Ufunuo
22 Naye akanionyesha mto wa maji ya uhai, mwangavu kama fuwele, ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo 2 kuteremka katikati ya njia pana yalo. Na upande huu wa mto na upande ule kulikuwa na miti ya uhai yenye kutokeza mazao kumi na mawili ya matunda, ikitoa matunda yayo kila mwezi. Na majani ya hiyo miti yalikuwa ya kuponya mataifa.
3 Na hakutakuwa tena na laana yoyote huko. Bali kiti cha ufalme cha Mungu na cha Mwana-Kondoo kitakuwa katika hilo jiji, na watumwa wake watamtolea yeye utumishi mtakatifu; 4 nao wataona uso wake, na jina lake litakuwa juu ya vipaji vya nyuso zao. 5 Pia, hakutakuwa usiku tena kamwe, na hawana uhitaji wowote wa nuru ya taa wala kuwa na nuru ya jua, kwa sababu Yehova Mungu atatoa nuru juu yao, nao watatawala wakiwa wafalme milele na milele.
6 Naye akaniambia: “Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli; ndiyo, Yehova Mungu wa semi zilizopuliziwa za manabii alimtuma malaika wake kuonyesha watumwa wake mambo ambayo lazima yatukie upesi. 7 Na, tazama! mimi ninakuja upesi. Mwenye furaha ni yeyote anayeshika maneno ya unabii wa hati-kunjo hii.”
8 Basi, mimi Yohana ndimi niliyekuwa nikisikia na kuona mambo haya. Na nilipokuwa nimesikia na kuona, nikaanguka chini kuabudu mbele ya miguu ya malaika aliyekuwa akinionyesha mambo haya. 9 Lakini yeye aniambia: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa tu mwenzako na wa ndugu zako walio manabii na wa wale wanaoshika maneno ya hati-kunjo hii. Abudu Mungu.”
10 Pia yeye aniambia: “Usitie muhuri maneno ya unabii wa hati-kunjo hii, kwa maana wakati uliowekwa rasmi uko karibu. 11 Yeye anayetenda ukosefu wa uadilifu; acha azidi kutenda ukosefu wa uadilifu; na acha mwenye uchafu azidi kufanywa kuwa mwenye uchafu wa kuchukiza; lakini acha mwadilifu azidi kufanya uadilifu, na acha mtakatifu azidi kufanywa kuwa mtakatifu.
12 “‘Tazama! Mimi ninakuja upesi, na thawabu niitoayo ipo pamoja nami, kulipa kila mmoja kama kazi yake ilivyo. 13 Mimi ndiye Alfa na Omega, wa kwanza na wa mwisho, mwanzo na mwisho. 14 Wenye furaha ni wale ambao hufua kanzu zao, ili mamlaka ya kwenda kwenye miti ya uhai ipate kuwa yao na kwamba waweze kupata kuingia katika jiji kwa malango yalo. 15 Nje kuna mbwa na wale wazoeao kuwasiliana na roho na waasherati na wauaji-kimakusudi na waabudu-sanamu na kila mtu anayependezwa na uwongo na kuuendeleza.’
16 “‘Mimi, Yesu, nilimtuma malaika wangu kuwatolea nyinyi watu ushahidi juu ya mambo haya kwa ajili ya yale makutaniko. Mimi ndiye mzizi na uzao wa Daudi, na nyota nyangavu ya asubuhi.’”
17 Na roho na bibi-arusi hufuliza kusema: “Njoo!” Na acha yeyote anayesikia aseme: “Njoo!” Na acha yeyote anayeona kiu aje; acha yeyote atakaye achukue maji ya uhai bure.
18 “Mimi ninamtolea ushahidi kila mtu asikiaye maneno ya unabii wa hati-kunjo hii: Yeyote akiongezea mambo haya, Mungu atamwongezea tauni ambazo zimeandikwa katika hati-kunjo hii; 19 na yeyote akiondolea mbali lolote kutoka katika maneno ya hati-kunjo ya unabii huu, Mungu ataondolea mbali fungu lake kutoka katika miti ya uhai na kutoka katika jiji takatifu, mambo ambayo yameandikwa katika hati-kunjo hii.
20 “Yeye atoaye ushahidi juu ya mambo haya asema, ‘Ndiyo; mimi ninakuja upesi.’”
“Ameni! Njoo, Bwana Yesu.”
21 Fadhili isiyostahiliwa ya Bwana Yesu Kristo na iwe pamoja na watakatifu.