Marko
10 Kutoka hapo akaondoka na kuja kwenye mipaka ya Yudea na ng’ambo ya Yordani, na tena umati ukamjia, na kama alivyokuwa na desturi ya kufanya akaanza tena kuwafundisha.+ 2 Mafarisayo sasa wakamkaribia na, ili kumjaribu, wakaanza kumuuliza kama ni halali mwanamume kumtaliki mke wake.+ 3 Akajibu akawaambia: “Musa aliwaamuru ninyi nini?” 4 Wakasema: “Musa aliruhusu kuandika cheti cha kufukuza na kumtaliki.”+ 5 Lakini Yesu akawaambia: “Kwa kufikiria ugumu wenu wa moyo+ aliwaandikia ninyi amri hiyo. 6 Hata hivyo, tangu mwanzo wa kuumba ‘Yeye aliwafanya mwanamume na mwanamke.+ 7 Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake, 8 na hao wawili watakuwa mwili mmoja’;+ hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. 9 Kwa hiyo kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”+ 10 Alipokuwa tena katika nyumba+ wanafunzi wakaanza kumuuliza kuhusu hilo. 11 Naye akawaambia: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine anafanya uzinzi+ dhidi yake, 12 na mwanamke, baada ya kumtaliki mume wake, akiolewa na mwingine, anafanya uzinzi.”+
13 Sasa watu wakaanza kumletea watoto wachanga ili awaguse; lakini wanafunzi wakawakemea.+ 14 Alipoona hilo, Yesu akaghadhibika na kuwaambia: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.+ 15 Kwa kweli ninawaambia ninyi, Yeyote yule asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mchanga hataingia kamwe ndani yake.”+ 16 Naye akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.+
17 Naye alipokuwa akitoka aende, mtu fulani akamkimbilia akapiga magoti mbele yake na kumuuliza: “Mwalimu Mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 18 Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniita mwema?+ Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.+ 19 Wewe unazijua amri, ‘Usiue,+ Usifanye uzinzi,+ Usiibe,+ Usitoe ushahidi wa uwongo,+ Usipunje,+ Mheshimu baba yako na mama yako.’ ”+ 20 Mtu huyo akamwambia: “Mwalimu, mambo yote hayo nimeyashika tangu ujana wangu na kuendelea.” 21 Yesu akamtazama akampenda na kumwambia: “Umekosa jambo moja: Nenda, ukauze vitu ulivyo navyo uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni, kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 22 Lakini akasikitishwa na neno hilo na kwenda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.+
23 Baada ya kutazama huku na huku Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Jinsi itakavyokuwa vigumu kwa wale wenye pesa+ kuingia katika ufalme wa Mungu!”+ 24 Lakini wanafunzi wakashangaa+ kwa sababu ya maneno yake. Yesu akajibu akawaambia tena: “Wanangu, jinsi ilivyo vigumu kuingia katika ufalme wa Mungu! 25 Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.”+ 26 Bado wakazidi kustaajabu na kumwambia: “Ni nani ambaye, kwa kweli, anaweza kuokolewa?”+ 27 Akiwatazama moja kwa moja Yesu akasema: “Kwa wanadamu haiwezekani, lakini sivyo ilivyo kwa Mungu, kwa maana mambo yote yanawezekana kwa Mungu.”+ 28 Petro akaanza kumwambia: “Tazama! Sisi tuliacha vitu vyote na tumekuwa tukikufuata wewe.”+ 29 Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Hakuna mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema+ 30 ambaye hatapata mara mia+ sasa katika kipindi hiki cha wakati, nyumba na ndugu na dada na mama na watoto na mashamba, pamoja na mateso,+ na katika mfumo wa mambo unaokuja uzima wa milele. 31 Hata hivyo, wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na wa mwisho watakuwa wa kwanza.”+
32 Sasa walikuwa barabarani, wakipanda kwenda Yerusalemu, na Yesu alikuwa akienda mbele yao, nao wakashangaa; lakini wale waliofuata wakaanza kuogopa. Mara nyingine tena akawachukua wale kumi na wawili kando na kuanza kuwaambia mambo haya yatakayompata:+ 33 “Tazama, tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani, na waandishi, nao watamhukumia kifo na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa,+ 34 nao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga mijeledi na kumuua, lakini siku tatu baadaye atafufuka.”+
35 Na Yakobo na Yohana, wana wawili wa Zebedayo,+ wakamwendea na kumwambia: “Mwalimu, tunataka utufanyie chochote tutakachokuomba.”+ 36 Akawaambia: “Mnataka niwafanyie nini?” 37 Wakamwambia: “Uturuhusu kuketi, mmoja kwenye mkono wako wa kuume na mmoja kwenye mkono wako wa kushoto, katika utukufu wako.”+ 38 Lakini Yesu akawaambia: “Hamjui kile mnachoomba. Je, mnaweza kunywa kikombe ambacho ninakunywa, au kubatizwa kwa ubatizo ninaobatizwa?”+ 39 Wakamwambia: “Tunaweza.” Ndipo Yesu akawaambia: “Kikombe ninachokunywa mtakunywa, na ubatizo ninaobatizwa mtabatizwa.+ 40 Hata hivyo, kuketi kwenye mkono wangu wa kuume au kwenye mkono wangu wa kushoto sina haki kutoa,+ bali wataketi wale ambao wametayarishiwa.”
41 Basi, wale wengine kumi waliposikia jambo hilo, wakaanza kuwaghadhibikia Yakobo na Yohana.+ 42 Lakini Yesu, baada ya kuwaita, akawaambia: “Mnajua kwamba wale ambao huonekana kuwa wanatawala mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu wao hutumia mamlaka juu yao.+ 43 Hivyo sivyo ilivyo katikati yenu; bali yeyote yule anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu,+ 44 na yeyote yule anayetaka kuwa wa kwanza katikati yenu lazima awe mtumwa wa wote.+ 45 Kwa maana hata Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa,+ bali kuhudumu na kutoa nafsi yake iwe fidia+ badala ya wengi.”+
46 Nao wakaingia Yeriko. Lakini yeye na wanafunzi wake na umati mkubwa walipokuwa wakitoka Yeriko, Bartimayo (mwana wa Timayo), kipofu aliye mwombaji, alikuwa ameketi kando ya barabara.+ 47 Aliposikia kwamba ni Yesu Mnazareti, akaanza kupaaza sauti na kusema: “Mwana wa Daudi,+ Yesu, unirehemu!”+ 48 Ndipo wengi wakaanza kumwambia kwa ukali anyamaze; lakini akazidi kupaaza sana sauti: “Mwana wa Daudi, unirehemu!”+ 49 Kwa hiyo Yesu akasimama na kusema: “Mwiteni.” Nao wakamwita yule mtu aliye kipofu, wakamwambia: “Jipe moyo, simama, anakuita.”+ 50 Akatupa vazi lake la nje, akaruka na kusimama kwa miguu yake, akamwendea Yesu. 51 Yesu akamjibu, akasema: “Unataka nikufanyie nini?”+ Yule mtu aliye kipofu akamwambia: “Raboni, acha nipate tena kuona.”+ 52 Na Yesu akamwambia: “Nenda, imani yako imekuponya.”+ Na mara moja akapata tena kuona,+ naye akaanza kumfuata barabarani.+