Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Hagai 1:1-2:23
  • Hagai

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hagai
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Hagai

HAGAI

1 Katika mwaka wa pili wa utawala wa Mfalme Dario, katika mwezi wa sita, siku ya kwanza ya mwezi huo, neno la Yehova lilikuja kupitia nabii Hagai*+ kwa Zerubabeli+ mwana wa Shealtieli, gavana wa Yuda, na kwa Yoshua mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, likisema:

2 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Watu hawa wanasema, “Wakati wa kujenga nyumba ya* Yehova bado haujafika.”’”+

3 Na neno la Yehova likaja tena kupitia nabii Hagai,+ likisema: 4 “Je, ni wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zilizopambwa kwa mbao, huku nyumba hii ikiwa magofu?+ 5 Sasa hivi ndivyo anavyosema Yehova wa majeshi, ‘Kazieni mioyo yenu juu ya* njia zenu. 6 Mmepanda mbegu nyingi, lakini mnavuna kidogo.+ Mnakula, lakini hamshibi. Mnakunywa, lakini hamtosheki. Mnavaa nguo, lakini hakuna yeyote anayepata joto. Kibarua huweka mshahara wake katika mfuko uliojaa mashimo.’”

7 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Kazieni mioyo yenu juu ya* njia zenu.’

8 “‘Pandeni juu mlimani mkalete miti.+ Jengeni nyumba hii,+ ili niifurahie na ili nitukuzwe,’+ asema Yehova.”

9 “‘Mlitazamia mavuno mengi lakini mlipata kidogo; na mlipoyaleta katika nyumba hii, niliyapeperusha mbali.+ Kwa nini?’ auliza Yehova wa majeshi. ‘Kwa sababu nyumba yangu ni magofu, huku kila mmoja wenu akikimbia huku na huku ili kuitunza nyumba yake mwenyewe.+ 10 Kwa hiyo mbingu zilizo juu yenu zikazuia umande wake, na dunia ikazuia mazao yake. 11 Nami niliendelea kuuita ukame uje duniani, milimani, kwenye nafaka, kwenye divai mpya, kwenye mafuta, kwenye mimea inayoota ardhini, juu ya wanadamu na mifugo, na juu ya kazi yote ya mikono yenu.’”

12 Zerubabeli+ mwana wa Shealtieli+ na Yoshua mwana wa Yehosadaki,+ kuhani mkuu, na watu wengine wote wakaisikiliza sauti ya Yehova Mungu wao na maneno ya nabii Hagai, kwa sababu Yehova Mungu wao alikuwa amemtuma; na watu wakaanza kuogopa kwa sababu ya Yehova.

13 Kisha Hagai, mjumbe wa Yehova, akawapa watu ujumbe huu kulingana na utume wake kutoka kwa Yehova: “‘Niko pamoja nanyi,’+ asema Yehova.”

14 Basi Yehova akaichochea roho+ ya Zerubabeli mwana wa Shealtieli, gavana wa Yuda,+ na roho ya Yoshua+ mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, na roho ya watu wengine wote; nao wakaja na kuanza kujenga nyumba ya Yehova wa majeshi, Mungu wao.+ 15 Ilikuwa siku ya 24 ya mwezi wa sita, katika mwaka wa pili wa Mfalme Dario.+

2 Katika mwezi wa saba, siku ya 21 ya mwezi huo, neno la Yehova lilikuja kupitia nabii Hagai,+ likisema: 2 “Tafadhali muulize hivi Zerubabeli+ mwana wa Shealtieli, gavana wa Yuda,+ na Yoshua+ mwana wa Yehosadaki,+ kuhani mkuu, na watu wengine wote: 3 ‘Ni nani aliyebaki miongoni mwenu ambaye aliiona nyumba hii* katika utukufu wake wa mwanzoni?+ Sasa mnaionaje? Je, hamwoni kwamba ni duni ikilinganishwa na ilivyokuwa?’+

4 “‘Lakini sasa jipe moyo Zerubabeli,’ asema Yehova, ‘jipe moyo Yoshua mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu.’

“‘Nanyi watu wote wa nchi, jipeni moyo,’+ asema Yehova, ‘na mfanye kazi.’

“‘Kwa maana niko pamoja nanyi,’+ asema Yehova wa majeshi. 5 ‘Kumbukeni ahadi niliyowapa mlipotoka Misri,+ na roho yangu bado imo miongoni mwenu.*+ Msiogope.’”+

6 “Kwa maana Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Kwa mara nyingine tena—baada ya muda mfupi—nitatikisa mbingu na dunia na bahari na nchi kavu.’+

7 “‘Nami nitayatikisa mataifa yote, na vitu vyenye thamani* vya mataifa yote vitaingia katika nyumba hii;+ nami nitaijaza nyumba hii utukufu,’+ asema Yehova wa majeshi.

8 “‘Fedha ni yangu, na dhahabu ni yangu,’ asema Yehova wa majeshi.

9 “‘Utukufu wa wakati ujao wa nyumba hii utakuwa mkubwa zaidi kuliko ule wa mwanzoni,’+ asema Yehova wa majeshi.

“‘Na mahali hapa nitawapa amani,’+ asema Yehova wa majeshi.”

10 Katika siku ya 24 ya mwezi wa 9, mwaka wa pili wa utawala wa Dario, neno la Yehova lilimjia nabii Hagai,+ likisema: 11 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Tafadhali, waulize hivi makuhani kuhusu sheria:+ 12 “Mtu akibeba nyama takatifu ndani ya upindo wa vazi lake, na vazi lake liguse mkate au mchuzi au divai au mafuta au chakula cha aina yoyote, je, kitakuwa kitakatifu?”’”

Makuhani wakajibu: “Hapana!”

13 Kisha Hagai akawauliza: “Mtu asiye safi kwa sababu ya kugusa maiti,* akigusa chochote kati ya vitu hivyo, je, kitu hicho kitakuwa kichafu?”+

Makuhani wakajibu: “Kitakuwa kichafu.”

14 Basi Hagai akasema: “‘Hivyo ndivyo watu hawa walivyo, na hivyo ndivyo taifa hili lilivyo mbele zangu,’ asema Yehova, ‘na hivyo ndivyo kazi yote ya mikono yao ilivyo; chochote wanachotoa huko ni kichafu.’

15 “‘Lakini sasa, tafadhali, kazeni moyo wenu juu ya* jambo hili kuanzia leo na kuendelea: Kabla jiwe halijawekwa juu ya jiwe katika hekalu la Yehova,+ 16 hali ilikuwaje wakati huo? Mtu alipoenda kwenye rundo la nafaka akitarajia kupata vipimo 20, alipata vipimo 10 tu; na mtu alipoenda kwenye mtungi wa kushinikizia divai kuchota vipimo 50 kutoka kwenye pipa la divai, alipata vipimo 20 tu;+ 17 niliwapiga ninyi—kazi zote za mikono yenu—kwa upepo unaochoma na kuvu+ na mvua ya mawe, lakini hakuna hata mmoja wenu aliyenirudia,’ asema Yehova.

18 “‘Tafadhali, kazeni moyo wenu juu ya* jambo hili kuanzia leo na kuendelea, kuanzia siku ya 24 ya mwezi wa 9, kuanzia siku ambayo msingi wa hekalu la Yehova uliwekwa;+ kazeni moyo wenu juu ya jambo hili: 19 Je, bado kuna mbegu katika ghala?*+ Mzabibu, mtini, mkomamanga, na mzeituni—haijazaa matunda, au je, imezaa? Kuanzia leo nitawaletea baraka.’”+

20 Neno la Yehova likamjia Hagai mara ya pili katika siku ya 24 ya mwezi huo,+ likisema: 21 “Mwambie Zerubabeli, gavana wa Yuda, ‘Nitazitikisa mbingu na dunia.+ 22 Nitapindua kiti cha ufalme cha falme na kuharibu kabisa nguvu za falme za mataifa;+ nami nitayapindua magari ya vita na wale wanaoyaendesha,+ na farasi na wapanda farasi watauawa, kila mmoja kwa upanga wa ndugu yake.’”

23 “‘Siku hiyo,’ asema Yehova wa majeshi, ‘nitakuchukua, mtumishi wangu Zerubabeli+ mwana wa Shealtieli,’+ asema Yehova, ‘nitakufanya kuwa kama pete ya muhuri, kwa sababu nimekuchagua wewe,’ asema Yehova wa majeshi.”

Maana yake “Aliyezaliwa Wakati wa Sherehe.”

Au “kujenga upya hekalu la.”

Au “Fikirieni kwa makini.”

Au “Fikirieni kwa makini.”

Au “hekalu hili.”

Au labda, “na roho yangu ilipokuwa ikisimama miongoni mwenu.”

Au “kutamanika.”

Au “nafsi iliyokufa.” Angalia Kamusi.

Au “fikirieni kwa makini.”

Au “fikirieni kwa makini.”

Au “shimo la nafaka?”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki