Mathayo
22 Yesu akawajibu kwa kuwaambia mifano tena, akisema:+ 2 “Ufalme wa mbinguni umekuwa kama mtu, mfalme, aliyefanya karamu ya ndoa+ kwa ajili ya mwana wake. 3 Naye akatuma watumwa wake wawaite wale walioalikwa kwenye karamu ya ndoa,+ lakini hawakutaka kuja.+ 4 Tena akawatuma watumwa wengine,+ akisema, ‘Waambieni wale walioalikwa: “Tazama! Nimetayarisha chakula changu cha mchana,+ ng’ombe-dume wangu na wanyama waliononeshwa wamechinjwa, na vitu vyote viko tayari. Njooni kwenye karamu ya ndoa.” ’+ 5 Lakini wakaenda zao bila kujali, mmoja kwenye shamba lake mwenyewe, mwingine kwenye kazi yake ya biashara;+ 6 lakini wale wengine wakawashika watumwa wake, wakawatendea kwa dharau na kuwaua.+
7 “Lakini mfalme akawa na ghadhabu, akayatuma majeshi yake na kuwaangamiza wauaji hao na kulichoma jiji lao.+ 8 Ndipo akawaambia watumwa wake, ‘Karamu ya ndoa kwa kweli iko tayari, lakini wale walioalikwa hawakustahili.+ 9 Kwa hiyo nendeni kwenye barabara zinazotoka jijini, na mtu yeyote mtakayemkuta mwalikeni kwenye karamu ya ndoa.’+ 10 Basi watumwa hao wakaenda barabarani na kuwakusanya wote waliowakuta, waovu na wema pia;+ na chumba cha sherehe za arusi kikajaa watu wenye kuketi+ mezani.
11 “Mfalme alipoingia kuwakagua wageni walioalikwa akamwona hapo mtu ambaye hakuwa amevaa vazi la ndoa.+ 12 Kwa hiyo akamwambia, ‘Mwenzangu, uliingiaje humu bila kuvaa vazi la ndoa?’+ Akakosa la kusema. 13 Ndipo mfalme akawaambia watumishi wake, ‘Mfungeni mikono na miguu na kumtupa gizani, kule nje. Huko ndiko atalia na kusaga meno yake.’+
14 “Kwa maana wanaoalikwa ni wengi, lakini wanaochaguliwa ni wachache.”+
15 Ndipo Mafarisayo wakaondoka, wakaenda na kushauriana pamoja kusudi wamtege kwa maneno yake.+ 16 Basi wakawatuma wanafunzi wao kwake, pamoja na wafuasi wa chama cha Herode,+ wakisema: “Mwalimu, tunajua wewe una ukweli nawe hufundisha njia ya Mungu katika kweli, na hujali mtu yeyote, kwa maana wewe hutazami sura ya mtu.+ 17 Kwa hiyo, tuambie, Unaonaje? Je, ni halali kumlipa Kaisari kodi au hapana?”+ 18 Lakini Yesu, akiujua uovu wao, akasema: “Kwa nini mnanijaribu, enyi wanafiki?+ 19 Nionyesheni sarafu ya kodi ya kichwa.” Wakamletea dinari. 20 Naye akawaambia: “Sanamu hii na mwandiko huu ni za nani?”+ 21 Wakasema: “Ni za Kaisari.” Ndipo akawaambia: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.”+ 22 Basi, waliposikia hilo, wakastaajabu, wakamwacha na kwenda zao.+
23 Siku hiyo Masadukayo, wale ambao husema hakuna ufufuo, wakamjia na kumuuliza:+ 24 “Mwalimu, Musa alisema, ‘Mtu yeyote akifa bila kuwa na watoto, ndugu yake amwoe mke wake na kumwinulia ndugu yake uzao.’+ 25 Basi kulikuwa na ndugu saba; naye wa kwanza akaoa na kufa, na, kwa kuwa hakuwa na uzao, akamwachia ndugu yake mke wake.+ 26 Ikawa vivyo hivyo pia kwa yule wa pili na yule wa tatu, mpaka wote saba.+ 27 Mwishowe yule mwanamke akafa. 28 Kwa hiyo, katika ufufuo, atakuwa mke wa nani kati ya hao saba? Kwa maana alikuwa mke wao wote.”+
29 Yesu akawajibu, akawaambia: “Ninyi mnakosea, kwa sababu hamjui Maandiko wala nguvu za Mungu;+ 30 kwa maana katika ufufuo wanaume hawaoi wala wanawake hawaolewi,+ bali wao ni kama malaika mbinguni. 31 Kwa habari ya ufufuo wa wafu, je, hamkusoma mliloambiwa na Mungu, akisema,+ 32 ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo’?+ Yeye ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai.”+ 33 Waliposikia hilo, umati wakastaajabishwa na mafundisho yake.+
34 Baada ya Mafarisayo kusikia kwamba alikuwa amewanyamazisha kimya Masadukayo, wakakusanyika pamoja katika kikundi kimoja. 35 Na mmoja wao, mwenye ujuzi wa Sheria,+ akauliza, akimjaribu: 36 “Mwalimu, amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?”+ 37 Akamwambia: “ ‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’+ 38 Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza. 39 Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’+ 40 Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.”+
41 Na Mafarisayo walipokuwa wamekusanyika pamoja, Yesu akawauliza:+ 42 “Mna maoni gani kuhusu Kristo? Ni mwana wa nani?” Wakamwambia: “Wa Daudi.”+ 43 Akawaambia: “Basi, kwa nini Daudi akiongozwa na roho+ anamwita ‘Bwana,’ akisema, 44 ‘Yehova alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako chini ya miguu yako” ’?+ 45 Kwa hiyo, ikiwa Daudi anamwita ‘Bwana,’ inawezekanaje kwamba yeye ni mwana wake?”+ 46 Na hakuna mtu aliyeweza kumjibu hata neno moja, na tangu siku hiyo na kuendelea hakuna mtu yeyote aliyethubutu tena kumuuliza swali.+