Waamuzi
1 Baada ya kifo cha Yoshua,+ Waisraeli* walimuuliza Yehova,+ “Ni nani kati yetu atakayeenda kwanza kupigana na Wakanaani?” 2 Yehova akawajibu, “Kabila la Yuda litaenda kwanza kupigana nao.+ Tazama! Ninaitia nchi hiyo mikononi mwao.”* 3 Ndipo watu wa kabila la Yuda wakawaambia ndugu zao wa kabila la Simeoni, “Twendeni pamoja katika eneo tulilopewa*+ tukapigane na Wakanaani. Nasi tutaenda nanyi katika eneo mlilopewa.” Basi watu wa kabila la Simeoni wakaenda pamoja nao.
4 Watu wa kabila la Yuda walipoenda, Yehova akawatia Wakanaani na Waperizi mikononi mwao,+ wakawashinda watu 10,000 huko Bezeki. 5 Wakamkuta Adoni-bezeki huko Bezeki, wakapigana naye na kuwashinda Wakanaani+ na Waperizi.+ 6 Adoni-bezeki akakimbia, wakamkimbiza na kumshika, wakamkata vidole gumba vya mikono na vya miguu. 7 Kisha Adoni-bezeki akasema, “Kuna wafalme 70 waliokatwa vidole gumba vya mikono na vya miguu wanaookota chakula chini ya meza yangu. Mungu amenilipa kulingana na matendo yangu.” Baadaye wakampeleka Yerusalemu,+ akafia huko.
8 Kisha watu wa Yuda wakashambulia jiji la Yerusalemu+ na kuliteka; wakawaua wakaaji wake kwa upanga na kuliteketeza jiji. 9 Baadaye watu wa Yuda wakaenda kupigana na Wakanaani waliokaa katika eneo lenye milima na waliokaa Negebu na Shefela.+ 10 Basi watu wa kabila la Yuda wakawashambulia Wakanaani waliokaa Hebroni (zamani Hebroni liliitwa Kiriath-arba), nao wakamuua Sheshai, Ahimani, na Talmai.+
11 Kisha wakawashambulia wakaaji wa Debiri.+ (Hapo awali Debiri liliitwa Kiriath-seferi.)+ 12 Ndipo Kalebu+ akasema, “Yeyote atakayeshambulia na kuteka jiji la Kiriath-seferi, nitampa binti yangu Aksa awe mke wake.”+ 13 Othnieli+ mwana wa Kenasi,+ ndugu mdogo wa Kalebu, akaliteka. Kwa hiyo akampa Aksa binti yake awe mke wake. 14 Mwanamke huyo alipokuwa akienda nyumbani kwake, akamsihi mume wake amwombe baba* yake shamba. Kisha mwanamke huyo akashuka kutoka juu ya punda wake.* Kalebu akamuuliza: “Unataka nini?” 15 Akamwambia, “Tafadhali nibariki, kwa maana umenipa shamba upande wa kusini;* nipe pia Guloth-maimu.”* Basi Kalebu akampa Gulothi ya Juu na Gulothi ya Chini.
16 Na wazao wa Mkeni,+ baba mkwe wa Musa,+ walitoka katika lile jiji la mitende+ pamoja na watu wa Yuda na kwenda katika nyika ya Yuda, upande wa kusini wa Aradi.+ Wakakaa huko pamoja na wenyeji.+ 17 Lakini watu wa kabila la Yuda wakasonga mbele pamoja na ndugu zao wa kabila la Simeoni, wakawashambulia Wakanaani waliokaa Sefathi na kuliangamiza jiji hilo.+ Kwa hiyo wakaliita Horma.*+ 18 Kisha watu wa kabila la Yuda wakateka Gaza+ na eneo lake, Ashkeloni+ na eneo lake, na Ekroni+ na eneo lake. 19 Yehova alikuwa pamoja na watu wa kabila la Yuda, nao wakamiliki eneo lenye milima, lakini hawakuweza kuwafukuza wakaaji wa bondeni,* kwa sababu walikuwa na magari ya vita yenye miundu ya chuma.*+ 20 Wakampa Kalebu jiji la Hebroni, kama Musa alivyoahidi,+ naye akawafukuza kutoka humo wale wana watatu wa Anaki.+
21 Lakini Wabenjamini hawakuwafukuza Wayebusi waliokaa Yerusalemu, kwa hiyo Wayebusi wanakaa na Wabenjamini jijini Yerusalemu mpaka leo.+
22 Wakati huo, watu wa nyumba ya Yosefu+ wakashambulia Betheli, na Yehova alikuwa pamoja nao.+ 23 Na nyumba ya Yosefu ikatuma watu wakapeleleze jiji la Betheli (zamani liliitwa Luzi),+ 24 na wapelelezi hao wakamwona mtu akitoka jijini. Wakamwambia, “Tafadhali tuonyeshe njia ya kuingia jijini, nasi tutakutendea kwa fadhili.”* 25 Basi akawaonyesha njia ya kuingia jijini, kisha wakawaua watu wote kwa upanga, lakini wakamwacha huru mtu huyo na familia yake.+ 26 Naye akaenda katika nchi ya Wahiti, akajenga jiji na kuliita Luzi. Hilo ndilo jina la jiji hilo mpaka leo.
27 Watu wa kabila la Manase hawakumiliki Beth-sheani na miji yake,* Taanaki+ na miji yake, Dori na miji yake, Ibleamu na miji yake, na Megido na miji yake.+ Wakanaani hawakukubali kutoka katika nchi hiyo. 28 Waisraeli walipopata nguvu, waliwatumikisha Wakanaani,+ lakini hawakuwafukuza wote.+
29 Wala Waefraimu hawakuwafukuza Wakanaani waliokaa Gezeri. Wakanaani waliendelea kukaa kati yao huko Gezeri.+
30 Watu wa kabila la Zabuloni hawakuwafukuza wakaaji wa Kitroni na wakaaji wa Nahaloli.+ Wakanaani waliendelea kukaa kati yao na kufanya kazi za kulazimishwa.+
31 Waasheri hawakuwafukuza wakaaji wa Ako, Sidoni,+ Alabu, Akzibu,+ Helba, Afiki,+ na Rehobu.+ 32 Basi Waasheri wakaendelea kukaa kati ya Wakanaani waliokaa katika nchi hiyo, kwa sababu hawakuwafukuza.
33 Watu wa kabila la Naftali hawakuwafukuza wakaaji wa Beth-shemeshi na Beth-anathi,+ lakini waliendelea kukaa kati ya Wakanaani.+ Wakawatumikisha wakaaji wa Beth-shemeshi na wa Beth-anathi.
34 Waamori waliwazuia watu wa kabila la Dani wasishuke bondeni,* hivyo wakabaki milimani.+ 35 Kwa hiyo Waamori hawakukubali kutoka kwenye Mlima Heresi, na Aiyaloni,+ na Shaalbimu.+ Lakini watu wa nyumba ya Yosefu walipopata nguvu zaidi, waliwatumikisha. 36 Eneo la Waamori lilianzia kwenye mwinuko wa Akrabimu,+ kuanzia Sela kwenda milimani.