Waamuzi
10 Na baada ya Abimeleki, akasimama Tola mwana wa Pua, mwana wa Dodo, mtu wa Isakari, ili kuwaokoa+ Israeli, naye alikuwa akikaa Shamiri katika eneo lenye milima la Efraimu.+ 2 Naye akaendelea kuhukumu Israeli kwa miaka 23, kisha akafa, akazikwa katika Shamiri.
3 Ndipo baada yake Yairi Mgileadi+ akasimama, naye akaendelea kuhukumu Israeli kwa miaka 22. 4 Naye akaja kuwa na wana 30 waliopanda punda 30 waliokomaa,+ nao walikuwa na majiji 30. Majiji hayo wanaendelea kuyaita Hawoth-yairi+ mpaka leo hii; yako katika nchi ya Gileadi. 5 Kisha Yairi akafa, akazikwa katika Kamoni.
6 Na wana wa Israeli wakaanza tena kufanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova,+ nao wakaanza kutumikia Mabaali+ na sanamu za Ashtorethi+ na miungu ya Siria+ na miungu ya Sidoni+ na miungu ya Moabu+ na miungu ya wana wa Amoni+ na miungu ya Wafilisti.+ Basi wakamwacha Yehova wala hawakumtumikia yeye.+ 7 Hivyo hasira ya Yehova ikawaka juu ya Israeli,+ naye akawauza+ mkononi mwa Wafilisti+ na mkononi mwa wana wa Amoni.+ 8 Kwa hiyo wakawavunja-vunja na kuwakandamiza sana wana wa Israeli mwaka huo—kwa miaka kumi na minane wana wote wa Israeli waliokuwa ng’ambo ya Yordani katika nchi ya Waamori iliyokuwa katika Gileadi. 9 Na wana wa Amoni wakawa wakivuka Yordani ili kupigana na Yuda na Benyamini na nyumba ya Efraimu; na Israeli walikuwa katika taabu kubwa sana.+ 10 Na wana wa Israeli wakaanza kumwomba Yehova msaada,+ wakisema: “Tumekutendea dhambi,+ kwa sababu tumemwacha Mungu wetu nasi tunatumikia Mabaali.”+
11 Ndipo Yehova akawaambia wana wa Israeli: “Je, mimi sikuwaokoa ninyi kutoka Misri+ na kutoka mkononi mwa Waamori+ na wana wa Amoni+ na Wafilisti+ 12 na Wasidoni+ na Amaleki+ na Midiani,+ walipowakandamiza,+ nanyi mkanililia, nami nikawaokoa kutoka katika mkono wao? 13 Lakini ninyi, mliniacha,+ mkaanza kuitumikia miungu mingine.+ Ndiyo sababu sitawaokoa tena.+ 14 Nendeni mwombe msaada kutoka kwa miungu+ ambayo mmechagua.+ Hiyo na iwaokoe wakati wa taabu yenu.” 15 Lakini wana wa Israeli wakamwambia Yehova: “Tumetenda dhambi.+ Wewe mwenyewe ututendee kulingana na lolote lililo jema machoni pako.+ Lakini tafadhali, utukomboe tu leo hii.”+ 16 Nao wakaanza kuiondoa miungu ya kigeni kutoka katikati yao,+ na kumtumikia Yehova,+ hivi kwamba nafsi+ yake ikawa haina subira kwa sababu ya taabu ya Israeli.+
17 Baadaye wana wa Amoni+ wakakusanywa pamoja, wakapiga kambi katika Gileadi.+ Kwa hiyo wana wa Israeli wakajikusanya pamoja, wakapiga kambi katika Mispa.+ 18 Ndipo watu na wakuu wa Gileadi wakaanza kuambiana: “Ni nani atakayeongoza katika kupigana na wana wa Amoni?+ Huyo na awe kichwa juu ya wakaaji wote wa Gileadi.”+