1 Samweli
5 Basi Wafilisti wakalichukua lile sanduku+ la Mungu wa kweli, wakalibeba kutoka Ebenezeri mpaka Ashdodi.+ 2 Na Wafilisti wakalichukua sanduku la Mungu wa kweli, wakaliingiza ndani ya nyumba ya Dagoni na kulisimamisha kando ya Dagoni.+ 3 Kisha Waashdodi wakaamka mapema kesho yake, na tazama, Dagoni alikuwa ameanguka kifudifudi mbele ya sanduku la Yehova.+ Basi wakamchukua Dagoni na kumrudisha mahali pake.+ 4 Walipoamka asubuhi na mapema siku iliyofuata, tazama, Dagoni alikuwa ameanguka kifudifudi mbele ya sanduku la Yehova, huku kichwa cha Dagoni na mikono yake miwili ikiwa imekatwa, mpaka kwenye kizingiti.+ Ni sehemu yenye umbo la samaki peke yake ndiyo iliyoachwa ikiwa juu yake. 5 Ndiyo sababu makuhani wa Dagoni na wote wanaoingia katika nyumba ya Dagoni hawakikanyagi kizingiti cha Dagoni katika Ashdodi mpaka leo hii.
6 Na mkono wa Yehova+ ukawa mzito juu ya Waashdodi, naye akaanza kusababisha wasiwasi mkubwa na kuwapiga kwa bawasiri,+ yaani, Ashdodi na maeneo yake. 7 Na watu wa Ashdodi wakaona kwamba iko hivyo, ndipo wakasema: “Msiache sanduku la Mungu wa Israeli likae pamoja nasi, kwa sababu mkono wake umekuwa mzito juu yetu na juu ya Dagoni mungu wetu.”+ 8 Basi wakawatuma watu wawakusanye kwao wakuu wote wa muungano wa Wafilisti, wakasema: “Tutalifanyia nini sanduku la Mungu wa Israeli?” Mwishowe wakasema: “Acheni sanduku la Mungu wa Israeli lizunguke kwenda Gathi.”+ Basi wakalibeba sanduku la Mungu wa Israeli kwa kuzunguka mpaka huko.
9 Na ikawa kwamba walipokuwa wamezunguka kulileta huko, mkono wa Yehova+ ukaja kuwa juu ya jiji hilo na kuleta mvurugo mkubwa sana, naye akaanza kuwapiga watu wa jiji, kuanzia mdogo hata mkubwa, na bawasiri+ zikaanza kulipuka juu yao. 10 Basi wakalipeleka sanduku la Mungu wa kweli mpaka Ekroni.+ Na ikawa kwamba mara tu sanduku la Mungu wa kweli lilipofika Ekroni, Waekroni wakaanza kulia, wakisema: “Wamelileta sanduku la Mungu wa Israeli kwangu kwa kuzunguka ili waniue mimi na watu wangu!”+ 11 Kwa hiyo wakatuma watu wakawakusanya wakuu wote wa muungano wa Wafilisti na kusema: “Ondoeni sanduku la Mungu wa Israeli, lirudi mahali pake, ili lisiniue mimi na watu wangu.” Kwa maana mvurugo wa kuleta kifo ulikuwa umetokea katika jiji zima;+ mkono wa Mungu wa kweli ulikuwa umekuwa mzito sana huko,+ 12 na watu ambao hawakufa walikuwa wamepigwa na bawasiri.+ Na kilio+ cha jiji hilo cha kuomba msaada kikaendelea kupanda mpaka mbinguni.