-
“Tazama! Huyu Ni Mungu Wetu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 1
“Tazama! Huyu Ni Mungu Wetu”
1, 2. (a) Ungependa kumwuliza Mungu maswali gani? (b) Musa alimwuliza Mungu swali gani?
JE, UNAWEZA kuwazia ukizungumza na Mungu? Hilo ni wazo lenye kutia kicho kama nini—kuzungumza na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu! Unasitasita mwanzoni, hatimaye unafaulu kumjibu. Anakusikiliza, anaitikia, na hata anakuruhusu kuuliza swali lolote ulilo nalo. Basi sasa, utamwuliza swali gani?
2 Hapo kale, mtu mmoja alijikuta katika hali hiyohiyo. Aliitwa Musa. Lakini, swali aliloamua kumwuliza Mungu huenda likakushangaza. Hakuuliza kuhusu hali yake binafsi, wakati wake ujao, wala hata matatizo ya wanadamu. Badala yake, aliuliza jina la Mungu. Huenda hilo likakushangaza, kwa kuwa tayari Musa alijua jina la Mungu. Basi, lazima swali lake liwe lilikuwa na maana kubwa zaidi. Kwa kweli, Musa aliuliza swali muhimu zaidi ya yote. Jibu la swali hilo linatuhusu sote. Linaweza kukusaidia kuchukua hatua muhimu sana ya kumkaribia Mungu. Jinsi gani? Hebu tuchunguze mazungumzo hayo ya pekee.
3, 4. Ni matukio gani yaliyotangulia mazungumzo ya Musa na Mungu, na jambo kuu la mazungumzo hayo lilikuwa nini?
3 Musa alikuwa na umri wa miaka 80. Kwa muda wa miaka 40 alikuwa uhamishoni mbali na watu wake Waisraeli, waliokuwa watumwa nchini Misri. Siku moja, alipokuwa akichunga mifugo ya baba-mkwe wake, aliona jambo la ajabu. Kichaka kiliwaka moto, lakini hakikuteketea. Kiliendelea kuwaka moto, na kung’aa kama ishara mlimani. Musa alikikaribia ili akitazame. Haikosi alishtuka sana aliposikia sauti ikizungumza naye kutoka katikati ya moto huo! Mungu alizungumza na Musa kwa muda mrefu kwa kutumia malaika. Na huenda unajua kwamba Mungu alimwagiza Musa aliyesitasita aache maisha yake matulivu na kurudi Misri ili kuwakomboa Waisraeli kutoka utumwani.—Kutoka 3:1-12.
4 Wakati huo, Musa angaliweza kumwuliza Mungu swali lolote. Hata hivyo, hebu ona swali aliloamua kuuliza: “Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n’nani? niwaambie nini?”—Kutoka 3:13.
5, 6. (a) Swali la Musa latufundisha ukweli gani sahili ulio muhimu sana? (b) Ni jambo gani lenye kuchukiza ambalo limefanywa kuhusiana na jina la Mungu? (c) Kwa nini ni muhimu kwamba Mungu amewafunulia wanadamu jina lake?
5 Kwanza kabisa, swali hilo latufundisha kwamba Mungu ana jina. Hatupaswi kamwe kupuuza ukweli huo sahili. Lakini, watu wengi hupuuza jambo hilo. Jina la Mungu limeondolewa kwenye tafsiri nyingi sana za Biblia na kubadilishwa na majina ya cheo, kama vile “Bwana” na “Mungu.” Hilo ni mojawapo ya mambo yenye kusikitisha sana na yenye kuchukiza ambayo yamefanywa kwa sababu za kidini. Kwani, wewe hufanya nini kwanza unapokutana na mtu fulani? Unamwuliza jina lake, sivyo? Ndivyo ilivyo na kumjua Mungu. Yeye si Mungu tu asiye na jina, asiye na hisia, asiyeweza kujulikana wala kufahamika. Ijapokuwa haonekani, ana utu, na ana jina—Yehova.
6 Zaidi ya hayo, Mungu anapofunua jina lake, yeye hukusudia kutenda mambo makuu na yenye kuvutia. Anatukaribisha tumjue. Anataka tufanye uamuzi bora zaidi maishani, yaani, kumkaribia yeye. Lakini Yehova amefanya mengi zaidi ya kutuambia jina lake. Ametufundisha pia kuhusu yule anayewakilishwa na jina hilo.
Maana ya Jina la Mungu
7. (a) Jina la Mungu linaweza kumaanisha nini? (b) Musa alitaka kujua nini alipomwuliza Mungu jina Lake?
7 Yehova alijichagulia jina lenye maana sana. Jina “Yehova“ linaweza kumaanisha “Yeye Husababisha Kuwe.“ Kwa kweli, Yeye ni wa pekee katika ulimwengu wote kwa kuwa aliumba vitu vyote, naye husababisha makusudi yake yote yatimie. Wazo hilo linatufanya tumheshimu sana. Lakini je, kuna maana nyingine ya jina la Mungu? Ni wazi kwamba Musa alitaka kujifunza mengi zaidi. Ukweli ni kwamba alijua kuwa Yehova ndiye Muumba, na alilijua jina la Mungu. Jina hilo la Mungu halikuwa geni. Watu walikuwa wamelitumia kwa karne nyingi. Hapana shaka kwamba Musa alipouliza kuhusu jina la Mungu, alitaka kumjua yule anayewakilishwa na jina hilo. Ni kama alikuwa akisema hivi: ‘Niwaambie nini watu wako Israeli kukuhusu ili waweze kukuamini na kusadiki kwamba kwa kweli utawakomboa?’
8, 9. (a) Yehova alijibuje swali la Musa, na kwa nini tafsiri nyingi zimekosea katika kutafsiri jibu Lake? (b) Usemi “Nitathibitika kuwa kile nitakachothibitika kuwa” unamaanisha nini”?
8 Yehova alimjibu kwa kufunua jambo lenye kusisimua kuhusu utu wake. Jambo hilo linahusiana na maana ya jina lake. Alimwambia Musa hivi: “Nitathibitika kuwa kile nitakachothibitika kuwa.” (Kutoka 3:14, NW) Andiko hilo husomeka hivi kwenye tafsiri nyingi za Biblia: “MIMI NIKO AMBAYE NIKO.” Lakini tafsiri sahihi zaidi ya maneno hayo inaonyesha kwamba Mungu hakuwa tu akithibitisha kwamba yeye yupo. Badala yeke, Yehova alikuwa akimfundisha Musa—na sisi sote—kwamba ’angethibitika kuwa,’ au angeamua kuwa chochote alichohitaji kuwa ili kutimiza ahadi Zake.” Tafsiri ya J.B. Rotherham yatafsiri waziwazi mstari huo: “Nitakuwa chochote nipendacho.” Mtaalamu mmoja wa Kiebrania cha Biblia aeleza hivi kuhusu maneno hayo: “Haidhuru ni hali au uhitaji gani uliopo . . . , Mungu ‘atakuwa’ suluhisho la uhitaji huo.”
9 Hilo lilimaanisha nini kwa Waisraeli? Licha ya kizuizi kilichowakabili au magumu ambayo wangepata, Yehova angewakomboa kutoka utumwani na kuwapeleka katika Nchi Iliyoahidiwa. Bila shaka jina hilo liliwatia moyo wamtumaini Mungu. Laweza kuwa na matokeo yayo hayo kwetu. (Zaburi 9:10) Kwa nini?
10, 11. Jina la Yehova linatusaidia jinsi gani kuwa na uhakika kwamba yeye ni Baba bora anayeweza kutimiza wajibu wowote ule? Toa mfano.
10 Kwa mfano: Wazazi wanajua jinsi wanavyotimiza wajibu mbalimbali wanapowatunza watoto wao. Kwa siku moja tu, mzazi anaweza kutenda kama muuguzi, mpishi, mwalimu, mtoa-nidhamu, hakimu, na kadhalika. Wengi hulemewa na wajibu mbalimbali walio nao. Wazazi wengi wanajua kwamba watoto wao huwatumaini kabisa, hawana shaka kwamba Baba au Mama anaweza kupunguza maumivu ya jeraha, kusuluhisha mabishano, kurekebisha kitu chochote cha kuchezea kilichoharibika, na kujibu maswali yoyote wanayouliza kwa sababu ya udadisi-dadisi wa kitoto. Wazazi fulani wanahisi kwamba hawastahili kutumainiwa na watoto wao na mara kwa mara wanavunjika moyo kwa sababu wanashindwa kutimiza kikamili wajibu mwingi walio nao. Jambo hilo linawasikitisha sana.
11 Yehova pia ni Baba mwenye upendo. Yeye huwa chochote atakacho ili kuwatunza watoto wake wa kidunia kwa njia nzuri zaidi, bila kukiuka sheria zake kamilifu. Kwa hiyo, maana ya jina lake, Yehova, inatuhakikishia kwamba yeye ni Baba bora kabisa. (Yakobo 1:17) Punde si punde, Musa na Waisraeli wengine waaminifu waliona kwamba kwa kweli Yehova hutenda kupatana na maana ya jina lake. Walistaajabu kwa kicho Mungu alipoamua kuwa Amiri Jeshi asiyeshindwa, Mdhibiti wa hali zote za asili, Mtunga-sheria asiye na kifani, Hakimu, Msanifu-ujenzi, Mpaji wa chakula na maji, Mtunzaji wa mavazi na viatu—na kadhalika.
12. Maoni ya Farao juu ya Yehova yalitofautiana na ya Musa jinsi gani?
12 Hivyo basi, Mungu amejulisha jina lake, amefunua mambo yenye kusisimua kuhusu yule anayewakilishwa na jina hilo, na hata ameonyesha kwamba yale anayosema kujihusu ni ya kweli. Hapana shaka kwamba Mungu anataka tumjue. Tunaitikiaje? Musa alitaka kumjua Mungu. Hamu hiyo kubwa iliongoza mwenendo wa Musa maishani na ikamsaidia kumkaribia sana Baba yake wa mbinguni. (Hesabu 12:6-8; Waebrania 11:27) Inasikitisha kwamba watu wengi walioishi pindi hiyo hawakuwa na hamu ya kumjua Mungu kama Musa. Musa alipomtajia Farao jina la Yehova, mfalme huyo wa Misri mwenye kiburi aliuliza hivi kwa ukali: “Yehova ni nani?” (Kutoka 5:2, NW) Farao hakutaka kujifunza mengi kumhusu Yehova. Badala yake, alimpuuza Mungu wa Israeli na kumdhihaki kuwa Mungu duni au asiyefaa. Watu wengi leo wana maoni hayohayo. Maoni hayo huwafanya watu wakose kutambua mojawapo ya kweli muhimu zaidi—kwamba Yehova ni Bwana Mwenye Enzi Kuu.
Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova
13, 14. (a) Kwa nini Yehova amepewa majina mengi ya cheo kwenye Biblia? Taja baadhi yake. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 14.) (b) Kwa nini Yehova peke yake ndiye anayestahili kuitwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu”?
13 Yehova anaweza kutimiza wajibu mbalimbali, hivi kwamba kwa kufaa Maandiko yanamtaja kwa majina mengi ya cheo. Majina hayo hayachukui mahali pa jina lake; badala yake, yanatufundisha mengi kuhusu maana ya jina lake. Kwa mfano, anaitwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (2 Samweli 7:22, NW) Cheo hicho kitukufu, ambacho kinatajwa tena na tena katika Biblia, hutufahamisha wadhifa wa Yehova. Yeye peke yake ndiye aliye na haki ya kuwa Mtawala wa ulimwengu mzima. Hebu chunguza sababu.
14 Yehova ni wa pekee kwa sababu ni Muumba. Andiko la Ufunuo 4:11 lasema hivi: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” Maneno hayo ya fahari hayawezi kurejezea mtu mwingine yeyote. Kila kitu ulimwenguni kiliumbwa na Yehova! Hapana shaka kwamba Yehova anastahili heshima, na nguvu, na utukufu kwa sababu yeye ni Bwana Mwenye Enzi Kuu na Muumba wa vitu vyote.
15. Kwa nini Yehova anaitwa “Mfalme wa umilele”?
15 Jina jingine la cheo linalotumiwa kumhusu Yehova peke yake ni “Mfalme wa umilele.” (1 Timotheo 1:17; Ufunuo 15:3) Hilo lamaanisha nini? Akili zetu duni haziwezi kufahamu maana yake, lakini Yehova ni Mungu wa umilele kwa sababu hana mwanzo wala mwisho. Andiko la Zaburi 90:2 lasema: “Na tangu milele hata milele ndiwe Mungu.” Kwa hiyo Yehova hakuwa na mwanzo; amekuwapo daima dawamu. Anaitwa kwa kufaa “Mzee wa Siku,” kwa sababu amekuwapo kwa umilele kabla ya mtu yeyote na kabla ya kitu chochote kuwapo! (Danieli 7:9, 13, 22) Ni nani anayeweza kupinga kihalali haki yake ya kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu?
16, 17. (a) Kwa nini hatuwezi kumwona Yehova, na kwa nini hilo halipasi kutushangaza? (b) Yehova yukoje halisi kuliko kitu chochote tunachoweza kuona au kugusa?
16 Lakini watu fulani hupinga haki yake kama alivyofanya Farao. Tatizo hilo linazuka kwa sababu wanadamu wasiokamilika huamini hasa vitu wanavyoweza kuona. Hatuwezi kumwona Bwana Mwenye Enzi Kuu. Yeye ni roho, na wanadamu hawawezi kumwona. (Yohana 4:24) Isitoshe, mwanadamu mwenye mwili wa damu na nyama hawezi kumwona Yehova Mungu uso kwa uso na aishi. Yehova mwenyewe alimwambia Musa hivi: “Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.”—Kutoka 33:20; Yohana 1:18.
17 Jambo hilo halipasi kutushangaza. Ni wazi kwamba Musa aliona kwa kiasi kidogo utukufu wa Yehova kupitia kwa malaika aliyemwakilisha. Matokeo yalikuwa nini? Uso wa Musa ‘uling’aa’ kwa muda fulani baadaye. Waisraeli hata waliogopa kumtazama Musa usoni. (Kutoka 33:21-23; 34:5-7, 29, 30) Hivyo basi, ni wazi kwamba hakuna mwanadamu awaye yote anayeweza kumtazama Bwana Mwenye Enzi Kuu katika utukufu wake wote! Je, hilo lamaanisha kwamba yeye si halisi kama vitu tunavyoweza kuona na kugusa? La hasha, kuna vitu vingi tunavyokubali ni halisi ijapokuwa hatuwezi kuviona—kwa mfano, upepo, mawimbi ya redio, na mawazo. Zaidi ya hayo, Yehova hudumu milele, haathiriwi na kupita kwa wakati, hata mabilioni mengi ya miaka! Katika maana hiyo, yeye ni halisi kuliko kitu chochote tunachoweza kugusa au kuona, kwa kuwa vitu vya kimwili huzeeka na kuoza. (Mathayo 6:19) Basi je, tumwone tu kuwa nguvu fulani isiyoonekana na isiyo na utu, au Kisababishi kisichoeleweka? Hebu tuone.
Mungu Mwenye Utu
18. Ezekieli alipewa ono gani, na zile nyuso nne za “viumbe hai” walio karibu na Yehova zinawakilisha nini?
18 Ijapokuwa hatuwezi kumwona Mungu, kuna maandiko ya Biblia yenye kusisimua yanayotusaidia kuelewa hali ya mbinguni. Mojawapo ni sura ya kwanza ya Ezekieli. Ezekieli alipewa ono la tengenezo la kimbingu la Yehova, lililofananishwa na gari kubwa mno la kimbingu. Jambo linalovutia zaidi ni maelezo kuhusu viumbe wa roho wenye nguvu wanaomzingira Yehova. (Ezekieli 1:4-10) Hao “viumbe hai” wanashirikiana kwa ukaribu na Yehova, na umbo lao latusaidia kuelewa jambo muhimu sana kuhusu Mungu wanayemtumikia. Kila kiumbe ana nyuso nne—uso wa fahali, simba, tai, na mwanadamu. Ni wazi kwamba nyuso hizo zinawakilisha sifa nne kuu za utu wa Yehova.—Ufunuo 4:6-8, 10.
19. Ni sifa ipi inayowakilishwa na (a) uso wa fahali? (b) uso wa simba? (c) uso wa tai? (d) uso wa mwanadamu?
19 Mara nyingi fahali hutumiwa katika Biblia kuwakilisha nguvu, na hilo linafaa kwa sababu ni mnyama mwenye nguvu sana. Kwa upande mwingine, simba mara nyingi huwakilisha haki, kwa sababu haki ya kweli inahitaji ujasiri, sifa kuu ya simba. Tai ni maarufu kwa sababu ya uwezo wao makini wa kuona, wanaweza kuona hata vitu vidogo sana vilivyo umbali wa kilometa nyingi. Kwa hiyo, uso wa tai unawakilisha ifaavyo hekima ya Mungu ya kutambua mambo kimbele. Vipi uso wa mwanadamu? Kwa kweli, mwanadamu, aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu, hana kifani katika kuonyesha sifa kuu zaidi ya Mungu—upendo. (Mwanzo 1:26) Sifa hizo mbalimbali za utu wa Yehova—nguvu, haki, hekima, na upendo—hukaziwa tena na tena katika Maandiko hivi kwamba zinaweza kuitwa sifa kuu za Mungu.
20. Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda utu wa Yehova umebadilika, na kwa nini unajibu hivyo?
20 Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda Mungu amebadilika tangu Biblia ilipotaja sifa zake maelfu ya miaka iliyopita? La, utu wa Mungu haubadiliki. Anatuambia hivi: “Mimi, BWANA, sina kigeugeu.” (Malaki 3:6) Yehova habadili maoni yake ovyoovyo, badala yake yeye hujithibitisha kuwa Baba anayefaa kabisa kwa kukabiliana na kila hali inayozuka. Yeye hudhihirisha sifa muhimu za utu wake kwa wakati unaofaa. Kati ya zile sifa nne, sifa kuu zaidi ni upendo. Upendo hudhihirika katika kila jambo ambalo Mungu anafanya. Yeye hutumia nguvu, haki, na hekima yake kwa njia ya upendo. Kwa kweli, Biblia husema jambo fulani la pekee kuhusu Mungu na sifa hii. Inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Hebu ona kwamba haisemi Mungu ana upendo wala haisemi Mungu hupenda. Badala yake, inasema kwamba Mungu ni upendo. Upendo, ambao ni utu wake wa asili, huongoza matendo yake yote.
“Tazama, Huyu Ndiye Mungu Wetu”
21. Tutahisije tunapoendelea kujua sifa za Yehova vizuri zaidi?
21 Je, umewahi kumwona mtoto mdogo akiwaonyesha rafiki zake babaye na kusema hivi kwa furaha na fahari, “Huyu ni baba yangu”? Waabudu wa Mungu wana sababu nzuri sana za kuhisi vivyo hivyo kumhusu Yehova. Biblia inatabiri kuhusu wakati ambapo watu waaminifu watasema hivi kwa shauku: “Tazama, huyu ndiye Mungu wetu.” (Isaya 25:8, 9) Kadiri unavyojua sifa za Yehova vizuri zaidi, ndivyo utakavyohisi kwamba una Baba bora zaidi.
22, 23. Biblia inasema Baba yetu wa mbinguni yukoje, nasi twajuaje kwamba anataka tumkaribie?
22 Huyu si Baba asiye na hisia au asiyejali kama vile wanadini na wanafalsafa fulani washupavu wanavyofundisha. Hatuwezi kumkaribia Mungu asiye na hisia, wala Biblia haisemi kwamba Baba yetu wa mbinguni yuko hivyo. Badala yake, inamwita “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Ana hisia changamfu na zenye upendo. Yeye ‘huhuzunika moyo’ viumbe wake wenye akili wanapokosa kutii maagizo anayowapa ili kuwalinda. (Mwanzo 6:6; Zaburi 78:41) Lakini tunapotenda kwa hekima kupatana na Neno lake, ‘tunaufurahisha moyo’ wake.—Mithali 27:11.
23 Baba yetu anataka tumkaribie. Neno lake hutuhimiza ‘tupapase-papase tukimtafuta na kwa kweli tumpate, ijapokuwa, kwa kweli yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.’ (Matendo 17:27) Lakini, wanadamu wanaweza kumkaribia jinsi gani Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu?
-
-
Je, Kweli Unaweza ‘Kumkaribia Mungu’?Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 2
Je, Kweli Unaweza ‘Kumkaribia Mungu’?
1, 2. (a) Huenda watu wengi wakaona jambo jipi kuwa lisilowezekana, lakini Biblia inatuhakikishia nini? (b) Abrahamu alifurahia uhusiano upi wa karibu, na kwa nini?
UNGEHISIJE ikiwa Muumba wa mbingu na dunia angesema hivi kukuhusu, “Huyu ni rafiki yangu”? Huenda watu wengi wakaliona kuwa jambo lisilowezekana. Kwani, mwanadamu anawezaje kuwa rafiki ya Yehova Mungu? Lakini, Biblia inatuhakikishia kwamba tunaweza kwa kweli kumkaribia Mungu.
2 Abrahamu aliyeishi nyakati za kale alifurahia uhusiano wa karibu na Mungu. Yehova alimwita huyo mzee wa ukoo “rafiki yangu.” (Isaya 41:8) Naam, Yehova alimwona Abrahamu kuwa rafiki yake mkubwa. Abrahamu alifurahia uhusiano huo wa karibu kwa sababu “aliweka imani katika Yehova.” (Yakobo 2:23) Hali kadhalika leo, Yehova hutafuta fursa za ‘kuwapenda kwa dhati’ wale wanaomtumikia kwa sababu wanampenda. (Kumbukumbu la Torati 10:15, Biblia Habari Njema) Neno lake linatusihi hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Anatualika tumkaribie na kututolea ahadi kwa maneno hayo.
3. Yehova anatualika tufanye nini, naye anatuahidi nini?
3 Yehova anatualika tumkaribie. Yuko tayari na ana nia ya kutukubali kuwa rafiki zake. Vilevile, anaahidi kwamba tukijitahidi kumkaribia, atatukaribia pia. Kwa hiyo, tunaweza kufurahia jambo muhimu sana—kuwa ‘msiri wa BWANA.’a (Zaburi 25:14) Neno ‘-a siri’ latoa maana ya mazungumzo ya siri na rafiki wa karibu.
4. Rafiki msiri ni rafiki wa aina gani, na Yehova huthibitikaje kuwa rafiki msiri kwa wale wanaomkaribia?
4 Je, una rafiki msiri unayezungumza naye mambo yako ya siri? Huyo ni rafiki anayekujali. Unamtumaini kwa sababu amekuwa mwaminifu. Unafurahi hata zaidi unapomwambia mambo yanayokufurahisha. Anasikiliza kwa huruma unapomweleza mambo yanayokuhuzunisha na hivyo unapata utulivu. Hata inapoonekana kwamba hakuna mtu mwingine anayeelewa hali yako, yeye hukuelewa. Vivyo hivyo, unapomkaribia Mungu, unapata Rafiki wa pekee ambaye anakuthamini sana, anakujali sana, na kukuelewa kabisa. (Zaburi 103:14; 1 Petro 5:7) Unamtumaini na kumweleza hisia zako za moyoni, kwa kuwa unajua kwamba yeye ni mwaminifu kwa wale walio waaminifu kwake. (Zaburi 18:25, Biblia Habari Njema) Hata hivyo, Mungu ndiye ametuandalia fursa ya kuwa na urafiki wa karibu sana pamoja naye.
Yehova Amefungua Njia
5. Yehova alifanya nini ili kutuwezesha tumkaribie?
5 Tukiwa wanadamu wenye dhambi hatungeweza kamwe kumkaribia Mungu pasipo msaada. (Zaburi 5:4) “Lakini Mungu apendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu,” akaandika mtume Paulo. (Waroma 5:8) Ndiyo, Yehova alipanga Yesu ‘atoe nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Imani yetu katika dhabihu hiyo ya fidia hutuwezesha kumkaribia Mungu. Kwa kuwa Mungu “alitupenda sisi kwanza,” alituwekea msingi ili tuwe na urafiki pamoja naye.—1 Yohana 4:19.
6, 7. (a) Tunajuaje kwamba Yehova si Mungu aliyejificha na asiyeeleweka? (b) Yehova amejifunua kwa njia zipi?
6 Yehova amechukua hatua nyingine: Amejifunua kwetu. Katika urafiki wowote ule, uhusiano wa karibu hutegemea kumjua mtu kabisa, kuthamini sifa na mwenendo wake. Kwa hiyo, hatungeweza kamwe kumkaribia Yehova endapo angekuwa Mungu aliyejificha na asiyeeleweka. Lakini, yeye hajifichi, anataka tumjue. (Isaya 45:19) Isitoshe, watu wote hata wale ambao huenda wanaonwa na ulimwengu kuwa watu wa hali ya chini wanaweza kujua mambo anayofunua kujihusu.—Mathayo 11:25.
Yehova amejifunua kupitia uumbaji wake na Neno lake lililoandikwa
7 Yehova amejifunuaje kwetu? Uumbaji wake unafunua sifa mbalimbali za utu wake—nguvu zake zisizo na mipaka, hekima yake isiyo na kifani, na upendo wake mkubwa. (Waroma 1:20) Lakini Yehova hujifunua kwa njia nyingine mbali na uumbaji wake. Yehova huwaelimisha watu daima kwa njia bora sana, na hivyo ametupatia Neno lake, Biblia, ambalo linafunua jinsi alivyo.
Kuutazama ‘Uzuri wa Bwana’
8. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Biblia yenyewe ni ushuhuda wa kwamba Yehova anatupenda?
8 Biblia yenyewe ni ushuhuda wa kwamba Yehova anatupenda. Katika Neno lake, yeye hujifunua kwa kutumia lugha tunayoweza kufahamu—na hilo huthibitisha kwamba anatupenda na anataka tumjue na kumpenda. Habari tunazosoma katika kitabu chake muhimu sana hutuwezesha tuutazame “uzuri wa BWANA” na hutufanya tutake kuwa karibu naye. (Zaburi 90:17) Na tuzungumzie baadhi ya njia zenye kuvutia ambazo Yehova hujifunua katika Neno lake.
9. Ni ipi baadhi ya mistari ya Biblia inayotaja sifa za Mungu moja kwa moja?
9 Maandiko yana mistari mingi inayotaja sifa za Mungu moja kwa moja. Angalia mifano kadhaa. “BWANA hupenda haki.” (Zaburi 37:28) Mungu ni “mkuu mwenye uweza.” (Ayubu 37:23) “‘Mimi ni mwaminifu,’ asema Yehova.” (Yeremia 3:12, NW) “Yeye ni mwenye hekima moyoni.” (Ayubu 9:4) Yeye ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.” (Kutoka 34:6) “Wewe, Bwana, u mwema, umekuwa tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Na kama ilivyotajwa katika sura iliyotangulia, kuna sifa moja kuu zaidi: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Unapotafakari sifa hizi zenye kupendeza, je, huvutiwi na Mungu huyu asiye na kifani?
Biblia inatusaidia tumkaribie Yehova
10, 11. (a) Ili kutusaidia kuelewa utu wake vizuri zaidi, Yehova ametaja nini katika Neno lake? (b) Ni simulizi gani la Biblia linalotusaidia kuona Mungu akidhihirisha nguvu zake?
10 Mbali na kutueleza sifa zake, kwa upendo Yehova ametaja pia katika Neno lake mifano hususa inayoonyesha jinsi alivyodhihirisha sifa hizo kwa matendo. Masimulizi hayo yanatokeza picha akilini inayotusaidia kufahamu vizuri zaidi sifa mbalimbali za utu wake. Na hilo hutusaidia kumkaribia. Fikiria mfano mmoja.
11 Ni jambo moja kusoma kwamba Mungu “ni hodari kwa nguvu.” (Isaya 40:26) Na ni jambo tofauti kabisa kusoma kuhusu jinsi alivyokomboa Israeli walipovuka Bahari Nyekundu kisha akalitunza taifa hilo jangwani kwa miaka 40. Hebu ona yale maji yenye nguvu yakigawanyika. Ona taifa hilo—lenye jumla ya watu 3,000,000 hivi—likitembea katika bonde kavu la bahari, maji yakiwa yamegandamana na kusimama wima kama kuta kubwa upande huu na upande huu. (Kutoka 14:21; 15:8) Unaweza kuona uthibitisho wa kwamba Mungu aliwatunza na kuwalinda jangwani. Maji yalitiririka mwambani. Chakula kilichokuwa mfano wa punje nyeupe, kilisambaa ardhini. (Kutoka 16:31; Hesabu 20:11) Kisa hicho chaonyesha kwamba Yehova ana nguvu na yeye huzitumia kuwasaidia watu wake. Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba sala zetu humfikia Mungu mwenye nguvu ambaye ‘ni kimbilio letu na nguvu yetu, na msaada wetu daima wakati wa taabu’?—Zaburi 46:1, BHN.
12. Yehova hutusaidiaje kufahamu jinsi alivyo kwa kutumia usemi tunaoweza kuelewa?
12 Yehova, ambaye ni roho, amefanya mengi zaidi ili kutusaidia kumjua. Tukiwa wanadamu, uwezo wetu wa kuona una mipaka na hivyo hatuwezi kuona makao ya roho. Kama Mungu angetueleza utu wake kwa kutumia usemi wa roho ingekuwa ni kama kujaribu kumweleza mtu aliyezaliwa kipofu kila jambo kuhusu sura yako, kama vile rangi ya macho yako au madoa uliyo nayo ngozini. Badala yake, Yehova hutusaidia kwa fadhili kufahamu jinsi alivyo kwa kutumia usemi tunaoweza kuelewa. Nyakati nyingine, yeye huongea kwa kutumia semi za mlinganisho na mifano, akijifananisha na vitu tunavyojua. Hata anajieleza kuwa na viungo fulani vya kibinadamu.b
13. Andiko la Isaya 40:11 linaleta picha gani akilini, nalo linakufanya uhisije?
13 Hebu tazama jinsi Yehova anavyofafanuliwa katika Isaya 40:11: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake.” Hapa Yehova analinganishwa na mchungaji ambaye hubeba wana-kondoo “mikononi mwake.” Hilo laonyesha uwezo wa Mungu wa kuwalinda na kuwategemeza watu wake, hata wale walio dhaifu. Tunaweza kuhisi tukiwa salama katika mikono yake yenye nguvu, kwa sababu hatatuacha kamwe tukiwa waaminifu kwake. (Waroma 8:38, 39) Mchungaji Mkuu huwachukua wana-kondoo “kifuani mwake”—usemi huo unarejezea mapindo mapana ya vazi la juu, ambamo nyakati nyingine mchungaji alibebea mwana-kondoo aliyetoka kuzaliwa. Kwa hiyo, tunahakikishiwa kwamba Yehova anatupenda sana naye anatutunza kwa upendo. Ni jambo la kawaida kutaka kuwa karibu naye.
‘Mwana Anapenda Kumfunua’
14. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yehova hujifunua kindani zaidi kupitia Yesu?
14 Yehova hujifunua kindani zaidi katika Neno lake kupitia Mwanaye mpendwa, Yesu. Hakuna mtu awaye yote angeweza kudhihirisha hisia na fikira za Mungu kwa njia bora zaidi au kueleza utu Wake kwa njia wazi zaidi kuliko Yesu. Kwani, Mwana huyo mzaliwa wa kwanza aliishi na Baba yake kabla ya viumbe wengine wa roho na ulimwengu kuumbwa. (Wakolosai 1:15) Yesu alimjua Yehova kabisa. Ndiyo sababu alisema: ‘Mwana ni nani hakuna ajuaye ila Baba; na ya kwamba Baba ni nani, hakuna ajuaye ila Mwana, na yeye ambaye Mwana anapenda kumfunua.’ (Luka 10:22) Alipokuwa mwanadamu duniani, Yesu alimfunua Baba yake kwa njia mbili muhimu.
15, 16. Yesu alimfunua Baba yake katika njia zipi mbili?
15 Kwanza, mafundisho ya Yesu yanatusaidia kumjua Baba yake. Yesu alieleza jinsi Yehova alivyo kwa kutumia maneno yanayotugusa hisia. Kwa mfano, alipokuwa akieleza kuhusu Mungu mwenye rehema anayewakaribisha tena watenda-dhambi wanaotubu, Yesu alimlinganisha Yehova na baba mwenye rehema. Baba huyo anasikitika sana anapomwona mwanaye aliyepotea akirudi, anamkimbilia na kumkumbatia na kumbusu kwa upendo. (Luka 15:11-24) Yesu pia alionyesha kwamba Yehova ni Mungu ambaye ‘anavuta’ watu wenye mioyo minyofu kwa sababu anampenda kila mmoja wao. (Yohana 6:44) Yeye hata hujua shore mdogo anapoanguka kwenye ardhi. “Msiwe na hofu, nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi,” akaeleza Yesu. (Mathayo 10:29, 31) Bila shaka tunavutiwa kumkaribia Mungu huyo mwenye kujali.
16 Pili, kielelezo cha Yesu kinatuonyesha utu wa Yehova. Yesu alimwiga kabisa Baba yake hata akasema hivi: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Kwa hiyo, tunaposoma habari za Yesu kwenye vitabu vya Injili—hisia alizokuwa nazo na jinsi alivyowatendea wengine—tunaweza kusema kwamba tunaona udhihirisho halisi wa Baba yake. Huo ndio ufunuo bora zaidi na ulio wazi zaidi wa sifa za Yehova. Kwa nini?
17. Toa mfano unaoonyesha jambo ambalo Yehova amefanya ili kutusaidia tumjue.
17 Kwa mfano: Hebu jiwazie ukijaribu kueleza maana ya fadhili. Huenda ukaifafanua kwa maneno. Lakini ukiashiria mtu fulani anayetenda tendo la fadhili na kusema, “Yule anafanya tendo la fadhili,” neno “fadhili” huwa wazi na hueleweka kwa urahisi zaidi. Yehova amefanya vivyo hivyo ili kutusaidia tumjue. Pamoja na kueleza utu wake kwa maneno, ametupa kielelezo halisi cha Mwanaye. Matendo ya Yesu yanadhihirisha sifa za Mungu waziwazi. Kupitia vitabu vya Injili vinavyosimulia habari za Yesu, ni kana kwamba Yehova anasema hivi: “Hivyo ndivyo nilivyo.” Maandiko yaliyopuliziwa yanasema Yesu alikuwaje alipokuwa duniani?
18. Yesu alionyeshaje sifa za nguvu, haki, na hekima?
18 Sifa nne kuu za Mungu zilidhihirishwa kwa njia ya pekee sana na Yesu. Alikuwa na nguvu za kukomesha magonjwa, njaa, hata kifo. Lakini, hakutumia kamwe nguvu zake za kufanya miujiza ili kujifaidi au kuwaumiza wengine kama wanadamu wenye ubinafsi wanavyotumia vibaya nguvu zao. (Mathayo 4:2-4) Alipenda haki. Alikasirika sana kwa njia ya uadilifu alipoona wafanyabiashara wenye hila wakiwapunja watu. (Mathayo 21:12, 13) Hakuwaonea maskini na wenye kudharauliwa, aliwasaidia kupata “burudisho” kwa ajili ya nafsi zao. (Mathayo 11:4, 5, 28-30) Mafundisho ya Yesu ambaye alikuwa “zaidi ya Solomoni,” yalikuwa na hekima isiyo na kifani. (Mathayo 12:42) Lakini Yesu hakujigamba kwa hekima hiyo. Maneno yake yaligusa hisia za watu wa hali ya chini, kwa kuwa mafundisho yake yalikuwa wazi, rahisi, na yenye kufaidi.
19, 20. (a) Yesu alionyeshaje upendo kwa njia ya pekee sana? (b) Tunaposoma na kutafakari kielelezo cha Yesu, tunapaswa kukumbuka nini?
19 Yeye alionyesha upendo kwa njia ya pekee sana. Katika huduma yake yote, alionyesha upendo kwa njia mbalimbali, alionyesha hisia-mwenzi na huruma. Alisikitika sana alipowaona watu wakiteseka. Mara nyingi, alichukua hatua kwa sababu ya kuwasikitikia wengine. (Mathayo 14:14) Ijapokuwa aliwaponya wagonjwa na kuwalisha wenye njaa, Yesu aliwahurumia watu kwa njia muhimu hata zaidi. Aliwasaidia wengine kujua, kukubali, na kupenda kweli kuhusu Ufalme wa Mungu ambao utawaletea wanadamu baraka za milele. (Marko 6:34; Luka 4:43) Zaidi ya yote, Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa kutoa nafsi yake kwa hiari kwa niaba ya wengine.—Yohana 15:13.
20 Si ajabu kwamba watu wa kila umri na malezi walivutiwa na mwanamume huyu mchangamfu na mwenye hisia sana. (Marko 10:13-16) Hata hivyo, tunaposoma na kutafakari maisha ya Yesu, tukumbuke daima kwamba Mwana huyo anatudhihirishia waziwazi utu wa Baba yake.—Waebrania 1:3.
Kitabu cha Kutusaidia Kujifunza
21, 22. Kumtafuta Yehova kwatia ndani nini, na kitabu hiki kina mambo yapi ya kutusaidia tufikie mradi huo?
21 Hapana shaka yoyote kwamba Yehova anataka tuwe karibu naye, kwa sababu amefunua utu wake waziwazi katika Neno lake. Lakini hatulazimishi kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye. Ni juu yetu kumtafuta Yehova “maadamu anapatikana.” (Isaya 55:6) Kumtafuta Yehova kwatia ndani kujua sifa zake na kujua njia yake ya kutenda mambo kama inavyoonyeshwa katika Biblia. Kitabu hiki kimekusudiwa kukusaidia ufikie mradi huo.
22 Utaona kwamba kitabu hiki kimegawanywa kwa sehemu zinazozungumzia sifa nne kuu za Yehova: nguvu, haki, hekima, na upendo. Kila sehemu huanza kwa kutoa muhtasari kuhusu sifa inayozungumziwa. Sura kadhaa zinazofuata zinazungumzia jinsi Yehova anavyodhihirisha sifa hiyo kwa njia mbalimbali. Kila sehemu pia ina sura inayoonyesha jinsi Yesu alivyodhihirisha sifa hiyo, na sura moja inayozungumzia jinsi tunavyoweza kudhihirisha sifa hiyo maishani mwetu.
23, 24. (a) Eleza kuhusu sehemu ya pekee ya “Maswali ya Kutafakari.” (b) Kutafakari kunatusaidiaje kumkaribia Mungu zaidi?
23 Kuanzia sura hii kuna sehemu ya pekee yenye kichwa “Maswali ya Kutafakari.” Kwa mfano, hebu angalia sanduku kwenye ukurasa wa 24. Maandiko na maswali yaliyoonyeshwa hayakusudiwi kurudia tu sura. Badala yake, yanakusudiwa kukusaidia utafakari mambo mengine muhimu kuhusiana na habari hiyo. Unaweza kutumiaje kwa manufaa sehemu hiyo? Fungua kila andiko lililotajwa, na ulisome kwa uangalifu sana. Kisha chunguza swali linaloambatana na kila andiko. Tafakari majibu yake. Unaweza kufanya utafiti. Jiulize maswali mengine ya ziada: ‘Habari hii inanifundisha nini kumhusu Yehova? Inanihusuje? Ninaweza kuitumiaje kuwasaidia wengine?’
24 Kutafakari kunaweza kutusaidia tumkaribie Yehova zaidi. Jinsi gani? Biblia inaonyesha kwamba kutafakari kunahusisha moyo. (Zaburi 19:14) Tunapothamini sana mambo tunayojifunza kumhusu Mungu, habari hizo hufika kwenye moyo wetu wa mfano, kisha zinabadili fikira zetu, zinagusa hisia zetu, na hatimaye tunachochewa kutenda. Upendo wetu kwa Mungu hutia mizizi, na upendo huo hutufanya tutake kumpendeza akiwa Rafiki yetu mpendwa. (1 Yohana 5:3) Ili kuwa na uhusiano huo, hatuna budi kujua sifa za Yehova na jinsi anavyotenda mambo. Kwanza, acheni tuzungumzie sifa moja ya utu wa Mungu ambayo hutuvutia sana tumkaribie—utakatifu wake.
a Jambo la kuvutia ni kwamba, neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘-a siri’ limetumiwa kwenye andiko la Amosi 3:7, lisemalo kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova huwafunulia watumishi wake “siri yake,” na kuwajulisha kimbele mambo anayokusudia kufanya.
b Kwa mfano, Biblia husema juu ya uso, macho, masikio, pua, kinywa, mikono, na miguu ya Mungu. (Zaburi 18:15; 27:8; 44:3; Isaya 60:13; Mathayo 4:4; 1 Petro 3:12) Semi hizo za mfano hazipasi kuchukuliwa kihalisi, kama tusivyoelewa kihalisi semi kama vile Yehova ni “Mwamba” au “ngao.”—Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 84:11.
-
-
“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Ni Bwana”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 3
“Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Ni Bwana”
1, 2. Isaya alipokea ono gani, na linatufundisha nini juu ya Yehova?
ISAYA alitiwa kicho na mandhari aliyoona—ono kutoka kwa Mungu. Ni kana kwamba lilikuwa halisi! Baadaye Isaya aliandika kwamba kwa kweli ‘alimwona Bwana’ ameketi katika kiti Chake cha enzi kilicho juu sana. Na pindo la vazi la Yehova lilijaza hekalu kubwa la Yerusalemu.—Isaya 6:1, 2.
2 Isaya alitiwa kicho pia na sauti aliyosikia—wimbo wenye nguvu sana hivi kwamba ulitikisa hekalu na misingi yake. Wimbo huo uliimbwa na maserafi, viumbe wa roho wenye cheo cha juu. Wimbo huo mtamu ulioimbwa kwa sauti ya juu na upatano ulivumisha maneno sahili ya fahari ya kifalme: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu, ni BWANA wa majeshi; dunia yote imejaa utukufu wake.” (Isaya 6:3, 4) Kuimba neno “mtakatifu” mara tatu kulikazia neno hilo kwa njia ya pekee sana. Jambo hilo lafaa kwa sababu utakatifu wa Yehova ni wa hali ya juu sana. (Ufunuo 4:8) Utakatifu wa Yehova unakaziwa katika Biblia nzima. Kuna mamia ya mistari ya Biblia inayotaja jina lake pamoja na maneno “takatifu” na “utakatifu.”
3. Kwa nini maoni yenye kosa kuhusu utakatifu wa Yehova yanawafanya watu wengi wakatae kumkaribia Mungu?
3 Hivyo basi, ni wazi kwamba mojawapo ya mambo muhimu ambayo Yehova anataka tujue kumhusu ni kuwa yeye ni mtakatifu. Lakini watu wengi leo huchukizwa na wazo hilo. Baadhi yao hudhani kimakosa kwamba kuwa mtakatifu kunamaanisha kujiona kuwa mwadilifu au kujidai kuwa mchaji-Mungu. Watu wanaojiona kuwa hawafai huenda wakahofu badala ya kuvutiwa na wazo la kuwa Mungu ni mtakatifu. Huenda wakahofu kwamba hawawezi kustahili kamwe kumkaribia Mungu huyo mtakatifu. Kwa hiyo, watu wengi hawataki kumkaribia Mungu kwa sababu ya utakatifu wake. Inasikitisha sana kwa sababu utakatifu wa Mungu kwa kweli ni kichocheo cha kumkaribia. Kwa nini? Kabla ya kujibu swali hilo, hebu tuzungumzie maana halisi ya utakatifu.
Utakatifu Ni Nini?
4, 5. (a) Neno “utakatifu” linamaanisha nini, nalo halimaanishi nini? (b) Yehova “amejitenga” katika njia zipi mbili muhimu?
4 Ingawa Mungu ni mtakatifu haimaanishi kwamba yeye anajivuna, ni mwenye kiburi, au anawadharau wengine. Badala yake, anachukia sifa hizo. (Mithali 16:5; Yakobo 4:6) Basi neno “-takatifu” linamaanisha nini? Katika Kiebrania cha Biblia, neno lililotafsiriwa “-takatifu” linatokana na neno linalomaanisha “kutenga.” Katika ibada, kitu “kitakatifu” ni kile kilichotengwa kwa ajili ya matumizi maalumu. Utakatifu pia hutoa wazo la usafi na utakato. Neno hilo hutumiwaje kuhusiana na Yehova? Je, yamaanisha kwamba yeye ‘hujitenga’ mbali na wanadamu wasiokamilika, au kwamba yuko mbali nasi?
5 La hasha. Akiwa “Mtakatifu wa Israeli,” Yehova alisema kuwa anakaa “katikati” ya watu wake, licha ya kwamba walikuwa wenye dhambi. (Isaya 12:6; Hosea 11:9) Kwa hiyo, hajitengi na watu kwa sababu yeye ni mtakatifu. Basi yeye “hujitengaje”? Yeye hujitenga katika njia mbili muhimu. Kwanza, yeye amejitenga na viumbe wote katika maana ya kwamba yeye peke yake ndiye Aliye Juu Sana. Usafi wake, na utakato wake, ni kamili kabisa na unadumu milele. (Zaburi 40:5; 83:18) Pili, Yehova amejitenga kabisa na dhambi, na hilo linatufariji. Kwa nini?
6. Kwa nini ni faraja kujua kwamba Yehova hana dhambi kabisa?
6 Tunaishi katika ulimwengu ambamo utakatifu wa kweli ni haba. Kila jambo linalofanywa na wanadamu waliojitenga na Mungu limepotoka kwa njia fulani, limechafuliwa na dhambi na kutokamilika. Sote tunapambana na dhambi iliyo mwilini mwetu. Sote tunakabili hatari ya kushindwa na dhambi tusipojihadhari. (Waroma 7:15-25; 1 Wakorintho 10:12) Yehova hakabili hatari hiyo. Yeye hana dhambi kabisa, hatachafuliwa kamwe na dhambi yoyote. Hilo latuthibitishia kwamba Yehova ndiye Baba bora, kwa sababu yeye ni mwenye kutegemeka kabisa. Tofauti na akina baba wengi wenye dhambi, Yehova hawezi kupotoka kamwe, wala kuwa na utovu wa maadili, au kuwadhuru kamwe watoto wake. Hawezi kutenda kamwe mambo hayo kwa sababu yeye ni mtakatifu. Yehova hata ameapa kwa utakatifu wake pindi fulani-fulani, na hilo linafanya viapo vyake viwe vyenye kutumainika kabisa. (Amosi 4:2) Je, hilo halitufariji?
7. Kwa nini tunaweza kusema kwamba utakatifu ni sehemu ya utu wa Yehova?
7 Utakatifu ni sehemu ya utu wa Yehova. Hilo lamaanisha nini? Kwa mfano: Fikiria maneno “mwanadamu” na “kutokamilika.” Huwezi kueleza hali ya wanadamu bila kufikiria hali ya kutokamilika. Hali ya kutokamilika inaathiri kila jambo tunalofanya. Sasa fikiria maneno mawili tofauti kabisa—“Yehova” na “utakatifu.” Yehova ana utakatifu kamili. Kila jambo kumhusu ni safi, limetakata, na ni adilifu. Hatuwezi kumjua Yehova kikweli bila kufikiria kwa uzito na kufahamu neno hili muhimu—“-takatifu.”
“Utakatifu Ni wa Yehova”
8, 9. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova huwasaidia wanadamu wasiokamilika kuwa watakatifu kwa kadiri fulani?
8 Kwa kuwa utakatifu ni sehemu ya utu wa Yehova, tunaweza kusema kwa kufaa kwamba yeye ndiye chanzo cha utakatifu wote. Yeye hajiwekei kwa ubinafsi sifa hii yenye thamani; yeye huwapa wengine, naye huwapa kwa ukarimu. Mungu aliponena na Musa kwa kutumia malaika kwenye kichaka kilichokuwa kikiwaka moto, ardhi yote iliyokuwa karibu ikawa takatifu kwa sababu Yehova alikuwa akitumia sehemu hiyo!—Kutoka 3:5.
9 Je, wanadamu wasiokamilika wanaweza kuwa watakatifu kwa msaada wa Yehova? Ndiyo, kwa kadiri fulani. Mungu aliwapa watu wake Israeli fursa ya kuwa “taifa takatifu.” (Kutoka 19:6) Alibariki taifa hilo kwa kuliandalia ibada iliyokuwa takatifu na safi. Kwa hiyo, Sheria ya Kimusa inakazia utakatifu tena na tena. Kwa kweli, kuhani mkuu alivaa bamba la dhahabu upande wa mbele wa kilemba chake, na watu wote waliweza kuliona likimetameta kwenye nuru. Maneno haya yalichongwa juu yake: “Utakatifu ni wa Yehova.” (Kutoka 28:36, NW) Kwa hiyo, kiwango cha juu cha usafi na utakato kingefanya ibada yao na hata njia yao ya maisha iwe ya pekee. Yehova aliwaambia hivi: “Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi BWANA, Mungu wenu ni mtakatifu.” (Mambo ya Walawi 19:2) Waisraeli walikuwa watakatifu kwa kadiri fulani maadamu waliishi kupatana na maagizo ya Mungu kwa kadiri ya uwezo wa wanadamu wasiokamilika.
10. Israeli la kale lilitofautianaje na mataifa yaliyolizunguka kwa habari ya utakatifu?
10 Utakatifu huo ulikaziwa sana katika Israeli, tofauti sana na ibada ya mataifa yaliyolizunguka. Mataifa hayo ya kipagani yaliabudu miungu bandia ambayo haikuishi kamwe, miungu ambayo ilisifiwa kuwa yenye jeuri, yenye pupa, na yenye maadili mapotovu. Haikuwa mitakatifu kwa njia yoyote. Kuabudu miungu hiyo kuliwafanya watu wasiwe watakatifu. Kwa hiyo, Yehova aliwaonya watumishi wake wajitenge na waabudu hao wapagani na kuepuka mazoea yao machafu ya kidini.—Mambo ya Walawi 18:24-28; 1 Wafalme 11:1, 2.
11. Utakatifu wa tengenezo la Yehova la kimbingu unadhihirishwaje na (a) malaika? (b) maserafi? (c) Yesu?
11 Hata lilipokuwa katika hali bora zaidi, taifa la Israeli la kale lililochaguliwa na Yehova lilidhihirisha kwa kiwango kidogo sana utakatifu wa tengenezo la Mungu la kimbingu. Mamilioni ya viumbe wa roho wanaomtumikia Mungu kwa uaminifu wanaitwa “elfu kumi za watakatifu.” (Kumbukumbu la Torati 33:2, Zaire Swahili Bible; Yuda 14) Wanadhihirisha kikamilifu uangavu, na uzuri wa utakatifu wa Mungu. Kumbuka maserafi ambao Isaya aliona katika ono. Maneno ya wimbo wao yanadokeza kwamba viumbe hao wa roho wenye nguvu wanatimiza fungu muhimu sana katika kutangaza utakatifu wa Yehova kotekote ulimwenguni. Hata hivyo, kuna kiumbe mmoja wa roho aliye juu ya wote—Mwana mzaliwa pekee wa Mungu. Yesu anadhihirisha utakatifu wa Yehova kwa kiwango cha juu zaidi. Anaitwa kwa kufaa, “Mtakatifu wa Mungu.”—Yohana 6:68, 69.
Jina Takatifu, Roho Takatifu
12, 13. (a) Kwa nini jina la Mungu linaelezwa kwa kufaa kuwa takatifu? (b) Kwa nini ni lazima jina la Mungu litakaswe?
12 Vipi jina la Mungu? Kama tulivyoona kwenye Sura ya Kwanza, hilo si jina la cheo tu au kitambulisho. Linamwakilisha Yehova Mungu na sifa zake zote. Ndiyo sababu Biblia inatuambia kuwa “jina lake ni takatifu.” (Isaya 57:15, NW) Kulingana na Sheria ya Musa, mtu yeyote aliyelikufuru jina la Mungu aliuawa. (Mambo ya Walawi 24:16) Hebu ona jambo ambalo Yesu alitaja kwanza katika sala: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kutakasa kitu kwamaanisha kukitenga kuwa kitakatifu na kukistahi. Lakini kwa nini jina la Mungu ambalo ni takatifu kabisa linahitaji kutakaswa?
13 Jina takatifu la Mungu limechambuliwa na kuchafuliwa kwa uwongo na uchongezi. Katika Edeni, Shetani alisema uwongo kumhusu Yehova na akadokeza kwamba Yeye ni Mtawala asiye na haki. (Mwanzo 3:1-5) Tangu hapo, Shetani—mtawala wa ulimwengu huu usio mtakatifu—amehakikisha kwamba uwongo kumhusu Mungu umesambazwa kote. (Yohana 8:44; 12:31; Ufunuo 12:9) Dini zimefundisha kwamba Mungu ni mdhalimu, hana hisia, au ni mkatili. Wamedai kwamba Mungu anaunga mkono vita vyao vya kikatili. Mara nyingi wamesema kwamba uumbaji wa Mungu wa kustaajabisha ulijitokeza wenyewe, au viumbe viligeuka-geuka. Naam, jina la Mungu limechafuliwa vibaya sana. Ni lazima litakaswe; na kurudishiwa tena utukufu unaostahili. Tuna hamu ya kuona jina lake likitakaswa na enzi yake kuu ikitetewa, nasi tunafurahi kushiriki kutimiza kusudi hilo tukufu.
14. Kwa nini roho ya Mungu inaitwa takatifu, na kwa nini kukufuru roho takatifu ni dhambi nzito?
14 Kuna kitu kingine ambacho kinahusiana sana na Yehova ambacho daima kinaitwa kitakatifu—roho yake, au kani yake ya utendaji. (Mwanzo 1:2) Yehova hutumia kani yake isiyoweza kushindwa kutimiza makusudi yake. Matendo yote ya Mungu ni Matakatifu na safi, kwa hiyo kani yake ya utendaji inaitwa kwa kufaa roho takatifu, au roho ya utakatifu. (Luka 11:13; Waroma 1:4) Kukufuru roho takatifu, yaani kupinga makusudi ya Yehova kwa kudhamiria, ni dhambi isiyoweza kusamehewa.—Marko 3:29.
Kwa Nini Utakatifu wa Mungu Unatufanya Tumkaribie?
15. Kwa nini inafaa kumhofu Yehova kwa sababu ya utakatifu wake, na hofu hiyo yahusisha nini?
15 Basi si vigumu kuelewa kwa nini Biblia inahusianisha utakatifu wa Mungu na hali ya mwanadamu ya kumhofu. Kwa mfano, Zaburi 99:3 husema hivi: “Na walishukuru jina lake kuu la kuhofiwa; ndiye mtakatifu.” Lakini hofu hiyo si woga wa kupatwa na mabaya. Badala yake, ni kuwa na kicho na heshima sana, staha ya hali ya juu sana. Inafaa kuhisi hivyo, kwa sababu hatuwezi kamwe kufikia utakatifu wa Mungu. Umetakata sana na ni wenye utukufu. Hata hivyo, haupaswi kutuzuia kumkaribia. Kinyume chake, tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu utakatifu wa Mungu tutaweza kumkaribia zaidi. Kwa nini?
Utakatifu unapaswa kutuvutia kama uzuri unavyotuvutia
16. (a) Utakatifu unahusianaje na uzuri? Toa mfano. (b) Maono kumhusu Yehova yanakaziaje usafi, utakato na nuru?
16 Kwanza, Biblia huhusianisha utakatifu na uzuri. Kwenye Isaya 63:15, NW, mbingu inasemwa kuwa ‘makao matukufu ya Mungu ya utakatifu na uzuri.’ Uzuri hutuvutia. Kwa mfano, tazama picha iliyo kwenye ukurasa wa 33. Je, mandhari hiyo haikuvutii? Kwa nini inavutia? Hebu tazama jinsi maji yalivyo safi. Bila shaka, hewa pia ni safi, kwa kuwa anga lina rangi ya buluu na ni kana kwamba nuru inang’aa. Endapo mandhari hiyo ingebadilishwa—kijito kijazwe takataka, miti na miamba ichafuliwe kwa maandishi, hewa ijae moshi—haingetuvutia tena; ingetuchukiza. Kwa kawaida sisi huhusianisha uzuri na usafi, utakato, na nuru. Maneno hayohayo yanaweza kutumiwa kufafanua utakatifu wa Yehova. Si ajabu kwamba maono kumhusu Yehova yanatusisimua! Uzuri wa Mungu wetu mtakatifu ni kama nuru inayong’aa, unametameta kama vito, unawaka kama moto au madini safi yenye thamani ambayo yanang’aa.—Ezekieli 1:25-28; Ufunuo 4:2, 3.
17, 18. (a) Mwanzoni Isaya aliathiriwaje na ono alilopata? (b) Yehova alimtumiaje serafi ili kumfariji Isaya, na jambo alilotenda serafi huyo lilikuwa na maana gani?
17 Lakini je, tunapaswa kujihisi kuwa duni kwa sababu ya utakatifu wa Mungu? Bila shaka, jibu ni ndiyo. Vyovyote iwavyo, sisi ni duni tunapojilinganisha na Yehova—sisi ni duni sana isivyoelezeka. Je, kujua hivyo kwapasa kutufanya tujitenge naye? Fikiria itikio la Isaya aliposikia maserafi wakitangaza utakatifu wa Yehova. “Ndipo niliposema, Ole wangu! kwa maana nimepotea; kwa sababu mimi ni mtu mwenye midomo michafu, nami ninakaa kati ya watu wenye midomo michafu; na macho yangu yamemwona Mfalme, BWANA wa majeshi.” (Isaya 6:5) Ndiyo, utakatifu wa Yehova usio na kikomo ulimkumbusha Isaya kwamba yeye ni mwenye dhambi na mtu asiyekamilika. Mwanzoni, mwanamume huyo mwaminifu alifadhaika sana. Lakini Yehova hakumwacha akiwa katika hali hiyo.
18 Serafi alimfariji nabii huyo mara moja. Jinsi gani? Kiumbe huyo wa roho mwenye nguvu alipaa kwenye madhabahu, akatwaa kaa la moto, akagusa kinywa cha Isaya kwa kaa hilo. Huenda hilo likaonekana kuwa jambo lenye kuumiza sana badala ya kufariji. Hata hivyo, kumbuka kwamba hilo lilikuwa ono lenye maana nyingi ya mfano. Isaya, Myahudi mwaminifu, alijua vyema kwamba dhabihu zilitolewa kila siku kwenye madhabahu ya hekalu ili kulipia dhambi. Na kwa upendo, serafi huyo alimkumbusha nabii huyo kwamba ijapokuwa alikuwa “mtu mwenye midomo michafu” asiyekamilika, bado angeweza kuwa mwadilifu machoni pa Mungu.a Yehova alikuwa tayari kumwona mwanadamu asiyekamilika, na mwenye dhambi kuwa mtakatifu—angalau kwa kadiri fulani.—Isaya 6:6, 7.
19. Tunawezaje kuwa watakatifu kwa kadiri fulani, ijapokuwa hatujakamilika?
19 Ndivyo ilivyo leo. Dhabihu zote zilizotolewa kwenye madhabahu huko Yerusalemu zilikuwa kivuli tu cha kitu fulani kikubwa zaidi—dhabihu pekee iliyokuwa kamilifu, iliyotolewa na Yesu Kristo mwaka wa 33.W.K. (Waebrania 9:11-14) Tukitubu dhambi zetu kikweli, na kurekebisha mwenendo wetu mbaya, na kudhihirisha imani katika dhabihu hiyo, tunapata msamaha. (1 Yohana 2:2) Sisi pia tunaweza kuwa waadilifu machoni pa Mungu. Kwa hiyo, mtume Petro anatukumbusha hivi: “Imeandikwa: ‘Lazima mwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Petro 1:16) Ona kwamba Yehova hakusema lazima tuwe watakatifu kwa kadiri ambayo yeye ni mtakatifu. Yeye hatarajii kamwe tutimize mambo tusiyoweza. (Zaburi 103:13, 14) Badala yake, Yehova anatuambia tuwe watakatifu kwa sababu yeye ni mtakatifu. ‘Tukiwa watoto wapendwa,’ tunajitahidi kumwiga kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasiokamilika. (Waefeso 5:1) Kwa hiyo, kuwa watakatifu ni jitihada inayoendelea. Kadiri tunavyokua kiroho, tunajitahidi ‘kukamilisha utakatifu’ siku baada ya siku.—2 Wakorintho 7:1.
20. (a) Kwa nini ni muhimu kufahamu kwamba tunaweza kuwa safi machoni pa Mungu wetu mtakatifu? (b) Isaya alihisije alipojua kwamba dhambi zake zilikuwa zimefunikwa?
20 Yehova, anapenda mambo ya uadilifu na yaliyo safi. Anachukia dhambi. (Habakuki 1:13) Lakini yeye hatuchukii. Maadamu tuna maoni kama yake juu ya dhambi—tukichukia lililo baya, na kupenda lililo jema—na tunajitahidi kufuata hatua kamilifu za Kristo Yesu, Yehova husamehe dhambi zetu. (Amosi 5:15; 1 Petro 2:21) Tunapofahamu kwamba tunaweza kuwa safi machoni pa Mungu wetu mtakatifu, matokeo yanaweza kuwa mazuri ajabu. Kumbuka kwamba, mwanzoni utakatifu wa Yehova ulimkumbusha Isaya kwamba hakuwa safi. Alipaaza kilio: “Ole wangu!” Lakini mara tu alipojua kwamba dhambi zake zilikuwa zimefunikwa, mtazamo wake ulibadilika. Yehova alipokuwa akitafuta mtu ambaye angejitolea kutimiza kazi fulani, Isaya aliitikia mara moja, japo hakujua kazi hiyo ilihusisha nini. Alisema hivi kwa shauku: “Mimi hapa, nitume mimi.”—Isaya 6:5-8.
21. Tuna uhakika gani kwamba tunaweza kusitawisha sifa ya utakatifu?
21 Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu wetu mtakatifu, tumepewa sifa za adili na uwezo wa kuelewa mambo ya kiroho. (Mwanzo 1:26) Tunaweza sote kuwa watakatifu. Yehova anafurahi kutusaidia kuendelea kuusitawisha utakatifu. Tufanyapo hivyo, tutamkaribia zaidi Mungu wetu mtakatifu. Zaidi ya hayo, tunapozungumzia sifa za Yehova katika sura zinazofuata, tutaona kwamba kuna sababu nyingi nzuri za kumkaribia!
a Maneno “mwenye midomo michafu” yanafaa, kwa kuwa midomo mara nyingi hutumiwa kitamathali katika Biblia kurejezea usemi au lugha. Sehemu kubwa ya dhambi za wanadamu wote wasiokamilika, yamkini zinahusiana na jinsi tunavyotumia uwezo wetu wa kusema.—Mithali 10:19; Yakobo 3:2, 6.
-
-
“Mwenyezi-Mungu . . . Amejaa Nguvu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 4
“Mwenyezi-Mungu Amejaa Nguvu”
1, 2. Eliya alikuwa ameona mambo gani ya ajabu maishani mwake, lakini aliona matukio gani ya kustaajabisha alipokuwa katika pango kwenye Mlima Horebu?
ELIYA alikuwa ameona mambo ya ajabu hapo awali. Alikuwa ameona kunguru wakimletea chakula mara mbili kwa siku alipokuwa mafichoni. Alikuwa ameona unga na mafuta yaliyokuwa katika vyombo viwili yakitumiwa kwa muda mrefu sana wakati wa njaa kali. Hata alikuwa ameona moto ukishuka kutoka mbinguni baada ya kutoa sala. (1 Wafalme, sura ya 17, 18) Na bado, Eliya hakupata kuona tukio lolote la kustaajabisha kama matukio yafuatayo.
2 Eliya aliyejikunyata kwenye mwingilio wa pango kwenye Mlima Horebu aliona mfululizo wa matukio yenye kustaajabisha. Kwanza upepo ulivuma. Haikosi ulivuma kwa nguvu sana, na kwa sauti kubwa sana kwa kuwa uliipasua milima na kuvunja-vunja miamba. Kisha kukawa na tetemeko la nchi, nishati kubwa sana iliibuka na kutikisa dunia kwa nguvu sana. Halafu kukawa na moto. Yaelekea Eliya alipigwa na joto kali sana moto huo uliposambaa kwenye eneo hilo.—1 Wafalme 19:8-12.
“Na tazama, BWANA akapita”
3. Eliya aliona uthibitisho wa sifa ipi ya Mungu, nasi tuna uthibitisho gani wa sifa hiyo?
3 Matukio hayo mbalimbali ambayo Eliya aliona yalikazia jambo moja tu—yalidhihirisha nguvu nyingi za Yehova Mungu. Bila shaka, si lazima tuone muujiza ili tufahamu kwamba Mungu ana sifa hii. Sifa hii yaonekana waziwazi. Biblia yatuambia kwamba uumbaji unathibitisha ‘nguvu za Yehova za milele na Uungu’ wake. (Waroma 1:20) Hebu fikiria nuru yenye kupofusha na ngurumo za dhoruba ya radi, poromoko kubwa maridadi la maji, na anga pana kupindukia lililotapakaa nyota! Je, unaona nguvu za Mungu katika vitu hivyo? Lakini ni watu wachache tu ulimwenguni wanaotambua kikweli nguvu za Mungu. Na ni watu wachache hata zaidi walio na maoni yanayofaa kuhusu nguvu hizo. Hata hivyo, kufahamu sifa hii ya Mungu kunatupa sababu nyingi za kumkaribia Yehova zaidi. Katika sehemu hii, tutajifunza kwa undani kuhusu nguvu za Yehova zisizo na kifani.
Sifa Muhimu ya Yehova
4, 5. (a) Kuna uhusiano gani kati ya jina la Yehova na uwezo wake, au nguvu zake? (b) Kwa nini inafaa kwamba Yehova alitumia fahali kuwakilisha nguvu zake?
4 Nguvu za Yehova hazina kifani. Andiko la Yeremia 10:6 lasema hivi: “Hapana hata mmoja aliye kama wewe, Ee BWANA; wewe ndiwe uliye mkuu, na jina lako ni kuu katika uweza.” Ona kwamba uweza, au nguvu, zinahusianishwa na jina la Yehova. Ni wazi kwamba jina hilo linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwe.” Ni nini kinachomwezesha Yehova aumbe kitu chochote anachotaka na awe chochote anachotaka? Sababu moja ni nguvu zake. Naam, uwezo wa Yehova wa kutenda, na wa kutimiza mapenzi yake hauna mipaka. Nguvu hizo ni mojawapo ya sifa zake muhimu.
5 Hatuwezi kamwe kufahamu nguvu kamili za Yehova, kwa hivyo yeye hutumia mifano ili kutusaidia. Kama tulivyoona, yeye hutumia fahali kuwakilisha nguvu zake. (Ezekieli 1:4-10) Mfano huo unafaa, kwa sababu hata fahali wa kufugwa ni kiumbe mkubwa na mwenye nguvu. Katika nyakati za Biblia, ilikuwa vigumu sana kwa wakazi wa Palestina kukutana na mnyama yeyote mwenye nguvu kuliko fahali. Lakini walimjua fahali mwingine mwenye kutisha zaidi—fahali-mwitu, au auroch, ambaye ametoweka kabisa sasa. (Ayubu 39:9-12) Maliki Mroma Yulio Kaisari alisema wakati mmoja kwamba fahali hao walikuwa na ukubwa unaokaribia wa ndovu. “Wana nguvu nyingi sana, na wanakimbia kasi sana,” akaandika. Hebu wazia jinsi ungehisi dhaifu na mdogo mno kama ungesimama karibu na kiumbe huyo!
6. Kwa nini ni Yehova peke yake anayeitwa “Mweza-Yote”?
6 Vivyo hivyo, mwanadamu ni duni na dhaifu sana anapolinganishwa na Mungu mwenye nguvu, Yehova. Yehova huona mataifa yenye nguvu kama mavumbi membamba katika mizani. (Isaya 40:15) Yehova ana nguvu zisizo na mipaka, yeye si kama viumbe, kwa kuwa yeye peke yake ndiye anayeitwa “Mweza-Yote.”a (Ufunuo 15:3) Yehova ni “hodari kwa nguvu zake.” (Isaya 40:26) Yeye ni chanzo cha kudumu cha nguvu maridhawa. Hategemei nishati kutoka kwa chanzo kingine chochote, kwa kuwa “nguvu ni mali ya Mungu.” (Zaburi 62:11, NW) Lakini Yehova hutumiaje nguvu zake?
Jinsi Yehova Anavyotumia Nguvu Zake
7. Roho takatifu ya Yehova ni nini, na maneno ya lugha ya awali yanayotumiwa katika Biblia yanadokeza nini?
7 Roho takatifu humiminika kutoka kwa Yehova kwa wingi sana, ni nguvu yake inayotenda kazi. Kwa kweli, kwenye Mwanzo 1:2, (NW) Biblia hurejezea roho hiyo kuwa “nguvu ya Mungu ya utendaji.” Maneno ya awali ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “roho” huenda nyakati nyingine, yakatafsiriwa “upepo,” “pumzi,” na “mkumbo wa hewa.” Watungaji wa kamusi wanasema kwamba maneno ya lugha ya awali yanadokeza nguvu isiyoonekana inayotenda kazi. Hatuwezi kuona roho ya Mungu kama tusivyoweza kuona upepo, lakini tunaweza kuona na kutambua matokeo yake.
8. Biblia hufananisha roho ya Mungu na nini, na kwa nini ufananisho huo mbalimbali unafaa?
8 Roho takatifu ya Mungu inaweza kutimiza mambo mengi sana. Yehova anaweza kuitumia kutimiza kusudi lolote alilo nalo. Ndiyo sababu Biblia hufananisha roho ya Mungu na viungo kama vile “kidole,” ‘mkono wenye nguvu,’ au ‘mkono ulionyoshwa.’ (Luka 11:20; Kumbukumbu la Torati 5:15; Zaburi 8:3) Kama vile tu mwanadamu anavyoweza kutumia mikono yake kufanya kazi mbalimbali zinazohitaji nguvu au uwezo mbalimbali, ndivyo Mungu anavyoweza kutumia roho yake kutimiza kusudi lolote lile—kama vile kuumba atomu ndogo sana au kugawanya Bahari Nyekundu au kuwawezesha Wakristo wa karne ya kwanza kuongea kwa lugha za kigeni.
9. Nguvu za Yehova za kutawala ni nyingi kadiri gani?
9 Yehova pia hudhihirisha nguvu zake kupitia mamlaka yake akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Je, waweza kuwazia ukiwa na mamilioni ya mamilioni ya viumbe wenye akili na uwezo, walio tayari kutekeleza amri yako? Yehova ana nguvu hizo za utawala. Ana wanadamu wanaomtumikia, ambao mara nyingi Maandiko huwafananisha na jeshi. (Zaburi 68:11; 110:3) Hata hivyo, mwanadamu ni kiumbe dhaifu sana anapolinganishwa na malaika. Kwani, wakati jeshi la Ashuri liliposhambulia watu wa Mungu, malaika mmoja tu aliua wanajeshi 185,000 wa Ashuri katika usiku mmoja! (2 Wafalme 19:35) Malaika wa Mungu wana “uwezo kwa nguvu.”—Zaburi 103:19, 20, ZSB.
10. (a) Kwa nini Mweza-Yote anaitwa Yehova wa majeshi? (b) Ni kiumbe yupi aliye na uwezo zaidi ya viumbe wote wa Yehova?
10 Kuna malaika wangapi? Nabii Danieli alipata ono la mbinguni ambapo aliona viumbe wa roho zaidi ya milioni 100 wakiwa mbele ya kiti cha enzi cha Yehova, lakini hakuna uthibitisho wa kwamba aliona malaika wote ambao Yehova alikuwa ameumba. (Danieli 7:10) Kwa hivyo, huenda kukawa na mamia ya mamilioni ya malaika. Ndiyo sababu Mungu anaitwa Yehova wa majeshi. Cheo hicho kinaonyesha wadhifa wake mkubwa akiwa Amiri wa kikosi kikubwa kilichopangwa cha malaika wenye nguvu. Amemweka Mwanaye mpendwa, “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote,” kusimamia viumbe hao wote wa roho. (Wakolosai 1:15) Akiwa malaika-mkuu—mkuu wa malaika, maserafi, na makerubi wote—Yesu ndiye kiumbe mwenye uwezo zaidi ya viumbe wote wa Yehova.
11, 12. (a) Neno la Mungu hukaziaje nguvu? (b) Yesu alisema nini kuhusu nguvu za Yehova?
11 Yehova hudhihirisha nguvu zake kwa njia nyingine pia. Andiko la Waebrania 4:12 lasema: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.” Je, umeona nguvu za ajabu za neno la Mungu, au za ujumbe uliopuliziwa na roho, ambao sasa umehifadhiwa katika Biblia? Unaweza kutuimarisha, kujenga imani yetu, na kutusaidia kufanya mabadiliko makubwa maishani mwetu. Mtume Paulo aliwaonya waamini wenzake wajiepushe na watu walioishi maisha mapotovu. Halafu akasema: “Hata hivyo baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa.” (1 Wakorintho 6:9-11) Naam, “neno la Mungu” lilikuwa na nguvu maishani mwao na liliwasaidia kubadilika.
12 Yehova ana nguvu nyingi sana naye huzitumia kwa matokeo hivi kwamba hakuna kitu kinachoweza kumzuia. Yesu alisema hivi: “Kwa Mungu mambo yote yawezekana.” (Mathayo 19:26) Yehova hutumia nguvu zake kutimiza makusudi yapi?
Anatumia Nguvu Zake Kupatana na Makusudi Yake
13, 14. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova si chanzo cha nguvu kisicho na utu? (b) Yehova anatumia nguvu zake kwa njia zipi?
13 Roho ya Yehova ni bora kuliko kani yoyote ile; na Yehova si kani tu isiyo na utu, chanzo tu cha nguvu. Yeye ni Mungu mwenye utu ambaye anadhibiti nguvu zake kikamili. Lakini ni nini kinachomchochea azitumie?
14 Kama tutakavyoona, Mungu hutumia nguvu zake kuumba, kuharibu, kulinda, au kuhuisha—kwa ufupi, yeye huzitumia kufanya jambo lolote linalofaa makusudi yake makamilifu. (Isaya 46:10) Pindi fulani-fulani, Yehova hutumia nguvu zake kufunua sifa na sheria zake muhimu. Na zaidi ya yote, anatumia nguvu zake kutimiza mapenzi yake—kutetea enzi yake kuu na kutakasa jina lake takatifu kupitia Ufalme wa Kimesiya. Hakuna kitu chochote kinachoweza kuzuia kusudi hilo.
15. Yehova hutumia nguvu zake kwa kusudi gani kuhusiana na watumishi wake, na hali iliyompata Eliya inathibitishaje jambo hilo?
15 Yehova hutumia pia nguvu zake kutusaidia tukiwa mtu mmoja-mmoja. Hebu angalia andiko la 2 Mambo ya Nyakati 16:9 linavyosema: “Kwa maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” Kisa cha Eliya kilichotajwa mwanzoni ni mfano unaofaa. Kwa nini Yehova alimwonyesha tukio hilo la kustaajabisha la nguvu Zake? Malkia mwovu Yezebeli alikuwa ameapa kumwua Eliya. Nabii huyo alitoroka ili asiuawe. Alihisi upweke, aliogopa, na alikuwa amevunjika moyo—kana kwamba kazi yake yote ilikuwa ya bure. Yehova alimfariji Eliya aliyekuwa taabani kwa kumkumbusha waziwazi kuhusu nguvu Zake. Upepo, tetemeko la nchi, na moto vilionyesha kwamba Mungu mwenye nguvu zaidi katika ulimwengu wote alikuwa pamoja na Eliya. Kwa nini amhofu Yezebeli huku Yehova akiwa upande wake?—1 Wafalme 19:1-12.b
16. Kwa nini tunaweza kupata faraja kwa kutafakari juu ya nguvu nyingi za Yehova?
16 Ijapokuwa huu si wakati wa Yehova wa kufanya miujiza, yeye hajabadilika tangu siku za Eliya. (1 Wakorintho 13:8) Yeye angali na hamu ileile ya kutumia nguvu zake kwa niaba ya wale wanaompenda. Ni kweli kwamba anaishi katika makao matukufu ya roho, lakini hayuko mbali nasi. Nguvu zake hazina mipaka, kwa hiyo umbali si kizuizi. Badala yake, “BWANA yu karibu na wote wamwitao.” (Zaburi 145:18) Pindi moja wakati nabii Danieli alipomwomba Yehova msaada, malaika alifika alipokuwa angali anasali! (Danieli 9:20-23) Hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yehova kuwasaidia na kuwaimarisha wale anaowapenda.—Zaburi 118:6.
Je, Nguvu za Mungu Hutuzuia Tusimkaribie?
17. Nguvu za Yehova hututiaje woga, lakini huo si woga wa aina gani?
17 Je, tunapaswa kumwogopa Mungu kwa sababu ya nguvu zake? Ni lazima tujibu ndiyo na la. Ndiyo, kwa sababu sifa hii hutupatia sababu nzuri ya kumwogopa Mungu, kuwa na kicho na staha ya hali ya juu ambayo tulizungumzia kwa ufupi katika sura iliyotangulia. Biblia inatuambia kwamba woga huo ni “mwanzo wa hekima.” (Zaburi 111:10) Hata hivyo, twajibu la kwa sababu nguvu za Mungu hazifanyi tuwe na woga usiofaa au tuhofu kumkaribia.
18. (a) Kwa nini watu wengi hukosa kuwatumaini wenye mamlaka? (b) Twajuaje kwamba Yehova hawezi kufisidiwa na mamlaka yake?
18 “Mamlaka hufisidi; na mamlaka kamili hufisidi kikamili.” Ndivyo alivyoandika mwanahistoria Mwingereza Bwana Acton mnamo mwaka wa 1887. Maneno yake yamerudiwa mara nyingi, na huenda ni kwa sababu watu wengi huyaona kuwa ya kweli kabisa. Mara nyingi, wanadamu wasiokamilika hutumia vibaya mamlaka waliyo nayo, jambo hilo limethibitishwa na historia tena na tena. (Mhubiri 4:1; 8:9) Ndiyo sababu watu wengi hukosa kuwatumaini na huwaepuka wenye mamlaka. Yehova ana mamlaka kamili. Je, mamlaka hayo yamemfisidi kwa njia yoyote? Bila shaka la! Kama tulivyoona, yeye ni mtakatifu, hawezi kamwe kufisidiwa. Yehova si kama wanaume na wanawake wasiokamilika wenye mamlaka katika ulimwengu huu wenye ufisadi. Hajawahi kutumia vibaya mamlaka yake na hatafanya hivyo kamwe.
19, 20. (a) Sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa kupatana na sifa gani nyingine, na kwa nini hilo linafariji? (b) Simulia mfano ambao unaonyesha jinsi Yehova anavyojidhibiti, na kwa nini hilo linakuvutia?
19 Kumbuka kwamba Yehova ana sifa nyingine mbali na nguvu. Baadaye tutajifunza kuhusu haki yake, hekima yake, na upendo wake. Lakini hatupaswi kudhani kwamba Yehova hudhihirisha sifa zake bila hisia wala ufikirio, kana kwamba anadhihirisha sifa moja tu kwa wakati mmoja. Kinyume chake, tutaona katika sura zijazo kwamba sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa kupatana na haki yake, hekima yake, na upendo wake. Fikiria sifa nyingine ya Mungu, sifa ambayo watawala wengi leo ulimwenguni hawana—kujidhibiti.
20 Wazia kama ungekutana na mtu mkubwa mno mwenye nguvu nyingi, anayetisha. Lakini baada ya muda, unagundua kwamba yeye ni mpole. Yuko tayari kila wakati kutumia nguvu zake kuwasaidia na kuwalinda watu, hasa wale walio dhaifu na wanyonge. Hatumii vibaya kamwe nguvu zake. Waona akichongewa bila sababu, lakini yeye ni thabiti na mtulivu, ana staha na hata ni mwenye fadhili. Washangaa iwapo ungebaki mpole na kujidhibiti endapo ungekuwa na nguvu kama mwanamume huyo! Kadiri unavyomjua mwanamume huyo, je, hungetaka kuwa karibu naye? Tuna sababu nzuri sana za kumkaribia Yehova aliye mweza-yote. Hebu angalia mstari ambao ni msingi wa kichwa kikuu cha sura hii: “Mwenyezi-Mungu hakasiriki upesi, lakini amejaa nguvu.” (Nahumu 1:3, BHN) Yehova hatumii nguvu zake haraka-haraka kuwaadhibu watu, hata watu waovu. Yeye ni mpole na mwenye fadhili. Amethibitika kuwa ‘asiyekasirika upesi’ ajapochukizwa mara nyingi.—Zaburi 78:37-41.
21. Kwa nini Yehova hawalazimishi watu kufanya mapenzi yake, na hilo latufundisha nini kumhusu?
21 Fikiria kujidhibiti kwa Yehova kwa njia nyingine. Kama ungekuwa na nguvu zisizo na mipaka, je, wafikiri kwamba nyakati nyingine, ungekuwa na mwelekeo wa kuwalazimisha watu wafanye mambo jinsi unavyotaka? Licha ya nguvu nyingi alizo nazo, Yehova hawalazimishi kamwe watu wamtumikie. Hata ingawa kumtumikia Mungu ndiyo njia pekee ya kupata uhai udumuo milele, Yehova hatulazimishi kumtumikia. Badala yake, kwa fadhili yeye humstahi kila mtu kwa kumpa uhuru wa kuchagua. Anaonya kuhusu matokeo ya kufanya uchaguzi usiofaa na kutuambia faida za kufanya uchaguzi mzuri. Lakini anaturuhusu kufanya uchaguzi wetu binafsi. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Yehova hataki kamwe watu wamtumikie kwa kulazimishwa au kwa sababu wanahofu isivyofaa nguvu zake za kutisha. Anatafuta watu watakaomtumikia kwa hiari, kwa sababu wanampenda.—2 Wakorintho 9:7.
22, 23. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hufurahia kuwapa wengine mamlaka? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?
22 Na tuchunguze sababu ya mwisho inayotufanya tusiwe na woga usiofaa kumwelekea Mungu Mweza-Yote. Wanadamu wenye uwezo huogopa kuwapa wengine mamlaka. Lakini Yehova hufurahia kuwapa waabudu wake waaminifu mamlaka. Yeye huwapa wengine mamlaka kubwa, kama vile Mwanaye. (Mathayo 28:18) Yehova pia huwapa watumishi wake uwezo kwa njia nyingine. Biblia yaeleza: “Ee BWANA, ukuu ni wako, na uweza, na utukufu, na kushinda, na enzi; maana vitu vyote vilivyo mbinguni na duniani ni vyako. . . . Mkononi mwako mna uweza na nguvu; tena mkononi mwako mna kuwatukuza na kuwawezesha wote.”—1 Mambo ya Nyakati 29:11, 12.
23 Ndiyo, Yehova atafurahi kukuimarisha. Yeye hata huwapa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” wale wanaotaka kumtumikia. (2 Wakorintho 4:7) Je, huvutiwi kumkaribia Mungu huyo mwenye nguvu sana, ambaye anatumia nguvu zake kwa fadhili na kupatana na kanuni za juu za maadili? Katika sura inayofuata, tutazungumzia jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake za kuumba.
a Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “Mweza-Yote” humaanisha kihalisi “Mtawala Juu ya Wote; Yule Aliye na Nguvu Zote.”
b Biblia inasema kwamba “BWANA hakuwamo katika upepo ule . . . , tetemeko la nchi . . . , moto ule.” Tofauti na wale wanaoabudu miungu ya kihekaya ya nguvu za asili, watumishi wa Yehova hawamtafuti katika nguvu za maumbile. Yeye ni mkuu sana hivi kwamba hawezi kuishi katika kitu chochote alichoumba.—1 Wafalme 8:27.
-
-
Nguvu za Kuumba—“Aliyezifanya Mbingu na Nchi”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 5
Nguvu za Kuumba—“Aliyezifanya Mbingu na Nchi”
1, 2. Jua linaonyeshaje nguvu za Yehova za kuumba?
JE, UMEWAHI kusimama karibu na moto usiku wenye baridi? Labda ulinyoosha mikono yako umbali ufaao kutoka kwenye miali ya moto ili ufurahie joto lake. Uliposonga karibu zaidi, ulishindwa kustahimili joto hilo kali. Uliporudi nyuma zaidi, hewa baridi ya usiku ilikulemea, nawe ukaanza kutetemeka.
2 Kuna “moto” unaopasha joto miili yetu wakati wa mchana. “Moto” huo uko umbali wa kilometa milioni 150!a Ni wazi kwamba jua lina nguvu nyingi kiasi cha kwamba unaweza kuhisi joto lake kutoka umbali huo! Lakini, dunia inazunguka tanuru hiyo kubwa yenye joto kali la nyuklia kwa umbali barabara. Ikiwa dunia ingekaribia jua, maji yote duniani yangekuwa mvuke; na ikiwa dunia ingesonga mbali zaidi, maji yote yangekuwa barafu. Joto au baridi kali ingeangamiza kila kiumbe duniani. Nuru ya jua ni muhimu sana kwa uhai duniani, ni safi na ina manufaa tele, na inapendeza.—Mhubiri 11:7.
Yehova ‘aliufanya mwanga na jua’
3. Jua huthibitisha ukweli upi muhimu?
3 Hata hivyo, watu wengi wanaona jua kuwa kitu cha kawaida tu, ingawa uhai wao unalitegemea. Hivyo basi, hawajifunzi somo lolote kutokana na jua. Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Ndiwe uliyeufanya mwanga na jua.” (Zaburi 74:16) Naam, jua humletea sifa Yehova, “Aliyezifanya mbingu na nchi.” (Zaburi 19:1; 146:6) Jua ni mojawapo ya sayari chungu nzima zilizo angani ambazo zinatufundisha kuhusu nguvu nyingi za Yehova za kuumba. Hebu tuchunguze baadhi ya sayari hizo kwa undani zaidi halafu tuchunguze dunia na viumbe mbalimbali waliomo.
“Inueni Macho Yenu Juu, Mkaone”
4, 5. Jua lina nguvu nyingi kadiri gani, na ni kubwa kadiri gani, lakini likoje linapolinganishwa na nyota nyinginezo?
4 Huenda unajua kwamba jua letu ni nyota. Jua huonekana kubwa kuliko nyota tunazoona usiku kwa sababu liko karibu sana kuliko nyota hizo. Lina nguvu nyingi kadiri gani? Kipimo cha joto kwenye kiini cha jua ni nyuzi Selsiasi 15,000,000 hivi. Kama ungeweza kuchukua kipande cha kiini cha jua kinachotoshana na kichwa cha pini ndogo na kukiweka duniani, ungeteketea hata ukiwa umbali wa kilometa 140 kutoka kwenye chanzo hicho kidogo sana cha joto! Kila sekunde, jua hutoa nishati inayolingana na mlipuko wa mamia ya mamilioni ya mabomu ya nyuklia.
5 Jua ni kubwa sana hivi kwamba zaidi ya dunia 1,300,000 zinaweza kutoshea ndani yake. Je, jua ni nyota kubwa kupindukia? La, wataalamu wa nyota husema kwamba jua ni nyota ndogo sana yenye mwangaza hafifu. Mtume Paulo aliandika kwamba “nyota hutofautiana na nyota kwa utukufu.” (1 Wakorintho 15:41) Paulo hakuweza kuelewa kabisa maneno hayo ya Mungu. Kuna nyota moja kubwa hivi kwamba ikiwa ingewekwa mahali lilipo jua, basi ingefika ilipo dunia yetu. Endapo nyota nyingine ambayo ni kubwa sana ingewekwa lilipo jua, ingefikia sayari ya Zohali—japo sayari hiyo iko mbali sana na dunia hivi kwamba roketi ya angani ilisafiri kwa muda wa miaka minne ili kufika huko. Mwendo wake ulizidi mara 40 mwendo wa risasi inayofyatuliwa na bunduki yenye nguvu!
6. Biblia inaonyeshaje kwamba idadi ya nyota ni kubwa sana wanadamu wasiweze kuhesabu?
6 Lakini idadi ya nyota inastaajabisha zaidi ya ukubwa wake. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba nyota haziwezi kuhesabiwa, kama vile “mchanga wa bahari” usivyoweza kuhesabiwa. (Yeremia 33:22) Maneno hayo yanadokeza kwamba kuna nyota nyingi sana ambazo hatuwezi kuona pasipo vifaa maalumu. Endapo mwandikaji wa Biblia, kama Yeremia, angetazama angani wakati wa usiku na kujaribu kuhesabu nyota zionekanazo, angefaulu kuhesabu nyota zipatazo 3,000 hivi. Wanadamu huweza kuona idadi hiyo tu ya nyota katika anga jangavu la usiku bila kutumia vifaa maalumu. Idadi hiyo yaweza kulinganishwa na idadi ya chembe za mchanga zinazoweza kujaza kiganja kimoja tu cha mkono. Hata hivyo, idadi halisi ya nyota haijulikani, ni nyingi kama mchanga wa bahari. Ni nani awezaye kuhesabu idadi kubwa hivyo?b
“Aziita zote kwa majina”
7. (a) Kundi letu la Kilimia lina nyota ngapi, na hiyo ni idadi kubwa kadiri gani? (b) Kushindwa kwa wataalamu wa nyota kuhesabu makundi ya nyota kwaonyesha nini, na hilo latufundisha nini kuhusu nguvu za Yehova za kuumba?
7 Andiko la Isaya 40:26 linajibu hivi: “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina.” Zaburi 147:4 yasema: “Huihesabu idadi ya nyota.” “Idadi ya nyota” ni ngapi? Hilo si swali rahisi. Wataalamu wa nyota wanakadiria kwamba kuna zaidi ya nyota bilioni 100 katika kundi letu la nyota la Kilimia peke yake. Lakini kuna makundi mengine mengi mbali na kundi letu, ambayo yana nyota nyingi zaidi. Kuna makundi mangapi? Baadhi ya wataalamu wa nyota wamekadiria kwamba kuna makundi bilioni 50. Wengine wamekadiria kwamba kuna makundi yapatayo bilioni 125. Kwa hiyo, mwanadamu hawezi hata kujua idadi ya makundi ya nyota, sembuse kujua idadi kamili ya mabilioni ya nyota zilizomo. Lakini, Yehova anajua idadi yake. Isitoshe, yeye huipa kila nyota jina lake!
8. (a) Kundi la Kilimia ni kubwa kadiri gani? (b) Yehova anapangaje mizunguko ya sayari na nyota mbinguni?
8 Tunakuwa na kicho zaidi kwa Mungu tunapotafakari juu ya ukubwa wa kundi moja la nyota. Kundi la Kilimia limekadiriwa kuwa na upana wa kipimo cha miaka 100,000 cha mwendo wa mwanga. Hebu wazia mwali wa mwanga unaosafiri kwa mwendo wa kasi sana wa kilometa 300,000 kwa sekunde. Ingechukua mwali huo miaka 100,000 kuvuka kundi letu la nyota!c Na makundi fulani ni makubwa zaidi ya Kilimia. Biblia inasema kwamba Yehova ‘amezitandika mbingu’ hizi pana kana kwamba ni pazia tu. (Zaburi 104:2) Pia anapanga mizunguko ya sayari na nyota alizoumba. Kila kitu kinazunguka kupatana na sheria za asili ambazo Mungu ametunga na kutekeleza, kuanzia chembe ndogo sana ya vumbi lililo angani hadi kundi kubwa zaidi la nyota. (Ayubu 38:31-33) Ndiyo sababu, wanasayansi wamelinganisha mizunguko barabara ya sayari na nyota na miendo hususa ya wachezaji-dansi wenye utaratibu wa hali ya juu! Basi fikiria Muumba wa vitu hivyo vyote. Je, hustaajabishwi na Mungu huyo mwenye nguvu nyingi hivyo za kuumba?
“Ameiumba Dunia kwa Uweza Wake”
9, 10. Nguvu za Yehova zinadhihirishwaje na mahali ambapo mfumo wetu wa jua, Jupita, dunia, na mwezi ulipo?
9 Nguvu za Yehova za kuumba zinadhihirishwa katika makao yetu, dunia. Ameiweka dunia mahali pafaapo katika ulimwengu huu mkubwa. Wanasayansi fulani wanaamini kwamba mazingira ya makundi mengi ya nyota huenda yasifae sayari yenye uhai kama sayari yetu. Ni dhahiri kwamba sehemu kubwa ya kundi letu la nyota la Kilimia haikubuniwa ili iwe makao ya viumbe. Sehemu ya katikati ya kundi hilo imejaa nyota. Mnururisho ni mkali mno, na mara nyingi nyota huponea chupuchupu kugongana. Kingo za kundi hilo la nyota hazina vitu vingi ambavyo ni muhimu kwa uhai. Mfumo wetu wa jua uko mahali pafaapo kabisa.
10 Dunia hulindwa na sayari moja kubwa iliyo mbali sana—sayari ya Jupita. Sayari hiyo ya Jupita yenye ukubwa ambao ni mara 1,000 zaidi ya ukubwa wa Dunia, ina nguvu nyingi za uvutano. Matokeo ni nini? Inafyonza au kugeuza mwelekeo wa vitu vinavyosonga kasi angani. Wanasayansi wanasema kwamba kama Jupita haingekuwapo, vitu vikubwa vinavyosonga kasi angani vingegonga dunia na kuiathiri mara 10,000 zaidi ya ilivyo sasa. Dunia yetu hunufaishwa pia na sayari nyingine ya pekee iliyo karibu zaidi—mwezi. Licha ya kuwa sayari maridadi sana na “taa ya usiku,” mwezi hudumisha mwinamo uleule wa dunia. Mwinamo huo huwezesha dunia kuwa na majira thabiti na yasiyobadilika—jambo jingine muhimu kwa uhai duniani.
11. Angahewa ya dunia imebuniwaje ili kulinda dunia?
11 Nguvu za Yehova za kuumba zinadhihirishwa na kila kitu duniani. Fikiria angahewa ambayo inalinda dunia. Jua hutoa miale inayonufaisha mwili na miale hatari. Miale hatari inapofika kwenye angahewa ya juu ya dunia, inabadili oksijeni katika hewa kuwa hewa ya ozoni. Tabaka la hewa ya ozoni linalofanyizwa, linafyonza sehemu kubwa ya miale hiyo. Kwa kweli, sayari yetu imebuniwa ikiwa na kifuniko kinachoilinda!
12. Mzunguko wa maji wa angahewa unathibitishaje nguvu za Yehova za kuumba?
12 Angahewa yetu, ambayo ni mchanganyiko tata wa gesi zifaazo zinazotegemeza viumbe wanaoishi karibu au juu ya uso wa dunia inahusisha mambo mengine mengi. Mzunguko wa maji ni mojawapo ya maajabu ya angahewa. Kila mwaka jua huvukiza zaidi ya kilometa 400,000 za kipimo cha ujazo wa maji kutoka kwa bahari zote duniani. Maji hayo hufanyiza mawingu, ambayo husambazwa kotekote na pepo za angahewa. Maji hayo ambayo yamechujwa na kusafishwa, hunyesha yakiwa mvua, theluji, na barafu, na hivyo kuongeza hifadhi za maji duniani. Ni kama vile Mhubiri 1:7 inavyosema: “Mito yote huingia baharini, walakini bahari haijai; huko iendako mito, ndiko irudiko tena.” Yehova tu ndiye aliye na uwezo wa kuanzisha mzunguko huo.
13. Mimea na udongo wa dunia vinadhihirishaje nguvu za Muumba?
13 Kila kitu kilicho hai kinatudhihirishia nguvu za Muumba. Miti mikubwa mno aina ya sequoia ambayo ni mirefu kushinda jengo lenye orofa 30, na mimea mingi midogo mno ya baharini inayotokeza kiasi kikubwa cha hewa tunayopumua, inadhihirisha nguvu za Yehova za kuumba. Hata udongo una mimea na wanyama wengi walio hai—minyoo, kuvu, na vijiumbe vidogo sana, ambavyo hushirikiana kwa njia za pekee sana ili kuchangia ukuzi wa mimea. Ndiyo sababu Biblia inasema kwamba udongo una nguvu.—Mwanzo 4:12, ZSB.
14. Atomu ndogo sana ina nguvu zipi zilizofichika?
14 Hapana shaka kwamba Yehova ndiye ‘Aliyeiumba dunia kwa uweza wake.’ (Yeremia 10:12) Nguvu za Yehova zinadhihirishwa pia na vitu vidogo sana alivyoumba. Kwa mfano, atomu milioni moja zikipangwa karibu-karibu haziwezi kufikia unene wa unywele wa mwanadamu. Na hata kama atomu ingerefushwa kufikia kimo cha jengo lenye orofa 14, kiini chake kingelingana na chembe moja tu ya chumvi iliyo kwenye orofa ya 7 ya jengo hilo. Lakini kiini hicho kidogo sana ndicho chanzo cha nguvu za kutisha za mlipuko wa kombora la nyuklia!
“Kila Mwenye Pumzi”
15. Yehova alimfunza Ayubu somo gani alipozungumzia wanyama mbalimbali wa mwitu?
15 Wanyama chungu nzima walio duniani wanathibitisha pia waziwazi nguvu za Yehova za kuumba. Zaburi 148 inaorodhesha baadhi ya viumbe wanaomsifu Yehova, na mstari wa 10 unataja “hayawani, na wanyama wafugwao.” Ili kuonyesha kwa nini mwanadamu anapaswa kuwa na kicho kumwelekea Muumba, pindi moja Yehova alizungumza na Ayubu kuhusu wanyama kama vile simba, punda-milia, nyati, kiboko, na mamba. Yehova alitaka kufunza somo gani? Ikiwa mwanadamu hupigwa na butwaa kwa sababu ya viumbe hao wakubwa, wenye kutisha, na wasioweza kufugwa, je, hapaswi kumhofu hata zaidi Muumba wa viumbe hao?—Ayubu, sura ya 38-41.
16. Ni nini kinachokuvutia kuhusu baadhi ya ndege ambao Yehova ameumba?
16 Andiko la Zaburi 148:10 linataja pia “ndege wenye mbawa.” Hebu fikiria jamii nyingi zilizopo! Yehova alimwambia Ayubu kuhusu mbuni ambaye “humdharau farasi na mwenye kumpanda.” Ijapokuwa ndege huyu mwenye kimo cha meta 2.5 hawezi kuruka, anaweza kukimbia kwa mwendo wa kilometa 65 kwa saa, na anafikia umbali wa meta 4.5 anapopiga hatua moja tu! (Ayubu 39:13, 18) Kwa upande mwingine, ndege aitwaye alibatrosi huruka juu ya bahari muda mwingi wa maisha yake. Kwa kawaida ndege huyo hunyiririka tu hewani, na kipimo cha mabawa yake ni meta 3 kutoka ncha hadi ncha. Anaweza kupaa angani kwa saa nyingi sana bila kupigapiga mabawa yake. Kwa upande mwingine, ndege aina ya bee hummingbird mwenye urefu wa sentimeta 5 tu ndiye ndege mdogo zaidi ulimwenguni. Anaweza kupigapiga mabawa yake mara 80 kwa sekunde! Ndege hao wanaomeremeta kama vito vidogo vyenye mabawa, wanaweza kuelea hewani kama helikopta na hata kupaa kinyumenyume.
17. Nyangumi wa rangi ya buluu-kijivu ni mkubwa kadiri gani, na tunapaswa kufikia mkataa gani baada ya kuchunguza wanyama walioumbwa na Yehova?
17 Andiko la Zaburi 148:7 linasema kwamba hata “nyangumi” wanamsifu Yehova. Mfikirie kiumbe anayedhaniwa na wengi kuwa kiumbe mkubwa zaidi aliyewahi kuishi duniani, nyangumi mwenye rangi ya buluu-kijivu. Mnyama huyo mkubwa sana anayeishi baharini anaweza kuwa na urefu wa meta 30 au zaidi. Anaweza kuwa na uzito wa ndovu 30 wakomavu. Ulimi wake peke yake una uzito wa ndovu mmoja. Moyo wake unalingana na gari ndogo. Moyo huo mkubwa hupigapiga mara 9 tu kwa dakika—tofauti na moyo wa ndege aina ya hummingbird, ambao unaweza kupigapiga mara 1,200 hivi kwa dakika. Angalau mshipa mmoja wa nyangumi huyo ni mkubwa sana hivi kwamba mtoto mdogo anaweza kutambaa ndani yake. Bila shaka mioyo yetu hutuchochea kutangaza himizo la mstari wa mwisho wa kitabu cha Zaburi: “Kila mwenye pumzi na amsifu BWANA.”—Zaburi 150:6.
Kujifunza Kutokana na Nguvu za Yehova za Kuumba
18, 19. Vitu ambavyo Yehova ameumba duniani ni vingi kadiri gani, na uumbaji hutufundisha nini kuhusu enzi yake kuu?
18 Twajifunza nini kutokana na jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake za kuumba? Tunatiwa kicho tunapotambua kwamba vitu vilivyoumbwa ni vingi sana. Mtunga-zaburi mmoja alisema hivi kwa mshangao: “Ee BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! . . . Dunia imejaa mali zako.” (Zaburi 104:24) Ni kweli kama nini! Wanabiolojia wamegundua jamii zaidi ya milioni moja za vitu hai duniani; lakini hawajui kama kuna jamii milioni 10, milioni 30, au zaidi. Wakati mwingine msanii anaweza kushindwa kubuni jambo jipya. Lakini ubuni wa Yehova—uwezo wake wa kubuni na kuumba vitu mbalimbali vipya—bila shaka hauna kikomo.
19 Tunajifunza kuhusu enzi kuu ya Yehova kutokana na jinsi anavyotumia nguvu zake za kuumba. Neno “Muumba” linamtofautisha Yehova na vitu vyote ulimwenguni, kwani vitu vyote “viliumbwa.” Hata Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova, ambaye alikuwa “stadi wa kazi” wakati wa uumbaji, haitwi kamwe Muumba au Muumba-msaidizi katika Biblia. (Mithali 8:30; Mathayo 19:4) Badala yake, yeye ni “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Cheo cha Yehova akiwa Muumba humpa haki kamili ya kuwa mwenye enzi kuu pekee wa ulimwengu wote.—Waroma 1:20; Ufunuo 4:11.
20. Yehova amepumzikaje tangu alipomaliza kuumba vitu duniani?
20 Je, Yehova ameacha kutumia nguvu zake za kuumba? Ni kweli kwamba Biblia inasema kuwa Yehova alipomaliza kazi yake ya kuumba siku ya sita ya uumbaji, ‘siku ya saba Mungu alipumzika baada ya kazi yake yote aliyoifanya.’ (Mwanzo 2:2, BHN) Mtume Paulo alionyesha kwamba hiyo “siku” ya saba ina urefu wa maelfu ya miaka, kwa kuwa ilikuwa ikiendelea katika siku zake. (Waebrania 4:3-6) Lakini je, neno ‘alipumzika’ lamaanisha kwamba Yehova ameacha kufanya kazi kabisa? La, Yehova hufanya kazi daima. (Zaburi 92:4; Yohana 5:17) Basi, bila shaka pumziko lake linarejezea tu kuacha kwake kufanya kazi ya kuumba vitu duniani. Hata hivyo, kazi yake ya kutimiza makusudi yake imeendelea bila kukatishwa. Kazi hiyo imetia ndani kupulizia Maandiko Matakatifu. Kazi yake imetia ndani pia kutokeza “kiumbe kipya.” Habari hiyo itazungumziwa katika Sura ya 19.—2 Wakorintho 5:17.
21. Nguvu za Yehova za kuumba zitakuwa na matokeo gani kwa wanadamu waaminifu kwa umilele wote?
21 Siku ya Yehova ya pumziko itakapofikia mwisho hatimaye, ndipo atakapoweza kutangaza kazi yake yote duniani kuwa ‘njema sana,’ kama alivyofanya mwishoni mwa siku sita za uumbaji. (Mwanzo 1:31) Bado tunangoja kuona jinsi atakavyoamua kutumia nguvu zake za kuumba zisizo na mipaka baadaye. Kwa vyovyote vile, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutaendelea kustaajabishwa na jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake za kuumba. Kwa umilele wote, tutajifunza mengi zaidi kumhusu Yehova kupitia uumbaji wake. (Mhubiri 3:11) Kadiri tunavyojifunza mengi kumhusu, ndivyo tutakavyokuwa na kicho zaidi—na ndivyo tutakavyomkaribia zaidi Muumba wetu Mtukufu.
a Ili kufahamu vyema umbali huo mkubwa, fikiria hili: Ukisafiri umbali huo kwa gari—linaloenda kwa mwendo wa kilometa 160 kwa saa, saa 24 kwa siku—ungehitaji kusafiri kwa muda wa zaidi ya miaka 100!
b Watu fulani hufikiri kwamba watu walioishi katika nyakati za Biblia walitumia darubini fulani ya kienyeji. Wanatoa sababu kwamba watu walioishi nyakati hizo hawangeweza kujua kwamba idadi ya nyota ni kubwa sana wanadamu wasiweze kuhesabu. Makisio hayo yasiyo na msingi hayamheshimu wala kumtambua Yehova, Mtungaji wa Biblia.—2 Timotheo 3:16.
c Fikiria muda ambao ungehitaji kutumia kuhesabu nyota bilioni 100 tu. Kama ungeweza kuhesabu nyota moja kila sekunde—kwa muda wa saa 24 kwa siku—ingekuchukua miaka 3,171!
-
-
Nguvu za Kuangamiza—Yehova, “Ni Mtu wa Vita”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 6
Nguvu za Kuangamiza—Yehova, “Ni Mtu wa Vita”
1-3. (a) Waisraeli walikabili tisho gani kutoka kwa Wamisri? (b) Yehova aliwapigania watu wake jinsi gani?
WAISRAELI walinaswa kati ya majabali makubwa yaliyochongoka ya mlima na bahari isiyopitika. Jeshi la Misri, ambalo liliua watu kikatili, lilikuwa likiwafukuza Waisraeli hima-hima. Lilikuwa limeazimia kuwaangamiza kabisa.a Hata hivyo, Musa aliwasihi watu wa Mungu wasikate tamaa. “BWANA atawapigania ninyi,” akawahakikishia.—Kutoka 14:14.
2 Hata hivyo, Musa alimlilia Yehova, Naye akamjibu hivi: “Mbona unanililia mimi? . . . Inua fimbo yako, ukanyoshe mkono wako juu ya bahari, na kuigawanya.” (Kutoka 14:15, 16) Hebu wazia mambo yanayotukia. Yehova anamwamuru malaika wake mara moja, na ile nguzo ya wingu inarudi nyuma ya Waisraeli, yaelekea inakuwa kama ukuta na kuwazuia Wamisri kushambulia. (Kutoka 14:19, 20; Zaburi 105:39) Musa aunyosha mkono wake. Bahari yapigwa na upepo wenye nguvu na maji yagawanyika. Kwa njia fulani maji yagandamana na kusimama wima kama kuta, na kutokeza njia pana inayotoshea taifa zima!—Kutoka 14:21; 15:8.
3 Farao anapaswa kuwaamuru wanajeshi wake warudi nyumbani baada ya kuona wonyesho huo wa kustaajabisha wa nguvu. Badala yake, Farao mwenye kiburi anawaamuru washambulie. (Kutoka 14:23) Wamisri watimua mbio na kuwafuata Waisraeli hima-hima katika bonde la bahari, lakini punde si punde mashambulizi yao yanaambulia patupu wakati magurudumu ya magari yao yanapoanza kutoka. Mara tu Waisraeli wafikapo ng’ambo ya bahari wakiwa salama, Yehova anamwamuru hivi Musa: “Nyosha mkono wako juu ya bahari, ili maji yarudi tena juu ya Wamisri, juu ya magari yao, na juu ya farasi zao.” Kuta za maji zaporomoka, na kumfunika Farao na majeshi yake!—Kutoka 14:24-28; Zaburi 136:15.
Kwenye Bahari Nyekundu Yehova alijithibitisha kuwa “mtu wa vita”
4. (a) Yehova alijithibitisha kuwa nani kwenye Bahari Nyekundu? (b) Huenda tendo hilo la Yehova likaathirije watu fulani?
4 Ukombozi wa taifa la Israeli katika Bahari Nyekundu ulikuwa tukio muhimu sana katika simulizi la matendo ya Mungu kuelekea wanadamu. Pindi hiyo, Yehova alijithibitisha kuwa “mtu wa vita.” (Kutoka 15:3) Lakini wewe unaonaje tendo hilo la Yehova? Kwa kweli, vita vimewaletea wanadamu majonzi na taabu nyingi sana. Je, yaweza kuwa kwamba unashindwa kumkaribia Mungu kwa sababu anatumia nguvu zake za kuangamiza?
Vita vya Mungu na Mapambano ya Wanadamu
5, 6. (a) Kwa nini Mungu anaitwa ifaavyo “BWANA wa majeshi”? (b) Vita vya Mungu vinatofautiana na vita vya wanadamu jinsi gani?
5 Mungu anaitwa kwa jina la cheo “BWANA wa majeshi” mara 300 hivi katika Maandiko ya Kiebrania, na mara 2 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. (1 Samweli 1:11) Akiwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu, Yehova anasimamia jeshi kubwa sana la malaika. (Yoshua 5:13-15; 1 Wafalme 22:19) Jeshi hilo lina uwezo mkubwa ajabu wa kuangamiza. (Isaya 37:36) Kuwaangamiza wanadamu si jambo lenye kufurahisha. Hata hivyo, ni sharti tukumbuke kwamba vita vya Mungu si kama mapambano ya wanadamu yasiyo na maana. Huenda viongozi wa kijeshi na wa kisiasa wakadai kwamba wanapigana kwa makusudi mazuri. Lakini vita vyote vya wanadamu huchochewa na pupa na ubinafsi.
6 Kinyume chake, Yehova hatendi bila kufikiri. Andiko la Kumbukumbu la Torati 32:4 latangaza hivi: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki na adili.” Neno la Mungu linashutumu hasira isiyodhibitiwa, ukatili, na jeuri. (Mwanzo 49:7; Zaburi 11:5) Kwa hiyo, Yehova hatendi kamwe bila sababu. Yeye hutumia nguvu zake za kuangamiza mara chache sana wakati jitihada nyingine zote zinaposhindwa. Ni kama alivyosema kupitia nabii wake Ezekieli: “Je, mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? asema Bwana MUNGU, si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake akaishi?”—Ezekieli 18:23.
7, 8. (a) Ayubu alifikiri nini kimakosa kuhusu mateso yake? (b) Elihu alisahihishaje maoni ya Ayubu kuhusu jambo hilo? (c) Tunajifunza somo gani kutokana na mambo yaliyompata Ayubu?
7 Basi kwa nini Yehova hutumia nguvu zake za kuangamiza? Kabla ya kujibu swali hilo, tumfikirie Ayubu yule mwanamume mwadilifu. Shetani alitilia shaka iwapo Ayubu, au mwanadamu yeyote angebaki mwaminifu chini ya jaribu. Yehova alijibu shtaka hilo kwa kumruhusu Shetani ajaribu uaminifu wa Ayubu. Tokeo ni kwamba Ayubu alitaabishwa na ugonjwa, akapoteza mali yake na watoto wake. (Ayubu 1:1–2:8) Bila kujua masuala yaliyohusika, Ayubu alifikiri kimakosa kwamba Mungu alikuwa akimwadhibu isivyo haki kupitia mateso hayo. Alimwuliza Mungu kwa nini Alimweka awe “shabaha” yake, na “adui” yake?—Ayubu 7:20; 13:24.
8 Mwanamume kijana aliyeitwa Elihu alionyesha kasoro ya maoni ya Ayubu, alipomwambia hivi: “Wasema, Haki yangu ni zaidi kuliko ya Mungu.” (Ayubu 35:2) Naam, si jambo la hekima kufikiri kwamba tunajua mengi kumliko Mungu au kudhani kwamba ametenda isivyo haki. “Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu, wala Mwenyezi kufanya uovu,” akasema Elihu. Baadaye, alisema hivi: “Yeye Mwenyezi hamwezi kumwona; Yeye ni mkuu mwenye uweza; tena mwenye hukumu, na mwingi wa haki, hataonea.” (Ayubu 34:10; 36:22, 23; 37:23) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anapopigana, anakuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Tukiwa na jambo hilo akilini, hebu tuchunguze baadhi ya sababu zinazomfanya Mungu wa amani aamue kuwa shujaa wa vita.—1 Wakorintho 14:33.
Mambo Yanayomfanya Mungu wa Amani Apigane
9. Kwa nini Mungu wa amani hupigana?
9 Baada ya kumsifu Mungu kuwa “mtu wa vita,” Musa aliuliza hivi: “Ee BWANA, katika miungu ni nani aliye kama wewe? Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu?” (Kutoka 15:11) Vivyo hivyo, nabii Habakuki aliandika hivi: “Wewe uliye na macho safi hata usiweze kuangalia uovu, wewe usiyeweza kutazama ukaidi.” (Habakuki 1:13) Ijapokuwa Yehova ni Mungu wa upendo, yeye pia ni Mungu wa utakatifu, uadilifu, na haki. Nyakati nyingine, yeye hutumia nguvu zake za kuangamiza kwa sababu ya sifa hizo. (Isaya 59:15-19; Luka 18:7) Kwa hiyo, Mungu hachafui utakatifu wake anapopigana. Badala yake, yeye hupigana kwa sababu yeye ni mtakatifu.—Kutoka 39:30.
10. (a) Mungu alihitaji kupigana vita kwa mara ya kwanza lini na jinsi gani? (b) Uadui uliotabiriwa kwenye Mwanzo 3:15 unaweza kukomeshwa tu kwa njia gani, na wanadamu waadilifu watapata baraka gani?
10 Hebu fikiria hali iliyotokea baada ya wenzi wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, kumwasi Mungu. (Mwanzo 3:1-6) Kama Yehova angalivumilia uasi wao, angalidunisha cheo chake mwenyewe akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Akiwa Mungu mwadilifu, alikuwa na wajibu wa kuwahukumia kifo. (Waroma 6:23) Katika unabii wa kwanza wa Biblia, alitabiri kwamba kungekuwa na uadui kati ya watumishi wake na wafuasi wa “nyoka,” yaani, Shetani. (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:15) Mwishowe, uadui huo ungekomeshwa tu kwa kumponda-ponda Shetani. (Waroma 16:20) Lakini tendo hilo la hukumu litawaletea wanadamu waadilifu baraka nyingi, litakomesha uvutano wa Shetani duniani halafu paradiso itaenea ulimwenguni pote. (Mathayo 19:28) Kabla ya wakati huo, wale waliomwunga mkono Shetani wangeendelea kuhatarisha hali ya kimwili na ya kiroho ya watu wa Mungu. Pindi kwa pindi, Yehova angelazimika kuchukua hatua.
Matendo ya Mungu ya Kuondoa Uovu
11. Kwa nini Mungu alikuwa na wajibu wa kuleta gharika duniani pote?
11 Gharika ya siku ya Noa ilikuwa mojawapo ya matendo hayo ya Mungu. Andiko la Mwanzo 6:11, 12 lasema hivi: “Dunia ikaharibika mbele za Mungu, dunia ikajaa dhuluma. Mungu akaiona dunia, na tazama, imeharibika; maana kila mwenye mwili amejiharibia njia yake duniani.” Je, Mungu angeruhusu waovu waharibu kabisa maadili yote duniani? La. Yehova alikuwa na wajibu wa kuleta gharika duniani pote ili kuwaangamiza wale walioazimia kuendeleza jeuri na ukosefu wa adili.
12. (a) Yehova alitabiri nini kuhusu “uzao” wa Abrahamu? (b) Waamori wangeangamizwa kwa sababu gani?
12 Ndivyo ilivyokuwa kuhusu hukumu ya Mungu dhidi ya Wakanaani. Yehova alifunua kwamba jamaa zote duniani zingejibariki kupitia “uzao” wa Abrahamu. Kwa kupatana na kusudi hilo, Mungu aliagiza kwamba uzao wa Abrahamu upewe nchi ya Kanaani, iliyokaliwa na Waamori. Je, Mungu alikuwa na sababu halali ya kuwafukuza watu hao kutoka nchi yao? Yehova alitabiri kwamba hangewafukuza kwa muda wa miaka 400—hadi ‘uovu wa Waamori utimie.’b (Mwanzo 12:1-3; 13:14, 15; 15:13, 16; 22:18) Katika kipindi hicho, Waamori walitumbukia katika ukosefu mbaya sana wa adili. Kanaani ikawa nchi iliyojaa ibada ya sanamu, umwagaji-damu, na mazoea machafu sana ya ngono. (Kutoka 23:24; 34:12, 13; Hesabu 33:52) Wenyeji wa nchi hiyo hata waliwaua watoto kwa kuwadhabihu katika moto. Je, Mungu mtakatifu angeweza kuwaacha watu wake waishi katika uovu huo? La hasha! Alisema hivi: “Hiyo nchi imekuwa najisi; kwa ajili ya hayo naipatiliza uovu wake juu yake, na hiyo nchi yatapika wenyeji wake na kuwatoa.” (Mambo ya Walawi 18:21-25) Hata hivyo, Yehova hakuwaua watu wote bila kujali. Wakanaani wenye mwelekeo unaofaa, kama vile Rahabu na Wagibeoni, hawakuuawa.—Yoshua 6:25; 9:3-27.
Anapigania Jina Lake
13, 14. (a) Kwa nini Yehova alikuwa na wajibu wa kutakasa jina lake? (b) Yehova aliondoleaje jina lake lawama?
13 Jina la Yehova ni takatifu kwa sababu yeye ni Mtakatifu. (Mambo ya Walawi 22:32) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Uasi katika Edeni ulichafua jina la Mungu na kutilia shaka sifa yake na utawala wake. Yehova hangeweza kamwe kuachilia tu uchongezi na uasi wa aina hiyo. Alikuwa na wajibu wa kutakasa jina lake.—Isaya 48:11.
14 Fikiria tena Waisraeli. Maadamu walikuwa watumwa nchini Misri, ahadi ya Mungu kwa Abrahamu kwamba kupitia uzao wake jamaa zote duniani zingejibarikia ilionekana kuwa ya bure. Lakini Yehova aliondolea jina lake lawama alipowakomboa na kuwafanya kuwa taifa. Kwa hiyo, nabii Danieli alisema hivi aliposali: ‘Ee Bwana Mungu wetu, uliwatoa watu wako hawa katika nchi ya Misri kwa mkono hodari, ukajipatia sifa.’—Danieli 9:15.
15. Kwa nini Yehova aliwaokoa Wayahudi kutoka utekwani Babiloni?
15 Inapendeza kwamba Danieli alisali hivyo Wayahudi walipohitaji Yehova achukue hatua mara nyingine ili kutetea jina Lake. Wayahudi hao wasiotii walikuwa utekwani huko Babiloni. Mji wao mkuu, Yerusalemu, ulikuwa magofu. Danieli alijua kwamba kurudishwa kwa Wayahudi nchini mwao kungelitukuza jina la Yehova. Hivyo Danieli alisali hivi: “Ee Bwana, usamehe; Ee Bwana, usikilize, ukatende, usikawie; kwa ajili yako wewe, Ee Mungu wangu; kwa sababu mji wako na watu wako wanaitwa kwa jina lako.”—Danieli 9:18, 19.
Anawapigania Watu Wake
16. Eleza kwa nini nia ya Yehova ya kutetea jina lake haimaanishi kwamba yeye hana hisia na ni mwenye ubinafsi.
16 Je, nia ya Yehova ya kutetea jina lake yamaanisha kwamba yeye hana hisia na ni mwenye ubinafsi? La, yeye huwalinda watu wake ili kutetea haki na utakatifu wake. Fikiria Mwanzo sura ya 14. Twasoma kuhusu wafalme wanne wavamizi waliomteka nyara mpwa wa kiume wa Abrahamu, Loti, na familia yake. Kwa msaada wa Yehova, Abrahamu alishinda kabisa majeshi makubwa sana! Yaelekea ushindi huo ulikuwa kisa cha kwanza kurekodiwa katika “kitabu cha vita vya Mwenyezi Mungu.” Na yaonekana kwamba mapambano kadhaa ya kijeshi ambayo hayakuandikwa katika Biblia yalirekodiwa pia katika kitabu hicho. (Hesabu 21:14, BHN) Ushindi mwingine mwingi ungefuata.
17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova aliwapigania Waisraeli baada ya wao kuingia katika nchi ya Kanaani? Toa mifano.
17 Muda mfupi kabla ya Waisraeli kuingia katika nchi ya Kanaani, Musa aliwahakikishia hivi: “BWANA, Mungu wenu, anayetangulia mbele yenu, ndiye atakayewapigania, kwa mfano wa yote aliyowafanyia huko Misri.” (Kumbukumbu la Torati 1:30; 20:1) Kwa kweli Yehova aliwapigania watu wake kuanzia wakati wa Yoshua yule mrithi wa Musa, hadi muhula wote wa Waamuzi na utawala wa Wafalme waaminifu wa Yuda. Mara nyingi, aliwasaidia kushinda kabisa maadui wao.—Yoshua 10:1-14; Waamuzi 4:12-17; 2 Samweli 5:17-21.
18. (a) Kwa nini tushukuru kwamba Yehova hajabadilika? (b) Ni nini kitakachotukia wakati uadui unaoelezwa kwenye Mwanzo 3:15 unapofikia kilele?
18 Yehova hajabadilika; wala kusudi lake la kuifanya dunia hii iwe paradiso yenye amani halijabadilika. (Mwanzo 1:27, 28) Bado Mungu anachukia uovu. Na vilevile, anawapenda mno watu wake, naye atawapigania hivi karibuni. (Zaburi 11:7) Kwa kweli, uadui unaoelezwa kwenye Mwanzo 3:15 unatarajiwa kufikia hatua muhimu sana ya ghafula na yenye msukosuko hivi karibuni. Kwa mara nyingine, Yehova atakuwa “mtu wa vita” ili kutakasa jina lake na kuwalinda watu wake!—Zekaria 14:3; Ufunuo 16:14, 16.
19. (a) Toa mfano unaoonyesha kwamba nguvu za Mungu za kuangamiza zinaweza kutuvuta karibu naye. (b) Tunapaswa kuhisije kuhusu utayari wa Mungu wa kupigana?
19 Fikiria mfano huu: Tuseme kwamba familia ya mwanamume mmoja ilikuwa ikishambuliwa na mnyama hatari kisha mwanamume huyo akaingilia pambano hilo na kumwua mnyama huyo mkali. Je, ungetarajia mke na watoto wake wakasirishwe na tendo lake? Kinyume chake, ungetarajia waguswe na upendo wake usio na ubinafsi. Vivyo hivyo, hatupaswi kukasirika Mungu anapotumia nguvu zake za kuangamiza. Tunapaswa kumpenda hata zaidi kwa sababu yu tayari kupigana ili kutulinda. Vilevile tunapaswa kumstahi hata zaidi kwa sababu ya nguvu zake zisizo na mipaka. Kwa hiyo, tunaweza “kumtolea Mungu . . . utumishi mtakatifu kwa hofu ya kimungu na kicho.”—Waebrania 12:28.
Mkaribie Yule “Mtu wa Vita”
20. Tunapaswa kufanya nini tunaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu vita vya Mungu ambavyo huenda tusielewe kikamili, na kwa nini tufanye hivyo?
20 Bila shaka, Biblia haielezi kila jambo linalohusika katika maamuzi ya Yehova kuhusu vita vyake. Lakini sikuzote tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hili: Yehova hatumii kamwe nguvu zake za kuangamiza kwa njia isiyo ya haki, bila sababu nzuri, au kwa ukatili. Mara nyingi, kuchunguza muktadha wa simulizi la Biblia au habari fulani za ziada kunaweza kutusaidia kuelewa visa hivyo. (Mithali 18:13) Hata tusipokuwa na habari zote, kujifunza mengi juu ya Yehova na kutafakari juu ya sifa zake tukufu kunaweza kutusaidia kuondoa shaka yoyote tunayoweza kuwa nayo. Kwa kufanya hivyo tunagundua kwamba tuna sababu nyingi sana za kumtumaini Mungu wetu Yehova.—Ayubu 34:12.
21. Ajapokuwa “mtu wa vita” nyakati nyingine, Yehova ana sifa zipi?
21 Ijapokuwa Yehova huwa “mtu wa vita” nyakati nyingine, hilo halimaanishi kwamba yeye ni mpenda-vita. Katika ono la Ezekieli kuhusu gari la kimbingu, Yehova anaonyeshwa akiwa tayari kupigana na maadui wake. Hata hivyo, Ezekieli alimwona Mungu akiwa amezungukwa na upinde wa mvua—ishara ya amani. (Mwanzo 9:13; Ezekieli 1:28; Ufunuo 4:3) Ni wazi kwamba Yehova ni mtulivu na mwenye kutafuta amani. “Mungu ni upendo,” akaandika mtume Yohana. (1 Yohana 4:8) Sifa zote za Yehova zimesawazika kikamili. Basi, tuna pendeleo lililoje la kuweza kumkaribia Mungu huyo mwenye nguvu na upendo!
a Mwanahistoria Myahudi Josephus anasema kwamba Waebrania, “walifukuzwa na magari 600 yanayokokotwa na farasi na wapanda-farasi 50,000 na askari 200,000 wa miguu.”—Jewish Antiquities, II, 324 [xv, 3].
b Kwa wazi, neno hili “Waamori” latia ndani wenyeji wote wa Kanaani.—Kumbukumbu la Torati 1:6-8, 19-21, 27; Yoshua 24:15, 18.
-
-
Nguvu za Kulinda—“Mungu Ni Kimbilio Letu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 7
Nguvu za Kulinda—“Mungu Ni Kimbilio Letu”
1, 2. Waisraeli walikabili hatari gani walipofika eneo la Sinai mwaka wa 1513 K.W.K., na Yehova aliwatiaje moyo?
WAISRAELI walikuwa hatarini walipofika eneo la Sinai mapema mwaka wa 1513 K.W.K. Wangefunga safari ndefu yenye kuogofya sana, wangesafiri katika “lile jangwa kubwa na la kutisha, lenye nyoka wenye sumu na ng’e.” (Kumbukumbu la Torati 8:15, BHN) Walikabili pia tisho la kushambuliwa na mataifa yenye uadui. Yehova aliwaleta watu wake katika hali hiyo. Je, angeweza kuwalinda akiwa Mungu wao?
2 Maneno ya Yehova yalikuwa yenye kutia moyo sana: “Mmeona jinsi nilivyowatendea Wamisri, na jinsi nilivyowachukua ninyi juu ya mbawa za tai, nikawaleta ninyi kwangu mimi.” (Kutoka 19:4) Yehova aliwakumbusha watu wake kwamba aliwakomboa kutoka kwa Wamisri, ni kama aliwachukua juu ya mbawa za tai na kuwapeleka mahali salama. Lakini kuna sababu nyingine zinazofanya “mbawa za tai” ziwe mfano ufaao wa ulinzi wa Mungu.
3. Kwa nini “mbawa za tai” ni mfano ufaao wa ulinzi wa Mungu?
3 Tai hutumia mbawa zake pana na zenye nguvu sana kwa sababu nyingine mbali na kupaa hewani. Kunapokuwa na joto kali wakati wa mchana, tai mama hukunja mbawa zake—ambazo zinaweza kuwa na upana wa zaidi ya meta mbili—ili kufunika na kulinda makinda yake dhaifu kutokana na joto kali sana la jua. Nyakati nyingine, yeye huyafunika makinda yake kwa mbawa zake na kuyalinda na upepo wenye baridi. Yehova alilinda na kukinga taifa changa la Israeli kama tai anavyolinda makinda yake. Sasa wakiwa jangwani, watu wake wangeendelea kukimbilia uvuli wa mbawa zake za mfano zenye nguvu maadamu walibaki waaminifu. (Kumbukumbu la Torati 32:9-11; Zaburi 36:7) Lakini je, leo tunaweza kutarajia kwa kufaa kupata ulinzi wa Mungu?
Ahadi ya Kupata Ulinzi wa Mungu
4, 5. Kwa nini tunaweza kutumaini kabisa ahadi ya Mungu ya kutulinda?
4 Bila shaka Yehova anaweza kuwalinda watumishi wake. Yeye ni “Mungu Mwenyezi”—cheo hicho kinamaanisha kwamba ana nguvu zisizoweza kushindwa. (Mwanzo 17:1) Kama wimbi lenye nguvu sana, nguvu za Yehova haziwezi kuzuiwa. Kwa kuwa anaweza kufanya jambo lolote kulingana na mapenzi yake, huenda tukauliza hivi, ‘Je, ni mapenzi ya Yehova kutumia nguvu zake ili kuwalinda watu wake?
5 Kwa neno moja, jibu ni ndiyo! Yehova anatuhakikishia kwamba atawalinda watu wake. “Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu, yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu,” yasema Zaburi 46:1, BHN. Kwa kuwa Mungu ‘hawezi kusema uwongo,’ tunaweza kutumaini kabisa ahadi yake ya kutulinda. (Tito 1:2) Hebu tuchunguze baadhi ya mifano dhahiri ambayo Yehova anatumia ili kuonyesha ulinzi wake.
6, 7. (a) Mchungaji katika nyakati za Biblia aliwalinda kondoo wake kutokana na nini? (b) Biblia inatoa mfano gani unaoonyesha jinsi Yehova anavyotaka kwa dhati kulinda na kutunza kondoo wake?
6 Yehova ni Mchungaji, nasi tu “watu wake, na kondoo wa malisho yake.” (Zaburi 23:1; 100:3) Wanyama wengi si hoi kama kondoo anayefugwa. Mchungaji katika nyakati za Biblia alihitaji kuwa jasiri ili kuwalinda kondoo wake kutoka kwa simba, mbwa-mwitu, na dubu, na vilevile wezi. (1 Samweli 17:34, 35; Yohana 10:12, 13) Lakini nyakati nyingine kuwalinda kondoo kulihitaji wororo. Kondoo alipozalia mbali na zizi, mchungaji mwenye kujali angemlinda mama huyo pindi hiyo alipohitaji sana ulinzi, kisha angembeba mwana-kondoo wake dhaifu na kumpeleka zizini.
’Atawachukua kifuani mwake’
7 Kwa kujilinganisha na mchungaji, Yehova anatuhakikishia kwamba anataka kwa dhati kutulinda. (Ezekieli 34:11-16) Hebu kumbuka jinsi Yehova anavyoelezwa kwenye Isaya 40:11, kama Sura ya 2 ya kitabu hiki ilivyoonyesha: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake.” Mwana-kondoo mchanga anafikaje “kifuani” mwa mchungaji—katika mapindo ya vazi lake la juu? Huenda mwana-kondoo huyo akamkaribia mchungaji, na hata kugusa mguu wake kwa upole. Hata hivyo, ni lazima mchungaji ainame, amchukue mwana-kondoo huyo, na kumweka taratibu kifuani penye usalama. Huo ni mfano wenye kugusa moyo kama nini unaoonyesha jinsi Mchungaji wetu Mkuu alivyo tayari kutukinga na kutulinda!
8. (a) Ni nani wanaoahidiwa kupata ulinzi wa Mungu, na hilo linaonyeshwaje na Mithali 18:10? (b) Kukimbilia jina la Mungu kunahusisha nini?
8 Ahadi ya Mungu ya kuandaa ulinzi ina masharti—wale tu wanaomkaribia ndiyo wanaopata ulinzi huo. Andiko la Mithali 18:10 lasema: “Jina la BWANA ni ngome imara. Mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Katika nyakati za Biblia, mara kwa mara ngome zilijengwa jangwani kama mahali salama pa kukimbilia. Lakini yule aliyekuwa hatarini ndiye aliyekuwa na daraka la kukimbilia kwenye ngome hizo ili kupata usalama. Ndivyo ilivyo na kukimbilia jina la Mungu. Hilo halimaanishi kurudia-rudia tu jina la Mungu; jina la Mungu si hirizi ya kimizungu. Badala yake, tunahitaji kumjua na kumtumaini Yule anayeitwa kwa jina hilo na kuishi kwa kupatana na viwango vyake vya uadilifu. Yehova ni mwenye fadhili kama nini kwa kutuhakikishia kwamba endapo tutamfikia kwa imani, atakuwa ngome ya kutulinda!
“Mungu Wetu . . . Aweza Kutuokoa”
9. Yehova amefanyaje mengi mbali na kuahidi ulinzi?
9 Yehova amefanya mengi mbali na kuahidi tu ulinzi. Katika nyakati za Biblia, alionyesha kupitia miujiza kwamba anaweza kuwalinda watu wake. Katika historia yote ya Waisraeli, mara nyingi “mkono” wa Yehova wenye uwezo uliwakomesha maadui wenye nguvu. (Kutoka 7:4) Lakini Yehova alitumia pia nguvu zake za kulinda kwa niaba ya watu fulani.
10, 11. Ni mifano gani ya Kibiblia inayoonyesha jinsi Yehova alivyotumia nguvu zake za kulinda kwa niaba ya watu fulani?
10 Vijana watatu Waebrania—Shadraka, Meshaki, na Abednego—walipokataa kuisujudia sanamu ya dhahabu ya Mfalme Nebukadneza, mfalme huyo mwenye hasira alitisha kuwatupa katika tanuru yenye moto mkali sana. “Ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu?” akadhihaki Nebukadneza, mtawala mwenye nguvu zaidi duniani. (Danieli 3:15) Vijana hao watatu walijua kwa hakika kwamba Mungu wao alikuwa na nguvu za kuwalinda, lakini hawakutarajia kwamba angewalinda. Kwa hiyo, walijibu hivi: “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa.” (Danieli 3:17) Kwa kweli, tanuru hiyo ijapotiwa moto mara saba kuliko ilivyo kawaida, haikuwa kitu kwa Mungu wao mwenye nguvu zote. Aliwalinda, na mfalme huyo alilazimika kukiri hivi: “Hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.”—Danieli 3:29.
11 Yehova alionyesha pia nguvu zake kuu za kulinda alipohamisha uhai wa Mwanaye mzaliwa-pekee hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi Maria. Malaika alimwambia Maria kwamba ‘angechukua mimba katika tumbo [lake] la uzazi na kuzaa mwana.’ Malaika huyo alieleza hivi: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana itakufunika kivuli.” (Luka 1:31, 35) Yaonekana kwamba Mwana wa Mungu angeweza kushambuliwa kwa urahisi sana pindi hiyo. Je, dhambi na kutokamilika kwa mama yake wa kibinadamu kungechafua kiini-tete hicho? Je, Shetani angeweza kumjeruhi au kumwua Mwana huyo kabla hajazaliwa? Haiwezekani! Kwa kweli Yehova alimlinda Maria tangu mimba ilipotungwa na kuendelea ili kitu chochote—iwe ni kutokamilika, hatari yoyote, mwanadamu yeyote mwenye nia ya kuua, wala roho yeyote mwovu asiweze kuharibu kiini-tete hicho. Yehova aliendelea kumlinda Yesu alipokuwa kijana. (Mathayo 2:1-15) Mwana mpendwa wa Mungu hangeweza kushambuliwa hadi wakati uliowekwa na Mungu.
12. Kwa nini Yehova aliwalinda kimuujiza watu fulani katika nyakati za Biblia?
12 Kwa nini Yehova aliwalinda watu fulani kimuujiza? Katika visa vingi, Yehova aliwalinda watu fulani akiwa na kusudi la kulinda jambo muhimu zaidi: kutimia kwa kusudi lake. Kwa kielelezo, kuokoka kwa mtoto mchanga Yesu kulikuwa muhimu katika utimizo wa kusudi la Mungu, ambalo litafaidi wanadamu wote hatimaye. Masimulizi ya maonyesho hayo ya nguvu za kulinda ni sehemu ya Maandiko yaliyopuliziwa, ambayo “yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Naam, mifano hiyo inaimarisha imani yetu katika Mungu wetu mwenye nguvu zote. Lakini tunaweza kutarajia kupata ulinzi gani kutoka kwa Mungu leo?
Ahadi ya Kupata Ulinzi wa Mungu Haimaanishi Nini?
13. Je, Yehova ana wajibu wa kutuokoa kimuujiza? Eleza.
13 Ahadi ya kupata ulinzi wa Mungu haimaanishi kwamba Yehova ana wajibu wa kutuokoa kimuujiza. La, Mungu wetu hajaahidi kwamba tutaishi bila matatizo katika mfumo huu wa kale. Watumishi wengi waaminifu wa Yehova wanakumbwa na taabu nyingi sana, kutia ndani umaskini, vita, magonjwa, na kifo. Yesu aliwaambia wanafunzi wake waziwazi kwamba huenda baadhi yao wakauawa kwa sababu ya imani yao. Ndiyo sababu Yesu alikazia uhitaji wa kuvumilia hadi mwisho. (Mathayo 24:9, 13) Ikiwa Yehova angetumia nguvu zake kuokoa watu kimuujiza kila wakati, yamkini Shetani angekuwa na sababu ya kumdhihaki Yehova na kutilia shaka unyofu wetu wa kumtumikia Mungu.—Ayubu 1:9, 10.
14. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba sikuzote Yehova hawalindi watumishi wake wote kwa njia ileile?
14 Hata katika nyakati za Biblia, Yehova hakutumia nguvu zake za kulinda ili kuwakinga watumishi wake wote na kifo cha mapema. Kwa mfano, Herode alimwua mtume Yakobo kwa upanga yapata mwaka wa 44 W.K.; lakini, muda mfupi baadaye, Petro alikombolewa “kutoka kwenye mkono wa Herode.” (Matendo 12:1-11) Na Yohana, ndugu ya Yakobo, aliishi kwa muda mrefu kuliko Petro na Yakobo. Ni wazi kwamba hatuwezi kumtarajia Mungu wetu awalinde watumishi wake wote kwa njia ileile. Isitoshe, “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11, NW) Basi, Yehova anatulindaje leo?
Yehova Anatulinda Kimwili
15, 16. (a) Kuna uthibitisho gani kwamba Yehova amewalinda kimwili waabudu wake wakiwa kikundi? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawalinda watumishi wake sasa na wakati wa ile “dhiki kubwa”?
15 Kwanza, fikiria kuhusu ulinzi wa kimwili. Tukiwa waabudu wa Yehova, tunaweza kutarajia kulindwa kimwili tukiwa kikundi. La sivyo, tungeshambuliwa kwa urahisi na Shetani. Hebu fikiria jambo hili: Shetani, “mtawala wa ulimwengu huu,” angependa sana kukomesha ibada ya kweli. (Yohana 12:31; Ufunuo 12:17) Baadhi ya serikali zenye nguvu sana duniani zimepiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri na kujaribu kutuangamiza kabisa. Hata hivyo, watu wa Yehova wamedumu wakiwa imara na wameendelea kuhubiri bila kuacha! Kwa nini mataifa yenye nguvu yameshindwa kukomesha utendaji wa kikundi hiki kidogo cha Wakristo kinachoonekana kuwa bila ulinzi? Kwa sababu Yehova ametufunika kwa mbawa zake za mfano zenye nguvu!—Zaburi 17:7, 8.
16 Je, atatulinda kimwili wakati wa ile “dhiki kubwa” inayokuja? Hatuhitaji kuogopa hukumu ya Mungu. Kwa sababu “Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, bali kuweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya siku ya hukumu ili kukatiliwa mbali.” (Ufunuo 7:14; 2 Petro 2:9) Kwa sasa, tunaweza kuwa na hakika kabisa kuhusu mambo mawili. Kwanza, Yehova hataruhusu kamwe watumishi wake waaminifu waangamizwe kabisa duniani. Pili, atawapa wale wanaobaki waaminifu zawadi ya kuishi milele katika ulimwengu wake mpya wa uadilifu—hata kama itambidi awafufue. Kwa wale wanaokufa, hakuna mahali pengine salama pa kuwa isipokuwa katika kumbukumbu ya Mungu.—Yohana 5:28, 29.
17. Yehova anatulindaje kupitia Neno lake?
17 Hata sasa, Yehova anatulinda kupitia “neno” lake lililo hai, ambalo lina nguvu ya kuponya watu mioyo na kubadili maisha yao. (Waebrania 4:12) Tunapoishi kwa kupatana na kanuni zake, tunaweza kulindwa kutokana na madhara fulani ya kimwili. “Mimi ni BWANA, . . . nikufundishaye ili upate faida,” yasema Isaya 48:17. Bila shaka, kuishi kwa kupatana na Neno la Mungu kunaweza kuboresha afya yetu na kurefusha maisha yetu. Kwa mfano, tunapotii shauri la Biblia la kujiepusha na uasherati na kujisafisha na kila unajisi, tunaepuka mazoea machafu na yenye kuumiza ambayo yanaharibu kabisa maisha ya watu wengi wasiomtii Mungu. (Matendo 15:29; 2 Wakorintho 7:1) Tunashukuru kama nini kwamba tunalindwa na Neno la Mungu!
Yehova Anatulinda Kiroho
18. Yehova anatulindaje kiroho?
18 Jambo muhimu zaidi ni kwamba Yehova anatulinda kiroho. Mungu wetu mwenye upendo anatulinda kutokana na madhara ya kiroho kwa kutupatia chochote tunachohitaji ili kuvumilia majaribu na kulinda uhusiano wetu naye. Kwa hiyo, Yehova huhifadhi uhai wetu, si kwa miaka michache tu bali kwa umilele. Fikiria baadhi ya maandalizi ya Mungu yanayoweza kutulinda kiroho.
19. Roho ya Yehova inaweza kutusaidiaje kukabiliana na jaribu lolote ambalo huenda likatukumba?
19 Yehova ni “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Tunaweza kupata kitulizo wakati mikazo ya maisha inapotulemea, kwa kumwambia mambo yaliyo mioyoni mwetu. (Wafilipi 4:6, 7) Huenda asiondoe majaribu yetu kimuujiza, lakini anaweza kujibu sala zetu za kutoka moyoni kwa kutupa hekima ya kukabiliana nayo. (Yakobo 1:5, 6) Na zaidi ya hayo, Yehova huwapa roho takatifu wale wanaomwomba. (Luka 11:13) Roho hiyo yenye nguvu inaweza kutusaidia kukabiliana na jaribu au tatizo lolote ambalo huenda likatukumba. Inaweza kututia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili tuvumilie hadi Yehova atakapoondoa matatizo yote yenye kuumiza katika ulimwengu mpya ulio karibu sana.—2 Wakorintho 4:7.
20. Nguvu za Yehova za kulinda zinaweza kuonekanaje kupitia waamini wenzetu?
20 Nyakati nyingine, nguvu za Yehova za kulinda zinaweza kuonekana kupitia waabudu wenzetu. Yehova amewakusanya watu wake katika ‘ushirika [wa ulimwenguni pote] wa ndugu.’ (1 Petro 2:17; Yohana 6:44) Kupitia ushirika huo wenye upendo, tunaona kihalisi jinsi roho takatifu ya Mungu ilivyo na nguvu za kuboresha maisha ya watu. Roho hiyo hukuza matunda ndani yetu, yaani, sifa muhimu zenye kuvutia sana kama vile upendo, fadhili, na wema. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hiyo, tunapokuwa taabani na mwamini mwenzetu anachochewa kutupa shauri lenye kusaidia au kututia moyo inapohitajika, tunaweza kumshukuru Yehova kwa sababu ya ulinzi na utunzaji anaotoa kwa njia hiyo.
21. (a) Yehova anaandaa chakula kipi cha kiroho kwa wakati ufaao kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (b) Je, wewe binafsi umefaidika na maandalizi ya Yehova ya kutulinda kiroho?
21 Yehova hutayarisha mambo mengine ya kutulinda: chakula cha kiroho kwa wakati ufaao. Ili kutusaidia kuimarishwa na Neno lake, Yehova amemwagiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aandae chakula cha kiroho. Mtumwa huyo mwaminifu hutumia vichapo, kama magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, vilevile mikutano, na makusanyiko ili kutupatia ‘chakula kwa wakati ufaao’—chochote tunachohitaji, wakati tunapokihitaji. (Mathayo 24:45) Je, umewahi kusikia jambo fulani kwenye mikutano ya Kikristo—katika maelezo, hotuba, au hata katika sala—ambalo lilikupa nguvu na kitia-moyo ulichohitaji sana? Je, maisha yako yamewahi kuathiriwa na makala fulani hususa iliyochapishwa katika mojawapo ya magazeti yetu? Kumbuka kwamba Yehova hutayarisha maandalizi hayo yote ili kutulinda kiroho.
22. Sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa njia gani, na kwa nini jambo hilo linatufaidi?
22 Hapana shaka kwamba Yehova ni ngao ‘ya wote wanaomkimbilia.’ (Zaburi 18:30) Tunafahamu kwamba yeye hatumii nguvu zake kutulinda tusipatwe na misiba sasa. Hata hivyo, sikuzote yeye hutumia nguvu zake za kulinda kuhakikisha kwamba kusudi lake linatimizwa. Yeye hufanya hivyo ili kuwafaidi watu wake hatimaye. Tukimkaribia na kudumu katika upendo wake, Yehova atatupatia uhai mkamilifu utakaodumu milele. Tukikumbuka tumaini hilo, kwa kweli tunaweza kuona mateso yoyote yanayotupata katika mfumo huu kuwa ‘ya dakika na mepesi.’—2 Wakorintho 4:17.
-
-
Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 8
Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’
1, 2. Wanadamu hukumbwa na matatizo gani leo, nayo yanatuathirije?
MTOTO hulia kwa uchungu sana kitu cha kuchezea anachopenda kinapoharibika. Kilio chake huhuzunisha sana! Lakini je, umewahi kuona jinsi mtoto anavyosisimuka mzazi anapokirekebisha kitu hicho na kukirudisha katika hali nzuri? Huenda mzazi akarekebisha kitu hicho kwa urahisi sana. Lakini mtoto anafurahi sana na kupigwa na bumbuazi. Kitu cha kuchezea alichofikiri kimeharibika kabisa kimerudishwa katika hali nzuri!
2 Yehova ambaye ni Baba bora zaidi, ana uwezo wa kurudisha katika hali nzuri vitu na hali mbalimbali ambazo watoto wake wa kidunia huenda wakadhani haziwezi kuboreshwa. Bila shaka, hatumaanishi vitu vya kuchezea. Hatuna budi kupatwa na matatizo makubwa zaidi katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1-5) Vitu ambavyo watu wanathamini sana, kama vile makao, mali, kazi, hata afya viko hatarini daima. Huenda pia tukafadhaika kuona mazingira yakiharibiwa na kuona hasara kubwa inayosababishwa na uharibifu huo, au kuona jamii nyingi za viumbe zikitoweka kabisa. Hata hivyo, hakuna jambo linalotuhuzunisha zaidi kuliko kifo cha mpendwa wetu. Uchungu wa kumpoteza mpendwa na kuhisi tukiwa hoi unaweza kutulemea sana.—2 Samweli 18:33.
3. Ni taraja gani lenye kufariji linalotajwa kwenye Matendo 3:21, na Yehova atalitimizaje?
3 Basi inafariji kama nini kujua kwamba Yehova ana uwezo wa kurudisha mambo yote katika hali nzuri! Kama tutakavyoona, Mungu ana uwezo wa kurudisha katika hali nzuri mambo mengi sana yaliyoharibika duniani. Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba Yehova anakusudia ‘kurudisha mambo yote.’ (Matendo 3:21) Yehova atatumia Ufalme wa Kimesiya, unaotawaliwa na Mwanaye, Yesu Kristo ili kutimiza hayo. Kuna uthibitisho kwamba Ufalme huo ulianza kutawala mbinguni mwaka wa 1914.a (Mathayo 24:3-14) Ni mambo gani yatakayorudishwa katika hali nzuri? Tuchunguze baadhi ya mambo matukufu ambayo Yehova amenuia kurudisha katika hali nzuri. Tunaweza kuona na kufurahia mojawapo ya mambo hayo hivi sasa. Mambo mengineyo yatarudishwa kikamili wakati ujao.
Kurudishwa kwa Ibada Safi
4, 5. Ni nini kilichowapata watu wa Mungu mwaka wa 607 K.W.K., na Yehova aliwaahidi nini?
4 Jambo moja ambalo Yehova tayari amerudisha sasa ni ibada safi. Ili kufahamu jambo hilo, tuchunguze kifupi historia ya ufalme wa Yuda. Uchunguzi huo wenye kusisimua utatusaidia kuelewa jinsi ambavyo Yehova amekuwa akitumia uwezo wake wa kurudisha mambo katika hali nzuri.—Waroma 15:4.
5 Hebu wazia jinsi Wayahudi waaminifu walivyohisi mwaka wa 607 K.W.K. wakati jiji la Yerusalemu lilipoharibiwa. Jiji lao walilopenda liliharibiwa, na kuta zake zikabomolewa. Jambo la kusikitisha hata zaidi ni kwamba hekalu tukufu lililojengwa na Solomoni, kitovu pekee cha ibada safi ya Yehova duniani kote, liliharibiwa kabisa. (Zaburi 79:1) Wale walionusurika walipelekwa uhamishoni Babiloni. Waliacha nchi yao ikiwa makao ya wanyama wa mwitu tu. (Yeremia 9:11) Kwa wanadamu, ilionekana ni kana kwamba hakukuwa na tumaini tena. (Zaburi 137:1) Lakini Yehova, aliyekuwa ametabiri hapo kale kuhusu uharibifu huo, aliwaahidi kwamba angewarudisha nchini mwao na kurudisha ibada safi.
6-8. (a) Manabii Waebrania waliandika tena na tena kuhusu nini, na unabii huo mbalimbali ulitimizwaje kwa mara ya kwanza? (b) Katika nyakati za kisasa, unabii mbalimbali wa kurudishwa umetimizwaje kuhusiana na watu wa Mungu?
6 Kwa kweli, manabii Waebrania waliandika tena na tena kuhusu kurudishwa huko.b Kupitia manabii hao, Yehova aliahidi kwamba angewarudisha katika nchi yenye rutuba, na kuwalinda dhidi ya maadui na wanyama wakali. Alieleza kuwa nchi yao iliyofanywa upya ingekuwa kama paradiso! (Isaya 65:25; Ezekieli 34:25; 36:35) Zaidi ya yote, ibada safi ingeanzishwa tena, na hekalu lingejengwa upya. (Mika 4:1-5) Unabii huo mbalimbali uliwapa Wayahudi hao waliohamishwa tumaini, na uliwasaidia kuvumilia kwa miaka 70 walipokuwa uhamishoni huko Babiloni.
7 Hatimaye, wakati wa kurudishwa ulifika. Wayahudi walipoachiliwa huru kutoka Babiloni, walirudi Yerusalemu na kujenga upya hekalu la Yehova. (Ezra 1:1, 2) Maadamu walishikamana na ibada safi, Yehova aliwabariki na kufanya nchi yao kuwa na rutuba na ufanisi. Aliwalinda dhidi ya maadui na wanyama wakali ambao walikuwa wamevamia nchi yao kwa miaka mingi. Walishangilia kama nini kuona Yehova akitumia uwezo wake wa kurudisha mambo katika hali nzuri! Lakini mambo hayo yalikuwa utimizo mdogo wa kwanza wa unabii mbalimbali wa kurudishwa. Utimizo mkubwa ungetukia “katika siku za mwisho,” katika siku zetu, wakati ambapo Mrithi aliyeahidiwa tangu kale wa Mfalme Daudi angetawazwa.—Isaya 2:2-4; 9:6, 7.
8 Punde tu baada ya Yesu kutawazwa katika Ufalme wa mbinguni mwaka wa 1914, alianza kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu waaminifu wa Mungu duniani. Kama vile mshindi Mwajemi aitwaye Koreshi alivyowaachilia huru mabaki ya Wayahudi kutoka Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., Yesu aliweka huru mabaki ya Wayahudi wa kiroho, yaani, wafuasi wake, kutoka kwa uvutano wa Babiloni la kisasa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. (Waroma 2:29; Ufunuo 18:1-5) Tangu mwaka wa 1919 na kuendelea, ibada safi imerudishwa mahali pafaapo katika maisha ya Wakristo wa kweli. (Malaki 3:1-5) Tangu hapo, watu wa Yehova wamekuwa wakimwabudu katika hekalu la kiroho lililosafishwa, yaani, mpango wa Mungu wa ibada safi. Kwa nini jambo hilo ni muhimu kwetu leo?
Kurudishwa kwa Ibada Safi Ni Muhimu Sana
9. Baada ya mitume kufa, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yaliathirije ibada ya Mungu, lakini Yehova amechukua hatua gani wakati wetu?
9 Fikiria matukio ya kihistoria. Wakristo walioishi katika karne ya kwanza walibarikiwa sana kiroho. Lakini Yesu na mitume walitabiri kwamba ibada ya kweli ingechafuliwa na kutokomea. (Mathayo 13:24-30; Matendo 20:29, 30) Jumuiya ya Wakristo ilitokea baada ya mitume kufa. Makasisi wake walifuata mafundisho na mazoea ya kipagani. Waliwazuia watu wasiwe na uhusiano na Mungu kwa sababu walifundisha fundisho la Utatu lisiloeleweka, na waliwafundisha watu kuungama mbele ya makasisi na kusali kwa Maria na “watakatifu” mbalimbali badala ya kusali kwa Yehova. Sasa, Yehova amechukua hatua gani baada ya watu kuacha ibada safi kwa miaka mingi? Katika ulimwengu wa leo uliojaa mafundisho ya uwongo ya dini na mazoea yake maovu, Yehova amechukua hatua ya kurudisha ibada safi! Si kutilia chumvi kusema kwamba kurudishwa kwa ibada safi ni mojawapo ya matukio muhimu katika nyakati za kisasa.
10, 11. (a) Paradiso ya kiroho inahusisha mambo gani mawili muhimu, na yanakuhusuje? (b) Yehova amekusanya watu wa aina gani katika paradiso ya kiroho, nao watakuwa na pendeleo la kuona nini?
10 Basi Wakristo wa kweli leo wanafurahia paradiso ya kiroho. Paradiso hiyo inahusisha nini? Inahusisha hasa mambo mawili muhimu. Jambo la kwanza ni ibada safi ya Mungu wa kweli, Yehova. Ametubariki kwa kutupatia ibada isiyo na upotovu wala uwongo. Ametuandalia chakula cha kiroho. Hilo hutusaidia tujifunze kuhusu Baba yetu wa mbinguni, tumpendeze, na tumkaribie. (Yohana 4:24) Jambo la pili katika paradiso ya kiroho linahusu watu. Kama Isaya alivyotabiri, “katika siku za mwisho,” Yehova amewafundisha waabudu wake njia za amani. Amekomesha vita miongoni mwetu. Licha ya hali yetu ya kutokamilika, yeye hutusaidia kuvaa “utu mpya.” Anabariki jitihada zetu kwa kutupatia roho yake takatifu, ambayo inatokeza matunda bora sana maishani mwetu. (Waefeso 4:22-24; Wagalatia 5:22, 23) Unapotenda kupatana na roho ya Mungu, unakuwa kwelikweli sehemu ya paradiso ya kiroho.
11 Yehova amekusanya watu anaowapenda katika paradiso hiyo ya kiroho, yaani, watu wanaompenda, wanaopenda amani, na ‘wanaona uhitaji wao wa kiroho.’ (Mathayo 5:3) Watu hao watakuwa na pendeleo la pekee la kuona wanadamu na dunia nzima ikirudishwa katika hali nzuri ajabu.
“Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
12, 13. (a) Kwa nini kutakuwa na utimizo mwingine wa unabii wa kurudisha hali nzuri? (b) Katika Edeni, Yehova alisema kusudi lake ni nini kwa dunia, na kwa nini hilo linatupatia tumaini la wakati ujao?
12 Yaonekana kwamba unabii mbalimbali wa kurudisha haurejezei tu kurudishwa kwa ibada safi. Kwa mfano, Isaya alitabiri kuhusu wakati ambapo wagonjwa, walemavu, vipofu, na viziwi wataponywa na hata kifo kitamezwa milele. (Isaya 25:8; 35:1-7) Ahadi hizo hazikutimizwa kihalisi katika Israeli la kale. Na ijapokuwa tumeona ahadi hizo zikitimizwa kwa njia ya kiroho nyakati zetu, kuna msingi thabiti wa kuamini kwamba ahadi hizo zitatimizwa kihalisi na kikamili wakati ujao.
13 Katika Edeni, Yehova alitaja waziwazi kusudi lake kwa dunia: Ilipasa kukaliwa na familia ya wanadamu wenye furaha, afya na umoja. Mwanamume na mwanamke walipaswa kutunza dunia na viumbe wake wote, na kufanya dunia yote iwe paradiso. (Mwanzo 1:28) Leo, hali ni tofauti kabisa. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba makusudi ya Yehova hayawezi kuzuiwa kamwe. (Isaya 55:10, 11) Yesu, ambaye ni Mfalme wa Kimesiya aliyeteuliwa na Yehova, atafanya dunia yote kuwa Paradiso.—Luka 23:43.
14, 15. (a) Yehova ‘atafanyaje vitu vyote viwe vipya’? (b) Maisha yatakuwaje katika Paradiso, na ni jambo gani linalokuvutia zaidi?
14 Hebu wazia dunia yote ikiwa Paradiso! Yehova anasema hivi kuhusu wakati huo: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Fikiria hali itakavyokuwa. Baada ya Yehova kuharibu mfumo huu mwovu wa kale kwa kutumia nguvu zake za kuangamiza, “mbingu mpya na dunia mpya” zitabaki. Hilo lamaanisha kwamba serikali mpya ikiwa mbinguni, itatawala jamii mpya ya kidunia ya wanadamu wanaompenda Yehova na kufanya mapenzi yake. (2 Petro 3:13) Shetani pamoja na mashetani wake, watafungwa ili wasiweze kutenda. (Ufunuo 20:3) Baada ya maelfu ya miaka kupita, kwa mara ya kwanza kabisa wanadamu hawataathiriwa tena na uvutano wake wenye kupotosha, wa chuki, na wenye kuumiza. Hapana shaka kwamba wanadamu watapata faraja isiyo na kifani.
15 Hatimaye, tutaweza kutunza dunia hii maridadi kama ilivyokusudiwa mwanzoni. Dunia ina uwezo wa kujisafisha yenyewe. Maziwa na mito michafu inaweza kujisafisha yenyewe isipoendelea kuchafuliwa; sehemu zilizoharibiwa na vita zinaweza kuwa nzuri endapo vita vitakoma. Itafurahisha kama nini kufanya kazi kwa kupatana na maumbile ya dunia, na kuifanya iwe bustani maridadi, yaani, Edeni ya duniani pote yenye viumbe na mimea ya kila namna! Badala ya kuangamiza wanyama na mimea mbalimbali, mwanadamu ataishi kwa amani na uumbaji wote. Hata watoto hawataogopa wanyama wa mwitu.—Isaya 9:6, 7; 11:1-9.
16. Katika Paradiso, watu wote waaminifu watarudishwa katika hali gani?
16 Tutafurahi pia kurudishiwa afya njema. Baada ya Har–Magedoni, waokokaji wataona maponyo ya kimuujiza ulimwenguni pote. Yesu atatumia nguvu alizopewa na Mungu kuwaponya vipofu, viziwi, walemavu na walio wagonjwa kama alivyofanya alipokuwa duniani. (Mathayo 15:30) Watu wazee watafurahi kuwa tena na nguvu, afya, na juhudi za ujanani. (Ayubu 33:25) Makunyanzi yatatoweka, viungo vitanyooka, na misuli itakuwa na nguvu tena. Wanadamu wote waaminifu wataona madhara ya dhambi na kutokamilika yakididimia hatua kwa hatua, na hatimaye kutokomea. Tutamshukuru Yehova Mungu kama nini kwa sababu ya nguvu zake za kustaajabisha za kufanya mambo yote kuwa mapya! Sasa tukazie fikira jambo moja lenye kuchangamsha litakalotukia wakati huo wenye kusisimua wa kufanya mambo kuwa mapya.
Kuwafufua Wafu
17, 18. (a) Kwa nini Yesu aliwashutumu Masadukayo? (b) Ni tukio gani lililomfanya Eliya amwombe Yehova amfufue mfu?
17 Katika karne ya kwanza W.K., viongozi fulani wa kidini, wanaoitwa Masadukayo, hawakuamini ufufuo. Yesu aliwashutumu hivi: “Mwakosea, kwa sababu hamjui wala Maandiko wala nguvu ya Mungu.” (Mathayo 22:29) Naam, Maandiko yanafunua kwamba Yehova ana nguvu za kufufua. Jinsi gani?
18 Hebu wazia jambo lililotukia siku za Eliya. Mjane mmoja alikuwa amebeba mwili wa mwanaye pekee. Mvulana huyo alikuwa mfu. Haikosi jambo hilo lilimshtua nabii Eliya, aliyekuwa ameishi katika nyumba ya mjane huyo kwa muda fulani. Mapema, alimwokoa mtoto huyo asife njaa. Yaelekea Eliya alimpenda sana mvulana huyo. Mamaye alihuzunika sana. Mvulana huyo pekee ndiye aliyemfanya amkumbuke mume wake aliyekuwa amekufa. Huenda alitumaini kwamba mwanaye angemtunza akizeeka. Mjane huyo aliyefadhaika alidhani kwamba labda alikuwa akiadhibiwa kwa sababu ya dhambi fulani aliyotenda zamani. Eliya hakuweza kuvumilia msiba huo wenye kusikitisha sana. Alitwaa huyo mfu kwa upole kutoka katika kifua cha mamaye, akampeleka katika chumba chake orofani, kisha akamwomba Yehova Mungu arudishe nafsi au uhai, wa mtoto huyo.—1 Wafalme 17:8-21.
19, 20. (a) Abrahamu alionyeshaje imani kwamba Yehova anaweza kufufua, na imani hiyo ilitegemea nini? (b) Yehova alimthawabishaje Eliya kwa sababu ya imani yake?
19 Eliya hakuwa mtu wa kwanza kuamini ufufuo. Miaka mingi mapema, Abrahamu aliamini kwamba Yehova ana uwezo wa kufufua. Na alikuwa na sababu nzuri ya kuamini hivyo. Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 100 na Sara miaka 90, Yehova alirudisha uwezo wao wa kuzaa, na Sara akamzaa mwana kimuujiza. (Mwanzo 17:17; 21:2, 3) Baadaye, kijana huyo alipokuwa mtu mzima, Yehova alimwamuru Abrahamu amtoe kuwa dhabihu. Abrahamu alikuwa na imani, alitambua kwamba Yehova angeweza kumfufua Isaka mwanaye mpendwa. (Waebrania 11:17-19) Yaonekana imani hiyo thabiti ndiyo iliyomfanya Abrahamu, kabla ya kukwea mlimani kumtoa mwanaye, awahakikishie watumishi wake kwamba yeye na Isaka wangerudi pamoja.—Mwanzo 22:5.
“Tazama, mwanao yu hai”!
20 Yehova aliingilia na Isaka hakuuawa, hivyo ufufuo haukuhitajiwa wakati huo. Hata hivyo, katika kisa cha Eliya, mwana wa mjane tayari alikuwa amekufa—lakini si kwa muda mrefu. Yehova alimthawabisha nabii huyo mwenye imani kwa kumfufua mwana huyo! Kisha Eliya akamrudisha mvulana huyo kwa mamaye, akanena maneno haya yasiyoweza kusahaulika: “Tazama, mwanao yu hai”!—1 Wafalme 17:22-24.
21, 22. (a) Ufufuo mbalimbali unaosimuliwa katika Maandiko ulikuwa na kusudi gani? (b) Ni watu wangapi watakaofufuliwa katika Paradiso, na ni nani atakayewafufua?
21 Hivyo basi, kwa mara ya kwanza kabisa katika Biblia, twaona Yehova akitumia uwezo wake wa kuwafufua wanadamu. Baadaye, Yehova pia aliwapa Elisha, Yesu, Paulo, na Petro uwezo wa kufufua wafu. Bila shaka, wale waliofufuliwa walikufa hatimaye. Hata hivyo, matukio hayo ya Biblia yanatuonyesha mambo mazuri yatakayotukia wakati ujao.
22 Katika Paradiso, Yesu atakuwa “ufufuo na uhai.” (Yohana 11:25) Atafufua mamilioni ya wafu, na kuwapa fursa ya kuishi milele katika Paradiso duniani. (Yohana 5:28, 29) Hebu wazia jinsi marafiki wapendwa na watu wa jamaa waliotenganishwa na kifo watakavyokumbatiana kwa shangwe kubwa ajabu! Wanadamu wote watamsifu Yehova kwa ajili ya uwezo wake wa kufufua.
23. Ni tukio gani lililokuwa uthibitisho mkuu zaidi wa uwezo wa Yehova, na hilo linatuhakikishia jinsi gani tumaini letu la wakati ujao?
23 Yehova ametuhakikishia kabisa kwamba tumaini hilo ni hakika. Yehova alithibitisha uwezo wake kwa njia kuu kupita zote alipomfufua Mwanaye, Yesu, akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo, na kumpa cheo cha pili katika ulimwengu mzima. Mamia ya watu walimwona Yesu aliyefufuliwa. (1 Wakorintho 15:5, 6) Ushahidi huo unatosha kuwasadikisha wale wanaotilia shaka jambo hilo. Yehova ana uwezo wa kufufua.
24. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atafufua wafu, na sote tunaweza kuthamini tumaini gani?
24 Si kwamba tu Yehova ana uwezo wa kufufua wafu bali pia ana tamaa ya kufanya hivyo. Mwanamume mwaminifu Yobu alipuliziwa kusema kwamba kwa kweli Yehova ana tamaa ya kuwafufua wafu. (Ayubu 14:15) Je, wewe huvutiwa na Mungu wetu, ambaye anatamani kutumia kwa upendo uwezo wake wa kufufua? Kumbuka kwamba ufufuo ni sehemu moja tu ya kazi kubwa ambayo Yehova atafanya wakati ujao ya kufanya mambo kuwa mapya. Kadiri unavyomkaribia zaidi, endelea kuthamini tumaini la pekee sana la kwamba huenda ukawapo Yehova ‘atakapofanya vitu vyote kuwa vipya.’—Ufunuo 21:5.
a “Nyakati za kurudishwa kwa mambo yote” zilianza wakati Ufalme wa Kimesiya uliposimamishwa, mrithi wa Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu alipowekwa kuwa mtawala wa Ufalme huo. Yehova alikuwa amemwahidi Daudi kwamba mrithi wake angetawala milele. (Zaburi 89:35-37) Lakini baada ya Babiloni kuharibu Yerusalemu mnamo mwaka wa 607 K.W.K., kiti cha enzi cha Mungu hakikukaliwa na mwanadamu mwingine yeyote aliye mzao wa Daudi. Yesu, aliyezaliwa duniani akiwa mrithi wa Daudi, akawa Mfalme aliyeahidiwa tangu kale alipotawazwa mbinguni.
b Kwa mfano, Musa, Isaya, Yeremia, Ezekieli, Hosea, Yoeli, Amosi, Obadia, Mika, na Sefania walikazia jambo hilo.
-
-
“Kristo Ni Nguvu ya Mungu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 9
“Kristo Ni Nguvu ya Mungu”
1-3. (a) Wanafunzi walipatwa na tukio gani lenye kutisha katika Bahari ya Galilaya, na Yesu alifanya nini? (b) Kwa nini inafaa kusema kwamba “Kristo ni nguvu ya Mungu”?
WANAFUNZI waliogopa sana. Dhoruba ilizuka ghafula walipokuwa wakivuka Bahari ya Galilaya kwa mashua. Hapana shaka kwamba walizoea kuona dhoruba katika bahari hiyo, kwa sababu baadhi yao walikuwa wavuvi hodari sana.a (Mathayo 4:18, 19) Lakini hiyo ilikuwa “dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi.” Bahari ilichafuka kwa sababu ya dhoruba hiyo. Wanaume hao walijikakamua sana kuongoza mashua, lakini dhoruba ilikuwa kali sana. Mawimbi makubwa yalikuwa ‘yanapiga kwa nguvu ndani ya mashua,’ hata ikaanza kujaa maji. Kujapokuwa na vurugu hiyo, Yesu alikuwa amelala usingizi katika tezi, akiwa amechoka baada ya kuwafundisha watu siku nzima. Huku wakiogopa kufa, wanafunzi walimwamsha na kumsihi hivi: “Bwana, tuokoe, tuko karibu kuangamia!”—Marko 4:35-38; Mathayo 8:23-25.
2 Yesu hakuogopa. Kwa ujasiri, aliukemea upepo na bahari: “Usu! Nyamaa!” Mara moja, upepo na bahari vikatii—dhoruba ikakoma, mawimbi yakatulia tuli, “kukawa shwari kubwa.” Wanafunzi wakahisi hofu isiyo ya kawaida. Wakanong’onezana: “Ni binadamu wa namna gani huyu?” Kwa kweli, ni mwanadamu gani angeweza kuukemea upepo na bahari kana kwamba anamkemea mtoto mtukutu?—Marko 4:39-41; Mathayo 8:26, 27.
3 Lakini Yesu hakuwa mwanadamu wa kawaida. Yehova alidhihirisha nguvu zake kupitia Yesu, naye Yesu alizitumia kwa njia za pekee sana. Mtume Paulo aliyepuliziwa alisema kwa kufaa kwamba “Kristo ni nguvu ya Mungu.” (1 Wakorintho 1:24) Mungu anaonyeshaje nguvu zake kupitia Yesu? Na jinsi Yesu anavyotumia nguvu hizo kunaweza kuwa na matokeo gani maishani mwetu?
Nguvu za Mwana Mzaliwa-Pekee wa Mungu
4, 5. (a) Yehova alimpa Mwana wake mzaliwa-pekee nguvu na mamlaka ya kufanya nini? (b) Mwana huyo angetumia nini kutimiza makusudi ya uumbaji ya Baba yake?
4 Fikiria nguvu alizokuwa nazo Yesu kabla hajawa mwanadamu. Yehova alitumia “nguvu zake za milele” alipomwumba Mwana wake mzaliwa-pekee, ambaye alikuja kuitwa Yesu Kristo. (Waroma 1:20; Wakolosai 1:15) Baadaye, Yehova alimpa Mwana huyo mamlaka na nguvu nyingi sana. Alimpa kazi ya kutimiza makusudi Yake ya uumbaji. Biblia yasema hivi kumhusu Mwana huyo: “Vitu vyote vilikuja kuwako kupitia yeye, na bila yeye hata kitu kimoja hakikuja kuwako.”—Yohana 1:3.
5 Hatuwezi kufahamu kikamili uzito wa kazi hiyo. Hebu wazia nguvu zinazohitajiwa kuumba mamilioni ya malaika wenye uwezo, mabilioni ya makundi ya nyota, dunia na viumbe wote waliomo. Mwana mzaliwa-pekee alifanya kazi hizo kwa kutumia roho takatifu ya Mungu ambayo ni nguvu isiyo na kifani katika ulimwengu mzima. Mwana huyo alifurahia kuwa Stadi wa Kazi, na alitumiwa na Yehova kuumba vitu vingine vyote.—Mithali 8:22-31.
6. Baada ya kufa na kufufuliwa, Yesu alipewa nguvu na mamlaka gani?
6 Je, Mwana huyo mzaliwa-pekee angeweza kupewa nguvu na mamlaka zaidi? Yesu alisema hivi baada ya kufa na kufufuliwa: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18) Naam, Yesu alikuwa amepewa uwezo na haki ya kutawala ulimwengu mzima. Akiwa “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” amepewa mamlaka ya kufanya “serikali yote na mamlaka yote na nguvu”—zinazoonekana na zile zisizoonekana—ambazo zinampinga Baba yake “kuwa si kitu.” (Ufunuo 19:16; 1 Wakorintho 15:24-26) ‘Vitu vyote vilitiishwa chini ya’ Yesu, ila Yehova Mungu mwenyewe.—Waebrania 2:8; 1 Wakorintho 15:27.
7. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu hatatumia vibaya kamwe nguvu ambazo Yehova amempa?
7 Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda Yesu akatumia nguvu zake vibaya? La hasha! Yesu anampenda sana Baba yake na hawezi kamwe kutenda jambo lolote lisilompendeza. (Yohana 8:29; 14:31) Yesu anajua vizuri kwamba Yehova hatumii vibaya nguvu na uweza wake. Yesu ameona kwamba Yehova hutafuta fursa za ‘kujionyesha mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.’ (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Bila shaka, Yesu anawapenda wanadamu kama Baba yake, kwa hiyo tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yesu atatumia nguvu zake kwa faida yetu. (Yohana 13:1) Yesu hajapata kamwe kutumia nguvu zake vibaya. Hebu tuone nguvu alizokuwa nazo alipokuwa duniani na jinsi alivyozitumia.
“Mwenye Nguvu Katika . . . Neno”
8. Baada ya kutiwa mafuta, Yesu alipewa nguvu za kufanya nini, naye alitumiaje nguvu zake?
8 Yesu hakufanya miujiza huko Nazareti alipokuwa mvulana. Lakini hali ilibadilika alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., akiwa na umri wa miaka 30 hivi. (Luka 3:21-23) Biblia yatuambia hivi: ‘Mungu alimtia mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akaenda akipita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote wale walioonewa na Ibilisi.’ (Matendo 10:38) Bila shaka, maneno “akitenda mema” yanaonyesha kwamba alitumia nguvu zake ifaavyo. Baada ya kutiwa mafuta, ‘akawa nabii mwenye nguvu katika kazi na neno.’—Luka 24:19.
9-11. (a) Mara nyingi Yesu alifundisha wapi, na alikabili tatizo gani? (b) Kwa nini umati wa watu ulistaajabia njia ya Yesu ya kufundisha?
9 Yesu alikuwa mwenye nguvu katika neno jinsi gani? Mara nyingi alifundisha nje—kando ya ziwa, milimani, mitaani, na pia masokoni. (Marko 6:53-56; Luka 5:1-3; 13:26) Wale waliomsikiliza walikuwa huru kuondoka iwapo maneno yake hayakuwapendeza. Wasikilizaji waliothamini mafundisho ya Yesu waliweza tu kuyahifadhi mafundisho hayo katika akili na mioyo yao kwa sababu hawakuwa na vitabu. Basi ilimbidi Yesu afundishe kwa njia yenye kugusa moyo sana, iliyo wazi na yenye kueleweka kwa urahisi. Lakini hilo halikuwa tatizo kwa Yesu. Hebu fikiria Mahubiri yake ya Mlimani.
10 Asubuhi moja mapema mwaka wa 31 W.K., umati wa watu ulikusanyika mlimani karibu na Bahari ya Galilaya. Baadhi yao walikuwa wametoka Yudea na Yerusalemu, umbali wa kilometa 100 hadi 110. Wengine walikuwa wametoka upande wa kaskazini katika mwambao wa pwani wa Tiro na Sidoni. Wagonjwa wengi walimkaribia Yesu na kumgusa, naye aliwaponya wote. Baada ya kuwaponya wagonjwa wote, alianza kufundisha. (Luka 6:17-19) Alipomaliza kuwafundisha, walistaajabia mambo waliyosikia. Kwa nini?
11 Miaka mingi baadaye, mmojawapo wa wale waliosikia mahubiri hayo aliandika hivi: “Umati ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka.” (Mathayo 7:28, 29) Waliweza kuhisi kwamba Yesu alizungumza kwa mamlaka. Alimwakilisha Mungu, na mafundisho yake yalitegemea Neno la Mungu. (Yohana 7:16) Yesu aliwafundisha kwa maneno yaliyoeleweka, aliwasadikisha, na kutoa sababu zisizoweza kupingwa. Alikazia mambo muhimu na kufikia mioyo ya wasikilizaji wake. Aliwafundisha jinsi ya kupata furaha, jinsi ya kusali, jinsi ya kutafuta Ufalme wa Mungu, na jinsi ya kuwa na wakati ujao salama. (Mathayo 5:3–7:27) Maneno yake yalichochea mioyo ya wale waliokuwa na njaa ya kweli na uadilifu. Watu hao walikuwa tayari ‘kujikana’ wenyewe na kuacha kila kitu ili wamfuate. (Mathayo 16:24; Luka 5:10, 11) Huo ni uthibitisho ulioje wa nguvu za maneno ya Yesu!
“Mwenye Nguvu Katika Kazi”
12, 13. Yesu alikuwa “mwenye nguvu katika kazi” jinsi gani, naye alifanya miujiza gani mbalimbali?
12 Yesu alikuwa pia “mwenye nguvu katika kazi.” (Luka 24:19) Vitabu vya Injili vinataja zaidi ya miujiza 30 hususa aliyofanya—kwa “nguvu ya Yehova.”b (Luka 5:17) Miujiza ya Yesu ilifaidi maelfu ya watu. Katika miujiza miwili peke yake—alipolisha wanaume 5,000 na baadaye wanaume 4,000, “bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga”—yaelekea alilisha jumla ya watu wapatao 20,000!—Mathayo 14:13-21; 15:32-38.
“Wakamwona Yesu akitembea juu ya bahari”
13 Yesu alifanya miujiza mbalimbali. Alikuwa na mamlaka ya kudhibiti roho waovu—aliwafukuza kwa urahisi sana. (Luka 9:37-43) Alikuwa na mamlaka juu ya vitu vya asili—aligeuza maji yakawa divai. (Yohana 2:1-11) Wanafunzi wake walishangaa walipomwona akitembea juu ya Bahari ya Galilaya yenye upepo mkali. (Yohana 6:18, 19) Alikuwa na uwezo wa kuponya ulemavu, magonjwa ya kudumu, na magonjwa ya kufisha. (Marko 3:1-5; Yohana 4:46-54) Aliponya kwa njia mbalimbali. Watu kadhaa waliponywa wakiwa mbali, ilhali aliwaponya wengine kwa kwa kuwagusa. (Mathayo 8:2, 3, 5-13) Baadhi ya watu waliponywa mara moja, wengine waliponywa hatua kwa hatua.—Marko 8:22-25; Luka 8:43, 44.
14. Yesu alionyesha kwamba alikuwa na nguvu za kufufua katika hali gani mbalimbali?
14 Yesu alikuwa na nguvu za pekee sana za kufufua wafu. Biblia inaonyesha kwamba alifufua wafu watatu. Alimfufua binti mwenye umri wa miaka 12 na kumrudisha kwa wazazi wake, alimfufua mwana-pekee wa mjane, na akamfufua ndugu mpendwa wa dada fulani. (Luka 7:11-15; 8:49-56; Yohana 11:38-44) Yesu aliweza kumfufua mtu katika hali zozote. Alimfufua yule msichana mwenye umri wa miaka 12 muda mfupi baada ya kufa. Alimfufua mwana wa mjane kutoka kwenye machela, siku ileile aliyokufa. Naye Lazaro alifufuliwa na Yesu baada ya kukaa siku nne kaburini.
Alitumia Nguvu kwa Busara, kwa Huruma na Bila Ubinafsi
15, 16. Kuna ushuhuda gani kwamba Yesu hakutumia nguvu zake kwa ubinafsi?
15 Hebu wazia jinsi ambavyo mtawala asiyekamilika angeweza kuwakandamiza watu kama angepewa nguvu za Yesu. Lakini Yesu hakuwa na dhambi. (1 Petro 2:22) Hakujiruhusu kuathiriwa na ubinafsi, tamaa ya makuu, na pupa ambayo huwafanya wanadamu wasiokamilika wenye mamlaka wawakandamize wengine.
16 Yesu hakutumia nguvu zake kwa ubinafsi ili kujifaidi. Alipohisi njaa, alikataa kugeuza mawe yawe mkate. (Mathayo 4:1-4) Yesu hakuwa na mali nyingi. Hiyo inaonyesha kwamba hakutumia nguvu zake ili kujitajirisha. (Mathayo 8:20) Kuna mambo mengine yanayothibitisha kwamba hakufanya miujiza kwa sababu ya ubinafsi. Alipofanya miujiza, alijidhabihu kwa kadiri fulani. Nguvu zilimtoka alipowaponya wagonjwa. Alihisi nguvu zikimtoka hata alipomponya mtu mmoja tu. (Marko 5:25-34) Na bado aliruhusu umati wa watu umguse, naye akawaponya. (Luka 6:19) Alionyesha roho isiyo ya ubinafsi kama nini!
17. Yesu alitumiaje nguvu zake kwa busara?
17 Yesu alitumia nguvu zake kwa busara. Hakufanya miujiza ili kujionyesha tu au kuwastaajabisha watu bila kusudi lolote. (Mathayo 4:5-7) Alikataa kufanya ishara ili kumfurahisha Herode mwenye nia mbaya. (Luka 23:8, 9) Badala ya kutangaza nguvu zake, mara nyingi Yesu aliwaagiza wale aliowaponya wasimwambie mtu yeyote. (Marko 5:43; 7:36) Hakutaka watu wamjue kupitia uvumi wenye kusisimua.—Mathayo 12:15-19.
18-20. (a) Yesu alionyesha sifa zipi alipotumia nguvu zake? (b) Wahisije kuhusu jinsi ambavyo Yesu alimponya mtu fulani aliyekuwa kiziwi?
18 Huyo Yesu mwenye nguvu sana, alikuwa tofauti kabisa na watawala ambao wamekuwa wakitumia nguvu zao bila kujali mahitaji na kuteseka kwa wengine. Yesu aliwajali watu. Alisikitika sana alipowaona watu wakiteseka hivi kwamba alichochewa kukomesha mateso yao. (Mathayo 14:14) Alijali hisia zao na mahitaji yao, kwa hiyo, alitumia nguvu zake kwa upendo. Kisa kimoja chenye kugusa moyo kinasimuliwa kwenye Marko 7:31-37.
19 Pindi hiyo, umati mkubwa ulimfikia Yesu na kumletea wagonjwa wengi, naye akawaponya wote. (Mathayo 15:29, 30) Lakini Yesu alimshughulikia mtu mmoja kwa njia ya pekee sana. Mtu huyo alikuwa kiziwi asiyeweza kuongea. Yaelekea Yesu alitambua wasiwasi au aibu ya mtu huyo. Hivyo kwa kuonyesha kwamba anamjali, Yesu alimpeleka faraghani, mbali na umati. Kisha Yesu akamwonyesha ishara fulani ili kumjulisha jambo ambalo alitaka kufanya. Alitia “vidole vyake ndani ya masikio ya yule mtu na, baada ya kutema mate, akamgusa ulimi wake.”c (Marko 7:33) Halafu, Yesu akatazama juu mbinguni na kutweta kwa sala. Ni kana kwamba alikuwa akimwambia mtu huyo, ‘Muujiza ninaotaka kukufanyia unategemea nguvu za Mungu.’ Hatimaye, Yesu akasema: “Funguka.” (Marko 7:34) Basi, akayaponya masikio yake, kisha mtu huyo akaanza kuongea kama kawaida.
20 Inagusa moyo kama nini kujua kwamba Yesu alijali hisia za wagonjwa hata ingawa aliwaponya kwa nguvu za Mungu! Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba Yehova amemchagua Mtawala mwenye kujali na mwenye huruma jinsi hiyo ili awe mtawala wa Ufalme wake wa Kimesiya?
Miujiza Ilionyesha Baraka Zitakazokuja
21, 22. (a) Miujiza ya Yesu ilionyesha nini? (b) Kwa kuwa Yesu anaweza kudhibiti nguvu za asili, tunaweza kutarajia nini wakati wa utawala wa Ufalme wake?
21 Miujiza ambayo Yesu alifanya duniani ilionyesha kwamba baraka nyingi ajabu zitaletwa na Ufalme wake. Katika ulimwengu mpya wa Mungu, Yesu atafanya tena miujiza—lakini ulimwenguni pote! Hebu chunguza baadhi ya mataraja yenye kufurahisha ya wakati ujao.
22 Yesu atarudisha uhusiano mzuri kati ya viumbe na mazingira. Kumbuka kwamba alionyesha uwezo wake wa kudhibiti nguvu za asili kwa kutuliza dhoruba kali. Basi, hapana shaka kwamba wakati wa utawala wa Ufalme wa Kristo, wanadamu hawatahitaji kuogopa vimbunga, matetemeko ya ardhi, volkeno, au misiba mingine ya asili. Kwa kuwa Yesu ni Stadi wa Kazi aliyetumiwa na Yehova kuumba dunia na viumbe wote, anaelewa kabisa maumbile ya dunia. Anajua jinsi ya kutumia ifaavyo rasilimali za dunia. Wakati wa utawala wake, dunia nzima itakuwa Paradiso.—Luka 23:43.
23. Akiwa Mfalme, Yesu atatoshelezaje mahitaji ya wanadamu?
23 Vipi mahitaji ya wanadamu? Uwezo wa Yesu wa kulisha maelfu ya watu kwa vyakula vichache tu unatuhakikishia kwamba utawala wake utakomesha kabisa njaa. Kwa kweli, njaa itakoma milele kwa sababu kila mtu atakuwa na chakula cha kutosha. (Zaburi 72:16) Uwezo wa Yesu wa kuponya waonyesha kwamba wagonjwa, vipofu, viziwi, na walemavu hawatakuwa wagonjwa tena kamwe. (Isaya 33:24; 35:5, 6) Uwezo wake wa kufufua wafu unatuhakikishia kwamba akiwa Mfalme wa mbinguni ana nguvu za kufufua mamilioni ya watu ambao Baba yake anawakumbuka.—Yohana 5:28, 29.
24. Tunapotafakari juu ya nguvu za Yesu, tukumbuke nini, na kwa nini?
24 Tunapotafakari juu ya nguvu za Yesu, tukumbuke kwamba Mwana huyo humwiga kikamili Baba yake. (Yohana 14:9) Kwa hivyo, jinsi Yesu anavyotumia nguvu zake kunatuonyesha waziwazi jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo Yesu alimponya kwa fadhili mtu fulani mwenye ukoma. Yesu alimsikitikia mtu huyo, akamgusa na kusema: “Mimi nataka.” (Marko 1:40-42) Kupitia masimulizi kama hayo, ni kana kwamba Yehova anasema, ‘Hivyo ndivyo ninavyotumia nguvu zangu!’ Je, wewe huchochewi kumsifu Mungu wetu mweza yote na kushukuru kwa sababu anatumia nguvu zake kwa upendo?
a Bahari ya Galilaya hupata dhoruba za ghafula mara nyingi. Kwa sababu bahari hiyo iko chini sana (meta 200 chini ya usawa wa bahari), eneo hilo lina joto kuliko maeneo ya karibu, kwa hiyo, hali ya hewa hubadilika ghafula. Pepo kali sana huvuma kwenye Bonde la Yordani kutoka kwenye Mlima Hermoni ulio upande wa kaskazini. Dhoruba kali inaweza kutokea ghafula na kuvuruga bahari.
b Isitoshe, nyakati nyingine Vitabu vya Injili hutaja miujiza mingi kwa ujumla. Kwa mfano, pindi moja “jiji lote” lilikuja kumwona, naye akaponya wagonjwa “wengi.”—Marko 1:32-34.
c Kutema mate kulikuwa njia au ishara ya kuponya iliyokubaliwa na Wayahudi na Wasio Wayahudi. Na maandishi ya marabi yanataja tiba ya kutumia mate. Huenda Yesu alitema mate ili kumjulisha mtu huyo kwamba alitaka kumponya. Vyovyote iwavyo, Yesu hakuwa akitumia mate yake kama dawa ya asili.
-
-
“Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia UwezoMkaribie Yehova
-
-
Sura ya 10
“Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Uwezo
1. Wanadamu wasiokamilika hutumbukia kwa urahisi katika mtego gani?
“PALIPO na uwezo hapakosi mtego.” Maneno hayo yaliyosemwa na mtungaji-mashairi wa karne ya 19 yanaonyesha hatari ya kutumia uwezo vibaya. Inasikitisha kwamba wanadamu wasiokamilika hutumbukia kwa urahisi katika mtego huo. Kwa kweli, katika muda wote wa historia ya mwanadamu, ‘mtu mmoja amekuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Wanadamu wameteseka sana kwa sababu ya kutawaliwa na watawala wasio na upendo.
2, 3. (a) Ni nini kinachostaajabisha kuhusu jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake? (b) Twaweza kuwa na uwezo gani, nasi twapaswa kutumiaje uwezo huo wote?
2 Hata hivyo, je, haistaajabishi kwamba Yehova Mungu hatumii kamwe vibaya nguvu zake zisizo na mipaka? Kama tulivyoona kwenye sura zilizotangulia, sikuzote yeye hutumia nguvu zake kupatana na makusudi yake ya upendo, iwe ni nguvu za uumbaji, za kuharibu, kulinda, au za kufanya hali upya. Tunapotafakari jinsi anavyotumia nguvu zake, tunachochewa kumkaribia. Na hilo linatutia moyo ‘tumwige Mungu’ tunapotumia uwezo tulio nao. (Waefeso 5:1) Lakini sisi wanadamu duni tuna uwezo gani?
3 Kumbuka kwamba mwanadamu aliumbwa kwa sura na “mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:26, 27) Hivyo basi, hata sisi tuna uwezo, angalau kwa kadiri fulani. Twaweza kutimiza mambo kwa kufanya kazi; kuwa na mamlaka juu ya wengine; kuwa na uvutano juu ya wengine, hasa wale wanaotupenda; pia tunaweza kuwa na nguvu ya kimwili; au uwezo wa kifedha. Mtunga-zaburi alisema hivi kumhusu Yehova: “Wewe ndiwe asili ya uhai.” (Zaburi 36:9, BHN) Kwa hiyo, kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja, Mungu ndiye chanzo cha uwezo wowote ufaao ambao huenda tukawa nao. Kwa hiyo, tunataka kutumia uwezo wetu katika njia zinazompendeza. Tutafanyaje hivyo?
Upendo Ni Muhimu
4, 5. (a) Tunahitaji sifa gani muhimu ili kutumia uwezo kwa njia ifaayo, na kielelezo cha Mungu kinaonyeshaje hivyo? (b) Upendo utatusaidiaje kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo?
4 Upendo ni muhimu ili kutumia uwezo kwa njia ifaayo. Je, kielelezo cha Mungu hakionyeshi hivyo? Kumbuka Sura ya 1 iliyozungumzia sifa nne kuu za Mungu, yaani, nguvu, haki, hekima na upendo. Kati ya sifa hizo nne ni ipi iliyo kuu zaidi? Upendo. Andiko la 1 Yohana 4:8 lasema kwamba “Mungu ni upendo.” Naam, upendo ni utu wa Yehova; unamwongoza katika kila jambo analotenda. Kwa hiyo, kila jambo analotenda kwa nguvu zake linachochewa na upendo na mwishowe huwafaidi wale wanaompenda.
5 Upendo utatusaidia pia kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo. Kwani, Biblia hutuambia kwamba upendo ni “wenye fadhili” na “hautafuti masilahi yao wenyewe.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Kwa hiyo, tukiwa na upendo hatutakuwa wakali au wakatili kwa wale walio chini ya mamlaka yetu. Badala yake, tutawatendea wengine kwa staha na kutanguliza mahitaji na hisia zao wala si zetu.—Wafilipi 2:3, 4.
6, 7. (a) Kumhofu Mungu kwamaanisha nini, na sifa hiyo itatusaidiaje kuepuka kutumia uwezo vibaya? (b) Simulia mfano ambao unaonyesha uhusiano uliopo kati ya kumpenda Mungu na hofu ya kutompendeza.
6 Upendo unahusiana na sifa nyingine ambayo inaweza kutusaidia kuepuka kutumia uwezo wetu vibaya: kumhofu Mungu. Sifa hii ni muhimu jinsi gani? Andiko la Mithali 16:6 lasema: “Kwa kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA watu hujiepusha na maovu.” Bila shaka kutumia uwezo vibaya ni miongoni mwa mambo maovu ambayo tunapaswa kuepuka. Kumhofu Mungu kutatuzuia kuwakandamiza wale walio chini ya mamlaka yetu. Kwa nini? Kwanza, tunajua kwamba tunawajibika kwa Mungu kwa sababu ya jinsi tunavyowatendea wengine. (Nehemia 5:1-7, 15) Lakini kumhofu Mungu kwatia ndani mambo mengi zaidi. Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “hofu” mara nyingi humaanisha staha nyingi sana na kicho kwa Mungu. Basi, Biblia inaonyesha kwamba hofu inahusiana na kumpenda Mungu. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Staha hiyo yenye kicho inatia ndani hofu inayofaa ya kutompendeza Mungu—si kwa sababu tu tunahofu kuadhibiwa bali kwa sababu tunampenda kikweli.
7 Kwa mfano: Fikiria uhusiano mzuri uliopo kati ya mvulana mdogo na baba yake. Mvulana huyo anajua kwamba baba yake anampenda sana naye humtendea kwa fadhili. Lakini anajua pia mambo ambayo baba yake anamtarajia afanye, na anajua kwamba atatiwa nidhamu akikosa adabu. Mvulana huyo hana hofu isiyofaa kumwelekea baba yake. Badala yake, anampenda sana baba yake. Anapenda kufanya mambo ambayo yatamfurahisha baba yake. Ndivyo ilivyo na kumhofu Mungu. Kwa sababu tunampenda Yehova, Baba yetu wa mbinguni, tunaogopa kutenda jambo lolote ambalo ‘litamhuzunisha moyo.’ (Mwanzo 6:6) Badala yake, tunataka sana kuufurahisha moyo wake. (Mithali 27:11) Ndiyo sababu tunataka kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo. Na tuchunguze jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.
Katika Familia
8. (a) Waume wana mamlaka gani katika familia, na wanapaswa kuitumiaje? (b) Mume anawezaje kuonyesha kwamba anamheshimu mkewe?
8 Fikiria kwanza familia. Andiko la Waefeso 5:23 lasema kwamba “mume ni kichwa cha mke wake.” Mume anapaswa kutumiaje mamlaka aliyopewa na Mungu? Biblia inawaambia waume wakae na wake zao ‘kulingana na ujuzi, wakiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi.’ (1 Petro 3:7) Nomino ya Kigiriki inayotafsiriwa “heshima” yamaanisha “thamani, ubora, . . . staha.” Neno hilo hutafsiriwa pia “zawadi” na “-enye bei.” (Matendo 28:10; 1 Petro 2:7) Mume anayemheshimu mkewe hawezi kamwe kumpiga; wala hawezi kumwaibisha au kumtukana, na kumfanya ajihisi hafai. Badala yake, anatambua kwamba yeye ni mwenye thamani sana na anamtendea kwa heshima. Anaonyesha kwa maneno na matendo kwamba anamthamini sana mkewe iwe faraghani au mbele ya watu. (Mithali 31:28) Mume kama huyo hupendwa na kuheshimiwa na mkewe, na la muhimu hata zaidi ni kwamba anapata kibali cha Mungu.
Waume na wake wanatumia uwezo wao kwa njia inayofaa kwa kuonyeshana upendo na heshima
9. (a) Wake wana uwezo gani katika familia? (b) Ni nini kinachoweza kumsaidia mke atumie vipawa vyake kumwunga mkono mumewe, na matokeo yatakuwa nini?
9 Wake pia wana uwezo fulani katika familia. Biblia hutaja wanawake fulani waliomhofu Mungu ambao walichukua hatua ya kuwasaidia waume zao kufanya maamuzi yanayofaa, au kuwasaidia kuepuka kufanya maamuzi yasiyofaa bila kudharau ukichwa wao. (Mwanzo 21:9-12; 27:46–28:2) Mke anaweza kuwa na akili nyingi kumshinda mumewe, au anaweza kuwa na vipawa vingine ambavyo mumewe hana. Hata hivyo, anahitaji “kuwa na staha yenye kina kirefu” kwa mume wake na ‘kujitiisha’ kwake “kama kwa Bwana.” (Waefeso 5:22, 33) Mke aliye na lengo la kumpendeza Mungu atatumia vipawa vyake kumwunga mkono mumewe, badala ya kumdharau au kujaribu kumtawala. “Mwanamke mwenye hekima ” kama huyo hushirikiana kabisa na mumewe kujenga familia. Kwa kufanya hivyo anakuwa na amani pamoja na Mungu.—Mithali 14:1, BHN.
10. (a) Mungu amewapa wazazi mamlaka gani? (b) Neno “nidhamu” linamaanisha nini, na inapasa kutolewaje? (Ona pia kielezi-chini.)
10 Wazazi pia wamepewa mamlaka na Mungu. Biblia inashauri hivi: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Katika Biblia, neno “nidhamu” linaweza kumaanisha “malezi, mazoezi, mafundisho.” Watoto wanahitaji nidhamu; wanafurahi na kufanikiwa wanapopewa maagizo yaliyo wazi, na wanapowekewa mipaka na vizuizi. Kulingana na Biblia, nidhamu au mafundisho huhusisha upendo. (Mithali 13:24) Kwa hiyo, “fimbo ya adhabu” haipaswi kamwe kuwaumiza watoto kihisia-moyo au kimwili.a (Mithali 22:15; 29:15) Mzazi anayetoa nidhamu kwa ukali bila upendo anatumia vibaya mamlaka yake. Kufanya hivyo kunaweza kumvunja moyo mtoto. (Wakolosai 3:21) Kwa upande mwingine, kutoa nidhamu kwa usawaziko na kwa njia ifaayo kunawathibitishia watoto kwamba wazazi wanawapenda na wanapendezwa na utu wanaositawisha.
11. Watoto wanawezaje kutumia nguvu zao ifaavyo?
11 Vipi watoto? Wanawezaje kutumia ifaavyo nguvu zao? Mithali 20:29 yasema kwamba “fahari ya vijana ni nguvu zao.” Kwa kweli, hakuna njia nyingine bora zaidi ya vijana kutumia nguvu na nishati yao isipokuwa kumtumikia ‘Muumba wetu Mtukufu.’ (Mhubiri 12:1, NW) Vijana wanapaswa kukumbuka kwamba matendo yao yanaweza kuathiri hisia za wazazi wao. (Mithali 23:24, 25) Watoto wanapotii na kufuata mwenendo unaofaa, wanafurahisha mioyo ya wazazi wao wanaomhofu Mungu. (Waefeso 6:1) Mwenendo huo ‘unapendeza vema katika Bwana.’—Wakolosai 3:20.
Kutanikoni
12, 13. (a) Wazee wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mamlaka yao kutanikoni? (b) Toa mfano ambao unaonyesha umuhimu wa wazee kuwatendea kondoo kwa fadhili.
12 Yehova ameweka waangalizi wa kuongoza kutaniko la Kikristo. (Waebrania 13:17) Wanaume hao wenye sifa za kustahili wanapaswa kutumia mamlaka waliyopewa na Mungu kutoa msaada unaohitajiwa na kulisaidia kutaniko likue kiroho. Je, wazee wana haki ya kupiga ubwana juu ya waamini wenzao kwa sababu ya wadhifa wao? La hasha! Wazee wanahitaji kuwa na usawaziko na unyenyekevu wanapotimiza daraka lao kutanikoni. (1 Petro 5:2, 3) Biblia inawaambia hivi waangalizi: ‘Lichungeni kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.’ (Matendo 20:28) Kwa sababu hiyo, wazee wanapaswa kumtendea kila mshiriki wa kutaniko kwa fadhili.
13 Mfano ufuatao unaonyesha jambo hilo: Rafiki yako mpendwa anakuomba umtunzie mali fulani yenye thamani kubwa. Wajua kwamba mali hiyo ilimgharimu pesa nyingi sana. Je, hutaitunza kwa tahadhari na uangalifu mkubwa mno ili isiharibike? Vivyo hivyo, Mungu amewakabidhi wazee wajibu wa kutunza mali yenye thamani kubwa sana: kutaniko, ambalo washiriki wake wanalinganishwa na kondoo. (Yohana 21:16, 17) Yehova anapenda sana kondoo wake—anawapenda kiasi cha kwamba aliwanunua kwa damu yenye thamani ya Mwana wake mzaliwa-pekee, Yesu Kristo. Yehova aliwanunua kondoo wake kwa bei ya juu sana. Wazee wanyenyekevu hukumbuka jambo hilo na kuwatendea kondoo wa Yehova kwa njia inayofaa.
“Uwezo wa Ulimi”
14. Ulimi una uwezo gani?
14 Biblia inasema kwamba “mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Kwa kweli, ulimi unaweza kusababisha madhara makubwa sana. Ni nani kati yetu hajapata kuumizwa moyoni na maneno ya madharau au yaliyonenwa bila kufikiri? Lakini ulimi unaweza pia kujenga. Mithali 12:18 yasema kwamba “ulimi wa mwenye haki ni afya.” Naam, maneno yenye kutia moyo na yenye kujenga yanaweza kufariji na kutuliza moyo kama dawa. Angalia mifano kadhaa.
15, 16. Tunawezaje kutumia ulimi wetu kuwatia moyo wengine?
15 Andiko la 1 Wathesalonike 5:14 linasihi hivi: “Semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.” Naam, hata watumishi waaminifu wa Yehova wanaweza kushuka moyo nyakati nyingine. Tunawezaje kuwasaidia watu hao? Toa pongezi hususa na ya kutoka moyoni ili watambue kwamba wanathaminiwa sana na Yehova. Wasomee maandiko ya Biblia yenye kuimarisha sana yanayoonyesha kwamba Yehova anawapenda na anawajali kikweli wale “waliovunjika moyo” na “waliopondeka roho.” (Zaburi 34:18) Tunapotumia uwezo wa ulimi kuwafariji wengine, tunaonyesha kwamba tunamwiga Mungu wetu mwenye rehema, “ambaye hufariji walioshuka moyo.”—2 Wakorintho 7:6, New American Standard Bible.
16 Tunaweza pia kutumia uwezo wetu wa ulimi kuwatia moyo wengine wanaohitaji sana kitia-moyo. Je, mwamini mwenzetu amefiwa na mpendwa wake? Tunaweza kumfariji aliyefiwa kwa kuzungumza naye kwa huruma na kumwonyesha kwamba tunamjali na tunamhangaikia. Je, kuna ndugu au dada mzee kwa umri ambaye anahisi kwamba hafai? Tunaweza kuwahakikishia wale walio wazee kwa umri kwamba wanathaminiwa sana kwa kuwaambia maneno yenye kujenga. Je, kuna mtu anayepambana na ugonjwa wa kudumu? Tunaweza kumtia moyo mgonjwa huyo kwa kuzungumza naye kwa fadhili tunapomtembelea au kumpigia simu. Muumba wetu hufurahi kama nini kuona tukitumia uwezo wa ulimi kusema mambo ‘yaliyo mema kwa ajili ya kujenga’!—Waefeso 4:29.
Kuhubiri habari njema—ni njia bora ya kutumia uwezo wetu
17. Tunaweza kutumia ulimi wetu kuwafaidi wengine kwa njia gani bora zaidi, na kwa nini tufanye hivyo?
17 Njia bora zaidi ya kutumia uwezo wa ulimi ni kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Mithali 3:27 yasema hivi: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” Tuna wajibu wa kuwaeleza wengine habari njema zinazookoa uhai. Ni kosa kuwanyima wengine ujumbe huo muhimu sana ambao Yehova ametupatia kwa ukarimu. (1 Wakorintho 9:16, 22) Lakini Yehova anataka tushiriki kwa kadiri gani katika kazi hiyo?
Kumtumikia Yehova kwa ‘Nguvu Zetu Zote’
18. Yehova anataka tufanye nini?
18 Upendo wetu kwa Yehova hutuchochea kushiriki kikamili zaidi katika huduma ya Kikristo. Yehova anataka tushiriki kwa kadiri gani katika huduma hiyo? Anataka tufanye yote tuwezayo haidhuru hali yetu maishani: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.” (Wakolosai 3:23) Yesu alisema kwamba amri kuu kupita zote ni hii: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Ndiyo, Yehova anataka kila mmoja wetu ampende na kumtumikia kwa nafsi yote.
19, 20. (a) Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? (b) Yamaanisha nini kumtumikia Yehova kwa nafsi yote?
19 Yamaanisha nini kumtumikia Mungu kwa nafsi yote? Nafsi ni mtu mwenyewe, akiwa na uwezo wake wote wa kimwili na kiakili. Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? Fikiria mfano mmoja. Katika nyakati za Biblia, mtu angeweza kujiuza (nafsi yake) na kuwa mtumwa. Lakini, huenda mtumwa asimtumikie bwana wake kwa moyo wake wote; huenda asitumie nguvu zake zote au uwezo wake wote wa akili kutunza masilahi ya bwana wake. (Wakolosai 3:22) Kwa hiyo, ni wazi kwamba Yesu alitaja moyo, akili, na nguvu ili kukazia kwamba tunapaswa kumtumikia Mungu kwa uwezo wetu wote. Kumtumikia Mungu kwa nafsi yote kwamaanisha kujitoa wenyewe, kutumia nguvu na nishati yetu yote katika utumishi wake.
20 Je, kutumikia kwa nafsi yote kwamaanisha kwamba ni lazima sote tutumie kiasi kilekile cha wakati na nishati katika huduma? Hilo haliwezekani, kwa kuwa sote tuna hali na uwezo mbalimbali. Kwa mfano, kijana mwenye nguvu na afya njema anaweza kuhubiri kwa saa nyingi zaidi kuliko mzee aliye dhaifu. Mseja asiye na wajibu wa familia anaweza kutimiza mengi zaidi kuliko mtu mwenye familia. Tunapaswa kushukuru sana ikiwa hali na nguvu zetu zinaturuhusu kufanya mengi katika huduma. Bila shaka, hatutaki kamwe kuwachambua-chambua wengine, wala kulinganisha utumishi wetu na wao. (Waroma 14:10-12) Badala yake, tunataka kutumia uwezo wetu kuwatia moyo wengine.
21. Ni njia ipi iliyo bora kabisa na muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu?
21 Yehova ametuwekea kielelezo bora kabisa cha kutumia uwezo kwa njia ifaayo. Tunataka kumwiga yeye kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasiokamilika. Tunaweza kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo kwa kuwatendea kwa heshima wale walio chini ya mamlaka yetu. Zaidi ya hayo, tunataka kutimiza kwa nafsi yote kazi ya kuhubiri inayookoa uhai ambayo Yehova ametukabidhi. (Waroma 10:13, 14) Kumbuka kwamba Yehova anafurahi unapomtolea yaliyo bora kabisa kulingana na uwezo wako. Je, huchochewi na moyo kutaka kumtumikia Mungu huyo mwenye kujali na mwenye upendo kulingana na uwezo wako? Hiyo ndiyo njia bora kabisa au muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu.
a Katika nyakati za Biblia, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fimbo” lilimaanisha kijiti au gongo kama lile lililotumiwa na mchungaji kuwaongoza kondoo. (Zaburi 23:4) Vivyo hivyo, “fimbo” ya mamlaka ya wazazi inaonyesha mwongozo wa upendo, wala si adhabu kali au ya kikatili.
-
-
“Njia Zake Zote Ni Haki”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 11
“Njia Zake Zote Ni Haki”
1, 2. (a) Yosefu alikumbwa na ukosefu upi mkubwa wa haki? (b) Yehova alikomeshaje ukosefu huo wa haki?
MWANAMUME fulani kijana mwenye sura nzuri alitendewa isivyo haki kabisa, hakuwa amefanya uhalifu wowote, lakini alitiwa gerezani kwa mashtaka ya uwongo ya kujaribu kumbaka mwanamke. Alitendewa isivyo haki pindi nyingine pia. Miaka mingi mapema, kijana huyo aitwaye Yosefu, akiwa na umri wa miaka 17, alisalitiwa na ndugu zake ambao nusura wamwue. Aliuzwa utumwani katika nchi ya kigeni. Akiwa huko alikataa kutongozwa na mke wa bwana wake. Mwanamke huyo alimsingizia Yosefu kwa mashtaka ya uwongo, ndipo Yosefu akatiwa gerezani. Kwa kusikitisha, ilionekana kwamba hakukuwa na mtu yeyote wa kumtetea Yosefu.
Yosefu aliteseka isivyo haki “gerezani”
2 Hata hivyo, Mungu ambaye ‘anapenda uadilifu na haki’ alikuwa akitazama. (Zaburi 33:5, BHN) Yehova alichukua hatua ya kukomesha ukosefu huo wa haki, aliingilia mambo na mwishowe Yosefu akaachiliwa. Isitoshe, Yosefu—aliyekuwa ametiwa “gerezani”—hatimaye alipewa cheo cha juu sana na heshima ya pekee. (Mwanzo 40:15; 41:41-43; Zaburi 105:17, 18) Mwishowe, mashtaka hayo ya uwongo yalifutiliwa mbali na Yosefu akatumia cheo chake cha juu kuendeleza kusudi la Mungu.—Mwanzo 45:5-8.
3. Kwa nini haishangazi kwamba sote hutamani kutendewa kwa haki?
3 Simulizi hilo linatugusa moyo, sivyo? Sote tumepata kutendewa isivyo haki au kuona mwingine akitendewa isivyo haki. Bila shaka, sote hutamani kutendewa kwa haki, bila uonevu. Hilo halishangazi, kwa kuwa Yehova alituumba tukiwa na sifa kama zake, na haki ni mojawapo ya sifa zake kuu. (Mwanzo 1:27) Ili kumjua Yehova vyema, tunahitaji kuelewa sifa yake ya haki. Ndipo tutakapothamini hata zaidi matendo yake ya ajabu na kuchochewa kumkaribia zaidi.
Haki Ni Nini?
4. Kwa kawaida wanadamu huelewaje haki?
4 Kwa kawaida, wanadamu huelewa haki kuwa utekelezaji wa sheria bila upendeleo. Kitabu Right and Reason—Ethics in Theory and Practice chasema kwamba ‘haki inahusiana na sheria, wajibu, haki za watu, na madaraka, nayo hutekelezwa bila kupendelea na kwa yule anayestahili.’ Hata hivyo, Yehova hatekelezi haki kwa kushikilia tu sheria bila kujali ili kutimiza tu wajibu.
5, 6. (a) Maneno ya lugha ya awali yanayotafsiriwa “haki” yanamaanisha nini? (b) Mungu ni mwenye haki katika maana gani?
5 Tunaweza kuelewa kwa undani haki ya Yehova kwa kuchunguza maneno ya lugha za awali yaliyotumiwa katika Biblia. Katika Maandiko ya Kiebrania, maneno matatu muhimu yanatumiwa. Neno ambalo mara nyingi hutafsiriwa “haki” laweza pia kumaanisha “yaliyo sawa.” (Mwanzo 18:25, BHN) Maneno mawili yanayosalia hutafsiriwa kwa kawaida kuwa “uadilifu.” Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno linalotafsiriwa “uadilifu” linafafanuliwa kuwa “sifa ya kuwa sawa au mwenye haki.” Hivyo basi, hakuna tofauti kati ya uadilifu na haki.—Amosi 5:24, BHN.
6 Basi, Biblia inaposema kwamba Mungu ni mwenye haki, inamaanisha kwamba sikuzote yeye hutenda yaliyo sawa bila kupendelea, na bila ubaguzi. (Waroma 2:11) Kwa kweli, Mungu hawezi kamwe kutenda isivyo haki. Elihu aliyekuwa mwaminifu alisema hivi: “Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu; wala Mwenyezi kufanya uovu.” (Ayubu 34:10) Ni kweli kwamba Yehova hawezi kamwe “kutenda udhalimu.” Kwa nini? Kwa sababu mbili muhimu.
7, 8. (a) Kwa nini Yehova hawezi kutenda isivyo haki? (b) Ni nini kinachomchochea Yehova atende kwa uadilifu, au kwa haki?
7 Kwanza, yeye ni mtakatifu. Kama tulivyoona kwenye Sura ya 3, Yehova ni mtakatifu na mwadilifu kabisa. Kwa hiyo, hawezi kutenda uovu au kutenda isivyo haki. Fikiria maana yake. Tunasadiki kabisa kwamba Baba yetu wa mbinguni hawezi kamwe kuwatesa watoto wake kwa sababu yeye ni mtakatifu. Yesu alisadiki vivyo hivyo. Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, alisali hivi: “Baba Mtakatifu, walinde [wanafunzi] kwa sababu ya jina lako mwenyewe.” (Yohana 17:11) Katika Maandiko, usemi “Baba Mtakatifu” humhusu Yehova peke yake. Usemi huo unafaa kwa sababu hakuna baba yeyote wa kibinadamu aliye mtakatifu kama Yehova. Yesu aliamini kabisa kwamba wanafunzi wake wangelindwa na Baba yake, ambaye ni mtakatifu na asiye na dhambi yoyote.—Mathayo 23:9.
8 Pili, upendo usio wa ubinafsi ni sifa kuu ya utu wa Mungu. Upendo huo humchochea kuwatendea wengine kwa uadilifu au haki. Lakini ukosefu mwingi wa haki—kutia ndani ukabila, ubaguzi wa rangi, na kupendelea—mara nyingi husababishwa na pupa na ubinafsi, mambo ambayo ni kinyume cha upendo. Biblia inatuhakikishia hivi kumhusu Mungu huyo mwenye upendo: “BWANA ndiye mwenye haki, apenda matendo ya haki.” (Zaburi 11:7) Yehova asema hivi kujihusu: “Mimi, BWANA, naipenda hukumu ya haki.” (Isaya 61:8) Bila shaka inatia moyo kujua kwamba Mungu wetu anapenda kutenda yaliyo sawa, au yaliyo haki.—Yeremia 9:24.
Rehema na Haki Kamilifu ya Yehova
9-11. (a) Kuna uhusiano gani kati ya haki ya Yehova na rehema yake? (b)Yehova anaonyeshaje haki na rehema anaposhughulika na wanadamu wenye dhambi?
9 Haki ya Yehova, kama sifa nyinginezo za utu wake usio na kifani, ni kamilifu, haijapungukiwa kwa vyovyote. Musa alimtukuza Yehova kwa kuandika hivi: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:3, 4) Yehova hutenda kwa haki kamilifu—yeye si mpole mno wala si mkali mno.
10 Haki ya Yehova inahusiana sana na rehema yake. Zaburi 116:5 yasema: “BWANA ni mwenye neema na haki, naam, Mungu wetu ni mwenye rehema.” Ndiyo, Yehova ni mwenye haki na mwenye rehema. Sifa hizo mbili hazipingani. Haki ya Yehova haiwezi kupita kiasi, kwa hivyo haonyeshi rehema ili kusawazisha haki yake. Badala yake, mara nyingi yeye huonyesha sifa hizo pamoja. Ona mfano ufuatao.
11 Wanadamu wote wamerithi dhambi na hivyo wanastahili kupata mshahara wa dhambi, yaani, kifo. (Waroma 5:12) Lakini Yehova hafurahii watenda-dhambi wakifa. Yeye ni ‘Mungu, aliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi.’ (Nehemia 9:17) Hata hivyo, kwa kuwa yeye ni mtakatifu, hawezi kupuuza tu uovu. Basi, angewezaje kuwaonyesha rehema wanadamu ambao wamerithi dhambi? Jibu linapatikana katika mojawapo ya kweli muhimu zinazopatikana katika Neno la Mungu: mpango wa Yehova wa kuwaokoa wanadamu kupitia fidia. Katika Sura ya 14 tutajifunza mengi zaidi kuhusu mpango huo wa upendo. Mpango huo unaonyesha haki na rehema ya pekee sana. Kupitia mpango huo, Yehova anaweza kuwaonyesha watenda-dhambi wanaotubu rehema yenye fadhili huku akidumisha kanuni zake za haki kamilifu.—Waroma 3:21-26.
Haki ya Yehova Inachangamsha Moyo
12, 13. (a) Kwa nini haki ya Yehova inatuvuta kwake? (b) Daudi alifikia mkataa gani kuhusu haki ya Yehova, na hilo linawezaje kututia moyo?
12 Haki ya Yehova si sifa inayochukiza, bali ni sifa ya kupendeza inayotuvuta kwake. Biblia inaeleza waziwazi kwamba haki au uadilifu wa Yehova unaambatana na huruma. Hebu tuchunguze baadhi ya njia za Yehova za haki zinazochangamsha moyo.
13 Haki kamilifu ya Yehova humchochea kuonyesha uaminifu na ushikamanifu kwa watumishi wake. Mtunga-zaburi Daudi alipata kuelewa na kuthamini wonyesho huo wa haki ya Yehova maishani mwake. Daudi alifikia mkataa gani kutokana na mambo yaliyompata na yale aliyojifunza kuhusu njia za Yehova za kufanya mambo? Alitangaza hivi: “BWANA hupenda haki, wala hawaachi watauwa wake. Wao hulindwa milele.” (Zaburi 37:28) Ahadi hiyo inatia moyo kama nini! Mungu wetu hatawaacha kamwe wale walio waaminifu kwake. Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatutunza kwa upendo na hatatuacha kamwe. Jambo hilo ni hakika kwa sababu yeye ni mwenye haki!—Mithali 2:7, 8.
14. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli inaonyeshaje kwamba anawajali wanaotaabika?
14 Mungu huzingatia mahitaji ya wale wanaotaabika kwa sababu yeye ni mwenye haki. Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli inaonyesha kwamba anawajali wanaotaabika. Kwa mfano, Sheria ilitaja mipango ya pekee ya kuhakikisha kwamba mayatima na wajane walitunzwa. (Kumbukumbu la Torati 24:17-21) Huku akitambua magumu ambayo yangekumba familia hizo, Yehova aliwajali akiwa Hakimu na Mlinzi wao, ambaye ‘anamfanyia yatima na mjane hukumu ya haki.’ (Kumbukumbu la Torati 10:18; Zaburi 68:5) Yehova aliwaonya Waisraeli kwamba endapo wangewatesa wanawake na watoto hao wasio na msaidizi, angesikia kilio chao pasina shaka yoyote. Alisema: “Hasira yangu itawaka moto.” (Kutoka 22:22-24) Ijapokuwa hasira si mojawapo ya sifa kuu za Yehova, hasira yake adilifu huwaka anapoona watu wa hali ya chini na wanyonge wakionewa kimakusudi.—Zaburi 103:6.
15, 16. Kuna uthibitisho gani wa pekee unaoonyesha kwamba Yehova hana upendeleo?
15 Yehova pia anatuhakikishia kwamba ‘hapendelei nyuso za watu, wala hakubali rushwa.’ (Kumbukumbu la Torati 10:17) Yehova si kama wanadamu wengi mashuhuri na wenye mamlaka ambao huangalia utajiri au sura ya mtu. Hana ubaguzi wala upendeleo wowote. Fikiria uthibitisho huu wa pekee ambao unaonyesha kwamba Yehova hana upendeleo. Hakuwapa watu wachache tu wenye elimu nafasi ya kuwa waabudu wake wa kweli wenye tumaini la kuishi milele. Badala yake, “katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Watu wote wanaweza kuwa na tumaini hilo zuri ajabu bila kujali wadhifa wao katika jamii, rangi yao, au nchi wanamoishi. Je, huo si uthibitisho bora kabisa wa haki ya kweli?
16 Tunastahili kufikiria na kuheshimu njia nyingine muhimu ambayo Yehova anaonyesha haki yake kamilifu: jinsi anavyoshughulika na wale wanaovunja kanuni zake za uadilifu.
Huwaadhibu Wenye Hatia
17. Eleza kwa nini maovu yaliyo ulimwenguni hayaonyeshi kwamba Yehova hatendi haki.
17 Huenda wengine wakauliza: ‘Kama Yehova hapuuzi uovu, kwa nini ufisadi na ukosefu wa haki unaosababisha kuteseka umeenea ulimwenguni leo?’ Maovu hayo hayaonyeshi kwa vyovyote kwamba Yehova hatendi haki. Ukosefu wa haki uliojaa katika ulimwengu huu mwovu umesababishwa na dhambi ambayo wanadamu wamerithi kutoka kwa Adamu. Ukosefu wa haki umeenea ulimwenguni kwa sababu wanadamu wasiokamilika wameamua kufuata njia zao wenyewe zenye dhambi. Lakini utakomeshwa hivi karibuni.—Kumbukumbu la Torati 32:5.
18, 19. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hatavumilia milele wale wanaovunja kimakusudi sheria zake adilifu?
18 Ijapokuwa Yehova huwarehemu kabisa wale wanaomkaribia kwa unyofu, hatavumilia milele hali inayoletea jina lake takatifu lawama. (Zaburi 74:10, 22, 23) Mungu mwenye haki hawezi kudhihakiwa; hawezi kuwalinda wale wanaotenda dhambi kimakusudi wasipate adhabu kali wanayostahili kwa sababu ya mwenendo wao. Yehova ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; . . . wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” (Kutoka 34:6, 7) Kwa kupatana na maneno hayo, nyakati nyingine imembidi Yehova kuwaadhibu wale wanaovunja kimakusudi sheria zake adilifu.
19 Kwa mfano, fikiria jinsi Mungu alivyoshughulika na Israeli la kale. Hata baada ya kumiliki Nchi ya Ahadi, Waisraeli waliasi tena na tena. Yehova hakuwatupilia mbali mara moja licha ya kwamba matendo yao maovu ‘yalimhuzunisha.’ (Zaburi 78:38-41) Badala yake, kwa rehema aliwapa nafasi ya kubadili mwenendo wao. Aliwasihi hivi: “Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu; bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?” (Ezekieli 33:11) Kwa sababu Yehova anathamini sana uhai, alituma manabii wake tena na tena ili Waisraeli waache njia zao mbaya. Lakini wengi wa watu hao wenye mioyo migumu walikataa kusikiliza na kutubu. Mwishowe, Yehova aliwatia mikononi mwa adui zao ili kutetea jina lake takatifu na kile kinachowakilishwa na jina hilo.—Nehemia 9:26-30.
20. (a) Twajifunza nini kumhusu Yehova kutokana na jinsi alivyoshughulika na Waisraeli? (b) Kwa nini simba ni mfano ufaao wa haki ya Yehova?
20 Tunajifunza mambo mengi kumhusu Yehova tunapochunguza jinsi alivyoshughulika na Waisraeli. Tunajifunza kwamba macho yake huona maovu yote nayo humhuzunisha sana. (Mithali 15:3) Pia, inatia moyo sana kujua kwamba yeye hujitahidi kuonyesha rehema inapofaa. Isitoshe, tunajifunza kwamba hatekelezi haki yake haraka-haraka. Kwa sababu ya subira na uvumilivu wa Yehova, watu wengi hufikiri kimakosa kwamba hatawaadhibu kamwe waovu. Lakini maoni hayo si kweli. Tunapofikiria jinsi Mungu alivyoshughulika na Waisraeli, tunajifunza kwamba subira yake ina mipaka. Yehova hutekeleza uadilifu kwa uthabiti. Tofauti na wanadamu, ambao mara nyingi huogopa kutenda haki, yeye hutetea kwa ujasiri yaliyo sawa. Kwa hiyo, simba ambaye anawakilisha haki ya kijasiri, anaonekana karibu na Mungu na kiti chake cha enzi.a (Ezekieli 1:10; Ufunuo 4:7) Kwa hiyo tunaweza kuwa na hakika kwamba atatimiza ahadi yake ya kukomesha ukosefu wa haki duniani. Naam, twaweza kusema hivi kwa ufupi kuhusu hukumu yake: Yehova hutekeleza hukumu yake kwa uthabiti inapohitajika na kwa rehema inapowezekana.—2 Petro 3:9.
Kumkaribia Mungu Mwenye Haki
21. Tunapotafakari jinsi Yehova anavyotekeleza haki yake, tunapaswa kumwonaje, na kwa nini?
21 Tunapotafakari jinsi Yehova anavyotekeleza haki, hatupaswi kumwona kama hakimu mkali asiye na hisia ambaye anapenda tu kuwahukumu watenda-maovu. Badala yake, tunapaswa kumwona kuwa Baba mwenye upendo, aliye thabiti, ambaye huwatunza watoto wake kwa njia bora kabisa. Akiwa Baba mwadilifu au mwenye haki, Yehova ni thabiti kwa mambo yaliyo sawa na vilevile huwaonyesha rehema nyororo watoto wake wa kidunia ambao wanahitaji msaada na msamaha wake.—Zaburi 103:10, 13.
22. Akiongozwa na haki yake, Yehova ametuwezesha kuwa na tumaini gani, na kwa nini anashughulika nasi kwa njia hiyo?
22 Tunashukuru kama nini kwamba haki ya Mungu haimaanishi kuwahukumu tu watenda-maovu! Akiongozwa na haki yake, Yehova ametuwezesha kuwa na tumaini lenye kusisimua sana—kuishi milele na kwa ukamilifu katika ulimwengu ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Mungu wetu anashughulika nasi kwa njia hiyo kwa sababu haki yake humchochea ajitahidi kuokoa badala ya kuhukumu. Kwa kweli, tunavutiwa kumkaribia Yehova tunapoelewa vyema haki yake! Katika sura zifuatazo, tutachunguza kwa undani zaidi jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo yenye kuvutia.
a Kwa kufaa, Yehova alijilinganisha na simba alipowahukumu Waisraeli wenye kuasi.—Yeremia 25:38; Hosea 5:14.
-
-
“Je, kwa Mungu Kuna Ukosefu wa Haki?”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 12
“Je, kwa Mungu Kuna Ukosefu wa Haki?”
1. Visa vya ukosefu wa haki vinaweza kutufanya tuhisije?
MJANE mmoja mzee aibiwa kwa ujanja pesa zote alizoweka akibani. Mtoto mchanga atupwa na mama yake asiye na huruma. Mwanamume fulani afungwa gerezani isivyo haki kwa shtaka la uhalifu. Unahisije kuhusu visa hivyo? Yaelekea kwamba kila kisa kinakuhuzunisha, na sababu ni wazi. Wanadamu wote wanatambua vyema mambo yaliyo sawa na yaliyo kosa. Tunakasirika tunapoona mtu akitendewa isivyo haki. Tunataka mtu huyo alipwe na mkosaji aadhibiwe. Haki isipotekelezwa, huenda tukajiuliza hivi: ‘Je, Mungu anaona yanayotukia? Mbona hachukui hatua?’
2. Habakuki alihisije kwa sababu ya ukosefu wa haki, na kwa nini Yehova hakumshutumu?
2 Katika historia yote, watumishi waaminifu wa Yehova wameuliza maswali kama hayo. Kwa mfano, nabii Habakuki alisali hivi kwa Mungu: “Kwa nini wanifanya nishuhudie ukosefu huu mbaya wa haki? Kwa nini unaruhusu jeuri, uasi-sheria, uhalifu na ukatili uenee kotekote?” (Habakuki 1:3, Contemporary English Version) Yehova hakumshutumu Habakuki kwa sababu ya kuuliza maswali hayo yaliyo wazi, kwa kuwa Ndiye aliyewaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuonyesha haki. Naam, Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kuonyesha kwa kadiri fulani haki yake kamilifu.
Yehova Anachukia Ukosefu wa Haki
3. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yehova anajua vyema ukosefu wa haki uliopo?
3 Yehova anajua kwamba kuna ukosefu wa haki. Anaona yanayotukia. Biblia yatuambia hivi kuhusu siku za Noa: “BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.” (Mwanzo 6:5) Fikiria maana ya maneno hayo. Mara nyingi, sisi hutambua kuna ukosefu wa haki baada ya kusikia visa kadhaa vya ukosefu wa haki au baada ya kutendewa isivyo haki. Kinyume chake, Yehova anaona ukosefu wote wa haki unaotukia ulimwenguni pote. Isitoshe, anaweza kutambua nia ya moyo—mawazo mapotovu yanayowafanya watu watende isivyo haki.—Yeremia 17:10.
4, 5. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba Yehova anawajali wanaotendewa isivyo haki? (b) Yehova alitendewaje isivyo haki?
4 Lakini Yehova haangalii tu ukosefu wa haki bila kuchukua hatua. Anawajali wale wanaoteseka kwa sababu ya kutendewa isivyo haki. Watu wake walipoteswa kikatili na mataifa adui, Yehova alihuzunika ‘kwa ajili ya kuugua kwao kwa sababu watu wale waliwaonea na kuwasumbua.’ (Waamuzi 2:18) Huenda umegundua kwamba watu fulani hawana huruma kwa sababu wameona visa vingi sana vya ukosefu wa haki. Lakini Yehova ni tofauti kabisa! Ameona ukosefu wa haki wa kila namna kwa miaka ipatayo 6,000, lakini bado unamchukiza. Isitoshe, Biblia inatuhakikishia kwamba mambo kama vile “ulimi wa uongo,” “mikono imwagayo damu isiyo na hatia,” na “shahidi wa uongo asemaye uongo,” yanamchukiza.—Mithali 6:16-19.
5 Fikiria pia jinsi Yehova alivyowashutumu vikali viongozi wasiofuata haki katika Israeli. Alimpulizia nabii wake kuwaambia hivi: “Nyinyi ndio mnaopaswa kujua mambo ya haki.” Baada ya kueleza waziwazi jinsi walivyotumia vibaya mamlaka yao, Yehova alitabiri mambo yatakayowapata watu hao wafisadi: ‘Watamlilia Mwenyezi-Mungu lakini yeye hatawajibu. Atauficha uso wake wakati huo, kwa sababu wamemtenda mambo maovu.’ (Mika 3:1-4, BHN) Yehova anachukia kabisa ukosefu wa haki kwa sababu yeye pia alitendewa isivyo haki! Kwa maelfu ya miaka, Shetani amekuwa akimlaumu Mungu isivyo haki. (Mithali 27:11) Isitoshe, Yehova aliathiriwa na tendo baya zaidi la ukosefu wa haki, wakati Mwanaye aliuawa kama mhalifu ingawa “hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:22; Isaya 53:9) Ni wazi kwamba Yehova hapuuzi wala kutojali mateso ya wale wanaotendewa isivyo haki.
6. Huenda tukahisije tunapotendewa isivyo haki, na kwa nini?
6 Licha ya hayo, tunapoona ukosefu wa haki—au tunapotendewa isivyo haki—kwa kawaida tunasononeka sana. Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, na ukosefu wa haki haupatani hata kidogo na utu wa Yehova. (Mwanzo 1:27) Basi, mbona Yehova anaruhusu ukosefu wa haki?
Suala la Enzi Kuu ya Mungu
7. Eleza jinsi enzi kuu ya Yehova ilivyotiliwa shaka.
7 Jibu la swali hilo linahusiana na suala la enzi kuu. Kama tulivyoona, Muumba ana haki ya kutawala dunia na wote wanaokaa humo. (Zaburi 24:1; Ufunuo 4:11) Hata hivyo, enzi kuu ya Yehova ilitiliwa shaka mapema katika historia ya wanadamu. Ilikuwaje? Yehova alimwamuru mwanadamu wa kwanza, Adamu, asile matunda ya mti fulani uliokuwa katika bustani ya Paradiso alimoishi. Ingekuwaje kama hangetii? Mungu alimwambia “utakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Amri ya Mungu haikumkandamiza Adamu au mkewe, Hawa. Hata hivyo, Shetani alimsadikisha Hawa kwamba Mungu alikuwa akiwawekea vizuizi vinavyopita kiasi. Hawa angepatwa na nini kama angekula kutokana na mti huo? Shetani alimwambia Hawa waziwazi: “Hakika hamtakufa, kwa maana Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:1-5.
8. (a) Mambo ambayo Shetani alimwambia Hawa yalidokeza nini? (b) Shetani alidai nini kuhusu enzi kuu ya Mungu?
8 Kwa kusema hivyo, Shetani alidokeza kwamba Yehova alimdanganya Hawa na vilevile alimnyima habari muhimu sana. Kwa tahadhari, Shetani hakupinga kwamba Mungu ndiye mtawala mwenye enzi kuu. Lakini alidai kwamba Mungu hakutawala kwa uadilifu wala hakuwa na haki ya kuwa mwenye enzi kuu. Yaani, alidai kwamba Yehova alikuwa akiwadhulumu raia wake na hakuwa akitawala kwa njia ya uadilifu.
9. (a) Adamu na Hawa walipatwa na nini kwa sababu ya kutotii, na hilo lilizusha maswali gani muhimu? (b) Kwa nini Yehova hakuwaangamiza waasi hao papo hapo?
9 Adamu na Hawa walimwasi Yehova wakala matunda ya mti uliokatazwa. Kwa sababu hawakutii, wangepokea adhabu ya kifo kama Mungu alivyokuwa amesema. Uwongo wa Shetani ulizusha maswali kadhaa muhimu. Je, kweli Yehova ana haki ya kutawala wanadamu, au wanadamu wanapaswa kujitawala? Je, Yehova anatawala kwa njia bora kabisa? Yehova angaliweza kuwaangamiza waasi hao papo hapo kwa kutumia nguvu zake kuu. Lakini masuala yaliyozushwa yalihusu utawala wa Mungu, wala si nguvu zake. Kwa hiyo, kumwangamiza Adamu, Hawa, na Shetani hakungethibitisha kwamba Mungu anatawala kwa uadilifu. Badala yake, huenda utawala wake ungetiliwa shaka hata zaidi. Njia pekee ya kujua iwapo wanadamu wangeweza kujitawala kwa mafanikio bila kumtegemea Mungu, ingekuwa ni kuwapa muda zaidi wa kuthibitisha madai hayo.
10. Historia imefunua nini kuhusu utawala wa wanadamu?
10 Historia imefunua nini? Kwa maelfu ya miaka, watu wamejaribu serikali nyingi mbalimbali, kama vile serikali za kimabavu, demokrasia, ujamaa na ukomunisti. Matokeo ya serikali hizo zote yanatajwa na maneno haya ya Biblia ambayo ni ya kweli: ‘Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Kwa kufaa, nabii Yeremia alisema hivi: “Ee, BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.
11. Kwa nini Yehova aliruhusu wanadamu wateseke?
11 Tangu mwanzoni, Yehova alijua kwamba wanadamu wangeteseka sana kwa sababu ya kujitegemea au kujitawala. Basi, je, alikosa haki kwa kuruhusu mateso hayo yaendelee? La hasha! Kwa mfano: Tuseme una mtoto anayehitaji kufanyiwa upasuaji ili kutibu ugonjwa hatari sana. Unahuzunika sana kwa sababu unatambua kwamba mtoto wako atateseka kwa kadiri fulani anapofanyiwa upasuaji. Lakini unajua pia kwamba upasuaji utamsaidia mtoto wako kuwa na afya bora baadaye. Vivyo hivyo, Mungu alijua—na hata alitabiri—kwamba utawala wa wanadamu ambao ameruhusu ungesababisha maumivu na mateso kwa kadiri fulani. (Mwanzo 3:16-19) Lakini alijua pia kwamba kitulizo cha kudumu na kinachofaa kingepatikana tu ikiwa angeacha wanadamu wote waone matokeo mabaya ya uasi. Hivyo suala la enzi kuu lingetatuliwa kabisa, kwa umilele wote.
Suala la Uaminifu wa Mwanadamu
12. Kama kisa cha Yobu kinavyoonyesha, Shetani ametoa shtaka gani dhidi ya wanadamu?
12 Kuna jambo jingine linalohusika. Alipodai kwamba Mungu hana haki ya kutawala na hatawali kwa uadilifu, Shetani hakusema tu uwongo kuhusu enzi kuu ya Yehova; alisema pia uwongo kuhusu uaminifu wa watumishi wa Mungu. Kwa mfano, angalia maneno ambayo Shetani alimwambia Yehova kuhusu yule mwanamume mwadilifu, Yobu: “Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi. Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.”—Ayubu 1:10, 11.
13. Shetani alidai nini alipomshtaki Yobu, na wanadamu wote wanahusikaje?
13 Shetani alidai kwamba Yehova alimhonga Yobu amtumikie kwa kumlinda kwa nguvu Zake. Na hilo lilimaanisha kwamba uaminifu wa Yobu ulikuwa wa kinafiki, na kwamba alimwabudu Mungu kwa ubinafsi tu. Shetani alidai kwamba Yobu angemkufuru Muumba wake kama hangebarikiwa. Shetani alijua kwamba Yobu alikuwa “mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu.”a Basi kama Shetani angeweza kuvunja uaminifu wa Yobu, yaelekea kwamba angeweza pia kuvunja uaminifu wa wanadamu wengine wote. Kwa hiyo, Shetani alikuwa akitilia shaka uaminifu wa wanadamu wote wanaotaka kumtumikia Mungu. Kwa kweli, Shetani alihusisha wengine katika suala hilo kwa kumwambia hivi Yehova: “Yote aliyo nayo mtu [si Yobu tu] atayatoa kwa ajili ya uhai wake.”—Ayubu 1:8; 2:4.
14. Historia imeonyesha nini kuhusu dai la Shetani dhidi ya wanadamu?
14 Historia imeonyesha kwamba dai la Shetani ni la uwongo kwa sababu wengi kama Yobu, wamedumisha uaminifu kwa Yehova wakati wa majaribu. Maisha yao ya uaminifu yamemfurahisha Yehova, na hivyo ameweza kumjibu Shetani aliyedai kwa kiburi kwamba wanadamu wataacha kumtumikia Mungu wakipata magumu. (Waebrania 11:4-38) Naam, watu waadilifu wamekataa kumpa Mungu kisogo. Hata wanapokumbwa na matatizo magumu sana, wamemtegemea hata zaidi Yehova ili awape nguvu za kuvumilia.—2 Wakorintho 4:7-10.
15. Ni swali gani linaloweza kuzuka kuhusu hukumu za Mungu za wakati uliopita na za wakati ujao?
15 Lakini Yehova huonyesha haki katika mambo mengine mbali na suala la enzi kuu na suala la uaminifu wa wanadamu. Biblia hutueleza jinsi Yehova alivyohukumu watu mmoja-mmoja na hata mataifa mazima. Pia ina unabii mbalimbali wa hukumu ambazo atatekeleza wakati ujao. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova amekuwa akihukumu kwa uadilifu na bado atahukumu kwa uadilifu wakati ujao?
Ubora wa Haki ya Mungu
Yehova ‘hataharibu kamwe mwenye haki pamoja na mwovu’
16, 17. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba wanadamu hawafahamu kikamili haki ya kweli?
16 Ni sahihi kusema hivi kumhusu Yehova: “Njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kudai hivyo, kwa kuwa mara nyingi tunashindwa kufahamu kikamili mambo yaliyo sawa. Kwa mfano, mfikirie Abrahamu. Alimsihi Yehova asiharibu Sodoma ingawa uovu ulikuwa umeenea sana. Alimwuliza Yehova hivi: “Je! Utaharibu mwenye haki pamoja na mwovu?” (Mwanzo 18:23-33) Bila shaka, jibu ni la. Yehova ‘alinyesha kiberiti na moto’ juu ya Sodoma, baada tu ya Loti mwadilifu na binti zake kufika mji wa Soari wakiwa salama. (Mwanzo 19:22-24) Kinyume chake, Yona ‘alikasirika’ sana wakati Mungu alipowaonyesha rehema watu wa Ninawi. Bila kujali toba yao ya kutoka moyoni, Yona alitaka tu waangamizwe kwa sababu tayari alikuwa ametangaza kwamba wangeangamizwa.—Yona 3:10–4:1.
17 Yehova alimhakikishia Abrahamu kwamba anatekeleza haki Yake kwa kuwaangamiza waovu na kuwaokoa pia waadilifu. Kwa upande mwingine, Yona alihitaji kujifunza kwamba Yehova ni mwenye rehema. Waovu wakiacha kabisa njia zao, yuko “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Tofauti na wanadamu fulani wanaojali mno vyeo vyao, Yehova hatoi hukumu kali ili kujionyesha ana nguvu, wala hakatai kuwahurumia watu eti kwa sababu ataonekana kuwa dhaifu. Yeye huonyesha rehema wakati wowote inapofaa kufanya hivyo.—Isaya 55:7; Ezekieli 18:23.
18. Tumia Biblia kuthibitisha kwamba Yehova haongozwi tu na hisia.
18 Hata hivyo, Yehova hapumbazwi na hisia. Watu wake walipoanza kuabudu sanamu, Yehova alisema hivi kwa uthabiti: “Nitawahukumu kadiri ya mwenendo wenu. Nitawaadhibu kwa machukizo yenu yote. Sitawaachia wala sitawaonea huruma; bali nitawaadhibu kulingana na mienendo yenu.” (Ezekieli 7:3, 4, BHN) Kwa hiyo, wanadamu wanapoendelea kufanya mabaya bila kujali, Yehova huwahukumu ifaavyo. Lakini hukumu yake inategemea ushahidi thabiti. Hivyo, Yehova aliposikia “kilio” kuhusu Sodoma na Gomora alisema hivi: “Nitashuka sasa nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia.” (Mwanzo 18:20, 21) Tunathamini kama nini kwamba Yehova si kama wanadamu wengi ambao huamua mambo haraka-haraka bila ushahidi kamili! Kwa kweli, Biblia yaeleza jinsi Yehova alivyo, “Mungu wa uaminifu . . . mwenye haki.”—Kumbukumbu la Torati 32:4.
Tumaini Haki ya Yehova
19. Tunaweza kufanya nini tukiwa na maswali yenye kutatanisha kuhusu hukumu za Yehova?
19 Biblia haijibu kila swali kuhusu matendo ya Yehova katika nyakati za kale; wala haielezi kila jambo kuhusu jinsi Yehova atakavyohukumu mtu mmoja-mmoja na vikundi vya watu wakati ujao. Tunapotatanishwa na masimulizi au unabii fulani wa Biblia ambao hauelezi kila jambo, tunaweza kuwa waaminifu kama nabii Mika, aliyeandika hivi: “Nitamngojea Mungu wa wokovu wangu.”—Mika 7:7.
20, 21. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova atafanya yaliyo sawa?
20 Tunaweza kuwa na hakika kwamba katika kila hali, Yehova atafanya yaliyo sawa. Hata inapoonekana kwamba wanadamu wanapuuza ukosefu wa haki, Yehova anaahidi hivi: “Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa.” (Waroma 12:19) Tukiwa na mtazamo wa kungoja, tutakuwa na usadikisho imara kama wa mtume Paulo aliyesema: “Je, kwa Mungu kuna ukosefu wa haki? Hilo lisipate kuwa hivyo kamwe!”—Waroma 9:14.
21 Hivi sasa tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Watu wengi wametendewa kikatili kwa sababu ya ‘dhuluma’ na ukosefu wa haki. (Mhubiri 4:1) Hata hivyo, Yehova hajabadilika. Bado anachukia ukosefu wa haki, naye anawajali sana wale wanaotendewa isivyo haki. Tukiendelea kuwa waaminifu kwa enzi kuu ya Yehova, atatupatia uwezo wa kuvumilia hadi Ufalme wake utakapokomesha ukosefu wote wa haki kwa wakati barabara.—1 Petro 5:6, 7.
-
-
“Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 13
“Sheria ya Bwana Ni Kamilifu”
1, 2. Kwa nini watu wengi wanapuuza sheria, lakini huenda sisi tukahisije kuhusu sheria za Mungu?
“SHERIA haina mipaka, . . . huharibu mambo yote.” Maneno hayo yaliandikwa katika kitabu kilichochapishwa mnamo mwaka wa 1712. Mwandishi wa kitabu hicho alilaumu mfumo wa sheria ambao uliendeleza kesi mahakamani miaka nenda miaka rudi. Wale waliotafuta haki mahakamani walifilisika kabisa. Katika nchi nyingi, watu wengi hawaheshimu kabisa sheria kwa sababu mifumo ya sheria na ya mahakama haieleweki, haifuati haki kabisa, inapendelea watu, na haitegemeki.
2 Tofauti na maelezo hayo, fikiria maneno yaliyoandikwa miaka ipatayo 2,700 iliyopita: “Sheria yako naipenda mno ajabu.” (Zaburi 119:97) Kwa nini mtunga-zaburi aliipenda mno sheria hiyo? Kwa sababu sheria aliyosifu ilitungwa na Yehova Mungu, wala si na serikali yoyote ya wanadamu. Kadiri unavyojifunza sheria za Yehova, huenda ukazipenda zaidi kama mtunga-zaburi. Kujifunza sheria hizo kutakusaidia kumjua vyema hakimu bora zaidi ulimwenguni.
Mpaji-Sheria Mkuu Zaidi
3, 4. Yehova amethibitika kuwa Mpaji-Sheria kwa njia zipi?
3 Biblia inatuambia kwamba “mmoja yuko ambaye ni mpaji-sheria na hakimu.” (Yakobo 4:12) Kwa hakika, Yehova peke yake ndiye Mpaji-Sheria wa kweli. Hata sayari zinafuata ‘sheria zake zinazoongoza mbingu.’ (Ayubu 38:33, The New Jerusalem Bible) Kundi kubwa sana la malaika watakatifu wa Yehova wanaongozwa pia na sheria zake, kwa kuwa wamepangwa kulingana na vyeo hususa, nao hufuata amri ya Yehova wakiwa wahudumu wake.—Zaburi 104:4; Waebrania 1:7, 14.
4 Yehova amewapa pia wanadamu sheria. Kila mmoja wetu ana dhamiri, ambayo inaonyesha haki ya Yehova. Dhamiri ni sheria fulani ya asili ambayo inaweza kutusaidia kupambanua mema na mabaya. (Waroma 2:14) Wazazi wetu wa kwanza walipewa dhamiri kamilifu, kwa hiyo walihitaji sheria chache sana. (Mwanzo 2:15-17) Hata hivyo, mwanadamu asiyekamilika anahitaji sheria nyingi zaidi za kumwongoza kufanya mapenzi ya Mungu. Wazee wa ukoo kama vile Noa, Abrahamu, na Yakobo walizipa familia zao sheria ambazo walipewa na Yehova Mungu. (Mwanzo 6:22; 9:3-6; 18:19; 26:4, 5) Yehova alijisababisha kuwa Mpaji-Sheria asiye na kifani alipopatia taifa la Israeli Sheria kupitia Musa. Sheria hizo zinatusaidia kuelewa kindani zaidi haki ya Yehova.
Muhtasari wa Sheria ya Musa
5. Je, Sheria ya Musa ilikuwa na amri ngumu na zenye kulemea, na kwa nini unajibu hivyo?
5 Watu wengi wanafikiri kwamba Sheria ya Musa ilikuwa na amri ngumu zenye kulemea. Jambo hilo si kweli. Sheria hiyo ilikuwa na zaidi ya amri 600. Huenda hizo zikaonekana kuwa nyingi, lakini hebu fikiria: Kufikia mwishoni mwa karne ya 20, sheria za serikali ya Marekani zilijaza zaidi ya kurasa 150,000 za vitabu vya sheria. Sheria zipatazo 600 huongezwa baada ya kila miaka miwili! Kwa hiyo, sheria za wanadamu ni nyingi sana kuliko Sheria ya Musa. Hata hivyo, Sheria ya Mungu iliwaongoza Waisraeli katika mambo mbalimbali ya maisha ambayo hata sheria za kisasa hazitaji. Chunguza muhtasari wa sheria hiyo.
6, 7. (a) Sheria ya Musa inatofautianaje na mfumo mwingine wowote wa sheria, na amri kuu ya Sheria hiyo ni ipi? (b) Waisraeli wangeweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanakubali enzi kuu ya Yehova?
6 Sheria ilitukuza enzi kuu ya Yehova. Kwa sababu hiyo, Sheria ya Musa haiwezi kulinganishwa na mfumo mwingine wowote wa sheria. Amri kuu zaidi ya sheria hiyo ilikuwa: “Sikiza, Ee Israeli; BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja. Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.” Watu wa Mungu wangeonyeshaje kwamba wanampenda? Walipaswa kumtumikia, kujitiisha kwa enzi yake kuu.—Kumbukumbu la Torati 6:4, 5; 11:13.
7 Kila Mwisraeli alionyesha kwamba anakubali enzi kuu ya Yehova kwa kujitiisha kwa wale waliopewa mamlaka. Wazazi, wakuu, waamuzi, makuhani na, hatimaye, mfalme waliwakilisha mamlaka ya Mungu. Yehova aliona uasi wowote dhidi ya wenye mamlaka kuwa uasi dhidi yake. Kwa upande mwingine, wale wenye mamlaka wangeadhibiwa na Yehova iwapo wangewaonea au kuwakandamiza watu wake. (Kutoka 20:12; 22:28; Kumbukumbu la Torati 1:16, 17; 17:8-20; 19:16, 17) Basi, watu wote walikuwa na wajibu wa kuunga mkono enzi kuu ya Mungu.
8. Sheria ilidumishaje utakatifu wa Yehova?
8 Sheria ilidumisha utakatifu wa Yehova. Sheria ya Musa inataja neno “takatifu” na “utakatifu” zaidi ya mara 280. Sheria iliwasaidia watu wa Mungu kutofautisha vitu safi na visivyo safi, ilitaja vitu 70 hivi ambavyo vingemfanya Mwisraeli awe najisi. Sheria hizo zilihusu usafi wa mwili, chakula, na hata kufunika kinyesi. Sheria hizo zililinda kabisa afya yao.a Lakini zilitimiza kusudi jingine muhimu zaidi—ziliwasaidia kupata kibali cha Yehova, ziliwatenga na mazoea yenye dhambi ya mataifa yasiyo na adili yaliyokuwa jirani. Fikiria mfano mmoja.
9, 10. Agano la Sheria lilisema nini kuhusu ngono na kujifungua mtoto, na sheria hizo zilikuwa na manufaa gani?
9 Agano la Sheria lilisema kwamba mtu aliyejifungua mtoto au kufanya ngono—hata kati ya wenzi wa ndoa—angekuwa najisi kwa kipindi fulani. (Mambo ya Walawi 12:2-4; 15:16-18) Sheria hizo hazikudharau zawadi hizo safi kutoka kwa Mungu. (Mwanzo 1:28; 2:18-25) Badala yake, sheria hizo zilidumisha utakatifu wa Yehova kwa kuwazuia waabudu wake wasichafuliwe. Kumbuka kwamba mataifa jirani ya Israeli yalikuwa yakichanganya dini na ibada za ngono na uzazi. Dini ya Wakanaani ilikuwa na makahaba wa kiume na wa kike. Walitenda mambo maovu kupindukia na yakaenea kotekote. Kinyume chake, Sheria ilitenga kabisa ibada ya Yehova na mambo ya ngono.b Kulikuwa na faida nyingine pia.
10 Sheria hizo pia zilifundisha ukweli fulani muhimu sana.c Dhambi ya Adamu inapitishwaje kutoka kizazi hadi kizazi? Ni kupitia ngono na kuzaa, sivyo? (Waroma 5:12) Ndiyo, Sheria ya Mungu iliwakumbusha watu wake kwamba wao ni watenda-dhambi. Kwa kweli, sote tunazaliwa katika dhambi. (Zaburi 51:5) Tunahitaji msamaha na ukombozi ili kumkaribia Mungu wetu mtakatifu.
11, 12. (a) Sheria ilitetea kanuni gani muhimu ya haki? (b) Sheria ilizuia upotoshaji wa haki katika mambo yapi?
11 Sheria ilidumisha haki kamilifu ya Yehova. Sheria ya Musa ilitetea kanuni ya usawa, au usawaziko, katika mambo ya haki. Kwa hiyo, Sheria ilisema hivi: “Uhai utalipwa kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono na mguu kwa mguu.” (Kumbukumbu la Torati 19:21, BHN) Hivyo basi, adhabu ya kesi za uhalifu ililingana na uhalifu uliofanywa. Kanuni hiyo ya haki ya Mungu ilikuwa muhimu sana katika Sheria. Na kanuni hiyo inaweza kutusaidia leo kuelewa dhabihu ya fidia ya Kristo Yesu, kama Sura ya 14 itakavyoonyesha.—1 Timotheo 2:5, 6.
12 Sheria ilizuia pia upotoshaji wa haki. Kwa mfano, angalau mashahidi wawili walihitajiwa ili kuthibitisha shtaka. Mashahidi wa uwongo walipata adhabu kali sana. (Kumbukumbu la Torati 19:15, 18, 19) Ufisadi na kupokea rushwa kulipigwa marufuku. (Kutoka 23:8; Kumbukumbu la Torati 27:25) Watu wa Mungu walihitaji kufuata kanuni za juu za Yehova za haki hata katika shughuli zao za kibiashara. (Mambo ya Walawi 19:35, 36; Kumbukumbu la Torati 23:19, 20) Mfumo huo wa sheria usiopendelea na usio na kifani ulinufaisha sana Israeli!
Sheria Zinazokazia Rehema na Kutopendelea Katika Hukumu
13, 14. Sheria ilikaziaje haki na kutopendelea kwa habari ya mwizi na yule aliyeibiwa?
13 Je, Sheria ya Musa ilikuwa kali mno, iliyotekelezwa bila rehema? La hasha! Mfalme Daudi aliongozwa kuandika hivi: “Sheria ya BWANA ni kamilifu.” (Zaburi 19:7) Daudi alijua vyema kwamba Sheria ilikazia rehema na kutopendelea. Jinsi gani?
14 Katika nchi fulani leo, yaonekana kwamba sheria huwapendelea na kuwalinda wahalifu na haiwajali waliotendewa uhalifu. Kwa mfano, huenda wezi wakafungwa gerezani. Lakini, wale walioibiwa huenda hawajarudishiwa mali yao, ingawa wanalazimika kulipa ushuru ili kuwalisha wahalifu hao wakiwa gerezani. Katika Israeli la kale, hakukuwa na magereza kama leo. Adhabu haikupaswa kupita mipaka iliyowekwa na Sheria. (Kumbukumbu la Torati 25:1-3) Mwizi alilazimika kulipa vitu alivyokuwa ameiba. Isitoshe, alitoa malipo zaidi. Alilipa kiasi gani? Ilitegemea hali. Inaonekana kwamba mahakimu waliruhusiwa kuzingatia mambo kadhaa, kama vile toba ya mtenda-dhambi. Ndiyo sababu malipo ambayo mwizi alihitajiwa kulipa yanayotajwa kwenye Mambo ya Walawi 6:1-7 ni chini zaidi kuliko malipo yanayotajwa kwenye Kutoka 22:7.
15. Sheria ilionyeshaje rehema na haki kwa mtu aliyemwua mwingine bila kukusudia?
15 Kwa rehema, Sheria ilitambua kwamba makosa yote hayakuwa ya kukusudia. Kwa mfano, mtu alipomwua mwingine bila kukusudia, hakuhitajika kulipa uhai kwa uhai ikiwa alichukua hatua ifaayo ya kukimbilia mojawapo ya miji ya makimbilio iliyokuwa kotekote katika Israeli. Baada ya kesi yake kuchunguzwa na waamuzi wa mji huo, alikaa humo hadi kifo cha kuhani mkuu. Kisha angekuwa huru kuishi popote alipotaka. Hivyo, alinufaishwa na rehema ya Mungu. Vilevile, sheria hiyo ilikazia thamani kubwa ya uhai wa mwanadamu.—Hesabu 15:30, 31; 35:12-25.
16. Sheria ililindaje haki fulani za watu?
16 Sheria ililinda haki za watu. Angalia jinsi ilivyolinda watu wenye madeni. Sheria ilikataza kuingia katika nyumba ya mdeni na kuchukua mali yake kama rehani. Badala yake, mkopeshaji alihitaji kusimama nje na kungoja mdeni amletee rehani hiyo. Hivyo, hakuna mtu aliyeruhusiwa kuvamia nyumba ya mwingine. Ikiwa mkopeshaji alichukua vazi la nje kama rehani, sharti angelirudisha jioni, kwa sababu huenda mdeni angehitaji kujifunika vazi hilo wakati wa usiku.—Kumbukumbu la Torati 24:10-14.
17, 18. Waisraeli walitofautianaje na mataifa mengine kuhusu vita, na kwa nini?
17 Hata pia kulikuwa na sheria kuhusu vita. Watu wa Mungu hawakupigana vita kwa sababu tu walitamani kupata mamlaka au ushindi, bali walimwakilisha Mungu katika “Vita vya BWANA.” (Hesabu 21:14) Mara nyingi, Waisraeli walitoa kwanza masharti ya kujisalimisha. Ikiwa jiji lilikataa masharti hayo, basi Israeli lingelizingira kupatana na amri za Mungu. Tofauti na wanajeshi wengi, wanajeshi Waisraeli hawakuruhusiwa kubaka wanawake au kuchinja watu ovyo-ovyo. Hata walihitaji kuheshimu mazingira, hawakupaswa kukata miti ya matunda ya maadui.d Wanajeshi wengine hawakuwa na sheria kama hizo.—Kumbukumbu la Torati 20:10-15, 19, 20; 21:10-13.
18 Je, wewe huudhika unaposikia kwamba katika nchi fulani watoto wadogo wanazoezwa kuwa wanajeshi? Katika Israeli la kale, mwanamume yeyote mwenye umri uliopungua miaka 20 hakuandikishwa jeshini. (Hesabu 1:2, 3) Hata mwanamume mzima mwenye hofu kubwa hakuruhusiwa kwenda vitani. Mwanamume aliyeoa karibuni hangeenda vitani kwa mwaka mzima ili aweze kumzaa mrithi kabla ya kushiriki utumishi huo hatari sana. Sheria ilieleza kwamba kwa kufanya hivyo, mume huyo kijana angepata ‘kumfurahisha’ mkewe.—Kumbukumbu la Torati 20:5, 6, 8; 24:5.
19. Sheria iliwalindaje wanawake, watoto, familia, wajane, na mayatima?
19 Sheria iliwalinda wanawake, watoto, na familia na kujali masilahi yao. Iliwaamuru wazazi wawatunze na kuwafundisha watoto mambo ya kiroho kila wakati. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Ilikataza ngono zote za maharimu, na yeyote aliyefanya hivyo aliuawa. (Mambo ya Walawi, sura ya 18) Vilevile ilikataza uzinzi, ambao mara nyingi huvunja na kuharibu amani na heshima ya familia. Sheria iliwajali sana wajane na mayatima na ilikataza katakata wasiteswe.—Kutoka 20:14; 22:22-24.
20, 21. (a) Kwa nini Sheria ya Musa iliwaruhusu Waisraeli wawe na wake wengi? (b) Kuhusu talaka, kwa nini Sheria ilitofautiana na kanuni ambazo Yesu alirudisha baadaye?
20 Hata hivyo, huenda wengine wakajiuliza hivi, ‘Mbona Sheria iliwaruhusu watu kuwa na wake wengi?’ (Kumbukumbu la Torati 21:15-17) Tunahitaji kuchunguza sheria kama hizo tukifikiria hali za wakati huo. Wale wanaojaribu kuelewa Sheria ya Musa kwa kutegemea maoni ya nyakati na tamaduni za kisasa bila shaka hawataielewa. (Mithali 18:13) Kulingana na kanuni ambazo Yehova aliweka zamani katika Edeni, ndoa ilikuwa kifungo cha kudumu kati ya mume mmoja na mke mmoja. (Mwanzo 2:18, 20-24) Hata hivyo, mazoea kama vile ndoa za wake wengi yalikuwa yameenea kwa miaka mingi sana kabla Yehova hajawapa Waisraeli Sheria. Yehova alijua vyema kwamba mara kwa mara ‘watu wake wenye shingo ngumu’ wangekosa kutii hata sheria rahisi sana, kama zile zilizokataza ibada ya sanamu. (Kutoka 32:9) Basi kwa hekima, hakuchagua wakati huo kuwa wakati wa kurekebisha mazoea yao yote ya ndoa. Lakini kumbuka kwamba Yehova hakuanzisha ndoa ya wake wengi. Hata hivyo, alitumia Sheria ya Musa kudhibiti ndoa za wake wengi miongoni mwa watu wake na kuwazuia wasitumie vibaya zoea hilo.
21 Vivyo hivyo, Sheria ya Musa ilimruhusu mwanamume kumtaliki mkewe kwa sababu mbalimbali nzito. (Kumbukumbu la Torati 24:1-4) Yesu alisema kwamba Mungu aliwapa Wayahudi idhini hiyo “kwa kufikiria ugumu [wao] wa moyo.” Hata hivyo, idhini kama hizo zilikuwa za muda tu. Yesu alirudisha tena kanuni za Yehova kuhusu ndoa ambazo zingefuatwa na wafuasi wake.—Mathayo 19:8.
Sheria Ilikazia Upendo
22. Sheria ya Musa ilikazia upendo kwa njia zipi, na kwa nani?
22 Je, waweza kuwazia mfumo wowote wa kisasa wa sheria unaokazia upendo? Sheria ya Musa ilikazia sana upendo. Kwani, katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati pekee, neno “upendo” limetumiwa zaidi ya mara 20 katika njia mbalimbali. Amri ya pili iliyo kuu zaidi katika Sheria ilikuwa, “umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mambo ya Walawi 19:18; Mathayo 22:37-40) Waisraeli walipaswa kuwapenda wenzao na pia wageni walioishi kati yao, huku wakikumbuka kwamba pindi moja wao pia walikuwa wageni. Walipaswa kuwapenda maskini na wanyonge, na kuwasaidia kimwili bila kuwadhulumu. Hata waliagizwa kuwa wenye fadhili na kuwajali wanyama wanaobeba mizigo.—Kutoka 23:6; Mambo ya Walawi 19:14, 33, 34; Kumbukumbu la Torati 22:4, 10; 24:17, 18.
23. Mtungaji wa Zaburi 119 alichochewa kufanya nini, nasi tunaweza kuazimia kufanya nini?
23 Hakuna taifa jingine lililobarikiwa na sheria kama hizo. Si ajabu kwamba mtunga-zaburi aliandika hivi: “Naipenda sana sheria yako!” Lakini hakuwa tu na hisia ya upendo. Upendo huo ulimchochea kutenda, kwa kuwa alijitahidi kutii sheria hiyo na kuishi kupatana nayo. Aliendelea kusema hivi: “Naitafakari [sheria yako] mchana kutwa.” (Zaburi 119:11, 97, BHN) Naam, alijifunza sheria za Yehova kwa ukawaida. Hapana shaka yoyote kwamba upendo wake uliongezeka kadiri alivyojifunza sheria hizo. Wakati huohuo, alizidi kumpenda Yehova Mungu, yule Mpaji-Sheria. Na umkaribie zaidi Yehova, Mpaji-Sheria Mkuu na Mungu wa haki unapoendelea kujifunza sheria zake.
a Kwa mfano, sheria zilizoamuru kinyesi cha mwanadamu kifunikwe, wagonjwa watengwe, na mtu yeyote anayegusa maiti aoge, zilikuwapo muda mrefu kabla ya manufaa yake kutambuliwa.—Mambo ya Walawi 13:4-8; Hesabu 19:11-13, 17-19; Kumbukumbu la Torati 23:13, 14.
b Mahekalu ya Wakanaani yalikuwa na vyumba vya kufanyia ngono, lakini Sheria ya Musa ilisema kwamba watu wote walio najisi hawangeweza hata kuingia hekaluni. Kwa hiyo, hakuna mtu yeyote angechanganya ngono na ibada katika nyumba ya Yehova, kwa sababu ngono ilimfanya mtu awe najisi kwa kipindi fulani.
c Kusudi kuu la Sheria lilikuwa kufundisha. Hata kichapo Encyclopaedia Judaica kinasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “sheria,” toh·rah’, linamaanisha “mafundisho.”
d Sheria iliuliza hivi waziwazi: “Mti wa kondeni, je! ni mtu, hata ukauzuie?” (Kumbukumbu la Torati 20:19) Philo, msomi Myahudi wa karne ya kwanza, alitaja sheria hiyo, na kusema kwamba Mungu anaona “haifai hasira inayoelekezwa kwa watu itumiwe kuharibu vitu ambavyo havina hatia yoyote.”
-
-
Yehova Atoa “Fidia Katika Kubadilishana kwa Ajili ya Wengi”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 14
Yehova Atoa “Fidia Katika Kubadilishana kwa Ajili ya Wengi”
1, 2. Biblia inasema nini kuhusu hali ya wanadamu, na suluhisho pekee ni nini?
“VIUMBE vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Maneno hayo ya mtume Paulo yanaeleza hali yetu yenye kusikitisha. Huenda mwanadamu akaona kwamba mateso, dhambi, na kifo haziwezi kukomeshwa. Lakini Yehova ana uwezo unaozidi wa wanadamu. (Hesabu 23:19) Mungu huyo wa haki ametuandalia suluhisho la matatizo yetu. Suluhisho hilo ni fidia.
2 Fidia ndiyo zawadi bora ambayo Yehova amewapa wanadamu. Kupitia fidia tutaweza kukombolewa kutoka kwa dhambi na kifo. (Waefeso 1:7) Ndiyo msingi wa tumaini la kuishi milele, ama mbinguni au katika paradiso duniani. (Luka 23:43; Yohana 3:16; 1 Petro 1:4) Lakini fidia ni nini hasa? Inatusaidiaje kuelewa haki ya Yehova isiyo na kifani?
Kwa Nini Fidia Ilihitajiwa?
3. (a) Kwa nini fidia ilihitajiwa? (b) Kwa nini Mungu hangeweza kupunguza adhabu ya kifo kwa wazao wa Adamu?
3 Fidia ilihitajiwa kwa sababu ya dhambi ya Adamu. Kwa sababu ya kutomtii Mungu, Adamu aliwaletea wazao wake magonjwa, kilio, maumivu, na kifo. (Mwanzo 2:17; Waroma 8:20) Mungu hangeweza kupunguza adhabu ya kifo kwa sababu tu ya kuwahurumia wazao wa Adamu. Kufanya hivyo kungekuwa kupuuza sheria yake mwenyewe inayosema kwamba “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Na endapo Yehova angevunja kanuni zake mwenyewe za haki, basi kungekuwa na mvurugo na uasi ulimwenguni pote!
4, 5. (a) Shetani alitoa mashtaka gani ya uwongo kumhusu Mungu, na kwa nini Yehova alikuwa na wajibu wa kujibu mashtaka hayo? (b) Shetani alitoa shtaka gani kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova?
4 Kama tulivyoona katika Sura ya 12, uasi uliotukia Edeni ulizusha masuala muhimu sana. Shetani alichafua jina zuri la Mungu. Ni kana kwamba alimshtaki Yehova kuwa mwongo na mtawala mkatili wa kimabavu, anayewanyima viumbe wake uhuru. (Mwanzo 3:1-5) Kwa kujaribu kukatisha kusudi la Mungu la kuwa na wanadamu waadilifu duniani, Shetani pia alitoa shtaka la kwamba Mungu hawezi kutimiza makusudi yake. (Mwanzo 1:28; Isaya 55:10, 11) Kama Yehova hangejibu mashtaka hayo, huenda viumbe wake wengi wenye akili wangetilia shaka utawala wake.
5 Shetani alieneza pia uwongo kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova. Alidai kwamba wanamtumikia Yehova kwa sababu ya ubinafsi na kwamba hakuna yeyote ambaye angeendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu akipata magumu. (Ayubu 1:9-11) Masuala hayo yalikuwa muhimu sana kuliko magumu ambayo yangewakabili wanadamu. Kwa kufaa, Yehova alihisi kwamba ana wajibu wa kujibu mashtaka ya uwongo ya Shetani. Lakini Mungu angesuluhishaje masuala hayo na kuwaokoa wanadamu?
Fidia—Bei Inayolingana
6. Ni maneno gani yanayotumiwa katika Biblia kueleza njia ya Mungu ya kuwaokoa wanadamu?
6 Yehova alisuluhisha jambo hilo kwa rehema nyingi sana na haki. Hakuna mwanadamu angeweza kusuluhisha jambo hilo kwa njia hiyo. Alisuluhisha jambo hilo kwa njia rahisi sana. Mara nyingine njia aliyotumia huitwa ununuzi, ukombozi, ufuniko, na upatanisho. (Zaburi 49:8, ZSB; Danieli 9:24, BHN; Wagalatia 3:13; Wakolosai 1:20; Waebrania 2:17) Lakini Yesu alitumia neno ambalo huenda linafaa kabisa. Alisema: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia [Kigiriki, lyʹtron] katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.”—Mathayo 20:28.
7, 8. (a) Neno “fidia” linamaanisha nini katika Maandiko? (b) Fidia inaonyeshaje ulinganifu?
7 Fidia ni nini? Neno la Kigiriki linalotumiwa hapa linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kuweka huru, kuachilia.” Neno hilo lilihusiana na pesa zinazolipwa ili wafungwa wa vita waweze kuachiliwa huru. Basi, kwa ufupi fidia inaweza kufafanuliwa kuwa kitu kinacholipwa ili kununua tena kitu fulani. Katika Maandiko ya Kiebrania, neno linalotafsiriwa “fidia” (koʹpher) linatokana na kitenzi kinachomaanisha “kufunika.” Kwa mfano, Mungu alimwambia Noa ‘aifunike’ (muundo fulani wa neno hilo) safina kwa lami. (Mwanzo 6:14) Habari hiyo inatusaidia kuelewa kwamba kutoa fidia humaanisha pia kufunika dhambi.—Zaburi 65:3.
8 Kichapo Theological Dictionary of the New Testament kinasema kwamba neno hilo (koʹpher) “sikuzote hudokeza usawa,” au ulinganifu. Kwa hiyo, kifuniko cha sanduku la agano kilikuwa na umbo sawa na sanduku hilo. Vivyo hivyo, ili kutoa fidia, au kufunika dhambi, ni lazima bei inayolipwa ilingane kabisa, au ifunike kikamili hasara iliyosababishwa na dhambi. Ndiyo sababu Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilisema hivi: “Uhai utalipwa kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono na mguu kwa mguu.”—Kumbukumbu la Torati 19:21, BHN.
9. Kwa nini watu waaminifu walitoa dhabihu za wanyama, na Yehova alionaje dhabihu hizo?
9 Watu waaminifu kuanzia Abeli na kuendelea walimtolea Mungu dhabihu za wanyama. Kwa kufanya hivyo, walionyesha kwamba walitambua kuwapo kwa dhambi na umuhimu wa ukombozi. Walikuwa na imani katika ahadi ya Mungu ya kuwakomboa wanadamu kupitia “uzao” wake. (Mwanzo 3:15; 4:1-4; Mambo ya Walawi 17:11; Waebrania 11:4) Yehova alikubali dhabihu hizo na wakawa na uhusiano mzuri naye. Hata hivyo, matoleo ya wanyama yalikuwa ishara tu ya jambo jingine. Wanyama hawangeweza kufunika kabisa dhambi za wanadamu, kwa kuwa wanyama ni viumbe wa hali ya chini wanapolinganishwa na wanadamu. (Zaburi 8:4-8) Hivyo basi, Biblia yasema hivi: “Haiwezekani damu ya mafahali na ya mbuzi kuziondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Dhabihu hizo zilikuwa mifano tu ya dhabihu ya kweli ya fidia ambayo ingetolewa.
“Fidia Inayolingana”
10. (a) Mfidi alihitaji kulingana na nani, na kwa nini? (b) Kwa nini ni mwanadamu mmoja tu aliyehitaji kutolewa dhabihu?
10 Mtume Paulo alisema kwamba “katika Adamu wote wanakufa.” (1 Wakorintho 15:22) Kwa hiyo mtu aliyelingana kabisa na Adamu—mwanadamu mkamilifu—alihitaji kufa ili kutoa fidia. (Waroma 5:14) Hakuna kiumbe mwingine yeyote ambaye angeweza kusawazisha mizani ya haki. Ni mwanadamu mkamilifu peke yake, mtu ambaye hakurithi dhambi ya Adamu, ndiye tu aliyeweza kutoa “fidia inayolingana” kikamili kabisa na Adamu. (1 Timotheo 2:6) Hakungekuwa na uhitaji wa mamilioni ya wanadamu kutolewa dhabihu ili kumkomboa kila mzao wa Adamu. Mtume Paulo alieleza hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” (Waroma 5:12) Na “kwa kuwa kifo ni kupitia mwanadamu,” Mungu alifanya mpango wa kuwakomboa wanadamu “kupitia mwanadamu.” (1 Wakorintho 15:21) Jinsi gani?
“Fidia inayolingana kwa ajili ya wote”
11. (a) Mfidi ‘angeonja kifo kwa ajili ya kila mtu’ jinsi gani? (b) Kwa nini Adamu na Hawa hawangefaidika kutokana na fidia? (Ona kielezi-chini.)
11 Yehova alipanga mwanadamu mmoja mkamilifu adhabihu uhai wake kwa hiari. Andiko la Waroma 6:23 lasema, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” Mfidi huyo ‘angeonja kifo kwa ajili ya kila mtu’ kwa kudhabihu uhai wake. Yaani, angelipa mshahara wa dhambi ya Adamu. (Waebrania 2:9; 2 Wakorintho 5:21; 1 Petro 2:24) Kufanya hivyo kungekuwa na matokeo makubwa kisheria. Fidia ingekomesha kabisa dhambi yenye kuangamiza kwa kuwaondolea wazao watiifu wa Adamu hukumu ya kifo.a—Waroma 5:16.
12. Toa mfano ambao unaonyesha jinsi watu wengi wanavyoweza kufaidika baada ya deni moja kulipwa.
12 Kwa mfano: Wazia kwamba wakazi wengi wa mji wenu wameajiriwa katika kiwanda kikubwa. Wewe na jirani zako mnalipwa mshahara mnono na mnaishi raha mustarehe. Siku moja kiwanda hicho kinafungwa kabisa na mambo yanabadilika. Kwa nini? Kiwanda hicho kimefilisika kwa sababu ya ufisadi wa meneja wake. Kwa ghafula, wewe na jirani zako mnafutwa kazi na hamwezi kulipa madeni yenu. Wenzi wa ndoa, watoto, na wakopeshaji wanateseka kwa sababu ya ufisadi wa mtu mmoja tu. Je, kuna suluhisho? Ndiyo! Mfadhili tajiri anaamua kuwasaidia. Anajua umuhimu wa kiwanda hicho. Anawahurumia pia watu wote walioajiriwa humo na familia zao. Kwa hiyo anapanga kulipa deni la kampuni hiyo ili kiwanda kifunguliwe. Kulipwa kwa deni hilo kunawafaidi watu wote walioajiriwa humo, familia zao na wakopeshaji. Vivyo hivyo, kulipwa kwa deni la Adamu kunawafaidi mamilioni ya watu.
Ni Nani Anayetoa Fidia?
13, 14. (a) Yehova aliwaandalia wanadamu fidia jinsi gani? (b) Ni nani anayelipwa fidia, na kwa nini malipo hayo ni muhimu?
13 Ni Yehova peke yake angeweza kumtoa “Mwana-Kondoo . . . ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29) Lakini Yehova hakumtuma malaika yeyote tu aje kuwaokoa wanadamu. Badala yake, alimtuma Yule ambaye angeweza kujibu kikamili na kwa uhakika shtaka la Shetani dhidi ya watumishi wa Yehova. Naam, Yehova alijitoa kabisa kwa kumtuma Mwanaye mzaliwa-pekee, ‘aliyekuwa furaha yake.’ (Mithali 8:30) Kwa hiari, Mwana wa Mungu “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu” kwa kuacha mwili wake wa kimbingu. (Wafilipi 2:7) Yehova alihamisha kimuujiza uhai na utu wa Mwanaye mzaliwa wa kwanza wa mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi aliyeitwa Maria. (Luka 1:27, 35) Akiwa mwanadamu, angeitwa Yesu. Lakini kisheria, angeweza kuitwa Adamu wa pili, kwa kuwa alilingana kikamili na Adamu. (1 Wakorintho 15:45, 47) Kwa hiyo, Yesu aliweza kujitoa mwenyewe kuwa dhabihu ya fidia kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi.
14 Ni nani ambaye angelipwa fidia? Zaburi 49:7 yasema wazi kwamba “Mungu” ndiye anayelipwa fidia. Lakini ni Yehova anayefanya mpango wa fidia, sivyo? Ndivyo, lakini hilo halimaanishi kwamba fidia ni badilishano lisilo na kusudi wala maana—kama kutoa pesa katika mfuko mmoja na kuzitia katika mfuko mwingine. Ni lazima tuelewe kwamba fidia si badilishano halisi, bali ni badilishano la kisheria. Yehova alithibitisha kwamba anafuata kabisa haki yake kamilifu kwa kulipa fidia, ijapokuwa ilimgharimu sana.—Mwanzo 22:7, 8, 11-13; Waebrania 11:17; Yakobo 1:17.
15. Kwa nini ilikuwa lazima Yesu ateseke na kufa?
15 Katika masika ya mwaka wa 33 W.K., Yesu Kristo alijitolea kuteseka ili alipe fidia. Alijiruhusu kukamatwa kwa mashtaka ya uwongo, kuhukumiwa kuwa na hatia, na kupigiliwa misumari kwenye mti wa mateso. Je, ilikuwa lazima Yesu apatwe na mateso hayo makali? Ndiyo, kwa sababu suala la uaminifu wa watumishi wa Mungu lilihitaji kuamuliwa. Mungu hakumruhusu Herode amwue Yesu akiwa mtoto mchanga. (Mathayo 2:13-18) Lakini akiwa mtu mzima, Yesu aliweza kuvumilia mashambulizi makali ya Shetani akiwa na ujuzi kamili wa masuala yaliyohusika.b Yesu alithibitisha waziwazi kwamba Yehova ana watumishi wanaobaki waaminifu chini ya majaribu kwa sababu ajapoteswa vibaya sana, aliendelea kuwa “mwaminifu-mshikamanifu, asiye na hila, asiyetiwa unajisi, aliyetengwa na watenda-dhambi.” (Waebrania 7:26) Ndiyo sababu kabla tu ya kufa, Yesu alipaaza kilio kwa ushindi: “Imetimizwa!”—Yohana 19:30.
Kumaliza Kazi Yake ya Ukombozi
16, 17. (a) Yesu aliendeleaje na kazi yake ya ukombozi? (b) Kwa nini ilikuwa lazima Yesu aonekane “mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu”?
16 Yesu hakuwa amemaliza kazi yake ya ukombozi. Yehova alimfufua Yesu siku ya tatu baada ya kufa. (Matendo 3:15; 10:40) Kupitia tendo hilo muhimu sana, Yehova alimthawabisha Mwanaye kwa sababu alimtumikia kwa uaminifu. Pia alimpa nafasi ya kumaliza kazi yake ya ukombozi akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu wa Mungu. (Waroma 1:4; 1 Wakorintho 15:3-8) Mtume Paulo aeleza hivi: “Kristo alipokuja akiwa kuhani wa cheo cha juu . . . , aliingia, si kwa damu ya mbuzi na ya mafahali wachanga, sivyo, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote ndani ya mahali patakatifu na kupata ukombozi udumuo milele kwa ajili yetu. Kwa maana Kristo aliingia, si mahali patakatifu palipofanywa kwa mikono, ambapo ni nakala ya uhalisi, bali mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele ya uso wa Mungu kwa ajili yetu.”—Waebrania 9:11, 12, 24.
17 Kristo hakuweza kupeleka damu yake halisi mbinguni. (1 Wakorintho 15:50) Badala yake, alipeleka kile kilichofananishwa na damu hiyo: thamani halali ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uliotolewa dhabihu. Halafu, akiwa mbele ya uso wa Mungu, alitoa rasmi thamani ya uhai wake iwe fidia ya kuwakomboa wanadamu wenye dhambi. Je, Yehova alikubali dhabihu hiyo? Ndiyo, na hilo lilithibitishwa wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi 120 hivi huko Yerusalemu wakati wa Pentekoste ya 33 W.K. (Matendo 2:1-4) Ingawa tukio hilo lilikuwa lenye kusisimua sana, fidia ilikuwa tu imeanza kuwafaidi wanadamu kwa njia kubwa ajabu.
Faida za Fidia
18, 19. (a) Ni vikundi gani viwili vya watu vinavyonufaika na upatanisho ambao umewezeshwa na damu ya Kristo? (b) Fidia inawafaidije wale wa “umati mkubwa,” sasa na wakati ujao?
18 Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo aeleza kwamba Mungu aliona vema kupitia Kristo kupatanisha kwake Mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu ya Yesu iliyomwagwa juu ya mti wa mateso. Paulo aeleza pia kwamba upatanisho huo unahusu vikundi viwili vya watu, yaani, “vitu vilivyomo katika mbingu” na “vitu vilivyo duniani.” (Wakolosai 1:19, 20; Waefeso 1:10) Kikundi cha kwanza ni cha Wakristo 144,000 ambao wanapewa tumaini la kutumikia wakiwa makuhani mbinguni na kutawala juu ya dunia pamoja na Kristo Yesu. (Ufunuo 5:9, 10; 7:4; 14:1-3) Kupitia wao, wanadamu watiifu watapata manufaa ya dhabihu hatua kwa hatua katika kipindi cha miaka 1,000.—1 Wakorintho 15:24-26; Ufunuo 20:6; 21:3, 4.
19 “Vitu vilivyo duniani” ni watu wanaotarajia kufurahia maisha makamilifu katika Paradiso duniani. Andiko la Ufunuo 7:9-17 linawaita “umati mkubwa” ambao utaokoka “dhiki kubwa” inayokuja. Lakini si lazima wangoje hadi wakati huo ili wanufaike na fidia. Tayari “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Hata sasa wanapata faida za kiroho za mpango huo wa upendo kwa sababu wanadhihirisha imani katika fidia. Wamehesabiwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu! (Yakobo 2:23) Kwa sababu ya dhabihu ya Yesu, wanaweza ‘kukaribia kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa.’ (Waebrania 4:14-16) Wanapokosea, wanasamehewa kikweli. (Waefeso 1:7) Wana dhamiri safi ijapokuwa hawajakamilika. (Waebrania 9:9; 10:22; 1 Petro 3:21) Kwa hiyo, kupatanishwa na Mungu si tukio tu la wakati ujao, bali ni jambo linalotukia leo! (2 Wakorintho 5:19, 20) Katika kile kipindi cha miaka 1,000, ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ hatua kwa hatua na mwishowe ‘watakuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Waroma 8:21.
20. Wewe unahisije unapotafakari juu ya fidia?
20 “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo” kwa ajili ya fidia! (Waroma 7:25) Mpango wa fidia ni rahisi sana, lakini ni wa hali ya juu sana hivi kwamba unatustaajabisha. (Waroma 11:33) Tunapotafakari na kuthamini sana fidia, mioyo yetu inatuchochea kumkaribia zaidi Mungu wa haki. Kama mtunga-zaburi, tuna sababu nyingi sana za kumsifu Yehova ambaye ‘anapenda haki na hukumu.’—Zaburi 33:5.
a Adamu na Hawa hawangefaidika kutokana na fidia. Sheria ya Musa ilisema hivi kumhusu mwuaji wa kukusudia: “Msipokee fidia kwa ajili ya uhai wa mwuaji, ambaye amekuwa na hatia ya mauti.” (Hesabu 35:31) Ni wazi kwamba Adamu na Hawa walistahili kufa kwa sababu walikataa kimakusudi kumtii Mungu. Hivyo wakapoteza tumaini lao la kuishi milele.
b Ili kufutilia mbali dhambi ya Adamu, Yesu alilazimika kufa akiwa mtu mzima mkamilifu wala si mtoto mkamilifu. Kumbuka kwamba Adamu alitenda dhambi kimakusudi, alijua vizuri kabisa ubaya na matokeo ya tendo lake. Kwa hiyo, ili kuwa “Adamu wa mwisho” na kufunika dhambi hiyo, Yesu alihitaji kuamua kudumisha uaminifu wake kwa Yehova kupatana na ujuzi aliokuwa nao. (1 Wakorintho 15:45, 47) Kwa hiyo, maisha ya Yesu ya uaminifu akiwa duniani kutia ndani kifo chake cha dhabihu yalikuwa “tendo moja la kutetewa kuwa haki.”—Waroma 5:18, 19.
-
-
Yesu ‘Aimarisha Haki Duniani’Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 15
Yesu ‘Aimarisha Haki Duniani’
1, 2. Yesu alikasirika pindi gani, na kwa nini?
YESU alikuwa amekasirika sana, na kwa sababu nzuri. Huenda ikawa vigumu kuwazia kwamba Yesu ambaye alikuwa mpole sana angeweza kukasirika. (Mathayo 21:5) Bila shaka alijidhibiti kikamili kwa kuwa hasira yake ilikuwa adilifu.a Lakini ni nini kilichomkasirisha mwanamume huyo aliyependa amani? Alikasirishwa na ukosefu mbaya wa haki.
2 Yesu alipenda mno hekalu la Yerusalemu. Lilikuwa ndilo jengo pekee takatifu ulimwenguni pote lililowekwa wakfu kwa ajili ya ibada ya Baba yake wa mbinguni. Wayahudi walisafiri kutoka nchi nyingi za mbali ili kuabudu huko. Hata watu wasio Wayahudi ambao walimcha Mungu walikuja katika ua wa hekalu uliotengwa kwa ajili yao. Lakini mapema katika huduma yake, Yesu aliingia hekaluni na kuona hali yenye kusikitisha sana. Hekalu lilikuwa kama soko badala ya kuwa nyumba ya ibada! Umati mkubwa wa wafanyabiashara na wavunja-fedha ulijaa hekaluni. Lakini kulikuwaje na ukosefu wa haki? Watu hao waliona hekalu la Mungu kuwa mahali pa kuwalaghai watu—hata kuwaibia. Jinsi gani?—Yohana 2:14.
3, 4. Ni ulaghai gani wa pupa ulioendelea katika nyumba ya Yehova, na Yesu alichukua hatua gani kuukomesha?
3 Viongozi wa kidini walikuwa wameamua kwamba ni aina moja tu ya sarafu ingeweza kutumiwa kulipa kodi ya hekalu. Wageni walilazimika kuvunja fedha zao ili kupata sarafu hizo. Kwa hiyo, wavunja-fedha walifanyia kazi yao hekaluni, na walitoza malipo fulani kwa ajili ya kuvunja fedha. Biashara ya kuuza wanyama ilileta faida kubwa pia. Wageni waliotaka kutoa dhabihu wangeweza kununua wanyama kutoka kwa mfanyabiashara yeyote mjini, lakini huenda wakuu wa hekalu wangekataa dhabihu hizo eti hazifai. Lakini, walikubali mara moja wanyama wa dhabihu walionunuliwa hekaluni. Nyakati nyingine watu hao wasio na uwezo waliuziwa wanyama kwa bei ghali sana.b Biashara hiyo ilikuwa mbaya kuliko ulaghai. Ulikuwa unyang’anyi!
“Ondoleeni mbali vitu hivi kutoka hapa!”
4 Yesu hakuweza kuvumilia ukosefu huo wa haki. Hiyo ilikuwa nyumba ya Baba yake! Alisokota mjeledi wa kamba akafukuza makundi ya ng’ombe na kondoo kutoka hekaluni. Kisha akazipindua meza za wavunja-fedha. Hebu wazia jinsi sarafu hizo zote zilivyobingirika kotekote kwenye sakafu ya marumaru! Akawaamuru hivi kwa ukali wale wauza-njiwa: “Ondoleeni mbali vitu hivi kutoka hapa!” (Yohana 2:15, 16) Yaonekana hakuna yeyote aliyethubutu kumpinga mwanamume huyo jasiri.
Mwana Humwiga Baba
5-7. (a) Maisha ya Yesu kabla ya kuwa mwanadamu yaliboreshaje sifa yake ya haki, na mfano wake unatufundisha nini? (b) Yesu amepambanaje na ukosefu wa haki kuelekea jina na enzi kuu ya Yehova?
5 Bila shaka, wafanyabiashara hao walirudi hekaluni. Miaka mitatu hivi baadaye, Yesu alishutumu tena ukosefu wao wa haki, alimnukuu Yehova ambaye aliwakemea wale waliofanya nyumba Yake kuwa “pango la wapokonyaji .” (Mathayo 21:13; Yeremia 7:11) Naam, Yesu alipoona watu wakipokonywa mali yao kwa pupa na hekalu la Mungu likitiwa unajisi, alihisi kama Baba yake. Na hilo halitushangazi. Kwa sababu Yesu alifundishwa na Baba yake wa mbinguni kwa mamilioni ya miaka. Hivyo, akawa na maoni kama ya Yehova kuhusu haki. Alionyesha kikweli jinsi ambavyo mwana anamwiga kabisa baba yake. Kwa hiyo, ikiwa twataka kuelewa vizuri zaidi haki ya Yehova, hatuna budi kutafakari mfano wa Yesu Kristo.—Yohana 14:9, 10.
6 Mwana huyo mzaliwa pekee alikuwapo Shetani alipomsingizia Yehova Mungu kuwa mwongo na kutilia shaka uadilifu wa utawala Wake. Ulikuwa uchongezi mbaya kama nini! Mwana huyo pia alimsikia Shetani akidai baadaye kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumtumikia Yehova kwa sababu anampenda na bila ubinafsi. Hapana shaka kwamba mashtaka hayo ya uwongo yalimtia uchungu Mwana huyo mwadilifu. Haikosi alifurahi sana alipojua kwamba angetimiza kazi muhimu sana ya kufutilia mbali mashtaka hayo ya uwongo! (2 Wakorintho 1:20) Angefanyaje hivyo?
7 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 14, Yesu Kristo alijibu kikamili na kwa uhakika shtaka la Shetani ambalo lilitilia shaka uaminifu wa viumbe wa Yehova. Kwa kufanya hivyo, Yesu aliweka msingi wa kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova na kutakaswa kwa jina Lake hatimaye. Akiwa Wakili Mkuu wa Yehova, Yesu ataimarisha haki Yake katika ulimwengu wote mzima. (Matendo 5:31) Vilevile, alidhihirisha haki ya Mungu kupitia maisha yake duniani. Yehova alisema hivi kumhusu: “Nitaweka roho yangu juu yake, na lililo haki atafanya kuwa wazi kwa mataifa.” (Mathayo 12:18) Yesu alitimizaje maneno hayo?
Yesu Afafanua “Lililo Haki”
8-10. (a) Mapokeo ya viongozi wa kidini Wayahudi yaliwadharau wanawake na watu wasio Wayahudi jinsi gani? (b) Mapokeo yaliifanyaje sheria ya Yehova ya Sabato iwe yenye kulemea?
8 Yesu aliipenda Sheria ya Yehova, naye aliishi kupatana nayo. Lakini viongozi wa kidini wa siku zake waliipotosha Sheria hiyo na kuitumia vibaya. Yesu aliwaambia hivi: “Ole wenu nyinyi, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! . . . Mmepuuza mambo yenye uzito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.” (Mathayo 23:23) Ni wazi kabisa kwamba walimu hao wa Sheria ya Mungu hawakuwa wakionyesha wazi “lililo haki.” Badala yake, walikuwa wakiipotosha haki ya Mungu. Jinsi gani? Fikiria mifano kadhaa.
9 Yehova aliwaagiza watu wake wajitenge na mataifa jirani ya kipagani. (1 Wafalme 11:1, 2) Hata hivyo, viongozi fulani washupavu wa kidini waliwatia watu moyo wawachukie watu wote wasio Wayahudi. Mishnah ilikuwa na sheria hii: “Ngo’mbe hawapaswi kuachwa kwenye hoteli ya watu wasio Wayahudi kwa sababu wanashukiwa kufanya ngono na wanyama.” Chuki yao kwa watu wote wasio Wayahudi ilikiuka haki na kusudi la Sheria ya Musa. (Mambo ya Walawi 19:34) Sheria nyingine zilizotungwa na wanadamu ziliwadharau wanawake. Mapokeo yalisema kwamba mke anapaswa kutembea nyuma ya mume wake wala si kando yake. Mwanamume hakuruhusiwa kuongea na mwanamke hadharani, hata iwe ni mke wake. Wanawake hawakuruhusiwa kutoa ushahidi kortini, hali moja na watumwa. Hata kulikuwa na sala maalumu ambayo wanaume walitoa na kumshukuru Mungu kwamba hawakuwa wanawake.
10 Viongozi hao wa kidini walificha Sheria ya Mungu kwa sheria na maagizo mengi sana yaliyotungwa na wanadamu. Kwa mfano, sheria ya Sabato ilikataza kazi isifanywe siku ya Sabato. Siku hiyo ilitengwa kwa ajili ya ibada, burudisho la kiroho, na kupumzika. Lakini Mafarisayo waliifanya sheria hiyo iwe yenye kulemea. Wao ndio walioamua mambo hususa ambayo yangeonwa kuwa “kazi.” Walitaja kihususa shughuli 39 kuwa kazi, kama vile kuvuna au kuwinda. Mambo hayo yalizusha maswali mengi sana. Je, mtu aliyemwua kiroboto siku ya Sabato, alikuwa akiwinda? Je, mtu aliyekwanyua punje chache ili ale akitembea, alikuwa akivuna? Je, mtu aliyemponya mgonjwa, alikuwa akifanya kazi? Walitunga sheria nyingi ngumu ambazo zilijibu maswali hayo.
11, 12. Yesu alipingaje mapokeo yasiyo ya kimaandiko ya Mafarisayo?
11 Katika hali hizo, Yesu aliwasaidiaje watu kuelewa maana ya haki? Kwa ujasiri, Yesu aliwashutumu viongozi hao wa kidini kupitia mafundisho na maisha yake. Kwanza angalia baadhi ya mafundisho yake. Alilaani waziwazi sheria zao nyingi zilizotungwa na wanadamu, aliposema hivi: “Mwalibatilisha neno la Mungu kwa mapokeo yenu ambayo nyinyi mlikabidhiwa.”—Marko 7:13.
12 Yesu alifundisha waziwazi kwamba Mafarisayo hawakuelewa sheria ya Sabato—na hata hawakufahamu kusudi la sheria hiyo. Aliwaambia kwamba Mesiya ni “Bwana wa sabato” na kwa hiyo alikuwa na haki ya kuwaponya watu siku ya Sabato. (Mathayo 12:8) Alikazia jambo hilo kwa kuwaponya watu kimuujiza na waziwazi siku ya Sabato. (Luka 6:7-10) Maponyo hayo yalionyesha maponyo ambayo atafanya duniani pote wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja. Miaka hiyo Elfu itakuwa Sabato kuu, wakati ambapo wanadamu wote waaminifu watapumzika hatimaye baada ya kulemewa na dhambi na kifo kwa karne nyingi sana.
13. Ni sheria gani iliyoanza mwishoni mwa huduma ya Kristo duniani, na ilitofautianaje na Sheria ya Musa?
13 Yesu pia alionyesha wazi lililo haki kupitia sheria mpya, “sheria ya Kristo,” ambayo ilianza mwishoni mwa huduma yake duniani. (Wagalatia 6:2) Tofauti na Sheria ya Musa, sheria hii mpya ilitegemea hasa kanuni wala si amri nyingi zilizoandikwa. Hata hivyo, ilitia ndani amri fulani za moja kwa moja. Yesu aliita mojawapo ya amri hizo “amri mpya.” Yesu aliwafundisha wafuasi wake wote wapendane kama alivyowapenda. (Yohana 13:34, 35) Ndiyo, wote wanaoishi kupatana na “sheria ya Kristo” wangekuwa na upendo huo wa kujidhabihu.
Mfano Halisi wa Haki
14, 15. Yesu alionyeshaje kwamba alitambua mipaka ya mamlaka yake, na kwa nini hilo linatia moyo?
14 Yesu hakuwafundisha watu kuhusu upendo tu. Aliishi kupatana na “sheria ya Kristo.” Aliionyesha waziwazi katika maisha yake. Fikiria njia tatu ambazo mfano wa Yesu ulionyesha wazi lililo haki.
15 Kwanza, Yesu aliepuka kabisa ukosefu wa haki. Labda umeona kwamba mara nyingi watu wasiokamilika hutenda isivyo haki wanapokuwa na kiburi na kuvuka mipaka ya mamlaka yao. Yesu hakufanya hivyo. Pindi moja, mtu mmoja alimwendea Yesu na kumwambia: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu anigawie urithi.” Yesu alimjibuje? “Wewe mtu, nani aliyeniweka mimi rasmi hakimu au mgawaji-fungu juu ya nyinyi watu?” (Luka 12:13, 14) Je, hilo si jambo la kustaajabisha? Uwezo wa Yesu wa kufikiri na kufanya maamuzi, na hata mamlaka aliyopewa na Mungu ilizidi mamlaka ya mtu yeyote duniani; lakini, alikataa kuingilia jambo hilo kwa sababu hakuwa amepewa mamlaka hususa ya kufanya hivyo. Yesu amekuwa mnyenyekevu daima, hata kwa maelfu ya miaka aliyoishi kabla ya kuwa mwanadamu. (Yuda 9) Kwa unyenyekevu, Yesu humtumaini Yehova aamue lililo haki. Jambo hilo linaonyesha kwamba ana sifa zinazovutia.
16, 17. (a) Yesu alionyeshaje haki alipohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu? (b) Yesu alionyeshaje kwamba haki yake ilikuwa yenye rehema?
16 Pili, Yesu alionyesha haki alipohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Hakuwa na ubaguzi. Badala yake, alijitahidi sana kuwahubiria watu wa kila aina, matajiri kwa maskini. Tofauti na Yesu, Mafarisayo waliwapuuza watu maskini wa kawaida na kuwaita kwa madharau ʽam-ha·ʼaʹrets, yaani, “watu wa ardhi.” Kwa ujasiri, Yesu alipinga ukosefu huo wa haki. Alipowafundisha watu habari njema, alipokula nao, alipowalisha, alipowaponya, au hata kuwafufua, aliunga mkono haki ya Mungu ambaye anataka “watu wa namna zote” waokolewe.c—1 Timotheo 2:4.
17 Tatu, Yesu alionyesha haki yenye rehema nyingi. Alijitahidi sana kuwasaidia watenda-dhambi. (Mathayo 9:11-13) Alikuwa tayari kuwasaidia watu ambao hawangeweza kujilinda. Kwa mfano, Yesu hakuwa kama viongozi wa kidini ambao waliwashuku watu wote wasio Wayahudi. Aliwasaidia na kuwafundisha baadhi yao kwa rehema, hata ingawa alitumwa hasa kwa Wayahudi. Alikubali kumponya kimuujiza mtumishi wa ofisa mmoja wa jeshi la Roma, na kusema: “Kwa yeyote katika Israeli sijapata imani kubwa sana kadiri hii.”—Mathayo 8:5-13.
18, 19. (a) Yesu aliwaheshimu wanawake kwa njia gani? (b) Mfano wa Yesu unatusaidiaje kuona uhusiano uliopo kati ya ujasiri na haki?
18 Vilevile, Yesu hakuunga mkono maoni yaliyoenea kuhusu wanawake. Badala yake, alitenda yaliyo haki kwa ujasiri. Wanawake Wasamaria walionwa kuwa wachafu kama watu wasio Wayahudi. Hata hivyo, Yesu hakusita kumhubiria yule mwanamke Msamaria penye kisima cha Sikari. Kwa kweli, Yesu alijitambulisha waziwazi kwa mara ya kwanza kuwa Mesiya aliyeahidiwa alipoongea na mwanamke huyo. (Yohana 4:6, 25, 26) Mafarisayo walisema kwamba wanawake hawakupaswa kufundishwa Sheria ya Mungu, lakini Yesu alitumia wakati mwingi na nguvu kuwafundisha wanawake. (Luka 10:38-42) Na ingawa mapokeo yalisema kwamba wanawake hawawezi kutoa ushahidi unaoaminika, Yesu aliwaheshimu wanawake kadhaa kwa kuwapa nafasi ya pekee ya kuwa watu wa kwanza kumwona baada ya kufufuliwa. Hata aliwaambia wawapashe wanafunzi wake wanaume habari za tukio hilo muhimu sana!—Mathayo 28:1-10.
19 Naam, Yesu alionyesha mataifa lililo haki. Mara nyingi alihatarisha uhai wake kwa kufanya hivyo. Mfano wa Yesu unatusaidia kuona kwamba mtu anahitaji ujasiri ili kudumisha haki ya kweli. Ndiyo sababu aliitwa ifaavyo “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda.” (Ufunuo 5:5) Kumbuka kwamba simba ni mfano ufaao wa haki yenye ujasiri. Hivi karibuni, Yesu atatekeleza haki kwa njia kubwa zaidi, “ataimarisha haki duniani” kwa ukamili zaidi.—Isaya 42:4, BHN.
Mfalme wa Kimesiya ‘Aimarisha Haki Duniani’
20, 21. Katika siku zetu, Mfalme wa Kimesiya ametekelezaje haki duniani pote na katika kutaniko la Kikristo?
20 Tangu alipowekwa kuwa Mfalme wa Kimesiya mwaka wa 1914, Yesu ametekeleza haki duniani. Jinsi gani? Amekuwa na jukumu la kuhakikisha kwamba unabii aliotoa kwenye Mathayo 24:14 unatimizwa. Wafuasi wa Yesu duniani wamewafundisha watu wa nchi zote ukweli kuhusu Ufalme wa Yehova. Kama Yesu, wamehubiri bila ubaguzi na kwa njia ya haki, wakijitahidi kumpa kila mtu—mtoto kwa mzee, tajiri kwa maskini, wanaume kwa wanawake—nafasi ya kumjua Yehova, Mungu wa haki.
21 Yesu, ambaye ni Kichwa cha kutaniko la Kikristo, anatekeleza haki kutanikoni pia. Kama ilivyotabiriwa, anatoa “zawadi zikiwa wanadamu,” yaani, wazee Wakristo waaminifu ambao wanaliongoza kutaniko. (Waefeso 4:8-12) Wanaume hao wanafuata mfano wa Yesu Kristo katika kutekeleza haki wanapolichunga kundi la Mungu lenye thamani sana. Daima wanakumbuka kwamba Yesu anataka kondoo wake watendewe kwa haki bila kujali cheo, umaarufu, au hali yao ya kifedha.
22. Yehova anahisije kuhusu ukosefu wa haki ulioenea ulimwenguni leo, na amemteua Mwanaye achukue hatua gani?
22 Hata hivyo, hivi karibuni Yesu ataimarisha haki duniani kwa njia isiyo na kifani. Ukosefu wa haki umeenea sana katika ulimwengu huu wenye ufisadi. Kila mtoto anayekufa njaa, hufa kwa sababu ya ukosefu wa haki usiovumilika hasa tunapozingatia kwamba pesa nyingi sana na wakati hutumiwa kutengeneza silaha za vita na kutosheleza tamaa za ubinafsi za watu wanaopenda raha. Mamilioni ya watu wanaokufa bure kila mwaka ni mojawapo tu ya mambo mengi yanayoonyesha ukosefu wa haki uliopo. Mambo hayo yote huchochea hasira adilifu ya Yehova. Amemteua Mwanaye apigane vita ya haki dhidi ya mfumo huu mwovu wa mambo na kukomesha kabisa ukosefu wote wa haki.—Ufunuo 16:14, 16; 19:11-15.
23. Baada ya Har-Magedoni, Kristo ataletaje haki kwa umilele wote?
23 Lakini ili kutekeleza haki Yehova anahitaji kufanya mengi zaidi kuliko kuwaangamiza tu waovu. Amemteua pia Mwanaye atawale akiwa “Mfalme wa Amani.” Baada ya vita ya Har-Magedoni, utawala wa Yesu utaleta amani duniani pote, naye atatawala “kwa haki.” (Isaya 9:6, 7) Ndipo Yesu atakapofurahi kukomesha ukosefu wote wa haki ambao umesababisha mateso na maumivu mengi sana ulimwenguni. Atadumisha kwa uaminifu haki kamilifu ya Yehova kwa umilele wote. Basi, ni muhimu kwetu kujitahidi kuiga haki ya Yehova sasa. Hebu tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.
a Katika kuonyesha hasira adilifu, Yesu alimwiga Yehova, aliye “mwingi wa hasira” kuelekea uovu wote. (Nahumu 1:2) Kwa mfano, baada ya Yehova kuwaambia watu wake waasi kwamba walikuwa wamefanya nyumba yake kuwa “pango la wanyang’anyi,” alisema hivi: “Hasira yangu na ghadhabu yangu zitamwagwa juu ya mahali hapa.”—Yeremia 7:11, 20.
b Mishnah inasema kwamba miaka kadhaa baadaye watu walilalamika kwa sababu njiwa waliuzwa kwa bei ghali sana hekaluni. Kisha bei ikapunguzwa mara moja kwa asilimia 99! Ni nani waliopata faida kubwa kutokana na biashara hiyo yenye ufanisi? Wanahistoria fulani wanadokeza kwamba masoko ya hekaluni yalimilikiwa na jamaa ya Anasi yule Kuhani wa Cheo cha Juu. Jamaa hiyo ya kikuhani ilipata ufanisi mkubwa sana kutokana na masoko hayo.—Yohana 18:13.
c Mafarisayo waliamini kwamba watu wa hali ya chini, ambao hawakujua Sheria, walikuwa watu “waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Walisema kwamba mtu hakupaswa kuwafundisha watu hao wala kufanya biashara nao wala kula nao wala kusali nao. Walisema kwamba mtu akimruhusu binti yake aolewe na mmoja wao lingekuwa jambo baya kuliko kumpeleka kwa wanyama wakali sana. Waliamini kwamba watu hao wa hali ya chini hawatafufuliwa.
-
-
‘Tenda Haki’ Unapotembea na MunguMkaribie Yehova
-
-
Sura ya 16
‘Tenda Haki’ Unapotembea na Mungu
1-3. (a) Kwa nini tunapaswa kumshukuru sana Yehova? (b) Mwokozi wetu mwenye upendo anataka tufanye nini?
JIWAZIE ukiwa ndani ya meli inayozama. Unapoanza kukata tamaa, mtu fulani anawasili na kukuokoa. Unafurahi kama nini mtu huyo anapokuokoa na kusema: “Sasa uko salama”! Je, hungemshukuru sana mtu huyo? Kwa kweli, ungekufa kama hangekuokoa.
2 Kwa njia fulani, mfano huo waonyesha jambo ambalo Yehova ametufanyia. Tunapaswa kumshukuru kwelikweli, kwa sababu ameandaa fidia ambayo inatuwezesha kuokolewa kutoka kwa utumwa wa dhambi na kifo. Tunajihisi tukiwa salama kwa sababu tunajua kwamba maadamu tunadhihirisha imani katika dhabihu hiyo yenye thamani, dhambi zetu zinasamehewa na tunakuwa na tumaini hakika la kuishi milele. (1 Yohana 1:7; 4:9) Kama tulivyoona katika Sura ya 14, fidia ni wonyesho mkuu zaidi wa upendo na haki ya Yehova. Tunapaswa kuionaje?
3 Inafaa tuchunguze mambo ambayo Mwokozi wetu mwenye upendo anataka tufanye. Yehova anasema hivi kupitia nabii Mika: “Amekuonyesha, Ee mutu, nini ni njema, na BWANA anataka nini kwako ila kutenda haki, na kupenda rehema na kutembea kwa unyenyekevu na Mungu wako?” (Mika 6:8, ZSB) Ona kwamba mojawapo ya mambo ambayo Yehova anataka tufanye ni “kutenda haki.” Tutafanyaje hivyo?
Kufuatia “Uadilifu wa Kweli”
4. Tunajuaje kwamba Yehova anatutarajia tuishi kupatana na kanuni zake za uadilifu?
4 Yehova anatutarajia tuishi kupatana na kanuni zake za mema na mabaya. Kwa kuwa kanuni zake ni za haki na za uadilifu, tunapozitii tunafuatia haki na uadilifu. Andiko la Isaya 1:17, ZSB, lasema: “Mujifundishe kufanya mema; mutafute hukumu za haki.” Neno la Mungu linatuhimiza ‘tutafute haki.’ (Sefania 2:3) Linatusihi pia ‘tuvae utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli.’ (Waefeso 4:24) Uadilifu wa kweli, au haki ya kweli, huchukia jeuri, uovu, na ukosefu wa adili, kwa sababu mambo hayo huchafua mambo matakatifu.—Zaburi 11:5; Waefeso 5:3-5.
5, 6. (a) Kwa nini si vigumu kwetu kuishi kupatana na kanuni za Yehova? (b) Biblia inaonyeshaje kwamba kufuatia uadilifu ni jambo lenye kuendelea?
5 Je, ni vigumu kwetu kuishi kupatana na kanuni za Yehova za uadilifu? La. Mtu anayempenda Yehova haoni matakwa Yake kuwa yenye kulemea. Tunataka kuishi kwa njia inayomfurahisha Mungu wetu kwa sababu tunampenda na tunapenda sifa zake. (1 Yohana 5:3) Kumbuka kwamba Yehova “apenda matendo ya haki.” (Zaburi 11:7) Ikiwa tunataka kuiga kikweli haki au uadilifu wa Mungu, ni lazima tupende mambo ambayo Yehova anapenda na kuchukia yale anayochukia.—Zaburi 97:10.
6 Si rahisi kwa wanadamu wasiokamilika kufuatia uadilifu. Ni lazima tuvue utu wa zamani pamoja na mazoea yake maovu na kujivika utu mpya. Biblia inasema kwamba utu huo mpya “unafanywa kuwa mpya” kupitia ujuzi sahihi. (Wakolosai 3:9, 10) Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “-fanywa kuwa mpya” yanaonyesha kwamba kujivika utu mpya ni jambo lenye kuendelea, ambalo linahitaji jitihada kubwa. Hata tukijitahidi kadiri gani kufanya yaliyo mema, nyakati nyingine tunakosea katika mawazo, maneno, au matendo kwa sababu ya hali yetu ya dhambi.—Waroma 7:14-20; Yakobo 3:2.
7. Tunahitaji kuonaje vipingamizi tunavyokabili tunapojitahidi kufuatia uadilifu?
7 Tunahitaji kuonaje vipingamizi tunavyokabili tunapojitahidi kufuatia uadilifu? Bila shaka hatungetaka kupunguza uzito wa dhambi. Hata hivyo, hatupaswi kamwe kukata tamaa, na kuhisi kwamba hatufai kumtumikia Yehova kwa sababu ya kasoro zetu. Mungu wetu mwenye fadhili amefanya mipango ili kuwasamehe wale wanaotubu kikweli. Fikiria maneno haya yenye kutia moyo ya mtume Yohana: “Nawaandikia nyinyi mambo haya ili msifanye dhambi.” Kisha akataja jambo hili hakika: “Na bado, ikiwa yeyote afanya hasa dhambi [kwa sababu ya kurithi kutokamilika], tuna msaidiaji kwa Baba, Yesu Kristo.” (1 Yohana 2:1) Naam, Yehova ametoa dhabihu ya fidia ya Yesu ili tuweze kumtumikia kwa njia inayofaa licha ya hali yetu ya dhambi. Je, hilo halituchochei kujitahidi kabisa kumpendeza Yehova?
Habari Njema na Haki ya Mungu
8, 9. Kuhubiriwa kwa habari njema kunaonyeshaje haki ya Yehova?
8 Tunaweza kutenda haki—hata kuiga haki ya Mungu—kwa kushiriki kikamili katika kazi ya kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Haki ya Yehova inahusianaje na habari njema?
9 Yehova hataharibu mfumo huu mwovu kabla onyo halijatolewa. Yesu alisema hivi alipotabiri kuhusu matukio ya siku za mwisho: “Katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Marko 13:10; Mathayo 24:3) Neno “kwanza” linamaanisha kwamba kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote itatangulia matukio mengine. Matukio hayo yatia ndani dhiki kubwa iliyotabiriwa, wakati ambapo waovu wataharibiwa ili ulimwengu mpya wenye uadilifu uwepo. (Mathayo 24:14, 21, 22) Bila shaka, hakuna mtu awaye yote anayeweza kudai kwamba Yehova anawaonea waovu. Kwa kuagiza onyo litolewe, anawapa waovu muda wa kutosha wa kubadili njia zao ili wasiangamizwe.—Yona 3:1-10.
Tunaonyesha haki ya Mungu tunapowahubiria wengine habari njema bila ubaguzi
10, 11. Tunaonyeshaje haki ya Mungu tunapohubiri habari njema?
10 Tunaonyeshaje haki ya Mungu tunapohubiri habari njema? Kwanza kabisa, inafaa tufanye yale tuwezayo ili kuwasaidia wengine wapate wokovu. Fikiria tena ule mfano wa kuokolewa kutoka kwenye meli inayozama. Bila shaka ukiwa salama kwenye mashua ya kuokolea, ungejitahidi kuwasaidia wengine ambao wangali baharini. Vivyo hivyo, tuna wajibu wa kuwasaidia wale ambao wangali wanatapatapa katika “bahari” ya ulimwengu huu mwovu. Ni kweli kwamba wengi hukataa ujumbe wetu. Lakini maadamu Yehova anaendelea kuwa mwenye subira, tuna wajibu wa kuwapa nafasi ya ‘kufikia toba’ na hivyo kuwa na tumaini la kupata wokovu.—2 Petro 3:9.
11 Tunapowahubiria watu wote tunaokutana nao habari njema, tunaonyesha haki katika njia nyingine muhimu sana: Kutoonyesha ubaguzi. Kumbuka kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Tunaweza tu kuiga haki Yake kwa kutoonyesha ubaguzi. Badala yake, tunapaswa kuwahubiria wengine habari njema bila kujali kabila lao, cheo chao katika jamii, au hali yao ya kifedha. Hivyo, tunawapa watu wote nafasi ya kusikia na kukubali habari njema.—Waroma 10:11-13.
Jinsi Tunavyowatendea Wengine
12, 13. (a) Kwa nini hatupaswi kufanya haraka kuwahukumu wengine? (b) Shauri la Yesu la ‘kukoma kuhukumu’ na ‘kukoma kulaumu’ linamaanisha nini? (Ona pia kielezi-chini.)
12 Tunaweza pia kuonyesha haki kwa kuwatendea wengine jinsi Yehova anavyotutendea. Ni rahisi sana kuwahukumu wengine, kuchambua makosa yao na kutilia shaka nia yao. Lakini ni nani kati yetu angependa Yehova achambue nia yake na kasoro zake bila huruma? Yehova hatutendei hivyo. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Kama wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zaburi 130:3) Je, hatuthamini kwamba Mungu wetu mwenye haki na mwenye rehema hakazii fikira makosa yetu? (Zaburi 103:8-10) Hivyo basi, tunapaswa kuwatendeaje wengine?
13 Tukielewa kwamba haki ya Mungu ni yenye rehema, hatutafanya haraka kuwahukumu wengine katika mambo ambayo hayatuhusu au mambo yasiyo na maana sana. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alionya hivi: “Komeni kuhukumu ili msipate kuhukumiwa.” (Mathayo 7:1) Kulingana na simulizi la Luka, Yesu aliongezea hivi: “Komeni kulaumu, nanyi hamtalaumiwa kwa vyovyote.”a (Luka 6:37) Yesu alitambua kwamba wanadamu wasiokamilika wana mwelekeo wa kuhukumu-hukumu. Msikilizaji yeyote aliyekuwapo mwenye tabia ya kuhukumu-hukumu wengine vikali alipaswa kukoma kufanya hivyo.
14. Kwa nini tunapaswa ‘kukoma kuhukumu’ wengine?
14 Kwa nini ni lazima ‘tukome kuhukumu’ wengine? Kwanza, mamlaka yetu ina mipaka. Mwanafunzi Yakobo atukumbusha hivi: “Mmoja yuko ambaye ni mpaji-sheria na hakimu,” yaani, Yehova. Kisha Yakobo anauliza hivi waziwazi: “Wewe ni nani uwe ukihukumu jirani yako?” (Yakobo 4:12; Waroma 14:1-4) Isitoshe, ni rahisi sana kuwahukumu wengine isivyo haki kwa sababu sisi ni wenye dhambi. Mitazamo na mielekeo mbalimbali—kama vile ubaguzi, kuudhika, wivu, na kujiona kuwa mwadilifu—inaweza kupotosha maoni yetu juu ya wanadamu wengine. Hatutafanya haraka kutafuta makosa ya wengine ikiwa tutakumbuka kwamba hata sisi tuna udhaifu. Hatuwezi kusoma mioyo; wala hatuwezi kujua kikamili hali za wengine. Basi, sisi ni nani hata tuwatilie shaka waamini wenzetu au kuchambua jitihada zao za kumtumikia Mungu? Itakuwa vyema tukimwiga Yehova kwa kukazia fikira mambo mazuri ambayo ndugu na dada zetu wanafanya badala ya kutafuta tu kasoro zao.
15. Waabudu wa Yehova hawapaswi kamwe kutenda kwa njia gani na kutumia maneno ya aina gani, na kwa nini?
15 Vipi kuhusu watu wa familia yetu? Inasikitisha kwamba leo hukumu kali zaidi hutolewa nyumbani, mahali ambapo panapaswa kuwa na amani. Ni kawaida kusikia kuhusu waume, wake, au wazazi wakatili ambao huwatukana daima au kuwajeruhi watu wa familia yao. Lakini waabudu wa Mungu hawapaswi kamwe kutumia maneno makali, kufanya mzaha wenye kuumiza, au kuwajeruhi wengine. (Waefeso 4:29, 31; 5:33; 6:4) Shauri la Yesu la ‘kukoma kuhukumu’ na ‘kukoma kulaumu’ linapasa kufuatwa nyumbani pia. Kumbuka kwamba kuonyesha haki kunatia ndani kuwatendea wengine jinsi Yehova anavyotutendea. Na Mungu wetu hatutendei kamwe kwa ukali au kwa ukatili. Badala yake, yeye “ni mwenye wororo sana katika shauku” kwa wale wanaompenda. (Yakobo 5:11) Yeye ni mfano bora sana wa kuiga!
Wazee Wanaotumikia “kwa Haki”
16, 17. (a) Yehova anawatarajia wazee wafanye nini? (b) Ni hatua gani inayopasa kuchukuliwa mtenda-dhambi anapokataa kuonyesha toba ya kweli, na kwa nini?
16 Sote tuna wajibu wa kuonyesha haki, lakini wazee katika kutaniko la Kikristo wana wajibu wa pekee wa kufanya hivyo. Hebu ona maelezo ya kiunabii yaliyoandikwa na Isaya kuhusu “wakuu,” au wazee: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu (“haki,” NW).” (Isaya 32:1) Naam, Yehova anawatarajia wazee watumikie kwa njia ya haki. Wanaweza kufanya hivyo jinsi gani?
17 Wanaume hao wenye sifa za ustahili wa kiroho wanajua kwamba ili kudumisha haki, au uadilifu, ni lazima wadumishe usafi kutanikoni. Nyakati nyingine, wazee wanalazimika kuwahukumu wale wanaotenda dhambi nzito. Wanapofanya hivyo, wanakumbuka kwamba Mungu huonyesha haki na rehema inapowezekana. Kwa hiyo, wanajaribu kumsaidia mtenda-dhambi aonyeshe toba. Lakini vipi ikiwa mtenda-dhambi anakataa kuonyesha toba ya kweli licha ya jitihada za kumsaidia? Neno la Yehova linaagiza kwamba hatua thabiti ya haki ichukuliwe: “Ondoeni yule mtu mwovu miongoni mwenu wenyewe.” Hilo lamaanisha kumtenga na ushirika wa kutaniko. (1 Wakorintho 5:11-13; 2 Yohana 9-11) Wazee wanahuzunika sana wanapolazimika kuchukua hatua hiyo, lakini wanatambua kwamba ni sharti wafanye hivyo ili kudumisha usafi wa kiadili na wa kiroho wa kutaniko. Hata hivyo, wanatumaini kwamba siku moja mtenda-dhambi huyo atarudiwa na fahamu na kurejea kutanikoni.—Luka 15:17, 18.
18. Wazee wanakumbuka nini wanapowashauri wengine kwa kutegemea Biblia?
18 Kutumikia kwa njia ya haki kunatia ndani pia kutoa shauri linalotegemea Biblia inapohitajika. Bila shaka, wazee hawajaribu kutafuta kasoro za wengine. Wala hawatumii kila nafasi wanayopata ili kutoa shauri. Lakini mwamini mwenzao anaweza ‘kuchukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua.’ Wazee ‘watajaribu kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole’ huku wakikumbuka kwamba Mungu anatekeleza haki kwa kujali hisia za wengine wala si kwa ukatili. (Wagalatia 6:1) Kwa hiyo, wazee hawatamfokea mkosaji wala kumshutumu kwa maneno makali. Badala yake, mtu hutiwa moyo na shauri linalotolewa kwa njia ya upendo. Hata wanapotoa shauri la moja kwa moja linaloonyesha waziwazi matokeo ya kufuata mwenendo usiofaa, wazee wanakumbuka kwamba mwamini mwenzao aliyekosea ni kondoo wa kundi la Yehova.b (Luka 15:7) Shauri au karipio linapotolewa kwa njia ya upendo, yaelekea kwamba litamrekebisha mkosaji.
19. Wazee hufanya maamuzi gani, na maamuzi hayo yanapasa kutegemea nini?
19 Mara nyingi wazee hufanya maamuzi yanayowahusu waamini wenzao. Kwa mfano, pindi kwa pindi wazee hukutana ili kuona iwapo ndugu wengine kutanikoni wanastahili kupendekezwa kuwa wazee au watumishi wa huduma. Wazee wanajua umuhimu wa kutopendelea. Wanafuata matakwa ya Mungu wanapowapendekeza wengine, na hawategemei maoni yao binafsi. Hivyo, wanaamua “bila kuhukumu mapema, bila kufanya jambo lolote kulingana na mwelekeo wenye kuegemea upande.”—1 Timotheo 5:21.
20, 21. (a) Wazee wanajitahidi kuwa nini, na kwa nini? (b) Wazee wanawezaje kusaidia “nafsi zilizoshuka moyo”?
20 Wazee huonyesha haki ya Mungu katika njia nyinginezo pia. Baada ya kutabiri kwamba wazee wangetumikia “kwa haki,” Isaya aliongeza hivi: “Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:2) Basi, wazee hujitahidi kuwafariji na kuwaburudisha waabudu wenzao.
21 Wengi wanahitaji kutiwa moyo leo kwa sababu ya matatizo mengi ambayo yanavunja moyo. Wazee, mnawezaje kusaidia “nafsi zilizoshuka moyo”? (1 Wathesalonike 5:14) Wasikilizeni mkiwa na hisia-mwenzi. (Yakobo 1:19) Huenda wakataka kuzungumza na mtu fulani wanayemtumaini kuhusu “wasiwasi” ulio katika moyo wao. (Mithali 12:25, BHN) Wahakikishieni kwamba wanahitajiwa, wanathaminiwa, na wanapendwa na Yehova na vilevile na ndugu na dada zao. (1 Petro 1:22; 5:6, 7) Zaidi ya hayo, mnaweza kusali pamoja nao na kwa ajili yao. Wanaweza kupata faraja sana wanapomsikia mzee akisali kwa hisia sana kwa niaba yao. (Yakobo 5:14, 15) Mungu mwenye haki anathamini jitihada zenu za upendo za kuwasaidia walioshuka moyo.
Wazee huonyesha haki ya Yehova wanapowatia moyo wale walioshuka moyo
22. Tunaweza kuiga haki ya Yehova katika njia zipi, na matokeo yatakuwa nini?
22 Kwa kweli, tunamkaribia Yehova zaidi tunapoiga haki yake! Tunaonyesha haki ya Mungu tunapofuata kanuni zake za haki, tunapowahubiria wengine habari njema zinazookoa uhai, na tunapokazia fikira mambo mazuri ambayo wengine wanafanya badala ya kutafuta kasoro zao. Wazee, mnaonyesha haki ya Mungu mnapodumisha usafi wa kutaniko, mnapotoa shauri la Kimaandiko lenye kujenga, mnapofanya maamuzi bila kupendelea, na mnapowatia moyo wale walioshuka moyo. Akiwa mbinguni, Yehova anafurahi kama nini kuona watu wake wakijitahidi kabisa “kutenda haki” wanapotembea na Mungu wao!
a Tafsiri nyingine husema “usihukumu” na “usilaumu.” Tafsiri hizo humaanisha “usianze kuhukumu” na “usianze kulaumu.” Hata hivyo, waandishi wa Biblia waliandika amri hizo katika njeo ya wakati uliopo ili kuonyesha kitendo kinachoendelea. Kwa hiyo, matendo hayo yalikuwa yakiendelea lakini yalihitaji kukoma kabisa.
b Kwenye 2 Timotheo 4:2, Biblia inasema kwamba nyakati nyingine ni lazima wazee ‘wakaripie, wakemee, na kuhimiza kwa bidii.’ Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “himiza kwa bidii” (pa·ra·ka·leʹo) linaweza kumaanisha “kutia moyo.” Neno jingine la Kigiriki linalohusiana nalo, pa·raʹkle·tos, linaweza kumaanisha wakili wa kisheria. Kwa hiyo, hata wakati wazee wanapokaripia kwa uthabiti, wanapaswa kuwa wasaidizi wa wale wanaohitaji msaada wa kiroho.
-
-
‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 17
‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’
1, 2. Kusudi la Yehova kwa siku ya saba lilikuwa nini, na hekima Yake ilijaribiwaje mwanzoni mwa siku hiyo?
WAMEHARIBIKA! Wanadamu, upeo wa fahari ya siku ya sita ya uumbaji, walitumbukia ghafula katika hali mbaya yenye kusikitisha. Yehova alikuwa ametangaza kwamba “kila kitu alichokifanya,” kutia ndani mwanadamu, “ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Lakini mwanzoni mwa siku ya saba, Adamu na Hawa waliamua kumfuata Shetani katika uasi. Wakatumbukia katika dhambi, kutokamilika, na kifo.
2 Huenda ilionekana kwamba kusudi la Yehova kwa siku ya saba lilikuwa limeenda mrama kabisa. Siku hiyo, kama siku sita zilizotangulia, ingekuwa na urefu wa maelfu ya miaka. Yehova alikuwa ameitangaza kuwa takatifu. Hatimaye katika siku hiyo, dunia yote ingekuwa paradiso iliyojaa wanadamu wakamilifu. (Mwanzo 1:28; 2:3) Lakini kusudi hilo lingetimizwaje baada ya ule uasi ulioleta msiba? Mungu angechukua hatua gani? Wakati huo, hekima ya Yehova ilijaribiwa kwa njia isiyo na kifani—labda hilo ndilo lililokuwa jaribu kuu zaidi.
3, 4. (a) Kwa nini hatua ambayo Yehova alichukua baada ya uasi katika Edeni inaonyesha hekima yake yenye kutia kicho? (b) Kwa unyenyekevu, tunapaswa kukumbuka jambo gani hakika tunapojifunza juu ya hekima ya Yehova?
3 Yehova alichukua hatua mara moja. Aliwahukumu hao waasi katika Edeni, na wakati huohuo, akatangaza tumaini zuri la wakati ujao: alikusudia kukomesha taabu ambazo walikuwa wameanzisha tu. (Mwanzo 3:15) Kusudi la Yehova la muda mrefu lilianzia Edeni na kuendelea kwa maelfu ya miaka ambayo mwanadamu amekuwapo, na litaendelea hadi wakati ujao. Ni kusudi rahisi sana lakini lenye mambo mengi muhimu hivi kwamba msomaji wa Biblia anaweza kufurahia kujifunza kusudi hilo na kulitafakari maisha yake yote. Isitoshe, hapana shaka yoyote kwamba kusudi la Yehova litafanikiwa. Litakomesha kabisa uovu, dhambi, na kifo. Mungu anakusudia kuwafanya wanadamu waaminifu wawe wakamilifu. Mambo hayo yote yatatukia kabla ya siku ya saba kwisha. Yehova atakuwa ametimiza kusudi lake kuhusu dunia na wanadamu kwa wakati barabara licha ya vipingamizi vyote!
4 Hekima ya aina hiyo inatutia kicho, sivyo? Mtume Paulo alichochewa kuandika hivi: ‘Lo! kina cha hekima ya Mungu!’ (Waroma 11:33) Tunapojifunza wonyesho mbalimbali wa sifa hii ya Mungu, na tukumbuke kwa unyenyekevu jambo moja hakika—kwamba hatuwezi kamwe kufahamu kikamili hekima ya Yehova yenye kina sana. (Ayubu 26:14) Kwanza, hebu tufafanue sifa hii yenye kutia kicho.
Hekima ya Mungu Ni Nini?
5, 6. Kuna uhusiano gani kati ya ujuzi na hekima, na ujuzi wa Yehova ni mwingi kadiri gani?
5 Hekima si sawa na ujuzi. Kompyuta zinaweza kuhifadhi ujuzi mwingi sana, lakini hakuna mtu anayeweza kusema kwamba mashine hizo ni zenye hekima. Hata hivyo, ujuzi na hekima zinahusiana. (Mithali 10:14) Kwa mfano, kama ungehitaji shauri la hekima ili kutibu ugonjwa hatari, je, ungemwomba msaada mtu asiye na ujuzi wowote au mwenye ujuzi wa kijuu-juu tu wa tiba? La hasha! Kwa hiyo, ujuzi sahihi ni muhimu ili kuwa na hekima ya kweli.
6 Yehova ana ujuzi usio na kikomo. Akiwa “Mfalme wa umilele,” yeye peke yake ndiye ambaye ameishi milele. (Ufunuo 15:3) Na amejua mambo yote yaliyotukia kwa miaka hiyo yote. Biblia inasema hivi: “Hakuna kiumbe kisichokuwa dhahiri machoni pake, bali vitu vyote viko uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni pake ambaye kwake sisi tuna kutoa hesabu.” (Waebrania 4:13; Mithali 15:3) Akiwa Muumba, Yehova anajua kabisa vitu alivyoumba, naye ameona utendaji wote wa wanadamu tangu mwanzo. Yeye huchunguza moyo wa kila mwanadamu, na anaona kila jambo. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Anafurahi anapoona tukifanya maamuzi ya hekima maishani kwa sababu alituumba tukiwa na hiari. Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye husikiliza sala nyingi sana kwa wakati mmoja! (Zaburi 65:2, NW) Na bila shaka Yehova ana kumbukumbu kamilifu.
7, 8. Yehova anaonyeshaje ufahamu, utambuzi, na hekima?
7 Mbali na ujuzi, Yehova ana uwezo mwingine. Anaona jinsi mambo mbalimbali yanavyohusiana, na anatambua matokeo kamili ya mambo yote. Anachanganua mambo na kufanya maamuzi, anatofautisha mema na mabaya, mambo muhimu na yasiyo muhimu. Zaidi ya hayo, hachunguzi mambo kijuujuu tu bali anachunguza ndani ya moyo. (1 Samweli 16:7) Kwa hiyo, Yehova ana ufahamu na utambuzi, sifa ambazo ni bora zaidi ya ujuzi. Lakini hekima ni bora zaidi ya sifa hizo zote.
8 Hekima ni kutumia ujuzi, utambuzi, na ufahamu ili kutekeleza jambo fulani. Kwa kweli, baadhi ya maneno ya awali ya Biblia yaliyotafsiriwa “hekima” yanamaanisha kihalisi “kufanya kazi kwa matokeo” au “hekima inayofanya kazi kwa matokeo.” Kwa hiyo, hekima ya Yehova si ya kuwazia tu, bali inafanya kazi na ina matokeo. Sikuzote Yehova hufanya maamuzi bora kabisa kwa kutumia hekima na ufahamu wake usio na mipaka, na anatekeleza maamuzi hayo kwa njia bora kabisa. Hiyo ni hekima ya kweli! Yehova anaonyesha ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kwa kazi yayo.” (Mathayo 11:19) Kazi za Yehova ulimwenguni pote huthibitisha pasina shaka yoyote kwamba ana hekima.
Uthibitisho wa Hekima ya Mungu
9, 10. (a) Yehova ana hekima ya aina gani, naye ameionyeshaje? (b) Chembe huthibitishaje hekima ya Yehova?
9 Je, umewahi kustaajabia ustadi wa fundi anayetengeneza vifaa maridadi vinavyofanya kazi vizuri? Hekima hiyo inavutia sana. (Kutoka 31:1-3) Yehova mwenyewe ndiye chanzo hasa cha hekima hiyo. Mfalme Daudi alisema hivi kumhusu Yehova: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Kwa kweli, kadiri tunavyojifunza kuhusu mwili wa mwanadamu, ndivyo tunavyozidi kutiwa kicho na hekima ya Yehova.
10 Kwa mfano: Uhai wako ulianza kwa chembe moja—mbegu ya mama yako iliungana na mbegu ya baba yako. Baada ya muda, chembe hiyo ilianza kugawanyika. Mwishowe mwili wako ukawa na chembe ndogo sana zipatazo trilioni 100. Chembe 10,000 hivi zenye ukubwa wa wastani zinaweza kutoshea kwenye kichwa kidogo sana cha pini. Lakini, kila chembe ina umbo tata sana. Chembe moja ni tata sana kushinda kiwanda au mashine yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu. Wanasayansi wanasema kwamba chembe moja ni kama jiji lililozingirwa na ukuta—lenye malango yanayolindwa, lenye mfumo wa usafiri, mfumo wa mawasiliano, mitambo ya nguvu, viwanda, mifumo ya kuondoa na kusafisha maji machafu, walinzi, na hata kuna aina fulani ya makao makuu ya serikali katika kiini chake. Isitoshe, chembe inaweza kutengeneza chembe nyingine pacha kwa saa chache tu!
11, 12. (a) Ni nini kinachofanya chembe za kiini-tete kinachokua zigawanyike, na hilo linapatanaje na Zaburi 139:16? (b) Ubongo wa mwanadamu unaonyeshaje kwamba ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu’?
11 Bila shaka chembe zote hazifanani. Chembe za kiini-tete zinapoendelea kugawanyika, chembe mpya zinafanya kazi mbalimbali. Baadhi yake zitakuwa chembe za neva; nyingine zitakuwa chembe za mifupa, misuli, damu, au za macho. Utaratibu huo wa kugawanyika kwa chembe umehifadhiwa kiasili katika “maktaba” yenye ramani za chembe za urithi, DNA. Inastaajabisha kwamba Daudi aliongozwa kumwambia Yehova hivi: “Wewe uliniona hata kabla sijazaliwa, uliandika kila kitu kitabuni mwako.”—Zaburi 139:16, BHN.
12 Viungo fulani vya mwili ni tata kupindukia. Kwa mfano, fikiria ubongo wa mwanadamu. Baadhi ya watu wamesema kwamba ubongo ndicho kitu tata zaidi katika ulimwengu wote. Una chembe za neva zipatazo bilioni 100—idadi hiyo inakaribia idadi ya nyota katika kundi letu la nyota. Kila moja ya chembe hizo inaungana na maelfu ya chembe nyingine. Wanasayansi wanasema kwamba ubongo wa mwanadamu unaweza kuhifadhi habari zilizo katika maktaba zote ulimwenguni na kwamba uwezo wake haupimiki. Licha ya kuchunguza kwa miaka mingi sana ubongo ‘ulioumbwa kwa jinsi ya ajabu,’ wanasayansi wanakubali kwamba huenda wasifaulu kamwe kufahamu kikamili jinsi unavyofanya kazi.
13, 14. (a) Chungu na viumbe wengine wanaonyeshaje kwamba wana “akili nyingi sana,” na hilo linatufundisha nini kumhusu Muumba? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba vitu vilivyoumbwa kama vile utando wa buibui vimefanywa “kwa hekima”?
13 Lakini wanadamu ni mojawapo tu ya mambo yanayoonyesha hekima ya Yehova ya uumbaji. Zaburi 104:24 yasema hivi: “Ee, BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” Kila kiumbe kinadhihirisha hekima ya Yehova. Kwa mfano, chungu ana “akili nyingi sana.” (Mithali 30:24) Kwa kweli, makundi ya chungu yana utaratibu wa hali ya juu sana. Makundi fulani ya chungu hutunza, hufuga, na kupata chakula kutoka kwa wadudu fulani kana kwamba ni mifugo. Chungu wengine ni kama wakulima, wanapanda “mimea” ya kuvu. Viumbe wengine wengi wanafanya mambo yenye kustaajabisha kwa kutumia hekima ya kisilika. Nzi wa kawaida huruka kwa njia za kustaajabisha sana ambazo ndege bora ya kisasa iliyobuniwa na mwanadamu haiwezi. Ndege wanaohama huongozwa na nyota, nguvu za sumaku za dunia, au aina fulani ya ramani iliyo akilini mwao. Wanabiolojia hujifunza kwa miaka mingi tabia tata za kisilika za viumbe hao. Mungu aliyeumba viumbe hao ana hekima iliyoje!
14 Wanasayansi wamejifunza mengi kutokana na hekima ya Yehova ya uumbaji. Hata kuna elimu fulani ya uhandisi inayojaribu kuiga ubuni wa maumbile inayoitwa biomimetics. Kwa mfano, labda umewahi kustaajabia umaridadi wa utando wa buibui. Lakini mhandisi anaona kwamba utando huo umebuniwa kwa njia ya pekee sana. Tando fulani nyembamba ni ngumu kuliko chuma, ni ngumu kushinda nyuzi za mavazi yasiyopenywa na risasi. Ni ngumu kadiri gani? Hebu wazia utando wa buibui uliorefushwa kufikia ukubwa wa wavu unaovutwa na mashua ya uvuvi. Utando wa aina hiyo ungeweza kusimamisha ndege ya abiria inayosafiri kwa kasi angani! Naam, Yehova amefanya vitu hivyo vyote “kwa hekima.”
Ni nani aliyeumba viumbe hawa ambao wana “akili nyingi sana”?
Hekima ya Vitu Visivyo Duniani
15, 16. (a) Nyota zinatoa uthibitisho gani kuhusu hekima ya Yehova? (b) Wadhifa wa Yehova akiwa Amiri Mkuu wa malaika wengi sana unaonyesha nini kuhusu hekima yake akiwa Msimamizi?
15 Hekima ya Yehova inaonekana wazi katika kazi zake ulimwenguni pote. Nyota ambazo tulizungumzia kwa undani katika Sura ya 5, hazijatapakaa kiholela-holela angani. Yehova amepanga nyota kwa njia maridadi sana katika magalaksi, kwa kutumia hekima yake ya “sheria za angani.” Magalaksi hayo yamepangwa katika makundi makubwa, ambayo huungana na kufanyiza makundi mengine makubwa hata zaidi. (Ayubu 38:33, The New Jerusalem Bible) Si ajabu Yehova anasema kwamba nyota zilizo mbinguni ni kama “jeshi”! (Isaya 40:26) Hata hivyo, kuna jeshi jingine ambalo linaonyesha wazi zaidi hekima ya Yehova.
16 Kama tulivyoona katika Sura ya 4, Mungu anaitwa “BWANA wa majeshi” kwa sababu ya wadhifa wake akiwa Amiri Mkuu wa jeshi la mamia ya mamilioni ya viumbe wa roho. Hilo lathibitisha nguvu za Yehova. Hata hivyo, hekima yake inahusikaje? Fikiria hili: Yehova na Yesu wanafanya kazi daima. (Yohana 5:17) Basi, ni jambo la kiakili kwamba hata malaika wanaomtumikia Mwenye Enzi Kuu wanafanya kazi daima. Na kumbuka kwamba malaika wana wadhifa wa juu kuliko mwanadamu, wana akili na nguvu nyingi sana. (Waebrania 1:7; 2:7) Lakini Yehova amewapa malaika hao wote kazi ya kutosha. Kwa furaha na uradhi, wamekuwa ‘wakitenda neno lake’ na ‘kufanya mapenzi yake,’ kwa mabilioni ya miaka. (Zaburi 103:20, 21) Msimamizi huyo ana hekima yenye kustaajabisha sana!
Yehova Ndiye “Mwenye Hekima Peke Yake”
17, 18. Kwa nini Biblia inasema kwamba Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake,” na kwa nini hekima yake inapaswa kututia kicho?
17 Tukizingatia ushuhuda huo wote, haishangazi kwamba Biblia hutukuza hekima ya Yehova. Kwa mfano, inasema kwamba Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake.” (Waroma 16:27) Ni Yehova peke yake aliye na hekima kamili. Ndiye chanzo cha hekima yote ya kweli. (Mithali 2:6) Ndiyo sababu Yesu, ajapokuwa na hekima nyingi kushinda viumbe wote wa Yehova, hakutegemea hekima yake mwenyewe bali alisema yale aliyoagizwa na Baba yake.—Yohana 12:48-50.
18 Angalia jinsi mtume Paulo alivyofafanua hekima ya pekee ya Yehova: “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyotafutikana na njia zake zapita uwezo wa kufuatilia!” (Waroma 11:33) Neno la mshangao, “Lo!” ambalo Paulo alitaja mwanzoni mwa mstari huo, lilionyesha hisia yenye nguvu—kicho cha hali ya juu sana. Neno la Kigiriki ambalo alitumia kurejezea “kina” linahusiana sana na neno “shimo lenye kina kirefu.” Kwa hiyo, maneno yake yanatokeza picha dhahiri sana akilini. Tunapotafakari hekima ya Yehova, ni kana kwamba tunatazama katika shimo kubwa sana lisilo na mwisho, shimo lenye kina kirefu sana hivi kwamba hatuwezi kamwe kufahamu ukubwa wake, sembuse kuweka mipaka au kuchora ramani yake kwa usahihi. (Zaburi 92:5) Wazo hilo linatunyenyekeza, sivyo?
19, 20. (a) Kwa nini tai ni mfano ufaao wa hekima ya Mungu? (b) Yehova ameonyeshaje kwamba ana uwezo wa kuona matukio ya wakati ujao!
19 Yehova ni “mwenye hekima peke yake” kwa njia nyingine: Ni yeye tu anayeweza kuona matukio ya wakati ujao. Kumbuka kwamba Yehova hutumia tai mwenye uwezo wa kuona mbali kuwa mfano wa hekima yake. Tai mkubwa anaweza kuwa na uzito wa kilogramu tano tu, lakini macho yake ni makubwa kuliko macho ya mtu mzima. Tai ana uwezo bora sana wa kuona. Ndege huyo anaweza kuona mnyama mdogo sana kutoka umbali wa mamia ya meta angani, au hata mamia ya kilometa! Pindi moja, Yehova alisema hivi kumhusu tai: ‘Macho yake huangalia toka mbali.’ (Ayubu 39:29) Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuona ‘mbali’ sana. Anaweza kuona matukio ya wakati ujao!
20 Biblia ina mambo chungu nzima yanayothibitisha jambo hilo. Ina mamia ya unabii, au mambo yaliyoandikwa kabla hayajatukia. Biblia ilitabiri matokeo ya vita, kutokea na kuanguka kwa serikali kuu za ulimwengu, na hata mbinu za kivita ambazo zingetumiwa na maamiri wa jeshi. Nyakati nyingine ilitabiri matukio hayo mamia ya miaka kabla hayajatukia.—Isaya 44:25–45:4; Danieli 8:2-8, 20-22.
21, 22. (a) Kwa nini haifai kusema kwamba Yehova anajua maamuzi ambayo utafanya maishani? Toa mfano. (b) Tunajuaje kwamba Yehova hatumii hekima yake bila kujali hisia za watu?
21 Lakini je, hilo lamaanisha kwamba tayari Mungu anajua maamuzi ambayo utafanya maishani? Baadhi ya watu ambao wanafundisha kwamba maisha yetu yameamuliwa kimbele husisitiza hivyo. Hata hivyo, imani hiyo kwa kweli inadharau hekima ya Yehova, kwa kuwa inamaanisha kwamba hawezi kudhibiti uwezo wake wa kujua matukio ya wakati ujao. Kwa mfano: Kama ungekuwa mwimbaji mwenye sauti tamu sana, je, ungeimba tu kila wakati? Hilo ni wazo la kipumbavu! Vivyo hivyo, Yehova ana uwezo wa kujua matukio ya wakati ujao, lakini hatumii uwezo huo kila wakati. Akifanya hivyo huenda akaingilia uhuru wetu wa kuchagua. Uhuru huo ni zawadi yenye thamani ambayo Yehova hawezi kutunyima kamwe.—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.
22 Imani ya kwamba maisha yameamuliwa kimbele inasikitisha hata zaidi kwa sababu inadokeza kuwa hekima ya Yehova haijali hisia za watu, haiambatani na upendo, hisia-mwenzi, au huruma. Lakini hilo si kweli hata kidogo! Biblia inafundisha kwamba Yehova ni “mwenye hekima moyoni.” (Ayubu 9:4) Si kwamba ana moyo halisi, lakini mara nyingi Biblia hutumia neno hilo kumaanisha utu wa ndani kabisa, kutia ndani nia ya mtu na hisia kama vile upendo. Kwa hiyo, hekima ya Yehova, kama sifa zake nyingine, inaongozwa na upendo.—1 Yohana 4:8.
23. Hekima ya Yehova iliyo bora sana inapaswa kutuchochea kufanya nini?
23 Bila shaka, hekima ya Yehova inaweza kutumainika kabisa. Ni bora kuliko hekima yetu ndiposa Neno la Mungu linatuhimiza hivi kwa upendo: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Na tuchunguze kwa undani hekima ya Yehova ili tuweze kumkaribia zaidi Mungu wetu mwenye hekima kamili.
-
-
Hekima ya “Neno la Mungu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 18
Hekima ya “Neno la Mungu”
1, 2. Yehova ametuandikia “barua” gani, na kwa nini?
JE, UNAKUMBUKA mara ya mwisho ulipopokea barua kutoka kwa mpendwa wako anayeishi mbali sana? Kupokea barua yenye kugusa moyo kutoka kwa mtu tunayempenda ni mojawapo ya mambo yanayotufurahisha sana. Tunafurahi sana anapotujulisha hali yake, maisha yake, na mipango yake. Tunakuwa na uhusiano wa karibu na wapendwa wetu tunapowasiliana nao, hata kama wanaishi mbali.
2 Basi, hakuna jambo jingine lolote linaloweza kutufurahisha sana kama kupokea ujumbe ulioandikwa na Mungu tunayempenda. Tunaweza kusema kwamba Yehova ametuandikia “barua,” yaani, Neno lake, Biblia. Katika Biblia, anatueleza yeye ni nani, amefanya nini, anakusudia kufanya nini, na mambo mengine mengi. Yehova ametupatia Neno lake kwa sababu anataka tumkaribie. Mungu wetu mwenye hekima kamili alichagua njia bora ya kuwasiliana nasi. Biblia imeandikwa kwa njia inayoonyesha hekima isiyo na kifani, na ujumbe wake unaonyesha hekima hiyo pia.
Kwa Nini Aliandika Neno Lake?
3. Yehova alimpa Musa Sheria kwa njia gani?
3 Huenda watu fulani wakauliza, ‘Kwa nini Yehova hakuwasiliana na wanadamu kwa njia nyingine yenye kutokeza zaidi kama vile sauti kutoka mbinguni?’ Kwa kweli, nyakati nyingine Yehova aliongea kutoka mbinguni kupitia malaika. Kwa mfano, alifanya hivyo alipowapa Waisraeli Sheria. (Wagalatia 3:19) Sauti iliyotoka mbinguni ilikuwa yenye kutia kicho sana hivi kwamba Waisraeli walioshikwa na woga walimwomba Yehova asiwasiliane nao kwa njia hiyo bali awasiliane nao kupitia Musa. (Kutoka 20:18-20) Kwa hiyo, Musa alipewa Sheria yenye amri zipatazo 600, kwa njia ya mdomo, neno kwa neno.
4. Eleza kwa nini kupitisha sheria za Mungu kwa njia ya mdomo hakungetegemeka.
4 Vipi kama Sheria haingaliandikwa? Je, Musa angaliweza kukumbuka vizuri kila neno la Sheria hiyo yenye mambo mengi, kisha aiwasilishe kwa taifa hilo bila kukosea? Vipi watu wa vizazi vijavyo? Je, wangehitaji kutegemea tu yale waliyoambiwa? Kupitisha sheria za Mungu kwa njia ya mdomo hakungetegemeka. Wazia jambo ambalo linaweza kutukia iwapo utamwambia mtu mmoja hadithi fulani kisha ipitishwe kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine kwenye mlolongo wa watu wengi. Yaelekea kwamba hadithi ambayo itamfikia mtu wa mwisho katika mlolongo huo itakuwa imebadilika kabisa. Sheria ya Mungu haikukabili hatari hiyo.
5, 6. Yehova alimwagiza Musa afanye nini kuhusiana na maneno Yake, na kwa nini tunafaidika kuwa na Neno la Yehova lililoandikwa?
5 Kwa hekima Yehova aliamua maneno yake yaandikwe. Alimwagiza Musa hivi: “Andika maneno haya; kwa kuwa mimi nimefanya agano nawe, na pamoja na Israeli, kwa mujibu wa maneno haya.” (Kutoka 34:27) Kwa hiyo, Biblia ikaanza kuandikwa mnamo mwaka wa 1513 K.W.K. Kwa miaka 1,610 iliyofuata, Yehova ‘alisema katika vipindi vingi na katika njia nyingi na’ wanadamu 40 hivi ambao waliandika Biblia. (Waebrania 1:1) Ili kuhifadhi Maandiko hayo, wanakili wenye bidii walifanyiza kwa uangalifu mkubwa nakala sahihi.—Ezra 7:6; Zaburi 45:1.
6 Yehova ametubariki kwelikweli kwa kuwasiliana nasi kupitia maandiko. Je, umewahi kupokea barua uliyothamini sana—labda kwa sababu ilikupa faraja uliyohitaji sana—hivi kwamba uliitunza na kuisoma tena na tena? Ndivyo ilivyo na “barua” ambayo Yehova ametuandikia. Kwa sababu Yehova aliandika maneno yake, tunaweza kuyasoma kwa ukawaida na kuyatafakari. (Zaburi 1:2) Tunaweza kupokea “faraja kutokana na Maandiko” wakati wowote tunapoihitaji.—Waroma 15:4.
Kwa Nini AlitumiaWanadamu Kuliandika?
7. Yehova alionyeshaje hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake?
7 Yehova alionyesha hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake. Hebu fikiria: Kama Yehova angalitumia malaika kuandika Biblia, je, ingalivutia kwa njia ileile? Kwa kweli, malaika wangeeleza jinsi Yehova alivyo kulingana na maoni yao yaliyotukuka, wangeeleza jinsi wanavyojitoa kwake, na kuandika kuhusu wanadamu waliomtumikia Mungu kwa uaminifu. Lakini je, tungeweza kweli kuelewa maoni ya viumbe wakamilifu wa roho, ambao wana ujuzi, ufahamu, na uwezo wa hali ya juu kuliko sisi?—Waebrania 2:6, 7.
“Andiko lote limepuliziwa na Mungu”
8. Waandishi wa Biblia waliruhusiwa kutumia akili zao jinsi gani? (Ona pia kielezi-chini.)
8 Kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake, Yehova alitupatia kile tunachohitaji—kitabu ambacho ‘kimepuliziwa na Mungu’ lakini kinachozingatia hali ya binadamu. (2 Timotheo 3:16) Alifanyaje hivyo? Mara nyingi, inaonekana kwamba aliwaruhusu waandishi watumie akili zao katika kuchagua “maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.” (Mhubiri 12:10, 11) Ndiyo sababu Biblia imeandikwa kwa njia mbalimbali; njia hizo hutegemea malezi na utu wa kila mwandishi.a Lakini, wanadamu hao “walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Kwa hiyo, Biblia ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.
9, 10. Kwa nini kutumia wanadamu kuiandika Biblia kunaifanya ipendeze na kuvutia zaidi?
9 Biblia inapendeza na kuvutia sana kwa sababu Mungu alitumia wanadamu kuiandika. Waandishi wa Biblia walikuwa wanadamu wenye hisia kama zetu. Wakiwa wanadamu wasiokamilika, walipata majaribu na mifadhaiko kama yetu. Nyakati nyingine, roho ya Yehova iliwaongoza kuandika kuhusu hisia zao na matatizo yaliyowapata. (2 Wakorintho 12:7-10) Kwa hiyo, waliandika kama wahusika, maneno ambayo hakuna malaika angeweza kuandika.
10 Kwa mfano, fikiria Mfalme Daudi wa Israeli. Baada ya kufanya dhambi nzito sana, Daudi alitunga zaburi ambayo inaeleza mambo yaliyokuwa moyoni mwake, na jinsi alivyomwomba Mungu msamaha. Aliandika hivi: ‘Unioshe kabisa na uovu wangu, unitakase dhambi zangu. Maana nimejua mimi makosa yangu na dhambi yangu i mbele yangu daima. Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani. Usinitenge na uso wako, wala roho yako takatifu usiniondolee. Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu hutaudharau.’ (Zaburi 51:2, 3, 5, 11, 17) Je, huguswi moyo na uchungu wa mwandishi huyo? Ni mwanadamu asiyekamilika tu ndiye angeweza kuandika maneno hayo yenye kugusa moyo, sivyo?
Kwa Nini Aandike Kitabu Kinachohusu Watu?
11. Ni masimulizi gani halisi yameandikwa katika Biblia ili ‘kutufunza’?
11 Kuna jambo jingine linalofanya Biblia ivutie. Kwa kadiri kubwa, ni kitabu kinachohusu watu—watu halisi, wale waliomtumikia Mungu na wale ambao hawakumtumikia. Tunasoma kuhusu maisha yao, magumu yao, na shangwe yao. Tunaona matokeo ya maamuzi waliyofanya maishani. Masimulizi hayo yaliandikwa ili ‘kutufunza.’ (Waroma 15:4) Kupitia masimulizi hayo halisi, Yehova anatufundisha kwa njia ambazo zinatugusa mioyo. Fikiria mifano kadhaa.
12. Masimulizi ya Biblia kuhusu wanadamu wasio waaminifu yanatusaidiaje?
12 Biblia inatuambia kuhusu wanadamu wasio waaminifu, na hata waovu na mambo yaliyowapata. Masimulizi hayo yanaonyesha jinsi watu walivyoonyesha sifa zisizofaa, na hilo linatusaidia kuelewa sifa hizo. Kwa mfano, hakuna amri inayoweza kukazia kikiki ubaya wa kutokuwa mwaminifu kuliko mfano halisi wa Yudasi akipanga njama ya kumsaliti Yesu, sivyo? (Mathayo 26:14-16, 46-50; 27:3-10) Masimulizi kama hayo hugusa sana mioyo yetu, na kutusaidia kutambua na kuzitupilia mbali sifa zinazochukiza.
13. Biblia inatusaidiaje kuelewa sifa zinazofaa?
13 Biblia pia inasimulia kuhusu watumishi wengi wa Mungu waliokuwa waaminifu. Tunasoma kuhusu ujitoaji wao na uaminifu wao. Tunasoma kuhusu watu wenye sifa ambazo tunahitaji kukuza ili kumkaribia Mungu. Kwa mfano, fikiria sifa ya imani. Biblia inatuambia imani ni nini na kwa nini tunahitaji kuwa nayo ili kumpendeza Mungu. (Waebrania 11:1, 6) Lakini Biblia pia inaeleza mifano halisi ya watu waliokuwa na imani. Fikiria imani ambayo Abrahamu alionyesha alipojaribu kumtoa Isaka. (Mwanzo, sura ya 22; Waebrania 11:17-19) Masimulizi kama hayo yanatusaidia kuthamini na kuelewa vizuri zaidi maana ya neno “imani.” Ni hekima iliyoje kwamba Yehova, mbali na kutuhimiza tukuze sifa zinazofaa anatuonyesha mifano ya watu waliokuwa na sifa hizo!
14, 15. Biblia inatuambia nini kuhusu mwanamke fulani aliyekuja hekaluni, na simulizi hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?
14 Masimulizi halisi yaliyo katika Biblia mara nyingi yanatufundisha kuhusu utu wa Yehova. Fikiria simulizi la mwanamke fulani ambaye Yesu alimwona hekaluni. Alipokuwa ameketi karibu na masanduku ya hazina, Yesu aliangalia jinsi watu walivyokuwa wakitumbukiza michango yao humo. Matajiri wengi walikuja na kutumbukiza “kutokana na ziada yao.” Lakini Yesu alimtazama sana mjane mmoja maskini. Mjane huyo alitoa mchango wa “sarafu ndogo mbili, ambazo zina thamani ndogo sana.”b Alitoa fedha zote alizokuwa nazo. Yesu, ambaye alidhihirisha kikamili maoni ya Yehova, alisema hivi: ‘Mjane huyu maskini alitumbukiza ndani zaidi ya wote wale waliokuwa wakitumbukiza fedha ndani ya masanduku ya hazina.’ Kulingana na maneno hayo, alitumbukiza fedha nyingi kuliko jumla ya fedha zilizotolewa na watu wengine wote.—Marko 12:41-44; Luka 21:1-4; Yohana 8:28.
15 Je, haishangazi kwamba kati ya watu wote waliokuja hekaluni siku hiyo, ni mjane huyo peke yake ndiye aliyetajwa katika Biblia? Kupitia mfano huo, Yehova anatufundisha kwamba yeye ni Mungu anayethamini mambo tunayofanya. Anakubali kwa furaha michango tunayomtolea kwa nafsi yetu yote, pasipo kuilinganisha na michango inayotolewa na wengine. Bila shaka Yehova ametumia njia bora sana kutufundisha ukweli huo wenye kutia moyo!
Mambo Ambayo Biblia Haitaji
16, 17. Yehova anaonyeshaje hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake?
16 Unapomwandikia mpendwa wako barua, huwezi kuandika kila jambo. Kwa hiyo, unachagua kwa busara mambo ya kuandika. Vivyo hivyo, Yehova alitaja watu fulani na matukio fulani katika Neno lake. Lakini Biblia haielezi kinagaubaga kila jambo kuhusiana na masimulizi hayo. (Yohana 21:25) Kwa mfano, Biblia inapozungumzia hukumu ya Mungu, haijibu kila swali tulilo nalo kuhusu hukumu hiyo. Yehova anaonyesha pia hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake. Jinsi gani?
17 Biblia imeandikwa kwa njia inayokusudiwa kutambua mambo yaliyo moyoni mwetu. Andiko la Waebrania 4:12 lasema hivi: “Neno [au, ujumbe] la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho . . . na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” Ujumbe wa Biblia hupenya ndani kabisa, na kufunua mawazo yetu na nia yetu halisi. Wale wanaoisoma wakiwa na nia ya kuichambua mara nyingi wanakwazwa wanapopata masimulizi ambayo hayana habari ya kutosha kuwaridhisha. Watu wa aina hiyo huenda hata wakawa na shaka kwamba Yehova ni mwenye upendo, hekima na haki.
18, 19. (a) Kwa nini hatupaswi kutatanika wakati simulizi fulani la Biblia linazusha maswali ambayo hatuwezi kujibu mara moja? (b) Tunahitaji kufanya nini ili kufahamu Neno la Mungu, na jambo hilo linaonyeshaje hekima kuu ya Yehova?
18 Kwa upande mwingine, tunapojifunza Biblia kwa uangalifu na kwa unyofu, tunapata kumjua Yehova kama anavyofafanuliwa katika Biblia nzima. Kwa hiyo, hatutataniki wakati simulizi fulani linazusha maswali ambayo hatuwezi kupata jibu mara moja. Kwa mfano: Tunapounganisha vipande vya mchezo wa chemshabongo, huenda tusipate kipande fulani mwanzoni au huenda tusielewe jinsi kipande fulani kinavyoungana na vingine. Lakini, labda tumeunganisha vipande vya kutosha kutusaidia kuelewa jinsi picha kamili itakavyokuwa. Vivyo hivyo, tunapojifunza Biblia, pole kwa pole tunajifunza jinsi Yehova Mungu alivyo, na hatimaye tunapata kumjua vizuri kabisa. Hata ikiwa mwanzoni hatuelewi simulizi fulani au hatuoni jinsi linavyopatana na utu wa Mungu, tayari tumejifunza kupitia funzo letu la Biblia mambo mengi sana ya kutusadikisha kwamba bila shaka Yehova ni Mungu mwenye upendo, asiyependelea, na mwenye haki.
19 Basi, ili kufahamu Neno la Mungu, ni lazima tusome na kujifunza Neno hilo kwa moyo mnyofu bila kushikilia mno maoni yetu. Jambo hilo linaonyesha hekima kuu ya Yehova, sivyo? Wanadamu wenye akili nyingi wanaweza kuandika vitabu ambavyo ni watu “wenye hekima na wenye akili” tu wanaovielewa. Lakini ni Mungu tu anayeweza kuandika kitabu ambacho watu wenye mwelekeo unaofaa tu wanaweza kukielewa!—Mathayo 11:25.
Kitabu Chenye “Hekima Kamili”
20. Kwa nini ni Yehova peke yake anayeweza kutuambia njia bora ya maisha, na Biblia ina nini kinachoweza kutusaidia?
20 Katika Neno lake, Yehova hutuambia njia bora ya maisha. Anajua mahitaji yetu vizuri zaidi kuliko tunavyoyajua kwa sababu yeye ni Muumba wetu. Na sikuzote wanadamu wamekuwa na mahitaji yaleyale ya msingi, kama vile, tamaa ya kupendwa, kuwa na furaha, na kuwa na mahusiano mazuri. Biblia ina “hekima kamili” ambayo inaweza kutusaidia kuwa na kusudi maishani. (Mithali 2:7) Kila sehemu ya kitabu hiki ina sura ambayo inaonyesha jinsi tunavyoweza kutumia shauri la Biblia lenye hekima. Lakini hebu tuone mfano mmoja tu.
21-23. Ni mashauri gani yenye hekima yanayoweza kutusaidia kuepuka kufungia hasira na kinyongo moyoni?
21 Je, umegundua kwamba watu ambao wanafungia uchungu na kinyongo moyoni mara nyingi hujiumiza wenyewe? Kinyongo humlemea sana mtu. Tunapofungia kinyongo moyoni, tunajawa na mawazo, na tunakosa utulivu na shangwe. Uchunguzi wa kisayansi unadokeza kwamba kufungia hasira moyoni kunaweza kuongeza uwezekano wa kupata ugonjwa wa moyo na magonjwa mengine mengi ya kudumu. Miaka mingi kabla ya uchunguzi huo wa kisayansi, Biblia ilisema hivi kwa hekima: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Lakini tunaweza kufanyaje hivyo?
22 Neno la Mungu linatoa shauri hili la hekima: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” (Mithali 19:11) Busara ni uwezo wa kuchanganua jambo kwa undani zaidi, kutambua sababu zisizoonekana wazi. Busara hutokeza ufahamu, kwa kuwa inaweza kutusaidia kutambua sababu iliyomfanya mtu mwingine aseme au kutenda kwa njia fulani. Kujitahidi kuelewa nia yake halisi, hisia zake, na hali zake kwaweza kutusaidia kuondoa mawazo au hisia zozote mbaya tulizo nazo kumwelekea.
23 Biblia ina shauri hivi tena: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” (Wakolosai 3:13) Usemi “endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake” unadokeza hali ya kuwastahimili wengine, kuvumilia sifa ambazo huenda zinatuudhi. Ustahimilivu wa aina hiyo unaweza kutusaidia kuepuka kufungia kinyongo moyoni kwa sababu ya mambo madogo-madogo. Neno “kusameheana” lamaanisha kuondoa kabisa kinyongo. Mungu wetu mwenye hekima anajua kwamba tunahitaji kuwasamehe wengine kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Tunapowasamehe wengine hatuwafaidi tu wale waliotukosea bali pia sisi wenyewe tunakuwa na amani ya akilini na ya moyoni. (Luka 17:3, 4) Neno la Mungu lina hekima iliyoje!
24. Inakuwaje tunapotumia hekima ya Mungu maishani?
24 Yehova alitaka kuwasiliana nasi kwa sababu ya upendo wake usio na kifani. Alichagua njia bora sana—“barua” iliyoandikwa na wanadamu walioongozwa na roho takatifu. Ndiyo sababu Biblia ina hekima ya Yehova mwenyewe. Hekima hiyo ni “amini sana.” (Zaburi 93:5) Kadiri tunavyotumia hekima hiyo maishani, na kadiri tunavyowafundisha wengine hekima hiyo, ndivyo tunavyozidi kumkaribia Mungu wetu mwenye hekima kamili. Katika sura inayofuata, tutazungumzia mfano mwingine wenye kutokeza wa hekima ya Yehova ya kuona matukio ya wakati ujao: uwezo wake wa kutabiri matukio ya wakati ujao na kutimiza kusudi lake.
a Kwa mfano, Daudi, aliyekuwa mchungaji, anatumia mifano inayohusiana na ufugaji wa wanyama. (Zaburi 23) Mathayo, ambaye alikuwa mtoza-kodi hapo awali, mara nyingi anataja tarakimu na thamani ya fedha. (Mathayo 17:27; 26:15; 27:3) Luka, ambaye alikuwa daktari, anatumia maneno yanayohusiana na kazi yake ya tiba.—Luka 4:38; 14:2; 16:20.
b Kila moja ya sarafu hizo iliitwa leptoni. Hiyo ndiyo iliyokuwa sarafu ya Kiyahudi yenye thamani ndogo zaidi wakati huo. Lepta mbili zilikuwa sawa na thamani ya 1/64 ya mshahara wa siku moja. Sarafu mbili hata hazikutosha kununua shore mmoja. Shore alikuwa ndege mwenye gharama ya chini sana aliyeliwa na watu maskini.
-
-
“Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 19
“Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu”
1, 2. Tunapaswa kupendezwa na ‘siri gani takatifu,’ na kwa nini?
SIRI! Mara nyingi wanadamu hushindwa kuficha siri, kwa sababu zinavutia na kustaajabisha. Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Ni utukufu wa Mungu kuficha jambo.” (Mithali 25:2) Naam, akiwa Muumba na Mtawala Mwenye Enzi Kuu, Yehova ana haki ya kuweka mambo fulani yakiwa siri kwa wanadamu hadi wakati wake wa kuyafunua unapowadia.
2 Lakini, kuna siri moja yenye kuvutia na kustaajabisha ambayo Yehova amefunua katika Neno lake. Inaitwa “siri takatifu ya mapenzi [ya Mungu].” (Waefeso 1:9) Kujifunza kuhusu siri hiyo si jambo la kufurahisha tu. Kujua siri hiyo kunaweza kukusaidia upate wokovu na kufahamu kidogo hekima ya Yehova isiyo na kifani.
Siri Takatifu Yafunuliwa Hatua kwa Hatua
3, 4. Unabii wa Mwanzo 3:15 ulitoaje tumaini, na ulikuwa na fumbo gani, au ‘siri gani takatifu’?
3 Adamu na Hawa walipofanya dhambi, huenda ilionekana kana kwamba kusudi la Yehova la wanadamu wakamilifu kuishi katika paradiso duniani lilikuwa limezuiwa. Lakini Mungu alishughulikia tatizo hilo mara moja. Alisema hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”—Mwanzo 3:15.
4 Maneno hayo yalikuwa ya kifumbo na yasiyoeleweka. Ni mwanamke yupi huyo? Nyoka alikuwa nani? Ni nani angekuwa “uzao” ambao ungemponda nyoka kichwa? Adamu na Hawa waliweza kukisia-kisia tu. Hata hivyo, maneno hayo ya Mungu yalimpa tumaini mzao yeyote mwaminifu wa wenzi hao walioasi. Uadilifu ungeshinda. Kusudi la Yehova lingetimizwa. Lakini jinsi gani? Ahaa, hilo lilikuwa fumbo! Biblia inasema kwamba fumbo hilo ni “hekima ya Mungu katika siri takatifu, hekima iliyofichwa.”—1 Wakorintho 2:7.
5. Toa mfano ambao unaonyesha kwa nini Yehova alifunua siri yake hatua kwa hatua.
5 Hatimaye, Yehova, “afunuaye siri,” angefunua kila jambo kuhusu utimizo wa siri hiyo. (Danieli 2:28) Lakini angeifunua siri hiyo polepole, hatua kwa hatua. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo baba mwenye upendo anavyomjibu mvulana wake mdogo anayemwuliza, “Baba, nilitoka wapi?” Baba mwenye hekima anamwambia mvulana huyo mdogo habari chache tu ambazo anaweza kuelewa. Kadiri mvulana huyo anavyokua, ndivyo baba anavyomweleza habari zaidi. Vivyo hivyo, Yehova huamua wakati ambapo watu wake wanaweza kuelewa unabii kuhusu mapenzi yake na kusudi lake.—Mithali 4:18; Danieli 12:4.
6. (a) Agano au mapatano hutimiza kusudi gani? (b) Kwa nini inavutia kwamba Yehova hufanya maagano na wanadamu?
6 Yehova alifunuaje siri hizo? Alifunua mambo mengi kwa kufanya maagano au mapatano kadhaa. Huenda wakati fulani umewahi kufanya mapatano—labda ya kununua nyumba au ya kuomba mkopo au ya kumkopesha mtu pesa. Mapatano hayo yalithibitisha kisheria kwamba masharti mliyokubaliana yatatimizwa. Lakini kwa nini Yehova alihitaji kufanya maagano rasmi au mapatano na wanadamu? Bila shaka, neno lake ni uthibitisho wa kutosha wa kwamba ahadi zake zitatimia. Hiyo ni kweli, lakini kwa fadhili Mungu amethibitisha neno lake katika visa kadhaa kwa kufanya maagano ya kisheria. Maagano hayo yenye masharti ya kisheria hutupatia sisi wanadamu wasiokamilika msingi thabiti zaidi wa kutumaini ahadi za Yehova.—Waebrania 6:16-18.
Agano Pamoja na Abrahamu
7, 8. (a) Yehova alifanya agano gani na Abrahamu, nalo lilifunua nini kuhusu ile siri takatifu? (b) Yehova alifunuaje hatua kwa hatua ukoo wa Mzao aliyeahidiwa?
7 Zaidi ya miaka elfu mbili baada ya mwanadamu kufukuzwa kutoka Paradiso, Yehova alimwambia hivi mtumishi wake mwaminifu Abrahamu: “Katika kuzidisha, nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni . . . na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:17, 18) Hiyo haikuwa ahadi tu; Yehova aliitoa kama agano la kisheria na kuithibitisha kwa kiapo chake kisichoweza kuvunjwa. (Mwanzo 17:1, 2; Waebrania 6:13-15) Ni jambo la pekee kama nini kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu kwa kweli alifanya agano la kuwabariki wanadamu!
“Nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni”
8 Agano la Kiabrahamu lilifunua kwamba Mzao aliyeahidiwa angekuwa mwanadamu, kwa sababu angekuwa mzao wa Abrahamu. Lakini angekuwa nani? Baada ya muda, Yehova alifunua kwamba Isaka, mmoja wa wana wa Abrahamu angekuwa babu ya Mzao huyo. Yakobo ndiye aliyechaguliwa kati ya wana wawili wa Isaka. (Mwanzo 21:12; 28:13, 14) Baadaye, Yakobo alimwambia mmoja wa wanaye 12 maneno haya ya kiunabii: “Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, wala mfanya sheria kati ya miguu yake, hata atakapokuja Yeye, mwenye milki, ambaye mataifa watamtii.” (Mwanzo 49:10) Basi ikawa wazi kwamba Mzao huyo angekuwa mfalme kutoka kwa kabila la Yuda!
Agano Pamoja na Israeli
9, 10. (a) Yehova alifanya agano gani na taifa la Israeli, na agano hilo lililinda nini? (b) Sheria ilionyeshaje kwamba wanadamu wanahitaji fidia?
9 Mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alifanya mpango ambao ungefunua mambo mengi zaidi kuhusu ile siri takatifu. Alifanya agano na wazao wa Abrahamu, taifa la Israeli. Ingawa agano hilo la Sheria ya Musa halitumiki leo, lilikuwa sehemu muhimu sana ya kusudi la Yehova la kutoa Mzao aliyeahidiwa. Jinsi gani? Fikiria njia hizi tatu. Kwanza, Sheria hiyo ilikuwa kama ukuta wenye kulinda. (Waefeso 2:14) Sheria zake adilifu ziliwatenganisha Wayahudi na wasio Wayahudi. Kwa hiyo, Sheria ilisaidia kulinda ukoo wa Mzao aliyeahidiwa. Kwa sababu ya ulinzi huo, taifa hilo bado lilikuwapo wakati wa Mungu ulipowadia wa Mesiya kuzaliwa katika kabila la Yuda.
10 Pili, Sheria ilionyesha waziwazi kwamba wanadamu wanahitaji fidia. Sheria hiyo kamilifu ilionyesha kwamba wanadamu wenye dhambi hawawezi kuitii kikamili. Kwa hiyo, ilikusudiwa “kufanya mikiuko-sheria iwe dhahiri, mpaka mbegu iwasili ambayo kwayo ahadi ilikuwa imetolewa.” (Wagalatia 3:19) Sheria hiyo ilikuwa na mipango ya kusamehe dhambi kwa muda kupitia dhabihu za wanyama. Lakini, dhabihu hizo ziliashiria dhabihu ya fidia ya Kristo, kwa kuwa kama Paulo alivyoandika, “haiwezekani damu ya mafahali na ya mbuzi kuziondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Kwa hiyo, kwa Wayahudi waaminifu, agano hilo lilikuwa ‘mfunzi aliyeongoza kwa Kristo.’—Wagalatia 3:24.
11. Agano la Sheria liliandalia Israeli tumaini gani tukufu, lakini kwa nini karibu taifa hilo lote lilipoteza tumaini hilo?
11 Tatu, agano hilo liliandalia taifa la Israeli tumaini tukufu. Yehova aliwaambia kwamba ikiwa wangetii agano hilo, wangekuwa “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6) Hatimaye, Waisraeli wa asili wakaja kuwa washiriki wa kwanza wa ufalme wa makuhani wa kimbingu. Hata hivyo, karibu taifa lote la Israeli liliasi agano la Sheria, likamkataa yule Mzao wa Kimesiya, na likapoteza tumaini hilo. Basi, ni nani wangekamilisha ufalme wa makuhani? Na taifa hilo lililobarikiwa lingekuwa na uhusiano gani na Mzao aliyeahidiwa? Mambo hayo ya siri takatifu yangefunuliwa katika wakati barabara wa Mungu.
Agano la Ufalme la Daudi
12. Yehova alifanya agano jipi na Daudi, na lilifunua mambo gani kuhusu siri takatifu ya Mungu?
12 Katika karne ya 11 K.W.K., Yehova alifunua mambo zaidi kuhusu ile siri takatifu alipofanya agano jingine. Alimwahidi hivi Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu: “Nitainua mzao wako nyuma yako, . . . nami nitaufanya imara ufalme wake. . . . Nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele.” (2 Samweli 7:12, 13; Zaburi 89:3) Wakati huo ilijulikana kwamba ukoo wa Mzao aliyeahidiwa ungetokea katika nyumba ya Daudi. Lakini je, mwanadamu wa kawaida angeweza kutawala “milele”? (Zaburi 89:20, 29, 34-36) Na je, mfalme huyo wa kibinadamu angeweza kuwaokoa wanadamu kutoka kwa dhambi na kifo?
13, 14. (a) Kulingana na Zaburi 110, Yehova anamwahidi nini Mfalme wake aliyetiwa mafuta? (b) Manabii wa Yehova walifunua mambo gani mengine kuhusu Mzao ambaye angekuja?
13 Daudi aliongozwa kuandika hivi: “Neno la BWANA kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. BWANA ameapa, wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, kwa mfano wa Melkizedeki.” (Zaburi 110:1, 4) Maneno hayo ya Daudi yalimhusu moja kwa moja, Mzao aliyeahidiwa, au Mesiya. (Matendo 2:35, 36) Mfalme huyo hangetawala kutoka Yerusalemu, bali kutoka mbinguni kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Yehova. Basi angekuwa na mamlaka, si juu ya nchi ya Israeli tu, bali juu ya dunia yote. (Zaburi 2:6-8) Jambo jingine lilifunuliwa. Angalia kwamba Yehova aliapa kwa dhati kwamba huyo Mesiya angekuwa “kuhani . . . kwa mfano wa Melkizedeki.” Kama Melkizedeki, ambaye alitumika akiwa mfalme na kuhani katika siku za Abrahamu, Mzao ambaye angekuja angechaguliwa na Mungu moja kwa moja awe Mfalme na Kuhani!—Mwanzo 14:17-20.
14 Kwa miaka mingi, Yehova alitumia manabii wake kufunua mambo zaidi kuhusu siri yake takatifu. Kwa mfano, Isaya alitabiri kwamba Mzao huyo angekufa kifo cha kidhabihu. (Isaya 53:3-12) Mika alitabiri mahali ambapo Mesiya angezaliwa. (Mika 5:2) Danieli hata alitabiri wakati hususa ambapo Mzao huyo angetokea na wakati ambapo angekufa.—Danieli 9:24-27.
Siri Takatifu Yafunuliwa!
15, 16. (a) Mwana wa Yehova ‘alitokana na mwanamke’ kwa njia gani? (b) Yesu alirithi nini kutoka kwa wazazi wake wa kibinadamu, naye akawa Mzao aliyeahidiwa lini?
15 Utimizo wa unabii huo mbalimbali haukujulikana hadi Mzao huyo alipotokea. Andiko la Wagalatia 4:4 lasema: “Kikomo kamili cha wakati kilipowasili, Mungu alimtuma Mwana wake, aliyekuja kuwa kutokana na mwanamke.” Mnamo mwaka wa 2 K.W.K., malaika alimwambia hivi bikira Myahudi aliyeitwa Maria: “Tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe itakupasa kumwita jina lake Yesu. Huyu atakuwa mkubwa na ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi Sana; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake . . . Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana itakufunika kivuli. Kwa sababu hiyo pia kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.”—Luka 1:31, 32, 35.
16 Baadaye, Yehova alihamisha uhai wa Mwanaye kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria, hivyo, akatokana na mwanamke. Maria hakuwa mwanamke mkamilifu. Lakini, Yesu hakurithi kutokamilika kutoka kwa Maria, kwa sababu alikuwa “Mwana wa Mungu.” Lakini, wazazi wa kibinadamu wa Yesu, ambao walikuwa wazao wa Daudi, walimwezesha kuwa mrithi wa Daudi kiasili na kisheria. (Matendo 13:22, 23) Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., Yehova alimtia mafuta kwa roho takatifu na kusema: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa.” (Mathayo 3:16, 17) Hatimaye, Mzao aliyeahidiwa alikuwa amewasili! (Wagalatia 3:16) Wakati wa kufunua mambo mengi zaidi kuhusu ile siri takatifu ulikuwa umewadia.—2 Timotheo 1:10.
17. Andiko la Mwanzo 3:15 lilifafanuliwaje?
17 Wakati wa huduma yake, Yesu alimtambulisha yule nyoka aliyetajwa katika Mwanzo 3:15 kuwa Shetani, na uzao wa nyoka kuwa wafuasi wa Shetani. (Mathayo 23:33; Yohana 8:44) Baadaye, ilifunuliwa jinsi ambavyo hao wote watapondwa milele. (Ufunuo 20:1-3, 10, 15) Na mwanamke alitambuliwa kuwa “Yerusalemu la juu,” tengenezo la Yehova la mbinguni la viumbe wa roho, ambalo ni kama mke.a—Wagalatia 4:26; Ufunuo 12:1-6.
Agano Jipya
18. Ni nini kusudi la “agano jipya”?
18 Huenda jambo la kutokeza hata zaidi lilifunuliwa siku iliyotangulia kifo cha Yesu, alipowaambia wanafunzi wake waaminifu kuhusu “agano jipya.” (Luka 22:20) Agano hilo jipya, sawa na agano la Sheria ya Musa, lilikusudiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani.” (Kutoka 19:6; 1 Petro 2:9) Hata hivyo, agano hilo halingefanyiza taifa la kiasili bali taifa la kiroho, yaani, “Israeli wa Mungu.” Taifa hilo lingekuwa tu na wafuasi waaminifu wa Kristo waliotiwa mafuta. (Wagalatia 6:16) Washiriki hao wa agano jipya wangeshirikiana na Yesu kubariki wanadamu!
19. (a) Kwa nini agano jipya linafanikiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani”? (b) Kwa nini Wakristo watiwa-mafuta wanaitwa “kiumbe kipya,” na ni wangapi watakaotawala na Kristo wakiwa mbinguni?
19 Lakini kwa nini agano jipya linafanikiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani” ambao utawabariki wanadamu? Kwa sababu badala ya kuwahukumu wanafunzi wa Kristo kuwa watenda-dhambi, linafungua njia ya dhambi zao kusamehewa kupitia dhabihu yake. (Yeremia 31:31-34) Mara tu baada ya kuhesabiwa kuwa waadilifu machoni pa Yehova, anawakubali kuwa wana wa familia yake ya mbinguni na kuwatia mafuta kwa roho takatifu. (Waroma 8:15-17; 2 Wakorintho 1:21) Kwa hiyo, wanapata ‘uzaliwa mpya kwenye tumaini lililo hai ambao umewekwa akiba katika mbingu.’ (1 Petro 1:3, 4) Wakristo watiwa-mafuta waliozaliwa kwa roho wanaitwa “kiumbe kipya,” kwa sababu cheo chao cha juu ni kipya kabisa kwa wanadamu. (2 Wakorintho 5:17) Biblia inafunua kwamba hatimaye watu 144,000 wakiwa mbinguni watashiriki kutawala wanadamu waliokombolewa.—Ufunuo 5:9, 10; 14:1-4.
20. (a) Ni jambo gani lililofunuliwa mwaka wa 36 W.K. kuhusu ile siri takatifu? (b) Ni nani watakaofurahia baraka ambazo Abrahamu aliahidiwa?
20 Yesu pamoja na hao watiwa-mafuta wanakuwa “mbegu ya Abrahamu.”b (Wagalatia 3:29) Wayahudi wa asili ndiyo waliochaguliwa kwanza. Lakini mwaka wa 36 W.K., jambo jingine la siri takatifu lilifunuliwa: Watu wa Mataifa, au wasio Wayahudi, wangekuwa pia na tumaini la kwenda mbinguni. (Waroma 9:6-8; 11:25, 26; Waefeso 3:5, 6) Je, ni Wakristo watiwa-mafuta peke yao ambao wangefurahia baraka ambazo Abrahamu aliahidiwa? La, kwa sababu dhabihu ya Yesu inafaidi ulimwengu wote. (1 Yohana 2:2) Baada ya muda, Yehova alifunua kwamba “umati mkubwa” usiohesabika ungeokoka mwisho wa mfumo wa mambo wa Shetani. (Ufunuo 7:9, 14) Halaiki kubwa zaidi ya watu wangefufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso!—Luka 23:43; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:11-15; 21:3, 4.
Hekima ya Mungu na Siri Takatifu
21, 22. Siri takatifu ya Yehova inaonyeshaje hekima yake?
21 Siri takatifu ni wonyesho wenye kustaajabisha wa “hekima ya Mungu ya namna nyingi.” (Waefeso 3:8-10) Yehova alionyesha hekima iliyoje alipotunga siri hiyo na kuifunua hatua kwa hatua! Kwa hekima alifikiria udhaifu wa wanadamu, akawaruhusu waonyeshe hali yao halisi ya moyoni.—Zaburi 103:14.
22 Yehova pia alionyesha hekima isiyo na kifani alipomchagua Yesu kuwa Mfalme. Mwana wa Yehova ni mwenye kutumainika kuliko kiumbe mwingine yeyote ulimwenguni. Yesu alipata magumu ya kila namna alipokuwa mwanadamu. Anaelewa kabisa matatizo yanayotupata. (Waebrania 5:7-9) Vipi watawala-wenzi wa Yesu? Kwa miaka mingi, wanaume na wanawake waliochaguliwa kutoka kwa makabila, lugha, na malezi mbalimbali wametiwa mafuta. Kila mmoja wao amepata matatizo ya kila namna na kuyashinda. (Waefeso 4:22-24) Itakuwa furaha iliyoje kutawaliwa na wafalme na makuhani hao wenye huruma!
23. Wakristo wana pendeleo gani kuhusiana na siri takatifu ya Yehova?
23 Mtume Paulo aliandika hivi: “Siri takatifu iliyokuwa imefichwa tangu mifumo ya mambo iliyopita na tangu vizazi vilivyopita . . . imefanywa dhahiri kwa watakatifu wake.” (Wakolosai 1:26) Naam, watakatifu wa Yehova waliotiwa mafuta wamepata kuelewa mengi kuhusu siri hiyo takatifu, nao wamewafundisha mamilioni ya watu ujuzi huo. Basi sote tuna pendeleo lililoje! Yehova ‘ametujulisha siri takatifu ya mapenzi yake.’ (Waefeso 1:9) Na tuwaambie wengine siri hiyo ya ajabu, na kuwasaidia pia wachunguze hekima isiyo na kifani ya Yehova Mungu!
a “Siri takatifu ya ujitoaji-kimungu” ilifunuliwa pia katika maisha ya Yesu. (1 Timotheo 3:16) Kwa muda mrefu, haikujulikana kama mwanadamu yeyote angeweza kubaki mwaminifu kabisa kwa Yehova. Yesu alijibu suala hilo. Alibaki mwaminifu licha ya majaribu yote ambayo Shetani alimletea.—Mathayo 4:1-11; 27:26-50.
b Yesu pia alifanya “agano . . . kwa ajili ya ufalme” na kikundi hichohicho. (Luka 22:29, 30) Kwa kweli, Yesu alifanya mapatano na “kundi [hilo] dogo” ili watawale pamoja naye mbinguni wakiwa sehemu ya pili ya mbegu ya Abrahamu.—Luka 12:32.
-
-
“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini MnyenyekevuMkaribie Yehova
-
-
Sura ya 20
“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini Mnyenyekevu
1-3. Tunajuaje kwamba Yehova ni mnyenyekevu?
BABA anataka kumfundisha mtoto wake mdogo somo muhimu. Ana hamu ya kugusa moyo wa mtoto huyo. Afanyeje hivyo? Je, asimame na kumtisha mtoto huyo? Au apaswa kuchuchumaa kufikia kimo cha mtoto huyo na kuzungumza naye kwa upole, na kwa urafiki? Bila shaka, baba mnyenyekevu na mwenye hekima humfikia mtoto wake kwa njia ya upole.
2 Yehova ni Baba wa aina gani—je, yeye ni mwenye kiburi au mnyenyekevu, mkali au mpole? Yehova anajua kila jambo, ana hekima kamili. Hata hivyo, je, umeona kwamba mara nyingi watu wenye ujuzi na akili hawawi wanyenyekevu? Ni kama Biblia inavyosema, ‘ujuzi hututumua.’ (1 Wakorintho 3:19; 8:1) Lakini Yehova, ni “mwenye hekima moyoni,” na mnyenyekevu pia. (Ayubu 9:4) Yehova hana kiburi licha ya kwamba ana cheo cha juu na fahari. Kwa nini?
3 Yehova ni mtakatifu. Kwa hiyo, hana sifa ya kiburi ambayo inamtia mtu unajisi. (Marko 7:20-22) Isitoshe, angalia maneno ambayo nabii Yeremia alimwambia Yehova: “Bila shaka nafsi yako [Yehova mwenyewe] itanikumbuka na kuniinamia.”a (Maombolezo 3:20, NW) Hebu wazia! Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, alikuwa tayari ‘kumwinamia,’ au kujinyenyekeza kufikia kiwango cha Yeremia. Alifanya hivyo ili kumpa uangalifu unaofaa mwanadamu huyo asiyekamilika. (Zaburi 113:7) Naam, Yehova ni mnyenyekevu. Lakini Mungu anaonyeshaje unyenyekevu? Unahusianaje na hekima? Na kwa nini unyenyekevu ni muhimu kwetu?
Jinsi Yehova Alivyo Mnyenyekevu
4, 5. (a) Unyenyekevu ni nini, na unaonyeshwaje, na kwa nini unyenyekevu haupasi kuonwa kuwa udhaifu au woga? (b) Yehova alionyeshaje unyenyekevu aliposhughulika na Daudi, na unyenyekevu wa Yehova unatufaidi jinsi gani?
4 Unyenyekevu unamaanisha kujiweka katika hali ya chini, kutojivuna na kutokuwa na kiburi. Unyenyekevu ni sifa ya moyoni na huonyeshwa kwa sifa kama vile upole, subira, na kuzingatia maoni ya wengine. (Wagalatia 5:22, 23) Lakini sifa hizo za kimungu hazipasi kamwe kuonwa kuwa udhaifu au woga. Sifa hizo zinapatana na hasira ya Yehova ya uadilifu au jinsi anavyotumia nguvu zake za kuangamiza. Lakini unyenyekevu na upole wa Yehova unaonyesha kwamba ana nguvu nyingi, yaani, uwezo wa kujidhibiti kikamili. (Isaya 42:14) Unyenyekevu unahusianaje na hekima? Kichapo kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema hivi: “Unyenyekevu unafafanuliwa kuwa . . . hali ya kutokuwa na ubinafsi na ni chanzo muhimu cha hekima yote.” Basi, hakuwezi kuwa na hekima ya kweli pasipo unyenyekevu. Unyenyekevu wa Yehova unatufaidi jinsi gani?
Baba mwenye hekima huwatendea watoto wake kwa upole na unyenyekevu
5 Mfalme Daudi alimwimbia Yehova hivi: “Umenipa ngao ya wokovu wako, mkono wako wa kuume umenitegemeza, na unyenyekevu wako umenikuza.” (Zaburi 18:35) Ni kana kwamba Yehova aliinama ili amsaidie mwanadamu huyo asiyekamilika, alimlinda na kumtunza siku kwa siku. Daudi alitambua kwamba hangeweza kamwe kuokolewa—na hata, hatimaye kuwa mfalme—endapo Yehova hangejinyenyekeza. Kwa kweli, ni nani kati yetu angeweza kuwa na tumaini lolote la kuokoka ikiwa Yehova hangekuwa mnyenyekevu, na kama hangekuwa tayari kujiweka katika hali ya chini ili kushughulika nasi akiwa Baba mpole mwenye upendo?
6, 7. (a) Kwa nini Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi kama wanadamu? (b) Kuna uhusiano gani kati ya upole na hekima, na ni nani aliye mfano bora kabisa wa sifa hizo?
6 Inafaa kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya unyenyekevu na kiasi. Kiasi ni sifa nzuri sana ambayo wanadamu waaminifu wanapaswa kukuza. Sifa hiyo, kama vile sifa ya unyenyekevu, inahusiana na hekima. Kwa mfano, Mithali 11:2, NW, yasema: “Hekima hukaa na wenye kiasi.” Hata hivyo, Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi kama wanadamu. Kwa nini? Kulingana na Maandiko, mtu mwenye kiasi ni mtu anayetambua mipaka yake mwenyewe. Mungu Mweza-Yote hana mipaka yoyote ila mipaka anayojiwekea mwenyewe kwa sababu ya kanuni zake adilifu. (Marko 10:27; Tito 1:2) Isitoshe, hajitiishi kwa yeyote kwa sababu yeye ni Mungu Mwenyezi. Kwa hiyo, Yehova si mwenye kiasi katika maana hiyo.
7 Hata hivyo, Yehova ni mnyenyekevu na mpole. Yeye huwafundisha watumishi wake kwamba hawawezi kuwa na hekima ya kweli wasipokuwa wapole. Neno lake hutaja “upole ulio wa hekima.”b (Yakobo 3:13) Fikiria jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hizo.
Yehova Huwakabidhi Wengine Madaraka Naye Huwasikiliza kwa Unyenyekevu
8-10. (a) Kwa nini inashangaza kwamba Yehova yu tayari kuwakabidhi wengine madaraka na kuwasikiliza? (b) Mwenyezi ameonyeshaje unyenyekevu anaposhughulika na malaika wake?
8 Utayari wa Yehova wa kusikiliza na kuwakabidhi wengine madaraka unaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu. Inashangaza kwamba Yehova yu tayari kufanya hivyo ingawa yeye hahitaji msaada wala shauri. (Isaya 40:13, 14; Waroma 11:34, 35) Hata hivyo, Biblia inaonyesha tena na tena kwamba Yehova hujinyenyekeza katika njia hizo.
9 Kwa mfano, fikiria kisa kimoja cha pekee kilichotukia katika maisha ya Abrahamu. Abrahamu alitembelewa na wageni watatu, alimwita mmoja wao “Bwana.” Wageni hao walikuwa malaika, lakini mmoja wao alikuja kwa jina la Yehova na alikuwa akitenda kwa jina hilo. Malaika huyo aliponena na kutenda, ni kana kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akinena na kutenda. Kupitia malaika hao, Yehova alimwambia Abrahamu kwamba Alikuwa amesikia “kilio cha Sodoma na Gomora.” Yehova alisema hivi: “Nitashuka sasa nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia; na kama sivyo, nitajua.” (Mwanzo 18:3, 20, 21) Bila shaka, ujumbe huo wa Yehova haukumaanisha kwamba Mweza Yote ‘angeshuka’ kihalisi. Badala yake, aliwatuma malaika wamwakilishe tena. (Mwanzo 19:1) Kwa nini? Je, Yehova ambaye ana uwezo wa kuona kila jambo hangeweza ‘kujua’ hali ya eneo hilo bila msaada? Bila shaka angeweza. Lakini badala yake, kwa unyenyekevu Yehova aliwapa malaika hao kazi ya kuchunguza hali na kumtembelea Loti na familia yake Sodoma.
10 Isitoshe, Yehova husikiliza. Pindi moja aliwaomba malaika wake watoe maoni kuhusu njia mbalimbali za kumshinda Mfalme Ahabu aliyekuwa mwovu. Yehova hakuhitaji msaada huo. Lakini, alikubali maoni ya malaika mmoja, naye akamtuma atekeleze jambo hilo. (1 Wafalme 22:19-22) Tukio hilo linaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu, sivyo?
11, 12. Abrahamu alipataje kuelewa unyenyekevu wa Yehova?
11 Yehova yu tayari pia kuwasikiliza wanadamu wasiokamilika ambao wanataka sana kumweleza mahangaiko yao. Kwa mfano, Yehova alipomwambia Abrahamu kwamba alikusudia kuharibu Sodoma na Gomora, mwanamume huyo mwaminifu alishtuka. Abrahamu akasema, “Hasha usifanye hivyo,” kisha akaongezea hivi: “Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?” Alimwuliza Yehova kama angeacha miji hiyo iwapo ingekuwa na watu 50 wenye haki. Yehova alimhakikishia kwamba Hangeiangamiza. Lakini Abrahamu akamwuliza swali hilo tena na tena, na kupunguza idadi hiyo hadi 45, kisha 40, na kuendelea. Abrahamu aliendelea kuuliza maswali hadi idadi hiyo ilipofikia kumi licha ya Yehova kumhakikishia kwamba hangeangamiza miji hiyo. Huenda Abrahamu hakufahamu vyema rehema ya Yehova. Vyovyote iwavyo, kwa subira Yehova alimruhusu rafiki na mtumishi wake Abrahamu aeleze mahangaiko yake.—Mwanzo 18:23-33.
12 Ni wanadamu wangapi wenye akili, na wenye elimu ambao wangemsikiliza kwa subira mtu asiye na akili nyingi sana?c Mungu wetu alionyesha unyenyekevu mkubwa kwa kumsikiliza Abrahamu kwa makini sana. Wakati wa mazungumzo hayo, Abrahamu alitambua pia kwamba Yehova “si mwepesi wa hasira.” (Kutoka 34:6) Huenda Abrahamu alitambua kwamba hakuwa na haki ya kumwuliza Mungu mambo aliyokusudia kufanya, kwa hiyo alimsihi hivi mara mbili: “Bwana asiwe na hasira.” (Mwanzo 18:30, 32) Bila shaka Yehova hakukasirika. Kwa kweli, Yehova ana “upole ulio wa hekima.”
Yehova Hukubali Sababu
13. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha nini, na kwa nini sifa hiyo inamfaa kabisa Yehova?
13 Unyenyekevu wa Yehova unadhihirishwa na sifa nyingine yenye kupendeza—kukubali sababu. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wanadamu wengi wasiokamilika hawana sifa hiyo. Yehova yuko tayari kuwasikiliza viumbe wake wenye akili, na yuko tayari pia kukubali maoni yao maadamu hayakiuki kanuni zake za uadilifu. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha kihalisi ‘kukubali maoni ya wengine.’ Hiyo pia ni sifa muhimu ya hekima ya Mungu. Andiko la Yakobo 3:17 lasema hivi: ‘Hekima ya kutoka juu ni yenye kukubali sababu.’ Yehova ambaye ni mwenye hekima kamilifu anakubali sababu kwa njia gani? Kwanza, yeye hujipatanisha na hali mbalimbali. Kumbuka kwamba jina lake linatufundisha kwamba Yeye hujisababisha kuwa chochote kinachohitajiwa ili kutimiza makusudi yake. (Kutoka 3:14) Je, hilo halionyeshi kwamba yeye hujipatanisha na hali na ni mwenye kukubali sababu?
14, 15. Ono la Ezekieli la gari la kimbingu la Yehova linatufunza nini kuhusu tengenezo Lake la kimbingu, na hilo linatofautianaje na mashirika ya wanadamu?
14 Kuna ono moja la Biblia linalotusaidia kuelewa kwa kadiri fulani jinsi Yehova anavyojipatanisha na hali mbalimbali. Nabii Ezekieli alipata ono la tengenezo la kimbingu la Yehova la viumbe wa roho. Aliona gari kubwa ajabu na Yehova mwenyewe ndiye anayelielekeza gari hilo daima. Lilienda kwa njia ya kustaajabisha sana. Magurudumu yake makubwa yenye pande nne, yalijaa macho hivi kwamba yaliweza kuona kila mahali na kusafiri kuelekea upande wowote ghafula bila kusimama wala kugeuka. Na gari hilo kubwa mno halikujikokota polepole kama gari lililotengenezwa na wanadamu. Liliweza kwenda kwa mwendo wa umeme, na hata kugeuka ghafula! (Ezekieli 1:1, 14-28) Naam, tengenezo la Yehova linaweza kujipatanisha kabisa na hali mbalimbali na kushughulikia mahitaji yanayotokea kama anavyofanya Mungu Mwenye Enzi Kuu na mweza-yote ambaye analiongoza.
15 Wanadamu hawawezi kamwe kujipatanisha kikamili na hali kwa njia hiyo. Mara nyingi wanadamu na mashirika yao hushikilia mno maoni yao bila kubadilika, na hawakubali sababu. Kwa mfano: Meli ya mafuta au garimoshi la kubeba mizigo laweza kuwa kubwa sana na lenye nguvu nyingi sana. Lakini je, garimoshi au meli inaweza kugeuka mara moja hali zikibadilika? Garimoshi la mizigo haliwezi kuepuka kitu fulani kinachoanguka kwenye reli yake. Haliwezi kusimama ghafula. Baada ya breki kufungwa, garimoshi lenye mizigo mizito laweza kwenda umbali wa kilometa mbili hivi kabla ya kusimama! Vivyo hivyo, huenda meli kubwa ya mafuta ikasafiri umbali wa kilometa nane baada ya injini kuzimwa. Hata injini zikiendeshwa kinyumenyume, bado meli hiyo inaweza kusonga mbele umbali wa kilometa tatu! Ndivyo ilivyo na mashirika ya wanadamu ambayo mara nyingi hushikilia sana sera zake na kutokubali mawazo mapya. Mara nyingi watu hukataa kubadilika kulingana na mahitaji na hali mpya kwa sababu ya kiburi. Mashirika mengi yamevunjika na hata serikali nyingi kupinduliwa kwa sababu ya kutobadilika kulingana na hali. (Mithali 16:18) Twaweza kushukuru kama nini kwamba Yehova na tengenezo lake ni tofauti sana na mashirika hayo ya wanadamu!
Jinsi Yehova Anavyokubali Sababu
16. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu aliposhughulika na Loti kabla ya kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora?
16 Fikiria tena kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora. Malaika wa Yehova alimpa Loti na familia yake maagizo yaliyo wazi kabisa: “Ujiponye mlimani.” Lakini maagizo hayo hayakumpendeza Loti. “Sivyo, bwana wangu!” akasihi. Akiamini kwamba angekufa kama angekimbilia milimani, Loti aliomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia mji wa karibu ulioitwa Soari. Kumbuka kwamba Yehova alikuwa amekusudia kuuangamiza mji huo. Isitoshe, Loti hakuwa na sababu nzuri ya kuogopa. Bila shaka Yehova angeweza kumlinda Loti huko milimani! Hata hivyo, Yehova alikubali ombi la Loti, hakuuangamiza mji wa Soari. Malaika akamwambia hivi Loti, “Tazama, nimekukubali hata kwa neno hili.” (Mwanzo 19:17-22) Je, jambo hilo halionyeshi kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu?
17, 18. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu kuhusiana na Waninawi?
17 Yehova hukubali pia toba ya kutoka moyoni. Sikuzote yeye huonyesha rehema na kutenda yaliyo sawa. Fikiria jambo lililotukia nabii Yona alipotumwa mji wa Ninawi wenye uovu na jeuri. Yona alitangaza ujumbe rahisi sana wa Mungu kotekote katika Ninawi: Mji huo mashuhuri ungeangamizwa baada ya siku 40. Lakini, mambo yalibadilika ghafula. Waninawi walitubu!—Yona, sura ya 3.
18 Tunajifunza jambo fulani tunapolinganisha jinsi Yehova alivyohisi na jinsi Yona alivyohisi hali ilipobadilika. Yehova alijipatanisha na hali hiyo mara moja, akawa Mwenye Kusamehe dhambi badala ya kuwa “mtu wa vita.”d (Kutoka 15:3) Lakini Yona hakuwa tayari kubadilika wala hakuonyesha rehema kama Yehova alivyofanya. Badala ya kukubali sababu kama Yehova, alikuwa kama garimoshi la mizigo au meli kubwa ya mafuta tuliyotaja awali. Alitaka mji huo uangamizwe tu kama alivyokuwa ametangaza. Hata hivyo, kwa subira Yehova alimfundisha nabii wake asiye na subira somo lisilosahaulika kuhusu kukubali sababu na kuonyesha rehema.—Yona, sura ya 4.
Yehova ni mwenye kukubali sababu na anajua udhaifu wetu
19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye? (b) Mithali 19:17 inaonyeshaje kwamba Yehova ni Bwana ‘mwema na mwenye kukubali sababu,’ na kwamba unyenyekevu wake hauna kifani?
19 Mwishowe, Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye. Mfalme Daudi alisema: “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14) Yehova anajua udhaifu wetu na kasoro zetu kuliko tunavyojijua. Hatarajii kamwe tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu. Biblia inasema kwamba mabwana fulani ni ‘wema na wenye kukubali sababu’ na wengine ni “wagumu kupendeza.” (1 Petro 2:18) Je, Yehova ni Bwana wa aina gani? Mithali 19:17 inasema: “Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA.” Ni wazi kwamba bwana aliye mwema na mwenye kukubali sababu ndiye tu anayezingatia kila tendo la fadhili ambalo maskini wanafanyiwa. Isitoshe, andiko hilo pia linadokeza kwamba Muumba wa ulimwengu anajiona kuwa na deni kwa wanadamu duni wanaofanya matendo hayo ya rehema! Huo ni unyenyekevu usio na kifani.
20. Tuna uhakika gani kwamba Yehova husikiliza na kujibu sala zetu?
20 Hata leo Yehova ni mpole na mwenye kukubali sababu anaposhughulika na watumishi wake. Yeye husikiliza sala zetu za imani. Hatupaswi kukata kauli kwamba hajibu sala zetu kwa sababu hawatumi malaika waongee nasi. Kumbuka kwamba mtume Paulo alipowaomba waamini wenzake ‘waendeleze sala’ ili aweze kuachiliwa kutoka gerezani, aliongeza hivi: “Ili nipate kurudishwa kwenu karibuni zaidi.” (Waebrania 13:18, 19) Kwa hiyo, sala zetu zinaweza kwa kweli kumfanya Yehova atende jambo ambalo huenda hangetenda!—Yakobo 5:16.
21. Hatupaswi kuwa na maoni gani kuhusu unyenyekevu wa Yehova, lakini tunapaswa kumthamini kwa sababu gani?
21 Bila shaka, sifa zinazoonyesha unyenyekevu wa Yehova, yaani, upole, utayari wa kutusikiliza, subira, na kukubali sababu, hazimaanishi kwamba Yehova hulegeza kanuni zake adilifu. Huenda makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wakadhani kwamba wanakubali sababu wanapotekenya masikio ya wafuasi wao kwa kulegeza kanuni za Yehova za maadili. (2 Timotheo 4:3) Lakini mwelekeo wa wanadamu wa kuridhiana ili wapendwe haupatani kabisa na sifa ya Mungu ya kukubali sababu. Yehova ni mtakatifu; hawezi kamwe kupotosha kanuni zake adilifu. (Mambo ya Walawi 11:44) Basi, na tupende sifa ya Yehova ya kukubali sababu kwa kuwa inathibitisha unyenyekevu wake. Je, hufurahi sana kujua kwamba Yehova Mungu ni mnyenyekevu sana licha ya kwamba ana hekima isiyo na kifani katika ulimwengu wote? Inapendeza kama nini kumkaribia Mungu huyu mtukufu ambaye ni mpole, mwenye subira, na mwenye kukubali sababu!
a Waandishi wa kale, au Wasoferi, walibadili mstari huu kusema kwamba ni Yeremia anayeinama wala si Yehova. Inaonekana kwamba walidhani haifai kusema kwamba Mungu alitenda kitendo hicho cha unyenyekevu. Ndiyo sababu tafsiri nyingi zinakosa maana ya mstari huu wenye kupendeza. Hata hivyo, The New English Bible inasema kwa usahihi kwamba Yeremia alimwambia Mungu hivi: “Kumbuka, Ee kumbuka, na uniinamie.”
b Tafsiri nyingine husema “unyenyekevu unaotokana na hekima” na “upole ambao ni wonyesho muhimu wa hekima.”
c Biblia inaonyesha kwamba subira ni kinyume cha kiburi. (Mhubiri 7:8) Subira ya Yehova inathibitisha hata zaidi kwamba yeye ni mnyenyekevu.—2 Petro 3:9.
d Zaburi 86:5 inasema kwamba Yehova ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’ Zaburi hiyo ilipotafsiriwa katika Kigiriki, usemi “tayari kusamehe” ulitafsiriwa e·pi·ei·kesʹ, au “mwenye kukubali sababu.”
-
-
Yesu Afunua “Hekima Kutoka kwa Mungu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 21
Yesu Afunua “Hekima Kutoka kwa Mungu”
1-3. Majirani wa awali wa Yesu waliitikiaje mafundisho yake, na hawakutambua nini kumhusu?
WASIKILIZAJI walistaajabu. Kijana Yesu alikuwa amesimama mbele yao katika sinagogi akiwafundisha. Walimfahamu sana kwa sababu alikulia na kufanya kazi ya useremala katika mji wao kwa miaka mingi. Huenda baadhi yao waliishi katika nyumba ambazo Yesu alisaidia kujenga, au huenda walilima mashamba yao kwa plau na nira ambazo Yesu alitengeneza.a Lakini je, wangekubali mafundisho ya mtu huyo aliyekuwa seremala hapo awali?
2 Watu wengi waliokuwa wakimsikiliza walistaajabu na kuuliza: “Mtu huyu alipata wapi hekima hii?” Walisema hivi pia: “Huyu si seremala mwana wa Maria?” (Mathayo 13:54-58; Marko 6:1-3) Kwa kusikitisha, watu hao waliokuwa majirani wa Yesu pindi fulani, walisababu hivi, ‘Huyu seremala ni mtu wa kawaida tu kama sisi.’ Walimkataa ingawa alinena maneno yenye hekima. Hawakujua kwamba alipewa hekima hiyo.
3 Yesu alipata wapi hekima hiyo? Alisema hivi: “Kile nifundishacho si changu, bali ni chake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Mtume Paulo alieleza kwamba Yesu “amekuwa kwetu hekima kutoka kwa Mungu.” (1 Wakorintho 1:30) Yehova anafunua hekima yake kupitia Mwanaye, Yesu. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi: “Mimi na Baba ni mmoja.” (Yohana 10:30) Hebu tuchunguze sehemu tatu ambazo Yesu alionyesha “hekima kutoka kwa Mungu.”
Mafundisho Yake
4. (a) Ujumbe wa Yesu ulihusu nini hasa, na kwa nini ujumbe huo ulikuwa muhimu sana? (b) Kwa nini mashauri ya Yesu yalifaa na kuwafaidi wasikilizaji wake sikuzote?
4 Kwanza, fikiria mafundisho ya Yesu. Ujumbe wake ulihusu hasa “habari njema ya ufalme.” (Luka 4:43) Huo ulikuwa ujumbe muhimu sana kwa sababu Ufalme huo utatetea enzi kuu ya Yehova na kuwaletea wanadamu baraka za kudumu. Alipokuwa akifundisha, Yesu alitoa pia mashauri ya hekima kuhusu maisha ya kila siku. Alijithibitisha kuwa yule “Mshauri wa Ajabu” aliyetabiriwa. (Isaya 9:6) Kwa kweli, mashauri yake yalikuwa bora sana. Alijua Neno la Mungu na mapenzi yake kwa undani, alifahamu vyema utu wa wanadamu, naye aliwapenda sana. Kwa hiyo, sikuzote alitoa mashauri yaliyofaa ambayo yaliwafaidi wasikilizaji wake. Yesu alinena “semi za uhai udumuo milele.” Naam, mtu anayefuata mashauri yake atapata wokovu.—Yohana 6:68.
5. Yesu alizungumzia mambo gani katika Mahubiri ya Mlimani?
5 Mahubiri ya Mlimani yanaonyesha hekima isiyo na kifani ya mafundisho ya Yesu. Mahubiri hayo yaliyo katika Mathayo 5:3–7:27, yanaweza kutolewa kwa muda wa dakika 20 tu. Hata hivyo, yana mashauri yenye faida ya kudumu, yanayofaa sana leo sawa na yalivyofaa wakati yalipotolewa. Yesu alizungumzia mambo mengi mbalimbali, kutia ndani jinsi ya kuboresha mahusiano na wengine (5:23-26, 38-42; 7:1-5, 12), jinsi ya kuwa safi kiadili (5:27-32), na jinsi ya kuishi maisha yenye kusudi (6:19-24; 7:24-27). Lakini Yesu hakuwaambia tu wasikilizaji wake jinsi ya kuishi kwa hekima; aliwaonyesha kwa kuwaeleza, kwa kusababu nao, na kwa kuwapa uthibitisho.
6-8. (a) Yesu anataja sababu zipi nzuri za kuepuka mahangaiko? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Shauri la Yesu lina hekima ya kutoka juu?
6 Kwa mfano, fikiria shauri la Yesu lenye hekima katika Mathayo sura ya 6 linaloonyesha jinsi ya kupambana na mahangaiko ya vitu vya kimwili. Yesu anatushauri hivi: “Komeni kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakula au ni nini mtakunywa, au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtavaa.” (Mstari wa 25) Chakula na mavazi ni mahitaji ya lazima, na ni jambo la kawaida tu kuhangaikia vitu hivyo. Lakini Yesu anatuambia ‘tukome kuhangaikia’ vitu hivyo.b Kwa nini?
7 Msikilize Yesu anaposababu kwa njia yenye kusadikisha. Kwa kuwa Yehova ametupatia uhai na mwili, je, anaweza kushindwa kutuandalia chakula cha kuendeleza uhai huo na mavazi ya kujivika? (Mstari wa 25) Ikiwa Mungu anawalisha ndege na kuyapamba maua, basi, hatawatunza zaidi wanadamu wanaomwabudu! (Mstari wa 26, 28-30) Kwa kweli, haifai kuwa na mahangaiko yasiyofaa. Hatuwezi kuongeza muda wetu wa uhai hata kwa dhiraa moja kwa kuhangaika.c (Mstari wa 27) Tunawezaje kuepuka mahangaiko? Yesu anatushauri hivi: Endeleeni kuitanguliza ibada ya Mungu maishani mwenu. Wale wanaofanya hivyo wanaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yao wa mbinguni ‘atawaongezea’ mahitaji yao ya kila siku. (Mstari wa 33) Mwishowe, Yesu atoa dokezo nzuri sana—usihangaikie mambo ya kesho. Mbona uzidishe mahangaiko ya leo kwa kuhangaikia mambo ya kesho? (Mstari wa 34) Licha ya hayo, mbona uhangaikie mambo ambayo huenda yasitukie kamwe? Tunaweza kuepuka maumivu makali ya moyoni tukifuata shauri hilo la hekima katika ulimwengu huu uliojaa mikazo.
8 Ni wazi kwamba shauri la Yesu linafaa sana leo kama lilivyofaa miaka 2,000 hivi iliyopita. Je, hilo halithibitishi kwamba hekima hiyo ni ya kutoka juu? Hata mashauri bora ya wanadamu huhitaji kurekebishwa au kubadilishwa baada ya muda kupita. Lakini, miaka nenda miaka rudi, mafundisho ya Yesu yangali yanatumika na ni yenye faida. Hilo halipaswi kutushangaza kwa sababu Mshauri huyo wa Ajabu alisema “semi za Mungu.”—Yohana 3:34.
Njia Yake ya Kufundisha
9. Askari fulani walisema nini kuhusu ufundishaji wa Yesu, na kwa nini hawakuwa wakitia chumvi?
9 Njia ya Yesu ya kufundisha ni sehemu ya pili inayoonyesha hekima ya Mungu. Pindi moja, askari fulani waliotumwa kumkamata Yesu walirudi mikono mitupu na kusema: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.” (Yohana 7:45, 46) Hawakuwa wakitia chumvi. Yesu, ambaye ‘alitoka kwenye makao ya juu,’ alikuwa na ujuzi na uzoefu mwingi sana kuliko wanadamu wote waliopata kuishi. (Yohana 8:23) Hakuna mwanadamu yeyote aliyeweza kufundisha kama Yesu. Hebu fikiria njia mbili alizotumia Mwalimu huyo mwenye hekima.
“Umati ulistaajabishwa na njia yake ya kufundisha”
10, 11. (a) Kwa nini tunastaajabia jinsi Yesu alivyotumia vielezi? (b) Vielezi ni nini, na ni mfano upi unaoonyesha kwamba vielezi vya Yesu vina matokeo katika kufundisha?
10 Alitumia vielezi vinavyofaa. Twaambiwa kwamba ‘Yesu alisema na umati kwa vielezi. ‘Kwa kweli, bila kielezi hakuwa akisema nao.’ (Mathayo 13:34) Tunastaajabia uwezo wake usio na kifani wa kufundisha kweli muhimu kwa kutumia mambo ya kawaida. Alitumia mambo ambayo wasikilizaji wake walizoea, kama vile wakulima wanaopanda mbegu, wanawake wanaojitayarisha kuoka mikate, watoto wanaocheza sokoni, wavuvi wanaokokota nyavu, na wachungaji wanaotafuta kondoo waliopotea. Kweli muhimu zinapohusianishwa na mambo ya kawaida, zinatia mizizi mara moja katika akili na moyo.—Mathayo 11:16-19; 13:3-8, 33, 47-50; 18:12-14.
11 Mara nyingi Yesu alitumia vielezi au hadithi fupi ili kufundisha kweli za kiroho na za kiadili. Watu waliweza kukumbuka mafundisho ya Yesu kwa sababu hadithi fupi hueleweka na kukumbukwa kwa urahisi kuliko hoja za kuwaziwa tu. Katika vielezi vingi, Yesu alitumia mifano rahisi isiyosahaulika ili kuonyesha jinsi Baba yake alivyo. Kwa mfano, ni nani asiyeweza kuelewa maana ya kielezi cha mwana mpotevu—kwamba Yehova atamhurumia na kumkaribisha kwa upendo mtu aliyeasi anayetubu kikweli?—Luka 15:11-32.
12. (a) Yesu alitumiaje maswali alipofundisha? (b) Yesu aliwanyamazishaje wale waliotilia shaka mamlaka yake?
12 Alitumia maswali kwa ustadi. Yesu alitumia maswali ili kuwasaidia wasikilizaji wake wafikie mikataa yao wenyewe, wachunguze madhumuni yao, au wafanye maamuzi. (Mathayo 12:24-30; 17:24-27; 22:41-46) Viongozi wa kidini walipotilia shaka mamlaka aliyopewa na Mungu, Yesu aliwauliza: “Je, ubatizo wa Yohana ulikuwa wa kutoka mbinguni au wa kutoka kwa wanadamu?” Swali hilo liliwaduwaza, wakaanza kusababu hivi miongoni mwao: “Tukisema, ‘Kutoka mbinguni,’ atatuambia, ‘Basi, kwa nini hamkumwamini?’ Ingawa hivyo, tukisema, ‘Kutoka kwa wanadamu,’ tunao umati kuuhofu, kwa maana wao wote wamchukua Yohana kuwa nabii.” Hatimaye, wakajibu: “Hatujui.” (Marko 11:27-33; Mathayo 21:23-27) Yesu aliwauliza swali rahisi ambalo liliwanyamazisha na kufunua unafiki wao.
13-15. Hadithi ya Msamaria mwema inaonyeshaje hekima ya Yesu?
13 Nyakati nyingine Yesu alitumia mbinu mbalimbali kwa pamoja, alitoa vielezi na kuuliza maswali yenye kuchochea fikira. Mwanasheria mmoja Myahudi alipomwuliza Yesu jambo ambalo alipaswa kufanya ili apate uhai wa milele, Yesu alimkumbusha Sheria ya Musa ambayo inawaamuru watu wampende Mungu na jirani. Mtu huyo aliuliza hivi ili kujithibitisha kuwa mwadilifu: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kusimulia hadithi. Myahudi fulani alikuwa akisafiri peke yake aliposhambuliwa na wanyang’anyi na kuachwa akiwa mahututi. Wayahudi wawili walimpita, kwanza kuhani kisha Mlawi. Wote wakampuuza. Lakini baadaye Msamaria fulani alipitia hapo na kumwona. Kwa huruma nyingi, alifunga kwa uangalifu majeraha ya mtu huyo na akaonyesha upendo kwa kumpeleka kwenye nyumba ndogo ya wageni ili apate nafuu. Alipomaliza hadithi hiyo, Yesu alimwuliza yule mwanasheria hivi: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani kwa mtu aliyeanguka miongoni mwa wapokonyaji?” Mwanasheria huyo hakuwa na budi kujibu: “Yeye aliyetenda kwa rehema kumwelekea.”—Luka 10:25-37.
14 Hadithi hiyo inaonyeshaje hekima ya Yesu? Katika siku za Yesu, Wayahudi walitumia neno “jirani” kuwarejelea tu wale waliofuata mapokeo yao, na bila shaka hawakuwaona Wasamaria kuwa “jirani.” (Yohana 4:9) Kama Yesu angesema kwamba Msamaria ndiye aliyeshambuliwa na akasaidiwa na Myahudi, je, hilo lingekomesha ubaguzi wao? Kwa hekima, Yesu alitunga hadithi hiyo kwa njia ya kwamba Msamaria ndiye anayemtunza kwa upendo Myahudi. Fikiria pia swali ambalo Yesu aliuliza baada ya kusimulia hadithi hiyo. Alionyesha maana nyingine ya neno “jirani.” Ni kana kwamba yule mwanasheria aliuliza: ‘Ni nani jirani ninayepaswa kumpenda?’ Lakini Yesu akamwuliza: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani?” Yesu alikazia fikira yule Msamaria aliyeonyesha fadhili, wala si yule Myahudi aliyeonyeshwa fadhili. Jirani wa kweli huchukua hatua ya kuwapenda wengine bila kujali kabila lao. Yesu alifundisha somo hilo kwa njia bora kabisa.
15 Haishangazi kwamba watu walivutiwa na Yesu na kustaajabia “njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 7:28, 29) Pindi moja, “umati mkubwa” ulikaa naye kwa siku tatu bila kula!—Marko 8:1, 2.
Maisha Yake
16. Yesu ‘alithibitishaje’ kwamba aliongozwa na hekima ya Mungu?
16 Maisha ya Yesu ni sehemu ya tatu inayoonyesha hekima ya Yehova. Hekima huonyeshwa kwa matendo; inazaa matunda. Mwanafunzi Yakobo aliuliza: “Ni nani mwenye hekima miongoni mwenu?” Kisha akajibu swali hilo kwa kusema: “Basi, mwenendo wake bora uthibitishe jambo hilo.” (Yakobo 3:13, The New English Bible) Mwenendo wa Yesu ‘ulithibitisha’ kwamba aliongozwa na hekima ya Mungu. Hebu tuone jinsi alivyotumia busara maishani mwake na aliposhughulika na wengine.
17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alikuwa na usawaziko kamili maishani?
17 Je, umeona kwamba mara nyingi watu wasio na busara hupita kiasi? Naam, mtu anahitaji hekima ili kuwa na usawaziko. Yesu alionyesha hekima ya Mungu kwa kuwa na usawaziko kamili. Zaidi ya yote, alitanguliza mambo ya kiroho maishani mwake. Alijishughulisha sana na kazi ya kutangaza habari njema. “Ni kwa kusudi hilo nimetokea,” akasema. (Marko 1:38) Bila shaka, vitu vya kimwili havikuwa muhimu sana kwake; inaonekana kwamba alikuwa na vitu vichache sana. (Mathayo 8:20) Hata hivyo, hakujinyima starehe. Yesu alikuwa mwenye shangwe kama Baba yake, ambaye ni “Mungu mwenye furaha,” naye alizidisha shangwe ya wengine. (1 Timotheo 1:11; 6:15) Yesu hakuhudhuria karamu ya arusi—ambayo kwa kawaida huwa na muziki, uimbaji, na furaha—ili awaharibie wengine starehe. Divai ilipokwisha, aligeuza maji yakawa divai bora, kinywaji ambacho ‘kinaufurahisha moyo wa mtu.’ (Zaburi 104:15; Yohana 2:1-11) Yesu alikubali mialiko mingi ya chakula, na mara nyingi alitumia pindi hizo kufundisha.—Luka 10:38-42; 14:1-6.
18. Yesu alishughulikaje na wanafunzi wake kwa njia ya busara?
18 Yesu alishughulika na wengine kwa njia ya busara. Aliwajua wanafunzi wake vizuri kwa sababu alifahamu kabisa utu wa wanadamu. Alijua kwamba hawakuwa wakamilifu. Lakini, alitambua sifa zao nzuri. Alitambua kwamba wanafunzi hao waliovutwa na Yehova wangeweza kufanya mengi. (Yohana 6:44) Yesu alikuwa tayari kuwatumaini licha ya kasoro zao. Kwa mfano, alionyesha kwamba aliwatumaini wanafunzi wake kwa kuwakabidhi daraka zito. Aliwaagiza wahubiri habari njema, na alikuwa na hakika kwamba wangeweza kutimiza kazi hiyo. (Mathayo 28:19, 20) Kitabu cha Matendo kinathibitisha kwamba walitimiza kwa uaminifu kazi ambayo aliwaamuru wafanye. (Matendo 2:41, 42; 4:33; 5:27-32) Basi ni wazi kwamba Yesu alionyesha hekima kwa kuwatumaini.
19. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni”?
19 Kama tulivyoona kwenye Sura ya 20, Biblia inaonyesha kwamba unyenyekevu na upole zinahusiana na sifa ya hekima. Bila shaka, Yehova ndiye mfano bora kabisa wa sifa hizo. Lakini vipi Yesu? Inapendeza kuona jinsi Yesu alivyoshughulika na wanafunzi wake kwa unyenyekevu. Alikuwa bora kuliko wanafunzi wake kwa sababu alikuwa mkamilifu. Lakini, hakuwadharau wanafunzi wake. Hakujaribu kamwe kuwafanya wajione hawafai au wao ni bure tu. Kinyume chake, alijua udhaifu wao na alikuwa mwenye subira walipokosea. (Marko 14:34-38; Yohana 16:12) Je, haipendezi kwamba hata watoto walifurahi sana kuwa na Yesu? Bila shaka, walivutiwa naye kwa sababu waliona kwamba alikuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni.”—Mathayo 11:29; Marko 10:13-16.
20. Yesu alionyeshaje kwamba anasikiliza maoni ya wengine aliposhughulika na yule mwanamke asiye Myahudi ambaye alikuwa na binti aliyesumbuliwa na roho waovu?
20 Yesu aliiga unyenyekevu wa Mungu kwa njia nyingine muhimu. Alizingatia maoni ya wengine, wakati ilipofaa kuonyesha rehema. Kwa mfano, kumbuka wakati mwanamke fulani asiye Myahudi alipomsihi Yesu amponye binti yake aliyesumbuliwa sana na roho waovu. Mwanzoni, Yesu alionyesha kwa njia tatu kwamba hangemsaidia—kwanza, hakumjibu; pili, alimwambia moja kwa moja kwamba alikuwa ametumwa kwa Wayahudi wala si kwa wasio Wayahudi; na tatu, alitoa mfano ambao ulikazia kwa fadhili jambo hilo. Hata hivyo, mwanamke huyo hakuchoka, alionyesha kwamba alikuwa na imani ya pekee sana. Yesu alifanya nini kuhusiana na kisa hicho cha pekee? Alifanya jambo ambalo alikuwa amesema hangefanya. Alimponya binti ya mwanamke huyo. (Mathayo 15:21-28) Huo ni unyenyekevu wa pekee sana, sivyo? Kumbuka kwamba unyenyekevu ndio msingi wa hekima ya kweli.
21. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuiga utu, usemi, na njia ya Yesu ya kutenda mambo?
21 Tunashukuru kama nini kwamba Vitabu vya Injili vinatujulisha maneno na matendo ya mtu mwenye hekima zaidi aliyepata kuishi! Na tukumbuke kwamba Yesu alimwiga Baba yake kikamili. Tukiiga utu, usemi, na njia ya Yesu ya kutenda mambo, tutakuwa tukikuza hekima ya kutoka juu. Katika sura ifuatayo, tutaona jinsi tunavyoweza kutumia hekima ya Mungu maishani mwetu.
a Katika nyakati za Biblia, maseremala walijenga nyumba, walitengeneza fanicha, na vifaa vya kilimo. Justin Martyr, aliyeishi katika karne ya pili W.K., aliandika hivi kumhusu Yesu: “Alikuwa seremala maarufu aliyetengeneza plau na nira alipokuwa duniani.”
b Kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “hangaikia” kinamaanisha “kukengeushwa fikira.” Katika Mathayo 6:25, neno hilo linamaanisha woga na wasiwasi ambao unakengeusha au kupotosha fikira, na kumfanya mtu akose shangwe maishani.
c Uchunguzi wa sayansi umeonyesha kwamba kuhangaika na kufadhaika kupita kiasi kwaweza kusababisha ugonjwa wa moyo na magonjwa mengine yanayoweza kusababisha kifo.
-
-
Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 22
Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?
1-3. (a) Solomoni alionyeshaje hekima ya pekee katika kuamua ni nani aliyekuwa mama ya mtoto? (b) Yehova anaahidi kutupatia nini, na ni maswali gani yanayozuka?
ILIKUWA kesi ngumu sana—wanawake wawili walibishania mtoto mmoja mchanga. Wanawake hao waliishi pamoja, na mmoja wao alijifungua mwana siku chache tu baada ya mwingine kujifungua. Mtoto mmoja alikuwa amekufa, na kila mwanamke alidai kwamba mtoto aliyekuwa hai alikuwa wake.a Hapakuwa na watu wengine walioshuhudia lililotukia. Yaelekea kwamba kesi hiyo ilikuwa imesikilizwa katika mahakama ya chini lakini haikusuluhishwa. Mwishowe, kesi hiyo ilipelekwa kwa Solomoni, mfalme wa Israeli. Je, angefunua ukweli wa mambo?
2 Baada ya kuwasikiliza wanawake hao wakibishana kwa muda, Solomoni aliomba upanga. Kisha, akaamuru mtoto huyo akatwe vipande viwili na kila mwanamke apewe kipande kimoja. Mara moja mama ya mtoto huyo akamsihi mfalme amkabidhi yule mwanamke mwingine mtoto wake mpendwa. Lakini mwanamke yule mwingine aliendelea kusisitiza mtoto huyo akatwe vipande viwili. Sasa Solomoni akajua ukweli wa mambo. Alijua jinsi ambavyo mama humhurumia na kumpenda sana mtoto wake, naye alitumia ujuzi huo kutatua kesi hiyo. Hebu wazia furaha ya mama huyo Solomoni alipompa mtoto wake na kusema: “Yeye ndiye mama yake.”—1 Wafalme 3:16-27.
3 Solomoni alikuwa na hekima ya pekee, sivyo? Watu walistaajabu sana waliposikia jinsi Solomoni alivyosuluhisha kesi hiyo, “maana waliona ya kuwa hekima ya Mungu ilikuwa ndani yake.” Naam, hekima ya Solomoni ilikuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Yehova alikuwa amempa “moyo wa hekima na wa akili.” (1 Wafalme 3:12, 28) Lakini vipi sisi? Je, Mungu anaweza pia kutupatia hekima? Ndiyo. Solomoni aliongozwa kuandika hivi: “BWANA huwapa watu hekima.” (Mithali 2:6) Yehova aahidi kuwapa hekima, yaani, uwezo wa kutumia ujuzi, ufahamu, na utambuzi, wale wanaoitafuta kwa unyofu. Tunawezaje kupata hekima inayotoka juu? Na tutaitumiaje maishani mwetu?
Unawezaje ‘Kujipatia Hekima’?
4-7. Ni matakwa gani manne yanayohitajiwa ili kujipatia hekima?
4 Je, ni lazima tuwe na akili nyingi au elimu ya juu ili Mungu atupatie hekima yake? La. Yehova yu tayari kutupatia hekima bila kujali malezi au elimu yetu. (1 Wakorintho 1:26-29) Lakini ni lazima tuchukue hatua fulani, kwa sababu Biblia inatuhimiza ‘tujipatie hekima.’ (Mithali 4:7) Tutajipatiaje hekima?
5 Kwanza, ni lazima tumhofu Mungu. “Kumhofu Yehova ni mwanzo wa hekima [“hatua ya kwanza ya kupata hekima,” The New English Bible],” yasema Mithali 9:10, NW. Kumhofu Mungu ndio msingi wa hekima ya kweli. Kwa nini? Kumbuka kwamba hekima inatia ndani uwezo wa kutumia ujuzi kwa mafanikio. Kumhofu Mungu si kutetemeka kwa wasiwasi, bali ni kumsujudia kwa kicho, heshima, na kumtumaini. Hofu ya aina hiyo inafaa na humchochea sana mtu. Hutuchochea kuishi kupatana na ujuzi tulio nao kuhusu mapenzi ya Mungu na njia zake. Hilo ndilo jambo la hekima zaidi tuwezalo kufanya, kwa sababu sikuzote kanuni za Yehova huwafaidi kabisa wale wanaozifuata.
6 Pili, ni lazima tuwe wanyenyekevu na wenye kiasi. Hatuwezi kuwa na hekima ya Mungu tusipokuwa wanyenyekevu na wenye kiasi. (Mithali 11:2) Kwa nini? Tukiwa wanyenyekevu na wenye kiasi, tutakuwa tayari kukubali kwamba hatujui kila jambo. Tutakubali kwamba nyakati nyingine maoni yetu si sawa na hivyo tunahitaji kujifunza maoni ya Yehova. Yehova “huwapinga wenye kiburi,” lakini hufurahi kuwapa hekima wale walio wanyenyekevu moyoni.—Yakobo 4:6.
Ili kupata hekima ya Mungu, ni lazima tuitafute kwa bidii
7 Jambo la tatu muhimu ni kujifunza Neno la Mungu. Hekima ya Yehova imefunuliwa katika Neno lake. Ili kupata hekima hiyo, ni lazima tujitahidi kabisa kuitafuta. (Mithali 2:1-5) Takwa la nne ni sala. Tukimwomba Yehova hekima kwa unyofu, atatupatia kwa ukarimu. (Yakobo 1:5) Tukiomba msaada wa roho yake hatakosa kujibu sala zetu. Na roho yake itatuongoza kupata hazina zilizo katika Neno lake ambazo zinaweza kutusaidia kutatua matatizo, kuepuka hatari, na kufanya maamuzi ya hekima.—Luka 11:13.
8. Ni nini kitakachoonyesha kwamba tumejipatia hekima ya Mungu?
8 Kama tulivyoona katika Sura ya 17, hekima ya Yehova inazaa matunda. Kwa hiyo, mwenendo wetu utaonyesha wazi kwamba tumejipatia hekima ya Mungu. Mwanafunzi Yakobo alitaja sifa za hekima ya Mungu alipoandika hivi: “Hekima ya kutoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, isiyofanya tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.” (Yakobo 3:17) Tunapozungumzia kila moja ya sifa hizo za hekima ya Mungu, huenda tukajiuliza, ‘Je, hekima ya kutoka juu inaniongoza maishani?’
“Ni Safi Kiadili, Kisha Yenye Kufanya Amani”
9. Kuwa safi kiadili kwamaanisha nini, na kwa nini inafaa kwamba usafi wa kiadili ndiyo sifa inayotajwa kwanza katika orodha ya sifa za hekima?
9 “Kwanza kabisa ni safi kiadili.” Kuwa safi kiadili kwamaanisha kutakata na kuwa bila unajisi, si kwa nje tu bali pia moyoni. Biblia inahusianisha hekima na moyo, lakini hekima itokayo mbinguni haiwezi kuingia katika moyo uliotiwa unajisi na tamaa na mawazo maovu, na nia mbovu. (Mithali 2:10; Mathayo 15:19, 20) Lakini, kama moyo wetu ni safi kiadili—yaani, kwa kadiri ambavyo wanadamu wasiokamilika wanaweza kuwa safi—‘tutajiepusha na uovu na tutatenda mema.’ (Zaburi 37:27; Mithali 3:7) Kwa kufaa, usafi wa kiadili unatajwa kwanza katika orodha ya sifa za hekima. Hatuwezi kuwa na sifa nyingine za hekima ya kutoka juu tusipokuwa safi kiadili na kiroho.
10, 11. (a) Kwa nini ni muhimu tuwe watu wanaofanya amani? (b) Ukigundua kwamba umemkosea mwabudu mwenzako, utaonyeshaje kwamba wewe ni mtu anayefanya amani? (Ona pia kielezi-chini.)
10 “Kisha yenye kufanya amani.” Hekima ya kutoka mbinguni hutuchochea kufuatia amani, ambayo ni tunda la roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Tunajitahidi sana kutoharibu ‘kifungo cha amani’ kinachowaunganisha watu wa Yehova. (Waefeso 4:3) Sisi pia hujitahidi kabisa kurudisha amani inapovurugwa. Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo? Biblia inasema: “Endeleeni . . . kuishi kwa kufanya amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.” (2 Wakorintho 13:11) Mungu wa amani atakuwa pamoja nasi maadamu tunaendelea kufanya amani. Uhusiano wetu na Yehova unategemea jinsi tunavyowatendea waabudu wenzetu. Tunawezaje kuwa watu wanaofanya amani? Fikiria mfano ufuatao.
11 Unapaswa kufanya nini ukigundua kwamba umemkosea mwabudu mwenzako? Yesu alisema: “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.” (Mathayo 5:23, 24) Unaweza kutumia shauri hilo kwa kuchukua hatua ya kwenda kumwona ndugu yako. Ukiwa na kusudi gani? Ili ‘ufanye amani yako’ naye.b Ili kutimiza kusudi hilo, huenda ukahitaji kukubali kwamba umemwumiza kihisia. Ukimfikia kwa kusudi la kufanya amani na udumishe mtazamo huo, yaelekea kwamba tatizo litasuluhishwa, utaomba msamaha na utasamehewa. Unapochukua hatua ya kufanya amani, unaonyesha kwamba unaongozwa na hekima ya Mungu.
“Yenye Kukubali Sababu, Tayari Kutii”
12, 13. (a) Neno linalotafsiriwa “-enye kukubali sababu” katika Yakobo 3:17 linamaanisha nini? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba sisi ni wenye kukubali sababu?
12 “Yenye kukubali sababu.” Ni nini maana ya kukubali sababu? Wasomi wa Biblia wanasema kwamba si rahisi kutafsiri neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “-enye kukubali sababu” kwenye Yakobo 3:17. Watafsiri wametumia maneno kama vile “upole,” “ustahimilivu,” na “mwenye kujali.” Neno la Kigiriki linamaanisha kihalisi “mwenye kukubali maoni ya wengine.” Tunawezaje kuonyesha kwamba tunaongozwa na sifa hiyo ya hekima ya kutoka juu?
13 Andiko la Wafilipi 4:5 lasema: “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote.” Tafsiri nyingine inasema: “Mjulikane kuwa watu wenye kukubali sababu.” (The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips) Ona kwamba jambo muhimu si jinsi tunavyojiona; bali ni jinsi wengine wanavyotuona. Mtu mwenye kukubali sababu hafuatilii mambo madogo-madogo ya sheria au hasisitizi mambo yafanywe jinsi anavyopenda. Badala yake, yuko tayari kuwasikiliza wengine na kukubali maoni yao inapowezekana. Yeye pia ni mpole, si mkali au mkatili. Hiyo ni sifa muhimu kwa Wakristo wote, lakini hasa kwa wazee wa kutaniko. Upole huvutia, kwa hiyo watu hujihisi huru kuongea na wazee wapole. (1 Wathesalonike 2:7, 8) Ni muhimu sote tujiulize hivi: ‘Je, wengine huniona kuwa mtu mwenye kuwajali wengine, mwenye kukubali sababu, na mpole?’
14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuko “tayari kutii”?
14 “Tayari kutii.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tayari kutii” linapatikana mara moja tu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Msomi mmoja anasema kwamba neno hilo “hutumiwa mara nyingi kuhusiana na nidhamu ya kijeshi.” Linaweza kumaanisha “mtu anayeshawishiwa kwa urahisi” na “mtiifu.” Mtu anayeongozwa na hekima ya kutoka juu huwa tayari kutii Maandiko. Hashikilii sana maoni yake na kukataa hoja zozote ambazo zinapinga maoni yake. Badala yake, yeye hubadili maoni mara moja anapothibitishiwa kwa Maandiko kwamba amefanya uamuzi mbaya au maoni yake ni yenye kosa. Je, ndivyo wengine wanavyokuona?
“Yenye Kujaa Rehema na Matunda Mema”
15. Rehema ni nini, na kwa nini inafaa kwamba andiko la Yakobo 3:17 linataja “rehema” pamoja na “matunda mema”?
15 “Yenye kujaa rehema na matunda mema.”c Rehema ni sifa muhimu ya hekima ya kutoka juu, kwa sababu inasemekana kwamba hekima hiyo ‘imejaa rehema.’ Ona kwamba “rehema” inatajwa pamoja na “matunda mema.” Jambo hilo linafaa kwa sababu katika Biblia, mara nyingi rehema humaanisha kuwajali sana wengine na kuwatendea mambo mengi ya fadhili kwa huruma. Kichapo kimoja cha marejeo chafafanua rehema kuwa “hali ya kuhuzunishwa na hali mbaya ya mtu mwingine na kujaribu kumsaidia.” Kwa hiyo, hekima ya Mungu si baridi wala haitegemei akili tu. Badala yake, ni yenye upendo na huruma, na inawajali wengine. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tumejaa rehema?
16, 17. (a) Mbali na kumpenda Mungu, ni nini kinachotuchochea tushiriki kazi ya kuhubiri, na kwa nini? (b) Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema?
16 Bila shaka njia bora ya kuonyesha sifa hiyo ni kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Ni nini kinachotuchochea kufanya kazi hiyo? Hasa ni kwa sababu tunampenda Mungu. Tunachochewa pia na rehema, au huruma. (Mathayo 22:37-39) Watu wengi leo ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Wamepuuzwa na kupofushwa kiroho na wachungaji wa uwongo wa kidini. Ndiyo sababu hawajui mwongozo wenye hekima ulio katika Neno la Mungu wala hawajui baraka zitakazoletwa duniani na Ufalme huo hivi karibuni. Kwa hiyo, tunapozingatia mahitaji ya kiroho ya jirani zetu, tunachochewa na huruma kutoka moyoni kujitahidi kadiri tuwezavyo kuwaambia kusudi la Yehova lenye upendo.
Tunapowaonyesha wengine rehema, au huruma, tunadhihirisha “hekima ya kutoka juu”
17 Ni katika njia zipi nyingine tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema? Kumbuka mfano wa Yesu wa yule Msamaria aliyemkuta msafiri fulani aliyelala kando ya barabara baada ya kupigwa na kuporwa. Msamaria huyo alimhurumia na ‘akatenda kwa rehema.’ Alimfunga majeraha na kumtunza. (Luka 10:29-37) Mfano huo waonyesha kwamba kuwa na rehema kwahusisha kuwasaidia wenye uhitaji. Biblia inatuambia “tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Fikiria mifano kadhaa. Huenda mwamini mwenzako aliye mzee kwa umri anahitaji kusaidiwa kusafiri kwenda kwenye mikutano ya Kikristo na kurudi. Huenda mjane fulani kutanikoni anahitaji kusaidiwa kurekebisha nyumba yake. (Yakobo 1:27) Huenda mtu fulani aliyeshuka moyo anahitaji kuambiwa “neno jema” la kumfariji. (Mithali 12:25) Tunapoonyesha rehema katika njia hizo, tunathibitisha kwamba tunaongozwa na hekima ya kutoka juu.
‘Isiyobagua, Si ya Kinafiki’
18. Ikiwa tunaongozwa na hekima ya kutoka juu, tunapaswa kujitahidi kuondoa nini mioyoni mwetu, na kwa nini?
18 “Isiyobagua.” Hekima ya Mungu hushinda kabisa ubaguzi wa kikabila na uzalendo. Ikiwa tunaongozwa na hekima hiyo, tunapaswa kujitahidi kuondoa kabisa mioyoni mwetu mwelekeo wowote wa kuonyesha upendeleo. (Yakobo 2:9) Hatuwapendelei watu fulani kwa sababu ya elimu yao, utajiri wao, au madaraka yao kutanikoni; wala hatumdharau mwabudu mwenzetu, hata ikiwa anaonekana kuwa na cheo cha chini sana katika jamii. Ikiwa Yehova anawapenda watu hao, hapana shaka kwamba sisi tunapaswa kuwapenda pia.
19, 20. (a) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” latokana na nini? (b) Tunaonyeshaje “shauku ya kidugu isiyo na unafiki,” na kwa nini jambo hilo ni muhimu?
19 “Si ya kinafiki.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” linaweza kurejelea “mwigizaji katika mchezo wa kuigiza.” Katika nyakati za kale, waigizaji Wagiriki na Waroma walivaa vinyago vikubwa usoni katika michezo ya kuigiza. Kwa hiyo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” likaanza kutumiwa kumaanisha mtu anayejifanya, au mtu anayejisingizia. Hekima ya Mungu inapaswa kuongoza jinsi tunavyowatendea waabudu wenzetu na pia jinsi tunavyowaona.
20 Mtume Petro alisema kwamba ‘tukitii ile kweli’ tutakuwa na “shauku ya kidugu isiyo na unafiki.” (1 Petro 1:22) Naam, shauku yetu kwa ndugu zetu haipaswi kuwa ya kujionyesha tu. Hatujifanyi wala kujisingizia ili tuwadanganye wengine. Ni lazima shauku yetu iwe ya kweli, ya kutoka moyoni. Tukiwa na shauku ya aina hiyo, waamini wenzetu watatuamini kwa sababu watajua kwamba sisi si wanafiki. Unyofu wa aina hiyo hutokeza uhusiano mzuri kati ya Wakristo na pia huchangia hali ya kuaminiana kutanikoni.
“Shika Hekima Kamili”
21, 22. (a) Solomoni alishindwaje kushika hekima kamili? (b) Tunawezaje kushika hekima, na tutapata faida gani tukifanya hivyo?
21 Tunahitaji kushika hekima kwa sababu ni zawadi kutoka kwa Yehova. Solomoni alisema: “Mwanangu, . . . shika hekima kamili na busara.” (Mithali 3:21) Kwa kusikitisha, Solomoni mwenyewe alishindwa kufanya hivyo. Alikuwa mwenye hekima maadamu alitii kutoka moyoni. Lakini mwishowe, wake zake wengi wa kigeni waliugeuza moyo wake kutoka kwa ibada safi ya Yehova. (1 Wafalme 11:1-8) Hali iliyompata Solomoni inaonyesha kwamba tusipotumia ifaavyo ujuzi tulio nao hautatufaidi.
22 Tunawezaje kushika hekima kamili? Haitoshi tu kusoma kwa ukawaida Biblia na vichapo vya Biblia vinavyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Ni lazima pia tujitahidi kutumia mambo tunayojifunza. (Mathayo 24:45) Tuna kila sababu ya kutumia hekima ya Mungu. Tukifanya hivyo, tutakuwa na maisha bora sasa. Inatuwezesha “kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi,” yaani, uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Timotheo 6:19) Na jambo la muhimu hata zaidi ni kwamba tunapokuza hekima ya kutoka juu tunamkaribia zaidi Yehova Mungu, chanzo cha hekima yote.
a Andiko la 1 Wafalme 3:16 linasema kwamba wanawake hao walikuwa makahaba. Kichapo Insight on the Scriptures chasema: “Huenda wanawake hao hawakuwa makahaba wa kulipwa bali walikuwa wamefanya uasherati. Labda walikuwa wanawake Wayahudi au wanawake wa kigeni.”—Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Usemi wa Kigiriki unaotafsiriwa “fanya amani yako” unatokana na kitenzi kinachomaanisha “‘kuleta badiliko, kubadilishana,’ na hivyo, ‘kupatanisha.’” Kwa hiyo, kusudi lako ni kubadilisha hali, na ikiwezekana, kuondoa chuki iliyo moyoni mwa yule aliyekosewa.—Waroma 12:18.
c Biblia Habari Njema inatafsiri hivi maneno hayo: “Imejaa huruma na huzaa matunda ya matendo mema.”
-
-
“Alitupenda Sisi Kwanza”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 23
“Alitupenda Sisi Kwanza”
1-3. Ni mambo yapi yaliyofanya kifo cha Yesu kiwe cha pekee sana katika historia yote?
SIKU moja miaka 2,000 hivi iliyopita, mtu fulani asiye na hatia alishtakiwa, akahukumiwa kwa sababu ya uhalifu ambao hakufanya, kisha akateswa hadi akafa. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba yeye ni baadhi tu ya watu ambao wameuawa kikatili katika historia. Lakini kifo chake kilikuwa cha pekee sana.
2 Mtu huyo alipokuwa akiteseka kwa maumivu makali saa chache kabla ya kufa, kulikuwa na ishara mbinguni kuonyesha kwamba hilo lilikuwa tukio muhimu sana. Giza liliifunika dunia yote ghafula yapata saa sita mchana. Mwanahistoria mmoja alisema kwamba “nuru ya jua ilikosekana.” (Luka 23:44, 45) Kisha, kabla tu ya kufa, akasema maneno haya yasiyosahaulika: “Imetimizwa!” Kwa kweli, alitimiza jambo zuri sana alipodhabihu uhai wake. Kwa kudhabihu uhai wake, alionyesha upendo ambao hakuna mwanadamu yeyote amewahi kuonyesha.—Yohana 15:13; 19:30.
3 Mtu huyo alikuwa Yesu Kristo. Mateso na kifo chake katika siku hiyo ya kuhuzunisha, Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., ni mambo yanayojulikana sana. Hata hivyo, jambo fulani muhimu limepuuzwa mara nyingi. Ingawa Yesu aliteseka sana, kuna mwingine aliyeteseka hata zaidi. Kwa kweli, kuna mwingine aliyejidhabihu kwa njia kubwa hata zaidi siku hiyo—alitenda tendo kuu zaidi la upendo ambalo halijawahi kufanywa na yeyote katika ulimwengu mzima. Ni tendo gani hilo? Jibu la swali hilo ni utangulizi ufaao wa habari muhimu zaidi ya habari zote: Upendo wa Yehova.
Tendo Kuu Zaidi la Upendo
4. Askari Mroma alipataje kujua kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida, naye alikata kauli gani?
4 Askari Mroma aliyesimamia mauaji ya Yesu alipigwa na bumbuazi alipoona giza lililotokea kabla ya Yesu kufa na tetemeko kubwa la dunia lililotokea baadaye. Alisema hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mathayo 27:54) Ni wazi kwamba Yesu hakuwa mtu wa kawaida. Askari huyo aliunga mkono mauaji ya Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu Mwenyezi! Mwana huyo alipendwa na Baba yake kwa kadiri gani?
5. Ni mfano gani umetolewa ili kutusaidia kuelewa kwamba Yehova na Mwanaye wamekuwa pamoja mbinguni kwa muda mrefu sana?
5 Biblia inamwita Yesu “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Hebu fikiria—Mwana wa Yehova alikuwapo kabla ya ulimwengu kuumbwa. Basi, Mwana huyo alikaa na Baba yake kwa muda gani? Wanasayansi fulani wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo kwa muda wa miaka bilioni 13. Huo ni muda usiowazika, sivyo? Ili kuwasaidia watu waelewe muda ambao wanasayansi wanakisia kwamba ulimwengu umekuwapo, jengo moja lenye mitambo ya kuigiza miendo ya sayari lina chati ya tarehe yenye urefu wa meta 110. Wageni wanapotembea kando ya chati hiyo, kila hatua wanayopiga inawakilisha miaka ipatayo milioni 75 ya muda ambao ulimwengu umekuwapo. Alama ndogo inayolingana na unene wa unywele wa mwanadamu imewekwa mwishoni mwa chati hiyo ili kuwakilisha muda ambao wanadamu wameishi duniani! Lakini, hata ikiwa makisio hayo ni sahihi, urefu wa chati hiyo hauwezi kamwe kuwakilisha umri wa Mwana wa Yehova! Alikuwa akifanya kazi gani wakati huo wote?
6. (a) Mwana wa Yehova alikuwa akifanya nini kabla ya kuwa mwanadamu? (b) Yehova na Mwanaye wanaunganishwa na kifungo cha aina gani?
6 Mwana huyo alifurahi kutumiwa na Baba yake akiwa “stadi wa kazi.” (Mithali 8:30) Biblia inasema hivi: “Na bila yeye [Mwana] hata kitu kimoja hakikuja kuwako.” (Yohana 1:3) Kwa hiyo Yehova na Mwanaye walishirikiana kuumba vitu vingine vyote. Walikuwa na kazi zenye kuvutia na kufurahisha kwelikweli. Watu wengi hukubali kwamba mzazi na mtoto hupendana sana. Na upendo “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Basi, ni nani kati yetu anayeweza kuelewa kwa ukamili nguvu za kifungo ambacho kimekuwapo kwa muda mrefu hivyo? Ni wazi kwamba Yehova Mungu na Mwanaye wameunganishwa na kifungo cha upendo chenye nguvu kuliko kifungo chochote kile.
7. Yesu alipobatizwa, Yehova alionyeshaje hisia zake kumwelekea?
7 Hata hivyo, Baba alimtuma Mwanaye duniani ili azaliwe akiwa mwanadamu. Kwa hivyo, Yehova hakuweza kushirikiana kwa ukaribu na Mwanaye mpendwa huko mbinguni kwa miaka kadhaa. Akiwa mbinguni, Yehova alipendezwa sana kumtazama Yesu akikua hadi akawa mwanamume mkamilifu. Yesu alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi. Tunajua jinsi Yehova Baba yake alivyohisi kumhusu, hata alisema moja kwa moja kutoka mbinguni: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Bila shaka Baba ya Yesu alifurahi sana kumwona akifanya kwa uaminifu yote yaliyotabiriwa, mambo yote ambayo alipaswa kufanya!—Yohana 5:36; 17:4.
8, 9. (a) Yesu alitendewaje Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., na Baba yake wa mbinguni alihisije? (b) Kwa nini Yehova alimruhusu Mwanaye ateseke na kufa?
8 Hata hivyo, Yehova alihisije Nisani 14, mwaka wa 33 W.K.? Alihisije Yesu aliposalitiwa na kukamatwa na umati usiku? Alihisije Yesu alipoachwa na rafiki zake na kushtakiwa isivyo haki? Alihisije Yesu alipodhihakiwa, kutemewa mate, na kupigwa ngumi? Alihisije alipopigwa mijeledi iliyochanachana mgongo wake? Alihisije mikono na miguu yake ilipopigiliwa misumari kwenye mti, kisha akaachwa akiwa amening’inia huku watu wakimtukana? Baba alihisije Mwanaye mpendwa alipokuwa akimlilia kwa maumivu makali? Yehova alihisije Yesu alipokata pumzi, na kwa mara ya kwanza kabisa tangu mwanzo wa uumbaji wote, Mwanaye mpendwa akakoma kuwapo?—Mathayo 26:14-16, 46, 47, 56, 59, 67; 27:38-44, 46; Yohana 19:1.
’Mungu alitoa Mwana wake mzaliwa pekee’
9 Hatuna la kusema. Kwa kuwa Yehova ana hisia, hatuwezi kamwe kueleza uchungu ambao alihisi kwa sababu ya kifo cha Mwanaye. Lakini tunaweza kueleza kusudi la Yehova la kuruhusu jambo hilo litukie. Kwa nini Baba ya Yesu alijiruhusu kupatwa na uchungu huo? Yehova anatueleza jambo la kupendeza katika Yohana 3:16—mstari huu wa Biblia ni muhimu sana hivi kwamba umeitwa Injili ndogo. Andiko hilo lasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” Kwa hiyo, Yehova alifanya hivyo kwa sababu ya upendo. Zawadi ambayo Yehova alitoa—kumtuma Mwanaye ateseke na kufa kwa ajili yetu—ndiyo tendo kuu zaidi la upendo ambalo limewahi kufanywa.
Maana ya Upendo wa Mungu
10. Wanadamu wana uhitaji gani, na kwa nini ni vigumu kuelewa maana ya neno “upendo”?
10 Neno “upendo” lamaanisha nini? Imesemwa kwamba upendo ndio uhitaji mkubwa zaidi wa wanadamu. Tangu wanapozaliwa hadi wanapokufa, watu hutamani sana kupendwa, wanaishi kwa furaha wanapopendwa, na hata wanadhoofika na kufa wasipopendwa. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba si rahisi kueleza maana ya upendo. Bila shaka, watu huongea sana kuhusu upendo. Watu wanaendelea kuandika vitabu, kutunga nyimbo, na mashairi mengi sana kuhusu upendo. Hata hivyo, nyakati nyingine hawafafanui ifaavyo maana ya upendo. Neno hilo limetumiwa sana hivi kwamba inaonekana limepoteza maana.
11, 12. (a) Ni wapi tu tunaweza kujifunza mambo mengi kuhusu upendo, na kwa nini? (b) Kigiriki cha awali kinataja kihususa upendo gani mbalimbali, na ni “upendo” gani unaotajwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? (Ona pia kielezi-chini.) (c) A·gaʹpe ni nini?
11 Hata hivyo, Biblia inafundisha waziwazi kuhusu upendo. Kamusi ya Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words yasema hivi: “Upendo unaweza kuonyeshwa tu kupitia matendo.” Masimulizi ya Biblia kuhusu matendo ya Yehova yanatufundisha mengi kuhusu upendo wake ambao unamchochea kuwatendea viumbe wake kwa fadhili. Kwa mfano, ni jambo gani linaloweza kuonyesha sifa hiyo kwa njia bora kuliko tendo kuu zaidi la upendo wa Yehova tulilozungumzia awali? Tutaona matendo mengi ya Yehova ya upendo katika sura zinazofuata. Zaidi ya hayo, tunaweza kupata ufahamu wa ndani kutokana na maneno ya awali yanayotafsiriwa “upendo” katika Biblia. Kigiriki cha awali kilikuwa na maneno manne yaliyotafsiriwa “upendo.”a Kati ya maneno hayo, a·gaʹpe hutumiwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kamusi moja ya Biblia inasema kwamba hilo “ndilo neno linaloeleza upendo kwa njia nzuri zaidi.” Kwa nini?
12 A·gaʹpe ni upendo unaoongozwa na kanuni. Si hisia tunayokuwa nayo bila kufikiri. Upendo huo unatia ndani mambo mengi, unahusisha fikira na una kusudi fulani. Zaidi ya yote, upendo wa a·gaʹpe hauna ubinafsi. Kwa mfano, soma tena Yohana 3:16. Ni “ulimwengu” upi ambao Mungu aliupenda sana hivi kwamba akamtoa Mwanaye mzaliwa-pekee? Ulimwengu huo ni wanadamu wanaoweza kukombolewa. Unatia ndani watu wengi ambao wanaendelea kutenda dhambi maishani. Je, Yehova anampenda kila mtu kama alivyompenda Abrahamu mwaminifu, aliyekuwa rafiki yake? (Yakobo 2:23) La, lakini kwa upendo, Yehova anawatendea watu wote mema hata kwa hasara yake. Anataka watu wote watubu na kubadili njia zao. (2 Petro 3:9) Wengi hufanya hivyo. Naye hufurahi kuwa rafiki yao.
13, 14. Ni nini kinachoonyesha kwamba mara nyingi a·gaʹpe huhusisha shauku ya kirafiki?
13 Hata hivyo, watu fulani wana maoni yasiyofaa kuhusu a·gaʹpe. Wanafikiri kwamba huo ni upendo usio na hisia, unaoongozwa na akili tu. Ukweli ni kwamba mara nyingi a·gaʹpe huhusisha uhusiano wa karibu wenye upendo. Kwa mfano, Yohana alipoandika, “Baba humpenda Mwana,” alitumia aina fulani ya neno a·gaʹpe. Je, upendo huo hauna shauku ya kirafiki? Ona kwamba Yesu alisema “Baba ana shauku na Mwana,” na hapo anatumia aina fulani ya neno phi·leʹo. (Yohana 3:35; 5:20) Mara nyingi upendo wa Yehova hutia ndani shauku ya moyoni. Lakini, upendo wake hautegemei kamwe hisia. Sikuzote unaongozwa na kanuni zake za hekima na haki.
14 Kama tulivyoona, sifa zote za Yehova ni bora sana, ni kamilifu, na zinavutia. Lakini upendo unavutia kuliko sifa nyingine zote. Hakuna kitu kinachotufanya tumkaribie Yehova kama upendo. Inafurahisha kwamba upendo ndio sifa kuu zaidi ya Yehova. Twajuaje?
“Mungu Ni Upendo”
15. Biblia inasema nini kuhusu sifa ya Yehova ya upendo, na kwa nini usemi huo ni wa pekee sana? (Ona pia kielezi-chini.)
15 Biblia inasema jambo fulani la pekee kuhusu upendo ambalo haisemi kuhusu zile sifa nyingine kuu za Yehova. Maandiko hayasemi kwamba Mungu ni nguvu wala hayasemi kwamba Mungu ni haki au hata Mungu ni hekima. Ana sifa hizo, yeye ndiye chanzo chake, na hana kifani katika sifa hizo tatu. Hata hivyo, kuhusu sifa ya nne, Biblia inasema jambo fulani la pekee sana: “Mungu ni upendo.”b (1 Yohana 4:8) Hilo lamaanisha nini?
16-18. (a) Kwa nini Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo”? (b) Kati ya viumbe wote duniani, kwa nini mwanadamu ni mfano unaofaa wa sifa ya Yehova ya upendo?
16 Usemi “Mungu ni upendo” haulingani na usemi, “Mungu ni sawa na upendo.” Hatuwezi kamwe kugeuza usemi huo na kusema “upendo ni Mungu.” Yehova si sifa fulani tu. Ana utu, na mbali na upendo ana hisia na sifa nyingi mbalimbali. Hata hivyo, Yehova ana upendo mwingi sana. Kichapo kimoja cha marejeo kinasema hivi kuhusu mstari huo: “Upendo ni utu au sifa ya asili ya Mungu.” Kwa ujumla, tunaweza kulifikiria jambo hilo kwa njia hii: Nguvu za Yehova humwezesha kutenda. Haki na hekima yake humwongoza kutenda. Lakini upendo wa Yehova humchochea kutenda. Naye sikuzote hutumia sifa nyingine zote kupatana na upendo wake.
17 Mara nyingi imesemwa kwamba Yehova ni wonyesho halisi wa upendo. Kwa hiyo, tukitaka kujifunza kuhusu upendo unaotegemea kanuni, ni lazima tujifunze kumhusu Yehova. Bila shaka, wanadamu pia wana sifa hiyo yenye kupendeza. Lakini kwa nini wanadamu wana sifa hiyo? Wakati wa uumbaji, Yehova alimwambia hivi Mwanaye: “Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” (Mwanzo 1:26) Kati ya viumbe wote duniani, ni wanaume na wanawake tu wanaoweza kupenda na hivyo kumwiga Baba yao wa mbinguni. Kumbuka kwamba Yehova alitumia viumbe mbalimbali kuwa mifano ya sifa zake kuu. Hata hivyo, Yehova alimtumia mwanadamu—kiumbe bora zaidi duniani—kuwa mfano wa sifa Yake kuu zaidi ya upendo.—Ezekieli 1:10.
18 Tunapowapenda wengine bila ubinafsi kupatana na kanuni, tunaonyesha sifa kuu zaidi ya Yehova. Ni kama mtume Yohana alivyoandika: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Lakini Yehova alitupenda kwanza kwa njia zipi?
Yehova Alitupenda Kwanza
19. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba upendo ndio uliomfanya Yehova aumbe?
19 Upendo si sifa mpya. Ni nini kilichomfanya Yehova aanze kuumba? Si kwa sababu alikuwa mpweke na alihitaji mwandani. Yehova ni kamili, hapungukiwi kwa vyovyote wala hahitaji msaada wa yeyote. Lakini alichochewa na sifa yake ya upendo ambayo inaonyeshwa kwa matendo, awape uhai viumbe wake wenye akili ambao wangeweza kuthamini zawadi hiyo. Mwanaye mzaliwa-pekee alikuwa “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufunuo 3:14) Yehova alimtumia Stadi huyo wa Kazi kuumba vitu vinginevyo vyote, kuanzia malaika. (Ayubu 38:4, 7; Wakolosai 1:16) Wakiwa wamepewa uhuru, akili, na hisia, viumbe hao wa roho wenye nguvu waliweza kuwa na uhusiano wenye upendo—kati yao wenyewe na, zaidi ya yote, pamoja na Yehova Mungu. (2 Wakorintho 3:17) Kwa hiyo, walipendana kwa sababu walipendwa kwanza.
20, 21. Ni mambo gani yaliyoonyesha kwamba Yehova aliwapenda Adamu na Hawa, lakini walitendaje?
20 Ndivyo na wanadamu. Tangu mwanzo, Adamu na Hawa walionyeshwa upendo mwingi sana. Kulikuwa na mambo mengi katika makao yao ya Paradiso ya Edeni yaliyowathibitishia kwamba Baba yao aliwapenda. Angalia jinsi Biblia inavyosema: “BWANA Mungu akapanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya.” (Mwanzo 2:8) Je, umewahi kutembelea bustani maridadi kwelikweli? Ni nini kilichokupendeza zaidi? Je, ni nuru iliyopenya majani ya miti kwenye sehemu ya bustani iliyo kimya na yenye kivuli? Je, ni rangi zenye kuvutia sana za maua? Je, ni sauti ya bubujiko la kijito, ndege wanaoimba, na wadudu wanaovuma? Vipi harufu nzuri ya miti, matunda na maua yaliyochanua? Kwa vyovyote vile, hakuna bustani leo inayoweza kulinganishwa na bustani ya Edeni. Kwa nini?
21 Bustani hiyo ilipandwa na Yehova mwenyewe! Bila shaka ilikuwa maridadi isivyoelezeka. Ilikuwa na kila aina ya mti wenye kuvutia na wenye matunda matamu. Bustani hiyo ilikuwa na maji ya kutosha, ilikuwa kubwa sana, na ilikuwa na wanyama mbalimbali wenye kuvutia. Adamu na Hawa walikuwa na kila kitu walichohitaji ili kuishi maisha yenye furaha na yenye kuridhisha, na walikuwa na kazi yenye kuridhisha na urafiki mkamilifu. Yehova aliwapenda kwanza, na walikuwa na kila sababu ya kumpenda vilevile. Lakini walishindwa kufanya hivyo. Badala ya kumtii Baba yao wa mbinguni kwa upendo, walimwasi kwa sababu ya ubinafsi.—Mwanzo, sura ya 2.
22. Hatua ambayo Yehova alichukua baada ya uasi katika Edeni ilithibitishaje kwamba upendo wake ni mwaminifu?
22 Jambo hilo lilimhuzunisha Yehova sana. Lakini je, uasi huo ulitia uchungu moyo wake wenye upendo? La! “Fadhili zake [au, “upendo-mwaminifu,” NW, kielezi-chini] ni za milele.” (Zaburi 136:1) Kwa hiyo, kwa upendo, alikusudia mara moja kufanya mipango ya kumkomboa mzao yeyote wa Adamu na Hawa ambaye ana mwelekeo unaofaa. Kama tulivyoona, mipango hiyo ilitia ndani dhabihu ya fidia ya Mwanaye mpendwa, ambayo ilimgharimu sana Baba yake.—1 Yohana 4:10.
23. Taja sababu moja inayomfanya Yehova awe “Mungu mwenye furaha,” na sura inayofuata itajibu swali gani muhimu?
23 Naam, tangu mwanzo Yehova amechukua hatua ya kwanza kuwapenda wanadamu. ‘Alitupenda kwanza’ katika njia nyingi sana. Upendo hudumisha amani na shangwe, ndiyo sababu Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Hata hivyo, swali muhimu linazuka. Je, kweli Yehova anampenda kila mmoja wetu? Sura inayofuata itajibu swali hilo.
a Kitenzi phi·leʹo, kinachomaanisha ‘kuwa na shauku, kuthamini, au kupenda (kama mtu anavyompenda rafiki wa karibu au ndugu),” hutumiwa mara nyingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Aina fulani ya neno stor·geʹ, au upendo uliopo kati ya watu wa familia, inatumiwa kwenye 2 Timotheo 3:3 kuonyesha kwamba upendo huo ungekuwa haba katika siku za mwisho. Neno Eʹros, au upendo wa kimahaba kati ya watu wa jinsia tofauti, halitajwi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ijapokuwa upendo huo unazungumziwa katika Biblia.—Mithali 5:15-20.
b Maandiko mengine yanatumia semi kama hizo. Kwa mfano, “Mungu ni nuru” na “Mungu . . . ni moto unaokula kabisa.” (1 Yohana 1:5; Waebrania 12:29) Lakini semi hizo zinapasa kuonwa kuwa milinganisho (sitiari), kwa kuwa zinamlinganisha Yehova na vitu vya asili. Yehova ni kama nuru, kwa kuwa yeye ni mtakatifu na mwadilifu. Hana “giza” wala uchafu wowote. Naye anaweza kulinganishwa na moto kwa sababu ya nguvu zake za kuangamiza.
-
-
Hakuna Kitu Kinachoweza “Kututenga na Upendo wa Mungu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 24
Hakuna Kitu Kinachoweza “Kututenga na Upendo wa Mungu”
1. Watu wengi, kutia ndani Wakristo fulani wa kweli, wana maoni gani yenye kuvunja moyo?
JE, YEHOVA anakupenda? Baadhi ya watu wanakubali kwamba Mungu anawapenda wanadamu kwa ujumla kama andiko la Yohana 3:16 linavyosema. Lakini wanahisi hivi: ‘Mungu hawezi kamwe kunipenda mimi.’ Mara kwa mara, hata Wakristo wa kweli huenda wakawa na shaka kuhusu jambo hilo. Mtu mmoja aliyevunjika moyo alisema: “Siwezi kuamini kwamba Mungu ananijali kwa vyovyote.” Je, unahisi hivyo nyakati nyingine?
2, 3. Ni nani anayetaka tuamini kwamba Yehova hatupendi au hatuthamini, na tunawezaje kupambana na maoni hayo?
2 Shetani anataka sana tuamini kwamba Yehova Mungu hatupendi wala hatuthamini. Ni kweli kwamba mara nyingi Shetani anawashawishi watu kupitia kiburi chao na majivuno yao. (2 Wakorintho 11:3) Lakini anafurahia pia kuwafanya wanyonge wajihisi hawafai kabisa. (Yohana 7:47-49; 8:13, 44) Shetani anafanya hivyo hasa katika hizi “siku za mwisho” zenye hatari. Watu wengi leo hulelewa katika familia ambazo hazina “shauku ya kiasili.” Wengine hukutana kila siku na watu wakali, wenye ubinafsi, na wenye vichwa vigumu. (2 Timotheo 3:1-5) Huenda watu hao wakaona kwamba hawafai au hakuna yeyote anayeweza kuwapenda kwa sababu wametendewa vibaya, kubaguliwa, au kuchukiwa kwa miaka mingi.
3 Ikiwa una hisia hizo zenye kuvunja moyo, usikate tamaa. Mara kwa mara, wengi wetu hujilaumu isivyofaa. Lakini kumbuka kwamba Neno la Mungu linakusudiwa “kunyoosha mambo” na “kupindua mambo yaliyotiwa kwa nguvu sana katika mahandaki.” (2 Timotheo 3:16; 2 Wakorintho 10:4) Biblia inasema hivi: “Tutahakikishia mioyo yetu mbele yake kwa habari ya chochote kile ambacho mioyo yetu huenda ikatulaumu katika hicho, kwa sababu Mungu ni mkubwa zaidi kuliko mioyo yetu na ajua mambo yote.” (1 Yohana 3:19, 20) Hebu tuchunguze njia nne ambazo Maandiko hutusaidia ‘kuhakikishia mioyo yetu’ kwamba Yehova anatupenda.
Yehova Anakuthamini
4, 5. Mfano wa shore ambao Yesu alitoa unaonyeshaje kwamba tuna thamani machoni pa Yehova?
4 Kwanza, Biblia inafundisha waziwazi kwamba Yehova anamthamini kila mmoja wa watumishi wake. Kwa mfano, Yesu alisema: “Je, shore wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka kwenye ardhi bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiwe na hofu: Nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi.” (Mathayo 10:29-31) Maneno hayo yalimaanisha nini kwa wale waliomsikiliza Yesu katika karne ya kwanza?
“Nyinyi ni bora zaidi kuliko shore wengi”
5 Huenda tukashangaa ni kwa nini mtu anunue shore? Katika siku za Yesu, shore alikuwa ndege wa bei rahisi sana aliyenunuliwa ili kuliwa. Ona kwamba mtu aliyelipa sarafu moja ya thamani ndogo sana, alipewa shore wawili. Lakini baadaye Yesu alisema kwamba mtu aliyelipa sarafu mbili, alipewa shore watano badala ya shore wanne. Shore mmoja aliongezwa kana kwamba hakuwa na thamani yoyote. Huenda viumbe hao hawakuwa na thamani yoyote machoni pa wanadamu, lakini Muumba aliwaonaje? Yesu alisema: “Hakuna hata mmoja wao [hata yule aliyeongezwa] hupata kusahaulika mbele ya Mungu.” (Luka 12:6, 7) Sasa huenda tumeanza kuelewa alilomaanisha Yesu. Ikiwa Yehova anamthamini sana shore mmoja, vipi mwanadamu? Kama Yesu alivyoeleza, Yehova anatujua vizuri sana. Kwani, hata nywele za kichwa chetu zimehesabiwa zote!
6. Kwa nini tuna hakika kwamba Yesu hakutia chumvi aliposema kwamba nywele za kichwa chetu zimehesabiwa?
6 Je, kweli nywele zetu zimehesabiwa? Huenda wengine wakadhani kwamba Yesu alitia chumvi. Hata hivyo, hebu fikiria tumaini la ufufuo. Ni lazima Yehova awe anatujua vizuri sana ili aweze kutuumba upya! Anatuthamini sana hivi kwamba anakumbuka kila jambo, hata chembe zetu za urithi, kumbukumbu na ujuzi wetu wa maisha yetu yote.a Kichwa cha wastani huwa na nywele 100,000 hivi, kwa hiyo kuhesabu nywele za vichwa vyetu ni jambo rahisi sana ikilinganishwa na kukumbuka mambo hayo yote.
Kwa Nini Yehova Anatuthamini?
7, 8. (a) Yehova hufurahia kuona sifa zipi anapotafuta-tafuta mioyo ya wanadamu? (b) Yehova anathamini kazi gani njema tunazofanya?
7 Pili, Biblia hutufundisha sababu zinazomfanya Yehova awathamini watumishi wake. Kwa ufupi, sifa zetu nzuri na jitihada zetu zinampendeza. Mfalme Daudi alimwambia hivi Solomoni mwanaye: “BWANA hutafuta-tafuta mioyo yote, na kuyatambua mawazo yote ya fikira.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Mungu anapotafuta-tafuta mioyo ya mabilioni ya wanadamu katika ulimwengu huu wenye jeuri na uliojaa chuki, anafurahi sana kumpata mtu mwenye moyo unaopenda amani, kweli, na uadilifu. Mungu hufanya nini anapompata mtu anayempenda kwa moyo wote, anayetaka kujifunza na kuwafundisha wengine kumhusu? Yehova anatuambia kwamba yeye anawaona wale wanaowafundisha wengine kumhusu. Hata ana “kitabu cha ukumbusho” kwa ajili ya wote ‘wanaomcha BWANA, na kulitafakari jina lake.’ (Malaki 3:16) Anathamini sana sifa hizo.
8 Ni baadhi ya kazi gani njema ambazo Yehova anathamini? Bila shaka anathamini jitihada zetu za kumwiga Mwanaye, Yesu Kristo. (1 Petro 2:21) Kazi moja muhimu ambayo Mungu anathamini ni ile ya kueneza habari njema za Ufalme wake. Twasoma hivi kwenye Waroma 10:15: “Jinsi ilivyo yenye kupendeza miguu ya wale watangazao habari njema ya mambo mema!” Huenda kwa kawaida tusiione miguu yetu duni kuwa “yenye kupendeza,” au mirembo. Lakini hapa miguu ni mfano wa jitihada za watumishi wa Yehova za kuhubiri habari njema. Jitihada hizo zote ni zenye kupendeza na zenye thamani sana machoni pake.—Mathayo 24:14; 28:19, 20.
9, 10. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anathamini uvumilivu wetu tunapokabili magumu mbalimbali? (b) Yehova hana maoni gani yasiyofaa kuwahusu watumishi wake waaminifu?
9 Yehova anathamini pia uvumilivu wetu. (Mathayo 24:13) Kumbuka kwamba Shetani anataka umpe Yehova kisogo. Kila siku unayodumu ukiwa mwaminifu kwa Yehova unasaidia kujibu lawama za Shetani. (Mithali 27:11) Nyakati nyingine si rahisi kuvumilia. Matatizo ya afya, matatizo ya kifedha, mifadhaiko, na vipingamizi vingine vinaweza kufanya maisha yawe magumu siku baada ya siku. Tunaweza kuvunjika moyo kwa sababu ya matumaini yasiyotimizwa. (Mithali 13:12) Yehova anathamini hata zaidi uvumilivu wetu tunapokabili majaribu hayo. Ndiyo sababu Mfalme Daudi alimwomba Yehova ahifadhi machozi yake katika “chupa” kisha akasema hivi kwa uhakika: “Je! hayamo katika kitabu chako?” (Zaburi 56:8) Naam, Yehova anathamini na kukumbuka machozi na mateso yote ambayo tunavumilia tunapoendelea kuwa waaminifu kwake. Machozi hayo ni yenye thamani machoni pake kama machozi ya Daudi.
Yehova anathamini uvumilivu wetu tunapokabili majaribu
10 Lakini mtu anayejihukumu moyoni anaweza kupuuza mambo yanayoonyesha kwamba anathaminiwa na Mungu. Huenda akajiambia hivi moyoni: ‘Lakini kuna watu wengine wengi ambao ni bora kuliko mimi. Haikosi Yehova anahuzunika sana anaponilinganisha nao!’ Yehova hawalinganishi watu; wala hashikilii mno maoni yake. (Wagalatia 6:4) Yeye husoma mioyo yetu kwa makini sana, naye huthamini sifa zozote nzuri ambazo tunazo—hata zile ndogo.
Yehova Huchunguza kwa Makini Jema na Baya
11. Tunaweza kujifunza nini kumhusu Yehova kutokana na jinsi alivyoshughulikia kisa cha Abiya?
11 Tatu, Yehova hutuchunguza kwa makini na kutafuta lililo jema. Kwa mfano, Yehova alipoagiza jamaa yote yenye kuasi ya Mfalme Yeroboamu iangamizwe, Aliamuru kwamba Abiya, mmoja wa wana wa mfalme, azikwe kwa heshima. Kwa nini? “Limeonekana ndani yake jambo lililo jema kwa BWANA, Mungu wa Israeli.” (1 Wafalme 14:1, 10-13) Basi Yehova alichunguza kwa makini moyo wa kijana huyo na kupata “jambo lililo jema.” Hata iwe jambo hilo jema lilikuwa dogo kadiri gani, Yehova aliona kwamba linafaa kuandikwa katika Neno lake. Hata alimthawabisha kwa sababu ya jambo hilo. Alimwonyesha rehema kwa kadiri ifaayo mtu huyo wa jamaa yenye kuasi.
12, 13. (a) Kisa cha Mfalme Yehoshafati kinaonyeshaje kwamba Yehova anaona sifa zetu nzuri hata tunapofanya dhambi? (b) Yehova hutendaje kama Baba mwenye upendo anapochunguza kazi na sifa zetu nzuri?
12 Mfano mzuri zaidi unahusiana na Mfalme Yehoshafati aliyekuwa mwema. Mfalme huyo alipotenda jambo la kipumbavu, nabii wa Yehova alimwambia hivi: “Kwa ajili ya hayo ghadhabu i juu yako itokayo kwa BWANA.” Ulikuwa ujumbe wenye kuogofya kama nini! Lakini ujumbe wa Yehova haukukomea hapo. Uliendelea kusema hivi: “Walakini yameonekana mema ndani yako.” (2 Mambo ya Nyakati 19:1-3) Kwa hiyo, Yehova hakupuuza wema wa Yehoshafati kwa sababu ya hasira Yake adilifu. Yeye hakutenda kama wanadamu wasiokamilika. Tunapokasirishwa na wengine, huenda tukapuuza wema wao. Na tunapofanya dhambi, sisi huaibika, hutamauka, na kuhisi hatia hivi kwamba tunapuuza wema wetu. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova anatusamehe tunapotubu na kujitahidi kabisa kutorudia dhambi zetu.
13 Yehova anapokuchunguza, anatupilia mbali dhambi hizo, kama vile mchimba-dhahabu anavyotupilia mbali changarawe zisizofaa. Vipi kazi na sifa zako nzuri? Aah, sifa hizo ni “dhahabu” kwake kwa hivyo anazihifadhi! Je, umeona jinsi ambavyo wazazi wenye upendo wanavyotunza sana picha au kazi za shuleni za watoto wao, nyakati nyingine kwa miaka mingi sana baada ya watoto wao kuzisahau? Yehova ni Baba asiye na kifani katika kuwapenda watoto wake. Maadamu tunaendelea kuwa waaminifu kwake, hasahau kamwe kazi na sifa zetu nzuri. Kwa kweli, kwa maoni yake, kusahau kazi hizo kungekuwa kukosa uadilifu, naye hawezi kamwe kukosa uadilifu. (Waebrania 6:10) Yeye pia hutuchunguza kwa njia nyingine.
14, 15. (a) Kwa nini Yehova hapuuzi kamwe sifa zetu nzuri kwa sababu ya kutokamilika kwetu? Toa mfano. (b) Yehova atafanya nini na sifa zetu nzuri, naye anawaonaje watu wake waaminifu?
14 Yehova hazingatii kasoro zetu bali anaona hasa uwezo wetu. Kwa mfano: Watu wanaopenda sanaa hufanya yote wawezayo ili kurekebisha michoro au sanaa zilizoharibika. Mtu fulani alipofyatua risasi na kuharibu mchoro wa msanii Leonardo da Vinci wenye thamani ya dola milioni 30 za Marekani, katika Jumba la Kitaifa la Sanaa huko London, Uingereza, hakuna mtu hata mmoja aliyedokeza kwamba mchoro huo utupwe kwa sababu ulikuwa umeharibika. Kazi ya kurekebisha mchoro huo bora sana uliodumu kwa miaka 500 hivi ilianza mara moja. Kwa nini? Kwa sababu watu wanaopenda sanaa waliuthamini sana. Wewe una thamani kuliko mchoro wa chokaa na makaa sivyo? Bila shaka, una thamani sana machoni pa Mungu—haidhuru hali mbaya ya kutokamilika uliyorithi. (Zaburi 72:12-14) Yehova Mungu, Muumba stadi wa wanadamu, atafanya yote yanayohitajika ili wote wanaokubali utunzaji wake wenye upendo wawe watu wakamilifu hatimaye.—Matendo 3:21; Waroma 8:20-22.
15 Naam, Yehova huona sifa zetu nzuri ambazo huenda tusione. Na tunapomtumikia, atakuza sifa hizo nzuri mpaka hatimaye tuwe wakamilifu. Yehova anawathamini watumishi wake waaminifu na anawaona kuwa wenye kutamanika, bila kujali jinsi ambavyo ulimwengu wa Shetani umetutendea.—Hagai 2:7.
Yehova Anatuthibitishia Upendo Wake
16. Ni uthibitisho gani bora kabisa unaoonyesha kwamba Yehova anatupenda, na twajuaje kwamba zawadi hiyo ilitolewa kwa ajili yetu?
16 Nne, Yehova anajitahidi kututhibitishia kwamba anatupenda. Hapana shaka kwamba dhabihu ya fidia ya Kristo ndiyo njia bora ya kupinga uwongo wa Shetani kwamba hatuthaminiwi wala hakuna yeyote anayeweza kutupenda. Hatupaswi kamwe kusahau kwamba maumivu ambayo Yesu alivumilia kwenye mti wa mateso kabla ya kufa, na maumivu makali zaidi ambayo Yehova alihisi alipomtazama Mwanaye mpendwa akifa ni uthibitisho wa kwamba wanatupenda. Kwa kusikitisha, watu wengi hawaamini kwamba zawadi hiyo ilitolewa kwa ajili yao. Wanajiona hawafai. Lakini, kumbuka kwamba mtume Paulo aliwanyanyasa wafuasi wa Kristo hapo awali. Hata hivyo, aliandika hivi: ‘Mwana wa Mungu alinipenda mimi na akajikabidhi mwenyewe kwa ajili yangu.’—Wagalatia 1:13; 2:20.
17. Yehova anatuvuta kwake na kwa Mwanaye kwa njia zipi?
17 Yehova anatuthibitishia upendo wake kwa kumsaidia kila mmoja wetu kufaidika na dhabihu ya Kristo. Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Ndiyo, Yehova humvuta kila mmoja wetu kwa Mwanaye na kwenye tumaini la uhai udumuo milele. Jinsi gani? Yehova humvuta kila mmoja wetu kupitia kazi ya kuhubiri, na kupitia roho yake takatifu ambayo hutusaidia kuelewa na kufuata kweli za kiroho licha ya udhaifu wetu na kutokamilika kwetu. Kwa hiyo, Yehova anaweza kutuambia kama alivyoliambia taifa la Israeli: “Nimekupenda kwa upendo wa milele, ndiyo maana nimekuvuta kwa fadhili zangu.”—Yeremia 31:3.
18, 19. (a) Yehova anatuonyesha upendo kupitia njia gani ya pekee sana, na tunajuaje kwamba anashughulikia jambo hilo yeye mwenyewe? (b) Neno la Mungu linatuhakikishiaje kwamba Yehova hutusikiliza kwa hisia-mwenzi?
18 Yamkini pendeleo la sala ndiyo njia ya pekee ya kufurahia upendo wa Yehova. Biblia inamsihi kila mmoja wetu ‘asali [kwa Mungu] bila kukoma.’ (1 Wathesalonike 5:17) Yeye husikiliza. Hata anaitwa “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Hajampa mtu mwingine yeyote, hata Mwanaye, mamlaka ya kusikiliza sala kwa niaba yake. Hebu fikiria: Muumba wa ulimwengu wote anatuhimiza tumfikie kwa sala, na kusema naye kwa uhuru. Naye husikilizaje? Je, anasikiliza tu bila hisia wala kujali? La hasha.
19 Yehova ana hisia-mwenzi. Hisia-mwenzi ni nini? Mkristo mmoja mwaminifu ambaye ni mzee kwa umri alisema: “Hisia-mwenzi ni kuhisi uchungu wako moyoni mwangu.” Je, kweli Yehova anaumizwa na uchungu wetu? Twasoma hivi kuhusu mateso ya watu wake wa taifa la Israeli: “Katika mateso yao yote yeye aliteswa.” (Isaya 63:9) Yehova hakuona tu taabu zao; bali alihisi uchungu kwa sababu ya taabu zao. Maneno ambayo Yehova aliwaambia watumishi wake yanaonyesha jinsi anavyohisi: “Anayewagusa nyinyi anagusa mboni ya jicho langu.”b (Zekaria 2:8, BHN) Mtu huhisi maumivu makali sana anapoguswa mboni ya jicho. Ndiyo, Yehova anahisi uchungu kwa ajili yetu. Tunapoteseka, anateseka pia.
20. Tunapaswa kuepuka maoni gani yasiyofaa kupatana na shauri la Waroma 12:3?
20 Mkristo mwenye usawaziko hapaswi kamwe kutumia uthibitisho huo wa upendo na staha ya Mungu kuwa udhuru wa kujivuna au kujiona kuwa bora. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia fadhili isiyostahiliwa niliyopewa naambia kila mtu huko miongoni mwenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali afikiri ili awe na akili timamu, kila mmoja kama vile Mungu amemgawia kipimo cha imani.” (Waroma 12:3) Tafsiri nyingine inasema hivi: “Ninamwambia kila mmoja wenu asijikadirie zaidi kuliko alivyo kikweli, lakini ajikadirie kwa kiasi.” (A Translation in the Language of the People, ya Charles B. Williams) Kwa hiyo, tunapofurahia kabisa upendo mchangamfu wa Baba yetu wa mbinguni, na tuwe wenye kiasi na kukumbuka kwamba hatustahili upendo wa Mungu kwa sababu ya jitihada zetu.—Luka 17:10.
21. Tunapaswa kuendelea kukataa kabisa uwongo gani wa Shetani, na tunahitaji kuendelea kujihakikishia mioyoni mwetu ukweli gani ulio katika Biblia?
21 Kila mmoja wetu na afanye yote awezayo kukataa katakata uwongo wote wa Shetani, hata uwongo kwamba hatufai au hatuwezi kupendwa. Ikiwa hali zilizokupata maishani zimekufunza ujione huwezi kamwe kunufaishwa na upendo mwingi wa Mungu, au kuona kazi zako nzuri kuwa duni mno hivi kwamba Yehova hawezi kuziona, au dhambi zako kuwa nyingi mno zisiweze kufunikwa na kifo cha Mwanaye mpendwa, umefunzwa uwongo mtupu. Kataa katakata uwongo huo kwa moyo wako wote! Na tuendelee kujihakikishia mioyoni mwetu ukweli wa maneno ya Paulo: “Nasadiki kwamba wala kifo wala uhai wala malaika wala serikali wala mambo yaliyo hapa sasa wala mambo yatakayokuja wala nguvu wala kimo wala kina wala kiumbe kingine chochote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 8:38, 39.
a Mara nyingi Biblia huhusianisha tumaini la ufufuo na kumbukumbu la Yehova. Yobu aliyekuwa mwaminifu alimwambia Yehova hivi: “Laiti . . . ungeniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka!” (Ayubu 14:13) Yesu alisema kwamba “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho” watafufuliwa. Hilo ni kweli kwa sababu Yehova anawakumbuka kabisa wafu ambao anakusudia kuwafufua.—Yohana 5:28, 29.
b Tafsiri fulani zinadokeza kwamba mtu anayegusa watu wa Mungu hagusi jicho la Mungu, bali anagusa jicho lake mwenyewe au jicho la Israeli. Kosa hilo lilitokana na waandishi fulani ambao walidhani kwamba andiko hilo halimheshimu Mungu na hivyo wakalibadili. Jitihada zao zilizopotoka zilificha wingi wa hisia-mwenzi za Yehova.
-
-
“Huruma Nyororo ya Mungu Wetu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 25
“Huruma Nyororo ya Mungu Wetu”
1, 2. (a) Mama hutendaje mtoto wake mchanga anapolia? (b) Ni hisia gani ambayo ni yenye nguvu zaidi kuliko huruma ya mama?
MTOTO mchanga aanza kulia usiku wa manane. Mama yake anaamka mara moja. Mama halali kwa utulivu tangu alipojifungua mtoto huyo. Amejua kutofautisha vilio mbalimbali vya mtoto wake mchanga. Kwa hiyo, kwa kawaida anaweza kujua iwapo mtoto wake anahitaji kunyonya, kubebwa, au kushughulikiwa kwa njia nyingine. Mama humshughulikia mtoto wake haidhuru sababu inayomfanya alie. Hawezi kupuuza mahitaji ya mtoto wake kwa sababu anampenda sana.
2 Huruma ya mama kwa mtoto wake ni mojawapo ya hisia zenye nguvu sana ambazo wanadamu huonyesha. Hata hivyo, kuna hisia ambayo ni yenye nguvu kupita hisia zote—huruma nyororo ya Mungu wetu Yehova. Tunaweza kumkaribia Yehova zaidi tukichunguza sifa hii yenye kuvutia. Basi na tuzungumzie maana ya huruma na jinsi ambavyo Mungu wetu huonyesha sifa hiyo.
Huruma Ni Nini?
3. Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa “onyesha rehema” au “hurumia” kinamaanisha nini?
3 Katika Biblia, huruma na rehema zinahusiana sana. Maneno kadhaa ya Kiebrania na Kigiriki yanadokeza sifa ya huruma yenye upendo. Kwa mfano, fikiria kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ, ambacho mara nyingi hutafsiriwa “onyesha rehema” au “hurumia.” Kichapo kimoja cha marejeo kinaeleza kwamba kitenzi ra·chamʹ “kinaonyesha huruma nyingi na yenye upendo, kama ile tunayohisi tunapowaona wapendwa wetu au wale wanaohitaji msaada wetu wakiteseka au kuumia.” Neno hilo la Kiebrania, ambalo Yehova anatumia kujihusu, linahusiana na neno linalomaanisha “tumbo la uzazi” nalo linaweza kufasiriwa kuwa “huruma ya mama.”a—Kutoka 33:19; Yeremia 33:26.
“Je, mwanamke aweza kumsahau . . . mwana wa tumbo lake? ”
4, 5. Biblia inatumiaje hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha kuhusu huruma ya Yehova?
4 Biblia inatumia hisia ambazo mama huwa nazo kwa mtoto wake mchanga kutufundisha maana ya huruma ya Yehova. Twasoma hivi kwenye Isaya 49:15: “Je! mwanamke aweza kumsahau mtoto wake anyonyaye, hata asimhurumie [ra·chamʹ] mwana wa tumbo lake? naam, hawa waweza kusahau, lakini mimi sitakusahau wewe.” Maelezo hayo yenye kugusa moyo yanakazia jinsi Yehova alivyo na huruma nyingi kwa watu wake. Jinsi gani?
5 Ni vigumu kuwazia kwamba mama anaweza kusahau kumnyonyesha na kumtunza mtoto wake mchanga. Kwani, mtoto mchanga ni hoi; anahitaji kupendwa na kutunzwa na mama yake usiku na mchana. Ingawa hivyo, inasikitisha kupata habari kuhusu akina mama wanaowatupa watoto wao, hasa katika ‘nyakati hizi za hatari’ kwa sababu watu hawana “shauku ya kiasili.” (2 Timotheo 3:1, 3) “Lakini mimi sitakusahau wewe,” atangaza Yehova. Yehova hakosi kamwe kuwaonyesha watumishi wake huruma nyororo. Huruma hiyo ni yenye nguvu zaidi ya hisia yenye nguvu tunayoweza kuwazia, yaani, huruma ambayo kwa kawaida mama humwonyesha mtoto wake mchanga. Haishangazi kwamba mtoa-maoni mmoja alisema hivi kuhusu Isaya 49:15: “Hili ni mojawapo, au ndilo neno linalofafanua upendo wa Mungu waziwazi zaidi katika Agano la Kale.”
6. Wanadamu wengi wasiokamilika wamekuwa na maoni gani kuhusu huruma nyororo, lakini Yehova anatuhakikishia nini?
6 Je, kuwa na huruma nyororo ni udhaifu? Wanadamu wengi wasiokamilika wamekuwa na maoni hayo. Kwa mfano, mwanafalsafa Mroma Seneca, msomi maarufu wa Roma ambaye aliishi wakati wa Yesu, alifundisha kwamba “huruma ni udhaifu wa akili.” Seneca aliunga mkono Ustoiki, falsafa inayokazia kuwa na utulivu bila hisia zozote. Mtu mwenye hekima anaweza kuwasaidia wale wanaotaabika, akasema Seneca, lakini hapaswi kuwahurumia kwa sababu atakosa utulivu akifanya hivyo. Maoni hayo ya ubinafsi kuhusu maisha yaliwazuia watu wasionyeshe huruma kutoka moyoni. Lakini sivyo alivyo Yehova! Yehova anatuhakikishia katika Neno lake kwamba yeye “ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema [kihalisi, “mwenye huruma”].” (Yakobo 5:11) Kama tutakavyoona, kuonyesha huruma si udhaifu bali ni sifa muhimu sana yenye nguvu. Hebu tuone jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hiyo kama mzazi mwenye upendo.
Yehova Alipolihurumia Taifa
7, 8. Waisraeli walitesekaje katika Misri ya kale, na Yehova alichukua hatua gani kwa sababu ya mateso yao?
7 Huruma ya Yehova yaonekana wazi kutokana na jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Kufikia mwishoni mwa karne ya 16 K.W.K., mamilioni ya Waisraeli waliteswa sana walipokuwa watumwa katika Misri ya kale. Wamisri ‘walifanya maisha yao kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na ya matofali.’ (Kutoka 1:11, 14) Waisraeli walimlilia Yehova awasaidie walipokuwa wakiteseka. Mungu mwenye huruma nyororo alichukua hatua gani?
8 Yehova aliwahurumia. Akasema: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu walioko Misri, nami nimekisikia kilio chao kwa sababu ya wasimamizi wao; maana nayajua maumivu yao.” (Kutoka 3:7) Yehova hakuweza kamwe kutazama watu wake wakiteseka au kusikia vilio vyao na asiwahurumie. Kama tulivyoona katika Sura ya 24 ya kitabu hiki, Yehova ni Mungu mwenye hisia-mwenzi. Na hisia-mwenzi, yaani, sifa ya kuguswa moyo na uchungu wa wengine inahusiana sana na huruma. Lakini Yehova hakuwahurumia tu watu wake; alichochewa kuwasaidia. Andiko la Isaya 63:9 lasema: “Kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe.” Yehova aliwaokoa Waisraeli kutoka Misri kwa “mkono hodari.” (Kumbukumbu la Torati 4:34) Baadaye, aliwalisha kimuujiza na kuwapa nchi yenye rutuba.
9, 10. (a) Kwa nini Yehova aliwakomboa Waisraeli tena na tena baada ya kuingia katika Nchi Iliyoahidiwa? (b) Katika siku za Yeftha, Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka katika mateso gani, ni nini kilichomchochea kufanya hivyo?
9 Huruma ya Yehova haikuishia hapo. Waisraeli walimwasi tena na tena baada ya kuingia katika Nchi Iliyoahidiwa na hivyo wakateseka. Lakini walirudiwa na fahamu na kumlilia Yehova. Aliwakomboa tena na tena. Kwa nini? “Kwa sababu aliwahurumia watu wake.”—2 Mambo ya Nyakati 36:15; Waamuzi 2:11-16.
10 Fikiria mambo yaliyotukia siku za Yeftha. Waisraeli walipoanza kuitumikia miungu ya uwongo, Yehova aliwaacha wateswe na Waamoni kwa miaka 18. Mwishowe, walitubu. Biblia inatuambia hivi: “Nao wakaiondoa hiyo miungu ya kigeni iliyokuwa kati yao, nao wakamtumikia BWANA; na roho yake ilihuzunika kwa sababu ya msiba wa Israeli.”b (Waamuzi 10:6-16) Mara tu baada ya watu wake kutubu kikweli, Yehova hakuweza kuvumilia kuwaona wakiteseka. Kwa hiyo, Mungu mwenye huruma nyororo alimpa Yeftha nguvu ili awakomboe Waisraeli kutoka mikononi mwa adui zao.—Waamuzi 11:30-33.
11. Twajifunza nini kuhusu huruma tunapozingatia jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli?
11 Twajifunza nini kuhusu huruma nyororo ya Yehova tunapozingatia jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli? Jambo moja ambalo tunajifunza ni kwamba hawaonei huruma watu wanaoteseka na kuwaacha tu. Kumbuka yule mama ambaye anachochewa na huruma kumsaidia mtoto wake mchanga anayelia. Vivyo hivyo, Yehova hapuuzi vilio vya watu wake. Huruma yake nyororo humchochea kukomesha mateso yao. Zaidi ya hayo, twajifunza pia kwamba huruma si udhaifu kamwe, kwa sababu sifa hii ya kutoka moyoni ilimchochea achukue hatua madhubuti ya kuwatetea watu wake. Lakini je, Yehova anawahurumia watumishi wake wakiwa kikundi tu?
Yehova Amhurumia Mtu Mmoja-Mmoja
12. Sheria ilionyeshaje huruma ya Yehova kwa mtu mmoja-mmoja?
12 Sheria ambayo Mungu alilipa taifa la Israeli ilionyesha kwamba alimhurumia mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, fikiria jinsi alivyowajali maskini. Yehova alijua kwamba Mwisraeli angeweza kuwa maskini kwa sababu ya hali zisizotazamiwa. Maskini walipaswa kutendewaje? Yehova aliwapa Waisraeli amri hii kali: “Usifanye moyo wako kuwa mgumu, wala usimfumbie mkono wako nduguyo maskini. Mpe kwa kweli, wala moyo wako usisikitike utakapompa; kwa kuwa atakubarikia BWANA, Mungu wako, kwa neno hili katika kazi yako yote.” (Kumbukumbu la Torati 15:7, 10) Yehova pia aliwaagiza Waisraeli wasivune kabisa pembeni mwa mashamba yao au kukusanya masazo. Masazo hayo yaliachwa kwa ajili ya maskini. (Mambo ya Walawi 23:22; Ruthu 2:2-7) Taifa la Israeli lilipotii sheria hiyo, maskini hawakuhitaji kuombaomba chakula. Hilo laonyesha huruma nyororo ya Yehova, sivyo?
13, 14. (a) Maneno ya Daudi yanatuhakikishiaje kwamba Yehova anamjali sana kila mmoja wetu? (b) Toa mfano kuonyesha kwamba Yehova yu karibu na wale “waliovunjika moyo” au “waliopondeka roho.”
13 Leo pia, Mungu wetu mwenye upendo anamjali sana kila mmoja wetu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba anajua kabisa mateso yoyote ambayo huenda yakatupata. Mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi: “Macho ya BWANA huwaelekea wenye haki, na masikio yake hukielekea kilio chao. BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:15, 18) Mtoa-maoni mmoja wa Biblia aeleza hivi kuhusu wale wanaotajwa na andiko hilo: “Ni watu waliovunjika moyo na wenye majuto, yaani, watu walionyenyekezwa na dhambi, wasiojiheshimu; wanaojiona kuwa duni, na wasiojiamini.” Huenda wakahisi kwamba Yehova yu mbali na wao, na kwamba wao ni duni hivi kwamba hawezi kuwajali. Lakini sivyo ilivyo. Maneno ya Daudi yanatuhakikishia kwamba Yehova hawaachi wale “wanaojiona kuwa duni.” Mungu wetu mwenye huruma anajua kwamba tunahitaji msaada wake sana tunapohisi hivyo, naye yu tayari kutusaidia.
14 Fikiria kisa hiki halisi. Mama mmoja nchini Marekani alimpeleka mwanaye mwenye umri wa miaka miwili hospitalini kwa sababu alikuwa na ugonjwa mbaya wa kifaduro. Baada ya kumchunguza, madaktari walimwambia mama kwamba mwanaye angelazwa hospitalini usiku huo. Mama alikesha wapi usiku huo? Alikesha kwenye kiti humohumo hospitalini, karibu na kitanda cha mwanaye! Mwanaye alikuwa mgonjwa kwa hiyo mama alitaka sana kuwa karibu naye. Bila shaka, tunaweza kumtarajia Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo atufanyie mengi zaidi! Kwani, tumeumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Maneno yenye kugusa moyo ya Zaburi 34:18 yanatueleza kwamba ‘tunapovunjika moyo’ au ‘kupondeka roho,’ Yehova, kama baba mwenye upendo, “yu karibu”—sikuzote akiwa mwenye huruma na tayari kutusaidia.
15. Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu?
15 Basi, Yehova anamsaidiaje kila mmoja wetu? Haondoi kisababishi cha mateso yetu sikuzote. Lakini Yehova amewapa maandalizi tele wale wanaomwomba msaada. Neno lake, Biblia, lina mashauri yanayofaa ambayo yanaweza kuboresha hali. Katika kutaniko, Yehova ameweka waangalizi wanaostahili kiroho, ambao wanajitahidi kuwa na huruma kama yeye wanapowasaidia waabudu wenzao. (Yakobo 5:14, 15) Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye huwapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Zaburi 65:2, NW; Luka 11:13) Roho hiyo inaweza kututia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili tuweze kuvumilia hadi Ufalme wa Mungu utakapokomesha matatizo yote yanayofadhaisha. (2 Wakorintho 4:7) Tunamshukuru kwelikweli kwa sababu ya maandalizi hayo yote, sivyo? Tusisahau kwamba maandalizi hayo ni uthibitisho wa huruma nyororo ya Yehova.
16. Yehova alionyesha huruma yake kwa njia gani bora, na inamfaidije kila mmoja wetu?
16 Hapana shaka kwamba Yehova alionyesha huruma yake kwa njia bora zaidi alipomtoa Yule anayempenda sana awe fidia kwa ajili yetu. Yehova alionyesha upendo kwa kutoa dhabihu hiyo ambayo ilitufungulia njia ya kupata wokovu. Kumbuka kwamba fidia hiyo inamfaidi kila mmoja wetu. Ndiyo sababu Zekaria, baba ya Yohana Mbatizaji, alitabiri kwamba zawadi hiyo ilithibitisha “huruma nyororo ya Mungu wetu.”—Luka 1:78.
Huruma ya Yehova Inapofikia Kikomo
17-19. (a) Biblia inaonyeshaje kwamba huruma ya Yehova ina kikomo? (b) Kwa nini huruma ya Yehova kwa watu wake ilifikia kikomo?
17 Je, tufikiri kwamba huruma nyororo ya Yehova haina kikomo? La hasha, Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Yehova hawahurumii watu ambao wanakataa njia zake adilifu. (Waebrania 10:28) Ili kuelewa sababu inayomfanya atende hivyo, kumbuka taifa la Israeli.
18 Ijapokuwa Yehova aliwakomboa tena na tena kutoka kwa maadui wao, mwishowe huruma yake ilifikia kikomo. Watu hao wakaidi waliabudu sanamu, hata walileta sanamu zao zenye kuchukiza ndani ya hekalu la Yehova! (Ezekieli 5:11; 8:17, 18) Zaidi ya hayo, twaambiwa hivi: “Waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.” (2 Mambo ya Nyakati 36:16) Hatimaye Waisraeli walizidi hivi kwamba hakukuwa na msingi wowote ufaao wa kuwahurumia, nao walichochea hasira adilifu ya Yehova. Matokeo yakawa nini?
19 Yehova hakuweza tena kuwahurumia watu wake. Alitangaza hivi: “Sitawahurumia, sitawaachia wala sitawarehemu, bali nitawaangamiza.” (Yeremia 13:14, BHN) Basi, Yerusalemu na hekalu lake liliharibiwa, na Waisraeli wakachukuliwa mateka hadi Babiloni. Matokeo yanakuwa mabaya kama nini wanadamu wenye dhambi wanapoasi sana hivi kwamba huruma ya Mungu inafikia kikomo!—Maombolezo 2:21.
20, 21. (a) Ni nini kitakachotukia huruma ya Mungu itakapofikia kikomo katika siku zetu? (b) Tutazungumzia zawadi gani ya huruma ya Yehova katika sura inayofuata?
20 Vipi leo? Yehova hajabadilika. Kwa sababu ya huruma yake, amewaamuru Mashahidi wake wahubiri ‘habari njema ya ufalme’ katika dunia yote inayokaliwa. (Mathayo 24:14) Watu wenye mioyo minyoofu wanapoitikia, Yehova huwasaidia kuelewa ujumbe wa Ufalme. (Matendo 16:14) Lakini kazi hii haitaendelea milele. Bila shaka ni kinyume cha huruma ya Yehova kuruhusu ulimwengu huu mwovu pamoja na mateso na taabu zake ziendelee milele. Yehova atahukumu mfumo huu wa mambo huruma yake itakapofikia kikomo. Hata wakati huo, atakuwa akionyesha huruma—huruma kwa ajili ya ‘jina lake takatifu’ na kwa ajili ya watumishi wake waaminifu. (Ezekieli 36:20-23) Yehova atakomesha kabisa uovu na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. Yehova atangaza hivi kuhusu waovu: “Jicho langu halitaachilia, wala sitaona huruma; lakini nitaleta njia yao juu ya vichwa vyao.”—Ezekieli 9:10.
21 Kabla ya wakati huo, Yehova anawahurumia watu, hata wale ambao wanakabili uharibifu. Wanadamu wenye dhambi ambao wanatubu kikweli wanaweza kufaidika na mojawapo ya zawadi bora zaidi za huruma ya Yehova, yaani, msamaha. Katika sura inayofuata, tutazungumzia baadhi ya masimulizi ya Biblia yanayoonyesha jinsi Yehova anavyosamehe kabisa.
a Hata hivyo, kwenye Zaburi 103:13, kitenzi cha Kiebrania ra·chamʹ kinamaanisha rehema, au huruma, ambayo baba huwaonyesha watoto wake.
b Usemi unaotafsiriwa “roho yake ilihuzunika” wamaanisha kihalisi ‘subira yake ilifikia kikomo.’ Biblia Habari Njema yasema: “Hakuweza kuvumilia zaidi kuona taabu za Waisraeli.” Kichapo Tanakh—A New Translation of the Holy Scriptures chasema hivi: “Hakuweza kustahimili kuona Israeli ikitaabika.”
-
-
Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 26
Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”
1-3. (a) Mtunga-zaburi Daudi alilemewa na nini, na alipataje faraja katika fadhaa zake? (b) Huenda tukalemewa na nini tunapofanya dhambi, lakini Yehova anatuhakikishia nini?
“DHAMBI zangu zimenifunikiza kichwa, kama mzigo mzito zimenilemea mno. Nimedhoofika na kuchubuka sana,” akaandika mtunga-zaburi Daudi. (Zaburi 38:4, 8) Daudi alijua jinsi dhamiri yenye hatia inavyolemea sana. Lakini alipata faraja katika fadhaa zake. Alifahamu kwamba Yehova anachukia dhambi, lakini hamchukii mtenda-dhambi ikiwa anatubu kikweli na kuacha mwenendo wake wa dhambi. Daudi alisema hivi akiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova yu tayari kuwasamehe wale wanaotubu: “Wewe, Bwana, . . . umekuwa tayari kusamehe.”—Zaburi 86:5.
2 Tunapofanya dhambi, huenda pia tukalemewa sana na dhamiri inayotuumiza. Kuhisi majuto ni jambo linalonufaisha. Kunaweza kutusukuma tuchukue hatua zinazofaa kusahihisha makosa yetu. Hata hivyo, kuna hatari ya kulemewa sana na hatia. Huenda tukajihukumu daima moyoni kwamba Yehova hatatusamehe hata tukitubu jinsi gani. Endapo ‘tutamezwa’ na hatia, huenda Shetani akajaribu kutuvunja moyo na kutufanya tuhisi kwamba hatuna thamani machoni pa Yehova, na hatufai kumwabudu.—2 Wakorintho 2:5-11.
3 Je, hivyo ndivyo Yehova anavyotuona? La hasha! Msamaha ni sifa ya upendo wa Yehova usio na kifani. Anatuhakikishia katika Neno lake kwamba yuko tayari kutusamehe tukitubu kikweli kutoka moyoni. (Mithali 28:13) Ili tusihisi kwamba Yehova hawezi kamwe kutusamehe, hebu tuone kinachomfanya atusamehe na jinsi anavyosamehe.
Kwa Nini Yehova Yuko “Tayari Kusamehe”?
4. Yehova anakumbuka nini kuhusu hali yetu, na hilo linamfanya ashughulike nasi kwa njia gani?
4 Yehova anajua udhaifu wetu. “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi,” yasema Zaburi 103:14. Hasahau kwamba sisi ni viumbe wa udongo, wenye kasoro, au udhaifu kwa sababu ya kutokamilika. Usemi kwamba anajua “umbo letu” unatukumbusha kuwa Biblia inamlinganisha Yehova na mfinyanzi na inatulinganisha na vyombo vya udongo anavyofinyanga.a (Yeremia 18:2-6) Mfinyanzi huyo Mkuu anashughulika nasi kupatana na hali yetu dhaifu yenye dhambi ikitegemea jinsi tunavyofuata au kutofuata mwongozo wake.
5. Kitabu cha Waroma kinaonyeshaje kwamba dhambi ina nguvu nyingi sana?
5 Yehova anaelewa jinsi dhambi ilivyo na nguvu nyingi. Neno lake hufafanua dhambi kuwa nguvu inayosababisha kifo kwa mwanadamu. Dhambi ina nguvu kadiri gani? Katika kitabu cha Waroma, mtume Paulo aeleza hivi: Tuko “chini ya dhambi,” kama vile wanajeshi walivyo chini ya amiri wao (Waroma 3:9); dhambi ‘imewatawala’ wanadamu wote kama mfalme (Waroma 5:21); ‘inakaa’ ndani yetu (Waroma 7:17, 20); “sheria” yake hufanya kazi ndani yetu daima, ikijaribu kuongoza maisha yetu. (Waroma 7:23, 25) Bila shaka dhambi ina nguvu nyingi sana juu ya mwili wetu usiokamilika.—Waroma 7:21, 24.
6, 7. (a) Yehova anawaonaje wale wanaotafuta rehema yake na kutubu kikweli? (b) Kwa nini hatupaswi kutumia vibaya rehema ya Mungu?
6 Kwa hiyo, Yehova anajua kwamba hatuwezi kumtii kikamili, hata tuwe tunatamani sana kufanya hivyo. Anatuhakikishia kwa upendo kwamba atatusamehe tukitafuta rehema yake na kutubu kikweli. Zaburi 51:17 yasema: “Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.” Yehova hatakataa kamwe, au kuupuuza moyo “uliovunjika na kupondeka” kwa sababu ya kulemewa na hatia.
7 Lakini je, hilo lamaanisha kwamba tunaweza kutumia vibaya rehema ya Mungu na kufanya dhambi huku tukitoa udhuru wa kwamba tumerithi dhambi? La hasha! Yehova haongozwi na hisia tu. Rehema yake ina mipaka. Hawezi kamwe kuwasamehe wale wanaofanya dhambi kimakusudi na kwa moyo mgumu, bila kutubu. (Waebrania 10:26) Kwa upande mwingine, yuko tayari kumsamehe mtu anayetubu kikweli. Hebu tuchunguze maneno yanayotumiwa katika Biblia kufafanua wazi sifa hiyo yenye kuvutia ya upendo wa Yehova.
Je, Yehova Husamehe Kabisa?
8. Yehova hufanya nini anapotusamehe dhambi zetu, na hilo latufanya tuwe na tumaini gani?
8 Daudi mwenye kutubu alisema hivi: “Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu. . . . Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu.” (Zaburi 32:5, italiki ni zetu.) Neno “ukanisamehe” ni tafsiri ya neno la Kiebrania ambalo hasa linamaanisha “inua” au “beba.” Linatumiwa hapa kumaanisha kuondolea mbali “hatia, dhambi, uasi-sheria.” Kwa hiyo, ni kana kwamba Yehova aliziinua dhambi za Daudi na kuziondolea mbali. Hapana shaka kwamba hilo lilipunguza hisia za hatia ambazo Daudi alikuwa nazo. (Zaburi 32:3) Sisi pia tunaweza kumtumaini kabisa Mungu ambaye anaondolea mbali dhambi za wale wanaotafuta msamaha wake kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya fidia ya Yesu.—Mathayo 20:28.
9. Yehova huweka dhambi zetu mbali nasi kadiri gani?
9 Daudi alitumia usemi mwingine ulio wazi zaidi kufafanua msamaha wa Yehova: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi.” (Zaburi 103:12, italiki ni zetu.) Mashariki ni mbali kadiri gani kutoka magharibi? Katika maana fulani, sikuzote mashariki huwa mbali kabisa na magharibi; pande hizo mbili haziwezi kamwe kukutana. Msomi mmoja anasema kwamba usemi huo unamaanisha “mbali iwezekanavyo; mbali kabisa.” Maneno ya Daudi yanatuambia kwamba Yehova anapotusamehe, anaweka dhambi zetu mbali kabisa nasi.
“Dhambi zenu . . . zitakuwa nyeupe kama theluji”
10. Yehova anapotusamehe dhambi zetu, kwa nini hatupaswi kuhisi kwamba tuna hatia ya dhambi hizo maisha yetu yote?
10 Je, umewahi kujaribu kuondoa doa katika nguo nyeupe? Huenda hukufaulu kuondoa doa hilo licha ya jitihada zako zote. Ona jinsi Yehova anavyoeleza msamaha wake: “Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.” (Isaya 1:18, italiki ni zetu.) Usemi “nyekundu sana” waonyesha kwamba rangi hiyo ni nyangavu.b Rangi “nyekundu” ilikuwa mojawapo ya rangi zilizotiwa kwenye nguo. (Nahumu 2:3) Hatuwezi kamwe kuondoa doa la dhambi kwa jitihada zetu. Lakini Yehova anaweza kuondoa dhambi ambazo ni nyekundu sana na kuzifanya nyeupe kama theluji au sufu isiyotiwa rangi. Yehova anapotusamehe dhambi zetu, hatupaswi kuhisi kwamba tuna hatia ya dhambi hizo maisha yetu yote.
11. Yehova anatupa dhambi zetu nyuma yake katika maana gani?
11 Hezekia alimwambia Yehova hivi katika wimbo wa shukrani wenye kugusa moyo ambao alitunga baada ya kuponywa ugonjwa wa kufisha: “Umezitupa dhambi zangu zote nyuma yako.” (Isaya 38:17, italiki ni zetu.) Ni kana kwamba Yehova anachukua dhambi za mtenda-dhambi mwenye kutubu na kuzitupa nyuma Yake ambako Hawezi tena kuziona wala kuzikazia fikira. Kichapo kimoja kinasema kwamba andiko hilo laweza kuelezwa hivi: ‘Umefanya iwe ni kana kwamba sikufanya dhambi.’ Je, hilo si jambo lenye kutia moyo?
12. Nabii Mika anaonyeshaje kwamba Yehova anapotusamehe Anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu?
12 Katika ahadi ya urudisho, nabii Mika alieleza usadikisho wake kwamba Yehova angewasamehe watu wake wenye kutubu: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye . . . kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? . . . Nawe utazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.” (Mika 7:18, 19, italiki ni zetu.) Hebu fikiria maana ya maneno hayo kwa watu walioishi nyakati za Biblia. Hakukuwa na uwezekano wowote wa kupata kitu kilichotupwa “katika vilindi vya bahari.” Kwa hiyo maneno ya Mika yanamaanisha kwamba Yehova anapotusamehe, anafutilia mbali dhambi zetu daima dawamu.
13. Yesu aliposema “Utusamehe madeni yetu,” alimaanisha nini?
13 Yesu alitumia mfano wa wakopeshaji na wadeni ili kuonyesha jinsi Yehova anavyosamehe. Yesu alituhimiza tusali hivi: “Utusamehe madeni yetu.” (Mathayo 6:12) Kwa hiyo, Yesu alilinganisha dhambi na madeni. (Luka 11:4) Tunapofanya dhambi, tunakuwa “wadeni” wa Yehova. Kichapo kimoja cha marejeo kinasema kwamba kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “samehe,” kinamaanisha ‘kuachilia au kufuta deni na kutodai malipo.’ Yehova anapotusamehe ni kana kwamba anafuta deni ambalo tungedaiwa tulipe. Kwa hiyo, jambo hilo linaweza kuwafariji watenda-dhambi wenye kutubu. Yehova hatadai kamwe malipo ya deni ambalo amelifuta!—Zaburi 32:1, 2.
14. Usemi “mpate kufutiwa dhambi zenu” unaleta wazo gani?
14 Andiko la Matendo 3:19 laeleza zaidi jinsi ambavyo Yehova anasamehe: “Kwa hiyo, tubuni na mgeuke kabisa ili mpate kufutiwa dhambi zenu.” Neno “kufutiwa” limetafsiriwa kutokana na kitenzi cha Kigiriki kinachoweza kumaanisha “kupangusa, . . . kufuta au kuharibu.” Wasomi fulani wanasema kwamba maneno hayo yanaleta wazo la kufuta maandishi. Hilo liliwezekanaje? Wino uliotumiwa nyakati za kale ulitengenezwa kwa mchanganyiko wa kaboni, gundi, na maji. Mara tu baada ya kuandika kwa wino huo, mtu aliweza kuchukua sifongo yenye maji na kufuta kabisa maandishi hayo. Jambo hilo latufunza somo zuri sana kuhusu rehema ya Yehova. Anapotusamehe dhambi zetu, ni kana kwamba anachukua sifongo na kuzifuta kabisa.
Yehova anataka tujue kwamba yuko “tayari kusamehe”
15. Yehova anataka tujue nini kumhusu?
15 Tunapotafakari semi hizo mbalimbali za mfano, je, si wazi kwamba Yehova anataka tujue kwamba yuko tayari kutusamehe dhambi zetu maadamu tunatubu kikweli? Hakuna haja ya kuogopa kwamba huenda akatuhukumu kwa sababu ya dhambi hizo wakati ujao. Hilo lakaziwa na jambo jingine ambalo Biblia inasema kuhusu rehema ya Yehova isiyo na kifani: Anaposamehe, anasahau.
“Dhambi Yao Sitaikumbuka Tena”
16, 17. Biblia inamaanisha nini inaposema kwamba Yehova anasahau dhambi zetu, na kwa nini unajibu hivyo?
16 Yehova aliahidi hivi kuhusu wale walio katika agano jipya: “Nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yeremia 31:34) Je, hilo lamaanisha kwamba Yehova anaposamehe hawezi kukumbuka tena dhambi hizo? Bila shaka la. Biblia inatueleza kuhusu dhambi za watu wengi ambao walisamehewa na Yehova, kutia ndani Daudi. (2 Samweli 11:1-17; 12:13) Kwa wazi, Yehova bado anakumbuka makosa waliyofanya. Habari ya dhambi zao, toba yao, na jinsi walivyosamehewa na Mungu, imehifadhiwa kwa faida yetu. (Waroma 15:4) Hivyo basi, Biblia inamaanisha nini inaposema kwamba Yehova ‘hakumbuki’ dhambi za wale ambao anawasamehe?
17 Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa ‘nitakumbuka’ hakimaanishi kukumbuka tu mambo yaliyopita. Kichapo Theological Wordbook of the Old Testament chasema kwamba neno hilo ‘ladokeza pia kuchukua hatua inayofaa.’ Kwa hivyo, ‘kukumbuka’ dhambi kwatia ndani kuwaadhibu watenda-dhambi. (Hosea 9:9) Lakini Mungu anaposema kwamba “dhambi yao sitaikumbuka tena,” anatuhakikishia kwamba akisha samehe watenda-dhambi wenye kutubu, hatawaadhibu wakati ujao kwa sababu ya dhambi hizo. (Ezekieli 18:21, 22) Kwa hiyo, Yehova anasahau katika maana ya kwamba hataji-taji dhambi zetu ili atushtaki au kutuadhibu tena na tena. Inatufariji sana kujua kwamba Mungu wetu anasamehe na kusahau, sivyo?
Vipi Matokeo ya Dhambi?
18. Kwa nini mtenda-dhambi aliyetubu hupatwa na matokeo ya dhambi yake ajaposamehewa?
18 Je, yamaanisha kwamba mtenda-dhambi aliyetubu hatapatwa na matokeo ya dhambi yake kwa sababu amesamehewa? Sivyo hata kidogo. Hatuwezi kufanya dhambi na kufikiri kwamba tutaepuka matokeo yake. Paulo aliandika hivi: “Lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia.” (Wagalatia 6:7) Huenda tukapata madhara fulani kwa sababu ya dhambi zetu. Hilo halimaanishi kwamba Yehova anatuletea misiba baada ya kutusamehe. Anapopatwa na taabu, Mkristo hapaswi kufikiri kwamba labda Yehova anamwadhibu kwa sababu ya dhambi alizofanya zamani. (Yakobo 1:13) Kwa upande mwingine, Yehova hatukingi tusipatwe na matokeo ya dhambi zetu. Mambo yafuatayo yaweza kuwa matokeo yenye kuhuzunisha na yasiyoepukika ya dhambi—talaka, mimba haramu, ugonjwa unaoambukizwa kingono, kutotumainiwa au kutoheshimiwa. Kumbuka kwamba Daudi alipozini na Bath-sheba na kumwua Uria, Yehova alimsamehe lakini hakumkinga na matokeo mabaya sana ya dhambi zake.—2 Samweli 12:9-12.
19-21. (a) Sheria iliyoandikwa kwenye Mambo ya Walawi 6:1-7 ilimfaidije mkosaji na yule aliyekosewa? (b) Ikiwa dhambi zetu zimewaumiza wengine, Yehova anafurahi tunapochukua hatua gani?
19 Dhambi zetu zinaweza kuwa na matokeo mengine, hasa ikiwa tumewaumiza wengine. Kwa mfano, fikiria simulizi la Mambo ya Walawi sura ya 6. Hapa Sheria ya Musa inashughulikia kisa cha mtu anayefanya dhambi nzito kwa kuchukua bidhaa za Mwisraeli mwenzake kupitia wizi, unyang’anyi, au ulaghai. Kisha mtenda-dhambi huyo anakataa kukubali kosa lake, na kuthubutu kuapa kwa uwongo. Ushuhuda wa mkosaji unapingana na ule wa mtu aliyekosewa. Hata hivyo, baadaye yule mkosaji anasumbuliwa na dhamiri na kuungamana dhambi yake. Mbali na kuungama ni lazima afanye mambo mengine matatu ili Mungu amsamehe: arudishe kitu alichokuwa amechukua, amlipe yule aliyekosewa faini ya jumla ya asilimia 20 ya thamani ya vitu alivyoiba, na atoe kondoo mume kama dhabihu ya hatia. Halafu sheria inasema: “Kuhani atafanya upatanisho kwa ajili yake mbele za BWANA, naye atasamehewa.”—Mambo ya Walawi 6:1-7.
20 Sheria hiyo ilikuwa mpango wenye rehema kutoka kwa Mungu. Sheria hiyo ilimfaidi aliyekosewa, kwa kuwa alirudishiwa mali yake na bila shaka alifurahi sana alipoona mkosaji akikiri dhambi zake. Vilevile, sheria hiyo ilimfaidi yule ambaye alichochewa na dhamiri kukiri kosa lake na kulirekebisha. Kwa kweli, kama angekataa kufanya hivyo, hangesamehewa na Mungu.
21 Ingawa hatuko chini ya Sheria ya Musa, Sheria hiyo inatusaidia kufahamu kindani fikira za Yehova, na maoni yake kuhusu msamaha. (Wakolosai 2:13, 14) Ikiwa dhambi zetu zimewaumiza wengine, Mungu anafurahi tunapofanya yote tuwezayo kurekebisha hali hiyo. (Mathayo 5:23, 24) Huenda tukahitaji kukiri dhambi yetu, kukubali kwamba tumekosea, na hata kumwomba msamaha yule tuliyemkosea. Kisha tunaweza kumwomba Yehova msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Yesu. Tukifanya hivyo tutakuwa na hakika kwamba Mungu ametusamehe kikweli.—Waebrania 10:21, 22.
22. Huenda msamaha wa Yehova ukaambatana na nini?
22 Kama mzazi yeyote mwenye upendo, huenda Yehova akatusamehe na kututia pia nidhamu kwa kadiri fulani. (Mithali 3:11, 12) Mkristo aliyetubu huenda akalazimika kuacha pendeleo la kutumikia akiwa mzee, mtumishi wa huduma, au mhubiri wa wakati wote. Huenda akahuzunika sana kwa sababu ya kupoteza kwa muda fulani mapendeleo aliyothamini sana. Hata hivyo, ijapokuwa mtu anatiwa nidhamu hiyo haimaanishi kwamba Yehova hajamsamehe. Ni lazima tukumbuke kwamba Yehova anatutia nidhamu kwa sababu anatupenda. Tutafaidika sana tukikubali na kujifunza kutokana na nidhamu hiyo.—Waebrania 12:5-11.
23. Kwa nini hatupaswi kamwe kufikiri kwamba hatuwezi kusamehewa na Yehova, na kwa nini tunapaswa kumwiga kwa kuwasamehe wengine?
23 Inatia moyo kama nini kujua kwamba Mungu wetu yuko “tayari kusamehe”! Licha ya makosa ambayo huenda tukawa tumefanya, hatupaswi kamwe kufikiri kwamba hatuwezi kusamehewa na Yehova. Tukitubu kikweli, na kuchukua hatua za kurekebisha kosa hilo, na kuomba msamaha kwa bidii kwa msingi wa damu ya Yesu iliyomwagwa, tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba Yehova atatusamehe. (1 Yohana 1:9) Na tumwige Yehova kwa kuwasamehe wengine. Ikiwa Yehova ambaye hafanyi dhambi, anatusamehe kwa upendo sana, je, sisi wanadamu wenye dhambi hatupaswi kufanya yote tuwezayo kusameheana?
a Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “umbo letu” linatumiwa pia kuhusiana na vyombo vya udongo vinavyofinyangwa na mfinyanzi.—Isaya 29:16.
b Msomi mmoja anasema kwamba rangi nyekundu “ilikuwa rangi isiyofifia, rangi ya kudumu. Haingeweza kuondolewa na umande, wala mvua, wala kwa kufuliwa, wala kwa kutumiwa kwa muda mrefu.”
-
-
“Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 27
“Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”
1, 2. Wema wa Mungu ni mwingi kadiri gani, na Biblia inakaziaje sifa hiyo?
KATIKA nuru nyangavu ya machweo, marafiki kadhaa wanafurahia kula chakula pamoja bustanini, wanacheka na kuzungumza huku wakifurahia mandhari. Mbali sana, mkulima anatazama mashamba yake na kutabasamu kwa sababu mawingu meusi yametanda angani na mvua imeanza kunyesha. Kwingineko, mume na mke wanafurahi sana kumwona mtoto wao mchanga akiyumba-yumba anapojaribu kutembea.
2 Iwe wanajua au hawajui, watu hao wote wananufaika na jambo moja—wema wa Yehova Mungu. Wanadini wengi hurudia-rudia maneno haya, “Mungu ni mwema.” Biblia inakazia sifa hiyo hata zaidi. Inasema: “Wema wake, jinsi ulivyo mwingi!” (Zekaria 9:17) Lakini yaonekana kwamba ni watu wachache sana leo wanaojua maana ya maneno hayo. Wema wa Yehova Mungu unahusisha nini, na sifa hiyo inamnufaishaje kila mmoja wetu?
Sifa Muhimu ya Upendo wa Mungu
3, 4. Wema ni nini, na kwa nini inaweza kusemwa kwamba wema wa Yehova ni wonyesho wa upendo wake?
3 Katika lugha nyingi leo, neno “wema” halina maana maalumu. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba wema ni sifa ya pekee sana. Sifa hiyo inamaanisha hasa wema wa kiadili. Kwa hivyo, tunaweza kusema kwamba Yehova ni mwema kabisa. Sifa zake zote, kutia ndani nguvu zake, haki yake, na hekima yake ni njema kabisa. Ingawa hivyo, wema unaweza kutajwa kwa kufaa kuwa wonyesho wa upendo wa Yehova. Kwa nini?
4 Wema ni sifa inayoonyeshwa kwa matendo. Mtume Paulo alisema kwamba mtu mwema huwavutia wengine zaidi kuliko mtu mwadilifu. (Waroma 5:7) Mtu mwadilifu hutii matakwa ya sheria kwa uaminifu, lakini mtu mwema hufanya mengi zaidi. Anachukua hatua na kujitahidi sana kuwasaidia wengine. Kama tutakavyoona, hapana shaka kwamba Yehova ni mwema katika njia hiyo. Kwa wazi, upendo wa Yehova usio na mipaka ndio chanzo cha wema wake.
5-7. Kwa nini Yesu alikataa kuitwa “Mwalimu Mwema,” na hivyo alithibitisha ukweli gani hakika?
5 Yehova ni mwema kwa njia isiyo na kifani. Muda mfupi kabla ya Yesu kufa, mtu fulani alimfikia ili kumwuliza swali na akamwita “Mwalimu Mwema.” Yesu akamjibu: “Kwa nini waniita mwema? Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.” (Marko 10:17, 18) Huenda ukashangazwa na jibu hilo. Mbona Yesu alimkosoa mtu huyo? Je, Yesu hakuwa “Mwalimu Mwema”?
6 Ni wazi kwamba mtu huyo alikuwa akimrairai Yesu kwa kutumia maneno “Mwalimu Mwema” kama cheo. Kwa unyenyekevu, Yesu alielekeza utukufu huo kwa Baba yake wa mbinguni, ambaye ni mwema kwa njia isiyo na kifani. (Mithali 11:2) Lakini Yesu alikuwa akithibitisha pia ukweli huu hakika: Ni Yehova peke yake anayeamua yaliyo mema. Akiwa Mwenye Enzi Kuu, ni yeye peke yake aliye na haki ya kuamua mambo mema na mabaya. Adamu na Hawa walijaribu kujitwalia haki hiyo walipoasi na kula tunda la mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Lakini Yesu kwa unyenyekevu anamwachia Baba yake haki ya kuamua mema na mabaya.
7 Isitoshe, Yesu alijua kwamba Yehova ndiye chanzo cha vitu vyote vyema. Yeye ni Mtoaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Hebu tuone jinsi ambavyo ukarimu wa Yehova unathibitisha wema wake.
Mambo Yanayothibitisha Wema Mwingi wa Yehova
8. Yehova amewaonyeshaje wanadamu wote wema?
8 Kila mtu aliyepata kuishi amenufaishwa na wema wa Yehova. Zaburi 145:9 yasema: “BWANA ni mwema kwa watu wote.” (Italiki ni zetu.) Ni mifano ipi inayoonyesha kwamba wema wake unamnufaisha kila mtu? Biblia inasema hivi: “Hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.” (Matendo 14:17) Je, umewahi kufurahia chakula kitamu? Hakungekuwa na chakula chochote kama Yehova hangekuwa mwema na kubuni mzunguko wa maji safi na “majira yenye kuzaa matunda.” Yehova amewatendea watu wote wema, hata wale wasiompenda. Yesu alisema hivi: “Hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:45.
Yehova ‘anawapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda’
9. Tofaa linaonyeshaje wema wa Yehova?
9 Wengi hupuuza ukarimu mkubwa ambao wanadamu wanaonyeshwa kupitia jua, mvua, na majira ya matunda. Kwa mfano, fikiria tofaa, tunda linalokuzwa sana katika maeneo yenye halijoto ya wastani duniani. Ni tunda tamu sana linalovutia, lina madini muhimu na maji tosha yanayoburudisha. Je, wajua kwamba ulimwenguni pote kuna aina 7,500 hivi za matofaa yenye rangi mbalimbali kama vile nyekundu, rangi ya dhahabu, manjano, na rangi ya kijani-kibichi, na yana ukubwa mbalimbali, mengine ni makubwa kidogo kuliko cheri na mengine ni kama balungi? Tofaa lina mbegu ndogo. Lakini mojawapo ya miti maridadi zaidi hukua kutoka kwa mbegu hiyo ndogo. (Wimbo Ulio Bora 2:3, BHN) Kila mwaka mtofaa huchanua maua mengi yenye kuvutia na kuzaa matunda. Kila mwaka, kwa muda wa miaka 75 hivi, mtofaa wa wastani huzaa katoni 20 za matunda, kila katoni ikiwa na uzito wa kilogramu 19!
Mti unaoweza kulisha na kuwafurahisha watu kwa miaka mingi sana hukua kutoka kwa mbegu hii ndogo
10, 11. Hisi zetu zinathibitishaje wema wa Mungu?
10 Kwa wema wake usio na kikomo, Yehova ametupatia mwili ambao ‘umeumbwa kwa jinsi ya ajabu.’ Tuna hisi ambazo zinakusudiwa kutusaidia kutambua kazi zake na kuzifurahia. (Zaburi 139:14) Hebu fikiria tena mambo yaliyotajwa mwanzoni mwa sura hii. Tunafurahia kuona mambo gani? Uso mwangavu wa mtoto anayeangua kicheko. Mvua kubwa inaponyesha. Machweo ya rangi nyekundu, ya dhahabu, na ya urujuani. Jicho la mwanadamu linaweza kuona zaidi ya rangi 300,000! Na tunaweza kusikia na kutofautisha sauti mbalimbali zinazovutia, kama vile mvumo wa upepo katika miti, na kicheko kichangamfu cha mtoto mchanga. Ni nini kinachotuwezesha kufurahia mambo hayo? Biblia inasema: “Sikio lisikialo, na jicho lionalo, BWANA ndiye aliyeyafanya yote mawili.” (Mithali 20:12) Lakini hizo ni hisi mbili tu.
11 Hisi yetu ya kunusa huthibitisha pia wema wa Yehova. Pua ya mwanadamu inaweza kutofautisha harufu zipatazo 10,000. Baadhi ya harufu hizo ni: harufu nzuri ya chakula upendacho kinapopikwa, harufu nzuri ya maua, ya majani makavu, harufu ya moshi. Na hisi yako ya kugusa inakuwezesha kuhisi upepo unapovuma kwa wanana usoni mwako, kupata utulivu unapokumbatiwa na mpendwa wako, kuhisi tunda lenye ganda laini mkononi mwako. Unapoliuma, hisi yako ya kuonja inaanza kufanya kazi. Unafurahia ladha mbalimbali vionjio vyako vinapoonja kemikali tata za tunda hilo. Naam, tuna kila sababu ya kutangaza hivi kumhusu Yehova: “Jinsi gani ulivyo mwingi wema wako, uliowawekea wale wanaokucha!” (Zaburi 31:19, BHN) Lakini Yehova ‘amewawekeaje’ wema wale ambao wanamhofu?
Wema Unaoleta Faida za Milele
12. Ni maandalizi gani kutoka kwa Yehova yaliyo muhimu zaidi, na kwa nini?
12 Yesu alisema: “Imeandikwa, ‘Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.’” (Mathayo 4:4) Kwa kweli, maandalizi ya kiroho kutoka kwa Yehova yanaweza kutufaidi kuliko maandalizi ya kimwili, kwa kuwa yatatuwezesha kuishi milele. Katika Sura ya 8 ya kitabu hiki, tuliona kwamba katika siku hizi za mwisho, Yehova ametumia uwezo wake wa kurudisha hali mpya kuleta paradiso ya kiroho. Jambo muhimu zaidi ni kwamba paradiso hiyo ina chakula tele cha kiroho.
13, 14. (a) Nabii Ezekieli aliona nini katika ono, nalo linatuhusuje leo? (b) Yehova amewapa watumishi wake waaminifu maandalizi gani ya kiroho kwa ajili ya uhai?
13 Katika mojawapo ya unabii mbalimbali muhimu wa urudisho, nabii Ezekieli alipata ono la hekalu jipya lenye utukufu. Kijito kilichotiririka kutoka hekaluni humo, kilizidi kupanuka na kina chake kuongezeka hatua kwa hatua mpaka kikawa “mto.” Mto huo ulikuwa na matokeo mazuri popote ulipopitia. Miti mingi sana ambayo ilitokeza chakula na maponyo ilisitawi kwenye kingo za mto huo. Na mto huo hata ulileta uhai na ufanisi katika Bahari ya Chumvi isiyo na uhai! (Ezekieli 47:1-12) Lakini ono hilo lilimaanisha nini?
14 Ono hilo lilimaanisha kwamba Yehova angerudisha mpango wake wa ibada safi ambao unawakilishwa na hekalu aliloona Ezekieli. Maandalizi ya Mungu kwa ajili ya uhai yangewamiminikia watu wake kwa wingi zaidi kama ule mto ulio katika ono. Tangu kurudishwa kwa ibada safi mwaka wa 1919, Yehova amewabariki watu wake kwa kuwapa maandalizi ya uhai. Jinsi gani? Biblia, vichapo vya Biblia, mikutano, na makusanyiko yamewasaidia mamilioni ya watu kupata kweli muhimu sana. Kupitia njia hizo, Yehova amewafundisha watu kuhusu mpango muhimu zaidi kwa ajili ya uhai—dhabihu ya fidia ya Kristo. Dhabihu hiyo huwawezesha wote wanaompenda na kumhofu Yehova kikweli wawe na uhusiano mzuri naye na kuwa na tumaini la kuishi milele.a Kwa hiyo, watu wa Yehova wamekuwa wakifurahia karamu ya kiroho katika siku hizi za mwisho, huku ulimwengu ukiteseka kwa sababu ya njaa ya kiroho.—Isaya 65:13.
15. Wema wa Yehova utawanufaishaje wanadamu waaminifu wakati wa Utawala wa Kristo wa miaka elfu moja?
15 Lakini mto alioona Ezekieli hautakoma kutiririka huu mfumo wa kale wa mambo utakapoharibiwa. Kinyume chake, utaendelea kutiririka kwa wingi zaidi wakati wa Utawala wa Kristo wa miaka elfu moja. Wakati huo, kupitia Ufalme wa Kimesiya, Yehova atatumia manufaa kamili ya dhabihu ya Yesu ili wanadamu waaminifu wafikie ukamilifu hatua kwa hatua. Ndipo tutakaposhangilia sana kwa sababu ya wema wa Yehova!
Sifa Nyingine za Wema wa Yehova
16. Biblia inaonyeshaje kwamba wema wa Yehova unatia ndani sifa nyingine? Taja baadhi ya sifa hizo.
16 Wema wa Yehova watia ndani sifa nyingine mbali na ukarimu. Mungu alimwambia Musa hivi: “Nitapitisha wema wangu wote mbele yako, nami nitalitangaza jina la BWANA mbele yako.” Simulizi hilo lasema kwamba baadaye ‘BWANA alipita mbele yake, akatangaza, BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.’ (Kutoka 33:19; 34:6) Kwa hiyo, wema wa Yehova unatia ndani sifa kadhaa zenye kuvutia. Hebu tuchunguze sifa mbili tu kati ya sifa hizo.
17. Fadhili ni nini, na Yehova amewaonyeshaje fadhili wanadamu duni wasiokamilika?
17 “Mwenye fadhili.” Sifa hii inatuonyesha jinsi ambavyo Yehova anashughulika na viumbe wake. Badala ya kuwa mkali sana, na asiyejali, au kuwa katili kama watu wengi wenye mamlaka, Yehova ni mpole na mwenye fadhili. Kwa mfano, Yehova alimwambia hivi Abramu: “Tafadhali inua macho yako ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi.” (Mwanzo 13:14, NW) Tafsiri nyingi hazitaji neno “tafadhali.” Lakini wasomi wa Biblia wanasema kwamba maandishi ya awali ya Kiebrania yana kishirikishi cha neno ambacho kinabadili taarifa hiyo kuwa ombi la heshima badala ya amri. Kuna mifano mingine. (Mwanzo 31:12, NW; Ezekieli 8:5, NW) Hebu wazia, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu anasema “tafadhali” anapoongea na wanadamu duni. Katika ulimwengu ambamo watu wengi ni wakali, wachokozi na wasio na adabu, inatia moyo kutafakari fadhili ya Mungu wetu Yehova.
18. Yehova ni “mwingi wa . . . kweli” katika maana gani, na kwa nini maneno hayo yanatia moyo?
18 “Mwingi wa . . . kweli.” Kusema uwongo ni zoea la kawaida ulimwenguni leo. Lakini Biblia inatukumbusha hivi: “Mungu si mtu, aseme uongo.” (Hesabu 23:19) Isitoshe, andiko la Tito 1:2 linasema kwamba ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ Hawezi kusema uwongo kwa sababu yeye ni mwema sana. Kwa hivyo, ahadi za Yehova zinategemeka kabisa; maneno yake hayawezi kamwe kukosa kutimia. Yehova anaitwa pia “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Mbali na kutosema uwongo, anaeneza ukweli kwa wingi. Yeye hafanyi mambo kwa kujificha au kisirisiri, bali yeye huwafundisha watumishi wake waaminifu hekima yake isiyo na mipaka.b Hata anawafundisha jinsi ya kuishi kupatana na kweli hizo ili ‘waendelee kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 3) Kwa ujumla, kila mmoja wetu anapaswa kuitikiaje wema wa Yehova?
‘Ukimbilieni Wema wa Bwana’
19, 20. (a) Shetani alidhoofishaje tumaini la Hawa katika wema wa Yehova, na matokeo yalikuwa nini? (b) Wema wa Yehova unapaswa kutuchochea tufanye nini, na kwa nini?
19 Shetani alipomshawishi Hawa katika bustani ya Edeni, alianza kwa kudhoofisha kwa hila tumaini lake katika wema wa Yehova. Yehova alikuwa amemwambia Adamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula.” Yehova alimkataza kula matunda ya mti mmoja tu kati ya maelfu ya miti yenye kuvutia iliyokuwa bustanini. Hata hivyo, angalia swali ambalo Shetani alimwuliza Hawa: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?” (Mwanzo 2:9, 16; 3:1) Shetani alipotosha maneno ya Yehova ili amsadikishe Hawa kwamba Yehova alikuwa akimnyima kitu fulani kizuri. Kwa kusikitisha, Hawa alidanganyika. Hawa alianza kutilia shaka wema wa Mungu ambaye alikuwa amempa kila kitu alichokuwa nacho. Wanaume na wanawake wengi walioishi baadaye walifuata mfano wake.
20 Tunajua huzuni na taabu nyingi sana zilizosababishwa na shaka hiyo. Basi na tutii maneno ya Yeremia 31:12: “Wataukimbilia wema wa BWANA.” Bila shaka tunapaswa kuukimbilia wema wa Yehova kwa shangwe. Hatupaswi kamwe kutilia shaka makusudi ya Mungu wetu ambaye ni mwema sana. Tunaweza kumtumaini kabisa kwa sababu anataka wale wanaompenda wawe na maisha bora.
21, 22. (a) Ungependa kuonyesha katika njia zipi kwamba unathamini wema wa Yehova? (b) Tutazungumzia sifa gani katika sura inayofuata, na sifa hiyo inatofautianaje na wema?
21 Zaidi ya hayo, tunafurahi tunapopata nafasi ya kuwaambia wengine kuhusu wema wa Mungu. Zaburi 145:7 yasema hivi kuhusu watu wa Yehova: “Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu.” Kila siku tunafaidika kwa njia fulani na wema wa Yehova. Kwa nini usimshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya jambo hususa linaloonyesha wema wake? Kutafakari na kumshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya wema wake, na kuwaambia wengine kuhusu sifa hiyo kutatusaidia kumwiga Mungu wetu mwema. Tutamkaribia Yehova zaidi tukitafuta njia za kuiga wema wake. Mtume Yohana aliyezeeka aliandika hivi: “Mpendwa, uwe mwigaji, si wa lililo baya, bali wa lililo jema. Yeye ambaye atenda mema hutokana na Mungu.”—3 Yohana 11.
22 Wema wa Yehova unahusiana pia na sifa nyingine. Kwa mfano, Mungu ni “mwingi wa fadhili-upendo,” au upendo mshikamanifu. (Kutoka 34:6, NW) Tofauti na wema, Yehova hawaonyeshi watu wote sifa hiyo bali anawaonyesha hasa watumishi wake waaminifu. Katika sura inayofuata, tutajifunza jinsi anavyofanya hivyo.
a Fidia ndiyo uthibitisho bora zaidi wa wema wa Yehova. Ajapokuwa na mamilioni ya viumbe wa roho, Yehova alimchagua Mwanaye mpendwa aliye mzaliwa-pekee afe kwa ajili yetu.
b Kwa kufaa, Biblia inaonyesha kwamba kweli inahusiana na nuru. Mtunga-zaburi aliimba hivi: ‘Niletee nuru yako na kweli yako.’ (Zaburi 43:3) Yehova anawaangazia nuru nyingi ya kiroho wale walio na nia ya kufundishwa au kuelimishwa naye.—2 Wakorintho 4:6; 1 Yohana 1:5.
-
-
“Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 28
“Wewe Peke Yako Ni Mwaminifu-Mshikamanifu”
1, 2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mfalme Daudi alijua matokeo mabaya ya kukosa uaminifu-mshikamanifu?
MFALME DAUDI alijua matokeo mabaya ya kukosa uaminifu-mshikamanifu. Pindi moja utawala wake wenye misukosuko ulikabili matatizo wakati watu wa taifa lake walipopanga njama ya kumwondoa mamlakani. Isitoshe, Daudi alisalitiwa na baadhi ya watu ambao tungetarajia wawe marafiki wake wa karibu. Fikiria Mikali, mke wa kwanza wa Daudi. Mwanzoni, “alimpenda Daudi” na hapana shaka kwamba alimuunga mkono katika madaraka yake ya kifalme. Hata hivyo, baadaye ‘alimdharau moyoni mwake,’ hata akamwona Daudi kama ‘mmojawapo wa watu baradhuli.’—1 Samweli 18:20; 2 Samweli 6:16, 20.
2 Mwingine alikuwa Ahithofeli, aliyekuwa mshauri wa Daudi. Shauri lake lilithaminiwa sana kana kwamba lilikuwa neno la Yehova mwenyewe. (2 Samweli 16:23) Lakini, mwishowe, mshauri huyo mwenye kutumainiwa alimsaliti Daudi na kujiunga na waasi. Ni nani aliyepanga njama hiyo? Absalomu, mwana wa Daudi! Mhaini huyo mwenye kujitafutia makuu ‘aliwadanganya watu wa Israeli,’ akajitawaza mwenyewe kuwa mfalme mpinzani. Uasi wa Absalomu ulipamba moto sana hivi kwamba Mfalme Daudi alilazimika kukimbia ili kujiokoa.—2 Samweli 15:1-6, 12-17.
3. Daudi alikuwa na uhakika gani?
3 Je, hakukuwa mtu yeyote aliyebaki mwaminifu-mshikamanifu kwa Daudi? Katika shida zake zote, Daudi alikuwa na uhakika kwamba kulikuwa na mmoja aliyekuwa mwaminifu-mshikamanifu kwake. Nani? Yehova Mungu mwenyewe. Daudi alisema hivi kumhusu: “Wewe ni mwaminifu kwa walio waaminifu.” (2 Samweli 22:26, BHN) Uaminifu-mshikamanifu ni nini, na Yehova anaonyeshaje sifa hii kwa njia bora zaidi?
Uaminifu-Mshikamanifu Ni Nini?
4, 5. (a) “Uaminifu-mshikamanifu” ni nini? (b) Uaminifu-mshikamanifu unatofautianaje na uaminifu?
4 Kulingana na Maandiko ya Kiebrania, “uaminifu-mshikamanifu” ni fadhili ambayo inashikamana kabisa kwa upendo na kitu fulani hadi kusudi lake kuhusiana na kitu hicho linapotimia. Uaminifu-mshikamanifu unahusisha mambo mengi mbali na uaminifu. Mtu anaweza kuwa mwaminifu kwa sababu tu ya wajibu. Kinyume chake, uaminifu-mshikamanifu unategemea upendo. Isitoshe, neno “-aminifu” linaweza kutumiwa kuhusiana na vitu visivyo hai. Kwa mfano, mtunga-zaburi alisema kwamba mwezi ni “shahidi aliye mbinguni mwaminifu” kwa sababu unaangaza kwa ukawaida wakati wa usiku. (Zaburi 89:37) Lakini hatuwezi kusema kwamba mwezi ni mwaminifu-mshikamanifu. Kwa nini? Kwa sababu uaminifu-mshikamanifu unategemea upendo. Na vitu visivyo hai haviwezi kuonyesha sifa hiyo.
Mwezi unaitwa shahidi mwaminifu, lakini ni viumbe wenye akili tu wanaoweza kuiga uaminifu-mshikamanifu wa Yehova
5 Maandiko yanaonyesha kwamba uaminifu-mshikamanifu hudhihirisha upendo. Ni wazi kwamba kuna uhusiano fulani kati ya mtu anayeonyeshwa sifa hiyo na yule anayeionyesha. Uaminifu-mshikamanifu hauna kigeugeu. Si kama mawimbi ya bahari yanayopeperushwa huku na huku. Kinyume chake, sifa ya uaminifu-mshikamanifu, au upendo-mwaminifu inaweza kushinda hali ngumu sana.
6. (a) Uaminifu-mshikamanifu ni haba kadiri gani miongoni mwa wanadamu, na Biblia inathibitishaje jambo hilo? (b) Njia bora ya kujifunza kuhusu uaminifu-mshikamanifu ni ipi, na kwa nini?
6 Ni kweli kwamba uaminifu-mshikamanifu ni haba sana leo. Mara nyingi, marafiki wa karibu ‘huangamizana.’ Tunasikia visa vingi sana vya watu wanaowaacha wenzi wao wa ndoa. (Mithali 18:24; Malaki 2:14-16) Matendo ya hiana ni mengi sana hivi kwamba tunaweza kurudia maneno ya nabii Mika: “Mtu mwaminifu-mshikamanifu ametoweka duniani.” (Mika 7:2, NW) Mara nyingi wanadamu hushindwa kuonyesha uaminifu-mshikamanifu, lakini Yehova huonyesha sifa hiyo kwa njia ya pekee sana. Njia bora ya kujifunza kuhusu uaminifu-mshikamanifu ni kwa kuchunguza jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hii kuu ya upendo wake.
Uaminifu-Mshikamanifu wa Yehova Usio na Kifani
7, 8. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mwaminifu-mshikamanifu?
7 Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Wewe peke yako ni mwaminifu-mshikamanifu.” (Ufunuo 15:4) Kwa nini Biblia inasema hivyo, hali wanadamu na malaika wameonyesha uaminifu-mshikamanifu wa pekee pindi kwa pindi? (Ayubu 1:1; Ufunuo 4:8) Vipi Yesu Kristo? Yeye ndiye mtu “mwaminifu-mshikamanifu” zaidi mbele za Mungu. (Zaburi 16:10, NW) Basi, kwa nini inaweza kusemwa kwamba ni Yehova peke yake aliye mwaminifu-mshikamanifu?
8 Kwanza, kumbuka kwamba uaminifu-mshikamanifu ni sifa ya upendo. Hakuna mtu awaye yote anayeweza kuwa mwaminifu-mshikamanifu kikamili zaidi kuliko Yehova, kwa sababu “Mungu ni upendo,” yaani, yeye ni wonyesho halisi wa upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa kweli, malaika na wanadamu wanaweza kuiga tu sifa za Mungu, lakini hawawezi kuwa na uaminifu-mshikamanifu wa hali ya juu sana kama yeye. Amekuwa akionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa muda mrefu kuliko kiumbe yeyote duniani au mbinguni, kwa sababu Yeye ni “mzee wa siku.” (Danieli 7:9) Kwa hiyo, Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa kadiri kubwa sana. Yehova anaonyesha sifa hiyo kwa njia isiyo na kifani. Fikiria mifano kadhaa.
9. Yehova ni “mwaminifu-mshikamanifu juu ya kazi zake zote” kwa njia gani?
9 Yehova ni “mwenye fadhili [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW] juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:17) Jinsi gani? Zaburi 136 inajibu swali hilo. Andiko hilo linataja matendo kadhaa ya Yehova ya kuokoa, kutia ndani alipowaokoa Waisraeli kwa njia ya kustaajabisha katika Bahari Nyekundu. Jambo la kutokeza ni kwamba kila mstari wa zaburi hiyo unakaziwa na usemi: “Kwa maana fadhili [au, uaminifu-mshikamanifu] zake ni za milele.” Zaburi hiyo imetajwa katika Maswali ya Kutafakari kwenye ukurasa wa 289. Unaposoma mistari hiyo, utavutiwa sana kuona jinsi Yehova alivyoonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watu wake kwa njia mbalimbali. Naam, Yehova huwa mwaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake waaminifu kwa kusikia vilio vyao vya kuomba msaada na kwa kuchukua hatua kwa wakati wake. (Zaburi 34:6) Yehova huendelea kuwaonyesha watumishi wake upendo-mshikamanifu maadamu wanaendelea kuwa waaminifu kwake.
10. Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kuhusiana na kanuni zake jinsi gani?
10 Zaidi ya hayo, Yehova huwaonyesha watumishi wake uaminifu-mshikamanifu kwa kushikilia kabisa kanuni zake. Yehova si kama wanadamu wasiotegemeka au wasio na msimamo ambao wanafuata tu hisia zao, maoni yake kuhusu mema na mabaya hayabadiliki. Miaka nenda miaka rudi, Yehova hajabadili kamwe maoni yake kuhusu uwasiliani-roho, ibada ya sanamu, na kuua. Alisema hivi kupitia nabii wake Isaya, “Mimi ni yuleyule hata katika uzee wenu.” (Isaya 46:4, BHN) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutafaidika tukifuata mwongozo wa kiadili unaoelezwa waziwazi katika Neno la Mungu.—Isaya 48:17-19.
11. Taja mifano inayoonyesha kwamba Yehova hutimiza ahadi zake kwa uaminifu-mshikamanifu.
11 Yehova huonyesha pia uaminifu-mshikamanifu kwa kutimiza ahadi zake. Kila jambo analotabiri linatimia. Yehova alisema hivi: “Neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isaya 55:11) Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watu wake kwa kutimiza ahadi zake. Yeye hawaahidi mambo ambayo hatatimiza. Yehova amethibitisha kabisa kwamba anatimiza ahadi zake hivi kwamba mtumishi wake Yoshua aliweza kusema: “Halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo BWANA alikuwa amelinena katika habari ya nyumba ya Israeli; yalitimia mambo yote.” (Yoshua 21:45) Hivyo basi, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatatukatisha tamaa kwa kukosa kutimiza ahadi zake.—Isaya 49:23; Waroma 5:5.
12, 13. Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova “ni wa milele” katika maana gani?
12 Kama tulivyoona hapo awali, Biblia inatuambia kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova “ni wa milele.” (Zaburi 136:1, NW) Jinsi gani? Kwanza, Yehova husamehe kabisa dhambi. Kama Sura ya 26 ilivyoonyesha, Yehova hakumbuki na kumhukumu mtu kwa sababu ya dhambi ambazo tayari amesamehewa. Kila mmoja wetu anapaswa kushukuru kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ni wa milele kwa sababu ‘sote tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’—Waroma 3:23.
13 Lakini uaminifu-mshikamanifu wa Yehova ni wa milele katika maana nyingine pia. Neno lake linasema kwamba mtu mwadilifu “atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.” (Zaburi 1:3) Hebu wazia mti mkubwa sana ambao majani yake hayanyauki! Vivyo hivyo, tukipendezwa kikweli na Neno la Mungu, tutaishi muda mrefu, tutakuwa na amani, na kufanikiwa. Yehova awaahidi watumishi wake waaminifu baraka za milele. Kwa kweli, katika ulimwengu mpya wenye uadilifu ambao Yehova ataleta, wanadamu watiifu watafurahia uaminifu-mshikamanifu wake milele.—Ufunuo 21:3, 4.
Yehova ‘Hatawaacha Waaminifu Wake’
14. Yehova anaonyeshaje kwamba anathamini uaminifu wa watumishi wake?
14 Yehova ameonyesha uaminifu-mshikamanifu tena na tena. Kwa sababu Yehova hana kigeugeu kamwe, yeye huwaonyesha watumishi wake uaminifu-mshikamanifu wa kudumu. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nilikuwa kijana na sasa ni mzee; kamwe sijaona mwadilifu ameachwa na Mungu, au: watoto wake wakiombaomba chakula. Maana Mwenyezi-Mungu hupenda uadilifu, wala hawaachi waaminifu wake.” (Zaburi 37:25, 28, BHN) Ni kweli kwamba Yehova anastahili ibada yetu kwa sababu yeye ni Muumba. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, Yehova anathamini sana uaminifu wetu kwa sababu yeye ni mwaminifu-mshikamanifu.—Malaki 3:16, 17.
15. Eleza jinsi Yehova alivyoonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Israeli.
15 Kwa uaminifu-mshikamanifu, sikuzote Yehova huwasaidia watu wake wanapokumbwa na matatizo. Mtunga-zaburi anatuambia hivi: “Huwalinda nafsi zao watauwa wake, na kuwaokoa na mkono wa wasio haki.” (Zaburi 97:10) Fikiria jinsi alivyoshughulika na taifa la Israeli. Baada ya kuokolewa kimuujiza katika Bahari Nyekundu, Waisraeli walitangaza hivi katika wimbo waliomwimbia Yehova: “Wewe kwa fadhili-upendo zako [au, “upendo-mshikamanifu,” kielezi-chini] umewaongoza watu uliowakomboa.” (Kutoka 15:13, NW) Hapana shaka kwamba Yehova alionyesha upendo-mshikamanifu alipowaokoa katika Bahari Nyekundu. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “BWANA hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; bali kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu BWANA akawatoa kwa mkono wa nguvu, akawakomboa katika nyumba ya utumwa, katika mkono wa Farao, mfalme wa Misri.”—Kumbukumbu la Torati 7:7, 8.
16, 17. (a) Waisraeli walikosa kabisa kuthamini nini, lakini Yehova aliwaonyeshaje rehema? (b) Waisraeli wengi walionyeshaje kwamba ‘hawangeweza kuponywa,’ na hilo linatupatia onyo gani?
16 Bila shaka, taifa la Israeli halikuthamini uaminifu-mshikamanifu wa Yehova. Baada ya kukombolewa, ‘walizidi kumtenda dhambi [Yehova], walipomwasi Aliye Juu.’ (Zaburi 78:17) Kadiri miaka ilivyopita, waliasi tena na tena, walimwacha Yehova na kugeukia miungu ya uwongo na mazoea ya kipagani ambayo yaliwatia unajisi. Hata hivyo, Yehova hakuvunja agano lake. Badala yake, Yehova aliwasihi hivi watu wake kupitia nabii Yeremia: “Rudi, Ee Israeli mwenye kuasi . . . Sitakutazama kwa hasira; maana mimi ni mwenye rehema [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW].” (Yeremia 3:12) Lakini, kama Sura ya 25 ilivyoonyesha, Waisraeli wengi walikataa kubadilika. Hata, “waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake.” Matokeo yalikuwa nini? Mwishowe, ‘ghadhabu ya BWANA ilizidi juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponywa.’—2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16.
17 Twajifunza nini kutokana na mambo hayo? Twajifunza kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Yehova haudanganyiki wala si wa kijinga. Ni kweli kwamba Yehova ni ‘mwingi wa rehema’ naye hupenda kuonyesha rehema kunapokuwa na msingi wa kufanya hivyo. Lakini Yehova huchukua hatua gani mtu mwovu anapokuwa sugu? Inapokuwa hivyo, Yehova hushikamana na kanuni zake adilifu naye humhukumu mtu mwovu. Musa aliambiwa kwamba Yehova “si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.”—Kutoka 34:6, 7.
18, 19. (a) Yehova anaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaadhibu waovu? (b) Yehova ataonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa?
18 Mungu huonyesha pia uaminifu-mshikamanifu kwa kuwaadhibu waovu. Vipi? Amri ambazo Yehova anawapa wale malaika saba katika kitabu cha Ufunuo zaonyesha jambo hilo: “Nendeni mkamwage mabakuli saba ya hasira ya Mungu ndani ya dunia.” Malaika wa tatu anapomwaga bakuli lake “ndani ya mito na mabubujiko ya maji,” yanakuwa damu. Kisha malaika huyo anamwambia Yehova hivi: “Wewe, Uliyeko na uliyekuwako, Mwaminifu-Mshikamanifu, ni mwadilifu, kwa sababu umetoa maamuzi haya, kwa sababu walimwaga damu ya watakatifu na ya manabii, nawe umewapa damu wanywe. Wao wastahili hilo.”—Ufunuo 16:1-6.
Yehova atawakumbuka na kuwafufua kwa uaminifu wale ambao wamedumu wakiwa waaminifu-washikamanifu hadi kifo
19 Ona kwamba malaika huyo anapotangaza ujumbe huo wa hukumu anasema kwamba Yehova ni “Mwaminifu-Mshikamanifu.” Kwa nini? Kwa sababu anapowaangamiza waovu, Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu kwa watumishi wake ambao wameteswa na kuuawa. Kwa uaminifu-mshikamanifu, Yehova anawakumbuka vizuri watumishi hao. Anatamani kuwaona tena waaminifu hao waliokufa, na Biblia inaonyesha waziwazi kwamba anakusudia kuwathawabisha kwa kuwafufua. (Ayubu 14:14, 15) Yehova hawasahau watumishi wake waaminifu eti kwa sababu wamekufa. Badala yake, “kwake, wao wote wako hai.” (Luka 20:37, 38) Kusudi la Yehova la kuwafufua wale walio katika kumbukumbu lake linathibitisha kabisa kwamba yeye ni mwaminifu-mshikamanifu.
Wanazi walimuua Bernard Luimes (kushoto) na Wolfgang Kusserow (katikati)
Kikundi cha kisiasa kilimuua Moses Nyamussua kwa kumchoma mkuki
Upendo-Mshikamanifu wa Yehova Huandaa Njia ya Wokovu
20. “Vyombo vya rehema” ni nani? na Yehova anawaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu?
20 Katika historia yote, Yehova ameonyesha uaminifu-mshikamanifu wa pekee kwa wanadamu. Kwa maelfu ya miaka, Yehova ‘amevumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira ya kisasi vilivyofanywa kufaa kwa ajili ya uharibifu.’ Kwa nini? “Ili apate kujulisha utajiri wa utukufu wake juu ya vyombo vya rehema, alivyotayarisha kimbele kwa ajili ya utukufu.” (Waroma 9:22, 23) “Vyombo vya rehema” ni wale walio na mtazamo ufaao ambao wametiwa mafuta kwa roho takatifu ili wawe warithi pamoja na Kristo katika Ufalme wake. (Mathayo 19:28) Kwa kuandaa njia ya wokovu kwa ajili ya vyombo hivyo vya rehema, Yehova alionyesha uaminifu-mshikamanifu kwa Abrahamu, kwa sababu alikuwa amemwahidi hivi alipofanya agano naye: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.
Watumishi wote waaminifu wa Yehova wana tumaini hakika la wakati ujao kwa sababu yeye ni mwaminifu-mshikamanifu
21. (a) Yehova anaonyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kubwa”? (b) Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova unakuchochea kufanya nini?
21 Yehova anaonyesha uaminifu-mshikamanifu pia kwa “umati mkubwa” ambao unatumaini kuokoka “dhiki kubwa” na kuishi milele katika paradiso duniani. (Ufunuo 7:9, 10, 14) Kwa uaminifu-mshikamanifu, Yehova anawapa watumishi wake fursa ya kuishi milele katika paradiso duniani ingawa wao si wakamilifu. Jinsi gani? Anawapa fursa hiyo kupitia fidia—wonyesho mkuu zaidi wa uaminifu-mshikamanifu wa Yehova. (Yohana 3:16; Waroma 5:8) Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova unawavuta wale ambao wana njaa ya uadilifu mioyoni mwao. (Yeremia 31:3) Je, huhisi ukiwa karibu zaidi na Yehova kwa sababu ya uaminifu-mshikamanifu wa dhati ambao amekuonyesha na atakuonyesha? Kwa sababu tunatamani kumkaribia Mungu, na tuthamini upendo wake kwa kuimarisha azimio letu la kumtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu.
-
-
“Kuujua Upendo wa Kristo”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 29
“Kuujua Upendo wa Kristo”
1-3. (a) Ni nini kilichomchochea Yesu atake kumwiga Baba yake? (b) Tutachunguza sehemu zipi za upendo wa Yesu?
JE, UMEWAHI kumwona mvulana mdogo akijaribu kumwiga baba yake? Huenda akaiga jinsi baba yake anavyotembea, anavyoongea, au anavyotenda. Muda si muda, huenda mvulana huyo akaanza kufuata maadili na kanuni za kiroho za baba yake. Naam, mvulana huyo hujitahidi kuwa kama baba yake kwa sababu anampenda na kumthamini.
2 Vipi uhusiano wa Yesu na Baba yake wa mbinguni? Yesu alisema hivi pindi moja: “Nampenda Baba.” (Yohana 14:31) Hakuna mtu yeyote anayeweza kumpenda Yehova kama Mwana huyo, ambaye alikaa na Baba yake kwa muda mrefu sana kabla kiumbe yeyote hajaumbwa. Upendo ulimchochea Mwana huyo mwaminifu kutaka kumwiga Baba yake.—Yohana 14:9.
3 Katika sura zilizotangulia za kitabu hiki, tulizungumzia jinsi ambavyo Yesu aliiga kikamili nguvu, haki, na hekima ya Yehova. Lakini Yesu alionyeshaje upendo wa Baba yake? Hebu tuchunguze sehemu tatu za upendo wa Yesu—roho yake ya kujidhabihu, huruma yake nyororo, na utayari wake wa kusamehe.
“Hakuna Aliye na Upendo Mkubwa Zaidi Kuliko Huu”
4. Yesu alionyeshaje mfano bora kabisa wa upendo wa kujidhabihu akiwa binadamu?
4 Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa njia bora sana. Kujidhabihu ni kutanguliza mahitaji na masilahi ya wengine bila ubinafsi. Yesu alionyeshaje upendo huo? Yeye mwenyewe alieleza hivi: “Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:13) Yesu alitoa uhai wake mkamilifu kwa hiari kwa ajili yetu. Huo ulikuwa wonyesho mkuu zaidi wa upendo kuwahi kuonyeshwa na mwanadamu yeyote. Lakini Yesu alionyesha upendo wa kujidhabihu kwa njia nyinginezo pia.
5. Kwa nini lile tendo la Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu kuondoka mbinguni lilikuwa kujidhabihu kwa upendo?
5 Kabla ya kuwa mwanadamu, Mwana huyo mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa na cheo cha juu na cha pekee huko mbinguni. Alishirikiana kwa ukaribu sana na Yehova na viumbe wengi wa roho. Licha ya mapendeleo hayo, Mwana huyo mpendwa “alijifanya mwenyewe kuwa mtupu na kuchukua umbo la mtumwa na kuja kuwa katika ufanani wa wanadamu.” (Wafilipi 2:7) Kwa hiari, alikuja kuishi na wanadamu wenye dhambi katika ulimwengu ambao “unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Bila shaka Mwana wa Mungu alijidhabihu kwa upendo, sivyo?
6, 7. (a) Yesu alijidhabihu kwa upendo katika njia zipi wakati wa huduma yake duniani? (b) Andiko la Yohana 19:25-27 lasimulia jambo gani lenye kugusa moyo kuhusu upendo wa kujidhabihu?
6 Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alijidhabihu kwa upendo katika njia mbalimbali. Hakuwa na ubinafsi wowote. Alijishughulisha mno na huduma yake hivi kwamba alijinyima mambo ya kawaida ambayo wanadamu wamezoea. “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Yesu alikuwa seremala stadi sana, kwa hiyo angeweza kujijengea nyumba nzuri sana au angeweza kupata pesa kwa kutengeneza na kuuza fanicha maridadi sana. Lakini hakutumia ustadi wake kupata vitu vya kimwili.
7 Andiko la Yohana 19:25-27 lasimulia jambo lenye kugusa moyo sana kuhusu upendo wa Yesu wa kujidhabihu. Fikiria mambo mengi ambayo yalikuwa katika akili na moyo wa Yesu alasiri ambayo angeuawa. Alipokuwa akiteseka kwenye mti wa mateso, aliwafikiria wanafunzi wake, kazi ya kuhubiri, na hasa uaminifu wake na sifa ambayo angeletea jina la Baba yake. Kwa kweli, wakati ujao wa wanadamu wote ulimtegemea! Hata hivyo, muda mfupi tu kabla ya kufa, Yesu alimhangaikia pia mama yake, Maria, ambaye yaelekea alikuwa mjane wakati huo. Yesu alimwomba mtume Yohana amtunze Maria kama mama yake. Kisha mtume Yohana alimchukua Maria na kwenda naye nyumbani. Kwa njia hiyo, Yesu alifanya mipango ili mama yake atunzwe kimwili na kiroho. Alionyesha upendo ulioje usio na ubinafsi!
‘Alisukumwa na Sikitiko’
8. Neno la Kigiriki ambalo linatumiwa na Biblia kufafanua huruma ya Yesu linamaanisha nini?
8 Yesu alikuwa na huruma kama Baba yake. Maandiko yanaonyesha jinsi ambavyo Yesu alijitahidi kuwasaidia watu waliotaabika kwa sababu aliwahurumia sana. Biblia inafafanua huruma ya Yesu kwa kutumia neno la Kigiriki linalotafsiriwa “sukumwa na sikitiko.” Msomi mmoja anasema hivi: ‘Neno hilo linafafanua hisia ya ndani sana ambayo inamchochea mtu kutoka moyoni. Hakuna neno jingine la Kigiriki linalofafanua hisia ya huruma kwa mkazo sana kama neno hilo.’ Ebu ona pindi fulani-fulani ambapo huruma ilimchochea Yesu kutenda.
9, 10. (a) Ni kwa nini Yesu na mitume wake walitafuta mahali pa faragha? (b) Yesu alihisije umati ulipovuruga faragha yake, na kwa nini?
9 Alichochewa kuwasaidia watu kiroho. Simulizi la Marko 6:30-34 laonyesha sababu iliyomfanya Yesu awasikitikie watu. Wazia hali ilivyokuwa. Mitume walifurahi sana baada ya kuhubiri kotekote. Walirudi kwa Yesu na kumsimulia kwa shauku mambo yote waliyoona na kusikia. Lakini umati mkubwa ukakusanyika, na Yesu na mitume wake wakakosa hata nafasi ya kula. Daima akiwa makini, Yesu akafahamu kwamba mitume wamechoka. Akawaambia: “Njoni, nyinyi wenyewe, kwa faragha mwingie katika mahali pa upweke mpumzike kidogo.” Walipanda mashua na kuvuka upande wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya hadi mahali pa faragha. Lakini umati uliwaona wakienda. Wengine walipata habari hizo pia. Watu hao wote walikimbia kuzunguka ufuko wa kaskazini wa bahari hiyo na kufika ng’ambo nyingine kabla ya ile mashua!
10 Je, Yesu alikasirika kwa sababu watu walivuruga faragha yake? La hasha! Alisikitika sana alipoona umati huo wa maelfu ya watu ukimsubiri. Marko aliandika hivi: “Akaona umati mkubwa, lakini akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” Yesu alitambua kwamba watu hao walikuwa na mahitaji ya kiroho. Walikuwa kama kondoo wanaozurura huku na huku bila mchungaji wa kuwaongoza au kuwalinda. Yesu alijua kwamba watu wa kawaida walipuuzwa na viongozi wa kidini ambao badala ya kuwa wachungaji wenye kujali, waliwatendea bila huruma. (Yohana 7:47-49) Aliwasikitikia sana watu, akaanza kuwafundisha “juu ya ufalme wa Mungu.” (Luka 9:11) Ona kwamba Yesu aliwasikitikia watu hata bila kujua jinsi ambavyo wangeitikia mafundisho yake. Yaani, Yesu hakuwahurumia watu kwa sababu tu walikubali mafundisho yake bali aliwafundisha kwa sababu alichochewa na huruma yake nyororo.
“Akanyoosha mkono wake akamgusa”
11, 12. (a) Wenye ukoma walitendewaje nyakati za Biblia, lakini Yesu alitendaje alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma”? (b) Huenda mtu mwenye ukoma aliyeguswa na Yesu alihisije, na kisa halisi cha daktari mmoja kinathibitishaje jambo hilo?
11 Alichochewa kukomesha mateso. Watu wenye magonjwa mbalimbali walivutiwa na Yesu kwa sababu walijua yeye ni mwenye huruma. Jambo hilo lilionekana wazi wakati Yesu huku akifuatwa na umati alipofikiwa na mtu “mwenye kujaa ukoma.” (Luka 5:11, 12) Katika nyakati za Biblia, wenye ukoma walitengwa ili wasiwaambukize wengine. (Hesabu 5:1-4) Lakini baada ya muda, marabi wasio na huruma walikuwa na maoni mabaya kuhusu ukoma, hivyo wakatunga sheria zao wenyewe zenye kukandamiza.a Ingawa hivyo, hebu ona jinsi Yesu alivyomtendea yule mtu mwenye ukoma: “Huko pia mwenye ukoma akaja kwake, akimsihi sana hata kwa kukunja magoti, akimwambia: ‘Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.’ Ndipo akasukumwa na sikitiko, naye akanyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Mimi nataka. Fanywa safi.’ Na mara hiyo ule ukoma ukamtoka.” (Marko 1:40-42) Yesu alijua kwamba mtu huyo mwenye ukoma hakupaswa kuwa miongoni mwa watu. Hata hivyo, badala ya kumfukuza, Yesu alimsikitikia sana hivi kwamba alifanya jambo la kushangaza. Yesu alimgusa!
12 Wafikiri mtu huyo alihisije alipoguswa na Yesu? Kwa mfano, hebu fikiria kisa hiki halisi. Dakt. Paul Brand, mtaalamu wa ukoma, asimulia kuhusu mtu mmoja mwenye ukoma ambaye alimtibu nchini India. Alipokuwa akimpima, daktari huyo alimshika begani na kumweleza kupitia mkalimani matibabu ambayo angepewa. Mtu huyo alianza kulia ghafula. Daktari akamwuliza, “Nimesema jambo baya?” Mkalimani akamwuliza kijana huyo swali hilo katika lugha yake kisha akajibu: “La, daktari. Anasema analia kwa sababu umemshika begani. Hajapata kamwe kuguswa na yeyote kwa miaka mingi isipokuwa wewe.” Yule mtu mwenye ukoma aliyemfikia Yesu alifaidika hata zaidi alipoguswa naye. Baada ya kuguswa mara moja tu, ugonjwa uliomfanya atengwe na watu ulitoweka kabisa!
13, 14. (a) Yesu alikutana na msafara gani alipokaribia jiji la Naini, na kwa nini kisa hicho kilihuzunisha sana? (b) Yesu alichochewaje na huruma kumsaidia yule mjane wa Naini?
13 Alichochewa kuondoa huzuni. Yesu alisikitishwa sana na huzuni ya wengine. Kwa mfano, fikiria simulizi la Luka 7:11-15. Jambo hilo lilitukia alipokuwa anakaribia kumaliza nusu ya huduma yake duniani. Yesu alikuwa amekaribia jiji la Naini huko Galilaya alipokutana na msafara wa mazishi karibu na lango la jiji hilo. Kilikuwa kisa chenye kuhuzunisha sana. Mwana pekee wa mjane mmoja alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba mjane huyo aliwahi kuwa katika msafara mwingine kama huo wakati wa mazishi ya mume wake. Sasa mwanaye ambaye huenda ndiye tu aliyemruzuku alikuwa amekufa. Yaelekea kwamba miongoni mwa umati ulioandamana naye mlikuwa na waombolezaji walioimba nyimbo za maombolezo na wanamuziki waliocheza miziki ya maombolezo. (Yeremia 9:17, 18; Mathayo 9:23) Hata hivyo, Yesu alimtazama sana mama huyo aliyekuwa na majonzi tele, ambaye yaelekea alifuata kwa ukaribu jeneza lililobeba maiti ya mwanaye.
14 Yesu ‘alimsikitikia’ mama huyo. Kwa sauti yenye kutia moyo, akamwambia hivi: “Koma kutoa machozi.” Akalikaribia jeneza na kuligusa. Wale waliokuwa wamelibeba—na labda umati wote—wakasimama tuli. Kwa sauti yenye nguvu, Yesu akamwambia hivi yule maiti: “Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!” Halafu ikawaje? “Huyo mfu akaketi na kuanza kusema” kana kwamba ameamshwa kutoka kwa usingizi mzito! Maneno yanayofuata yanagusa moyo sana: “Naye [Yesu] akampa huyo kwa mama yake.”
15. (a) Masimulizi ya Biblia yanayoeleza jinsi Yesu alivyowasikitikia watu, yanaonyesha kuna uhusiano gani kati ya huruma na matendo? (b) Tunawezaje kumwiga Yesu?
15 Twajifunza nini kutokana na visa hivyo? Katika kila kisa, angalia uhusiano uliopo kati ya huruma na matendo. Sikuzote Yesu aliwahurumia watu waliokuwa wakitaabika, na huruma hiyo ilimchochea kutenda. Tunawezaje kuiga mfano wake? Tukiwa Wakristo, tuna wajibu wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. Upendo wetu kwa Mungu ndio hasa unaotuchochea. Na tukumbuke kwamba kazi ya kuhubiri ni njia ya kuwaonyesha watu huruma. Tukiwahurumia watu kama alivyofanya Yesu, moyo wetu utatuchochea kujitahidi tuwezavyo kuwahubiria habari njema. (Mathayo 22:37-39) Tutawaonyeshaje huruma waamini wenzetu ambao wanateseka au wamefiwa? Hatuwezi kukomesha mateso yao kimuujiza au kufufua wafu. Lakini, tunaweza kuwahurumia kwa matendo kwa kuwaonyesha kwamba tunawajali au kwa kuwapa msaada wanaohitaji.—Waefeso 4:32.
“Baba, Wasamehe”
16. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa tayari kusamehe hata alipokuwa kwenye mti wa mateso?
16 Yesu aliiga kikamili upendo wa Baba yake katika njia nyingine muhimu—alikuwa “tayari kusamehe.” (Zaburi 86:5) Jambo hilo lilionekana wazi hata alipokuwa kwenye mti wa mateso. Yesu alisema nini alipokuwa amepigiliwa misumari mikononi na miguuni, kabla ya kufa kifo cha aibu? Je, alimlilia Yehova awaadhibu wale wanaomwua? La hasha! Kati ya maneno ya mwisho ambayo Yesu alisema ni: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui wanalofanya.”—Luka 23:34.b
17-19. Yesu alionyeshaje kwamba alimsamehe mtume Petro ambaye alikuwa amemkana mara tatu?
17 Labda kisa cha mtume Petro kinaonyesha kwa njia yenye kugusa moyo hata zaidi jinsi Yesu alivyokuwa mwenye kusamehe. Hapana shaka kwamba Petro alimpenda mno Yesu. Mnamo Nisani 14, usiku wa mwisho kabla ya Yesu kuuawa, Petro alimwambia hivi: “Bwana, mimi niko tayari kwenda pamoja nawe kuingia gerezani na pia kuingia katika kifo.” Hata hivyo, saa chache tu baadaye, Petro alikana mara tatu kwamba hata hamjui Yesu! Biblia inatueleza jambo lililotukia Petro alipokuwa akimkana mara ya tatu: “Bwana akageuka akamtazama Petro.” Petro alilemewa na majuto kwa sababu ya dhambi yake, hata ‘akaenda nje na kutoa machozi kwa uchungu.’ Yesu alipokufa baadaye siku hiyo, labda mtume huyo alijiuliza hivi: ‘Je, Bwana wangu alinisamehe?’—Luka 22:33, 61, 62.
18 Punde si punde, Petro alipata jibu. Yesu alifufuliwa asubuhi ya Nisani 16, na yaelekea kwamba alimtembelea Petro siku hiyohiyo. (Luka 24:34; 1 Wakorintho 15:4-8) Kwa nini Yesu alimzingatia mtume huyo ambaye alikuwa amemkana kabisa? Huenda Yesu alitaka kumhakikishia Petro aliyetubu kwamba angali anampenda na kumthamini. Lakini Yesu alimhakikishia jambo hilo kwa njia nyingine pia.
19 Pindi fulani baadaye, Yesu aliwatokea wanafunzi katika Bahari ya Galilaya. Wakati huo, Yesu alimwuliza mara tatu Petro (ambaye alikuwa amemkana Bwana wake mara tatu) iwapo anampenda. Baada ya swali la tatu, Petro alijibu: “Bwana, wewe wajua mambo yote; wewe wajua kwamba mimi nina shauku na wewe.” Bila shaka, Yesu, ambaye angeweza kusoma mioyo, alijua vizuri kwamba Petro alimpenda mno. Hata hivyo, Yesu akampa Petro nafasi ya kuthibitisha kwamba anampenda. Isitoshe, Yesu alimwambia Petro ‘alishe’ na ‘kuchunga kondoo Wake wadogo.’ (Yohana 21:15-17) Hapo awali, Petro alikuwa amepewa kazi ya kuhubiri. (Luka 5:10) Lakini sasa, Yesu alionyesha kwamba alimtumaini kabisa kwa kumpa daraka jingine zito—la kutunza wale ambao wangekuwa wafuasi wa Kristo. Muda mfupi baadaye, Yesu alimpa Petro pendeleo la pekee kuhusiana na utendaji wa wanafunzi. (Matendo 2:1-41) Haikosi Petro alifurahi sana alipojua kwamba Yesu alimsamehe na bado anamtumaini.
Je, ‘Wajua Upendo wa Kristo’?
20, 21. Tunawezaje ‘kuujua kikweli upendo wa Kristo’?
20 Neno la Yehova linaeleza kinaganaga juu ya upendo wa Kristo. Lakini tunapaswa kuuonaje upendo wa Yesu? Biblia inatuhimiza ‘tuujue upendo wa Kristo uzidio ujuzi.’ (Waefeso 3:19) Kama tulivyoona, masimulizi ya Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu yanatufundisha mengi kuhusu upendo wa Kristo. Hata hivyo, ili ‘kuujua kikweli upendo wa Kristo’ haitoshi tu kujifunza mambo ambayo Biblia inasema kumhusu.
21 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘kujua’ linamaanisha “kujua kupitia matendo, kupitia uzoefu.” Tunaweza kufahamu zaidi hisia za Yesu tunapoiga upendo wake kwa kuwatumikia wengine bila ubinafsi, kuwahurumia na kuwasaidia, na kuwasamehe kutoka moyoni. Hivyo, kupitia uzoefu tunapata “kuujua upendo wa Kristo uzidio ujuzi.” Tusisahau kamwe kwamba kadiri tunavyomwiga Kristo, ndivyo tunavyomkaribia Mungu wetu mwenye upendo, Yehova, ambaye Yesu alimwiga kikamili.
a Sheria za marabi zilisema kwamba hakuna yeyote aliyeruhusiwa kusimama umbali wa futi 6 hivi kutoka kwa mwenye ukoma. Lakini kukiwa na upepo, mwenye ukoma alisimama umbali wa futi 150 hivi. Kichapo Midrash Rabbah chataja rabi mmoja ambaye alijificha alipoona wenye ukoma, na rabi mwingine ambaye aliwatupia mawe wenye ukoma ili wasimkaribie. Kwa hiyo wenye ukoma walijua uchungu wa kukataliwa, kudharauliwa na kuchukiwa.
b Hati fulani za kale hazina sehemu ya kwanza ya Luka 23:34. Hata hivyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na tafsiri nyingine nyingi zina maneno hayo kwa sababu yanapatikana kwenye hati nyingi mashuhuri. Ni wazi kwamba Yesu alikuwa akizungumza kuhusu askari Waroma ambao walimtundika mtini. Hawakujua walilokuwa wanafanya, kwa sababu hawakujua Yesu ni nani. Bila shaka, viongozi wa kidini ambao walichochea mauaji hayo walikuwa na hatia kubwa zaidi, kwa sababu walifanya hivyo kimakusudi na kwa nia mbaya. Wengi wao hawangeweza kusamehewa.—Yohana 11:45-53.
-
-
“Endeleeni Kutembea Katika Upendo”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 30
“Endeleeni Kutembea Katika Upendo”
1-3. Tunapata nini tunapomwiga Yehova katika kuonyesha upendo?
‘KUNA furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’ (Matendo 20:35) Maneno hayo ya Yesu yanakazia ukweli huu ulio muhimu sana: Upendo usio na ubinafsi unathawabisha. Ingawa kuna furaha nyingi kuonyeshwa upendo, kuna furaha nyingi hata zaidi kuwaonyesha wengine upendo.
2 Hakuna anayeelewa jambo hilo vizuri kama Baba yetu wa mbinguni. Kama tulivyoona katika sura zilizotangulia za sehemu hii, Yehova hana kifani katika kuonyesha upendo. Yehova ameonyesha upendo kwa njia za pekee sana na kwa muda mrefu kuliko mtu yeyote. Ndiyo sababu Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11.
3 Mungu wetu mwenye upendo anataka tujitahidi kumwiga, hasa katika kuonyesha upendo. Andiko la Waefeso 5:1, 2 latuambia hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.” Tunapomwiga Yehova katika kuonyesha upendo, tunapata furaha zaidi ya kutoa. Tunaridhika pia kujua kwamba tunampendeza Yehova, kwa sababu Neno lake linatuhimiza ‘tupendane.’ (Waroma 13:8) Lakini kuna sababu nyingine za kutufanya ‘tuendelee kutembea katika njia ya upendo.’
Kwa Nini Upendo Ni Muhimu?
4, 5. Kwa nini ni muhimu tuwaonyeshe waamini wenzetu upendo wa kujidhabihu?
4 Kwa nini ni muhimu tuwapende waamini wenzetu? Kwa ufupi, upendo ndio msingi wa Ukristo wa kweli. Hatuwezi kuwa na uhusiano mzuri na Wakristo wenzetu iwapo hatuwapendi, na jambo baya hata zaidi ni kwamba bila upendo tunakuwa bure machoni pa Yehova. Fikiria jinsi ambavyo Neno la Mungu linakazia ukweli huo.
5 Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake usiku wa mwisho wa maisha yake duniani: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane. Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Usemi “kama vile nimewapenda nyinyi” unatuamuru tuwe na upendo kama wa Yesu. Katika Sura ya 29, tuliona kwamba Yesu alikuwa mfano bora katika kuonyesha upendo wa kujidhabihu, akitanguliza masilahi ya wengine. Ni lazima pia tupendane bila ubinafsi. Wale ambao si washiriki wa kutaniko la Kikristo wanahitaji kuona kwamba tunapendana kikweli. Kwa kweli, upendo wa kidugu wa kujidhabihu unatutambulisha kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo.
6, 7. (a) Twajuaje kwamba Neno la Yehova linakazia sana umuhimu wa kuonyesha upendo? (b) Maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 13:4-8 yanakazia nini kuhusu upendo?
6 Vipi ikiwa hatuna upendo? Mtume Paulo alisema kwamba ikiwa “sina upendo, nimekuwa kipande cha shaba-nyeupe inayovuma au toazi lenye kulia.” (1 Wakorintho 13:1) Toazi hulia kwa sauti kali sana. Kipande cha shaba-nyeupe huvumaje? Tafsiri nyingine zinasema “sauti ya kengele yenye kelele” au “kengele inayolia-lia.” Mifano hiyo inafaa sana. Mtu asiye na upendo ni kama ala ya muziki inayolia kwa sauti kubwa yenye kuchukiza inayofukuza watu badala ya kuwavutia. Je, mtu kama huyo anaweza kweli kuwa na uhusiano mzuri na wengine? Paulo alisema hivi pia: “Ikiwa nina imani yote ili kung’oa na kuhamisha milima, lakini sina upendo, mimi si kitu.” (1 Wakorintho 13:2) Hebu wazia, mtu asiye na upendo “ni bure kabisa,” hata akifanya nini! (The Amplified Bible) Je, hilo halionyeshi kwamba Neno la Yehova linakazia sana umuhimu wa kuonyesha upendo?
7 Lakini tutaonyeshaje sifa hiyo tunaposhughulika na wengine? Tujibu swali hilo kwa kuchanganua maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 13:4-8. Mistari hii haikazii jinsi Mungu anavyotupenda au jinsi tunavyompenda Mungu. Badala yake, Paulo alikazia jinsi sisi tunavyoweza kupendana. Alieleza mambo fulani kuhusu jinsi upendo ulivyo na jinsi usivyo.
Jinsi Upendo Ulivyo
8. Ustahimilivu unawezaje kutusaidia tunaposhughulika na wengine?
8 “Upendo ni wenye ustahimilivu.” Kustahimili ni kuwavumilia wengine kwa subira. (Wakolosai 3:13) Tunahitaji kuwa na subira, sivyo? Kwa sababu ya kufanya kazi bega kwa bega katika hali yetu ya kutokamilika, ni kawaida kwamba mara kwa mara huenda tukakosewa au tukawakosea ndugu zetu Wakristo. Lakini subira na ustahimilivu unaweza kutusaidia kuvumilia na kutovuruga amani ya kutaniko tunapokosana au kuhitilafiana na wengine kwa sababu ya mambo madogo-madogo.
9. Tunawezaje kuwaonyesha wengine fadhili?
9 ‘Upendo ni wenye fadhili.’ Fadhili huonyeshwa kwa kuwasaidia wengine na kuzungumza nao kwa njia yenye kujali. Upendo hutuchochea kutafuta fursa za kuwaonyesha wengine fadhili, hasa wale wanaohitaji sana msaada. Kwa mfano, huenda mwamini mwenzetu ambaye ni mzee kwa umri ni mpweke na anahitaji kutembelewa na kutiwa moyo. Huenda mama asiye na mume au dada anayeishi katika familia ambayo imegawanyika kidini anahitaji msaada fulani. Huenda mgonjwa fulani au mtu aliyepata msiba anahitaji kutiwa moyo kwa fadhili na rafiki mwaminifu. (Mithali 12:25; 17:17) Tunapochukua hatua ya kuonyesha fadhili kwa njia kama hizo, tunathibitisha kwamba upendo wetu ni halisi.—2 Wakorintho 8:8.
10. Upendo unatusaidiaje kutetea na kusema kweli, hata wakati ambapo si rahisi kufanya hivyo?
10 ‘Upendo hushangilia pamoja na kweli.’ Tafsiri nyingine inasema: “Upendo . . . huunga mkono ukweli kwa shangwe.” Upendo unatuchochea kutetea kweli na ‘kusema kweli na jirani yetu.’ (Zekaria 8:16) Kwa mfano, ikiwa mtu tunayempenda amefanya dhambi nzito, upendo kwa Yehova na kwa yule aliyefanya dhambi, utatusaidia tushikamane na kanuni za Mungu badala ya kujaribu kuficha, kutoa udhuru au hata kusema uwongo kuhusu dhambi yake. Ni kweli kwamba huenda isiwe rahisi kukubali amefanya dhambi. Lakini ikiwa tunamjali kikweli mpendwa wetu, tungetaka akubali na kunufaika na nidhamu ya upendo kutoka kwa Mungu. (Mithali 3:11, 12) Tukiwa Wakristo wenye upendo, tunataka pia “kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.”—Waebrania 13:18.
11. Kwa sababu upendo “huhimili mambo yote,” tunapaswa kujitahidi kufanya nini kuhusu kasoro za waamini wenzetu?
11 ‘Upendo huhimili mambo yote.’ Usemi huo unamaanisha kihalisi kwamba upendo “unafunika mambo yote.” (Kingdom Interlinear) Andiko la 1 Petro 4:8 lasema: “Upendo hufunika wingi wa dhambi.” Naam, Mkristo ambaye anaongozwa na upendo hakimbilii kutangaza kasoro na mapungufu ya ndugu zake Wakristo. Mara nyingi, makosa na kasoro za waamini wenzetu huwa ndogo-ndogo mno na zinaweza kufunikwa na upendo.—Mithali 10:12; 17:9.
Upendo hutuchochea tuwaamini ndugu zetu
12. Mtume Paulo alionyeshaje aliamini kwamba Filemoni angetenda ifaavyo, na mfano wa Paulo unatufunza nini?
12 ‘Upendo huamini mambo yote.’ Tafsiri ya Moffat inasema kwamba upendo “sikuzote hujitahidi kuamini mambo mazuri.” Hatuwashuku isivyofaa waamini wenzetu na kutilia shaka kila jambo wanalofanya. Upendo unatusaidia “kuamini mambo mazuri” kuhusu ndugu zetu na kuwatumaini.a Fikiria mfano unaotajwa katika barua ya Paulo kwa Filemoni. Paulo alimwandikia Filemoni ili kumtia moyo amkaribishe kwa fadhili Onesimo yule mtumwa mtoro, ambaye sasa alikuwa Mkristo. Paulo alimsihi Filemoni kwa upendo badala ya kujaribu kumlazimisha. Aliamini kwamba Filemoni angetenda ifaavyo, kwa kusema: “Nikiitibari ukubalifu wako wa kufuata agizo, ninakuandikia wewe, nikijua utafanya hata zaidi ya mambo nisemayo.” (Mstari wa 21) Upendo unapotuchochea kuwaamini ndugu zetu, tunawatia moyo kufanya yote wawezayo.
13. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawatakia ndugu zetu mema?
13 ‘Upendo hutumaini mambo yote.’ Mbali na kuamini, upendo hutumaini mambo yote. Kwa upendo, tunawatakia mema ndugu zetu. Kwa mfano, ndugu ‘akichukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua,’ tunatumaini kwamba atakubali jitihada za upendo za kumrekebisha. (Wagalatia 6:1) Tunatumaini pia kwamba wale walio dhaifu katika imani watapata nguvu tena. Kwa subira, tunawasaidia tuwezavyo wawe na imani yenye nguvu. (Waroma 15:1; 1 Wathesalonike 5:14) Hata mpendwa wetu akiacha njia ya kweli, bado tunatumaini kwamba siku moja atarudiwa na fahamu na kumrudia Yehova, kama yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu.—Luka 15:17, 18.
14. Uvumilivu wetu unaweza kujaribiwa jinsi gani kutanikoni, na upendo utatusaidia tutendeje?
14 ‘Upendo huvumilia mambo yote.’ Uvumilivu hutuwezesha kubaki imara tunapokabili magumu au mambo yanayovunja moyo. Majaribu ya uvumilivu hayatokani tu na mambo yaliyo nje ya kutaniko. Nyakati nyingine, uvumilivu wetu unajaribiwa kutanikoni. Ndugu zetu wanaweza kutuvunja moyo nyakati nyingine kwa sababu ya kutokamilika. Tunaweza kuumizwa na mtu anayenena bila kufikiri. (Mithali 12:18) Labda jambo fulani kutanikoni halishughulikiwi jinsi tunavyotarajia. Ndugu fulani anayeheshimiwa anaweza kutuudhi, na kutufanya tujiulize, ‘Mkristo anawezaje kufanya hivyo?’ Tunapokabili hali kama hizo, je, tutajitenga na kutaniko na kuacha kumtumikia Yehova? Hatuwezi kufanya hivyo ikiwa tuna upendo! Naam, tukiwa na upendo hatuwezi kukazia tu kasoro za ndugu yetu na kukosa kuona sifa yoyote nzuri aliyo nayo au kukosa kuona uzuri wowote wa kutaniko. Upendo unatusaidia kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu na kuunga mkono kutaniko bila kujali mwanadamu mwingine asiyekamilika anasemaje au anatendaje.—Zaburi 119:165.
Jinsi Upendo Usivyo
15. Wivu usiofaa ni nini, na upendo unatusaidiaje kuepuka hisia hii hatari?
15 “Upendo hauna wivu.” Wivu usiofaa unaweza kutufanya tuwaonee wengine kijicho kwa sababu ya vitu walivyo navyo—mali zao, mapendeleo yao, au vipawa vyao. Wivu huo ni hisia hatari sana ya ubinafsi ambayo inaweza kuvuruga amani ya kutaniko isipodhibitiwa. Ni nini kitakachotusaidia tukinze “mwelekeo wa kuhusudu”? (Yakobo 4:5) Ni upendo. Sifa hiyo muhimu sana itatufanya tushangilie pamoja na wale ambao wana mapendeleo fulani ambayo hatuna. (Waroma 12:15) Upendo hutuzuia kukasirika mtu fulani anapopongezwa kwa sababu ya kuwa na kipawa fulani cha pekee au kwa kutimiza jambo fulani kubwa.
16. Ikiwa tunawapenda ndugu zetu kikweli, kwa nini tunapaswa kuepuka kujigamba kwa sababu ya mapendeleo yetu katika utumishi wa Yehova?
16 ‘Upendo haujigambi, haujitutumui.’ Upendo hutuzuia kujigamba kwa sababu ya vipawa vyetu au mafanikio yetu. Ikiwa tunawapenda ndugu zetu kikweli, je, tutajigamba daima kwa sababu ya mafanikio yetu katika huduma au kwa sababu ya mapendeleo yetu kutanikoni? Kujigamba kwa njia hiyo kunaweza kuwavunja wengine moyo, na kuwafanya wajione hawafai. Upendo hutuzuia kujigamba kwa sababu ya mapendeleo ya utumishi ambayo Mungu ametupatia. (1 Wakorintho 3:5-9) Zaidi ya hayo, upendo “haujitutumui,” au kama tafsiri moja inavyosema ‘haujioni kuwa bora.’ Upendo hutuzuia kujiona kuwa bora.—Waroma 12:3.
17. Upendo hutuchochea kuwajali wengine kwa njia gani, na hivyo tutaepuka mwenendo wa aina gani?
17 ‘Upendo haujiendeshi bila adabu.’ Mtu asiye na adabu anatenda kwa njia mbaya sana au yenye kuudhi. Mtu anayejiendesha hivyo hana upendo kwa sababu hajali hisia na hali njema ya wengine. Kinyume chake, upendo ni wenye fadhili na unatuchochea kuwajali wengine. Tukiwa na upendo tutakuwa na adabu, tutajiendesha kwa njia inayompendeza Mungu, na tutawaheshimu waamini wenzetu. Kwa hiyo, tukiwa na upendo tutaepuka “mwenendo wa aibu,” au tabia yoyote ile ambayo itawashtua au kuwaudhi ndugu zetu Wakristo.—Waefeso 5:3, 4.
18. Kwa nini mtu mwenye upendo hasisitizi kila jambo lifanywe jinsi anavyopenda?
18 ‘Upendo hautafuti masilahi yao wenyewe.’ Tafsiri nyingine inasema hivi: “Upendo hausisitizi kufuata njia yake.” Mtu mwenye upendo hasisitizi kila jambo lifanywe jinsi anavyopenda, kana kwamba maoni yake ni sawa sikuzote. Hawashawishi wengine ili kuwashurutisha wenye maoni tofauti wafuate maoni yake. Ukaidi wa aina hiyo unaonyesha kwamba ana kiasi fulani cha kiburi, na Biblia inasema: “Kiburi hutangulia uangamivu.” (Mithali 16:18) Ikiwa tunawapenda kikweli ndugu zetu, tutaheshimu maoni yao, na tutakuwa tayari kuyakubali inapowezekana. Maneno haya ya Paulo yanatutia moyo kuwa na roho hiyo: “Acheni kila mmoja afulize kutafuta sana, si faida yake mwenyewe, bali ya mtu yule mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.
19. Upendo unatusaidia tutendeje tunapokosewa na wengine?
19 ‘Upendo hauchokozeki, hauweki hesabu ya ubaya.’ Upendo haukasirishwi ovyoovyo na mambo ambayo wengine wanasema au kufanya. Ni jambo la kawaida kukasirika tunapokosewa. Lakini hata tukiwa na sababu nzuri ya kukasirika, hatutaendelea kuchokozeka ikiwa tuna upendo. (Waefeso 4:26, 27) Hatutaweka hesabu ya maneno au matendo yenye kuumiza kana kwamba tunayaandika katika kitabu ili tusiyasahau. Badala yake, upendo unatuchochea kumwiga Mungu wetu mwenye upendo. Kama tulivyoona katika Sura ya 26, Yehova husamehe kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Yeye husamehe na kusahau, yaani, hatuadhibu baadaye kwa sababu ya dhambi hizo. Je, hatushukuru kwamba Yehova haweki hesabu ya ubaya?
20. Tunapaswa kuhisije mwamini mwenzetu anapotenda dhambi na kupata madhara?
20 ‘Upendo haushangilii ukosefu wa uadilifu.’ Tafsiri nyingine inasema: “Upendo . . . haushangilii dhambi za wengine.” Tafsiri ya Moffat yasema: “Upendo haufurahii kamwe wengine wanapokosea.” Upendo haufurahii uovu, kwa hiyo tunakataa kabisa ukosefu wowote wa adili. Tunahisije mwamini mwenzetu anapotenda dhambi na kupata madhara? Tukiwa na upendo hatutashangilia kana kwamba tunasema, ‘Shauri yake! Asiyesikia la mkuu huvunjika guu!’ (Mithali 17:5) Hata hivyo, tunashangilia ndugu aliyetenda dhambi anapochukua hatua zifaazo za kujirekebisha na kufanya maendeleo ya kiroho.
“Njia Izidiyo”
21-23. (a) Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba “upendo haushindwi kamwe”? (b) Tutazungumzia nini katika sura ya mwisho?
21 “Upendo haushindwi kamwe.” Paulo alimaanisha nini aliposema hivyo? Muktadha unaonyesha kwamba alikuwa anazungumzia zawadi za roho za Wakristo wa mapema. Zawadi hizo zilithibitisha kwamba Mungu aliunga mkono kutaniko hilo jipya. Lakini si Wakristo wote wangeweza kuponya, kutoa unabii, au kuzungumza kwa lugha mbalimbali. Hata hivyo, hilo halikuwa muhimu; mwishowe zawadi hizo zote zingekoma. Lakini sifa fulani haingekoma, sifa ambayo kila Mkristo angeweza kukuza. Sifa yenye kutokeza sana, na yenye kudumu kuliko zawadi yoyote ya kimuujiza. Paulo aliiita sifa hiyo “njia izidiyo.” (1 Wakorintho 12:31) ‘Njia hiyo izidiyo’ ni gani? Ni njia ya upendo.
Watu wa Yehova wanajulikana kwa sababu ya jinsi wanavyopendana
22 Upendo wa Kikristo ambao Paulo alizungumzia “haushindwi kamwe,” yaani, hautafikia kikomo. Hadi leo, upendo wa kidugu wa kujidhabihu unawatambulisha wafuasi wa kweli wa Kristo. Je, hatuoni upendo huo katika makutaniko ya waabudu wa Yehova duniani kote? Upendo huo utadumu milele, kwa sababu Yehova anawaahidi watumishi wake waaminifu uhai wa milele. (Zaburi 37:9-11, 29) Na tujitahidi tuwezavyo ‘kuendelea kutembea katika upendo.’ Tukifanya hivyo, tunaweza kupata furaha nyingi sana ya kutoa. Isitoshe, tunaweza kuendelea kuishi—naam, kuendelea kupenda—milele na milele kama Mungu wetu mwenye upendo, Yehova.
23 Katika sura hii inayomalizia sehemu ya upendo, tumezungumzia jinsi tunavyoweza kupendana. Kwa kuwa tunafaidika kwa njia nyingi kutokana na upendo wa Yehova—na vilevile kutokana na nguvu, haki, na hekima yake—twapaswa kujiuliza hivi, ‘Nitamthibitishiaje Yehova kwamba kwa kweli nampenda?’ Swali hilo litazungumziwa katika sura ya mwisho.
a Bila shaka, upendo wa Kikristo si wa kijinga. Biblia inatuhimiza hivi: “Mfulize kuangalia wale wasababishao migawanyiko na sababu za kukwaza . . . , na mwaepuke.”—Waroma 16:17.
-
-
“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 31
“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”
1-3. (a) Tunaweza kujifunza nini kuhusu wanadamu tunapofikiria uhusiano uliopo kati ya wazazi na mtoto wao? (b) Kwa kawaida sisi hutendaje tunapopendwa na mtu fulani, na ni swali gani muhimu tunaloweza kujiuliza?
WAZAZI hufurahi sana kumwona mtoto wao mchanga akitabasamu. Kwa kawaida wao humkaribia mtoto huyo, wakichekacheka na kutabasamu kwa hisia. Wana hamu ya kumwona akitabasamu pia. Na muda si muda, mtoto anaanza kutabasamu kwa shauku nyingi. Ni kana kwamba tabasamu hiyo inaonyesha upendo kwa njia fulani ya pekee. Ndivyo mtoto anavyoitikia upendo anaoonyeshwa na wazazi wake.
2 Tabasamu ya mtoto mchanga inatukumbusha jambo fulani muhimu kuhusu wanadamu. Kwa kawaida, sisi huonyesha upendo tunapoonyeshwa upendo. Tumeumbwa kwa njia hiyo. (Zaburi 22:9) Kadiri tunavyokua, ndivyo tunavyoweza kuonyesha upendo zaidi. Labda unakumbuka jinsi ambavyo wazazi wako, watu wa ukoo, au marafiki walivyokupenda ulipokuwa mtoto mchanga. Upendo huo mchangamfu ulianza kukua moyoni mwako na ulikuchochea kutenda. Ukaanza kuwapenda pia. Je, ndivyo uhusiano wako na Yehova Mungu ulivyo?
3 Biblia yasema hivi: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.” (1 Yohana 4:19) Sehemu ya 1 hadi ya 3 ya kitabu hiki ilikukumbusha kwamba Yehova Mungu ametumia nguvu zake, haki yake, na hekima yake kwa njia za upendo na kwa faida yako. Katika Sehemu ya 4 ulijifunza jinsi ambavyo ameonyesha waziwazi kwamba anakupenda na kuwapenda wanadamu wote kwa njia za pekee sana. Lakini swali lazuka na huenda likawa ndilo swali muhimu zaidi unaloweza kujiuliza: ‘Nitaonyeshaje kwamba nathamini upendo wa Yehova?’
Kumpenda Mungu Kwamaanisha Nini?
4. Watu wametatanikaje kuhusu maana ya kumpenda Mungu?
4 Yehova, aliye Chanzo cha upendo, anajua vizuri kwamba upendo una nguvu za kuwachochea wengine wafanye yote wawezayo. Kwa hiyo, licha ya kwamba wanadamu wameendelea kumwasi, ana hakika kwamba baadhi yao watampenda. Na kwa kweli, mamilioni wamefanya hivyo. Hata hivyo, inasikitisha kwamba dini za ulimwengu huu mwovu zimewatatanisha watu kiasi cha kwamba hawajui maana ya kumpenda Mungu. Watu wengi husema wanampenda Mungu, lakini wanafikiri kwamba upendo ni hisia inayoonyeshwa tu kwa maneno. Kuhisi hivyo kwaweza kuwa hatua ya kwanza ya kumpenda Mungu, kama vile mtoto mchanga anavyoanza kuwaonyesha wazazi wake upendo kwa kutabasamu. Hata hivyo, upendo wa watu wazima unatia ndani mambo mengi zaidi.
5. Biblia inafafanuaje kumpenda Mungu, na kwa nini ufafanuzi huo unatuvutia?
5 Yehova anatueleza maana ya kumpenda. Neno lake lasema: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake.” Basi, tunahitaji kuonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa matendo. Ni kweli kwamba watu wengi hawapendi kutii. Lakini mstari huohuo wasema hivi kwa fadhili: “Na bado amri zake [za Mungu] si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Sheria na kanuni za Yehova zinakusudiwa kutufaidi wala si kutukandamiza. (Isaya 48:17, 18) Neno la Mungu lina kanuni nyingi sana ambazo zinatusaidia kumkaribia. Jinsi gani? Hebu tuzungumzie mambo matatu yanayohusu uhusiano wetu na Mungu. Mambo hayo ni: kuwasiliana naye, kumwabudu, na kumwiga.
Kuwasiliana na Yehova
6-8. (a) Tunaweza kumsikilizaje Yehova? (b) Twawezaje kusoma Maandiko kana kwamba tunaona matukio halisi?
6 Swali hili liliulizwa mwanzoni mwa Sura ya 1, “Je, waweza kuwazia ukizungumza na Mungu?” Tuliona kwamba hiyo si ndoto tu. Musa alizungumza na Mungu. Vipi sisi? Huu si wakati wa Yehova kutuma malaika wake ili wazungumze na wanadamu. Lakini Yehova anawasiliana nasi leo kwa njia bora sana. Tunaweza kumsikilizaje Yehova?
7 Kwa kuwa “andiko lote limepuliziwa na Mungu,” tunamsikiliza Yehova kwa kusoma Neno lake, Biblia. (2 Timotheo 3:16) Ndiyo sababu Mfalme Daudi aliwahimiza watumishi wa Yehova wasome Neno hilo “mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Ni lazima tujitahidi sana kufanya hivyo. Lakini jitihada hizo zina faida. Kama tulivyoona katika Sura ya 18, Biblia ni kama barua muhimu kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Kwa hiyo hatupaswi kuisoma tu kidesturi. Twapaswa kusoma Maandiko kana kwamba tunaona matukio halisi. Jinsi gani?
8 Piga picha akilini unaposoma masimulizi ya Biblia. Jaribu kuwazia watu wanaotajwa. Jaribu kufahamu malezi yao, hali zao, na nia zao. Kisha, tafakari yale unayosoma, jiulize maswali kama haya: ‘Simulizi hili linanifundisha nini kumhusu Yehova? Linakazia sifa gani ya Yehova? Yehova anataka nijifunze kanuni gani, na ninawezaje kuitumia maishani mwangu?’ Neno la Mungu litakufaidi ukilisoma, ukilitafakari, na kulitumia maishani.—Zaburi 77:12; Yakobo 1:23-25.
9. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ni nani, na kwa nini tunapaswa kumsikiliza kwa makini “mtumwa” huyo?
9 Pia Yehova anazungumza nasi kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Kama Yesu alivyotabiri, kikundi kidogo cha wanaume Wakristo watiwa-mafuta kimewekwa rasmi ili kitoe ‘chakula [cha kiroho] kwa wakati ufaao’ katika hizi siku za mwisho zenye magumu. (Mathayo 24:45-47) Tunaposoma vichapo ambavyo vinakusudiwa kutusaidia kupata ujuzi sahihi wa Biblia, na tunapohudhuria mikutano ya Kikristo na makusanyiko, tunalishwa kiroho na mtumwa huyo. Kwa kuwa yeye ni mtumwa wa Kristo, tunatii kwa hekima maneno haya ya Yesu: “Kazieni uangalifu jinsi msikilizavyo.” (Luka 8:18) Tunasikiliza kwa makini kwa sababu tunatambua kwamba njia moja ambayo Yehova hutumia kuwasiliana nasi ni kupitia mtumwa huyo mwaminifu.
10-12. (a) Kwa nini sala ni zawadi bora kutoka kwa Yehova? (b) Tunawezaje kusali kwa njia inayomfurahisha Yehova, na kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba anathamini sala zetu?
10 Lakini vipi kuhusu kuwasiliana na Mungu? Je, tunaweza kuzungumza na Yehova? Ni wazo lenye kutia kicho. Je, ni rahisi kumfikia mtawala mwenye nguvu katika nchi yenu ili umwambie matatizo yako? Nyakati nyingine, inaweza kuwa hatari sana kujaribu kufanya hivyo! Katika siku za Esta na Mordekai, mtu ambaye angeenda kumtembelea mfalme wa Uajemi bila mwaliko rasmi angeuawa. (Esta 4:10, 11) Sasa wazia kumfikia Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu mzima, ambaye ni mkuu hivi kwamba wanadamu wenye mamlaka zaidi “huwa kama panzi” wanapolinganishwa naye. (Isaya 40:22) Je, tuogope kumfikia? La hasha!
11 Yehova ameandaa njia rahisi ya kumfikia—sala. Hata mtoto mchanga anaweza kusali kwa Yehova kwa imani, katika jina la Yesu. (Yohana 14:6; Waebrania 11:6) Isitoshe, sala inatuwezesha kueleza mawazo na hisia zetu za ndani sana—hata zile zenye kuumiza ambazo tunashindwa kutamka. (Waroma 8:26) Hakuna haja ya kujaribu kumfurahisha Yehova kwa kutoa sala zenye ufasaha na zenye madoido au sala ndefu-ndefu zenye maneno mengi. (Mathayo 6:7, 8) Kwa upande mwingine, Yehova hatuwekei muda wa kusali au mara ambazo tunaweza kufanya hivyo. Neno lake linatusihi ‘tusali bila kukoma.’—1 Wathesalonike 5:17.
12 Kumbuka kwamba ni Yehova peke yake anayeitwa “Msikiaji wa Sala,” naye husikiliza kwa hisia-mwenzi kabisa. (Zaburi 65:2, NW) Je, yeye hustahimili tu sala za watumishi wake waaminifu? La, sala zao zinamfurahisha. Neno lake linalinganisha sala hizo na uvumba ambao ukichomwa, moshi wake wenye manukato hupaa juu. (Zaburi 141:2; Ufunuo 5:8; 8:4) Bila shaka inafariji sana kujua kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu husikiliza na kufurahia sala zetu za kutoka moyoni ambazo ni kama uvumba, sivyo? Kwa hiyo, ikiwa unataka kumkaribia Yehova, sali kwa unyenyekevu mara nyingi kila siku. Mwambie mambo yote yaliyo moyoni mwako; mfunulie yote. (Zaburi 62:8) Mwambie Baba yako wa mbinguni mahangaiko yako, shangwe zako, na umshukuru na kumsifu. Ukifanya hivyo uhusiano wako naye utazidi kuimarika.
Kumwabudu Yehova
13, 14. Kumwabudu Yehova kwamaanisha nini, na kwa nini tunapaswa kumwabudu?
13 Tunapowasiliana na Yehova Mungu, hatumsikilizi na kuzungumza naye kama tunavyozungumza na rafiki au mtu wetu wa ukoo. Kwa kweli, tunamwabudu Yehova na kumpa staha yenye kicho ambayo anastahili kabisa. Maisha yetu yote yanaongozwa na ibada ya kweli. Kwa njia hiyo tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na tunamtumikia kwa nafsi yetu yote. Ibada ya kweli inawaunganisha viumbe wote wa Yehova ambao ni waaminifu, ama mbinguni au duniani. Katika ono, mtume Yohana alimsikia malaika akitangaza amri hii: “Mwabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na mabubujiko ya maji.”—Ufunuo 14:7.
14 Kwa nini tumwabudu Yehova? Hebu fikiria sifa ambazo tumezungumzia, kama vile utakatifu, nguvu, kujidhibiti, haki, ujasiri, rehema, hekima, unyenyekevu, upendo, huruma, uaminifu-mshikamanifu, na wema. Tumeona kwamba Yehova ndiye mfano bora kabisa, na hana kifani katika kuonyesha kila sifa inayopendeza. Tunapojaribu kuelewa sifa zote za Mungu, tunatambua kwamba yeye ni mkuu zaidi, anastahili sifa zote, ni mtukufu ajabu, na yuko juu sana kuliko sisi. (Isaya 55:9) Hapana shaka kwamba Yehova ana haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu, naye anastahili ibada yetu. Lakini tunapaswa kumwabuduje?
15. Tunawezaje kumwabudu Yehova “kwa roho na kweli,” na mikutano ya Kikristo hutupatia fursa ya kufanya nini?
15 Yesu alisema: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Hiyo yamaanisha kumwabudu Yehova kwa moyo uliojaa imani na upendo, na kuongozwa na roho yake. Yamaanisha pia kumwabudu kupatana na kweli na ujuzi sahihi ulio katika Neno la Mungu. Tunapokutana na waabudu wenzetu, tunapata fursa ya kumwabudu Yehova “kwa roho na kweli.” (Waebrania 10:24, 25) Tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova katika ibada safi tunapomsifu kwa nyimbo, tunaposali kwake kwa umoja, tunaposikiliza na kushiriki mazungumzo ya Neno lake.
Mikutano ya Kikristo ni pindi zenye kupendeza za kumwabudu Yehova
16. Ni amri gani iliyo kati ya amri kuu zaidi ambazo Wakristo wa kweli wanapaswa kutii, ni nini kinachotuchochea kutii amri hiyo?
16 Tunamwabudu Yehova pia tunapowaambia wengine juu yake, tukimsifu hadharani. (Waebrania 13:15) Kwa kweli, kuhubiri habari njema za Ufalme wa Yehova ni kati ya amri kuu zaidi ambazo Wakristo wa kweli wanapaswa kutii. (Mathayo 24:14) Tunatii kwa moyo wetu wote kwa sababu tunampenda Yehova. Tunapofikiria jinsi ambavyo “mungu wa huu mfumo wa mambo,” Shetani Ibilisi, “amepofusha akili za wasioamini,” na kusambaza uwongo kumhusu Yehova, je, hilo halituchochei tuazimie kuwa Mashahidi wa Mungu wetu, na kukomesha uchongezi huo? (2 Wakorintho 4:4; Isaya 43:10-12) Na tunapotafakari sifa nzuri sana za Yehova, je, hatuchochewi kuwaambia wengine juu yake? Kwa kweli, hakuna pendeleo linaloweza kulinganishwa na pendeleo la kuwasaidia wengine wamjue na kumpenda Baba yetu wa mbinguni kama tunavyofanya.
17. Kumwabudu Yehova kunahusisha nini, na kwa nini ni lazima tumwabudu kwa uaminifu?
17 Kumwabudu Yehova kunahusisha mambo mengi zaidi. Kunahusisha kila jambo tunalofanya maishani. (Wakolosai 3:23) Tukimkubali kikweli Yehova awe Bwana wetu Mwenye Enzi Kuu, basi tutajitahidi kufanya mapenzi yake katika kila jambo—katika maisha yetu ya familia, kazini, jinsi tunavyowatendea wengine, na hata tunapostarehe. Tutajitahidi kumtumikia Yehova “kwa moyo mkamilifu,” na kwa uaminifu. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Hatuwezi kumwabudu Yehova kwa moyo nusunusu au huku tunaishi maisha maradufu—yaani, tunajifanya kwa unafiki kwamba tunamtumikia Yehova na huku tunatenda dhambi nzito kisiri-siri. Watu waaminifu si wanafiki; anayempenda Mungu anachukia kabisa unafiki. Kumhofu Mungu kunasaidia pia. Biblia inaonyesha kwamba tutakuwa na uhusiano mzuri na Yehova tukiwa na hofu hiyo yenye kicho.—Zaburi 25:14.
Kumwiga Yehova
18, 19. Kwa nini si kosa kufikiri kwamba wanadamu wasiokamilika wanaweza kumwiga Yehova Mungu?
18 Sura ya mwisho katika kila sehemu ya kitabu hiki inaonyesha jinsi ya ‘kumwiga Mungu, tukiwa watoto wapendwa.’ (Waefeso 5:1) Ni muhimu kukumbuka kwamba ingawa hatujakamilika, tunaweza kuiga jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake, haki yake, jinsi anavyotenda kwa hekima, na kuonyesha upendo. Tunajuaje kwamba kwa kweli tunaweza kumwiga Mweza Yote? Kumbuka kwamba jina Yehova linatufundisha kwamba yeye hujisababisha kuwa chochote atakacho ili atimize makusudi yake. Bila shaka uwezo huo unatutia kicho, lakini je, tunaweza kweli kumwiga Yehova? Bila shaka tunaweza.
19 Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:26) Kwa hiyo, wanadamu ni tofauti kabisa na viumbe wote duniani. Hatuongozwi tu na silika, sifa tulizorithi, au mazingira yetu. Yehova ametupatia zawadi nzuri sana—uhuru wa kuchagua. Licha ya udhaifu wetu na kutokamilika, tuna uhuru wa kuchagua tunavyotaka kuwa. Je, ungependa kuwa mtu mwenye upendo, hekima na haki, anayetumia uwezo wake ifaavyo? Roho ya Yehova inaweza kukusaidia kuwa na sifa hizo zote! Hebu fikiria mambo unayoweza kutimiza ukiwa na sifa hizo.
20. Tunatimiza mambo gani mazuri tunapomwiga Yehova?
20 Utampendeza Baba yako wa mbinguni na kuufurahisha moyo wake. (Mithali 27:11) Hata unaweza ‘kumpendeza Yehova kikamili,’ kwa sababu anajua udhaifu wako. (Wakolosai 1:9, 10) Utapata pendeleo la pekee sana unapoendelea kukuza sifa nzuri kama za Baba yako mpendwa. Utawaangazia watu nuru katika ulimwengu huu ulio gizani na uliotengwa na Mungu. (Mathayo 5:1, 2, 14) Utasaidia kutangaza duniani pote sifa za utu wa Yehova wenye utukufu. Ni heshima iliyoje!
“Mkaribieni Mungu, Naye Atawakaribia”
Na uzidi kumkaribia Yehova daima
21, 22. Wale wanaompenda Yehova watakuwa na mradi gani usio na mwisho?
21 Himizo rahisi lililo katika Yakobo 4:8 halitimizwi mara moja. Ni mradi usio na mwisho. Tutaendelea kumkaribia Yehova maadamu tunadumisha uaminifu wetu. Tutazidi kumkaribia Yehova daima kwa sababu sikuzote tutakuwa na mengi ya kujifunza kumhusu. Hatupaswi kamwe kufikiri kwamba kitabu hiki kimetufunza mambo yote kumhusu Yehova. Huu ni mwanzo tu wa kujifunza yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu wetu. Na hata Biblia haituelezi mambo yote kumhusu Yehova. Mtume Yohana alikisia kwamba ikiwa mambo yote ambayo Yesu alifanya wakati wa huduma yake duniani yangeandikwa, “ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafsi ya kuziweka hati-kunjo ambazo zingeandikwa.” (Yohana 21:25) Ikiwa ilisemwa hivyo kumhusu Mwana, basi mengi zaidi yanaweza kusemwa kumhusu Baba!
22 Hata tukiishi milele, hatutaweza kujifunza mambo yote kumhusu Yehova. (Mhubiri 3:11) Basi fikiria tumaini tulilo nalo. Baada ya kuishi mamia, maelfu, mamilioni au hata mabilioni ya miaka, tutajua mengi zaidi kumhusu Yehova Mungu kuliko tujuavyo sasa. Lakini bado tutatambua kwamba kuna mambo mengi mazuri tutakayohitaji kujifunza. Tutakuwa na hamu ya kujifunza mengi zaidi, kwa kuwa sikuzote tutakuwa na sababu ya kuhisi kama mtunga-zaburi aliyeimba hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” (Zaburi 73:28) Uhai udumuo milele utakuwa na kusudi na utapendeza isivyowazika—kwa sababu tutazidi kumkaribia Yehova daima.
23. Unatiwa moyo kufanya nini?
23 Thamini upendo wa Yehova sasa kwa kumpenda kwa moyo wako wote, nafsi yako yote, akili zako zote, na nguvu zako zote. (Marko 12:29, 30) Mpende kwa uaminifu-mshikamanifu. Na maamuzi unayofanya kila siku, madogo kwa makubwa, yaonyeshe kwamba una azimio moja—kwamba sikuzote utafuata njia itakayoimarisha uhusiano wako na Baba yako wa mbinguni. Zaidi ya yote, na umkaribie Yehova zaidi, naye aendelee kukukaribia milele na milele!
-
-
“Hodari Kwa Nguvu”Mkaribie Yehova
-
-
Sehemu ya 1
“Hodari Kwa Nguvu”
Katika sehemu hii tutachunguza masimulizi ya Biblia yanayothibitisha kwamba Yehova ana nguvu za kuumba, kuangamiza, kulinda, na kurudisha hali upya. Mioyo yetu itajaa kicho tukielewa jinsi ambavyo Yehova Mungu, ambaye ni “hodari kwa nguvu,” anatumia “uweza” wake.—Isaya 40:26.
-
-
“Bwana Hupenda Haki”Mkaribie Yehova
-
-
Sehemu ya 2
“Bwana Hupenda Haki”
Mungu hulaumiwa isivyofaa kwa sababu ya ukosefu wa haki unaoenea ulimwenguni leo. Lakini, Biblia hufundisha ukweli unaotia moyo, yaani, “BWANA hupenda haki.” (Zaburi 37:28) Katika sehemu hii tutajifunza jinsi ambavyo ametenda kupatana na maneno hayo, na kuwapa wanadamu wote tumaini.
-
-
“Mwenye Hekima Moyoni”Mkaribie Yehova
-
-
Sehemu ya 3
“Mwenye Hekima Moyoni”
Hekima ya kweli ni mojawapo ya mambo yenye thamani sana unayoweza kutafuta. Yehova peke yake ndiye chanzo cha hekima hiyo. Katika sehemu hii tutachunguza kindani hekima ya Yehova Mungu isiyo na mipaka. Mwanamume mwaminifu Ayubu alisema hivi kumhusu: “Yeye ni mwenye hekima moyoni.”—Ayubu 9:4.
-
-
“Mungu Ni Upendo”Mkaribie Yehova
-
-
Sehemu ya 4
“Mungu Ni Upendo”
Upendo ndiyo sifa kuu zaidi ya Mungu. Pia ndiyo sifa inayovutia zaidi. Tunapochunguza baadhi ya mambo yenye kupendeza ya sifa hii bora, tutaelewa kwa nini Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
-