1 Samweli
4 Na neno la Samweli likaendelea kuwajia Israeli wote.
Ndipo Israeli wakatoka ili kukutana na Wafilisti katika pigano; nao wakapiga kambi kando ya Ebenezeri,+ Wafilisti nao wakapiga kambi katika Afeki.+ 2 Na Wafilisti wakajipanga+ ili kukutana na Israeli, na pigano hilo likaenda vibaya, hivi kwamba Israeli wakashindwa mbele ya Wafilisti,+ ambao waliwapiga na kuwaua karibu watu elfu nne katika pigano uwanjani. 3 Watu walipokuja kambini, wanaume wazee wa Israeli wakaanza kusema: “Kwa nini Yehova alitushinda leo mbele ya Wafilisti?+ Na tujichukulie kutoka Shilo sanduku la agano la Yehova,+ ili lije katikati yetu na kutuokoa kutoka mkononi mwa adui zetu.” 4 Basi watu wakatuma ujumbe huko Shilo na kuchukua kutoka huko sanduku la agano la Yehova wa majeshi, anayeketi juu ya makerubi.+ Na wale wana wawili wa Eli walikuwa hapo pamoja na sanduku la agano la Mungu wa kweli, yaani, Hofni na Finehasi.+
5 Na ikawa kwamba mara sanduku la agano la Yehova lilipoingia katika kambi, Waisraeli wote wakaanza kupiga kelele kubwa,+ hata dunia ikavurugika. 6 Nao Wafilisti pia wakasikia sauti ya kelele hizo, wakaanza kusema: “Hii sauti ya hizi kelele kubwa+ katika kambi ya Waebrania inamaanisha nini?” Mwishowe wakaja kujua kwamba sanduku la Yehova lilikuwa limekuja katika kambi. 7 Nao Wafilisti wakaogopa, kwa sababu walisema: “Mungu ameingia kambini!”+ Basi wakasema: “Ole wetu, kwa maana jambo kama hili halijatokea kamwe tangu hapo mwanzoni! 8 Ole wetu! Ni nani atakayetuokoa kutoka katika mkono wa huyu Mungu mtukufu? Huyu ndiye Mungu aliyepiga Misri kwa kila namna ya mauaji katika nyika.+ 9 Mjionyeshe kuwa hodari na kujiendesha kama wanaume, enyi Wafilisti, ili msije kuwatumikia Waebrania kama vile wao walivyowatumikia ninyi;+ mjiendeshe kama wanaume, mkapigane!” 10 Basi Wafilisti wakapigana, na Israeli wakashindwa,+ nao wakakimbia kila mmoja kwenda katika hema lake;+ na mauaji hayo yakawa makubwa sana,+ hivi kwamba katika Israeli wakaanguka watu 30,000 wenye kwenda kwa miguu.+ 11 Nalo sanduku la Mungu likatekwa,+ na wale wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi, wakafa.+
12 Na mtu fulani wa Benyamini akakimbia kutoka katika uwanja wa mapigano, akafika Shilo siku hiyo huku mavazi yake yakiwa yameraruliwa,+ na mavumbi yakiwa juu ya kichwa chake.+ 13 Alipofika, Eli alikuwa amekalia kiti kando ya barabara, akitazama, kwa kuwa moyo wake ulikuwa ukitetemeka kwa sababu ya lile sanduku la Mungu wa kweli.+ Na yule mtu akaenda kutoa habari jijini, na jiji lote likaanza kulia. 14 Na Eli akasikia sauti za vilio hivyo. Basi akasema: “Sauti ya machafuko haya inamaanisha nini?”+ Yule mtu akafanya haraka ili aingie na kumpa Eli habari. 15 (Basi Eli alikuwa na umri wa miaka 98, na macho yake yalikuwa yameganda, asiweze kuona.)+ 16 Na yule mtu akamwambia Eli: “Mimi ndiye ninayetoka katika uwanja wa mapigano, nami—nimekimbia leo kutoka katika uwanja wa mapigano.” Naye akasema: “Ni jambo gani limetendeka, mwanangu?” 17 Basi yule mleta-habari akajibu na kusema: “Israeli wamekimbia mbele ya Wafilisti, na pia watu wameshindwa vibaya sana;+ hata wana wako wawili wamekufa pia—Hofni na Finehasi+—nalo sanduku la Mungu wa kweli limetekwa.”+
18 Na ikawa kwamba mara alipotaja sanduku la Mungu wa kweli, akaanguka nyuma kutoka kwenye kiti kando ya lango, na shingo yake ikavunjika, akafa, kwa sababu mwanamume huyo alikuwa mzee tena mzito; naye alikuwa amehukumu Israeli kwa miaka 40. 19 Na binti-mkwe wake, mke wa Finehasi, alikuwa na mimba karibu na kuzaa, naye akasikia habari kwamba sanduku la Mungu wa kweli limetekwa na kwamba baba-mkwe wake na mume wake wamekufa. Kwa hiyo akainama, akaanza kuzaa, kwa sababu uchungu wake ulimjia bila kutazamiwa.+ 20 Na karibu na wakati wa kifo chake, wanawake waliokuwa wamesimama kando yake wakaanza kusema: “Usiogope, kwa maana umezaa mwana.”+ Naye hakujibu wala kuweka moyo wake juu ya maneno hayo. 21 Lakini akamwita mvulana huyo jina Ikabodi,+ akisema: “Utukufu umeondoka katika Israeli kwenda uhamishoni,”+ hayo alisema kuhusu sanduku la Mungu wa kweli lililotekwa na kuhusu baba-mkwe wake na mume wake.+ 22 Basi akasema: “Utukufu umeondoka katika Israeli kwenda uhamishoni,+ kwa sababu sanduku la Mungu wa kweli limetekwa.”+