-
Kitabu Kipasacho KusomwaKitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Kitabu Kipasacho Kusomwa
“Biblia haipasi kuchukuliwa kwa uzito.” Ndivyo profesa wa chuo kikuu alivyomwambia mwanamke kijana mwenye kusema mambo waziwazi.
“Je, umepata kuisoma Biblia?” mwanamke huyo akauliza.
Kwa kushtuka, huyo profesa alilazimika kukiri kwamba hakuwa ameisoma.
“Waweza kutoaje usadikisho wenye nguvu juu ya kitabu ambacho hujakisoma kamwe?”
Huyo mwanamke alitoa hoja thabiti. Profesa aliamua kuisoma Biblia kisha atoe maoni juu yayo.
BIBLIA, inayotia ndani maandishi 66, imefafanuliwa kuwa “labda ndio mkusanyo wa vitabu wenye uvutano zaidi katika historia ya kibinadamu.”1 Kwa kweli, imeathiri baadhi ya sanaa, fasihi, na muziki, zilizo kuu kupita zote ulimwenguni. Imekuwa na uvutano mkubwa juu ya sheria. Imesifiwa kwa ajili ya mtindo wayo wa kifasihi na imestahiwa sana na wataalamu wengi. Matokeo yayo juu ya maisha za watu katika matabaka yote ya jamii yamekuwa yenye kina hasa. Imetokeza katika wengi wa wasomaji wayo kiwango chenye kutokeza cha uaminifu-mshikamanifu. Baadhi yao hata wamehatarisha uhai wao ili kuisoma tu.
Wakati uleule, kuna hali ya kutia shaka juu ya Biblia. Kuna watu walio na maoni thabiti juu yayo ingawa wao binafsi hawajaisoma kamwe. Huenda wakakiri thamani yayo ya kifasihi au ya kihistoria, lakini wanataka kujua: Kitabu kilichoandikwa maelfu ya miaka iliyopita chawezaje kuhusu ulimwengu huu wa kisasa? Twaishi katika “enzi ya habari.” Sisi hupata kwa urahisi sana habari za sasa hivi tu juu ya matukio na tekinolojia ya karibuni. Shauri lenye “ustadi” juu ya karibu matatizo yote ya maisha ya kisasa linapatikana kwa urahisi. Je, Biblia yaweza kwa kweli kuwa na habari yenye kutumika leo?
Broshua hii inajaribu kujibu maswali ya aina hiyo. Haikusudiwi kukulazimisha ufuate maoni au itikadi fulani za kidini, bali ina nia ya kuonyesha kwamba kitabu hiki chenye uvutano wa kihistoria, yaani, Biblia, chastahili uchunguzi wako. Ripoti iliyochapishwa mwaka wa 1994 ilionyesha kwamba waelimishaji fulani huona kwa dhati kwamba Biblia imekazwa imara sana katika tamaduni za Magharibi hivi kwamba “mtu yeyote, awe ni mwamini au asiyeamini, ambaye hafahamu mafundisho na masimulizi ya Kibiblia hatakuwa na elimu yoyote ya kitamaduni.”2
Labda, baada ya kusoma yaliyochapishwa humu ndani, utakubali kwamba—mtu awe ni wa kidini au la —Biblia ndiyo, kwa msingi kabisa, kitabu kipasacho kusomwa.
-
-
Kitabu Kinachowakilishwa VibayaKitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Kitabu Kinachowakilishwa Vibaya
“Fundisho la mwendo maradufu wa dunia izungukapo mhimili wayo na izungukapo jua si la kweli, na lapinga kabisa Maandiko Matakatifu.” Ndivyo lilivyotaarifu baraza liitwalo Congregation of the Index la Kanisa Katoliki ya Kiroma katika amri ya mwaka wa 1616.1 Je, kwa kweli Biblia hupinga mambo ya hakika ya kisayansi? Au imewakilishwa vibaya?
KATIKA majira ya baridi kali ya mwaka wa 1609/1610, Galileo Galilei aligeuza kuelekea mbingu darubini-upeo yake iliyotoka tu kufanyiwa maendeleo, naye akavumbua miezi minne ya angani ikizunguka sayari Sumbula. Kile alichoona kilidhoofisha kabisa dhana iliyoenea ya kwamba lazima magimba yote ya kimbingu yaizunguke dunia. Mapema, mwaka wa 1543, mwastronomia wa Poland Nicolaus Copernicus alikuwa ametoa nadharia ya kwamba sayari zinalizunguka jua. Galileo alithibitisha kwamba hiyo ilikuwa kweli ya kisayansi.
Hata hivyo, kwa wanatheolojia Wakatoliki, maoni hayo yalikuwa uzushi. Hilo kanisa lilikuwa limeamini kwa muda mrefu kwamba dunia ilikuwa kitovu cha ulimwengu wote mzima.2 Maoni hayo yalitegemea fasiri halisi ya maandiko yaliyoonyesha dunia kuwa imewekwa imara “juu ya misingi yake, ili isitikisike milele.” (Zaburi 104:5, Biblia Habari Njema) Akiwa ameitwa aende Roma, Galileo alifika mbele ya Baraza la Kuhukumu Wazushi. Kwa kuhojiwa chini ya hali ngumu, alilazimishwa aache mambo yote aliyokuwa amevumbua, na alitumia sehemu iliyobaki ya maisha yake akiwa amezuiliwa nyumbani.
Mwaka wa 1992, miaka ipatayo 350 baada ya kifo cha Galileo, Kanisa Katoliki lilikiri hatimaye kwamba kumbe alikuwa amesema kweli.3 Lakini ikiwa Galileo alikuwa amesema kweli, je, Biblia ilikuwa imekosea?
Kupata Maana ya Kweli ya Mafungu ya Kibiblia
Galileo aliamini Biblia kuwa kweli. Uvumbuzi wake wa kisayansi ulipopinga fasiri iliyoenea ya mistari fulani ya Biblia, alisababu kwamba wanatheolojia walikuwa wakikosa maana ya kweli ya hayo mafungu. Kwa vyovyote, “kweli mbili haziwezi kupingana kamwe,” akaandika.4 Alidokeza kwamba maneno dhahiri ya sayansi hayapingi maneno ya kila siku ya Biblia. Lakini wanatheolojia hawakuweza kujiruhusu washawishike. Walisisitiza kwamba taarifa zote za Kibiblia juu ya dunia zapasa kuchukuliwa kihalisi. Tokeo ni kwamba, hawakukataa tu uvumbuzi mbalimbali wa Galileo bali pia walikosa maana ya kweli ya maneno hayo ya Kimaandiko.
Kwa kweli, akili ya kawaida yapaswa ituambie kwamba Biblia irejezeapo “pembe nne za dunia,” haimaanishi kwamba waandikaji wa Biblia waliiona dunia kuwa mraba kihalisi. (Ufunuo 7:1) Biblia imeandikwa katika lugha ya watu wa kawaida, mara nyingi ikitumia tamathali za usemi zilizo dhahiri. Kwa hiyo isemapo juu ya dunia kuwa na “pembe nne,” “msingi” wenye kudumu, “nguzo,” na ‘jiwe la pembeni,’ Biblia haitoi ufafanuzi wa kisayansi wa dunia; kwa wazi inasema kwa njia ya kulinganisha vitu, kama vile tufanyavyo mara nyingi katika usemi wa kila siku.a—Isaya 51:13; Ayubu 38:6, BHN.
Katika kitabu chake kiitwacho Galileo Galilei, mwandika wasifu L. Geymonat, alisema hivi: “Wanatheolojia wasio tayari kupokea mawazo mapya ambao walitaka kuiwekea sayansi mipaka kwa msingi wa sababu za kibiblia wangefanya tu Biblia yenyewe isiaminiwe.”5 Na ndivyo walivyofanya. Kwa kweli, ni fasiri ya wanatheolojia iliyowekea sayansi mipaka, si Biblia yenyewe.
Vivyo hivyo, wale leo wafuatao kanuni za msingi za kidini huipotosha Biblia wanaposisitiza kwamba dunia iliumbwa katika siku sita za muda wa saa 24. (Mwanzo 1:3-31) Maoni hayo hayapatani wala na sayansi wala na Biblia. Katika Biblia, sawa na katika usemi wa kila siku, neno “siku” ni neno la kunyumbuka, likionyesha sehemu za wakati zenye muda tofauti-tofauti. Kwenye Mwanzo 2:4, siku zote sita za uumbaji zinarejezewa kuwa “siku” moja iliyotia ndani mambo yote. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “siku” katika Biblia laweza kumaanisha “wakati mrefu” tu.6 Kwa hiyo, hakuna sababu ya Kibiblia kusisitiza kwamba siku za uumbaji zilikuwa za muda wa saa 24 kila moja. Kwa kufundisha vingine, wale wafuatao kanuni za msingi huiwakilisha Biblia vibaya.—Ona pia 2 Petro 3:8.
Muda wa karne zote zilizopita, mara nyingi wanatheolojia wameipotosha Biblia. Chunguza baadhi ya njia ambazo dini za Jumuiya ya Wakristo zimewakilisha vibaya mambo ambayo Biblia husema.
Kuwakilishwa Vibaya na Dini
Mara nyingi matendo ya wale wasemao wanaifuata Biblia huharibu sifa njema ya kitabu wanachodai kustahi sana. Wale waitwao Wakristo isivyofaa wamemwaga damu ya mmoja na mwenzake katika jina la Mungu. Hata hivyo, Biblia huwaonya kwa upole wafuasi wa Kristo “wapendane.”—Yohana 13:34, 35; Mathayo 26:52.
Makasisi fulani hukumba mali za vikundi vyao kwa udanganyifu, wakiwavuta kwa maneno matamu ili wapate kutoka kwao fedha zilizochumwa kwa jasho—tofauti sana na agizo hili la Kimaandiko: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:8; 1 Petro 5:2, 3.
Kwa wazi, Biblia haiwezi kuhukumiwa kulingana na maneno na matendo ya wale wanaoinukuu tu au wanaodai kuishi kulingana nayo. Huenda basi mtu aliye tayari kupokea mawazo mapya akataka kujivumbulia yale ambayo Biblia husema hasa na kwa nini ni kitabu chenye kutokeza sana.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kielelezo, hata leo waastronomia wenye kuona mambo kihalisi zaidi watasema juu ya “kupanda” na “kushuka” kwa jua, nyota, na vikundinyota—ingawa kwa hakika, hizo huonekana kujongea kwa sababu tu ya kuzunguka kwa dunia.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Mbili kati ya darubini-upeo za Galileo
[Picha katika ukurasa wa 5]
Galileo akikabili mahakimu wake wa baraza la kuhukumu wazushi
-
-
Kitabu Chenye Kutawanywa Zaidi Sana UlimwenguniKitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Kitabu Chenye Kutawanywa Zaidi Sana Ulimwenguni
“Biblia ndiyo kitabu chenye kusomwa zaidi sana katika historia. . . . Nakala nyingi zaidi za Biblia zimetawanywa kuliko za kitabu kingine chochote. Biblia imetafsiriwa mara nyingi zaidi pia, na katika lugha nyingi zaidi, kuliko kitabu kingine chochote.”—“The World Book Encyclopedia.”1
KWA njia fulani, vitabu vingi ni kama watu. Vinatokea, huenda vikapendwa na watu wengi, na—isipokuwa vichache vilivyo bora kabisa—vinazeeka na havitumiki tena. Mara nyingi maktaba huwa kama makaburi ya vitabu visivyohesabika ambavyo si vya kisasa, havisomwi na kwa kweli, havitumiki tena.
Hata hivyo, Biblia ni ya kipekee hata miongoni mwa vitabu vilivyo bora kabisa. Ingawa ilianza kuandikwa miaka 3,500 iliyopita, hiyo ingali hai sana. Ni kitabu chenye kutawanywa zaidi sana duniani.a Kila mwaka, nakala zipatazo milioni 60 za Biblia nzima au sehemu-sehemu zayo hutawanywa. Chapa ya kwanza iliyotumia uchapaji kwa mashine ilitokezwa na matbaa ya mbuni Mjerumani Johannes Gutenberg mwaka wa 1455 hivi. Tangu wakati huo Biblia (zikiwa nzima au sehemu-sehemu) zinazokadiriwa kuwa bilioni nne zimechapwa. Hakuna kitabu kingine, cha kidini au kingine chochote, kikaribiacho hata idadi hiyo.
Biblia pia ndiyo kitabu chenye kutafsiriwa zaidi sana katika historia. Biblia nzima au sehemu-sehemu zayo imetafsiriwa katika lugha na lahaja zaidi ya 2,100.b Asilimia zaidi ya 90 ya familia ya kibinadamu wanaweza kupata angalau sehemu ya Biblia katika lugha yao wenyewe.2 Hivyo kitabu hiki kimepatikana katika mataifa mengi na kimevuka mipaka ya kijamii na ya kikabila.
Takwimu zenyewe huenda zisiandae sababu ya kukuvutia sana uichunguze Biblia. Hata hivyo, tarakimu za nakala zinazogawanywa na za tafsiri ni zenye kuvutia, zikithibitisha uvutio wa Biblia kwa wote. Kwa hakika kitabu kinachouzwa kwa wingi zaidi sana na ambacho kimetafsiriwa zaidi sana katika historia yote ya kibinadamu chastahili uchunguzi wako.
[Maelezo ya Chini]
a Kichapo cha pili chenye kutawanywa zaidi sana chafikiriwa kuwa kile kijitabu chenye jalada nyekundu kiitwacho Quotations From the Works of Mao Tse-tung, ambacho nakala zikadiriwazo kuwa milioni 800 zimeuzwa au kutawanywa.
b Takwimu kuhusu idadi ya lugha zinategemea tarakimu zilizochapishwa na United Bible Societies.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Biblia ya Gutenberg, katika Latini, kitabu kamili cha kwanza kilichochapwa kwa kutumia uchapaji kwa mashine
-
-
Hicho Kitabu Kiliokokaje?Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Hicho Kitabu Kiliokokaje?
Maandishi ya kale yalikuwa na maadui wa asili—moto, unyevu, ukungu. Biblia haikuepuka hatari hizo. Rekodi juu ya jinsi ambavyo Biblia imeokoka uharibifu usababishwao na upitaji wa wakati ikapata kuwa kitabu kipatikanacho zaidi sana ulimwenguni, inatokeza miongoni mwa maandishi ya kale. Historia hiyo yastahili kupewa upendezi mkubwa zaidi kuliko ule wa kijuujuu tu.
WAANDIKAJI wa Biblia hawakunakshi maneno yao kwenye jiwe; wala hawakuyachora kwenye mabamba ya udongo yenye kudumu. Yaonekana walirekodi maneno yao kwenye vifaa viwezavyo kuharibika—mafunjo (yaliyofanyizwa kutokana na mmea wa Misri wenye jina lilo hilo) na ngozi (za wanyama).
Ilikuwaje kwa maandishi ya awali? Labda yalichanguka muda mrefu uliopita, mengi yayo katika Israeli la kale. Msomi Oscar Paret afafanua hivi: “Vifaa vyote hivyo vilivyotumiwa kuandikia [mafunjo na ngozi] huhatarishwa kadiri ileile na unyevuanga, ukungu, na funza mbalimbali. Twajua kutokana na mambo tunayoona kila siku jinsi ambavyo karatasi, na hata ngozi yenye nguvu, huharibika kwa urahisi inapowekwa wazi nje au katika chumba chenye unyevunyevu.”1
Ikiwa maandishi ya awali hayako tena, basi maneno ya waandikaji wa Biblia yaliokokaje hadi siku yetu?
Kuhifadhiwa na Wanakiliji Waangalifu Sana
Upesi baada ya maandishi ya awali kuandikwa, nakala zilizoandikwa kwa mkono zilianza kutokezwa. Kwa kweli kunakili Maandiko kulipata kuwa kazi ya kuajiriwa katika Israeli la kale. (Ezra 7:6; Zaburi 45:1) Hata hivyo, nakala hizo pia zilirekodiwa kwenye vifaa viwezavyo kuharibika. Hatimaye nakala nyingine zilizoandikwa kwa mkono zikahitaji kuchukua mahali pa nakala hizo. Maandishi ya awali yalipotoweka, nakala hizi zikawa msingi wa kufanyiza hati za wakati ujao. Kunakili nakala kulikuwa utaratibu ulioendelea kwa karne nyingi. Karne zilipopita, je, makosa ya wanakiliji yalibadili sana maandishi ya Biblia? Uthibitisho wasema la.
Wanakiliji wenye kuajiriwa walikuwa wenye kujitoa sana. Waliyastahi sana maneno waliyoyanakili. Pia walikuwa waangalifu sana. Neno la Kiebrania lifasiriwalo “mnakiliji” ni so·pherʹ, inayorejezea kuhesabu na kurekodi. Ili kutolea kielezi usahihi wa wanakiliji, fikiria Wamasora.a Kuhusu wao, msomi Thomas Hartwell Horne afafanua hivi: “Wao . . . walihesabu ni ipi iliyo herufi ya katikati ya Pentateuki [vitabu vitano vya kwanza vya Biblia], ni kipi kishazi cha katikati cha kila kitabu, na ni mara ngapi kila herufi ya alfabeti [ya Kiebrania] hutokea katika Maandiko yote ya Kiebrania.”3
Hivyo, wanakiliji wastadi walitumia njia kadhaa za kuchunguza kutoka pande mbalimbali. Ili kuepuka kuacha herufi hata moja katika maandishi ya Biblia, walifikia hatua ya kuhesabu si maneno tu yaliyonakiliwa bali pia na herufi. Fikiria ule uangalifu mwingi uliohusika katika hilo: Yaripotiwa kwamba walihesabu herufi mojamoja 815,140 katika Maandiko ya Kiebrania!4 Jitihada hizo nyingi zilihakikisha usahihi wa kadiri ya juu.
Hata hivyo, wanakiliji hawakuwa wasioweza kukosea. Je, kuna uthibitisho wowote wa kwamba, zijapokuwa karne kadhaa za kunakili upya, maandishi ya Biblia yameokoka katika namna ya kutegemeka?
Msingi Thabiti wa Kuwa na Uhakika
Kuna sababu nzuri ya kuamini kwamba Biblia imepitishwa kwa usahihi hadi siku yetu. Uthibitisho watia ndani hati zilizoko zilizoandikwa kwa mkono—hati zikadiriwazo kuwa 6,000 za Maandiko ya Kiebrania yote au sehemu-sehemu na hati zipatazo 5,000 za Maandiko ya Kikristo katika Kigiriki. Miongoni mwazo ni hati ya Maandiko ya Kiebrania iliyovumbuliwa mwaka wa 1947 inayotoa kielelezo cha kadiri ambavyo kunakili Maandiko kulivyokuwa sahihi. Tangu wakati huo hiyo imeitwa “uvumbuzi wa hati ulio mkubwa kupita wote katika nyakati za kisasa.”5
Alipokuwa akichunga vikundi vyake mapema mwaka huo, mchungaji mchanga Mbeduini alivumbua pango karibu na Bahari Iliyokufa. Ndani yayo alipata mitungi kadhaa ya udongo, mingi yayo ikiwa mitupu. Hata hivyo, katika mmojawapo mitungi hiyo, iliyokuwa imefungwa ndindindi, alipata hatikunjo ya ngozi iliyokuwa imefungwa kwa uangalifu katika kitani na ilikuwa na kitabu kamili cha Isaya cha Biblia. Hatikunjo hiyo yenye kuhifadhiwa vizuri lakini iliyochakaa ilionyesha ishara za kuwa imetengenezwa. Huyo mchungaji mchanga hakutambua hata kidogo kwamba ile hatikunjo ya kale aliyokuwa akishika mikononi mwake hatimaye ingekaziwa uangalifu ulimwenguni pote.
Ni nini juu ya hati hiyo hasa kilichokuwa cha maana sana? Mwaka wa 1947 hati kamili za Kiebrania za zamani zaidi kupatikana zilikuwa za tarehe ya karibu karne ya kumi W.K. Lakini hatikunjo hii ilikuwa ya tarehe ya kufikia karne ya pili K.W.K.b—muda wa miaka zaidi ya elfu moja mapema.c Wasomi walipendezwa sana kupata matokeo ya kulinganisha hatikunjo hiyo na hati zilizotokezwa baadaye.
Katika uchunguzi mmoja, wasomi walilinganisha sura ya 53 ya Isaya katika Hatikunjo ya Bahari Iliyokufa na maandishi ya Kimasora yaliyotokezwa miaka elfu moja baadaye. Kitabu A General Introduction to the Bible, chafafanua matokeo ya uchunguzi huo: “Kati ya yale maneno 166 katika Isaya 53, kuna herufi kumi na saba tu zinazotilika shaka. Kumi kati ya herufi hizo zinahusu tu kuendelezwa kwa maneno, ambako hakuathiri maana. Herufi nyingine nne ni mabadiliko madogo katika mtindo, kama viunganishi. Herufi tatu zinazobaki zafanyiza neno ‘nuru,’ ambalo limeongezwa katika mstari wa 11, na haliathiri maana sana. . . . Hivyo, katika sura moja yenye maneno 166, kuna neno moja tu (herufi tatu) linalotilika shaka baada ya miaka elfu moja ya kupitishwa—na neno hilo halibadili sana maana ya hilo fungu.”7
Profesa Millar Burrows, aliyefanyia kazi hizo hatikunjo kwa miaka kadhaa, akichanganua yaliyomo, alifikia mkataa uo huo: “Tofauti zilizo nyingi kati ya . . . hatikunjo ya Isaya na maandishi ya Kimasora yaweza kufafanuliwa kuwa makosa katika kunakili. Kando na hayo, kwa ujumla kuna mwafaka wenye kutokeza na maandishi yapatikanayo katika hati za enzi ya kati. Mwafaka wa aina hiyo katika hati iliyo ya zamani zaidi sana watoa ushuhuda wenye kuhakikishia wa usahihi wa ujumla wa maandishi ya zamani.”8
“Ushuhuda wenye kuhakikishia” waweza kutolewa pia kuhusu unakiliji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa kielelezo, uvumbuzi wa karne ya 19 wa Codex Sinaiticus, hati ya kufanyizwa kwa ngozi nyororo ya mwana-kondoo iliyopewa tarehe ya karne ya nne W.K., ilisaidia kuhakikisha usahihi wa hatikunjo za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilizotokezwa karne kadhaa baadaye. Kipande cha mafunjo ya Gospeli ya Yohana, kilichovumbuliwa katika wilaya ya Faiyūm, Misri, kimepewa tarehe ya nusu ya kwanza ya karne ya pili W.K., miaka isiyozidi 50 baada ya ile Gospeli ya awali kuandikwa. Kilikuwa kimehifadhiwa kwa karne kadhaa katika mchanga mkavu. Maandishi hayo yanaafikiana na yale yapatikanayo katika hati za baadaye sana.9
Hivyo uthibitisho unahakikisha kwamba kwa hakika, wanakiliji walikuwa sahihi sana. Hata hivyo, walifanya makosa. Hakuna hati moja isiyo na makosa—kutia ndani Hatikunjo ya Isaya ya Bahari Iliyokufa. Hata hivyo, wasomi wameweza kupata na kusahihisha tofauti kati ya nakala na maandishi ya awali.
Kusahihisha Makosa ya Wanakiliji
Tuseme watu 100 wangeombwa kunakili hati ndefu kwa mkono. Bila shaka angalau baadhi ya hao wanakiliji wangefanya makosa. Hata hivyo, wote wasingefanya makosa yaleyale. Ikiwa ungechukua nakala zote 100 na kuzilinganisha kwa uangalifu sana, ungeweza kutenga makosa na kuamua ni yapi yaliyo maandishi barabara ya hati ya awali, hata ikiwa hukuiona kamwe.
Vivyo hivyo, wanakiliji wote wa Biblia hawakufanya makosa yaleyale. Kukiwa na maelfu ya hati za Biblia zinazopatikana sasa kihalisi za kutumiwa katika uchanganuzi wa kulinganisha, wasomi wa maandishi wameweza kutenga makosa, kuamua ni yapi yaliyo maandishi ya awali, na kurekodi masahihisho yanayohitajiwa. Kwa sababu ya uchunguzi huo mwangalifu, wasomi wa maandishi wametokeza maandishi makuu katika lugha za awali. Chapa hizo zilizosahihishwa za maandishi ya Kiebrania na Kigiriki zinatumia maneno yaliyoafikiwa kwa ujumla kuwa ya awali, mara nyingi zikiorodhesha katika vielezi-chini namna mbalimbali au maandishi mengine ambayo huenda yakawamo katika hati fulani-fulani. Chapa zilizosahihishwa na wasomi wa maandishi ndizo hutumiwa na watafsiri wa Biblia ili kuitafsiri Biblia katika lugha za kisasa.
Kwa hiyo usomapo tafsiri ya Biblia ya kisasa, kuna sababu za kutosha za kuwa na uhakika kwamba maandishi ya Kiebrania na ya Kigiriki ambayo ndiyo msingi wa tafsiri hiyo yanawakilisha maneno ya waandikaji wa awali wa Biblia kwa unyoofu wenye kutokeza.d Kwa kweli, rekodi ya jinsi Biblia ilivyookoka maelfu ya miaka ya kunakiliwa upya kwa mkono si ya kawaida. Sir Frederic Kenyon, aliyekuwa msimamizi wa British Museum kwa muda mrefu, aliweza basi kutaarifu hivi: “Si kusisitiza mno kusema kwamba kwa msingi maandishi ya Biblia ni hakika . . . Haiwezi kusemwa hivyo juu ya kitabu kingine chochote cha kale katika ulimwengu.”10
[Maelezo ya Chini]
a Wamasora (jina limaanishalo “Mabwana-Wakubwa wa Desturi”) walikuwa wanakiliji wa Maandiko ya Kiebrania walioishi kati ya karne ya sita na kumi W.K. Nakala za hati walizotokeza zinarejezewa kuwa maandishi ya Kimasora.2
b K.W.K. humaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida.” W.K. huonyesha “Wakati wa Kawaida,” ambao mara nyingi huitwa A.D., kwa Anno Domini, ikimaanisha “katika mwaka wa Bwana wetu.”
c Kitabu Textual Criticism of the Hebrew Bible, cha Emanuel Tov, chataarifu hivi: “Kwa msaada wa uchunguzi wa kaboni 14, 1QIsaa [Hatikunjo ya Isaya ya Bahari Iliyokufa] sasa imepewa tarehe ya kati ya mwaka wa 202 na 107 KWK (tarehe ya uchunguzaji wa maandishi ya kale: 125-100 KWK) . . . Njia iliyotajwa ya kuchunguza maandishi ya kale, iliyoboreshwa katika miaka ya majuzi, na inayoruhusu uwekaji wa tarehe ulio mkamilifu kwa msingi wa kulinganisha umbo na mpangilio wa herufi na vyanzo vya nje kama sarafu na michoro, imejithibitisha kuwa njia yenye kutegemeka kwa kulinganisha.”6
d Bila shaka, watafsiri mmoja-mmoja huenda wakawa wenye kufuata sana kanuni au walegevu katika kushikamana kwao na maandishi ya awali ya Kiebrania na Kigiriki.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Biblia ilihifadhiwa na wanakiliji wastadi
[Picha katika ukurasa wa 9]
Hatikunjo ya Isaya ya Bahari Iliyokufa (picha imeonyeshwa) ni karibu sawasawa na maandishi ya Kimasora yaliyotokezwa miaka elfu moja baadaye
-
-
Kitabu “Kisemacho” Lugha Zilizo HaiKitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Kitabu “Kisemacho” Lugha Zilizo Hai
Ikiwa lugha inayotumiwa kuandika kitabu inakufa, kwa kufaa kabisa kitabu hicho pia kinakufa. Ni watu wachache leo wawezao kusoma lugha za kale zilizotumiwa kuiandika Biblia. Hata hivyo hiyo iko hai. Imeokoka kwa sababu “imejifunza kusema” lugha za wanadamu zilizo hai. Nyakati nyingine wale watafsiri “walioifunza” kusema lugha nyingine walikabili vizuizi vilivyoonekana kutoshindika.
KUITAFSIRI Biblia—ikiwa na sura zayo zaidi ya 1,100 na mistari 31,000—ni kazi kubwa. Hata hivyo, muda wa karne zilizopita, watafsiri wenye kujitoa walianza kazi hiyo ngumu kwa mteremo. Wengi wao walikuwa tayari kupatwa na magumu na hata kufa kwa ajili ya kazi yao. Historia ya jinsi ambavyo Biblia ilikuja kutafsiriwa katika lugha za wanadamu ni simulizi lenye kutokeza la udumifu na ustadi. Chunguza sehemu ndogo tu ya rekodi hiyo yenye kuvutia sana.
Magumu Yanayokabili Watafsiri
Unatafsirije kitabu katika lugha ambayo haina herufi za kuiandika? Watafsiri wengi wa Biblia walikabili ugumu huo barabara. Kwa kielelezo, Ulfilas, wa karne ya nne W.K., alikusudia kuitafsiri Biblia katika lugha ambayo wakati huo ilikuwa ya kisasa lakini ambayo haikuwa imeandikwa—Kigothi. Ulfilas alishinda ugumu huo kwa kubuni alfabeti ya Kigothi yenye herufi 27, alizopata kutokana na alfabeti za Kigiriki na Kilatini. Tafsiri yake ya karibu Biblia nzima katika Kigothi ilikamilishwa kabla ya mwaka wa 381 W.K.
Katika karne ya tisa, ndugu wawili wa kimwili wenye kusema Kigiriki, Cyril (aliyeitwa Constantine hapo awali) na Methodius, wote wakiwa wasomi na wastadi wa lugha wenye kutokeza, walitaka kuwatafsiria Biblia watu wenye kusema Kislavi. Lakini Kislavoni—lugha iliyotangulia lugha za Kislavi za leo—haikuwa na herufi za kuiandika. Kwa hiyo hao ndugu wawili walibuni alfabeti ili kutokeza tafsiri ya Biblia. Hivyo Biblia iliweza sasa “kusema” na watu wengi zaidi, wale waliokuwa katika ulimwengu wa Kislavi.
Katika karne ya 16, William Tyndale alikusudia kuitafsiri Biblia katika Kiingereza kutoka lugha za awali, lakini alikabili upinzani mkali kutoka Kanisa na pia Serikali. Tyndale, aliyeelimishwa katika chuo kikuu cha Oxford, alitaka kutokeza tafsiri ambayo hata “kijana mkulima” angeweza kuielewa.1 Lakini ili kutimiza hilo, alilazimika kukimbilia Ujerumani, ambako tafsiri yake ya Kiingereza ya “Agano Jipya” ilichapwa mwaka wa 1526. Nakala zilipoingizwa Uingereza kisiri, wenye mamlaka walighadhibika sana hivi kwamba walianza kuziteketeza hadharani. Baadaye Tyndale alisalitiwa. Kabla tu ya kunyongwa na mwili wake kuteketezwa, alisema maneno haya kwa sauti kubwa: “Bwana, yafumbue macho ya Mfalme wa Uingereza!”2
Utafsiri wa Biblia uliendelea; watafsiri wasingekomeshwa. Kufikia mwaka wa 1800, angalau sehemu za Biblia zilikuwa “zimejifunza kusema” lugha 68. Kisha, Sosaiti za Biblia zilipofanyizwa—hasa Sosaiti ya Biblia ya Uingereza na Nchi za Kigeni, iliyoanzishwa mwaka wa 1804 —Biblia “ilijifunza” upesi lugha mpya zilizo nyingi hata zaidi. Mamia ya wanaume vijana walijitolea kwenda nchi za kigeni wakiwa wamishonari, wengi wakiwa na kusudi hasa la kuitafsiri Biblia.
Kujifunza Lugha za Afrika
Mwaka wa 1800, kulikuwa na karibu lugha 12 tu zilizoandikwa katika Afrika. Mamia ya lugha nyingine zilizosemwa zilihitaji kungojea mpaka mtu fulani alipobuni mfumo wa kuandika. Wamishonari walikuja wakajifunza hizo lugha, bila msaada wa vitabu vya kuwafunza au kamusi. Kisha wakajitahidi kusitawisha namna ya kuandika, na baada ya hilo walifunza wale watu jinsi ya kuzisoma herufi. Walifanya hayo ili siku fulani watu waweze kujisomea Biblia katika lugha yao wenyewe.3
Mishonari mmoja aliyefanya hivyo ni Mskochi aitwaye Robert Moffat. Mwaka wa 1821, akiwa na umri wa miaka 25, Moffat alianzisha misheni miongoni mwa watu wa kusini mwa Afrika wenye kusema Kitswana. Ili ajifunze lugha yao isiyoandikwa, alichangamana na hao watu, nyakati nyingine akisafiri sehemu za barani ili aishi miongoni mwao. “Watu walikuwa wenye fadhili,” aliandika baadaye, “na kukosea kwangu katika lugha kulitokeza kuangua kicheko mara nyingi. Hakuna wakati hata mmoja ambapo, mtu angesahihisha neno au sentensi, kabla ya mtu huyo kumwiga Moffat kwa matokeo sana, hivi kwamba akawafurahisha sana wengine.”4 Moffat alidumu na hatimaye akaijua kabisa hiyo lugha, akisitawisha namna ya kuiandika.
Mwaka wa 1829, baada ya kufanya kazi miongoni mwa Watswana kwa muda wa miaka minane, Moffat alimaliza kutafsiri Gospeli ya Luka. Ili kuichapa, alisafiri kilometa zaidi ya 900 kwa kutumia gari la kukokotwa na ng’ombe hadi pwani kisha akasafiri kwa meli hadi Cape Town. Huko gavana alimpa ruhusa ya kutumia matbaa ya serikali, lakini Moffat alilazimika kujipangia herufi za kupigia chapa na kujichapia, hatimaye akichapisha hiyo Gospeli mwaka wa 1830. Kwa mara ya kwanza, Watswana waliweza kusoma sehemu ya Biblia katika lugha yao wenyewe. Mwaka wa 1857, Moffat alimaliza tafsiri ya Biblia nzima katika Kitswana.
Baadaye Moffat alifafanua itikio la Watswana wakati Gospeli ya Luka ilipotolewa kwao kwa mara ya kwanza. Alisema hivi: “Nimejua juu ya watu ambao wamekuja mamia ya kilometa ili kujipatia nakala za Mtakatifu Luka. . . . Nimewaona wakipokea sehemu za Mtakatifu Luka, na kutoa machozi juu yazo, na kuzishika kifuani, na kububujika machozi ya shukrani nyingi, mpaka nikasema kwa zaidi ya mmoja, ‘Utaviharibu vitabu vyako kwa machozi yako.’”5
Hivyo watafsiri wenye kujitoa kama Moffat waliwapa Waafrika wengi—baadhi yao ambao mwanzoni hawakuona uhitaji wa kuwa na lugha yenye kuandikwa —fursa ya kwanza ya kuwasiliana kwa kuandika. Hata hivyo, hao watafsiri waliamini kwamba walikuwa wakiwapa watu wa Afrika zawadi yenye thamani hata zaidi—Biblia katika lugha yao wenyewe. Leo Biblia, nzima au kwa sehemu, “husema” katika lugha zaidi ya 600 za Afrika.
Kujifunza Lugha za Asia
Huku watafsiri katika Afrika waking’ang’ana ili kusitawisha namna za kuandika lugha zilizosemwa, ule upande mwingine wa ulimwengu, watafsiri wengine walikabili kizuizi kilicho tofauti kabisa—kutafsiri katika lugha ambazo tayari zilikuwa na herufi tata. Huo uliokuwa ndio ugumu uliokabili wale waliotafsiri Biblia katika lugha za Asia.
Mwanzoni mwa karne ya 19, William Carey na Joshua Marshman walikwenda India wakapata kujua sana lugha zayo nyingi zilizoandikwa. Kwa msaada wa William Ward, aliyekuwa mchapaji, walitokeza tafsiri za angalau sehemu za Biblia katika karibu lugha 40.6 Kuhusu William Carey, mtungaji J. Herbert Kane afafanua hivi: “Alibuni mtindo mzuri wa kimazungumzo, wenye kutiririka kama maji [wa lugha ya Kibengali] iliyochukua mahali pa ule mtindo bora wa zamani, hivyo akiifanya iwe yenye kueleweka zaidi na yenye kuwavutia wasomaji wa kisasa.”7
Adoniram Judson, aliyezaliwa na kulelewa Marekani, alisafiri kwenda Burma, na mwaka wa 1817 alianza kuitafsiri Biblia katika Kiburma. Akifafanua ugumu wa kujua sana lugha ya Mashariki kwa kadiri ya kutosha ili kuitafsiri Biblia, aliandika hivi: ‘Tunapojifunza lugha inayosemwa na watu sehemu ile nyingine ya dunia, ambao njia zao za kufikiri ni tofauti kabisa na zetu, na ambao kwa hiyo hatufahamu misemo yao, na herufi na maneno hayafanani hata kidogo na yale ya lugha yoyote ile ambayo tumeona; wakati ambapo hatuna kamusi wala mkalimani na ni lazima tuielewe lugha hiyo kidogo kabla hatujaweza kujipatia msaada wa mwalimu wa mahali hapo—hilo lamaanisha kazi!’8
Katika kisa cha Judson, hilo lilimaanisha miaka ipatayo 18 ya kazi yenye kujitahidi. Sehemu ya mwisho ya Biblia ya Kiburma ilichapwa mwaka wa 1835. Hata hivyo, kukaa kwake Burma kulimgharimu sana. Alipokuwa akifanyia kazi hiyo tafsiri, alishtakiwa kuwa mpelelezi na kwa sababu hiyo alitumia karibu miaka miwili katika jela iliyojaa mbu. Muda mfupi baada ya kuachiliwa, mke na binti yake mchanga walikufa kutokana na homa.
Robert Morrison mwenye umri wa miaka 25 alipowasili China mwaka wa 1807, alianza ile kazi ngumu sana ya kuitafsiri Biblia katika Kichina, mojawapo ya lugha tata zaidi zilizoandikwa. Alijua kiasi kidogo tu cha Kichina, alichokuwa ameanza kujifunza miaka miwili tu mapema. Morrison alilazimika pia kushindana na sheria ya Kichina, iliyojaribu kudumisha hali ya kujitenga ya China. Wachina walikatazwa, chini ya adhabu ya kifo, kuwafunza wageni hiyo lugha. Lilikuwa kosa lenye adhabu ya kifo kwa mgeni kuitafsiri Biblia katika Kichina.
Bila hofu bali mwenye uangalifu, Morrison aliendelea kujifunza hiyo lugha, akijifunza upesi. Katika miaka miwili alipata kazi akiwa mtafsiri wa kampuni iitwayo East India Company. Mchana, aliifanyia kazi kampuni, lakini sirini na akiwa na tisho la daima la kupatikana, alifanya kazi ya kuitafsiri Biblia. Mwaka wa 1814, miaka saba baadaye ya kuwasili China, alikuwa ametayarisha Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwa uchapaji.9 Miaka mitano baadaye, kwa msaada wa William Milne, aliyakamilisha Maandiko ya Kiebrania.
Huo ulikuwa utimizo mkubwa mno—sasa Biblia iliweza “kusema” katika lugha iliyotumiwa na watu wengi zaidi kuliko lugha nyingine yoyote ulimwenguni. Kwa sababu ya watafsiri wastadi, tafsiri katika lugha nyingine za Asia zilifuata. Leo, sehemu za Biblia zinapatikana katika lugha zaidi ya 500 za Asia.
Kwa nini watu kama Tyndale, Moffat, Judson, na Morrison walijitahidi kwa miaka mingi—baadhi yao hata wakihatarisha maisha zao —ili kutafsiri kitabu kwa ajili ya watu wasiowajua na, katika visa fulani, kwa ajili ya watu ambao hawakuwa na lugha iliyoandikwa? Kwa hakika, si ili kupata utukufu au faida ya kifedha. Waliamini kwamba Biblia ndiyo Neno la Mungu na kwamba yapaswa “kusema” na watu—watu wote—katika lugha yao wenyewe.
Uwe unahisi kwamba Biblia ndiyo Neno la Mungu au la, labda ungeafiki kwamba aina ya roho ya kujidhabihu iliyoonyeshwa na watafsiri hao wenye kujitoa ni haba sana katika ulimwengu wa leo. Je, kitabu ambacho huchochea hali hiyo ya kutokuwa na ubinafsi hakistahili uchunguzi?
[Chati katika ukurasa wa 12]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Idadi ya lugha ambazo sehemu za Biblia zimechapwa tangu 1800
68 107 171 269 367 522 729 971 1,199 1,762 2,123
1800 1900 1995
[Picha katika ukurasa wa 10]
Tyndale akiitafsiri Biblia
[Picha katika ukurasa wa 11]
Robert Moffat
[Picha katika ukurasa wa 12]
Adoniram Judson
[Picha katika ukurasa wa 13]
Robert Morrison
-
-
Yaliyomo Katika Hicho KitabuKitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Yaliyomo Katika Hicho Kitabu
Huenda mtu anayeingia katika maktaba kwa mara ya kwanza akapata unamna-namna wa vitabu kuwa wenye kutatanisha. Lakini kwa kufafanuliwa kidogo jinsi ambavyo vitabu vimepangwa, anapata kujua upesi jinsi ya kupata vitabu hususa. Vivyo hivyo, unaweza kupata mambo hususa katika Biblia kwa urahisi zaidi unapoelewa jinsi ambavyo yaliyomo katika Biblia yamepangwa.
NENO “Biblia” limetolewa katika neno la Kigiriki bi·bliʹa, lililomaanisha “makunjo ya mafunjo” au “vitabu.”1 Kwa kweli Biblia ni mkusanyo wa—maktaba ya —vitabu 66, ambavyo kuandikwa kwavyo kulienea kwa muda wa miaka ipatayo 1,600, kutoka mwaka wa 1513 K.W.K. hadi karibu mwaka wa 98 W.K.
Vitabu 39 vya kwanza, karibu robo tatu za yaliyomo katika Biblia, vinajulikana kuwa Maandiko ya Kiebrania, kwa kuwa viliandikwa katika lugha hiyo hasa. Vitabu hivyo vyaweza kwa ujumla kugawanywa katika vikundi vitatu: (1) Vya kihistoria, Mwanzo hadi Esta, vitabu 17; (2) Vya kishairi, Ayubu hadi Wimbo Ulio Bora, vitabu 5; na (3) Vya kiunabii, Isaya hadi Malaki, vitabu 17. Maandiko ya Kiebrania hutia ndani historia ya mapema ya dunia na wanadamu na pia historia ya taifa la Israeli la kale tangu mwanzo walo hadi karne ya tano K.W.K.
Vitabu 27 vinavyobaki vinajulikana kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kwa kuwa viliandikwa katika Kigiriki, lugha ya kimataifa ya hiyo siku. Kwa msingi vimepangwa kulingana na habari vilivyo nayo: (1) vitabu 5 vya kihistoria—Gospeli na Matendo, (2) zile barua 21, na (3) Ufunuo. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hukazia mafundisho na utendaji mbalimbali wa Yesu Kristo na wanafunzi wake katika karne ya kwanza W.K.
-
-
Je, Kitabu Hiki Chaweza Kutumainiwa?Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Je, Kitabu Hiki Chaweza Kutumainiwa?
“Katika Biblia ninapata alama za hakika zaidi za uasilia kuliko katika historia yoyote ile isiyo ya kidini [ya kilimwengu].”—Sir Isaac Newton, mwana-sayansi maarufu Mwingereza.1
JE, KITABU hiki—Biblia—chaweza kutumainiwa? Je, kinarejezea watu halisi walioishi, mahali halisi palipokuwako, na mambo halisi yaliyotukia? Ikiwa ndivyo, lazima kuwe na uthibitisho wa kwamba iliandikwa na waandikaji waangalifu, wenye kufuatia haki. Ithibati iko. Kiasi kikubwa chayo kimepatikana kikiwa kimezikwa ardhini, na kiasi kikubwa hata zaidi kimo katika hicho kitabu chenyewe.
Kuchimbua Uthibitisho
Uvumbuzi wa vyombo vya kale vilivyozikwa katika nchi zilizotajwa katika Biblia umetegemeza usahihi wa kihistoria na wa kijiografia wa Biblia. Chunguza baadhi tu ya uthibitisho ambao waakiolojia wamechimbua.
Daudi, yule mchungaji mchanga mwenye moyo mkubwa aliyepata kuwa mfalme wa Israeli, anajulikana sana na wasomaji wa Biblia. Jina lake huonekana mara 1,138 katika Biblia, na maneno “Nyumba ya Daudi”—mara nyingi yakirejezea nasaba yake ya wafalme—hutukia mara 25. (1 Samweli 16:13; 20:16) Lakini, hadi majuzi, hakukuwa na uthibitisho wa wazi wa kwamba Daudi alikuwako isipokuwa ule wa Biblia. Je, Daudi alikuwa mtu wa kubuniwa tu?
Mwaka wa 1993 kikundi cha waakiolojia, chenye kuongozwa na Profesa Avraham Biran, kilivumbua jambo la kushangaza, lililoripotiwa katika jarida Israel Exploration Journal. Mahali pa kilima cha kale kiitwacho Tel Dan, katika sehemu ya kaskazini mwa Israeli, walichimbua jiwe la basalti. Maneno “Nyumba ya Daudi” na “Mfalme wa Israeli” yalikuwa yamechongwa katika hilo jiwe.2 Mchoro huo, uliopewa tarehe ya karne ya tisa K.W.K., unasemwa kuwa sehemu ya nguzo ya ukumbusho ya ushindi iliyojengwa na Waaramae—maadui wa Israeli walioishi kuelekea mashariki. Kwa nini mchoro huo wa kale ni wa maana sana?
Kwa msingi wa ripoti ya Profesa Biran na mfanyakazi mwenzake, Profesa Joseph Naveh, makala katika Biblical Archaeology Review ilitaarifu hivi: “Hii ni mara ya kwanza ambayo jina Daudi limepatikana katika mchoro wowote wa kale zaidi ya Biblia.”3a Kuna jambo jingine lenye kutokeza juu ya huo mchoro. Maneno “Nyumba ya Daudi” yameandikwa yakiwa neno moja. Mstadi wa lugha Profesa Anson Rainey afafanua hivi: “Mara nyingi kitenganisha-maneno . . . hakitiwi ndani, hasa ikiwa maneno yaliyounganishwa ni jina pekee lililothibitishwa kabisa. ‘Nyumba ya Daudi’ lilikuwa kwa hakika jina pekee la aina hiyo kisiasa na kijiografia katikati ya karne ya tisa K.W.K.”5 Kwa hiyo ni wazi kwamba Mfalme Daudi na nasaba yake ya wafalme walijulikana sana katika ulimwengu wa kale.
Je, Ninawi—lile jiji kubwa la Ashuru litajwalo katika Biblia—lilikuwako kwa kweli? Majuzi sana kufikia mapema karne ya 19, wachambuzi fulani wa Biblia walikataa kuamini hivyo. Lakini mwaka wa 1849, Sir Austen Henry Layard alifukua magofu ya jumba la mfalme la Mfalme Senakeribu katika Kuyunjik, mahali palipothibitika kuwa sehemu ya Ninawi la kale. Hivyo wachambuzi walinyamazishwa kwa habari hiyo. Lakini magofu hayo yalifunua habari zaidi. Kwenye kuta za kimojawapo cha vyumba vilivyohifadhiwa vizuri kulikuwa na mchoro ukionyesha kutekwa nyara kwa jiji lililozingirwa vizuri, mateka wakipelekwa kwa miguu mbele ya huyo mfalme mwenye kushambulia. Juu ya huyo mfalme kuna maandishi haya: “Senakeribu, mfalme wa ulimwengu, mfalme wa Ashuru, aliketi kwenye kiti cha ufalme cha nîmedu naye akakagua kirasmi nyara (zilizotekwa) kutoka Lakishi (La-ki-su).”6
Mchoro na maandishi hayo, yawezayo kuonwa katika British Museum, yaafikiana na simulizi la Biblia la kutekwa nyara kwa jiji la Yuda la Lakishi na Senakeribu, kulikorekodiwa kwenye 2 Wafalme 18:13, 14. Akieleza juu ya umaana wa uvumbuzi huo, Layard aliandika hivi: “Ni nani angaliamini kuwa yamkini au yawezekana, kabla ya mambo hayo kuvumbuliwa, kwamba chini ya fungu la udongo na takataka lililotia alama mahali pa Ninawi, kungepatikana historia ya vita kati ya Hezekia [mfalme wa Yuda] na Senakeribu, iliyoandikwa na Senakeribu mwenyewe wakati uleule ambapo vita hivyo vilitukia, na kuhakikisha hata katika mambo madogo-madogo sana rekodi ya Kibiblia?”7
Waakiolojia wamechimbua vyombo vingine vingi—vyombo vya udongo, magofu ya majengo, mabamba ya udongo, sarafu, hati, nguzo za ukumbusho, na michoro—vinavyohakikisha usahihi wa Biblia. Wachimbuaji wamefukua lile jiji la Ukaldayo la Uru, kitovu cha kibiashara na cha kidini alikoishi Abrahamu.8 (Mwanzo 11:27-31) Maandishi ya Tarehe ya Matukio ya Nabonido, yaliyofukuliwa katika karne ya 19, hufafanua anguko la Babiloni kupitia Sairasi Mkubwa mwaka wa 539 K.W.K., tukio lililosimuliwa katika Danieli sura ya 5.9 Mchoro (ambao vipande vyao vimehifadhiwa katika British Museum) uliopatikana katika njia inayopitia chini ya tao katika Thesalonike la kale lina majina ya watawala wa jiji wafafanuliwao kuwa “mapolitaki,” neno lisilojulikana katika fasihi bora kabisa ya Kigiriki lakini lililotumiwa na mwandikaji wa Biblia Luka.10 (Matendo 17:6, NW, kielezi-chini) Hivyo usahihi wa Luka ulitetewa katika jambo hilo dogo—kama vile ulivyokuwa tayari umetetewa katika mambo mengine madogo-madogo.—Linganisha Luka 1:3.
Hata hivyo, waakiolojia hawaafikiani kati yao sikuzote, wala hawaafikiani na Biblia sikuzote. Hata hivyo, ndani yayo yenyewe Biblia ina uthibitisho wenye nguvu kwamba ni kitabu kiwezacho kutumainiwa.
Masimulizi Yametolewa kwa Unyoofu
Wanahistoria wenye kufuatia haki wasingerekodi ushindi tu (kama ule mchoro kuhusu tendo la Senakeribu la kuteka nyara Lakishi) bali wangeripoti ushinde pia, si mafanikio tu bali kutofaulu pia, si nguvu tu bali udhaifu pia. Ni historia chache za kilimwengu zinazoonyesha ufuatiaji huo wa haki.
Kuhusu wanahistoria Waashuri, Daniel D. Luckenbill afafanua hivi: “Mara nyingi ni wazi kwamba kiburi cha kifalme kilidai kwamba usahihi wa kihistoria ubadilishwe kwa udanganyifu.”11 Zikitolea kielezi “kiburi [hicho] cha kifalme,” kumbukumbu za kihistoria za Mfalme Mwashuri Ashurnasirpali zajivuna hivi: “Mimi ni wa kifalme, mimi ni wa kibwana, mimi nimekwezwa, mimi ni mweza-yote, mimi ni mwenye kuheshimiwa, mimi ni mwenye kutukuzwa, mimi ni mashuhuri, mimi ni mwenye nguvu, mimi ni shujaa, mimi ni jasiri kama simba, na mimi ni hodari!”12 Je, ungekubali mambo yote usomayo katika kumbukumbu hizo za kihistoria kuwa historia sahihi?
Kinyume cha hilo, waandikaji wa Biblia walionyesha unyoofu wenye kuburudisha. Musa, kiongozi wa Israeli, aliripoti kwa unyoofu kasoro za nduguye, Aroni, za dadaye Miriamu, za wapwa wake wa kiume Nadabu na Abihu, na za watu wake, pamoja na zake mwenyewe. (Kutoka 14:11, 12; 32:1-6; Mambo ya Walawi 10:1, 2; Hesabu 12:1-3; 20:9-12; 27:12-14) Makosa mazito ya Mfalme Daudi hayakufichwa bali yalirekodiwa—na rekodi hiyo iliandikwa Daudi alipokuwa angali akitawala akiwa mfalme. (2 Samweli, sura ya 11 na ya 24) Mathayo, mwandikaji wa kitabu chenye jina lake, atuambia jinsi mitume (ambao alikuwa mmoja wao) walivyobishania umaana wao wa kibinafsi na jinsi walivyomwacha Yesu usiku wa kukamatwa kwake. (Mathayo 20:20-24; 26:56) Waandikaji wa barua za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walikiri kwa wazi matatizo, kutia na ukosefu wa adili katika ngono na mitengano, katika baadhi ya makutaniko ya Kikristo ya mapema. Na walisema mambo waziwazi katika kushughulikia matatizo hayo.—1 Wakorintho 1:10-13; 5:1-13.
Kuripoti huko kwa unyoofu, kuliko wazi kwaonyesha kuhangaikia kweli kwa moyo mweupe. Kwa kuwa waandikaji wa Biblia walikuwa tayari kuripoti habari mbaya juu ya wale waliowapenda, watu wao, na hata juu yao wenyewe, je, hakuna sababu nzuri ya kutumaini maandishi yao?
Sahihi Katika Mambo Madogo-Madogo
Katika kesi za mahakamani ustahilifu wa ushuhuda wa shahidi waweza mara nyingi kuamuliwa kwa msingi wa mambo madogo ya hakika. Mwafaka juu ya mambo madogo-madogo waweza kuuthibitisha ushuhuda kuwa sahihi na wa haki, ilhali tofauti kubwa zaweza kuufunua kuwa maneno ya kubuniwa. Kwa upande mwingine, simulizi lenye utaratibu mno—ambalo katika hilo kila jambo dogo limepangwa vizuri—laweza pia kufunua ushuhuda usio wa kweli.
“Ushuhuda” wa Biblia unafaanaje kwa habari hiyo? Waandikaji wa Biblia walionyesha upatano wa ajabu. Kuna mwafaka wa karibu hata juu ya mambo madogo-madogo sana. Hata hivyo, upatano huo si wenye kupangwa kimakusudi, ambao ungezusha shaka kwamba kulikuwa na maafikiano ya kisiri. Ni wazi kwamba hakukuwa na mpango wa kisiri katika hali za sadfa, mara nyingi waandikaji walikuwa wakiafikiana bila kukusudia. Chunguza baadhi ya vielelezo.
Mwandikaji wa Biblia Mathayo aliandika hivi: “Na Yesu, alipokuja ndani ya nyumba ya Petro, aliona mama-mkwe wake amelala chini akiwa mgonjwa akiwa na homa.” (Mathayo 8:14) Hapo Mathayo aliandaa jambo dogo lenye kupendeza lakini lisilo muhimu: Petro alikuwa ameoa. Jambo hilo dogo la hakika linategemezwa na Paulo aliyeandika hivi: “Je, hatuna ruhusa kumchukua mke Mkristo katika ziara zetu, kama vile wafanyavyo mitume wengine . . . na Kefa?”b (1 Wakorintho 9:5, BHN) Muktadha unaonyesha kwamba Paulo alikuwa akijitetea dhidi ya uchambuzi usio wa haki. (1 Wakorintho 9:1-4) Kwa wazi, jambo hilo dogo la hakika—kwamba Petro alikuwa ameoa —halitokezwi na Paulo ili kutegemeza usahihi wa simulizi la Mathayo bali linatolewa kwa kutukia tu.
Waandikaji wote wanne wa Gospeli—Mathayo, Marko, Luka, na Yohana —wanarekodi kwamba usiku wa kukamatwa kwa Yesu, mmoja wa wanafunzi wake alitoa upanga akampiga mtumwa wa kuhani wa cheo cha juu, akikatilia mbali sikio la huyo mtu. Ni Gospeli ya Yohana pekee inayoripoti jambo dogo hili lionekanalo kutohitajika: “Jina la mtumwa huyo lilikuwa ni Malko.” (Yohana 18:10, 26) Kwa nini Yohana pekee ndiye atoaye jina la huyo mtu? Mistari michache baadaye simulizi laandaa jambo dogo la hakika lisilotaarifiwa kwingine kokote: Yohana “alijulikana na kuhani wa cheo cha juu.” Alijulikana pia na watu wa nyumbani mwa kuhani wa cheo cha juu; watumishi walimfahamu, naye aliwafahamu. (Yohana 18:15, 16) Basi, lilikuwa jambo la asili tu kwamba Yohana ataje jina la huyo mtu aliyejeruhiwa, ilhali wale waandikaji wengine wa Gospeli, ambao huyo mtu hakujulikana kwao, hawalitaji.
Nyakati nyingine, mafafanuzi yenye mambo madogo-madogo hayatiwi ndani katika simulizi moja lakini yanaandaliwa kwingineko kwa taarifa za kutukia tu. Mathalani, simulizi la Mathayo la kesi ya Yesu mbele ya Sanhedrini ya Kiyahudi lasema kwamba watu fulani waliokuwapo “wakampiga makofi usoni, wakisema: ‘Tutolee unabii, wewe Kristo. Ni nani aliyekupiga?’” (Mathayo 26:67, 68) Kwa nini wangemwomba Yesu ‘awatolee unabii’ ni nani aliyekuwa amempiga, ilhali mwenye kumpiga alikuwa amesimama hapo mbele yake? Mathayo hafafanui. Lakini waandikaji wengine wawili wa Gospeli wanatoa lile jambo dogo ambalo halikutiwa ndani: Wanyanyasi wa Yesu waliufunika uso wake kabla ya yeye kupigwa makofi. (Marko 14:65; Luka 22:64) Mathayo atoa habari yake bila kuhangaika kama kila jambo dogo liliandaliwa.
Gospeli ya Yohana yasimulia juu ya pindi ambayo umati mkubwa ulikusanyika ili kumsikia Yesu akifundisha. Kulingana na hiyo rekodi, Yesu alipouona umati, “alimwambia Filipo: ‘Tutainunua wapi mikate ili hawa wale?’” (Yohana 6:5) Kati ya wanafunzi wote waliokuwapo, kwa nini Yesu alimwuliza Filipo ni wapi wangenunua mikate? Mwandikaji hasemi. Lakini, katika simulizi linalolingana na hilo, Luka aripoti kwamba hilo lilitukia karibu na Bethsaida, jiji lililoko katika ukingo wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya, na mapema katika Gospeli ya Yohana inasema kwamba “Filipo alikuwa wa kutoka Bethsaida.” (Yohana 1:44; Luka 9:10) Kwa hiyo Yesu kwa kupatana na akili alimwuliza mtu ambaye mji aliotoka ulikuwa karibu. Mwafaka kati ya mambo hayo madogo-madogo ni wa ajabu, hata hivyo si wa kukusudia.
Katika visa vingine kutotiwa ndani kwa mambo fulani madogo-madogo kwaongezea tu ustahilifu wa mwandikaji wa Biblia. Mwandikaji wa kitabu cha 1 Wafalme husema juu ya ukame mkali katika Israeli. Ulikuwa mkali sana hivi kwamba mfalme hakuweza kupata maji ya kutosha wala nyasi za kuokoa uhai wa farasi na nyumbu zake. (1 Wafalme 17:7; 18:5) Hata hivyo, simulizi hilohilo laripoti kwamba nabii Eliya aliamuru aletewe maji ya kutosha akiwa juu ya Mlima Karmeli (ili yatumiwe kuhusiana na dhabihu) kujaza mtaro uliotia ndani eneo la labda meta 1,000 za mraba. (1 Wafalme 18:33-35) Maji hayo yote yalitoka wapi katikati ya huo ukame? Mwandikaji wa kitabu cha 1 Wafalme hakujitahidi kufafanua hilo. Hata hivyo, mtu yeyote aliyeishi Israeli alijua kwamba Karmeli ulikuwa katika pwani ya Bahari ya Mediterania, kama vile maneno ya baadaye ya kutukia tu yaonyeshavyo katika hilo simulizi. (1 Wafalme 18:43) Hivyo, maji ya bahari yangepatikana kwa urahisi. Ikiwa kitabu hiki ambacho vinginevyo hutia ndani mambo madogo-madogo kingekuwa kitabu cha kubuniwa tu kinachojifanya kuwa cha kweli, kwa nini mwandikaji wacho, ambaye basi angekuwa mwandishi mdanganyifu stadi, angeacha katika maandishi jambo hili lionekanalo kuwa hitilafu?
Kwa hiyo je, Biblia yaweza kutumainiwa? Waakiolojia wamechimbua vyombo vya kutosha kuhakikisha kwamba Biblia hurejezea watu halisi, mahali halisi, na matukio halisi. Hata hivyo, jambo la kuvutia zaidi ni ule uthibitisho unaopatikana katika Biblia yenyewe. Waandikaji wanyoofu hawakuficha habari za yeyote yule—hata zao wenyewe —katika kurekodi mambo barabara yaliyotendeka. Upatano wa kindani wa maandishi, kutia na hali za sadfa zisizopangwa kimbele, zatolea huo “ushuhuda” sifa ya wazi ya kuwa kweli. Kukiwa na ‘alama hizo za hakika za uasilia,’ kwa kweli Biblia ni kitabu uwezacho kutumaini.
[Maelezo ya Chini]
a Baada ya uvumbuzi huo, Profesa André Lemaire aliripoti kwamba kufanyizwa upya kwa mstari ulioharibika kwenye jiwe liitwalo Mesha stela (liitwalo pia Jiwe la Moabu), lililovumbuliwa mwaka wa 1868, kwafunua kwamba hilo pia lina rejezeo kwenye “Nyumba ya Daudi.”4
b “Kefa” ni jina la Kiyahudi lililo sawasawa na “Petro.”—Yohana 1:42.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kipande cha Tel Dan
[Picha katika ukurasa wa 16]
Maandishi ya Ashuru yaliyochongwa ukutani yakionyesha kuzingiwa kwa Lakishi, kulikotajwa kwenye 2 Wafalme 18:13, 14
-
-
Je, Kitabu Hiki Chaafikiana Na Sayansi?Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Je, Kitabu Hiki Chaafikiana Na Sayansi?
Dini haijaona sayansi kuwa rafiki yayo sikuzote. Katika karne zilizotangulia wanatheolojia fulani walikinza uvumbuzi mbalimbali wa kisayansi walipohisi kwamba huo ulihatarisha ufasiri wao wa Biblia. Lakini je, kwa kweli sayansi ni adui wa Biblia?
IKIWA waandikaji wa Biblia wangalikuwa wamekubali maoni yenye kuenea ya kisayansi ya siku yao, tokeo lingalikuwa kitabu chenye taarifa za kisayansi zisizo sahihi kabisa. Hata hivyo waandikaji hawakuendeleza maoni hayo yasiyokuwa ya kisayansi. Kinyume cha hilo, waliandika taarifa kadhaa zilizo thabiti kisayansi na pia zilizopinga moja kwa moja kauli zilizokubaliwa hiyo siku.
Dunia Ina Umbo Jipi?
Swali hilo limevutia wanadamu sana kwa maelfu ya miaka. Maoni ya kawaida katika nyakati za kale yalikuwa kwamba dunia ilikuwa tambarare. Kwa kielelezo, Wababiloni waliamini kwamba ulimwengu wote mzima ulikuwa sanduku au chumba ambacho dunia ilikuwa sakafu yacho. Makuhani wa Kivedi wa India waliwazia kwamba dunia ilikuwa tambarare na kwamba upande mmoja tu wayo ulikuwa umekaliwa na watu. Kabila la kikale katika Asia liliiona dunia kuwa sinia kubwa ya kubebea vikombe vya chai.
Mapema sana kuanzia karne ya sita K.W.K., mwanafalsafa Mgiriki Pythagoras alitoa nadharia kwamba kwa kuwa mwezi na jua ni tufe, lazima dunia pia iwe tufe. Aristotle (karne ya nne K.W.K.) aliafiki baadaye, akifafanua kwamba hali ya dunia kuwa tufe inathibitishwa na kupatwa mbalimbali kwa mwezi. Kivuli cha dunia kwenye mwezi ni mviringo.
Hata hivyo, dhana ya dunia tambarare (ikiwa imekaliwa na watu kwenye sehemu yayo ya juu tu) haikutoweka kabisa. Watu fulani hawakuweza kukubali lile dokezo la kupatana na akili la dunia iliyo duara—dhana ya antipodi.a Lactantius, mtetea-imani Mkristo wa karne ya nne W.K., alidhihaki hilo wazo lenyewe. Alisababu hivi: “Je, kuna mtu aliye mpumbavu sana aweze kuamini kwamba kuna watu ambao nyayo zao ziko juu kuliko vichwa vyao? . . . kwamba mimea na miti hukua kuelekea chini? kwamba mvua, na theluji, na mvua-barafu huanguka kuelekea juu?”2
Dhana ya antipodi ilitokeza hali ya kutatanisha kwa wanatheolojia wachache. Nadharia fulani zilishikilia kwamba ikiwa kulikuwa na watu wanaoishi katika upande ule mwingine wa dunia, wasingeweza kuwasiliana hata kidogo na wanadamu wajulikanao ama kwa sababu bahari ilikuwa pana mno isiweze kusafiriwa ama kwa sababu kanda yenye joto kali isiyoweza kupitika iliizunguka ikweta. Basi watu walioishi kwenye ule upande mwingine wa dunia wangeweza kuwa walitoka wapi? Kwa kutatanishwa, wanatheolojia fulani walipendelea kuamini kwamba kusingeweza kuwa na watu wanaoishi kwenye ule upande mwingine wa dunia, au hata, kama alivyojadili Lactantius, kwamba dunia hata isingeweza kuwa tufe!
Bado, dhana ya kwamba dunia ni tufe ilienea, na hatimaye ilikubaliwa na watu wengi sana. Hata hivyo, ni baada tu ya enzi ya anga kuanza katika karne ya 20, ndipo imewezekana kwa wanadamu kusafiri mbali angani vya kutosha kuthibitisha kwa kujionea moja kwa moja kwamba dunia ni tufe.b
Na msimamo wa Biblia ulikuwa nini katika suala hili? Katika karne ya nane K.W.K., wakati maoni yaliyoenea yalipokuwa kwamba dunia ilikuwa tambarare, karne kadhaa kabla ya wanafalsafa wa Kigiriki kutoa nadharia kwamba dunia yamkini ilikuwa tufe, na maelfu ya miaka kabla ya wanadamu kuiona dunia ikiwa tufe kutoka angani, nabii Mwebrania Isaya alitaarifu hivi kwa usahili wa ajabu: “Yeye ndiye anayeketi juu ya duara ya dunia.” (Isaya 40:22, italiki ni zetu.) Neno la Kiebrania chugh, linalotafsiriwa hapa “duara,” laweza pia kufasiriwa kuwa “tufe.”3 Tafsiri nyingine za Biblia husema, “tufe la dunia” (Douay Version) na “dunia mviringo.”—Moffatt.c
Mwandikaji wa Biblia Isaya aliepuka ngano za kawaida juu ya dunia. Badala ya hivyo, aliandika taarifa ambayo haikutishwa na maendeleo ya uvumbuzi wa kisayansi.
Ni Nini Kinachoitegemeza Dunia?
Katika nyakati za kale, wanadamu walitatanishwa na maswali mengine juu ya ulimwengu: Dunia inakalia nini? Jua, mwezi, na nyota hutegemezwa na nini? Hawakuwa na ujuzi wowote juu ya sheria ya nguvu za uvutano za ulimwengu wote mzima, zilizofanyizwa na Isaac Newton na kuchapishwa mwaka wa 1687. Wazo la kwamba kwa kweli, magimba ya kimbingu huning’inia katika anga tupu pasipo kitu halikujulikana kwao. Hivyo, mafafanuzi yao mara nyingi yalidokeza kwamba vitu au dutu zenye kugusika ziliitegemeza dunia na magimba mengine ya kimbingu huko juu.
Kwa kielelezo, nadharia moja ya kale, labda yenye kuanzishwa na watu walioishi kwenye kisiwa fulani, ilikuwa kwamba dunia ilizungukwa na maji na kwamba ilielea katika maji hayo. Wahindu waliwazia kwamba dunia ilikuwa na misingi kadhaa, mmoja juu ya mwingine. Ilikalia ndovu wanne, hao ndovu walisimama juu ya kobe mkubwa mno, huyo kobe alisimama juu ya nyoka mkubwa sana, na nyoka huyo aliyejikunja alielea juu ya maji ya ulimwengu wote mzima. Empedocles, mwanafalsafa Mgiriki wa karne ya tano K.W.K., aliamini kwamba dunia ilikalia kisulisuli na kwamba kisulisuli hicho kilikuwa ndicho kisababishi cha mwendo wa magimba ya kimbingu.
Miongoni mwa maoni yenye uvutano zaidi yalikuwa yale ya Aristotle. Ingawa alitoa nadharia kwamba dunia ni tufe, alikana kwamba ingeweza kwa vyovyote kuning’inia katika anga tupu. Katika maandishi yake On the Heavens, alipokuwa akikanusha dhana ya kwamba dunia hukalia maji, alisema hivi: “Si asili ya maji, sawa na vile si asili ya dunia, kuning’inia hewani: lazima yakalie kitu.”4 Kwa hiyo, dunia ‘hukalia kitu gani’? Aristotle alifundisha kwamba jua, mwezi, na nyota zilikuwa zimeshikamana na sehemu ya juu ya tufe zito, jangavu. Tufe moja lilikuwa ndani ya jingine, dunia ikiwa—bila kujongea —katikati. Matufe hayo yalipozunguka moja likiwa ndani ya jingine, vitu vilivyokuwa juu yayo—jua, mwezi, na sayari —vilijongea kuivuka anga.
Ufafanuzi wa Aristotle ulionekana kuwa wenye kupatana na akili. Ikiwa magimba ya kimbingu hayakuwa yameshikamana imara na kitu fulani, yangeweza kukaa juu kwa njia gani nyingine? Maoni ya Aristotle aliyestahiwa yalikubaliwa kuwa jambo la hakika kwa miaka ipatayo 2,000. Kulingana na The New Encyclopædia Britannica, katika karne ya 16 na ya 17 mafundisho yake “yalifikia kiwango cha kuwa fundisho la kidini” machoni pa kanisa.5
Darubini-upeo ilipobuniwa, waastronomia walianza kutilia shaka nadharia ya Aristotle. Bado, jibu liliwaepuka mpaka Sir Isaac Newton alipofafanua kwamba sayari zinaning’inia katika anga tupu, zikiwa zimeshikiliwa katika mizingo yao na kani isiyoonekana—nguvu za uvutano. Ilionekana kutosadikika, na baadhi ya wafanyakazi wa Newton waliona ni vigumu kuamini kwamba anga lingeweza kuwa tupu, bila dutu yoyote kwa ujumla.d6
Biblia ina mambo gani ya kusema juu ya swali hilo? Miaka karibu 3,500 iliyopita, Biblia ilitaarifu kwa uwazi usio wa kawaida kwamba dunia inaning’inia “pasipo na kitu.” (Ayubu 26:7, BHN) Katika Kiebrania cha awali, neno litumiwalo hapa kwa “pasipo na kitu” (beli-mahʹ) humaanisha kihalisi “bila kitu.”7 Union Version ya Kiswahili hutumia maneno, “nafasi isiyo na kitu.”
Watu walio wengi katika siku hizo hawakuifikiria hata kidogo dunia kuwa sayari inayoning’inia katika “nafasi isiyo na kitu.” Hata hivyo, kimbele sana kuliko wakati wake, mwandikaji wa Biblia alirekodi taarifa iliyo thabiti kisayansi.
Biblia na Sayansi ya Kitiba—Je, Zaafikiana?
Sayansi ya kitiba ya kisasa imetufunza mengi juu ya kuenea na kuzuia kwa maradhi. Maendeleo ya kitiba katika karne ya 19 yaliongoza kwenye kuingizwa katika zoea la kitiba uzuiaji wa ukuzi au ongezeko la viini—usafi ili kupunguza maambukizo. Tokeo lilikuwa la kutazamisha. Kulikuwa na upunguo mkubwa katika maambukizo na vifo vya kabla ya wakati wavyo.
Hata hivyo, matabibu wa kale hawakuelewa kikamili jinsi maradhi huenea, wala hawakung’amua umaana wa usafi wa kutunza afya katika kuzuia magonjwa. Si ajabu sana kwamba mazoea yao mengi ya kitiba yangeonekana kuwa ya kikatili kulingana na viwango vya kisasa.
Mojawapo ya maandishi ya zamani zaidi ya kitiba yapatikanayo ni Mafunjo ya Ebers, mkusanyiko wa ujuzi wa kitiba wa Kimisri, wenye tarehe inayorudi nyuma kuanzia karibu mwaka wa 1550 K.W.K. Hatikunjo hiyo ina tiba 700 kwa maradhi mbalimbali “kuanzia umo la mamba hadi maumivu ya ukucha wa kidole cha mguu.”8 Kichapo The International Standard Bible Encyclopaedia chataarifu hivi: “Ujuzi wa kitiba wa matabibu hao ulikuwa wa kimajaribio tu, wa kimizungu sanasana na usio wa kisayansi hata kidogo.”9 Tiba zilizo nyingi zilikuwa hazina matokeo kabisa, lakini baadhi yazo zilikuwa za hatari sana. Ili kutibu jeraha, agizo moja la daktari lilidokeza kupaka mchanganyiko uliofanyizwa kwa kinyesi cha kibinadamu pamoja na dutu nyinginezo.10
Maandishi hayo ya matibabu ya Kimisri yaliandikwa karibu wakati uleule ambapo vitabu vya kwanza vya Biblia viliandikwa, vilivyotia ndani Sheria ya Kimusa. Musa, aliyezaliwa mwaka wa 1593 K.W.K., alikulia Misri. (Kutoka 2:1-10) Akiwa mshiriki wa nyumba ya Farao, “[ali]funzwa katika hekima yote ya Wamisri.” (Matendo 7:22) Aliwafahamu “waganga” wa Misri. (Mwanzo 50:1-3) Je, mazoea yao ya kitiba yasiyokuwa na matokeo au yaliyokuwa hatari yaliathiri maandishi yake?
La. Kinyume cha hilo, Sheria ya Kimusa ilitia ndani kanuni za usafi wa kutunza afya zilizokuwa za kimbele sana kuliko wakati wazo. Kwa kielelezo, sheria kuhusu kambi za kijeshi ilitaka kuzikwa kwa kinyesi mbali na kambi. (Kumbukumbu la Torati 23:13) Hilo lilikuwa hatua ya kimaendeleo sana ya kuzuia maradhi. Ilisaidia kuzuia maji yasichafuliwe na iliandaa kinga dhidi ya ugonjwa uitwao shigellosis uenezwao na mainzi na magonjwa mengine ya kuhara ambayo bado huua mamilioni ya watu kila mwaka katika nchi zilizo na hali mbaya zenye uchafu na takataka.
Sheria ya Kimusa ilikuwa na kanuni nyingine za usafi wa kutunza afya zilizokinga Israeli dhidi ya mweneo wa maradhi ya kuambukiza. Mtu aliyekuwa na maradhi ya kuambukiza au aliyeshukiwa kuwa nayo aliwekwa karantini. (Mambo ya Walawi 13:1-5) Mavazi au vyombo vilivyogusa mnyama aliyekuwa amekufa mwenyewe (labda kutokana na maradhi fulani) vilipasa ama kuoshwa kabla ya kutumiwa tena ama kuharibiwa. (Mambo ya Walawi 11:27, 28, 32, 33) Mtu yeyote aliyegusa maiti alionwa kuwa asiye safi na alihitaji kufuata utaratibu wa kusafishwa uliotia ndani kuosha mavazi yake na kuoga. Katika kile kipindi cha siku saba cha kutokuwa safi, alipaswa aepuke uhusiano wa kimwili na wengine.—Hesabu 19:1-13.
Sheria hiyo ya usafi wa kutunza afya inafunua hekima isiyokuwa ya matabibu wa mataifa ya jirani wakati huo. Maelfu ya miaka kabla ya sayansi ya kitiba kupata kujua juu ya njia ambazo maradhi huenea, Biblia iliagiza hatua zifaazo za kuzuia zikiwa kinga dhidi ya maradhi. Si ajabu kwamba, Musa aliweza kusema juu ya Waisraeli kwa ujumla katika siku yake kuwa wakiishi hadi umri wa miaka 70 au 80.e—Zaburi 90:10.
Huenda ukakiri kwamba taarifa za Kibiblia zilizotangulia ni sahihi kisayansi. Lakini kuna taarifa nyingine katika Biblia zisizoweza kuthibitishwa kisayansi. Je, hilo lamaanisha kwamba ni lazima iwe kwamba Biblia hupingana na sayansi?
Kukubali Yasiyothibitika
Taarifa isiyothibitika si lazima iwe isiyo ya kweli. Ithibati ya kisayansi inawekewa mipaka na uwezo wa binadamu wa kuvumbua uthibitisho wa kutosha na wa kufasiri habari kwa usahihi. Lakini kweli fulani hazithibitiki kwa sababu hakuna uthibitisho ambao umehifadhiwa, uthibitisho si dhahiri au haujavumbuliwa, au uwezo na ustadi wa kisayansi hautoshi ili kufikia mkataa usiokanushika. Je, huenda hali ikawa hivyo kwa habari ya taarifa fulani za Kibiblia ambazo hazina uthibitisho wa kiasili wenye kujitegemea?
Kwa kielelezo, marejezeo ya Biblia kwenye makao yasiyoonekana yanayokaliwa na watu wa roho hayawezi kuthibitishwa—au kukanushwa—kisayansi. Hilohilo laweza kusemwa juu ya matukio ya kimuujiza yanayotajwa katika Biblia. Hakuna uthibitisho dhahiri wa kijiolojia wa kutosha unaopatikana kuridhisha watu fulani juu ya Furiko la tufeni pote la siku ya Noa. (Mwanzo, sura ya 7) Je, lazima tufikie mkataa wa kwamba hilo halikutukia? Matukio ya kihistoria yaweza kufanywa yasiwe dhahiri kwa sababu ya kupita kwa wakati na kubadilika kwa mambo. Kwa hiyo, je, haiwezekani kwamba maelfu ya miaka ya utendaji wa kijiolojia imefuta uthibitisho mwingi wa kuwako kwa Furiko?
Kweli, Biblia ina taarifa zisizoweza kuthibitishwa au kukanushwa na uthibitisho wa kiasili unaopatikana. Lakini je, hilo litushangaze? Biblia si kitabu cha mafundisho ya sayansi. Hata hivyo, hiyo ni kitabu chenye kweli. Tayari tumechunguza uthibitisho wenye nguvu wa kwamba waandikaji wayo walikuwa wanaume wenye uaminifu-maadili na wenye kufuatia haki. Na wanapotaja mambo kuhusiana na sayansi, maneno yao ni sahihi na hayatii ndani kabisa “nadharia” za kale za kisayansi ambazo baadaye zilithibitika kuwa ngano tu. Hivyo sayansi si adui wa Biblia. Kuna sababu za kutosha za kupima yale ambayo Biblia husema ukiwa tayari kupokea mawazo mapya.
[Maelezo ya Chini]
a “Antipodi . . . ni mahali pawili panapokabiliana barabara tufeni. Mstari wenye kunyooka kati ya mahali hapo pawili hupitia katikati ya dunia. Neno la Kiingereza antipodes lamaanisha wayo kwa wayo katika Kigiriki. Watu wawili wanaosimama kwenye antipodi wangekuwa karibu zaidi kwenye nyayo za miguu yao.”1—The World Book Encyclopedia.
b Kulingana na maana hususa, dunia ni tufe lililo na sehemu tambarare kidogo kwenye ncha zalo.
c Kwa kuongezea, ni kitu kilicho tufe tu ndicho kionekanacho kuwa duara kutoka kila upande kinakoonwa. Diski bapa ingeonekana mara nyingi zaidi ikiwa umbo yai, si duara.
d Maoni ya watu wengi katika siku ya Newton yalikuwa kwamba ulimwengu wote mzima ulikuwa umejaa kiowevu—“mchuzi” wa kilimwengu —na kwamba mizunguko ya maji katika kiowevu hicho ilifanya sayari zizunguke.
e Mwaka wa 1900, urefu wa uhai katika nchi nyingi za Ulaya na katika Marekani ulitarajiwa kuwa usiozidi miaka 50. Tangu wakati huo, urefu huo umeongezeka kwa njia ya kutazamisha si kwa sababu tu ya maendeleo ya kitiba katika kudhibiti maradhi bali pia kwa sababu ya usafi wa kutunza afya na hali nzuri zaidi za maisha.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Taarifa isiyothibitika si lazima iwe isiyo ya kweli
[Picha katika ukurasa wa 18]
Maelfu ya miaka kabla ya wanadamu kuiona dunia ikiwa tufe kutoka angani, Biblia ilirejezea “duara ya dunia”
[Picha katika ukurasa wa 20]
Sir Isaac Newton alifafanua kwamba sayari zinashikiliwa katika mizingo yazo na nguvu za uvutano
-
-
Kitabu Chenye Kutumika Kwa Maisha Ya KisasaKitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Kitabu Chenye Kutumika Kwa Maisha Ya Kisasa
Vitabu vinavyotoa shauri vinapendwa sana katika ulimwengu wa leo. Lakini vinaelekea kupitwa na wakati na upesi vinasahihishwa au vingine vinachukua mahali pavyo. Namna gani Biblia? Ilikamilishwa karibu miaka 2,000 iliyopita. Hata hivyo, ujumbe wayo wa awali haujaboreshwa kamwe au kufanywa uwe wa kisasa. Je, kitabu cha aina hiyo kingeweza kuwa na mwongozo wenye kutumika kwa siku yetu?
WATU fulani husema la. “Hakuna mtu ambaye angetetea utumizi wa chapa ya mwaka wa 1924 ya [kitabu cha] mafundisho cha kemia katika darasa la kemia la kisasa,” akaandika Dakt. Eli S. Chesen, akifafanua ni kwa nini alihisi kwamba Biblia imepitwa na wakati.1 Kijuujuu, hoja hiyo yaonekana kupatana na akili. Kwa vyovyote, mwanadamu amejifunza mengi juu ya afya ya akilini na tabia ya kibinadamu tangu Biblia ilipoandikwa. Kwa hiyo kitabu cha kale hivyo kingewezaje kuhusu maisha ya kisasa?
Kanuni za Sikuzote
Ingawa ni kweli kwamba nyakati zimebadilika, mahitaji ya binadamu ya msingi yamebaki yaleyale. Muda wote wa historia watu wamekuwa na uhitaji wa upendo na shauku. Wametaka kuwa na furaha na kuwa na maisha yenye kusudi. Wamehitaji shauri juu ya jinsi ya kukabiliana na misongo ya kiuchumi, jinsi ya kufanikisha ndoa, na jinsi ya kutia ndani ya watoto wao kanuni nzuri za kiadili na za kinidhamu. Biblia ina shauri linaloshughulikia mahitaji hayo ya msingi.—Mhubiri 3:12, 13; Waroma 12:10; Wakolosai 3:18-21; 1 Timotheo 6:6-10.
Shauri la Biblia hudhihirisha ufahamu makini wa utu wa kibinadamu. Chunguza baadhi ya vielelezo vya kanuni zayo mahususi, za sikuzote ambazo ni zenye kutumika kwa maisha ya kisasa.
Mwongozo Wenye Kutumika kwa Ndoa
Familia, lasema jarida UN Chronicle, “ni kisehemu cha zamani zaidi na cha msingi kabisa cha shirika la kibinadamu; kiungo cha maana zaidi kati ya vizazi.” Hata hivyo, “kiungo [hicho] cha maana,” kinavunjika kwa kadiri yenye kutisha. “Katika ulimwengu wa leo,” lasema jarida Chronicle, “familia nyingi hukabili magumu ya kukatisha tamaa yanayotisha uwezo wazo wa kutenda kazi na, kwa kweli, uwezo wazo wa kuokoka.”2 Biblia hutoa shauri gani la kusaidia familia iokoke?
Kwanza, Biblia ina mengi ya kusema juu ya jinsi waume na wake wapaswavyo kutendeana. Kwa kielelezo, kuhusu waume, hiyo husema hivi: “Waume wapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye apendaye mke wake ajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu aliyepata wakati wowote kuuchukia mwili wake mwenyewe; bali huulisha na kuutunza sana.” (Waefeso 5:28, 29) Mke alishauriwa “kuwa na staha yenye kina kirefu kwa mume wake.”—Waefeso 5:33.
Fikiria yale yanayohusishwa katika kutumia shauri hilo la Biblia. Mume ampendaye mkewe ‘kama mwili wake mwenyewe’ hamchukii wala kumtenda kinyama. Hampigi kimwili, wala hamtendi vibaya kwa maneno au kihisia-moyo. Badala ya hivyo, yeye humpa staha na ufikirio uleule anaojionyesha. (1 Petro 3:7) Hivyo mke wake huhisi anapendwa na huhisi usalama katika ndoa yake. Kwa njia hiyo yeye huwaandalia watoto wake kielelezo chema cha jinsi wanawake wapasavyo kutendewa. Kwa upande mwingine, mke aliye na “staha yenye kina kirefu” kwa mumewe hamwondolei adhama yake kwa kumchambua daima au kumdharau. Kwa sababu mke anamstahi, mume huhisi anatumainiwa, anakubaliwa, na anathaminiwa.
Je, shauri hilo ni lenye kutumika katika ulimwengu wa kisasa? Ni jambo lenye kupendeza kwamba wale ambao kazi-maisha yao ni kuchunguza familia leo wamefikia mikataa hiyohiyo. Msimamizi mmoja wa programu ya kushauri familia alisema hivi: “Familia zenye uthabiti na mafanikio zaidi ninazojua ni zile ambazo katika hizo mama na baba wana uhusiano wenye nguvu na upendo kati yao wenyewe. . . . Uhusiano huo wenye nguvu ulio wa maana waonekana kuleta hali ya usalama katika watoto.”3
Muda wa miaka iliyopita, shauri la Biblia juu ya ndoa limethibitika kuwa lenye kutegemeka zaidi kuliko shauri la washauri wasiohesabika wa familia yenye nia njema. Kwa vyovyote, si muda mrefu sana uliopita kwamba wastadi wengi walikuwa wakitetea talaka kuwa suluhisho la upesi na lililo rahisi la ndoa mbaya. Leo, wengi wao wanawasihi sana watu wafanye ndoa zao zidumu kwa vyovyote ikiwezekana. Lakini badiliko hili la maoni limekuja baada tu ya madhara mengi kutokea.
Kinyume cha hilo, Biblia hutoa shauri lenye kutegemeka na lenye usawaziko kwa habari ya ndoa. Inakiri kwamba hali fulani za kupita kiasi hufanya talaka iruhusike. (Mathayo 19:9) Wakati uo huo, inalaumu kutaliki kwa sababu zisizo za maana. (Malaki 2:14-16) Inalaumu pia ukosefu wa uaminifu katika ndoa. (Waebrania 13:4) Inasema kwamba ndoa huhusisha kujifunga wajibu: ‘Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.’a—Mwanzo 2:24; Mathayo 19:5, 6.
Shauri la Biblia juu ya ndoa linahusu leo kadiri ileile lilivyohusu wakati Biblia ilipoandikwa. Mume na mke wanapotendeana kwa upendo na staha na kuiona ndoa kuwa uhusiano wa pekee, ni yamkini zaidi ndoa kuokoka—na familia kuokoka pamoja nayo.
Mwongozo Wenye Kutumika kwa Wazazi
Miongo kadhaa iliyopita wazazi wengi—kwa kuchochewa na “mawazo mapya” juu ya kuzoeza watoto —walifikiri “haipasi kuwatia watoto nidhamu.”8 Walihofu kwamba kuwawekea watoto mipaka kungesababisha vurugu na kukatisha tamaa. Washauri wenye nia njema juu ya kulea watoto walikuwa wakisisitiza kwamba wazazi wapaswa tu kuwapa watoto wao usahihisho wenye upole sana. Lakini sasa wengi wa wastadi hao wanachunguza tena fungu la nidhamu, na wazazi wenye kuhangaika wanatafuta uwazi fulani juu ya hiyo habari.
Hata hivyo, sikuzote Biblia imetoa shauri la wazi na lifaalo juu ya uleaji wa watoto. Karibu miaka 2,000 iliyopita, ilisema hivi: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Nomino ya Kigiriki inayotafsiriwa “nidhamu” humaanisha “malezi, mazoezi, mafunzo.”9 Biblia husema kwamba nidhamu hiyo, au mafunzo hayo, ni uthibitisho wa upendo wa mzazi. (Mithali 13:24) Watoto husitawi wakiwa na miongozo dhahiri ya kiadili na ufahamu uliositawishwa wa lililo jema na lililo baya. Nidhamu huwaambia kwamba wazazi wao huwajali na hujali juu ya aina ya watu wanaopata kuwa.
Lakini mamlaka ya mzazi—“fimbo ya nidhamu”—haipaswi kamwe kuwa yenye kutenda vibaya.b (Mithali 22:15, BHN; 29:15) Biblia huwaonya wazazi hivi: “Msiwasahihishe watoto wenu kupita kiasi, au mtawakatisha tamaa kabisa.” (Wakolosai 3:21, Phillips) Hiyo hukiri pia kwamba kwa kawaida adhabu ya kimwili siyo njia yenye matokeo zaidi ya kufunza. Mithali 17:10 husema hivi: “Lawama hupenya moyoni mwa mwenye ufahamu, kuliko mapigo mia moyoni mwa mpumbavu.” Zaidi ya hayo, Biblia hupendekeza nidhamu ya kuzuia. Kwenye Kumbukumbu la Torati 11:19 wazazi wanasihiwa sana watumie wasaa kwa faida yao ili kutia ndani katika watoto wao kanuni za kiadili.—Ona pia Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.
Shauri la Biblia la sikuzote kwa wazazi liko wazi. Watoto wanahitaji nidhamu yenye upatano na upendo. Uzoefu wenye kutumika waonyesha kwamba shauri hilo hufanya kazi kwa kweli.c
Kushinda Mipaka Inayogawanya Watu
Leo watu wamegawanywa na mipaka ya kijamii, kitaifa, na kikabila. Kuta hizo bandia zimechangia uchinjaji wa wanadamu wasio na hatia katika vita vya kotekote ulimwenguni. Tukifikiria yaliyotendeka katika historia, kwa kweli hakuna tazamio la kwamba wanaume na wanawake wa jamii na mataifa tofauti-tofauti wataona na kutendeana kuwa sawasawa. “Suluhisho,” asema mwanasiasa Mwafrika, “limo mioyoni mwetu.”11 Lakini si rahisi kuibadili mioyo ya kibinadamu. Lakini, fikiria jinsi ambavyo ujumbe wa Biblia huuvutia moyo na kuendeleza mitazamo ya usawa.
Fundisho la Biblia la kwamba Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu” huzuia wazo lolote la ubora wa kijamii. (Matendo 17:26) Unaonyesha kwamba kwa kweli kuna jamii moja tu—jamii ya kibinadamu. Biblia huendelea kututia moyo “[tuwe] waigaji wa Mungu,” ambaye inasema hivi juu yake: “[Yeye] si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Waefeso 5:1; Matendo 10:34, 35) Kwa wale wanaoichukua Biblia kwa uzito na wanaojaribu kwa kweli kuishi kulingana na mafundisho yayo, ujuzi huo hutokeza muungano. Unakazia uvutano wao katika kina cha ndani kabisa, katika moyo wa kibinadamu, ukiyeyusha mipaka yenye kugawanya ya kutengenezwa na watu. Fikiria kielelezo kimoja.
Hitler alipopiga vita kotekote Ulaya, kulikuwa na kikundi kimoja cha Wakristo—Mashahidi wa Yehova —waliokataa kwa uthabiti kujiunga katika uchinjaji wa wanadamu wasio na hatia. Wao ‘wasingeinua upanga’ dhidi ya mwanadamu mwenzao. Walichukua msimamo huo kwa sababu ya tamaa yao ya kumpendeza Mungu. (Isaya 2:3, 4; Mika 4:3, 5) Waliamini kwa kweli yale ambayo Biblia hufundisha—kwamba hakuna taifa wala jamii iliyo bora zaidi ya nyingine. (Wagalatia 3:28) Kwa sababu ya msimamo wao wa kupenda amani, Mashahidi wa Yehova walikuwa miongoni mwa wafungwa wa kwanza katika kambi za mateso.—Waroma 12:18.
Lakini si wote waliodai kuifuata Biblia waliochukua msimamo huo. Punde baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, Martin Niemöller, kasisi Mprotestanti Mjerumani, aliandika hivi: “Yeyote yule atakaye kumlaumu Mungu kwa [vita] hajui, au hataki kujua, Neno la Mungu. . . . Makanisa ya Kikristo yamejitoa yenyewe tena na tena, kwa muda wa enzi zote ambazo zimepita, katika kubariki vita, majeshi, na silaha na . . . yalisali kwa njia isiyopatana hata kidogo na Ukristo yakiomba uharibifu wa maadui wayo vitani. Yote hayo ni makosa yetu na makosa ya babu zetu, lakini Mungu si wa kulaumiwa hata kidogo. Na sisi Wakristo wa leo tunaaibika mbele ya lile lenye kuitwa eti farakano kama wale Wanafunzi wa Biblia Wenye Bidii [Mashahidi wa Yehova], walioingia kambi za mateso kwa mamia na maelfu na [hata] wakafa kwa sababu walikataa utumishi wa kijeshi nao wakakataa kuua wanadamu.”12
Hadi leo hii, Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kwa udugu wao, unaounganisha pamoja Waarabu na Wayahudi, Wakroatia na Waserbia, Wahutu na Watutsi. Hata hivyo, Mashahidi hukiri kwa utayari kwamba muungano huo unawezekana, si kwa sababu wao ni bora kuliko wengine, bali kwa sababu wanachochewa na nguvu ya ujumbe wa Biblia.—1 Wathesalonike 2:13.
Mwongozo Wenye Kutumika Uendelezao Afya Nzuri ya Akilini
Afya ya mtu ya kimwili huathiriwa mara nyingi na hali yake ya akilini na afya ya kihisia-moyo. Mathalani, uchunguzi mbalimbali wa kisayansi umethibitisha matokeo yenye kudhuru ya hasira. “Mwingi wa uthibitisho unaopatikana hudokeza kwamba watu wenye uhasama wamo katika hatari zaidi ya kupatwa na maradhi ya moyo (pamoja na magonjwa mengine) kwa sababu mbalimbali, kutia ndani kuwa na marafiki wachache zaidi, ongezeko la matokeo ya kimwili wanapokasirishwa, na kujihusisha zaidi katika mazoea yenye kuudhuru mwili,” wasema Dakt. Redford Williams, Mkurugenzi wa Utafiti wa Tabia kwenye Duke University Medical Center, na mkewe, Virginia Williams, katika kitabu chao Anger Kills.13
Maelfu ya miaka kabla ya uchunguzi huo wa kisayansi, Biblia, katika maneno sahili lakini ya wazi, ilihusianisha hali yetu ya kihisia-moyo na afya yetu ya kimwili hivi: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili; bali husuda ni ubovu wa mifupa.” (Mithali 14:30; 17:22) Kwa hekima, Biblia ilishauri hivi: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu,” na “Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako.”—Zaburi 37:8; Mhubiri 7:9.
Pia Biblia ina shauri lifaalo la kudhibiti hasira. Kwa kielelezo, andiko la Mithali 19:11 lasema hivi: “Busara ya [“ufahamu wenye kina wa,” NW] mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” Neno la Kiebrania kwa “ufahamu wenye kina” linatokana na kitenzi kinachovuta uangalifu kwenye “ujuzi wa sababu” ya jambo fulani.14 Shauri lenye hekima ni: “Fikiri kabla ya kutenda.” Kujitahidi kuelewa sababu za msingi zinazofanya wengine waongee au watende katika njia fulani kwaweza kumsaidia mtu awe mvumilivu zaidi—na asielekee sana kukasirika.—Mithali 14:29.
Shauri jingine lenye kutumika linapatikana kwenye andiko la Wakolosai 3:13, lisemalo: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” Maudhiko madogo ni sehemu ya maisha. Maneno “endeleeni kuchukuliana” yadokeza kuvumilia mambo tusiyopenda katika wengine. ‘Kusamehe’ kwamaanisha kuacha uchungu wa moyo. Nyakati nyingine ni jambo la hekima kuacha hisia zenye uchungu badala ya kuzidumisha; kuweka hasira kutaongezea tu mzigo wetu wenye kulemea.—Ona sanduku “Mwongozo Wenye Kutumika kwa Mahusiano ya Kibinadamu.”
Leo, kuna vyanzo vingi vya shauri na mwongozo. Lakini Biblia kwa kweli ni ya kipekee. Shauri layo si nadharia tu, wala shauri layo halitudhuru kamwe. Badala ya hivyo, hekima yayo imethibitika kuwa “amini sana.” (Zaburi 93:5) Zaidi ya hayo, shauri la Biblia ni la sikuzote. Ingawa ilikamilishwa karibu miaka 2,000 iliyopita, maneno yayo yangali yenye kutumika. Nayo yanatumika kwa kadiri ileile iwe ngozi yetu ni ya rangi gani au ni nchi gani tunamoishi. Maneno ya Biblia yana nguvu pia—nguvu ya kubadili watu wawe bora. (Waebrania 4:12) Hivyo kukisoma kitabu hicho na kuzitumia kanuni zacho kwaweza kuongeza ubora wa maisha yako.
[Maelezo ya Chini]
a Neno la Kiebrania da·vaqʹ, linalotafsiriwa hapa ‘-shikamana,’ “latia ndani maana ya kuambatana na mtu fulani katika shauku na uaminifu-mshikamanifu.”4 Katika Kigiriki, neno linalofasiriwa “atashikamana” kwenye Mathayo 19:5 linahusiana na neno linalomaanisha “kuunga kwa gundi,” “kuunga kwa saruji,” “kuunganisha pamoja ndindindi.”5
b Katika nyakati za Biblia, neno “fimbo” (sheʹvet, katika Kiebrania) lilimaanisha “kijiti” au “gongo,” kama lile lililotumiwa na mchungaji.10 Katika muktadha huu fimbo ya mamlaka hudokeza mwongozo wenye upendo, sio unyama wenye udhalimu.—Linganisha Zaburi 23:4.
c Ona zile sura “Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana,” “Saidia Tineja Wako Asitawi,” “Je, Kuna Mwasi Nyumbani?,” na “Ilinde Familia Yako Dhidi ya Mavutano Yaletayo Uharibifu” katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Blabu katika ukurasa wa 24]
Biblia hutoa shauri la wazi na lifaalo juu ya maisha ya familia
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Sifa za Familia Zenye Uthabiti na Mafanikio
Miaka kadhaa iliyopita mwelimishaji ambaye pia ni mtaalamu wa familia aliongoza ukaguzi wenye kuenea ambao katika huo wastadi zaidi ya 500 ambao huandalia familia mashauri waliombwa watoe maelezo juu ya vitabia walivyoona katika familia “zenye uthabiti na mafanikio.” Kwa kupendeza, miongoni mwa vitabia vya kawaida zaidi vilivyoorodheshwa vilikuwa mambo yaliyopendekezwa na Biblia muda mrefu uliopita.
Mazoea mazuri ya uwasiliano yalikuwa ya kwanza katika hiyo orodha, kutia na njia zenye matokeo za kusuluhisha tofauti. Sera ya kawaida inayopatikana katika familia zenye uthabiti na mafanikio ni kwamba “hakuna aendaye kulala usingizi akiwa amemkasirikia mwingine,” akasema mwanzilishi wa huo ukaguzi.6 Hata hivyo, miaka zaidi ya 1,900 iliyopita, Biblia ilishauri hivi: “Iweni na hasira ya kisasi, na bado msifanye dhambi; msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Katika nyakati za Biblia siku zilihesabiwa kutoka mshuko wa jua hadi mshuko wa jua. Kwa hiyo, muda mrefu kabla ya wastadi wa kisasa kuchunguza familia, Biblia ilishauri kwa hekima hivi: Suluhisheni upesi mambo yenye kugawanya—kabla ya siku kuisha na nyingine kuanza.
Familia zenye uthabiti na mafanikio “hazianzishi mazungumzo juu ya habari ziwezazo kuongoza kwenye mabishano kabla tu ya kuondoka nyumbani au kabla ya wakati wa kulala,” ndivyo alivyoona huyo mwandikaji. “Tena na tena nilisikia lile fungu la maneno ‘wakati ufaao.’”7 Familia hizo zilirudia bila kukusudia mithali hii ya Biblia iliyorekodiwa miaka zaidi ya 2,700 iliyopita: “Neno linenwalo wakati wa kufaa. Ni kama machungwa [“matofaa ya dhahabu,” NW] katika vyano vya fedha.” (Mithali 15:23; 25:11, italiki ni zetu.) Huenda tashbihi hiyo ikadokeza mapambo ya dhahabu yenye umbo la matofaa yaliyowekwa juu ya sinia za fedha zilizotiwa nakshi—mali nzuri na zenye kuthaminiwa sana katika nyakati za Biblia. Inawasilisha uzuri na thamani ya maneno yanayosemwa kwa wakati unaofaa. Katika hali zenye mkazo, maneno sahihi yasemwayo kwa wakati sahihi ni yenye thamani sana.—Mithali 10:19.
[Sanduku katika ukurasa wa 26]
Mwongozo Wenye Kutumika kwa Mahusiano ya Kibinadamu
“Mwe na hofu [“fadhaikeni,” “NW”] wala msitende dhambi, tafakarini vitandani mwenu na kutulia.” (Zaburi 4:4) Katika visa vilivyo vingi vinavyohusisha maudhiko madogo, huenda likawa jambo la hekima kuzuia maneno yako, hivyo ukiepa kabiliano la kihisia-moyo.
“Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” (Mithali 12:18) Fikiri kabla ya kusema. Maneno yasemwayo bila kufikiri yaweza kuwajeruhi wengine na kuharibu urafiki mbalimbali.
“Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” (Mithali 15:1) Hali ya kujidhibiti inatakwa ili kujibu kwa upole, lakini mara nyingi mwendo huo hulainisha matatizo na huendeleza mahusiano yenye amani.
“Mwanzo wa ugomvi ni kama kutoboa penye maji; basi acheni ugomvi kabla haujafurika.” (Mithali 17:14) Ni jambo la hekima kujiondoa katika hali iwezayo kubadilika upesi kuwa jeuri kabla ya kupatwa na hamaki.
“Usiwe mwepesi wa kuonyesha uchungu wa moyo; kwa kuwa uchungu wa moyo hudumishwa na wapumbavu.” (Mhubiri 7:9, The New English Bible) Mara nyingi hisia-moyo hutangulia matendo. Mtu aliye mwepesi wa kuudhika ni mpumbavu, kwa maana mwendo wake huenda ukaongoza kwenye maneno au matendo ya kutofikiri.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Mashahidi wa Yehova walikuwa miongoni mwa wafungwa wa kwanza katika kambi za mateso
-
-
Kitabu Cha UnabiiKitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Kitabu Cha Unabii
Watu wanapendezwa na wakati ujao. Wanatafuta matabiri yenye kutegemeka kuhusu habari nyingi, kuanzia matabiri ya halihewa hadi ishara za kitakwimu za hali ya kiuchumi. Hata hivyo, watendapo kulingana na matabiri hayo, mara nyingi wanatamauka. Biblia ina matabiri, au unabii mwingi. Unabii huo mbalimbali ni sahihi kadiri gani? Je, ni historia iliyoandikwa kabla ya kutukia? Au ni historia iliyoandikwa baada ya kutukia inayofanywa ionekane tu kuwa unabii?
MWANASIASA Mroma Cato (234-149 K.W.K.) aripotiwa kuwa alisema hivi: “Nashangaa kwamba mtabiri hacheki amwonapo mtabiri mwingine.”1 Kwa kweli, hadi siku hii watu wengi hutilia shaka wabashiri, wanajimu, na watabiri wengine. Mara nyingi maneno ya matabiri yao si dhahiri na yaweza kufasiriwa kwa njia mbalimbali.
Lakini, namna gani unabii mbalimbali wa Biblia? Je, kuna sababu ya kutia shaka? Au kuna msingi wa kuwa na uhakika?
Si Makisio Tu ya Baada ya Kuarifiwa
Watu wenye ujuzi huenda wakajaribu kutumia mielekeo wanayoona ili kukisia kwa usahihi kuhusu wakati ujao, lakini wao si sahihi sikuzote. Kitabu Future Shock, chasema hivi: “Kila jamii haikabili tu mfuatano wa wakati ujao uwezekanao, bali pia inakabili wakati ujao mwingi uwezekanao, na hitilafiano kati ya wakati ujao mbalimbali ambao ungependwa zaidi.” Chaongezea hivi: “Bila shaka, hakuna awezaye ‘kujua’ wakati ujao kikamili kabisa. Twaweza tu kutumia utaratibu fulani na kuongezea makisio yetu na kujaribu kukata maneno juu ya matokeo yawezekanayo zaidi.”2
Lakini waandikaji wa Biblia ‘hawakukata maneno tu juu ya matokeo yawezekanayo zaidi’ kulingana na “makisio” juu ya wakati ujao. Wala matabiri yao hayawezi kupuuzwa kuwa taarifa zisizo dhahiri zinazoruhusu unamna-namna mwingi wa fasiri. Kinyume cha hilo, mwingi wa unabii wao ulisemwa kwa uwazi usio wa kawaida na ulikuwa wa kimahususi isivyo kawaida, mara nyingi ukitabiri kinyume tu cha mambo ambayo huenda yakatarajiwa. Kikiwa kielelezo chukua yale ambayo Biblia ilisema kimbele juu ya jiji la kale la Babiloni.
‘Lingefagiliwa Mbali na Ufagio wa Maangamizi’
Babiloni la kale lilipata kuwa “kito cha falme.” (Isaya 13:19, The New American Bible) Jiji hili kuu lenye kuenea lilikuwa mahali muhimu penye njia ya biashara kutoka Ghuba ya Uajemi hadi Bahari ya Mediterania, likitumika likiwa depo ya biashara ya barani na pia ya baharini kati ya Mashariki na Magharibi.
Kufikia karne ya saba K.W.K., Babiloni lilionekana kuwa jiji kuu lisiloshindika la Milki ya Kibabiloni. Jiji hilo lilitagaa Mto Eufrati, na maji ya huo mto yalitumiwa kufanyiza mtaro mpana, wenye kina na mfumo wa mifereji. Kwa kuongezea, hilo jiji lilikingwa na mfumo mkubwa mno wa kuta maradufu, zilizoegemezwa na minara kadhaa ya ulinzi. Si ajabu kwamba wakaaji walo walihisi kuwa salama.
Hata hivyo, katika karne ya nane K.W.K., kabla ya Babiloni kufikia upeo wa utukufu walo, nabii Isaya alitabiri kwamba Babiloni ‘lingefagiliwa mbali kwa ufagio wa maangamizi.’ (Isaya 13:19; 14:22, 23, BHN) Isaya alifafanua pia njia yenyewe ambayo Babiloni lingeanguka. Washambulizi ‘wangekausha’ mito yalo—chanzo cha ulinzi walo wenye mfano wa mtaro—wakilifanya jiji liwe rahisi kushambulika. Isaya aliandaa hata jina la huyo mshindi—“Koreshi [“Sairasi,” NW],” mfalme mkuu wa Uajemi, ‘ambaye milango ingefunguliwa mbele yake.’—Isaya 44:27–45:2.
Hayo yalikuwa matabiri yenye ujasiri. Lakini je, yalitimia? Historia hutoa jibu.
‘Bila Pigano’
Karne mbili baada ya Isaya kurekodi unabii wake, usiku wa Oktoba 5, 539 K.W.K., majeshi ya Umedi na Uajemi chini ya amri ya Sairasi Mkuu yalikuwa yamepiga kambi karibu na Babiloni. Lakini Wababiloni walikuwa na uhakika. Kulingana na mwanahistoria Mgiriki Herodotus (karne ya tano K.W.K.), walikuwa na maandalizi ya kutosha yaliyokuwa yamewekwa akiba ili kudumu miaka kadhaa.3 Pia walikuwa na Mto Eufrati na kuta za Babiloni zenye uweza za kuwakinga. Hata hivyo, usiku uo huo, kulingana na Masimulizi ya Matukio ya Nabonido, “jeshi la Sairasi liliingia Babiloni bila pigano.”4 Hilo liliwezekanaje?
Herodotus afafanua kwamba ndani ya jiji, watu walikuwa “wakicheza dansi na kujifurahisha kwenye sikukuu.”5 Hata hivyo, huko nje, Sairasi alikuwa amegeuza njia ya maji ya Eufrati. Kiwango cha maji kilipokuwa kikipungua, jeshi lake lilitembea majini katika bonde la mto, maji yakiwa yamefika kwenye mapaja yao. Walitembea hadi kupita zile kuta za juu sana, wakaingia kupitia yale yaliyoitwa na Herodotus “malango yaliyofunguka kuelekea mto,” malango yaliyokuwa yameachwa wazi kizembe.6 (Linganisha Danieli 5:1-4; Yeremia 50:24; 51:31, 32.) Wanahistoria wengine, kutia na Xenophon (karibu 431–karibu 352 K.W.K.), pamoja na mabamba ya kikabari yaliyopatikana na waakiolojia, wanathibitisha anguko la ghafula la Babiloni kwa Sairasi.7
Hivyo unabii wa Isaya juu ya Babiloni ulitimizwa. Au je, yawezekana kwamba huo haukuwa unabii uliotimizwa? Je, yawezekana kwamba huo haukuwa utabiri bali ulikuwa umeandikwa baada ya Babiloni kuanguka? Kwa kweli, swali lilo hilo lingeweza kuulizwa juu ya unabii mwingine mbalimbali wa Biblia.
Historia Inayofanywa Ionekane Tu Kuwa Unabii?
Ikiwa manabii wa Biblia—kutia ndani Isaya—waliandika upya historia ionekane tu kuwa unabii, basi wanaume hao walikuwa wapunjaji werevu tu. Lakini kusudi lao la kufanya ujanja huo lingekuwa nini? Manabii wa kweli walijulisha bila kusita kwamba wasingeweza kuhongwa. (1 Samweli 12:3; Danieli 5:17) Na tumechunguza tayari uthibitisho wenye nguvu wa kwamba waandikaji wa Biblia (wengi wao waliokuwa manabii) walikuwa wanaume wenye kutumainika waliokuwa tayari hata kufunua makosa yao wenyewe yenye kuaibisha. Haionekani yamkini kwamba wanaume wa aina hiyo wangekuwa na mbetuko wa kutenda upunjaji wenye kupangwa kwa uangalifu sana, wakifanya historia ionekane kuwa unabii.
Kuna jambo jingine la kufikiria. Unabii mwingi wa Biblia ulikuwa na mashutumu makali ya hadharani dhidi ya taifa la manabii hao wenyewe, lililotia ndani makuhani na watawala. Kwa kielelezo, Isaya alilaumu hali mbaya ya kiadili ya Waisraeli—watawala na pia watu kwa ujumla —katika siku yake. (Isaya 1:2-10) Manabii wengine walifunua kwa nguvu dhambi za makuhani. (Sefania 3:4; Malaki 2:1-9) Ni vigumu kuelewa ni kwa nini wangebuni tu unabii uliotia ndani mashutumu makali zaidi yawezavyo kuwazika dhidi ya watu wao wenyewe na kwa nini makuhani wangeshirikiana na ujanja huo.
Kwa kuongezea, manabii—ikiwa wangekuwa walaghai tu —wangaliwezaje kutimiza ubuni huo? Kujua kusoma na kuandika kulitiwa moyo katika Israeli. Kutoka umri wa mapema, watoto walifundishwa jinsi ya kusoma na kuandika. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9) Usomaji wa kibinafsi wa Maandiko ulisihiwa sana. (Zaburi 1:2) Katika masinagogi wakati wa Sabato ya kila juma, kulikuwa na usomaji wa hadharani wa Maandiko. (Matendo 15:21) Laonekana kuwa jambo lisilowezekana kwamba taifa zima lililojua kusoma na kuandika, lenye kuyajua Maandiko vizuri, lingaliweza kudanganywa na hila ya aina hiyo.
Isitoshe, unabii wa Isaya unatia ndani zaidi kuliko anguko la Babiloni. Linalotiwa ndani ya unabii huo ni jambo dogo ambalo lisingaliweza hata kidogo kuandikwa baada ya utimizo.
‘Halitakaliwa na Watu Tena Kabisa’
Babiloni lingepatwa na nini baada ya anguko lalo? Isaya alitabiri hivi: “[Halitakaliwa] na watu tena kabisa, wala watu hawatakaa ndani yake tangu kizazi hata kizazi. Mwarabu hatapiga hema yake huko, wala wachungaji hawatalaza makundi yao huko.” (Isaya 13:20) Bila kutia chumvi, huenda ikawa lilionekana kuwa jambo la ajabu kutabiri kwamba jiji lililokuwa mahali pafaapo hivyo lingekuwa lisilokaliwa daima. Je, maneno ya Isaya yangaliweza kuwa yaliandikwa baada ya yeye kuona Babiloni likiwa ukiwa?
Baada ya Sairasi kuliteka, Babiloni lenye kukaliwa—ingawa halikuwa lenye ukuu sana—liliendelea kwa karne kadhaa. Kumbuka kwamba Hatikunjo za Bahari Iliyokufa zinatia ndani nakala ya kitabu kamili cha Isaya iliyopewa tarehe ya karne ya pili K.W.K. Karibu na wakati ambapo hatikunjo hiyo ilikuwa ikinakiliwa, Waparthia walitwaa utawala wa Babiloni. Katika karne ya kwanza W.K., kulikuwa na kijiji kidogo cha Wayahudi katika Babiloni, na mwandikaji wa Biblia Petro alizuru huko. (1 Petro 5:13) Kufikia wakati huo, Hatikunjo ya Bahari Iliyokufa ya Isaya ilikuwa imekamilishwa kwa muda wa karibu karne mbili. Kwa hiyo kufikia karne ya kwanza W.K., bado Babiloni halikuwa ukiwa kikamili, hata hivyo kitabu cha Isaya kilikuwa kimekuwako kwa muda mrefu kabla ya wakati huo.a
Kama ilivyotabiriwa, hatimaye Babiloni lilipata kuwa “magofu.” (Yeremia 51:37) Kulingana na yule msomi Mwebrania Jerome (karne ya nne W.K.), kufikia siku yake Babiloni lilikuwa mahali pa uwindaji ambapo “mahayawani wa kila aina” walizurura.9 Babiloni limeendelea kuwa ukiwa hadi siku hii.
Isaya hakupata kamwe kuishi kuona Babiloni likiwa bila kukaliwa na watu. Lakini magofu ya jiji hilo lililokuwa lenye nguvu wakati mmoja, yaliyo karibu kilometa 80 kusini mwa Baghdad, katika Iraki ya kisasa, yanatoa ushuhuda wa kimya wa utimizo wa maneno yake: “[Halitakaliwa] na watu tena kabisa.” Kurudishwa kokote kwa Babiloni kuwa mahali pa kuvutia watalii huenda kukavutia wageni, lakini “mwana na mjukuu” wa Babiloni wametoweka milele.—Isaya 13:20; 14:22, 23.
Hivyo nabii Isaya hakutoa matabiri yasiyo dhahiri ambayo yangeweza kutumiwa kuhusu tukio lolote lile la wakati ujao. Wala hakuandika upya historia kuifanya ionekane kuwa unabii. Ebu fikiria hili: Kwa nini mlaghai athubutu “kutoa unabii” juu ya jambo ambalo asingaliweza kudhibiti hata kidogo—kwamba Babiloni lenye uweza lisingekaliwa tena kamwe?
Unabii huo juu ya anguko la Babiloni ni kielelezo kimoja tu kutoka katika Biblia.b Watu wengi huona katika utimizo wa unabii wayo mbalimbali wonyesho wa kwamba ni lazima Biblia iwe inatoka kwenye chanzo cha juu zaidi kuliko mwanadamu. Labda ungekubali kwamba kitabu hiki cha unabii chastahili kuchunguzwa, angalau. Jambo moja ni la hakika: Kuna tofauti kubwa kati ya matabiri yasiyo dhahiri au ya ajabu ya watabiri wa siku ya kisasa na ule unabii mbalimbali ulio wazi, wa makini, na wa kimahususi wa Biblia.
[Maelezo ya Chini]
a Kuna uthibitisho thabiti wa kwamba vitabu vya Maandiko ya Kiebrania—kutia ndani Isaya —viliandikwa muda mrefu kabla ya karne ya kwanza W.K. Yule mwanahistoria Josephus (karne ya kwanza W.K.) alionyesha kwamba maandishi yanayokubalika ya Maandiko ya Kiebrania yalikuwa yamethibitishwa muda mrefu kabla ya siku yake.8 Kwa kuongezea, Septuagint ya Kigiriki, tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania katika Kigiriki, ilianzwa katika karne ya tatu K.W.K. na ilikamilishwa kufikia karne ya pili K.W.K.
b Ili kupata mazungumzo zaidi juu ya unabii mbalimbali wa Biblia na mambo ya hakika ya kihistoria yanayoonyesha utimizo wao, tafadhali ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., ukurasa wa 117-133.
[Blabu katika ukurasa wa 28]
Je, waandikaji wa Biblia walikuwa manabii walio sahihi au wapunjaji werevu?
[Picha katika ukurasa wa 29]
Magofu ya Babiloni la kale
-
-
Kitabu Kwa Ajili Yako?Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
-
-
Kitabu Kwa Ajili Yako?
“Hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi,” akataarifu Solomoni miaka ipatayo 3,000 iliyopita. (Mhubiri 12:12) Jambo hilo aliloona lafaa kadiri iyo hiyo leo. Kwa kuongezea vile vitabu vilivyo bora kabisa vya kale, maelfu ya vitabu vipya vinachapwa kila mwaka. Kukiwa na vitabu vingi sana vya kuchagua kati yavyo, kwa nini uisome Biblia?
WATU wengi husoma vitabu ama ili wapate kutumbuizwa ama wapate kuarifiwa, au labda kwa sababu zote mbili. Ndivyo iwezavyo kuwa kuhusu kuisoma Biblia. Yaweza kuandaa usomaji wenye kuchangamsha na hata kutumbuiza. Lakini Biblia si kitabu cha kuchangamsha na kutumbuiza tu. Ni chanzo cha kipekee cha ujuzi.—Mhubiri 12:9, 10.
Biblia hujibu maswali ambayo wanadamu wamefikiria kwa uzito kwa muda mrefu—maswali juu ya wakati wetu uliopita, wakati wetu uliopo, na wakati wetu ujao. Wengi hutaka kujua: Tulitoka wapi? Kusudi la uhai ni nini? Twaweza kupataje furaha maishani? Je, kutakuwa na uhai duniani sikuzote? Wakati wetu ujao una nini kwa ajili yetu?
Kani ya pamoja ya uthibitisho wote uliotolewa hapa yathibitisha kwa wazi kwamba Biblia ni sahihi na ni asilia. Tayari tumechunguza jinsi shauri layo lenye kutumika liwezavyo kutusaidia kuishi maisha yenye maana na yenye furaha leo. Kwa kuwa majibu yayo juu ya wakati uliopo ni yenye kuridhisha, kwa hakika majibu yayo juu ya wakati uliopita na unabii wayo mbalimbali juu ya wakati ujao yanastahili uangalifu makini.
Jinsi ya Kupata Manufaa Kamili Zaidi
Watu wengi wameanza kuisoma Biblia lakini wameacha walipoona sehemu zayo kuwa ngumu kuelewa. Ikiwa umeona hivyo, kuna mambo fulani ambayo huenda yakawa yenye kusaidia.
Watu fulani huanza kwa kusoma masimulizi ya Gospeli ya maisha ya Yesu, ambaye mafundisho yake yenye hekima, kama yale yapatikanayo katika Mahubiri ya Mlimani, hudhihirisha ufahamu makini wa asili ya binadamu na huonyesha jinsi ya kuboresha fungu letu maishani.—Ona Mathayo sura ya 5 hadi 7.
Kwa kuongezea kuisoma Biblia nzima moja kwa moja, njia ya kuisoma kulingana na vichwa mbalimbali yaweza kuwa yenye kuarifu sana. Hiyo yatia ndani kuchanganua yale ambayo Biblia husema juu ya habari hususa. Huenda ukashangaa kujifunza yale ambayo Biblia husema kwa kweli juu ya vichwa kama nafsi, mbingu, dunia, uhai, na kifo, na pia Ufalme wa Mungu—huo ni nini na yale ambayo utatimiza.a Mashahidi wa Yehova wana programu ya kujifunza Biblia kulingana na vichwa mbalimbali, inayotolewa bila malipo. Waweza kuuliza juu yayo kwa kuandikia wachapishaji, ukitumia anwani ihusuyo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa wa 2.
Baada ya kuuchunguza uthibitisho, watu wengi wamefikia mkataa wa kwamba Biblia imetoka kwa Mungu, ambaye Maandiko hutambulisha kuwa “Yehova.” (Zaburi 83:18) Huenda usisadiki kwamba Biblia ina chanzo cha kimungu. Lakini kwa nini usijichunguzie? Tuna uhakika kwamba baada ya hatua ya kujifunza, kutafakari, na labda kujionea mwenyewe thamani yenye kutumika ya hekima yayo ya milele, utakuja kuhisi kwamba Biblia kwa kweli ni kitabu kwa ajili ya watu wote, na zaidi—ni kitabu kwa ajili yako.
-