Yoshua
5 Na ikawa kwamba, mara tu wafalme wote wa Waamori,+ waliokuwa ng’ambo ya Yordani upande wa magharibi, na wafalme wote wa Wakanaani,+ waliokuwa kando ya bahari, waliposikia kwamba Yehova alikuwa amekausha maji ya Yordani mbele ya wana wa Israeli mpaka walipokuwa wamevuka, ndipo mioyo yao ikaanza kuyeyuka,+ wala haikuwamo roho yoyote ya nguvu iliyobaki ndani yao tena kwa sababu ya wana wa Israeli.+
2 Na wakati huo Yehova akamwambia Yoshua: “Jitengenezee visu vya jiwe gumu, uwatahiri+ tena wana wa Israeli mara ya pili.” 3 Basi Yoshua akajitengenezea visu vya jiwe gumu, akawatahiri wana wa Israeli katika Gibeath-haaralothi.+ 4 Na hii ndiyo sababu iliyomfanya Yoshua awatahiri: watu wote waliotoka Misri, waume, wanaume wote wa vita, walikuwa wamekufa+ njiani katika nyika walipokuwa wakitoka Misri. 5 Kwa maana watu wote waliotoka walikuwa wametahiriwa, lakini watu wote waliozaliwa katika nyika njiani walipokuwa wakitoka Misri hawakuwa wamewatahiri. 6 Kwa maana wana wa Israeli walikuwa wametembea miaka 40+ nyikani, mpaka lilipokwisha taifa lote la wale wanaume wa vita waliotoka Misri ambao hawakuisikiliza sauti ya Yehova, ambao Yehova alikuwa amewaapia kwamba hatawaruhusu kamwe waione nchi+ ambayo Yehova alikuwa amewaapia mababu zao kwamba atatupa sisi,+ nchi inayotiririka maziwa na asali.+ 7 Naye akawasimamisha wana wao badala yao.+ Yoshua akawatahiri hao wana, kwa sababu walikuwa hawajatahiriwa, kwa maana hawakuwa wamewatahiri njiani.
8 Kisha ikawa kwamba walipokuwa wamemaliza kutahiri taifa lote, wakaendelea kukaa mahali pao kambini mpaka walipopona.+
9 Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: “Leo nimeondolea mbali aibu ya Misri itoke juu yenu.”+ Basi jina la mahali hapo likaitwa Gilgali+ mpaka leo hii.
10 Na wana wa Israeli wakaendelea kupiga kambi katika Gilgali, nao wakasherehekea pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi huo,+ wakati wa jioni, katika nchi tambarare za jangwa la Yeriko. 11 Nao wakaanza kula mazao ya nchi siku iliyofuata pasaka, keki zisizo na chachu+ na nafaka zilizochomwa, siku ileile. 12 Ndipo mana ikaacha kuanguka siku iliyofuata walipokuwa wamekula mazao ya nchi, wala mana haikuja tena kwa ajili ya wana wa Israeli,+ nao wakaanza kula mazao ya nchi ya Kanaani mwaka huo.+
13 Kisha ikawa kwamba Yoshua alipokuwa karibu na Yeriko, akainua macho yake na kuangalia, na tazama, palikuwa na mwanamume+ aliyesimama mbele yake akiwa na upanga uliochomolewa mkononi mwake.+ Kwa hiyo Yoshua akamwendea na kumwambia: “Je, wewe uko upande wetu au upande wa adui zetu?” 14 Ndipo yeye akasema: “Hapana, lakini mimi—nikiwa mkuu wa jeshi la Yehova nimekuja sasa.”+ Basi Yoshua akaanguka kifudifudi,+ akasujudu na kumwambia: “Bwana wangu anamwambia nini mtumishi wake?” 15 Ndipo mkuu wa jeshi la Yehova akamwambia Yoshua: “Vua viatu vyako kutoka miguuni mwako, kwa sababu mahali ambapo umesimama ni patakatifu.” Yoshua akavua mara moja.+