Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • nwt 1 Wathesalonike 1:1-5:28
  • 1 Wathesalonike

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • 1 Wathesalonike
  • Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
1 Wathesalonike

BARUA YA KWANZA KWA WATHESALONIKE

1 Paulo, Silvano,*+ na Timotheo,+ kwa kutaniko la Wathesalonike walio katika muungano na Mungu Baba na Bwana Yesu Kristo:

Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani.

2 Sikuzote tunamshukuru Mungu tunapowataja nyote katika sala zetu,+ 3 kwa maana tunaendelea kukumbuka kazi yenu ya uaminifu, kazi yenu ngumu ya upendo, na jinsi ambavyo mmevumilia kwa sababu ya tumaini lenu+ katika Bwana wetu Yesu Kristo mbele za Mungu, Baba yetu. 4 Akina ndugu, tunajua Mungu anawapenda na amewachagua, 5 kwa sababu hatukuwahubiria habari njema kwa maneno tu, bali pia kwa nguvu na kwa roho takatifu na kwa usadikisho thabiti, kama mnavyojua jinsi tulivyotenda miongoni mwenu kwa ajili yenu. 6 Nanyi mlituiga sisi+ na Bwana pia,+ kwa kuwa mlilikubali neno kwa shangwe ya roho takatifu ingawa mlikuwa na dhiki nyingi,+ 7 na hivyo mkawa mfano mzuri kwa waamini wote katika Makedonia na Akaya.

8 Kwa kweli, mmelitangaza neno la Yehova* katika Makedonia na Akaya, na pia kila mahali watu wamesikia kuhusu imani yenu katika Mungu,+ hivi kwamba hatuhitaji kusema lolote. 9 Watu hao wanaendelea kusema jinsi tulivyowahubiria ninyi mara ya kwanza na jinsi mlivyomgeukia Mungu na kuacha kuabudu sanamu+ ili kumtumikia Mungu wa kweli aliye hai, 10 na kumsubiri Mwana wake aje kutoka mbinguni,+ ambaye alifufuliwa kutoka kwa wafu, yaani, Yesu, anayetukomboa kutoka kwenye ghadhabu inayokuja.+

2 Kwa kweli, ninyi wenyewe akina ndugu mnajua kwamba ziara yetu kwenu ilikuwa na mafanikio.+ 2 Kwa maana ingawa kwanza tulikuwa tumeteseka na kudharauliwa huko Filipi,+ kama mnavyojua, tulijipa ujasiri* kupitia Mungu wetu ili tuwatangazie ninyi habari njema ya Mungu+ licha ya upinzani.* 3 Kwa maana mambo tunayowahimiza hayatokani na kosa, uchafu, wala udanganyifu, 4 lakini kwa kuwa tumekubaliwa na Mungu kukabidhiwa habari njema, hatusemi ili tuwapendeze wanadamu, bali tumpendeze Mungu ambaye huchunguza mioyo yetu.+

5 Kwa kweli, mnajua hatukutumia kamwe maneno ya kuwasifusifu au kuwa wanafiki tukiwa na makusudi yenye pupa;+ Mungu ni shahidi! 6 Wala hatujatafuta utukufu kutoka kwa wanadamu, iwe ni kutoka kwenu au kwa watu wengine, ingawa tukiwa mitume wa Kristo tungeweza kuwa mzigo wenye gharama kwenu.+ 7 Badala yake, tuliwatendea kwa upole, kama vile mama anayenyonyesha anavyowatunza* watoto wake kwa wororo. 8 Basi, kwa maana tulikuwa na upendo mwororo kwenu, tulijitahidi* kuwapa habari njema ya Mungu na hata uhai wetu* wenyewe,+ kwa sababu tuliwapenda sana.+

9 Hakika akina ndugu, mnakumbuka kazi yetu ngumu na yenye kutaabisha. Tulifanya kazi usiku na mchana, ili tusimpe yeyote kati yenu mzigo wenye gharama,+ tulipowahubiria habari njema ya Mungu. 10 Ninyi ni mashahidi, na Mungu vilevile, wa jinsi tulivyokuwa washikamanifu na waadilifu na wasiolaumika kwenu. 11 Mnajua jinsi tulivyoendelea kumhimiza, kumfariji, na kumshauri kila mmoja wenu,+ kama baba+ anavyowatendea watoto wake, 12 ili mwendelee kutembea kwa kumstahili Mungu+ anayewaita kwenye Ufalme+ na utukufu wake.+

13 Kwa kweli, hii ndiyo sababu tunamshukuru Mungu bila kuacha,+ kwa kuwa mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali si kama neno la wanadamu, bali kama lilivyo kwa kweli, neno la Mungu, ambalo pia linafanya kazi ndani yenu waamini. 14 Kwa maana, akina ndugu mliiga makutaniko ya Mungu yaliyo katika muungano na Kristo Yesu huko Yudea, kwa sababu mliteswa na wananchi wenzenu,+ kama vile wao pia wanavyoteswa na Wayahudi, 15 ambao hata walimuua Bwana Yesu+ na manabii na wakatutesa.+ Zaidi ya hayo, hawafanyi mambo yanayompendeza Mungu, na wanapinga mambo yanayowafaa wanadamu wote, 16 wakijaribu kutuzuia kuzungumza na watu wa mataifa ili waokolewe.+ Kwa hiyo, sikuzote wanajaza kipimo cha dhambi zao. Lakini hatimaye hasira yake imekuja juu yao.+

17 Hata hivyo, akina ndugu, tulipotenganishwa nanyi* kwa muda mfupi (katika mwili, bali si moyoni), kwa kuwa tulitamani sana, tulijitahidi kabisa kuwaona tena uso kwa uso.* 18 Kwa sababu hiyo, tulitaka kuja kwenu, ndiyo, mimi Paulo, nilijaribu si mara moja tu bali mara mbili; lakini Shetani aliifunga njia yetu. 19 Ni nini tumaini letu au shangwe au taji la furaha mbele ya Bwana wetu Yesu wakati wa kuwapo kwake? Je, kwa kweli si ninyi?+ 20 Kwa kweli ninyi ndio utukufu na shangwe yetu.

3 Basi tuliposhindwa kuvumilia, tuliamua kubaki Athene peke yetu;+ 2 tukamtuma Timotheo,+ ndugu yetu na mhudumu wa Mungu* katika habari njema kuhusu Kristo, ili awaimarishe* na kuwafariji kuhusiana na imani yenu, 3 ili yeyote asitikiswe* na dhiki hizo. Kwa maana ninyi wenyewe mnajua hatuwezi kuepuka mateso hayo.*+ 4 Kwa kuwa tulipokuwa pamoja nanyi, tulikuwa tukiwaambia mapema kwamba tutapatwa na dhiki, na imekuwa hivyo, kama mnavyojua.+ 5 Ndiyo sababu, niliposhindwa kuvumilia hilo, nilimtuma mtu ili nijue kuhusu uaminifu wenu,+ isiwe kwamba Mjaribu+ alikuwa amewajaribu, na kazi yetu ngumu ikawa ya bure.

6 Lakini Timotheo amerudi sasa hivi kutoka kwenu+ na kutujulisha habari njema kuhusu uaminifu na upendo wenu, kwamba mnaendelea kutukumbuka kwa upendo na kwamba mnatamani kutuona kama sisi pia tunavyotamani kuwaona. 7 Hiyo ndiyo sababu, katika taabu* na dhiki zetu zote, tumefarijiwa kwa sababu yenu na uaminifu mnaoonyesha.+ 8 Kwa sababu tunapata nguvu* ikiwa mnasimama imara katika Bwana. 9 Kwa maana tunawezaje kumshukuru Mungu kwa ajili yenu kutokana na shangwe kubwa tuliyo nayo mbele za Mungu wetu kwa sababu yenu? 10 Usiku na mchana tunasali kwa bidii kadiri tunavyoweza ili tuwaone uso kwa uso na kuongeza chochote kilichopungua katika imani yenu.+

11 Sasa Mungu Baba yetu na Bwana wetu Yesu na watufungulie njia ili tuje kwenu. 12 Zaidi ya hayo, Bwana na awawezeshe mwongezeke, ndiyo, mpendane zaidi+ na kuwapenda wote, kama tunavyowapenda ninyi, 13 ili afanye mioyo yenu kuwa imara, isiyolaumika katika utakatifu mbele za Mungu+ na Baba yetu wakati wa kuwapo kwa Bwana wetu Yesu+ pamoja na watakatifu wake wote.

4 Mwishowe, akina ndugu, kama tulivyowaagiza jinsi mnavyopaswa kutembea ili kumpendeza Mungu,+ kama vile kwa kweli mnavyotembea, tunawaomba na kuwahimiza katika Bwana Yesu mwendelee kufanya hivyo kwa ukamili zaidi. 2 Kwa maana mnajua mwongozo tuliowapa* kupitia kwa Bwana Yesu.

3 Kwa maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kwamba mnapaswa kuwa watakatifu+ na mjiepushe na uasherati.*+ 4 Kila mmoja wenu anapaswa kujua jinsi ya kuudhibiti mwili wake* mwenyewe+ katika utakatifu+ na heshima, 5 si kwa hamu yenye pupa ya ngono+ kama ya watu wa mataifa wasiomjua Mungu.+ 6 Mtu yeyote hapaswi kuvuka mipaka inayofaa na kumdhulumu ndugu yake katika jambo hilo, kwa sababu Yehova* ndiye hutoa adhabu kwa mambo yote haya, kama tulivyowaambia mapema na pia kuwaonya kwa uthabiti. 7 Kwa maana Mungu hakutuita tuishi maisha ya uchafu, bali tuwe watakatifu.+ 8 Kwa hiyo, mtu anayepuuza jambo hili, hampuuzi mwanadamu, bali Mungu,+ anayewapa ninyi roho yake takatifu.+

9 Hata hivyo, kuhusu upendo wa kindugu,+ hatuhitaji kuwaandikia ninyi, kwa maana ninyi wenyewe mmefundishwa na Mungu kupendana.+ 10 Kwa kweli, mnawatendea hivyo ndugu zenu wote katika Makedonia. Hata hivyo, tunawahimiza, akina ndugu, endeleeni kufanya hivyo kwa ukamili zaidi. 11 Muwe na lengo la kuishi kwa utulivu+ na kushughulika na mambo yenu wenyewe+ na kufanya kazi kwa mikono yenu,+ kama tulivyowaagiza, 12 ili mtembee kwa adabu machoni pa watu walio nje+ na msipungukiwe chochote.

13 Zaidi ya hayo, akina ndugu, tunataka mwelewe* kuhusu wale wanaolala usingizi katika kifo,+ ili msihuzunike kama wanavyofanya watu wasio na tumaini.+ 14 Kwa maana ikiwa tunaamini kwamba Yesu alikufa na kufufuliwa,+ vivyo hivyo Mungu atawafufua wale ambao wamelala usingizi katika kifo kupitia Yesu.+ 15 Kwa maana tunawaambia hivi kwa neno la Yehova,* kwamba sisi tulio hai ambao tutabaki mpaka kuwapo kwa Bwana hatutawatangulia kwa vyovyote wale ambao wamelala usingizi katika kifo; 16 kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wenye amri, kwa sauti ya malaika mkuu+ na tarumbeta ya Mungu, na wale waliokufa katika muungano na Kristo watafufuliwa kwanza.+ 17 Baadaye, sisi tulio hai ambao tumebaki, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu+ ili tukutane na Bwana+ hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana sikuzote.+ 18 Kwa hiyo endeleeni kufarijiana kwa maneno hayo.

5 Sasa akina ndugu, hamhitaji kuandikiwa chochote kuhusu nyakati na majira. 2 Kwa maana ninyi wenyewe mnajua vema kwamba siku ya Yehova*+ inakuja kama vile mwizi anavyokuja usiku.+ 3 Wakati watakapokuwa wakisema: “Amani na usalama!” ndipo uharibifu wa ghafla utakapowapata mara moja,+ kama vile maumivu ya kuzaa ya mwanamke mwenye mimba, nao hawataponyoka kamwe. 4 Lakini ninyi, akina ndugu, hamko gizani, hivi kwamba siku hiyo iwafikie ghafla kama vile ingewafikia wezi, 5 kwa maana ninyi nyote ni wana wa nuru na wana wa mchana.+ Sisi si wa usiku wala wa giza.+

6 Basi, tusiendelee kulala usingizi kama wengine wanavyofanya,+ bali tukae macho+ na kutunza akili zetu.+ 7 Kwa maana wale wanaolala usingizi hulala usiku, na wale wanaolewa, hulewa usiku.+ 8 Lakini sisi tulio wa mchana, na tutunze akili zetu na kuvaa bamba la kifuani la imani na upendo na tumaini la wokovu kama kofia ya chuma+ 9 kwa sababu Mungu hakutuchagua ili tupatwe na hasira, bali tupate wokovu+ kupitia Bwana wetu Yesu Kristo. 10 Alikufa kwa ajili yetu,+ ili kama tuko macho au tumelala usingizi,* tuishi pamoja naye.+ 11 Kwa hiyo endeleeni kutiana moyo* na kujengana,+ kama vile kwa kweli mnavyofanya.

12 Sasa tunawaomba, akina ndugu, waheshimuni wale wanaofanya kazi kwa bidii miongoni mwenu na wanaowasimamia katika Bwana na kuwaonya ninyi; 13 na mwafikirie kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao.+ Dumisheni amani miongoni mwenu.+ 14 Kwa upande mwingine, tunawahimiza akina ndugu, waonyeni* wale wasiofuata utaratibu,+ wafarijini wale walioshuka moyo,* wasaidieni walio dhaifu, iweni na subira kwa watu wote.+ 15 Hakikisheni hakuna yeyote anayelipa ubaya kwa ubaya,+ bali sikuzote mwendelee kutendeana mema kati yenu na kwa wengine wote.+

16 Shangilieni sikuzote.+ 17 Salini bila kuacha.+ 18 Toeni shukrani kuhusu kila jambo.+ Hayo ndiyo mapenzi ya Mungu kwa ajili yenu katika Kristo Yesu. 19 Msiuzime moto wa roho.+ 20 Msitendee unabii kwa dharau.+ 21 Hakikisheni mambo yote;+ shikamaneni na yaliyo mema. 22 Epukeni kila aina ya uovu.+

23 Mungu wa amani na awatakase kikamili. Na bila kasoro yoyote, roho na nafsi* na mwili wenu akina ndugu, na vihifadhiwe bila lawama wakati wa kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo.+ 24 Yule anayewaita ninyi ni mwaminifu, na kwa hakika atafanya hivyo.

25 Akina ndugu, endeleeni kusali kwa ajili yetu.+

26 Wasalimuni ndugu wote kwa busu takatifu.

27 Ninawaweka chini ya wajibu mzito kwa Bwana mhakikishe kwamba ndugu wote wanasomewa barua hii.+

28 Fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo ziwe pamoja nanyi.

Pia anaitwa Sila.

Angalia Nyongeza A5.

Au “uhodari.”

Au labda, “licha ya kupambana sana.”

Au “anavyowalea kwa upendo.”

Tnn., “tulipendezwa vema.”

Au “nafsi zetu.”

Au “tulipoachwa mayatima.”

Tnn., “kuona nyuso zenu.”

Au labda, “mfanyakazi mwenzi wa Mungu.”

Au “awatie nguvu.”

Tnn., “asiyumbishwe.”

Au “tumewekwa rasmi kwa ajili ya hilo.”

Tnn., “uhitaji.”

Tnn., “tunaishi.”

Au “maagizo tuliyowapa.”

Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.

Tnn., “chombo chake.”

Angalia Nyongeza A5.

Au “msikose kujua.”

Angalia Nyongeza A5.

Angalia Nyongeza A5.

Au “tumelala usingizi katika kifo.”

Au “kufarijiana.”

Au “mwakaripie.”

Au “wale waliovunjika moyo.” Tnn., “wale walio na nafsi ndogo.”

Au “uhai.” Angalia Kamusi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki