Ruthu
3 Basi Naomi mama-mkwe wake akamwambia: “Binti yangu, je, sipaswi kukutafutia mahali pa kupumzika,+ ili mambo yapate kukuendea vema? 2 Basi sasa, je, Boazi, ambaye ulikuwa na wanawake wake vijana, si mtu wa ukoo wetu?+ Tazama! Usiku wa leo anapepeta+ shayiri kwenye uwanja wa kupuria. 3 Oga basi, ujipake mafuta,+ uvae nguo yako ya kujitanda,+ na uende mpaka kwenye uwanja wa kupuria. Usijitambulishe kwake mpaka amalize kula na kunywa. 4 Atakapolala, uangalie mahali ambapo atalala; uende ukamfunue miguuni pake, ulale hapo; naye atakuambia jambo utakalofanya.”
5 Basi akamwambia: “Yote ambayo umeniambia nitafanya.” 6 Naye akaenda kwenye uwanja wa kupuria na kufanya yote ambayo mama-mkwe wake alikuwa amemwamuru. 7 Basi Boazi akala na kunywa, nao moyo wake ukachangamka.+ Kisha akaenda kulala mwishoni mwa rundo la nafaka. Kisha Ruthu akaja kisirisiri akamfunua miguuni pake, akalala. 8 Ilipofika usiku wa manane mwanamume huyo akashtuka. Akageuka, na, tazama! mwanamke alikuwa amelala miguuni pake! 9 Ndipo akauliza: “Wewe ni nani?” Naye akajibu: “Mimi ni Ruthu kijakazi wako, basi mfunike kijakazi wako kwa upindo wa nguo yako, kwa maana wewe ni mkombozi.”+ 10 Basi Boazi akasema: “Yehova na akubariki,+ binti yangu. Umeonyesha fadhili zako zenye upendo+ kwa njia bora zaidi mara hii ya mwisho kuliko mara ya kwanza.+ Hukuwafuata vijana, wawe ni wa hali ya chini au matajiri. 11 Basi sasa, binti yangu, usiogope. Yote utakayosema nitakufanyia,+ kwa maana kila mtu aliye katika lango la watu wangu anajua kwamba wewe ni mwanamke bora sana.+ 12 Na sasa ingawa ni kweli kwamba mimi ni mkombozi,+ pia kuna mkombozi aliye wa jamaa ya karibu kuliko mimi.+ 13 Lala hapa usiku wa leo, na asubuhi ikiwa atakukomboa,+ sawa! Basi na akukomboe. Lakini asipotaka kukukomboa, nitakukomboa, mimi mwenyewe, kama anavyoishi Yehova.+ Endelea kulala mpaka asubuhi.”
14 Naye akalala miguuni pake mpaka asubuhi kisha akaamka kabla yeyote hajaweza kumtambua mwingine. Ndipo Boazi akasema: “Usiache ijulikane kwamba mwanamke alikuja kwenye uwanja wa kupuria.”+ 15 Naye akaendelea kusema: “Ulete ushungi ambao umevaa, uutandaze.” Basi Ruthu akautandaza, naye Boazi akampimia vipimo sita vya shayiri na kumtwika, kisha akaenda jijini.
16 Ruthu akaondoka na kuenda kwa mama-mkwe wake, ambaye alimuuliza: “Wewe ni nani, binti yangu?” Ndipo akamwambia kila kitu ambacho mwanamume huyo alikuwa amemfanyia. 17 Kisha akasema: “Vipimo hivi sita vya shayiri alinipa, kwa maana aliniambia, ‘Usiende mikono mitupu kwa mama-mkwe wako.’”+ 18 Basi Naomi akamwambia: “Keti utulie, binti yangu, mpaka utakapojua jinsi jambo hilo litakavyokuwa, kwa maana mwanamume huyo hatapumzika mpaka amalize jambo hilo leo.”+