-
Marko 2:3-12Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
3 Wakamletea mtu aliyepooza, akiwa amebebwa na watu wanne.+ 4 Lakini kwa sababu ya umati, hawakuweza kumleta moja kwa moja kwa Yesu, basi baada ya kutoboa sehemu ya paa lililokuwa juu ya Yesu, wakamteremsha yule mtu aliyepooza, akiwa amelala juu ya kitanda.* 5 Yesu alipoona imani yao,+ akamwambia yule mtu aliyepooza: “Mwanangu, umesamehewa dhambi zako.”+ 6 Sasa baadhi ya waandishi waliokuwa wameketi hapo wakaanza kuwaza mioyoni mwao:+ 7 “Kwa nini mtu huyu anasema hivyo? Anakufuru. Ni nani anayeweza kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”+ 8 Lakini mara moja Yesu akatambua rohoni mwake kwamba walikuwa wakiwaza hivyo, basi akawaambia: “Kwa nini mnawaza mambo hayo katika mioyo yenu?+ 9 Ni jambo gani rahisi zaidi, kumwambia mtu huyu aliyepooza, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama, uchukue kitanda chako utembee’? 10 Lakini ili mjue kwamba Mwana wa binadamu+ ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani—”+ akamwambia yule mtu aliyepooza: 11 “Ninakuambia, Simama, chukua kitanda chako, uende nyumbani.” 12 Ndipo akasimama, na mara moja akachukua kitanda chake akatembea mbele yao wote na kwenda nje. Basi, wote wakashangaa, na kumtukuza Mungu wakisema: “Hatujawahi kamwe kuona jambo kama hilo.”+
-
-
Luka 5:18-26Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
18 Na tazama! kulikuwa na wanaume waliombeba kwenye kitanda* mtu aliyepooza, nao wakajaribu kumwingiza ndani na kumweka mbele ya Yesu.+ 19 Waliposhindwa kumwingiza kwa sababu ya umati, wakapanda kwenye paa, wakaondoa vigae na kumshusha akiwa kwenye kitanda kati ya wale waliokuwa mbele ya Yesu. 20 Alipoona imani yao, akamwambia yule mtu: “Ewe mtu, umesamehewa dhambi zako.”+ 21 Ndipo waandishi na Mafarisayo wakaanza kujadiliana: “Huyu ni nani anayesema makufuru? Ni nani anayeweza kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”+ 22 Lakini Yesu, akifahamu mawazo yao akawauliza: “Mnawaza nini katika mioyo yenu? 23 Ni jambo gani rahisi zaidi kusema, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama utembee’? 24 Lakini ili mjue kwamba Mwana wa binadamu ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani—” akamwambia yule mtu aliyepooza: “Ninakuambia, Simama, uchukue kitanda chako, uende nyumbani.”+ 25 Ndipo akasimama mbele yao, akachukua kitanda chake, akaenda nyumbani, akimtukuza Mungu. 26 Kisha wote wakashangaa wakaanza kumtukuza Mungu, wakastaajabu na kusema: “Leo tumeona mambo ya ajabu!”
-