1 Timotheo
6 Acha wengi kadiri walivyo watumwa chini ya nira wafulize kuwaona wamiliki wao kuwa wenye kustahili heshima kamili, ili jina la Mungu na fundisho lisipate kamwe kusemewa vibaya. 2 Zaidi ya hayo, wale walio na wamiliki wenye kuamini wasiwadharau, kwa sababu wao ni ndugu. Kinyume chake, waache wawe watumwa kwa utayari zaidi, kwa sababu wale wanaopokea manufaa ya utumishi wao mwema ni waamini na wapendwa.
Fuliza kufundisha mambo haya na kutoa mahimizo haya yenye bidii. 3 Ikiwa mtu yeyote afundisha fundisho jingine na hakubaliani na maneno yenye afya, yale ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala na fundisho ambalo lapatana na ujitoaji-kimungu, 4 yeye ametutumuka kwa kiburi, akiwa asiyeelewa kitu chochote, bali akiwa mwenye maradhi ya kiakili juu ya maswali-maswali na mashindano juu ya maneno. Kutoka katika mambo haya huchipuka husuda, zogo, semi zenye kuudhi, shuku zenye uovu, 5 mabishano makali sana juu ya mambo madogo-madogo kwa upande wa watu waliofisidika katika akili na kuporwa ile kweli, wakifikiri kwamba ujitoaji-kimungu ni njia ya kupata faida. 6 Kwa hakika, huo ni njia ya kupata faida kubwa, ujitoaji-kimungu huu pamoja na ujitoshelevu. 7 Kwa maana hatukuleta kitu katika ulimwengu, wala hatuwezi kupeleka kitu chochote nje. 8 Kwa hiyo, tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.
9 Hata hivyo, wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo. 10 Kwa maana kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.
11 Hata hivyo, wewe, Ewe mtu wa Mungu, kimbia mambo hayo. Lakini fuatia uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, tabia-pole. 12 Pigana pigano bora la imani, pata mshiko imara juu ya uhai udumuo milele ambao uliitiwa nawe ukatoa tangazo bora la hadharani mbele ya mashahidi wengi.
13 Machoni pa Mungu, ambaye huhifadhi vitu vyote hai, na pa Kristo Yesu, ambaye akiwa shahidi alifanya tangazo bora la hadharani mbele ya Pontio Pilato, mimi nakupa wewe maagizo 14 kwamba ushike amri katika njia isiyo na doa na isiyolaumika mpaka udhihirisho wa Bwana wetu Yesu Kristo. 15 Mungu aliye mweza pekee na mwenye furaha, ataonyesha udhihirisho huu katika nyakati zao wenyewe zilizowekwa, yeye Mfalme wa wale watawalao wakiwa wafalme na Bwana wa wale watawalao wakiwa mabwana, 16 yeye peke yake aliye na hali ya kutokufa, akaaye katika nuru isiyokaribika, ambaye hakuna hata mmoja kati ya watu ambaye amemwona au aweza kumwona. Kwake kuwe heshima na uweza udumuo milele. Ameni.
17 Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo uliopo wasiwe wenye kunia ya juu, na waweke tumaini lao, si juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu; 18 kufanya mema, kuwa matajiri katika kazi zilizo bora, kuwa wakarimu, tayari kushiriki, 19 wakijiwekea wenyewe kuwa hazina salama msingi bora kwa ajili ya wakati ujao, ili wao wapate kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi.
20 Ewe Timotheo, linda lililowekwa amana kwako, ukigeuka mbali kutoka kwenye semi tupu ambazo huhalifu lililo takatifu na kutoka kwenye mapinganisho yenye kuitwa “ujuzi” isivyo kweli. 21 Kwa kufanya wonyesho wa ujuzi wa namna hiyo wengine wamekengeuka kutoka kwenye imani.
Fadhili isiyostahiliwa na iwe pamoja na nyinyi watu.