita sifa hiyo “njia izidiyo.” (1 Wakorintho 12:31) ‘Njia hiyo izidiyo’ ni gani? Ni njia ya upendo.
Watu wa Yehova wanajulikana kwa sababu ya jinsi wanavyopendana
22 Upendo wa Kikristo ambao Paulo alizungumzia “haushindwi kamwe,” yaani, hautafikia kikomo. Hadi leo, upendo wa kidugu wa kujidhabihu unawatambulisha wafuasi wa kweli wa Kristo. Je, hatuoni upendo huo katika makutaniko ya waabudu wa Yehova duniani kote? Upendo huo utadumu milele, kwa sababu Yehova anawaahidi watumishi wake waaminifu uhai wa milele. (Zaburi 37:9-11, 29) Na tujitahidi tuwezavyo ‘kuendelea kutembea katika upendo.’ Tukifanya hivyo, tunaweza kupata furaha nyingi sana ya kutoa. Isitoshe, tunaweza kuendelea kuishi—naam, kuendelea kupenda—milele na milele kama Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.
23 Katika sura hii inayomalizia sehemu ya upendo, tumezungumzia jinsi tunavyoweza kupendana. Kwa kuwa tunafaidika kwa njia nyingi kutokana na upendo wa Yehova—na vilevile kutokana na nguvu, haki, na hekima yake—twapaswa kujiuliza hivi, ‘Nitamthibitishiaje Yehova kwamba kwa kweli nampenda?’ Swali hilo litazungumziwa katika sura ya mwisho.
-