Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt Wakolosai 1:1-4:18
  • Wakolosai

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakolosai
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Wakolosai

KWA WAKOLOSAI

1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu kupitia mapenzi ya Mungu, na Timotheo+ ndugu yetu, 2 kwa watakatifu na ndugu waaminifu katika muungano na Kristo huko Kolosai:

Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu.

3 Sikuzote tunamshukuru Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, tunaposali kwa ajili yenu, 4 kwa kuwa tulisikia kuhusu imani yenu katika Kristo Yesu na upendo mlio nao kwa watakatifu wote 5 kwa sababu ya tumaini mlilowekewa akiba mbinguni.+ Hapo mwanzoni, mlisikia kuhusu tumaini hili kupitia ujumbe wa kweli ya habari njema 6 ambayo imekuja kwenu. Kama vile habari njema inavyozaa matunda na kuongezeka ulimwenguni kote,+ ndivyo pia inavyofanya miongoni mwenu, tangu siku mliposikia na kujua kwa usahihi fadhili zisizostahiliwa za Mungu katika kweli. 7 Hivyo ndivyo mmejifunza kutoka kwa mtumwa mwenzetu mpendwa Epafra,+ ambaye ni mhudumu mwaminifu wa Kristo kwa ajili yetu. 8 Pia alitujulisha kuhusu upendo wenu katika njia ya kiroho.*

9 Hiyo ndiyo sababu pia tangu siku tuliposikia kuhusu jambo hilo, hatujaacha kamwe kusali kwa ajili yenu+ na kuomba mjazwe ujuzi sahihi+ wa mapenzi yake katika hekima yote na utambuzi wa kiroho,+ 10 na hivyo mtembee kwa kumstahili Yehova* ili kumpendeza kikamili mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu;+ 11 nanyi mwimarishwe kwa nguvu zote kwa uwezo wake wenye utukufu+ ili mvumilie kikamili kwa subira na shangwe, 12 huku mkimshukuru Baba, aliyewafanya mstahili kushiriki urithi wa watakatifu+ katika nuru.

13 Alituokoa kutoka kwenye mamlaka ya giza+ na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wake mpendwa, 14 ambaye kupitia kwake tunaachiliwa huru kwa fidia, kusamehewa dhambi zetu.+ 15 Yeye ndiye mfano wa Mungu asiyeonekana,+ mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote;+ 16 kwa sababu kupitia kwake vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani, vitu vinavyoonekana na vitu visivyoonekana,+ iwe ni viti vya ufalme au utawala au serikali au mamlaka. Vitu vingine vyote vimeumbwa kupitia kwake+ na kwa ajili yake. 17 Pia, yeye ni wa kabla ya vitu vingine vyote,+ na kupitia kwake vitu vingine vyote vilifanywa kuwapo, 18 naye ndiye kichwa cha mwili, kutaniko.+ Yeye ndiye mwanzo, mzaliwa wa kwanza kutoka kwa wafu,+ ili awe wa kwanza katika mambo yote; 19 kwa sababu Mungu alipenda ujazo wote ukae ndani yake,+ 20 na kupitia yeye apatanishe kwake mwenyewe vitu vingine vyote+ kwa kufanya amani kupitia damu+ aliyomwaga juu ya mti wa mateso,* iwe ni vitu vilivyo duniani au vitu vilivyo mbinguni.

21 Kwa kweli, ninyi ambao zamani mlikuwa mmetengwa, nanyi mlikuwa adui kwa sababu akili zenu zilikuwa zikifikiria matendo maovu, 22 sasa amewapatanisha tena kwa njia ya mwili wenye nyama wa huyo kupitia kifo chake, ili awatoe ninyi mkiwa watakatifu na wasio na dosari na bila shtaka lolote mbele zake+— 23 bora tu, bila shaka, mwendelee katika imani,+ mkiwekwa imara juu ya msingi+ na kuwa thabiti,+ bila kuondoshwa kwenye tumaini la habari njema mliyoisikia, na ambayo ilihubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.+ Mimi Paulo, nilikuja kuwa mhudumu wa hii habari njema.+

24 Ninashangilia sasa katika mateso yangu kwa ajili yenu,+ nami ninakabili dhiki za Kristo ambazo bado hazimo katika mwili wangu kwa ajili ya mwili wake,+ ambao ni kutaniko.+ 25 Nilikuja kuwa mhudumu wa kutaniko hili kupatana na usimamizi+ kutoka kwa Mungu niliopewa kwa ajili yenu ili kulihubiri neno la Mungu kwa ukamili, 26 siri takatifu+ iliyokuwa imefichwa tangu mifumo ya mambo iliyopita*+ na tangu vizazi vilivyopita. Lakini sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake,+ 27 ambao Mungu amependezwa kuwajulisha kati ya mataifa utajiri wenye utukufu wa hii siri takatifu,+ ambayo ni Kristo katika muungano nanyi, tumaini la utukufu wake.+ 28 Yeye ndiye tunayemtangaza, tukimwonya kila mtu na kumfundisha kila mtu katika hekima yote, ili tumtoe kila mtu akiwa kamili katika muungano na Kristo.+ 29 Kwa kusudi hili kwa kweli ninafanya kazi kwa bidii, nikijikaza kwa uwezo wake unaotenda ndani yangu kwa nguvu.+

2 Kwa maana ninataka mjue jinsi ninavyopambana sana kwa ajili yenu na kwa ajili ya wale walio huko Laodikia+ na kwa ajili ya wote ambao hawajaniona mimi binafsi.* 2 Ninafanya hivyo ili mioyo yao ifarijiwe+ na ili waunganishwe kwa upatano katika upendo+ na wawe na utajiri wote unaotokana na uhakikisho kamili wa uelewaji wao, ili wapate ujuzi sahihi wa siri takatifu ya Mungu, yaani, Kristo.+ 3 Hazina zote za hekima na za ujuzi zimefichwa kwa uangalifu ndani yake.+ 4 Ninasema hivyo ili mtu yeyote asiwadanganye kwa hoja zenye kushawishi. 5 Ingawa sipo katika mwili, nipo pamoja nanyi katika roho, nikishangilia kuona utaratibu wenu mzuri+ na uthabiti wa imani yenu katika Kristo.+

6 Kwa hiyo, kama vile ambavyo mmempokea Kristo Yesu aliye Bwana, endeleeni kutembea katika muungano naye, 7 mkiwa mmetia mizizi na kujengwa katika yeye+ na kuimarishwa katika imani,+ kama vile mlivyofundishwa, mkijawa kabisa na shukrani.+

8 Jihadharini ili mtu yeyote asiwachukue mateka* kupitia falsafa na udanganyifu+ mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo; 9 kwa sababu ndani yake ujazo wote wa sifa ya Mungu hukaa kimwili.+ 10 Basi mmepata ujazo kupitia kwake, yule aliye kichwa cha serikali na mamlaka yote.+ 11 Kwa uhusiano wenu pamoja naye, ninyi pia mlitahiriwa kwa tohara iliyofanywa bila mikono kwa kuuvua mwili wenye nyama,+ kwa tohara ambayo ni ya Kristo.+ 12 Kwa maana mlizikwa pamoja naye katika ubatizo wake,+ na kwa uhusiano wenu pamoja naye mlifufuliwa+ pia pamoja kupitia imani yenu katika matendo yenye nguvu ya Mungu, aliyemfufua Kristo kutoka kwa wafu.+

13 Zaidi ya hilo, ingawa mlikuwa wafu katika makosa yenu na katika hali ya kutotahiriwa ya mwili wenu, Mungu aliwafanya muwe hai pamoja naye.+ Alitusamehe kwa fadhili makosa yetu yote+ 14 na kuifuta* hati iliyoandikwa kwa mkono+ ambayo ilikuwa na amri+ na iliyokuwa ikitupinga.+ Ameiondoa njiani kwa kuipigilia misumari kwenye mti wa mateso.*+ 15 Na kupitia mti huo,* amezivua na kuziacha uchi serikali na mamlaka naye amezionyesha hadharani kwamba zimeshindwa,+ akiziongoza katika maandamano ya ushindi.

16 Kwa hiyo, msimruhusu mtu yeyote awahukumu kuhusu mnachokula na kunywa+ au kuhusu kushika sherehe au mwezi mpya+ au sabato.+ 17 Mambo hayo ni kivuli cha mambo yanayokuja,+ bali uhalisi ni wa Kristo.+ 18 Msimruhusu mtu yeyote anayependezwa na unyenyekevu wa uwongo na namna ya ibada ya malaika awanyang’anye tuzo,+ “akichukua msimamo juu ya”* mambo ambayo ameona. Kwa kweli, anajivuna bila sababu inayofaa kwa akili yake ya kimwili, 19 naye hashiki imara kichwa,+ yeye ambaye kupitia kwake mwili wote huandaliwa na kuunganishwa kwa upatano kupitia viungo na kano zake, na kufanywa ukue kwa ukuzi unaotoka kwa Mungu.+

20 Ikiwa mlikufa pamoja na Kristo kuhusiana na mambo ya msingi ya ulimwengu,+ kwa nini mnaishi kana kwamba bado ninyi ni sehemu ya ulimwengu kwa kuendelea kujitiisha chini ya amri hizi:+ 21 “Usishike, wala usionje, wala usiguse,” 22 kuhusiana na mambo yote ambayo huangamia pamoja na matumizi yake, kulingana na amri na mafundisho ya wanadamu?+ 23 Ingawa mambo hayo huonekana kana kwamba yana hekima katika ibada ya kujitungia wenyewe na unyenyekevu wa uwongo, na kuutendea mwili kwa ukali,+ hayana thamani yoyote katika kuzuia kuutosheleza mwili.

3 Hata hivyo, ikiwa mlifufuliwa pamoja na Kristo,+ endeleeni kutafuta mambo yaliyo juu, ambako Kristo ameketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu.+ 2 Endeleeni kukaza akili zenu kwenye mambo yaliyo juu,+ si kwenye mambo yaliyo duniani.+ 3 Kwa maana mlikufa, na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika muungano na Mungu. 4 Wakati Kristo, aliye uhai wetu,+ atakapofunuliwa, ndipo ninyi pia mtakapofunuliwa pamoja naye katika utukufu.+

5 Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu+ vilivyo duniani kuhusiana na uasherati,* uchafu, hamu isiyodhibitiwa ya ngono,+ tamaa yenye madhara, na pupa, ambayo ni ibada ya sanamu. 6 Kwa sababu ya mambo hayo ghadhabu ya Mungu inakuja. 7 Hivyo ndivyo pia ninyi mlikuwa mkijiendesha* katika maisha yenu ya zamani.*+ 8 Lakini sasa, kwa kweli, lazima myaondoe mambo haya yote kutoka kwenu: ghadhabu, hasira, ubaya,+ matusi,+ na maneno machafu+ kutoka kinywani mwenu. 9 Msiambiane uwongo.+ Uvueni utu* wa zamani+ pamoja na mazoea yake, 10 na mjivike utu mpya,+ ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba,+ 11 ambapo hakuna Mgiriki wala Myahudi, kutahiriwa wala kutotahiriwa, mgeni, Msikithe,* mtumwa, au mtu huru; bali Kristo ni kila kitu na yumo katika vitu vyote.+

12 Basi, kama waliochaguliwa wa Mungu,+ watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma,+ fadhili, unyenyekevu,*+ upole,+ na subira.+ 13 Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari+ hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.+ Kama vile Yehova* alivyowasamehe kwa hiari, nanyi lazima mfanye vivyo hivyo.+ 14 Lakini zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo,+ kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.+

15 Pia, acheni amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu,*+ kwa maana ninyi, mliitwa kwenye amani hiyo katika mwili mmoja. Na mjionyeshe kuwa wenye shukrani. 16 Neno la Kristo na likae ndani yenu kwa wingi katika hekima yote. Endeleeni kufundishana na kutiana moyo* kwa zaburi,+ sifa kwa Mungu, nyimbo za kiroho zinazoimbwa kwa shukrani,* mkimwimbia Yehova* mioyoni mwenu.+ 17 Jambo lolote mnalofanya kwa maneno au kwa matendo, fanyeni mambo yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kupitia kwake.+

18 Enyi wake, jitiisheni kwa waume zenu,+ kwa kuwa inafaa katika Bwana. 19 Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu+ nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.*+ 20 Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo,+ kwa maana hilo humpendeza Bwana. 21 Enyi akina baba, msiwe mkiwakasirisha* watoto wenu,+ ili wasivunjike moyo.* 22 Enyi watumwa, watiini katika kila jambo wale ambao ni mabwana wenu wanadamu,*+ si wakati tu wanapowatazama, ili tu kuwapendeza wanadamu,* bali kwa unyoofu wa moyo, kwa kumwogopa Yehova.* 23 Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi* yote kama kwa Yehova,*+ na si kwa wanadamu, 24 kwa maana mnajua kwamba mtapokea kutoka kwa Yehova* urithi kama thawabu.+ Mtumikieni Bwana, Kristo. 25 Hakika yule anayetenda kosa atapokea malipo kwa lile kosa alilotenda,+ na hakuna ubaguzi wowote.+

4 Enyi mabwana, watendeeni watumwa wenu kwa njia ya uadilifu na haki, mkijua kwamba ninyi pia mna Bwana mbinguni.+

2 Dumuni katika sala,+ mkikaa macho katika sala pamoja na kutoa shukrani.+ 3 Wakati huohuo, salini pia kwa ajili yetu,+ ili Mungu afungue mlango kwa ajili ya neno ili tutangaze siri takatifu kumhusu Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa gerezani,+ 4 na ili niitangaze waziwazi kama ninavyopaswa.

5 Endeleeni kutembea kwa hekima kuelekea wale walio nje, mkitumia vizuri kabisa wakati wenu.*+ 6 Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote,+ yaliyokolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.+

7 Tikiko,+ ndugu yangu mpendwa na mhudumu mwaminifu na mtumwa mwenzangu katika Bwana, atawaambia habari zote kunihusu. 8 Ninamtuma kwenu ili mjue jinsi tunavyoendelea na ili aifariji mioyo yenu. 9 Anakuja pamoja na Onesimo,+ ndugu yangu mwaminifu na mpendwa, ambaye anatoka kwenu; watawaambia kuhusu mambo yote yanayoendelea huku.

10 Aristarko,+ mateka mwenzangu anawatumia salamu zake, na pia Marko,+ binamu ya Barnaba (ambaye mlipokea maagizo ya kumkaribisha+ ikiwa atakuja kwenu), 11 na Yesu anayeitwa Yusto, walio kati ya wale waliotahiriwa. Ni hawa tu walio wafanyakazi wenzangu kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, nao wamekuwa chanzo cha faraja* nyingi kwangu. 12 Epafra,+ mtumwa wa Kristo Yesu, ambaye ametoka kwenu, anawatumia salamu zake. Sikuzote anajikaza kwa ajili yenu katika sala zake, ili mwishowe msimame mkiwa kamili na kwa usadikisho imara katika mapenzi yote ya Mungu. 13 Kwa maana ninamtolea ushahidi kwamba anajitahidi sana kwa ajili yenu na kwa ajili ya wale walio Laodikia na Hierapoli.

14 Luka,+ daktari mpendwa anawatumia salamu zake, na pia Dema.+ 15 Wapeni salamu zangu ndugu huko Laodikia na pia msalimuni Nimfa na kutaniko lililo katika nyumba yake.+ 16 Na baada ya kusoma barua hii miongoni mwenu, pangeni isomwe+ pia katika kutaniko la Walaodikia, nanyi pia msome ile ya kutoka Laodikia. 17 Pia, mwambieni Arkipo hivi:+ “Zingatia huduma uliyoikubali katika Bwana, ili uitimize.”

18 Hii ni salamu yangu, Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe.+ Endeleeni kukumbuka vifungo vyangu vya gereza.+ Fadhili zisizostahiliwa ziwe pamoja nanyi.

Tnn., “katika roho.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Kamusi.

Au “vizazi vya kale.” Angalia Kamusi.

Tnn., “hawajauona uso wangu katika mwili.”

Au “asiwachukue kama mawindo yake.”

Au “kuiondoa.”

Angalia Kamusi.

Au labda, “kupitia yeye.”

Yamenukuliwa kutoka kwenye desturi za mafumbo (jando) ya kipagani.

Neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.

Au “mlikuwa mkitembea.”

Au “mlipokuwa mkiishi hivyo.”

Tnn., “Mvueni mtu.”

Neno “Msikithe” lilimaanisha mtu asiye mstaarabu.

Au “unyenyekevu wa akili.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “idhibiti mioyo yenu.”

Au “kuonyana.”

Au “neema.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “msiwe wakali kwao.”

Au “msiwachokoze; msiwaudhi.”

Au “wasife moyo.”

Tnn., “kwa njia ya kimwili.”

Tnn., “si kwa matendo ya utumishi wa macho, kama wanaowapendeza wanadamu.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Kamusi, “Nafsi.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Tnn., “mkijinunulia wakati unaofaa.”

Au “msaada wa kunitia nguvu.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki