Isaya
13 Tangazo juu ya Babiloni+ ambalo Isaya mwana wa Amozi+ aliona katika maono: 2 “Simamisheni ishara+ juu ya mlima wa miamba mitupu. Wapaazieni sauti, tikiseni mkono,+ ili waingie katika milango ya watu wenye vyeo.+ 3 Mimi mwenyewe nimetoa amri kwa watu wangu waliotakaswa.+ Pia nimewaita watu wangu wenye nguvu kwa ajili ya kuonyesha hasira yangu,+ watu wangu wenye kufurahi kwa njia yenye kutokeza. 4 Sikilizeni! Umati katika milima, kitu kama kikundi cha watu wengi sana!+ Sikilizeni! Ghasia za falme, za mataifa yaliyokusanyika pamoja!+ Yehova wa majeshi anakusanya jeshi la vita.+ 5 Wanakuja kutoka katika nchi iliyo mbali,+ kutoka katika mwisho wa mbingu, Yehova na silaha za shutuma yake, ili kuivunja dunia yote.+
6 “Pigeni mayowe,+ kwa maana siku ya Yehova iko karibu!+ Itakuja kama uporaji kutoka kwa Mweza-Yote.+ 7 Ndiyo sababu mikono yote itaanguka, na moyo wote wa mwanadamu anayeweza kufa utayeyuka.+ 8 Na watu wamekuwa na wasiwasi.+ Utungu na uchungu wa kuzaa zimewashika; wana uchungu kama mwanamke anayezaa.+ Wanatazamana kwa mshangao. Nyuso zao ni nyuso zilizowaka.+
9 “Tazama! Siku ya Yehova inakuja, ikiwa na ukali pamoja na ghadhabu na pamoja na hasira inayowaka, ili kuifanya nchi iwe kitu cha kushangaza,+ na ili kuwaangamiza watenda-dhambi wa nchi kutoka ndani yake.+ 10 Kwa maana nyota za mbinguni na makundi-nyota yake ya Kesili+ hazitatoa nuru yake; jua litakuwa na giza linapochomoza, na mwezi hautatoa nuru yake. 11 Nami hakika nitaleta ubaya wake juu ya nchi yenye kuzaa,+ na kosa lao wenyewe juu ya waovu. Nami kwa kweli nitakifanya kiburi cha wenye kimbelembele kikome, na majivuno ya waonevu nitayashusha.+ 12 Nitamfanya mwanadamu anayeweza kufa kuwa haba kuliko dhahabu safi,+ na mtu wa udongo kuwa haba kuliko dhahabu ya Ofiri.+ 13 Ndiyo sababu nitaifadhaisha mbingu,+ na dunia itatikisika itoke mahali pake kutokana na ghadhabu ya Yehova wa majeshi+ na katika siku ya hasira yake inayowaka.+ 14 Na itatukia kwamba, kama swala aliyefukuzwa na kama kundi ambalo halina mtu wa kulikusanya pamoja,+ watageuka, kila mmoja kwenda kwa watu wake mwenyewe; nao watakimbia, kila mmoja kwenda katika nchi yake.+ 15 Kila mtu atakayepatikana atachomwa kwa silaha, na kila mtu atakayekamatwa katika mfagio huo ataanguka kwa upanga;+ 16 na watoto wao watavunjwa vipande-vipande mbele ya macho yao.+ Nyumba zao zitaporwa, na wake zao watalalwa kinguvu.+
17 “Tazama, ninawaamsha Wamedi+ juu yao, ambao hawaioni fedha kuwa kitu na ambao, kwa habari ya dhahabu, hawapendezwi nayo. 18 Na pinde zao zitawavunja vipande-vipande hata vijana.+ Nao hawatauhurumia uzao wa tumbo;+ macho yao hayatawasikitikia wana. 19 Na Babiloni, lile pambo la falme,+ uzuri wa fahari ya Wakaldayo,+ litakuwa kama wakati Mungu alipoangamiza Sodoma na Gomora.+ 20 Hatakaliwa kamwe,+ wala hatakuwa na makao kwa kizazi baada ya kizazi.+ Na hapo Mwarabu hatapiga hema lake, na hakuna wachungaji watakaoruhusu makundi yao kulala hapo. 21 Na hapo wakaaji wa maeneo yasiyo na maji hakika watalala, na nyumba zao zitajaa bundi-tai.+ Na hapo mbuni watakaa, na roho waovu wenye umbo la mbuzi watarukaruka hapo.+ 22 Na mbwa-mwitu watapiga mayowe katika minara yake ya makao,+ na nyoka mkubwa atakuwa katika majumba ya mfalme yenye furaha tele. Na majira yake yamekaribia kuja, na siku zake hazitakawishwa.”+