2 Samweli
6 Na Daudi akawakusanya tena wanaume wote bora wa Israeli,+ 30,000. 2 Kisha Daudi na watu wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka, wakaenda Baale-yuda+ ili kuleta kutoka hapo sanduku+ la Mungu wa kweli, ambalo juu yake jina+ limeitwa, jina la Yehova wa majeshi,+ anayeketi juu ya makerubi.+ 3 Hata hivyo, wakalipandisha sanduku la Mungu wa kweli juu ya gari jipya la kukokotwa,+ ili walichukue kutoka katika nyumba ya Abinadabu,+ iliyokuwa juu ya mlima; na Uza na Ahio,+ wana wa Abinadabu, walikuwa wakiliongoza lile gari jipya.
4 Hivyo wakalichukua kutoka katika nyumba ya Abinadabu, iliyokuwa juu ya mlima—pamoja na sanduku la Mungu wa kweli; na Ahio alikuwa akitembea mbele ya lile Sanduku. 5 Na Daudi na nyumba yote ya Israeli walikuwa wakisherehekea mbele za Yehova kwa namna zote za vyombo vya mbao za mberoshi na kwa vinubi+ na kwa vinanda+ na kwa matari+ na kwa matasa na kwa matoazi.+ 6 Nao mwishowe wakaja mpaka uwanja wa kupuria wa Nakoni, na sasa Uza+ akanyoosha mkono wake kwenye lile sanduku la Mungu wa kweli, akalishika,+ kwa maana wale ng’ombe karibu waliangushe. 7 Ndipo hasira+ ya Yehova ikamwakia Uza, na Mungu wa kweli akampiga+ hapo kwa sababu ya hilo tendo lisilo la heshima kwa Mungu, naye akafa hapo karibu na lile sanduku la Mungu wa kweli.+ 8 Na Daudi akakasirika kwa sababu Yehova alikuwa amemlipukia Uza, na mahali hapo pakaitwa Peres-uza mpaka leo hii.+ 9 Naye Daudi akamwogopa Yehova+ siku hiyo, akaanza kusema: “Sanduku la Yehova litakujaje kwangu?”+ 10 Na Daudi hakutaka kulileta kwake sanduku la Yehova katika Jiji la Daudi.+ Kwa hiyo Daudi akaagiza lipelekwe kando kwenye nyumba ya Obed-edomu,+ Mgathi.+
11 Nalo sanduku la Yehova likaendelea kukaa katika nyumba ya Obed-edomu Mgathi miezi mitatu; na Yehova akazidi kumbariki+ Obed-edomu na nyumba+ yake yote. 12 Mwishowe Mfalme Daudi akaletewa habari, kusema: “Yehova ameibariki nyumba ya Obed-edomu na vitu vyake vyote kwa sababu ya lile sanduku la Mungu wa kweli.” Kwa hiyo Daudi akaenda, akalitoa lile sanduku la Mungu wa kweli kutoka katika nyumba ya Obed-edomu, akaliweka katika Jiji la Daudi kwa kushangilia.+ 13 Na ikawa kwamba wakati wachukuzi+ wa lile sanduku la Yehova walipokuwa wamepiga hatua sita, akatoa mara moja dhabihu ya ng’ombe na kinono.+
14 Naye Daudi alikuwa anacheza dansi mbele za Yehova kwa nguvu zake zote, na wakati huo wote Daudi alikuwa amejifunga efodi+ ya kitani. 15 Na Daudi na nyumba yote ya Israeli wakawa wanalipandisha sanduku+ la Yehova kwa sauti za shangwe+ na sauti za baragumu.+ 16 Na ikawa kwamba wakati sanduku la Yehova lilipokuja ndani ya Jiji la Daudi, Mikali,+ binti ya Sauli, akaangalia chini kutoka dirishani, akamwona Mfalme Daudi akiruka na kucheza dansi huku na huku mbele za Yehova; naye akaanza kumdharau+ moyoni+ mwake. 17 Kwa hiyo wakaliingiza ndani sanduku la Yehova na kuliweka mahali pake ndani ya hema ambalo Daudi alikuwa amelisimamishia;+ kisha Daudi akatoa dhabihu za kuteketezwa+ na dhabihu za ushirika+ mbele za Yehova. 18 Daudi alipomaliza kutoa zile dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika, akawabariki+ watu katika jina la Yehova+ wa majeshi. 19 Zaidi ya hayo, akawagawia+ watu wote, umati wote wa Israeli, mwanamume na mwanamke vilevile, kila mmoja keki ya mkate ya mviringo na keki ya tende na keki ya zabibu kavu,+ kisha watu wote wakaenda, kila mmoja nyumbani kwake.
20 Basi Daudi akarudi kuwabariki watu wa nyumba yake mwenyewe,+ na Mikali,+ binti ya Sauli, akatoka nje kumpokea Daudi na kusema: “Lo! Jinsi mfalme wa Israeli alivyojitukuza leo+ wakati alipojifunua leo mbele ya macho ya vijakazi wa watumishi wake, kama vile mmoja wa watu wapumbavu anavyojifunua!”+ 21 Lakini Daudi akamwambia Mikali: “Ilikuwa mbele za Yehova, aliyenichagua mimi badala ya baba yako na nyumba yake yote, akanipa amri+ niwe kiongozi juu ya Israeli, watu wa Yehova, nami nitasherehekea mbele za Yehova.+ 22 Nami nitajipuuza hata zaidi kuliko hivi,+ nitajishusha machoni pangu mwenyewe; nami nimeamua kujitukuza pamoja na wale vijakazi uliowataja.”+ 23 Basi, kwa habari ya Mikali,+ binti ya Sauli, hakupata mtoto yeyote mpaka siku ya kifo chake.