Mhubiri
8 Ni nani aliye kama mwenye hekima?+ Na ni nani anayeweza kujua tafsiri ya jambo?+ Hekima ya mwanadamu huufanya uso wake ung’ae, na hata ukali wa uso wake ubadilike uwe afadhali.+
2 Nasema: “Shika agizo la mfalme,+ na ufanye hivyo kwa kujali kiapo cha Mungu.+ 3 Usifanye haraka kuondoka mbele yake.+ Usisimame katika jambo baya.+ Kwa maana yote anayopenda kufanya, atafanya.+ 4 Kwa sababu neno la mfalme ndilo nguvu za kudhibiti;+ na ni nani anayeweza kumwambia: ‘Unafanya nini?’”
5 Anayeishika amri hatajua jambo lolote lenye msiba,+ na moyo wenye hekima utajua wakati na hukumu.+ 6 Kwa maana kuna wakati na hukumu hata kwa kila jambo,+ kwa sababu misiba iliyo juu ya wanadamu ni mingi.+ 7 Kwa maana hakuna mtu anayejua yatakayokuja kuwako,+ kwa sababu ni nani anayeweza kumwambia jinsi yatakavyokuja kuwa?
8 Hakuna mwanadamu aliye na nguvu juu ya roho ili kuizuia roho;+ wala hakuna nguvu zozote za kuzuia katika siku ya kifo;+ wala hakuna kuachiliwa katika vita.+ Wala uovu hautawaokoa wanaouzoea.+
9 Yote haya nimeyaona, nikatia moyoni mwangu kila kazi ambayo imefanywa chini ya jua, wakati ambao mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.+ 10 Lakini, ingawa iko hivyo, nimewaona waovu wakizikwa,+ jinsi walivyokuja na jinsi walivyokuwa wakiondoka mahali patakatifu+ na kusahaulika katika jiji walikotenda hivyo.+ Hilo pia ni ubatili.
11 Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi,+ ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.+ 12 Ijapokuwa huenda mtenda-dhambi akawa anatenda yaliyo mabaya+ mara mia moja na kuendelea kwa muda mrefu anavyopenda, ninajua pia kwamba mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu+ wa kweli, kwa sababu walimwogopa.+ 13 Lakini mambo hayatakuwa mema kwa mwovu,+ wala hatarefusha siku zake zilizo kama kivuli,+ kwa sababu hamwogopi Mungu.+
14 Kuna ubatili unaofanyika duniani, kwamba kuna watu waadilifu wanaopatwa na mambo kana kwamba ni kazi ya waovu,+ na kuna waovu wanaopatwa na mambo kana kwamba ni kazi ya waadilifu.+ Nilisema hilo pia ni ubatili.
15 Nami nikapongeza kushangilia,+ kwa sababu wanadamu hawana jambo bora chini ya jua kuliko kula na kunywa na kushangilia, na kwamba hilo liambatane nao katika kazi yao ngumu muda wa siku za maisha yao,+ ambazo Mungu wa kweli amewapa chini ya jua.+ 16 Kupatana na hayo, niliutia moyo wangu+ kujua hekima na kuona shughuli inayofanywa duniani,+ kwa sababu kuna mtu ambaye macho yake hayapati usingizi, mchana wala usiku.+
17 Nami nikaona kazi yote ya Mungu wa kweli,+ jinsi ambavyo wanadamu hawawezi kuvumbua kazi ambayo imefanywa chini ya jua;+ lakini hata wanadamu waendelee namna gani kufanya kazi kwa bidii kutafuta, bado hawagundui.+ Na hata wakisema kwamba wana hekima ya kutosha kuweza kujua,+ hawawezi kuvumbua.+