1 Samweli
30 Na ikawa kwamba, wakati Daudi na watu wake walipokuwa wakija Siklagi+ siku ya tatu, Waamaleki+ wakavamia upande wa kusini na pia Siklagi; wakapiga Siklagi, wakaliteketeza kwa moto, 2 nao wakachukua mateka wanawake+ na vyote vilivyokuwa ndani yake, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi. Hawakumuua yeyote, bali waliwachukua na kwenda zao. 3 Daudi alipokuja jijini na watu wake, tazama, jiji lilikuwa limeteketezwa kwa moto, na wake zao na wana wao na binti zao walikuwa wamechukuliwa mateka. 4 Na Daudi na watu waliokuwa pamoja naye wakaanza kupaaza sauti zao, wakalia,+ mpaka nguvu za kuendelea kulia zilipokwisha ndani yao. 5 Na wake wawili wa Daudi walikuwa wamechukuliwa mateka, Ahinoamu+ Myezreeli, na Abigaili+ mke wa Nabali Mkarmeli. 6 Naye Daudi akataabika sana,+ kwa sababu watu walisema apigwe kwa mawe;+ kwa maana nafsi za watu wote zilikuwa zimeingiwa na uchungu;+ kila mmoja kwa sababu ya wanawe na binti zake. Basi Daudi akajitia nguvu kwa Yehova Mungu wake.+
7 Hivyo Daudi akamwambia Abiathari+ kuhani, mwana wa Ahimeleki: “Tafadhali ilete hapa efodi.”+ Naye Abiathari akamletea Daudi ile efodi. 8 Daudi akaanza kumuuliza Yehova,+ akisema: “Je, nikifuatilie kikundi hiki cha waporaji? Je, nitawafikia?”+ Ndipo akamwambia: “Nenda, uwafuatilie, kwa maana bila shaka utawafikia, nawe bila shaka utaleta ukombozi.”+
9 Mara moja Daudi akaondoka, yeye pamoja na wale watu mia sita+ waliokuwa naye, wakaenda mpaka bonde la mto la Besori, na watu ambao walipaswa kuachwa nyuma wakasimama tuli. 10 Na Daudi akaendelea kufuatilia,+ yeye pamoja na watu mia nne, lakini watu mia mbili waliokuwa wamechoka sana wasiweze kuvuka lile bonde la mto la Besori+ wakasimama tuli.
11 Nao wakakuta mtu, Mmisri,+ shambani. Basi wakampeleka kwa Daudi na kumpa mkate ale, na kumpa maji anywe. 12 Zaidi ya hayo, wakampa kipande cha keki ya tini zilizoshinikizwa na keki mbili za zabibu kavu.+ Ndipo akala na roho+ yake ikarudi kwake; kwa maana hakuwa amekula mkate wala kunywa maji kwa siku tatu, mchana na usiku. 13 Sasa Daudi akamwambia: “Wewe ni wa nani, nawe unatoka wapi?” naye akasema: “Mimi ni mtumishi Mmisri, mtumwa wa mtu Mwamaleki, lakini bwana wangu aliniacha kwa sababu nilishikwa na ugonjwa siku tatu zilizopita.+ 14 Sisi ndio tuliovamia upande wa kusini wa Wakerethi+ na nchi ya Yuda na upande wa kusini wa Kalebu;+ nasi tukateketeza Siklagi kwa moto.” 15 Naye Daudi akamwambia: “Je, utaniongoza, nishuke mpaka kwenye hiki kikundi cha waporaji?” Naye akasema: “Niapie+ kwa Mungu kwamba hutaniua, wala kunitia mkononi mwa bwana wangu,+ nami nitakuongoza, ushuke mpaka kwenye hiki kikundi cha waporaji.”
16 Basi akamwongoza, akashuka,+ na tazama, walikuwa wameenea bila utaratibu juu ya uso wote wa nchi, wakila na kunywa na kufanya karamu+ kwa sababu ya nyara yote kubwa ambayo walikuwa wamechukua kutoka katika nchi ya Wafilisti na nchi ya Yuda.+ 17 Na Daudi akawapiga kuanzia giza la asubuhi mpaka jioni, apate kuwaangamiza; wala hakuna mtu kati yao aliyeponyoka+ ila vijana mia nne waliopanda ngamia na kukimbia. 18 Naye Daudi akakomboa vyote ambavyo Waamaleki walikuwa wamechukua,+ na Daudi akakomboa wake zake wawili. 19 Na hakuna kitu chochote chao kilichokosekana, kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi na wana na mabinti na kuanzia nyara, mpaka chochote ambacho walikuwa wamejichukulia.+ Daudi alirudisha kila kitu. 20 Basi Daudi akachukua makundi yote na mifugo, ambayo waliitanguliza mbele ya ile mifugo mingine. Kisha wakasema: “Hii ni nyara ya Daudi.”+
21 Mwishowe Daudi akawafikia wale wanaume mia mbili+ ambao walikuwa wamechoka sana wasiweze kwenda na Daudi, na ambao waliwaacha waketi kando ya bonde la mto la Besori; nao wakatoka kuja kumpokea Daudi na kuwapokea watu waliokuwa pamoja naye. Daudi alipowakaribia watu hao, akaanza kuwauliza hali yao. 22 Hata hivyo, kila mtu mbaya na asiyefaa kitu+ kati ya watu walioenda pamoja na Daudi akajibu na kuzidi kusema: “Kwa kuwa hawakwenda pamoja nasi, hatutawapa nyara yoyote ambayo tumekomboa, isipokuwa kila mmoja atapewa mke wake na wanawe, wawachukue na kwenda.” 23 Lakini Daudi akasema: “Ndugu zangu, msifanye hivyo na vitu ambavyo Yehova ametupa sisi,+ kwa kuwa alitulinda+ na kukitia mkononi mwetu kile kikundi cha waporaji kilichokuja juu yetu.+ 24 Na ni nani atakayewasikiliza kwa neno hili? Kwa maana kama lilivyo fungu la yule aliyeshuka kwenda vitani ndivyo litakavyokuwa fungu la yule aliyeketi kando ya mizigo.+ Wote watapata fungu pamoja.”+ 25 Na ikawa kwamba kuanzia siku hiyo na kuendelea, akaliweka hilo kuwa sharti na uamuzi wa hukumu+ kwa ajili ya Israeli mpaka leo hii.
26 Wakati Daudi alipofika Siklagi, akapeleka sehemu ya nyara kwa wanaume wazee wa Yuda, rafiki zake,+ akisema: “Tazameni, hii ni zawadi+ ya baraka kwa ajili yenu kutoka katika nyara za adui za Yehova.” 27 Kwa wale waliokuwa Betheli,+ na kwa wale waliokuwa Ramothi+ la kusini, na kwa wale waliokuwa Yatiri,+ 28 na kwa wale waliokuwa Aroeri, na kwa wale waliokuwa Sifmothi, na kwa wale waliokuwa Eshtemoa,+ 29 na kwa wale waliokuwa Rakali, na kwa wale waliokuwa katika majiji ya Wayerahmeeli,+ na kwa wale waliokuwa katika majiji ya Wakeni,+ 30 na kwa wale waliokuwa Horma,+ na kwa wale waliokuwa Borashani,+ na kwa wale waliokuwa Athaki, 31 na kwa wale waliokuwa Hebroni,+ na mahali pote ambapo Daudi alikuwa ametembea, yeye pamoja na watu wake.