Obadia
Obadia
1 Maono ya Obadia:
Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amesema hivi kuhusu Edomu:+ “Kuna habari ambayo tumesikia kutoka kwa Yehova, na kuna mjumbe ambaye ametumwa kati ya mataifa, ‘Simameni, na tusimame tupigane naye.’ ”+
2 “Tazama! Nimekufanya mdogo kati ya mataifa.+ Unadharauliwa sana.+ 3 Kimbelembele cha moyo wako ndicho kimekudanganya,+ wewe unayekaa katika makimbilio ya mwamba,+ kwenye kilele ambapo yeye hukaa, akisema moyoni mwake, ‘Ni nani atakayenishusha chini duniani?’ 4 Ukipafanya mahali pako pawe juu kama tai, au ikiwa kiota chako kingewekwa kati ya nyota, ningekushusha chini kutoka hapo,”+ asema Yehova.
5 “Ikiwa wezi ndio wangekuja kwako, ikiwa waporaji wangekuja wakati wa usiku, ungenyamazishwa kwa kadiri gani?+ Je, hawangeiba kadiri wanavyotaka? Au ikiwa wakusanya-zabibu ndio wangekuja kwako, je, hawangeacha masalio fulani?+ 6 Lo! jinsi ambavyo walio wa Esau wametafutwa!+ Jinsi hazina zake zilizofichwa zimetafutwa! 7 Wamekufukuza hadi mpakani. Watu walewale walio katika agano pamoja nawe wamekudanganya+ wote. Watu walio na amani pamoja nawe wamekushinda.+ Wale wanaokula chakula pamoja nawe wataweka wavu chini yako kama mtu asiye na utambuzi.+ 8 Je, haitakuwa katika siku hiyo?” asema Yehova.
“Nami nitawaangamiza wenye hekima kutoka Edomu,+ na utambuzi kutoka eneo lenye milima la Esau. 9 Na wanaume wako wenye nguvu wataingiwa na woga,+ Ee Temani,+ kwa kuwa kila mmoja atakatiliwa mbali+ kutoka katika eneo lenye milima la Esau, kwa sababu ya kuuawa.+ 10 Kwa sababu ya jeuri uliyomtendea ndugu yako Yakobo,+ aibu itakufunika,+ nawe utakatiliwa mbali mpaka wakati usio na kipimo.+ 11 Siku uliyosimama kando, siku ambayo wageni walichukua jeshi lake na kulipeleka utekwani+ na wageni kabisa walipoingia katika lango lake,+ wakapiga kura+ juu ya Yerusalemu, wewe pia ulikuwa kama mmoja wao.
12 “Nawe hupaswi kutazama tukio katika siku ya ndugu yako,+ katika siku ya maafa yake; wala kushangilia juu ya wana wa Yuda katika siku ya kuangamia kwao;+ wala usiseme makuu katika siku ya taabu yao. 13 Hupaswi kuja katika lango la watu wangu siku ya maafa yao.+ Wewe, naam, wewe, hupaswi kukaza macho juu ya msiba wake siku ya maafa yake; wala kunyoosha mkono wako juu ya mali yake siku ya maafa yake.+ 14 Nawe hupaswi kusimama kwenye makutano ya njia, ili kukatilia mbali watu wake walioponyoka;+ wala kuwakabidhi waokokaji wake siku ya taabu.+ 15 Kwa maana siku ya Yehova juu ya mataifa yote iko karibu.+ Kama ulivyofanya, ndivyo utakavyofanyiwa.+ Matendo yako yatakurudia juu ya kichwa chako mwenyewe.+ 16 Kwa maana kama ninyi mlivyokunywa kwenye mlima wangu mtakatifu, ndivyo mataifa yote watakavyoendelea kunywa daima.+ Nao watakunywa na kumeza wawe kana kwamba hawakupata kuwapo kamwe.
17 “Na katika Mlima Sayuni ndipo watakapokuwa wale wanaoponyoka,+ nao utakuwa kitu kitakatifu;+ na nyumba ya Yakobo itamiliki mali yao.+ 18 Na nyumba ya Yakobo itakuwa moto,+ nyumba ya Yosefu itakuwa mwali wa moto, nyumba ya Esau itakuwa kama majani makavu;+ nao watayateketeza na kuyameza. Na hakutakuwapo waokokaji katika nyumba ya Esau;+ kwa maana Yehova mwenyewe amesema hayo. 19 Nao watamiliki Negebu, eneo lenye milima la Esau,+ na Shefela, ya Wafilisti.+ Nao watamiliki shamba la Efraimu+ na shamba la Samaria;+ na Benyamini atamiliki Gileadi.+ 20 Nao wahamishwa wa boma hili,+ wana wa Israeli, eneo lililomilikiwa na Wakanaani+ mpaka Sarefathi+ litakuwa lao. Na wahamishwa wa Yerusalemu, waliokuwa katika Sefaradi, watamiliki majiji ya Negebu.+
21 “Na waokozi+ watapanda Mlima Sayuni,+ ili kuhukumu eneo lenye milima la Esau;+ na lazima ufalme utakuwa wa Yehova.”+