Mwanzo
40 Sasa ikawa kwamba baada ya mambo hayo, mnyweshaji+ wa mfalme wa Misri na mwokaji walimtendea dhambi bwana wao, mfalme wa Misri.+ 2 Farao akakasirishwa na hao watumishi wake wawili,+ mkuu wa wanyweshaji na mkuu wa waokaji.+ 3 Basi akawatia katika jela ya nyumba ya mkuu wa walinzi,+ katika ile nyumba ya gereza,+ mahali ambapo Yosefu alikuwa mfungwa. 4 Kisha mkuu wa walinzi akampa Yosefu mgawo awe nao ili awahudumie;+ nao wakakaa jela siku kadhaa.
5 Na wote wawili wakaota ndoto,+ kila mmoja ndoto yake katika huo usiku mmoja,+ kila mmoja ndoto yake yenye tafsiri yake,+ mnyweshaji na mwokaji wa mfalme wa Misri waliokuwa wafungwa katika nyumba ya gereza.+ 6 Yosefu alipowajia asubuhi na kuwaona, tazama, walionekana wana huzuni.+ 7 Naye akawauliza hao maofisa wa Farao waliokuwa naye katika jela ya nyumba ya bwana wake, akisema: “Kwa nini nyuso zenu zina huzuni leo?”+ 8 Wakamjibu: “Tumeota ndoto, wala hatuna mtafsiri.” Basi Yosefu akawaambia: “Je, tafsiri si za Mungu?+ Tafadhali, nisimulieni.”
9 Naye mkuu wa wanyweshaji akamsimulia Yosefu ndoto yake akisema: “Katika ndoto yangu, kulikuwako mzabibu mbele yangu. 10 Na kwenye mzabibu kulikuwako matawi matatu, na ulionekana unaota machipukizi.+ Ukachanua maua. Vishada vyake vikaivisha zabibu zake. 11 Kikombe cha Farao kilikuwa mkononi mwangu, nami nikachukua zabibu na kuziminya ndani ya kikombe cha Farao.+ Halafu nikakiweka kikombe mkononi mwa Farao.”+ 12 Kisha Yosefu akamwambia: “Hii ndiyo tafsiri yake.+ Yale matawi matatu ni siku tatu. 13 Baada ya siku tatu Farao atakiinua kichwa chako naye atakurudisha katika cheo chako;+ nawe bila shaka utampa Farao kikombe mkononi mwake, kulingana na desturi ya zamani ulipokuwa mnyweshaji wake.+ 14 Hata hivyo, unikumbuke mara tu mambo yatakapokuendea vema,+ tafadhali, usikose kunitendea fadhili zenye upendo na kunitaja kwa Farao,+ nawe unitoe nje ya nyumba hii. 15 Kwa maana kwa kweli nilitekwa nyara kutoka katika nchi ya Waebrania;+ na hapa pia sijafanya jambo lolote kamwe hata wanitie katika tundu hili la gereza.”+
16 Mkuu wa waokaji alipoona kwamba Yosefu ametafsiri jambo jema, yeye naye akamwambia Yosefu: “Mimi pia nilikuwa katika ndoto yangu, na tazama, vikapu vitatu vya mkate mweupe vilikuwa kichwani pangu. 17 Ndani ya kikapu cha juu kabisa mlikuwemo namna zote za vyakula vya Farao,+ vitu vya mwokaji, pia kulikuwako ndege+ wakizila katika kikapu juu ya kichwa changu.” 18 Kisha Yosefu akajibu na kusema: “Hii ndiyo tafsiri yake:+ Vile vikapu vitatu ni siku tatu. 19 Baada ya siku tatu tokea sasa Farao atakiinua kichwa chako na kukiondoa juu yako naye atakutundika juu ya mti;+ nao ndege wataila nyama yako.”+
20 Basi siku ya tatu ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Farao,+ naye akawafanyia karamu watumishi wake wote na kukiinua kichwa cha mkuu wa wanyweshaji na kichwa cha mkuu wa waokaji katikati ya watumishi wake.+ 21 Akamrudisha mkuu wa wanyweshaji kwenye cheo chake cha kunywesha,+ naye akaendelea kumpa Farao kikombe mkononi mwake. 22 Lakini akamtundika mkuu wa waokaji,+ kama vile Yosefu alivyokuwa amewatafsiria.+ 23 Hata hivyo, mkuu wa wanyweshaji hakumkumbuka Yosefu, naye akaendelea kumsahau.+