Waroma
4 Kwa kuwa iko hivyo, tutasema nini juu ya Abrahamu babu+ yetu kulingana na mwili? 2 Kwa mfano, kama Abrahamu angetangazwa kuwa mwadilifu kwa sababu ya matendo,+ angekuwa na sababu ya kujisifu; lakini si mbele za Mungu. 3 Kwa maana andiko linasema nini? “Abrahamu alionyesha imani katika Yehova, na hilo likahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu.”+ 4 Basi kwa mtu anayefanya kazi,+ malipo yanahesabiwa kuwa ni deni,+ wala si kuwa ni fadhili zisizostahiliwa.+ 5 Kwa upande mwingine, kwa mtu asiyefanya kazi bali anayeweka imani+ katika yeye anayemtangaza kuwa mwadilifu yule asiyemwogopa Mungu, imani yake inahesabiwa kuwa ni uadilifu.+ 6 Kama vile Daudi pia anavyosema juu ya furaha ya mtu ambaye Mungu humhesabia kuwa ni uadilifu bila matendo: 7 “Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa+ na ambao dhambi zao zimefunikwa;+ 8 mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hatahesabu dhambi yake kamwe.”+
9 Basi, je, furaha hiyo huja juu ya watu waliotahiriwa au pia juu ya watu wasiotahiriwa?+ Kwa maana tunasema: “Imani yake ilihesabiwa kwa Abrahamu kuwa ni uadilifu.”+ 10 Basi, ilihesabiwa chini ya hali gani? Alipokuwa katika kutahiriwa au katika kutotahiriwa?+ Si katika kutahiriwa, bali katika kutotahiriwa. 11 Naye alipokea ishara,+ yaani, kutahiriwa, kuwa muhuri wa uadilifu kwa imani aliyokuwa nayo alipokuwa katika hali yake ya kutotahiriwa, ili yeye awe baba+ ya wale wote walio na imani+ wakiwa katika kutotahiriwa, kusudi wahesabiwe uadilifu; 12 na baba ya uzao uliotahiriwa, si kwa wale tu wanaoshikamana na kutahiriwa, bali pia kwa wale wanaotembea kwa utaratibu katika hatua za imani hiyo wakiwa katika hali ya kutotahiriwa ambayo baba+ yetu Abrahamu alikuwa nayo.
13 Kwa maana ahadi+ ile kwamba awe mrithi wa ulimwengu hakuipata Abrahamu au uzao wake kupitia sheria, bali ilikuwa kupitia uadilifu kwa njia ya imani.+ 14 Kwa maana ikiwa wale ambao hushikamana sana na sheria ni warithi, imani imefanywa kuwa isiyofaa kitu na ahadi imefutwa.+ 15 Kwa kweli Sheria hutokeza ghadhabu,+ lakini mahali ambapo hapana sheria, hapana pia kosa lolote.+
16 Kwa hiyo ilitokana na imani, ili iwe kulingana na fadhili zisizostahiliwa,+ kusudi ahadi+ iwe hakika kwa uzao+ wake wote, si kwa ule tu unaoshikamana na Sheria, bali pia kwa ule unaoshikamana na imani ya Abrahamu. (Yeye ndiye baba+ yetu sote, 17 kama ilivyoandikwa: “Nimekuweka wewe kuwa baba ya mataifa mengi.”)+ Hili lilikuwa machoni pa Yule ambaye katika yeye alikuwa na imani, ndiyo, machoni pa Mungu, anayewafanya wafu kuwa hai+ na kuyaita mambo yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako.+ 18 Ijapokuwa alikuwa amepita hali ya kuwa na tumaini,+ bado kwa kutegemea tumaini alikuwa na imani, ili awe baba ya mataifa+ mengi kwa kupatana na yale yaliyokuwa yamesemwa: “Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.”+ 19 Na, ijapokuwa hakudhoofika katika imani, alifikiria juu ya mwili wake mwenyewe, ukiwa sasa tayari umekufa,+ kwa kuwa alikuwa mwenye umri wa karibu miaka mia moja,+ pia hali ya kufa ya tumbo la uzazi la Sara.+ 20 Lakini kwa sababu ya ahadi+ ya Mungu yeye hakusitasita kwa ukosefu wa imani,+ bali akawa mwenye nguvu kwa imani+ yake, akimpa Mungu utukufu 21 na akiwa amesadikishwa kikamili kwamba lile alilokuwa ameahidi alikuwa na uwezo pia wa kulifanya.+ 22 Kwa sababu hiyo “ikahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu.”+
23 Hata hivyo, haikuandikwa kwa ajili yake tu+ kwamba “ilihesabiwa+ kwake,” 24 bali pia kwa ajili yetu ambao itahesabiwa, kwa sababu tunamwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu kutoka kwa wafu.+ 25 Yeye alitolewa kwa ajili ya makosa+ yetu na kufufuliwa kwa ajili ya kututangaza sisi kuwa waadilifu.+