Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt 2 Wathesalonike 1:1-3:18
  • 2 Wathesalonike

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • 2 Wathesalonike
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
2 Wathesalonike

BARUA YA PILI KWA WATHESALONIKE

1 Paulo, Silvano,* na Timotheo,+ kwa kutaniko la Wathesalonike katika muungano na Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo:

2 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba na Bwana Yesu Kristo.

3 Tuna wajibu wa kumshukuru Mungu sikuzote kwa sababu yenu, akina ndugu. Hilo linafaa kwa kuwa imani yenu inakua sana na upendo wa kila mmoja wenu unaongezeka kati yenu.+ 4 Ndiyo maana tunajivunia ninyi+ kati ya makutaniko ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu na imani yenu katika mateso yenu yote na taabu* mnayopata.*+ 5 Huu ni uthibitisho wa hukumu ya uadilifu ya Mungu, inayowaongoza kuhesabiwa kuwa mnastahili Ufalme wa Mungu, ambao kwa kweli mnateseka kwa ajili yake.+

6 Hii inazingatia kwamba ni jambo la uadilifu kwa Mungu kuwalipa dhiki wale wanaowasababishia ninyi dhiki.+ 7 Lakini ninyi mnaopata dhiki mtapata kitulizo pamoja nasi wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu+ kutoka mbinguni akiwa pamoja na malaika wake wenye nguvu+ 8 katika mwali wa moto, atakapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema kumhusu Bwana wetu Yesu.+ 9 Watu hao watapata hukumu ya adhabu ya uharibifu wa milele+ kutoka mbele za Bwana na kutoka kwa utukufu wa nguvu zake, 10 wakati atakapokuja kutukuzwa kuhusiana na watakatifu wake na kustaajabiwa siku hiyo kati ya wote walioonyesha imani, kwa sababu ushahidi tuliotoa ulikubaliwa kwa imani kati yenu.

11 Kwa hiyo, tunasali sikuzote kwa ajili yenu, kwamba Mungu wetu awahesabu kuwa mnastahili mwito wake+ na kwa nguvu zake kufanya kikamili mambo yote yanayompendeza na kila kazi ya imani. 12 Ili jina la Bwana wetu Yesu litukuzwe ndani yenu nanyi katika muungano naye, kulingana na fadhili zisizostahiliwa za Mungu wetu na za Bwana Yesu Kristo.

2 Hata hivyo, akina ndugu, kuhusu kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo+ na kukusanywa kwetu pamoja kwake,+ tunawaomba 2 msitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwenu wala msitishwe na maneno yaliyoongozwa na roho*+ au ujumbe uliosemwa au barua inayodhaniwa kutoka kwetu, kwamba siku ya Yehova*+ imefika.

3 Msiruhusu mtu yeyote awapotoshe* kwa njia yoyote, kwa sababu siku hiyo haitafika kabla uasi imani+ haujatokea kwanza na yule mtu wa uasi sheria+ kufunuliwa, mwana wa maangamizi.+ 4 Yeye ni mpinzani na hujiinua juu ya wale wanaoitwa mungu au vitu vinavyoabudiwa,* na hivyo huketi katika hekalu la Mungu, akijionyesha waziwazi kuwa mungu. 5 Je, hamkumbuki kwamba nilikuwa nikiwaambia mambo hayo nilipokuwa pamoja nanyi?

6 Sasa mnajua kinachomzuia, ili afunuliwe wakati wake unaofaa. 7 Kwa kweli, fumbo la uasi sheria huu tayari linafanya kazi,+ lakini ni mpaka tu yule anayeuzuia sasa atakapoondolewa. 8 Ndipo, kwa kweli, yule mwasi sheria atafunuliwa, ambaye Bwana Yesu atamwangamiza kwa roho ya kinywa chake+ na kumharibu kupitia ufunuo+ wa kuwapo kwake. 9 Lakini kuwapo kwa huyo mwasi sheria ni kupitia kazi ya Shetani+ pamoja na kila tendo lenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu*+ 10 na kila namna ya udanganyifu usio wa uadilifu+ kwa wale wanaoangamia, kama malipo kwa sababu hawakukubali kuipenda kweli ili waokolewe. 11 Ndiyo sababu Mungu anaacha wapotoshwe kupitia udanganyifu, na hivyo waamini uwongo,+ 12 ili wote wahukumiwe kwa sababu hawakuiamini kweli, bali walipenda ukosefu wa uadilifu.

13 Hata hivyo, tuna wajibu wa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu akina ndugu mnaopendwa na Yehova,* kwa sababu tangu mwanzo Mungu aliwachagua+ ili mwokolewe kwa kuwatakasa+ kupitia roho yake na imani yenu katika kweli. 14 Aliwaita kupitia habari njema tunayotangaza, ili mpate utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo.+ 15 Basi, akina ndugu, simameni imara+ na mwendelee kufuata desturi mlizofundishwa,+ iwe ni kupitia ujumbe wa maneno au barua kutoka kwetu. 16 Zaidi ya hayo, Bwana wetu Yesu Kristo, na Mungu Baba yetu aliyetupenda+ na kutupatia faraja ya milele na tumaini jema+ kupitia fadhili zisizostahiliwa, 17 na aifariji mioyo yenu na kuwaimarisha* katika kila tendo na neno jema.

3 Mwishowe, akina ndugu, endeleeni kusali kwa ajili yetu,+ ili neno la Yehova* lizidi kuenea upesi+ na kutukuzwa, kama ilivyo kwenu, 2 na kwamba tukombolewe kutoka kwa watu hatari na waovu,+ kwa maana imani si mali ya watu wote.+ 3 Lakini Bwana ni mwaminifu, naye atawaimarisha na kuwalinda dhidi ya yule mwovu. 4 Zaidi ya hayo, tuna uhakika katika Bwana kuwahusu ninyi, kwamba mnafanya na mtaendelea kufanya mambo tunayowaagiza. 5 Bwana na aendelee kuongoza mioyo yenu ili mfanikiwe kumpenda Mungu+ na kuvumilia+ kwa ajili ya Kristo.

6 Sasa akina ndugu, tunawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, mjiepushe na kila ndugu asiyefuata utaratibu+ na desturi* mlizopokea* kutoka kwetu.+ 7 Kwa maana ninyi wenyewe mnajua jinsi mnavyopaswa kutuiga,+ kwa sababu hatukukosa kufuata utaratibu tulipokuwa nanyi, 8 wala hatukula chakula cha yeyote bure.*+ Badala yake, tulifanya kazi ngumu na yenye kutaabisha usiku na mchana ili tusimpe yeyote kati yenu mzigo wenye gharama.+ 9 Si kwamba hatuna mamlaka,+ bali tulitaka kuwawekea mfano ili mtuige.+ 10 Kwa kweli, tulipokuwa nanyi tulikuwa tukiwaagiza hivi: “Mtu yeyote asiyetaka kufanya kazi, asile chakula.”+ 11 Kwa maana tunasikia watu fulani miongoni mwenu hawafuati utaratibu,+ hawafanyi kazi yoyote, bali wanajiingiza katika mambo yasiyowahusu.+ 12 Tunawaagiza watu hao na kuwahimiza katika Bwana Yesu Kristo wafanye kazi kwa utulivu na kula chakula ambacho wao wenyewe wamekifanyia kazi.+

13 Nanyi akina ndugu, msichoke kutenda mema. 14 Lakini ikiwa yeyote hatii maneno yetu kupitia barua hii, mtieni alama na mwache kushirikiana naye,+ ili aone aibu. 15 Lakini msimwone mtu huyo kama adui, bali endeleeni kumwonya+ kama ndugu.

16 Basi, Bwana wa amani na aendelee kuwapa amani kwa kila njia.+ Bwana awe nanyi nyote.

17 Hii ni salamu yangu, mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe,+ ambayo ni ishara katika kila barua; hivi ndivyo ninavyoandika.

18 Fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo na ziwe pamoja nanyi nyote.

Pia anaitwa Sila.

Au “dhiki.”

Au “mnayovumilia.”

Au “kupitia kwa roho.” Angalia Kamusi, “Roho.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “awashawishi.”

Au “vinavyoheshimiwa.”

Au “miujiza.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “kuwatia nguvu.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “maagizo.”

Au labda, “walizopokea.”

Au “bila kulipa.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki