Kutoka
13 Na Yehova akanena zaidi na Musa, na kusema: 2 “Nitakasie kila mzaliwa wa kwanza wa kiume anayefungua kila tumbo la uzazi kati ya wana wa Israeli, kati ya wanadamu na wanyama. Ni wangu.”+
3 Naye Musa akawaambia watu: “Na ikumbukwe siku hii ambayo mlitoka Misri,+ katika nyumba ya watumwa, kwa sababu kwa nguvu za mkono Yehova aliwatoa hapa.+ Basi chochote kilicho na chachu kisiliwe.+ 4 Leo mnaondoka katika mwezi wa Abibu.+ 5 Na itakuwa kwamba Yehova atakapokuwa amekuingiza katika nchi ya Wakanaani na Wahiti na Waamori na Wahivi na Wayebusi,+ ambayo aliwaapia mababu zako kuwa atakupa,+ nchi inayotiririka maziwa na asali,+ ndipo utatoa utumishi huu katika mwezi huu. 6 Siku saba utakula keki zisizo na chachu,+ na katika siku ya saba ni sherehe kwa Yehova.+ 7 Keki zisizo na chachu zitaliwa kwa siku hizo saba;+ na chochote kilicho na chachu kisionekane kwako,+ wala unga wowote uliokandwa wenye chachu usionekane kwako ndani ya mipaka yako yote.+ 8 Nawe utamwambia mwana wako siku hiyo, na kusema, ‘Ni kwa sababu ya jambo ambalo Yehova amenifanyia nilipotoka Misri.’+ 9 Nayo itatumika kwako kama ishara mkononi mwako na ukumbusho katikati ya macho yako,+ ili sheria ya Yehova iwe katika kinywa chako;+ kwa sababu kwa mkono wenye nguvu Yehova alikutoa Misri.+ 10 Nawe lazima uishike sheria hii kwa wakati wake uliowekwa mwaka baada ya mwaka.+
11 “Na itakuwa kwamba wakati Yehova anapokuingiza katika nchi ya Wakanaani,+ kama alivyokuapia wewe na mababu zako,+ na wakati anapokupa hiyo, 12 ndipo lazima umtoe kila anayefungua tumbo la uzazi kwa ajili ya Yehova,+ na kila mzaliwa wa kwanza, mtoto wa mnyama,+ ambaye atakuwa mali yako. Walio wa kiume ni wa Yehova.+ 13 Na kila mzaliwa wa kwanza wa punda utamkomboa kwa kondoo, nawe usipomkomboa, basi utaivunja shingo yake.+ Na kila mzaliwa wa kwanza wa mwanadamu kati ya wana wako utamkomboa.+
14 “Na itakuwa kwamba ikiwa mwana wako atakuuliza baadaye,+ na kusema, ‘Hili linamaanisha nini?’ basi utamwambia, ‘Kwa nguvu za mkono, Yehova alitutoa Misri,+ katika nyumba ya watumwa.+ 15 Na ikawa kwamba Farao alipoonyesha ukaidi kwa kukataa kuturuhusu twende zetu,+ ndipo Yehova akamuua kila mzaliwa wa kwanza katika nchi ya Misri,+ kuanzia mzaliwa wa kwanza wa mwanadamu kufikia mzaliwa wa kwanza wa mnyama.+ Ndiyo sababu mimi ninamtolea Yehova dhabihu wote wa kiume wanaofungua tumbo la uzazi,+ na kila mzaliwa wa kwanza wa wanangu ninamkomboa.’+ 16 Nayo itatumika kuwa ishara mkononi mwako na utepe wa kipaji katikati ya macho yako,+ kwa sababu kwa nguvu za mkono Yehova alitutoa Misri.”+
17 Na ikawa kwamba wakati Farao alipowaruhusu watu waende zao, Mungu hakuwaongoza kupitia njia ya nchi ya Wafilisti kwa kuwa tu ilikuwa karibu, kwa maana Mungu alisema: “Huenda hao watu watajuta watakapoona vita nao hakika watarudi Misri.”+ 18 Basi Mungu akawafanya watu wazunguke kupitia njia ya nyika ya Bahari Nyekundu.+ Hata hivyo wana wa Israeli walitoka nchini Misri wakiwa wamejipanga kivita.+ 19 Na Musa akaichukua mifupa ya Yosefu pamoja naye, kwa sababu alikuwa amewafanya wana wa Israeli waape rasmi, na kusema: “Bila shaka Mungu atawaelekezea ninyi fikira,+ nanyi lazima mwichukue mifupa yangu kutoka hapa pamoja nanyi.”+ 20 Nao wakaondoka Sukothi na kupiga kambi katika Ethamu ukingoni mwa nyika.+
21 Naye Yehova alikuwa akienda mbele yao wakati wa mchana katika nguzo ya wingu ili kuwaongoza njiani,+ na wakati wa usiku katika nguzo ya moto ili kuwapa nuru ya kwenda wakati wa mchana na wakati wa usiku.+ 22 Ile nguzo ya wingu haikuondoka mbele ya watu wakati wa mchana wala ile nguzo ya moto wakati wa usiku.+