Ufunuo
Ufunuo kwa Yohana
1 Ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimpa, kuonyesha watumwa wake mambo ambayo lazima yatukie upesi. Naye alituma malaika wake na kupitia yeye akautoa kwa njia ya ishara kwa mtumwa wake Yohana, 2 aliyetoa ushahidi kuhusu neno ambalo Mungu alitoa na kuhusu ushahidi ambao Yesu Kristo alitoa, hata kuhusu mambo yote aliyoyaona. 3 Mwenye furaha ni yeye asomaye kwa sauti kubwa na wale wasikiao maneno ya unabii huu, na washikao mambo yaliyoandikwa katika huo; kwa maana wakati uliowekwa rasmi uko karibu.
4 Yohana kwa makutaniko saba yaliyoko wilaya ya Asia:
Na mwe na fadhili isiyostahiliwa na amani kutoka kwa “Yule Aliyeko na aliyekuwako na anayekuja,” na kutoka kwa roho saba zilizoko mbele ya kiti chake cha ufalme, 5 na kutoka kwa Yesu Kristo, “Shahidi aliye Mwaminifu,” “Mzaliwa wa kwanza kutoka kwa wafu,” na “Mtawala wa wafalme wa dunia.”
Kwake yeye atupendaye na aliyetufungua kutoka katika dhambi zetu kwa njia ya damu yake mwenyewe— 6 naye alitufanya tuwe ufalme, makuhani kwa Mungu aliye Baba yake—ndiyo, kwake uwe utukufu na uweza milele. Ameni.
7 Tazama! Anakuja pamoja na mawingu, na kila jicho litamwona, na wale ambao walimdunga; na makabila yote ya dunia yatajipiga yenyewe kwa kihoro kwa sababu yake. Ndiyo, Ameni.
8 “Mimi ndiye Alfa na Omega,” asema Yehova Mungu, “yule Aliyeko na aliyekuwako na anayekuja, Mweza-Yote.”
9 Mimi Yohana, ndugu yenu na mshiriki pamoja nanyi katika dhiki na ufalme na uvumilivu katika ushirika na Yesu, nilikuja kuwa katika kisiwa kidogo kiitwacho Patmosi kwa ajili ya kusema juu ya Mungu na kutoa ushahidi kuhusu Yesu. 10 Kwa upulizio nilikuja kuwa katika siku ya Bwana, nami nikasikia nyuma yangu sauti yenye nguvu kama ile ya tarumbeta, 11 ikisema: “Lile ulionalo liandike katika hati-kunjo na ulipeleke kwenye makutaniko saba, katika Efeso na katika Smirna na katika Pergamamu na katika Thiatira na katika Sardisi na katika Filadelfia na katika Laodikia.”
12 Nami nikageuka ili nione sauti iliyokuwa ikisema nami, na, nikiisha kugeuka, nikaona vinara saba vya taa vya dhahabu, 13 na katikati ya vinara vya taa mtu fulani kama mwana wa binadamu, aliyevishwa vazi lililofika chini kwenye miguu, na aliyefungwa kifuani mshipi wa dhahabu. 14 Zaidi ya hayo, kichwa chake na nywele zake zilikuwa nyeupe kama sufu nyeupe, kama theluji, na macho yake kama mwali wa moto; 15 na miguu yake ilikuwa kama shaba nyekundu bora inapowaka katika tanuri; na sauti yake ilikuwa kama mvumo wa maji mengi. 16 Na katika mkono wake wa kuume alikuwa na nyota saba, na kutoka katika kinywa chake upanga mkali, mrefu wenye makali kuwili ulikuwa ukitokeza, na sura yake ilikuwa kama jua ling’aapo katika nguvu yalo. 17 Nami nilipomwona, nikaanguka kama mfu miguuni pake.
Naye akaweka mkono wake wa kuume juu yangu na kusema: “Usiwe mwenye hofu. Mimi ndiye Wa-Kwanza na Wa-Mwisho, 18 na aliye hai; na nikawa mfu, lakini, tazama! mimi niko hai milele na milele, nami nina funguo za kifo na za Hadesi. 19 Kwa hiyo andika mambo uliyoyaona, na mambo ambayo yako na mambo ambayo yatatukia baada ya hayo. 20 Kwa habari ya siri takatifu ya zile nyota saba ulizoona juu ya mkono wangu wa kuume, na ya vile vinara saba vya taa vya dhahabu: Zile nyota saba zamaanisha wale malaika wa makutaniko saba, na vile vinara saba vya taa vyamaanisha makutaniko saba.