KWA WAFILIPI
1 Paulo na Timotheo, watumwa wa Kristo Yesu, kwa watakatifu wote katika muungano na Kristo Yesu walio huko Filipi,+ pamoja na waangalizi na watumishi wa huduma:+
2 Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.
3 Sikuzote ninamshukuru Mungu wangu ninapowakumbuka ninyi 4 katika dua zangu zote kwa ajili yenu nyote. Ninatoa kila dua kwa shangwe,+ 5 kwa sababu ya mchango ambao mmeutoa kwa ajili ya* habari njema tangu siku ya kwanza mpaka sasa. 6 Kwa maana nina uhakika kuhusu jambo hili, kwamba yule aliyeanzisha kazi njema ndani yenu ataikamilisha+ kufikia siku ya Kristo Yesu.+ 7 Ni sawa kwangu kufikiri hivyo kuwahusu ninyi nyote, kwa sababu mko katika moyo wangu, ninyi mlio washiriki pamoja nami katika fadhili zisizostahiliwa katika vifungo vyangu vya gereza+ na katika kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema.+
8 Kwa maana Mungu ni shahidi wangu kuhusu jinsi ninavyotamani kuwaona ninyi nyote kwa upendo mwororo kama alio nao Kristo Yesu. 9 Na hili ndilo ninaloendelea kusali, kwamba upendo wenu uwe mwingi zaidi na zaidi+ pamoja na ujuzi sahihi+ na utambuzi kamili;+ 10 kwamba mhakikishe mambo muhimu zaidi,+ ili muwe bila kasoro na msiwe mkiwakwaza wengine+ mpaka siku ya Kristo; 11 na kwamba mjazwe tunda la uadilifu, ambalo ni kupitia Yesu Kristo,+ kwa utukufu na sifa kwa Mungu.
12 Basi ninataka mjue, akina ndugu, kwamba hali yangu kwa kweli imesaidia kuendeleza habari njema, 13 hivi kwamba vifungo vyangu vya gereza+ kwa ajili ya Kristo vimejulikana wazi+ kati ya Walinzi wote wa Mfalme na watu wengine wote. 14 Sasa akina ndugu wengi katika Bwana wamekuwa na uhakika kwa sababu ya vifungo vyangu vya gereza, nao wanaonyesha uhodari mwingi wa kulisema neno la Mungu bila woga.
15 Ni kweli, wengine wanamhubiri Kristo kwa wivu na kushindana, lakini wengine kwa nia njema. 16 Hao wa mwisho wanamtangaza Kristo kutokana na upendo, kwa maana wanajua kwamba nimechaguliwa ili kuitetea habari njema;+ 17 lakini wale wa kwanza hufanya hivyo kutokana na ugomvi, si kwa kusudi safi, kwa maana wanataka kunisababishia dhiki katika vifungo vyangu vya gereza. 18 Matokeo ni nini? Ni kwamba katika kila njia, iwe ni kwa unafiki au ni kwa ukweli, Kristo anatangazwa, nami ninashangilia kuhusu jambo hilo. Kwa kweli, nitaendelea pia kushangilia, 19 kwa maana ninajua hilo litanisaidia kupata wokovu kupitia dua yenu+ na kwa msaada wa roho ya Yesu Kristo.+ 20 Hilo linapatana na tarajio langu lenye hamu na tumaini kwamba sitaona aibu kwa njia yoyote, bali kwamba kwa uhuru wote wa kusema, sasa Kristo, kama sikuzote hapo mwanzoni, atatukuzwa kupitia mwili wangu, iwe ni kupitia uzima au kupitia kifo.+
21 Kwa maana kwangu mimi, kuishi ni Kristo+ na kifo ni faida.+ 22 Basi ikiwa nitaendelea kuishi katika mwili, hilo ni tunda la kazi yangu; hata hivyo, mimi sisemi kile nitakachochagua. 23 Ninakabiliwa na mambo haya mawili, kwa maana ninatamani kufunguliwa na kuwa pamoja na Kristo,+ ambako, kwa hakika, ni bora zaidi.+ 24 Hata hivyo, ni muhimu zaidi kwangu kubaki katika mwili kwa ajili yenu. 25 Basi, nikiwa na uhakika wa jambo hili, ninajua nitabaki na kuendelea pamoja nanyi nyote ili msonge mbele na muwe na shangwe katika imani, 26 ili kwa sababu yangu furaha yenu ifurike katika Kristo Yesu nitakapokuwa tena pamoja nanyi.
27 Ila tu jiendesheni* kwa njia inayostahili habari njema kumhusu Kristo,+ ili kama nitakuja kuwaona au nisipokuja, nisikie kuwahusu na nisikie kwamba mnasimama imara katika roho moja, kwa nafsi moja,*+ mkijitahidi pamoja kwa ajili ya imani ya habari njema, 28 bila kuogopeshwa kamwe na wapinzani wenu. Jambo hili ni uthibitisho wa uharibifu+ kwao, lakini wa wokovu kwenu;+ na hili linatoka kwa Mungu. 29 Kwa maana mlipewa pendeleo kwa ajili ya Kristo, si muwe tu na imani katika yeye, bali pia mteseke kwa ajili yake.+ 30 Kwa maana mna pambano kama lile mliloona nikikabili,+ ambalo mnasikia kwamba bado ninakabili.
2 Basi, ikiwa kuna jambo lolote la kutia moyo katika Kristo, ikiwa kuna faraja yoyote ya upendo, ikiwa kuna ushirika wowote wa kiroho,* ikiwa kuna upendo mwororo na huruma zozote, 2 fanyeni shangwe yangu ijae kwa kuwa na akili ileile na kuwa na upendo uleule, mkiwa mmeunganishwa kabisa,* mkiwa na wazo moja akilini.+ 3 Msifanye jambo lolote kwa ugomvi+ au kwa kujisifu,+ bali kwa unyenyekevu* mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi,+ 4 huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe,+ bali pia faida za wengine.+
5 Iweni na mtazamo huu wa akili ambao pia Kristo Yesu alikuwa nao,+ 6 ambaye, ingawa alikuwa katika umbo la Mungu,+ hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu.+ 7 Hapana, bali alijiondolea hali yake na kuchukua umbo la mtumwa+ na kuwa mwanadamu.*+ 8 Zaidi ya hayo, alipokuja akiwa mwanadamu,* alijinyenyekeza na kuwa mtiifu mpaka kifo,+ ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.*+ 9 Kwa sababu hiyo, Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi+ na kumpa kwa fadhili jina lililo juu kuliko kila jina lingine,+ 10 ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe—la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya ardhi+— 11 na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana+ kwa utukufu wa Mungu Baba.
12 Kwa hiyo, wapendwa wangu, kama vile ambavyo mmekuwa mkitii sikuzote, si wakati tu ninapokuwapo, bali kwa utayari zaidi sasa nisipokuwapo, endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka. 13 Kwa maana Mungu ndiye ambaye kwa mapenzi yake mema anawachochea, na kuwapa hamu na nguvu za kutenda. 14 Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika+ wala kubishana,+ 15 ili mje kuwa bila lawama wala hatia, watoto wa Mungu+ wasio na dosari katikati ya kizazi kilicho kombo na kilichopotoka,+ ambao kati yao mnaangaza kama mianga katika ulimwengu,+ 16 mkiendelea kulishika sana neno la uzima.+ Ndipo nitakuwa na sababu ya kushangilia katika siku ya Kristo, nikijua kwamba sikukimbia bure wala sikufanya kazi kwa bidii bure. 17 Hata hivyo, hata ikiwa ninamiminwa kama toleo la kinywaji+ juu ya dhabihu+ na utumishi mtakatifu* ambao imani yenu imewaongoza, ninafurahi na kushangilia pamoja nanyi nyote. 18 Vivyo hivyo, ninyi pia mnapaswa kufurahi na kushangilia pamoja nami.
19 Sasa ninatumaini katika Bwana Yesu kumtuma Timotheo+ kwenu upesi, ili nitiwe moyo nitakapopata habari kuwahusu ninyi. 20 Kwa maana sina mtu mwingine aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mahangaiko yenu. 21 Kwa maana wengine wote wanatafuta faida zao wenyewe, si za Yesu Kristo. 22 Lakini ninyi mnajua jinsi alivyojithibitisha mwenyewe, kwamba kama mtoto+ na baba yake alitumikia pamoja nami katika kuendeleza habari njema. 23 Kwa hiyo, yeye ndiye ninayetumaini kumtuma mara tu nitakapoona jinsi mambo yangu yatakavyokuwa. 24 Kwa kweli, nina uhakika katika Bwana kwamba mimi mwenyewe pia nitakuja hivi karibuni.+
25 Lakini sasa ninaona ni lazima nimtume kwenu Epafrodito, ndugu yangu na mfanyakazi mwenzangu na mwanajeshi mwenzangu, na mjumbe wenu na mtumishi wa kibinafsi kwa ajili ya uhitaji wangu,+ 26 kwa kuwa anatamani kuwaona ninyi nyote naye amehuzunika kwa sababu mlisikia alikuwa mgonjwa. 27 Kwa hakika, alikuwa mgonjwa karibu kufa; lakini Mungu alimhurumia. Kwa kweli, hakumhurumia yeye tu, bali mimi pia, ili nisipatwe na huzuni juu ya huzuni. 28 Kwa hiyo ninamtuma haraka bila kukawia, ili mtakapomwona, mshangilie tena, nami nipunguziwe wasiwasi. 29 Basi mkaribisheni kama ilivyo desturi katika Bwana kwa shangwe yote, nanyi mwendelee kuwaheshimu sana watu wa namna hiyo,+ 30 kwa kuwa alikaribia kufa kwa sababu ya kazi ya Kristo,* akihatarisha uhai wake,* ili ajazie kutokuwapo kwenu hapa kunitolea utumishi wa kibinafsi.+
3 Mwishowe, ndugu zangu, endeleeni kushangilia katika Bwana.+ Sioni vibaya kuendelea kuwaandikia mambo yaleyale, na ni kwa ajili ya usalama wenu.
2 Jihadharini na mbwa; jihadharini na wale wanaosababisha madhara; jihadharini na wale wanaoukata mwili.+ 3 Kwa maana sisi ndio wenye tohara ya kweli,+ sisi tunaotoa utumishi mtakatifu kupitia roho ya Mungu na tunaojisifu katika Kristo Yesu+ na ambao uhakika wetu hautegemei mwili, 4 ingawa mimi kati ya watu wote, nina sababu za kuwa na uhakika katika mwili.
Mtu yeyote akifikiri ana sababu za kuwa na uhakika katika mwili, mimi ninazo zaidi: 5 nilitahiriwa siku ya nane,+ mimi ni wa taifa la Israeli, wa kabila la Benjamini, Mwebrania aliyezaliwa kwa Waebrania;+ kuhusu sheria, Farisayo;+ 6 kuhusu bidii, nililitesa kutaniko;+ kuhusu uadilifu unaotegemea sheria, mtu ambaye hakuwa na hatia. 7 Lakini vitu vilivyokuwa faida kwangu, nimeviona kuwa hasara* kwa sababu ya Kristo.+ 8 Isitoshe, kwa kweli ninaviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa ajili yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami ninaviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo 9 nami nipatikane katika muungano naye, si kwa sababu ya uadilifu wangu mwenyewe, kwa kufuata Sheria, bali kwa sababu ya uadilifu kupitia imani+ katika Kristo,+ uadilifu unaotoka kwa Mungu na unaotegemea imani.+ 10 Lengo langu ni kumjua yeye na nguvu za ufufuo wake+ na kushiriki katika mateso yake,+ nikijitiisha kwenye kifo kama chake,+ 11 ili kuona kama ikiwezekana nitaufikia ufufuo wa mapema kutoka kwa wafu.+
12 Si kwamba tayari nimelipokea au tayari nimefanywa kuwa mkamilifu, bali ninaendelea kujitahidi+ ili kuona kama pia ninaweza kulishika lile ambalo lilifanya Kristo Yesu anichague.*+ 13 Akina ndugu, sijioni kuwa tayari nimelishika hilo; lakini jambo moja ni hakika: Ninayasahau mambo ya nyuma+ na kujinyoosha kuelekea mambo yaliyo mbele,+ 14 ninaendelea kujitahidi kuelekea mradi* kwa ajili ya tuzo+ ya mwito wa Mungu wa kwenda juu+ kupitia Kristo Yesu. 15 Kwa hiyo, wale walio wakomavu kati yetu+ na wawe na mtazamo huu wa akili, na ikiwa mna mwelekeo wa akili ulio tofauti kwa njia yoyote, Mungu atawafunulia mtazamo ulio hapo juu. 16 Kwa vyovyote, kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.
17 Kwa muungano, iweni waigaji wangu,+ akina ndugu, na mwendelee kuwaangalia wale wanaotembea katika njia inayopatana na mfano tuliowawekea. 18 Kwa maana kuna wengi—nilikuwa nikiwataja mara nyingi lakini sasa ninawataja pia nikilia—wanaotembea kama adui za mti wa mateso* wa Kristo. 19 Mwisho wao ni uharibifu, na mungu wao ni tumbo lao, na utukufu wao kwa kweli ni aibu yao, na akili zao zinafikiria vitu vya duniani.+ 20 Lakini uraia wetu+ uko mbinguni,+ nasi tunamsubiri kwa hamu mwokozi kutoka huko, Bwana Yesu Kristo,+ 21 ambaye ataugeuza mwili wetu wa hali ya chini uwe kama* mwili wake wenye utukufu+ kwa nguvu zake nyingi zinazomwezesha kuvitiisha vitu vyote kwake mwenyewe.+
4 Kwa hiyo, ndugu zangu ninaowapenda na ninaotamani kuwaona, shangwe yangu na taji langu,+ simameni imara+ kwa njia hii katika Bwana, wapendwa wangu.
2 Ninawahimiza Euodia na Sintike wawe na akili moja katika Bwana.+ 3 Ndiyo, ninakuomba pia, ukiwa mfanyakazi mwenzangu wa kweli,* uendelee kuwasaidia wanawake hao ambao wamejitahidi* sana pamoja nami kwa ajili ya habari njema, pamoja na Klementi na vilevile wale wafanyakazi wenzangu wengine, ambao majina yao yamo katika kitabu cha uzima.+
4 Shangilieni sikuzote katika Bwana. Nitasema tena, Shangilieni!+ 5 Usawaziko wenu+ na ujulikane kwa watu wote. Bwana yuko karibu. 6 Msihangaike kuhusiana na jambo lolote,+ bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu;+ 7 na amani+ ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu+ na nguvu zenu za akili* kupitia Kristo Yesu.
8 Mwishowe, akina ndugu, mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yanayopendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, mambo yoyote ya wema wa adili, na mambo yoyote yanayostahili sifa, endeleeni kuyafikiria* mambo hayo.+ 9 Mambo mliyojifunza na vilevile mkayakubali na kuyasikia na kuyaona kuhusiana nami, mzoee kuyafanya hayo,+ na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.
10 Ninashangilia sana katika Bwana kwamba sasa mwishowe mmeanza tena kunihangaikia.+ Ingawa mlinihangaikia, hamkupata nafasi ya kuonyesha jambo hilo. 11 Sisemi hivyo kwa sababu nina uhitaji, kwa maana hata hali zangu ziweje nimejifunza kuridhika.*+ 12 Ninajua jinsi ya kupungukiwa na chakula,+ na jinsi ya kuwa na vitu vingi. Katika mambo yote na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kuishi bila kitu. 13 Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.+
14 Hata hivyo, mlifanya vema kwa kushiriki pamoja nami katika dhiki yangu. 15 Kwa kweli, ninyi Wafilipi pia mnajua kwamba mwanzoni mlipojifunza habari njema, nilipoondoka Makedonia, hakuna kutaniko lililoshiriki pamoja nami katika kutoa na kupokea, isipokuwa ninyi peke yenu;+ 16 kwa maana nilipokuwa Thesalonike, mlinitumia kitu kwa ajili ya uhitaji wangu si mara moja tu bali mara mbili. 17 Si kwamba ninatafuta zawadi, bali ninataka tunda linalowaletea faida zaidi kwenye akiba yenu. 18 Hata hivyo, nina kila kitu ninachohitaji, na hata zaidi. Nimejaziwa kila kitu, kwa kuwa sasa nimepokea kutoka kwa Epafrodito+ vitu mlivyotuma, harufu tamu,+ dhabihu yenye kukubalika, inayompendeza Mungu vema. 19 Naye Mungu wangu atawajazia kikamili uhitaji wenu+ kulingana na utajiri wake katika utukufu kupitia Kristo Yesu. 20 Sasa kwa Mungu na Baba yetu kuwe na utukufu milele na milele. Amina.
21 Mpeni kila mtakatifu salamu zangu katika muungano na Kristo Yesu. Ndugu walio pamoja nami wanawatumia salamu zao. 22 Watakatifu wote, lakini hasa wale wa nyumbani mwa Kaisari,+ wanawatumia salamu zao.
23 Fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo ziwe pamoja na roho mnayoonyesha.
Au “kwa sababu mmeshiriki kuendeleza.”
Au “jiendesheni kama raia.”
Au “kwa nia moja.”
Tnn., “ushirika wowote wa roho.”
Au “mkiwa mmeunganishwa katika nafsi.”
Au “unyenyekevu wa akili.”
Tnn., “na kuwa kama wanadamu.”
Tnn., “alipopatikana katika umbo la mwanadamu.”
Angalia Kamusi.
Au “utumishi wa watu wote.”
Au labda, “kazi ya Bwana.”
Au “akiihatarisha nafsi yake.”
Au labda, “nimeviacha kwa hiari.”
Tnn., “ambalo aliliweka juu yangu.”
Au “lengo.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “ufanane na.”
Tnn., “mwenzangu kihalisi katika nira.”
Au “wamepambana.”
Au “akili zenu; mawazo yenu.”
Au “kuyatafakari.”
Au “kutosheka.”