-
“Bwana Hupenda Haki”Mkaribie Yehova
-
-
Sehemu ya 2
“Bwana Hupenda Haki”
Mungu hulaumiwa isivyofaa kwa sababu ya ukosefu wa haki unaoenea ulimwenguni leo. Lakini, Biblia hufundisha ukweli unaotia moyo, yaani, “BWANA hupenda haki.” (Zaburi 37:28) Katika sehemu hii tutajifunza jinsi ambavyo ametenda kupatana na maneno hayo, na kuwapa wanadamu wote tumaini.
-
-
“Njia Zake Zote Ni Haki”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 11
“Njia Zake Zote Ni Haki”
1, 2. (a) Yosefu alikumbwa na ukosefu upi mkubwa wa haki? (b) Yehova alikomeshaje ukosefu huo wa haki?
MWANAMUME fulani kijana mwenye sura nzuri alitendewa isivyo haki kabisa, hakuwa amefanya uhalifu wowote, lakini alitiwa gerezani kwa mashtaka ya uwongo ya kujaribu kumbaka mwanamke. Alitendewa isivyo haki pindi nyingine pia. Miaka mingi mapema, kijana huyo aitwaye Yosefu, akiwa na umri wa miaka 17, alisalitiwa na ndugu zake ambao nusura wamwue. Aliuzwa utumwani katika nchi ya kigeni. Akiwa huko alikataa kutongozwa na mke wa bwana wake. Mwanamke huyo alimsingizia Yosefu kwa mashtaka ya uwongo, ndipo Yosefu akatiwa gerezani. Kwa kusikitisha, ilionekana kwamba hakukuwa na mtu yeyote wa kumtetea Yosefu.
Yosefu aliteseka isivyo haki “gerezani”
2 Hata hivyo, Mungu ambaye ‘anapenda uadilifu na haki’ alikuwa akitazama. (Zaburi 33:5, BHN) Yehova alichukua hatua ya kukomesha ukosefu huo wa haki, aliingilia mambo na mwishowe Yosefu akaachiliwa. Isitoshe, Yosefu—aliyekuwa ametiwa “gerezani”—hatimaye alipewa cheo cha juu sana na heshima ya pekee. (Mwanzo 40:15; 41:41-43; Zaburi 105:17, 18) Mwishowe, mashtaka hayo ya uwongo yalifutiliwa mbali na Yosefu akatumia cheo chake cha juu kuendeleza kusudi la Mungu.—Mwanzo 45:5-8.
3. Kwa nini haishangazi kwamba sote hutamani kutendewa kwa haki?
3 Simulizi hilo linatugusa moyo, sivyo? Sote tumepata kutendewa isivyo haki au kuona mwingine akitendewa isivyo haki. Bila shaka, sote hutamani kutendewa kwa haki, bila uonevu. Hilo halishangazi, kwa kuwa Yehova alituumba tukiwa na sifa kama zake, na haki ni mojawapo ya sifa zake kuu. (Mwanzo 1:27) Ili kumjua Yehova vyema, tunahitaji kuelewa sifa yake ya haki. Ndipo tutakapothamini hata zaidi matendo yake ya ajabu na kuchochewa kumkaribia zaidi.
Haki Ni Nini?
4. Kwa kawaida wanadamu huelewaje haki?
4 Kwa kawaida, wanadamu huelewa haki kuwa utekelezaji wa sheria bila upendeleo. Kitabu Right and Reason—Ethics in Theory and Practice chasema kwamba ‘haki inahusiana na sheria, wajibu, haki za watu, na madaraka, nayo hutekelezwa bila kupendelea na kwa yule anayestahili.’ Hata hivyo, Yehova hatekelezi haki kwa kushikilia tu sheria bila kujali ili kutimiza tu wajibu.
5, 6. (a) Maneno ya lugha ya awali yanayotafsiriwa “haki” yanamaanisha nini? (b) Mungu ni mwenye haki katika maana gani?
5 Tunaweza kuelewa kwa undani haki ya Yehova kwa kuchunguza maneno ya lugha za awali yaliyotumiwa katika Biblia. Katika Maandiko ya Kiebrania, maneno matatu muhimu yanatumiwa. Neno ambalo mara nyingi hutafsiriwa “haki” laweza pia kumaanisha “yaliyo sawa.” (Mwanzo 18:25, BHN) Maneno mawili yanayosalia hutafsiriwa kwa kawaida kuwa “uadilifu.” Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno linalotafsiriwa “uadilifu” linafafanuliwa kuwa “sifa ya kuwa sawa au mwenye haki.” Hivyo basi, hakuna tofauti kati ya uadilifu na haki.—Amosi 5:24, BHN.
6 Basi, Biblia inaposema kwamba Mungu ni mwenye haki, inamaanisha kwamba sikuzote yeye hutenda yaliyo sawa bila kupendelea, na bila ubaguzi. (Waroma 2:11) Kwa kweli, Mungu hawezi kamwe kutenda isivyo haki. Elihu aliyekuwa mwaminifu alisema hivi: “Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu; wala Mwenyezi kufanya uovu.” (Ayubu 34:10) Ni kweli kwamba Yehova hawezi kamwe “kutenda udhalimu.” Kwa nini? Kwa sababu mbili muhimu.
7, 8. (a) Kwa nini Yehova hawezi kutenda isivyo haki? (b) Ni nini kinachomchochea Yehova atende kwa uadilifu, au kwa haki?
7 Kwanza, yeye ni mtakatifu. Kama tulivyoona kwenye Sura ya 3, Yehova ni mtakatifu na mwadilifu kabisa. Kwa hiyo, hawezi kutenda uovu au kutenda isivyo haki. Fikiria maana yake. Tunasadiki kabisa kwamba Baba yetu wa mbinguni hawezi kamwe kuwatesa watoto wake kwa sababu yeye ni mtakatifu. Yesu alisadiki vivyo hivyo. Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, alisali hivi: “Baba Mtakatifu, walinde [wanafunzi] kwa sababu ya jina lako mwenyewe.” (Yohana 17:11) Katika Maandiko, usemi “Baba Mtakatifu” humhusu Yehova peke yake. Usemi huo unafaa kwa sababu hakuna baba yeyote wa kibinadamu aliye mtakatifu kama Yehova. Yesu aliamini kabisa kwamba wanafunzi wake wangelindwa na Baba yake, ambaye ni mtakatifu na asiye na dhambi yoyote.—Mathayo 23:9.
8 Pili, upendo usio wa ubinafsi ni sifa kuu ya utu wa Mungu. Upendo huo humchochea kuwatendea wengine kwa uadilifu au haki. Lakini ukosefu mwingi wa haki—kutia ndani ukabila, ubaguzi wa rangi, na kupendelea—mara nyingi husababishwa na pupa na ubinafsi, mambo ambayo ni kinyume cha upendo. Biblia inatuhakikishia hivi kumhusu Mungu huyo mwenye upendo: “BWANA ndiye mwenye haki, apenda matendo ya haki.” (Zaburi 11:7) Yehova asema hivi kujihusu: “Mimi, BWANA, naipenda hukumu ya haki.” (Isaya 61:8) Bila shaka inatia moyo kujua kwamba Mungu wetu anapenda kutenda yaliyo sawa, au yaliyo haki.—Yeremia 9:24.
Rehema na Haki Kamilifu ya Yehova
9-11. (a) Kuna uhusiano gani kati ya haki ya Yehova na rehema yake? (b)Yehova anaonyeshaje haki na rehema anaposhughulika na wanadamu wenye dhambi?
9 Haki ya Yehova, kama sifa nyinginezo za utu wake usio na kifani, ni kamilifu, haijapungukiwa kwa vyovyote. Musa alimtukuza Yehova kwa kuandika hivi: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:3, 4) Yehova hutenda kwa haki kamilifu—yeye si mpole mno wala si mkali mno.
10 Haki ya Yehova inahusiana sana na rehema yake. Zaburi 116:5 yasema: “BWANA ni mwenye neema na haki, naam, Mungu wetu ni mwenye rehema.” Ndiyo, Yehova ni mwenye haki na mwenye rehema. Sifa hizo mbili hazipingani. Haki ya Yehova haiwezi kupita kiasi, kwa hivyo haonyeshi rehema ili kusawazisha haki yake. Badala yake, mara nyingi yeye huonyesha sifa hizo pamoja. Ona mfano ufuatao.
11 Wanadamu wote wamerithi dhambi na hivyo wanastahili kupata mshahara wa dhambi, yaani, kifo. (Waroma 5:12) Lakini Yehova hafurahii watenda-dhambi wakifa. Yeye ni ‘Mungu, aliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi.’ (Nehemia 9:17) Hata hivyo, kwa kuwa yeye ni mtakatifu, hawezi kupuuza tu uovu. Basi, angewezaje kuwaonyesha rehema wanadamu ambao wamerithi dhambi? Jibu linapatikana katika mojawapo ya kweli muhimu zinazopatikana katika Neno la Mungu: mpango wa Yehova wa kuwaokoa wanadamu kupitia fidia. Katika Sura ya 14 tutajifunza mengi zaidi kuhusu mpango huo wa upendo. Mpango huo unaonyesha haki na rehema ya pekee sana. Kupitia mpango huo, Yehova anaweza kuwaonyesha watenda-dhambi wanaotubu rehema yenye fadhili huku akidumisha kanuni zake za haki kamilifu.—Waroma 3:21-26.
Haki ya Yehova Inachangamsha Moyo
12, 13. (a) Kwa nini haki ya Yehova inatuvuta kwake? (b) Daudi alifikia mkataa gani kuhusu haki ya Yehova, na hilo linawezaje kututia moyo?
12 Haki ya Yehova si sifa inayochukiza, bali ni sifa ya kupendeza inayotuvuta kwake. Biblia inaeleza waziwazi kwamba haki au uadilifu wa Yehova unaambatana na huruma. Hebu tuchunguze baadhi ya njia za Yehova za haki zinazochangamsha moyo.
13 Haki kamilifu ya Yehova humchochea kuonyesha uaminifu na ushikamanifu kwa watumishi wake. Mtunga-zaburi Daudi alipata kuelewa na kuthamini wonyesho huo wa haki ya Yehova maishani mwake. Daudi alifikia mkataa gani kutokana na mambo yaliyompata na yale aliyojifunza kuhusu njia za Yehova za kufanya mambo? Alitangaza hivi: “BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake. Wao hulindwa milele.” (Zaburi 37:28) Ahadi hiyo inatia moyo kama nini! Mungu wetu hatawaacha kamwe wale walio waaminifu kwake. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatutunza kwa upendo na hatatuacha kamwe. Jambo hilo ni hakika kwa sababu yeye ni mwenye haki!—Mithali 2:7, 8.
14. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli inaonyeshaje kwamba anawajali wanaotaabika?
14 Mungu huzingatia mahitaji ya wale wanaotaabika kwa sababu yeye ni mwenye haki. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli inaonyesha kwamba anawajali wanaotaabika. Kwa mfano, Sheria ilitaja mipango ya pekee ya kuhakikisha kwamba mayatima na wajane walitunzwa. (Kumbukumbu la Torati 24:17-21) Huku akitambua magumu ambayo yangekumba familia hizo, Yehova aliwajali akiwa Hakimu na Mlinzi wao, ambaye ‘anamfanyia yatima na mjane hukumu ya haki.’ (Kumbukumbu la Torati 10:18; Zaburi 68:5) Yehova aliwaonya Waisraeli kwamba endapo wangewatesa wanawake na watoto hao wasio na msaidizi, angesikia kilio chao pasina shaka yoyote. Alisema: “Hasira yangu itawaka moto.” (Kutoka 22:22-24) Ijapokuwa hasira si mojawapo ya sifa kuu za Yehova, hasira yake adilifu huwaka anapoona watu wa hali ya chini na wanyonge wakionewa kimakusudi.—Zaburi 103:6.
15, 16. Kuna uthibitisho gani wa pekee unaoonyesha kwamba Yehova hana upendeleo?
15 Yehova pia anatuhakikishia kwamba ‘hapendelei nyuso za watu, wala hakubali rushwa.’ (Kumbukumbu la Torati 10:17) Yehova si kama wanadamu wengi mashuhuri na wenye mamlaka ambao huangalia utajiri au sura ya mtu. Hana ubaguzi wala upendeleo wowote. Fikiria uthibitisho huu wa pekee ambao unaonyesha kwamba Yehova hana upendeleo. Hakuwapa watu wachache tu wenye elimu nafasi ya kuwa waabudu wake wa kweli wenye tumaini la kuishi milele. Badala yake, “katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Watu wote wanaweza kuwa na tumaini hilo zuri ajabu bila kujali wadhifa wao katika jamii, rangi yao, au nchi wanamoishi. Je, huo si uthibitisho bora kabisa wa haki ya kweli?
16 Tunastahili kufikiria na kuheshimu njia nyingine muhimu ambayo Yehova anaonyesha haki yake kamilifu: jinsi anavyoshughulika na wale wanaovunja kanuni zake za uadilifu.
Huwaadhibu Wenye Hatia
17. Eleza kwa nini maovu yaliyo ulimwenguni hayaonyeshi kwamba Yehova hatendi haki.
17 Huenda wengine wakauliza: ‘Kama Yehova hapuuzi uovu, kwa nini ufisadi na ukosefu wa haki unaosababisha kuteseka umeenea ulimwenguni leo?’ Maovu hayo hayaonyeshi kwa vyovyote kwamba Yehova hatendi haki. Ukosefu wa haki uliojaa katika ulimwengu huu mwovu umesababishwa na dhambi ambayo wanadamu wamerithi kutoka kwa Adamu. Ukosefu wa haki umeenea ulimwenguni kwa sababu wanadamu wasiokamilika wameamua kufuata njia zao wenyewe zenye dhambi. Lakini utakomeshwa hivi karibuni.—Kumbukumbu la Torati 32:5.
18, 19. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hatavumilia milele wale wanaovunja kimakusudi sheria zake adilifu?
18 Ijapokuwa Yehova huwarehemu kabisa wale wanaomkaribia kwa unyofu, hatavumilia milele hali inayoletea jina lake takatifu lawama. (Zaburi 74:10, 22, 23) Mungu mwenye haki hawezi kudhihakiwa; hawezi kuwalinda wale wanaotenda dhambi kimakusudi wasipate adhabu kali wanayostahili kwa sababu ya mwenendo wao. Yehova ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; . . . wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” (Kutoka 34:6, 7) Kwa kupatana na maneno hayo, nyakati nyingine imembidi Yehova kuwaadhibu wale wanaovunja kimakusudi sheria zake adilifu.
19 Kwa mfano, fikiria jinsi Mungu alivyoshughulika na Israeli la kale. Hata baada ya kumiliki Nchi ya Ahadi, Waisraeli waliasi tena na tena. Yehova hakuwatupilia mbali mara moja licha ya kwamba matendo yao maovu ‘yalimhuzunisha.’ (Zaburi 78:38-41) Badala yake, kwa rehema aliwapa nafasi ya kubadili mwenendo wao. Aliwasihi hivi: “Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?” (Ezekieli 33:11) Kwa sababu Yehova anathamini sana uhai, alituma manabii wake tena na tena ili Waisraeli waache njia zao mbaya. Lakini wengi wa watu hao wenye mioyo migumu walikataa kusikiliza na kutubu. Mwishowe, Yehova aliwatia mikononi mwa adui zao ili kutetea jina lake takatifu na kile kinachowakilishwa na jina hilo.—Nehemia 9:26-30.
20. (a) Twajifunza nini kumhusu Yehova kutokana na jinsi alivyoshughulika na Waisraeli? (b) Kwa nini simba ni mfano ufaao wa haki ya Yehova?
20 Tunajifunza mambo mengi kumhusu Yehova tunapochunguza jinsi alivyoshughulika na Waisraeli. Tunajifunza kwamba macho yake huona maovu yote nayo humhuzunisha sana. (Mithali 15:3) Pia, inatia moyo sana kujua kwamba yeye hujitahidi kuonyesha rehema inapofaa. Isitoshe, tunajifunza kwamba hatekelezi haki yake haraka-haraka. Kwa sababu ya subira na uvumilivu wa Yehova, watu wengi hufikiri kimakosa kwamba hatawaadhibu kamwe waovu. Lakini maoni hayo si kweli. Tunapofikiria jinsi Mungu alivyoshughulika na Waisraeli, tunajifunza kwamba subira yake ina mipaka. Yehova hutekeleza uadilifu kwa uthabiti. Tofauti na wanadamu, ambao mara nyingi huogopa kutenda haki, yeye hutetea kwa ujasiri yaliyo sawa. Kwa hiyo, simba ambaye anawakilisha haki ya kijasiri, anaonekana karibu na Mungu na kiti chake cha enzi.a (Ezekieli 1:10; Ufunuo 4:7) Kwa hiyo tunaweza kuwa na hakika kwamba atatimiza ahadi yake ya kukomesha ukosefu wa haki duniani. Naam, twaweza kusema hivi kwa ufupi kuhusu hukumu yake: Yehova hutekeleza hukumu yake kwa uthabiti inapohitajika na kwa rehema inapowezekana.—2 Petro 3:9.
Kumkaribia Mungu Mwenye Haki
21. Tunapotafakari jinsi Yehova anavyotekeleza haki yake, tunapaswa kumwonaje, na kwa nini?
21 Tunapotafakari jinsi Yehova anavyotekeleza haki, hatupaswi kumwona kama hakimu mkali asiye na hisia ambaye anapenda tu kuwahukumu watenda-maovu. Badala yake, tunapaswa kumwona kuwa Baba mwenye upendo, aliye thabiti, ambaye huwatunza watoto wake kwa njia bora kabisa. Akiwa Baba mwadilifu au mwenye haki, Yehova ni thabiti kwa mambo yaliyo sawa na vilevile huwaonyesha rehema nyororo watoto wake wa kidunia ambao wanahitaji msaada na msamaha wake.—Zaburi 103:10, 13.
22. Akiongozwa na haki yake, Yehova ametuwezesha kuwa na tumaini gani, na kwa nini anashughulika nasi kwa njia hiyo?
22 Tunashukuru kama nini kwamba haki ya Mungu haimaanishi kuwahukumu tu watenda-maovu! Akiongozwa na haki yake, Yehova ametuwezesha kuwa na tumaini lenye kusisimua sana—kuishi milele na kwa ukamilifu katika ulimwengu ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Mungu wetu anashughulika nasi kwa njia hiyo kwa sababu haki yake humchochea ajitahidi kuokoa badala ya kuhukumu. Kwa kweli, tunavutiwa kumkaribia Yehova tunapoelewa vyema haki yake! Katika sura zifuatazo, tutachunguza kwa undani zaidi jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo yenye kuvutia.
a Kwa kufaa, Yehova alijilinganisha na simba alipowahukumu Waisraeli wenye kuasi.—Yeremia 25:38; Hosea 5:14.
-
-
“Je, kwa Mungu Kuna Ukosefu wa Haki?”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 12
“Je, kwa Mungu Kuna Ukosefu wa Haki?”
1. Visa vya ukosefu wa haki vinaweza kutufanya tuhisije?
MJANE mmoja mzee aibiwa kwa ujanja pesa zote alizoweka akibani. Mtoto mchanga atupwa na mama yake asiye na huruma. Mwanamume fulani afungwa gerezani isivyo haki kwa shtaka la uhalifu. Unahisije kuhusu visa hivyo? Yaelekea kwamba kila kisa kinakuhuzunisha, na sababu ni wazi. Wanadamu wote wanatambua vyema mambo yaliyo sawa na yaliyo kosa. Tunakasirika tunapoona mtu akitendewa isivyo haki. Tunataka mtu huyo alipwe na mkosaji aadhibiwe. Haki isipotekelezwa, huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, Mungu anaona yanayotukia? Mbona hachukui hatua?’
2. Habakuki alihisije kwa sababu ya ukosefu wa haki, na kwa nini Yehova hakumshutumu?
2 Katika historia yote, watumishi waaminifu wa Yehova wameuliza maswali kama hayo. Kwa mfano, nabii Habakuki alisali hivi kwa Mungu: “Kwa nini wanifanya nishuhudie ukosefu huu mbaya wa haki? Kwa nini unaruhusu jeuri, uasi-sheria, uhalifu na ukatili uenee kotekote?” (Habakuki 1:3, Contemporary English Version) Yehova hakumshutumu Habakuki kwa sababu ya kuuliza maswali hayo yaliyo wazi, kwa kuwa Ndiye aliyewaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuonyesha haki. Naam, Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kuonyesha kwa kadiri fulani haki yake kamilifu.
Yehova Anachukia Ukosefu wa Haki
3. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yehova anajua vyema ukosefu wa haki uliopo?
3 Yehova anajua kwamba kuna ukosefu wa haki. Anaona yanayotukia. Biblia yatuambia hivi kuhusu siku za Noa: “BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.” (Mwanzo 6:5) Fikiria maana ya maneno hayo. Mara nyingi, sisi hutambua kuna ukosefu wa haki baada ya kusikia visa kadhaa vya ukosefu wa haki au baada ya kutendewa isivyo haki. Kinyume chake, Yehova anaona ukosefu wote wa haki unaotukia ulimwenguni pote. Isitoshe, anaweza kutambua nia ya moyo—mawazo mapotovu yanayowafanya watu watende isivyo haki.—Yeremia 17:10.
4, 5. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova anawajali wanaotendewa isivyo haki? (b) Yehova alitendewaje isivyo haki?
4 Lakini Yehova haangalii tu ukosefu wa haki bila kuchukua hatua. Anawajali wale wanaoteseka kwa sababu ya kutendewa isivyo haki. Watu wake walipoteswa kikatili na mataifa adui, Yehova alihuzunika ‘kwa ajili ya kuugua kwao kwa sababu watu wale waliwaonea na kuwasumbua.’ (Waamuzi 2:18) Huenda umegundua kwamba watu fulani hawana huruma kwa sababu wameona visa vingi sana vya ukosefu wa haki. Lakini Yehova ni tofauti kabisa! Ameona ukosefu wa haki wa kila namna kwa miaka ipatayo 6,000, lakini bado unamchukiza. Isitoshe, Biblia inatuhakikishia kwamba mambo kama vile “ulimi wa uongo,” “mikono imwagayo damu isiyo na hatia,” na “shahidi wa uongo asemaye uongo,” yanamchukiza.—Mithali 6:16-19.
5 Fikiria pia jinsi Yehova alivyowashutumu vikali viongozi wasiofuata haki katika Israeli. Alimpulizia nabii wake kuwaambia hivi: “Nyinyi ndio mnaopaswa kujua mambo ya haki.” Baada ya kueleza waziwazi jinsi walivyotumia vibaya mamlaka yao, Yehova alitabiri mambo yatakayowapata watu hao wafisadi: ‘Watamlilia Mwenyezi-Mungu lakini yeye hatawajibu. Atauficha uso wake wakati huo, kwa sababu wamemtenda mambo maovu.’ (Mika 3:1-4, BHN) Yehova anachukia kabisa ukosefu wa haki kwa sababu yeye pia alitendewa isivyo haki! Kwa maelfu ya miaka, Shetani amekuwa akimlaumu Mungu isivyo haki. (Mithali 27:11) Isitoshe, Yehova aliathiriwa na tendo baya zaidi la ukosefu wa haki, wakati Mwanaye aliuawa kama mhalifu ingawa “hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:22; Isaya 53:9) Ni wazi kwamba Yehova hapuuzi wala kutojali mateso ya wale wanaotendewa isivyo haki.
6. Huenda tukahisije tunapotendewa isivyo haki, na kwa nini?
6 Licha ya hayo, tunapoona ukosefu wa haki—au tunapotendewa isivyo haki—kwa kawaida tunasononeka sana. Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, na ukosefu wa haki haupatani hata kidogo na utu wa Yehova. (Mwanzo 1:27) Basi, mbona Yehova anaruhusu ukosefu wa haki?
Suala la Enzi Kuu ya Mungu
7. Eleza jinsi enzi kuu ya Yehova ilivyotiliwa shaka.
7 Jibu la swali hilo linahusiana na suala la enzi kuu. Kama tulivyoona, Muumba ana haki ya kutawala dunia na wote wanaokaa humo. (Zaburi 24:1; Ufunuo 4:11) Hata hivyo, enzi kuu ya Yehova ilitiliwa shaka mapema katika historia ya wanadamu. Ilikuwaje? Yehova alimwamuru mwanadamu wa kwanza, Adamu, asile matunda ya mti fulani uliokuwa katika bustani ya Paradiso alimoishi. Ingekuwaje kama hangetii? Mungu alimwambia “utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Amri ya Mungu haikumkandamiza Adamu au mkewe, Hawa. Hata hivyo, Shetani alimsadikisha Hawa kwamba Mungu alikuwa akiwawekea vizuizi vinavyopita kiasi. Hawa angepatwa na nini kama angekula kutokana na mti huo? Shetani alimwambia Hawa waziwazi: “Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:1-5.
8. (a) Mambo ambayo Shetani alimwambia Hawa yalidokeza nini? (b) Shetani alidai nini kuhusu enzi kuu ya Mungu?
8 Kwa kusema hivyo, Shetani alidokeza kwamba Yehova alimdanganya Hawa na vilevile alimnyima habari muhimu sana. Kwa tahadhari, Shetani hakupinga kwamba Mungu ndiye mtawala mwenye enzi kuu. Lakini alidai kwamba Mungu hakutawala kwa uadilifu wala hakuwa na haki ya kuwa mwenye enzi kuu. Yaani, alidai kwamba Yehova alikuwa akiwadhulumu raia wake na hakuwa akitawala kwa njia ya uadilifu.
9. (a) Adamu na Hawa walipatwa na nini kwa sababu ya kutotii, na hilo lilizusha maswali gani muhimu? (b) Kwa nini Yehova hakuwaangamiza waasi hao papo hapo?
9 Adamu na Hawa walimwasi Yehova wakala matunda ya mti uliokatazwa. Kwa sababu hawakutii, wangepokea adhabu ya kifo kama Mungu alivyokuwa amesema. Uwongo wa Shetani ulizusha maswali kadhaa muhimu. Je, kweli Yehova ana haki ya kutawala wanadamu, au wanadamu wanapaswa kujitawala? Je, Yehova anatawala kwa njia bora kabisa? Yehova angaliweza kuwaangamiza waasi hao papo hapo kwa kutumia nguvu zake kuu. Lakini masuala yaliyozushwa yalihusu utawala wa Mungu, wala si nguvu zake. Kwa hiyo, kumwangamiza Adamu, Hawa, na Shetani hakungethibitisha kwamba Mungu anatawala kwa uadilifu. Badala yake, huenda utawala wake ungetiliwa shaka hata zaidi. Njia pekee ya kujua iwapo wanadamu wangeweza kujitawala kwa mafanikio bila kumtegemea Mungu, ingekuwa ni kuwapa muda zaidi wa kuthibitisha madai hayo.
10. Historia imefunua nini kuhusu utawala wa wanadamu?
10 Historia imefunua nini? Kwa maelfu ya miaka, watu wamejaribu serikali nyingi mbalimbali, kama vile serikali za kimabavu, demokrasia, ujamaa na ukomunisti. Matokeo ya serikali hizo zote yanatajwa na maneno haya ya Biblia ambayo ni ya kweli: ‘Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Kwa kufaa, nabii Yeremia alisema hivi: “Ee, BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.
11. Kwa nini Yehova aliruhusu wanadamu wateseke?
11 Tangu mwanzoni, Yehova alijua kwamba wanadamu wangeteseka sana kwa sababu ya kujitegemea au kujitawala. Basi, je, alikosa haki kwa kuruhusu mateso hayo yaendelee? La hasha! Kwa mfano: Tuseme una mtoto anayehitaji kufanyiwa upasuaji ili kutibu ugonjwa hatari sana. Unahuzunika sana kwa sababu unatambua kwamba mtoto wako atateseka kwa kadiri fulani anapofanyiwa upasuaji. Lakini unajua pia kwamba upasuaji utamsaidia mtoto wako kuwa na afya bora baadaye. Vivyo hivyo, Mungu alijua—na hata alitabiri—kwamba utawala wa wanadamu ambao ameruhusu ungesababisha maumivu na mateso kwa kadiri fulani. (Mwanzo 3:16-19) Lakini alijua pia kwamba kitulizo cha kudumu na kinachofaa kingepatikana tu ikiwa angeacha wanadamu wote waone matokeo mabaya ya uasi. Hivyo suala la enzi kuu lingetatuliwa kabisa, kwa umilele wote.
Suala la Uaminifu wa Mwanadamu
12. Kama kisa cha Yobu kinavyoonyesha, Shetani ametoa shtaka gani dhidi ya wanadamu?
12 Kuna jambo jingine linalohusika. Alipodai kwamba Mungu hana haki ya kutawala na hatawali kwa uadilifu, Shetani hakusema tu uwongo kuhusu enzi kuu ya Yehova; alisema pia uwongo kuhusu uaminifu wa watumishi wa Mungu. Kwa mfano, angalia maneno ambayo Shetani alimwambia Yehova kuhusu yule mwanamume mwadilifu, Yobu: “Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi. Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.”—Ayubu 1:10, 11.
13. Shetani alidai nini alipomshtaki Yobu, na wanadamu wote wanahusikaje?
13 Shetani alidai kwamba Yehova alimhonga Yobu amtumikie kwa kumlinda kwa nguvu Zake. Na hilo lilimaanisha kwamba uaminifu wa Yobu ulikuwa wa kinafiki, na kwamba alimwabudu Mungu kwa ubinafsi tu. Shetani alidai kwamba Yobu angemkufuru Muumba wake kama hangebarikiwa. Shetani alijua kwamba Yobu alikuwa “mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.”a Basi kama Shetani angeweza kuvunja uaminifu wa Yobu, yaelekea kwamba angeweza pia kuvunja uaminifu wa wanadamu wengine wote. Kwa hiyo, Shetani alikuwa akitilia shaka uaminifu wa wanadamu wote wanaotaka kumtumikia Mungu. Kwa kweli, Shetani alihusisha wengine katika suala hilo kwa kumwambia hivi Yehova: “Yote aliyo nayo mtu [si Yobu tu] atayatoa kwa ajili ya uhai wake.”—Ayubu 1:8; 2:4.
14. Historia imeonyesha nini kuhusu dai la Shetani dhidi ya wanadamu?
14 Historia imeonyesha kwamba dai la Shetani ni la uwongo kwa sababu wengi kama Yobu, wamedumisha uaminifu kwa Yehova wakati wa majaribu. Maisha yao ya uaminifu yamemfurahisha Yehova, na hivyo ameweza kumjibu Shetani aliyedai kwa kiburi kwamba wanadamu wataacha kumtumikia Mungu wakipata magumu. (Waebrania 11:4-38) Naam, watu waadilifu wamekataa kumpa Mungu kisogo. Hata wanapokumbwa na matatizo magumu sana, wamemtegemea hata zaidi Yehova ili awape nguvu za kuvumilia.—2 Wakorintho 4:7-10.
15. Ni swali gani linaloweza kuzuka kuhusu hukumu za Mungu za wakati uliopita na za wakati ujao?
15 Lakini Yehova huonyesha haki katika mambo mengine mbali na suala la enzi kuu na suala la uaminifu wa wanadamu. Biblia hutueleza jinsi Yehova alivyohukumu watu mmoja-mmoja na hata mataifa mazima. Pia ina unabii mbalimbali wa hukumu ambazo atatekeleza wakati ujao. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova amekuwa akihukumu kwa uadilifu na bado atahukumu kwa uadilifu wakati ujao?
Ubora wa Haki ya Mungu
Yehova ‘hataharibu kamwe mwenye haki pamoja na mwovu’
16, 17. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba wanadamu hawafahamu kikamili haki ya kweli?
16 Ni sahihi kusema hivi kumhusu Yehova: “Njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kudai hivyo, kwa kuwa mara nyingi tunashindwa kufahamu kikamili mambo yaliyo sawa. Kwa mfano, mfikirie Abrahamu. Alimsihi Yehova asiharibu Sodoma ingawa uovu ulikuwa umeenea sana. Alimwuliza Yehova hivi: “Je! Utaharibu mwenye haki pamoja na mwovu?” (Mwanzo 18:23-33) Bila shaka, jibu ni la. Yehova ‘alinyesha kiberiti na moto’ juu ya Sodoma, baada tu ya Loti mwadilifu na binti zake kufika mji wa Soari wakiwa salama. (Mwanzo 19:22-24) Kinyume chake, Yona ‘alikasirika’ sana wakati Mungu alipowaonyesha rehema watu wa Ninawi. Bila kujali toba yao ya kutoka moyoni, Yona alitaka tu waangamizwe kwa sababu tayari alikuwa ametangaza kwamba wangeangamizwa.—Yona 3:10–4:1.
17 Yehova alimhakikishia Abrahamu kwamba anatekeleza haki Yake kwa kuwaangamiza waovu na kuwaokoa pia waadilifu. Kwa upande mwingine, Yona alihitaji kujifunza kwamba Yehova ni mwenye rehema. Waovu wakiacha kabisa njia zao, yuko “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Tofauti na wanadamu fulani wanaojali mno vyeo vyao, Yehova hatoi hukumu kali ili kujionyesha ana nguvu, wala hakatai kuwahurumia watu eti kwa sababu ataonekana kuwa dhaifu. Yeye huonyesha rehema wakati wowote inapofaa kufanya hivyo.—Isaya 55:7; Ezekieli 18:23.
18. Tumia Biblia kuthibitisha kwamba Yehova haongozwi tu na hisia.
18 Hata hivyo, Yehova hapumbazwi na hisia. Watu wake walipoanza kuabudu sanamu, Yehova alisema hivi kwa uthabiti: “Nitawahukumu kadiri ya mwenendo wenu. Nitawaadhibu kwa machukizo yenu yote. Sitawaachia wala sitawaonea huruma; bali nitawaadhibu kulingana na mienendo yenu.” (Ezekieli 7:3, 4, BHN) Kwa hiyo, wanadamu wanapoendelea kufanya mabaya bila kujali, Yehova huwahukumu ifaavyo. Lakini hukumu yake inategemea ushahidi thabiti. Hivyo, Yehova aliposikia “kilio” kuhusu Sodoma na Gomora alisema hivi: “Nitashuka sasa nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia.” (Mwanzo 18:20, 21) Tunathamini kama nini kwamba Yehova si kama wanadamu wengi ambao huamua mambo haraka-haraka bila ushahidi kamili! Kwa kweli, Biblia yaeleza jinsi Yehova alivyo, “Mungu wa uaminifu . . . mwenye haki.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.
Tumaini Haki ya Yehova
19. Tunaweza kufanya nini tukiwa na maswali yenye kutatanisha kuhusu hukumu za Yehova?
19 Biblia haijibu kila swali kuhusu matendo ya Yehova katika nyakati za kale; wala haielezi kila jambo kuhusu jinsi Yehova atakavyohukumu mtu mmoja-mmoja na vikundi vya watu wakati ujao. Tunapotatanishwa na masimulizi au unabii fulani wa Biblia ambao hauelezi kila jambo, tunaweza kuwa waaminifu kama nabii Mika, aliyeandika hivi: “Nitamngojea Mungu wa wokovu wangu.”—Mika 7:7.
20, 21. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova atafanya yaliyo sawa?
20 Tunaweza kuwa na hakika kwamba katika kila hali, Yehova atafanya yaliyo sawa. Hata inapoonekana kwamba wanadamu wanapuuza ukosefu wa haki, Yehova anaahidi hivi: “Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa.” (Waroma 12:19) Tukiwa na mtazamo wa kungoja, tutakuwa na usadikisho imara kama wa mtume Paulo aliyesema: “Je, kwa Mungu kuna ukosefu wa haki? Hilo lisipate kuwa hivyo kamwe!”—Waroma 9:14.
21 Hivi sasa tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Watu wengi wametendewa kikatili kwa sababu ya ‘dhuluma’ na ukosefu wa haki. (Mhubiri 4:1) Hata hivyo, Yehova hajabadilika. Bado anachukia ukosefu wa haki, naye anawajali sana wale wanaotendewa isivyo haki. Tukiendelea kuwa waaminifu kwa enzi kuu ya Yehova, atatupatia uwezo wa kuvumilia hadi Ufalme wake utakapokomesha ukosefu wote wa haki kwa wakati barabara.—1 Petro 5:6, 7.
-
-
“Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 13
“Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”
1, 2. Kwa nini watu wengi wanapuuza sheria, lakini huenda sisi tukahisije kuhusu sheria za Mungu?
“SHERIA haina mipaka, . . . huharibu mambo yote.” Maneno hayo yaliandikwa katika kitabu kilichochapishwa mnamo mwaka wa 1712. Mwandishi wa kitabu hicho alilaumu mfumo wa sheria ambao uliendeleza kesi mahakamani miaka nenda miaka rudi. Wale waliotafuta haki mahakamani walifilisika kabisa. Katika nchi nyingi, watu wengi hawaheshimu kabisa sheria kwa sababu mifumo ya sheria na ya mahakama haieleweki, haifuati haki kabisa, inapendelea watu, na haitegemeki.
2 Tofauti na maelezo hayo, fikiria maneno yaliyoandikwa miaka ipatayo 2,700 iliyopita: “Sheria yako naipenda mno ajabu.” (Zaburi 119:97) Kwa nini mtunga-zaburi aliipenda mno sheria hiyo? Kwa sababu sheria aliyosifu ilitungwa na Yehova Mungu, wala si na serikali yoyote ya wanadamu. Kadiri unavyojifunza sheria za Yehova, huenda ukazipenda zaidi kama mtunga-zaburi. Kujifunza sheria hizo kutakusaidia kumjua vyema hakimu bora zaidi ulimwenguni.
Mpaji-Sheria Mkuu Zaidi
3, 4. Yehova amethibitika kuwa Mpaji-Sheria kwa njia zipi?
3 Biblia inatuambia kwamba “mmoja yuko ambaye ni mpaji-sheria na hakimu.” (Yakobo 4:12) Kwa hakika, Yehova peke yake ndiye Mpaji-Sheria wa kweli. Hata sayari zinafuata ‘sheria zake zinazoongoza mbingu.’ (Ayubu 38:33, The New Jerusalem Bible) Kundi kubwa sana la malaika watakatifu wa Yehova wanaongozwa pia na sheria zake, kwa kuwa wamepangwa kulingana na vyeo hususa, nao hufuata amri ya Yehova wakiwa wahudumu wake.—Zaburi 104:4; Waebrania 1:7, 14.
4 Yehova amewapa pia wanadamu sheria. Kila mmoja wetu ana dhamiri, ambayo inaonyesha haki ya Yehova. Dhamiri ni sheria fulani ya asili ambayo inaweza kutusaidia kupambanua mema na mabaya. (Waroma 2:14) Wazazi wetu wa kwanza walipewa dhamiri kamilifu, kwa hiyo walihitaji sheria chache sana. (Mwanzo 2:15-17) Hata hivyo, mwanadamu asiyekamilika anahitaji sheria nyingi zaidi za kumwongoza kufanya mapenzi ya Mungu. Wazee wa ukoo kama vile Noa, Abrahamu, na Yakobo walizipa familia zao sheria ambazo walipewa na Yehova Mungu. (Mwanzo 6:22; 9:3-6; 18:19; 26:4, 5) Yehova alijisababisha kuwa Mpaji-Sheria asiye na kifani alipopatia taifa la Israeli Sheria kupitia Musa. Sheria hizo zinatusaidia kuelewa kindani zaidi haki ya Yehova.
Muhtasari wa Sheria ya Musa
5. Je, Sheria ya Musa ilikuwa na amri ngumu na zenye kulemea, na kwa nini unajibu hivyo?
5 Watu wengi wanafikiri kwamba Sheria ya Musa ilikuwa na amri ngumu zenye kulemea. Jambo hilo si kweli. Sheria hiyo ilikuwa na zaidi ya amri 600. Huenda hizo zikaonekana kuwa nyingi, lakini hebu fikiria: Kufikia mwishoni mwa karne ya 20, sheria za serikali ya Marekani zilijaza zaidi ya kurasa 150,000 za vitabu vya sheria. Sheria zipatazo 600 huongezwa baada ya kila miaka miwili! Kwa hiyo, sheria za wanadamu ni nyingi sana kuliko Sheria ya Musa. Hata hivyo, Sheria ya Mungu iliwaongoza Waisraeli katika mambo mbalimbali ya maisha ambayo hata sheria za kisasa hazitaji. Chunguza muhtasari wa sheria hiyo.
6, 7. (a) Sheria ya Musa inatofautianaje na mfumo mwingine wowote wa sheria, na amri kuu ya Sheria hiyo ni ipi? (b) Waisraeli wangeweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanakubali enzi kuu ya Yehova?
6 Sheria ilitukuza enzi kuu ya Yehova. Kwa sababu hiyo, Sheria ya Musa haiwezi kulinganishwa na mfumo mwingine wowote wa sheria. Amri kuu zaidi ya sheria hiyo ilikuwa: “Sikiza, Ee Israeli; BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja. Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.” Watu wa Mungu wangeonyeshaje kwamba wanampenda? Walipaswa kumtumikia, kujitiisha kwa enzi yake kuu.—Kumbukumbu la Torati 6:4, 5; 11:13.
7 Kila Mwisraeli alionyesha kwamba anakubali enzi kuu ya Yehova kwa kujitiisha kwa wale waliopewa mamlaka. Wazazi, wakuu, waamuzi, makuhani na, hatimaye, mfalme waliwakilisha mamlaka ya Mungu. Yehova aliona uasi wowote dhidi ya wenye mamlaka kuwa uasi dhidi yake. Kwa upande mwingine, wale wenye mamlaka wangeadhibiwa na Yehova iwapo wangewaonea au kuwakandamiza watu wake. (Kutoka 20:12; 22:28; Kumbukumbu la Torati 1:16, 17; 17:8-20; 19:16, 17) Basi, watu wote walikuwa na wajibu wa kuunga mkono enzi kuu ya Mungu.
8. Sheria ilidumishaje utakatifu wa Yehova?
8 Sheria ilidumisha utakatifu wa Yehova. Sheria ya Musa inataja neno “takatifu” na “utakatifu” zaidi ya mara 280. Sheria iliwasaidia watu wa Mungu kutofautisha vitu safi na visivyo safi, ilitaja vitu 70 hivi ambavyo vingemfanya Mwisraeli awe najisi. Sheria hizo zilihusu usafi wa mwili, chakula, na hata kufunika kinyesi. Sheria hizo zililinda kabisa afya yao.a Lakini zilitimiza kusudi jingine muhimu zaidi—ziliwasaidia kupata kibali cha Yehova, ziliwatenga na mazoea yenye dhambi ya mataifa yasiyo na adili yaliyokuwa jirani. Fikiria mfano mmoja.
9, 10. Agano la Sheria lilisema nini kuhusu ngono na kujifungua mtoto, na sheria hizo zilikuwa na manufaa gani?
9 Agano la Sheria lilisema kwamba mtu aliyejifungua mtoto au kufanya ngono—hata kati ya wenzi wa ndoa—angekuwa najisi kwa kipindi fulani. (Mambo ya Walawi 12:2-4; 15:16-18) Sheria hizo hazikudharau zawadi hizo safi kutoka kwa Mungu. (Mwanzo 1:28; 2:18-25) Badala yake, sheria hizo zilidumisha utakatifu wa Yehova kwa kuwazuia waabudu wake wasichafuliwe. Kumbuka kwamba mataifa jirani ya Israeli yalikuwa yakichanganya dini na ibada za ngono na uzazi. Dini ya Wakanaani ilikuwa na makahaba wa kiume na wa kike. Walitenda mambo maovu kupindukia na yakaenea kotekote. Kinyume chake, Sheria ilitenga kabisa ibada ya Yehova na mambo ya ngono.b Kulikuwa na faida nyingine pia.
10 Sheria hizo pia zilifundisha ukweli fulani muhimu sana.c Dhambi ya Adamu inapitishwaje kutoka kizazi hadi kizazi? Ni kupitia ngono na kuzaa, sivyo? (Waroma 5:12) Ndiyo, Sheria ya Mungu iliwakumbusha watu wake kwamba wao ni watenda-dhambi. Kwa kweli, sote tunazaliwa katika dhambi. (Zaburi 51:5) Tunahitaji msamaha na ukombozi ili kumkaribia Mungu wetu mtakatifu.
11, 12. (a) Sheria ilitetea kanuni gani muhimu ya haki? (b) Sheria ilizuia upotoshaji wa haki katika mambo yapi?
11 Sheria ilidumisha haki kamilifu ya Yehova. Sheria ya Musa ilitetea kanuni ya usawa, au usawaziko, katika mambo ya haki. Kwa hiyo, Sheria ilisema hivi: “Uhai utalipwa kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono na mguu kwa mguu.” (Kumbukumbu la Torati 19:21, BHN) Hivyo basi, adhabu ya kesi za uhalifu ililingana na uhalifu uliofanywa. Kanuni hiyo ya haki ya Mungu ilikuwa muhimu sana katika Sheria. Na kanuni hiyo inaweza kutusaidia leo kuelewa dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu, kama Sura ya 14 itakavyoonyesha.—1 Timotheo 2:5, 6.
12 Sheria ilizuia pia upotoshaji wa haki. Kwa mfano, angalau mashahidi wawili walihitajiwa ili kuthibitisha shtaka. Mashahidi wa uwongo walipata adhabu kali sana. (Kumbukumbu la Torati 19:15, 18, 19) Ufisadi na kupokea rushwa kulipigwa marufuku. (Kutoka 23:8; Kumbukumbu la Torati 27:25) Watu wa Mungu walihitaji kufuata kanuni za juu za Yehova za haki hata katika shughuli zao za kibiashara. (Mambo ya Walawi 19:35, 36; Kumbukumbu la Torati 23:19, 20) Mfumo huo wa sheria usiopendelea na usio na kifani ulinufaisha sana Israeli!
Sheria Zinazokazia Rehema na Kutopendelea Katika Hukumu
13, 14. Sheria ilikaziaje haki na kutopendelea kwa habari ya mwizi na yule aliyeibiwa?
13 Je, Sheria ya Musa ilikuwa kali mno, iliyotekelezwa bila rehema? La hasha! Mfalme Daudi aliongozwa kuandika hivi: “Sheria ya BWANA ni kamilifu.” (Zaburi 19:7) Daudi alijua vyema kwamba Sheria ilikazia rehema na kutopendelea. Jinsi gani?
14 Katika nchi fulani leo, yaonekana kwamba sheria huwapendelea na kuwalinda wahalifu na haiwajali waliotendewa uhalifu. Kwa mfano, huenda wezi wakafungwa gerezani. Lakini, wale walioibiwa huenda hawajarudishiwa mali yao, ingawa wanalazimika kulipa ushuru ili kuwalisha wahalifu hao wakiwa gerezani. Katika Israeli la kale, hakukuwa na magereza kama leo. Adhabu haikupaswa kupita mipaka iliyowekwa na Sheria. (Kumbukumbu la Torati 25:1-3) Mwizi alilazimika kulipa vitu alivyokuwa ameiba. Isitoshe, alitoa malipo zaidi. Alilipa kiasi gani? Ilitegemea hali. Inaonekana kwamba mahakimu waliruhusiwa kuzingatia mambo kadhaa, kama vile toba ya mtenda-dhambi. Ndiyo sababu malipo ambayo mwizi alihitajiwa kulipa yanayotajwa kwenye Mambo ya Walawi 6:1-7 ni chini zaidi kuliko malipo yanayotajwa kwenye Kutoka 22:7.
15. Sheria ilionyeshaje rehema na haki kwa mtu aliyemwua mwingine bila kukusudia?
15 Kwa rehema, Sheria ilitambua kwamba makosa yote hayakuwa ya kukusudia. Kwa mfano, mtu alipomwua mwingine bila kukusudia, hakuhitajika kulipa uhai kwa uhai ikiwa alichukua hatua ifaayo ya kukimbilia mojawapo ya miji ya makimbilio iliyokuwa kotekote katika Israeli. Baada ya kesi yake kuchunguzwa na waamuzi wa mji huo, alikaa humo hadi kifo cha kuhani mkuu. Kisha angekuwa huru kuishi popote alipotaka. Hivyo, alinufaishwa na rehema ya Mungu. Vilevile, sheria hiyo ilikazia thamani kubwa ya uhai wa mwanadamu.—Hesabu 15:30, 31; 35:12-25.
16. Sheria ililindaje haki fulani za watu?
16 Sheria ililinda haki za watu. Angalia jinsi ilivyolinda watu wenye madeni. Sheria ilikataza kuingia katika nyumba ya mdeni na kuchukua mali yake kama rehani. Badala yake, mkopeshaji alihitaji kusimama nje na kungoja mdeni amletee rehani hiyo. Hivyo, hakuna mtu aliyeruhusiwa kuvamia nyumba ya mwingine. Ikiwa mkopeshaji alichukua vazi la nje kama rehani, sharti angelirudisha jioni, kwa sababu huenda mdeni angehitaji kujifunika vazi hilo wakati wa usiku.—Kumbukumbu la Torati 24:10-14.
17, 18. Waisraeli walitofautianaje na mataifa mengine kuhusu vita, na kwa nini?
17 Hata pia kulikuwa na sheria kuhusu vita. Watu wa Mungu hawakupigana vita kwa sababu tu walitamani kupata mamlaka au ushindi, bali walimwakilisha Mungu katika “Vita vya BWANA.” (Hesabu 21:14) Mara nyingi, Waisraeli walitoa kwanza masharti ya kujisalimisha. Ikiwa jiji lilikataa masharti hayo, basi Israeli lingelizingira kupatana na amri za Mungu. Tofauti na wanajeshi wengi, wanajeshi Waisraeli hawakuruhusiwa kubaka wanawake au kuchinja watu ovyo-ovyo. Hata walihitaji kuheshimu mazingira, hawakupaswa kukata miti ya matunda ya maadui.d Wanajeshi wengine hawakuwa na sheria kama hizo.—Kumbukumbu la Torati 20:10-15, 19, 20; 21:10-13.
18 Je, wewe huudhika unaposikia kwamba katika nchi fulani watoto wadogo wanazoezwa kuwa wanajeshi? Katika Israeli la kale, mwanamume yeyote mwenye umri uliopungua miaka 20 hakuandikishwa jeshini. (Hesabu 1:2, 3) Hata mwanamume mzima mwenye hofu kubwa hakuruhusiwa kwenda vitani. Mwanamume aliyeoa karibuni hangeenda vitani kwa mwaka mzima ili aweze kumzaa mrithi kabla ya kushiriki utumishi huo hatari sana. Sheria ilieleza kwamba kwa kufanya hivyo, mume huyo kijana angepata ‘kumfurahisha’ mkewe.—Kumbukumbu la Torati 20:5, 6, 8; 24:5.
19. Sheria iliwalindaje wanawake, watoto, familia, wajane, na mayatima?
19 Sheria iliwalinda wanawake, watoto, na familia na kujali masilahi yao. Iliwaamuru wazazi wawatunze na kuwafundisha watoto mambo ya kiroho kila wakati. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Ilikataza ngono zote za maharimu, na yeyote aliyefanya hivyo aliuawa. (Mambo ya Walawi, sura ya 18) Vilevile ilikataza uzinzi, ambao mara nyingi huvunja na kuharibu amani na heshima ya familia. Sheria iliwajali sana wajane na mayatima na ilikataza katakata wasiteswe.—Kutoka 20:14; 22:22-24.
20, 21. (a) Kwa nini Sheria ya Musa iliwaruhusu Waisraeli wawe na wake wengi? (b) Kuhusu talaka, kwa nini Sheria ilitofautiana na kanuni ambazo Yesu alirudisha baadaye?
20 Hata hivyo, huenda wengine wakajiuliza hivi, ‘Mbona Sheria iliwaruhusu watu kuwa na wake wengi?’ (Kumbukumbu la Torati 21:15-17) Tunahitaji kuchunguza sheria kama hizo tukifikiria hali za wakati huo. Wale wanaojaribu kuelewa Sheria ya Musa kwa kutegemea maoni ya nyakati na tamaduni za kisasa bila shaka hawataielewa. (Mithali 18:13) Kulingana na kanuni ambazo Yehova aliweka zamani katika Edeni, ndoa ilikuwa kifungo cha kudumu kati ya mume mmoja na mke mmoja. (Mwanzo 2:18, 20-24) Hata hivyo, mazoea kama vile ndoa za wake wengi yalikuwa yameenea kwa miaka mingi sana kabla Yehova hajawapa Waisraeli Sheria. Yehova alijua vyema kwamba mara kwa mara ‘watu wake wenye shingo ngumu’ wangekosa kutii hata sheria rahisi sana, kama zile zilizokataza ibada ya sanamu. (Kutoka 32:9) Basi kwa hekima, hakuchagua wakati huo kuwa wakati wa kurekebisha mazoea yao yote ya ndoa. Lakini kumbuka kwamba Yehova hakuanzisha ndoa ya wake wengi. Hata hivyo, alitumia Sheria ya Musa kudhibiti ndoa za wake wengi miongoni mwa watu wake na kuwazuia wasitumie vibaya zoea hilo.
21 Vivyo hivyo, Sheria ya Musa ilimruhusu mwanamume kumtaliki mkewe kwa sababu mbalimbali nzito. (Kumbukumbu la Torati 24:1-4) Yesu alisema kwamba Mungu aliwapa Wayahudi idhini hiyo “kwa kufikiria ugumu [wao] wa moyo.” Hata hivyo, idhini kama hizo zilikuwa za muda tu. Yesu alirudisha tena kanuni za Yehova kuhusu ndoa ambazo zingefuatwa na wafuasi wake.—Mathayo 19:8.
Sheria Ilikazia Upendo
22. Sheria ya Musa ilikazia upendo kwa njia zipi, na kwa nani?
22 Je, waweza kuwazia mfumo wowote wa kisasa wa sheria unaokazia upendo? Sheria ya Musa ilikazia sana upendo. Kwani, katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati pekee, neno “upendo” limetumiwa zaidi ya mara 20 katika njia mbalimbali. Amri ya pili iliyo kuu zaidi katika Sheria ilikuwa, “umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:18; Mathayo 22:37-40) Waisraeli walipaswa kuwapenda wenzao na pia wageni walioishi kati yao, huku wakikumbuka kwamba pindi moja wao pia walikuwa wageni. Walipaswa kuwapenda maskini na wanyonge, na kuwasaidia kimwili bila kuwadhulumu. Hata waliagizwa kuwa wenye fadhili na kuwajali wanyama wanaobeba mizigo.—Kutoka 23:6; Mambo ya Walawi 19:14, 33, 34; Kumbukumbu la Torati 22:4, 10; 24:17, 18.
23. Mtungaji wa Zaburi 119 alichochewa kufanya nini, nasi tunaweza kuazimia kufanya nini?
23 Hakuna taifa jingine lililobarikiwa na sheria kama hizo. Si ajabu kwamba mtunga-zaburi aliandika hivi: “Naipenda sana sheria yako!” Lakini hakuwa tu na hisia ya upendo. Upendo huo ulimchochea kutenda, kwa kuwa alijitahidi kutii sheria hiyo na kuishi kupatana nayo. Aliendelea kusema hivi: “Naitafakari [sheria yako] mchana kutwa.” (Zaburi 119:11, 97, BHN) Naam, alijifunza sheria za Yehova kwa ukawaida. Hapana shaka yoyote kwamba upendo wake uliongezeka kadiri alivyojifunza sheria hizo. Wakati huohuo, alizidi kumpenda Yehova Mungu, yule Mpaji-Sheria. Na umkaribie zaidi Yehova, Mpaji-Sheria Mkuu na Mungu wa haki unapoendelea kujifunza sheria zake.
a Kwa mfano, sheria zilizoamuru kinyesi cha mwanadamu kifunikwe, wagonjwa watengwe, na mtu yeyote anayegusa maiti aoge, zilikuwapo muda mrefu kabla ya manufaa yake kutambuliwa.—Mambo ya Walawi 13:4-8; Hesabu 19:11-13, 17-19; Kumbukumbu la Torati 23:13, 14.
b Mahekalu ya Wakanaani yalikuwa na vyumba vya kufanyia ngono, lakini Sheria ya Musa ilisema kwamba watu wote walio najisi hawangeweza hata kuingia hekaluni. Kwa hiyo, hakuna mtu yeyote angechanganya ngono na ibada katika nyumba ya Yehova, kwa sababu ngono ilimfanya mtu awe najisi kwa kipindi fulani.
c Kusudi kuu la Sheria lilikuwa kufundisha. Hata kichapo Encyclopaedia Judaica kinasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “sheria,” toh·rah’, linamaanisha “mafundisho.”
d Sheria iliuliza hivi waziwazi: “Mti wa kondeni, je! ni mtu, hata ukauzuie?” (Kumbukumbu la Torati 20:19) Philo, msomi Myahudi wa karne ya kwanza, alitaja sheria hiyo, na kusema kwamba Mungu anaona “haifai hasira inayoelekezwa kwa watu itumiwe kuharibu vitu ambavyo havina hatia yoyote.”
-
-
Yehova Atoa “Fidia Katika Kubadilishana kwa Ajili ya Wengi”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 14
Yehova Atoa “Fidia Katika Kubadilishana kwa Ajili ya Wengi”
1, 2. Biblia inasema nini kuhusu hali ya wanadamu, na suluhisho pekee ni nini?
“VIUMBE vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Maneno hayo ya mtume Paulo yanaeleza hali yetu yenye kusikitisha. Huenda mwanadamu akaona kwamba mateso, dhambi, na kifo haziwezi kukomeshwa. Lakini Yehova ana uwezo unaozidi wa wanadamu. (Hesabu 23:19) Mungu huyo wa haki ametuandalia suluhisho la matatizo yetu. Suluhisho hilo ni fidia.
2 Fidia ndiyo zawadi bora ambayo Yehova amewapa wanadamu. Kupitia fidia tutaweza kukombolewa kutoka kwa dhambi na kifo. (Waefeso 1:7) Ndiyo msingi wa tumaini la kuishi milele, ama mbinguni au katika paradiso duniani. (Luka 23:43; Yohana 3:16; 1 Petro 1:4) Lakini fidia ni nini hasa? Inatusaidiaje kuelewa haki ya Yehova isiyo na kifani?
Kwa Nini Fidia Ilihitajiwa?
3. (a) Kwa nini fidia ilihitajiwa? (b) Kwa nini Mungu hangeweza kupunguza adhabu ya kifo kwa wazao wa Adamu?
3 Fidia ilihitajiwa kwa sababu ya dhambi ya Adamu. Kwa sababu ya kutomtii Mungu, Adamu aliwaletea wazao wake magonjwa, kilio, maumivu, na kifo. (Mwanzo 2:17; Waroma 8:20) Mungu hangeweza kupunguza adhabu ya kifo kwa sababu tu ya kuwahurumia wazao wa Adamu. Kufanya hivyo kungekuwa kupuuza sheria yake mwenyewe inayosema kwamba “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Na endapo Yehova angevunja kanuni zake mwenyewe za haki, basi kungekuwa na mvurugo na uasi ulimwenguni pote!
4, 5. (a) Shetani alitoa mashtaka gani ya uwongo kumhusu Mungu, na kwa nini Yehova alikuwa na wajibu wa kujibu mashtaka hayo? (b) Shetani alitoa shtaka gani kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova?
4 Kama tulivyoona katika Sura ya 12, uasi uliotukia Edeni ulizusha masuala muhimu sana. Shetani alichafua jina zuri la Mungu. Ni kana kwamba alimshtaki Yehova kuwa mwongo na mtawala mkatili wa kimabavu, anayewanyima viumbe wake uhuru. (Mwanzo 3:1-5) Kwa kujaribu kukatisha kusudi la Mungu la kuwa na wanadamu waadilifu duniani, Shetani pia alitoa shtaka la kwamba Mungu hawezi kutimiza makusudi yake. (Mwanzo 1:28; Isaya 55:10, 11) Kama Yehova hangejibu mashtaka hayo, huenda viumbe wake wengi wenye akili wangetilia shaka utawala wake.
5 Shetani alieneza pia uwongo kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova. Alidai kwamba wanamtumikia Yehova kwa sababu ya ubinafsi na kwamba hakuna yeyote ambaye angeendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu akipata magumu. (Ayubu 1:9-11) Masuala hayo yalikuwa muhimu sana kuliko magumu ambayo yangewakabili wanadamu. Kwa kufaa, Yehova alihisi kwamba ana wajibu wa kujibu mashtaka ya uwongo ya Shetani. Lakini Mungu angesuluhishaje masuala hayo na kuwaokoa wanadamu?
Fidia—Bei Inayolingana
6. Ni maneno gani yanayotumiwa katika Biblia kueleza njia ya Mungu ya kuwaokoa wanadamu?
6 Yehova alisuluhisha jambo hilo kwa rehema nyingi sana na haki. Hakuna mwanadamu angeweza kusuluhisha jambo hilo kwa njia hiyo. Alisuluhisha jambo hilo kwa njia rahisi sana. Mara nyingine njia aliyotumia huitwa ununuzi, ukombozi, ufuniko, na upatanisho. (Zaburi 49:8, ZSB; Danieli 9:24, BHN; Wagalatia 3:13; Wakolosai 1:20; Waebrania 2:17) Lakini Yesu alitumia neno ambalo huenda linafaa kabisa. Alisema: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia [Kigiriki, lyʹtron] katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.”—Mathayo 20:28.
7, 8. (a) Neno “fidia” linamaanisha nini katika Maandiko? (b) Fidia inaonyeshaje ulinganifu?
7 Fidia ni nini? Neno la Kigiriki linalotumiwa hapa linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kuweka huru, kuachilia.” Neno hilo lilihusiana na pesa zinazolipwa ili wafungwa wa vita waweze kuachiliwa huru. Basi, kwa ufupi fidia inaweza kufafanuliwa kuwa kitu kinacholipwa ili kununua tena kitu fulani. Katika Maandiko ya Kiebrania, neno linalotafsiriwa “fidia” (koʹpher) linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kufunika.” Kwa mfano, Mungu alimwambia Noa ‘aifunike’ (muundo fulani wa neno hilo) safina kwa lami. (Mwanzo 6:14) Habari hiyo inatusaidia kuelewa kwamba kutoa fidia humaanisha pia kufunika dhambi.—Zaburi 65:3.
8 Kichapo Theological Dictionary of the New Testament kinasema kwamba neno hilo (koʹpher) “sikuzote hudokeza usawa,” au ulinganifu. Kwa hiyo, kifuniko cha sanduku la agano kilikuwa na umbo sawa na sanduku hilo. Vivyo hivyo, ili kutoa fidia, au kufunika dhambi, ni lazima bei inayolipwa ilingane kabisa, au ifunike kikamili hasara iliyosababishwa na dhambi. Ndiyo sababu Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilisema hivi: “Uhai utalipwa kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono na mguu kwa mguu.”—Kumbukumbu la Torati 19:21, BHN.
9. Kwa nini watu waaminifu walitoa dhabihu za wanyama, na Yehova alionaje dhabihu hizo?
9 Watu waaminifu kuanzia Abeli na kuendelea walimtolea Mungu dhabihu za wanyama. Kwa kufanya hivyo, walionyesha kwamba walitambua kuwapo kwa dhambi na umuhimu wa ukombozi. Walikuwa na imani katika ahadi ya Mungu ya kuwakomboa wanadamu kupitia “uzao” wake. (Mwanzo 3:15; 4:1-4; Mambo ya Walawi 17:11; Waebrania 11:4) Yehova alikubali dhabihu hizo na wakawa na uhusiano mzuri naye. Hata hivyo, matoleo ya wanyama yalikuwa ishara tu ya jambo jingine. Wanyama hawangeweza kufunika kabisa dhambi za wanadamu, kwa kuwa wanyama ni viumbe wa hali ya chini wanapolinganishwa na wanadamu. (Zaburi 8:4-8) Hivyo basi, Biblia yasema hivi: “Haiwezekani damu ya mafahali na ya mbuzi kuziondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Dhabihu hizo zilikuwa mifano tu ya dhabihu ya kweli ya fidia ambayo ingetolewa.
“Fidia Inayolingana”
10. (a) Mfidi alihitaji kulingana na nani, na kwa nini? (b) Kwa nini ni mwanadamu mmoja tu aliyehitaji kutolewa dhabihu?
10 Mtume Paulo alisema kwamba “katika Adamu wote wanakufa.” (1 Wakorintho 15:22) Kwa hiyo mtu aliyelingana kabisa na Adamu—mwanadamu mkamilifu—alihitaji kufa ili kutoa fidia. (Waroma 5:14) Hakuna kiumbe mwingine yeyote ambaye angeweza kusawazisha mizani ya haki. Ni mwanadamu mkamilifu peke yake, mtu ambaye hakurithi dhambi ya Adamu, ndiye tu aliyeweza kutoa “fidia inayolingana” kikamili kabisa na Adamu. (1 Timotheo 2:6) Hakungekuwa na uhitaji wa mamilioni ya wanadamu kutolewa dhabihu ili kumkomboa kila mzao wa Adamu. Mtume Paulo alieleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” (Waroma 5:12) Na “kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu,” Mungu alifanya mpango wa kuwakomboa wanadamu “kupitia mwanadamu.” (1 Wakorintho 15:21) Jinsi gani?
“Fidia inayolingana kwa ajili ya wote”
11. (a) Mfidi ‘angeonja kifo kwa ajili ya kila mtu’ jinsi gani? (b) Kwa nini Adamu na Hawa hawangefaidika kutokana na fidia? (Ona kielezi-chini.)
11 Yehova alipanga mwanadamu mmoja mkamilifu adhabihu uhai wake kwa hiari. Andiko la Waroma 6:23 lasema, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” Mfidi huyo ‘angeonja kifo kwa ajili ya kila mtu’ kwa kudhabihu uhai wake. Yaani, angelipa mshahara wa dhambi ya Adamu. (Waebrania 2:9; 2 Wakorintho 5:21; 1 Petro 2:24) Kufanya hivyo kungekuwa na matokeo makubwa kisheria. Fidia ingekomesha kabisa dhambi yenye kuangamiza kwa kuwaondolea wazao watiifu wa Adamu hukumu ya kifo.a—Waroma 5:16.
12. Toa mfano ambao unaonyesha jinsi watu wengi wanavyoweza kufaidika baada ya deni moja kulipwa.
12 Kwa mfano: Wazia kwamba wakazi wengi wa mji wenu wameajiriwa katika kiwanda kikubwa. Wewe na jirani zako mnalipwa mshahara mnono na mnaishi raha mustarehe. Siku moja kiwanda hicho kinafungwa kabisa na mambo yanabadilika. Kwa nini? Kiwanda hicho kimefilisika kwa sababu ya ufisadi wa meneja wake. Kwa ghafula, wewe na jirani zako mnafutwa kazi na hamwezi kulipa madeni yenu. Wenzi wa ndoa, watoto, na wakopeshaji wanateseka kwa sababu ya ufisadi wa mtu mmoja tu. Je, kuna suluhisho? Ndiyo! Mfadhili tajiri anaamua kuwasaidia. Anajua umuhimu wa kiwanda hicho. Anawahurumia pia watu wote walioajiriwa humo na familia zao. Kwa hiyo anapanga kulipa deni la kampuni hiyo ili kiwanda kifunguliwe. Kulipwa kwa deni hilo kunawafaidi watu wote walioajiriwa humo, familia zao na wakopeshaji. Vivyo hivyo, kulipwa kwa deni la Adamu kunawafaidi mamilioni ya watu.
Ni Nani Anayetoa Fidia?
13, 14. (a) Yehova aliwaandalia wanadamu fidia jinsi gani? (b) Ni nani anayelipwa fidia, na kwa nini malipo hayo ni muhimu?
13 Ni Yehova peke yake angeweza kumtoa “Mwana-Kondoo . . . ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29) Lakini Yehova hakumtuma malaika yeyote tu aje kuwaokoa wanadamu. Badala yake, alimtuma Yule ambaye angeweza kujibu kikamili na kwa uhakika shtaka la Shetani dhidi ya watumishi wa Yehova. Naam, Yehova alijitoa kabisa kwa kumtuma Mwanaye mzaliwa-pekee, ‘aliyekuwa furaha yake.’ (Mithali 8:30) Kwa hiari, Mwana wa Mungu “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu” kwa kuacha mwili wake wa kimbingu. (Wafilipi 2:7) Yehova alihamisha kimuujiza uhai na utu wa Mwanaye mzaliwa wa kwanza wa mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi aliyeitwa Maria. (Luka 1:27, 35) Akiwa mwanadamu, angeitwa Yesu. Lakini kisheria, angeweza kuitwa Adamu wa pili, kwa kuwa alilingana kikamili na Adamu. (1 Wakorintho 15:45, 47) Kwa hiyo, Yesu aliweza kujitoa mwenyewe kuwa dhabihu ya fidia kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi.
14 Ni nani ambaye angelipwa fidia? Zaburi 49:7 yasema wazi kwamba “Mungu” ndiye anayelipwa fidia. Lakini ni Yehova anayefanya mpango wa fidia, sivyo? Ndivyo, lakini hilo halimaanishi kwamba fidia ni badilishano lisilo na kusudi wala maana—kama kutoa pesa katika mfuko mmoja na kuzitia katika mfuko mwingine. Ni lazima tuelewe kwamba fidia si badilishano halisi, bali ni badilishano la kisheria. Yehova alithibitisha kwamba anafuata kabisa haki yake kamilifu kwa kulipa fidia, ijapokuwa ilimgharimu sana.—Mwanzo 22:7, 8, 11-13; Waebrania 11:17; Yakobo 1:17.
15. Kwa nini ilikuwa lazima Yesu ateseke na kufa?
15 Katika masika ya mwaka wa 33 W.K., Yesu Kristo alijitolea kuteseka ili alipe fidia. Alijiruhusu kukamatwa kwa mashtaka ya uwongo, kuhukumiwa kuwa na hatia, na kupigiliwa misumari kwenye mti wa mateso. Je, ilikuwa lazima Yesu apatwe na mateso hayo makali? Ndiyo, kwa sababu suala la uaminifu wa watumishi wa Mungu lilihitaji kuamuliwa. Mungu hakumruhusu Herode amwue Yesu akiwa mtoto mchanga. (Mathayo 2:13-18) Lakini akiwa mtu mzima, Yesu aliweza kuvumilia mashambulizi makali ya Shetani akiwa na ujuzi kamili wa masuala yaliyohusika.b Yesu alithibitisha waziwazi kwamba Yehova ana watumishi wanaobaki waaminifu chini ya majaribu kwa sababu ajapoteswa vibaya sana, aliendelea kuwa “mwaminifu-mshikamanifu, asiye na hila, asiyetiwa unajisi, aliyetengwa na watenda-dhambi.” (Waebrania 7:26) Ndiyo sababu kabla tu ya kufa, Yesu alipaaza kilio kwa ushindi: “Imetimizwa!”—Yohana 19:30.
Kumaliza Kazi Yake ya Ukombozi
16, 17. (a) Yesu aliendeleaje na kazi yake ya ukombozi? (b) Kwa nini ilikuwa lazima Yesu aonekane “mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu”?
16 Yesu hakuwa amemaliza kazi yake ya ukombozi. Yehova alimfufua Yesu siku ya tatu baada ya kufa. (Matendo 3:15; 10:40) Kupitia tendo hilo muhimu sana, Yehova alimthawabisha Mwanaye kwa sababu alimtumikia kwa uaminifu. Pia alimpa nafasi ya kumaliza kazi yake ya ukombozi akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu wa Mungu. (Waroma 1:4; 1 Wakorintho 15:3-8) Mtume Paulo aeleza hivi: “Kristo alipokuja akiwa kuhani wa cheo cha juu . . . , aliingia, si kwa damu ya mbuzi na ya mafahali wachanga, sivyo, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote ndani ya mahali patakatifu na kupata ukombozi udumuo milele kwa ajili yetu. Kwa maana Kristo aliingia, si mahali patakatifu palipofanywa kwa mikono, ambapo ni nakala ya uhalisi, bali mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu.”—Waebrania 9:11, 12, 24.
17 Kristo hakuweza kupeleka damu yake halisi mbinguni. (1 Wakorintho 15:50) Badala yake, alipeleka kile kilichofananishwa na damu hiyo: thamani halali ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uliotolewa dhabihu. Halafu, akiwa mbele ya uso wa Mungu, alitoa rasmi thamani ya uhai wake iwe fidia ya kuwakomboa wanadamu wenye dhambi. Je, Yehova alikubali dhabihu hiyo? Ndiyo, na hilo lilithibitishwa wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi 120 hivi huko Yerusalemu wakati wa Pentekoste ya 33 W.K. (Matendo 2:1-4) Ingawa tukio hilo lilikuwa lenye kusisimua sana, fidia ilikuwa tu imeanza kuwafaidi wanadamu kwa njia kubwa ajabu.
Faida za Fidia
18, 19. (a) Ni vikundi gani viwili vya watu vinavyonufaika na upatanisho ambao umewezeshwa na damu ya Kristo? (b) Fidia inawafaidije wale wa “umati mkubwa,” sasa na wakati ujao?
18 Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo aeleza kwamba Mungu aliona vema kupitia Kristo kupatanisha kwake Mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu ya Yesu iliyomwagwa juu ya mti wa mateso. Paulo aeleza pia kwamba upatanisho huo unahusu vikundi viwili vya watu, yaani, “vitu vilivyomo katika mbingu” na “vitu vilivyo duniani.” (Wakolosai 1:19, 20; Waefeso 1:10) Kikundi cha kwanza ni cha Wakristo 144,000 ambao wanapewa tumaini la kutumikia wakiwa makuhani mbinguni na kutawala juu ya dunia pamoja na Kristo Yesu. (Ufunuo 5:9, 10; 7:4; 14:1-3) Kupitia wao, wanadamu watiifu watapata manufaa ya dhabihu hatua kwa hatua katika kipindi cha miaka 1,000.—1 Wakorintho 15:24-26; Ufunuo 20:6; 21:3, 4.
19 “Vitu vilivyo duniani” ni watu wanaotarajia kufurahia maisha makamilifu katika Paradiso duniani. Andiko la Ufunuo 7:9-17 linawaita “umati mkubwa” ambao utaokoka “dhiki kubwa” inayokuja. Lakini si lazima wangoje hadi wakati huo ili wanufaike na fidia. Tayari “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Hata sasa wanapata faida za kiroho za mpango huo wa upendo kwa sababu wanadhihirisha imani katika fidia. Wamehesabiwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu! (Yakobo 2:23) Kwa sababu ya dhabihu ya Yesu, wanaweza ‘kukaribia kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa.’ (Waebrania 4:14-16) Wanapokosea, wanasamehewa kikweli. (Waefeso 1:7) Wana dhamiri safi ijapokuwa hawajakamilika. (Waebrania 9:9; 10:22; 1 Petro 3:21) Kwa hiyo, kupatanishwa na Mungu si tukio tu la wakati ujao, bali ni jambo linalotukia leo! (2 Wakorintho 5:19, 20) Katika kile kipindi cha miaka 1,000, ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ hatua kwa hatua na mwishowe ‘watakuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Waroma 8:21.
20. Wewe unahisije unapotafakari juu ya fidia?
20 “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo” kwa ajili ya fidia! (Waroma 7:25) Mpango wa fidia ni rahisi sana, lakini ni wa hali ya juu sana hivi kwamba unatustaajabisha. (Waroma 11:33) Tunapotafakari na kuthamini sana fidia, mioyo yetu inatuchochea kumkaribia zaidi Mungu wa haki. Kama mtunga-zaburi, tuna sababu nyingi sana za kumsifu Yehova ambaye ‘anapenda haki na hukumu.’—Zaburi 33:5.
a Adamu na Hawa hawangefaidika kutokana na fidia. Sheria ya Musa ilisema hivi kumhusu mwuaji wa kukusudia: “Msipokee fidia kwa ajili ya uhai wa mwuaji, ambaye amekuwa na hatia ya mauti.” (Hesabu 35:31) Ni wazi kwamba Adamu na Hawa walistahili kufa kwa sababu walikataa kimakusudi kumtii Mungu. Hivyo wakapoteza tumaini lao la kuishi milele.
b Ili kufutilia mbali dhambi ya Adamu, Yesu alilazimika kufa akiwa mtu mzima mkamilifu wala si mtoto mkamilifu. Kumbuka kwamba Adamu alitenda dhambi kimakusudi, alijua vizuri kabisa ubaya na matokeo ya tendo lake. Kwa hiyo, ili kuwa “Adamu wa mwisho” na kufunika dhambi hiyo, Yesu alihitaji kuamua kudumisha uaminifu wake kwa Yehova kupatana na ujuzi aliokuwa nao. (1 Wakorintho 15:45, 47) Kwa hiyo, maisha ya Yesu ya uaminifu akiwa duniani kutia ndani kifo chake cha dhabihu yalikuwa “tendo moja la kutetewa kuwa haki.”—Waroma 5:18, 19.
-
-
Yesu ‘Aimarisha Haki Duniani’Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 15
Yesu ‘Aimarisha Haki Duniani’
1, 2. Yesu alikasirika pindi gani, na kwa nini?
YESU alikuwa amekasirika sana, na kwa sababu nzuri. Huenda ikawa vigumu kuwazia kwamba Yesu ambaye alikuwa mpole sana angeweza kukasirika. (Mathayo 21:5) Bila shaka alijidhibiti kikamili kwa kuwa hasira yake ilikuwa adilifu.a Lakini ni nini kilichomkasirisha mwanamume huyo aliyependa amani? Alikasirishwa na ukosefu mbaya wa haki.
2 Yesu alipenda mno hekalu la Yerusalemu. Lilikuwa ndilo jengo pekee takatifu ulimwenguni pote lililowekwa wakfu kwa ajili ya ibada ya Baba yake wa mbinguni. Wayahudi walisafiri kutoka nchi nyingi za mbali ili kuabudu huko. Hata watu wasio Wayahudi ambao walimcha Mungu walikuja katika ua wa hekalu uliotengwa kwa ajili yao. Lakini mapema katika huduma yake, Yesu aliingia hekaluni na kuona hali yenye kusikitisha sana. Hekalu lilikuwa kama soko badala ya kuwa nyumba ya ibada! Umati mkubwa wa wafanyabiashara na wavunja-fedha ulijaa hekaluni. Lakini kulikuwaje na ukosefu wa haki? Watu hao waliona hekalu la Mungu kuwa mahali pa kuwalaghai watu—hata kuwaibia. Jinsi gani?—Yohana 2:14.
3, 4. Ni ulaghai gani wa pupa ulioendelea katika nyumba ya Yehova, na Yesu alichukua hatua gani kuukomesha?
3 Viongozi wa kidini walikuwa wameamua kwamba ni aina moja tu ya sarafu ingeweza kutumiwa kulipa kodi ya hekalu. Wageni walilazimika kuvunja fedha zao ili kupata sarafu hizo. Kwa hiyo, wavunja-fedha walifanyia kazi yao hekaluni, na walitoza malipo fulani kwa ajili ya kuvunja fedha. Biashara ya kuuza wanyama ilileta faida kubwa pia. Wageni waliotaka kutoa dhabihu wangeweza kununua wanyama kutoka kwa mfanyabiashara yeyote mjini, lakini huenda wakuu wa hekalu wangekataa dhabihu hizo eti hazifai. Lakini, walikubali mara moja wanyama wa dhabihu walionunuliwa hekaluni. Nyakati nyingine watu hao wasio na uwezo waliuziwa wanyama kwa bei ghali sana.b Biashara hiyo ilikuwa mbaya kuliko ulaghai. Ulikuwa unyang’anyi!
“Ondoleeni mbali vitu hivi kutoka hapa!”
4 Yesu hakuweza kuvumilia ukosefu huo wa haki. Hiyo ilikuwa nyumba ya Baba yake! Alisokota mjeledi wa kamba akafukuza makundi ya ng’ombe na kondoo kutoka hekaluni. Kisha akazipindua meza za wavunja-fedha. Hebu wazia jinsi sarafu hizo zote zilivyobingirika kotekote kwenye sakafu ya marumaru! Akawaamuru hivi kwa ukali wale wauza-njiwa: “Ondoleeni mbali vitu hivi kutoka hapa!” (Yohana 2:15, 16) Yaonekana hakuna yeyote aliyethubutu kumpinga mwanamume huyo jasiri.
Mwana Humwiga Baba
5-7. (a) Maisha ya Yesu kabla ya kuwa mwanadamu yaliboreshaje sifa yake ya haki, na mfano wake unatufundisha nini? (b) Yesu amepambanaje na ukosefu wa haki kuelekea jina na enzi kuu ya Yehova?
5 Bila shaka, wafanyabiashara hao walirudi hekaluni. Miaka mitatu hivi baadaye, Yesu alishutumu tena ukosefu wao wa haki, alimnukuu Yehova ambaye aliwakemea wale waliofanya nyumba Yake kuwa “pango la wapokonyaji .” (Mathayo 21:13; Yeremia 7:11) Naam, Yesu alipoona watu wakipokonywa mali yao kwa pupa na hekalu la Mungu likitiwa unajisi, alihisi kama Baba yake. Na hilo halitushangazi. Kwa sababu Yesu alifundishwa na Baba yake wa mbinguni kwa mamilioni ya miaka. Hivyo, akawa na maoni kama ya Yehova kuhusu haki. Alionyesha kikweli jinsi ambavyo mwana anamwiga kabisa baba yake. Kwa hiyo, ikiwa twataka kuelewa vizuri zaidi haki ya Yehova, hatuna budi kutafakari mfano wa Yesu Kristo.—Yohana 14:9, 10.
6 Mwana huyo mzaliwa pekee alikuwapo Shetani alipomsingizia Yehova Mungu kuwa mwongo na kutilia shaka uadilifu wa utawala Wake. Ulikuwa uchongezi mbaya kama nini! Mwana huyo pia alimsikia Shetani akidai baadaye kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumtumikia Yehova kwa sababu anampenda na bila ubinafsi. Hapana shaka kwamba mashtaka hayo ya uwongo yalimtia uchungu Mwana huyo mwadilifu. Haikosi alifurahi sana alipojua kwamba angetimiza kazi muhimu sana ya kufutilia mbali mashtaka hayo ya uwongo! (2 Wakorintho 1:20) Angefanyaje hivyo?
7 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 14, Yesu Kristo alijibu kikamili na kwa uhakika shtaka la Shetani ambalo lilitilia shaka uaminifu wa viumbe wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, Yesu aliweka msingi wa kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova na kutakaswa kwa jina Lake hatimaye. Akiwa Wakili Mkuu wa Yehova, Yesu ataimarisha haki Yake katika ulimwengu wote mzima. (Matendo 5:31) Vilevile, alidhihirisha haki ya Mungu kupitia maisha yake duniani. Yehova alisema hivi kumhusu: “Nitaweka roho yangu juu yake, na lililo haki atafanya kuwa wazi kwa mataifa.” (Mathayo 12:18) Yesu alitimizaje maneno hayo?
Yesu Afafanua “Lililo Haki”
8-10. (a) Mapokeo ya viongozi wa kidini Wayahudi yaliwadharau wanawake na watu wasio Wayahudi jinsi gani? (b) Mapokeo yaliifanyaje sheria ya Yehova ya Sabato iwe yenye kulemea?
8 Yesu aliipenda Sheria ya Yehova, naye aliishi kupatana nayo. Lakini viongozi wa kidini wa siku zake waliipotosha Sheria hiyo na kuitumia vibaya. Yesu aliwaambia hivi: “Ole wenu nyinyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! . . . Mmepuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.” (Mathayo 23:23) Ni wazi kabisa kwamba walimu hao wa Sheria ya Mungu hawakuwa wakionyesha wazi “lililo haki.” Badala yake, walikuwa wakiipotosha haki ya Mungu. Jinsi gani? Fikiria mifano kadhaa.
9 Yehova aliwaagiza watu wake wajitenge na mataifa jirani ya kipagani. (1 Wafalme 11:1, 2) Hata hivyo, viongozi fulani washupavu wa kidini waliwatia watu moyo wawachukie watu wote wasio Wayahudi. Mishnah ilikuwa na sheria hii: “Ngo’mbe hawapaswi kuachwa kwenye hoteli ya watu wasio Wayahudi kwa sababu wanashukiwa kufanya ngono na wanyama.” Chuki yao kwa watu wote wasio Wayahudi ilikiuka haki na kusudi la Sheria ya Musa. (Mambo ya Walawi 19:34) Sheria nyingine zilizotungwa na wanadamu ziliwadharau wanawake. Mapokeo yalisema kwamba mke anapaswa kutembea nyuma ya mume wake wala si kando yake. Mwanamume hakuruhusiwa kuongea na mwanamke hadharani, hata iwe ni mke wake. Wanawake hawakuruhusiwa kutoa ushahidi kortini, hali moja na watumwa. Hata kulikuwa na sala maalumu ambayo wanaume walitoa na kumshukuru Mungu kwamba hawakuwa wanawake.
10 Viongozi hao wa kidini walificha Sheria ya Mungu kwa sheria na maagizo mengi sana yaliyotungwa na wanadamu. Kwa mfano, sheria ya Sabato ilikataza kazi isifanywe siku ya Sabato. Siku hiyo ilitengwa kwa ajili ya ibada, burudisho la kiroho, na kupumzika. Lakini Mafarisayo waliifanya sheria hiyo iwe yenye kulemea. Wao ndio walioamua mambo hususa ambayo yangeonwa kuwa “kazi.” Walitaja kihususa shughuli 39 kuwa kazi, kama vile kuvuna au kuwinda. Mambo hayo yalizusha maswali mengi sana. Je, mtu aliyemwua kiroboto siku ya Sabato, alikuwa akiwinda? Je, mtu aliyekwanyua punje chache ili ale akitembea, alikuwa akivuna? Je, mtu aliyemponya mgonjwa, alikuwa akifanya kazi? Walitunga sheria nyingi ngumu ambazo zilijibu maswali hayo.
11, 12. Yesu alipingaje mapokeo yasiyo ya kimaandiko ya Mafarisayo?
11 Katika hali hizo, Yesu aliwasaidiaje watu kuelewa maana ya haki? Kwa ujasiri, Yesu aliwashutumu viongozi hao wa kidini kupitia mafundisho na maisha yake. Kwanza angalia baadhi ya mafundisho yake. Alilaani waziwazi sheria zao nyingi zilizotungwa na wanadamu, aliposema hivi: “Mwalibatilisha neno la Mungu kwa mapokeo yenu ambayo nyinyi mlikabidhiwa.”—Marko 7:13.
12 Yesu alifundisha waziwazi kwamba Mafarisayo hawakuelewa sheria ya Sabato—na hata hawakufahamu kusudi la sheria hiyo. Aliwaambia kwamba Mesiya ni “Bwana wa sabato” na kwa hiyo alikuwa na haki ya kuwaponya watu siku ya Sabato. (Mathayo 12:8) Alikazia jambo hilo kwa kuwaponya watu kimuujiza na waziwazi siku ya Sabato. (Luka 6:7-10) Maponyo hayo yalionyesha maponyo ambayo atafanya duniani pote wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja. Miaka hiyo Elfu itakuwa Sabato kuu, wakati ambapo wanadamu wote waaminifu watapumzika hatimaye baada ya kulemewa na dhambi na kifo kwa karne nyingi sana.
13. Ni sheria gani iliyoanza mwishoni mwa huduma ya Kristo duniani, na ilitofautianaje na Sheria ya Musa?
13 Yesu pia alionyesha wazi lililo haki kupitia sheria mpya, “sheria ya Kristo,” ambayo ilianza mwishoni mwa huduma yake duniani. (Wagalatia 6:2) Tofauti na Sheria ya Musa, sheria hii mpya ilitegemea hasa kanuni wala si amri nyingi zilizoandikwa. Hata hivyo, ilitia ndani amri fulani za moja kwa moja. Yesu aliita mojawapo ya amri hizo “amri mpya.” Yesu aliwafundisha wafuasi wake wote wapendane kama alivyowapenda. (Yohana 13:34, 35) Ndiyo, wote wanaoishi kupatana na “sheria ya Kristo” wangekuwa na upendo huo wa kujidhabihu.
Mfano Halisi wa Haki
14, 15. Yesu alionyeshaje kwamba alitambua mipaka ya mamlaka yake, na kwa nini hilo linatia moyo?
14 Yesu hakuwafundisha watu kuhusu upendo tu. Aliishi kupatana na “sheria ya Kristo.” Aliionyesha waziwazi katika maisha yake. Fikiria njia tatu ambazo mfano wa Yesu ulionyesha wazi lililo haki.
15 Kwanza, Yesu aliepuka kabisa ukosefu wa haki. Labda umeona kwamba mara nyingi watu wasiokamilika hutenda isivyo haki wanapokuwa na kiburi na kuvuka mipaka ya mamlaka yao. Yesu hakufanya hivyo. Pindi moja, mtu mmoja alimwendea Yesu na kumwambia: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu anigawie urithi.” Yesu alimjibuje? “Wewe mtu, nani aliyeniweka mimi rasmi hakimu au mgawaji-fungu juu ya nyinyi watu?” (Luka 12:13, 14) Je, hilo si jambo la kustaajabisha? Uwezo wa Yesu wa kufikiri na kufanya maamuzi, na hata mamlaka aliyopewa na Mungu ilizidi mamlaka ya mtu yeyote duniani; lakini, alikataa kuingilia jambo hilo kwa sababu hakuwa amepewa mamlaka hususa ya kufanya hivyo. Yesu amekuwa mnyenyekevu daima, hata kwa maelfu ya miaka aliyoishi kabla ya kuwa mwanadamu. (Yuda 9) Kwa unyenyekevu, Yesu humtumaini Yehova aamue lililo haki. Jambo hilo linaonyesha kwamba ana sifa zinazovutia.
16, 17. (a) Yesu alionyeshaje haki alipohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu? (b) Yesu alionyeshaje kwamba haki yake ilikuwa yenye rehema?
16 Pili, Yesu alionyesha haki alipohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Hakuwa na ubaguzi. Badala yake, alijitahidi sana kuwahubiria watu wa kila aina, matajiri kwa maskini. Tofauti na Yesu, Mafarisayo waliwapuuza watu maskini wa kawaida na kuwaita kwa madharau ʽam-ha·ʼaʹrets, yaani, “watu wa ardhi.” Kwa ujasiri, Yesu alipinga ukosefu huo wa haki. Alipowafundisha watu habari njema, alipokula nao, alipowalisha, alipowaponya, au hata kuwafufua, aliunga mkono haki ya Mungu ambaye anataka “watu wa namna zote” waokolewe.c—1 Timotheo 2:4.
17 Tatu, Yesu alionyesha haki yenye rehema nyingi. Alijitahidi sana kuwasaidia watenda-dhambi. (Mathayo 9:11-13) Alikuwa tayari kuwasaidia watu ambao hawangeweza kujilinda. Kwa mfano, Yesu hakuwa kama viongozi wa kidini ambao waliwashuku watu wote wasio Wayahudi. Aliwasaidia na kuwafundisha baadhi yao kwa rehema, hata ingawa alitumwa hasa kwa Wayahudi. Alikubali kumponya kimuujiza mtumishi wa ofisa mmoja wa jeshi la Roma, na kusema: “Kwa yeyote katika Israeli sijapata imani kubwa sana kadiri hii.”—Mathayo 8:5-13.
18, 19. (a) Yesu aliwaheshimu wanawake kwa njia gani? (b) Mfano wa Yesu unatusaidiaje kuona uhusiano uliopo kati ya ujasiri na haki?
18 Vilevile, Yesu hakuunga mkono maoni yaliyoenea kuhusu wanawake. Badala yake, alitenda yaliyo haki kwa ujasiri. Wanawake Wasamaria walionwa kuwa wachafu kama watu wasio Wayahudi. Hata hivyo, Yesu hakusita kumhubiria yule mwanamke Msamaria penye kisima cha Sikari. Kwa kweli, Yesu alijitambulisha waziwazi kwa mara ya kwanza kuwa Mesiya aliyeahidiwa alipoongea na mwanamke huyo. (Yohana 4:6, 25, 26) Mafarisayo walisema kwamba wanawake hawakupaswa kufundishwa Sheria ya Mungu, lakini Yesu alitumia wakati mwingi na nguvu kuwafundisha wanawake. (Luka 10:38-42) Na ingawa mapokeo yalisema kwamba wanawake hawawezi kutoa ushahidi unaoaminika, Yesu aliwaheshimu wanawake kadhaa kwa kuwapa nafasi ya pekee ya kuwa watu wa kwanza kumwona baada ya kufufuliwa. Hata aliwaambia wawapashe wanafunzi wake wanaume habari za tukio hilo muhimu sana!—Mathayo 28:1-10.
19 Naam, Yesu alionyesha mataifa lililo haki. Mara nyingi alihatarisha uhai wake kwa kufanya hivyo. Mfano wa Yesu unatusaidia kuona kwamba mtu anahitaji ujasiri ili kudumisha haki ya kweli. Ndiyo sababu aliitwa ifaavyo “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda.” (Ufunuo 5:5) Kumbuka kwamba simba ni mfano ufaao wa haki yenye ujasiri. Hivi karibuni, Yesu atatekeleza haki kwa njia kubwa zaidi, “ataimarisha haki duniani” kwa ukamili zaidi.—Isaya 42:4, BHN.
Mfalme wa Kimesiya ‘Aimarisha Haki Duniani’
20, 21. Katika siku zetu, Mfalme wa Kimesiya ametekelezaje haki duniani pote na katika kutaniko la Kikristo?
20 Tangu alipowekwa kuwa Mfalme wa Kimesiya mwaka wa 1914, Yesu ametekeleza haki duniani. Jinsi gani? Amekuwa na jukumu la kuhakikisha kwamba unabii aliotoa kwenye Mathayo 24:14 unatimizwa. Wafuasi wa Yesu duniani wamewafundisha watu wa nchi zote ukweli kuhusu Ufalme wa Yehova. Kama Yesu, wamehubiri bila ubaguzi na kwa njia ya haki, wakijitahidi kumpa kila mtu—mtoto kwa mzee, tajiri kwa maskini, wanaume kwa wanawake—nafasi ya kumjua Yehova, Mungu wa haki.
21 Yesu, ambaye ni Kichwa cha kutaniko la Kikristo, anatekeleza haki kutanikoni pia. Kama ilivyotabiriwa, anatoa “zawadi zikiwa wanadamu,” yaani, wazee Wakristo waaminifu ambao wanaliongoza kutaniko. (Waefeso 4:8-12) Wanaume hao wanafuata mfano wa Yesu Kristo katika kutekeleza haki wanapolichunga kundi la Mungu lenye thamani sana. Daima wanakumbuka kwamba Yesu anataka kondoo wake watendewe kwa haki bila kujali cheo, umaarufu, au hali yao ya kifedha.
22. Yehova anahisije kuhusu ukosefu wa haki ulioenea ulimwenguni leo, na amemteua Mwanaye achukue hatua gani?
22 Hata hivyo, hivi karibuni Yesu ataimarisha haki duniani kwa njia isiyo na kifani. Ukosefu wa haki umeenea sana katika ulimwengu huu wenye ufisadi. Kila mtoto anayekufa njaa, hufa kwa sababu ya ukosefu wa haki usiovumilika hasa tunapozingatia kwamba pesa nyingi sana na wakati hutumiwa kutengeneza silaha za vita na kutosheleza tamaa za ubinafsi za watu wanaopenda raha. Mamilioni ya watu wanaokufa bure kila mwaka ni mojawapo tu ya mambo mengi yanayoonyesha ukosefu wa haki uliopo. Mambo hayo yote huchochea hasira adilifu ya Yehova. Amemteua Mwanaye apigane vita ya haki dhidi ya mfumo huu mwovu wa mambo na kukomesha kabisa ukosefu wote wa haki.—Ufunuo 16:14, 16; 19:11-15.
23. Baada ya Har-Magedoni, Kristo ataletaje haki kwa umilele wote?
23 Lakini ili kutekeleza haki Yehova anahitaji kufanya mengi zaidi kuliko kuwaangamiza tu waovu. Amemteua pia Mwanaye atawale akiwa “Mfalme wa Amani.” Baada ya vita ya Har-Magedoni, utawala wa Yesu utaleta amani duniani pote, naye atatawala “kwa haki.” (Isaya 9:6, 7) Ndipo Yesu atakapofurahi kukomesha ukosefu wote wa haki ambao umesababisha mateso na maumivu mengi sana ulimwenguni. Atadumisha kwa uaminifu haki kamilifu ya Yehova kwa umilele wote. Basi, ni muhimu kwetu kujitahidi kuiga haki ya Yehova sasa. Hebu tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.
a Katika kuonyesha hasira adilifu, Yesu alimwiga Yehova, aliye “mwingi wa hasira” kuelekea uovu wote. (Nahumu 1:2) Kwa mfano, baada ya Yehova kuwaambia watu wake waasi kwamba walikuwa wamefanya nyumba yake kuwa “pango la wanyang’anyi,” alisema hivi: “Hasira yangu na ghadhabu yangu zitamwagwa juu ya mahali hapa.”—Yeremia 7:11, 20.
b Mishnah inasema kwamba miaka kadhaa baadaye watu walilalamika kwa sababu njiwa waliuzwa kwa bei ghali sana hekaluni. Kisha bei ikapunguzwa mara moja kwa asilimia 99! Ni nani waliopata faida kubwa kutokana na biashara hiyo yenye ufanisi? Wanahistoria fulani wanadokeza kwamba masoko ya hekaluni yalimilikiwa na jamaa ya Anasi yule Kuhani wa Cheo cha Juu. Jamaa hiyo ya kikuhani ilipata ufanisi mkubwa sana kutokana na masoko hayo.—Yohana 18:13.
c Mafarisayo waliamini kwamba watu wa hali ya chini, ambao hawakujua Sheria, walikuwa watu “waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Walisema kwamba mtu hakupaswa kuwafundisha watu hao wala kufanya biashara nao wala kula nao wala kusali nao. Walisema kwamba mtu akimruhusu binti yake aolewe na mmoja wao lingekuwa jambo baya kuliko kumpeleka kwa wanyama wakali sana. Waliamini kwamba watu hao wa hali ya chini hawatafufuliwa.
-
-
‘Tenda Haki’ Unapotembea na MunguMkaribie Yehova
-
-
Sura ya 16
‘Tenda Haki’ Unapotembea na Mungu
1-3. (a) Kwa nini tunapaswa kumshukuru sana Yehova? (b) Mwokozi wetu mwenye upendo anataka tufanye nini?
JIWAZIE ukiwa ndani ya meli inayozama. Unapoanza kukata tamaa, mtu fulani anawasili na kukuokoa. Unafurahi kama nini mtu huyo anapokuokoa na kusema: “Sasa uko salama”! Je, hungemshukuru sana mtu huyo? Kwa kweli, ungekufa kama hangekuokoa.
2 Kwa njia fulani, mfano huo waonyesha jambo ambalo Yehova ametufanyia. Tunapaswa kumshukuru kwelikweli, kwa sababu ameandaa fidia ambayo inatuwezesha kuokolewa kutoka kwa utumwa wa dhambi na kifo. Tunajihisi tukiwa salama kwa sababu tunajua kwamba maadamu tunadhihirisha imani katika dhabihu hiyo yenye thamani, dhambi zetu zinasamehewa na tunakuwa na tumaini hakika la kuishi milele. (1 Yohana 1:7; 4:9) Kama tulivyoona katika Sura ya 14, fidia ni wonyesho mkuu zaidi wa upendo na haki ya Yehova. Tunapaswa kuionaje?
3 Inafaa tuchunguze mambo ambayo Mwokozi wetu mwenye upendo anataka tufanye. Yehova anasema hivi kupitia nabii Mika: “Amekuonyesha, Ee mutu, nini ni njema, na BWANA anataka nini kwako ila kutenda haki, na kupenda rehema na kutembea kwa unyenyekevu na Mungu wako?” (Mika 6:8, ZSB) Ona kwamba mojawapo ya mambo ambayo Yehova anataka tufanye ni “kutenda haki.” Tutafanyaje hivyo?
Kufuatia “Uadilifu wa Kweli”
4. Tunajuaje kwamba Yehova anatutarajia tuishi kupatana na kanuni zake za uadilifu?
4 Yehova anatutarajia tuishi kupatana na kanuni zake za mema na mabaya. Kwa kuwa kanuni zake ni za haki na za uadilifu, tunapozitii tunafuatia haki na uadilifu. Andiko la Isaya 1:17, ZSB, lasema: “Mujifundishe kufanya mema; mutafute hukumu za haki.” Neno la Mungu linatuhimiza ‘tutafute haki.’ (Sefania 2:3) Linatusihi pia ‘tuvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli.’ (Waefeso 4:24) Uadilifu wa kweli, au haki ya kweli, huchukia jeuri, uovu, na ukosefu wa adili, kwa sababu mambo hayo huchafua mambo matakatifu.—Zaburi 11:5; Waefeso 5:3-5.
5, 6. (a) Kwa nini si vigumu kwetu kuishi kupatana na kanuni za Yehova? (b) Biblia inaonyeshaje kwamba kufuatia uadilifu ni jambo lenye kuendelea?
5 Je, ni vigumu kwetu kuishi kupatana na kanuni za Yehova za uadilifu? La. Mtu anayempenda Yehova haoni matakwa Yake kuwa yenye kulemea. Tunataka kuishi kwa njia inayomfurahisha Mungu wetu kwa sababu tunampenda na tunapenda sifa zake. (1 Yohana 5:3) Kumbuka kwamba Yehova “apenda matendo ya haki.” (Zaburi 11:7) Ikiwa tunataka kuiga kikweli haki au uadilifu wa Mungu, ni lazima tupende mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia yale anayochukia.—Zaburi 97:10.
6 Si rahisi kwa wanadamu wasiokamilika kufuatia uadilifu. Ni lazima tuvue utu wa zamani pamoja na mazoea yake maovu na kujivika utu mpya. Biblia inasema kwamba utu huo mpya “unafanywa kuwa mpya” kupitia ujuzi sahihi. (Wakolosai 3:9, 10) Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “-fanywa kuwa mpya” yanaonyesha kwamba kujivika utu mpya ni jambo lenye kuendelea, ambalo linahitaji jitihada kubwa. Hata tukijitahidi kadiri gani kufanya yaliyo mema, nyakati nyingine tunakosea katika mawazo, maneno, au matendo kwa sababu ya hali yetu ya dhambi.—Waroma 7:14-20; Yakobo 3:2.
7. Tunahitaji kuonaje vipingamizi tunavyokabili tunapojitahidi kufuatia uadilifu?
7 Tunahitaji kuonaje vipingamizi tunavyokabili tunapojitahidi kufuatia uadilifu? Bila shaka hatungetaka kupunguza uzito wa dhambi. Hata hivyo, hatupaswi kamwe kukata tamaa, na kuhisi kwamba hatufai kumtumikia Yehova kwa sababu ya kasoro zetu. Mungu wetu mwenye fadhili amefanya mipango ili kuwasamehe wale wanaotubu kikweli. Fikiria maneno haya yenye kutia moyo ya mtume Yohana: “Nawaandikia nyinyi mambo haya ili msifanye dhambi.” Kisha akataja jambo hili hakika: “Na bado, ikiwa yeyote afanya hasa dhambi [kwa sababu ya kurithi kutokamilika], tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo.” (1 Yohana 2:1) Naam, Yehova ametoa dhabihu ya fidia ya Yesu ili tuweze kumtumikia kwa njia inayofaa licha ya hali yetu ya dhambi. Je, hilo halituchochei kujitahidi kabisa kumpendeza Yehova?
Habari Njema na Haki ya Mungu
8, 9. Kuhubiriwa kwa habari njema kunaonyeshaje haki ya Yehova?
8 Tunaweza kutenda haki—hata kuiga haki ya Mungu—kwa kushiriki kikamili katika kazi ya kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Haki ya Yehova inahusianaje na habari njema?
9 Yehova hataharibu mfumo huu mwovu kabla onyo halijatolewa. Yesu alisema hivi alipotabiri kuhusu matukio ya siku za mwisho: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10; Mathayo 24:3) Neno “kwanza” linamaanisha kwamba kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote itatangulia matukio mengine. Matukio hayo yatia ndani dhiki kubwa iliyotabiriwa, wakati ambapo waovu wataharibiwa ili ulimwengu mpya wenye uadilifu uwepo. (Mathayo 24:14, 21, 22) Bila shaka, hakuna mtu awaye yote anayeweza kudai kwamba Yehova anawaonea waovu. Kwa kuagiza onyo litolewe, anawapa waovu muda wa kutosha wa kubadili njia zao ili wasiangamizwe.—Yona 3:1-10.
Tunaonyesha haki ya Mungu tunapowahubiria wengine habari njema bila ubaguzi
10, 11. Tunaonyeshaje haki ya Mungu tunapohubiri habari njema?
10 Tunaonyeshaje haki ya Mungu tunapohubiri habari njema? Kwanza kabisa, inafaa tufanye yale tuwezayo ili kuwasaidia wengine wapate wokovu. Fikiria tena ule mfano wa kuokolewa kutoka kwenye meli inayozama. Bila shaka ukiwa salama kwenye mashua ya kuokolea, ungejitahidi kuwasaidia wengine ambao wangali baharini. Vivyo hivyo, tuna wajibu wa kuwasaidia wale ambao wangali wanatapatapa katika “bahari” ya ulimwengu huu mwovu. Ni kweli kwamba wengi hukataa ujumbe wetu. Lakini maadamu Yehova anaendelea kuwa mwenye subira, tuna wajibu wa kuwapa nafasi ya ‘kufikia toba’ na hivyo kuwa na tumaini la kupata wokovu.—2 Petro 3:9.
11 Tunapowahubiria watu wote tunaokutana nao habari njema, tunaonyesha haki katika njia nyingine muhimu sana: Kutoonyesha ubaguzi. Kumbuka kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Tunaweza tu kuiga haki Yake kwa kutoonyesha ubaguzi. Badala yake, tunapaswa kuwahubiria wengine habari njema bila kujali kabila lao, cheo chao katika jamii, au hali yao ya kifedha. Hivyo, tunawapa watu wote nafasi ya kusikia na kukubali habari njema.—Waroma 10:11-13.
Jinsi Tunavyowatendea Wengine
12, 13. (a) Kwa nini hatupaswi kufanya haraka kuwahukumu wengine? (b) Shauri la Yesu la ‘kukoma kuhukumu’ na ‘kukoma kulaumu’ linamaanisha nini? (Ona pia kielezi-chini.)
12 Tunaweza pia kuonyesha haki kwa kuwatendea wengine jinsi Yehova anavyotutendea. Ni rahisi sana kuwahukumu wengine, kuchambua makosa yao na kutilia shaka nia yao. Lakini ni nani kati yetu angependa Yehova achambue nia yake na kasoro zake bila huruma? Yehova hatutendei hivyo. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Je, hatuthamini kwamba Mungu wetu mwenye haki na mwenye rehema hakazii fikira makosa yetu? (Zaburi 103:8-10) Hivyo basi, tunapaswa kuwatendeaje wengine?
13 Tukielewa kwamba haki ya Mungu ni yenye rehema, hatutafanya haraka kuwahukumu wengine katika mambo ambayo hayatuhusu au mambo yasiyo na maana sana. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alionya hivi: “Komeni kuhukumu ili msipate kuhukumiwa.” (Mathayo 7:1) Kulingana na simulizi la Luka, Yesu aliongezea hivi: “Komeni kulaumu, nanyi hamtalaumiwa kwa vyovyote.”a (Luka 6:37) Yesu alitambua kwamba wanadamu wasiokamilika wana mwelekeo wa kuhukumu-hukumu. Msikilizaji yeyote aliyekuwapo mwenye tabia ya kuhukumu-hukumu wengine vikali alipaswa kukoma kufanya hivyo.
14. Kwa nini tunapaswa ‘kukoma kuhukumu’ wengine?
14 Kwa nini ni lazima ‘tukome kuhukumu’ wengine? Kwanza, mamlaka yetu ina mipaka. Mwanafunzi Yakobo atukumbusha hivi: “Mmoja yuko ambaye ni mpaji-sheria na hakimu,” yaani, Yehova. Kisha Yakobo anauliza hivi waziwazi: “Wewe ni nani uwe ukihukumu jirani yako?” (Yakobo 4:12; Waroma 14:1-4) Isitoshe, ni rahisi sana kuwahukumu wengine isivyo haki kwa sababu sisi ni wenye dhambi. Mitazamo na mielekeo mbalimbali—kama vile ubaguzi, kuudhika, wivu, na kujiona kuwa mwadilifu—inaweza kupotosha maoni yetu juu ya wanadamu wengine. Hatutafanya haraka kutafuta makosa ya wengine ikiwa tutakumbuka kwamba hata sisi tuna udhaifu. Hatuwezi kusoma mioyo; wala hatuwezi kujua kikamili hali za wengine. Basi, sisi ni nani hata tuwatilie shaka waamini wenzetu au kuchambua jitihada zao za kumtumikia Mungu? Itakuwa vyema tukimwiga Yehova kwa kukazia fikira mambo mazuri ambayo ndugu na dada zetu wanafanya badala ya kutafuta tu kasoro zao.
15. Waabudu wa Yehova hawapaswi kamwe kutenda kwa njia gani na kutumia maneno ya aina gani, na kwa nini?
15 Vipi kuhusu watu wa familia yetu? Inasikitisha kwamba leo hukumu kali zaidi hutolewa nyumbani, mahali ambapo panapaswa kuwa na amani. Ni kawaida kusikia kuhusu waume, wake, au wazazi wakatili ambao huwatukana daima au kuwajeruhi watu wa familia yao. Lakini waabudu wa Mungu hawapaswi kamwe kutumia maneno makali, kufanya mzaha wenye kuumiza, au kuwajeruhi wengine. (Waefeso 4:29, 31; 5:33; 6:4) Shauri la Yesu la ‘kukoma kuhukumu’ na ‘kukoma kulaumu’ linapasa kufuatwa nyumbani pia. Kumbuka kwamba kuonyesha haki kunatia ndani kuwatendea wengine jinsi Yehova anavyotutendea. Na Mungu wetu hatutendei kamwe kwa ukali au kwa ukatili. Badala yake, yeye “ni mwenye wororo sana katika shauku” kwa wale wanaompenda. (Yakobo 5:11) Yeye ni mfano bora sana wa kuiga!
Wazee Wanaotumikia “kwa Haki”
16, 17. (a) Yehova anawatarajia wazee wafanye nini? (b) Ni hatua gani inayopasa kuchukuliwa mtenda-dhambi anapokataa kuonyesha toba ya kweli, na kwa nini?
16 Sote tuna wajibu wa kuonyesha haki, lakini wazee katika kutaniko la Kikristo wana wajibu wa pekee wa kufanya hivyo. Hebu ona maelezo ya kiunabii yaliyoandikwa na Isaya kuhusu “wakuu,” au wazee: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu (“haki,” NW).” (Isaya 32:1) Naam, Yehova anawatarajia wazee watumikie kwa njia ya haki. Wanaweza kufanya hivyo jinsi gani?
17 Wanaume hao wenye sifa za ustahili wa kiroho wanajua kwamba ili kudumisha haki, au uadilifu, ni lazima wadumishe usafi kutanikoni. Nyakati nyingine, wazee wanalazimika kuwahukumu wale wanaotenda dhambi nzito. Wanapofanya hivyo, wanakumbuka kwamba Mungu huonyesha haki na rehema inapowezekana. Kwa hiyo, wanajaribu kumsaidia mtenda-dhambi aonyeshe toba. Lakini vipi ikiwa mtenda-dhambi anakataa kuonyesha toba ya kweli licha ya jitihada za kumsaidia? Neno la Yehova linaagiza kwamba hatua thabiti ya haki ichukuliwe: “Ondoeni yule mtu mwovu miongoni mwenu wenyewe.” Hilo lamaanisha kumtenga na ushirika wa kutaniko. (1 Wakorintho 5:11-13; 2 Yohana 9-11) Wazee wanahuzunika sana wanapolazimika kuchukua hatua hiyo, lakini wanatambua kwamba ni sharti wafanye hivyo ili kudumisha usafi wa kiadili na wa kiroho wa kutaniko. Hata hivyo, wanatumaini kwamba siku moja mtenda-dhambi huyo atarudiwa na fahamu na kurejea kutanikoni.—Luka 15:17, 18.
18. Wazee wanakumbuka nini wanapowashauri wengine kwa kutegemea Biblia?
18 Kutumikia kwa njia ya haki kunatia ndani pia kutoa shauri linalotegemea Biblia inapohitajika. Bila shaka, wazee hawajaribu kutafuta kasoro za wengine. Wala hawatumii kila nafasi wanayopata ili kutoa shauri. Lakini mwamini mwenzao anaweza ‘kuchukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua.’ Wazee ‘watajaribu kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole’ huku wakikumbuka kwamba Mungu anatekeleza haki kwa kujali hisia za wengine wala si kwa ukatili. (Wagalatia 6:1) Kwa hiyo, wazee hawatamfokea mkosaji wala kumshutumu kwa maneno makali. Badala yake, mtu hutiwa moyo na shauri linalotolewa kwa njia ya upendo. Hata wanapotoa shauri la moja kwa moja linaloonyesha waziwazi matokeo ya kufuata mwenendo usiofaa, wazee wanakumbuka kwamba mwamini mwenzao aliyekosea ni kondoo wa kundi la Yehova.b (Luka 15:7) Shauri au karipio linapotolewa kwa njia ya upendo, yaelekea kwamba litamrekebisha mkosaji.
19. Wazee hufanya maamuzi gani, na maamuzi hayo yanapasa kutegemea nini?
19 Mara nyingi wazee hufanya maamuzi yanayowahusu waamini wenzao. Kwa mfano, pindi kwa pindi wazee hukutana ili kuona iwapo ndugu wengine kutanikoni wanastahili kupendekezwa kuwa wazee au watumishi wa huduma. Wazee wanajua umuhimu wa kutopendelea. Wanafuata matakwa ya Mungu wanapowapendekeza wengine, na hawategemei maoni yao binafsi. Hivyo, wanaamua “bila kuhukumu mapema, bila kufanya jambo lolote kulingana na mwelekeo wenye kuegemea upande.”—1 Timotheo 5:21.
20, 21. (a) Wazee wanajitahidi kuwa nini, na kwa nini? (b) Wazee wanawezaje kusaidia “nafsi zilizoshuka moyo”?
20 Wazee huonyesha haki ya Mungu katika njia nyinginezo pia. Baada ya kutabiri kwamba wazee wangetumikia “kwa haki,” Isaya aliongeza hivi: “Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:2) Basi, wazee hujitahidi kuwafariji na kuwaburudisha waabudu wenzao.
21 Wengi wanahitaji kutiwa moyo leo kwa sababu ya matatizo mengi ambayo yanavunja moyo. Wazee, mnawezaje kusaidia “nafsi zilizoshuka moyo”? (1 Wathesalonike 5:14) Wasikilizeni mkiwa na hisia-mwenzi. (Yakobo 1:19) Huenda wakataka kuzungumza na mtu fulani wanayemtumaini kuhusu “wasiwasi” ulio katika moyo wao. (Mithali 12:25, BHN) Wahakikishieni kwamba wanahitajiwa, wanathaminiwa, na wanapendwa na Yehova na vilevile na ndugu na dada zao. (1 Petro 1:22; 5:6, 7) Zaidi ya hayo, mnaweza kusali pamoja nao na kwa ajili yao. Wanaweza kupata faraja sana wanapomsikia mzee akisali kwa hisia sana kwa niaba yao. (Yakobo 5:14, 15) Mungu mwenye haki anathamini jitihada zenu za upendo za kuwasaidia walioshuka moyo.
Wazee huonyesha haki ya Yehova wanapowatia moyo wale walioshuka moyo
22. Tunaweza kuiga haki ya Yehova katika njia zipi, na matokeo yatakuwa nini?
22 Kwa kweli, tunamkaribia Yehova zaidi tunapoiga haki yake! Tunaonyesha haki ya Mungu tunapofuata kanuni zake za haki, tunapowahubiria wengine habari njema zinazookoa uhai, na tunapokazia fikira mambo mazuri ambayo wengine wanafanya badala ya kutafuta kasoro zao. Wazee, mnaonyesha haki ya Mungu mnapodumisha usafi wa kutaniko, mnapotoa shauri la Kimaandiko lenye kujenga, mnapofanya maamuzi bila kupendelea, na mnapowatia moyo wale walioshuka moyo. Akiwa mbinguni, Yehova anafurahi kama nini kuona watu wake wakijitahidi kabisa “kutenda haki” wanapotembea na Mungu wao!
-