Barua ya Pili kwa Wathesalonike
1 Paulo na Silvano na Timotheo+ kwa kutaniko la Wathesalonike katika muungano na Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo:
2 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba na Bwana Yesu Kristo.+
3 Tuna wajibu wa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu,+ akina ndugu, kwa kuwa inafaa, kwa sababu imani yenu inakua+ sana na upendo wa kila mmoja wenu na wa ninyi nyote unaongezeka kwa mtu na mwenzake.+ 4 Matokeo ni kwamba sisi wenyewe tunajivunia+ ninyi kati ya makutaniko ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu wenu na imani katika mateso yenu yote na dhiki mnazovumilia.+ 5 Huo ni uthibitisho wa hukumu ya uadilifu ya Mungu,+ inayowaongoza ninyi kwenye hali ya kuhesabiwa kuwa mnastahili ufalme wa Mungu,+ ambao mnateseka kwa ajili yake.+
6 Hii inazingatia kwamba ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu kuwalipa dhiki wale wanaowafanyia ninyi dhiki,+ 7 lakini, kwenu ninyi mnaopata dhiki, kitulizo pamoja nasi wakati wa ufunuo+ wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu+ 8 katika mwali wa moto, anapoleta kisasi+ juu ya wale wasiomjua Mungu+ na wale wasiotii+ habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.+ 9 Watu hao watahukumiwa adhabu+ ya uharibifu wa milele+ kutoka mbele ya Bwana na kutoka kwenye utukufu wa nguvu zake,+ 10 wakati atakapokuja kutukuzwa kuhusiana na watakatifu+ wake na kustaajabiwa katika siku hiyo kuhusiana na wote walioonyesha imani, kwa sababu ushahidi tulioutoa ulikubaliwa kwa imani kati yenu.
11 Kwa hiyo sisi tunasali sikuzote kwa ajili yenu, ili Mungu wetu awahesabu ninyi kuwa mnastahili mwito+ wake na kufanya kwa ukamili yote anayopenda yaliyo ya wema na ile kazi ya imani pamoja na nguvu; 12 ili jina la Bwana wetu Yesu litukuzwe ndani yenu,+ nanyi katika muungano+ na yeye, kupatana na fadhili zisizostahiliwa+ za Mungu wetu na za Bwana Yesu Kristo.
2 Hata hivyo, akina ndugu, kwa habari ya kuwapo+ kwa Bwana wetu Yesu Kristo na kukusanywa kwetu pamoja kwake,+ tunawaomba ninyi 2 msitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwenu wala msisisimuliwe ama kupitia neno lililoongozwa na roho+ au kupitia ujumbe wa maneno+ au kupitia barua+ kana kwamba inatoka kwetu, ya kuwa siku+ ya Yehova ipo hapa.
3 Msiache mtu yeyote awashawishi ninyi kwa namna yoyote, kwa sababu hiyo haitakuja isipokuwa uasi-imani+ uje kwanza na yule mtu wa uasi-sheria+ afunuliwe,+ mwana wa maangamizi.+ 4 Yeye anapinga+ na kujiinua juu ya kila anayeitwa “mungu” au kitu cha kupewa heshima ya ibada, hivi kwamba yeye huketi katika hekalu la Mungu, akijionyesha mwenyewe hadharani kuwa mungu.+ 5 Je, hamkumbuki kwamba, nilipokuwa ningali pamoja nanyi, nilikuwa nikiwaambia+ mambo hayo?
6 Na hivyo sasa mnajua kile kitu+ ambacho kinatenda kama kizuizi,+ ili afunuliwe katika wakati wake mwenyewe unaofaa.+ 7 Ni kweli, fumbo la uasi-sheria huu tayari linafanya kazi;+ lakini ni mpaka tu wakati atakapoondolewa njiani yule ambaye sasa ni kizuizi.+ 8 Ndipo, kwa kweli, yule mwasi-sheria atafunuliwa, ambaye Bwana Yesu atamwangamiza kwa roho ya kinywa+ chake na kumfanya kuwa si kitu kwa ufunuo+ wa kuwapo kwake.+ 9 Lakini kuwapo kwa huyo mwasi-sheria ni kulingana na utendaji+ wa Shetani pamoja na kila tendo lenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu+ 10 na pamoja na kila udanganyifu+ usio wa uadilifu kwa wale wanaoangamia,+ kuwa malipo kwa sababu hawakukubali kuipenda+ ile kweli ili wapate kuokolewa.+ 11 Hiyo ndiyo sababu Mungu huacha utendaji wa kosa uwaendee wao, ili wauamini uwongo,+ 12 ili wote wahukumiwe kwa sababu hawakuiamini kweli+ bali waliupenda ukosefu wa uadilifu.+
13 Hata hivyo, sisi tuna wajibu wa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, akina ndugu mnaopendwa na Yehova, kwa sababu Mungu aliwachagua+ ninyi tangu mwanzo kwa ajili ya wokovu kwa kuwatakasa+ ninyi kwa roho+ na kwa imani yenu katika kweli.+ 14 Kwa lengo hili aliwaita ninyi kupitia habari njema tunayoitangaza,+ kwa kusudi la kujipatia utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo.+ 15 Basi, akina ndugu, simameni imara+ na mwendelee kuyashika mapokeo+ mliyofundishwa, iwe kwamba ilikuwa kupitia ujumbe wa maneno au kupitia barua yetu. 16 Zaidi ya hayo, Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe na Mungu Baba yetu, aliyetupenda+ na kutupa sisi faraja ya milele na tumaini jema+ kwa njia ya fadhili zisizostahiliwa, 17 na aifariji mioyo yenu na kuwaimarisha ninyi katika kila tendo na neno jema.+
3 Mwishowe, akina ndugu, endeleeni kusali kwa ajili yetu,+ ili neno la Yehova+ liendelee kusonga haraka+ na kutukuzwa kama vile linavyofanya kwenu; 2 na ili tukombolewe kutoka kwa watu wenye madhara na waovu,+ kwa maana imani si mali ya watu wote.+ 3 Lakini Bwana ni mwaminifu, naye atawafanya ninyi kuwa imara na kuwaepusha na yule mwovu.+ 4 Zaidi ya hayo, tuna uhakika+ katika Bwana kuwahusu ninyi, kwamba mnafanya nanyi mtaendelea kufanya mambo tunayoagiza.+ 5 Bwana na aendelee kuielekeza mioyo yenu kwa mafanikio katika kumpenda+ Mungu na katika uvumilivu+ kwa ajili ya Kristo.
6 Sasa tunawapa ninyi maagizo,+ akina ndugu, katika jina la Bwana Yesu Kristo, mjiepushe+ na kila ndugu anayetembea bila utaratibu+ na si kulingana na pokeo mlilopokea kutoka kwetu.+ 7 Kwa maana ninyi wenyewe mnajua njia mnayopaswa kutuiga,+ kwa sababu hatukujiendesha bila utaratibu katikati yenu+ 8 wala hatukula chakula kwa yeyote bure.+ Kinyume cha hilo, kwa kazi ya jasho na kutaabika+ usiku na mchana tulikuwa tukifanya kazi ili tusimtwike yeyote kati yenu mzigo wenye gharama.+ 9 Si kwamba hatuna mamlaka,+ bali ili tujitoe kuwa kielelezo kwenu ili mtuige sisi.+ 10 Kwa kweli, pia, tulipokuwa pamoja nanyi, tulikuwa tukiwapa ninyi agizo hili:+ “Ikiwa yeyote hataki kufanya kazi, basi na asile chakula.”+ 11 Kwa maana tunasikia watu fulani wanatembea bila utaratibu+ katikati yenu, hawafanyi kazi hata kidogo bali wanajiingiza katika mambo yasiyowahusu wao.+ 12 Kwa watu wa namna hiyo tunawapa agizo na kuwahimiza katika Bwana Yesu Kristo kwamba kwa kufanya kazi kwa utulivu wale chakula ambacho wao wenyewe wanafanyia kazi.+
13 Kwa upande wenu, akina ndugu, msiache kutenda yaliyo sawa.+ 14 Lakini ikiwa yeyote hatii neno letu+ kupitia barua hii, mtieni alama mtu huyo,+ acheni kushirikiana naye,+ ili aone aibu.+ 15 Na bado msimwone yeye kuwa adui, bali endeleeni kumwonya+ kama ndugu.
16 Sasa Bwana wa amani mwenyewe na awape ninyi amani daima katika kila njia.+ Bwana na awe pamoja nanyi nyote.
17 Hii ni salamu yangu, ya Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe,+ ambayo ni ishara katika kila barua; hivi ndivyo mimi huandika.
18 Fadhili zisizostahiliwa+ za Bwana wetu Yesu Kristo na ziwe pamoja nanyi nyote.