Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mmejaza Yerusalemu Fundisho Lenu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Wanafunzi wa Yesu wakiwahubiria Wayahudi na wageuzwa imani katika eneo lenye shughuli nyingi.

      SEHEMU YA 1 • MATENDO 1:1–6:7

  • “Kutaniko. . .Likaanza Kuteswa Sana”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Stefano amesimama kwa utulivu mbele ya Sanhedrini.

      Sehemu Ya 2 • MATENDO 6:8–9:43

      “Kutaniko . . . Likaanza Kuteswa Sana”

      MATENDO 8:1

      Je, upinzani uliwazuia Wakristo wa karne ya kwanza kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu? Hapana. Katika sehemu hii, tutaona jinsi mateso hayo makali yalivyochangia kuenea kwa kazi ya kuhubiri.

      Akina ndugu wakiwa katika mahakama ya Kikomunisti iliyokuwa Ujerumani Mashariki.
  • “Watu wa Mataifa . . . Wamelikubali Neno la Mungu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Petro na ndugu wengine wakiingia kwenye nyumba ya Kornelio.

      SEHEMU YA 3 • MATENDO 10:1–12:25

      “Watu Wa Mataifa . . . Wamelikubali Neno La Mungu”

      MATENDO 11:1

      Je, Wayahudi ambao sasa ni wafuasi wa Yesu watakubali kuwahubiria habari njema Watu wa Mataifa wasiotahiriwa? Katika sehemu hii tutaona jinsi roho ya Yehova ilivyowasaidia Wakristo kushinda ubaguzi, na kuwa na bidii katika kazi ya kutoa ushahidi kwa watu wa mataifa yote.

      Wenzi wa ndoa wakimhubiria mvuvi.
  • “Waliotumwa na Roho Takatifu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Barnaba akitupwa nje ya jiji la Antiokia ya Pisidia na wapinzani wenye hasira.

      SEHEMU YA 4 • MATENDO 13:1–14:28

      “Waliotumwa Na Roho Takatifu”

      MATENDO 13:4

      Katika sehemu hii, tutachunguza safari ya kwanza ya umishonari ya mtume Paulo. Mtume huyo aliteswa katika jiji moja baada ya lingine. Hata hivyo, akiongozwa na roho takatifu, aliendelea kutoa ushahidi, na kuanzisha makutaniko mapya. Masimulizi hayo yenye kusisimua yatatuchochea kuwa na bidii hata zaidi katika huduma yetu.

      Mashahidi wa Yehova nchini Kanada wakifuatwa na kikundi cha watu wenye hasira na wanaotishia usalama wao mwaka wa 1945.
  • “Mitume na Wazee Wakakusanyika Pamoja”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Sila na Yuda wakisoma kitabu cha kukunjwa katika kutaniko la Antiokia ya Siria.

      SEHEMU YA 5 • MATENDO 15:1-35

      “Mitume Na Wazee Wakakusanyika Pamoja”

      MATENDO 15:6

      Suala zito lililotishia amani na umoja wa makutaniko lilitokea. Makutaniko yangepata wapi mwongozo wa kutatatua suala hilo? Katika sehemu hii, tutajifunza jinsi kutaniko la karne ya kwanza lilivyopangwa. Mpango huo unafuatwa na watu wa Mungu leo.

      Mwangalizi wa mzunguko akitoa hotuba kutanikoni.
  • “Turudi Tukawatembelee Akina Ndugu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Mtume Paulo na Timotheo wakiwa wamesimama kwenye meli. Timotheo akionyesha kitu fulani kilicho mbali huku wafanyakazi wa meli wakiendelea na kazi.

      SEHEMU YA 6 • MATENDO 15:36–18:22

      “Turudi Tukawatembelee Akina Ndugu”

      MATENDO 15:36

      Waangalizi wa mzunguko wana jukumu gani muhimu katika kutaniko la Kikristo? Ni baraka gani tunazopata tunapokubali kwa hiari migawo ya Kitheokrasi? Tunawezaje kuitumia Biblia vizuri tunapojadiliana na watu, na kwa nini tunapaswa kubadilika kulingana na hali za watu? Tutapata majibu ya maswali hayo na mengine tunaposafiri na mtume Paulo katika safari yake ya pili ya umishonari.

      Ndugu mkomavu akizungumza na ndugu wawili vijana wakiwa ndani ya gari.
  • “Kufundisha Hadharani na Nyumba kwa Nyumba”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Paulo akihubiria kikundi cha watu sokoni jijini Efeso huku watu wengine wakiendelea na shughuli zao.

      SEHEMU YA 7 • MATENDO 18:23–21:17

      ‘Kufundisha Hadharani Na Nyumba Kwa Nyumba’

      MATENDO 20:20

      Kwa nini tunahitaji kuwa wanyenyekevu na kubadilika kulingana na hali tunapowafundisha wengine? Ni njia gani kuu ya kuhubiri tunayotumia? Tunawezaje kuonyesha kwamba kufanya mapenzi ya Mungu ni muhimu kuliko shughuli zetu za kibinafsi? Masimulizi yenye kusisimua ya safari ya tatu na ya mwisho ya umishonari ya Paulo yanaweza kutusaidia kujibu maswali hayo muhimu.

      Ndugu akimhubiria mwanamke kwenye kituo cha garimoshi chenye shughuli nyingi.
  • “Akiwahubiria Ufalme wa Mungu . . . Bila Kizuizi”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • Mpwa wa Paulo akiongea na Klaudio Lisia.

      SEHEMU YA 8 • MATENDO 21:18–28:31

      “Akiwahubiria Ufalme Wa Mungu . . . Bila Kizuizi”

      MATENDO 28:31

      Katika sehemu hii, tutaandamana na Paulo anapokabiliana na umati wenye vurugu, akiwa gerezani, na anapofikishwa mbele ya maofisa mbalimbali Waroma. Licha ya yote hayo, mtume huyo anaendelea kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu. Unapochunguza sehemu ya kumalizia yenye kusisimua ya kitabu cha Matendo, jiulize: ‘Ninaweza kumwigaje mweneza–injili huyu jasiri na mwenye bidii?’

      Igizo linaloonyesha mvulana mdogo akiendesha baiskeli na kwa tahadhari anasambaza machapisho ya Biblia yaliyopigwa marufuku katika miaka ya 1940.
  • “Mtakuwa Mashahidi Wangu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 2

      “Mtakuwa Mashahidi Wangu”

      Yesu awatayarisha mitume wake kwa ajili ya kazi ya kuhubiri

      Matendo 1:1-26

      1-3. Yesu aliondoka duniani jinsi gani, na ni maswali gani yanayotokea?

      KWA majuma kadhaa sasa mitume wana shangwe sana! Majuma machache yaliyopita walikuwa na huzuni na majonzi, lakini kwa kuwa sasa Yesu amefufuka, wana furaha sana. Kwa siku 40 Yesu amewatokea wafuasi wake katika pindi mbalimbali, akawafundisha na kuwatia moyo. Hata hivyo, leo anawatokea kwa mara ya mwisho.

      2 Wakiwa wamesimama pamoja naye katika Mlima wa Mizeituni, mitume wake wanasikiliza kwa makini sana kila neno analosema. Anapomaliza kuzungumza, wanaona kana kwamba wakati umepita haraka sana. Kisha, baada ya kuinua mikono yake na kuwabariki, Yesu anaanza kupaa kutoka duniani! Huku wafuasi wake wakiendelea kumtazama, anaingia mawinguni. Mwishowe, anafunikwa na wingu hivi kwamba hawawezi kumwona tena. Ingawa hawamwoni bado wanatazama mbinguni.​—Luka 24:50; Mdo. 1:9, 10.

      3 Huo ni mwanzo wa badiliko kubwa maishani mwa mitume wa Yesu. Kwa kuwa sasa Bwana wao, Yesu Kristo, amerudi mbinguni, watafanya nini? Bwana wao amewatayarisha vizuri kwa ajili ya kazi aliyoanzisha. Yesu aliwapa maagizo gani? Je, waliyafuata? Wakristo leo wanawezaje kunufaika na habari hiyo? Majibu ya maswali hayo yanapatikana katika sura ya kwanza ya kitabu cha Matendo.

      Yesu anapaa mbinguni huku mitume wake wakimwangalia.

      “Uthibitisho Mwingi Wenye Kusadikisha” (Mdo. 1:1-5)

      4. Katika kitabu cha Matendo, Luka anaanza masimulizi yake jinsi gani?

      4 Luka anaanza masimulizi yake kwa kuzungumza na Theofilo.a Kwa kuwa Theofilo ndiye aliyeandikiwa kitabu cha Luka, ni wazi kwamba masimulizi haya ni mwendelezo wa Injili hiyo. Katika kitabu cha Matendo, Luka anaanza kwa kutoa muhtasari wa mambo yanayotajwa mwishoni mwa Injili yake, akitumia maneno tofauti kidogo na kuongezea habari mpya.

      5, 6. (a) Ni nini kilichoimarisha imani ya wafuasi wa Yesu? (b) Ni kwa njia gani imani ya Wakristo leo inategemea “uthibitisho mwingi wenye kusadikisha”?

      5 Ni nini kilichoimarisha imani ya wafuasi wa Yesu? Andiko la Matendo 1:3 linasema hivi kumhusu Yesu: “Alijionyesha kwao akiwa hai kupitia uthibitisho mwingi wenye kusadikisha.” Katika Biblia, Luka peke yake, yule “daktari mpendwa,” ndiye anayetumia maneno ‘uthibitisho wenye kusadikisha.’ (Kol. 4:14) Maneno hayo yalitumiwa katika maandishi ya kitiba, na yanamaanisha uthibitisho unaoonekana wazi, uliohakikishwa, na wenye kutegemeka. Yesu alitoa uthibitisho wa aina hiyo. Aliwatokea wafuasi wake mara nyingi. Nyakati fulani alimtokea mmoja au wawili, nyakati nyingine akawatokea mitume wote, na pindi moja aliwatokea ndugu zaidi ya 500. (1 Kor. 15:3-6) Uthibitisho wenye kusadikisha kwelikweli!

      6 Imani ya Wakristo wa kweli leo pia inategemea “uthibitisho mwingi wenye kusadikisha.” Je, kuna uthibitisho wowote kwamba Yesu aliishi duniani, akafa kwa ajili ya dhambi zetu, kisha akafufuliwa? Ndiyo! Masimulizi yenye kutegemeka ya watu waliojionea matukio hayo yaliyo katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho, yanatoa uthibitisho wa kutosha wenye kusadikisha. Kusoma masimulizi hayo na kumwomba Yehova atusaidie kutumia mambo tunayojifunza maishani kutaimarisha sana imani yetu. Imani ya kweli hutegemea uthibitisho ulio wazi nayo ni muhimu ili kupata uzima wa milele.​—Yoh. 3:16.

      7. Yesu aliwawekea wafuasi wake mfano gani katika kazi ya kuhubiri na kufundisha?

      7 Yesu alikuwa ‘akizungumza nao kuhusu Ufalme wa Mungu.’ Kwa mfano, alieleza unabii mbalimbali ulioonyesha kwamba Masihi angeteseka na kufa. (Luka 24:13-32, 46, 47) Akiwa Mfalme Aliyechaguliwa, Yesu aliwasaidia watu kuelewa jukumu lake akiwa Masihi, kwa kuukazia Ufalme wa Mungu. Sikuzote, kichwa kikuu cha mahubiri yake kilikuwa Ufalme. Leo pia wafuasi wake hukazia Ufalme huo wanapohubiri.​—Mt. 24:14; Luka 4:43.

      “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia” (Mdo. 1:6-12)

      8, 9. (a) Ni mambo gani mawili ambayo mitume wa Yesu hawakuelewa vizuri? (b) Yesu aliwasaidia jinsi gani, na Wakristo leo wanaweza kujifunza nini?

      8 Yesu alifanya mkutano wa mwisho na mitume wake katika Mlima wa Mizeituni. Wakiwa na hamu kubwa ya kujua walimuuliza: “Bwana, je, unaurudisha ufalme kwa Israeli wakati huu?” (Mdo. 1:6) Swali hilo lilifunua mambo mawili ambayo hawakuelewa vizuri. Kwanza, walifikiri kwamba Ufalme wa Mungu ungerudishwa kwa Waisraeli. Pili, walitarajia Ufalme ulioahidiwa uanze kutawala ‘wakati huo.’ Yesu aliwasaidiaje?

      9 Kuhusu jambo la kwanza, yaelekea Yesu alijua wangelielewa vizuri baada ya siku chache. Kwa kweli, siku kumi tu baadaye, wafuasi wake wangejionea kuzaliwa kwa taifa jipya, Israeli la kiroho! Baada ya muda mfupi, Mungu angeacha kushughulika na taifa la Israeli. Kuhusu jambo la pili, Yesu aliwakumbusha hivi kwa fadhili: “Si juu yenu kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.” (Mdo. 1:7) Yehova ndiye huamua nyakati na majira. Kabla ya kufa, Yesu mwenyewe alisema kwamba hata Mwana hakujua “siku hiyo na saa hiyo” ambayo mwisho ungekuja. Aliyejua ni “Baba tu.” (Mt. 24:36) Leo pia, Wakristo wakihangaikia kupita kiasi kuhusu wakati ambapo mwisho utakuja, watakuwa wanajihangaisha na jambo ambalo haliwahusu.

      10. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani ulioonyeshwa na mitume, na kwa nini?

      10 Hata hivyo, haimaanishi kwamba mitume wa Yesu hawakuwa na imani. Walionyesha unyenyekevu kwa kukubali kurekebishwa. Isitoshe, ijapokuwa waliuliza kwa kutojua, swali hilo lilifunua mtazamo mzuri waliokuwa nao. Yesu alikuwa amewahimiza wafuasi wake mara nyingi ‘waendelee kukesha.’ (Mt. 24:42; 25:13; 26:41) Hivyo, swali lao lilionyesha kwamba walikuwa macho kiroho, wakitafuta kwa hamu uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba Yehova yuko karibu kuchukua hatua. Tunapaswa kuwa na mtazamo kama huo leo, hasa kwa kuwa tunaishi mwishoni mwa “siku za mwisho.”​—2 Tim. 3:1-5.

      11, 12. (a) Yesu aliwapa wafuasi wake kazi gani? (b) Kwa nini Yesu alitaja roho takatifu alipokuwa akiwapa wafuasi wake kazi ya kuhubiri?

      11 Yesu aliwakumbusha mitume wake jambo kuu wanalopaswa kuhangaikia. Alisema: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Habari za kufufuliwa kwa Yesu zingetangazwa kwanza katika jiji la Yerusalemu, ambapo aliuawa. Kisha, ujumbe huo ungeenezwa sehemu zote za Yudea, Samaria, na maeneo ya mbali zaidi.

      12 Yesu aliwapa kazi ya kuhubiri baada ya kuwakumbusha ahadi yake kwamba atatuma roho takatifu iwasaidie. Maneno “roho takatifu” yanatajwa katika kitabu cha Matendo zaidi ya mara 40. Kitabu hiki cha Biblia kinaonyesha wazi kwamba hatuwezi kutimiza mapenzi ya Yehova bila msaada wa roho takatifu. Hivyo, tunapaswa kusali kwa ukawaida ili tupate roho hiyo. (Luka 11:13) Leo, kuliko wakati mwingine wowote tunaihitaji sana roho hiyo.

      13. Kazi ya kuhubiri ambayo watu wa Mungu wamepewa leo ni kubwa kadiri gani, na kwa nini tunapaswa kuikubali kwa moyo wote?

      13 Katika siku zetu, “sehemu ya mbali zaidi ya dunia” inatia ndani maeneo mengi zaidi kuliko ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Hata hivyo, kama tulivyoona katika sura ya kwanza, Mashahidi wa Yehova wamekubali mgawo huo kwa moyo wote, wakijua kwamba Mungu anataka watu wa namna zote wahubiriwe habari njema ya Ufalme wake. (1 Tim. 2:3, 4) Je, unafanya kazi hiyo ya kuokoa uhai kwa bidii? Hiyo ndiyo kazi yenye kuridhisha sana! Yehova atakupa nguvu unazohitaji kutimiza kazi hiyo. Kitabu cha Matendo kitakueleza mbinu zinazofaa na mtazamo unaopaswa kuwa nao ili ufanikiwe.

      14, 15. (a) Malaika walisema Kristo atarudi jinsi gani, nao walimaanisha nini? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Ni katika maana gani Kristo alirudi “vivyo hivyo” alivyoondoka?

      14 Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa sura hii, Yesu alipokuwa akipaa kuelekea mbinguni, mitume wake 11 walibaki wakiwa wamesimama huku wakikaza macho yao kuelekea mbinguni. Mwishowe, malaika wawili wakatokea na kuwashauri hivi kwa fadhili: “Wanaume wa Galilaya, kwa nini mnasimama mkitazama angani? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda angani atakuja vivyo hivyo kama vile ambavyo mmemwona akienda angani.” (Mdo. 1:11) Je, walimaanisha kwamba Yesu angerudi katika mwili uleule kama vile viongozi fulani wa dini wanavyofundisha? Hapana. Tunajuaje?

      15 Malaika hao hawakusema kwamba Yesu angerudi katika umbo au mwili uleule, bali kwamba angerudi “vivyo hivyo,” au kwa njia hiyohiyo.b Aliondoka jinsi gani? Tayari alikuwa amefunikwa na mawingu malaika hao walipokuwa wakizungumza. Ni watu wachache tu, yaani mitume, ndio waliojua kwamba Yesu ameondoka duniani na kurudi mbinguni kwa Baba yake. Kristo angerudi vivyo hivyo. Na ndivyo alivyorudi. Leo, ni wale tu walio na utambuzi wa kiroho ndio wanaotambua kwamba Yesu amerudi katika maana ya kwamba sasa anatawala. (Luka 17:20) Tunahitaji kuwa macho ili kuona mambo mbalimbali yanayothibitisha kuwapo kwake na kuwaeleza wengine ili wao pia watambue kwamba mwisho unakaribia sana.

      “Onyesha Ni Nani . . . Ambaye Umemchagua” (Mdo. 1:13-26)

      16-18. (a) Tunajifunza nini katika Matendo 1:13, 14, kuhusu mikutano ya Kikristo? (b) Ni kwa njia gani Maria mama ya Yesu ni mfano mzuri kwetu leo? (c) Kwa nini mikutano ya Kikristo ni muhimu leo?

      16 Ni wazi kwamba mitume ‘walirudi Yerusalemu wakiwa na shangwe kubwa.’ (Luka 24:52) Hata hivyo, walitumia jinsi gani mwongozo na maagizo ya Kristo? Matendo 1:13, 14, inasema kwamba walikuwa wamekusanyika katika “chumba cha juu.” Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mistari hiyo kuhusu mikutano. Nyumba za Palestina zilikuwa na vyumba vya juu. Mtu angeweza kuingia katika chumba cha juu kwa kutumia ngazi iliyojengwa nje ya nyumba. Je, inawezekana kwamba “chumba cha juu” kinachotajwa katika mistari hiyo kilikuwa juu ya nyumba ya mama ya Marko ambayo inatajwa katika Matendo 12:12? Vyovyote vile, palikuwa mahali panapofaa kwa ajili ya mikutano ya wafuasi wa Kristo. Ni nani waliokutanika hapo, nao walifanya nini?

      17 Mkutano huo haukuhudhuriwa na mitume, au wanaume tu. Ulihudhuriwa pia na “wanawake fulani” kutia ndani Maria mama ya Yesu. Hii ndiyo mara ya mwisho Maria huyo anatajwa moja kwa moja katika Biblia. Inapendeza kuona Maria hatafuti umashuhuri, bali ni mnyenyekevu na amekusanyika ili kuabudu pamoja na ndugu na dada zake wa kiroho. Lazima alifurahi sana kuona watoto wake wanne ambao hawakumwamini Yesu alipokuwa duniani, wakiwa pamoja naye. (Mt. 13:55; Yoh. 7:5) Walibadili mtazamo wao baada ya Yesu kufa na kufufuliwa.​—1 Kor. 15:7.

      18 Pia, usisahau kusudi la mkutano huo: “Wote hawa walidumu katika sala kwa kusudi moja.” (Mdo. 1:14) Wakristo huiona mikutano kuwa sehemu muhimu ya ibada yao. Sisi hukutana ili kutiana moyo, kufundishwa na kupata mashauri, na zaidi ya yote, kumwabudu pamoja Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Sala na nyimbo zetu humpendeza sana, na ni muhimu. Tusikose kamwe kuhudhuria pindi hizo takatifu na zenye kujenga!—Ebr. 10:24, 25.

      19-21. (a) Tunajuaje kwamba Petro alifanya maendeleo ya kiroho, na hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova? (b) Kwa nini nafasi ya Yuda ilihitaji kujazwa, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi jambo hilo lilivyoshughulikiwa?

      19 Sasa, suala muhimu lilitokea katika kutaniko la Kikristo, naye mtume Petro akalishughulikia. (Mstari wa 15-26) Inatia moyo sana kuona kwamba Petro alikuwa amepiga hatua kubwa kiroho hasa tunapokumbuka kwamba majuma kadhaa yaliyotangulia alikuwa amemkana Bwana wake mara tatu! (Marko 14:72) Sote ni watenda dhambi, na mara kwa mara tunahitaji kukumbushwa kwamba Yehova ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe’ wale wanaotubu kutoka moyoni.​—Zab. 86:5.

      20 Petro alitambua kwamba mtu mwingine anapaswa kuchukua mahali pa Yuda, mtume aliyemsaliti Yesu. Lakini ni nani angechukua mahali pake? Mtume atakayechaguliwa anapaswa kuwa mfuasi wa Yesu tangu mwanzo wa huduma yake na ambaye alishuhudia ufufuo wake. (Mdo. 1:21, 22) Hilo lapatana na ahadi hii ya Yesu: “Ninyi ambao mmenifuata mtaketi katika viti vya ufalme 12, mkiyahukumu makabila 12 ya Israeli.” (Mt. 19:28) Inaonekana Yehova alikusudia kwamba kati ya wafuasi wa Yesu, kuwe na mitume 12 ambao baadaye wangekuja kuwa “mawe ya msingi 12” ya Yerusalemu Jipya. (Ufu. 21:2, 14) Hivyo, Mungu alimwezesha Petro kutambua kwamba unabii unaosema “mtu mwingine na achukue cheo chake cha uangalizi,” unamhusu Yuda.​—Zab. 109:8.

      21 Mtu huyo angechaguliwa jinsi gani? Kwa kupiga kura, kama ilivyokuwa kawaida katika nyakati za Biblia. (Met. 16:33) Hata hivyo, hii ndiyo mara ya mwisho katika Biblia ambapo kura ilitumiwa kwa njia hiyo. Inaonekana kwamba baadaye, roho takatifu ilipomiminwa, zoea hilo lilikoma. Hata hivyo, kwa nini kura zilitumiwa? Mitume walisali: “Wewe, Ee Yehova, unayejua mioyo ya wote, onyesha ni nani kati ya watu hawa wawili ambaye umemchagua.” (Mdo. 1:23, 24) Walitaka Yehova achague. Mathia, ambaye yaelekea alikuwa mmoja wa wale wanafunzi 70 ambao Yesu aliwatuma kuhubiri, alichaguliwa. Hivyo, Mathia akawa mmoja wa “wale 12.”c—Mdo. 6:2.

      22, 23. Kwa nini tunapaswa kunyenyekea na kuwatii wale wanaoongoza katika kutaniko leo?

      22 Kisa hicho kinatukumbusha kwamba watu wa Mungu wanapaswa kufanya mambo kitengenezo. Leo pia, wanaume wanaostahili huwekwa rasmi kutumikia wakiwa waangalizi katika makutaniko. Wazee huchunguza kwa makini sifa ambazo waangalizi hao wanapaswa kutimiza, nao huomba mwongozo wa roho takatifu. Hivyo, kutaniko huwaona wanaume hao kuwa wamewekwa rasmi na roho takatifu. Sisi hufuata mwongozo wao na kuchochea roho ya ushirikiano kutanikoni.​—Ebr. 13:17.

      Baraza la wazee likiwa katika mkutano.

      Sisi hunyenyekea na kuwatii waangalizi waliowekwa rasmi

      23 Kwa kuwa sasa wanafunzi hao walikuwa wameimarishwa kwa kutokewa na Yesu baada ya ufufuo wake na kutiwa nguvu na mabadiliko ya kitengenezo, walikuwa tayari kabisa kwa ajili ya mambo ambayo yangetokea. Sura inayofuata itazungumzia tukio hilo la pekee.

      a Watu fulani huamini kwamba Theofilo alikuwa mtu mashuhuri ambaye hakuwa mwamini wakati huo, kwa kuwa katika Injili yake, Luka anamwita “mheshimiwa Theofilo.” (Luka 1:3) Lakini kwa sababu katika kitabu cha Matendo, Luka anamwita, “Ewe Theofilo,” wasomi fulani wanasema kwamba Theofilo alikuja kuwa mwamini baada ya kusoma Injili ya Luka; na ndiyo sababu Luka anaacha kumwita “mheshimiwa” na kumwandikia kama ndugu Mkristo.

      b Biblia inatumia neno la Kigiriki troʹpos, linalomaanisha “jinsi,” bali si neno mor·pheʹ, linalomaanisha “umbo.”

      c Baadaye Paulo alichaguliwa kuwa “mtume kwa mataifa,” lakini hakuhesabiwa kamwe miongoni mwa wale Kumi na Wawili. (Rom. 11:13; 1 Kor. 15:4-8) Kwa kuwa hakuwa mfuasi wa Yesu wakati wa huduma yake hapa duniani, hakustahili pendeleo hilo la pekee.

  • “Wakajazwa Roho Takatifu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 3

      “Wakajazwa Roho Takatifu”

      Matokeo ya kumiminwa kwa roho takatifu siku ya Pentekoste

      Matendo 2:1-47

      1. Eleza hali ilivyokuwa wakati wa Sherehe ya Pentekoste.

      KUNA msisimuko mwingi katika jiji la Yerusalemu.a Moshi unapaa kutoka katika madhabahu ya hekalu huku Walawi wakiimba Haleli (Zaburi 113 hadi 118). Huenda kikundi kimoja kiliimba huku kingine kikiitikia. Kuna watu wengi barabarani. Wametoka sehemu za mbali sana kama vile Elamu, Mesopotamia, Kapadokia, Ponto, Misri, na Roma.b Wamekuja kwa kusudi gani? Ili kusherehekea Pentekoste, ambayo pia inaitwa “siku ya mavuno ya kwanza yaliyokomaa.” (Hes. 28:26) Sherehe hii hufanywa mara moja kila mwaka mwishoni mwa mavuno ya shayiri, kabla ya mavuno ya ngano kuanza. Ni siku ya shangwe sana.

      Ramani inayoonyesha maeneo waliyotoka wale waliohubiriwa habari njema katika Pentekoste 33 W.K. 1. Mikoa: Libya, Misri, Ethiopia, Bithinia, Ponto, Kapadokia, Yudea, Mesopotamia, Babilonia, Elamu, Umedi, na Parthia. 2. Miji: Roma, Aleksandria, Memfisi, Antiokia (ya Siria), Yerusalemu, na Babiloni. 3. Bahari: Bahari ya Mediterania, Bahari Nyeusi, Bahari Nyekundu, Bahari ya Kaspian, na Ghuba ya Uajemi.

      YERUSALEMU—CHIMBUKO LA DINI YA KIYAHUDI

      Mambo mengi yanayotajwa katika sura za mwanzoni za kitabu cha Matendo yanatendeka Yerusalemu. Jiji hilo liko kwenye milima ya Yudea, kilomita 55 hivi upande wa mashariki mwa Bahari ya Mediterania. Katika mwaka wa 1070 K.W.K., Mfalme Daudi alishambulia na kuteka ngome iliyokuwa juu ya Mlima Sayuni, nalo jiji hilo ambalo lilizunguka mlima huo likaja kuwa jiji kuu la taifa la kale la Israeli.

      Karibu na Mlima Sayuni, kuna Mlima Moria, ambao kulingana na mapokeo ya Wayahudi, Abrahamu alijaribu kumtoa Isaka kuwa dhabihu, miaka 1,900 hivi kabla ya matukio yanayosimuliwa katika kitabu cha Matendo. Mlima Moria ulikuja kuwa sehemu ya jiji hilo, Sulemani alipojenga hekalu la kwanza la Yehova juu ya mlima huo. Hekalu hilo likawa kituo cha ibada na shughuli mbalimbali za Wayahudi.

      Wayahudi waliomwogopa Mungu kutoka sehemu mbalimbali duniani walikwenda katika hekalu la Yehova ili kutoa dhabihu, kuabudu, na kuadhimisha sherehe za kila mwaka. Walikuwa wakitii amri hii ya Mungu: “Mara tatu kwa mwaka, wanaume wenu wote wanapaswa kwenda mbele za Yehova Mungu wenu mahali atakapochagua.” (Kum. 16:16) Sanhedrini, mahakama kuu ya Wayahudi iliyokuwa pia baraza lililosimamia mambo ya kitaifa, ilikuwa katika jiji hilo la Yerusalemu.

      2. Ni mambo gani yenye kushangaza yanayotokea siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K.?

      2 Saa tatu hivi asubuhi, mwaka wa 33 W.K., jambo fulani la ajabu latokea, ambalo litawashangaza watu kwa karne nyingi zijayo. Ghafla kukatokea “kelele kutoka mbinguni, kama ya upepo wenye nguvu unaovuma.” (Mdo 2:2) Mvumo huo waijaza nyumba ambapo wanafunzi wa Yesu wapatao 120 walikuwa wamekusanyika. Kisha, jambo la kushangaza latokea. Ndimi, kama za moto, zaonekana. Wanafunzi hao wakaona ndimi kama za moto zikitua juu ya kila mmoja wao.c Ndipo, wanafunzi hao ‘wakajazwa roho takatifu’ na kuanza kusema katika lugha mbalimbali! Wanafunzi wanapotoka tu katika nyumba hiyo, watu kutoka sehemu mbalimbali walio katika barabara za Yerusalemu wanashangaa sana! Kila mtu anawasikia wanafunzi hao “wakiongea katika lugha yake mwenyewe.”​—Mdo. 2:1-6.

      3. (a) Kwa nini Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. inaweza kuitwa tukio muhimu sana katika ibada ya kweli? (b) Kuna uhusiano gani kati ya hotuba ya Petro na zile “funguo za Ufalme”?

      3 Masimulizi hayo yenye kusisimua yanahusu tukio muhimu sana katika ibada ya kweli—kuanzishwa kwa taifa la Israeli la kiroho, kutaniko la Wakristo watiwa mafuta. (Gal. 6:16) Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika. Petro anapotoa hotuba yake mbele ya umati uliokusanyika siku hiyo, anatumia ufunguo wa kwanza kati ya zile ‘funguo tatu za Ufalme.’ Kila moja ya funguo hizo ingefungulia kikundi fulani cha watu mapendeleo ya pekee. (Mt. 16:18, 19) Ufunguo huo wa kwanza uliwawezesha Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani kukubali habari njema na kutiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu.d Wangeweza kuwa sehemu ya Israeli la kiroho, na hivyo, kuwa na tumaini la kutawala wakiwa wafalme na makuhani katika Ufalme wa Kimasihi. (Ufu. 5:9, 10) Kisha, Wasamaria na baadaye watu wa mataifa wangepata pendeleo hilo pia. Leo, Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na matukio hayo muhimu ya siku ya Pentekoste?

      “Walikuwa Pamoja Mahali Palepale” (Mdo. 2:1-4)

      4. Eleza jinsi kutaniko la Kikristo lilivyoanza na kuendelea mpaka leo hii.

      4 Kutaniko la kwanza la Kikristo lilianza likiwa na wanafunzi 120 hivi ambao “walikuwa pamoja mahali palepale,” katika chumba cha juu. Wote walikuwa wametiwa mafuta na roho takatifu. (Mdo. 2:1) Kufikia mwishoni mwa siku hiyo, washiriki waliobatizwa wa kutaniko hilo walikuwa elfu kadhaa. Huo ulikuwa mwanzo tu wa tengenezo ambalo linaendelea kukua hadi leo! Katika kutaniko la Kikristo leo, wanaume na wanawake wanaomwogopa Mungu, wanahubiri “habari njema ya Ufalme” katika “dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote” kabla ya mwisho wa mfumo huu wa mambo.​—Mt. 24:14.

      5. Ni baraka gani zinazotokana na kushirikiana na kutaniko la Kikristo?

      5 Kutaniko la Kikristo lingewaimarisha kiroho washiriki wake, watiwa mafuta, na baadaye “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Paulo alithamini jinsi washiriki wa kutaniko wanavyotegemezana alipowaandikia Wakristo huko Roma: “Ninatamani kuwaona ninyi ili niwape zawadi ya kiroho kusudi mfanywe imara; au badala yake, tutiane moyo, kila mmoja kupitia imani ya mwenzake, yenu na yangu pia.”​—Rom. 1:11, 12.

      Roma—jiji Kuu La Milki Ya Roma

      Kipindi ambacho kinazungumziwa katika kitabu cha Matendo, Roma lilikuwa jiji kubwa zaidi na muhimu kisiasa katika ulimwengu wa wakati huo. Lilikuwa jiji kuu la milki ambayo wakati huo ilitawala nchi nyingi kuanzia Uingereza mpaka Afrika Kaskazini na toka Bahari ya Atlantiki mpaka Ghuba ya Uajemi.

      Katika jiji la Roma kulikuwa na tamaduni, jamii, lugha, na ushirikina kutoka nchi mbalimbali. Kwa kuwa kulikuwa na barabara nzuri, jiji hilo lilipata wageni wengi na bidhaa nyingi kutoka katika kila pembe ya milki hiyo. Meli za biashara zilizokuwa na shehena ya vyakula na bidhaa nyingine za starehe zilitia nanga katika bandari ya Ostia na kupakua shehena hizo.

      Kufikia karne ya kwanza W.K., zaidi ya watu milioni moja walikuwa wakiishi Roma. Huenda nusu yao walikuwa watumwa—wahalifu, watoto waliouzwa au kuachwa na wazazi wao, na wafungwa waliotekwa nyara na majeshi ya Roma. Baadhi ya watu walioletwa Roma wakiwa watumwa walikuwa Wayahudi kutoka Yerusalemu waliokamatwa baada ya jiji lao kushindwa vitani na Jenerali Mroma, Pompey, mwaka wa 63 K.W.K.

      Wengi kati ya wale ambao hawakuwa watumwa walikuwa maskini sana na waliishi katika nyumba za ghorofa zilizojengwa kwa ajili ya maskini waliotegemea misaada kutoka serikalini. Hata hivyo, watawala wa milki hiyo walijenga majengo ya kifahari na ya kipekee sana yaliyofanya jiji hilo liwe lenye kupendeza. Baadhi ya majengo hayo ni yale majumba ya maonyesho na viwanja vya michezo. Majengo hayo yalitumiwa kwa ajili ya tamasha, mapigano yenye jeuri, na mashindano ya magari ya farasi ili kuwatumbuiza wakaaji wa Roma bila malipo yoyote.

      6, 7. Kutaniko la Kikristo leo linatimizaje kazi ya kuwahubiria watu wa mataifa yote?

      6 Leo, kutaniko la Kikristo linatimiza mambo yaleyale yaliyotimizwa na kutaniko la karne ya kwanza. Yesu aliwapa wanafunzi wake kazi yenye kusisimua licha ya upinzani ambao wangepata. Aliwaagiza hivi: “Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”​—Mt. 28:19, 20.

      7 Yehova analitumia kutaniko la Kikristo kutimiza kazi hiyo leo. Si rahisi kuwahubiria watu wanaozungumza lugha tofauti. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wamechapisha machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha zaidi ya 1,000. Ikiwa unahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na unashiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi, una kila sababu ya kushangilia. Wewe ni mmoja wa watu wachache duniani ambao wana pendeleo la kutoa ushahidi kamili kuhusu jina la Yehova!

      8. Kushirikiana na kutaniko la Kikristo kunatusaidiaje?

      8 Ili kutusaidia kuendelea kuwa na shangwe katika nyakati hizi za hatari, Yehova Mungu ametupatia ushirika wa ulimwenguni pote wa akina ndugu. Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Yehova ameandaa kutaniko la Kikristo ili tutiane moyo. Shirikiana kwa ukaribu pamoja na ndugu na dada zako wa kiroho. Usiache kamwe kuhudhuria mikutano ya Kikristo!

      “Kila Mmoja Wao Aliwasikia . . . Katika Lugha Yake Mwenyewe” (Mdo. 2:5-13)

      Wanafunzi wa Yesu wakiwahubiria Wayahudi na wageuzwa imani kwenye mtaa wenye shughuli nyingi.

      “Tunawasikia wakisema katika lugha zetu kuhusu mambo makuu ya Mungu.”—Matendo 2:11

      9, 10. Wahubiri fulani wamefanya jitihada gani ili kuwahubiria watu wanaozungumza lugha nyingine?

      9 Wazia msisimuko waliokuwa nao Wayahudi na wageuzwa imani katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K. Yaelekea wengi wao walijua Kigiriki au Kiebrania, lugha kuu za wakati huo. Lakini sasa “kila mmoja wao aliwasikia [wanafunzi] wakiongea katika lugha yake mwenyewe.” (Mdo. 2:6) Bila shaka hisia za watu hao zilichochewa sana waliposikia habari njema katika lugha zao wenyewe. Ijapokuwa Wakristo leo hawana uwezo wa kimuujiza wa kuzungumza lugha za kigeni, wengi wamejitolea kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa watu wa mataifa yote. Wamefanya hivyo jinsi gani? Baadhi yao wamejifunza lugha nyingine ili watumikie katika kutaniko la lugha ya kigeni lililo karibu au hata kuhamia nchi nyingine. Mara nyingi wahubiri hao wameona kwamba watu huvutiwa sana wanapoona jinsi wanavyojitahidi kuzungumza lugha zao.

      10 Kwa mfano, Christine na Mashahidi wengine saba walijifunza Kigujarati. Siku moja alimsalimu mfanyakazi mwenzake Mgujarati, kwa Kigujarati. Mwanamke huyo alivutiwa sana, akataka kujua kwa nini Christine anajifunza lugha ngumu kama Kigujarati. Christine alitumia nafasi hiyo kumhubiria. Mwanamke huyo alimwambia Christine: “Lazima ujumbe wenu ni wa muhimu sana.”

      11. Tunawezaje kujitayarisha kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa watu wanaozungumza lugha nyingine?

      11 Bila shaka, si kila mtu anayeweza kujifunza lugha nyingine. Hata hivyo, tunaweza kuwa tayari kuwahubiria watu wanaozungumza lugha nyingine. Jinsi gani? Njia moja ni kwa kujifunza salamu rahisi katika lugha zinazotumiwa kwa ukawaida katika eneo lenu kwa kutumia programu ya JW Language®. Pia, unaweza kujifunza maneno machache ya lugha hiyo yatakayokusaidia kuchochea upendezi wa watu wanaozungumza lugha hiyo. Waelekeze kwenye tovuti ya jw.org, na unaweza kuwaonyesha video na machapisho mbalimbali yanayopatikana katika lugha yao. Kwa kutumia vifaa kama hivyo katika huduma yetu, tunaweza kupata shangwe kama ile waliyoipata ndugu katika karne ya kwanza, watu wa mataifa mbalimbali waliposhangaa kusikia habari njema “kila mmoja . . . katika lugha yake mwenyewe.”

      Wayahudi Nchini Misri Na Mesopotamia

      Kitabu fulani kinasema hivi: “Katika maeneo ya Mesopotamia, Umedi na Babilonia kulikuwa na watu waliotoka katika familia za ufalme wa makabila kumi [ya Israeli], na ufalme wa Yuda, waliohamishiwa huko na Wasiria na Wababiloni.” (The History of the Jewish People in the Age of Jesus Christ—175 B.C.–A.D. 135) Kulingana na Ezra 2:64, Waisraeli waliorudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. kutoka uhamishoni Babiloni walikuwa 42,360. Flavio Yosefu anasema kwamba katika karne ya kwanza W.K., idadi ya Wayahudi waliokuwa “wakiishi Babilonia” ilikuwa makumi ya maelfu. Katika karne ya tatu mpaka ya tano W.K., jamii hizo ziliandika kitabu kinachoitwa Talmud ya Babiloni.

      Kuna hati zinazothibitisha kwamba Wayahudi waliishi Misri angalau kuanzia karne ya sita K.W.K. Wakati huo Yeremia alituma ujumbe kwa Wayahudi walioishi katika sehemu mbalimbali za Misri, kutia ndani Memfisi. (Yer. 44:1, maelezo ya chini) Kuna uwezekano kwamba watu wengi walihamia Misri wakati wa utawala wa Ugiriki. Mwanahistoria Yosefu anasema kwamba Wayahudi walikuwa miongoni mwa watu wa kwanza kuishi Aleksandria. Baada ya muda, walimiliki sehemu kubwa ya jiji hilo. Katika karne ya kwanza W.K., Philo mwandishi Myahudi, alidai kwamba Wayahudi milioni moja hivi walikuwa wakiishi katika maeneo mbalimbali nchini Misri, “kuanzia Libya hadi Ethiopia.”

      “Petro Akasimama” (Mdo. 2:14-37)

      12. (a) Nabii Yoeli alirejelea matukio ya Pentekoste jinsi gani? (b) Kwa nini watu wa karne ya kwanza walitazamia utimizo wa unabii wa Yoeli?

      12 “Petro akasimama” ili kuzungumza na umati huo wa watu kutoka mataifa mbalimbali. (Mdo. 2:14) Alieleza kwamba Mungu alikuwa amewapa uwezo wa kimuujiza wa kusema katika lugha mbalimbali ili kutimiza unabii wa Yoeli unaosema: “Nitaimimina roho yangu juu ya kila aina ya mwili.” (Yoe. 2:28) Kabla ya kurudi mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Nitamwomba Baba naye atawapa msaidizi mwingine.” Yesu alisema msaidizi huyo ni “roho.”​—Yoh. 14:16, 17.

      13, 14. Petro alifanya nini ili kuichochea mioyo ya wasikilizaji wake, nasi tunaweza kumwiga jinsi gani?

      13 Petro alimalizia hotuba yake kwa maneno haya ya moja kwa moja: “Nyumba yote ya Israeli na ijue kwa hakika kwamba Mungu alimfanya Bwana na pia Kristo, Yesu huyu ambaye ninyi mlimuua kwenye mti.” (Mdo. 2:36) Ijapokuwa wengi kati ya watu waliokuwa wakimsikiliza Petro hawakuwapo Yesu alipouawa juu ya mti wa mateso, taifa lote lilikuwa na hatia. Hata hivyo, Petro alizungumza na Wayahudi wenzake kwa heshima naye alijali hisia zao. Kusudi la Petro lilikuwa kuwachochea wasikilizaji wake watubu bali si kuwashutumu. Je, umati uliokuwa ukimsikiliza ulikasirishwa na maneno ya Petro? Hapana. Badala yake, watu hao “walichomwa moyoni.” Wakauliza: “Tufanye nini?” Yaelekea njia ya Petro ya kuzungumza nao kwa heshima ilimsaidia kuifikia mioyo ya wengi, hata wakachochewa kutubu.​—Mdo. 2:37.

      14 Sisi pia, tunaweza kufanya kama Petro. Tunapohubiri, hatuhitaji kupinga kila jambo lisilopatana na Maandiko ambalo huenda mwenye nyumba akasema. Badala yake, ingefaa kuzungumzia mambo tunayoweza kukubaliana. Tukishakubaliana na wasikilizaji wetu, kwa busara tunaweza kuwasaidia kuona maoni ya Neno la Mungu. Mara nyingi, kweli za Biblia zinapozungumziwa kwa njia hiyo, watu wenye mioyo minyoofu wanaweza kukubali ujumbe wetu.

      Ukristo Katika Mkoa Wa Ponto

      Kati ya watu waliosikiliza hotuba ya Petro siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. walikuwa Wayahudi kutoka Ponto, wilaya iliyo kaskazini mwa Asia Ndogo. (Mdo. 2:9) Kwa kuwa wale ambao Petro aliwatumia barua yake ya kwanza walitia ndani waamini “waliotawanyika” katika mkoa wa Ponto, inaonekana kwamba baadhi ya Wayahudi walirudi na habari njema nyumbani kwao.g (1  Pet. 1:1) Aliandika kwamba Wakristo hao walikuwa ‘wamehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali’ kwa sababu ya imani yao. (1 Pet. 1:6) Huenda majaribu hayo yalitia ndani upinzani na mateso.

      Majaribu mengine yaliyowapata Wakristo huko Ponto yanarejelewa kwa njia isiyo ya moja kwa moja katika mawasiliano kati ya Plini Mdogo, aliyekuwa gavana wa jimbo la Bithinia na Ponto, na Maliki Trajani. Akiandika kutoka Ponto karibu mwaka wa 112 W.K., Plini alisema kwamba kila mtu, haidhuru jinsia yake, umri wake, au cheo chake angeweza “kuambukizwa” Ukristo. Plini aliwapa wale waliokuwa Wakristo nafasi ya kukana imani yao la sivyo, wauawe. Yeyote aliyemlaani Kristo au kusali kwa miungu au kwa sanamu ya Trajani, aliachiliwa huru. Plini alikiri kwamba hayo ni mambo ambayo “Wakristo wa kweli hawangeweza kufanya.”

      g Maneno yanayotafsiriwa “waliotawanyika” ni tafsiri ya neno la Kigiriki Di·a·spo·raʹ linalorejelea Wayahudi waliokuwa wametawanyika katika mataifa mengine. Maneno hayo yanadokeza kwamba wengi wa wageuzwa imani wa kwanza walitoka katika jamii za Wayahudi.

      “Kila Mmoja Wenu Abatizwe” (Mdo. 2:38-47)

      15. (a) Petro alisema nini, na watu waliitikiaje? (b) Iliwezekanaje kwamba maelfu ya watu waliosikia habari njema walistahili kubatizwa siku hiyohiyo?

      15 Katika siku hiyo yenye kusisimua ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Petro aliwaambia hivi Wayahudi na wageuzwa imani: “Tubuni, na kila mmoja wenu abatizwe.” (Mdo. 2:38) Kisha watu 3,000 hivi wakabatizwa, huenda katika vidimbwi vilivyokuwa Yerusalemu au karibu na jiji hilo.e Je, watu hao walichukua hatua hiyo bila kufikiri? Je, hilo linamaanisha kwamba wanafunzi wa Biblia na watoto ambao wazazi wao ni Wakristo wakimbilie kubatizwa kabla ya kuwa tayari? Hapana. Kumbuka, Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani waliobatizwa siku hiyo walikuwa wamejifunza Neno la Mungu, na taifa lao lilikuwa wakfu kwa Yehova. Isitoshe, tayari walikuwa na bidii, walikuwa wakifunga safari ndefu kwenda kuhudhuria sherehe hiyo ya kila mwaka. Baada ya kukubali kweli muhimu kuhusu jukumu la Yesu Kristo katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu, walikuwa tayari kuendelea kumtumikia Mungu—lakini sasa wakiwa wafuasi waliobatizwa wa Kristo.

      Wageuzwa Imani Ni Nani?

      “Wayahudi na pia wageuzwa imani” walimsikiliza Petro akihubiri katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K.​—Matendo 2:10.

      Nikolao ambaye alikuwa mmoja wa wanaume waliowekwa rasmi juu ya ‘kazi muhimu’ ya kugawa chakula kila siku, anatajwa kuwa “mgeuzwa-imani wa Antiokia.” (Matendo 6:3-5) Wageuzwa imani walikuwa watu wa mataifa mengine, wasio Wayahudi, ambao walijiunga na dini ya Kiyahudi. Walionwa kuwa Wayahudi, kwa sababu walimkubali Mungu wa Israeli na kuikubali Sheria ya Waisraeli, walikataa miungu mingine yote, (wanaume) walitahiriwa, nao walijiunga na taifa la Israeli.

      Baada ya Wayahudi kutoka uhamishoni Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., wengi wao waliishi mbali na nchi ya Israeli lakini waliendelea kuwa wafuasi wa dini ya Kiyahudi. Hivyo, watu wengi katika maeneo ya Mashariki ya Kati na hata mbali zaidi wakaifahamu dini ya Kiyahudi. Waandikaji wa zamani, kama vile, Horace na Seneca, wanaeleza kwamba watu wengi wa nchi mbalimbali waliovutiwa na Wayahudi na imani zao, walijiunga nao na kuwa wageuzwa imani.

      16. Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha jinsi gani roho ya kujidhabihu?

      16 Bila shaka, Yehova alibariki kikundi hicho. Masimulizi hayo yanasema: “Wale wote ambao sasa walikuwa waamini walikusanyika pamoja na wakashirikiana katika mambo yote, nao walikuwa wakiuza mali zao na vitu walivyomiliki na kuwagawia wote pesa walizopata, kulingana na uhitaji wa kila mtu.”f (Mdo. 2:44, 45) Kwa hakika, Wakristo wote wa kweli wanapaswa kuiga roho hiyo ya kujidhabihu kwa upendo.

      17. Ili mtu astahili kubatizwa anapaswa kufanya nini?

      17 Ili mtu ajiweke wakfu na kubatizwa lazima atimize matakwa fulani muhimu ya Kimaandiko. Lazima ajifunze Neno la Mungu. (Yoh. 17:3) Anahitaji kuwa na imani, atubu mwenendo wake wa zamani, na kujuta kikweli. (Mdo. 3:19) Kisha, lazima ageuke, au abadili mwenendo wake, na kuanza kufanya kazi nzuri zinazopatana na mapenzi ya Mungu. (Rom. 12:2; Efe. 4:23, 24) Baada ya kutimiza hatua hizo zote, anajiweka wakfu kwa Mungu katika sala na kubatizwa.​—Mt. 16:24; 1 Pet. 3:21.

      18. Wanafunzi waliobatizwa wa Kristo wana pendeleo gani?

      18 Je, wewe ni mwanafunzi wa Yesu Kristo, uliyejiweka wakfu na kubatizwa? Ikiwa ndivyo, unapaswa kuthamini sana pendeleo hilo. Kama wanafunzi wa karne ya kwanza waliojazwa roho takatifu, wewe pia unaweza kutoa ushahidi kamili na kufanya mapenzi ya Yehova!

      a Ona sanduku lenye kichwa “Yerusalemu—Chimbuko la Dini ya Kiyahudi.”

      b Ona sanduku lenye kichwa “Roma—Jiji Kuu la Milki ya Roma,” “Wayahudi Nchini Misri na Mesopotamia,”; na pia “Ukristo Katika Mkoa wa Ponto,”.

      c “Ndimi” hizo hazikuwa za moto halisi, bali “kama za moto,” yaani, ziling’aa na kuonekana kama ndimi za moto juu ya kila mwanafunzi.

      d Ona sanduku “Wageuzwa Imani Ni Nani?”.

      e Agosti 7, 1993, katika kusanyiko la kimataifa la Mashahidi wa Yehova huko Kiev, Ukrainia, watu 7,402 walibatizwa katika vidimbwi sita. Ubatizo huo ulichukua muda wa saa mbili na robo.

      f Mpango huo wa muda ulitosheleza uhitaji uliotokea kwa kuwa wageni walibaki Yerusalemu ili kujifunza mengi zaidi kuhusu imani hiyo mpya. Huo ulikuwa mpango wa hiari wa mtu kutoa mali yake, ili vitu vyote vitumiwe kwa ushirika. Haukuwa sera ya ujamaa.​—Mdo. 5:1-4.

  • “Watu Wasio na Elimu na wa Kawaida Tu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 4

      “Watu Wasio na Elimu na wa Kawaida Tu”

      Mitume watenda kwa ujasiri, Yehova awabariki

      Matendo 3:1–5:11

      1, 2. Petro na Yohana walifanya muujiza gani karibu na lango la hekalu?

      JUA la alasiri laangaza huku umati ukisongamana. Wayahudi wenye kumwogopa Mungu na wanafunzi wa Yesu wanamiminika kuingia katika ua wa hekalu. “Saa ya sala” inakaribia.a (Mdo. 2:46; 3:1) Wakiwa kati ya umati huo, Petro na Yohana wanaingia kuelekea lango la hekalu lililoitwa Lango Zuri. Katikati ya kelele za umati huo na vishindo vya miguu, mwombaji mwenye umri wa zaidi ya miaka 40, aliyezaliwa akiwa kilema, anaomba zawadi za rehema.​—Mdo. 3:2; 4:22.

      2 Petro na Yohana wanapokaribia, mwombaji huyo anawaomba pesa kama ilivyo kawaida yake. Mitume hao wanasimama, jambo linalompa mtu huyo matumaini. “Sina fedha wala dhahabu,” Petro akamwambia, “lakini kile nilicho nacho ndicho ninachokupa. Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, tembea!” Hebu wazia jinsi umati ulivyoshangaa ulipomwona Petro akimshika mkono, na kwa mara ya kwanza maishani mwake, anasimama wima! (Mdo. 3:6, 7) Wazia mtu huyo akitazama miguu yake iliyoponywa na kupiga hatua za kwanza maishani! Ndiyo sababu anaanza kurukaruka na kumsifu Mungu kwa sauti kubwa!

      3. Ni zawadi gani ambayo mtu aliyeponywa na umati ungepata?

      3 Umati huo wenye msisimko unawakimbilia Petro na Yohana walio kwenye safu ya nguzo za Sulemani. Wakiwa hapo, mahali ambapo wakati mmoja Yesu alisimama na kufundisha, Petro anawaambia maana ya mambo ambayo wamejionea. (Yoh. 10:23) Anasema kwamba umati huo, kutia ndani mtu aliyeponywa, wanaweza kupata zawadi yenye thamani zaidi kuliko fedha na dhahabu. Zawadi hiyo inatia ndani mengi zaidi kuliko afya nzuri. Anawapa nafasi ya kutubu ili dhambi zao zifutiliwe mbali, kisha wawe wafuasi wa Yesu Kristo, “Wakili Mkuu wa uzima,” aliyewekwa rasmi na Yehova.​—Mdo. 3:15.

      4. (a) Muujiza wa uponyaji ulitokeza mzozo gani? (b) Ni maswali gani mawili yatakayojibiwa?

      4 Ni siku ya furaha sana! Mtu mmoja ameponywa kimwili na sasa anaweza kutembea. Maelfu ya watu wamepewa nafasi ya kuponywa kiroho, ili waweze kutembea kwa kumstahili Mungu. (Kol. 1:9, 10) Isitoshe, mambo yaliyotokea siku hiyo yalitokeza mzozo kati ya wafuasi waaminifu wa Kristo na watu wenye mamlaka waliokuwa wakijaribu kuwazuia wasitimize amri ya Yesu ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Mdo. 1:8) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mtazamo na mbinu ambazo Petro na Yohana—“watu wasio na elimu na wa kawaida tu”​—walitumia walipouhubiria umati uliokuwa umekusanyika?b (Mdo. 4:13) Na tunapokabili upinzani, tunawezaje kuwaiga wanafunzi?

      Si “kwa Nguvu Zetu” (Mdo. 3:11-26)

      5. Petro aliuhubiria umati jinsi gani, nasi tunaweza kujifunza nini?

      5 Petro na Yohana walisimama mbele ya umati. Walijua kwamba huenda baadhi ya watu katika umati huo, ndio waliokuwa wakipiga kelele wakitaka Yesu atundikwe siku chache tu zilizopita. (Marko 15:8-15; Mdo. 3:13-15) Wazia ujasiri wa Petro alipotangaza kwamba mtu huyo aliyekuwa kilema ameponywa katika jina la Yesu. Petro hakujaribu kuficha ukweli. Maneno yake yalionyesha waziwazi kwamba umati huo ulikuwa na hatia ya kumuua Kristo. Hata hivyo, Petro hakuwa na kinyongo chochote kuelekea watu hao, kwa kuwa ‘walitenda kwa kutojua.’ (Mdo. 3:17) Aliwasihi kama ndugu zake na kukazia fikira mambo yenye kupendeza ya ujumbe wa Ufalme. Ikiwa wangetubu na kumwamini Kristo, wangepata “majira yenye kuburudisha” kutoka kwa Yehova. (Mdo. 3:19) Sisi pia tunapaswa kuwa na ujasiri, na kusema mambo waziwazi tunapotangaza hukumu ya Mungu inayokaribia. Hata hivyo, hatupaswi kuwa wakali, wasiojali hisia za watu, au kuwahukumu. Badala yake, tunawaona watu hao kuwa ndugu zetu wa wakati ujao. Na kama alivyofanya Petro, tunakazia hasa mambo yenye kupendeza ya ujumbe wa Ufalme.

      6. Petro na Yohana walionyesha unyenyekevu jinsi gani?

      6 Mitume hao walikuwa na sifa ya kiasi. Hawakudai kwamba walifanya muujiza huo kwa uwezo wao. Petro aliuliza umati huo: “Kwa nini mnatutazama kana kwamba tumemfanya atembee kwa nguvu zetu au kwa sababu ya ujitoaji-kimungu?” (Mdo. 3:12) Petro na wale mitume wengine walijua kwamba huduma yao ilikuwa na matokeo mazuri, si kwa sababu ya nguvu zao wenyewe, bali kwa sababu ya nguvu za Mungu. Walionyesha unyenyekevu kwa kumpa sifa Yehova na Yesu kwa sababu ya mafanikio waliyopata.

      7, 8. (a) Ni zawadi gani tunayoweza kuwapa watu? (b) Ahadi ya “kurudishwa kwa mambo yote” inatimizwa jinsi gani leo?

      7 Sisi pia tunapaswa kuonyesha unyenyekevu tunapotangaza Ufalme. Ni kweli kwamba leo roho ya Mungu haiwapi Wakristo nguvu za kuwaponya watu kimuujiza. Hata hivyo, tunaweza kuwasaidia watu kumwamini Mungu na Kristo na kupokea zawadi ileile ambayo Petro aliahidi—wasamehewe dhambi na kuburudishwa na Yehova. Kila mwaka, mamia ya maelfu hupokea zawadi hiyo, na kuwa wanafunzi waliobatizwa wa Kristo.

      8 Kwa kweli tunaishi nyakati ambazo Petro aliziita nyakati za “kurudishwa kwa mambo yote.” Mambo ambayo “Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu walioishi zamani” yalitimia Ufalme ulipoanza kutawala mbinguni mwaka wa 1914. (Mdo. 3:21; Zab. 110:1-3; Dan. 4:16, 17) Muda mfupi baadaye, kazi ya kurudisha au kuwaponya watu kiroho ilianza hapa duniani, Kristo akiwa msimamizi. Mamilioni ya watu wameingizwa katika paradiso ya kiroho, na hivyo kuwa raia wa Ufalme wa Mungu. Wamevua utu wa zamani uliopotoka na “kuvaa utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu.” (Efe. 4:22-24) Kama yule kilema aliyeponywa, kazi hiyo imetimizwa kwa nguvu za roho ya Mungu, bali si kwa nguvu za wanadamu. Kama alivyofanya Petro, lazima tulitumie Neno la Mungu kwa ujasiri na kwa njia inayofaa tunapowafundisha wengine. Mafanikio yoyote tunayopata tunapowasaidia watu wawe wanafunzi wa Kristo yanatokana na nguvu za Mungu, bali si zetu wenyewe.

      “Hatuwezi Kuacha Kusema” (Mdo. 4:1-22)

      9-11. (a) Viongozi wa Wayahudi walifanyaje walipousikia ujumbe wa Petro na Yohana? (b) Mitume waliazimia kufanya nini?

      9 Hotuba ya Petro, zile kelele na kurukaruka kwa yule mtu aliyekuwa kilema, kulileta vurugu. Basi, kapteni wa hekalu—aliyekuwa na wajibu wa kuhakikisha usalama hekaluni—pamoja na wakuu wa makuhani, wakaja haraka kuona kilichokuwa kikiendelea. Inawezekana kwamba walikuwa Masadukayo, kikundi cha matajiri chenye uwezo kisiasa kilichojitahidi kudumisha uhusiano mzuri na Waroma, ambacho kilikataa sheria ya mdomo iliyopendwa sana na Mafarisayo, na kilichodhihaki imani ya ufufuo.c Walikasirika sana walipowakuta Petro na Yohana hekaluni wakifundisha bila woga kwamba Yesu amefufuliwa!

      10 Wapinzani hao wenye hasira waliwaweka Petro na Yohana kizuizini, kisha siku iliyofuata wakawaburuta hadi mahakama kuu ya Wayahudi. Machoni pa watawala hao wenye cheo, Petro na Yohana walikuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu” ambao hawakuwa na haki ya kufundisha hekaluni. Hawakusomea katika shule zozote za kidini zilizokuwa maarufu. Hata hivyo, mahakama hiyo ilishangazwa na maneno yao yaliyo wazi na yenye usadikisho. Ni nini kilichowasaidia Petro na Yohana? Sababu moja ni kwamba “walikuwa pamoja na Yesu.” (Mdo. 4:13) Bwana wao alikuwa mwalimu stadi, tofauti kabisa na waandishi.​—Mt. 7:28, 29.

      11 Mahakama hiyo iliwaagiza mitume hao waache kuhubiri. Siku hizo, amri za mahakama zilichukuliwa kwa uzito. Majuma machache yaliyotangulia, Yesu alipopelekwa kwenye mahakama hiyo, washiriki wa mahakama hiyo walisema: “Anastahili kufa.” (Mt. 26:59-66) Licha ya mambo hayo yote, Petro na Yohana hawaogopi. Wakiwa wamesimama mbele za wanaume hao matajiri, wenye elimu, na uvutano mkubwa, Petro na Yohana wanajibu kwa heshima lakini bila woga wowote: “Kama ni sawa machoni pa Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”​—Mdo. 4:19, 20.

      KUHANI MKUU NA WAKUU WA MAKUHANI

      Kuhani mkuu alikuwa mwakilishi wa taifa lake mbele za Mungu. Katika karne ya kwanza, kuhani mkuu alikuwa pia mkuu wa Sanhedrini. Wakuu wa makuhani waliokuwa viongozi wa Wayahudi walifanya kazi chini yake. Wakuu hao wa makuhani walitia ndani makuhani wakuu wastaafu, kama vile Anasi, na pia wanaume wengine, huenda kutoka katika familia nne au tano ambamo makuhani wakuu walichaguliwa. Kulingana na kitabu cha Emil Schürer, “kuwa tu mtu wa familia hizo za pekee kulimwezesha mtu kupata cheo fulani” miongoni mwa makuhani.

      Maandiko yanaonyesha kwamba makuhani wakuu walitumikia hadi walipokufa. (Hes. 35:25) Hata hivyo, wakati wa kipindi kinachozungumziwa katika kitabu cha Matendo, magavana Waroma na wafalme waliotawala wakiwa vibaraka wa Roma waliteua na kuwaondoa makuhani wakuu kama walivyopenda. Vyovyote vile, inaonekana kwamba watawala hao wapagani walichagua makuhani kutoka katika ukoo wa kikuhani wa Haruni.

      12. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa na ujasiri na usadikisho?

      12 Je, unaweza kuonyesha ujasiri kama huo? Inakuwaje unapopata nafasi ya kuwahubiria watu matajiri, wenye elimu ya juu, au watu mashuhuri? Namna gani wakati ambapo watu wa familia yako, wanafunzi, au wafanyakazi wenzako wanapokashifu imani yako? Unaogopa? Ikiwa wewe huogopa, jipe moyo. Alipokuwa duniani, Yesu aliwafundisha mitume wake jinsi ya kutetea imani yao kwa usadikisho na kwa heshima. (Mt. 10:11-18) Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwaahidi wanafunzi wake kwamba angeendelea kuwa pamoja nao “sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Chini ya mwelekezo wa Yesu, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatufundisha jinsi ya kutetea imani yetu. (Mt. 24:45-47; 1 Pet. 3:15) Anafanya hivyo kupitia mikutano ya kutaniko kama vile Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo, na kupitia machapisho yanayotegemea Biblia, kama vile makala za “Majibu ya Maswali ya Biblia,” zinazopatikana kwenye tovuti ya jw.org. Je, unatumia vizuri maandalizi hayo? Ukifanya hivyo, utakuwa na ujasiri na usadikisho hata zaidi. Na kama walivyofanya mitume, hutakubali chochote kikuzuie kuzungumza kuhusu kweli za kiroho zenye thamani ambazo umeona na kusikia.

      Dada akimhubiria mfanyakazi mwenzake wakati wa mapumziko.

      Usikubali chochote kikuzuie kusema kuhusu kweli za kiroho zenye thamani ambazo umejifunza

      ‘Wakasema kwa Sauti Kubwa kwa Mungu’ (Mdo. 4:23-31)

      13, 14. Tukikabili upinzani, tunapaswa kufanya nini, na kwa nini?

      13 Mara tu baada ya kuachiliwa, Petro na Yohana walijiunga na washiriki wengine wa kutaniko. Wote kwa pamoja, ‘wakasema kwa sauti kubwa kwa Mungu’ na kumwomba awape ujasiri wa kuendelea kuhubiri. (Mdo. 4:24) Petro alijua vizuri ubatili wa kujaribu kufanya mapenzi ya Mungu kwa kutegemea nguvu zake mwenyewe. Majuma kadhaa yaliyopita, alikuwa amemwambia Yesu kwa kimbelembele: “Hata wengine wote wakikwazika kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe!” Lakini kama Yesu alivyokuwa ametabiri, Petro aliwaogopa wanadamu na kumkana rafiki na mwalimu wake. Hata hivyo, Petro alijifunza kutokana na kosa lake.​—Mt. 26:33, 34, 69-75.

      14 Huwezi kutimiza utume wako wa kuhubiri kuhusu Kristo kwa kuwa tu umeazimia kufanya hivyo. Wapinzani wanapojaribu kuvunja imani yako, au kukuzuia usihubiri, fuata mfano wa Petro na Yohana. Mwombe Yehova akupe nguvu. Tafuta msaada wa kutaniko. Waambie wazee na wengine wakomavu kutanikoni hali ngumu unazokabili. Sala za wengine zinaweza kukutia nguvu.​—Efe. 6:18; Yak. 5:16.

      15. Kwa nini wale ambao wakati fulani waliacha kuhubiri kwa muda hawapaswi kuvunjika moyo?

      15 Ikiwa wakati fulani uliacha kuhubiri kwa muda kwa sababu ya upinzani, jipe moyo. Kumbuka kwamba, Yesu alipokufa, mitume wote waliacha kuhubiri kwa muda, lakini upesi wakawa watendaji tena. (Mt. 26:56; 28:10, 16-20) Badala ya kuruhusu makosa ya wakati uliopita yakulemee, je, unaweza kujifunza kutokana na hali hiyo na kutumia mambo hayo kuwaimarisha wengine?

      16, 17. Sala ambayo wafuasi wa Kristo walitoa huko Yerusalemu inatufundisha nini?

      16 Tunapoonewa na wenye mamlaka, tunapaswa kusali kuhusu nini? Kumbuka kwamba wanafunzi hawakuomba waepushwe na majaribu. Walikumbuka vizuri maneno ya Yesu: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Wanafunzi hao washikamanifu walimwomba Yehova ‘aangalie’ vitisho vya wapinzani. (Mdo. 4:29) Ni wazi kwamba wanafunzi hao walielewa mambo yote yaliyohusika, wakitambua kwamba unabii ulikuwa ukitimia. Walijua kwamba, kama vile Yesu alivyowafundisha kusali, mapenzi ya Mungu ‘yangetendeka duniani,’ hata watawala wa kibinadamu waseme nini.​—Mt. 6:9, 10.

      17 Ili kufanya mapenzi ya Mungu, wanafunzi walisali kwa Yehova hivi: “Uwawezeshe watumwa wako waendelee kutangaza neno lako kwa ujasiri wote.” Yehova alijibuje sala yao? “Mahali walipokuwa wamekusanyika pakatikiswa, na kila mmoja wao akajazwa roho takatifu nao walikuwa wakitangaza neno la Mungu kwa ujasiri.” (Mdo. 4:29-31) Hakuna chochote kinachoweza kuzuia mapenzi ya Mungu yasitimizwe. (Isa. 55:11) Hata hali ziwe ngumu kadiri gani, au adui awe mwenye nguvu kadiri gani, tukimwinulia Mungu sauti zetu katika sala, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatupatia nguvu za kuendelea kutangaza neno lake kwa ujasiri.

      Hawakuwajibika Mbele za “Wanadamu, Bali Mungu” (Mdo. 4:32–5:11)

      18. Washiriki wa kutaniko la Yerusalemu walisaidiana jinsi gani?

      18 Washiriki wa kutaniko hilo dogo lililokuwa Yerusalemu waliongezeka na kuwa zaidi ya 5,000.d Ijapokuwa walikuwa watu wenye malezi mbalimbali, wanafunzi walikuwa na “moyo na nafsi moja.” Walikuwa wameunganishwa katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri. (Mdo. 4:32; 1 Kor. 1:10) Baada ya wanafunzi hao kumwomba Yehova abariki jitihada zao hawakuketi tu. Walitegemezana kiroho na, ilipohitajika, kimwili pia. (1 Yoh. 3:16-18) Kwa mfano, mwanafunzi Yosefu, ambaye mitume walikuwa wakimwita Barnaba, aliuza shamba lake, na pasipo ubinafsi, akachanga fedha zote ziwasaidie waliokuwa wametoka mbali wakae Yerusalemu kwa muda mrefu zaidi ili wajifunze mengi zaidi kuhusu imani yao mpya.

      19. Kwa nini Yehova alimwangamiza Anania na Safira?

      19 Anania na Safira pia waliuza mali yao na kutoa mchango. Walijifanya kwamba wametoa kiasi chote, lakini kumbe walikuwa ‘wamejiwekea kisiri kiasi fulani.’ (Mdo. 5:2) Yehova aliwaangamiza, si kwa sababu mchango wao haukutosha, bali nia yao ya kutoa ilikuwa mbaya na pia kwa sababu walisema uwongo. Walidanganya, “si wanadamu, bali Mungu.” (Mdo. 5:4) Anania na Safira walitaka sana kusifiwa na watu badala ya kupata kibali cha Mungu, kama walivyofanya wale wanafiki walioshutumiwa na Yesu.​—Mt. 6:1-3.

      20. Tunajifunza nini kuhusu michango tunayotoa?

      20 Leo, kama walivyofanya wanafunzi waaminifu wa karne ya kwanza huko Yerusalemu, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova huonyesha roho ya ukarimu kwa kutegemeza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote kwa michango yao ya hiari. Hakuna anayewalazimisha watumie wakati wao au pesa zao kutegemeza kazi ya Ufalme. Kwa kweli, Yehova hapendi tumtumikie kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa. (2 Kor. 9:7) Tunapotoa michango yetu, Yehova hapendezwi na kiasi tunachotoa, bali hupendezwa na nia yetu. (Marko 12:41-44) Hatungetaka kamwe kuwa kama Anania na Safira kwa kumtumikia Mungu kwa sababu za kibinafsi au kujitafutia sifa. Badala yake, kama Petro, Yohana, na Barnaba, upendo wa kweli kwa Mungu na wanadamu wenzetu na utuchochee kumtumikia Yehova.​—Mt. 22:37-40.

      PETRO—MTUME MWENYE BIDII AMBAYE MWANZONI ALIKUWA MVUVI

      Biblia inamtaja Petro kwa majina matano. Anaitwa Simioni katika Kiebrania na Simoni katika Kigiriki. Pia, anaitwa Petro, jina ambalo katika Kiyahudi ni Kefa. Nyakati nyingine, mtume huyo anaitwa kwa majina mawili, Simoni Petro.​—Mt. 10:2; Yoh. 1:42; Mdo. 15:14.

      Mtume Petro akiwa amebeba kikapu chenye samaki.

      Petro alikuwa na mke na nyumbani kwake aliishi pamoja na mama mkwe wake na ndugu yake. (Marko 1:29-31) Alikuwa mvuvi wa Bethsaida, mji uliokuwa upande wa kaskazini mwa Bahari ya Galilaya. (Yoh. 1:44) Baadaye aliishi Kapernaumu. (Luka 4:31, 38) Yesu aliketi ndani ya mashua ya Petro alipokuwa akiuhubiria umati uliokuwa umekusanyika kando ya Bahari ya Galilaya. Baadaye, Petro alitii agizo la Yesu, akashusha nyavu na kuvua samaki wengi sana kimuujiza. Akiwa na woga, Petro alianguka magotini mwa Yesu, lakini Yesu akamwambia: “Acha kuogopa. Kuanzia sasa utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” (Luka 5:1-11) Petro alikuwa akifanya kazi ya uvuvi pamoja na ndugu yake Andrea na pia Yakobo na Yohana. Wote wanne waliacha kazi yao ya uvuvi na kukubali mwaliko wa Yesu wa kuwa wafuasi wake. (Mt. 4:18-22; Marko 1:16-18) Mwaka mmoja hivi baadaye, Petro alikuwa mmoja wa “mitume” 12 waliochaguliwa na Yesu.​—Marko 3:13-16.

      Kwenye matukio fulani ya pekee, Yesu alikwenda na Petro, Yakobo na Yohana. Wanafunzi hao walishuhudia pindi ambayo Yesu aligeuka sura, walikuwa pamoja naye alipomfufua binti ya Yairo, na walikuwa naye alipokuwa na huzuni nyingi katika bustani ya Gethsemane. (Mt. 17:1, 2; 26:36-46; Marko 5:22-24, 35-42; Luka 22:39-46) Petro, Yakobo, Yohana, pamoja na Andrea, walimwuliza Yesu maswali kuhusu ishara ya kuwapo kwake.​—Marko 13:1-4.

      Petro alipenda kusema mambo waziwazi, alikuwa mwenye bidii, na nyakati nyingine alifanya mambo haraka bila kufikiria. Inaonekana kwamba mara nyingi alikuwa wa kwanza kuongea. Vitabu vya Injili vinanukuu maneno yake mara nyingi zaidi kuliko maneno ya wale mitume wengine wote. Petro hakusita kuuliza maswali, wengine walipokaa kimya. (Mt. 15:15; 18:21; 19:27-29; Luka 12:41; Yoh. 13:36-38) Petro alikataa kuoshwa miguu na Yesu, kisha alipokaripiwa, akamwambia Yesu amwoshe mikono na kichwa pia!—Yoh. 13:5-10.

      Petro alisukumwa na hisia kujaribu kumsadikisha Yesu kwamba hatateseka na kuuawa. Yesu alimkemea kwa sababu ya tendo hilo la kukosa hekima. (Mt. 16:21-23) Usiku uliotangulia kifo cha Yesu, Petro alisema kwamba ingawa huenda mitume wengine wote wangemwacha Yesu, yeye hangemwacha kamwe. Yesu alipokamatwa na adui, Petro alionyesha ujasiri kwa kumpigania Yesu kwa upanga, na baadaye akamfuata hadi kwenye ua wa kuhani mkuu. Hata hivyo, muda mfupi baadaye, Petro alimkana Bwana wake mara tatu, kisha akalia kwa uchungu alipotambua kosa lake.​—Mt. 26:31-35, 51, 52, 69-75.

      Muda mfupi baada ya ufufuo wa Yesu na kabla hajawatokea mitume wake huko Galilaya, Petro alisema kwamba anaenda kuvua samaki, na mitume wengine wakajiunga naye. Alipomwona Yesu kando ya bahari, alijitumbukiza ndani ya maji na kuogelea hadi nchi kavu. Walipokuwa wakila samaki ambao Yesu alikuwa amewatayarishia mitume wake, Yesu alimwuliza Petro ikiwa anampenda kuliko “hawa”​—yaani, samaki waliokuwa mbele yao. Yesu alikuwa akimhimiza Petro achague kuwa mfuasi wake sikuzote badala ya kufuatia kazi ya kimwili, kama vile kazi ya uvuvi.​—Yoh. 21:1-22.

      Karibu mwaka wa 62-64 W.K., Petro alihubiri habari njema Babiloni (Iraki ya leo), ambako kulikuwa na Wayahudi wengi wakati huo. (1 Pet. 5:13) Akiwa Babiloni, Petro aliongozwa na roho kuandika barua ya kwanza yenye jina lake. Huenda pia aliandika barua yake ya pili akiwa huko. Yesu ndiye “aliyemtia Petro nguvu,” na kumpatia ‘utume kwa ajili ya watu waliotahiriwa.’ (Gal. 2:8, 9) Petro aliutimiza utume huo kwa fadhili na bidii.

      YOHANA—MWANAFUNZI AMBAYE YESU ALIMPENDA

      Mtume Yohana alikuwa mwana wa Zebedayo na ndugu ya mtume Yakobo. Inaonekana kwamba mama yake ni Salome, ambaye huenda alikuwa dada ya Maria, mama ya Yesu. (Mt. 10:2; 27:55, 56; Marko 15:40; Luka 5:9, 10) Kwa hiyo, huenda Yohana alikuwa mtu wa ukoo wa Yesu. Inaonekana kwamba familia ya Yohana ilikuwa na mali za kimwili. Zebedayo alikuwa ameajiri wavuvi kadhaa. (Marko 1:20) Salome aliandamana na Yesu, alimhudumia Yesu alipokuwa Galilaya, na baadaye alileta manukato ili kuutayarisha mwili wa Yesu kwa ajili ya maziko. (Marko 16:1; Yoh. 19:40) Inaonekana Yohana alikuwa na nyumba yake mwenyewe.​—Yoh. 19:26, 27.

      Mtume Yohana akiwa ameshika kitabu cha kukunjwa.

      Huenda Yohana ndiye mwanafunzi wa Yohana Mbatizaji aliyekuwa pamoja na Andrea wakati Yohana Mbatizaji alipomtazama Yesu na kusema: “Ona, Mwanakondoo wa Mungu!” (Yoh. 1:35, 36, 40) Kisha, Yohana mwana wa Zebedayo alisafiri na Yesu hadi Kana na kujionea muujiza wa kwanza wa Yesu. (Yoh. 2:1-11) Njia yake ya kusimulia mambo waziwazi kuhusu utendaji uliofuata wa Yesu huko Yerusalemu, Samaria, na Galilaya inaonyesha kwamba alishuhudia mambo hayo. Yesu alipomwita awe mfuasi wake, Yohana hakusita kuacha nyavu, mashua, na kazi yake ya uvuvi, kama alivyofanya Yakobo, Petro, na Andrea. Alikuwa na imani yenye nguvu!—Mt. 4:18-22.

      Yohana hatajwi mara nyingi katika Injili kama Petro anavyotajwa. Hata hivyo, yeye pia alikuwa mwenye bidii. Yesu alimwita yeye na ndugu yake Yakobo, Boanerge, jina linalomaanisha “Wana wa Ngurumo.” (Marko 3:17) Mwanzoni, Yohana alijitakia makuu sana hivi kwamba yeye na ndugu yake walimtumia mama yao kumwomba Yesu awapatie vyeo vya juu katika Ufalme wake. Ingawa walionyesha ubinafsi, tendo hilo lilionyesha kwamba walikuwa na imani katika Ufalme. Kisa hicho pia kilimpa Yesu nafasi ya kuwashauri mitume wake kuhusu sifa ya unyenyekevu.​—Mt. 20:20-28.

      Mtu fulani ambaye hakuwa mfuasi wa Yesu alipokuwa akiwafukuza roho waovu kwa jina la Yesu, Yohana alionyesha ujasiri kwa kujaribu kumzuia. Pindi nyingine, Yohana alitaka kuomba moto ushuke kutoka mbinguni na kuteketeza kijiji cha Wasamaria ambao hawakuwakaribisha, Yesu alipomtuma yeye na ndugu yake kufanya matayarisho fulani. Kwa sababu hizo, Yesu alimkemea Yohana. Kadiri wakati ulivyopita, ndivyo Yohana alivyozidi kuwa na usawaziko na mwenye rehema, sifa ambazo ilionekana ni kana kwamba hakuwa nazo. (Luka 9:49-56) Ijapokuwa alikosea mara kwa mara, Yohana ndiye “mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda.” Hivyo, kabla ya kufa, Yesu alimwomba Yohana amtunze Maria, mama yake mzazi.​—Yoh. 19:26, 27; 21:7, 20, 24.

      Kama Yesu alivyotabiri, Yohana alikuwa mtume wa mwisho kufa. (Yoh. 21:20-22) Yohana alimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka 70 hivi. Alipokuwa amezeeka, katika kipindi ambacho Maliki Domitian alitawala Roma, Yohana alipelekwa uhamishoni katika kisiwa cha Patmo “kwa sababu ya kuzungumza kumhusu Mungu na kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” Akiwa huko, mwaka wa 96 hivi, Yohana aliona maono ambayo aliyaandika katika kitabu cha Ufunuo. (Ufu. 1:1, 2, 9) Inasemekana kwamba Yohana alipoachiliwa alienda Efeso, ambako aliandika kitabu cha Injili chenye jina lake na zile barua tatu za Yohana, na kisha akafa mwaka wa 100 hivi katika jiji la Efeso.

      a Katika hekalu, sala zilikuwa zikitolewa wakati wa dhabihu za asubuhi na za jioni. Dhabihu ya jioni ilikuwa ikitolewa “saa tisa,” au karibu saa 9 alasiri.

      b Ona sanduku lenye kichwa “Petro—Mtume Mwenye Bidii Ambaye Mwanzoni Alikuwa Mvuvi,”, na pia “Yohana—Mwanafunzi Ambaye Yesu Alimpenda,”.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Kuhani Mkuu na Wakuu wa Makuhani,”.

      d Mwaka wa 33 W.K., huenda kulikuwa na Mafarisayo 6,000 hivi na Masadukayo wachache katika jiji la Yerusalemu. Huenda ndiyo sababu vikundi hivyo viwili vilianza kuyaona mafundisho ya Yesu kuwa tishio.

  • “Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 5

      “Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala”

      Mitume wachukua msimamo unaowawekea kielelezo Wakristo wote wa kweli

      Mdo. 5:12–6:7

      1-3. (a) Kwa nini mitume wamepelekwa mbele ya Sanhedrini, na ni suala gani kuu linalohusika? (b) Kwa nini tupendezwe sana na msimamo wa mitume?

      MAHAKAMA ya Sanhedrini imewaka hasira! Mitume wa Yesu wamefikishwa mbele ya mahakama hiyo. Kwa sababu gani? Yosefu Kayafa, kuhani mkuu aliyekuwa pia mkuu wa Sanhedrini, anawaambia hivi kwa ukali: “Tuliwakataza kabisa msifundishe kwa msingi wa jina hili.” Kwa sababu ya hasira hawezi hata kutamka jina la Yesu. Kayafa anaendelea kusema, “na bado tazama! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu, nanyi mmeazimia kuileta damu ya mtu huyu juu yetu.” (Mdo. 5:28) Ujumbe wake uko wazi: Acheni kuhubiri!

      2 Mitume hao watafanya nini? Yesu, aliye na mamlaka kamili kutoka kwa Mungu, ndiye aliyewapa kazi hiyo ya kuhubiri. (Mt. 28:18-20) Je, mitume hao wataogopa na kuacha kuhubiri? Au je, watasimama imara na kuendelea kuhubiri kwa ujasiri? Jambo kuu ni: Watamtii Mungu au mwanadamu? Bila kusita, mtume Petro anazungumza bila woga wowote kwa niaba ya mitume wengine.

      3 Tukiwa Wakristo, tunaweza kujifunza mengi kutokana na jinsi mitume walivyotenda walipotishwa na Sanhedrini. Sisi pia tumepewa kazi ya kuhubiri. Tunapotimiza kazi hiyo tuliyopewa na Mungu, huenda pia tukakabili upinzani. (Mt. 10:22) Wapinzani wanaweza kujaribu kuzuia au kupinga kazi yetu. Tutafanya nini? Acheni tufikirie msimamo wa mitume na mambo yaliyotokea kabla ya kupelekwa kwao mbele ya Sanhedrini. Kufikiria mambo hayo kunaweza kutusaidia tunapokabili hali kama hizo.a

      SANHEDRINI​—MAHAKAMA KUU YA WAYAHUDI

      Roma iliwaruhusu Wayahudi waendeleze utamaduni wao na wajitawale ingawa Yudea ilikuwa mkoa wa Milki ya Roma. Kesi ndogo za uhalifu zilitatuliwa na mahakama ndogo, lakini kesi ambazo mahakama hizo hazingeweza kutatua zilipelekwa mbele ya Sanhedrini iliyokuwa Yerusalemu. Sanhedrini ilikuwa mahakama kuu ya Wayahudi. Pia, ilikuwa baraza lililosimamia mambo ya kitaifa. Iliamua mambo yaliyohusu sheria ya Kiyahudi, na mamlaka yake iliheshimiwa na Wayahudi wote.

      Vikao vya Sanhedrini vilikuwa vikifanywa katika majengo ya hekalu au karibu na hekalu. Baraza hilo lilikuwa na washiriki 71—kuhani mkuu, alikuwa mkuu wa mahakama hiyo; washiriki wengine walikuwa makuhani, kutia ndani Masadukayo, watu kutoka katika jamii za wakuu, na waandishi wenye elimu. Uamuzi wa mahakama hiyo haungeweza kubatilishwa.

      “Malaika wa Yehova Akaifungua Milango” (Mdo. 5:12-21a)

      4, 5. Kwa nini Kayafa na Masadukayo ‘walijawa na wivu’?

      4 Kumbuka kwamba Petro na Yohana walipokatazwa kuhubiri mara ya kwanza, walisema: “Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Mdo. 4:20) Walipoachiliwa, Petro na Yohana pamoja na wale mitume wengine waliendelea kuhubiri katika hekalu. Walifanya ishara kubwa, kama vile kuponya wagonjwa na kufukuza roho waovu. Hata inaonekana kwamba watu walioangukiwa na kivuli cha Petro waliponywa! Walifanya hivyo “kwenye Safu ya Nguzo za Sulemani” zilizokuwa upande wa mashariki wa hekalu, ambapo Wayahudi wengi walipenda kukusanyika. Wengi walioponywa kimwili walikubali pia kuponywa kiroho. Kwa sababu hiyo, “waliomwamini Bwana wakazidi kuongezeka, idadi kubwa ya wanaume na wanawake.”​—Mdo. 5:12-15.

      5 Kayafa na Masadukayo, ‘wakajawa na wivu’ na kuagiza mitume wafungwe jela. (Mdo. 5:17, 18) Ni nini kilichowakasirisha Masadukayo? Mitume walikuwa wakifundisha kwamba Yesu amefufuliwa, nao Masadukayo hawakuamini ufufuo. Pia, mitume walifundisha kwamba ili mtu aokolewe anahitaji kumwamini Yesu, Masadukayo walihofu kwamba ikiwa watu wangekuwa wafuasi wa Yesu, Waroma wangewachukulia hatua kali. (Yoh. 11:48) Ndiyo sababu Masadukayo walikuwa wameazimia kabisa kuwanyamazisha mitume!

      6. Ni nani hasa leo wanaochochea watumishi wa Yehova wateswe, na kwa nini hilo halitushangazi?

      6 Leo pia, wapinzani wa kidini ndio hasa wanaochochea watu wawatese watumishi wa Yehova. Wapinzani hao hujaribu kutunyamazisha kwa kutumia serikali au vyombo vya habari. Wanafanya hivyo kwa sababu ujumbe wetu unafunua uwongo wa dini. Wanapokubali kweli za Biblia, watu wenye mioyo minyoofu huwekwa huru kutokana na imani na mazoea yasiyo ya kimaandiko. (Yoh. 8:32) Ndiyo sababu mara nyingi ujumbe wetu huwafanya viongozi wa kidini wawe na wivu na chuki.

      7, 8. Amri ya malaika ilikuwa na matokeo gani kwa mitume, nasi tunapaswa kujiuliza swali gani?

      7 Wakiwa jela kabla ya kupelekwa mahakamani, huenda mitume hao waliona kwamba watauawa kwa sababu ya imani yao. (Mt. 24:9) Lakini usiku huo, jambo lisilo la kawaida likatokea—“malaika wa Yehova akaifungua milango ya gereza.”b (Mdo. 5:19) Kisha malaika huyo akawaagiza: “Mkasimame hekaluni, na mwendelee kuwaambia” watu. (Mdo. 5:20) Bila shaka, amri hiyo iliwahakikishia mitume kwamba walikuwa wakifanya jambo linalofaa. Pia, huenda maneno hayo yaliwapa nguvu za kubaki imara hata hali ziweje. Wakiwa na imani yenye nguvu na ujasiri, mitume “wakaingia hekaluni wakati wa mapambazuko na kuanza kufundisha.”​—Mdo. 5:21.

      8 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Nina imani na ujasiri unaohitajiwa kuendelea kuhubiri katika hali kama hizo?’ Kujua kwamba tunategemezwa na kuongozwa na malaika tunapofanya kazi hiyo muhimu ya “kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu,” kunaweza kutupatia nguvu za kuendelea kuhubiri.​—Mdo. 28:23; Ufu. 14:6, 7.

      “Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Badala ya Wanadamu” (Mdo. 5:21b-33)

      Kayafa akiwashutumu mitume kwa hasira mbele ya washiriki wengine wa Sanhedrini.

      “Basi wakawaleta na kuwasimamisha mbele ya Sanhedrini.”—Matendo 5:27

      9-11. Mitume walifanya nini mahakama ya Sanhedrini ilipowaamuru waache kuhubiri, na Wakristo wa kweli leo wanawezaje kuwaiga?

      9 Kayafa na wale mahakimu wengine wa Sanhedrini wako tayari kuwachukulia hatua mitume hao. Kwa kuwa hawakujua yaliyokuwa yametokea usiku uliotangulia, wakawatuma maofisa wakawachukue wafungwa. Wazia jinsi maofisa hao walivyoshangaa walipogundua kwamba wafungwa hawapo, ijapokuwa jela ilikuwa imefungwa kabisa na “walinzi wakiwa wamesimama kwenye milango.” (Mdo. 5:23) Muda mfupi baadaye, kapteni wa hekalu ajulishwa kwamba mitume wamerudi hekaluni, na wanatoa ushahidi kumhusu Yesu Kristo—kazi ileile ambayo ilifanya wafungwe katika jela! Bila kupoteza wakati kapteni na maofisa wake wanaenda hekaluni kuwakamata na kuwaleta mbele ya Sanhedrini.

      10 Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa sura hii, viongozi hao wa kidini wenye hasira kali waliwaagiza mitume hao waache kabisa kuhubiri. Ikawaje? Petro akiwa msemaji wao, alijibu hivi kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.” (Mdo. 5:29) Wakristo wote wa kweli wanaweza kuiga mfano huo mzuri uliowekwa na mitume. Hatuwezi kuwatii watawala wa kibinadamu wanapotukataza kufanya kile ambacho Mungu anataka tufanye au wanapotaka tufanye kile ambacho Mungu anatukataza. Hivyo, “mamlaka zilizo kubwa” zikipiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri tuliyopewa na Mungu, hatutaacha. (Rom. 13:1) Badala yake, tutaendelea kwa busara kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.

      11 Si ajabu kwamba jibu la ujasiri ambalo mitume walitoa liliwafanya mahakimu hao wawe na hasira. Waliazimia “kuwaangamiza” mitume hao. (Mdo. 5:33) Mashahidi hao wenye ujasiri waliamini kabisa kwamba sasa wangeuawa kwa sababu ya imani yao. Hata hivyo, hawakujua kwamba msaada ulikuwa njiani!

      “Hamtaweza Kuwaangamiza” (Mdo. 5:34-42)

      12, 13. (a) Gamalieli aliwapa wenzake shauri gani, nao walifanya nini? (b) Yehova anawezaje kuwasaidia watu wake leo, na tunaweza kuwa na uhakika gani iwapo ataruhusu ‘tuteseke kwa ajili ya uadilifu’?

      12 Gamalieli, “mwalimu wa Sheria aliyeheshimiwa na watu wote,” akaanza kuzungumza.c Gamalieli aliheshimiwa sana na mahakimu wenzake ndiyo sababu angeweza kuamuru “[mitume] hao watolewe nje kwa muda mfupi.” (Mdo. 5:34) Gamalieli alitaja vikundi fulani ambavyo vilisambaratika baada ya viongozi wao kufa. Kisha akahimiza mahakama hiyo iwe na subira inaposhughulika na mitume hao, ambao Kiongozi wao, Yesu, alikuwa amekufa hivi karibuni. Gamalieli alikuwa mwenye kusadikisha kwelikweli. Aliwaambia hivi: “Msiingilie mambo ya watu hawa, bali waacheni. Kwa maana, ikiwa mpango huu au kazi hii ni ya wanadamu, itaangamizwa; lakini ikiwa imetoka kwa Mungu, hamtaweza kuwaangamiza. La sivyo, huenda ikawa mnapigana na Mungu mwenyewe.” (Mdo. 5:38, 39) Mahakimu hao walimsikiliza, hata hivyo, wakawapiga viboko mitume na kuwaagiza “waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu.”​—Mdo. 5:40.

      13 Leo, kama ilivyokuwa wakati huo, Yehova anaweza kuwatumia watu mashuhuri kama Gamalieli kuwasaidia watu Wake. (Met. 21:1) Anaweza kutumia roho yake kuwafanya watawala wenye nguvu, mahakimu, au wanasheria watende kulingana na mapenzi yake. (Neh. 2:4-8) Hata hivyo, huenda wakati mwingine akaruhusu ‘tuteseke kwa ajili ya uadilifu.’ (1 Pet. 3:14) Akiruhusu iwe hivyo, tunaweza kuwa na uhakika wa mambo mawili. Kwanza, anaweza kutupatia nguvu za kuvumilia. (1 Kor. 10:13) Pili, wapinzani ‘hawataweza kuiangamiza’ kazi ya Mungu.​—Isa. 54:17.

      14, 15. (a) Mitume walifanya nini walipopigwa, na kwa nini? (b) Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha kwamba watu wa Yehova huvumilia kwa shangwe.

      14 Je, mitume hao walivunjika moyo au kukata tamaa baada ya kupigwa viboko? Hapana! ‘Walitoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia.’ (Mdo. 5:41) “Wakishangilia”​—kwa nini? Hawakuwa wakishangilia maumivu waliyokuwa nayo kwa sababu ya kupigwa. Walishangilia kwa kuwa walijua kwamba wameteswa kwa sababu ya kuwa waaminifu kwa Yehova na kwa kufuata hatua za Kielelezo chao, Yesu.​—Mt. 5:11, 12.

      15 Kama walivyofanya ndugu zetu wa karne ya kwanza, sisi pia huvumilia kwa shangwe tunapoteseka kwa sababu ya habari njema. (1 Pet. 4:12-14) Si kwamba tunafurahia tunapotishwa, tunapoteswa, au kufungwa gerezani. Hata hivyo, tunaridhika kwa kujua kwamba tunadumisha uaminifu wetu kwa Yehova. Kwa mfano, fikiria kisa cha Henryk Dornik, aliyeteswa kwa miaka mingi katika nchi iliyokuwa ikitawaliwa kimabavu. Anakumbuka kwamba mnamo Agosti 1944, wenye mamlaka waliamua kumpeleka yeye pamoja na ndugu yake katika kambi ya mateso. Wapinzani hao walisema hivi: “Huwezi kuwalazimisha kufanya chochote. Hata ukiwaua wanashangilia.” Ndugu Dornik anaeleza: “Ingawa si kwamba nilitaka kufa, kuteseka kwa sababu ya ushikamanifu wangu kwa Yehova kuliniletea shangwe.”​—Yak. 1:2-4.

      Wenzi wakitumia Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia kumhubiria mwanamume mbele ya nyumba yake.

      Kama walivyofanya mitume, leo pia tunahubiri “nyumba kwa nyumba”

      16. Mitume walionyesha jinsi gani kwamba walikuwa wameazimia kutoa ushahidi kamili, nasi tunafuata mfano wao kwa kufanya nini?

      16 Mitume hao walirudia kazi yao bila kukawia. Bila woga, waliendelea “kila siku hekaluni na nyumba kwa nyumba” kufanya kazi ya “kutangaza habari njema kumhusu Kristo.”d (Mdo. 5:42) Wahubiri hao wenye bidii walikuwa wameazimia kutoa ushahidi kamili. Ona kwamba waliwapelekea watu ujumbe nyumbani kwao, kama vile Yesu Kristo alivyokuwa amewaagiza. (Mt. 10:7, 11-14) Ndiyo sababu ilidaiwa kwamba wamejaza Yerusalemu mafundisho yao. Leo pia, kama walivyofanya mitume, Mashahidi wa Yehova huhubiri nyumba kwa nyumba. Tunapohubiri kila nyumba katika eneo letu, tunaonyesha waziwazi kwamba sisi pia tunatoa ushahidi kamili, tukimpa kila mtu nafasi ya kusikia habari njema. Je, Yehova amebariki huduma yetu ya nyumba kwa nyumba? Ndiyo! Mamilioni ya watu wameitikia ujumbe wa Ufalme wakati huu wa mwisho. Wengi walisikia habari njema kwa mara ya kwanza Shahidi alipowatembelea.

      KUHUBIRI “NYUMBA KWA NYUMBA”

      Ingawa Sanhedrini ilikuwa imepiga marufuku kazi ya kuhubiri, wanafunzi waliendelea kuhubiri na kufundisha “kila siku hekaluni na nyumba kwa nyumba.” (Mdo. 5:42) Maneno “nyumba kwa nyumba” yanamaanisha nini?

      Maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa “nyumba kwa nyumba,” katʼ oiʹkon, kihalisi yanamaanisha “kulingana na nyumba.” Watafsiri kadhaa wanasema neno ka·taʹ linamaanisha kwamba wanafunzi walihubiri kutoka nyumba moja hadi nyingine. Neno hilo ka·taʹ linatumiwa katika maana hiyohiyo katika andiko la Luka 8:1, linalosema kwamba Yesu alikuwa akihubiri “kutoka jiji mpaka jiji na kijiji mpaka kijiji.”

      Katika Matendo 20:20, neno hilo linatumiwa katika wingi, yaani, katʼ oiʹkous. Mtume Paulo aliwaambia waangalizi Wakristo: “Sikuepuka . . . kuwafundisha hadharani na nyumba kwa nyumba.” Tofauti na maoni ya watu fulani, inaonekana Paulo hakuwa akisema kwamba alifundisha nyumbani kwa wazee hao, kama vile mstari unaofuata unavyoonyesha: “Lakini nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.” (Mdo. 20:21) Waabudu wenzake tayari walikuwa wametubu na kumwamini Yesu. Hivyo, alihubiri na kufundisha nyumba kwa nyumba, akiwatolea ushahidi wasio waamini.

      Wanaume Wanaostahili Washughulikie “Kazi Hii Muhimu” (Mdo. 6:1-6)

      17-19. Ni jambo gani lililoleta mgawanyiko, na mitume walitoa maagizo gani?

      17 Jambo fulani lenye kuhatarisha amani ya kutaniko lilikuwa limeanza kutokea. Ni jambo gani hilo? Wanafunzi wengi waliobatizwa walikuwa wageni Yerusalemu nao walitaka kujifunza mengi kabla ya kurudi kwao. Wanafunzi waliokuwa wakiishi Yerusalemu walitoa michango kwa hiari ili kuwalisha wageni hao na kuwaandalia mahitaji mengine. (Mdo. 2:44-46; 4:34-37) Ndipo, tatizo fulani likatokea. Wajane waliozungumza Kigiriki “walikuwa wakipuuzwa katika ugawaji wa kila siku.” (Mdo. 6:1) Hata hivyo, mahitaji ya wajane Waebrania hayakukosa kuangaliwa. Hivyo, inaonekana kwamba tatizo lilikuwa ubaguzi. Ubaguzi ni mojawapo ya matatizo ambayo huleta mgawanyiko mkubwa.

      18 Mitume, waliokuwa wakitenda kama baraza linaloongoza la kutaniko hilo lililokuwa likizidi kuongezeka, waliona kwamba haifai ‘waache neno la Mungu ili kugawa chakula.’ (Mdo. 6:2) Ili kutatua jambo hilo, waliwaagiza wanafunzi watafute wanaume saba “waliojaa roho na hekima,” ambao mitume wangeweza kuwaweka rasmi juu ya “kazi [hiyo] muhimu.” (Mdo. 6:3) Mbali na kugawa chakula, huenda kazi hiyo ilitia ndani kushughulikia pesa, kununua bidhaa, na kuweka rekodi kwa uangalifu. Hivyo, wanaume wanaostahili walihitajika. Wanaume wote waliochaguliwa walikuwa na majina ya Kigiriki, jambo ambalo huenda lingewafanya wajane waliolalamika wahisi kwamba watatendewa haki. Baada ya kusali na kutafakari mapendekezo yaliyotolewa, mitume waliwaweka rasmi wanaume hao saba washughulikie “kazi [hiyo] muhimu.”e

      19 Kwa kuwa wanaume hao walipewa kazi ya kugawa chakula, je, hawakuwa na wajibu wa kuhubiri habari njema? Hapana! Stefano, mmoja wa wanaume waliochaguliwa, alikuwa mhubiri jasiri na mwenye bidii. (Mdo. 6:8-10) Filipo, ambaye pia alikuwa mmoja wao, aliitwa “mweneza-injili.” (Mdo. 21:8) Ni wazi kwamba wanaume hao saba waliendelea kutangaza Ufalme kwa bidii.

      20. Watu wa Yehova leo huigaje kielelezo cha mitume?

      20 Watumishi wa Yehova leo hufanya kazi waliyofanya mitume. Lazima wanaume wanaopendekezwa kutimiza majukumu mbalimbali kutanikoni waonyeshe kwamba roho takatifu inatenda kazi ndani yao. Chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza, wanaume wanaotimiza sifa za Kimaandiko huwekwa rasmi watumikie wakiwa wazee wa kutaniko au watumishi wa huduma.f (1 Tim. 3:1-9, 12, 13) Kwa kuwa wanatimiza sifa hizo, basi wamewekwa rasmi na roho takatifu. Wanaume hao wenye bidii hutimiza kazi mbalimbali muhimu. Kwa mfano, huenda wazee wa kutaniko wakapanga ndugu na dada waaminifu waliozeeka wapate msaada wanaohitaji. (Yak. 1:27) Wazee wengine wana kazi nyingi katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, kupanga makusanyiko, au kazi ya Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali. Watumishi wa huduma hutimiza majukumu mengi ambayo hayahusiani moja kwa moja na kazi ya uchungaji au ufundishaji. Wanaume wote hao wenye sifa za kustahili wanapaswa kuwa na usawaziko waposhughulikia majukumu ya kutaniko, mapendeleo katika tengenezo, na wajibu waliopewa na Mungu wa kuhubiri habari njema za Ufalme.​—1 Kor. 9:16.

      “Neno la Mungu Likazidi Kuenea” (Mdo. 6:7)

      21, 22. Tunajuaje kwamba Yehova alilibariki kutaniko la karne ya kwanza?

      21 Yehova alitegemeza kutaniko hilo jipya kukabiliana na mateso kutoka nje ya kutaniko na pia tatizo lenye kutokeza mgawanyiko lililozuka ndani ya kutaniko. Ni wazi kwamba Yehova alilibariki kutaniko. Tunasoma hivi: “Neno la Mungu likazidi kuenea, na idadi ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana huko Yerusalemu; na umati mkubwa wa makuhani wakawa waamini.” (Mdo. 6:7) Hiyo ni mojawapo ya ripoti nyingi zilizo katika kitabu cha Matendo, zinazoonyesha maendeleo ya kutaniko la Kikristo. (Mdo. 9:31; 12:24; 16:5; 19:20; 28:31) Je, si ni kweli kwamba sisi pia hutiwa moyo tunaposikia ripoti kuhusu maendeleo ya kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme katika maeneo mengine?

      22 Katika karne ya kwanza, viongozi wa kidini wenye hasira hawakuchoka. Baada ya muda mfupi wafuasi wa Yesu wangeanza kuteswa. Kwa mfano, Stefano aliteswa vikali, kama sura inayofuata itakavyoonyesha.

      GAMALIELI​—RABI ALIYEHESHIMIWA SANA

      Gamalieli anayetajwa katika kitabu cha Matendo, kwa kawaida anaitwa Mzee Gamalieli, mjukuu wa Hilleli, mwanzilishi wa mojawapo ya shule za Mafarisayo, ambayo haikushikilia mambo kupita kiasi. Gamalieli alikuwa na cheo kikubwa katika Sanhedrini, naye aliheshimiwa sana kati ya marabi hivi kwamba ndiye wa kwanza kuitwa kwa jina la cheo, “Rabani.” Mishna inasema hivi: “Rabani Mzee Gamalieli alipokufa, Sheria ilipoteza utukufu, na huo ukawa mwisho wa watakatifu na watawa.” Inasemekana kwamba alileta mabadiliko mengi yaliyowanufaisha watu mbalimbali. “Uamuzi mmoja muhimu aliofanya,” kulingana na Encyclopaedia Judaica, “ni kumruhusu mwanamke aolewe tena iwapo kuna ushahidi wa angalau mtu mmoja aliyeshuhudia kifo cha mume wa mwanamke huyo.” Pia, inasemekana kwamba alitunga sheria za kuwalinda wake dhidi ya waume wasiowajali na wajane dhidi ya watoto wasiowajali. Na pia inadaiwa kwamba alisema Watu wa Mataifa waliokuwa maskini walipaswa kuwa na haki sawa za kuokota vyakula kama Wayahudi maskini.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Sanhedrini—Mahakama Kuu ya Wayahudi,.”

      b Hii ndiyo mara ya kwanza kati ya mara 20 hivi ambapo malaika wanatajwa moja kwa moja katika kitabu cha Matendo. Mapema zaidi, andiko la Matendo 1:10 linazungumzia malaika kwa njia isiyo ya moja kwa moja likiwaita ‘wanaume wenye mavazi meupe.’

      c Ona sanduku lenye kichwa “Gamalieli—Rabi Aliyeheshimiwa Sana,.”.

      d Ona sanduku lenye kichwa “Kuhubiri ‘Nyumba kwa Nyumba,’.”

      e Yawezekana kwamba wanaume hao walikuwa wametimiza sifa za kustahili kuwa wazee, kwa sababu “kazi [hiyo] muhimu” ilikuwa mgawo mzito. Hata hivyo, Maandiko hayataji wakati hususa ambapo akina ndugu walianza kuwekwa rasmi kutumikia wakiwa wazee au waangalizi katika kutaniko la Kikristo.

      f Katika karne ya kwanza, wanaume wanaostahili waliruhusiwa kuwaweka rasmi wazee. (Mdo. 14:23; 1 Tim. 5:22; Tito 1:5) Leo, Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi waangalizi wa mzunguko, na waangalizi hao wana jukumu la kuwaweka rasmi wazee wa kutaniko na watumishi wa huduma.

  • Stefano—“Amejaa Kibali cha Mungu na Nguvu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 6

      Stefano—“Akiwa Amejaa Kibali cha Mungu na Nguvu”

      Ujasiri wa Stefano akiwa mbele ya Sanhedrini

      MATENDO 6:8–8:3

      1-3. (a) Stefano anakabili hali gani ngumu, naye anatendaje? (b) Tutachunguza maswali gani?

      STEFANO yuko mahakamani, mbele ya wanaume 71 katika jumba kubwa ambalo huenda liko karibu na hekalu la Yerusalemu. Mahakama hiyo inayoitwa Sanhedrini, imekutana ili kusikiliza kesi ya Stefano. Mahakimu wenyewe ni watu mashuhuri, wenye mamlaka, na wengi wao wanamdharau mwanafunzi huyo wa Yesu. Kuhani Mkuu Kayafa, ambaye alikuwa mkuu wa mahakama hiyo Yesu Kristo ilipohukumiwa kifo miezi michache iliyopita, ndiye aliyeitisha kikao hicho. Je, Stefano anaogopa?

      2 Sura ya Stefano inaonekana tofauti kabisa. Mahakimu wanapomkazia macho, wanaona kwamba uso wake ni “kama uso wa malaika.” (Mdo. 6:15) Malaika ni wajumbe wa Yehova Mungu, nao hawana sababu yoyote ya kuogopa bali huwa watulivu na wenye amani. Ndivyo alivyo Stefano—hata mahakimu hao wenye chuki kali wanaona hilo wazi. Ni nini kinachomwezesha kuwa mtulivu hivyo?

      3 Leo, Wakristo wanaweza kujifunza mengi kutokana na jibu la swali hilo. Pia, tunahitaji kujua jinsi Stefano alivyojikuta katika hali hiyo mbaya. Alikuwa ameiteteaje imani yake awali? Nasi tunaweza kumwiga jinsi gani?

      “Wakawachochea Watu” (Mdo. 6:8-15)

      4, 5. (a) Kwa nini Stefano alithaminiwa sana kutanikoni? (b) Stefano alikuwa “amejaa kibali cha Mungu na nguvu” jinsi gani?

      4 Tayari tumejifunza kwamba Stefano alithaminiwa sana katika kutaniko changa la Kikristo. Katika sura ya tano ya kitabu hiki, tuliona kwamba alikuwa miongoni mwa wanaume saba wanyenyekevu waliojitolea kuwasaidia mitume walipoombwa wafanye hivyo. Unyenyekevu wake unaonekana wazi unapozingatia vipawa alivyokuwa navyo. Andiko la Matendo 6:8 linasema kwamba alikuwa akifanya “mambo makubwa ya ajabu na ishara,” kama baadhi ya mitume. Pia, tunaambiwa kwamba alikuwa “amejaa kibali cha Mungu na nguvu.” Maneno hayo yanamaanisha nini?

      5 Neno la Kigiriki “kibali cha Mungu” linaweza kutafsiriwa pia “neema.” Inaonekana watu wengi walivutiwa sana na Stefano kwa sababu alishughulika nao kwa fadhili na heshima. Alizungumza kwa usadikisho sana hivi kwamba wasikilizaji wake waliona unyoofu wake wa moyoni na kweli muhimu alizokuwa akizungumzia. Alikuwa na nguvu nyingi kwa sababu alikuwa na roho ya Yehova, naye alikubali mwongozo wake. Badala ya kuwa na kiburi kwa sababu ya vipawa na uwezo wake, alielekeza sifa zote kwa Yehova na kuwahangaikia kwa upendo watu aliokuwa akizungumza nao. Si ajabu kwamba hata wapinzani wake walimwogopa!

      6-8. (a) Stefano alishtakiwa nini, na kwa nini? (b) Kwa nini mfano wa Stefano ni muhimu kwa Wakristo leo?

      6 Wanaume kadhaa walisimama ili kubishana na Stefano, lakini “hawakuweza kumshinda kwa sababu ya hekima yake na roho iliyomwongoza kusema.”a Wakiwa wamekasirika, “wakawashawishi watu kwa siri” walete mashtaka dhidi ya mfuasi huyo wa Kristo asiye na hatia. Pia, “wakawachochea watu,” wazee na waandishi, ili Stefano akamatwe kwa nguvu na kumpeleka kwenye Sanhedrini. (Mdo. 6:9-12) Washtaki hao walidai kwamba anamkufuru Mungu na Musa. Jinsi gani?

      7 Washtaki hao wa uwongo walidai kwamba Stefano amemkufuru Mungu na kwamba amesema makufuru dhidi ya “mahali hapa patakatifu,” yaani, hekalu la Yerusalemu. (Mdo. 6:13) Pia, walidai amemkufuru Musa, kwa kuwa aliidharau Sheria ya Musa, kwa kubadili desturi na mapokeo yaliyoanzishwa na Musa. Hilo lilikuwa shtaka zito sana, kwa sababu Wayahudi wa wakati huo walikazia sana hekalu, Sheria ya Musa, na mapokeo mengi yaliyopitishwa kwa mdomo, waliyoyaongeza kwenye Sheria. Kwa sababu hiyo, Stefano alionwa kuwa mtu hatari, anayestahili kifo!

      8 Kwa kusikitisha, watu wengi wa dini hutumia mbinu hizo kuwasumbua watumishi wa Mungu. Leo, wafuasi wa dini huwachochea wenye mamlaka wawatese Mashahidi wa Yehova. Tunaweza kufanya nini tunapokabili mashtaka ya uwongo? Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wa Stefano.

      Kutoa Ushahidi kwa Ujasiri Kuhusu “Mungu wa Utukufu” (Mdo. 7:1-53)

      9, 10. Wachambuzi fulani hudai nini, na ni jambo gani tunalopaswa kukumbuka?

      9 Kama ilivyotajwa mwanzoni, uso wa Stefano ulikuwa mtulivu kama wa malaika, alipokuwa akisikiliza mashtaka dhidi yake. Kwa hiyo Kayafa akamgeukia na kumwuliza: “Je, mambo hayo ni ya kweli?” (Mdo. 7:1) Sasa ulikuwa wakati wa Stefano kuongea, naye hakusita kufanya hivyo!

      10 Wachambuzi fulani hudai kwamba Stefano aliongea kwa muda mrefu na hakujibu mashtaka aliyoshtakiwa. Lakini, ukweli ni kwamba Stefano alituwekea mfano mzuri sana wa ‘kutetea’ habari njema. (1 Pet. 3:15) Kumbuka, alishtakiwa kwamba amemkufuru Mungu kwa kulivunjia heshima hekalu na amemkufuru Musa kwa kuidharau Sheria. Stefano alijibu kwa kuzungumzia vipindi vitatu katika historia ya taifa la Israeli, akikazia mambo fulani hususa. Acheni tuzungumzie vipindi hivyo.

      11, 12. (a) Stefano aliutumiaje vizuri mfano wa Abrahamu? (b) Kwa nini Stefano alimtaja Yosefu?

      11 Kipindi cha wazee wa ukoo. (Mdo. 7:1-16) Stefano alianza kwa kuzungumza kuhusu Abrahamu, aliyeheshimiwa na Wayahudi kwa sababu ya imani yake. Akianza kwa kuzungumzia jambo ambalo wote walikubaliana, Stefano alikazia kwamba Yehova, “Mungu wa utukufu,” alimtokea Abrahamu alipokuwa Mesopotamia. (Mdo. 7:2) Abrahamu alikuwa mkaaji mgeni katika Nchi ya Ahadi. Wakati huo, hakukuwa na hekalu wala Sheria ya Musa. Hivyo, mtu anawezaje kusisitiza kwamba uaminifu wa mtu kwa Mungu unategemea hekalu na Sheria ya Musa?

      12 Yosefu, aliyezaliwa katika ukoo wa Abrahamu, aliheshimiwa sana pia na baraza hilo lililokuwa likimsikiliza Stefano. Hata hivyo, Stefano aliwakumbusha kwamba ndugu za Yosefu, mababa wa makabila ya Israeli, walimtesa mtu huyo mwadilifu na kumuuza utumwani. Hata hivyo, Mungu alimtumia kuokoa Israeli wakati wa njaa kali. Inaonekana kwamba Stefano aliona ulinganisho huo ulio wazi kati ya maisha ya Yosefu na ya Yesu Kristo. Lakini, ili umati huo uendelee kumsikiliza kwa makini, hakutaja jambo hilo wakati huo.

      13. Mazungumzo kuhusu Musa yalijibu jinsi gani mashtaka yaliyoletwa dhidi ya Stefano, na ni jambo gani linalojitokeza wazi katika mazungumzo ya Stefano?

      13 Nyakati za Musa. (Mdo. 7:17-43) Stefano alisema mengi kuhusu Musa. Alikuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa wengi katika Sanhedrini walikuwa Masadukayo, waliokataa vitabu vingine vyote vya Biblia isipokuwa vile vilivyoandikwa na Musa. Pia, kumbuka Stefano alishtakiwa kwamba amemkufuru Musa. Maneno ya Stefano yalijibu shtaka hilo moja kwa moja, kwa kuwa yalionyesha wazi kwamba anamheshimu sana Musa na Sheria. (Mdo. 7:38) Alitaja kwamba Musa pia alikataliwa na watu aliokuwa akijaribu kuwaokoa. Walimkataa alipokuwa na umri wa miaka 40. Zaidi ya miaka 40 baadaye, walipinga uongozi wake mara kadhaa.b Jambo moja linajitokeza wazi katika mazungumzo ya Stefano: Mara kwa mara, watu wa Mungu waliwakataa watu waliowekwa rasmi na Yehova kuwaongoza.

      14. Stefano alitumia masimulizi ya Musa jinsi gani ili kutegemeza hoja yake?

      14 Stefano aliwakumbusha wasikilizaji wake kuwa Musa alikuwa ametabiri kwamba nabii kama Musa angetokea katika Israeli. Nabii huyo ni nani, naye angepokewa jinsi gani? Stefano aliamua kutojibu swali hilo hadi mwisho wa mazungumzo yake. Alitaja jambo lingine muhimu: Musa alijua kwamba mahali popote panaweza kuwa patakatifu, kama vile mahali palipokuwa na kichaka kinachowaka moto, ambapo Yehova alizungumza naye. Basi, je, ni lazima Yehova aabudiwe katika jengo fulani hususa, kama vile hekalu la Yerusalemu? Acheni tuone.

      15, 16. (a) Kwa nini hoja ya hema la ibada ilikuwa muhimu katika mazungumzo ya Stefano? (b) Stefano alisema nini kuhusu hekalu la Sulemani?

      15 Hema la ibada na hekalu. (Mdo. 7:44-50) Stefano aliikumbusha mahakama hiyo kwamba kabla hekalu lolote lile halijajengwa Yerusalemu, Mungu alimwagiza Musa ajenge hema la ibada ambalo lingeweza kuhamishwa. Kwa kuwa Musa mwenyewe aliabudu kwenye hema la ibada, hakuna yeyote kati yao angeweza kudai kwamba hema hilo la ibada halikufaa kwa sababu halikuwa hekalu.

      16 Baadaye, Sulemani alijenga hekalu Yerusalemu. Roho ya Mungu ilimchochea kusema jambo muhimu katika sala yake. Kama Stefano alivyosema, “Aliye Juu Zaidi haishi katika nyumba zilizojengwa kwa mikono.” (Mdo. 7:48; 2 Nya. 6:18) Yehova anaweza kutumia hekalu kutimiza makusudi yake, lakini si kwamba hana njia nyingine. Basi, mbona waabudu wake wahisi kwamba ibada ya kweli inategemea jengo fulani lililojengwa kwa mikono ya wanadamu? Stefano alimalizia hoja yake kwa kishindo kwa kunukuu kitabu cha Isaya: “Mbingu ni kiti changu cha ufalme, nayo dunia ni kiti cha miguu yangu. Mtanijengea nyumba ya aina gani? Asema Yehova. Au pako wapi mahali pangu pa kupumzikia? Mkono wangu uliumba vitu hivi vyote, sivyo?”​—Mdo. 7:49, 50; Isa. 66:1, 2.

      17. Katika mazungumzo yake, Stefano (a) alionyesha nini kuhusu mtazamo wa wasikilizaji wake na (b) alijibuje mashtaka dhidi yake?

      17 Unapochunguza mambo ambayo Stefano alisema mbele ya Sanhedrini, je, huoni kwamba alijibu kwa ustadi mambo aliyoshtakiwa? Alionyesha kwamba sikuzote kusudi la Yehova hutimizwa, na halizuiwi na mapokeo au desturi za wanadamu. Wale waliokuwa wakiabudu katika jengo hilo lenye kuvutia lililokuwa Yerusalemu na kushikilia desturi na mapokeo yaliyohusiana na Sheria ya Musa hawakuelewa kusudi la Sheria na hekalu! Ni kana kwamba Stefano alikuwa akisema: Njia bora zaidi ya kuheshimu Sheria na hekalu ni kumtii Yehova. Ni wazi kwamba maneno ya Stefano yalitetea vizuri matendo yake mwenyewe, kwa kuwa alifanya yote awezayo ili kumtii Yehova.

      18. Tunawezaje kumwiga Stefano?

      18 Tunaweza kujifunza nini kutokana na hotuba ya Stefano? Aliyajua Maandiko vizuri. Sisi pia tunapaswa kujifunza kwa bidii Neno la Mungu ili tuweze kulitumia “sawasawa neno la kweli.” (2 Tim. 2:15) Lazima pia tujifunze kuwa na neema na kutumia busara kama alivyofanya Stefano. Watu waliokuwa wakimsikiliza walikuwa wabishi sana! Hata hivyo, aliweza kuzungumza nao kwa muda mrefu, akizungumzia mambo ambayo hata wao waliyakubali na kuyathamini. Pia, alizungumza nao kwa heshima, akiwaita wazee wa mahakama hiyo, “akina baba.” (Mdo. 7:2) Sisi pia tunapaswa kutangaza kweli za Neno la Mungu “kwa upole na heshima kubwa.”​—1 Pet. 3:15.

      19. Stefano alitangaza hukumu za Yehova mbele ya Sanhedrini jinsi gani?

      19 Hata hivyo, hatuepuki kutangaza kweli za Neno la Mungu ili tu tusiwakasirishe watu; wala hatupunguzi uzito wa ujumbe wa hukumu za Yehova. Stefano alituwekea mfano mzuri. Bila shaka, aliona wazi kwamba uthibitisho wote aliotoa mbele ya Sanhedrini haukuwa na maana yoyote machoni pa mahakimu hao wenye mioyo migumu. Kwa hiyo, akichochewa na roho takatifu, alimalizia mazungumzo yake kwa kuwaambia bila woga kwamba walikuwa tu kama baba zao waliomkataa Yosefu, Musa, na manabii wote. (Mdo. 7:51-53) Isitoshe, mahakimu hao wa Sanhedrini walikuwa wamemuua Masihi, ambaye Musa na manabii wengine wote walitabiri kuja kwake. Kwa kweli, walikuwa wameivunja kabisa Sheria ya Musa!

      “Bwana Yesu, Pokea Roho Yangu” (Mdo. 7:54–8:3)

      Stefano amesimama kwa utulivu mbele ya Sanhedrini.

      “Waliposikia mambo hayo wakawaka hasira moyoni na kuanza kumsagia meno yao.”—Matendo 7:54

      20, 21. Sanhedrini ilitendaje iliposikia maneno ya Stefano, naye Yehova alimtia nguvu jinsi gani?

      20 Mahakimu hao walikasirishwa sana na mambo ya kweli ambayo Stefano aliwaambia. Bila kukawia, wakaanza kumsagia meno yao. Haikosi mwanamume huyo mwadilifu alikumbuka jinsi Bwana wake Yesu alivyotendewa kikatili, naye alijua kwamba hataonyeshwa rehema hata kidogo.

      21 Stefano alihitaji ujasiri ili kukabili hali iliyokuwa mbele yake. Bila shaka alitiwa moyo sana na maono ambayo Yehova alimwonyesha. Stefano aliuona utukufu wa Mungu, akamwona Yesu akiwa amesimama upande wa kulia wa Yehova! Stefano alipokuwa akisimulia maono hayo, mahakimu hao waliziba masikio kwa mikono yao. Kwa nini? Mapema, Yesu alikuwa ameiambia mahakama hiyo kwamba yeye ndiye Masihi na kwamba angeketi upande wa kulia wa Baba yake. (Marko 14:62) Maono ya Stefano yalithibitisha kwamba Yesu alisema kweli. Hakuna shaka kwamba mahakama hiyo ilikuwa imemsaliti na kumuua Masihi! Kwa pamoja wakamrukia wamtoe nje ili apigwe kwa mawe na kufa.c

      22, 23. Kifo cha Stefano kilifanana jinsi gani na kifo cha Bwana wake, na kwa nini Wakristo leo wanaweza kuwa na usadikisho kama wa Stefano?

      22 Stefano alikufa kama vile Bwana wake alivyokufa, akiwa na amani moyoni, akimtumaini kabisa Yehova na hakuwa na kinyongo chochote kuelekea waliomuua. Alisema, “Bwana Yesu, pokea roho yangu,” labda kwa sababu bado angeweza kumwona Mwana wa binadamu pamoja na Yehova katika maono. Huenda Stefano alijua maneno haya yenye kutia moyo yaliyosemwa na Yesu: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yoh. 11:25) Mwishowe, Stefano alisali moja kwa moja kwa Mungu kwa sauti kubwa: “Yehova, usiwahesabie dhambi hii.” Baada ya kusema hayo, akalala usingizi katika kifo.​—Mdo. 7:59, 60.

      23 Hivyo, Stefano akawa mfia-imani wa kwanza kati ya wafuasi wa Kristo. (Ona sanduku lenye kichwa “Stefano—Alikuwa Shahidi au Mfia-Imani?”) Hata hivyo, jambo la kusikitisha ni kwamba hakuwa wa mwisho. Leo, watumishi waaminifu wa Yehova wameuawa na wafuasi wa dini, wanasiasa, na wapinzani wengine wakatili. Hata hivyo, tuna sababu nzuri ya kuwa na usadikisho kama aliokuwa nao Stefano. Sasa, Yesu anatawala akiwa Mfalme, na ana nguvu nyingi alizopewa na Baba yake. Hakuna kitakachomzuia kuwafufua wafuasi wake waaminifu.​—Yoh. 5:28, 29.

      STEFANO—ALIKUWA SHAHIDI AU MFIA-IMANI?

      Biblia humrejelea Stefano kwa neno la Kigiriki marʹtys, linalomaanisha “shahidi,” yaani, mtu anayeshuhudia tendo au tukio fulani. Hata hivyo, neno hilo la Kigiriki lina maana pana. Kamusi moja ya Kigiriki inataja kwamba watu wanaorejelewa kwa neno hilo katika Biblia, “walikuwa na wajibu wa kuwajulisha wengine mambo waliyokuwa wamejionea na kusikia, na kutangaza waliyojua.” Wakristo wote wa kweli wana wajibu wa kutangaza mambo wanayojua kumhusu Yehova na makusudi yake. (Luka 24:48; Mdo. 1:8) Maandiko yanamwita Stefano “shahidi” kwa sababu alihubiri kumhusu Yesu.​—Mdo. 22:20.

      Mara nyingi Wakristo wanaotoa ushahidi hupingwa, hukamatwa, hupigwa, na hata kuuawa. Hivyo, tangu karne ya pili, neno la Kigiriki marʹtys lilianza pia kumaanisha mtu anayepingwa, kukamatwa, kupigwa, au hata kuuawa kwa sababu ya imani yake. Katika maana hiyo, tunaweza kusema kwamba Stefano ndiye Mkristo wa kwanza kufa kwa sababu ya imani. Vyovyote vile, mwanzoni mtu aliitwa marʹtys kwa sababu ya kutoa ushahidi, wala si kwa kuwa ni mfia-imani.

      24. Sauli alichangiaje kuuawa kwa Stefano, na kifo cha Stefano kilikuwa na matokeo gani mazuri baadaye?

      24 Kijana Sauli alikuwa akitazama mambo yote yaliyokuwa yakiendelea. Aliunga mkono kuuawa kwa Stefano, hata alitunza mavazi ya nje ya wale waliokuwa wakimpiga kwa mawe. Muda mfupi baadaye aliongoza katika kuwanyanyasa vikali Wakristo. Lakini kifo cha Stefano kingekuwa na matokeo mazuri baadaye. Mfano wake uliwaimarisha Wakristo wengine waendelee kuwa waaminifu mpaka mwisho kama alivyofanya. Isitoshe, Sauli, ambaye baadaye alikuja kujulikana kama Paulo, alisikitishwa sana baadaye kwa sababu ya msimamo wake Stefano alipokuwa akiuawa. (Mdo. 22:20) Alichangia kumwua Stefano, lakini baadaye alitambua makosa yake na kukiri hivi: “Nilikuwa mkufuru na mtesaji na mtu mwenye dharau.” (1 Tim. 1:13) Ni wazi kwamba, Paulo hakumsahau kamwe Stefano, na mambo yenye kuchochea sana aliyosema siku hiyo. Isitoshe, katika baadhi ya hotuba zake na barua alizoandika, Paulo alitia ndani mambo ambayo Stefano alitaja. (Mdo. 7:48; 17:24; Ebr. 9:24) Baadaye, Paulo aliiga imani na ujasiri wa Stefano, mtu aliyekuwa “amejaa kibali cha Mungu na nguvu.” Je, sisi pia tutafanya hivyo?

      a Baadhi ya wapinzani hao walikuwa sehemu ya “Sinagogi la Watu Waliowekwa Huru.” Huenda walikuwa watu waliokuwa wamekamatwa na Waroma kisha wakaachiliwa, au huenda walikuwa watumwa waliowekwa huru kisha wakawa Wayahudi wageuzwa imani. Baadhi yao walikuwa wenyeji wa Kilikia, alikotoka Sauli wa Tarso. Masimulizi hayo hayataji iwapo Sauli alikuwa miongoni mwa Wakilikia waliokuwa wameshindwa kuthibitisha kwamba walikuwa sahihi kuhusu madai yao dhidi ya Stefano.

      b Stefano anazungumzia habari ambazo hazipatikani kwingineko katika Biblia. Habari hizo zinatia ndani elimu ambayo Musa alipata alipokuwa Misri, umri aliokuwa nao alipokimbia Misri, na muda aliokaa Midiani.

      c Chini ya sheria ya Roma, inaelekea kwamba Sanhedrini haikuwa na mamlaka ya kumhukumu mtu kifo. (Yoh. 18:31) Vyovyote vile, inaonekana kwamba Stefano aliuawa na umati uliokuwa na hasira, bali si hukumu ya kifo iliyokuwa ikitekelezwa.

  • Kutangaza “Habari Njema Kumhusu Yesu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 7

      Kutangaza “Habari Njema Kumhusu Yesu”

      Filipo aweka mfano mzuri katika kueneza Injili

      MATENDO 8:4-40

      1, 2. Ni kwa njia gani jitihada za kuzuia kazi ya kuhubiri habari njema katika karne ya kwanza hazikufanikiwa?

      MATESO makali yameanza, na Sauli akaanza “kulishambulia” kutaniko—maneno ambayo katika lugha ya awali, yanamaanisha kulitesa kutaniko kikatili. (Mdo. 8:3) Wanafunzi wanatawanyika. Huenda kwa watu fulani ikaonekana kwamba lengo la Sauli la kuumaliza Ukristo litatimia. Hata hivyo, kwa sababu ya kutawanyika kwa Wakristo jambo fulani lisilotarajiwa linatokea. Jambo gani?

      2 Wakristo hao waliotawanyika wakaanza ‘kutangaza habari njema ya lile neno’ katika nchi ambazo wamekimbilia. (Mdo. 8:4) Hebu wazia! Mateso hayakuzuia habari njema bali yalichangia kuenea kwa ujumbe huo! Kwa kuwatawanya wanafunzi, bila kukusudia, watesaji hao wamesaidia kazi ya kuhubiri Ufalme ienee katika maeneo ya mbali. Kama tutakavyoona, jambo fulani linalofanana na hilo limetokea katika siku zetu.

      “Wale Waliotawanyika” (Mdo. 8:4-8)

      3. (a) Filipo alikuwa nani? (b) Kwa nini Samaria haikuwa imehubiriwa sana, na Yesu alitabiri nini kuhusu eneo hilo?

      3 Filipo ni mmoja wa “wale waliotawanyika.”a (Mdo. 8:4; ona sanduku “Filipo ‘Mweneza-Injili,’”) Alienda Samaria, jiji ambalo halikuwa limehubiriwa sana kwa sababu wakati fulani Yesu aliwaagiza mitume hivi: “Msiingie katika jiji lolote la Wasamaria; badala yake, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mt. 10:5, 6) Hata hivyo, Yesu alijua kwamba baada ya muda fulani ushahidi kamili ungetolewa Samaria, kwa sababu kabla ya kurudi mbinguni, alisema: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”​—Mdo. 1:8.

      4. Wasamaria walipokeaje habari njema alizowatangazia Filipo, na huenda ni kwa sababu gani?

      4 Filipo aliona kwamba shamba la Samaria lilikuwa ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’ (Yoh. 4:35) Ujumbe wake uliwaburudisha watu waliokuwa wakiishi huko, na tunaweza kuelewa sababu. Wayahudi hawakuchangamana na Wasamaria, na wengi wao walionyesha chuki yao waziwazi. Kinyume na hilo, Wasamaria waliona kwamba ujumbe wa habari njema uliwapa tumaini watu wote bila ubaguzi, nao ulikuwa kinyume kabisa na mtazamo wa ubaguzi wa Mafarisayo. Kwa kuwahubiria Wasamaria kwa bidii na bila ubaguzi, Filipo alionyesha kwamba hakuathiriwa na maoni ya ubaguzi ya wale waliokuwa wanawadharau. Kwa hiyo, haishangazi kwamba umati wote wa Wasamaria ulikuwa ukimsikiliza Filipo “kwa pamoja.”​—Mdo. 8:6.

      5-7. Toa mifano inayoonyesha jinsi kutawanywa kwa Wakristo kumesaidia kueneza habari njema.

      5 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, mateso hayajawazuia watu wa Mungu kuendelea na kazi yao ya kuhubiri leo. Wakristo waliolazimika kuhama, iwe kwa sababu ya kufungwa gerezani au kuhamishiwa nchi nyingine, wametumia fursa hiyo kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika maeneo hayo mapya. Kwa mfano, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova waliwahubiria wafungwa wenzao katika kambi za mateso za Nazi. Myahudi mmoja aliyekutana na Mashahidi katika kambi hizo alisema hivi: “Ujasiri wa wafungwa waliokuwa Mashahidi wa Yehova ulinihakikishia kwamba imani yao ilikuwa na msingi wa Kimaandiko—nami nikawa Shahidi.”

      6 Katika visa fulani hata wale waliowatesa walihubiriwa na kukubali ujumbe. Kwa mfano, Ndugu Franz Desch alipokuwa katika kambi ya mateso ya Gusen nchini Austria, alijifunza Biblia na ofisa mmoja wa Nazi. Wazia shangwe yao, miaka mingi baadaye, wanaume hao wawili walipokutana kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, wote wakiwa wahubiri wa habari njema!

      7 Ndivyo ilivyokuwa wakati mateso yaliposababisha Wakristo katika nchi moja wakimbilie nchi nyingine. Miaka ya 1970, ushahidi mkubwa ulitolewa nchini Msumbiji wakati Mashahidi kutoka Malawi walipolazimika kukimbilia huko. Baadaye upinzani ulipotokea nchini Msumbiji, kazi ya kuhubiri iliendelea. Francisco Coana anasema: ‘Baadhi yetu tulikamatwa mara kadhaa kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri. Lakini, tulipoona wengi wakiitikia ujumbe wa Ufalme, tulikuwa na hakika kwamba Mungu anatusaidia, kama alivyowasaidia Wakristo wa karne ya kwanza.’

      8. Mabadiliko ya kisiasa na ya kiuchumi yamekuwa na matokeo gani katika kazi ya kuhubiri?

      8 Bila shaka, si mateso tu yaliyochangia kuenea kwa Ukristo katika maeneo mengine. Mabadiliko ya kisiasa na ya kiuchumi yamewezesha ujumbe wa Ufalme uhubiriwe kwa watu wa lugha na mataifa mengi. Watu fulani kutoka katika maeneo yenye vita na hali ngumu za kiuchumi wamehamia katika nchi zenye utulivu na kujifunza Biblia wakiwa huko. Ongezeko la wakimbizi limefungua maeneo mapya ya lugha za kigeni. Je, unafanya yote uwezayo ili kuwahubiria watu “kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha” walio katika eneo lenu?​—Ufu. 7:9.

      “Nipeni Mimi Pia Mamlaka Hii” (Mdo. 8:9-25)

      Simoni ambaye zamani alikuwa akifanya uchawi, anamkaribia mtume huku akiwa ameshika mfuko wa pesa. Mtume ameweka mikono yake mabegani mwa mwanamume Mkristo. Nyuma yao, mwanamume mwingine Mkristo anamponya binti mlemavu mbele ya watazamaji wenye furaha.

      “Simoni alipoona kwamba watu walipokea roho takatifu mitume walipoweka mikono juu yao, akawatolea pesa.”—Matendo 8:18

      9. Simoni alikuwa nani, na kwa nini alivutiwa na Filipo?

      9 Filipo alifanya ishara nyingi jijini Samaria. Aliwaponya walemavu na kuwafukuza roho waovu. (Mdo. 8:6-8) Mtu mmoja alivutiwa sana na uwezo wa Filipo wa kufanya miujiza. Aliitwa Simoni, naye alikuwa mchawi ambaye aliheshimiwa sana hivi kwamba watu walikuwa wakisema: “Mtu huyu ndiye Nguvu za Mungu.” Simoni alijionea mwenyewe nguvu za kweli za Mungu kutokana na miujiza iliyofanywa na Filipo, naye akawa mwamini. (Mdo. 8:9-13) Hata hivyo, baadaye nia ya Simoni ilijaribiwa. Jinsi gani?

      10. (a) Petro na Yohana walifanya nini jijini Samaria? (b) Simoni alifanya nini alipoona wapya wakipokea roho takatifu baada ya Petro na Yohana kuwawekea mikono?

      10 Mitume walipoona kwamba kulikuwa na ongezeko kubwa jijini Samaria, waliwatuma Petro na Yohana huko. (Ona sanduku “Petro Atumia ‘Funguo za Ufalme.’”) Mitume hao wawili walipofika waliweka mikono yao juu ya wanafunzi wapya, na kila mmoja wao akapokea roho takatifu.b Simoni alipoona hivyo, alistaajabu. Akawaambia mitume hao: “Nipeni mimi pia mamlaka hii, ili yeyote nitakayeweka mikono juu yake apokee roho takatifu.” Simoni hata alitaka kuwapa pesa wamuuzie pendeleo hilo takatifu!—Mdo. 8:14-19.

      11. Petro alimwambia Simoni nini, naye Simoni aliitikiaje?

      11 Petro alimkaripia Simoni na kumwambia: “Fedha yako na iangamie pamoja nawe, kwa sababu ulidhani utanunua zawadi ya bure ya Mungu kwa kutumia pesa. Wewe huna sehemu wala fungu katika jambo hili, kwa maana moyo wako si mnyoofu machoni pa Mungu.” Kisha, Petro akamhimiza Simoni atubu na kuomba msamaha. Petro akasema: ‘Mwombe Yehova dua, ili ikiwezekana, usamehewe nia mbaya ya moyo wako.’ Inaonekana kwamba Simoni hakuwa mtu mwovu; alitaka kufanya yaliyo sawa, lakini kwa muda hakuwa na maoni yanayofaa. Kwa hiyo, akawasihi mitume: “Mwombeni Yehova dua kwa ajili yangu ili nisipatwe na lolote kati ya mambo mliyosema.”​—Mdo. 8:20-24.

      12. “Usimoni” ni nini, na dini zinazodai kuwa za Kikristo zimetumbukiaje katika mtego huo?

      12 Karipio hilo lapaswa pia kuwa onyo kwa Wakristo leo. Neno “usimoni” latokana na kisa hicho nalo linamaanisha kununua au kuuza vyeo, hasa vya kanisa. Usimoni umeenea sana katika dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kitabu kimoja kinasema: ‘Historia ya mabaraza ya siri ya Mapapa inaonyesha wazi kwamba hakujawahi kuwa na uchaguzi wowote wa kanisa usiokuwa na usimoni, na katika visa vingi, usimoni wenyewe ulikuwa usimoni mbaya sana, wenye kuaibisha, tena ulifanywa waziwazi.’​—The Encyclopædia Britannica (1878).

      13. Wakristo wanapaswa kuepuka usimoni kwa njia gani?

      13 Wakristo wanapaswa kujihadhari na dhambi ya usimoni. Kwa mfano, hawapaswi kujaribu kupata mapendeleo kutanikoni kwa kuwapa zawadi au kuwasifu kupita kiasi ndugu wenye madaraka. Kwa upande mwingine, ndugu hao wenye madaraka wanapaswa kuwa waangalifu wasiwaonyeshe watu wenye mali upendeleo. Yote hayo ni usimoni. Watumishi wote wa Mungu wanapaswa kujiendesha kama ‘walio wadogo,’ na kuonyesha subira huku wakiiruhusu roho takatifu ya Yehova iweke rasmi wale wanaostahili. (Luka 9:48) Katika tengenezo la Mungu, hakuna nafasi kwa ajili ya watu wanaojaribu ‘kujitafutia utukufu wao wenyewe.’​—Met. 25:27.

      PETRO ATUMIA “FUNGUO ZA UFALME”

      Yesu alimwambia Petro: “Nitakupa funguo za Ufalme wa mbinguni.” (Mt. 16:19) Yesu alimaanisha nini? “Funguo” zinazotajwa na Yesu zinadokeza kwamba Petro angefungulia vikundi vya watu fulani hususa nafasi ya kupata ujuzi na pendeleo la kuingia katika Ufalme wa Kimasihi. Petro alitumia funguo hizo wakati gani?

      • Petro aliutumia ufunguo wa kwanza siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., alipowatia moyo Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani watubu na kubatizwa. Watu wapatao 3,000 walifanya hivyo na wakawa warithi watarajiwa wa Ufalme.​—Mdo. 2:1-41.

      • Ufunguo wa pili ulitumiwa baada ya Stefano kuuawa. Katika pindi hiyo, Petro na Yohana waliweka mikono yao juu ya Wasamaria waliokuwa wametoka kubatizwa, nao wakapokea roho takatifu.​—Mdo. 8:14-17.

      • Petro aliutumia ufunguo wa tatu mwaka wa 36 W.K. Mwaka huo, aliwafungulia watu wa Mataifa wasiotahiriwa tumaini la kupata urithi wa mbinguni. Hilo lilitokea wakati ambapo mtume huyo alimtolea ushahidi Kornelio, mtu wa kwanza asiyetahiriwa aliyekuwa mwanafunzi wa Yesu.​—Mdo. 10:1-48.

      “Je, Kweli Unajua Unayosoma?” (Mdo. 8:26-40)

      14, 15. (a) “Towashi Mwethiopia” alikuwa nani, na Filipo alikutana naye jinsi gani? (b) Mwethiopia huyo aitikiaje ujumbe wa Filipo, na kwa nini uamuzi wake wa kubatizwa haukutokana tu na msisimko? (Ona maelezo ya chini.)

      14 Malaika wa Yehova anamwambia Filipo aende kwenye barabara inayoshuka kutoka Yerusalemu mpaka Gaza. Muda mfupi baadaye, Filipo anaelewa sababu ya kutumwa baada ya kukutana na towashi Mwethiopia ambaye “alikuwa akimsoma kwa sauti kubwa nabii Isaya.” (Ona sanduku “‘Towashi’ Katika Maana Gani?”) Roho takatifu ya Yehova ilimwongoza Filipo alikaribie gari la mtu huyo. Huku akikimbia kandokando ya gari hilo, Filipo alimuuliza Mwethiopia huyo: “Je, kweli unajua unayosoma?” Mwethiopia akajibu: “Ninawezaje kuyaelewa mtu fulani asiponiongoza?”​—Mdo. 8:26-31.

      15 Mwethiopia akamsihi Filipo apande kwenye gari. Wazia mazungumzo yaliyofuata! Kwa muda mrefu, haikujulikana ni nani anayezungumziwa katika unabii unaohusu “kondoo,” au “mtumishi,” katika kitabu cha Isaya. (Isa. 53:1-12) Hata hivyo, walipokuwa wakiendelea na safari, Filipo alimfafanulia kwamba Yesu Kristo ndiye anayezungumziwa katika unabii huo. Kama wale waliobatizwa siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., Mwethiopia huyo ambaye tayari alikuwa Myahudi mgeuzwa imani akajua mara moja jambo analopaswa kufanya. Kisha akamwambia Filipo. “Tazama! Hapa kuna maji; ni nini kinachonizuia kubatizwa?” Bila kukawia, Filipo akambatiza Mwethiopia huyo!c (Ona sanduku “Kubatizwa ‘Mahali Penye Maji.’”) Kisha, roho ya Mungu ikamwongoza Filipo kwenda katika mgawo mwingine huko Ashdodi, ambako aliendelea kutangaza habari njema.​—Mdo. 8:32-40.

      “TOWASHI” KATIKA MAANA GANI?

      Neno la Kigiriki eu·nouʹkhos, linalotafsiriwa “towashi,” linaweza kurejelea mwanamume asiyeweza kuzaa au ofisa mwenye cheo kikubwa katika makao ya mfalme. Inawezekana kwamba maofisa hao, ambao walikuwa na jukumu la kusimamia nyumba za wake wa mfalme, walihasiwa. Hata hivyo, maofisa wengine, kama vile mnyweshaji wa mfalme au mtunza hazina, hawakuhitaji kuhasiwa. Inaonekana kwamba towashi Mwethiopia ambaye Filipo alimbatiza hakuwa ofisa aliyehasiwa, kwa sababu alikuwa mtunza hazina ya mfalme, au waziri wa fedha.

      Pia, Mwethiopia huyo alikuwa mgeuzwa imani. Kwa ujumla, wageuzwa imani walikuwa watu wasio Wayahudi ambao waliamua kumwabudu Yehova. Alikuwa anatoka Yerusalemu kuabudu. (Mdo. 8:27) Ndiyo sababu tunaweza kusema kwamba Mwethiopia huyo hakuwa towashi katika maana halisi, kulingana na Sheria ya Musa, mwanamume yeyote aliyehasiwa hakupaswa kujiunga na kutaniko la Israeli.​—Kum. 23:1.

      KUBATIZWA “MAHALI PENYE MAJI”

      Wakristo wanapaswa kubatizwa jinsi gani? Watu fulani huamini kwamba mtu anaweza kubatizwa kwa kumwagiwa au kunyunyiziwa maji kichwani. Hata hivyo, towashi Mwethiopia alibatizwa “mahali penye maji.” Simulizi hilo linasema: “Wote wawili Filipo na towashi wakaingia ndani ya maji.” (Mdo. 8:36, 38) Ikiwa ubatizo ungeweza kufanywa kwa kumwagiwa au kunyunyiziwa maji, towashi huyo hakuhitaji kuamuru gari lisimamishwe mahali penye maji. Hata maji kidogo tu katika kiriba cha ngozi yangetosha. Kwa kuwa alisafiri kwenye “barabara ya jangwani,” huenda alibeba maji ya kunywa.​—Mdo. 8:26.

      Kulingana na kitabu kimoja cha Liddell na Scott, neno la Kigiriki ba·ptiʹzo, linalotafsiriwa “batiza” katika Kiswahili, linamaanisha “kuzamisha, au kutumbukiza.” (A Greek-English Lexicon) Ufafanuzi huo unapatana na maelezo ya Biblia kuhusu ubatizo. Andiko la Yohana 3:23 linasema kwamba Yohana “alikuwa akibatiza huko Ainoni karibu na Salimu, kwa sababu kulikuwa na maji mengi huko.” Vivyo hivyo, simulizi kuhusu ubatizo wa Yesu linasema: “Alipotoka katika maji [Yesu] akaona mbingu zikifunguka.” (Marko 1:9, 10) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli wanapaswa kubatizwa kwa kuzamishwa kabisa ndani ya maji.

      16, 17. Malaika wanahusika jinsi gani katika kazi ya kuhubiri leo?

      16 Wakristo leo wana pendeleo la kushiriki kazi kama iliyofanywa na Filipo. Mara nyingi, wanaposafiri wanatumia nafasi hiyo kuwahubiria watu ujumbe wa Ufalme. Katika visa vingi, wanapopata mtu mnyoofu, hawashangai kwa sababu Biblia inaonyesha wazi kwamba malaika wanaelekeza kazi ya kuhubiri ili ujumbe huo ufikie “kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6) Yesu alitabiri kwamba malaika wangeelekeza kazi ya kuhubiri. Katika mfano wa ngano na magugu, Yesu alisema kwamba wakati wa mavuno, au umalizio wa mfumo wa mambo, “wavunaji ni malaika.” Pia, alisema, viumbe hao wa kiroho “watakusanya kutoka katika Ufalme wake vitu vyote vinavyosababisha kukwazika na watu wenye mazoea ya kuasi sheria.” (Mt. 13:37-41) Wakati huohuo, malaika watakusanya watu watakaorithi Ufalme wa mbinguni, kisha watakusanya “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” ambao Yehova anawavuta katika tengenezo lake.​—Ufu. 7:9; Yoh. 6:44, 65; 10:16.

      17 Jambo moja linalothibitisha kwamba malaika wanaelekeza kazi yetu ni kwamba watu fulani tunaowapata katika huduma yetu husema kwamba wamekuwa wakisali ili wapate mwongozo wa kiroho. Fikiria jambo moja lililoonwa: Wahubiri wawili wa Ufalme walikuwa wakihubiri pamoja na mtoto mdogo. Ilipofika mchana, wahubiri hao walipotaka kuondoka kwenye eneo, yule mtoto alitaka sana waende nyumba inayofuata. Alienda kubisha mlango huo! Mwanamke alipoufungua mlango, Mashahidi hao wawili wakakaribia ili kuzungumza naye. Walishangaa kusikia kwamba mwanamke huyo alikuwa ametoka tu kusali mtu amtembelee na kumsaidia kuelewa Biblia. Funzo la Biblia likaanzishwa!

      Wenzi wa ndoa walio katika huduma wakibonyeza kengele ya mlango katika nyumba ya mwanamke anayesali.

      “Mungu, ikiwa upo, tafadhali nisaidie”

      18. Kwa nini hatupaswi kamwe kuipuuza huduma yetu?

      18 Ukiwa mmoja wa wahubiri katika kutaniko la Kikristo, una pendeleo la kushiriki bega kwa bega katika kazi ya kuhubiri ambayo leo inafanywa kwa kiwango kikubwa zaidi. Usilipuuze kamwe pendeleo hilo. Ukidumu katika kazi hiyo, utapata shangwe kubwa inayotokana na kutangaza “habari njema kumhusu Yesu.”​—Mdo. 8:35.

      FILIPO “MWENEZA-INJILI”

      Wafuasi wa Kristo walipotawanyika kwa sababu ya mateso, Filipo alienda Samaria. Inaonekana kwamba alishirikiana sana na baraza linaloongoza la karne ya kwanza, ndiyo sababu “mitume huko Yerusalemu waliposikia kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawatuma Petro na Yohana kwao.” Kisha, waamini wapya katika eneo hilo wakapokea zawadi ya bure ya roho takatifu.​—Mdo. 8:14-17.

      Filipo amekaa ndani ya gari la towashi Mwethiopia.

      Baada ya matukio yaliyo katika sura ya 8 ya kitabu cha Matendo, Filipo anatajwa tena mara moja tu. Miaka 20 hivi baadaye, mtume Paulo na wenzake walikuwa wakisafiri kuelekea Yerusalemu mwishoni mwa safari ya tatu ya umishonari ya Paulo. Wakatia nanga katika bandari ya Tolemai. Luka anasema hivi: “Siku iliyofuata tukaondoka na kufika Kaisaria, tukaingia katika nyumba ya Filipo mweneza-injili, aliyekuwa mmoja wa wale wanaume saba, nasi tukakaa pamoja naye. Mtu huyo alikuwa na binti wanne ambao hawakuwa wameolewa, nao walitoa unabii.”​—Mdo. 21:8, 9.

      Inaonekana kwamba Filipo na familia yake waliamua kukaa katika eneo walilokuwa wakihubiri. Ndiyo sababu Luka anamwita “mweneza-injili.” Katika Maandiko, neno hilo hurejelea watu ambao wamehamia maeneo mengine ili kuhubiri habari njema kwenye maeneo ambayo hayajahubiriwa. Hivyo, ni wazi kwamba Filipo aliendelea kuwa mwenye bidii katika huduma. Na kwa kuwa alikuwa na binti wanne waliokuwa wakitoa unabii, bila shaka alifundisha familia yake kumpenda na kumtumikia Yehova.

      a Filipo huyu si mtume Filipo. Badala yake, ni Filipo ambaye, kama Sura ya 5 ya kitabu hiki inavyoeleza, alikuwa mmoja wa “wanaume saba wenye sifa nzuri” ambao waliwekwa rasmi kusimamia ugawaji wa kila siku wa chakula kati ya Wakristo wajane waliozungumza Kigiriki na waliozungumza Kiebrania katika jiji la Yerusalemu.​—Mdo. 6:1-6.

      b Inaonekana kwamba kwa kawaida wanafunzi wapya walitiwa mafuta, au kupokea roho takatifu walipobatizwa. Baada ya kupokea roho hiyo, wakawa na tumaini la kutawala wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Yesu mbinguni. (2 Kor. 1:21, 22; Ufu. 5:9, 10; 20:6) Hata hivyo, katika kisa hiki, Wakristo wapya hawakutiwa mafuta walipobatizwa. Walipokea roho takatifu pamoja na uwezo wa kufanya miujiza walipowekewa mikono na Petro na Yohana.

      c Huo haukuwa msisimko tu. Kwa kuwa alikuwa Myahudi mgeuzwa imani, tayari alikuwa na ujuzi wa Maandiko, kutia ndani unabii kuhusu Masihi. Baada ya kuelewa jukumu la Yesu katika mpango wa Mungu, hakuna jambo lililomzuia kubatizwa.

  • Kutaniko “Likaingia Katika Kipindi cha Amani”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 8

      Kutaniko “Likaingia Katika Kipindi cha Amani”

      Sauli, aliyekuwa mtesaji mkatili awa mhubiri mwenye bidii

      Matendo 9:1-43

      1, 2. Sauli alikusudia kufanya nini Damasko?

      WASAFIRI wenye hasira kali wanakaribia Damasko, ambapo wanakusudia kutekeleza njama yao. Wanawachukia wanafunzi wa Yesu. Wanataka kuwakamata kwa nguvu, kuwafunga, kuwaaibisha, na kuwapeleka Yerusalemu mbele ya Sanhedrini.

      2 Tayari kiongozi wa kikundi hicho, Sauli, ana hatia ya damu ya mmoja wa wanafunzi hao.a Siku chache zilizopita, wenzake walipokuwa wakimuua Stefano, mwanafunzi mwenye bidii wa Yesu kwa kumpiga mawe, Sauli alikuwa akiwatazama na kuunga mkono jambo hilo. (Mdo. 7:57–8:1) Sauli hajatosheka kuwatesa wafuasi wa Yesu wanaoishi Yerusalemu, naye anachochea zaidi mateso. Alitaka kuangamiza kabisa kikundi hicho cha dini kinachoitwa “Ile Njia.”​—Mdo. 9:1, 2; ona sanduku lenye kichwa “Mamlaka ya Sauli Jijini Damasko,”.

      3, 4. (a) Ni nini kilimpata Sauli? (b) Tutachunguza maswali gani?

      3 Ghafla, nuru nyangavu yamfunika Sauli. Wasafiri wenzake wanaiona nuru hiyo na kushangaa sana. Sauli apigwa kwa upofu na kuanguka. Kisha, akasikia sauti kutoka mbinguni ikisema: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Sauli akauliza hivi kwa mshangao: “Wewe ni nani, Bwana?” Anapata jibu lenye kushangaza: “Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa.”​—Mdo. 9:3-5; 22:9.

      4 Tunaweza kujifunza nini kutokana na swali ambalo Yesu alimwuliza Sauli? Tunaweza kunufaikaje kwa kuchunguza mambo yaliyotokea pindi hiyo? Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi kutaniko lilivyotumia kipindi cha amani kilichofuata baada ya kugeuzwa imani kwa Sauli?

      MAMLAKA YA SAULI JIJINI DAMASKO

      Sauli alitoa wapi mamlaka ya kuwakamata Wakristo katika jiji lingine? Sanhedrini na kuhani mkuu walikuwa na mamlaka juu ya Wayahudi wote, naye kuhani mkuu alikuwa na mamlaka ya kuwarudisha wakosaji ili wahukumiwe. Kwa sababu hiyo, wazee wa masinagogi ya Damasko walikuwa na wajibu wa kufuata maagizo ya barua zilizotoka kwa kuhani mkuu.​—Mdo. 9:1, 2.

      Isitoshe, Waroma walikuwa wamewapa Wayahudi uhuru wa kuamua kesi zao wenyewe. Ndiyo sababu mara tano Wayahudi walimpiga mtume Paulo “viboko 40 kasoro kimoja.” (2 Kor. 11:24) Kitabu cha Kwanza cha Wamakabayo kinataja pia barua ambayo balozi wa Waroma alimwandikia Tolemayo wa Nane wa Misri mwaka wa 138 K.W.K., inayosema: “Kama waasi wowote wametoroka nchi yao na kukimbilia kwenu, warudisheni kwa Simoni, kuhani mkuu, awaadhibu kwa sheria yao.” (1 Wamakabayo 15:21) Katika mwaka wa 47 K.W.K., Kaisari Yulio, aliidhinisha rasmi mamlaka ya kuhani mkuu na jukumu lake la kushughulikia mambo yoyote yanayohusiana na desturi za Kiyahudi.

      “Kwa Nini Unanitesa?” (Mdo. 9:1-5)

      5, 6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na swali ambalo Yesu alimuuliza Sauli?

      5 Yesu alipomsimamisha Sauli akiwa njiani kuelekea Damasko, hakumuuliza: “Kwa nini unawatesa wanafunzi wangu?” Badala yake, alimuuliza: “Kwa nini unanitesa?” (Mdo. 9:4) Naam, majaribu yanayowapata wafuasi wake, ni kana kwamba yanampata Yesu mwenyewe.​—Mt. 25:34-40, 45.

      6 Ikiwa unateswa kwa sababu ya kumwamini Kristo, uwe na hakika kwamba Yehova na Yesu wanaelewa hali yako. (Mt. 10:22, 28-31) Kwa sasa, huenda jaribu hilo lisiondolewe. Kumbuka, Stefano alipokuwa akiuawa, na pia wanafunzi waaminifu walipokuwa wakikokotwa kutoka katika nyumba zao huko Yerusalemu, Yesu alikuwa akimtazama Sauli na kuona yote aliyokuwa akifanya. (Mdo. 8:3) Lakini, Yesu hakuingilia kati wakati huo. Badala yake, Yehova, kupitia Kristo, alimpa Stefano na wanafunzi wengine nguvu walizohitaji ili waendelee kuwa waaminifu.

      7. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuvumilia mateso?

      7 Wewe pia unaweza kuvumilia mateso ikiwa utafanya mambo yafuatayo: (1) Azimia kuendelea kuwa mshikamanifu, hata hali iweje. (2) Mwombe Yehova akusaidie. (Flp. 4:6, 7) (3) Mwachie Yehova alipize kisasi. (Rom. 12:17-21) (4) Uwe na uhakika kwamba Yehova atakupatia nguvu za kuvumilia mpaka wakati ambapo yeye mwenyewe ataona inafaa kuliondoa jaribu.​—Flp. 4:12, 13.

      “Sauli, Ndugu, Bwana . . . Amenituma” (Mdo. 9:6-17)

      8, 9. Anania aliuonaje mgawo wake?

      8 Baada ya kujibu swali la Sauli, “Wewe ni nani, Bwana?” Yesu anamwambia: “Inuka uende jijini, nawe utaambiwa unachopaswa kufanya.” (Mdo. 9:6) Kisha, Sauli asiyeweza kuona anaongozwa hadi mahali atakapokaa katika jiji la Damasko, ambapo anafunga na kusali kwa siku tatu. Wakati huohuo, Yesu anamwambia mwanafunzi anayeishi katika mji huo kuhusu Sauli. Mwanafunzi huyo anaitwa Anania, naye ‘alishuhudiwa vema na Wayahudi wote’ walioishi Damasko.​—Mdo. 22:12.

      9 Wazia jinsi Anania alivyochanganyikiwa! Kiongozi wa kutaniko, Yesu Kristo aliyefufuliwa alikuwa akizungumza naye na akampatia mgawo wa pekee. Ni pendeleo kubwa sana ijapokuwa mgawo wenyewe haukuwa rahisi! Alipoambiwa kwamba anapaswa kuzungumza na Sauli, Anania alijibu hivi: “Bwana, nimesikia kutoka kwa watu wengi kuhusu mtu huyu, jinsi alivyowatesa watakatifu wako huko Yerusalemu. Na sasa amepewa mamlaka na wakuu wa makuhani ili awakamate wote wanaoliitia jina lako.”​—Mdo. 9:13, 14.

      10. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyoshughulika na Anania?

      10 Yesu hakumkaripia Anania kwa kutoa maoni yake. Hata hivyo, Yesu alimpa maagizo yaliyo wazi. Naye alionyesha anamjali Anania kwa kumweleza ni kwa nini anataka ashughulikie mgawo huo usio wa kawaida. Yesu alimwambia hivi: “Mtu huyu ni chombo nilichokichagua ili kupeleka jina langu kwa mataifa na pia kwa wafalme na wana wa Israeli. Kwa maana nitamwonyesha waziwazi mateso mengi yatakayompata kwa sababu ya jina langu.” (Mdo. 9:15, 16) Anania hakusita kutii maagizo ya Yesu. Alimtafuta Sauli, aliyekuwa mtesaji, na kumwambia: “Sauli, ndugu, Bwana Yesu aliyekutokea barabarani ulipokuwa ukija, amenituma ili uweze kuona tena na ujazwe roho takatifu.”​—Mdo. 9:17.

      11, 12. Tunajifunza nini kutokana na matukio yaliyowahusisha Yesu, Anania, na Sauli?

      11 Kuna mambo mengi tunayoweza kujifunza kutokana na matukio hayo yaliyowahusisha Yesu, Anania, na Sauli. Kwa mfano, Yesu ndiye anayeongoza kazi ya kuhubiri kama alivyoahidi. (Mt. 28:20) Ingawa hazungumzi moja kwa moja na watu leo, Yesu anaongoza kazi ya kuhubiri kupitia mtumwa mwaminifu, ambaye sasa amewekwa rasmi juu ya watumishi wake. (Mt. 24:45-47) Chini ya mwongozo wa Baraza Linaloongoza, wahubiri na mapainia hutumwa kwenda kuwatafuta wale wanaotaka kujua mengi kumhusu Kristo. Kama ilivyotajwa katika sura ya saba, watu wengi wametembelewa na Mashahidi wa Yehova baada ya kusali wapate mwongozo.​—Mdo. 9:11.

      12 Anania aliukubali mgawo aliopewa naye akapata baraka. Namna gani wewe? Unatii amri ya kutoa ushahidi kikamili, hata ikiwa una mashaka fulani kuhusu mgawo wako? Kwa wengine, kwenda nyumba kwa nyumba na kukutana na watu wasiowafahamu huwatia wasiwasi. Wengine huona ni vigumu kuwahubiria watu katika sehemu za biashara, barabarani, au kupitia simu au barua. Anania aliushinda woga wake naye akapata pendeleo la kumsaidia Sauli kuipokea roho takatifu.b Anania alifanikiwa kwa sababu alimwamini Yesu na kumwona Sauli kama ndugu yake. Kama alivyofanya Anania, sisi pia tunaweza kushinda woga wetu, kwa kutambua kwamba Yesu ndiye anayeongoza kazi ya kuhubiri, kuwajali watu na kuwaona kuwa wanaweza kuwa ndugu zetu hata wale wanaoonekana kuwa wenye kutisha.​—Mt. 9:36.

      “Akaanza Kuhubiri . . . Kuhusu Yesu” (Mdo. 9:18-30)

      13, 14. Ikiwa unajifunza Biblia lakini hujabatizwa, unaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Sauli?

      13 Sauli hakusita kutenda kulingana na mambo aliyojifunza. Baada ya kuponywa, alibatizwa na kuanza kushirikiana kwa ukaribu na wanafunzi huko Damasko. Si hayo tu, “mara moja akaanza kuhubiri katika masinagogi kuhusu Yesu, kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.”​—Mdo. 9:20.

      14 Ikiwa unajifunza Biblia lakini hujabatizwa, je, utakuwa kama Sauli kwa kutenda kulingana na mambo unayojifunza? Ni kweli kwamba muujiza uliofanywa na Kristo, ulimchochea Sauli kutenda. Hata hivyo, wengine walijionea miujiza iliyofanywa na Yesu. Kwa mfano, kikundi kimoja cha Mafarisayo kilishuhudia wakati ambapo Yesu alimponya mtu aliyepooza mkono, na Wayahudi wengi walijua kwamba Yesu alimfufua Lazaro. Lakini, wengi wao hawakuchukua hatua yoyote, na hata wengine walimpinga. (Marko 3:1-6; Yoh. 12:9, 10) Tofauti nao, Sauli alifanya mabadiliko. Kwa nini Sauli alichukua hatua ingawa wengine hawakufanya hivyo? Kwa sababu alimwogopa Mungu kuliko wanadamu naye alithamini sana rehema aliyoonyeshwa na Kristo. (Flp. 3:8) Wewe pia, kama alivyofanya Sauli, usiruhusu chochote kikuzuie kufanya kazi ya kuhubiri au kubatizwa.

      15, 16. Sauli alifanya nini katika masinagogi, na Wayahudi huko Damasko walichukua hatua gani?

      15 Wazia jinsi watu walivyoshangaa na kushtuka huku wengine wakikasirika Sauli alipoanza kuhubiri kumhusu Yesu katika masinagogi. Waliuliza: “Je, huyu si yule mtu aliyewashambulia wale wanaoliitia jina hilo huko Yerusalemu?” (Mdo. 9:21) Alipokuwa akieleza sababu iliyomfanya abadilike, Sauli ‘alithibitisha kupatana na akili kwamba huyu ndiye Kristo.’ (Mdo. 9:22) Hata hivyo, si watu wote wanaoweza kusadikishwa kwa njia hiyo. Kwa mfano, si wote wanaoshikilia desturi au wenye kiburi wanaoweza kusadikishwa kwa kuwathibitishia mambo “kupatana na akili.” Hata hivyo, Sauli hakukata tamaa.

      16 Miaka mitatu baadaye, bado Wayahudi mjini Damasko walikuwa wakimpinga Sauli. Mwishowe, wakapanga kumuua. (Mdo. 9:23; 2 Kor. 11:32, 33; Gal. 1:13-18) Njama yao ilipojulikana, Sauli alitenda kwa busara na kuondoka jijini kwa kushushwa katika kapu kupitia shimo lililokuwa katika ukuta wa jiji. Luka anasema kwamba waliomsaidia Sauli kutoroka usiku huo walikuwa “wanafunzi” wa Sauli. (Mdo. 9:25) Maneno hayo yanaonyesha kwamba watu fulani waliomsikiliza Sauli huko Damasko, walichukua hatua na kuwa wafuasi wa Kristo.

      17. (a) Watu huitikiaje kweli ya Biblia? (b) Tunapaswa kuendelea kufanya nini, na kwa nini?

      17 Ulipoanza kuzungumza na watu wa familia, marafiki, na wengine kuhusu mambo mazuri uliyokuwa unajifunza, huenda ulitazamia kwamba kila mmoja angekubali kweli ya Biblia kwa sababu ni habari inayopatana na akili. Ijapokuwa huenda baadhi yao walikubali, wengi walikataa. Huenda hata watu wa nyumbani kwako mwenyewe walikuona kuwa adui. (Mt. 10:32-38) Hata hivyo, ukiendelea kukuza uwezo wako wa kujadiliana kwa kutumia Maandiko na ukiwa na mwenendo mzuri wa Kikristo, huenda mwishowe hata wale wanaokupinga wakabadili maoni yao.​—Mdo. 17:2; 1 Pet. 2:12; 3:1, 2, 7.

      18, 19. (a) Barnaba alipomtetea Sauli, matokeo yalikuwa nini? (b) Tunawezaje kuwaiga Barnaba na Sauli?

      18 Sauli alipoingia Yerusalemu, inaeleweka ni kwa nini wanafunzi hawakuamini kwamba sasa yeye ni mwanafunzi. Hata hivyo, Barnaba alipomtetea Sauli, mitume walimkubali naye akakaa nao kwa muda. (Mdo. 9:26-28) Ingawa Sauli hakuionea aibu habari njema, nyakati nyingine alilazimika kutenda kwa busara. (Rom. 1:16) Alihubiri kwa ujasiri katika jiji la Yerusalemu, ambapo aliwatesa vikali wanafunzi wa Yesu Kristo. Wakiwa na hofu, Wayahudi katika jiji la Yerusalemu wanatambua kwamba mtu waliyetegemea aangamize Ukristo, amewakimbia, nao wanataka kumuua. “Akina ndugu walipogundua hilo, wakampeleka [Sauli] Kaisaria na kumtuma aende Tarso.” (Mdo. 9:30) Sauli alinyenyekea mwongozo ambao Yesu alitoa kupitia kutaniko. Hivyo, Sauli na kutaniko likanufaika.

      19 Kumbuka kwamba Barnaba hakusita kumtetea Sauli. Bila shaka, tendo hilo la fadhili lilichangia urafiki wa karibu kati ya watumishi hao wa Yehova wenye bidii. Kama alivyofanya Barnaba, je, wewe hujitolea kuwasaidia wapya kutanikoni, kwa kuhubiri pamoja nao na kuwasaidia kufanya maendeleo ya kiroho? Utabarikiwa sana ukifanya hivyo. Ikiwa wewe ni mhubiri mpya wa habari njema, je, unamwiga Sauli kwa kukubali msaada wa wengine? Ukishirikiana na wahubiri wenye uzoefu, utapata ustadi katika kazi ya kuhubiri, shangwe nyingi na marafiki wa kudumu.

      “Wengi Wakamwamini” (Mdo. 9:31-43)

      20, 21. Watumishi wa Mungu, wa zamani na wa sasa, wametumia jinsi gani ‘vipindi vya amani’?

      20 Baada ya Sauli kugeuzwa-imani na kuondoka akiwa salama, “kutaniko katika eneo lote la Yudea, Galilaya, na Samaria likaingia katika kipindi cha amani.” (Mdo. 9:31) Wanafunzi walitumiaje ‘nyakati hizo zinazofaa?’ (2 Tim. 4:2) Maandiko yanasema kwamba walikuwa ‘wakijengwa.’ Mitume na ndugu wengine wenye kutegemeka kutanikoni waliimarisha imani ya wanafunzi na kutoa mwongozo uliohitajika huku kutaniko “likitembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu.” Kwa mfano, Petro alitumia kipindi hicho kuwatia nguvu wanafunzi katika mji wa Lida katika Nchi Tambarare ya Sharoni. Bidii yake iliwafanya wengi waliokuwa wakiishi karibu na mahali hapo ‘wamgeukie Bwana.’ (Mdo. 9:32-35) Mitume hawakukengeushwa na shughuli za kimwili, bali walijitahidi sana kusaidiana na kuhubiri habari njema, nalo kutaniko “likaendelea kuongezeka.”

      21 Kufikia mwisho wa karne ya 20, Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingi waliingia katika “kipindi cha amani.” Serikali zilizokuwa zikiwatesa watu wa Mungu kwa miaka mingi zilitoka mamlakani, na marufuku katika nchi fulani zikapunguzwa au kuondolewa. Makumi ya maelfu ya Mashahidi wa Yehova walitumia nafasi hiyo kuhubiri, nao wakapata matokeo mazuri.

      22. Unaweza kutumia jinsi gani uhuru ulio nao?

      22 Je, unatumia vizuri uhuru ulio nao? Ikiwa unaishi katika nchi iliyo na uhuru wa kidini, huenda Shetani akakushawishi utafute utajiri badala ya kumtumikia Yehova. (Mt. 13:22) Usikengeushwe. Tumia vizuri vipindi vyovyote vya amani ambavyo huenda vipo kwa sasa. Vione kuwa nafasi za kutoa ushahidi kikamili na kujenga kutaniko. Kumbuka kwamba hali zinaweza kubadilika ghafla.

      23, 24. (a) Ni mambo gani tunayojifunza kutokana na masimulizi kumhusu Tabitha? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

      23 Fikiria kilichompata mwanafunzi anayeitwa Tabitha, au Dorkasi. Alikuwa akiishi Yopa, mji uliokuwa karibu na Lida. Dada huyo mwaminifu alitumia wakati na mali zake kwa hekima, “alikuwa akitenda matendo mema na kutoa zawadi za rehema.” Hata hivyo, aliugua na kisha akafa ghafla.c Wanafunzi wa Yopa, hasa wajane ambao alikuwa amewatendea kwa fadhili walihuzunika sana. Petro alipofika katika nyumba ambamo mwili wa Tabitha ulikuwa unatayarishwa kwa ajili ya maziko, alifanya muujiza ambao ulikuwa wa kwanza kufanywa na mitume wa Yesu Kristo. Petro alisali, kisha akamfufua Tabitha! Wazia jinsi wajane na wanafunzi wengine walivyoshangilia Petro alipowaita na kuwakabidhi Tabitha akiwa hai! Tukio hilo liliwaimarisha sana kukabiliana na majaribu yaliyokuwa mbele yao! Muujiza huo ‘ukajulikana kotekote huko Yopa, na wengi wakamwamini Bwana.’​—Mdo. 9:36-42.

      Dada akimpatia maua dada mzee na aliye na ulemavu.

      Unawezaje kumwiga Tabitha?

      24 Tunajifunza mambo mawili muhimu kutokana na masimulizi yenye kutia moyo kumhusu Tabitha. (1) Maisha ni mafupi hivyo ni muhimu tujifanyie jina zuri na Mungu tukiwa hai. (Mhu. 7:1) (2) Tumaini la ufufuo ni hakika. Yehova aliona matendo mengi yenye fadhili aliyofanya Tabitha, naye alimthawabisha. Yehova hatasahau bidii yetu na atatufufua ikiwa tutakufa kabla ya Har–Magedoni. (Ebr. 6:10) Kwa hiyo, iwe tunavumilia “nyakati ngumu” au tunaishi katika “kipindi cha amani,” na tuendelee kutoa ushahidi kamili kumhusu Kristo.​—2 Tim. 4:2.

      Sauli Aliyekuwa Farisayo

      “Kijana aliyeitwa Sauli,” anayetajwa katika kitabu cha Matendo, wakati ambapo Stefano alikuwa akipigwa mawe, alikuwa mwenyeji wa Tarso. Hilo lilikuwa jiji kuu la Kilikia, mkoa wa Roma, ambapo leo ni kusini mwa Uturuki. (Mdo. 7:58) Wayahudi wengi waliishi katika jiji hilo. Sauli mwenyewe alisema hivi: “Nilitahiriwa siku ya nane, mimi ni wa taifa la Israeli, wa kabila la Benjamini, Mwebrania aliyezaliwa kwa Waebrania; kuhusu sheria, Farisayo.” Hiyo ndiyo sababu Paulo alikuwa Myahudi aliyeheshimiwa sana!—Flp. 3:5.

      Sauli aliyekuwa Farisayo.

      Sauli alikuwa akiishi katika jiji kubwa lenye ufanisi wa kibiashara lililojaa utamaduni wa Kigiriki. Kwa kuwa alilelewa Tarso, alijua Kigiriki. Huenda alipata elimu ya msingi katika shule ya Kiyahudi. Alijifunza kazi ya kutengeneza mahema, ambayo ilikuwa ikifanywa na watu wengi wa eneo hilo. Kuna uwezekano mkubwa kwamba akiwa kijana, alifundishwa kazi hiyo na baba yake.​—Mdo. 18:2, 3.

      Masimulizi ya Matendo pia yanaonyesha kwamba Sauli alikuwa raia wa Roma kwa kuzaliwa. (Mdo. 22:25-28) Hilo linamaanisha kwamba mmoja wa babu zake alikuwa raia wa Roma. Haijulikani jinsi familia yao ilivyopata uraia wa Roma. Vyovyote vile, walikuwa watu wenye kuheshimika katika mkoa wao kwa sababu ya uraia wao. Kwa sababu ya malezi na elimu yake, Sauli alielewe vizuri utamaduni wa Wayahudi, Wagiriki, na Waroma.

      Alipokuwa na umri miaka 13 hivi, inaonekana kwamba Sauli alihamia Yerusalemu, kilomita 840, ili kuendeleza masomo yake. Akiwa Yerusalemu, Sauli alijifunza miguuni pa Gamalieli, mwalimu aliyeheshimiwa sana katika utamaduni wa Mafarisayo.​—Mdo. 22:3.

      Masomo hayo ya ziada, yanayoweza kulinganishwa na elimu ya chuo kikuu leo, yalitia ndani kufundishwa na kukariri Maandiko na sheria za Wayahudi zilizopitishwa kwa mdomo. Mwanafunzi aliyefuzu wa Gamalieli angeweza kupata kazi nzuri maishani, na inaonekana Sauli alikuwa na matumaini makubwa maishani. Baadaye aliandika hivi: “Nami nilikuwa nikifanya maendeleo makubwa katika dini ya Kiyahudi kuliko watu wengi wa umri wangu katika taifa langu, kwa maana nilikuwa na bidii zaidi kwa ajili ya mapokeo ya baba zangu.” (Gal. 1:14) Bila shaka bidii ya Sauli kwa ajili ya mapokeo ya Kiyahudi ndiyo iliyomchochea alitese kikatili kutaniko la Kikristo lililokuwa limeanzishwa hivi karibuni.

      TABITHA—“ALIKUWA AKITENDA MATENDO MEMA”

      Tabitha akimpatia zawadi mtu mwenye uhitaji.

      Tabitha alikuwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo lililokuwa katika mji wa Yopa. Waamini wenzake walimpenda sana kwa sababu “alikuwa akitenda matendo mema na kutoa zawadi za rehema.” (Mdo. 9:36) Kama Wayahudi wengi walioishi katika maeneo ambayo yalikuwa na mchanganyiko wa Wayahudi na watu wa mataifa, Tabitha alikuwa na majina mawili, moja la Kiebrania au Kiaramu na lingine la Kigiriki au Kilatini. Jina lake la Kigiriki Dorkasi, ni Tabitha katika Kiaramu. Majina yote mawili yanamaanisha “Swala.”

      Inaonekana Tabitha aliugua na kisha akafa ghafla. Kama ilivyokuwa desturi, mwili wake ulioshwa ili kutayarishwa kwa ajili ya maziko. Huenda uliwekwa katika chumba cha juu cha nyumba yake mwenyewe. Kwa sababu ya joto huko Mashariki ya Kati, mtu akifa angezikwa siku hiyohiyo, au kesho yake. Wakristo jijini Yopa walikuwa wamesikia kwamba Petro yuko Lida, jiji lililokuwa karibu. Kulikuwa na wakati wa kutosha kwa mtume Petro kufika Yopa kabla ya Tabitha kuzikwa, kwa sababu Lida lilikuwa kilomita 18 tu kutoka Yopa, safari ya saa nne hivi kwa miguu. Kwa hiyo, kutaniko likawatuma wanaume wawili wakamsihi Petro aje bila kukawia. (Mdo. 9:37, 38) Msomi mmoja anasema hivi: “Ilikuwa kawaida ya Wayahudi kutuma wajumbe wawili, kwa sababu mmoja angeweza kuthibitisha ujumbe wa mwingine kuwa ni wa kweli.”

      Ni nini kilichotokea Petro alipofika? Masimulizi yanasema: “Wakampeleka kwenye kile chumba cha juu; nao wajane wote wakaja kwake wakilia na kuonyesha mavazi mengi na majoho ambayo Dorkasi alikuwa ametengeneza alipokuwa pamoja nao.” (Mdo. 9:39) Jambo moja lililofanya Tabitha apendwe sana lilikuwa ni mazoea yake ya kuwashonea nguo washiriki wa kutaniko. Alikuwa akitengeneza kanzu, zinazovaliwa kwa ndani, na majoho yanayovaliwa juu ya kanzu hizo. Biblia haisemi ikiwa Tabitha aligharimia vitambaa alivyotumia kushona nguo hizo, au alikuwa akiwashonea watu nguo bure. Vyovyote vile, alipendwa kwa sababu alikuwa mwenye fadhili na alitoa “zawadi za rehema.”

      Mambo aliyojionea Petro katika chumba hicho yalimgusa moyo sana. Msomi Richard Lenski anasema: “Maombolezo haya yalikuwa tofauti kabisa na yale yaliyokuwa katika nyumba ya Yairo, iliyojaa kelele za wapiga filimbi na za wanawake waombolezaji wa kukodiwa. Hayakuwa maombolezo ya kujifanya.” (Mt. 9:23) Yalikuwa maombolezo ya kweli na ya kutoka moyoni. Kwa kuwa hakuna mume anayetajwa, watu wengi huamini kwamba Tabitha alikuwa mseja.

      Yesu alipowatuma mitume wake, aliwapa nguvu za ‘kufufua wafu.’ (Mt. 10:8) Petro alikuwa amemwona Yesu akifanya miujiza kama hiyo, kutia ndani kufufuliwa kwa binti ya Yairo, lakini kabla ya kisa hiki, hakuna mahali popote tunaposoma kuhusu mtume yeyote aliyemfufua mtu. (Marko 5:21-24, 35-43) Petro aliwaomba watu watoke katika chumba cha juu, akasali kwa bidii, naye Tabitha akafungua macho yake na kuketi wima. Wakristo huko Yopa walifurahi sana Petro alipowakabidhi watakatifu na wajane mpendwa wao Tabitha akiwa hai! —Mdo. 9:40-42.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Sauli Aliyekuwa Farisayo,” katika ukurasa wa 62.

      b Kwa kawaida, zawadi za roho takatifu zilipitishwa kupitia mitume. Hata hivyo, katika hali hii isiyo ya kawaida, inaonekana Yesu alimwamuru Anania apitishe zawadi za roho takatifu kwa Sauli. Baada ya kugeuzwa imani, kwa muda fulani, Sauli alikuwa peke yake, mbali na wale mitume wengine 12. Hata hivyo, inaonekana kwamba aliendelea kuwa mtendaji katika kipindi hicho. Inaonekana kwamba Yesu alihakikisha Sauli amepata nguvu zinazohitajika ili kuutimiza mgawo wake wa kuhubiri.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Tabitha—‘Alikuwa Akitenda Matendo Mema,’”.

  • “Mungu Hana Ubaguzi”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 9

      “Mungu Hana Ubaguzi”

      Watu wa Mataifa wasiotahiriwa waanza kuhubiriwa

      Matendo 10:1–11:30

      1-3. Petro aliona nini katika njozi, na kwa nini tunahitaji kuelewa maana yake?

      NI MWAKA wa 36 W.K. Petro anasali kwenye paa ya nyumba iliyo karibu na bahari, katika bandari ya Yopa. Amekuwa akiishi katika nyumba hiyo kwa siku kadhaa sasa. Kwa kiasi fulani, kukaa kwake hapo kunaonyesha kwamba hana ubaguzi. Mwenye nyumba hiyo anayeitwa Simoni ni mtengenezaji wa ngozi. Kwa kweli, si kila Myahudi angekubali kukaa na mtu kama huyo.a Hata hivyo, Petro ataelewa vizuri zaidi maoni ya Yehova kuhusu ubaguzi.

      2 Petro anaposali anaanza kuona njozi. Mambo anayoona katika maono hayo yangeweza kumchukiza Myahudi yeyote. Anaona kitu fulani, kama shuka kubwa, kikishuka kutoka mbinguni kikiwa na wanyama ambao kulingana na Sheria si safi. Anapoambiwa achinje na kula, Petro anajibu hivi: “Sijawahi kula kitu chochote kilicho najisi na kisicho safi.” Mara tatu anaambiwa: “Acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” (Mdo. 10:14-16) Baada ya maono hayo, Petro anachanganyikiwa, ijapokuwa si kwa muda mrefu.

      3 Mambo aliyoona Petro yanamaanisha nini? Maono hayo ni muhimu kwa kuwa yanatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyowaona watu. Tukiwa Wakristo wa kweli, tutaweza kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu ikiwa tutakuwa na maoni kama ya Mungu kuelekea watu. Ili kuelewa maana ya mambo hayo, acheni tuchunguze matukio fulani yaliyotukia karibu na wakati huo.

      “Aliomba Dua Sikuzote kwa Mungu” (Mdo. 10:1-8)

      4, 5. Kornelio ni nani, na ni nini kilichotokea alipokuwa akisali?

      4 Petro hakuwa na habari kwamba siku moja kabla, kilomita 50 hivi upande wa kaskazini huko Kaisaria, mtu anayeitwa Kornelio alikuwa pia amepata maono kutoka kwa Mungu. Kornelio, ofisa katika jeshi la Roma, alikuwa mtu ‘aliyemwogopa Mungu.’b Pia, aliisimamia nyumba yake vizuri kwa sababu alikuwa “mtu aliyemheshimu na kumwogopa Mungu, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake.” Kornelio hakuwa Myahudi mgeuzwa imani; bali alikuwa Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa. Hata hivyo, aliwahurumia Wayahudi wenye uhitaji, na aliwasaidia kimwili. Mtu huyo mnyoofu “aliomba dua sikuzote kwa Mungu.”​—Mdo. 10:2.

      5 Karibu saa 9 hivi mchana, Kornelio alikuwa akisali. Kisha akaanza kuona maono, na katika maono hayo malaika anamwambia: “Mungu amesikia sala zako na kuona zawadi zako za rehema, naye anazikumbuka.” (Mdo. 10:4) Kornelio anatii agizo la malaika na kuwatuma watu wakamwite mtume Petro. Kornelio angekuwa wa kwanza kati ya Watu wa Mataifa wasiotahiriwa kupata pendeleo la pekee. Angepata pendeleo la kusikia ujumbe wa wokovu.

      6, 7. (a) Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha kwamba Mungu anajibu sala za watu wanyoofu ambao wanataka kujua ukweli kumhusu. (b) Tunaweza kusema nini kuhusu mambo kama hayo yaliyoonwa?

      6 Je, Mungu anasikiliza sala za watu wanyoofu wanaotaka kujua ukweli kumhusu? Fikiria jambo hili lililoonwa. Mwanamke mmoja huko Albania alipewa gazeti la Mnara wa Mlinzi linalozungumzia jinsi ya kulea watoto.c Alimwambia hivi Shahidi aliyemtembelea: “Kwa kweli nilikuwa nikisali kwa Mungu ili anisaidie kujua jinsi ya kulea binti zangu! Bila shaka amekutuma! Nimepata ninachohitaji!” Mwanamke huyo na binti zake wakaanza kujifunza, baadaye mume wake pia akaanza kujifunza.

      7 Je, hicho ni kisa cha pekee? Hapana! Mambo kama hayo hutokea sehemu mbalimbali duniani, na yanatokea mara nyingi sana. Tuseme nini? Kwanza, Yehova hujibu sala za watu wanaomtafuta. (1 Fal. 8:41-43; Zab. 65:2) Pili, malaika wanatusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri.​—Ufu. 14:6, 7.

      “Petro Akiwa . . . Anashangaa” (Mdo. 10:9-23a)

      8, 9. Roho ilimjulisha nini Petro, na aliitikiaje?

      8 Watumishi waliotumwa na Kornelio walipofika, Petro alikuwa juu ya paa, “akiwa bado anashangaa” kuhusu maana ya maono hayo. (Mdo. 10:17) Je, Petro, ambaye mara tatu alikataa kula vyakula vilivyokuwa najisi kulingana na Sheria, atakubali kwenda na watu hao na kuingia kwenye nyumba ya Mtu wa Mataifa? Roho takatifu ilifunua kusudi la Mungu katika kisa hicho. Petro aliambiwa hivi: “Tazama! Wanaume watatu wanakutafuta. Basi simama, ushuke na kwenda pamoja nao, usiwe na shaka kamwe, kwa sababu nimewatuma.” (Mdo. 10:19, 20) Bila shaka, maono ambayo Petro aliona yalimtayarisha kutii mwongozo wa roho takatifu.

      9 Baada ya kujua kwamba Mungu alimwelekeza Kornelio awatume watu waje kumchukua, Petro akawakaribisha “na kukaa nao.” (Mdo. 10:23a) Tayari mtume huyo mtiifu ameanza kubadili maoni yake yapatane na mapenzi ya Mungu.

      10. Yehova anawaongozaje watu wake, na ni maswali gani tunayohitaji kujiuliza?

      10 Hadi leo hii, Yehova amekuwa akiwaongoza watu wake hatua kwa hatua. (Met. 4:18) Kupitia roho takatifu, anamwongoza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Mara kwa mara, huenda tukapokea marekebisho fulani katika uelewaji wetu wa Neno la Mungu au mabadiliko fulani katika utaratibu wa tengenezo. Ingefaa kujiuliza: ‘Ninaitikiaje mabadiliko hayo yanapotokea? Ninakubali kwa unyenyekevu mwongozo wa roho ya Mungu katika mambo hayo?’

      Petro “Akawaamuru Wabatizwe” (Mdo. 10:23b-48)

      11, 12. Petro alifanya nini alipofika Kaisaria, na alijifunza jambo gani?

      11 Siku iliyofuata, Petro na wengine tisa—watatu waliotumwa na Kornelio na “ndugu sita” Wayahudi kutoka Yopa—wakafunga safari kuelekea Kaisaria. (Mdo. 11:12) Akiwa anamtarajia Petro, Kornelio aliwakusanya “watu wake wa ukoo na rafiki zake wa karibu”​—inaonekana wote walikuwa Watu wa Mataifa. (Mdo. 10:24) Anapofika, Petro anafanya jambo ambalo awali asingeweza kufanya: Anaingia kwenye nyumba ya Mtu wa Mataifa ambaye hajatahiriwa! Petro anaeleza hivi: “Mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kushirikiana au kumkaribia mtu wa jamii nyingine, lakini Mungu amenionyesha kwamba sipaswi kumwita mtu yeyote najisi au asiye safi.” (Mdo. 10:28) Kufikia sasa, Petro anaelewa kwamba maono aliyopata yalikusudiwa kumfundisha kanuni ambayo haikuhusu tu vyakula ambavyo mtu anaweza kula. Hapaswi “kumwita mtu yeyote [hata wa Mataifa] najisi.”

      Petro na ndugu wengine wakiingia kwenye nyumba ya Kornelio.

      “Bila shaka, Kornelio alikuwa akiwatarajia naye alikuwa amekusanya watu wake wa ukoo na rafiki zake wa karibu.”—Matendo 10:24

      12 Kila mtu aliyekuwapo alitaka kumsikiliza Petro. Kornelio akasema: “Sote tupo mbele za Mungu ili kuyasikia mambo yote ambayo Yehova amekuamuru useme.” (Mdo. 10:33) Hebu wazia jinsi ambavyo ungehisi ikiwa mtu anayependezwa angekuambia hivyo! Petro anaanza kwa kusema hivi kwa usadikisho: “Kwa hakika ninaona kwamba Mungu hana ubaguzi, lakini katika kila taifa mtu anayemwogopa na kutenda uadilifu anakubaliwa naye.” (Mdo. 10:34, 35) Petro alikuwa amejifunza kwamba Mungu haangalii rangi, taifa, au jinsi mtu alivyo kwa nje. Kisha Petro akaendelea kuwahubiria kuhusu huduma, kifo, na ufufuo wa Yesu.

      13, 14. (a) Kugeuzwa imani kwa Kornelio na watu wengine wa Mataifa mwaka wa 36 W.K. kuliashiria nini? (b) Kwa nini hatupaswi kuwahukumu watu kwa jinsi wanavyoonekana?

      13 Sasa jambo fulani lisilo la kawaida latokea: “Petro alipokuwa akizungumza,” roho takatifu ikamiminwa juu ya “watu wa mataifa.” (Mdo. 10:44, 45) Hiki ndicho kisa cha pekee kinachotajwa katika Maandiko cha kumiminwa kwa roho kabla ya ubatizo. Akiwa ametambua hiyo ni ishara kwamba Mungu amewakubali, Petro “akawaamuru [kikundi hicho cha Watu wa Mataifa] wabatizwe.” (Mdo. 10:48) Kugeuzwa kwa Watu hao wa Mataifa mwaka wa 36 W.K. kuliashiria mwisho wa nyakati za kupendelewa kwa Wayahudi. (Dan. 9:24-27) Katika pindi hiyo, Petro aliutumia ufunguo wa tatu na wa mwisho wa Ufalme. (Mt. 16:19) Ufunguo huo ulitoa nafasi kwa Watu wa Mataifa wasiotahiriwa kuwa Wakristo watiwa-mafuta.

      14 Tukiwa watangazaji wa Ufalme leo, tunatambua kwamba “Mungu hana ubaguzi.” (Rom. 2:11) Ni mapenzi yake kwamba “watu wa namna zote waokolewe.” (1 Tim. 2:4) Hivyo, tusiwahukumu watu kwa kutegemea jinsi wanavyoonekana. Jukumu letu ni kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu, na hilo linatia ndani kuwahubiria watu wote, bila kujali rangi, taifa, jinsi wanavyoonekana, au dini zao.

      “Wakaacha Kupinga, Nao Wakamtukuza Mungu” (Mdo. 11:1-18)

      15, 16. Kwa nini baadhi ya Wakristo Wayahudi walimkosoa Petro, naye alitoa sababu gani?

      15 Bila shaka, akiwa na hamu ya kuripoti yaliyotokea, Petro anafunga safari kuelekea Yerusalemu. Habari hizo kwamba Watu wa Mataifa wasiotahiriwa walikuwa “wamelikubali neno la Mungu,” zilikuwa zimefika Yerusalemu. Muda mfupi baada ya Petro kufika, “wale waliounga mkono kutahiriwa wakaanza kumkosoa.” Walichukizwa kwa sababu aliingia ‘ndani ya nyumba ya watu ambao hawajatahiriwa naye akala pamoja nao.’ (Mdo. 11:1-3) Tatizo halikuwa ikiwa Watu wa Mataifa wangeweza kuwa wafuasi wa Kristo au la. Badala yake, wanafunzi hao Wayahudi walisisitiza kwamba Watu wa Mataifa wanapaswa kushika Sheria—kutia ndani sheria ya kutahiriwa—ili waweze kumwabudu Yehova kwa njia inayokubalika. Ni wazi kwamba haikuwa rahisi kwa baadhi ya wanafunzi Wayahudi kuacha kufuata Sheria ya Musa.

      16 Petro alitoa sababu gani? Kulingana na Matendo 11:4-16, alizungumzia mambo manne yanayothibitisha kwamba huo ulikuwa mwongozo kutoka mbinguni: (1) maono aliyopokea kutoka kwa Mungu (Mstari 4-10); (2) amri aliyopewa na roho (Mstari 11, 12); (3) malaika kumtembelea Kornelio (Mstari 13, 14); na (4) Watu wa Mataifa kumiminiwa roho takatifu. (Mstari 15, 16) Petro alimalizia hotuba yake kwa kuuliza swali hili lenye kuchochea: “Kwa hiyo, ikiwa Mungu aliwapa [Watu wa Mataifa walioamini] zawadi ileile ya bure [roho takatifu] kama alivyotupatia sisi [Wayahudi] ambao tumemwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani hata niweze kumzuia Mungu?”​—Mdo. 11:17.

      17, 18. (a) Kwa nini ushahidi wa Petro ulikuwa mtihani mkubwa kwa Wakristo Wayahudi? (b) Kwa nini huenda ikawa vigumu kudumisha umoja kutanikoni, na tunapaswa kujiuliza maswali gani?

      17 Ushahidi huo wa Petro ulikuwa mtihani mkubwa kwa Wakristo Wayahudi. Je, wataondoa ubaguzi wowote walio nao na kuwakubali wanafunzi wapya wa Mataifa wawe Wakristo wenzao? Simulizi hilo linatuambia: “[Mitume na Wakristo wengine Wayahudi] Waliposikia mambo hayo, wakaacha kupinga, nao wakamtukuza Mungu wakisema: ‘Kwa hiyo basi, Mungu pia ameruhusu watu wa mataifa watubu ili wapate uzima.’” (Mdo. 11:18) Maoni hayo mazuri yalidumisha umoja wa kutaniko.

      18 Leo, huenda isiwe rahisi kudumisha umoja, kwa sababu waabudu wa kweli wametoka “mataifa yote na makabila na jamii na lugha.” (Ufu. 7:9) Kwa sababu hiyo, katika makutaniko mengi kuna watu wa rangi, tamaduni na malezi mbalimbali. Tunapaswa kujiuliza: ‘Je, nimeondoa dalili zozote za ubaguzi moyoni mwangu? Je, nimeazimia kutoruhusu mambo yanayowagawanya watu leo—kama vile utaifa, ukabila, utamaduni, na ubaguzi—yaongoze jinsi ninavyowatendea Wakristo wenzangu?’ Kumbuka jinsi Petro (Kefa) alivyotenda miaka kadhaa baada ya Watu wa Mataifa kugeuzwa imani. Ubaguzi wa watu wengine ulifanya ‘ajitenge’ na Wakristo wa Mataifa mengine, naye alirekebishwa na Paulo. (Gal. 2:11-14) Na tuendelee kuwa macho sikuzote ili tusinaswe na mtego huo wa kuwa na ubaguzi.

      “Idadi Kubwa Wakawa Waamini” (Mdo. 11:19-26a)

      19. Wakristo Wayahudi huko Antiokia walianza kuwahubiria nani, nao walipata matokeo gani?

      19 Je, wafuasi wa Yesu walianza kuwahubiria Watu wa Mataifa wasiotahiriwa? Fikiria kilichotokea baadaye huko Antiokia ya Siria.d Jiji hilo lilikuwa na idadi kubwa ya Wayahudi, hata hivyo hakukuwa na uadui mkubwa kati ya Wayahudi na Watu wa Mataifa. Hivyo, haikuwa vigumu kuwahubiria Watu wa Mataifa waliokuwa wakiishi Antiokia. Hapo ndipo baadhi ya wanafunzi Wayahudi walipoanza kuwahubiria habari njema “watu waliozungumza Kigiriki.” (Mdo. 11:20) Waliwahubiria Wayahudi waliozungumza Kigiriki na Watu wa Mataifa wasiotahiriwa. Yehova alibariki kazi hiyo, na “idadi kubwa wakawa waamini.”​—Mdo. 11:21.

      ANTIOKIA YA SIRIA

      Antiokia ya Siria ilikuwa katika eneo la mto Orontes, kilomita 30 hivi kutoka bandari ya Seleukia katika bahari ya Mediterania na karibu kilomita 550 kaskazini mwa Yerusalemu. (Mdo. 13:4) Niketa Seleuko wa Kwanza, mtawala wa kwanza wa Milki ya Seleukia, alianzisha jiji la Antiokia mwaka wa 300 K.W.K. Jiji hilo lililokuwa makao makuu ya milki yake lilipata umaarufu haraka. Mwaka wa 64 K.W.K., Jenerali Mroma Pompey aliifanya Siria kuwa mkoa wa Roma, na Antiokia kuwa makao makuu ya mkoa huo. Kufikia karne ya kwanza W.K., jiji hilo lilikuwa la tatu kwa ukubwa na utajiri katika Milki ya Roma, la kwanza lilikuwa Roma na la pili Aleksandria.

      Antiokia lilikuwa jiji la kibiashara na vilevile kituo cha kisiasa. Bidhaa zote za Siria zilikuwa zikipitia hapo kabla ya kusafirishwa kwenda sehemu nyingine za eneo hilo la Mediterania. Msomi mmoja anasema hivi: “Kwa kuwa [jiji hilo] lilikuwa kati ya eneo la Wagiriki wa Roma na majimbo ya mashariki, lilikuwa la kimataifa zaidi kuliko majiji mengi yaliyofuata tamaduni za Kigiriki.” Kulikuwa na Wayahudi wengi jijini Antiokia, na kulingana na mwanahistoria Myahudi Flavio Yosefo, “waliwageuza imani Wagiriki wengi [waliokuwa wakiishi huko] wafuate desturi za Kiyahudi.”

      20, 21. Barnaba alionyeshaje unyenyekevu, na tunaweza kuonyeshaje unyenyekevu tunapokuwa katika huduma?

      20 Ili kuhakikisha kwamba watu katika eneo la Antiokia wanahubiriwa, kutaniko la Yerusalemu lilimtuma Barnaba aende huko. Bila shaka hangeweza kuwahudumia watu wote wanaopendezwa katika eneo hilo akiwa peke yake. Sauli, ambaye baadaye angekuwa mtume kwa mataifa, alikuwa katika nafasi nzuri zaidi ya kumsaidia. (Mdo. 9:15; Rom. 1:5) Je, Barnaba alianza kushindana na Sauli? Hapana, badala yake, Barnaba alionyesha unyenyekevu. Alienda Tarso kumtafuta Sauli, na kwenda naye Antiokia. Walikaa huko mwaka mzima wakiwaimarisha wanafunzi katika kutaniko hilo.​—Mdo. 11:22-26a.

      21 Tunawezaje kuonyesha unyenyekevu katika huduma yetu? Tukiwa wanyenyekevu tutajua mipaka yetu. Tuna uwezo na vipawa mbalimbali. Kwa mfano, huenda wengine wakawa na ustadi wa kuhubiri isivyo rasmi au nyumba kwa nyumba lakini ikawa vigumu kwao kufanya ziara za kurudia au kuanzisha mafunzo ya Biblia. Kwa nini usiombe msaada ikiwa ungependa kuboresha sehemu fulani ya utumishi wako? Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kupata matokeo mazuri katika huduma na shangwe zaidi.​—1 Kor. 9:26.

      ‘Walituma Msaada’ (Mdo. 11:26b-30)

      22, 23. Ndugu wa Antiokia walionyeshaje upendo wa kindugu, na watu wa Mungu leo wanaigaje mfano wao?

      22 Antiokia ndipo ambapo kwa mara ya kwanza “wanafunzi waliitwa Wakristo kupitia mwongozo wa Mungu.” (Mdo. 11:26b) Jina hilo lililotolewa kwa mwongozo wa Mungu liliwafaa watu hao waliofuata mfano wa Kristo katika maisha yao. Kadiri Watu wa Mataifa walivyokuwa wakijiunga na kutaniko la Kikristo, je, kulikuwa na umoja wa kindugu kati yao na Wayahudi? Fikiria kilichotokea wakati wa njaa kali ya karibu mwaka wa 46 W.K.e Wakati huo, njaa iliwaathiri hasa maskini ambao hawakuwa na akiba ya fedha wala chakula. Wakati huo wa njaa, Wakristo Wayahudi walioishi Yudea, ambao wengi wao walikuwa maskini, walihitaji msaada. Walipojua kwamba kuna uhitaji huo, akina ndugu huko Antiokia—kutia ndani Watu wa Mataifa waliokuwa Wakristo, ‘walituma msaada’ kwa akina ndugu walioishi Yudea. (Mdo. 11:29) Huo ulikuwa upendo wa kindugu!

      23 Ndivyo ilivyo pia miongoni mwa watu wa Mungu leo. Tunaposikia kwamba ndugu zetu—katika nchi nyingine au eneo letu—wana uhitaji fulani, tunajitoa kwa hiari ili kuwasaidia. Halmashauri za Tawi huunda Halmashauri za Kutoa Misaada ili kuwasaidia ndugu ambao wameathiriwa na majanga ya asili, kama vile vimbunga, matetemeko ya nchi, na tsunami. Jitihada hizo zote za kutoa misaada zinaonyesha kwamba tuna undugu wa kweli.​—Yoh. 13:34, 35; 1 Yoh. 3:17.

      24. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunazingatia maana ya maono ambayo Petro aliona?

      24 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunazingatia maana ya maono ambayo Petro aliona akiwa kwenye paa ya nyumba huko Yopa katika karne ya kwanza. Tunamwabudu Mungu asiye na ubaguzi. Mapenzi yake ni kwamba tutoe ushahidi kamili kuhusu Ufalme wake. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwahubiria watu bila kujali rangi, taifa au hali yao. Na tuazimie kuwapa nafasi watu wote wanaotaka kusikiliza habari njema.​—Rom. 10:11-13.

      Ndugu na dada wakirekebisha paa.

      Ndugu zetu wanapokuwa na uhitaji, tunakuwa tayari kuwasaidia

      KORNELIO NA JESHI LA ROMA

      Makao makuu ya jeshi na serikali ya Roma huko Yudea yalikuwa katika jiji la Kaisaria. Jeshi, lililokuwa likisimamiwa na gavana, lilikuwa na askari wapanda-farasi 500 hadi 1,000 na vikosi au vikundi vitano vya askari wa miguu. Kila kikosi kilikuwa na askari 600 hivi. Kwa kawaida askari hawa hawakuwa raia wa Roma. Wengi wao walitumikia huko Kaisaria, na vikundi vichache vilikuwa katika kambi zilizokuwa kotekote Yudea. Nyakati zote kulikuwa na kikosi kimoja katika Mnara wa Antonia huko Yerusalemu ili kulinda Hekalu la Mlimani na jiji. Waroma waliongeza ulinzi katika jiji wakati wa sherehe za Wayahudi ili kukabiliana na vurugu zozote ambazo zingeweza kutokea.

      Kikosi cha askari 100 hivi kilisimamiwa na ofisa wa jeshi. Andiko la Matendo 10:1 linamtaja Kornelio kuwa ofisa wa jeshi wa kikosi cha Italia, ambacho huenda kilikuwa Kaisaria. Huenda kilikuwa kikosi cha Pili cha Italia kilichokuwa na Askari wa Kujitolea waliokuwa Waroma.f Maofisa wa jeshi walikuwa na madaraka makubwa ya kijeshi na ya kijamii, nao walikuwa na mali. Mshahara wao ulikuwa karibu mara 16 zaidi ya ule wa askari wa kawaida.

      f Katika Kilatini waliitwa Cohors II Italica voluntariorum civium Romanorum. Kuna uthibitisho wa kwamba kikosi hicho kilikuwa Siria mwaka wa 69 W.K.

      a Baadhi ya Wayahudi waliwadharau watengenezaji wa ngozi kwa sababu walikuwa wakishika ngozi, mizoga ya wanyama na vitu vingine vyenye kuchukiza katika kazi yao. Watengenezaji wa ngozi walionwa kuwa hawastahili kuingia hekaluni, nao walipaswa kufanyia kazi yao umbali usiopungua mita 22 kutoka mjini. Huenda hiyo ndiyo sababu nyumba ya Simoni ilikuwa “kando ya bahari.”​—Mdo. 10:6.

      b Ona sanduku lenye kichwa “Kornelio na Jeshi la Roma.”

      c Makala yenye kichwa “Mashauri Yenye Kutegemeka Kuhusu Kulea Watoto,” toleo la Novemba 1, 2006, ukurasa wa 4 hadi 7.

      d Ona sanduku lenye kichwa “Antiokia ya Siria.”

      e Mwanahistoria Myahudi Yosefo, aliandika kuhusu “njaa kali” iliyotokea wakati wa utawala wa Maliki Klaudio (41-54 W.K.).

  • “Neno la Yehova Likazidi Kukua”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 10

      “Neno la Yehova Likazidi Kukua”

      Petro aokolewa; habari njema yaenea licha ya mateso

      Matendo 12:1-25

      1-4. Petro anakabili hali gani ngumu, na ungefanya nini ikiwa ungekuwa katika hali hiyo?

      BAADA ya Petro kutiwa gerezani, lango kubwa ya chuma likafungwa kwa kishindo. Akiwa amefungwa minyororo katikati ya walinzi wawili Waroma, mmoja upande huu na mwingine upande ule, anapelekwa na kuingizwa katika chumba cha gereza. Anakaa humo kwa muda mrefu huenda hata kwa siku kadhaa akisubiri kujua kitakachompata. Akiwa huko, hakuna kitu kingine alichoona zaidi ya minyororo aliyofungwa, kuta, nondo za chumba cha gereza, na walinzi walio kando yake.

      2 Hukumu inayotolewa ni kali sana. Mfalme Herode Agripa wa Kwanza aliazimia kumuua Petro.a Alipanga kumleta Petro mbele ya watu baada ya Pasaka, na kumhukumu adhabu ya kifo ili kuwafurahisha. Hicho si kitisho tu kwa kuwa muda mfupi uliopita, mtawala huyo alikuwa amemuua mtume Yakobo.

      3 Ni usiku wa kuamkia siku ambayo angeuawa. Petro anafikiria nini akiwa gerezani? Je, inawezekana anakumbuka miaka kadhaa iliyopita, wakati ambapo Yesu alitabiri kwamba siku moja Petro angefungwa na kupelekwa asikotaka, yaani, angeuawa? (Yoh. 21:18, 19) Huenda Petro anafikiri kwamba wakati huo umefika.

      4 Kama ungekuwa Petro, ungefanya nini? Wengi wangekata tamaa wakifikiri kwamba hakuna tumaini lolote. Hata hivyo, je, kuna hali yoyote inayoweza kuwafanya wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo wakose kuwa na tumaini? Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Petro na Wakristo wenzake walivyotenda walipoteswa? Acheni tuone.

      “Kutaniko Lilikuwa Likisali kwa Mungu kwa Bidii Sana” (Mdo. 12:1-5)

      5, 6. (a) Mfalme Herode Agripa wa Kwanza alilishambulia kutaniko la Kikristo jinsi gani na kwa nini? (b) Kwa nini kifo cha Yakobo kilikuwa pigo kubwa kwa kutaniko?

      5 Kama tulivyojifunza katika sura ya tisa ya kitabu hiki, kutaniko la Kikristo lilifurahia sana kugeuzwa imani kwa Kornelio na familia yake. Lakini lazima Wayahudi wasiokuwa waamini walishangaa sana kuona Wakristo wengi Wayahudi wakiabudu pamoja na watu wasio Wayahudi.

      6 Herode, mwanasiasa mwenye hila, aliona hiyo kuwa nafasi nzuri ya kujitafutia sifa miongoni mwa Wayahudi, naye akaanza kuwatesa Wakristo. Bila shaka alikuwa amesikia kwamba mtume Yakobo alikuwa rafiki wa karibu wa Yesu Kristo. Kwa hiyo, Herode “alimuua kwa upanga Yakobo ndugu ya Yohana.” (Mdo. 12:2) Hilo lilikuwa pigo kubwa sana kwa kutaniko! Yakobo alikuwa mmoja kati ya mitume watatu walioshuhudia sura ya Yesu ilipogeuka na alijionea miujiza mingine ambayo wale mitume wengine hawakuiona. (Mt. 17:1, 2; Marko 5:37-42) Yesu alimwita Yakobo na ndugu yake Yohana, “Wana wa Ngurumo” kwa sababu ya bidii yao. (Marko 3:17) Kwa hiyo Yakobo alipouawa, kutaniko lilipoteza shahidi mwaminifu, mwenye ujasiri, na mtume mpendwa.

      7, 8. Kutaniko lilifanya nini Petro alipokuwa gerezani?

      7 Kama Agripa alivyotazamia, kuuawa kwa Yakobo kuliwafurahisha Wayahudi. Hivyo, akapata ujasiri wa kupanga njama ya kumwua Petro. Kama inavyosimuliwa mwanzoni mwa sura hii, aliagiza Petro akamatwe. Hata hivyo, kama tulivyoona katika Sura ya 5 ya kitabu hiki, huenda Agripa alikumbuka kutokana na matukio ya wakati uliopita kwamba magereza hayangeweza kuwazuia mitume. Ili kuhakikisha kwamba hatoroki, Herode anaagiza Petro afungwe minyororo katikati ya walinzi 2 na kuagiza walinzi wengine 16 wamlinde kwa zamu usiku na mchana. Akitoroka, walinzi hao watapata adhabu kali. Katika hali hizo, Wakristo wenzake wangefanya nini?

      8 Kutaniko lilijua jambo la kufanya. Andiko la Matendo 12:5 linasema: “Petro alikuwa gerezani lakini kutaniko lilikuwa likisali kwa Mungu kwa bidii sana kwa ajili yake.” Walisali kwa bidii na kutoka moyoni kwa ajili ya ndugu yao mpendwa. Kifo cha Yakobo hakikuwavunja moyo wala kuwafanya wapuuze sala. Yehova anathamini sana sala za watumishi wake naye huzijibu ikiwa zinapatana na mapenzi yake. (Ebr. 13:18, 19; Yak. 5:16) Wakristo leo wanapaswa kukumbuka hilo.

      9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano uliowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza kuhusu sala?

      9 Je, unajua waabudu wenzako wanaokabili majaribu? Huenda wanavumilia mateso, wamepigwa marufuku na serikali, au wamepatwa na majanga ya asili. Unaweza kuwakumbuka katika sala zako. Labda unawajua wengine wanaokabili hali ngumu kama vile matatizo ya familia, kuvunjika moyo, au mambo yanayojaribu imani yao. Ukitafakari kabla ya kusali, unaweza kukumbuka ndugu na dada ambao utawataja unaposali kwa Yehova, “Msikiaji wa sala.” (Zab. 65:2) Bila shaka wewe pia ungependa ndugu na dada zako wafanye hivyo unapokabili hali ngumu.

      Ndugu alifungwa pingu akipelekwa gerezani na askari.

      Tunasali kwa ajili ya ndugu zetu walio gerezani kwa sababu ya imani yao

      “Uendelee Kunifuata” (Mdo. 12:6-11)

      10, 11. Eleza jinsi malaika wa Yehova alivyomtoa Petro gerezani.

      10 Je, Petro alikuwa na wasiwasi? Hatujui. Hata hivyo, usiku wa mwisho akiwa gerezani, alikuwa amelala usingizi mzito huku akilindwa na walinzi wawili. Bila shaka mwanamume huyo mwenye imani alijua kwamba hata nini kitokee, yuko salama mikononi mwa Yehova. (Rom. 14:7, 8) Vyovyote vile, Petro hakutazamia kamwe mambo yaliyotokea muda mfupi baadaye. Ghafla, nuru ikang’aa katika chumba cha gereza. Malaika akasimama kwenye chumba hicho bila kuonekana na walinzi na kumwamsha Petro. Minyororo aliyofungwa—iliyoonekana haiwezi kukatika—ikaanguka!

      Petro akimfuata malaika wanawapita walinzi kwenye lango la chuma linaloelekea jijini.

      “Wakafika kwenye lango la chuma linaloelekea jijini, nalo likafunguka lenyewe mbele yao.”—Matendo 12:10

      11 Malaika huyo aanza kumhimiza Petro: “Simama upesi! . . . Vaa nguo na uvae viatu vyako . . . Vaa vazi lako la nje.” Petro akafanya hivyo bila kusita. Mwishowe malaika akamwambia: “Uendelee kunifuata,” naye Petro akafanya hivyo. Wakatoka katika chumba hicho, wakawapita walinzi waliokuwa nje kimyakimya hadi kwenye lango kubwa la chuma. Watapitaje? Ikiwa Petro alijiuliza swali hilo, alipata jibu mara moja. Walipokaribia, lango likafunguka “lenyewe.” Ghafla, wakatoka nje na kuingia barabarani, kisha malaika akamwacha. Baada ya Petro kuachwa, alitambua kwamba jambo hilo halikuwa ndoto wala maono, bali alikuwa huru.​—Mdo. 12:7-11.

      12. Kwa nini tunaweza kufarijika tunapotafakari jinsi Yehova alivyomkomboa Petro?

      12 Bila shaka tunafarijika sana tunapotafakari nguvu za Yehova zisizo na mipaka za kuwakomboa watumishi wake. Petro alifungwa na mfalme wa serikali iliyokuwa na nguvu zaidi katika ulimwengu wa wakati huo. Hata hivyo, Petro aliokolewa kutoka gerezani. Ni kweli kwamba Yehova hafanyi miujiza kama hiyo kwa watumishi wake wote. Hakufanya hivyo kwa Yakobo, wala baadaye wakati unabii wa Yesu kumhusu mtume Petro ulipotimia. Leo, Wakristo hawatazamii kukombolewa kimuujiza. Hata hivyo, tunajua kwamba Yehova hajabadilika. (Mal. 3:6) Hivi karibuni, atamtumia Mwana wake kuwaweka huru mamilioni ya watu kutoka katika gereza kuu zaidi, yaani, kifo. (Yoh. 5:28, 29) Ahadi kama hizo zinaweza kututia moyo tunapokabili majaribu.

      “Wakamwona Nao Wakashangaa” (Mdo. 12:12-17)

      13-15. (a) Washiriki wa kutaniko waliokutanika katika nyumba ya Maria walitendaje Petro alipofika? (b) Kitabu cha Matendo kinaanza kuzungumzia nini, na Petro aliendelea kuwasaidiaje ndugu na dada zake wa kiroho?

      13 Petro alisimama barabarani usiku huku akifikiria aende wapi. Kisha akaamua. Maria, mwanamke Mkristo alikuwa akiishi karibu na eneo hilo. Huenda alikuwa mjane mwenye mali na nyumba kubwa ambayo ingeweza kutumiwa na kutaniko. Maria alikuwa mama ya Yohana Marko, anayetajwa hapa kwa mara ya kwanza katika kitabu cha Matendo na ambaye baadaye Petro alimwita mwanangu. (1 Pet. 5:13) Usiku huo, washiriki wengi wa kutaniko walikuwa nyumbani kwa Maria wakisali kwa bidii, ingawa ilikuwa usiku sana. Walikuwa wakisali ili Petro afunguliwe, hata hivyo hawakutazamia kwamba Yehova angejibu sala yao mara moja!

      14 Petro anapiga hodi kwenye lango la kuingia kwenye ua wa nyumba hiyo. Kijakazi anayeitwa Roda—jina la Kigiriki ambalo humaanisha “Waridi”​—akaenda kumfungulia. Haamini anachosikia. Alisikia sauti ya Petro. Badala ya kufungua lango, msichana huyo mwenye shangwe anarudi haraka ndani ya nyumba na kuwaambia washiriki wa kutaniko kwamba Petro amekuja. Wanasema amerukwa na akili, lakini anaendelea kusisitiza. Haachi kusema ukweli. Wakiwa hawamwamini, baadhi yao wanasema huenda ni malaika anayemwakilisha Petro. (Mdo. 12:12-15) Wakati huo wote, Petro anaendelea kupiga hodi, na mwishowe wanaenda langoni na kumfungulia.

      15 Walipofungua mlango, “wakamwona nao wakashangaa”! (Mdo. 12:16) Petro analazimika kuwanyamazisha ili awaeleze yaliyokuwa yametokea. Kisha anawaagiza wamwambie Yakobo na akina ndugu, naye anaondoka kabla hajakamatwa na askari wa Herode. Halafu anaenda eneo lingine lililo salama na kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Petro anatajwa kwenye sura ya 15 wakati suala la tohara lilipokuwa likizungumziwa, na baada ya hapo hatajwi tena katika kitabu cha Matendo. Sasa kitabu hicho kinazungumzia kazi na safari za mtume Paulo. Hata hivyo, tuna uhakika kwamba popote alipoenda, Petro aliimarisha imani ya ndugu na dada. Alipoondoka, alikiacha kikundi kilichokuwa katika nyumba ya Maria kikiwa na furaha.

      16. Kwa nini tunaweza kutazamia kufurahia mambo mengi wakati ujao?

      16 Nyakati nyingine Yehova hujibu sala za watumishi wake kuliko walivyotarajia, nao huwa na shangwe nyingi sana. Hivyo ndivyo ndugu na dada walivyohisi usiku huo, Petro alipoachiliwa. Sisi pia, huenda tukahisi hivyo tunapopata baraka nyingi za Yehova. (Met. 10:22) Wakati ujao, tutaona ahadi zote za Yehova zikitimizwa duniani pote. Ahadi hizo zitatimizwa kwa kiwango kikubwa kuliko tunavyowazia. Kwa hiyo, tukiendelea kuwa waaminifu, tunaweza kutazamia kufurahia mambo mengi wakati ujao.

      “Malaika wa Yehova Akampiga” (Mdo. 12:18-25)

      17, 18. Kwa nini umati ulianza kumsifu Herode?

      17 Herode alishangaa sana kwamba Petro alitoka gerezani lakini hakufurahishwa na jambo hilo. Mara moja akaamuru Petro atafutwe na walinzi waliokuwa wakimlinda wahojiwe. ‘Wakapelekwa kuadhibiwa.’ Huenda waliuawa. (Mdo. 12:19) Herode Agripa hakuwa na huruma wala rehema. Je, mtu huyo mkatili alipata adhabu anayostahili?

      18 Huenda Agripa aliaibika kwa sababu hakufaulu kumuua Petro, hata hivyo, baada ya muda mfupi alipata nafasi nyingine ya kujitukuza. Kulikuwa na mkutano na adui zake ambao walitaka kufanya amani. Bila shaka alikuwa na hamu ya kutoa hotuba mbele ya umati huo. Luka anasema kwamba “Herode alivaa mavazi ya kifalme” ili kujitayarisha kwa ajili ya mkutano huo. Yosefo, mwanahistoria Myahudi aliandika kwamba vazi la Herode lilikuwa la fedha, naye mfalme alipopigwa na jua, vazi hilo lilionekana liking’aa kwa utukufu. Kisha mwanasiasa huyo mwenye kiburi akatoa hotuba. Umati uliokuwa ukimsifu ukapaaza sauti na kusema: “Hii ni sauti ya mungu, si ya mwanadamu!”​—Mdo. 12:20-22.

      19, 20. (a) Kwa nini Yehova alimwadhibu Herode? (b) Kwa nini tunaweza kupata faraja kutokana na kilichompata Herode Agripa?

      19 Mungu tu ndiye anayestahili utukufu huo, naye alikuwa akitazama! Herode angeweza kuepuka msiba. Angeweza kuukemea umati huo au kukataa sifa hizo. Badala yake, alionyesha waziwazi ukweli wa methali hii: “Kiburi hutangulia kuanguka kwa kishindo.” (Met. 16:18) “Papo hapo malaika wa Yehova akampiga,” na kusababisha mtu huyo mbinafsi na mwenye kiburi afe kifo chenye maumivu. Herode “akaliwa na wadudu akafa.” (Mdo. 12:23) Yosefo anasema kuwa Agripa alishambuliwa ghafla, na mfalme huyo alitambua kwamba anakufa kwa sababu ya kukubali kusifiwa na umati. Kulingana na Yosefo, Agripa aliendelea kuteseka katika hali hiyo kwa siku tano kabla ya kufa.b

      20 Wakati mwingine huenda ikaonekana kwamba watu wasiomwogopa Mungu wanaendelea kufanya uovu bila kuadhibiwa. Hilo halipaswi kutushangaza, kwa kuwa “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Hata hivyo, watumishi waaminifu wa Mungu huumia sana wanapowaona waovu wakiendelea kufanya uovu bila kuadhibiwa. Ndiyo sababu masimulizi kama haya yanawafariji sana. Ni kana kwamba tunamwona Yehova akiingilia kati, na kuwakumbusha watumishi wake wote kwamba anapenda haki. (Zab. 33:5) Hivi karibuni, Yehova ataleta haki duniani pote.

      21. Matendo sura ya 12 inahusu nini hasa, na kwa nini kujua jambo hilo kunatufariji?

      21 Masimulizi hayo yanamalizia kwa kitia moyo hiki: “Neno la Yehova likazidi kukua na kuenea.” (Mdo. 12:24) Ripoti hiyo kuhusu kuenea kwa kazi ya kuhubiri inatukumbusha jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi yetu ya kuhubiri. Habari zilizo katika Matendo sura ya 12 si masimulizi tu ya kifo cha mtume mmoja na kuokolewa kwa mwingine. Masimulizi hayo pia yanahusu jinsi Yehova anavyovunja mipango ya Shetani ya kujaribu kuangamiza kutaniko la Kikristo na kukomesha kazi ya kuhubiri. Mashambulizi yote ya Shetani hayakufanikiwa kama tu ambavyo hila zake zote hazitafanikiwa. (Isa. 54:17) Hata hivyo, wale walio upande wa Yehova na Yesu Kristo hawatashindwa kamwe. Jambo hilo linatia moyo sana. Leo, tuna pendeleo kubwa la kueneza “neno la Yehova.”

      MFALME HERODE AGRIPA WA KWANZA

      Herode Agripa wa Kwanza, aliyeagiza Yakobo auawe na Petro afungwe, alikuwa mjukuu wa Herode Mkuu. Herode walitokana na familia ya watawala wa Kiyahudi. Familia hiyo ilikuwa ya Waidumea, yaani, Waedomu. Waidumea walionwa kuwa Wayahudi kwa kuwa katika mwaka wa 125 K.W.K., walilazimishwa kutahiriwa.

      Herode Agripa wa Kwanza alizaliwa mwaka wa 10 K.W.K. na alisomea Roma. Alifanya urafiki na washiriki mbalimbali wa familia ya kifalme. Mmoja wao ni Gayo, aliyejulikana na watu wengi kwa jina la Kaligula, na alikuwa maliki mwaka wa 37 K.W.K. Muda mfupi baadaye akamtawaza Agripa kuwa mfalme wa Iturea, Trakoniti, na Abilene. Baadaye, Kaligula akapanua eneo la utawala wa Agripa litie ndani Galilaya na Perea.

      Agripa alikuwa katika jiji la Roma Kaligula alipouawa mwaka wa 41 W.K. Inasemekana kwamba Agripa alichangia sana kutatua mzozo uliozuka. Pia, alishiriki katika majadiliano mengine makali kati ya Klaudio, rafiki yake mwenye mamlaka, na Bunge la Roma. Hatimaye Klaudio akatawazwa kuwa maliki na vita vya wenyewe kwa wenyewe vikaepukwa. Ili kumshukuru kwa kutatua mzozo huo, Klaudio alimtawaza Agripa kuwa mtawala wa Yudea na Samaria, majimbo yaliyokuwa yakitawaliwa na maliwali wa Roma tangu mwaka wa 6 W.K. Kwa njia hiyo, Agripa akawa mtawala wa maeneo mengi sawa na Herode Mkuu.

      Yerusalemu lilikuwa jiji kuu la eneo alilotawala Agripa, naye alifanya urafiki na viongozi wa dini ya Kiyahudi. Inasemekana kwamba alishika kabisa sheria na desturi za Kiyahudi, kutia ndani mambo kama vile kutoa dhabihu hekaluni kila siku, kusoma Sheria hadharani, na kutekeleza jukumu la kuwa “mteteaji mwenye bidii wa imani ya Kiyahudi.” Hata hivyo, dai lake la kuwa mwabudu wa Mungu lilikuwa la uwongo kwa sababu alikuwa akiandaa mapigano na matamasha ya kipagani katika majumba ya maonyesho. Wengine husema kwamba Agripa alikuwa mtu “mwenye hila, mnafiki, na fisadi.”

      a Ona sanduku lenye kichwa “Mfalme Herode Agripa wa Kwanza.”

      b Daktari mmoja ambaye pia ni mwandishi wa vitabu, aliandika kwamba huenda ugonjwa ambao Yosefo na Luka wanataja ulisababishwa na minyoo iliyoziba utumbo. Nyakati nyingine mtu mwenye ugonjwa huo hutapika minyoo au, anapokaribia kufa, minyoo hiyo hutoka. Kitabu kimoja kinasema: “Maneno hususa ya kidaktari anayotumia Luka yanafafanua vizuri kifo chenye maumivu kilichompata [Herode].”

  • “Kujawa na Shangwe na Roho Takatifu”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 11

      “Kujawa na Shangwe na Roho Takatifu”

      Paulo anatuwekea mfano mzuri wa kushughulika na watu wakali, wasiotaka kusikiliza

      Matendo 13:1-52

      1, 2. Safari ya Barnaba na Sauli ina tofauti gani na zile safari nyingine za umishonari, na safari hiyo itasaidiaje kutimiza andiko la Matendo 1:8?

      NI SIKU ya shangwe sana katika kutaniko la Antiokia. Kati ya manabii na walimu wote, Barnaba na Sauli ndio waliochaguliwa na roho takatifu kwenda kutangaza habari njema katika sehemu za mbali.a (Mdo. 13:1, 2) Ni kweli kwamba wanaume wanaostahili walitumwa wakati uliopita. Hata hivyo, wakati huo wamishonari hao walienda maeneo ambayo Ukristo ulikuwa umetia mizizi. (Mdo. 8:14; 11:22) Sasa, Barnaba na Sauli—pamoja na Yohana Marko, atakayewahudumia—wanatumwa nchi ambazo watu wengi hawajasikia kamwe habari njema.

      2 Miaka 14 hivi iliyopita, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kuwekwa rasmi kwa Barnaba na Sauli kuwa wamishonari kutachangia sana kutimizwa kwa unabii huo wa Yesu!b

      ‘Wawekeni kando kwa Ajili ya Kazi’ (Mdo. 13:1-12)

      3. Kwa nini haikuwa rahisi kusafiri katika karne ya kwanza?

      3 Kuna maendeleo mengi sana katika ulimwengu wa leo. Kwa muda wa saa moja au mbili, watu wanaweza kusafiri mbali sana kwa kutumia magari na ndege. Hali hii ni tofauti na ile ya karne ya kwanza W.K. Siku hizo, watu walitembea kwa miguu katika barabara mbaya. Kwa siku nzima mtu angeweza kusafiri kilomita 30 hivi, na safari hiyo ilikuwa yenye kuchosha sana.c Ingawa Barnaba na Sauli walitazamia kwa hamu kwenda kwenye mgawo wao, bila shaka walijua kwamba watalazimika kufanya jitihada nyingi na kujinyima mengi.​—Mt. 16:24.

      SAFARI KATIKA SIKU ZA MITUME

      Zamani, kusafiri kwa kutumia barabara kulichukua muda mrefu, kulichosha, na kugharimu pesa nyingi kuliko kusafiri kwa mashua. Hata hivyo, ili kufika sehemu nyingi, njia pekee ilikuwa kutembea kwa miguu.

      Msafiri angeweza kutembea kilomita 30 hivi kwa siku. Angekumbana na hali ngumu kama vile jua kali, mvua, baridi, au kushambuliwa na wezi. Mtume Paulo alisema kwamba aliposafiri, ‘mara nyingi alikabili hatari za kutokana na mito, hatari za kutokana na wezi.’​—2 Kor. 11:26.

      Milki ya Roma ilikuwa na barabara nyingi nzuri za mawe. Kando ya barabara kuu, kulikuwa na nyumba za wageni kila baada ya umbali wa safari ya siku moja hivi kwa miguu. Karibu nusu ya safari, kulikuwa na hoteli ambazo mtu angeweza kupata chakula au mahitaji mengine ya msingi. Waandishi wa enzi hizo walitaja kwamba hoteli na nyumba hizo za wageni zilikuwa chafu, zilijaa watu, viroboto na zilikuwa na joto sana. Hazikuheshimika na zilipendwa na watu wanaotenda mambo mabaya. Mara nyingi, wahudumu wa sehemu hizo waliwaibia wasafiri na walitoa huduma za ukahaba.

      Bila shaka Wakristo waliepuka sehemu hizo kadiri walivyoweza. Hata hivyo, waliposafiri kwenda sehemu ambazo hawakuwa na watu wa ukoo au marafiki, walilazimika kukaa humo.

      4. (a) Barnaba na Sauli walichaguliwaje, na waabudu wenzao waliitikiaje? (b) Tunawezaje kuwaunga mkono wale wanaopewa mapendeleo ya kitheokrasi?

      4 Lakini, kwa nini roho takatifu iliagiza moja kwa moja Barnaba na Sauli wawekwe kando ‘kwa ajili ya kazi’? (Mdo. 13:2) Biblia haisemi. Hata hivyo, tunajua kwamba roho takatifu ilielekeza wanaume hao wachaguliwe. Hatusomi popote kwamba manabii na walimu huko Antiokia walipinga uamuzi huo bali waliunga mkono kabisa uamuzi huo. Wazia jinsi Barnaba na Sauli walivyohisi wakati ndugu zao wa kiroho bila wivu wowote ‘walipofunga na kusali na kuweka mikono juu yao, na kuwaacha waende.’ (Mdo. 13:3) Sisi pia, tunapaswa kuwaunga mkono wale wanaopata mapendeleo ya kitheokrasi, kutia ndani wanaume wanaowekwa rasmi kuwa waangalizi katika kutaniko. Badala ya kuwaonea wivu, tunapaswa ‘kuwafikiria kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao.’​—1 The. 5:13.

      5. Eleza jinsi kisiwa cha Kipro kilivyohubiriwa.

      5 Baada ya kutembea hadi Seleukia, bandari iliyokuwa karibu na Antiokia, Barnaba na Sauli walisafiri kwa mashua hadi kisiwa cha Kipro, umbali wa kilomita 200 hivi.d Kwa kuwa alikuwa mzaliwa wa Kipro, bila shaka Barnaba alikuwa na hamu kubwa ya kutangaza habari njema katika eneo la nyumbani kwao. Walipofika Salami, jiji lililokuwa kwenye ufuo wa mashariki wa kisiwa hicho, wanaume hao hawakupoteza wakati wowote. Mara moja, “wakaanza kulitangaza neno la Mungu katika masinagogi ya Wayahudi.”e (Mdo. 13:5) Barnaba na Sauli walisafiri kutoka upande mmoja hadi upande wa pili wa Kipro, wakihubiri katika majiji makubwa yaliyokuwa njiani. Ikitegemea barabara waliyopitia, huenda wamishonari hao walitembea kilomita 160 hivi!

      MASINAGOGI YA WAYAHUDI

      Neno “sinagogi” linamaanisha “kukusanya pamoja.” Mwanzoni, neno hilo lilimaanisha kusanyiko au kutaniko la Wayahudi na baadaye likapata maana mpya yaani mahali au jengo lililotumiwa kwa ajili ya kusanyiko hilo.

      Inaaminika kwamba masinagogi yalianza kutumiwa wakati wa ile miaka 70 Wayahudi walipokuwa uhamishoni Babiloni au muda mfupi baada ya kutoka huko. Masinagogi yalikuwa mahali pa kutoa elimu, kuabudu, kusoma na kufafanua Maandiko, na kuchochea watu kiroho. Katika karne ya kwanza W.K., kila mji katika maeneo ya Palestina ulikuwa na sinagogi. Majiji makubwa, kama Yerusalemu, yalikuwa na masinagogi kadhaa.

      Hata hivyo, si Wayahudi wote waliorudi Palestina baada ya uhamisho wa Babiloni. Wengi walihamia nchi nyingine ili kufanya biashara. Kufikia karne ya tano hivi K.W.K., Wayahudi walikuwa wakiishi katika wilaya zote 127 za Milki ya Uajemi. (Esta 1:1; 3:8) Baada ya muda, wakaanza kuishi katika majiji yaliyozunguka Bahari ya Mediterania. Wayahudi hao walioishi katika maeneo hayo wakaanza kujenga masinagogi.

      Katika masinagogi, Sheria ilisomwa na kufafanuliwa kila Sabato. Kulikuwa na jukwaa la kusomea lililozungukwa na viti katika pande tatu. Mwanamume yeyote Myahudi aliyekuwa mwamini angeweza kusoma, kuhubiri, au kuwahimiza wengine katika sinagogi.

      6, 7. (a) Sergio Paulo ni nani, na kwa nini Bar-Yesu alijaribu kumzuia asisikilize habari njema? (b) Sauli alishughulikiaje upinzani wa Bar-Yesu?

      6 Katika karne ya kwanza, ibada ya uwongo ilikuwa imeenea sana Kipro. Hilo lilionekana wazi Barnaba na Sauli walipofika Pafo, kwenye ufuo wa magharibi wa kisiwa hicho. Huko walikutana “na mwanamume Myahudi aliyeitwa Bar-Yesu, ambaye alikuwa mlozi na nabii wa uwongo, [naye] alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mwanamume mwenye akili.”f Katika karne ya kwanza, Waroma wengi wenye kuheshimika—hata ‘wanaume wenye akili,’ kama Sergio Paulo—waliwaendea walozi au wanajimu kutafuta msaada wa kufanya maamuzi mazito. Hata hivyo, Sergio Paulo alivutiwa sana na ujumbe wa Ufalme naye “alitamani kulisikia neno la Mungu.” Hilo halikumpendeza Bar-Yesu, ambaye jina lake la cheo lilikuwa Elima, yaani, “Mlozi.”​—Mdo. 13:6-8.

      7 Bar-Yesu aliupinga ujumbe wa Ufalme. Njia pekee ambayo angeweza kutumia ili kudumisha cheo chake kikubwa akiwa mshauri wa Sergio Paulo ilikuwa ni kwa “kumzuia yule liwali asiwe mwamini.” (Mdo. 13:8) Hata hivyo, Sauli hakumruhusu mlozi huyo amkengeushe Sergio Paulo. Alifanya nini? Masimulizi yanasema: “Sauli, aitwaye pia Paulo, akiwa amejaa roho takatifu, akamtazama kwa makini [Bar-Yesu] na kumwambia: “Ewe mtu uliyejaa kila aina ya upunjaji na kila aina ya ulaghai, wewe mwana wa Ibilisi, wewe adui wa kila jambo la uadilifu, je, hutaacha kuzipotosha njia za Yehova zilizo sawa? Tazama! mkono wa Yehova uko juu yako, nawe utakuwa kipofu, hutaona nuru ya jua kwa kipindi fulani.” Mara moja akaangukiwa na ukungu mzito na giza, naye akazunguka akitafuta mtu wa kumshika mkono ili amwongoze.”g Matokeo? “Yule liwali alipoona jambo lililotokea, akawa mwamini kwa sababu alistaajabishwa na fundisho la Yehova.”​—Mdo. 13:9-12.

      Ndugu ameshika Biblia iliyofunguliwa, akitetea kweli mbele ya hakimu mahakamani.

      Kama Paulo, tunaitetea kweli kwa ujasiri hata tukikabili upinzani

      8. Tunawezaje kuiga ujasiri wa Paulo?

      8 Paulo hakumwogopa Bar-Yesu. Vivyo hivyo, hatupaswi kuogopa wapinzani wanapojaribu kuvuruga imani ya wale wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme. Ni kweli kwamba maneno yetu yanapaswa kuwa “yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi.” (Kol. 4:6) Hata hivyo, hatuwezi kuacha hali ya kiroho ya mtu anayependezwa iwe hatarini kwa sababu tu tunataka kuepuka ubishi. Wala hatupaswi kuogopa kufichua dini za uwongo kama za Bar-Yesu, ambazo zinaendelea ‘kupotosha njia za Yehova zilizo sawa.’ (Mdo. 13:10) Kama Paulo, na tuendelee kutangaza kweli kwa ujasiri na kuichochea mioyo ya watu wanyoofu. Ingawa huenda tusione waziwazi utegemezo wa Mungu, kama ilivyokuwa katika kisa cha Paulo, tuna uhakika kwamba Yehova atatumia roho yake takatifu kuwavuta watu wanaostahili kwenye ile kweli.​—Yoh. 6:44.

      ‘Neno la Kitia Moyo’ (Mdo. 13:13-43)

      9. Paulo na Barnaba waliweka mfano gani mzuri unaoweza kuigwa na wale wanaosimamia kutaniko leo?

      9 Inaonekana kulikuwa na badiliko fulani wanaume hao walipoondoka Pafo kuelekea Perga, pwani ya Asia Ndogo, umbali wa kilomita 250 hivi kupitia baharini. Katika Matendo 13:13 kikundi hicho, kinaitwa cha “Paulo na wenzake.” Inaonekana tangu wakati huo, Paulo ndiye aliyesimamia kikundi hicho. Hata hivyo, hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba Barnaba alianza kumwonea wivu Paulo. Badala yake, wanaume hao wawili waliendelea kumtumikia Mungu bega kwa bega. Paulo na Barnaba wanawawekea mfano mzuri wale wanaosimamia kutaniko leo. Badala ya kujitafutia makuu, Wakristo wanakumbuka maneno haya ya Yesu: “[Ninyi] nyote ni ndugu.” Pia alisema: “Yeyote anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”​—Mt. 23:8, 12.

      10. Eleza jinsi safari ya kutoka Perga kuelekea Antiokia ya Pisidia ilivyokuwa.

      10 Walipofika Perga, Yohana Marko aliwaacha Paulo na Barnaba, akarudi Yerusalemu. Haieleweki kwa nini aliondoka. Paulo na Barnaba waliendelea na safari kutoka Perga hadi Antiokia ya Pisidia, jiji lililokuwa katika wilaya ya Galatia. Safari hiyo haikuwa rahisi, kwa kuwa Antiokia ya Pisidia iko mita 1,100 juu ya usawa wa bahari. Mara nyingi njia za milimani zilikuwa na wanyang’anyi. Isitoshe, huenda Paulo alikuwa na matatizo ya afya pia.h

      11, 12. Alipotoa hotuba katika sinagogi huko Antiokia ya Pisidia, Paulo alitumia njia gani ili kuwavutia wasikilizaji wake?

      11 Wakiwa Antiokia ya Pisidia, Paulo na Barnaba waliingia katika sinagogi siku ya Sabato. Masimulizi hayo yanasema: “Baada ya kusoma hadharani Sheria na Manabii, maofisa wasimamizi wa sinagogi wakawatuma watu kwao, wakisema: ‘Wanaume, akina ndugu, ikiwa mna neno lolote la kuwatia moyo watu, lisemeni.’” (Mdo. 13:15) Basi Paulo akasimama na kuanza kuzungumza.

      12 Paulo alianza hotuba yake kwa kusema: “Wanaume, Waisraeli nanyi wengine mnaomwogopa Mungu.” (Mdo. 13:16) Watu hao waliomsikiliza Paulo walikuwa Wayahudi na wageuzwa imani. Paulo alitumia njia gani ili kuwavutia watu hao ambao hawakutambua jukumu la Yesu katika kusudi la Mungu? Paulo alianza kwa kusimulia historia ya Wayahudi. Alieleza jinsi Yehova ‘alivyowainua watu hao walipokuwa wakiishi wakiwa wageni katika nchi ya Misri’ na jinsi ambavyo baada ya kuachiliwa huru, Mungu ‘aliwavumilia huko nyikani’ kwa miaka 40. Pia, Paulo alisimulia jinsi Waisraeli walivyomiliki Nchi ya Ahadi na jinsi ambavyo Yehova ‘aliwapa nchi yao iwe urithi wao.’ (Mdo. 13:17-19) Inasemekana kwamba Paulo alikuwa akirejelea Maandiko fulani yaliyokuwa yamesomwa kwa sauti muda mfupi uliopita kulingana na desturi za Sabato. Ikiwa ndivyo, huo ni mfano mzuri unaoonyesha kwamba Paulo alijua jinsi ya kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.”​—1 Kor. 9:22.

      13. Tunaweza kufanya nini ili kuwavutia watu tunaowahubiria?

      13 Sisi pia tunapaswa kujitahidi kuwavutia watu tunaowahubiria. Kwa mfano, kujua dini ya mtu kunaweza kutusaidia kuchagua habari zitakazompendeza. Pia, tunaweza kunukuu Maandiko ambayo huenda mtu huyo anajua. Huenda tukapata matokeo mazuri kwa kumwomba mtu huyo asome Biblia yake mwenyewe. Jitahidi kuchochea mioyo ya watu unaozungumza nao.

      14. (a) Paulo alianza kuzungumzia habari njema kuhusu Yesu jinsi gani, naye alitoa onyo gani? (b) Umati ulifanya nini baada ya kusikia maneno ya Paulo?

      14 Kisha, Paulo akazungumzia ukoo wa wafalme wa Israeli uliomtokeza “mwokozi, yaani, Yesu” ambaye alitayarishiwa njia na Yohana Mbatizaji. Halafu akaeleza jinsi Yesu alivyouawa na kufufuliwa. (Mdo. 13:20-37) “Acheni ijulikane kwenu,” Paulo akasema, “kwamba kupitia mtu huyo mnatangaziwa msamaha wa dhambi . . . kila mtu anayeamini anatangazwa kuwa bila hatia kupitia mtu huyu.” Naye akawaonya: “Jihadharini ili msipatwe na mambo haya yanayosemwa katika Manabii: ‘Tazameni, ninyi wenye dharau, na mshangae na kuangamia, kwa sababu ninafanya kazi fulani katika siku zenu, kazi ambayo hamtaiamini kamwe hata mtu yeyote akiwaeleza kirefu.’” Matokeo yalikuwa yenye kushangaza. Biblia inasema: “Watu wakawasihi wazungumzie mambo hayo Sabato iliyofuata.” Isitoshe, baada ya kusanyiko la sinagogi kumalizika, “Wayahudi wengi na wageuzwa imani waliomwabudu Mungu wakawafuata Paulo na Barnaba.”​—Mdo. 13:38-43.

      “Tunawageukia Mataifa” (Mdo. 13:44-52)

      15. Baada ya Paulo kutoa hotuba, ni nini kilichotokea Sabato iliyofuata?

      15 Sabato iliyofuata, “karibu jiji lote” lilikusanyika ili kumsikiliza Paulo. Hilo halikuwafurahisha Wayahudi fulani, nao wakaanza “kupinga wakikufuru mambo ambayo Paulo alikuwa akisema.” Paulo na Barnaba wakawaambia hivi kwa ujasiri: “Ilikuwa lazima neno la Mungu lihubiriwe kwenu kwanza. Kwa kuwa mnalikataa na kujiona hamstahili uzima wa milele, tazameni! tunawageukia mataifa. Kwa maana Yehova ametuamuru kwa maneno haya: ‘Nimewachagua muwe nuru ya mataifa, na muwe wokovu mpaka miisho ya dunia.’”​—Mdo. 13:44-47; Isa. 49:6.

      Paulo na Barnaba wakitupwa nje ya jiji la Antiokia ya Pisidia na wapinzani wenye hasira.

      “Wakaanza kuwatesa Paulo na Barnaba . . .  Nao wanafunzi wakaendelea kujawa na shangwe na roho takatifu.”—Matendo 13:50-52

      16. Wayahudi walifanya nini waliposikia maneno makali ya wamishonari hao, nao Paulo na Barnaba walifanya nini upinzani ulipotokea?

      16 Watu wa Mataifa waliokuwa wakisikiliza walishangilia, na “wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.” (Mdo. 13:48) Baada ya muda mfupi, neno la Yehova likaenea nchini kote. Hata hivyo, Wayahudi waliitikia kwa njia tofauti. Wamishonari hao waliwaambia kwamba ingawa walikuwa wa kwanza kutangaziwa Neno la Mungu, walimkataa Masihi na hivyo hawangeweza kuepuka hukumu kali ya Mungu. Wayahudi hao wakawachochea wanawake mashuhuri na wakuu wa jiji hilo, “nao wakaanza kuwatesa Paulo na Barnaba na kuwatupa nje ya mipaka yao.” Paulo na Barnaba walifanya nini? “Wakawakung’utia mavumbi yaliyokuwa kwenye miguu yao na kwenda Ikoniamu.” Je, huo ndio mwisho wa Ukristo katika Antiokia ya Pisidia? Hapana! Wanafunzi waliobaki “wakaendelea kujawa na shangwe na roho takatifu.”​—Mdo. 13:50-52.

      17-19. Tunawezaje kuiga mfano mzuri uliowekwa na Paulo na Barnaba, na ni kwa njia gani kufanya hivyo kutatuletea shangwe?

      17 Tunaweza kujifunza jambo muhimu kutokana na hatua ambayo wanaume hao walichukua upinzani ulipotokea. Hatuachi kamwe kuhubiri, hata wakati watu mashuhuri ulimwenguni wanapojaribu kutuzuia tusitangaze ujumbe wetu. Pia, kumbuka kwamba watu wa Antiokia walipoukataa ujumbe, Paulo na Barnaba ‘walikung’uta mavumbi kutoka miguuni mwao.’ Hawakufanya hivyo kwa sababu ya hasira, bali walitaka kuonyesha kwamba hawana lawama. Wamishonari hao walitambua kwamba hawangeweza kuwalazimisha watu wakubali ujumbe wao. Hata hivyo, watu hao hawangeweza kuwazuia kuhubiri. Paulo na Barnaba hawakupunguza bidii yao badala yake walienda Ikoniamu, na kuendelea kuhubiri!

      18 Namna gani wanafunzi waliobaki Antiokia? Ni kweli kwamba lilikuwa eneo gumu. Hata hivyo, shangwe yao haikutegemea matokeo waliyopata. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:28) Hivyo ndivyo wanafunzi waliobaki Antiokia ya Pisidia walivyofanya.

      19 Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, na tukumbuke kwamba jukumu letu ni kuhubiri habari njema, iwe watu watasikiliza au la. Hata ikiwa watu tunaowahubiria hawapendezwi, tusisahau jinsi hali ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Tukiithamini kweli tuliyo nayo, na kukubali kuongozwa na roho takatifu, sisi pia tunaweza kuwa na shangwe, hata tukikabili upinzani.​—Gal. 5:18, 22.

      BARNABA—“MWANA WA FARAJA”

      Yosefu, Mlawi, mzaliwa wa Kipro, alijulikana sana katika kutaniko la Yerusalemu. Mitume walimpatia jina lingine, lililopatana na utu wake. Walimwita Barnaba, yaani, “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Barnaba alipoona waamini wenzake wana uhitaji fulani, hakusita kuwasaidia.

      Barnaba akitoa mchango wa mifuko miwili ya sarafu.

      Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wapya 3,000 walibatizwa. Inawezekana wengi kati yao walisafiri kwenda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe hiyo na hawakupanga kukaa katika jiji hilo kwa muda mrefu. Kutaniko lilihitaji pesa na vitu vingine ili kuhudumia umati huo. Kwa hiyo, Barnaba akauza sehemu ya shamba na kuwaletea mitume mchango wa pesa.​—Mdo. 4:32-37.

      Barnaba alikuwa mwangalizi Mkristo mkomavu, na sikuzote alikuwa tayari kuwasaidia wengine. Wanafunzi wengine wote walipomwogopa Sauli wa Tarso aliyejulikana kuwa mtesaji, Barnaba alimsaidia. (Mdo. 9:26, 27) Barnaba alikubali kwa unyenyekevu Paulo alipompa shauri zito yeye na Petro kuhusu jinsi Wakristo Wayahudi na wa Mataifa wanavyopaswa kujiendesha. (Gal. 2:9, 11-14) Mifano hiyo michache inaonyesha kwamba kwa kweli Barnaba aliishi kulingana na jina lake, yaani “Mwana wa Faraja.”

      a Ona Sanduku lenye kichwa “Barnaba—‘Mwana wa Faraja.’”

      b Kufikia wakati huo, makutaniko yalikuwa yameenea sehemu za mbali sana kama vile Antiokia ya Siria—lililokuwa kilomita 550 hivi kaskazini mwa Yerusalemu.

      c Ona sanduku lenye kichwa “safari katika siku za mitume.”

      d Katika karne ya kwanza, meli zingeweza kusafiri kilomita 150 hivi kwa siku ikitegemea upepo. Safari hiyo ingechukua muda mrefu zaidi ikiwa hali ya hewa ni mbaya.

      e Ona Sanduku lenye kichwa “Masinagogi ya Wayahudi.”

      f Kisiwa cha Kipro kilikuwa chini ya utawala wa Roma. Mkuu wa kisiwa hicho alikuwa liwali.

      g Tangu wakati huo na kuendelea, Sauli alianza kuitwa Paulo. Watu fulani husema kwamba alijipa jina hilo la Kiroma kwa heshima ya Sergio Paulo. Hata hivyo, kwa kuwa aliendelea kuitwa Paulo hata alipoondoka Kipro, lazima kulikuwa na sababu nyingine, kwamba Paulo, “mtume wa mataifa,” aliamua kwamba tangu wakati huo na kuendelea atatumia jina lake la Kiroma. Huenda pia alitumia jina Paulo kwa sababu matamshi ya Kigiriki ya jina lake la Kiebrania, Sauli, yanafanana sana na neno la Kigiriki lenye maana mbaya.​—Rom. 11:13.

      h Miaka kadhaa baadaye Paulo aliwaandikia barua Wagalatia. Katika barua hiyo, Paulo alisema: “kwa sababu ya ugonjwa wa kimwili kwamba nilipata nafasi yangu ya kwanza ya kuwatangazia habari njema.”​—Gal. 4:13.

  • “Wakizungumza kwa Ujasiri kwa Mamlaka ya Yehova”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 12

      “Wakizungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova”

      Paulo na Barnaba waonyesha unyenyekevu, uvumilivu, na ujasiri

      Matendo 14:1-28

      1, 2. Ni mambo gani yanayotokea, Paulo na Barnaba wakiwa Listra?

      KUNA vurugu jijini Listra. Mwanamume aliyezaliwa kilema anarukaruka kwa shangwe baada ya kuponywa na watu wawili asiowajua. Watu wanastaajabishwa na jambo hilo, na kuhani wa Zeu anawaletea mashada ya maua watu hao wawili ambao umati unaamini kuwa ni miungu. Ng’ombe-dume wanavuta pumzi kwa nguvu na kutoa mlio huku kuhani huyo akiwa tayari kuwachinja. Mara moja Paulo na Barnaba wanamkataza asifanye hivyo. Wanayararua mavazi yao, wanaruka ndani ya umati na kuwasihi sana wasiwaabudu.

      2 Kisha, Wayahudi wapinzani kutoka Antiokia ya Pisidia na Ikoniamu wakafika. Wakawachongea kwa chuki na kuwapotosha watu wa Listra. Umati huohuo, uliotaka kumwabudu Paulo, sasa ukamzunguka na kumpiga kwa mawe mpaka akapoteza fahamu. Baada ya hasira yao kupoa, wanamburuta Paulo, wanamtoa nje ya malango ya jiji, na kumwacha afe.

      3. Tutazungumzia maswali gani katika sura hii?

      3 Ni nini kilichosababisha vurugu hiyo? Wahubiri wa habari njema leo wanaweza kujifunza nini kutokana na matukio hayo? Wazee Wakristo wanawezaje kuiga mfano wa Barnaba na Paulo ambao walivumilia katika huduma yao, na ‘kuzungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova?’​—Mdo. 14:3.

      “Umati Mkubwa . . . Wakawa Waamini” (Mdo. 14:1-7)

      4, 5. Kwa nini Paulo na Barnaba walienda Ikoniamu, na ni nini kilichotokea huko?

      4 Siku chache zilizotangulia, Paulo na Barnaba walikuwa wametupwa nje ya jiji la Antiokia ya Pisidia baada ya Wayahudi wapinzani kuwachochea watu wawatese. Lakini, badala ya kuvunjika moyo, wanaume hao wawili “wakawakung’utia mavumbi yaliyokuwa kwenye miguu yao” wakaaji wa jiji hilo walioukataa ujumbe wao. (Mdo. 13:50-52; Mt. 10:14) Paulo na Barnaba wakaondoka kwa amani na kuacha mambo mikononi mwa Mungu. (Mdo. 18:5, 6; 20:26) Wamishonari hao wawili hawakupoteza shangwe yao, bali waliendelea na safari yao ya kuhubiri. Wakasafiri karibu kilomita 150 kuelekea upande wa kusini-mashariki na kufika nchi tambarare yenye rutuba iliyo katikati ya safu za milima ya Taurus na Sultan.

      5 Mwanzoni, Paulo na Barnaba waliamua kukaa Ikoniamu. Jiji hilo lenye utamaduni wa Kigiriki ni mojawapo ya majiji ya mkoa wa Galatia, katika milki ya Roma.a Jiji hilo lilikuwa na Wayahudi wengi mashuhuri na idadi kubwa ya wageuzwa imani wasio Wayahudi. Kulingana na desturi yao, Paulo na Barnaba waliingia ndani ya sinagogi na kuanza kuhubiri. (Mdo. 13:5, 14) “Wakazungumza vizuri hivi kwamba umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki wakawa waamini.”​—Mdo. 14:1.

      IKONIAMU—JIJI LA WAFRIGIA

      Jiji la Ikoniamu lilikuwa kwenye eneo tambarare, lenye maji ya kutosha na rutuba. Jiji hilo lilikuwa kwenye makutano ya njia muhimu ya biashara iliyounganisha Siria na Roma, Ugiriki, na mkoa wa Asia wa Roma.

      Waikoniamu waliabudu Cybele, mungu wa uzazi wa Frigia, na ibada hiyo ilihusisha mambo fulani yaliyotokana na ibada ya Wagiriki wakati wa enzi za utawala wa Wagiriki. Jiji hilo lilichukuliwa na Roma mwaka wa 65 K.W.K., na katika karne ya kwanza W.K., likawa kituo chenye ufanisi cha biashara na kilimo. Ingawa Wayahudi mashuhuri waliishi Ikoniamu, inaonekana jiji hilo lilidumisha utamaduni wa Kigiriki. Masimulizi ya kitabu cha Matendo yanasema kwamba Wayahudi na “Wagiriki” waliishi huko.​—Mdo. 14:1.

      Jiji la Ikoniamu lilikuwa katikati ya Likaonia na Frigia, katika maeneo ya Galatia. Waandishi fulani wa zamani, kutia ndani Cicero na Strabo, walisema kwamba Ikoniamu lilikuwa jiji la Likaonia, na inaonekana kwamba jiji hilo lilikuwa katika eneo la Likaonia. Hata hivyo, kulingana na masimulizi ya kitabu cha Matendo jiji la Ikoniamu ni tofauti na Likaonia, ambapo “lugha ya Kilikaonia” ilizungumzwa. (Mdo. 14:1-6, 11) Kwa sababu hiyo, wachambuzi hudai kwamba kitabu cha Matendo si sahihi. Hata hivyo, mwaka wa 1910, wachimbuzi wa vitu vya kale walipata maandishi katika jiji hilo yanayoonyesha kwamba Kifrigia ndiyo lugha iliyozungumzwa Ikoniamu kwa karne mbili baada ya Paulo na Barnaba kutembelea jiji hilo. Hivyo, mwandikaji wa kitabu cha Matendo hakukosea kwa kutofautisha Ikoniamu na majiji ya Likaonia.

      6. Kwa nini Paulo na Barnaba walipata matokeo mazuri, nasi tunawezaje kuwaiga?

      6 Kwa nini Paulo na Barnaba walipata matokeo mazuri? Paulo aliyajua Maandiko vizuri. Aliyahusianisha kwa ustadi na historia, unabii, na Sheria ya Musa ili kuthibitisha kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. (Mdo. 13:15-31; 26:22, 23) Barnaba aliwajali sana watu. (Mdo. 4:36, 37; 9:27; 11:23, 24) Wanaume hao hawakutegemea uelewaji wao wenyewe bali walizungumza “kwa mamlaka ya Yehova.” Unawezaje kuwaiga wamishonari hao unapohubiri? Kwa kufanya mambo yafuatayo: Lijue kabisa Neno la Mungu. Chagua Maandiko yatakayowavutia wasikilizaji wako. Tafuta njia za kuwafariji wale unaowahubiria. Na sikuzote mafundisho yako yategemee mamlaka ya Neno la Yehova, bali si hekima yako.

      7. (a) Habari njema huwa na matokeo gani? (b) Ikiwa familia yenu imegawanyika kwa sababu ya habari njema, unapaswa kukumbuka nini?

      7 Hata hivyo, si kila mtu jijini Ikoniamu aliyefurahi kusikia ujumbe wa Paulo na Barnaba. Luka anasema hivi: “Wayahudi ambao hawakuamini wakawachochea watu wa mataifa na kuwafanya wawachukie akina ndugu.” Paulo na Barnaba waliamua kukaa huko na kutetea habari njema, na “wakatumia muda mrefu wakizungumza kwa ujasiri.” Hata hivyo, “umati wa jiji ulikuwa umegawanyika; baadhi yao walikuwa upande wa Wayahudi lakini wengine upande wa mitume.” (Mdo. 14:2-4) Ndivyo ilivyo leo, ujumbe wa habari njema huleta umoja kwa watu fulani, lakini kwa wengine huleta mgawanyiko. (Mt. 10:34-36) Ikiwa familia yenu imegawanyika kwa sababu ya habari njema, kumbuka kwamba mara nyingi upinzani hutokea kwa sababu ya uchongezi au uvumi usio na msingi. Mwenendo wako unaweza kubadili mtazamo wa wale wanaokupinga.​—1 Pet. 2:12; 3:1, 2.

      8. Kwa nini Paulo na Barnaba waliondoka Ikoniamu, nasi tunaweza kujifunza nini?

      8 Baada ya muda, wapinzani huko Ikoniamu wakapanga njama ya kuwapiga mawe Paulo na Barnaba. Wamishonari hao wawili walipopata habari, waliamua kwenda kuhubiri katika eneo lingine. (Mdo. 14:5-7) Leo, wahubiri wa Ufalme hutumia busara. Tunaposhambuliwa kwa maneno, sisi huendelea kuhubiri kwa ujasiri. (Flp. 1:7; 1 Pet. 3:13-15) Lakini tukiona kwamba kuna uwezekano wa kutendewa kwa jeuri, tunaepuka kufanya jambo la kipumbavu linaloweza kuhatarisha uhai wetu au wa waabudu wenzetu.​—Met. 22:3.

      “Mgeuke . . . Mje kwa Mungu Aliye Hai” (Mdo. 14:8-19)

      9, 10. Jiji la Listra lilikuwa wapi, na ni mambo gani tunayojua kuhusu wenyeji wake?

      9 Paulo na Barnaba wakaelekea Listra, eneo la milki ya Roma lililokuwa kilomita 30 hivi kusini-magharibi mwa Ikoniamu. Jiji la Listra lilikuwa na uhusiano wa karibu sana na Antiokia ya Pisidia, lakini jiji hilo halikuwa na Wayahudi wengi maarufu. Ingawa wenyeji walizungumza Kigiriki, lugha yao ya asili ilikuwa Kilikaonia. Paulo na Barnaba walianza kuhubiri katika eneo la umma huenda kwa sababu jiji hilo halikuwa na sinagogi. Petro alimponya mtu aliyezaliwa kilema jijini Yerusalemu. Paulo pia alimponya mtu aliyezaliwa kilema jijini Listra. (Mdo. 14:8-10) Kwa sababu ya muujiza ambao Petro alifanya, umati mkubwa wa watu ukaamini. (Mdo. 3:1-10) Lakini muujiza ambao Paulo alifanya ulikuwa na matokeo tofauti kabisa.

      10 Kama tulivyoona mwanzoni mwa sura hii, yule mtu aliyekuwa kilema aliporuka na kuanza kutembea, mara moja umati wa wapagani huko Listra ukafikiri kwamba wao ni miungu. Walimwita Barnaba Zeu, mkuu wa miungu, naye Paulo wakamwita Herme, mwana wa Zeu na msemaji wa miungu. (Ona sanduku lenye kichwa “Jiji la Listra na Madhehebu ya Zeu na Herme.”) Hata hivyo, Barnaba na Paulo waliazimia kuusadikisha umati kwamba wanazungumza na kutenda kwa mamlaka ya Yehova, Mungu wa kweli, bali si kwa mamlaka ya miungu ya kipagani.​—Mdo. 14:11-14.

      JIJI LA LISTRA NA MADHEHEBU YA ZEU NA HERME

      Jiji la Listra lilikuwa katika bonde lililokuwa mbali na barabara kuu. Kaisari Augusto aliliteka jiji hilo na kulifanya kuwa sehemu ya milki ya Roma na kuliita Julia Felix Gemina Lustra. Kikosi cha jeshi cha jiji hilo kilitumiwa kulinda mkoa wa Galatia dhidi ya mashambulizi kutoka kwa makabila ya watu walioishi milimani. Jiji hilo lilitawaliwa kulingana na utaratibu wa Kiroma, na maofisa wa jiji hilo walikuwa na majina ya cheo ya Kilatini. Hata hivyo, jiji la Listra liliendelea kudumisha utamaduni wake wa Kilikaonia kuliko utamaduni wa Kiroma. Ndio sababu watu wa Listra wanaotajwa katika kitabu cha Matendo walizungumza Kilikaonia.

      Kati ya vitu vya kale vilivyopatikana karibu na jiji la Listra ni maandishi yanayowataja “makuhani wa Zeu” na sanamu ya mungu Herme. Hekalu la Zeu na Herme lilipatikana katika eneo hilo pia.

      Hadithi za kale zilizoandikwa na Ovid, mshairi Mroma (43 K.W.K. hadi 17 W.K.) zinatupatia habari zaidi kuhusu masimulizi ya kitabu cha Matendo. Kulingana na Ovid, Jupiter na Mercury, miungu wa Kiroma wanaoitwa Zeu na Herme katika Kigiriki, walitembelea Frigia wakiwa na umbo la wanadamu. Walienda katika nyumba elfu moja, lakini hakuna mtu hata mmoja aliyewakaribisha isipokuwa Philemon na Baucis, wenzi wa ndoa waliozeeka, ambao waliwakaribisha katika nyumba yao duni. Ili kuonyesha shukrani zao, Zeu na Herme walibadili nyumba hiyo na kuwa hekalu lililojengwa kwa marumaru na dhahabu, na kuwafanya Philemon na Baucis kuwa makuhani. Kisha wakaharibu nyumba za watu wote ambao hawakuwakaribisha. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Iwapo watu wa Listra walikumbuka hadithi hiyo walipowaona Paulo na Barnaba wakimponya mtu aliyekuwa mlemavu, huenda ndio sababu walitaka kuwakaribisha na kuwatolea dhabihu.”​—The Book of Acts in Its Graeco-Roman Setting.

      Paulo na Barnaba wakikataa kusifiwa na umati jijini Listra. Watu hao wanacheza muziki, wanatayarisha dhabihu na kuinama mbele yao.

      “Mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia.”—Matendo 14:15

      11-13. (a) Paulo na Barnaba waliwaambia nini wenyeji wa Listra? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Paulo na Barnaba?

      11 Licha ya mambo hayo yote, Paulo na Barnaba walijitahidi kufikia mioyo ya wasikilizaji wao kwa njia bora zaidi. Katika kisa hiki, Luka anaeleza njia yenye mafanikio iliyotumiwa kuwahubiria wapagani habari njema. Ona jinsi Paulo na Barnaba walivyowasihi wasikilizaji wao: “Wanaume, kwa nini mnafanya mambo haya? Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu kama wenu. Nasi tunawatangazia habari njema, ili mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo. Katika vizazi vilivyopita aliruhusu watu wa mataifa yote waendelee kutembea katika njia zao, ingawa hakujiacha bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno, akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.”​—Mdo. 14:15-17.

      12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno hayo yenye kuchochea? Kwanza, Paulo na Barnaba hawakujiona kuwa bora kuliko wasikilizaji wao. Hawakujifanya kuwa watu wenye uwezo wa pekee. Badala yake, walikubali kwamba walikuwa na udhaifu uleule kama wa wapagani waliowasikiliza. Ni kweli kwamba Paulo na Barnaba walikuwa wamepokea roho takatifu na kuwekwa huru kutokana na utumwa wa mafundisho ya uwongo. Pia, walikuwa na tumaini la pekee la kutawala pamoja na Kristo. Hata hivyo, walijua kwamba watu wa Listra wangeweza kupata zawadi hizohizo ikiwa wangemtii Kristo.

      13 Tunawaonaje wale tunaowahubiria? Je, tunaona wako sawa na sisi? Tunapowasaidia wengine kujifunza kweli za Neno la Mungu, je, tunawaiga Paulo na Barnaba kwa kuepuka kujitafutia sifa? Charles Taze Russell, mwalimu stadi aliyeongoza kazi ya kuhubiri mwishoni mwa karne ya 19 na mwanzoni mwa karne ya 20, aliweka mfano mzuri. Aliandika: ‘Hatujitafutii sifa wala heshima kwa sababu ya habari tunazoandika; wala hatutaki kuitwa Viongozi au Marabi.’ Ndugu Russell alikuwa mnyenyekevu kama Paulo na Barnaba. Vivyo hivyo, tunapohubiri, kusudi letu ni kuwasaidia watu wamgeukie “Mungu aliye hai” si kujitafutia utukufu.

      14-16. Ni masomo gani mengine tunayojifunza kutokana na mambo ambayo Paulo na Barnaba waliwaambia watu wa Listra?

      14 Jambo la pili tunaloweza kujifunza kutokana na mazungumzo hayo ni; Paulo na Barnaba walibadilika kulingana na hali. Wayahudi na wageuzwa imani waliokuwa Ikoniamu walijua mengi kuhusu Maandiko au jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli, lakini watu wa Listra walijua mambo machache au hawakujua kabisa mambo hayo. Hata hivyo, wale waliowasikiliza Paulo na Barnaba walikuwa wakulima. Jiji la Listra lilikuwa na hali nzuri ya hewa na mashamba yenye rutuba. Watu hao wangeweza kuona uthibitisho wa kutosha wa sifa za Muumba kupitia mambo kama vile majira ya mavuno, na wamishonari hao walitumia jambo hilo kama msingi wa kuwahubiria.​—Rom. 1:19, 20.

      15 Je, sisi pia tunaweza kubadilika kulingana na hali? Ingawa mkulima anaweza kupanda mbegu ileile katika mashamba tofauti, anahitaji kutumia mbinu tofauti za kuutayarisha udongo. Huenda udongo fulani ukawa laini na tayari kwa ajili ya kupanda mbegu, lakini udongo mwingine ukahitaji matayarisho zaidi. Vivyo hivyo, tunapanda mbegu ileile, yaani, ujumbe wa Ufalme unaopatikana katika Neno la Mungu. Hata hivyo, kama Paulo na Barnaba, tutajitahidi kutambua hali na dini za watu tunaowahubiria. Jambo hilo litatusaidia kuwahubiria ujumbe wa Ufalme kulingana na hali zao.​—Luka 8:11, 15.

      16 Tunaweza kujifunza jambo la tatu kutokana na masimulizi kuhusu Paulo, Barnaba, na watu wa Listra. Licha ya jitihada zetu, wakati mwingine mbegu tunazopanda zinanyakuliwa au kuanguka kwenye miamba. (Mt. 13:18-21) Jambo hilo likitokea, usikate tamaa. Kama Paulo alivyowakumbusha wanafunzi huko Roma, “kila mmoja wetu [kutia ndani kila mtu tunayezungumza naye Neno la Mungu] atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”​—Rom. 14:12.

      “Wakawakabidhi kwa Yehova” (Mdo. 14:20-28)

      17. Baada ya kuondoka Derbe, Paulo na Barnaba walienda wapi, na kwa nini?

      17 Paulo alipoburutwa na kutolewa nje ya jiji la Listra akiwa mahututi, wanafunzi walimzunguka, akasimama, akaingia jijini na kukaa hapo usiku kucha. Siku iliyofuata, Paulo na Barnaba wakaanza safari ya kilomita 100 kwenda Derbe. Wazia maumivu makali ambayo Paulo alikuwa nayo wakati wa safari hiyo, kwani saa chache zilizopita alikuwa amepigwa mawe! Hata hivyo, yeye na Barnaba walivumilia, na walipofika Derbe, wakafanya “watu wengi kuwa wanafunzi.” Kisha, badala ya kwenda nyumbani kwao huko Antiokia ya Siria, “wakarudi Listra, Ikoniamu, na Antiokia [ya Pisidia].” Kwa nini? Ili kuwatia nguvu “wanafunzi na kuwatia moyo wabaki katika imani.” (Mdo. 14:20-22) Waliweka mfano mzuri sana! Walitanguliza mahitaji ya kutaniko badala ya starehe zao. Waangalizi wanaosafiri na wamishonari wa siku zetu wanaiga mfano wao.

      18. Wanaume wazee huwekwa rasmi jinsi gani?

      18 Zaidi ya kuwatia nguvu wanafunzi kwa maneno na mfano wao, Paulo na Barnaba waliwaweka rasmi “wazee kwa ajili yao katika kila kutaniko.” Ingawa Paulo na Barnaba ‘walitumwa na roho takatifu’ katika safari hiyo ya umishonari, walisali na kufunga, nao “wakawakabidhi [wazee hao] kwa Yehova.” (Mdo. 13:1-4; 14:23) Ndivyo ilivyo leo. Kabla ya mapendekezo, baraza la wazee husali na kuchanganua ili kutambua ikiwa ndugu anatimiza sifa za Kimaandiko. (1 Tim. 3:1-10, 12, 13; Tito 1:5-9; Yak. 3:17, 18; 1 Pet. 5:2, 3) Jambo kuu si muda ambao amekuwa Mkristo. Badala yake, maneno na mwenendo wake unapaswa kuonyesha wazi kwamba roho takatifu inafanya kazi katika maisha yake. Mtu anastahili kutumikia akiwa mwangalizi ikiwa anatimiza sifa zilizo katika Maandiko. (Gal. 5:22, 23) Mwangalizi wa mzunguko huwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma.​—Linganisha 1 Timotheo 5:22.

      19. Wazee wanawajibika kwa nani, na wanawaigaje Paulo na Barnaba?

      19 Wazee waliowekwa rasmi wanajua kwamba wanawajibika mbele za Mungu. (Ebr. 13:17) Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, wazee wanaongoza katika kazi ya kuhubiri. Wanawatia nguvu Wakristo wenzao kwa maneno yao. Wanatanguliza faida za kutaniko badala ya starehe zao.​—Flp. 2:3, 4.

      20. Tunanufaikaje tunaposoma ripoti kuhusu kazi ya uaminifu ya ndugu zetu?

      20 Mwishowe Paulo na Barnaba waliporudi kwenye makao yao huko Antiokia ya Siria, walisimulia “mambo mengi ambayo Mungu alikuwa amefanya kupitia kwao, na kwamba alikuwa amewafungulia mataifa mlango wa kuingia kwenye imani.” (Mdo. 14:27) Tunaposoma kuhusu kazi ya uaminifu ya ndugu zetu Wakristo na jinsi ambavyo Yehova amebariki jitihada zao, tunatiwa moyo kuendelea ‘kuzungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova.’

      a Ona sanduku lenye kichwa “Ikoniamu—Jiji la Wafrigia.”

  • “Baada ya . . . Kutoelewana”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 13

      “Baada ya . . . Kutoelewana”

      Suala la tohara lapelekwa kwenye baraza linaloongoza

      Matendo 15:1-12

      1-3. (a) Ni suala gani lililotishia kuvunja kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza? (b) Tunaweza kunufaikaje na masimulizi ya kitabu cha Matendo?

      PAULO na Barnaba wamerudi Antiokia ya Siria wakiwa na shangwe baada ya safari yao ya kwanza ya umishonari. Wana furaha nyingi kwa sababu Yehova “amewafungulia mataifa mlango wa kuingia kwenye imani.” (Mdo. 14:26, 27) Kwa kweli, habari njema zinahubiriwa kotekote jijini Antiokia na “idadi kubwa” ya Watu wa Mataifa wanajiunga na kutaniko.​—Mdo. 11:20-26.

      2 Baada ya muda mfupi, habari hizo zenye kusisimua kuhusu ongezeko zinafika Yudea. Lakini si watu wote waliofurahishwa na habari hizo; ongezeko hili linasababisha mabishano kuhusu suala la tohara. Waamini Wayahudi wanapaswa kuwaonaje waamini wasio Wayahudi, na wale ambao si Wayahudi wanapaswa kuionaje Sheria ya Musa? Suala hilo linatokeza mgawanyiko mkubwa unaotishia kulivunja kutaniko la Kikristo. Suala hilo lingetatuliwaje?

      3 Tunapoendelea kuchunguza kitabu cha Matendo, tutajifunza mambo mengi muhimu. Mambo hayo yatatusaidia kutenda kwa busara suala linaloleta mgawanyiko litakapotokea.

      “Msipotahiriwa” (Mdo. 15:1)

      4. Watu fulani walieneza maoni gani yasiyofaa, na ni swali gani linalotokea?

      4 Luka anaandika: “Watu fulani wakashuka [Antiokia] kutoka Yudea na kuanza kuwafundisha akina ndugu: ‘Msipotahiriwa kulingana na desturi ya Musa, hamwezi kuokolewa.’” (Mdo. 15:1) Huenda hao “watu fulani” wanaotajwa walikuwa Mafarisayo kabla ya kuwa Wakristo. Na inaonekana kwamba waliathiriwa na mtazamo wa Mafarisayo wa kushikilia sheria kupita kiasi. Pia, huenda walidai wametumwa na mitume na wanaume wazee wa Yerusalemu. (Mdo. 15:23, 24) Hivyo, kwa nini Wakristo Wayahudi bado walifikiri kwamba tohara ilikuwa muhimu, hata baada ya Mungu kuweka wazi kupitia mtume Petro kwamba amekubali watu wasio Wayahudi waingie katika kutaniko la Kikristo?a—Mdo. 10:24-29, 44-48.

      5, 6. (a) Kwa nini baadhi ya Wakristo Wayahudi waliamini kwamba tohara ni muhimu? (b) Eleza ni kwa nini agano la tohara halikuwa sehemu ya agano la Kiabrahamu. (Ona maelezo ya chini.)

      5 Huenda kulikuwa na sababu kadhaa. Kwanza, Yehova ndiye aliyeagiza wanaume watahiriwe, na tohara ilikuwa ishara ya uhusiano wa pekee pamoja naye. Tohara ilianza kabla ya agano la Sheria na baadaye ikaja kuwa sehemu ya agano hilo. Abrahamu na nyumba yake walikuwa watu wa kwanza kutahiriwa.b (Law. 12:2, 3) Kulingana na Sheria ya Musa, hata wageni walipaswa kutahiriwa kabla ya kupata mapendeleo fulani, kama vile kula mlo wa Pasaka. (Kut. 12:43, 44, 48, 49) Hivyo, Wayahudi walimwona mtu ambaye hajatahiriwa kuwa si safi na mwenye kuchukiza.​—Isa. 52:1.

      6 Waabudu Wayahudi walihitaji imani na unyenyekevu ili kukubali fundisho hilo jipya. Agano jipya lilichukua nafasi ya agano la Sheria. Hivyo, mtu hakuwa sehemu ya watu wa Mungu kwa kuwa tu alizaliwa akiwa Myahudi. Na Wakristo Wayahudi walioishi na Wayahudi wengine—kama wale walioishi Yudea—walihitaji ujasiri ili kumkiri Kristo na kuwakubali Watu wa Mataifa ambao hawakutahiriwa wawe waabudu wenzao.​—Yer. 31:31-33; Luka 22:20.

      7. “Watu . . . kutoka Yudea” hawakuelewa kweli gani?

      7 Bila shaka, viwango vya Mungu havikubadilika. Agano jipya lina kanuni fulani za msingi zilizokuwa katika Sheria ya Musa. (Mt. 22:36-40) Kwa mfano, Paulo aliandika hivi baadaye kuhusu tohara: “Yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani, na kutahiriwa kwake ni kule kwa moyo kupitia roho, wala si kupitia sheria zilizoandikwa.” (Rom. 2:29; Kum. 10:16) “Watu . . . kutoka Yudea” waliotajwa mwanzoni, hawakuelewa kweli hizo bali walifikiri kwamba Mungu hakuondoa kamwe sheria ya tohara. Je, wangebadili maoni yao?

      MAFUNDISHO YA WAYUDAIZA

      Hata baada ya baraza linaloongoza la karne ya kwanza kutatua suala la tohara, watu fulani waliodai kuwa Wakristo walikaidi uamuzi uliotolewa. Mtume Paulo aliwaita Wayudaiza, ‘ndugu wa uwongo’ waliotaka “kupotosha habari njema kuhusu Kristo.”​—Gal. 1:7; 2:4; Tito 1:10.

      Inaonekana lengo la ndugu hao wa uwongo lilikuwa kuwatuliza Wayahudi ili wasipinge vikali Ukristo. (Gal. 6:12, 13) Ndugu hao wa uwongo walidai kwamba ili mtu aonwe kuwa mwadilifu lazima ashike Sheria ya Musa kuhusu mambo kama vile chakula, tohara, na sherehe za Kiyahudi.​—Kol. 2:16.

      Haishangazi kwamba watu walioshikilia maoni hayo hawakuwa huru kushirikiana na waabudu wenzao kutoka kwa Watu wa Mataifa. Inasikitisha kwamba hata watu wenye kuheshimika katika kutaniko la Kikristo, ambao walikuwa na asili ya Kiyahudi, walionyesha mtazamo huo usiofaa. Kwa mfano, ndugu kutoka kutaniko la Yerusalemu walipoenda Antiokia, walijitenga na ndugu zao wa Mataifa. Hata Petro ambaye alikuwa akishirikiana kwa uhuru na Watu wa Mataifa kabla ya wakati huo, alijitenga—hata hakutaka kula pamoja nao. Alitenda kinyume kabisa na kanuni ambayo mwanzoni yeye mwenyewe aliitetea. Ndiyo sababu Petro alipata shauri kali kutoka kwa Paulo.​—Gal. 2:11-14.

      “Kutoelewana na Kubishana” (Mdo. 15:2)

      8. Kwa nini suala la tohara lilipelekwa kwenye baraza linaloongoza lililokuwa jijini Yerusalemu?

      8 Luka anasema hivi: “Baada ya Paulo na Barnaba kutoelewana na kubishana sana na watu hao [“kutoka Yudea”], wakapanga Paulo na Barnaba na wengine wapande kwenda kwa mitume na wazee huko Yerusalemu kuuliza kuhusu jambo hilo.”c (Mdo. 15:2) Maneno “kutoelewana na kubishana” yanaonyesha kwamba kila upande ulishikilia maoni yake, na kutaniko la Antiokia halingeweza kushughulikia jambo hilo. Ili kudumisha amani na umoja, kutaniko lilitenda kwa hekima lilipoamua kuwauliza “mitume na wazee huko Yerusalemu,” waliokuwa baraza linaloongoza. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa wazee hao wa Antiokia?

      Wakristo wa karne ya kwanza wa kutaniko la Yerusalemu wakibishana na Paulo na Barnaba.

      Wengine wakasisitiza: “Ni lazima . . . kuwaamuru [Watu wa Mataifa] washike Sheria ya Musa”

      9, 10. Ndugu wa Antiokia na pia Paulo na Barnaba walituwekea mfano gani?

      9 Jambo moja muhimu tunalojifunza ni kwamba tunapaswa kuliamini tengenezo la Mungu. Fikiria hili: Ndugu wa Antiokia walijua kwamba washiriki wote wa baraza linaloongoza ni Wakristo wenye asili ya Kiyahudi. Hata hivyo, waliamini kwamba baraza hilo lingetatua suala la kutahiriwa kupatana na Maandiko. Kwa nini? Kutaniko lilikuwa na uhakika kwamba Yehova ataongoza mambo kupitia roho yake takatifu na Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu Kristo. (Mt. 28:18, 20; Efe. 1:22, 23) Masuala mazito yanapotokea, na tuige mfano mzuri wa Wakristo wa Antiokia kwa kuliamini tengenezo la Mungu na Baraza Linaloongoza.

      10 Pia, kisa hicho kinatukumbusha faida ya unyenyekevu na uvumilivu. Paulo na Barnaba waliwekwa rasmi na roho takatifu ili wawahubirie watu wa mataifa, lakini, waliamua kutotumia mamlaka hiyo kutatua suala la tohara lilipotokea Antiokia. (Mdo. 13:2, 3) Isitoshe, Paulo aliandika hivi baadaye: “Nilienda [Yerusalemu] kutokana na ufunuo”​—akionyesha alipata mwongozo kutoka kwa Mungu. (Gal. 2:2) Leo, wazee hujitahidi kuwa wanyenyekevu na wavumilivu hasa mambo yanayoweza kusababisha mgawanyiko yanapotokea. Badala ya kubishana, wao humtegemea Yehova kwa kuchunguza Maandiko na pia maagizo na miongozo inayotolewa na mtumwa mwaminifu.​—Flp. 2:2, 3.

      11, 12. Kwa nini tunahitaji kumsubiri Yehova?

      11 Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kumsubiri Yehova atusaidie kuelewa vizuri jambo fulani. Kumbuka kwamba katika siku za Paulo, akina ndugu walihitaji kungoja kwa miaka 13 hivi, tangu mwaka wa 36 W.K. Kornelio alipotiwa mafuta mpaka mwaka wa 49 W.K., Yehova alipotatua suala la tohara. Kwa nini muda mrefu ulipita? Huenda Mungu alitaka muda wa kutosha upite ili kuwasaidia Wayahudi wanyoofu wabadili maoni yao kuhusu badiliko hilo kubwa. Kwa kweli, kukomeshwa kwa agano la tohara lililodumu kwa miaka 1,900, ambalo Yehova alifanya na babu yao mpendwa Abrahamu, kulikuwa badiliko kubwa!—Yoh. 16:12.

      12 Ni pendeleo kubwa sana kufundishwa na kufinyangwa na Baba yetu wa mbinguni mwenye subira na fadhili! Sikuzote mambo anayotufundisha yanatunufaisha. (Isa. 48:17, 18; 64:8) Kwa hiyo, tusishikilie kamwe maoni yetu kwa kiburi au kupinga mabadiliko yanayofanywa na tengenezo au mabadiliko ya uelewaji wetu wa maandiko fulani. (Mhu. 7:8) Ukigundua kwamba una mtazamo kama huo, hata kwa kiasi kidogo, sali na utafakari kanuni zinazopatikana katika Matendo sura ya 15.d

      13. Tunawezaje kuiga subira ya Yehova katika huduma yetu?

      13 Subira inahitajika hasa tunapojifunza Biblia na watu ambao huona ni vigumu kuacha desturi au mafundisho yasiyopatana na maandiko. Katika hali kama hizo, tunahitaji kusubiri ili roho takatifu ya Mungu ichochee moyo wa mwanafunzi kufanya mabadiliko. (1 Kor. 3:6, 7) Pia, ni vizuri kusali kwa ajili yao. Mwishowe, Yehova atatusaidia tupate njia bora ya kuwasaidia.​—1 Yoh. 5:14.

      ‘IMANI YA MASHAHIDI WA YEHOVA INATEGEMEA BIBLIA’

      Kama ilivyokuwa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, sikuzote nuru ya kweli huangaza hatua kwa hatua. (Met. 4:18; Dan. 12:4, 9, 10; Mdo. 15:7-9) Leo, watu wa Yehova hupatanisha imani yao na kweli inayofunuliwa; hawalazimishi Maandiko yapatane na maoni yao. Watu wasio Mashahidi wa Yehova wameona wazi jambo hilo. Katika kitabu chake Truth in Translation, Jason David BeDuhn, profesa katika Chuo Kikuu cha Northern Arizona nchini Marekani, aliyesomea mambo ya dini, aliandika kwamba Mashahidi wa Yehova huisoma Biblia “kwa unyoofu na [hujenga] imani yao na kutenda kulingana na yale wanayosoma kutoka katika Biblia badala ya kuamua kulingana na maoni yao mambo ambayo Biblia itasema.”

      “Wakisimulia Kirefu” Mambo Yaliyoonwa Yenye Kutia Moyo (Mdo. 15:3-5)

      14, 15. Kutaniko la Antiokia liliwaonyeshaje heshima Paulo, Barnaba, na wale ndugu wengine waliosafiri pamoja nao, na ndugu hao waliwatia moyo waabudu wenzao jinsi gani?

      14 Masimulizi ya Luka yanaendelea: “Baada ya kusindikizwa umbali fulani na kutaniko, watu hao wakaenda wakapitia Foinike na Samaria, wakisimulia kirefu kuhusu kugeuka kwa watu wa mataifa, nao wakafanya akina ndugu washangilie sana.” (Mdo. 15:3) Kutaniko liliwasindikiza Paulo, Barnaba na ndugu wengine waliosafiri pamoja nao. Kwa kufanya hivyo, walionyesha ndugu hao heshima na upendo wa Kikristo na waliwatakia baraka za Mungu. Ndugu wa Antiokia wanatuwekea mfano mzuri sana! Je, unawaonyesha heshima ndugu na dada zako Wakristo, “hasa wale [wazee] wanaofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha”?​—1 Tim. 5:17.

      15 Wakiwa njiani, wasafiri hao waliwatia moyo Wakristo wenzao waliokuwa Foinike na Samaria, “wakisimulia kirefu” mambo yaliyoonwa kuhusu matokeo mazuri waliyopata kwa kuwahubiria Watu wa Mataifa. Huenda baadhi ya watu waliowasikiliza walikuwa Wakristo Wayahudi waliokimbilia maeneo hayo baada ya Stefano kuuawa. Ndivyo ilivyo leo. Ripoti kuhusu jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi ya kufanya wanafunzi huwatia moyo sana ndugu zetu, hasa wale walio katika hali ngumu. Je, wewe hufaidika kikamili kutokana na ripoti hizo kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, makusanyiko, na kwa kusoma mambo yaliyoonwa au masimulizi ya maisha yaliyo kwenye machapisho yetu yaliyochapishwa au kwenye tovuti yetu ya jw.org?

      16. Ni nini kinachoonyesha kwamba suala la tohara lilikuwa tatizo kubwa?

      16 Baada ya kusafiri kuelekea kusini, kilomita 550 hivi, Paulo na wenzake walifika mwisho wa safari yao. Luka anaandika: “Walipofika Yerusalemu, walikaribishwa kwa fadhili na kutaniko na mitume na wazee, nao wakawasimulia mambo mengi ambayo Mungu alifanya kupitia kwao.” (Mdo. 15:4) Hata hivyo, “baadhi ya wale wa madhehebu ya Mafarisayo ambao sasa walikuwa waamini wakasimama kutoka kwenye viti vyao na kusema: ‘Ni lazima watahiriwe na kuwaamuru washike Sheria ya Musa.’” (Mdo. 15:5) Ni wazi kwamba suala la kutahiriwa kwa Wakristo wasio Wayahudi lilikuwa tatizo kubwa, na lilipaswa kutatuliwa.

      “Mitume na Wazee Wakakusanyika Pamoja” (Mdo. 15:6-12)

      17. Ni nani waliofanyiza baraza linaloongoza la Yerusalemu, na huenda ni kwa nini baraza hilo lilitia ndani “wazee”?

      17 Methali 13:10 inasema: “Hekima ni ya wale wanaotafuta ushauri.” Wakitenda kulingana na kanuni hiyo, “mitume na wazee wakakusanyika pamoja ili kulichunguza [suala la tohara].” (Mdo. 15:6) “Mitume na wazee” waliwakilisha kutaniko lote la Kikristo, kama Baraza Linaloongoza linavyofanya leo. Kwa nini “wazee” walitumikia pamoja na mitume? Kumbuka kwamba mtume Yakobo alikuwa ameuawa, na kwa kipindi fulani mtume Petro alikuwa gerezani. Je, mitume wengine pia wangepatwa na mambo kama hayo? Wazee hao wenye sifa za kustahili ambao walitiwa mafuta wangesaidia kusimamia kazi vizuri hata ikiwa hali zingebadilika.

      18, 19. Ni maneno gani yenye kusadikisha ambayo Petro alisema, na waliomsikiliza walifikia mkataa gani?

      18 Luka anaendelea: “Baada ya kujadiliana sana, Petro akasimama na kuwaambia: ‘Wanaume, akina ndugu, mnajua vema kwamba tangu siku za zamani Mungu alinichagua kati yenu ili kupitia kinywa changu watu wa mataifa wasikie neno la habari njema na kuamini. Pia, Mungu anayeujua moyo, alitoa ushahidi kwa kuwapa roho takatifu, kama vile alivyotupatia sisi. Naye hakutofautisha hata kidogo kati yetu na wao, bali aliisafisha mioyo yao kwa imani.’” (Mdo. 15:7-9) Kulingana na kitabu kimoja cha marejeo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kujadiliana” katika mstari wa 7 linaweza kumaanisha pia “kutafuta,” au “mahojiano.” Inaonekana kwamba maoni ya ndugu hao yalitofautiana, na waliyazungumzia waziwazi.

      19 Maneno yenye kusadikisha ya Petro yaliwakumbusha wote kwamba yeye mwenyewe alikuwepo wakati watu wa kwanza wa Mataifa wasiotahiriwa—Kornelio na nyumba yake—walipotiwa mafuta kwa roho takatifu mwaka wa 36 W.K. Kwa hiyo, ikiwa Yehova aliacha kutofautisha Myahudi na asiye Myahudi, wanadamu wana mamlaka gani ya kutenda kinyume? Isitoshe, mtu hutangazwa kuwa mwadilifu kwa sababu ya imani yake kwa Kristo bali si kupitia Sheria ya Musa.​—Gal. 2:16.

      20. Watu waliopendekeza tohara walikuwa ‘wakimjaribu Mungu’ jinsi gani?

      20 Akitoa uthibitisho usioweza kupingwa wa neno la Mungu na roho takatifu, Petro akamalizia kwa kusema: “Basi kwa nini sasa mnamjaribu Mungu kwa kuweka kwenye shingo za wanafunzi nira ambayo mababu zetu na sisi wenyewe tulishindwa kuibeba? Badala yake, sisi tunaamini kwamba tunaokolewa kupitia fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu katika njia ileile wanayookolewa.” (Mdo. 15:10, 11) Kwa kweli wale waliopendekeza tohara, walikuwa ‘wakimjaribu Mungu.’ Walitaka kuwabebesha Watu wa Mataifa mfumo wa sheria ambao Wayahudi wenyewe hawakuwa wakifuata kikamili, na kwa sababu hiyo walistahili kufa. (Gal. 3:10) Badala yake, Wayahudi waliomsikiliza Petro walipaswa kuthamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu kupitia Yesu.

      21. Barnaba na Paulo walisimulia mambo gani yaliyowasaidia akina ndugu kufanya uamuzi mzuri?

      21 Bila shaka, maneno ya Petro yalikuwa yenye kusadikisha sana, hivi kwamba “kikundi chote kikanyamaza.” Kisha, Barnaba na Paulo wakasimulia “ishara nyingi na mambo ya ajabu ambayo Mungu alifanya kupitia kwao miongoni mwa mataifa.” (Mdo. 15:12) Sasa, mitume na wanaume wazee wangeweza kuchanganua uthibitisho wote uliotolewa na kufanya uamuzi ambao ungeonyesha waziwazi mapenzi ya Mungu kuhusu suala hilo la tohara.

      22-24. (a) Baraza Linaloongoza leo, linafuata jinsi gani mfano uliowekwa na baraza linaloongoza la karne ya kwanza? (b) Wazee wote wanaweza kuonyeshaje kwamba wanashughulikia mambo kwa njia ya Yehova?

      22 Leo, washiriki wa Baraza Linaloongoza wanapokutana, wanachunguza Neno la Mungu ili kupata mwongozo, na kusali kwa bidii ili wapate roho takatifu. (Zab. 119:105; Mt. 7:7-11) Ndiyo sababu kila mshiriki wa Baraza Linaloongoza hupokea ajenda mapema ili aweze kutafakari na kusali kuhusu mambo yatakayozungumziwa. (Met. 15:28) Wanapokutana, ndugu hao watiwa-mafuta huzungumza kwa uhuru na kwa heshima. Biblia hutumiwa mara nyingi katika mazungumzo yao.

      23 Wazee wa kutaniko wanapaswa kuiga mfano huo. Ikiwa kuna jambo zito ambalo wameshindwa kulitatua katika mkutano wa wazee, baraza la wazee linaweza kuwasiliana na ofisi ya tawi au mwakilishi aliyewekwa rasmi na ofisi ya tawi, kama vile, mwangalizi wa mzunguko. Ikihitajika, ofisi ya tawi italiandikia Baraza Linaloongoza.

      24 Yehova huwabariki wanyenyekevu, washikamanifu na wenye subira na wale wanaofuata kwa hiari miongozo inayotolewa kwenye tengenezo na kutanikoni. Kama tutakavyoona katika sura inayofuata, Mungu huwapa wote wanaofanya hivyo amani ya kweli, ufanisi wa kiroho, na umoja wa Kikristo.

      a Ona sanduku “Mafundisho ya Wayudaiza.”

      b Agano la tohara halikuwa sehemu ya agano la Kiabrahamu linalotumika mpaka leo. Agano la Kiabrahamu lilianzishwa mwaka wa 1943 K.W.K., wakati ambapo Abrahamu (aliyekuwa akiitwa Abramu), alivuka Mto Efrati akielekea Kanaani. Alikuwa na umri wa miaka 75. Agano la tohara lilianzishwa baadaye, mwaka wa 1919 K.W.K., Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 99.​—Mwa. 12:1-8; 17:1, 9-14; Gal. 3:17.

      c Inaonekana kwamba Tito, Mkristo Mgiriki ambaye baadaye alifanya kazi bega kwa bega na Paulo, alikuwa miongoni mwa wale waliotumwa Yerusalemu. (Gal. 2:1; Tito 1:4) Alikuwa Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa, lakini alitiwa mafuta kwa roho takatifu na alikuwa ndugu mwenye mfano mzuri.​—Gal. 2:3.

      d Ona sanduku lenye kichwa ‘Imani ya Mashahidi wa Yehova Inategemea Biblia.’

  • “Tumefikia Kauli Moja”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 14

      “Tumefikia Kauli Moja”

      Jinsi baraza linaloongoza lilivyofikia uamuzi na jinsi uamuzi huo ulivyoyaunganisha makutaniko

      Matendo 15:13-35

      1, 2. (a) Ni maswali gani mazito ambayo baraza linaloongoza la kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza linahitaji kuyashughulikia? (b) Ni nini kilichowasaidia ndugu hao kufanya uamuzi unaofaa?

      KIMYA kimetanda! Mitume na wazee waliokusanyika katika chumba kimoja jijini Yerusalemu watazamana, wakijua kwamba suala lililo mbele yao ni zito. Suala la tohara limetokeza maswali kadhaa mazito. Je, Wakristo wako chini ya Sheria ya Musa? Je, kunapaswa kuwa na tofauti yoyote kati ya Wakristo Wayahudi na Wakristo wa Mataifa?

      2 Wanaume hao wanaoongoza wamesikia uthibitisho mbalimbali. Wanakumbuka unabii wa Neno la Mungu na mambo yaliyoonwa yenye kusadikisha, yanayoonyesha baraka za Yehova. Kila mmoja ameeleza waziwazi maoni yake na wana habari zote wanazohitaji ili kufanya uamuzi. Roho takatifu ya Yehova iko juu yao. Je, wanaume hao watakubali mwongozo wa roho hiyo?

      3. Tunaweza kufaidikaje kwa kuchunguza masimulizi ya Matendo sura ya  15?

      3 Ili kukubali mwongozo wa roho takatifu, wanaume hao wanahitaji kuwa na imani ya kweli na ujasiri. Huenda uamuzi wao ukazidisha chuki ya viongozi wa dini ya Kiyahudi. Isitoshe, wangekabili upinzani kutoka kwa watu fulani ndani ya kutaniko ambao waliazimia kuwalazimisha watu wa Mungu waendelee kuishika Sheria ya Musa. Baraza linaloongoza litafanya nini? Acheni tuone. Tunapochanganua habari hii, tutaona jinsi wanaume hao waaminifu walivyoweka mfano mzuri unaoweza kuigwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo. Ni mfano ambao sisi pia tunapaswa kuiga tunapohitaji kufanya uamuzi au tunapokabili hali fulani ngumu katika maisha yetu ya Kikristo.

      “Maneno ya Manabii Yanaunga Mkono Jambo Hilo” (Mdo. 15:13-21)

      4, 5. Yakobo alinukuu maneno gani ya manabii?

      4 Mwanafunzi Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, akaanza kuzungumza.a Inaonekana alikuwa mwenyekiti katika mkutano huo. Huenda maneno yake yalikuwa muhtasari wa mambo waliyokubaliana wakiwa baraza. Yakobo akawaambia hivi wanaume waliokusanyika: “Simioni amesimulia kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya Manabii yanaunga mkono jambo hilo.”​—Mdo. 15:14, 15.

      5 Huenda baada ya kusikiliza hotuba ya Simioni, au Simoni Petro, na uthibitisho uliotolewa na Barnaba na Paulo, Yakobo alikumbuka maandiko kadhaa yaliyotaja jambo hilo muhimu lililozungumziwa. (Yoh. 14:26) Baada ya kusema “maneno ya Manabii yanaunga mkono jambo hilo,” Yakobo akanukuu maneno ya Amosi 9:11, 12. Kitabu hicho kiliorodheshwa kati ya Maandiko ya Kiebrania yanayoitwa “Manabii.” (Mt. 22:40; Mdo. 15:16-18) Utaona kwamba maneno yaliyonukuliwa na Yakobo yanatofautiana kidogo na yale yaliyo katika kitabu cha Amosi leo. Huenda Yakobo alinukuu Septuajinti, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania.

      6. Maandiko yaliwasaidiaje akina ndugu kujua mapenzi ya Mungu?

      6 Kupitia nabii Amosi, Yehova alitabiri kwamba angesimamisha “kibanda cha Daudi,” yaani, ukoo wa kifalme ambao hatimaye ungetokeza Ufalme wa Kimasihi. (Eze. 21:26, 27) Je, Yehova angeshughulika tena kwa njia ya pekee na Wayahudi wa asili? Hapana. Unabii huo unasema kwamba “watu wa mataifa yote” watakusanywa pamoja wakiwa “watu wanaoitwa kwa jina [la Mungu].” Kumbuka, Petro alitoa ushahidi kwamba Mungu “hakutofautisha hata kidogo kati yetu [Wakristo Wayahudi] na wao [Watu wa Mataifa walioamini], bali aliisafisha mioyo yao kwa imani.” (Mdo. 15:9) Kwa hiyo, mapenzi ya Mungu ni kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa, wawe warithi wa Ufalme. (Rom. 8:17; Efe. 2:17-19) Hakuna unabii wowote ulioongozwa kwa roho unaoonyesha kwamba waamini wasio Wayahudi walipaswa kwanza kutahiriwa au kugeuzwa imani kabla ya kuwa warithi wa Ufalme.

      7, 8. (a) Yakobo alipendekeza nini? (b) Yakobo alimaanisha nini aliposema “uamuzi wangu”?

      7 Akichochewa na uthibitisho huo wa Maandiko na mambo yenye kusadikisha aliyosikia, Yakobo akapendekeza hivi: “Kwa hiyo uamuzi wangu ni kutowataabisha watu wa mataifa wanaomgeukia Mungu, bali kuwaandikia wajiepushe na vitu vilivyochafuliwa na sanamu, na uasherati, na vitu vilivyonyongwa, na damu. Kwa maana tangu nyakati za kale kuna watu ambao wamekuwa wakihubiri kumhusu Musa katika kila jiji, kwa sababu yeye husomwa kwa sauti kubwa katika masinagogi kila sabato.”​—Mdo. 15:19-21.

      8 Yakobo aliposema “kwa hiyo uamuzi wangu,” je, alikuwa akitumia mamlaka yake—labda kwa sababu alikuwa mwenyekiti wa mkutano huo—ili kuwalazimisha wale ndugu wengine wakubaliane na jambo analosema? Hapana! Katika Kigiriki, neno linalotafsiriwa “uamuzi wangu,” linaweza pia kumaanisha “nafikiria” au “maoni yangu ni.” Hivyo basi, Yakobo hakuwa akitoa uamuzi kwa niaba ya baraza zima, bali, baada ya kusikia ushahidi uliotolewa na Maandiko yaliyochunguzwa alipendekeza hatua inayoweza kuchukuliwa.

      9. Pendekezo la Yakobo lilikuwa na manufaa gani?

      9 Je, Yakobo alitoa pendekezo zuri? Bila shaka, kwa sababu baadaye mitume na wazee waliamua kufuata pendekezo hilo. Uamuzi huo ungetimiza nini? Kwa upande mmoja, ‘haungewataabisha’ Wakristo wasio Wayahudi kwa kuwalazimisha kufuata matakwa ya Sheria ya Musa. (Mdo. 15:19) Kwa upande mwingine, uamuzi huo ungeheshimu dhamiri za Wakristo Wayahudi, ambao kwa muda mrefu walisikia “Musa . . . [akisomwa] kwa sauti kubwa katika masinagogi kila sabato.”b (Mdo. 15:21) Kwa kweli pendekezo hilo lingeleta umoja kati ya Wakristo Wayahudi na Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa. Zaidi ya yote, lingempendeza Yehova Mungu kwa kuwa linapatana na kusudi lake. Hiyo ilikuwa njia nzuri ya kutatua tatizo lililohatarisha umoja na hali njema ya kutaniko zima la watu wa Mungu! Nao ni mfano mzuri kwa kutaniko la Kikristo leo!

      Albert Schroeder akitoa hotuba katika kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1998

      10. Baraza Linaloongoza leo, linafuata jinsi gani mfano uliowekwa na baraza linaloongoza la karne ya kwanza?

      10 Kama tulivyoona katika Sura ya 13, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo hufuata mfano uliowekwa katika karne ya kwanza, kwa kumtegemea Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, na Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, ili kupata mwongozo katika mambo yote.c (1 Kor. 11:3) Wanafanyaje hivyo? Albert D. Schroeder, aliyetumikia katika Baraza Linaloongoza tangu mwaka wa 1974 hadi alipofikia mwisho wa maisha yake hapa duniani Machi 2006, alieleza: “Baraza Linaloongoza huanza mkutano wao wa Jumatano kwa sala ili kuomba mwongozo wa roho ya Yehova. Baraza Linaloongoza huhakikisha kwamba kila jambo linalozungumziwa na uamuzi unaofanywa unapatana na Neno la Mungu Biblia.” Naye Milton G. Henschel, aliyekuwa mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza ambaye alikufa Machi 2003 na kwenda mbinguni, aliwauliza swali lenye kuchochea fikira wahitimu wa darasa la 101 la Shule ya Gileadi. Aliwauliza, “Je, kuna tengenezo lingine duniani ambalo Baraza lake Linaloongoza hutumia ushauri kutoka katika Neno la Mungu, Biblia, kabla ya kufanya maamuzi muhimu?” Hakuna.

      “Kuwatuma Wanaume Waliochaguliwa” (Mdo. 15:22-29)

      11. Uamuzi wa baraza linaloongoza ulifikaje makutanikoni?

      11 Baraza linaloongoza huko Yerusalemu, lilifanya uamuzi wa pamoja kuhusu suala la tohara. Hata hivyo, ili akina ndugu makutanikoni watende kwa umoja, walihitaji kujulishwa uamuzi huo kwa njia iliyo wazi na yenye kutia moyo. Ni njia gani iliyotumiwa? Masimulizi hayo yanaeleza: “Ndipo mitume na wazee, pamoja na kutaniko lote wakaamua kuwatuma wanaume waliochaguliwa kutoka miongoni mwao waende Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba; waliwatuma Yuda aliyeitwa Barsaba, na Sila, wanaume waliokuwa wakiongoza kati ya akina ndugu.” Pia, wanaume waliotumwa walipewa barua ambayo ingesomwa katika makutaniko yote ya Antiokia, Siria, na Kilikia.​—Mdo. 15:22-26.

      12, 13. Ni mambo gani mazuri yaliyotimizwa baada ya (a) Yuda na Sila kutumwa? (b) baraza linaloongoza kutuma barua?

      12 Wakiwa “wanaume waliokuwa wakiongoza kati ya akina ndugu,” Yuda na Sila, walistahili kuliwakilisha baraza linaloongoza. Wanaume wanne wangethibitisha kwamba habari waliyokuwa nayo haikuwa tu jibu la swali lililoulizwa bali ni maagizo ya baraza linaloongoza. Kuwepo kwa ‘wanaume hao waliochaguliwa’ kungesaidia kuleta umoja kati ya Wakristo Wayahudi waliokuwa Yerusalemu na Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa waliokuwa katika maeneo mengine. Huo ulikuwa mpango mzuri na wenye upendo. Bila shaka, ulichangia umoja na amani kati ya watu wa Mungu.

      JINSI BARAZA LINALOONGOZA LILIVYOPANGWA LEO

      Kama Wakristo wa karne ya kwanza, Mashahidi wa Yehova leo wanaongozwa na Baraza Linaloongoza lenye wanaume waliotiwa mafuta kwa roho. Baraza Linaloongoza hukutana kila juma. Washiriki wa baraza hilo wamepangwa katika halmashauri sita zifuatazo, kila halmashauri ikiwa na jukumu tofauti.

      • Halmashauri ya Waratibu inasimamia mambo ya kisheria na inatumika kutoa habari sahihi kuhusu imani yetu kwenye vyombo vya habari inapohitajika kufanya hivyo. Hushughulikia pia majanga, mateso, na mambo mengine ya dharura yanayowapata Mashahidi wa Yehova mahali popote duniani.

      • Halmashauri ya Wafanyakazi hushughulikia hali ya kiroho na ya kimwili ya washiriki wa familia ya Betheli wanaotumikia kwenye ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Pia, halmashauri hii huidhinisha washiriki wapya wa Betheli wanapoalikwa kutumikia katika ofisi za tawi.

      • Halmashauri ya Utangazaji husimamia uchapishaji, utangazaji, na usafirishaji wa vitabu na magazeti yanayotegemea Biblia. Inasimamia viwanda vya uchapishaji na majengo yanayomilikiwa na kuendeshwa na mashirika yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova na ujenzi wa majengo ya ofisi za tawi, Majumba ya Ufalme na ya Kusanyiko. Halmashauri hii husimamia matumizi ya michango pia.

      • Halmashauri ya Utumishi inasimamia kazi ya kuhubiri pamoja na mambo yanayohusu wazee wa makutaniko, waangalizi wa mzunguko, na watumishi wa wakati wote. Pia, halmashauri hii huwaalika na kuwapatia migawo wanafunzi wa Shule ya Gileadi, ambayo kusudi lake ni kuimarisha kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.

      • Halmashauri ya Ufundishaji inasimamia ufundishaji katika makusanyiko na mikutano ya kutaniko, na pia programu zinazorekodiwa katika video na sauti. Hupanga mitaala ya Shule ya Gileadi, Shule ya Utumishi wa Painia, na shule nyingine. Pia, hutayarisha programu zinazotegemea Biblia kwa ajili ya wajitoleaji katika ofisi za tawi.

      • Halmashauri ya Uandikaji inasimamia utayarishaji wa chakula cha kiroho kwa ajili ya makutaniko na watu wote. Pia, halmashauri hii hujibu maswali ya Biblia, husimamia kazi ya kutafsiri ulimwenguni pote, na huidhinisha hati za drama na mihtasari ya hotuba.

      Baraza Linaloongoza hutegemea roho takatifu ya Mungu. Washiriki wa baraza hilo hawajioni kuwa viongozi wa Mashahidi wa Yehova. Badala yake, sawa na Wakristo wengine wote watiwa-mafuta walio duniani, ‘wanaendelea kumfuata Mwanakondoo, Yesu Kristo, popote anapoenda.’​—Ufu. 14:4.

      13 Barua hizo zilikuwa na maagizo yaliyokuwa wazi kwa ajili ya Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa kuhusu suala la tohara na mambo waliyopaswa kufanya ili kupata baraka na kibali cha Yehova. Sehemu muhimu ya barua hiyo ilisema: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumeona ni vizuri tusiwaongezee ninyi mzigo zaidi ila mambo haya ya lazima: kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu, na damu, na vitu vilivyonyongwa, na uasherati. Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya, mtafanikiwa. Afya njema kwenu!”​—Mdo. 15:28, 29.

      14. Inawezekanaje kwa watu wa Yehova kufanya kazi kwa umoja katika ulimwengu huu uliogawanyika?

      14 Leo, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 8,000,000, katika makutaniko zaidi ya 100,000 ulimwenguni pote, wanaamini na kutenda kwa umoja. Kwa kuwa ulimwengu wa leo umejaa misukosuko na migawanyiko, inawezekanaje kuwa na umoja huo? Kwanza kabisa, umoja huo unatokana na mwongozo ulio wazi ambao Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, anatoa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” yaani, Baraza Linaloongoza. (Mt. 24:45-47) Umoja huo pia unawezekana kwa sababu ndugu ulimwenguni pote hufuata kwa hiari mwongozo wa Baraza Linaloongoza.

      “Wakashangilia kwa Sababu ya Kutiwa Moyo” (Mdo. 15:30-35)

      15, 16. Suala la tohara lilitatuliwaje, na kwa nini uamuzi uliofikiwa ulikuwa na matokeo mazuri?

      15 Kitabu cha Matendo kinaendelea kusema kwamba ndugu hao waliotumwa kutoka Yerusalemu walipofika Antiokia, “wakakusanya kundi lote pamoja na kuwapa barua hiyo.” Akina ndugu waliitikiaje mwongozo huo wa baraza linaloongoza? “Baada ya kuisoma[barua hiyo], wakashangilia kwa sababu ya kutiwa moyo.” (Mdo. 15:30, 31) Isitoshe, Yuda na Sila “wakawatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwaimarisha.” Wanaume hao wawili walikuwa “manabii,” kama vile Barnaba, Paulo na wengine walioitwa manabii—walipewa jina hilo kwa sababu walikuwa wakitangaza au kujulisha mapenzi ya Mungu.​—Mdo. 13:1; 15:32; Kut. 7:1, 2.

      16 Ilionekana wazi kwamba Yehova alibariki uamuzi wa baraza linaloongoza na hivyo suala hilo likatatuliwa vizuri. Kwa nini matokeo yalikuwa mazuri? Kwa sababu ya mwongozo ulio wazi na unaotegemea Neno la Mungu na roho takatifu uliotolewa na baraza linaloongoza kwa wakati unaofaa. Sababu nyingine ni kwamba makutaniko yalijulishwa moja kwa moja na kwa upendo kuhusu uamuzi huo.

      17. Waangalizi wa mzunguko leo hufuata mfano gani?

      17 Leo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hufuata mfano huo kwa kuwapa ndugu ulimwenguni pote mwongozo kwa wakati unaofaa. Uamuzi fulani unapofanywa, makutaniko hujulishwa moja kwa moja na kwa njia inayoeleweka wazi. Njia moja ni kupitia ziara za waangalizi wa mzunguko. Ndugu hao wanaojitolea kwa moyo wote, hutembelea makutaniko wakiyatia moyo na kutoa mwelekezo. Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, wao pia hutumia wakati mwingi “wakifundisha na kutangaza habari njema ya neno la Yehova, wakiwa pamoja na wengine wengi.” (Mdo. 15:35) Kama Yuda na Sila, wanawaimarisha akina ndugu na kuwatia ‘moyo kwa hotuba nyingi.’

      18. Watu wa Yehova wanawezaje kuendelea kupokea baraka zake?

      18 Kwa upande mwingine, ni nini kitakachoyawezesha makutaniko ulimwenguni pote kuendelea kuwa na amani na umoja katika ulimwengu uliogawanyika leo? Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi baadaye: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii . . . Zaidi ya hayo, tunda la uadilifu hupandwa katika hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” (Yak. 3:17, 18) Hatujui ikiwa kilichomchochea kuandika hivyo ni ule mkutano wa Yerusalemu au la. Hata hivyo, matukio yanayozungumziwa katika Matendo sura ya 15 yanaonyesha wazi kwamba Yehova hubariki roho ya umoja na ushirikiano.

      19, 20. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba kulikuwa na amani na umoja katika kutaniko la Antiokia? (b) Paulo na Barnaba wangeweza kufanya nini sasa?

      19 Ni wazi kwamba kulikuwa na amani na umoja katika kutaniko la Antiokia. Badala ya kubishana na ndugu waliotumwa kutoka Yerusalemu, akina ndugu wa Antiokia walithamini sana kutembelewa na Yuda na Sila. Ndugu wa Antiokia hawakuwaruhusu waondoke. Hata hivyo, “baada ya kukaa huko kwa muda fulani, ndugu hao wakawaacha warudi kwa amani kwa wale waliokuwa wamewatuma,” yaani, warudi Yerusalemu.d (Mdo. 15:33) Bila shaka, ndugu waliokuwa Yerusalemu walifurahi pia walipowasikia Yuda na Sila wakisimulia matokeo ya safari yao. Fadhili zisizostahiliwa za Yehova ziliwawezesha kuutimiza mgawo wao!

      20 Paulo na Barnaba, ambao walibaki Antiokia, wangeweza sasa kukazia fikira kazi ya kuhubiri kama vile waangalizi wa mzunguko wanavyofanya wanapotembelea makutaniko. (Mdo. 13:2, 3) Ndugu hao ni baraka kubwa sana! Hata hivyo, Yehova aliwatumia waeneza-injili hao wawili wenye bidii kutimiza mambo gani zaidi? Tutaona katika sura inayofuata.

      Mama na binti yake wakiwa kusanyikoni, wakitazama buku la 2 la kitabu “Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.”

      Leo, Wakristo hufaidika kutokana na maagizo kutoka kwa Baraza Linaloongoza na wawakilishi wake

      YAKOBO—“NDUGU YA BWANA”

      Yakobo, mwana wa Yosefu na Maria, anatajwa kwanza kati ya ndugu wa kambo wa Yesu. (Mt. 13:54, 55) Kwa hiyo huenda alikuwa mwana wa pili wa Maria. Yakobo alilelewa pamoja na Yesu, alimwona akihubiri, na alijua kwamba Yesu alifanya ‘matendo yenye nguvu.’ Hatujui ikiwa alijionea miujiza hiyo au la. Hata hivyo, wakati wa huduma ya Yesu, Yakobo na ndugu zake “hawakuwa wakimwamini,” ndugu yao mkubwa. (Yoh. 7:5) Huenda Yakobo alikuwa na maoni yaliyofanana na baadhi ya watu wa ukoo wa Yesu waliosema hivi kumhusu: “Amerukwa na akili.”​—Marko 3:21.

      Yakobo akisoma kitabu cha kukunjwa.

      Yote hayo yalibadilika baada ya Yesu kufa na kufufuliwa. Ingawa kuna watu wengine watatu wanaoitwa Yakobo katika Maandiko ya Kigiriki, inaonekana kwamba katika kile kipindi cha siku 40 baada ya kufufuliwa, Yesu alimtokea Yakobo aliyekuwa ndugu yake wa kambo. (1 Kor. 15:7) Huenda hilo lilimfanya Yakobo amfahamu vizuri zaidi ndugu yake mkubwa. Vyovyote vile, siku 10 hivi baada ya Yesu kurudi mbinguni, Yakobo, mama yake, na ndugu zake walikuwa wamekusanyika pamoja na mitume wengine katika chumba cha juu wakisali.​—Mdo. 1:13, 14.

      Baadaye, Yakobo alikuja kuwa mshiriki aliyeheshimiwa sana katika kutaniko la Yerusalemu, akionwa kuwa mtume katika kutaniko hilo. (Gal. 1:18, 19) Ni wazi kwamba Yakobo alikuwa mtu muhimu kutanikoni kwa sababu baada ya mtume Petro kufunguliwa kimuujiza kutoka gerezani, aliwaambia hivi wanafunzi: “Waambieni Yakobo na akina ndugu mambo haya.” (Mdo. 12:12, 17) Suala la tohara lilipofikishwa mbele ya “mitume na wazee” jijini Yerusalemu, inaonekana Yakobo ndiye aliyekuwa mwenyekiti wa mazungumzo hayo. (Mdo. 15:6-21) Pia, mtume Paulo alisema kwamba Yakobo, Kefa (Petro) na Yohana “walionekana kuwa nguzo” za kutaniko la Yerusalemu. (Gal. 2:9) Baada ya miaka kadhaa, Paulo alirudi Yerusalemu kutoka katika safari yake ya tatu ya umishonari, na aliposimulia kuhusu huduma yake, “Yakobo, na wazee wote walikuwapo.”​—Mdo. 21:17-19.

      Inaonekana Yakobo huyu, ambaye Paulo anamwita “ndugu ya Bwana,” ndiye aliyeandika barua, au kitabu cha Biblia, kinachoitwa kwa jina lake. (Gal. 1:19) Katika barua hiyo, Yakobo hajitambulishi kama mtume wala ndugu ya Yesu, bali kwa unyenyekevu anajiita “mtumwa wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo.” (Yak. 1:1) Kama Yesu, Yakobo alichunguza kwa makini vitu vya asili na tabia za wanadamu. Alilinganisha kweli za Mungu na vitu vya asili kama vile bahari inayoendeshwa na upepo, anga lenye nyota, jua kali, maua, moto, na wanyama wa kufugwa. (Yak. 1:6, 11, 17; 3:5, 7) Kwa kuwa aliongozwa na roho ya Mungu kuelewa vizuri mitazamo na matendo ya watu, alitoa ushauri mzuri kuhusu jinsi ya kuwa na mahusiano mazuri na wengine.​—Yak. 1:19, 20; 3:2, 8-18.

      Maneno ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 9:5 yanadokeza kwamba Yakobo alikuwa na mke. Biblia haisemi Yakobo alikufa lini au jinsi gani. Hata hivyo, mwanahistoria Myahudi Yosefo aliandika kwamba muda mfupi baada ya kifo cha Gavana Mroma Porkio Festo mwaka wa 62 hivi W.K., na kabla ya Albino kuwa gavana, kuhani mkuu Ananu (Anania) “aliitisha kikao cha Sanhedrini na kumleta mbele yao Yakobo, ndugu ya Yesu aliyekuwa akiitwa Kristo, pamoja na wengine.” Kulingana na Yosefo, Ananu “alidai kuwa wamevunja sheria kisha akawatoa ili wapigwe mawe.”

      a Ona sanduku lenye kichwa “Yakobo—‘Ndugu ya Bwana.’”

      b Yakobo alirejelea kwa busara maandishi ya Musa ambayo zaidi ya kuwa na Sheria, yalitia ndani masimulizi ya jinsi Mungu alivyoshughulika na watu wake na maoni yake kabla ya Sheria kutolewa. Kwa mfano, maoni ya Mungu kuhusu damu, uzinzi, na ibada ya sanamu yanaonekana wazi katika kitabu cha Mwanzo. (Mwa. 9:3, 4; 20:2-9; 35:2, 4) Hivyo, Yehova alionyesha kanuni zinazowahusu wanadamu wote iwe ni Wayahudi au Watu wa Mataifa.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Jinsi Baraza Linaloongoza Lilivyopangwa Leo.”

      d Katika mstari wa 34, tafsiri fulani za Biblia husema kwamba Sila aliamua kubaki Antiokia. (Union Version) Hata hivyo, inaonekana kwamba maneno hayo yaliongezwa baadaye.

  • “Kuyaimarisha Makutaniko”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 15

      ‘Kuyaimarisha Makutaniko’

      Waangalizi wa mzunguko huyasaidia makutaniko yawe na imani yenye nguvu

      Matendo 15:36–16:5

      1-3. (a) Paulo anasafiri na nani, na mwandamani huyo ni mtu wa aina gani? (b) Tutajifunza nini katika sura hii?

      WANAPOVUKA milima na mabonde kutoka mji mmoja hadi mwingine, mtume Paulo anamfikiria kijana anayesafiri pamoja naye. Kijana huyo ni Timotheo mwenye umri wa miaka 20 hivi. Kadiri kijana huyo anavyotembea katika safari hii ndivyo anavyokuwa mbali zaidi na nyumbani kwao. Kadiri siku inavyopita, ndivyo wanavyozidi kuwa mbali na majiji ya Listra na Ikoniamu. Ni mambo gani yatakayotokea? Huenda Paulo alijua kwa sababu hii ni safari yake ya pili ya umishonari. Anajua kwamba kutakuwa na hatari na matatizo mengi. Timotheo atatendaje atakapokabili hali hizo?

      2 Paulo anamwamini Timotheo, labda kuliko Timotheo anavyojiamini. Matukio ya karibuni yalimfanya Paulo aone umuhimu wa kuchagua mwandamani anayefaa. Paulo anajua kwamba kazi ya kutembelea makutaniko na kuyatia nguvu, inahitaji waangalizi walio thabiti na wenye nia moja. Kwa nini? Huenda sababu moja ni kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulikosababisha mgawanyiko.

      3 Katika sura hii tutajifunza mengi kuhusu njia bora ya kutatua kutoelewana. Pia, tutajua ni kwa nini Paulo alichagua kusafiri na Timotheo, nasi tutajifunza mengi kuhusu kazi muhimu inayotimizwa na waangalizi wa mzunguko.

      “Turudi Tukawatembelee Akina Ndugu” (Mdo. 15:36)

      4. Paulo alikusudia kufanya nini katika safari yake ya pili ya umishonari?

      4 Katika sura iliyotangulia tuliona jinsi ndugu wanne, Paulo, Barnaba, Yuda, na Sila, walivyolitia nguvu kutaniko la Antiokia kwa kulijulisha uamuzi wa baraza linaloongoza kuhusu suala la tohara. Paulo alifanya nini baadaye? Alimwendea Barnaba akiwa na mikakati mipya ya safari, akamwambia: “Turudi tukawatembelee akina ndugu katika kila jiji ambalo tulitangaza neno la Yehova tuone jinsi wanavyoendelea.” (Mdo. 15:36) Paulo hakuwa akipendekeza wawatembelee Wakristo hao wapya kirafiki tu. Kitabu cha Matendo kinaonyesha wazi kusudi halisi la safari ya pili ya umishonari ya Paulo. Kwanza, kuyajulisha makutaniko maagizo yaliyotolewa na baraza linaloongoza. (Mdo. 16:4) Pili, akiwa mwangalizi wa mzunguko, Paulo alikuwa ameazimia kuyajenga makutaniko kiroho, na kusaidia kuimarisha imani yao. (Rom. 1:11, 12) Tengenezo la Mashahidi wa Yehova linafanyaje hivyo leo?

      5. Baraza Linaloongoza huwasiliana na makutaniko na kuyatia moyo jinsi gani?

      5 Leo, Kristo anatumia Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kuongoza kutaniko lake. Kupitia barua, machapisho ya mtandaoni na yaliyochapishwa, mikutano, na njia nyingine, ndugu hao watiwa-mafuta huyaongoza na kuyatia moyo makutaniko ulimwenguni pote. Pia, Baraza Linaloongoza hujitahidi kudumisha mawasiliano pamoja na kila kutaniko. Ili kufanya hivyo, wanatumia waangalizi wa mzunguko. Baraza Linaloongoza huwaweka rasmi maelfu ya wazee wanaostahili ulimwenguni pote kuwa waangalizi wa mzunguko.

      6, 7. Waangalizi wa mzunguko wana majukumu gani?

      6 Waangalizi wa mzunguko leo huwahangaikia na kuwatia moyo wote katika makutaniko wanayotembelea. Jinsi gani? Kwa kufuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza kama Paulo. Alimhimiza hivi mwangalizi mwenzake: “Lihubiri neno; fanya hivyo kwa uharaka katika nyakati zinazofaa na nyakati ngumu; karipia, kemea, himiza, kwa subira yote na ustadi wa kufundisha. . . . Fanya kazi ya mweneza-injili.”​—2 Tim. 4:2, 5.

      7 Waangalizi wa mzunguko—pamoja na wake zao ikiwa wameoa—hutii maneno hayo kwa kushiriki katika huduma ya shambani pamoja na wahubiri wa kutaniko wanalotembelea. Kwa sababu wao ni walimu stadi, na wanapenda huduma, mfano wao unawachochea ndugu na dada. (Rom. 12:11; 2 Tim. 2:15) Waangalizi wa mzunguko huonyesha upendo usio na ubinafsi na kujidhabihu. Huwatumikia wengine kwa hiari, nyakati nyingine wanasafiri wakati ambapo kuna hali mbaya ya hewa na hata katika maeneo yenye hatari. (Flp. 2:3, 4) Pia, waangalizi wa mzunguko hutia moyo, hufundisha, na kuonya makutaniko kupitia hotuba zinazotegemea Biblia. Ni vizuri kwa wote kutanikoni kutafakari mfano mzuri wa waangalizi hao na kujitahidi kuiga imani yao.​—Ebr. 13:7.

      “Wakagombana kwa Ukali” (Mdo. 15:37-41)

      8. Barnaba aliitikiaje mwaliko wa Paulo?

      8 Barnaba alikubali pendekezo la Paulo la ‘kuwatembelea akina ndugu.’ (Mdo. 15:36) Wawili hao walifanya kazi bega kwa bega wakisafiri pamoja, na tayari walijua maeneo na watu waliohitaji kutembelewa. (Mdo. 13:2–14:28) Kwa hiyo, huenda waliona ingefaa wasafiri pamoja kwa ajili ya mgawo huo. Hata hivyo, tatizo likatokea. Andiko la Matendo 15:37 linasema: “Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Yohana, aliyeitwa Marko.” Barnaba hakuwa akitoa pendekezo. “Alikuwa ameazimia” waende pamoja binamu yake, Marko, katika safari hiyo ya umishonari.

      9. Kwa nini Paulo na Barnaba hawakuelewana?

      9 Paulo hakukubali. Kwa nini? Masimulizi yanasema: “Lakini Paulo hakutaka waende pamoja naye [Marko], kwa sababu alikuwa amewaacha huko Pamfilia na hakuenda pamoja nao kwenye kazi.” (Mdo. 15:38) Marko alikuwa amesafiri pamoja na Paulo na Barnaba katika safari yao ya kwanza ya umishonari lakini hakuendelea na safari hiyo mpaka mwisho. (Mdo. 12:25; 13:13) Mwanzoni katika safari yao ya kwanza, wakiwa Pamfilia, Marko aliuacha mgawo wake na kurudi nyumbani Yerusalemu. Biblia haisemi ni kwa nini aliondoka, lakini inaonekana kwamba mtume Paulo alimwona Marko kuwa mtu asiyechukua mambo kwa uzito. Huenda Paulo alikuwa na mashaka kuhusu kutegemeka kwa Marko.

      10. Kutoelewana kati ya Paulo na Barnaba kulisababisha nini, na matokeo yalikuwa nini?

      10 Hata hivyo, Barnaba alikuwa ameazimia kwenda na Marko. Na Paulo alikataa kwenda naye. Matendo 15:39 inasema: “Ndipo wakagombana kwa ukali hivi kwamba wakaachana.” Barnaba akapanda meli kuelekea Kipro, kisiwa cha nyumbani kwao, akiwa pamoja na Marko. Naye Paulo akaenda zake. Masimulizi hayo yanasema: “Paulo akamchagua Sila na kuondoka baada ya akina ndugu kumkabidhi kwenye fadhili zisizostahiliwa za Yehova.” (Mdo. 15:40) Wakasafiri pamoja ‘kupitia Siria na Kilikia, wakiyaimarisha makutaniko.’​—Mdo. 15:41.

      11. Ni sifa gani zinazohitajiwa ili kudumisha urafiki na mtu aliyetukosea?

      11 Huenda masimulizi hayo yakatukumbusha hali yetu ya kutokamilika. Paulo na Barnaba walikuwa wamewekwa rasmi kuwa wawakilishi wa pekee wa baraza linaloongoza. Inaonekana baadaye Paulo aliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa baraza hilo. Hata hivyo, ingawa Paulo na Barnaba walikuwa ndugu wazuri sana, wakati huu walishindwa kudhibiti hasira yao. Je, wangeruhusu hali hiyo ivunje kabisa urafiki wao? Ingawa hawakuwa wakamilifu, Paulo na Barnaba walikuwa wanyenyekevu, na walikuwa na akili ya Kristo. Ndiyo sababu baada ya muda mfupi, walionyesha roho ya undugu wa Kikristo na kusameheana. (Efe. 4:1-3) Baadaye, Paulo na Marko walifanya kazi pamoja katika migawo mingine ya Kikristo.a—Kol. 4:10.

      12. Kama Paulo na Barnaba, waangalizi wanapaswa kuwa na sifa gani?

      12 Tukio hilo moja halimaanishi kwamba Barnaba na Paulo walikuwa na utu huo. Barnaba alikuwa mwenye upendo na mkarimu sana hivi kwamba badala ya mitume kumwita kwa jina lake, Yosefu, walikuwa wakimwita Barnaba, yaani, “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Paulo alikuwa mpole na mwenye upendo mwororo. (1 The. 2:7, 8) Waangalizi Wakristo leo, kutia ndani waangalizi wa mzunguko, wanapaswa kujitahidi kuwa wanyenyekevu na kuwatendea wazee wenzao na kundi zima kwa wororo.​—1 Pet. 5:2, 3.

      “Alishuhudiwa Vema” (Mdo. 16:1-3)

      13, 14. (a) Timotheo alikuwa nani, na alikutana jinsi gani na Paulo? (b) Kwa nini Paulo alipendezwa na Timotheo? (c) Timotheo alipewa mgawo gani?

      13 Katika safari yake ya pili ya umishonari, Paulo alienda Galatia, mkoa wa Roma, ambako makutaniko kadhaa yalikuwa yameanzishwa. Mwishowe, “akafika Derbe na pia Listra.” Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Huko kulikuwa na mwanafunzi aliyeitwa Timotheo, mama yake alikuwa Myahudi aliyekuwa mwamini, lakini baba yake alikuwa Mgiriki.”​—Mdo. 16:1.b

      14 Inaonekana kwamba, Paulo alikuwa amekutana na familia ya Timotheo alipotembelea eneo hilo karibu mwaka wa 47 W.K. Baada ya miaka miwili au mitatu hivi, wakati wa safari yake ya pili, Paulo alipendezwa kwa njia ya pekee na kijana Timotheo. Kwa nini? Kwa sababu Timotheo “alishuhudiwa vema na akina ndugu.” Sifa nzuri za Timotheo zilijulikana kutanikoni kwao na hata katika makutaniko mengine. Masimulizi ya Matendo yanasema kwamba akina ndugu wa Listra na Ikoniamu, waliokuwa umbali wa kilomita 30 hivi, walijua sifa nzuri za Timotheo. (Mdo. 16:2) Wakiongozwa na roho takatifu, wazee walimpa kijana Timotheo mgawo mzito wa kusafiri pamoja na Paulo na Sila ili kufanya kazi nao.​—Mdo. 16:3.

      15, 16. Timotheo aliwezaje kupata sifa nzuri?

      15 Timotheo alipataje sifa nzuri hivyo akiwa kijana? Je, ni kwa sababu alikuwa na akili nyingi, sura nzuri, au vipawa vyake? Mara nyingi wanadamu huvutiwa na mambo kama hayo. Hata nabii Samweli alidanganyika wakati fulani kwa kuangalia mwonekano wa nje. Hata hivyo, Yehova alimkumbusha: “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona ndani ya moyo.” (1 Sam. 16:7) Timotheo alikuwa na sifa za ndani zilizowavutia Wakristo wenzake.

      16 Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo alirejelea sifa fulani za Timotheo. Paulo alitaja mtazamo wake mzuri, upendo wake wa kujidhabihu, na bidii yake katika kushughulikia migawo ya kiroho. (Flp. 2:20-22) Timotheo alijulikana pia kwa kuwa na ‘imani isiyo na unafiki.’​—2 Tim. 1:5.

      17. Vijana wanawezaje kumwiga Timotheo?

      17 Leo, vijana wengi humwiga Timotheo kwa kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu. Wanajifanyia jina zuri pamoja na Yehova na watu wake, hata wakiwa na umri mdogo. (Met. 22:1; 1 Tim. 4:15) Wanaonyesha imani isiyo na unafiki. (Zab. 26:4) Hivyo, vijana wengi, kama Timotheo, wanaweza kutimiza mengi katika kutaniko. Wanapostahili kuwa wahubiri wa habari njema na hatimaye kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, wao huwatia moyo wote wanaompenda Yehova!

      “Kuimarishwa Katika Imani” (Mdo. 16:4, 5)

      18. (a) Paulo na Timotheo walilisaidiaje baraza linaloongoza wakiwa wahudumu wanaosafiri? (b) Makutaniko yalipata baraka gani?

      18 Paulo na Timotheo walifanya kazi pamoja kwa miaka mingi. Wakiwa wahudumu wanaosafiri, walifanya mambo mbalimbali waliyoagizwa na baraza linaloongoza. Biblia inasema: “Walipokuwa wakipita katika majiji, walikuwa wakiwapa maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu ili wayashike.” (Mdo. 16:4) Bila shaka makutaniko yalifuata mwongozo wa mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu. Kwa sababu ya kutii “makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”​—Mdo. 16:5.

      19, 20. Kwa nini Wakristo wanapaswa kuwatii “wale wanaoongoza”?

      19 Leo pia Mashahidi wa Yehova hupata baraka nyingi wanapofuata mwongozo wa “wale wanaoongoza” kati yao. (Ebr. 13:17) Kwa kuwa tamasha ya ulimwengu huu inabadilika, Wakristo wanapaswa kukubali na kujitiisha chini ya mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; 1 Kor. 7:29-31) Tukifanya hivyo tutaepuka madhara ya kiroho na kubaki bila doa kutokana na ulimwengu.​—Yak. 1:27.

      20 Waangalizi Wakristo leo kutia ndani washiriki wa Baraza Linaloongoza si wakamilifu kama walivyokuwa Paulo, Barnaba, Marko na wazee wengine watiwa mafuta wa karne ya kwanza. (Rom. 5:12; Yak. 3:2) Hata hivyo, Baraza Linaloongoza linategemeka kwa sababu linashikamana kabisa na Neno la Mungu na kufuata mfano uliowekwa na mitume. (2 Tim. 1:13, 14) Matokeo ni kwamba makutaniko yanatiwa nguvu na kuimarishwa katika imani.

      TIMOTHEO ATUMIKA “KATIKA KUENDELEZA HABARI NJEMA”

      Paulo alithamini sana kazi nzuri iliyofanywa na Timotheo. Baada ya kufanya kazi pamoja kwa miaka 11 hivi, Paulo aliandika hivi kuhusu Timotheo: “Sina mtu mwingine aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mahangaiko yenu. . . . Ninyi mnajua jinsi alivyojithibitisha mwenyewe, kwamba kama mtoto na baba yake alitumikia pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” (Flp. 2:20, 22) Timotheo alijitolea ili kuendeleza kazi ya kuhubiri, na kwa sababu hiyo Paulo alimpenda sana naye ni mfano mzuri sana kwetu.

      Timotheo.

      Inaonekana kwamba Timotheo, ambaye baba yake alikuwa Mgiriki na mama yake Myahudi, alilelewa Listra. Tangu utotoni, Timotheo alikuwa amefundishwa Maandiko na mama yake, Eunike, na nyanya yake Loisi. (Mdo. 16:1, 3; 2 Tim. 1:5; 3:14, 15) Huenda Eunike, Loisi, na Timotheo walikubali kuwa Wakristo, Paulo alipotembelea Listra kwa mara ya kwanza.

      Paulo aliporudi miaka kadhaa baadaye, Timotheo, ambaye huenda alikuwa na umri wa miaka 20 hivi wakati huo, “alishuhudiwa vema na akina ndugu huko Listra na Ikoniamu.” (Mdo. 16:2) Roho ya Mungu iliongoza kutolewa kwa “unabii” kumhusu kijana huyo, na kulingana na unabii huo, Paulo na wazee wengine walipendekeza Timotheo afanye utumishi wa pekee. (1 Tim. 1:18; 4:14; 2 Tim. 1:6) Alipaswa kwenda pamoja na Paulo akiwa mmishonari. Timotheo angeiacha familia yao na pia alikubali kutahiriwa ili Wayahudi wasiwe na sababu yoyote ya kulalamika.​—Mdo. 16:3.

      Timotheo alisafiri sana. Alihubiri pamoja na Paulo na Sila huko Filipi, halafu akahubiri Beroya akiwa na Sila, kisha akahubiri Thesalonike akiwa peke yake. Walipokutana tena katika jiji la Korintho, Timotheo alimjulisha Paulo kuhusu upendo na uaminifu wa Wathesalonike licha ya dhiki walizokabili. (Mdo. 16:6–17:14; 1 The. 3:2-6) Paulo aliposikia habari mbaya kuhusu kutaniko la Korintho, alifikiria kumtuma Timotheo aende Korintho ili akawasaidie. (1 Kor. 4:17) Baadaye, Paulo akiwa Efeso aliwatuma Timotheo na Erasto waende Makedonia. Paulo aliwaandikia Waroma akiwa Korintho na alikuwa pamoja na Timotheo, aliyekuwa amerudi tena Korintho. (Mdo. 19:22; Rom. 16:21) Hayo ni baadhi ya maeneo ambayo Timotheo alienda ili kutimiza migawo yake.

      Inaonekana kwamba Timotheo alisita kwa kiasi fulani kutumia mamlaka yake, ndiyo sababu Paulo alimtia moyo hivi: “Usiruhusu kamwe mtu yeyote audharau ujana wako.” (1 Tim. 4:12) Hata hivyo, Paulo alimwamini Timotheo naye alimtuma aende katika kutaniko lililokuwa na matatizo na kumwagiza: “Uwaamuru watu fulani wasifundishe mambo tofauti.” (1 Tim. 1:3) Pia, Paulo alimpa Timotheo mamlaka ya kuwaweka rasmi waangalizi na watumishi wa huduma katika makutaniko.​—1 Tim. 5:22.

      Paulo alimpenda sana Timotheo kwa sababu ya sifa zake nzuri. Maandiko yanaonyesha kwamba kijana huyo alikuwa kama mwana kwa sababu alishirikiana na Paulo kwa ukaribu, uaminifu na kwa upendo. Paulo aliandika kwamba anakumbuka machozi ya Timotheo, anatamani kumwona, na anasali kwa ajili yake. Pia, akiwa kama baba mwenye kujali, Paulo alimpa Timotheo ushauri kuhusu ‘ugonjwa wake wa mara kwa mara’​—huenda ulikuwa ugonjwa wa tumbo.​—1 Tim. 5:23; 2 Tim. 1:3, 4.

      Paulo alipofungwa kwa mara ya kwanza huko Roma, Timotheo alikuwa pamoja naye. Timotheo pia alifungwa kwa muda fulani. (Flm. 1; Ebr. 13:23) Ni wazi kwamba wanaume hao walipendana kikweli, kwa sababu Paulo alipotambua kwamba anakaribia kufa, alimtumia Timotheo ujumbe huu: “Jitahidi kabisa ili uje kwangu upesi.” (2 Tim. 4:6-9) Maandiko hayasemi ikiwa Timotheo alifika kabla ya Paulo kufa, na kumwona tena mshauri wake mpendwa.

      MARKO APATA MAPENDELEO MENGI

      Injili ya Marko inasimulia kwamba wale waliomkamata Yesu walijaribu pia kumkamata “kijana fulani” aliyeponyoka, “akakimbia akiwa uchi.” (Marko 14:51, 52) Kwa kuwa Marko, ambaye pia anaitwa Yohana Marko, ndiye peke yake aliyeandika kuhusu tukio hilo, huenda kijana huyo ni yeye mwenyewe. Ikiwa ndivyo, basi Marko alikuwa amekutana kibinafsi na Yesu.

      Marko akisikiliza na kuandika mwanamume mzee anapoongea.

      Miaka 11 hivi baadaye, Herode Agripa alipokuwa akiwatesa Wakristo, “watu wengi” waliokuwa washiriki wa kutaniko la Yerusalemu walikuwa wamekusanyika katika nyumba ya Maria, mama ya Marko, wakisali. Petro alienda katika nyumba hiyo alipofunguliwa kimuujiza kutoka gerezani. (Mdo. 12:12) Hivyo, inawezekana kwamba Marko alilelewa katika nyumba ambayo baadaye ilitumiwa kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. Huenda aliwafahamu wanafunzi wa mwanzoni wa Yesu, nao walimsaidia sana kufanya maendeleo ya kiroho.

      Marko alitumikia bega kwa bega na waangalizi kadhaa wa kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. Inaonekana mgawo wake wa kwanza ulikuwa katika jiji la Antiokia ya Siria alipotumikia pamoja na binamu yake, Barnaba, na mtume Paulo. (Mdo. 12:25) Barnaba na Paulo walipoanza safari yao ya kwanza ya umishonari, Marko alisafiri pamoja nao, kwanza walienda Kipro kisha Asia Ndogo. Wakiwa huko, Marko akarudi Yerusalemu kwa sababu zisizojulikana. (Mdo. 13:4, 13) Baada ya Barnaba na Paulo kutoelewana kwa sababu ya Marko, kama inavyosimuliwa katika Matendo sura ya 15, Marko na Barnaba waliendelea na kazi ya umishonari katika kisiwa cha Kipro.​—Mdo. 15:36-39.

      Inaonekana kufikia mwaka wa 60 au 61 W.K., tayari walikuwa wametatua kutoelewana kwao kwa sababu Marko anatajwa kwa mara nyingine kwamba alikuwa akitumikia pamoja na Paulo jijini Roma. Paulo aliyekuwa mfungwa katika jiji hilo, aliliandikia hivi kutaniko la Kolosai: “Aristarko, mateka mwenzangu anawatumia salamu zake, na pia Marko, binamu ya Barnaba, (ambaye mlipokea maagizo ya kumkaribisha ikiwa atakuja kwenu).” (Kol. 4:10) Kwa hiyo, Paulo alikuwa akifikiria kumtuma Yohana Marko aende Kolosai, akamwakilishe.

      Kati ya mwaka 62 na 64 hivi, Marko alitumikia pamoja na mtume Petro katika jiji la Babiloni. Kama tulivyoona katika Sura ya 10 ya kitabu hiki, walikuwa na uhusiano wa karibu, kwa kuwa Petro anamwita kijana huyo “Marko, mwanangu.”​—1 Pet. 5:13.

      Mwishowe, mwaka wa 65 W.K. hivi, mtume Paulo alipofungwa kwa mara ya pili jijini Roma, alimwandikia hivi Timotheo, mtumishi mwenzake aliyekuwa Efeso: “Mchukue Marko uje pamoja naye, kwa maana ni mwenye faida kwangu katika huduma.” (2 Tim. 4:11) Bila shaka Marko alikubali mwaliko huo na kurudi Roma. Ndiyo sababu Barnaba, Paulo, na Petro walimthamini sana kijana huyo!

      Pendeleo kubwa zaidi la Marko ni lile la kuongozwa na roho ya Yehova kuandika masimulizi ya Injili. Inaaminika kwamba Marko alipata habari nyingi kutoka kwa mtume Petro. Kuna mambo yanayounga mkono wazo hilo. Kwa mfano, masimulizi ya Marko yanataja mambo fulani hususa ambayo yangeweza kusimuliwa tu na mtu aliyejionea matukio hayo, kama vile Petro. Hata hivyo, inaonekana Marko aliandika Injili yake akiwa Roma bali si akiwa Babiloni pamoja na Petro. Marko anatumia maneno mengi ya Kilatini na kutafsiri maneno ya Kiebrania ili watu wasio Wayahudi waelewe kwa urahisi. Kwa hiyo inaonekana aliandika hasa kwa ajili ya Watu wa Mataifa.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Marko Apata Mapendeleo Mengi.”

      b Ona sanduku lenye kichwa “Timotheo Atumika ‘Kuendeleza Habari Njema’.”

  • “Vuka Uingie Makedonia”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 16

      “Vuka Uingie Makedonia”

      Baraka zinazotokana na kukubali mgawo na kuvumilia mateso kwa shangwe

      Matendo 16:6-40

      1-3. (a) Roho takatifu iliwaongozaje Paulo na wenzake? (b) Tutachunguza mambo gani?

      KIKUNDI cha wanawake kinaondoka jijini Filipi, huko Makedonia. Baada ya muda mfupi wanawake hao wanafika kwenye mto mdogo unaoitwa Gangites. Kama ilivyo desturi yao, wanaketi kwenye ukingo wa mto huo ili kusali kwa Mungu wa Israeli. Yehova anaona wanalofanya.​—2 Nya. 16:9; Zab. 65:2.

      2 Wakati huohuo, zaidi ya kilomita 800 upande wa mashariki wa Filipi, kikundi cha wanaume kinaondoka katika jiji la Listra, lililo upande wa kusini mwa Galatia. Siku kadhaa baadaye, wanaume hao wanafika kwenye barabara kuu ya Roma inayoelekea upande wa magharibi katika eneo la wilaya ya Asia lenye idadi kubwa zaidi ya watu. Wanaume hao—Paulo, Sila, na Timotheo—wana hamu ya kutembelea Efeso na miji mingine ambayo maelfu ya watu wanahitaji kusikia kumhusu Kristo. Lakini, kabla ya kuondoka, roho takatifu inawazuia kwa njia fulani. Wanazuiwa kuhubiri Asia. Kwa nini? Kwa sababu Yesu anatumia roho ya Mungu kukiongoza kikundi hicho cha Paulo kupitia Asia Ndogo na kuvuka Bahari ya Aegea ili kwenda kwenye kingo za mto huo mdogo unaoitwa Gangites.

      3 Tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na jinsi Yesu alivyowaongoza Paulo na wenzake katika safari hiyo ya pekee ya kwenda Makedonia. Kwa hiyo, tuchunguze mambo fulani yaliyotukia katika safari hii ya pili ya Paulo ya umishonari, iliyoanza mwaka wa 49 hivi W.K.

      “Mungu Alikuwa Ametuita” (Mdo. 16:6-15)

      4, 5. (a) Ni nini kilichotokea Paulo na wenzake walipokaribia Bithinia? (b) Wanafunzi hao waliamua kufanya nini, na matokeo yalikuwa nini?

      4 Walipozuiwa kuhubiri Asia, Paulo na wenzake walienda upande wa kaskazini ili kuhubiri katika majiji ya Bithinia. Huenda walitembea kwa siku kadhaa kwenye vijia katika maeneo yasiyo na watu wengi ya Frigia na Galatia ili wafike huko. Hata hivyo, walipokaribia Bithinia, Yesu alitumia tena roho takatifu kuwazuia. (Mdo. 16:6, 7) Kufikia wakati huo, huenda wanaume hao hawakuelewa wafanye nini. Walikuwa na ujumbe wa kuhubiri, walijua jinsi ya kuhubiri, lakini hawakujua mahali pa kuhubiri. Ni kana kwamba walikuwa wamepiga hodi kwenye mlango wa kuingia Asia, lakini hawakuruhusiwa kuingia. Walipiga hodi kwenye mlango wa kuingia Bithinia, na hapo pia, hawakuruhusiwa kuingia. Paulo alikuwa ameazimia kuendelea kupiga hodi mpaka apate mlango utakaofunguka. Kisha, wanaume hao wakafanya uamuzi ambao huenda ukaonekana kuwa usiopatana na akili. Waliamua kwenda upande wa magharibi na kutembea kilomita 550, wakipita majiji mengi mpaka wakafika bandari ya Troa, ambako wangeweza kusafiri baharini kwenda Makedonia. (Mdo. 16:8) Naam, kwa mara ya tatu, Paulo alipiga hodi na mlango ukafunguka wazi kabisa.

      5 Luka, mwandishi wa Injili, aliyejiunga na Paulo na wenzake huko Troa, aliandika kilichotokea: “Paulo akaona maono usiku—mwanamume Mmakedonia alikuwa amesimama hapo akimsihi: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” Mara tu alipoona maono hayo, tukajaribu kuingia Makedonia, tukikata kauli kwamba Mungu alikuwa ametuita tuwatangazie habari njema.”a (Mdo. 16:9, 10) Sasa, Paulo alijua mahali pa kuhubiri. Bila shaka alifurahi sana kwa sababu hakukata tamaa alipokuwa njiani! Mara moja, wanaume hao wanne wakasafiri kwa mashua kwenda Makedonia.

      Mtume Paulo na Timotheo wakiwa wamesimama kwenye meli. Timotheo akionyesha kitu fulani kilicho mbali huku wafanyakazi wa meli wakiendelea na kazi.

      “Basi tukatoka Troa na kusafiri . . . baharini.”—Matendo 16:11

      6, 7. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo yaliyotokea katika safari ya Paulo? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani kutokana na mambo yaliyompata Paulo?

      6 Tunaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo? Kumbuka jambo hili: Roho ya Mungu iliingilia kati baada ya Paulo kufunga safari kwenda Asia. Yesu aliingilia kati baada ya Paulo kukaribia Bithinia. Na Yesu alimwelekeza Paulo aende Makedonia, baada ya Paulo kufika Troa. Yesu akiwa Kichwa cha kutaniko anaweza kutuongoza kwa njia kama hiyo pia. (Kol. 1:18) Kwa mfano, huenda tumefikiria kuwa mapainia au kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Hata hivyo, Yesu anaweza kutumia roho ya Mungu kutuongoza baada ya sisi kuchukua hatua zinazohitajika ili kutimiza malengo yetu. Kwa nini? Fikiria mfano huu: Dereva anaweza kuongoza gari kuelekea upande wa kushoto au kulia likiwa mwendoni, lakini hawezi kufanya hivyo ikiwa gari hilo limesimama. Vivyo hivyo, Yesu hutusaidia kupanua utumishi wetu, ikiwa tuko mwendoni, yaani, tunajitahidi kabisa kufikia malengo yetu.

      7 Tufanye nini ikiwa mwanzoni hatupati matokeo yoyote? Je, tukate tamaa tukifikiri kwamba hatuna roho ya Mungu? Hapana. Kumbuka kwamba haikuwa rahisi pia kwa Paulo kufikia malengo yake. Lakini aliendelea kutafuta mpaka alipopata mlango uliofunguka. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu tukivumilia na kuendelea kutafuta “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.”​—1 Kor. 16:9.

      8. (a) Filipi lilikuwa jiji la aina gani? (b) Ni jambo gani lenye kufurahisha lililotokea baada ya Paulo kuhubiri “mahali pa sala”?

      8 Baada ya kufika wilaya ya Makedonia, Paulo na wenzake walielekea Filipi, jiji lenye wakaaji waliojivunia kuwa raia wa Roma. Askari-jeshi Waroma waliostaafu waliishi huko na waliona jiji hilo kuwa Italia ndogo, Roma ndogo ya Makedonia. Wakiwa nje ya lango la jiji, kando ya mto mwembamba, wamishonari hao walifika katika eneo ambalo walifikiri ni “mahali pa sala.”b Walipoenda huko siku ya Sabato, waliwakuta wanawake kadhaa waliokuwa wamekusanyika hapo ili kumwabudu Mungu. Wanafunzi hao wakaketi chini na kuzungumza nao. Mwanamke aliyeitwa Lidia “alikuwa akisikiliza, na Yehova akaufungua moyo wake.” Lidia alichochewa sana na mambo aliyojifunza kutoka kwa wamishonari hao hivi kwamba yeye na watu wa nyumba yake wakabatizwa. Kisha, Lidia akamsihi Paulo na wenzake wakae nyumbani kwake.c—Mdo. 16:13-15.

      9. Wengi leo wanafuata mfano wa Paulo jinsi gani, na wamepata baraka gani?

      9 Wazia shangwe iliyotokea Lidia alipobatizwa! Bila shaka Paulo alifurahi sana kwamba alikubali mwaliko wa ‘kuvuka na kuingia Makedonia’ na Yehova aliona inafaa kumtumia yeye na wenzake kujibu sala za wanawake hao wanaomwogopa Mungu! Leo, ndugu na dada wengi, vijana kwa wazee, waliofunga ndoa kwa waseja, uhamia maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Ni kweli kwamba kuna hali nyingi ngumu, hata hivyo, haziwezi kulinganishwa na uradhi unaotokana na kuwapata watu kama Lidia, ambao hukubali kweli za Biblia. Je, unaweza kufanya marekebisho ili ‘uvuke na kuingia’ katika eneo lenye uhitaji? Utapata baraka nyingi. Kwa mfano, mfikirie Aaron, ndugu mwenye umri wa miaka 20 hivi, ambaye alihamia nchi moja ya Amerika ya Kati. Maoni yake yanafanana na ya wengi, anaposema: “Kutumikia nchi ya kigeni kumenisaidia kukua kiroho na kumkaribia Yehova zaidi. Na utumishi wa shambani unafurahisha—ninaongoza mafunzo nane ya Biblia!”

      Dada wawili wakimhubiria mwanamke mtaani. Kijana anajaribu kuangalia ili aone wanachozungumzia.

      Tunawezaje ‘kuvuka na kuingia Makedonia?’

      “Umati Ukasimama . . . Dhidi Yao” (Mdo. 16:16-24)

      10. Roho waovu walijaribu kuzuia kazi ya Paulo na wenzake jinsi gani?

      10 Shetani alikasirika sana kuona watu wakijifunza habari njema na kubatizwa katika eneo ambalo yeye na roho wake waovu hawakuwa na upinzani. Si ajabu kwamba roho waovu walihusika kusababisha kipingamizi katika kazi ya kuhubiri ya Paulo na wenzake! Walipokuwa wakienda mahali pale pa kusali, kijakazi fulani mwenye roho mwovu, aliyewapatia mabwana zake faida nyingi kwa kubashiri, alikuwa akimfuata Paulo na wenzake na kusema kwa sauti kubwa: “Watu hawa ni watumwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi nao wanawatangazia ninyi njia ya wokovu.” Huenda roho huyo mwovu alimfanya msichana huyo aseme maneno hayo ili ionekane kana kwamba mabashiri yake na mafundisho ya Paulo yanatoka katika chanzo kimoja. Kwa kufanya hivyo, watazamaji wangekengeushwa wasiwasikilize wafuasi wa kweli wa Kristo. Lakini Paulo alimnyamazisha msichana huyo kwa kumfukuza roho huyo mwovu.​—Mdo. 16:16-18.

      11. Baada ya roho mwovu kufukuzwa, ni nini kilichowapata Paulo na Sila?

      11 Mabwana wa kijakazi huyo walipoona kwamba njia yao ya kupata faida imetoweka, wakakasirika sana. Wakawakamata Paulo na Sila na kuwapeleka sokoni, mahali ambapo mahakimu—maofisa wanaowakilisha Roma—walikuwa wakihukumu. Kwa kuwa mabwana hao walijua kwamba mahakimu waliwachukia Wayahudi na walijivunia kuwa Waroma, walitoa madai yanayoonyesha kuwa Paulo na Sila wanasumbua. Ni kana kwamba walisema: ‘Wayahudi hawa wanasumbua kwa kufundisha mapokeo ambayo sisi Waroma hatuwezi kuyakubali.’ Matokeo ya maneno yao yalionekana mara moja. “Umati [uliokuwa sokoni] ukasimama pamoja dhidi yao [Paulo na Sila],” nao mahakimu wakatoa amri “wapigwe kwa fimbo.” Kisha, Paulo na Sila wakapelekwa gerezani. Mlinzi akawatupa ndani ya gereza la ndani zaidi na kuifunga miguu yao katika mikatale. (Mdo. 16:19-24) Mlinzi huyo alipoufunga mlango wa gereza, kulikuwa giza zito hivi kwamba Paulo na Sila hawangeweza kuonana. Hata hivyo, Yehova alikuwa akitazama.​—Zab. 139:12.

      12. (a) Wanafunzi wa Kristo waliyaonaje mateso na kwa nini? (b) Shetani na wale walio chini ya uvutano wake wanawapingaje wafuasi wa Kristo leo?

      12 Miaka kadhaa iliyotangulia, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Watawatesa ninyi.” (Yoh. 15:20) Hivyo, Paulo na wenzake walipovuka ili kuingia Makedonia, walitarajia kukabili upinzani. Walipoanza kuteswa walijua kwamba ni kwa sababu ya hasira ya Shetani na haimaanishi walipoteza kibali cha Yehova. Leo, watu walio chini ya uvutano wa Shetani wanatenda kama watu waliompinga Paulo katika jiji la Filipi. Tukiwa shuleni au kazini, wapinzani hao wasio wanyoofu husema mambo yalipotoka kutuhusu ili kuwachochea wengine watupinge. Katika nchi fulani, wapinzani wa kidini wanatushtaki mahakamani, ni kana kwamba wanasema: ‘Mashahidi hawa wanasumbua kwa kufundisha mapokeo ambayo sisi “waumini wa zamani” hatuwezi kuyakubali.’ Katika maeneo mengine, waabudu wenzetu hupigwa na kutupwa gerezani. Hata hivyo, Yehova anatazama.​—1 Pet. 3:12.

      “Wakabatizwa Bila Kukawia” (Mdo. 16:25-34)

      13. Kwa nini mlinzi aliuliza: “Nifanye nini ili niokolewe?”

      13 Paulo na Sila walihitaji wakati wa kutafakari mambo yaliyowapata. Hata hivyo, kufikia usiku wa manane, walijihisi nafuu kutokana na maumivu hivi kwamba “walikuwa wakisali na kumsifu Mungu kwa wimbo.” Kisha, ghafla, tetemeko la ardhi likatikisa gereza! Mlinzi akaamka, na alipoona milango ya gereza imefunguka, akafikiri wafungwa wametoroka. Akijua kwamba ataadhibiwa kwa kuwaacha wafungwa watoroke, “akauchomoa upanga wake naye karibu ajiue.” Lakini Paulo akamwambia kwa sauti kubwa: “Usijiumize, kwa maana sisi sote tupo hapa!” Mlinzi huyo mwenye wasiwasi akauliza: “Mabwana zangu, nifanye nini ili niokolewe?” Paulo na Sila hawangeweza kumwokoa lakini Yesu pekee angeweza. Kwa hiyo, wakamjibu: “Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa.”​—Mdo. 16:25-31.

      14. (a) Paulo na Sila walimsaidiaje mlinzi wa jela? (b) Paulo na Sila walipata baraka gani kwa kuvumilia mateso kwa shangwe?

      14 Je, mlinzi huyo aliuliza swali hilo kwa unyoofu? Paulo hakutilia shaka unyoofu wake. Mlinzi huyo alikuwa Mtu wa Mataifa, asiyejua Maandiko. Kabla ya kuwa Mkristo, alihitaji kujifunza na kukubali kweli za msingi za Maandiko. Hivyo, Paulo na Sila walitumia wakati ‘kumhubiria neno la Yehova.’ Kwa kuwa walikazia fikira kumfundisha mtu huyo Maandiko huenda walisahau maumivu waliyokuwa nayo. Hata hivyo, mlinzi huyo aliona vidonda migongoni mwao, naye akaviosha. Kisha yeye na familia yake “wakabatizwa bila kukawia.” Paulo na Sila walipata baraka kubwa sana kwa kuvumilia mateso kwa shangwe!—Mdo. 16:32-34.

      15. (a) Mashahidi wengi leo wanafuata mfano wa Paulo na Sila jinsi gani? (b) Kwa nini tuwatembelee tena na tena watu wanaoishi katika eneo letu?

      15 Kama Paulo na Sila, leo, Mashahidi wengi waliofungwa kwa sababu ya imani yao wamepata matokeo mazuri kwa kuhubiri habari njema wakiwa gerezani. Kwa mfano, wakati mmoja kulikuwa na asilimia 40 ya Mashahidi waliojifunza ukweli kumhusu Yehova wakiwa gerezani katika nchi moja ambayo utendaji wetu ulipigwa marufuku. (Isa. 54:17) Pia, kumbuka kwamba mlinzi huyo aliomba msaada baada ya tetemeko la ardhi. Vivyo hivyo, watu fulani leo ambao hawajawahi kukubali ujumbe wa Ufalme huenda wakaukubali baada tu ya ulimwengu wao kutikiswa na jambo fulani lenye kuhuzunisha. Kuwarudia tena na tena watu wanaoishi katika eneo letu, huonyesha kwamba tuko tayari kutoa msaada wakati wowote unapohitajika.

      “Je, Sasa Wanatufukuza kwa Siri?” (Mdo. 16:35-40)

      16. Ni nini kilichotokea siku moja baada ya Paulo na Sila kupigwa viboko?

      16 Siku iliyofuata mahakimu waliamuru Paulo na Sila wafunguliwe. Lakini Paulo akasema: “Walitupiga viboko hadharani bila kutuhukumu, ingawa sisi ni Waroma, na wakatutupa gerezani. Je, sasa wanatufukuza kwa siri? Hapana, haiwezekani! Acha waje watutoe nje wao wenyewe.” Baada ya kutambua kwamba wanaume hao wawili ni raia wa Roma, mahakimu hao “wakaogopa,” kwa sababu walikuwa wamekiuka haki zao.d Mambo yakageuka. Wanafunzi hao walipigwa viboko hadharani; sasa mahakimu walilazimika kuwaomba msamaha hadharani. Wakawasihi Paulo na Sila waondoke Filipi. Walikubali, lakini kwanza wakakitia moyo kikundi kipya cha wanafunzi kilichokuwa kikikua. Kisha wakaondoka.

      17. Uvumilivu wa Paulo na Sila ungeweza kuwafundisha nini wanafunzi wapya?

      17 Ikiwa Paulo na Sila wangesema mwanzoni kwamba wao ni raia wa Roma, huenda hawangepigwa viboko. (Mdo. 22:25, 26) Hata hivyo, huenda wanafunzi wa Filipi wangefikiri kwamba Paulo na Sila walitumia uraia wao kuepuka kuteseka kwa ajili ya Kristo. Kufanya hivyo kungeathirije imani ya wanafunzi ambao hawakuwa raia wa Roma? Sheria haingewazuia wao wasipigwe viboko. Hivyo, kwa kuvumilia adhabu ya viboko Paulo na mwenzake waliwawekea waabudu hao wapya kielelezo kwamba wafuasi wa Kristo wanaweza kusimama imara licha ya mateso. Isitoshe, kwa kusisitiza uraia wao utambuliwe, Paulo na Sila walitaka ijulikane hadharani kwamba mahakimu hao wametenda kinyume cha sheria. Kufanya hivyo kungeweza kuwazuia wasiwatendee vibaya waamini wengine na badala yake kuwapa ulinzi wa kisheria mashambulizi kama hayo yatakapotokea wakati ujao.

      18. (a) Waangalizi Wakristo leo hufuata kielelezo cha Paulo jinsi gani? (b) Tunawezaje “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema?”

      18 Leo, waangalizi katika kutaniko la Kikristo huliwekea kutaniko kielelezo cha kufuata. Chochote wanachotazamia waabudu wenzao wafanye, Wachungaji hao Wakristo wako tayari kufanya. Kama Paulo, sisi pia huchunguza mambo kwa uangalifu kabla ya kutumia haki zetu za kisheria. Ikihitajika, sisi hukata rufaa katika mahakama za kitaifa na hata za kimataifa ili kutetea uhuru wetu wa ibada. Tunapofanya hivyo, lengo letu si kuleta mapinduzi ya kijamii, bali “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema” kama Paulo alivyoliandikia kutaniko la Filipi miaka kumi hivi baada ya kufungwa huko. (Flp. 1:7) Hata mahakama itoe uamuzi gani, tumeazimia kuendelea ‘kutangaza habari njema’ popote ambapo roho ya Mungu itatuongoza kama Paulo na wenzake walivyofanya.​—Mdo. 16:10.

      LUKA—MWANDISHI WA KITABU CHA MATENDO

      Kuanzia sura ya 1 hadi sura ya 16 mstari wa 9 wa kitabu cha Matendo, mwandishi wa kitabu cha matendo anazungumzia mambo ambayo wengine wanasema na kufanya. Hata hivyo, kuanzia Matendo 16:10, 11, mtindo wa uandikaji unabadilika. Kwa mfano, katika mstari wa 11, mwandishi anasema: “Tukatoka Troa na kusafiri moja kwa moja baharini hadi Samothrake.” Hapa ndipo mwandishi Luka, alianza kujihusisha katika matukio yanayosimuliwa. Hata hivyo, kwa kuwa jina la Luka halipatikani mahali popote katika kitabu cha Matendo ya Mitume, tunajuaje kwamba yeye ndiye mwandishi wa kitabu hicho?

      Luka amekaa akiandika kwenye kitabu cha kukunjwa kilicho mezani.

      Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza utangulizi wa kitabu cha Matendo na Injili ya Luka. Utangulizi wa vitabu vyote viwili unataja mtu anayeitwa “Theofilo.” (Luka 1:1, 3; Mdo. 1:1) Utangulizi wa kitabu cha Matendo unasema: “Lile simulizi la kwanza, ewe Theofilo, niliandika kuhusu mambo yote ambayo Yesu alianza kufanya na kufundisha.” Kwa kuwa wasomi wenye kutegemeka wamekubali kwa muda mrefu kwamba “lile simulizi la kwanza,” yaani, Injili, liliandikwa na Luka, basi lazima pia aliandika kitabu cha Matendo.

      Hatujui mengi kumhusu Luka. Jina lake linapatikana mara tatu tu katika Biblia. Mtume Paulo anamwita Luka “daktari mpendwa” na ‘mfanyakazi mwenzake.’ (Kol. 4:14; Flm. 24) Sehemu za kitabu cha Matendo ambazo Luka anajihusisha katika masimulizi zinaonyesha kwamba Luka alisafiri pamoja na mtume Paulo kutoka Troa mpaka Filipi mwaka wa 50 W.K. hivi, lakini Paulo alipoondoka Filipi, Luka hakusafiri pamoja naye. Wanaume hao wawili walikutana tena Filipi mwaka wa 56 W.K. hivi na kusafiri pamoja na ndugu wengine saba kutoka Filipi kwenda Yerusalemu, ambapo Paulo alikamatwa. Miaka miwili baadaye, Luka alisafiri pamoja na Paulo, akiwa mfungwa, kutoka Kaisaria kwenda Roma. (Mdo. 16:10-17, 40; 20:5–21:17; 24:27; 27:1–28:16) Paulo alifungwa Roma kwa mara ya pili, na hata alipotambua kwamba anakaribia kuuawa, ni “Luka tu” ndiye aliyekuwa pamoja naye. (2 Tim. 4:6, 11) Ni wazi kwamba Luka alisafiri maeneo ya mbali na alikuwa tayari kuteseka kwa ajili ya habari njema.

      Luka hakudai kwamba alijionea mambo aliyoandika kumhusu Yesu. Badala yake, anasema kwamba alijitahidi ‘kukusanya habari kuhusu mambo aliyosadiki kabisa’ yaliyosimuliwa na “mashahidi wa kujionea.” Anaendelea kusema, “nimefuatilia mambo yote kwa usahihi tangu mwanzo, nami nimeamua kukuandikia mambo hayo kwa utaratibu mzuri.” (Luka 1:1-3) Kitabu cha Luka kinaonyesha wazi kwamba alifanya utafiti kwa makini. Huenda alimhoji Elisabeti, Maria, mama ya Yesu, na wengine ili kukusanya habari za kuandika. Mambo mengi aliyoandika hayapatikani katika vitabu vingine vya Injili.​—Luka 1:5-80.

      Mtume Paulo alisema kwamba Luka alikuwa daktari, na masimulizi yake ya Injili yanaonyesha wazi alihangaishwa na afya ya watu walioteseka. Kwa mfano: Luka aliandika kwamba Yesu alipomponya mtu aliyesumbuliwa na roho mwovu, “yule roho mwovu akamtoka bila kumuumiza.” Pia, aliandika kwamba mama mkwe wa mtume Petro alikuwa na “homa kali,” na kwamba mwanamke ambaye Yesu alimsaidia alisumbuliwa na “roho ya udhaifu kwa miaka 18, mwili wake ulikuwa umepindika na hangeweza kusimama wima.”​—Luka 4:35, 38; 13:11.

      Luka alitanguliza “kazi ya Bwana” maishani mwake. (1 Kor. 15:58) Lengo lake lilikuwa kuwasaidia wengine wamjue na kumtumikia Yehova bali si kutafuta utajiri au umashuhuri.

      LIDIA—MUUZAJI WA BIDHAA ZA RANGI YA ZAMBARAU

      Lidia aliishi Filipi, jiji mashuhuri katika wilaya ya Makedonia. Alitoka Thiatira, jiji lililokuwa magharibi mwa Asia Ndogo katika eneo linaloitwa Lidia. Ili kuendeleza biashara yake, Lidia alihamia eneo la ng’ambo ya Bahari ya Aegea. Inawezekana aliuza bidhaa mbalimbali za rangi ya zambarau, kama vile mazulia, mapambo, vitambaa, na hata rangi yenyewe. Maandishi yaliyopatikana Filipi yanathibitisha kwamba kulikuwa na kikundi cha wauzaji wa bidhaa za zambarau katika jiji hilo.

      Lidia akionyesha kitambaa.

      Kwa kuwa Lidia anatajwa kuwa “mwabudu wa Mungu,” huenda aligeuzwa imani na kuwa mfuasi wa dini ya Kiyahudi. (Mdo. 16:14) Inawezekana alikuwa amepata habari fulani kuhusu ibada ya Yehova katika jiji la nyumbani kwao. Tofauti na Filipi, jiji la kwao lilikuwa na sinagogi la Wayahudi. Watu fulani wanaamini kwamba Lidia lilikuwa jina la utani—linalomaanisha “Mwanamke kutoka Lidia”​—ambalo alipewa alipokuwa Filipi. Hata hivyo, kuna uthibitisho unaoonyesha kwamba kulikuwa na wanawake wengine walioitwa Lidia.

      Tangu siku za Homer, katika karne ya tisa au nane K.W.K., watu wa Lidia na majirani zao walijulikana kwa ustadi wao wa kutia rangi ya zambarau kwenye vitambaa. Maji ya Thiatira yalijulikana kwa kutokeza “rangi nyangavu na zinazodumu sana.”

      Bidhaa za zambarau zilikuwa ghali sana na zingeweza kununuliwa na matajiri tu. Ingawa rangi ya zambarau ingeweza kupatikana kutoka katika vitu mbalimbali, rangi bora na iliyokuwa ghali zaidi—iliyowekwa kwenye vitambaa laini—ilitokana na samaki-gamba wa Mediterania. Kila samaki angeweza kutokeza tone moja tu la rangi hiyo, na ili kupata gramu moja ya rangi hiyo ya pekee, samaki 8,000 hivi walihitajika. Ndiyo sababu nguo za rangi hiyo zilikuwa ghali sana.

      Inawezekana Lidia alikuwa mfanyabiashara tajiri kwa sababu biashara yake ilihitaji awe na pesa nyingi na pia alikuwa na nyumba kubwa ambapo Paulo, Sila, Timotheo, na Luka wangeweza kukaa. Biblia inataja “watu wa nyumbani mwake,” huenda alikuwa anaishi na watu wake wa ukoo, au alikuwa na vijakazi na watumishi. (Mdo. 16:15) Na kwa kuwa kabla ya kuondoka katika jiji hilo, Paulo na Sila walikutana na ndugu kadhaa katika nyumba ya mwanamke huyo mkarimu, inawezekana kwamba baadaye nyumba hiyo ilikuwa mahali ambapo Wakristo wa kwanza katika jiji la Filipi walikutana kwa ajili ya ibada.​—Mdo. 16:40.

      Miaka kumi baadaye, Paulo alipoliandikia barua kutaniko la Filipi, hakumtaja Lidia. Kwa hiyo habari pekee tulizo nazo kumhusu ni zile zinazopatikana katika sura ya 16 ya kitabu cha Matendo.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Luka—Mwandishi wa Kitabu cha Matendo.”

      b Huenda Wayahudi hawakuruhusiwa kuwa na sinagogi katika jiji la Filipi kwa sababu lilikuwa jiji la kijeshi. Au labda jiji hilo halikuwa na angalau wanaume kumi Wayahudi—idadi ya chini zaidi iliyohitajiwa ili kuwa na sinagogi.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Lidia—Muuzaji wa Bidhaa za Rangi ya Zambarau.”

      d Kulingana na sheria ya Roma, raia alikuwa na haki ya kusikilizwa kabla ya kuhukumiwa naye hakupaswa kamwe kuadhibiwa hadharani kabla ya kuthibitishwa kuwa mwenye hatia.

  • “Akajadiliana Nao Akitumia Maandiko”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 17

      “Akajadiliana Nao Akitumia Maandiko”

      Msingi mzuri wa kufundisha; mfano mzuri uliowekwa na Waberoya

      Matendo 17:1-15

      1, 2. Ni nani wanaosafiri kutoka Filipi kwenda Thesalonike, na huenda wanafikiria nini?

      BARABARA nzuri sana iliyojengwa na wahandisi stadi kutoka Roma. Barabara hiyo iliyojipinda inapitia milimani. Kuna kelele nyingi—milio ya punda, kelele za magurudumu ya magari ya kukokotwa, na kelele za wasafiri. Huenda wasafiri walitia ndani wanajeshi, wafanyabiashara, na mafundi. Paulo, Sila na Timotheo wanatumia barabara hiyo kusafiri kutoka Filipi kwenda Thesalonike, umbali wa zaidi ya kilomita 130. Safari hiyo si rahisi, hasa kwa Paulo na Sila kwa kuwa bado walikuwa na majeraha waliyopata Filipi, ambako walipigwa kwa fimbo.​—Mdo. 16:22, 23.

      2 Ni nini kitakachowasaidia wasivunjwe moyo na safari ndefu iliyo mbele yao? Ni mazungumzo yao wanapokuwa njiani. Bado wanakumbuka vizuri jambo la kustaajabisha lililotokea huko Filipi, jinsi yule mlinzi wa jela pamoja na familia yake walivyokuwa waamini. Tukio hilo limewachochea waazimie hata zaidi kuendelea kutangaza neno la Mungu. Hata hivyo, wanapokaribia jiji la Thesalonike lililo pwani, hawajui jinsi watakavyotendewa na Wayahudi katika jiji hilo. Je, watashambuliwa, na hata kupigwa kama ilivyokuwa Filipi?

      3. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Paulo wa kujipa ujasiri ili kuhubiri?

      3 Baadaye Paulo alieleza hisia zake alipowaandikia Wakristo katika jiji la Thesalonike: “Ingawa kwanza tulikuwa tumeteseka na kudharauliwa huko Filipi, kama mnavyojua, tulijipa ujasiri kupitia Mungu wetu ili tuwatangazie ninyi habari njema ya Mungu licha ya upinzani.” (1 The. 2:2) Inaonekana Paulo alisitasita kwenda Thesalonike, hasa baada ya mambo yaliyotokea Filipi. Je, unaweza kuelewa hisia za Paulo? Je, kuna wakati unahisi ni vigumu kuhubiri habari njema? Paulo alimtegemea Yehova ili apate nguvu, na kumwezesha kujipa ujasiri. Mfano wake unaweza kukusaidia kufanya hivyo pia.​—1 Kor. 4:16.

      “Akajadiliana . . . Akitumia Maandiko” (Mdo. 17:1-3)

      4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Paulo alikaa jijini Thesalonike kwa zaidi ya majuma matatu?

      4 Masimulizi yanasema kwamba Paulo alipokuwa Thesalonike, alihubiri katika sinagogi kwa Sabato tatu. Hilo halimaanishi kwamba alikaa jijini humo kwa majuma matatu tu. Huenda Paulo hakuweza kwenda kwenye sinagogi mara tu alipofika Thesalonike. Isitoshe, barua za Paulo zinaonyesha kwamba wakiwa Thesalonike, yeye na wenzake walifanya kazi ili kupata mahitaji yao. (1 The. 2:9; 2 The. 3:7, 8) Akiwa huko, Paulo alipokea vitu fulani mara mbili kwa ajili ya mahitaji yake kutoka kwa akina ndugu wa Filipi. (Flp. 4:16) Hivyo inaonekana alikaa jijini Thesalonike kwa zaidi ya majuma matatu.

      5. Paulo alichocheaje fikira za wasikilizaji wake?

      5 Baada ya kujipa ujasiri wa kuhubiri, Paulo alizungumza na watu waliokuwa wamekusanyika katika sinagogi. Kulingana na desturi yake, ‘akajadiliana nao akitumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu, akisema: “Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia ninyi.”’ (Mdo. 17:2, 3) Lengo la Paulo halikuwa kuwasisimua tu wasikilizaji wake bali kuchochea fikira zao. Alijua kwamba watu waliokuwa katika sinagogi waliyajua Maandiko na kuyaheshimu lakini hawakuyaelewa. Hivyo, Paulo alijadili, akafafanua, na kuthibitisha kwa kutumia Maandiko kwamba Yesu wa Nazareti ndiye Masihi, au Kristo, aliyeahidiwa.

      6. Yesu aliwathibitishiaje wanafunzi wake kwa kutumia Maandiko, na matokeo yalikuwa nini?

      6 Paulo alifuata mfano wa Yesu wa kutumia Maandiko kama msingi wa mafundisho yake. Kwa mfano, katika huduma yake, Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba kulingana na Maandiko, lazima Mwana wa binadamu ateseke na kufa, kisha afufuliwe. (Mt. 16:21) Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea wanafunzi wake, na hivyo kuthibitisha kwamba alikuwa amesema kweli. Hata hivyo, Yesu aliwapa uthibitisho zaidi. Tunasoma hivi kuhusu mazungumzo yake na wanafunzi fulani: “Akawafafanulia kuanzia Musa na Manabii wote, mambo yote ambayo Maandiko yalisema kumhusu.” Ikawaje? Wanafunzi wakasema hivi kwa mshangao: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akizungumza nasi barabarani, na alipokuwa akitufungulia Maandiko waziwazi?”​—Luka 24:13, 27, 32.

      7. Kwa nini ni muhimu kutumia Maandiko kama msingi wa mafundisho yetu?

      7 Ujumbe wa Neno la Mungu una nguvu. (Ebr. 4:12) Kama Yesu, Paulo, na mitume wengine, Wakristo leo hutegemea Neno la Mungu wanapowafundisha watu. Sisi pia hujadili, hufafanua Maandiko, na kuwathibitishia watu mambo tunayowafundisha kwa kuwafungulia Biblia na kuwaonyesha kile ambacho inasema. Ujumbe tunaohubiri si wetu. Tunapotumia Biblia, tunawasaidia kutambua kwamba hatufundishi maoni yetu, bali mafundisho ya Mungu. Pia, tunakumbuka kwamba msingi wa ujumbe wetu ni Neno la Mungu. Neno hilo linategemeka kabisa. Kwa kuwa tunajua kwamba ujumbe wetu unategemeka, tunahubiri kwa ujasiri kama Paulo.

      “Baadhi . . . Wakaamini” (Mdo. 17:4-9)

      8-10. (a) Watu jijini Thesalonike waliitikiaje habari njema? (b) Kwa nini baadhi ya Wayahudi walimwonea wivu Paulo? (c) Wapinzani Wayahudi walitendaje?

      8 Tayari Paulo alikuwa amejionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia; ikiwa wamelishika neno langu, watalishika lenu pia.” (Yoh. 15:20) Jijini Thesalonike, Paulo alikutana na watu wenye maoni mbalimbali, baadhi yao walikuwa tayari kutii neno na wengine walipinga. Kuhusu wale waliokubali, Luka anaandika hivi: “Baadhi yao [Wayahudi] wakaamini [wakawa Wakristo] na kujiunga na Paulo na Sila, pia umati mkubwa wa Wagiriki waliomwabudu Mungu, vilevile wanawake wengi mashuhuri.” (Mdo. 17:4) Wanafunzi hao wapya walifurahi kusaidiwa kuyaelewa Maandiko.

      9 Ingawa baadhi yao walithamini maneno ya Paulo, wengine walimkasirikia sana. Wayahudi fulani jijini Thesalonike walimwonea wivu Paulo kwa sababu “umati mkubwa wa Wagiriki” ulikubali ujumbe wake. Wayahudi hao, wakiwa na lengo la kupata wafuasi, waliwafundisha Watu wa Mataifa waliokuwa Wagiriki mafundisho kutoka katika Maandiko ya Kiebrania, na waliwaona Wagiriki hao kuwa mali yao. Hata hivyo, ilianza kuonekana kana kwamba Paulo anawanyakua Wagiriki hao, tena hapohapo kwenye sinagogi! Wayahudi hao walikasirika sana.

      Paulo na Sila wakitoroka umati wenye hasira kupitia lango la nyuma. Mwanamume amesimama langoni akizungumza na umati wenye hasira.

      ‘Walitaka Paulo na Sila waletwe nje kwenye kile kikundi.’—Matendo 17:5

      10 Luka anatueleza kilichofuata: “Wayahudi wakawa na wivu, wakakusanya wanaume fulani waovu waliokuwa wakizurura sokoni, wakafanyiza kikundi chenye ghasia kisha wakazusha fujo jijini. Wakaishambulia nyumba ya Yasoni wakitaka Paulo na Sila waletwe nje kwenye kile kikundi. Walipowakosa wakamkokota Yasoni na baadhi ya akina ndugu mpaka kwa watawala wa jiji, wakisema kwa sauti kubwa: ‘Watu hawa ambao wameipindua dunia inayokaliwa wako hapa pia, naye Yasoni amewakaribisha. Watu hao wote wanapinga maagizo ya Kaisari, wakisema kuna mfalme mwingine, Yesu.’” (Mdo. 17:5-7) Mashambulizi hayo yangewaathirije Paulo na wenzake?

      11. Paulo na wenzake walishtakiwa kwa makosa gani, na huenda waliowashtaki walidai wamevunja amri gani? (Ona maelezo ya chini)

      11 Kikundi chenye ghasia ni kama mto uliovunja kingo zake, wenye nguvu nyingi na usiozuilika. Wayahudi walitumia kikundi hicho ili kujaribu kuwafukuza Paulo na Sila. Baada ya “kuzusha fujo jijini,” wakajaribu kuwasadikisha watawala kwamba mashtaka yao yalikuwa mazito. Shtaka la kwanza lilikuwa kwamba Paulo na wenzake “wameipindua dunia inayokaliwa,” ingawa Paulo na wenzake hawakusababisha fujo jijini Thesalonike! Shtaka la pili lilikuwa zito zaidi. Wayahudi walidai kwamba wamishonari hao wanamtangaza Mfalme mwingine, Yesu, na hivyo wanavunja sheria ya maliki.a

      12. Ni nini kinachoonyesha kwamba mashtaka dhidi ya Wakristo jijini Thesalonike yangeweza kuwa na matokeo mabaya?

      12 Kumbuka kwamba viongozi wa kidini walimshtaki Yesu kwa madai yanayofanana na hayo. Walimwambia Pilato: “Tulimkuta mtu huyu akipindua taifa letu . . . akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo mfalme.” (Luka 23:2) Huenda Pilato aliogopa kuwa maliki angefikiri ameachilia kosa kubwa la uhaini, ndio sababu alimhukumu Yesu kwamba anastahili kufa. Vivyo hivyo, mashtaka dhidi ya Wakristo jijini Thesalonike yangekuwa na matokeo mabaya. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema: “Mashtaka hayo yalikuwa hatari sana. Ikiwa mtu angetuhumiwa kuwa anataka kumsaliti Maliki, angeweza kuhukumiwa kifo.’” Je, mashtaka hayo yenye chuki yangefanikiwa?

      13, 14. (a) Kwa nini kikundi chenye ghasia hakikufanikiwa? (b) Paulo alifuata jinsi gani ushauri wa Kristo wa kuwa waangalifu, nasi tunawezaje kuiga mfano wake?

      13 Umati huo wenye ghasia ulishindwa kukomesha kazi ya kuhubiri jijini Thesalonike. Kwa nini? Kwanza, Paulo na Sila hawakupatikana. Isitoshe, inaonekana kwamba watawala wa jiji hilo hawakuamini mashtaka hayo. Baada ya kuchukua “dhamana ya kutosha,” walimwachilia Yasoni na ndugu wengine waliofikishwa mbele yao. (Mdo. 17:8, 9) Paulo alifuata ushauri wa Yesu wa kuwa ‘mwangalifu kama nyoka na asiye na hatia kama njiwa.’ (Mt. 10:16) Alifanya hivyo kwa kuondoka kwa busara mahali penye hatari na kwenda kuhubiri mahali pengine. Bila shaka, ujasiri wa Paulo haukuwa wa kijinga. Wakristo wanawezaje kuiga mfano wake?

      14 Leo, mara nyingi viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo huwachochea watu wawafanyie fujo Mashahidi wa Yehova. Wamewachochea watawala wawatese kwa kudai kwamba Mashahidi wanaipinga serikali au si wazalendo. Kama karne ya kwanza, wapinzani wa leo huchochewa na wivu. Wakristo wa kweli hawajihatarishi bila sababu. Sisi huepuka kubishana na watu wenye hasira na wakaidi, badala yake tunaendelea kufanya kazi yetu kwa amani, na ikiwezekana tunawarudia baadaye wanapokuwa wametulia.

      KAISARI WANAOTAJWA KATIKA KITABU CHA MATENDO

      Matukio yote yaliyoandikwa katika kitabu cha Matendo na katika Maandiko yote ya Kigiriki ya Kikristo, yalitokea katika Milki ya Roma. Kwa hiyo, sikuzote maliki Mroma ndiye aliyekuwa na mamlaka kuu zaidi. Wayahudi wa Thesalonike walipozungumzia “maagizo ya Kaisari” walikuwa wakimrejelea maliki (Mdo. 17:7) Maliki wanne walitawala wakati wa kipindi kinachozungumziwa katika kitabu cha Matendo—Tiberio, Gayo, Klaudio wa Kwanza, na Nero.

      • Tiberio (14-37 W.K.) alikuwa maliki wakati wa huduma ya Yesu na miaka michache ya kwanza ya kutaniko la Kikristo. Yesu alipohukumiwa, Wayahudi walikuwa wakirejelea Tiberio walipopiga kelele na kusema: “Ukimfungua mtu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari. . . . Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.”​—Yoh. 19:12, 15.

      • Gayo, ambaye pia anaitwa Caligula (37-41 W.K.), hatajwi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

      • Klaudio wa Kwanza (41-54 W.K.) anatajwa mara mbili katika kitabu cha Matendo. Kama ilivyotabiriwa na nabii Mkristo Agabo, “njaa kubwa” ya mwaka wa 46 hivi W.K., ilitokea “juu ya dunia yote inayokaliwa . . . wakati wa Klaudio.” Pia, mwaka wa 49 au mapema mwaka wa 50 W.K., Klaudio ‘aliagiza Wayahudi wote waondoke Roma,’ amri iliyofanya Akila na Prisila kuhamia Korintho, ambapo walikutana na mtume Paulo.​—Mdo. 11:28; 18:1, 2.

      • Nero (54-68 W.K.) ndiye Kaisari ambaye Paulo alikata rufaa kwake. (Mdo. 25:11) Inasemekana kwamba baadaye maliki huyo alidai kwamba Wakristo ndio waliowasha moto ulioharibu sehemu kubwa ya Roma mwaka wa 64 hivi W.K. Muda mfupi baadaye, mwaka wa 65 hivi W.K., mtume Paulo alifungwa jijini Roma na kuuawa.

      “Walikuwa Wasikivu” (Mdo. 17:10-15)

      15. Waberoya waliitikiaje habari njema?

      15 Kwa ajili ya usalama wao, Paulo na Sila walitumwa Beroya, kilomita 65 hivi kutoka Thesalonike. Walipofika huko, Paulo alienda katika sinagogi na kuanza kuzungumza na watu waliokusanyika huko. Walifurahi sana kwa sababu walipata watu waliosikiliza. Luka aliandika kwamba Wayahudi wa Beroya walikuwa “wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, kwa maana walilikubali neno kwa hamu kubwa ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo ndivyo yalivyo.” (Mdo. 17:10, 11) Hili halimaanishi kwamba Wathesalonike waliokubali kweli walikuwa na mtazamo mbaya. Baadaye Paulo aliwaandikia: “Tunamshukuru Mungu bila kuacha, kwa kuwa mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali si kama neno la wanadamu, bali kama lilivyo kwa kweli, neno la Mungu, ambalo pia linafanya kazi ndani yenu waamini.” (1 The. 2:13) Hata hivyo, ni nini kilichowafanya Wayahudi waliokuwa Beroya kuwa wasikivu zaidi?

      16. Kwa nini Waberoya waliitwa “wasikivu”?

      16 Ingawa ilikuwa habari mpya kwa Waberoya, hawakutilia shaka au kuichambua. Haimaanishi walidanganyika kwa urahisi. Kwanza walimsikiliza Paulo kwa makini. Kisha, wakahakikisha mambo waliyojifunza kwa kusoma Maandiko ambayo Paulo aliwasaidia kuyaelewa. Isitoshe, walikuwa wakijifunza Neno la Mungu kila siku, si siku ya Sabato tu. Na walifanya hivyo “kwa hamu kubwa ya akili,” wakijitahidi kujua mambo ambayo Maandiko yanasema kuhusu mafundisho hayo mapya. Pia, walionyesha unyenyekevu kwa kufanya mabadiliko na “wengi wao wakawa waamini.” (Mdo. 17:12) Ndiyo sababu Luka anasema kwamba walikuwa “wasikivu”!

      17. Kwa nini Waberoya ni mfano mzuri wa kuigwa, na tunawezaje kudumisha mtazamo huo hata ikiwa tumekuwa katika kweli kwa muda mrefu?

      17 Waberoya hao hawakujua kwamba mtazamo wao mzuri kuelekea habari njema ungeandikwa katika Neno la Mungu kwa faida ya wengine. Walifanya kama vile Paulo alivyotarajia na jinsi Yehova Mungu alivyotaka wafanye. Leo, sisi huwatia moyo watu wachunguze Biblia kwa makini ili imani yao itegemee Neno la Mungu. Hata hivyo, baada ya kuwa waamini, je, huo ndio mwisho wa kuwa wasikivu? Hapana, usikivu ni muhimu hata zaidi nasi tunapaswa kuwa na hamu kubwa zaidi ya kujifunza kutoka kwa Yehova na kutumia mambo tunayojifunza maishani. Kwa kufanya hivyo, tunamruhusu Yehova atufinyange na kutuzoeza kulingana na mapenzi yake. (Isa. 64:8) Hivyo, tunampendeza Baba yetu wa mbinguni naye ataendelea kututumia kutimiza makusudi yake.

      18, 19. (a) Kwa nini Paulo aliondoka Beroya, na tunajifunza nini kutokana na mfano wake? (b) Paulo anapaswa kuwahubiria nani sasa, na wapi?

      18 Paulo hakukaa Beroya kwa muda mrefu. Tunasoma hivi: “Wayahudi kutoka Thesalonike waliposikia kwamba Paulo alikuwa akitangaza pia neno la Mungu huko Beroya, wakaja huko ili kuchochea na kuuvuruga umati. Mara moja akina ndugu wakamsindikiza Paulo mpaka baharini, lakini Sila na Timotheo wakabaki huko. Hata hivyo, wale waliomsindikiza Paulo wakaenda naye mpaka Athene, kisha wakarudi baada ya kupokea maagizo kwamba Sila na Timotheo wamfuate Paulo haraka iwezekanavyo.” (Mdo. 17:13-15) Adui hao wa habari njema hawakukata tamaa! Hawakutosheka kwamba Paulo ameondoka Thesalonike; walimfuata mpaka Beroya na kujaribu kuwachochea watu wa huko pia, lakini hawakufanikiwa. Paulo alijua kwamba eneo ni kubwa, kwa hiyo alienda kuhubiri eneo lingine. Sisi pia, tuazimie kusimama imara dhidi ya wale wanaotaka kukomesha kazi yetu ya kuhubiri!

      19 Baada ya kutoa ushahidi kamili kwa Wayahudi wa Thesalonike na Beroya, Paulo alikuwa amejifunza mengi kuhusu umuhimu wa kuhubiri kwa ujasiri na kujadiliana na watu kwa kutumia Maandiko. Sisi pia tumejifunza mengi. Hata hivyo, sasa Paulo anakutana na wasikilizaji tofauti—Watu wa Mataifa jijini Athene. Mambo yatakuwaje katika jiji hilo? Tutaona katika sura inayofuata.

      a Kulingana na msomi mmoja, wakati huo kulikuwa na sheria ya Kaisari iliyokataza utabiri wowote kuhusu “kuja kwa mfalme au ufalme mpya, hasa mfalme anayeweza kumwondoa au kumhukumu maliki anayetawala.” Huenda adui za Paulo walifanya ujumbe wa mtume huyo uonekane kana kwamba unakiuka sheria hiyo. Ona sanduku lenye kichwa “Kaisari Wanaotajwa Katika Kitabu cha Matendo.”

  • “Wamtafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wampate”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 18

      “Wamtafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wampate”

      Paulo aweka msingi mzuri wa mazungumzo na kubadilika kulingana na hali ya wasikilizaji wake

      Matendo 17:16-34

      1-3. (a) Ni nini kilichomkasirisha mtume Paulo akiwa Athene? (b) Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza mfano wa Paulo?

      PAULO amekasirika sana. Yuko jijini Athene, kitovu cha elimu nchini Ugiriki, ambako wakati fulani wanafalsafa kama vile Sokratesi, Plato, na Aristoto walifundisha. Athene ni jiji la kidini. Pande zote—mahekaluni, katika viwanja vya watu wote, na barabarani—Paulo anaona sanamu nyingi, kwa sababu Waathene huabudu miungu mingi sana. Paulo anajua maoni ya Mungu wa kweli, Yehova, kuhusiana na ibada ya sanamu. (Kut. 20:4, 5) Mtume huyo mwaminifu ana maoni kama ya Yehova—anachukia sanamu!

      2 Paulo anashangazwa sana na mambo anayoona anapoingia sokoni. Kuna sanamu nyingi za mungu Herme zenye umbo la kiungo cha uzazi cha kiume zilizowekwa upande wa kaskazini-magharibi, karibu na lango kuu. Soko hilo lina madhabahu nyingi. Mtume huyo mwenye bidii atahubiri jinsi gani katika jiji hilo ambalo ibada ya sanamu imekita mizizi? Je, ataonyesha sifa ya kujizuia na kuweka msingi mzuri wa mazungumzo kwa wasikilizaji wake? Je, atafaulu kumsaidia yeyote amtafute Mungu wa kweli na kumwabudu?

      3 Hotuba ya Paulo, iliyo katika Matendo 17:22-31, ambayo aliitoa mbele za watu hao wenye elimu inaonyesha kwamba alitumia ushawishi, busara, na utambuzi. Mfano wa Paulo unaweza kutusaidia sana kujua jinsi ya kuweka msingi mzuri wa mazungumzo na kuwasaidia wasikilizaji wetu kufikiri.

      Kufundisha “Sokoni” (Mdo. 17:16-21)

      4, 5. Paulo alihubiri wapi akiwa Athene, naye alikutana na watu wa aina gani?

      4 Katika safari yake ya pili ya umishonari, mwaka wa 50 hivi W.K., Paulo alitembelea jiji la Athene.a Alipokuwa akiwasubiri Sila na Timotheo wafike kutoka Beroya, Paulo “akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi,” kama ilivyokuwa desturi yake. Pia alienda “sokoni,” mahali ambapo angeweza kuwapata watu wa Athene wasio Wayahudi. (Mdo. 17:17) Soko hilo lililokuwa na ukubwa wa ekari 12 hivi, lilikuwa upande wa kaskazini-magharibi mwa Ngome ya Athene. Halikuwa mahali pa kuuza na kununua tu, bali pia uwanja wa watu wote. Kitabu fulani cha marejeo kinasema kwamba mahali hapo palikuwa “kituo cha kibiashara, kisiasa na kitamaduni jijini humo.” Waathene walipenda kukusanyika hapo na kuzungumzia mambo mbalimbali ya kitaalamu.

      ATHENE—KITUO CHA UTAMADUNI KATIKA ULIMWENGU WA KALE

      Watu walianza kuandika historia ya jiji la Athene katika karne ya saba K.W.K. Hata hivyo, jiji hilo lilikuwa jiji lenye ngome hata kabla ya wakati huo. Athene lilikuja kuwa jiji kuu la wilaya ya Attica na lilikuwa na ukubwa wa kilomita za mraba 2,500. Jiji hilo lilizungukwa na milima na bahari. Inaonekana kuna uhusiano kati ya jina la jiji hilo na jina la mungu wa jiji hilo, Athena.

      Katika karne ya sita K.W.K., Solon, mtunga sheria Mwathene, alianzisha mabadiliko ya kijamii, kisiasa, kisheria, na kiuchumi katika jiji hilo. Aliboresha maisha ya maskini na kuweka msingi wa mfumo wa serikali za kidemokrasia. Hata hivyo, ilikuwa demokrasia ya watu huru tu, walio wengi bado walikuwa watumwa.

      Baada ya ushindi mbalimbali wa Wagiriki dhidi ya Waajemi katika karne ya tano K.W.K., Athene likawa jiji kuu la milki ndogo iliyokuwa ikifanya biashara kupitia bahari kuanzia Italia na Sisili upande wa magharibi hadi Kipro na Siria upande wa mashariki. Jiji hilo lilipofanya maendeleo makubwa, likawa kituo cha utamaduni katika ulimwengu wa kale, likifanya vizuri katika sanaa, michezo ya kuigiza, falsafa, ufasaha wa kusema, uandishi, na sayansi. Jiji hilo lilikuwa na majengo ya umma na mahekalu mengi. Kutoka mbali, mtu angeweza kukiona kilima kilichokuwa kwenye jiji hilo, ambacho juu yake kulikuwa na hekalu la Parthenon, lililokuwa na sanamu ya Athena, yenye urefu wa mita 12, iliyotengenezwa kwa dhahabu na pembe za tembo.

      Jiji la Athene lilishindwa na kuporwa, kwanza na Wasparta, kisha Wamakedonia, na mwishowe Waroma. Hata hivyo, wakati wa mtume Paulo, bado Athene lilikuwa jiji maarufu kwa sababu ya sifa zake za wakati uliopita. Jiji hilo halikuwa kamwe sehemu ya mikoa ya Roma, bali lilipewa mamlaka ya kujitawala na kutunga sheria zake na halikuhitajika kulipa kodi zilizotozwa na serikali ya Roma. Ingawa Athene lilipoteza umashuhuri, liliendelea kuwa jiji lenye chuo kikuu, ambako watoto wa matajiri walienda kusoma.

      5 Akiwa sokoni, Paulo alikutana na watu ambao hawakuwa tayari kumsikiliza. Baadhi ya wasikilizaji wake walikuwa Waepikurea na Wastoa, ambao waliamini falsafa mbili tofauti.b Waepikurea waliamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe tu. Kwa ufupi, waliamini hivi: “Mungu hawezi kutufanya lolote; Hakuna maumivu yoyote katika kifo; Mambo mema yanaweza kufanywa; Mambo mabaya yanaweza kuvumiliwa.” Wastoa walikazia falsafa za kibinadamu nao hawakuamini kwamba kuna Mungu. Waepikurea na Wastoa hawakuamini ufufuo ambao wanafunzi wa Kristo walifundisha. Ni wazi kwamba maoni ya kifalsafa ya vikundi hivyo viwili hayakupatana hata kidogo na Ukristo wa kweli, ambao Paulo alikuwa akitangaza.

      6, 7. Wasomi Wagiriki waliyaonaje mafundisho ya Paulo, na hali ikoje leo?

      6 Wasomi Wagiriki walionaje mafundisho ya Paulo? Baadhi yao walimwita “mpigadomo.” (Mdo. 17:18) Kuhusu neno la Kigiriki linalotumika katika mstari huo, msomi mmoja anasema hivi: “Mwanzoni neno hilo lilitumiwa kurejelea ndege mdogo anayerukaruka akiokota punje, pia lilitumiwa kurejelea watu waliokuwa wakiokota masalio ya vyakula na vitu vingine vilivyoanguka sokoni. Baadaye, neno hilo lilianza kutumiwa kwa njia ya mfano kurejelea mtu anayekusanya habari hapa na pale, na hasa yule ambaye haelewi habari zenyewe.” Kwa kumwita “mpiga-domo,” ni kana kwamba wasomi hao walisema kwamba Paulo ni mtu anayerudia-rudia mambo asiyoelewa, ambayo amesikia kutoka kwa wengine. Kama tutakavyoona, Paulo hakuvunjika moyo kwa kuitwa jina hilo.

      7 Ndivyo ilivyo leo. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, mara nyingi tunasemwa vibaya kwa sababu ya imani yetu inayotegemea Biblia. Kwa mfano, walimu fulani hudai kwamba fundisho la mageuzi ni la kweli na kwamba ikiwa una akili, utaliamini. Ni kana kwamba wanadai wote wanaopinga fundisho hilo ni wajinga. Wasomi hao wanataka watu wengine watuone sisi kuwa wajinga kwa sababu tunafundisha mambo ambayo Biblia inasema na kuthibitisha kwamba vitu vyote viliumbwa. Hata hivyo, hilo halituvunji moyo. Badala yake, tunasema tukiwa na uhakika kwamba uhai uliopo duniani ulitokana na Muumba mwenye akili, Yehova Mungu.​—Ufu. 4:11.

      8. (a) Baadhi ya watu waliomsikia Paulo akihubiri walikuwa na maoni gani? (b) Kwa nini Paulo alipelekwa Areopago? (Ona maelezo ya chini katika ukurasa wa 142.)

      8 Wengine waliomsikiliza Paulo akihubiri sokoni walikuwa na maoni tofauti. Walisema: “Inaonekana anatangaza miungu ya kigeni.” (Mdo. 17:18) Je, ni kweli Paulo alikuwa akiwatangazia Waathene miungu ya kigeni? Hilo lilikuwa jambo zito. Karne kadhaa mapema, Sokratesi alihukumiwa kifo kwa mashtaka kama hayo. Hivyo, haishangazi kwamba Paulo alipelekwa Areopago na kuambiwa afafanue mafundisho hayo yaliyokuwa mageni kwa Waathene.c Paulo angeuteteaje ujumbe wake mbele ya watu hao wasiojua Maandiko?

      WAEPIKUREA NA WASTOA

      Waepikurea na Wastoa walikuwa na falsafa mbili zinazotofautiana. Vikundi vyote viwili havikuamini ufufuo.

      Waepikurea waliamini kwamba kuna miungu lakini walifikiri kwamba miungu hiyo haipendezwi na wanadamu, nayo haingewathawabisha wala kuwaadhibu, kwa hiyo kusali au kutoa dhabihu ni kazi bure. Waepikurea waliona kwamba anasa ndilo jambo kuu maishani. Fikira na matendo yao hayakuzingatia maadili hata kidogo. Watu walihimizwa wawe na kiasi ili tu kuepuka madhara ya kufanya mambo kupita kiasi. Waliamini kwamba elimu ni muhimu ikiwa tu inamsaidia mtu asiamini mafundisho ya dini yanayosababisha hofu na ya ushirikina.

      Kwa upande mwingine, Wastoa waliamini kwamba vitu vyote ni sehemu ya mungu asiye na utu na kwamba nafsi ya binadamu inatoka katika chanzo kama hicho. Wastoa fulani waliamini kwamba hatimaye nafsi ingeharibiwa pamoja na ulimwengu. Wastoa wengine waliamini kwamba hatimaye nafsi ingechukuliwa tena na mungu huyo. Kulingana na wanafalsafa Wastoa, furaha ingeweza kupatikana kwa kutii sheria za asili.

      “Wanaume wa Athene, Ninaona” (Mdo. 17:22, 23)

      9-11. (a) Paulo aliwekaje msingi mzuri wa mazungumzo? (b) Tunawezaje kufuata mfano wa Paulo katika huduma?

      9 Kumbuka kwamba Paulo alikasirika kwa sababu ya ibada ya sanamu aliyojionea, ambayo ilienea sana. Badala ya kuanza kuishambulia ibada ya sanamu, alikuwa mtulivu. Alitumia busara, na kujitahidi kuwavutia wasikilizaji wake kwa kuweka msingi mzuri wa mazungumzo. Alianza kwa kusema hivi: “Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa mnaogopa sana miungu kuliko watu wengine.” (Mdo. 17:22) Ni kana kwamba Paulo alikuwa akisema ‘Naona mnapenda sana mambo ya dini.’ Paulo alitenda kwa hekima alipowapongeza kwa sababu walipendezwa na mambo ya dini. Alitambua kwamba baadhi ya watu waliopofushwa na imani za uwongo wanaweza kusikiliza. Isitoshe, alijua kwamba wakati fulani hata yeye mwenyewe ‘alitenda bila ujuzi na hakuwa na imani.’​—1 Tim. 1:13.

      10 Baada ya kuweka msingi mzuri, Paulo alieleza kwamba ameona jambo linalothibitisha kuwa watu wa Athene wanapenda mambo ya dini. Aliona madhabahu iliyotengwa kwa ajili ya “Mungu Asiyejulikana.” Kulingana na kitabu kimoja, “Wagiriki walikuwa na mazoea ya kutenga madhabahu kwa ajili ya ‘miungu isiyojulikana,’ ili wasimsahau mungu fulani katika ibada yao, na hivyo kumkasirisha.” Kwa kutenga madhabahu hiyo, Waathene walikiri kwamba kuna Mungu ambaye hawamjui. Paulo alitumia madhabahu hiyo kuwa msingi wa kuwahubiria habari njema. Alieleza: “Kile mnachoabudu bila kujua, hicho ndicho ninachowatangazia.” (Mdo. 17:23) Paulo alitoa hoja zenye nguvu kwa busara. Hakuwa akiwahubiria mungu mpya au wa kigeni, kama watu fulani walivyodai. Alikuwa akiwaeleza kuhusu Mungu ambaye hawakumjua—Mungu wa kweli.

      11 Tunawezaje kumwiga Paulo katika huduma yetu? Tukiwa wenye utambuzi, tunaweza kugundua ikiwa mtu anapendezwa na mambo ya dini, labda kwa kuona vitu fulani vya kidini ambavyo amevaa au vilivyo katika nyumba yake au kwenye uwanja wake. Tunaweza kusema: ‘Naona unapendezwa na mambo ya dini. Nilitaka kuzungumza na mtu kama wewe.’ Kwa kumpongeza, tunaweza kuweka msingi mzuri wa mazungumzo. Kumbuka kwamba lengo letu si kuwahukumu watu kwa sababu ya imani yao. Wakati fulani, baadhi ya waabudu wenzetu waliamini mafundisho ya uwongo kwa kutojua.

      Mvulana akiwaeleza jambo fulani mwalimu na wanafunzi wenzake katika darasa la Sayansi.

      Jitahidi kuweka msingi mzuri wa mazungumzo

      Mungu “Hayuko Mbali na Kila Mmoja Wetu” (Mdo. 17:24-28)

      12. Paulo alibadili mazungumzo yake jinsi gani ili yawafae wasikilizaji wake?

      12 Tayari Paulo aliweka msingi mzuri wa mazungumzo, lakini je, alijenga vizuri juu ya msingi huo? Akijua kwamba wasikilizaji wake wamefunzwa falsafa za Kigiriki na hawayajui Maandiko, alitumia mbinu mbalimbali. Kwanza alitaja mafundisho ya Biblia bila kunukuu Maandiko moja kwa moja. Pili, alijihusisha kwenye mazungumzo, nyakati nyingine alitumia maneno kama vile “sisi,” na “tuna-.” Tatu, alinukuu vitabu vya Kigiriki ili kuonyesha kwamba mambo fulani aliyokuwa akifundisha yalikuwa katika vitabu vyao wenyewe. Acheni sasa tuchanganue hotuba ya Paulo iliyokuwa na matokeo mazuri. Aliwajulisha Waathene kweli gani muhimu kuhusu Mungu ambaye hawakumjua?

      13. Paulo alieleza nini kuhusu ulimwengu, na maneno yake yalikuwa na ujumbe gani?

      13 Mungu aliumba ulimwengu. Paulo alisema hivi: “Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama alivyo, Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyotengenezwa kwa mikono.”d (Mdo. 17:24) Ulimwengu haukujitokeza wenyewe. Mungu wa kweli ndiye Muumba wa vitu vyote. (Zab. 146:6) Tofauti na Athena au miungu mingine ambayo utukufu wao ulitegemea mahekalu na madhabahu, mahekalu yaliyojengwa na mikono ya wanadamu hayawezi kumtosha Bwana Mwenye Enzi Kuu wa mbingu na dunia. (1 Fal. 8:27) Ujumbe wa Paulo ulikuwa wazi: Mungu wa kweli ni mkuu kuliko sanamu yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu iliyo katika mahekalu yaliyojengwa na wanadamu.​—Isa. 40:18-26.

      14. Paulo alionyeshaje kwamba Mungu hawategemei wanadamu?

      14 Mungu hawategemei wanadamu. Waabudu-sanamu walipamba sanamu zao kwa nguo maridadi, walizipatia zawadi za bei ghali, au kuzipelekea vyakula na vinywaji—kana kwamba sanamu zilihitaji vitu hivyo! Hata hivyo, huenda baadhi ya wanafalsafa Wagiriki waliomsikiliza Paulo hawakuamini kwamba mungu anahitaji chochote kutoka kwa wanadamu. Ikiwa ndivyo, basi walikubaliana na maneno ya Paulo kwamba Mungu “hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote.” Hakuna kitu chochote cha kimwili ambacho wanadamu wanaweza kumpa Muumba! Badala yake, Mungu huwapa wanadamu wanachohitaji—“uhai na pumzi na vitu vyote,” kutia ndani jua, mvua, na udongo wenye rutuba. (Mdo. 17:25; Mwa. 2:7) Kwa hiyo, Mungu aliye Mpaji, hawezi kuwategemea wanadamu ambao ni wapokeaji.

      15. Paulo alishughulikiaje maoni ya Waathene kwamba wao ni bora kuliko watu wasio Wagiriki, nasi tunajifunza nini kutokana na mfano wake?

      15 Mungu alimuumba mwanadamu. Waathene waliamini kwamba wao ni bora kuliko watu wasio Wagiriki. Lakini ubaguzi haupatani na kweli ya Biblia. (Kum. 10:17) Paulo alizungumzia kwa busara na ustadi jambo hilo ambalo lingeweza kutokeza ubishi. Huenda waliomsikiliza walitulia na kufikiri aliposema, “[Mungu] alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja.” (Mdo. 17:26) Alikuwa akirejelea masimulizi ya Mwanzo kuhusu Adamu, baba ya wanadamu wote. (Mwa. 1:26-28) Kwa kuwa wanadamu wote wana baba mmoja, hakuna jamii au taifa bora kuliko lingine. Wasikilizaji wa Paulo walielewa vizuri hoja yake. Mfano huu unatufundisha jambo muhimu. Ingawa tunapaswa kutumia busara na kuwa wenye usawaziko katika kazi yetu ya kuhubiri, hatupaswi kamwe kupunguza uzito wa kweli ya Biblia ili kufanya watu wakubali ujumbe wetu.

      16. Muumba ana kusudi gani kwa wanadamu?

      16 Mungu alikusudia wanadamu wawe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Hata ikiwa wanafalsafa waliomsikiliza Paulo walikuwa wamejadiliana kwa muda mrefu kuhusu kusudi la uhai wa binadamu, hawangeweza kamwe kutoa jibu sahihi na linaloeleweka. Hata hivyo, Paulo alieleza waziwazi kusudi la Muumba kwa wanadamu, kwamba “wamtafute Mungu, ikiwa watapapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ingawa, kwa hakika, hayuko mbali na kila mmoja wetu.” (Mdo. 17:27) Mungu ambaye Waathene hawakumjua anaweza kujulikana. Hayuko mbali na wale ambao kwa kweli wanataka kumtafuta na kumjua. (Zab. 145:18) Ona kwamba Paulo anatumia maneno “kila mmoja wetu,” akijitia ndani kati ya wale wanaohitaji ‘kumtafuta’ na ‘kupapasa-papasa wakimtafuta’ Mungu.

      17, 18. Kwa nini wanadamu wanapaswa kumkaribia Mungu, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Paulo alivyozungumza na wasikilizaji wake?

      17 Wanadamu wanapaswa kumkaribia Mungu. Paulo alisema kwamba, kwa sababu ya Mungu “tuko hai, tunatembea, na tunaishi.” Wasomi fulani husema kwamba Paulo alikuwa akirejelea maneno ya Epimenide, mshairi Mgiriki wa karne ya sita K.W.K. “aliyeheshimiwa sana katika utamaduni wa dini ya Waathene.” Paulo alitaja sababu nyingine inayopaswa kuwafanya wanadamu wahisi wako karibu na Mungu, aliposema: “Baadhi ya washairi wenu wamesema, ‘Kwa maana sisi pia ni watoto wake.’” (Mdo. 17:28) Wanadamu wanapaswa kujiona kuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu, kwa kuwa Yeye ndiye Baba ya mwanadamu wa kwanza ambaye wanadamu wote walitoka kwake. Ili kuwavutia wasikilizaji wake, Paulo alitumia busara kwa kunukuu moja kwa moja vitabu vya Kigiriki ambavyo bila shaka watu waliomsikiliza waliviheshimu sana.e Kama Paulo, nyakati nyingine tunaweza kunukuu vitabu vya historia, ensaiklopedia, au vitabu vingine vya marejeo vinavyoheshimika. Kwa mfano, nukuu inayofaa kutoka katika chanzo kinachotegemeka, inaweza kumsaidia mtu ambaye si Shahidi kujua chanzo cha mazoea au maadhimisho fulani ya dini za uwongo.

      18 Kufikia hapa, Paulo ameeleza kweli za msingi kumhusu Mungu, akitumia maneno yake kwa ustadi ili yawafae wasikilizaji wake. Mtume huyo alitaka Waathene hao watumie jinsi gani habari hizo muhimu? Bila kukawia, aliendelea kutoa hotuba yake na kuwaambia wanalopaswa kufanya.

      “Wanadamu Wote Kila Mahali . . . Wanapaswa Kutubu” (Mdo. 17:29-31)

      19, 20. (a) Paulo alitumia busara jinsi gani kuonyesha ubatili wa kuabudu sanamu zilizotengenezwa na wanadamu? (b) Waliomsikiliza Paulo walihitaji kuchukua hatua gani?

      19 Paulo alikuwa tayari kuwahimiza wasikilizaji wake wachukue hatua. Akirejelea tena nukuu kutoka kwa waandishi Wagiriki, alisema: “Kwa hiyo, kwa kuwa sisi ni watoto wa Mungu, hatupaswi kufikiri kwamba Mungu ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa kwa ufundi na ubunifu wa wanadamu.” (Mdo. 17:29) Kwa kweli, ikiwa wanadamu wametoka kwa Mungu, inawezekanaje Mungu awe sanamu zinazotengenezwa na wanadamu? Njia ya Paulo ya kujadiliana nao ilionyesha ubatili wa kuabudu sanamu zilizotengenezwa na wanadamu. (Zab. 115:4-8; Isa. 44:9-20) Huenda Paulo alifanya iwe rahisi kwa wasikilizaji wake kukubali ushauri wake kwa kujihusisha katika mazungumzo na kusema, “hatupaswi.”

      20 Paulo alionyesha wazi kabisa kwamba wanahitaji kuchukua hatua. Alisema: “Mungu ameachilia nyakati hizo za kutojua [za kufikiri kwamba Mungu angependezwa na watu wanaoabudu sanamu]; lakini sasa anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.” (Mdo. 17:30) Huenda baadhi wa wasikilizaji wa Paulo walishangaa kusikia kwamba wanapaswa kutubu. Hata hivyo, hotuba yake yenye nguvu ilionyesha wazi kwamba Mungu ndiye chanzo cha uhai wao na kwa sababu hiyo wanawajibika mbele Zake. Wanahitaji kumtafuta Mungu, kujifunza ukweli kumhusu, na kupatanisha maisha yao na ukweli huo. Kwa Waathene, hilo lilimaanisha kutambua na kuacha kabisa dhambi ya kuabudu sanamu.

      21, 22. Paulo alimaliza hotuba yake kwa maneno gani yenye kuchochea, nayo yanatuhusu jinsi gani?

      21 Paulo alimaliza hotuba yake kwa maneno yenye kuchochea sana: “[Mungu] ameweka siku ambayo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:31) Siku ya Hukumu inayokuja—hiyo ni sababu nzuri ya kumtafuta na kumpata Mungu wa kweli! Paulo hakutaja jina la Hakimu huyo aliyewekwa rasmi. Badala yake, alisema jambo la kustaajabisha kumhusu Hakimu huyo: Aliishi akiwa mwanadamu, akafa, na kufufuliwa na Mungu!

      22 Umalizio huo wenye kuchochea una umuhimu mkubwa kwetu. Tunajua kwamba Yesu Kristo aliyefufuliwa ndiye Hakimu aliyewekwa rasmi na Mungu. (Yoh. 5:22) Pia tunajua kwamba Siku ya Hukumu ina urefu wa miaka elfu moja, nayo inakaribia sana. (Ufu. 20:4, 6) Hatuogopi Siku ya Hukumu, kwa kuwa tunajua itawaletea baraka nyingi wale watakaohukumiwa kuwa waaminifu. Kufufuliwa kwa Yesu Kristo kunatuhakikishia kwamba tumaini letu la kuwa na maisha bora ya wakati ujao litatimia hakika!

      “Wanaume . . . [Wakawa] Waamini” (Mdo. 17:32-34)

      23. Watu waliitikia hotuba ya Paulo katika njia gani mbalimbali?

      23 Watu waliitikia hotuba ya Paulo kwa njia mbalimbali. Waliposikia kuhusu ufufuo, “baadhi yao wakaanza kumdhihaki.” Wengine walikuwa watulivu lakini hawakutaka kuchukua hatua yoyote, nao wakamwambia: “Tutakusikiliza kuhusu jambo hili wakati mwingine.” (Mdo. 17:32) Hata hivyo, wachache kati yao waliitikia vizuri: “Wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini. Miongoni mwao kulikuwa na Dionisio, aliyekuwa mwamuzi wa mahakama ya Areopago, na mwanamke aliyeitwa Damari, na wengineo.” (Mdo. 17:34) Ndivyo inavyokuwa pia katika huduma yetu. Huenda watu fulani wakatudhihaki, na wengine ingawa wanatuheshimu, lakini hawataki kuchukua hatua yoyote. Hata hivyo, sisi hufurahi sana baadhi yao wanapokubali ujumbe wa Ufalme na kuwa waamini.

      24. Tunaweza kujifunza nini kutokana na hotuba aliyotoa Paulo alipokuwa amesimama Areopago?

      24 Tunapochanganua hotuba ya Paulo, tunaweza kujifunza mengi kuhusu mpangilio mzuri wa habari, hoja zenye kusadikisha, na jinsi ya kubadilika kulingana na hali za wasikilizaji wetu. Pia, tunaweza kujifunza faida ya kuwa na subira na busara tunapozungumza na watu ambao wamepofushwa na imani za uwongo za kidini. Pia, tunaweza kujifunza somo hili muhimu: Hatupaswi kamwe kupunguza uzito wa kweli za Biblia ili tu kuwafurahisha wasikilizaji wetu. Hata hivyo, tukifuata mfano wa Paulo, tunaweza kuwa walimu wenye matokeo mazuri katika utumishi wa shambani. Isitoshe, waangalizi wanaweza kuwa walimu stadi kutanikoni. Hivyo, tutakuwa tayari kuwasaidia wengine “wamtafute Mungu . . . na kwa kweli wampate.”​—Mdo. 17:27.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Athene—Kituo cha Utamaduni Katika Ulimwengu wa Kale.”

      b Ona sanduku lenye kichwa “Waepikurea na Wastoa.”

      c Kilima cha Areopago kilikuwa upande wa kaskazini-magharibi mwa Ngome ya Athene, mahali ambapo baraza kuu la Athene lilikutana. Huenda jina “Areopago” lilirejelea baraza hilo au kilima chenyewe. Hivyo, wasomi hawajui kihususa ikiwa Paulo alipelekwa kwenye kilima hicho au karibu na eneo, au mahali pengine ambapo baraza hilo lilikutana, labda sokoni.

      d Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ulimwengu” ni koʹsmos. Ijapokuwa Wagiriki walilitumia neno hilo kurejelea ulimwengu halisi, neno koʹsmos kwa kawaida hutumika katika Biblia kurejelea watu. Inawezekana kwamba Paulo, aliyekuwa akijaribu kuweka msingi mzuri wa mazungumzo kati yake na Wagiriki waliomsikiliza, alitumia neno hilo katika maana hiyo.

      e Paulo alinukuu shairi linaloitwa Phaenomena, la Arato, mshairi Mstoa. Maneno kama hayo yanapatikana katika vitabu vingine vya Kigiriki kutia ndani wimbo unaoitwa Hymn to Zeus, uliotungwa na Kleanthe, mwandikaji Mstoa.

  • “Endelea Kusema na Usinyamaze”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 19

      “Endelea Kusema na Usinyamaze”

      Paulo ajitegemeza kimwili na kutanguliza huduma

      Matendo 18:1-22

      1-3. Mtume Paulo ameenda Korintho kufanya nini, na anakabili changamoto gani?

      NI MWISHONI mwa mwaka wa 50 W.K. Mtume Paulo yuko Korintho, jiji tajiri lenye wakaaji wengi Wagiriki, Waroma, na Wayahudi.a Paulo hakwenda kununua wala kuuza bidhaa au kutafuta kazi ya kimwili. Ameenda hapo ili kufanya kazi muhimu zaidi—kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, Paulo anahitaji mahali pa kuishi, na hataki kuwa mzigo kwa wengine. Hataki mtu yeyote afikiri kwamba anajiruzuku kutokana na neno la Mungu. Atafanya nini?

      2 Paulo ana ujuzi wa kutengeneza mahema. Kazi ya kutengeneza mahema si rahisi, hata hivyo, yuko tayari kufanya kazi kwa mikono yake ili ajitegemeze. Je, atapata kazi katika jiji hili lenye shughuli nyingi? Je, atapata mahali pazuri pa kuishi? Ingawa ana mahitaji mengi, Paulo hasahau kamwe kazi yake kuu, kazi ya kuhubiri.

      3 Paulo alikaa Korintho kwa muda fulani, naye alipata matokeo mazuri katika huduma yake. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na utendaji mbalimbali wa Paulo alipokuwa Korintho ambayo yanaweza kutusaidia kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu katika eneo letu?

      KORINTHO—JIJI LENYE BAHARI MBILI

      Jiji la kale la Korintho lilikuwa kwenye kipande cha eneo kinachounganisha nchi ya Ugiriki na rasi ya kusini inayoitwa Peloponesia. Sehemu nyembamba zaidi ya eneo hilo ilikuwa na upana usiozidi kilomita sita, na kwa sababu hiyo Korintho lilikuwa na bandari mbili. Bandari ya Lekayo, ilikuwa kwenye Ghuba ya Korintho, na ilitumiwa na meli zilizokuwa zikielekea magharibi hadi Hispania, Italia, na Sisili. Na bandari ya Kenkrea, iliyokuwa katika Ghuba ya Saroni, ilitumiwa na meli zinazoenda na zinazotoka eneo la Aegea, Asia Ndogo, Siria, na Misri.

      Kwa kuwa kulikuwa na upepo mkali kwenye eneo la kusini la Ugiriki, ilikuwa hatari kusafiri kwa meli. Ndio sababu manahodha walipendelea kutia nanga katika mojawapo ya bandari hizo mbili za Korintho, kisha kusafirisha shehena yao juu ya nchi kavu, na kuipakia tena katika bandari ya pili. Ikiwa meli ilikuwa nyepesi ingeweza kuvushwa kupitia barabara ya pekee kutoka bandari moja hadi bandari nyingine. Kwa sababu ya mahali lilipokuwa, jiji hilo lilitawala biashara za meli pande zote mbili za bahari, mashariki na magharibi, na pia za nchi kavu, kaskazini na kusini. Mbali na utajiri, jiji la Korintho lilikuwa na ufisadi mwingi ambao hupatikana katika bandari nyingi.

      Katika siku za Paulo, Korintho lilikuwa jiji kuu la mkoa wa Roma ya Akaya na kituo muhimu cha kuendesha shughuli za serikali. Kulikuwa na dini nyingi sana katika jiji hilo. Kwa mfano kulikuwa na hekalu la kumwabudu Maliki wa Roma, maeneo mengi ya ibada kwa ajili ya kuabudu miungu ya Wagiriki na Wamisri, na pia sinagogi la Wayahudi.​—Mdo. 18:4.

      Mashindano ya mbio yaliyofanywa Isthmia kila baada ya miaka miwili yalikuwa ya pili kwa umaarufu, Michezo ya Olimpiki ikiwa katika nafasi ya kwanza. Huenda mtume Paulo alikuwa Korintho mashindano ya mwaka wa 51 W.K. yalipokuwa yakiendelea. Kamusi moja ya Biblia inasema, “haishangazi kwamba Paulo alitumia mfano wa mashindano ya mbio kwa mara ya kwanza katika barua yake kwa Wakorintho.”​—1 Kor. 9:24-27.

      “Kazi Yao Ilikuwa ya Kutengeneza Mahema” (Mdo. 18:1-4)

      4, 5. (a) Paulo aliishi wapi alipokuwa Korintho, naye alifanya kazi gani ya kimwili? (b) Huenda Paulo alijifunzaje kazi ya kutengeneza mahema?

      4 Baada ya kufika Korintho, Paulo alikutana na wenzi wa ndoa wakarimu—Akila mwenye asili ya Kiyahudi, na mke wake, Prisila, au Priska. Akila na Prisila walihamia Korintho kwa sababu Maliki Klaudio aliagiza “Wayahudi wote waondoke Roma.” (Mdo. 18:1, 2) Akila na Prisila walimkaribisha Paulo nyumbani kwao na pia katika kazi yao ya kimwili. Tunasoma: “Kwa sababu [Paulo alifanya] kazi ileile, akakaa nyumbani kwao na kufanya kazi pamoja nao, kwa maana kazi yao ilikuwa ya kutengeneza mahema.” (Mdo. 18:3) Kipindi chote cha huduma yake jijini Korintho, Paulo alikaa nyumbani kwa wenzi hao wenye fadhili na wakarimu. Inawezekana Paulo aliandika baadhi ya barua ambazo baadaye zilikuwa sehemu ya Biblia alipokuwa akiishi nyumbani kwa Akila na Prisila.b

      5 Paulo, mtu aliyeelimishwa “miguuni pa Gamalieli,” angewezaje kuwa na ujuzi wa kutengeneza mahema? (Mdo. 22:3) Inaonekana kwamba Wayahudi wa karne ya kwanza hawakuona aibu kuwafundisha watoto wao kazi fulani ya mikono, ingawa watoto hao walipata elimu ya ziada pia. Kwa kuwa alikuwa mwenyeji wa Tarso ya Kilikia, eneo lililojulikana sana kwa sababu ya kitambaa kinachoitwa cilicium kilichotumiwa kutengeneza mahema, inaelekea Paulo alijifunza kazi hiyo alipokuwa kijana. Kazi hiyo ya kutengeneza mahema ilifanywaje? Huenda ilitia ndani kufuma kitambaa cha hema au kukata na kushona kitambaa hicho kigumu ili kutengeneza mahema. Bila shaka, kazi hiyo ilikuwa ngumu sana.

      6, 7. (a) Paulo aliionaje kazi ya kutengeneza mahema, na ni nini kinachoonyesha kwamba Akila na Prisila walikuwa na maoni hayohayo? (b) Wakristo leo wanafuataje mfano wa Paulo, Akila, na Prisila?

      6 Paulo hakuiona kazi ya kutengeneza mahema kuwa kazi muhimu sana maishani mwake. Alifanya kazi hiyo ili kujitegemeza na lengo lake lilikuwa kuhubiri habari njema “bila gharama.” (2 Kor. 11:7) Akila na Prisila waliionaje kazi yao ya kimwili? Kwa kuwa walikuwa Wakristo, bila shaka walikuwa na maoni kama ya Paulo. Isitoshe, Paulo alipoondoka Korintho mwaka wa 52 W.K., Akila na Prisila waliacha biashara yao na kusafiri pamoja na Paulo hadi Efeso, ambapo nyumba yao ilitumiwa kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. (1 Kor. 16:19) Baadaye, walirudi Roma, halafu wakaenda tena Efeso. Wenzi hao wenye bidii walitanguliza Ufalme na walijitoa kwa hiari ili kuwatumikia wengine. Kwa sababu hiyo “makutaniko yote ya mataifa” yaliwashukuru.​—Rom. 16:3-5; 2 Tim. 4:19.

      7 Leo, Wakristo hufuata mfano wa Paulo, Akila, na Prisila. Wahubiri wenye bidii leo hufanya yote wawezayo ili ‘wasimpe yeyote kati yetu mzigo wenye gharama.’ (1 The. 2:9) Mapainia wengi wanatuwekea mfano mzuri kwa kufanya kazi kwa siku kadhaa katika juma au miezi fulani katika mwaka ili waweze kulipia gharama zao za maisha. Hata hivyo, wanatanguliza kazi ya upainia. Kama Akila na Prisila, watumishi wengi wa Yehova huonyesha ukarimu kwa kuwakaribisha nyumbani kwao waangalizi wa mzunguko. ‘Wakaribishaji wageni’ wanajua kwamba kuwa wakarimu hutia moyo na kujenga.​—Rom. 12:13.

      BARUA ZENYE KUTIA MOYO ZILIZOONGOZWA NA ROHO YA MUNGU

      Katika kipindi cha miezi 18 ambacho mtume Paulo alikaa Korintho, mwaka wa 50-52 hivi W.K., aliandika barua mbili zilizokuja kuwa sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo—Barua ya Kwanza na ya Pili kwa Wathesalonike. Huenda pia aliandika barua yake kwa Wagalatia wakati huohuo au muda mfupi baadaye.

      Barua ya Kwanza kwa Wathesalonike ndiyo maandishi ya kwanza ambayo Paulo aliongozwa na roho kuyaandika. Paulo alitembelea Thesalonike mwaka wa 50 hivi W.K., alipokuwa katika safari yake ya pili ya kuhubiri. Muda mfupi baadaye, kutaniko jipya lililokuwa limeanzishwa lilikumbwa na upinzani uliowalazimu Paulo na Sila kuondoka jijini humo. (Mdo. 17:1-10, 13) Akihangaikia hali ya kutaniko hilo jipya, Paulo alijaribu mara mbili kurudi huko lakini “Shetani aliifunga njia [yake].” Hivyo Paulo akamtuma Timotheo awafariji na kuwaimarisha akina ndugu. Mwishoni mwa mwaka wa 50 hivi W.K., Timotheo aliungana na Paulo jijini Korintho na kumweleza habari njema kuhusu kutaniko la Thesalonike. Kisha, Paulo akawaandikia barua ya kwanza.​—1 The. 2:17–3:7.

      Huenda Barua ya Pili kwa Wathesalonike iliandikwa muda mfupi baada ya ile ya kwanza, mnamo mwaka wa 51 hivi W.K. Katika barua zote mbili, Timotheo na Silvano (anayeitwa Sila katika kitabu cha Matendo) walituma salamu zao pamoja na Paulo, na hakuna uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba watu hao watatu walikuwa pamoja tena baada ya wakati huo ambao Paulo alikuwa akikaa Korintho. (Mdo. 18:5, 18; 1 The. 1:1; 2 The. 1:1) Kwa nini Paulo aliwaandikia Wathesalonike barua ya pili? Inaonekana alipata habari zaidi kuhusu kutaniko, labda kupitia mtu aliyemtuma apeleke barua ya kwanza. Habari alizopata zilimchochea Paulo kuwapongeza akina ndugu kwa upendo na uvumilivu wao na pia kurekebisha maoni ya baadhi ya Wathesalonike ya kwamba kuwapo kwa Bwana kumefika.​—2 The. 1:3-12; 2:1, 2.

      Kutokana na barua ya Paulo kwa Wagalatia inaonekana alikuwa amewatembelea angalau mara mbili kabla ya kuwaandikia. Mwaka wa 47-48 W.K., Paulo na Barnaba walitembelea Antiokia ya Pisidia, Ikoniamu, Listra, na Derbe, majiji yaliyokuwa katika jimbo la Roma lililoitwa Galatia. Mwaka wa 49 W.K., Paulo alirudi katika eneo hilo akiwa na Sila. (Mdo. 13:1–14:23; 16:1-6) Paulo aliandika barua hii kwa sababu ndugu wa uwongo, waliotokea mara tu baada ya ziara ya Paulo, walikuwa wakifundisha kwamba Wakristo wanapaswa kutahiriwa na kushika Sheria ya Musa. Bila shaka, Paulo aliwaandikia Wagalatia mara tu aliposikia kuhusu mafundisho hayo ya uongo. Huenda aliandika barua hiyo akiwa Korintho, lakini inawezekana pia aliiandika akiwa Efeso, muda mfupi alipofika huko akiwa safarini kurudi Antiokia ya Siria au akitoka Antiokia kwenyewe.​—Mdo. 18:18-23.

      “Wakorintho Wengi . . . Wakaanza Kuamini” (Mdo. 18:5-8)

      8, 9. Paulo alifanya nini alipopingwa na Wayahudi aliowahubiria, naye alienda kuhubiri wapi?

      8 Paulo aliiona kazi ya kimwili kuwa njia ya kumtegemeza katika huduma yake. Hilo lilionekana wazi Sila na Timotheo walipowasili kutoka Makedonia wakiwa na zawadi nyingi. (2 Kor. 11:9) Mara moja, Paulo “akaanza kushughulika sana na lile neno [“alianza kutumia wakati wake wote kwa ajili ya kuhubiri,” Biblia Habari Njema].” (Mdo. 18:5) Hata hivyo, Wayahudi aliowahubiria walimpinga. Alijiondolea lawama kwa sababu walikataa ujumbe unaookoa uhai kumhusu Kristo. Paulo alikung’uta mavazi yake na kuwaambia Wayahudi hao waliompinga: “Damu yenu na iwe juu ya vichwa vyenu wenyewe. Mimi ni safi. Kuanzia sasa nitaenda kwa watu wa mataifa.”​—Mdo. 18:6; Eze. 3:18, 19.

      9 Paulo angehubiri wapi? Mtu anayeitwa Titio Yusto, huenda alikuwa Myahudi mgeuzwa imani na ambaye nyumba yake ilikuwa karibu na sinagogi, alimkaribisha Paulo. Hivyo, Paulo akaacha kuhubiri kwenye Sinagogi na kuendelea kuhubiri akiwa kwenye nyumba ya Yusto. (Mdo. 18:7) Paulo aliendelea kuishi katika nyumba ya Akila na Prisila alipokuwa Korintho, lakini aliitumia nyumba ya Yusto kwa ajili ya huduma yake.

      10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo hakuazimia kuwahubiria tu watu wa mataifa?

      10 Paulo aliposema angeenda kwa watu wa mataifa, je alimaanisha hangewahubiria kabisa Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani, kutia ndani wale waliokubali ujumbe wake? Hapana. Kwa mfano, “Krispo, ofisa msimamizi wa sinagogi akamwamini Bwana, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake.” Inaonekana kwamba wengi kati ya wale waliokuwa wakienda katika sinagogi walijiunga na Krispo, kwa sababu Biblia inasema: “Wakorintho wengi waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa.” (Mdo. 18:8) Basi, kutaniko jipya la Kikristo lililoanzishwa jijini Korintho likaanza kukutanika katika nyumba ya Titio Yusto. Ikiwa masimulizi ya kitabu cha Matendo yanafuata mtindo wa Luka—yaani, yanafuatana kulingana na wakati yalipotukia—basi hilo linamaanisha kwamba Wayahudi hao au Wayahudi wageuzwa imani walikuwa Wakristo baada ya Paulo kukung’uta mavazi yake. Ikiwa ndivyo, basi ni wazi kwamba Paulo alikuwa tayari kubadilika kulingana na hali.

      11. Mashahidi wa Yehova leo wanafuata mfano wa Paulo jinsi gani wanapowahubiria watu walio katika dini zinazodai kuwa za Kikristo?

      11 Leo watu katika nchi nyingi wanadai kwamba wao ni washiriki wa kanisa fulani linalomfuata Kristo. Na makanisa hayo yana uvutano mkubwa katika maisha yao. Wamishonari wa dini hizo wamepata wafuasi wengi. Watu wanaodai kuwa Wakristo mara nyingi huwa watumwa wa desturi, kama walivyokuwa Wayahudi wa karne ya kwanza jijini Korintho. Hata hivyo, kama Paulo, sisi hujitahidi kuwasaidia watu hao waelewe mambo wanayosoma katika Biblia zao. Hata wanapotupinga, au viongozi wao wa kidini wanapotunyanyasa, hatukati tamaa. Huenda kuna wapole kadhaa miongoni mwa watu wenye “bidii kwa ajili ya Mungu, lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” Tunahitaji kuwatafuta wapole hao.​—Rom. 10:2.

      “Nina Watu Wengi Katika Jiji Hili” (Mdo. 18:9-17)

      12. Paulo alihakikishiwa nini katika maono?

      12 Ikiwa Paulo alikuwa na mashaka yoyote kuhusu kuendelea na huduma yake jijini Korintho, mashaka hayo yaliisha Bwana Yesu alipomtokea katika maono ya usiku na kumwambia: “Usiogope, bali endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe na hakuna mtu atakayekushambulia ili kukudhuru; kwa maana nina watu wengi katika jiji hili.” (Mdo. 18:9, 10) Hayo yalikuwa maono yenye kutia moyo sana! Bwana mwenyewe alimhakikishia Paulo kwamba angelindwa ili asipatwe na madhara na kuna wengi wanaostahili katika jiji hilo. Paulo alitendaje baada ya kuona maono hayo? Tunasoma hivi: “Akakaa huko kwa mwaka mmoja na miezi sita, akifundisha neno la Mungu kati yao.”​—Mdo. 18:11.

      13. Huenda Paulo alikumbuka tukio gani alipokaribia kiti cha hukumu, lakini kwa nini hali yake ingekuwa tofauti?

      13 Baada ya kukaa Korintho mwaka mmoja hivi, Paulo alipata uthibitisho zaidi kwamba Bwana angemsaidia. “Wayahudi wakaungana, wakamshambulia Paulo na kumpeleka kwenye kiti cha hukumu,” kinachoitwa beʹma. (Mdo. 18:12) Baadhi ya watu husema kwamba kiti hicho cha hukumu kilikuwa juu ya jukwaa lililokuwa karibu na eneo la katikati ya soko la Korintho. Kiti hicho kilitengenezwa kwa marumaru za rangi ya bluu na nyeupe zilizochongwa vizuri. Eneo la mbele la beʹma lilikuwa kubwa na umati mkubwa wa watu ungeweza kukusanyika hapo. Uvumbuzi wa vitu vya kale unaonyesha kwamba huenda kiti hicho cha hukumu kilikuwa karibu sana na sinagogi, na ikiwa ndivyo, basi hakikuwa mbali na nyumba ya Yusto. Paulo alipokaribia beʹma, huenda alikumbuka jinsi Stefano, ambaye huitwa mfia-imani wa kwanza, alivyopigwa mawe. Paulo, ambaye wakati huo aliitwa Sauli, aliunga mkono “kuuawa kwa Stefano.” (Mdo. 8:1) Je, sasa jambo hilohilo lingempata Paulo? Hapana, kwa kuwa Yesu alimwahidi hivi: “Hakuna mtu atakayekushambulia ili kukudhuru.”​—Mdo. 18:10.

      Galio akitupilia mbali kesi ya Paulo mbele ya watu wenye hasira wanaomshtaki. Askari Waroma wakijaribu kutuliza umati wa wanaume wenye hasira.

      “Ndipo akawafukuza kutoka mbele ya kiti cha hukumu.”—Matendo 18:16

      14, 15. (a) Wayahudi walimshtaki Paulo kwa kosa gani, na kwa nini Galio aliitupilia mbali kesi hiyo? (b) Ni nini kilichompata Sosthene, na huenda baadaye alifanya nini?

      14 Ni nini kilichotokea Paulo alipofika kwenye kiti cha hukumu? Hakimu aliyekuwa ameketi juu ya kiti hicho alikuwa liwali Akaya, anayeitwa Galio—kaka ya mwanafalsafa Mroma Seneka. Wayahudi wakamshtaki Paulo: “Mtu huyu anawashawishi watu wamwabudu Mungu kwa njia iliyo kinyume cha sheria.” (Mdo. 18:13) Walidai kwamba Paulo anageuza imani ya watu kinyume cha sheria. Hata hivyo, Galio akaona kwamba Paulo hajafanya “kosa” lolote na hana hatia ya “uhalifu mkubwa.” (Mdo. 18:14) Galio hakuwa na nia yoyote ya kujiingiza katika mizozo ya Wayahudi. Hata kabla ya Paulo kusema neno lolote ili kujitetea, Galio akaitupilia mbali kesi hiyo! Washtaki hao wakakasirika sana. Walimalizia hasira yao kwa Sosthene, ofisa msimamizi wa sinagogi, ambaye huenda alichukua nafasi ya Krispo. Walimkamata Sosthene “na kuanza kumpiga mbele ya kiti cha hukumu.”​—Mdo. 18:17.

      15 Kwa nini Galio hakuuzuia umati usimpige Sosthene? Huenda Galio alifikiri kwamba Sosthene ndiye aliyeuchochea umati huo dhidi ya Paulo na kwa hiyo anapata haki yake. Iwe ndivyo ilivyokuwa au la, kulikuwa na matokeo mazuri. Katika barua yake ya kwanza kwa kutaniko la Korintho, iliyoandikwa miaka kadhaa baadaye, Paulo alimtaja mtu fulani anayeitwa Sosthene akimwita ndugu. (1 Kor. 1:1, 2) Je, huyo ni Sosthene yuleyule aliyepigwa jijini Korintho? Ikiwa ndiye, kisa hicho kilimsaidia Sosthene kuukubali Ukristo.

      16. Maneno ya Bwana, “endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe,” yanatutiaje moyo katika huduma yetu?

      16 Kumbuka kwamba baada ya Wayahudi kumpinga Paulo, Bwana Yesu alimwimarisha na kumwambia, “Usiogope, bali endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe.” (Mdo. 18:9, 10) Tusisahau kamwe maneno hayo, hasa watu wanapokataa ujumbe wetu. Usisahau kamwe kwamba Yehova anasoma mioyo na huwavuta watu wanyofu kwake. (1 Sam. 16:7; Yoh. 6:44) Jambo hilo linatutia moyo tuendelee kuwa na bidii katika huduma! Kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu hubatizwa, hilo linamaanisha kila siku mamia ya watu hubatizwa. Wale wanaotii amri ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ Yesu anawahakikishia hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Mt. 28:19, 20.

      “Yehova Akipenda” (Mdo. 18:18-22)

      17, 18. Huenda Paulo alitafakari nini alipokuwa njiani kuelekea Efeso?

      17 Hatujui ikiwa maoni ya Galio kuelekea watu waliomshtaki Paulo yaliliwezesha kutaniko hilo changa la Kikristo jijini Korintho kukaa kwa amani kwa muda. Hata hivyo, Paulo alikaa “siku kadhaa” kabla ya kuwaaga ndugu zake wa Korintho. Mwaka wa 52 W.K., alipanga kusafiri hadi Siria kutoka bandari ya Kenkrea, kilomita 11 hivi upande wa mashariki wa Korintho. Hata hivyo, kabla ya kuondoka Kenkrea, Paulo “alikuwa amekata nywele zake . . . , kwa sababu alikuwa ameweka nadhiri.”c (Mdo. 18:18) Baadaye, aliwachukua Akila na Prisila na kusafiri katika bahari ya Aegea hadi Efeso katika Asia Ndogo.

      18 Paulo aliposafiri kutoka Kenkrea, inawezekana alikuwa akitafakari maisha yake jijini Korintho. Alikuwa na kumbukumbu kadhaa nzuri na sababu nyingi za kuridhika. Huduma yake ya miezi 18 jijini humo ilikuwa na matokeo mazuri. Kutaniko la kwanza jijini Korintho lilianzishwa, na lilikutana katika nyumba ya Yusto. Yusto, Krispo na familia yake, na wengine wengi walikuwa waamini. Paulo aliwapenda sana waamini hao wapya, kwa sababu aliwasaidia kuwa Wakristo. Baadaye aliwaandikia barua na kuwaita barua za pendekezo zilizoandikwa moyoni mwake. Sisi pia huwa na uhusiano wa karibu na watu tunaowasaidia kukubali ibada ya kweli. Ni jambo lenye kuridhisha sana kuona ‘barua hizo za pendekezo!’​—2 Kor. 3:1-3.

      19, 20. Paulo alifanya nini alipofika Efeso, na tunaweza kujifunza nini kutoka kwake kuhusu kufuatia malengo ya kiroho?

      19 Alipofika Efeso, Paulo alianza kazi yake mara moja. “Akaingia ndani ya sinagogi na kujadiliana na Wayahudi.” (Mdo. 18:19) Pindi hiyo, Paulo alikaa Efeso kwa muda mfupi tu. Ingawa aliombwa akae muda mrefu, “hakukubali.” Alipokuwa akiwaaga, aliwaambia Waefeso: “Nitarudi kwenu tena, Yehova akipenda.” (Mdo. 18:20, 21) Paulo alijua kwamba bado kulikuwa na kazi kubwa ya kuhubiri jijini Efeso. Alipanga kurudi, hata hivyo aliamua kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Je, huo si mfano mzuri tunaoweza kuiga? Tunapofuatia malengo ya kiroho, lazima tuchukue hatua zinazohitajika. Hata hivyo, lazima sikuzote tutegemee mwongozo wa Yehova na kujitahidi kutenda kupatana na mapenzi yake.​—Yak. 4:15.

      20 Akiwaacha Akila na Prisila, Paulo alisafiri baharini hadi Kaisaria. Huenda ‘alipanda’ kwenda Yerusalemu na kulisalimu kutaniko lililokuwa huko. (Mdo. 18:22) Kisha Paulo akarudi nyumbani kwake—Antiokia ya Siria. Alikuwa ameimaliza kwa mafanikio safari yake ya pili ya umishonari. Ni nini kinachomsubiri katika safari yake ya mwisho ya umishonari?

      NADHIRI YA PAULO

      Andiko la Matendo 18:18 linasema kwamba alipokuwa Kenkrea, Paulo “alikuwa amekata nywele zake . . . , kwa sababu alikuwa ameweka nadhiri.” Hiyo ilikuwa nadhiri ya aina gani?

      Kwa kawaida, nadhiri ni ahadi nzito ambayo mtu huweka kwa Mungu kwa hiari, akiahidi kufanya jambo fulani, kutoa toleo, au kuingia katika utumishi fulani. Watu fulani husema kwamba Paulo alikata nywele zake ili kutimiza nadhiri ya Wanadhiri. Hata hivyo, kulingana na Maandiko, baada ya Mnadhiri kumaliza kipindi cha utumishi fulani wa pekee kwa Yehova, alipaswa kunyoa kichwa chake “kwenye mlango wa hema la mkutano.” Inaonekana takwa hilo lingeweza kutekelezwa Yerusalemu wala si Kenkrea.​—Hes. 6:5, 18.

      Masimulizi ya kitabu cha Matendo hayataji Paulo aliweka nadhiri yake wakati gani. Huenda hata aliiweka kabla ya kuwa Mkristo. Pia, masimulizi hayo hayataji iwapo Paulo alimwomba Yehova jambo lolote hususa. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba huenda Paulo alikata nywele zake ili “kumshukuru Mungu kwa ulinzi wake, uliomwezesha kutimiza huduma yake huko Korintho.”

      a Ona Sanduku lenye kichwa “Korintho—Jiji Lenye Bahari Mbili.”

      b Ona Sanduku lenye kichwa “Barua Zenye Kutia Moyo Zilizoongozwa na Roho ya Mungu.”

      c Ona sanduku lenye kichwa “Nadhiri ya Paulo.”

  • Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Upinzani
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 20

      Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Upinzani

      Jinsi Apolo na Paulo walivyochangia ukuzi wa habari njema

      Matendo 18:23–19:41

      1, 2. (a) Paulo na wenzake wanakabili hatari gani Efeso? (b) Tutazungumzia nini katika sura hii?

      WATU jijini Efeso wanapiga kelele na kukimbia mitaani. Umati wa watu unakusanyika, ghasia inatokea! Baadhi ya watu wanawakamata wanaume wawili waliosafiri pamoja na Paulo na kuwaburuta. Watu wamejaa kwenye barabara pana yenye maduka kandokando. Wanajiunga na umati huo wenye hasira, na wote wanaelekea kwenye uwanja wa michezo wa jiji hilo. Uwanja huo ulikuwa mkubwa sana na mashabiki 25,000 wangeweza kukusanyika hapo. Wengi kati ya watu wanaokusanyika hapo hawajui kwa nini ghasia hiyo imetokea, lakini wanahisi kwamba hekalu lao na mungu wao wa kike Artemi yumo hatarini. Hivyo, wote wanaanza kupaaza sauti kwa pamoja kwa kurudia-rudia wakisema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”​—Mdo. 19:34.

      2 Kwa mara nyingine tena, Shetani anajaribu kutumia umati wenye hasira kuzuia habari njema ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, jeuri ni mojawapo tu ya njia anazotumia Shetani. Katika sura hii, tutazungumzia mbinu mbalimbali ambazo Shetani alitumia ili kudhoofisha kazi na umoja wa Wakristo hao wa karne ya kwanza. Lakini, tutaona jinsi ambavyo mbinu zake zote zilishindwa, kwa sababu ‘kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova lilizidi kukua na kusitawi.’ (Mdo. 19:20) Ni nini kilichowasaidia Wakristo hao kusimama imara? Ni kilekile kinachotusaidia leo. Bila shaka, hatutegemei nguvu zetu wenyewe, bali tunamtegemea Yehova. Hata hivyo, kama Wakristo wa karne ya kwanza, lazima tutimize sehemu yetu. Roho takatifu ya Yehova inaweza kutusaidia kukuza sifa zitakazotuwezesha kutimiza huduma yetu kwa mafanikio. Kwanza, acheni tuzungumzie mfano wa Apolo.

      “Alikuwa . . . na Ujuzi Mwingi wa Maandiko” (Mdo. 18:24-28)

      3, 4. Akila na Prisila walitambua nini kuhusu Apolo, nao walimsaidiaje?

      3 Paulo alipoelekea Efeso, katika safari ya tatu ya umishonari, Myahudi anayeitwa Apolo aliwasili jijini humo. Alitoka katika jiji maarufu la Aleksandria, nchini Misri. Apolo alikuwa na sifa za pekee. Alikuwa mwenye ufasaha wa kuzungumza. Isitoshe, “alikuwa . . . na ujuzi mwingi wa Maandiko.” Pia, ‘alikuwa amewaka roho.’ Akiwa mwenye bidii, Apolo alizungumza kwa ujasiri mbele za Wayahudi waliokuwa katika sinagogi.​—Mdo. 18:24, 25.

      4 Akila na Prisila walimsikia Apolo akizungumza. Bila shaka walifurahi walipomwona ‘akifundisha kwa usahihi kumhusu Yesu.’ Mambo aliyosema kumhusu Yesu yalikuwa sahihi. Lakini, baada ya muda mfupi Akila na Prisila wakatambua kwamba kuna jambo muhimu ambalo Apolo haelewi. “Alifahamu ubatizo wa Yohana tu.” Wenzi hao, waliokuwa watengenezaji wa mahema, hawakumwogopa Apolo kwa sababu ya ufasaha na elimu yake. Badala yake, “wakamchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.” (Mdo. 18:25, 26) Mtu huyo mwenye ufasaha na elimu aliitikiaje? Alionyesha mojawapo ya sifa muhimu zaidi ambazo Mkristo anapaswa kusitawisha—sifa ya unyenyekevu.

      5, 6. Ni nini kilichomsaidia Apolo kupata matokeo mazuri katika utumishi wa Yehova, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Apolo?

      5 Kwa kuwa Apolo alikubali msaada wa Akila na Prisila, alipata matokeo mazuri katika utumishi wa Yehova. Alisafiri kwenda Akaya, na akiwa huko, “akawasaidia sana” waabudu wenzake. Pia, aliwahubiria Wayahudi waliokuwa katika eneo hilo ambao walidai kwamba Yesu si Masihi aliyeahidiwa. Luka anasema hivi: “Alithibitisha kikamili . . . kwa juhudi nyingi kwamba Wayahudi walikuwa wamekosea, na kuwaonyesha kwa Maandiko kuwa Yesu ndiye Kristo.” (Mdo. 18:27, 28) Apolo alisaidia sana kutaniko! Kwa kweli, alichangia kusitawi kwa “neno la Yehova.” Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Apolo?

      6 Lazima Wakristo wasitawishe sifa ya unyenyekevu. Kila mmoja wetu ana vipawa mbalimbali—iwe ni uwezo wa asili, uzoefu, au ujuzi ambao tumepata. Hata hivyo, tunapaswa kutambuliwa kwa sababu ya unyenyekevu bali si vipawa vyetu. La sivyo, huenda vipawa vyetu vikatusababishia matatizo. Tunaweza kuanza kuwa na kiburi. (1 Kor. 4:7; Yak. 4:6) Ikiwa kwa kweli sisi ni wanyenyekevu, tutajitahidi kuwaona wengine kuwa bora kuliko sisi. (Flp. 2:3) Hatutakasirika tunaporekebishwa au kukataa tunapofundishwa na wengine. Hatutaendelea kushikilia maoni yetu kwa ushupavu tukijua kwamba hayapatani na mwongozo wa sasa wa roho takatifu. Tukiendelea kuwa wanyenyekevu, Yehova na Mwana wake wataendelea kututumia.​—Luka 1:51, 52.

      7. Paulo na Apolo walionyeshaje sifa ya unyenyekevu, na tunaweza kuwaiga kwa njia gani?

      7 Pia, unyenyekevu huzuia roho ya mashindano. Bila shaka Shetani angependa Wakristo wa karne ya kwanza wawe na migawanyiko. Angefurahi sana ikiwa watu wawili mashuhuri kama vile Apolo na mtume Paulo wangeanza kushindana, huenda hata kuoneana wivu na kujaribu kutafuta wafuasi katika makutaniko! Jambo hilo lingeweza kutokea. Katika jiji la Korintho, Wakristo fulani walianza kusema, “Mimi ni wa Paulo,” huku wengine wakisema, “Lakini mimi ni wa Apolo.” Je, Paulo na Apolo walitaka ndugu na dada wawe na mgawanyiko? Hapana! Badala yake, Paulo alionyesha unyenyekevu kwa kutambua mchango wa Apolo katika kazi ya kuhubiri, na kumpa mapendeleo ya utumishi. Na Apolo alifuata maagizo ya Paulo. (1 Kor. 1:10-12; 3:6, 9; Tito 3:12, 13) Ndugu hao wawili walituwekea mfano mzuri sana wa kufanya kazi bega kwa bega!

      “Kujadiliana kwa Ushawishi Kuhusu Ufalme” (Mdo. 18:23; 19:1-10)

      8. Paulo alipitia njia gani ili kufika Efeso, na kwa nini?

      8 Paulo aliahidi atarudi Efeso, naye alitimiza ahadi hiyo.a (Mdo. 18:20, 21) Hata hivyo, alirudi jinsi gani? Kwa kuwa alikuwa Antiokia ya Siria, angeweza kwenda Seleukia, apande meli, na kusafiri baharini hadi Efeso. Badala yake, alimua ‘kupitia bara.’ Inakadiriwa kwamba, safari ya Paulo inayozungumziwa katika Matendo 18:23 na 19:1, ilikuwa na urefu wa kilomita 1,600 hivi! Kwa nini Paulo aliamua kuzunguka? Kwa sababu lengo lake lilikuwa ‘kuwaimarisha wanafunzi wote.’ (Mdo. 18:23) Safari yake ya tatu ya umishonari, kama zile safari mbili za kwanza, haikuwa rahisi, hata hivyo, hakujuta. Waangalizi wa mzunguko na wake zao leo wanaonyesha roho hiyohiyo. Tunauthamini sana upendo wao wa kujidhabihu!

      EFESO—JIJI KUU LA ASIA

      Efeso lilikuwa jiji kubwa zaidi katika eneo la magharibi la Asia Ndogo. Katika siku za mtume Paulo, inawezekana kwamba jiji hilo lilikuwa na wakazi zaidi ya 250,000. Kwa kuwa lilikuwa jiji kuu la Asia, mkoa wa Roma, lilipewa jina la kifahari “Jiji la Kwanza na Kubwa Zaidi la Asia.”

      Utajiri mkubwa wa Efeso ulitokana na biashara na dini. Jiji la Efeso lilikuwa na bandari ambayo ilikuwa karibu sana na mto ambao mashua zingeweza kupita, na meli za biashara zilitumia bandari hiyo. Lile hekalu maarufu la Artemi na pia mahekalu mengine mengi ya miungu ya Wagiriki, Waroma, Wamisri, na Waasia yalikuwa katika jiji la Efeso.

      Hekalu la Artemi, ambalo ni mojawapo ya maajabu saba ya ulimwengu wa kale, lilikuwa na urefu wa mita 105 na upana wa mita 50 hivi. Lilikuwa na nguzo 100 hivi za marumaru, sehemu ya chini ya kila nguzo ilikuwa na kipenyo cha mita 1.8 hivi na ilikuwa na urefu wa karibu mita 17. Hekalu hilo lilionwa kuwa takatifu katika eneo lote la Mediterania ya kale na fedha nyingi ziliwekwa humo ili zitunzwe na Artemi, hivyo hekalu hilo lilikuwa kituo kikuu cha mabenki barani Asia.

      Majengo mengine muhimu jijini Efeso yalikuwa uwanja wa riadha na huenda ulitumiwa katika maonyesho ya kupigana na watu au wanyama, jumba la maonyesho, ofisi za serikali na masoko na barabara ambazo pembeni kulikuwa na maduka.

      Mwanajiografia Mgiriki, Strabo anasema kwamba bandari ya Efeso ilikuwa ikijaa matope kutoka kwenye mto. Kwa hiyo, baada ya muda meli ziliacha kutumia bandari hiyo. Kwa kuwa leo hakuna jiji lolote la kisasa lililo mahali ambapo jiji hilo la kale lilikuwa, wageni wanaotembelea magofu ya jiji la Efeso, ni kana kwamba wanatembelea ulimwengu wa kale.

      9. Kwa nini wanafunzi fulani walihitaji kubatizwa tena, na tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa chao?

      9 Alipofika Efeso, Paulo alikuta kikundi cha watu kumi na wawili hivi waliokuwa wanafunzi wa Yohana Mbatizaji. Walikuwa wamebatizwa ubatizo wa Yohana ambao haukuwa na maana tena. Isitoshe, hawakuelewa vizuri kazi ya roho takatifu. Paulo aliwasaidia kuelewa ni kwa nini wanapaswa kubatizwa katika jina la Yesu. Kama Apolo, walikuwa wanyenyekevu na wenye hamu ya kujifunza. Baada ya kubatizwa katika jina la Yesu, walipokea roho takatifu na zawadi fulani za kufanya miujiza. Kwa kweli, Yehova huwabariki wale ambao wako tayari kufuata mwongozo mpya unatolewa na tengenezo lake.​—Mdo. 19:1-7.

      10. Kwa nini Paulo alihama kutoka katika sinagogi na kwenda katika ukumbi wa shule, na tunawezaje kumwiga katika huduma yetu?

      10 Si hao tu, wengine pia walifanya maendeleo. Paulo alihubiri kwa ujasiri katika sinagogi kwa miezi mitatu. Ingawa “[alijadiliana] kwa ushawishi kuhusu Ufalme wa Mungu,” baadhi ya wasikilizaji wake walikataa kumsikiliza na kuanza kumpinga. Paulo aliamua kutoa hotuba katika ukumbi wa shule badala ya kupoteza wakati akizungumza na watu waliokuwa “wakizungumza vibaya kuhusu Ile Njia.” (Mdo. 19:8, 9) Watu waliotaka kufanya maendeleo ya kiroho walihitaji kutoka katika sinagogi na kwenda katika ukumbi huo. Kama Paulo, tunaweza kukatisha mazungumzo tunapotambua kwamba mwenye nyumba hataki kusikiliza au anataka tu kubishana. Bado kuna watu wengi walio mfano wa kondoo wanaohitaji kusikiliza ujumbe wetu wenye kutia moyo!

      11, 12. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo alikuwa na bidii na alibadilika kulingana na hali? (b) Mashahidi wa Yehova wanaonyeshaje kwamba wana bidii na wako tayari kubadilika kulingana na hali wanapohubiri?

      11 Inawezekana Paulo alizungumza katika ukumbi huo kuanzia saa tano asubuhi hadi saa kumi jioni. (Mdo. 19:9) Inaonekana kulikuwa na joto kali muda huo na watu wengi waliacha kazi zao ili wale chakula na kupumzika. Ikiwa Paulo alifanya hivyo kwa miaka miwili, basi alitumia zaidi ya saa 3,000 akifundisha.b Hiyo ni sababu nyingine iliyofanya neno la Yehova lizidi kukua na kusitawi. Paulo alikuwa mwenye bidii naye alibadilika kulingana na hali. Alibadili ratiba ya kuhubiri ili aweze kuwasaidia watu wengi zaidi. Alipata matokeo gani? “Wote walioishi katika mkoa wa Asia wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia.” (Mdo. 19:10) Bila shaka alitoa ushahidi kikamili.

      Dada wawili wakihubiri kupitia simu.

      Sisi hujitahidi kuwahubiria watu popote wanapopatikana

      12 Mashahidi wa Yehova leo huhubiri kwa bidii na kubadilika kulingana na hali. Tunajitahidi kuwafikia watu popote walipo na wakati wowote wanapoweza kupatikana. Tunawahubiria barabarani, sokoni, na katika maegesho ya magari. Tunawasiliana na watu kupitia simu au barua. Na tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunajitahidi kufanya hivyo wakati ambapo kuna uwezekano mkubwa wa kuwapata nyumbani.

      Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Roho Waovu (Mdo. 19:11-22)

      13, 14. (a) Yehova alimwezesha Paulo kufanya nini? (b) Wana wa Skewa walifanya kosa gani, na watu wengi leo katika dini zinazodai kuwa za Kikristo wanafanyaje kosa kama hilo?

      13 Luka anatujulisha kwamba kwa muda fulani mambo yalikuwa shwari, na Yehova alimwezesha Paulo kufanya “matendo yenye nguvu yasiyo ya kawaida.” Hata nguo na vitambaa ambavyo Paulo alivaa vilichukuliwa na kupelekwa kwa wagonjwa, nao wakapona. Roho waovu walitolewa kwa njia hiyo pia.c (Mdo. 19:11, 12) Ushindi huo dhidi ya majeshi ya Shetani uliwashangaza watu wengi. Hata hivyo si watu wote waliofurahia jambo hilo.

      14 “Baadhi ya Wayahudi waliosafiri huku na huku wakifukuza roho waovu” walijaribu kuiga miujiza ya Paulo. Baadhi yao walijaribu kufukuza roho waovu kwa kutumia jina la Yesu na Paulo. Luka anasema kwamba wana saba wa Skewa—kutoka katika familia ya kikuhani—walijaribu kufanya hivyo. Roho mwovu aliwaambia: “Ninamjua Yesu nami ninamfahamu Paulo; lakini ninyi ni nani?” Kisha mtu huyo aliyekuwa na roho mwovu, akawarukia na kuwashambulia matapeli hao kama mnyama mwitu, akawajeruhi na kuwatimua wakiwa uchi. (Mdo. 19:13-16) Huo ulikuwa ushindi mkubwa wa “neno la Yehova,” kwa sababu ilionekana wazi kwamba Yehova alimpatia Paulo nguvu nyingi lakini wale wafuasi wa dini za uwongo hawakuwa na nguvu kutoka kwa Yehova. Leo, mamilioni ya watu hufikiri kwamba kuliitia tu jina la Yesu, au kujiita “Mkristo” kunatosha. Hata hivyo, kama Yesu alivyosema, wale wanaofanya mapenzi ya Baba yake ndio tu walio na tumaini hakika la wakati ujao.​—Mt. 7:21-23.

      15. Tunawezaje kuwaiga Waefeso kuhusiana na mazoea ya kuwasiliana na roho, au vitu vinavyohusiana na mazoea hayo?

      15 Ilipojulikana wazi kwamba wana wa Skewa hawana nguvu, watu wengi waliamua kuwa Wakristo na kuacha mazoea ya kuwasiliana na roho. Waefeso wengi waliamini mambo ya uchawi. Watu walifanya mambo ya uchawi na walikuwa na vitu na vitabu vingi vilivyohusiana na mambo hayo. Hivyo, Waefeso wengi walichochewa kutoa vitabu vyao vya uchawi na kuviteketeza hadharani. Kulingana na viwango vya leo, vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya pesa nyingi sana.d Luka anasema: “Hivyo kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi.” (Mdo. 19:17-20) Ulikuwa ushindi mkubwa wa ile kweli dhidi ya uwongo na roho waovu! Watu hao waaminifu walituwekea mfano mzuri tunaoweza kuiga leo. Sisi pia tunaishi katika ulimwengu ambao watu wengi wana mazoea ya kuwasiliana na roho. Tukigundua kwamba tuna kitu fulani kinachohusiana na mazoea hayo, tunapaswa kufanya kama walivyofanya Waefeso—kukiharibu kabisa! Na tuepuke kabisa mazoea hayo yenye kuchukiza, hata ikiwa ni vigumu kufanya hivyo.

      “Kukatokea Mvurugo Mkubwa” (Mdo. 19:23-41)

      Demetrio ameshika sanamu ya fedha ya Artemi, akizungumza kwa hasira na mafundi wa kutengeneza sanamu za fedha jijini Efeso. Nyuma yao, Paulo akiwahubiria watu waliokusanyika sokoni.

      “Wanaume, mnajua vema kwamba tunapata mafanikio yetu kutokana na biashara hii.”—Matendo 19:25

      16, 17. (a) Eleza jinsi Demetrio alivyoanzisha vurugu jijini Efeso. (b) Waefeso walionyeshaje wanashikilia kupita kiasi maoni ya dini yao?

      16 Sasa, hila ya Shetani inaonekana wazi Luka anaposema kwamba “kukatokea mvurugo mkubwa kuhusu Ile Njia.” Ilikuwa hali ya hatari sana.e (Mdo. 19:23) Fundi fulani wa fedha anayeitwa Demetrio ndiye aliyeanzisha vurugu hizo. Aliwachochea mafundi wenzake kwa kuwakumbusha kwamba utajiri wao unatokana na kazi ya kuuza sanamu. Alidai kwamba ujumbe ambao Paulo alihubiri ungeharibu kazi yao, kwa sababu Wakristo hawaabudu sanamu. Kisha akijua kwamba Waefeso hao walijivunia jiji na taifa lao, akawaonya kwamba ikiwa watu watamsikiliza Paulo, mungu wao wa kike Artemi, na hekalu lao linalojulikana ulimwenguni pote, “litaonwa kuwa si kitu.”​—Mdo. 19:24-27.

      17 Njama ya Demetrio ilifanikiwa. Mafundi hao walikasirika na kuanza kupiga kelele “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” Kisha vurugu ikatokea katika jiji hilo kama ilivyosimuliwa mwanzoni mwa sura hii.f Paulo alikuwa jasiri sana na alitaka kwenda kwenye uwanja huo ili azungumze na watu hao, lakini wanafunzi wakasisitiza asijihatarishe. Mtu fulani anayeitwa Aleksanda akasimama mbele ya umati huo na kujaribu kuzungumza. Kwa kuwa alikuwa Myahudi, huenda alitaka kueleza tofauti kati ya Wayahudi na Wakristo hao. Lakini watu hao hawakumsikiliza. Walipotambua kwamba ni Myahudi, walianza kumzomea, na kurudia tena na tena maneno yao “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” kwa muda wa saa mbili hivi. Leo pia kuna watu wanaoshikilia sana maoni au itikadi zao za kidini, na si rahisi kuwafundisha.​—Mdo. 19:28-34.

      18, 19. (a) Karani wa jiji aliunyamazisha jinsi gani umati jijini Efeso? (b) Watu wa Yehova wamelindwa jinsi gani na wenye mamlaka, na wakati mwingine ulinzi huo unategemea nini?

      18 Mwishowe, karani wa jiji akaunyamazisha umati huo. Ofisa huyo alikuwa na usawaziko. Kwanza aliwaambia watu hao wenye hasira kwamba Wakristo hawangeweza kuhatarisha hekalu lao na mungu wao wa kike. Pia aliwaambia kwamba Paulo na wenzake hawajafanya kosa lolote dhidi ya hekalu la Artemi. Na pia aliwaeleza kwamba kuna njia rasmi za kushughulikia mambo kama hayo. Huenda walinyamaza kabisa karani huyo alipowaambia kwamba wasipotulia, watashtakiwa chini ya sheria za Roma kwa kukusanyika kinyume cha sheria na kuanzisha vurugu. Kisha, akawaagiza waondoke. Maneno yenye usawaziko ya ofisa huyo yalituliza hasira za watu hao.​—Mdo. 19:35-41.

      19 Hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa ofisa wa serikali mwenye usawaziko kuingilia kati na kuwalinda wafuasi wa Yesu, na wala haikuwa ya mwisho. Mtume Yohana aliona katika maono kwamba katika siku za mwisho, wenye mamlaka katika ulimwengu huu, wanaofananishwa na dunia, wangemeza maji ya mafuriko ya mateso ya Shetani dhidi ya wafuasi wa Yesu. (Ufu. 12:15, 16) Ndivyo ilivyo leo. Katika visa vingi, mahakimu wenye usawaziko wamelinda haki za Mashahidi wa Yehova za kukutana kwa ajili ya ibada na kuwahubiria wengine habari njema. Bila shaka, nyakati nyingine mwenendo wetu huchangia matokeo mazuri tunayopata. Mwenendo wa Paulo ulifanya apendwe na kuheshimiwa na maofisa fulani wa serikali huko Efeso, nao walitaka awe salama. (Mdo. 19:31) Sikuzote na tujiendeshe kwa unyoofu na heshima. Kufanya hivyo kunaweza kuwa na matokeo mazuri.

      20. (a) Unahisije unapotafakari jinsi neno la Yehova lilivyositawi katika karne ya kwanza na linavyositawi leo? (b) Umeazimia kufanya nini kuhusiana na ushindi wa Yehova katika siku zetu?

      20 Inasisimua kutafakari jinsi ‘neno la Yehova lilivyozidi kukua na kusitawi’ katika karne ya kwanza. Leo, pia, inasisimua kuona jinsi Yehova ametusaidia kupata ushindi mbalimbali. Je, ungependa kushiriki katika ushindi huo hata ikiwa ni kwa kiwango kidogo? Basi jifunze kutokana na mifano ambayo imezungumziwa. Endelea kuwa mnyenyekevu. Mwongozo wa tengenezo la Yehova unapotolewa, ufuate bila kukawia. Endelea kuwa na bidii. Epuka kabisa mazoea ya kuwasiliana na roho. Fanya kila uwezalo ili kutoa ushahidi kamili kupitia mwenendo wako wa unyoofu na heshima.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Efeso—Jiji Kuu la Asia.”

      b Akiwa Efeso, Paulo aliandika barua ya kwanza kwa Wakorintho.

      c Huenda “nguo” zinazotajwa ni vitambaa vya mkononi ambavyo Paulo alijifunga kichwani ili kuzuia jasho lisiingie machoni. Na “vitambaa” alivyojifunga vinadokeza kwamba alikuwa akiendelea na kazi yake ya kutengeneza mahema wakati ambapo hakuwa akihubiri, labda mapema asubuhi.​—Mdo. 20:34, 35.

      d Kulingana na Luka, vitabu hivyo viligharimu vipande 50,000 vya fedha. Ikiwa alikuwa akizungumzia dinari, basi mfanyakazi wa nyakati hizo angehitaji kufanya kazi kila siku kwa siku 50,000—miaka 137 hivi ili kupata pesa hizo.

      e Watu fulani husema kwamba Paulo alikuwa akirejelea tukio hili alipowaambia Wakorintho “hatukuwa na uhakika hata kuhusu uhai wetu.” (2 Kor. 1:8) Hata hivyo, huenda alikuwa akizungumzia pindi nyingine iliyokuwa hatari zaidi. Paulo alipoandika kwamba ‘alipigana na wanyama wa mwituni huko Efeso,’ huenda alikuwa akizungumzia wanyama wakali katika uwanja fulani wa michezo au wanadamu wapinzani. (1 Kor. 15:32) Inawezekana alikabili hali hizo kihalisi au kwa njia ya mfano.

      f Vyama au mashirika kama hayo ya wafanyakazi yanaweza kuwa na nguvu sana. Kwa mfano, karne moja hivi baadaye, chama cha waokaji kilichochea vurugu kama hizo jijini Efeso.

  • “Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 21

      “Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”

      Bidii ya Paulo katika huduma na ushauri wake kwa wazee

      Matendo 20:1-38

      1-3. (a) Eleza matukio ya siku ambayo Eutiko alikufa. (b) Paulo afanya nini, na tukio hilo laonyesha nini kumhusu Paulo?

      PAULO yuko katika chumba cha juu huko Troa. Chumba hicho kimejaa watu. Ana mazungumzo marefu pamoja na akina ndugu, kwa kuwa huu ndio usiku wa mwisho atakaokuwa pamoja nao. Ni usiku wa manane. Kuna taa nyingi zinazowaka chumbani, na kwa hiyo kuna joto jingi na moshi pia. Kijana mmoja anayeitwa Eutiko ameketi dirishani. Paulo anapozungumza, Eutiko analala usingizi mzito na kuanguka nje ya chumba hicho kilicho katika ghorofa ya tatu!

      2 Kwa kuwa ni daktari, huenda Luka ndiye wa kwanza kufika nje ili kuona hali ya kijana huyo. Eutiko ‘anaokotwa akiwa amekufa.’ (Mdo. 20:9) Hata hivyo, muujiza watokea. Paulo akajitupa juu ya kijana huyo na kuuambia umati: “Acheni kupiga kelele, kwa maana yuko hai.” Paulo amemfufua Eutiko!—Mdo. 20:10.

      3 Tukio hilo linaonyesha nguvu za roho takatifu ya Mungu. Paulo hakusababisha kifo cha Eutiko. Hata hivyo, hakutaka kifo cha kijana huyo kivuruge pindi hiyo muhimu au kumkwaza mtu yeyote kiroho. Kwa kumfufua Eutiko, Paulo aliliacha kutaniko likiwa limefarijiwa na likiwa tayari kuendeleza huduma yao. Ni wazi kwamba Paulo alithamini uhai wa wengine. Kumbuka alivyosema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote.” (Mdo. 20:26) Acheni tuone jinsi mfano wa Paulo unavyoweza kutusaidia.

      “Akaanza Safari Yake ya Kwenda Makedonia” (Mdo. 20:1, 2)

      4. Paulo alikabili hali gani yenye kuogopesha?

      4 Kama tulivyoona katika sura ya 20, Paulo alikuwa amekabili hali yenye kuogopesha. Huduma yake katika jiji la Efeso ilisababisha mvurugo. Mafundi wa fedha ambao biashara yao ilitegemea ibada ya Artemi ndio waliochochea mvurugo huo! “Baada ya ghasia kutulia,” andiko la Matendo 20:1 linasema, “Paulo akatuma watu wawaite wanafunzi, akawatia moyo na kuwaaga, kisha akaanza safari yake ya kwenda Makedonia.”

      5, 6. (a) Huenda Paulo alikaa Makedonia kwa muda gani, na aliwafanyia nini akina ndugu huko? (b) Paulo aliwaonaje waamini wenzake?

      5 Alipokuwa akielekea Makedonia, Paulo alifika katika bandari ya Troa na kukaa huko kidogo. Paulo alitazamia kukutana na Tito, aliyekuwa ametumwa Korintho. (2 Kor. 2:12, 13) Hata hivyo, alipoona kwamba Tito hafiki, Paulo akaenda Makedonia, ambako yaelekea alikaa kwa mwaka mmoja hivi na “kuwatia moyo kwa maneno mengi.”a (Mdo. 20:2) Mwishowe, Tito alijiunga na Paulo huko Makedonia, na kumweleza habari njema kuhusu jinsi Wakorintho walivyoitikia barua ya kwanza ya Paulo. (2 Kor. 7:5-7) Hilo lilimchochea Paulo kuwaandikia barua nyingine, ambayo leo twaijua kama Barua ya Pili kwa Wakorintho.

      6 Luka anatumia maneno “akawatia moyo,” na “kuwatia moyo,” anapofafanua ziara ya Paulo kwa akina ndugu wa Efeso na Makedonia. Maneno hayo yanaonyesha vizuri jinsi Paulo alivyowaona waamini wenzake! Tofauti na Mafarisayo, waliowadharau watu, Paulo aliwaona kondoo hao kuwa wafanyakazi wenzake. (Yoh. 7:47-49; 1 Kor. 3:9) Paulo alikuwa na maoni hayo sikuzote, hata wakati ambapo alilazimika kuwapa shauri kali.​—2 Kor. 2:4.

      7. Wazee Wakristo wanaweza kuigaje mfano wa Paulo?

      7 Leo, wazee wa kutaniko na waangalizi wa mzunguko hujitahidi kuiga mfano wa Paulo. Hata wanapotoa karipio, lengo lao ni kuwatia nguvu wale wanaohitaji msaada. Wazee na waangalizi huwahangaikia wengine na kujitahidi kuwatia moyo badala ya kuwashutumu. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi: “Ndugu na dada zetu wengi wanataka kufanya yaliyo sawa, lakini mara nyingi wao huvunjika moyo, huogopa na huhisi kwamba hawajui jambo la kufanya.” Wazee wanaweza kuwatia nguvu waamini wenzao wanaokabili hali kama hizo.​—Ebr. 12:12, 13.

      BARUA AMBAZO PAULO ALIANDIKA ALIPOKUWA MAKEDONIA

      Katika barua yake ya pili kwa Wakorintho, Paulo anasema kwamba alipofika Makedonia, alitaka sana kujua hali ya ndugu wa Korintho. Hata hivyo, Tito alimletea habari njema kutoka Korintho, naye Paulo akafarijika. Kisha, mwaka wa 55 W.K. hivi, Paulo aliandika barua ya Pili kwa Wakorintho, ambamo alionyesha kwamba bado alikuwa Makedonia. (2 Kor. 7:5-7; 9:2-4) Mojawapo ya mambo ambayo Paulo alikuwa nayo akilini wakati huo ni kukamilishwa kwa kazi ya kukusanya michango kwa ajili ya watakatifu huko Yudea. (2 Kor. 8:18-21) Alikuwa pia na wasiwasi kuhusu kuwapo kwa “mitume wa uwongo, wafanyakazi wadanganyifu” katika kutaniko la Korintho.​—2 Kor. 11:5, 13, 14.

      Inawezekana kwamba Paulo aliandika barua ya Tito akiwa Makedonia. Kati ya mwaka wa 61 na 64 W.K., baada ya kufunguliwa kutoka katika utekwa huko Roma, Paulo alitembelea kisiwa cha Krete. Alimwacha Tito huko arekebishe matatizo fulani na kuweka rasmi wazee katika kutaniko. (Tito 1:5) Paulo alimwomba Tito akutane naye huko Nikopoli. Kulikuwa na majiji mengi yaliyoitwa hivyo katika Mediterania ya kale, hata hivyo, yaonekana kwamba Paulo alikuwa akizungumzia jiji la Nikopoli lililokuwa kaskazini magharibi mwa Ugiriki. Yawezekana kwamba Paulo alikuwa akihubiri eneo hilo alipomwandikia Tito.​—Tito 3:12.

      Paulo aliandika barua yake ya kwanza kwa Timotheo katika kipindi hicho pia, alipokuwa amefunguliwa na kabla ya kufungwa tena huko Roma, kati ya mwaka wa 61 na 64 W.K. Katika utangulizi wa barua hiyo, Paulo anataja kwamba alipokuwa akienda Makedonia, alimwomba Timotheo abaki Efeso. (1 Tim. 1:3) Akiwa huko, yaonekana kwamba Paulo alimwandikia Timotheo barua hiyo ili kumpa ushauri kama baba, kumtia moyo, na kumpa maelekezo kuhusu miongozo fulani iliyopaswa kufuatwa katika makutaniko.

      ‘Walitunga Hila Dhidi Yake’ (Mdo. 20:3, 4)

      8, 9. (a) Ni nini kilichokatiza safari ya Paulo kuelekea Siria? (b) Huenda ni nini kilichochochea chuki ya Wayahudi dhidi ya Paulo?

      8 Alipotoka Makedonia, Paulo alienda Korintho.b Baada ya kukaa miezi mitatu huko, alitamani kwenda Kenkrea, ambapo angepanda mashua hadi Siria. Akiwa huko angeweza kwenda Yerusalemu na kuwapa msaada ndugu wenye uhitaji.c (Mdo. 24:17; Rom. 15:25, 26) Lakini, mambo yasiyotazamiwa yalibadili mipango yake. Andiko la Matendo 20:3 linasema hivi: “Wayahudi walikuwa wametunga hila dhidi yake”!

      9 Si ajabu kwamba Wayahudi walimchukia Paulo kwa kuwa walimwona kuwa mwasi imani. Mwanzoni, Paulo alipohubiri Korintho, alimsaidia Krispo kuwa mwamini. Krispo alikuwa kiongozi katika sinagogi. (Mdo. 18:7, 8; 1 Kor. 1:14) Pindi nyingine, Wayahudi waliokuwa Korintho walimshtaki Paulo kwa Galio, liwali wa Akaya. Hata hivyo, Galio aliyatupilia mbali mashtaka hayo na kusema kwamba hayana msingi. Uamuzi huo uliwakasirisha sana adui za Paulo. (Mdo. 18:12-17) Huenda Wayahudi waliokuwa Korintho walijua au walidhani kwamba karibuni Paulo angesafiri kutoka Kenkrea, hivyo wakapanga njama ya kumvamia. Paulo angefanya nini?

      10. Eleza kwa nini Paulo hakutenda kwa woga alipoamua kutoenda Kenkrea.

      10 Akihangaikia usalama wake—na ili kuhakikisha kwamba michango aliyokabidhiwa iko salama—Paulo aliamua kurudi Makedonia badala ya kwenda Kenkrea. Ni kweli kwamba kusafiri barabarani kulikuwa na hatari nyingi. Mara nyingi wezi waliwaibia watu barabarani. Hata nyumba za wageni hazikuwa salama. Hata hivyo, Paulo aliamua kwamba yote hayo ni afadhali kuliko yaliyokuwa yakimsubiri huko Kenkrea. Jambo zuri ni kwamba hakusafiri peke yake. Katika safari hiyo ya umishonari, aliandamana na Aristarko, Gayo, Sekundo, Sopatro, Timotheo, Trofimo, na Tikiko.​—Mdo. 20:3, 4.

      11. Ni kwa njia gani Wakristo leo huchukua hatua zinazohitajika ili kujilinda, na Yesu aliwawekea mfano mzuri jinsi gani?

      11 Kama alivyofanya Paulo, Wakristo leo huchukua hatua zinazohitajika ili kujilinda wanapokuwa katika huduma. Katika maeneo fulani, wao huhubiri wakiwa vikundi—au angalau wawili—badala ya kwenda peke yao. Namna gani mateso? Wakristo wanatambua kwamba hawawezi kuepuka mateso. (Yoh. 15:20; 2 Tim. 3:12) Hata hivyo, hawajiweki katika hali ya hatari. Fikiria mfano wa Yesu. Pindi moja, wapinzani wake katika jiji la Yerusalemu walipookota mawe ili wampige, ‘Yesu alijificha na kuondoka hekaluni.’ (Yoh. 8:59) Baadaye, Wayahudi walipopanga njama ya kumuua, “Yesu hakutembea tena hadharani kati ya Wayahudi, bali alienda katika eneo lililo karibu na nyika.” (Yoh. 11:54) Yesu alichukua hatua zinazohitajika ili kujilinda, maadamu kufanya hivyo hakukupingana na mapenzi ya Mungu. Wakristo pia hufanya hivyo leo.​—Mt. 10:16.

      PAULO APELEKA MISAADA

      Baada ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., Wakristo jijini Yerusalemu walikumbwa na hali nyingi ngumu—njaa, minyanyaso, na uporaji. Kwa sababu hiyo, baadhi yao walikuwa na uhitaji. (Mdo. 11:27–12:1; Ebr. 10:32-34) Hivyo, mnamo mwaka wa 49 W.K., wazee waliokuwa Yerusalemu walipomwagiza Paulo azingatie kazi yake ya kuhubiri hasa miongoni mwa Watu wa Mataifa, walimhimiza ‘awakumbuke maskini.’ Paulo alifanya hivyo kwa kusimamia kutolewa kwa michango katika makutaniko.​—Gal. 2:10.

      Mwaka wa 55 W.K., Paulo aliwaambia Wakorintho hivi: “Fuateni mwongozo niliotoa kwa makutaniko ya Galatia. Siku ya kwanza ya kila juma, kila mmoja wenu anapaswa kuweka kando kitu fulani kulingana na uwezo wake, ili michango isikusanywe nitakapofika. Lakini nitakapofika huko, nitawatuma watu mtakaopendekeza katika barua zenu, wapeleke zawadi yenu ya fadhili Yerusalemu.” (1 Kor. 16:1-3) Mwaka mmoja baadaye, Paulo alipoandika barua yake ya pili kwa Wakorintho, aliwahimiza watayarishe zawadi yao, naye akataja kwamba Wamakedonia pia walikuwa wakitoa michango.​—2 Kor. 8:1–9:15.

      Kwa hiyo, mwaka wa 56 W.K., wawakilishi wa makutaniko mbalimbali walikutana na Paulo na kumkabidhi michango yao. Kwa kuwa wanaume tisa waliandamana na Paulo, kulikuwa na ulinzi, na pia hakuna mtu ambaye angeweza kudai kwamba Paulo ametumia vibaya michango iliyokuwa imetolewa. (2 Kor. 8:20) Kusudi kuu la Paulo kwenda Yerusalemu lilikuwa kupeleka michango hiyo. (Rom. 15:25, 26) Baadaye, Paulo alimwambia hivi Gavana Feliksi: “Baada ya miaka kadhaa, nilirudi ili kuleta zawadi za rehema kwa taifa langu na kutoa matoleo.”​—Mdo. 24:17.

      “Wakafarijika Sana” (Mdo. 20:5-12)

      12, 13. (a) Ufufuo wa Eutiko ulikuwa na matokeo gani kutanikoni? (b) Ni tumaini gani linalopatikana katika Biblia ambalo huwafariji wale wanaofiwa leo?

      12 Baada ya kupita Makedonia, Paulo na wenzake waligawanyika na kwenda sehemu tofauti. Yaonekana kwamba kikundi hicho kilikutana tena Troa.d Masimulizi yanasema: “Siku tano baadaye tukawafikia huko Troa.”e (Mdo. 20:6) Wakiwa Troa ndipo yule kijana Eutiko alipofufuliwa, kama tulivyosoma mwanzoni mwa sura hii. Wazia jinsi akina ndugu walivyohisi walipomwona mwenzao Eutiko akifufuliwa! Masimulizi hayo yanasema kwamba ‘walifarijika sana.’​—Mdo. 20:12.

      13 Bila shaka, miujiza kama hiyo haitokei leo. Hata hivyo, wale ambao wamefiwa ‘hufarijiwa sana’ na tumaini la ufufuo linalopatikana katika Biblia. (Yoh. 5:28, 29) Fikiria hili: Kwa kuwa Eutiko hakuwa mkamilifu, alikufa tena baadaye. (Rom. 6:23) Hata hivyo, watakaofufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu wana tumaini la kuishi milele! Isitoshe, wale wanaofufuliwa wakatawale pamoja na Yesu huko mbinguni huvikwa kutoweza kufa. (1 Kor. 15:51-53) Wakristo leo—iwe ni watiwa mafuta au ni “kondoo wengine”​—wana sababu nzuri ya ‘kufarijiwa sana.’​—Yohana 10:16.

      “Hadharani na Nyumba kwa Nyumba” (Mdo. 20:13-24)

      14. Paulo aliwaambia nini wazee wa Efeso walipokutana naye huko Mileto?

      14 Paulo na wenzake walisafiri kutoka Troa hadi Aso, kisha wakaenda Mitilene, Kio, Samo, na Mileto. Paulo alikusudia kufika Yerusalemu kabla ya Sherehe ya Pentekoste. Kwa kuwa alikuwa na haraka ya kurudi Yerusalemu kabla ya Pentekoste, huenda ndiyo sababu aliamua kutopitia Efeso. Hata hivyo, kwa kuwa Paulo alitaka kuongea na wazee wa Efeso, aliwaomba wakutane naye Mileto. (Mdo. 20:13-17) Walipofika, Paulo aliwaambia hivi: “Mnajua vema jinsi nilivyotenda kati yenu tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia, nilivyomtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote na machozi na majaribu yaliyonipata kupitia hila za Wayahudi, nami sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida na kuwafundisha hadharani na nyumba kwa nyumba. Lakini nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.”​—Mdo. 20:18-21.

      15. Kwa nini sisi huhubiri nyumba kwa nyumba?

      15 Leo, kuna njia nyingi za kuwahubiria watu habari njema. Kama alivyofanya Paulo, sisi hujitahidi kwenda mahali ambapo watu wanapatikana, iwe ni katika vituo vya mabasi, barabara zenye watu wengi, au sokoni. Hata hivyo, njia kuu inayotumiwa na Mashahidi wa Yehova ni kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba kuhubiri nyumba kwa nyumba huwapa watu wote nafasi ya kutosha kuusikia ujumbe wa Ufalme kwa ukawaida, na hilo huonyesha wazi kwamba Mungu hana ubaguzi. Pia, tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kuwasaidia kibinafsi watu wanaopendezwa na ujumbe wetu. Tena, kufanya hivyo hutusaidia kuimarisha imani yetu na kusitawisha sifa ya uvumilivu. Wakristo wa kweli wanajulikana kwa bidii yao katika kuhubiri “hadharani na nyumba kwa nyumba.”

      16, 17. Paulo alionyesha ujasiri wake jinsi gani, na Wakristo leo wanawezaje kufuata mfano wake?

      16 Paulo aliwaeleza wazee wa Efeso kwamba hajui hatari ambazo angepata baada ya kurudi Yerusalemu. Aliwaambia hivi: “Hata hivyo, sioni uhai wangu kuwa muhimu kwangu, mradi tu nimalize mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (Mdo. 20:24) Paulo hakuogopa wala kuruhusu hali yoyote—iwe ni afya mbaya au upinzani mkali—imzuie kutimiza mgawo wake.

      17 Leo pia, Wakristo huvumilia hali nyingi ngumu. Katika nchi fulani wamepigwa marufuku na kuteswa. Wengine hupambana kwa ujasiri na magonjwa ya kimwili au kihisia. Vijana Wakristo hushinikizwa na marafiki shuleni. Vyovyote vile, Mashahidi wa Yehova huonyesha ushikamanifu, kama alivyofanya Paulo. Wameazimia “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.”

      “Jiangalieni Wenyewe na Kundi Lote” (Mdo. 20:25-38)

      18. Paulo aliepuka hatia ya damu jinsi gani, nao wazee wa Efeso wangeweza kufuata mfano wake kwa njia gani?

      18 Paulo aliwahimiza wazee wa Efeso, akitumia mfano wake mwenyewe. Kwanza aliwaambia kwamba huenda hawatamwona tena. Kisha akasema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote, kwa maana sikukosa kuwaambia mashauri yote ya Mungu.” Wazee wa Efeso wangeweza kufuata mfano wa Paulo kwa kuepuka hatia ya damu jinsi gani? Paulo aliwaambia: “Jiangalieni wenyewe na kundi lote, ambalo kati yake roho takatifu imewaweka ninyi rasmi muwe waangalizi, mlichunge kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:26-28) Paulo alionya kwamba “mbwamwitu wenye kukandamiza” wangeingia kutanikoni na “kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” Wazee hao walipaswa kufanya nini? Paulo aliwahimiza hivi: “Endeleeni kukesha, na kukumbuka kwamba kwa miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mmoja kwa machozi.”​—Mdo. 20:29-31.

      19. Ni uasi imani gani uliotokea kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza, nao ulitokeza nini katika karne zilizofuata?

      19 “Mbwamwitu wenye kukandamiza” walianza kutokea mwishoni mwa karne ya kwanza. Mwaka wa 98 hivi W.K., mtume Yohana aliandika: “Hata sasa wapinga-Kristo wengi wametokea . . .  Waliondoka miongoni mwetu, lakini hawakuwa wa namna yetu; kwa maana kama wangekuwa wa namna yetu, wangebaki pamoja nasi.” (1 Yoh. 2:18, 19) Kufikia karne ya tatu, uasi imani ulitokeza makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, na katika karne ya nne, Maliki Konstantino akaidhinisha rasmi “Ukristo” huo bandia. Viongozi wa dini ‘walisema mambo yaliyopotoka’ kwa kuchukua mazoea ya kipagani na kuyafanya yaonekane kuwa ya “Kikristo.” Hata leo hii, matokeo ya uasi imani huo yanaonekana katika mafundisho na desturi ya dini zinazodai kuwa za Kikristo.

      20, 21. Paulo alionyeshaje roho ya kujidhabihu, nao wazee Wakristo wanaweza kufuata mfano wake kwa njia gani leo?

      20 Maisha ya Paulo yalikuwa tofauti kabisa na ya wale ambao baadaye walilitumia kundi vibaya. Alifanya kazi ya kimwili na kujitegemeza ili asiwe mzigo kutanikoni. Paulo aliwatumikia ndugu zake na hakutarajia kupata pesa kutoka kwao. Aliwahimiza wazee wa Efeso waonyeshe roho ya kujidhabihu. Aliwaambia hivi: “Lazima mwasaidie walio dhaifu, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, aliposema: ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’”​—Mdo. 20:35.

      21 Kama alivyofanya Paulo, wazee Wakristo hujidhabihu. Tofauti na makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, wanaofilisi makundi yao, wale walio na jukumu la ‘kulichunga kutaniko la Mungu’ hufanya hivyo bila ubinafsi. Watu wenye kiburi na wanaojitakia makuu hawana nafasi yoyote katika kutaniko la Kikristo. Wale wanaotafuta ‘utukufu wao wenyewe’ mwishowe wataambulia patupu. (Met. 25:27) Sikuzote, kimbelembele huleta aibu.​—Met. 11:2.

      Paulo na waandamani wenzake wakipanda meli. Wazee wa Efeso wakimkumbatia Paulo na kulia.

      “Wote wakalia sana.”—Matendo 20:37

      22. Kwa nini wazee wa Efeso walimpenda sana Paulo?

      22 Kwa kuwa Paulo aliwapenda akina ndugu kikweli, ndugu hao walimpenda sana. Kwa kweli, wakati wake wa kuondoka ulipofika, ‘wote walilia sana, nao wakamkumbatia Paulo na kumbusu kwa upendo.’ (Mdo. 20:37, 38) Wakristo huwathamini na kuwapenda ndugu ambao, kama alivyofanya Paulo, hujitoa wenyewe bila ubinafsi kwa manufaa ya kundi. Unapotafakari mfano mzuri wa Paulo, je, hukubali kwamba hakuwa akijisifu wala kutilia chumvi aliposema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote”?​—Mdo. 20:26.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Barua Ambazo Paulo Aliandika Alipokuwa Makedonia.”

      b Inawezekana Paulo aliandika barua yake kwa Waroma alipokuwa Korintho.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Paulo Apeleka Misaada.”

      d Maneno ya Luka katika Matendo 20:5, 6 yanadokeza kwamba Luka aliungana tena na Paulo huko Filipi. Mapema Paulo alimwacha Luka huko.​—Mdo. 16:10-17, 40.

      e Safari ya kutoka Filipi hadi Troa iliwachukua siku tano. Yawezekana kwamba kulikuwa na upepo mkali, kwa sababu awali safari hiyo iliwachukua siku mbili tu.​—Mdo. 16:11.

  • “Mapenzi ya Yehova na Yatendeke”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 22

      “Mapenzi ya Yehova na Yatendeke”

      Akiwa ameazimia kufanya mapenzi ya Mungu, Paulo anaenda Yerusalemu

      Matendo 21:1-17

      1-4. Kwa nini Paulo anaenda Yerusalemu, na nini kinachomngojea huko?

      WATU wengi wamehuzunika baada ya Paulo kuondoka huko Mileto. Si rahisi kwa Paulo na Luka kuachana na wazee wa Efeso, waliowapenda sana! Wamishonari hao wawili wamesimama kwenye sitaha. Mizigo yao ina vitu wanavyohitaji kwa ajili ya safari. Pia wamebeba michango iliyokusanywa kwa ajili ya Wakristo wenye uhitaji huko Yudea nao wanakusudia kuwasilisha salama zawadi hizo.

      2 Upepo mwanana unajaza matanga na meli yang’oa nanga. Wanaume hao wawili, na wengine saba wanaosafiri pamoja nao, wanawatazama ndugu zao wenye huzuni waliobaki ufuoni. (Mdo. 20:4, 14, 15) Wasafiri hao wanaendelea kupunga mikono mpaka wanapokuwa mbali wasiweze tena kuwaona rafiki zao.

      3 Kwa miaka mitatu hivi, Paulo amekuwa akifanya kazi pamoja na wazee wa Efeso. Lakini sasa, akiongozwa na roho takatifu, anaelekea Yerusalemu. Kwa kiasi fulani, anajua yatakayompata. Awali, aliwaambia wazee hao hivi: “Nikiwa nimefungwa katika roho, ninasafiri kwenda Yerusalemu, ingawa sijui mambo yatakayonipata huko, isipokuwa kutoka jiji mpaka jiji roho takatifu inanitolea ushahidi tena na tena, ikisema kwamba nitafungwa gerezani na kupatwa na dhiki.” (Mdo. 20:22, 23) Licha ya hatari anazokabili, Paulo anahisi kwamba ‘amefungwa katika roho,’ yaani anawajibika na yuko tayari kufuata mwongozo wa roho wa kwenda Yerusalemu. Anathamini uhai wake, hata hivyo, kufanya mapenzi ya Mungu ndilo jambo kuu zaidi maishani mwake.

      4 Je, unahisi hivyo? Tulipojiweka wakfu kwa Yehova, tuliahidi kwamba tutatanguliza mapenzi yake maishani mwetu. Tunaweza kunufaika kwa kuchunguza mfano mzuri wa mtume Paulo.

      Kukiacha Nyuma “Kisiwa cha Kipro” (Mdo. 21:1-3)

      5. Paulo na wenzake walipitia njia gani kwenda Tiro?

      5 Meli ambayo Paulo na wenzake walipanda ‘ilienda moja kwa moja.’ Hilo linamaanisha kwamba kulikuwa na upepo mzuri uliovuma, na meli haikushusha matanga hadi walipofika Kosi siku hiyo. (Mdo. 21:1) Inaonekana kwamba meli hiyo ilitia nanga huko usiku kucha kabla ya kuelekea Rode na Patara. Walipofika Patara, katika pwani ya kusini ya Asia Ndogo, ndugu hao walipanda meli kubwa ya shehena, iliyowapeleka moja kwa moja hadi Tiro, Foinike. Wakiwa njiani, walikiacha nyuma “kisiwa cha Kipro . . . upande wa kushoto.” (Mdo. 21:3) Kwa nini Luka, aliyeandika kitabu cha Matendo, anataja jambo hilo?

      6. (a) Kwa nini yawezekana kwamba Paulo alitiwa moyo alipokiona kisiwa cha Kipro? (b) Unapotafakari jinsi Yehova amekubariki na kukusaidia, unafikia mkataa gani?

      6 Huenda Paulo aliwaonyesha wasafiri wenzake kisiwa hicho na kusimulia mambo aliyojionea alipokuwa huko. Katika safari yake ya kwanza ya umishonari, miaka tisa hivi iliyopita, Paulo, pamoja na Barnaba na Yohana Marko, walikutana na Elima mlozi, aliyepinga kazi yao ya kuhubiri. (Mdo. 13:4-12) Paulo aliimarishwa kukabiliana na mambo yaliyokuwa mbele yao baada ya kukiona kisiwa hicho na kutafakari yaliyotokea. Sisi pia tunaweza kunufaika kwa kutafakari jinsi Yehova ametubariki na kutusaidia kuvumilia majaribu. Tukitafakari kwa njia hiyo tunaweza kuchochewa kusema kama Daudi: “Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.”​—Zab. 34:19.

      ‘Tukawatafuta Wanafunzi na Tukawapata’ (Mdo. 21:4-9)

      7. Paulo na wenzake walifanya nini walipofika Tiro?

      7 Paulo alithamini sana ushirika wa Kikristo naye alipenda kuwa pamoja na waamini wenzake. Walipofika Tiro, Luka anaandika, ‘tukawatafuta wanafunzi na tukawapata.’ (Mdo. 21:4) Wakijua kwamba kuna Wakristo wenzao Tiro, wasafiri hao waliwatafuta na huenda walikaa pamoja nao. Mojawapo ya baraka kubwa za kujua kweli ni kwamba popote tunapoenda, tunaweza kupata waabudu wenzetu ambao watatukaribisha. Waabudu wa Mungu wa kweli wana marafiki ulimwenguni pote.

      8. Andiko la Matendo 21:4 linamaanisha nini?

      8 Akieleza kuhusu siku saba walizokaa Tiro, Luka anataja jambo ambalo mwanzoni linaonekana kuwa lenye kushangaza: “Kupitia roho [akina ndugu wa Tiro] wakamwambia Paulo tena na tena asikanyage Yerusalemu.” (Mdo. 21:4) Je, Yehova alikuwa amebadili nia yake? Je, sasa alikuwa akimzuia Paulo asiende Yerusalemu? Hapana. Roho ilionyesha kwamba Paulo angeteswa Yerusalemu, bali si kwamba asiende huko. Inaonekana kwamba kupitia roho takatifu, ndugu wa Tiro walikuwa sahihi kwamba Paulo angepatwa na matatizo Yerusalemu. Hivyo, wakimhangaikia Paulo, walimhimiza asiende huko. Hangaiko lao la kutaka kumlinda Paulo asipatwe na hatari zilizokuwa zikimngojea linaeleweka. Hata hivyo, akiwa ameazimia kufanya mapenzi ya Yehova, Paulo aliendelea na safari yake hadi Yerusalemu.​—Mdo. 21:12.

      9, 10. (a) Aliposikia mahangaiko ya ndugu zake huko Tiro, inawezekana Paulo alikumbuka hali gani inayofanana na hiyo? (b) Ni maoni gani ambayo yameenea sana ulimwenguni leo, nayo yanatofautiana jinsi gani na maneno ya Yesu?

      9 Aliposikia mahangaiko ya akina ndugu, huenda Paulo alikumbuka kwamba wanafunzi wa Yesu pia, walijaribu kumzuia alipowaambia ataenda Yerusalemu, ateswe, na kuuawa. Akisukumwa na hisia, Petro alimwambia Yesu: “Bwana jihurumie; hutapatwa kamwe na mambo hayo.” Yesu alimjibu: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.” (Mt. 16:21-23) Yesu aliazimia kuishi maisha ya kujidhabihu, jambo ambalo Mungu alikuwa amemtuma afanye. Paulo alihisi hivyo pia. Bila shaka, kama mtume Petro, ndugu wa Tiro walikuwa na nia nzuri, hata hivyo, hawakutambua mapenzi ya Mungu.

      Ndugu asiye na subira anaangalia saa yake akiwa katika huduma ya shambani. Mhubiri mwenzake anamtazama.

      Ili kuwa mfuasi wa Yesu, lazima mtu awe na roho ya kujidhabihu

      10 Watu wengi leo hupenda kujitendea kwa fadhili au kuishi maisha ya starehe. Kwa ujumla watu hutafuta dini ambayo haidai mengi ili wastarehe. Hata hivyo, Yesu aliwahimiza wafuasi wake wawe na maoni tofauti kabisa. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso na aendelee kunifuata.” (Mt. 16:24) Ni jambo la hekima na linalofaa kumfuata Yesu. Hata hivyo, si rahisi kufanya hivyo sikuzote.

      11. Wanafunzi wa Tiro walionyesha jinsi gani upendo wao kwa Paulo na kwamba wanamuunga mkono?

      11 Punde si punde, wakati wa Paulo, Luka, na wenzao kuondoka ukafika. Mambo yaliyotokea wanapoondoka yanagusa moyo sana. Yanaonyesha jinsi akina ndugu wa Tiro walivyompenda Paulo na walivyounga mkono kabisa huduma yake. Wanaume, wanawake, na watoto walimsindikiza Paulo na wenzake hadi ufuoni. Walipiga magoti na kusali pamoja kisha wakaagana. Baadaye, Paulo, Luka, na wenzao wakapanda meli na kuendelea na safari yao hadi Tolemai, ambako waliwakuta akina ndugu na kukaa pamoja nao kwa siku moja.​—Mdo. 21:5-7.

      12, 13. (a) Filipo alikuwa na rekodi ya aina gani ya kutumikia kwa uaminifu? (b) Akina baba Wakristo leo, wanaweza kuiga jinsi gani mfano wa Filipo?

      12 Kisha, Luka anaripoti kwamba Paulo na wasafiri wenzake wakaelekea Kaisaria. Walipofika huko, ‘wakaingia katika nyumba ya Filipo mweneza-injili.’a (Mdo. 21:8) Lazima walifurahi sana kumwona Filipo. Miaka 20 hivi iliyopita huko Yerusalemu, Filipo alikuwa amewekwa rasmi na mitume asaidie kugawanya chakula katika kutaniko jipya la Kikristo. Filipo alikuwa mhubiri mwenye bidii kwa muda mrefu. Kumbuka kwamba wanafunzi walipotawanyika kwa sababu ya mateso, Filipo alienda Samaria na kuanza kuhubiri. Baadaye, alimhubiria na kumbatiza towashi Mwethiopia. (Mdo. 6:2-6; 8:4-13, 26-38) Alikuwa na rekodi nzuri sana ya kutumikia kwa uaminifu!

      13 Filipo hakupunguza bidii yake katika huduma. Akiwa Kaisaria, bado alikuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri, kama Luka anavyoonyesha kwa kumwita “mweneza-injili.” Pia, tunaambiwa kwamba alikuwa na binti wanne waliokuwa wakitoa unabii, jambo linaloonyesha kwamba walifuata mfano wa baba yao.b (Mdo. 21:9) Hivyo, lazima Filipo alikuwa amefanya mengi ili kuijenga nyumba yake kiroho. Akina baba Wakristo wanapaswa kufuata mfano wake, kwa kuwa na bidii katika huduma na kuwasaidia watoto wao waipende kazi ya kuhubiri.

      14. Ziara za Paulo zilitokeza nafasi ya nini, nasi tuna nafasi gani kama hizo leo?

      14 Popote alipoenda, Paulo aliwatafuta waabudu wenzake na kukaa pamoja nao. Akina ndugu walikuwa tayari kumkaribisha mmishonari huyo na wenzake. Bila shaka, ziara hizo zilikuwa pindi za ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12) Kuna nafasi nyingi kama hizo leo. Unaweza kupata baraka nyingi kwa kumkaribisha mwangalizi wa mzunguko na mke wake nyumbani kwako, hata ikiwa hauna vitu vingi vya kimwili.​—Rom. 12:13.

      KAISARIA—JIJI KUU LA MKOA WA YUDEA

      Wakati wa kipindi kinachozungumziwa katika Matendo, Kaisaria lilikuwa jiji kuu la mkoa wa Roma unaoitwa Yudea, alikokuwa gavana na makao makuu ya kijeshi. Herode Mkuu alijenga jiji hilo na kulipa jina kwa heshima ya Kaisari Agusto. Jiji la Kaisaria lilikuwa na mazoea ya kipagani yaliyokuwa yameenea katika majiji ya Kigiriki ya wakati huo. Kulikuwa na hekalu lililowekwa wakfu kwa “mungu” Kaisari, uwanja wa michezo, uwanja wa mashindano ya magari ya kukokotwa, na jumba la maonyesho. Wakazi wengi wa jiji hilo walikuwa Watu wa Mataifa.

      Kaisaria lilikuwa bandari yenye ngome. Herode alitaka bandari yake mpya iwe kubwa kuliko Aleksandria na kuwa kituo kikuu cha kibiashara upande wa mashariki wa Mediterania. Aliiita bandari hiyo Sebasto (au Agusto katika Kigiriki), nayo ilikuwa na ukuta wa kuzuia maji katika ufuo ambao la sivyo meli hazingeweza kutia nanga. Ijapokuwa jiji hilo halikupata umaarufu wa Aleksandria, lilitambuliwa kimataifa kwa sababu lilikuwa mahali ambapo meli nyingi za biashara zilipitia.

      Mweneza-injili Filipo alihubiri habari njema katika jiji hilo la Kaisaria, na yaonekana kwamba alilea familia yake katika jiji hilo. (Mdo. 8:40; 21:8, 9) Lilikuwa kituo cha ofisa wa jeshi Kornelio, na huko ndiko alikopata kuwa mwamini.​—Mdo. 10:1.

      Mtume Paulo alitembelea jiji la Kaisaria mara kadhaa. Muda mfupi baada ya kuwa mwamini, adui zake walipopanga njama ya kumuua, wanafunzi walimpeleka haraka ndugu yao mpya umbali wa kilomita 90 kutoka Yerusalemu hadi Kaisaria kisha wakampandisha meli aende Tarso. Paulo alipitia bandari ya Kaisaria alipokuwa akielekea Yerusalemu mwishoni mwa safari yake ya pili na ya tatu ya umishonari. (Mdo. 9:28-30; 18:21, 22; 21:7, 8) Alizuiliwa kwa miaka miwili jijini Kaisaria katika jumba la kifalme la Herode. Akiwa huko, Paulo alizungumza na Feliksi, Festo, na Agripa, na alipotoka huko akasafiri hadi Roma.​—Mdo. 23:33-35; 24:27–25:4; 27:1.

      JE, WANAWAKE WANAWEZA KUWA WAHUDUMU WAKRISTO?

      Wanawake walikuwa na jukumu gani katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza? Je, wangeweza kuwa wahudumu?

      Yesu aliwaagiza wafuasi wake wahubiri habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 1:8) Wakristo wote wana jukumu la kuwa wahudumu wa habari njema, iwe ni wanaume, wanawake, wavulana, au wasichana. Hilo linaonekana wazi katika unabii wa Yoeli 2:28, 29, ambao mtume Petro alisema kwamba ulitimizwa siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K.: “‘Katika siku za mwisho,’ Mungu asema, ‘Nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila aina ya mwili, na wana wenu na mabinti wenu watatoa unabii, . . . na hata juu ya watumwa wangu wa kiume na watumwa wa kike nitaimimina sehemu ya roho yangu siku hizo, nao watatoa unabii.’” (Mdo. 2:17, 18) Kama tunavyojua mweneza-injili Filipo alikuwa na binti wanne waliokuwa wakitoa unabii.​—Mdo. 21:8, 9.

      Lakini kuhusu kufundisha kutanikoni, Neno la Mungu linasema kwamba wanaume tu ndio wanaoweza kuwekwa rasmi kuwa waangalizi Wakristo na watumishi wa huduma. (1 Tim. 3:1-13; Tito 1:5-9) Paulo alisema hivi: “Simruhusu mwanamke afundishe wala kuwa na mamlaka juu ya mwanamume, bali akae kimya.”​—1 Tim. 2:12.

      “Niko Tayari . . . Kufa” (Mdo. 21:10-14)

      15, 16. Agabo alileta habari gani, nazo zilikuwa na matokeo gani kwa wale waliozisikia?

      15 Paulo alipokuwa akikaa na Filipo, mgeni mwingine aliyeheshimiwa akafika. Jina lake ni Agabo. Waliokuwa wamekusanyika nyumbani kwa Filipo walijua kwamba Agabo ni nabii; alikuwa ametabiri njaa kubwa wakati wa utawala wa Klaudio. (Mdo. 11:27, 28) Huenda walianza kujiuliza: ‘Kwa nini Agabo amekuja? Ana ujumbe gani?’ Walipokuwa wakimtazama kwa makini, alichukua mshipi wa Paulo—kitambaa kirefu ambacho kingeweza kubeba pesa na vitu vingine, nacho kilikuwa kikifungwa kiunoni. Agabo akafunga miguu na mikono yake. Kisha akaanza kuzungumza. Ujumbe wake ulikuwa mzito: “Hivi ndivyo roho takatifu inavyosema, ‘Wayahudi kule Yerusalemu watamfunga hivi mwanamume ambaye mshipi huu ni wake, nao watamtia mikononi mwa watu wa mataifa.’”​—Mdo. 21:11.

      16 Kulingana na unabii huo, ni wazi kwamba Paulo angeenda Yerusalemu. Pia, unabii huo ulionyesha kwamba baadaye Wayahudi wangemtia “mikononi mwa watu wa mataifa.” Unabii huo uliwahangaisha sana wale waliokuwako. Luka anaandika: “Tuliposikia hayo, sisi na wale waliokuwa hapo tukaanza kumsihi Paulo asipande kwenda Yerusalemu. Kisha Paulo akasema: ‘Kwa nini mnalia na kujaribu kunivunja moyo? Muwe na hakika kwamba niko tayari si kufungwa tu bali pia kufa huko Yerusalemu kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.’”​—Mdo. 21:12, 13.

      17, 18. Paulo alionyesha azimio lake jinsi gani, na akina ndugu walitendaje?

      17 Wazia hali hiyo. Akina ndugu, kutia ndani Luka, wanamsihi Paulo asiende. Baadhi yao wanalia. Akichochewa na hangaiko lao lenye upendo kwake, Paulo anasema kwa upole kwamba ‘wanajaribu kumvunja moyo,’ au kama tafsiri fulani zinavyosema, ‘wanaudhoofisha moyo wangu.’ Hata hivyo, azimio lake ni thabiti, na kama vile ilivyokuwa alipokutana na ndugu wa Tiro, hatakubali sihi zao au machozi yao yamfanye akengeuke. Badala yake, anawaeleza kwa nini lazima aende. Alikuwa ameazimia na alionyesha ujasiri! Kama alivyofanya Yesu, Paulo ameazimia kabisa kwenda Yerusalemu. (Ebr. 12:2) Paulo hakutaka kufa kimakusudi kwa sababu ya imani yake, lakini ikiwa angeuawa, angeona kuwa ni jambo la heshima kufa akiwa mfuasi wa Kristo Yesu.

      18 Akina ndugu walitendaje? Waliheshimu msimamo wake. Tunasoma hivi: “Tuliposhindwa kumshawishi, tukaacha kumkataza, tukasema: ‘Mapenzi ya Yehova na yatendeke.’” (Mdo. 21:14) Waliojaribu kumshawishi Paulo asiende Yerusalemu hawakushikilia maoni yao. Walimsikiliza Paulo na kukubali maoni yake, wakitambua na kukubali mapenzi ya Yehova yatendeke, ingawa haikuwa rahisi kwao. Paulo alikuwa ameanza safari ambayo baadaye ingeweza kusababisha kifo chake. Mambo yangekuwa rahisi zaidi kwa Paulo ikiwa ndugu zake wapendwa wasingejaribu kumshawishi asiende.

      19. Tunajifunza jambo gani muhimu kutokana na mambo yaliyompata Paulo?

      19 Tunajifunza jambo muhimu kutokana na mambo yaliyompata Paulo: Hatupaswi kamwe kuwavunja moyo wengine wasiishi maisha ya kujidhabihu katika utumishi wao kwa Mungu. Tunaweza kutumia kanuni hiyo katika hali nyingi, si wakati tu ambapo uhai uko hatarini. Kwa mfano, ingawa wazazi wengi Wakristo huhuzunika watoto wao wanapoondoka nyumbani na kwenda kumtumikia Yehova katika nchi za kigeni, wameazimia kutowavunja moyo. Phyllis, anayeishi Uingereza, anakumbuka jinsi alivyolia sana wakati binti yake wa pekee alipoenda kutumikia akiwa mmishonari barani Afrika. Phyllis anasema hivi: “Nilihuzunika sana. Haikuwa rahisi kwangu kukubali kwamba atakuwa mbali sana. Nilihuzunika, lakini pia nilimwonea fahari. Nilisali sana. Hata hivyo, ulikuwa uamuzi wake, nami sikujaribu kamwe kuubadili. Sikuzote nilikuwa nimemfundisha kutanguliza Ufalme! Ametumikia katika nchi za kigeni kwa miaka 30, nami humshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya uaminifu wake.” Ni jambo zuri sana tunapowatia moyo waabudu wenzetu wanaojidhabihu!

      Picha: Wazazi na wenzi wa ndoa wamishonari. 1. Wazazi wanafurahi kuongea nao kupitia simu. 2. Wenzi wa ndoa wanafurahi kuzungumza nao wanapokuwa katika mgawo wao kwenye nchi ya kigeni.

      Ni vizuri kuwatia moyo waabudu wenzetu wanaojidhabihu

      “Akina Ndugu Wakatukaribisha kwa Furaha” (Mdo. 21:15-17)

      20, 21. Tunajuaje kwamba Paulo alipenda kuwa pamoja na ndugu zake, na kwa nini alipenda kuwa pamoja na waabudu wenzake?

      20 Matayarisho yalifanywa, naye Paulo akaendelea na safari yake, akisindikizwa na akina ndugu ambao kwa kufanya hivyo walimhakikishia kwamba wanamuunga mkono. Kila mahali walipopita katika safari yao kuelekea Yerusalemu, Paulo na wenzake walishirikiana na ndugu na dada zao Wakristo. Katika jiji la Tiro, walipata wanafunzi na kukaa nao siku saba. Walipokuwa Tolemai, waliwasalimu dada na ndugu zao na kukaa huko siku moja. Kaisaria, walikaa siku kadhaa katika nyumba ya Filipo. Kisha, baadhi ya wanafunzi kutoka Kaisaria wakamsindikiza Paulo na wenzake hadi Yerusalemu, ambapo walikaa kwa Mnasoni, mwanafunzi wa awali. Hatimaye, wasafiri hao walipofika Yerusalemu, Luka anaripoti kwamba ‘akina ndugu waliwakaribisha kwa furaha.’​—Mdo. 21:17.

      21 Ni wazi kwamba Paulo alipenda kuwa pamoja na waabudu wenzake. Mtume huyo alitiwa moyo na ndugu na dada zake, kama ilivyo leo. Bila shaka, baada ya Paulo kutiwa moyo na kuimarishwa na akina ndugu, angeweza kukabiliana na wapinzani wenye hasira waliotaka kumuua.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Kaisaria—Jiji Kuu la Mkoa wa Yudea.”

      b Ona sanduku lenye kichwa “Je, Wanawake Wanaweza Kuwa Wahudumu Wakristo?.”

  • “Nisikilizeni Ninapojitetea”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 23

      “Nisikilizeni Ninapojitetea”

      Paulo anaitetea kweli mbele ya umati wenye vurugu na mbele ya Sanhedrini

      Matendo 21:18–23:10

      1, 2. Kwa nini Paulo amerudi Yerusalemu, na atakabili hali gani ngumu?

      YERUSALEMU! Kwa mara nyingine tena Paulo anatembea katika barabara za jiji hilo zenye watu wengi. Jiji hilo ni la pekee katika historia ya watu wa Yehova. Wakazi wengi wa jiji hilo hujivunia historia hiyo ya pekee. Paulo anajua kwamba Wakristo wengi katika jiji hilo wanazingatia kupita kiasi historia hiyo, na si rahisi kwao kukubali njia mpya ya kumwabudu Yehova. Paulo aliamua kutembelea jiji hilo si tu kwa sababu ya uhitaji wa kimwili waliokuwa nao, bali pia uhitaji wa kiroho wa ndugu katika jiji hilo. (Mdo. 19:21) Ameazimia kabisa kulitembelea jiji hilo licha ya hatari zilizopo.

      2 Paulo atakabili hali gani katika jiji la Yerusalemu? Kwanza, kuna uvumi usio wa kweli kumhusu miongoni mwa wafuasi wa Kristo. Hata hivyo, atakabili changamoto kubwa zaidi kutoka kwa adui za Kristo. Watatoa mashtaka ya uwongo dhidi ya Paulo, watampiga, na kujaribu kumuua. Yote hayo yatampa Paulo nafasi ya kujitetea. Unyenyekevu, ujasiri na imani yake katika kushughulikia hali hizo ngumu ni mfano mzuri kwa Wakristo leo. Jinsi gani? Acheni tuone.

      “Wakaanza Kumtukuza Mungu” (Mdo. 21:18-20a)

      3-5. (a) Paulo alihudhuria mkutano gani jijini Yerusalemu, na ni mambo gani yaliyozungumziwa? (b) Tunajifunza nini kutokana na mkutano huo wa Paulo na wazee jijini Yerusalemu?

      3 Siku ya pili baada ya kufika Yerusalemu, Paulo na wenzake walienda kuwaona wazee wenye madaraka kutanikoni. Hakuna yeyote kati ya mitume anayetajwa; huenda kufikia wakati huo walienda kutumikia katika maeneo mengine. Hata hivyo, Yakobo ndugu ya Yesu bado alikuwa huko. (Gal. 2:9) Inawezekana kwamba Yakobo alikuwa mwenyekiti wa mkutano huo, ambapo “wazee wote walikuwapo,” pamoja na Paulo.​—Mdo. 21:18.

      4 Paulo aliwasalimu wazee “na kuanza kusimulia kirefu mambo ambayo Mungu alifanya miongoni mwa mataifa kupitia huduma yake.” (Mdo. 21:19) Wazia jinsi habari hizo zilivyowatia moyo! Leo, sisi pia hufurahia ripoti za maendeleo ya kazi katika nchi nyingine.​—Met. 25:25.

      5 Katika mazungumzo hayo, haikosi Paulo alitaja michango aliyoleta kutoka Ulaya. Lazima ndugu hao waliokuwa wakimsikiliza Paulo waliguswa moyo sana kuona jinsi ndugu zao katika sehemu nyingine wanavyowahangaikia. Baada ya kuisikiliza ripoti ya Paulo, masimulizi yanasema: “[Wazee hao] wakaanza kumtukuza Mungu”! (Mdo. 21:20a) Leo pia, wengi ambao wamekumbwa na majanga au magonjwa huchochewa sana wakati ambapo waabudu wenzao wanatoa misaada na kuwafariji.

      Bado Wengi “Wanafuata Sheria kwa Bidii” (Mdo. 21:20b, 21)

      6. Paulo alijulishwa tatizo gani?

      6 Kisha wazee wakamweleza Paulo kwamba kuna tatizo Yudea ambalo linamhusu. Walisema: “Ndugu, unaona jinsi ambavyo maelfu ya Wayahudi wamekuwa waamini, na wote wanafuata Sheria kwa bidii. Lakini wamesikia uvumi kukuhusu kwamba umekuwa ukiwafundisha Wayahudi wote kati ya mataifa kuiasi sheria ya Musa, ukiwaambia wasiwatahiri watoto wao wala kufuata desturi zilizowekwa.”a—Mdo. 21:20b, 21.

      7, 8. (a) Wakristo wengi wa Yudea walikuwa na maoni gani? (b) Kwa nini maoni yao hayakuwafanya waasi imani?

      7 Miaka 20 baada ya Sheria ya Musa kuondolewa, kwa nini bado Wakristo wengi walikuwa wakiishikilia kwa bidii? (Kol. 2:14) Mwaka wa 49 W.K., mitume na wazee jijini Yerusalemu waliyatumia makutaniko barua wakieleza kwamba waamini kutoka kwa mataifa hawahitaji kutahiriwa wala kuwa chini ya Sheria ya Musa. (Mdo. 15:23-29) Hata hivyo, barua hiyo haikutaja waamini Wayahudi, ambao wengi kati yao hawakuelewa kwamba Sheria ya Musa haitumiki tena.

      8 Je, kutoelewa kwa waabudu hao Wayahudi kulimaanisha kwamba hawakustahili kuendelea kuwa Wakristo? Hapana. Si kwamba walikuwa waabudu wa miungu ya kipagani awali, na sasa walikuwa wakiendeleza mapokeo ya dini zao za zamani. Sheria hiyo ambayo ilikuwa muhimu sana kwa waamini hao Wayahudi, ilitoka kwa Yehova. Sheria yenyewe haikuwa na ubaya wowote, wala haikuwa ya kikatili. Tofauti ni kwamba Sheria hiyo ilikuwa sehemu ya agano la kale, nao Wakristo walikuwa chini ya agano jipya. Kwa hiyo, ibada safi haikutegemea tena kuendelea kulishikilia agano la Sheria. Wakristo Waebrania waliokuwa wakishikilia Sheria kwa bidii hawakuelewa vizuri utendaji wa kutaniko la Kikristo. Walihitaji kupatanisha maoni yao na kweli iliyokuwa ikifunuliwa hatua kwa hatua.b—Yer. 31:31-34; Luka 22:20.

      “Uvumi Walioambiwa Kukuhusu si wa Kweli” (Mdo. 21:22-26)

      9. Paulo alifundisha nini kuhusu Sheria ya Musa?

      9 Namna gani ule uvumi wa kwamba Paulo alikuwa akiwafundisha Wayahudi kati ya mataifa “wasiwatahiri watoto wao wala kufuata desturi zilizowekwa”? Paulo alikuwa mtume kwa Watu wa Mataifa, naye aliposhughulika nao, aliunga mkono uamuzi uliopitishwa wa kwamba Watu wa Mataifa hawahitaji kufuata matakwa ya Sheria. Pia, alifafanua kwa nini ni kosa kwa mtu yeyote kujaribu kuwalazimisha waabudu wa Mataifa watahiriwe ili tu kuonyesha kwamba wanaiheshimu Sheria ya Musa. (Gal. 5:1-7) Katika majiji aliyotembelea, Paulo aliwahubiria habari njema Wayahudi pia. Bila shaka, aliwaeleza waliokuwa tayari kumsikiliza kwamba kifo cha Yesu kiliondolea mbali Sheria na kwamba uadilifu ungepatikana kwa imani, bali si kwa kushika Sheria.​—Rom. 2:28, 29; 3:21-26.

      10. Paulo alionyesha usawaziko jinsi gani kuhusu Sheria na tohara?

      10 Hata hivyo, Paulo alielewa hisia za wale waliokuwa wakiendelea kufuata baadhi ya desturi za Kiyahudi, kama vile kutofanya kazi siku ya Sabato au kutokula vyakula fulani. (Rom. 14:1-6) Naye hakuweka sheria kuhusu tohara. Paulo alimtahiri Timotheo ili Wayahudi wasiwe na shaka kumhusu Timotheo, ambaye baba yake alikuwa Mgiriki. (Mdo. 16:3) Suala la tohara lilikuwa la kibinafsi. Paulo aliwaambia Wagalatia: “Kutahiriwa au kutotahiriwa hakuna faida yoyote, bali imani inayotenda kupitia upendo ina faida.” (Gal. 5:6) Hata hivyo, kutahiriwa ili tu kutimiza Sheria au kudai kwamba lazima mtu atahiriwe ili apate kibali cha Yehova ni kukosa imani.

      11. Wazee walimwagiza Paulo afanye nini, na huenda ni nini kilichohusika? (Ona pia maelezo ya chini.)

      11 Ijapokuwa uvumi uliokuwa umeenea haukuwa wa kweli, bado uliwasumbua waamini Wayahudi. Ndiyo sababu wazee walimwagiza Paulo: “Tuna wanaume wanne waliojiwekea nadhiri. Nenda pamoja na watu hawa ukajitakase kisherehe pamoja nao na kuwagharimia, ili wanyolewe vichwa vyao. Ndipo kila mtu atajua kwamba uvumi walioambiwa kukuhusu si wa kweli, bali unatembea kwa utaratibu, na pia unashika Sheria.”c—Mdo. 21:23, 24.

      12. Paulo alionyeshaje kwamba alikuwa tayari kubadilika kulingana na hali na kufuata maagizo ya wazee wa Yerusalemu?

      12 Paulo angeweza kushikilia msimamo wake na kudai kwamba tatizo si uvumi ulioenea kumhusu, bali ni maoni ya waamini hao Wayahudi kuhusu Sheria ya Musa. Badala ya kufanya hivyo, alikuwa tayari kubadilika kulingana na hali maadamu kufanya hivyo hakungevunja viwango vya Mungu. Mapema alikuwa ameandika hivi: “Kwa wale walio chini ya sheria nilikuwa kama aliye chini ya sheria, ingawa mimi mwenyewe siko chini ya sheria, ili niwapate wale walio chini ya sheria.” (1 Kor. 9:20) Katika kisa hiki, Paulo aliamua kufuata maagizo ya wazee wa Yerusalemu na kuwa “kama aliye chini ya sheria.” Kwa kufanya hivyo, alituwekea kielelezo kizuri cha kufuata maagizo ya wazee badala ya kuamua kufanya mambo kwa njia yetu.​—Ebr. 13:17.

      Picha: 1. Paulo akisikiliza mwongozo wa wazee wa Yerusalemu. 2. Mkutano wa wazee katika siku zetu, ndugu akifikiria kwa makini wazee wengine wanaponyoosha mikono.

      Ikiwa hakuna kanuni za Kimaandiko zilizohusika, Paulo alikuwa tayari kubadilika kulingana na hali. Je, wewe hufanya hivyo?

      SHERIA YA WAROMA NA RAIA WA ROMA

      Kwa kawaida serikali ya Roma haikuingilia mambo ya serikali za mikoa. Kwa ujumla Wayahudi walikuwa na sheria zao. Waroma waliingilia kesi ya Paulo kwa sababu ghasia zilizotokea zingeweza kuvuruga amani.

      Watawala wa Roma walikuwa na mamlaka kubwa juu ya watu wengine waliokuwa wakiishi katika mikoa ya Roma ambao hawakuwa raia wa Roma. Hata hivyo, wenye mamlaka walishughulika kwa njia tofauti na raia wa Roma.f Kuwa raia wa Roma kulimpa mtu haki na uhuru fulani ulioheshimiwa katika milki hiyo yote. Kwa mfano, ilikuwa kinyume cha sheria kwa mtu kumfunga au kumpiga Mroma yeyote ambaye hajahukumiwa hatia, kwa sababu watumwa tu ndio waliotendewa hivyo. Pia, Waroma walikuwa na haki ya kukata rufani kwa maliki aliye Roma dhidi ya uamuzi uliofanywa na mtawala wa mkoa.

      Uraia wa Roma ungeweza kupatikana kwa njia mbalimbali. Kwanza, kupitia urithi. Mara chache Maliki mbalimbali waliwapatia uraia watu au wakaaji wa majiji au wilaya nzima kwa sababu ya huduma zao. Mtumwa aliyenunua uhuru wake kutoka kwa raia wa Roma, mtumwa aliyewekwa huru na Mroma, au askari asiye Mroma ambaye aliachishwa kazi kutoka katika jeshi la Roma angeweza kuwa raia wa Roma. Inaonekana katika hali fulani ingewezekana kununua uraia. Ndiyo sababu kiongozi wa kijeshi Klaudio Lisia alimwambia hivi Paulo: “Mimi nilinunua haki hizo za kuwa raia kwa pesa nyingi.” Paulo akasema: “Lakini mimi nina haki hizo kwa kuzaliwa.” (Mdo. 22:28) Hivyo, inawezekana kwamba mmoja wa babu za Paulo alipata uraia wa Roma, ingawa hakuna uthibitisho.

      f Katika karne ya kwanza W.K., hakukuwa na Waroma wengi katika mkoa wa Yudea. Kuanzia karne ya tatu ndipo watu waliokuwa wakiishi katika mikoa ya Roma walianza kupewa uraia.

      “Hafai Kuishi!” (Mdo. 21:27–22:30)

      13. (a) Kwa nini baadhi ya Wayahudi walisababisha mvurugo hekaluni? (b) Paulo aliokolewaje?

      13 Mambo hayakwenda vizuri hekaluni. Kadiri siku za nadhiri zilivyokuwa zinakaribia kwisha, Wayahudi kutoka Asia walimwona Paulo, wakamshtaki kwa uwongo kwamba amewaingiza Watu wa Mataifa hekaluni, na kusababisha mvurugo. Kama kiongozi wa jeshi la Roma hangeingilia kati, Paulo angepigwa na kuuawa. Hata hivyo, kiongozi huyo akamfunga. Tangu siku hiyo, Paulo alikaa gerezani kwa zaidi ya miaka minne kabla ya kufunguliwa. Nazo hatari zilizomkabili hazikuwa zimeisha. Kiongozi alipowauliza Wayahudi kwa nini walimshambulia Paulo, umati huo ulitoa mashtaka mbalimbali. Kwa sababu kulikuwa na vurugu, kiongozi huyo hangeweza kusikia chochote. Ilibidi Paulo aondolewe hapo. Paulo na askari jeshi wa Roma walipokaribia kuingia katika makao ya askari jeshi, Paulo alimwambia kiongozi huyo: “Nakuomba uniruhusu nizungumze na watu hawa.” (Mdo. 21:39) Kiongozi alikubali, naye Paulo akaitetea imani yake kwa ujasiri.

      14, 15. (a) Paulo aliwaeleza Wayahudi nini? (b) Kiongozi wa jeshi la Roma alichukua hatua gani ili kujua kwa nini Wayahudi wana hasira kali hivyo?

      14 Paulo alianza kwa kusema: “Nisikilizeni ninapojitetea.” (Mdo. 22:1) Paulo alihutubia umati huo kwa Kiebrania, jambo lililowatuliza. Aliwaeleza kwa unyoofu kwa nini yeye ni mfuasi wa Kristo. Kwa ustadi, Paulo alitoa hoja ambazo Wayahudi hao wangeweza kuthibitisha ikiwa wangetaka. Paulo alikuwa amesomea miguuni pa Gamalieli, aliyejulikana sana, naye alikuwa amewanyanyasa wafuasi wa Kristo, kama vile baadhi ya watu katika umati huo wanavyojua. Hata hivyo, alipokuwa njiani kuelekea Damasko aliona maono. Katika maono hayo, Kristo aliyekuwa amefufuliwa alizungumza naye. Watu waliokuwa wakisafiri na Paulo waliona nuru nyangavu na kusikia sauti, lakini hawakuelewa maana ya maneno yaliyosemwa. (Mdo. 9:7; 22:9) Kisha, Paulo aliyekuwa amepofushwa na maono hayo, aliongozwa na wenzake hadi Damasko. Akiwa huko Anania, aliyejulikana na Wayahudi wa eneo hilo, alimponya Paulo kimuujiza.

      15 Paulo alisema kwamba baada ya kurudi Yerusalemu, Yesu alimtokea tena akiwa hekaluni. Waliposikia hilo, Wayahudi wakakasirika sana na kuanza kupiga kelele wakisema: “Mwondoeni duniani mtu kama huyu, hafai kuishi!” (Mdo. 22:22) Ili kumwokoa Paulo, kiongozi wa jeshi akaagiza apelekwe ndani ya kambi ya askari jeshi. Akitaka kujua ni kwa nini Wayahudi hao wana hasira kali hivyo kumwelekea Paulo, kiongozi huyo akaamuru ahojiwe huku akipigwa mijeledi. Paulo aliamua kutumia ulinzi wa kisheria na kusema kwamba yeye ni raia wa Roma. Leo pia, waabudu wa Yehova hutumia ulinzi wa kisheria kutetea imani yao. (Ona sanduku lenye kichwa “Sheria ya Waroma na Raia wa Roma,” na “Kesi za Kisheria Katika Siku Zetu.”) Baada ya kusikia kwamba Paulo ni raia wa Roma, kiongozi huyo alihitaji kutafuta njia nyingine ya kupata habari. Siku iliyofuata, alimleta Paulo mbele ya mkutano wa pekee wa mahakama kuu ya Wayahudi inayoitwa Sanhedrini.

      KESI ZA KISHERIA KATIKA SIKU ZETU

      Kama mtume Paulo alivyofanya, Mashahidi wa Yehova katika siku zetu wamechukua hatua za kisheria kupinga vizuizi vyovyote vinavyowekwa katika kazi yao ya kuhubiri. Wamekuwa na bidii katika “kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”​—Flp. 1:7.

      Katika miaka ya 1920 na 1930, mamia ya akina ndugu walikamatwa kwa sababu ya kugawanya vitabu na magazeti yanayotegemea Biblia. Kwa mfano, kufikia mwaka 1926, kulikuwa na kesi 897 katika mahakama za Ujerumani. Ili kushughulikia kesi zote hizo, Idara ya Sheria ilianzishwa katika ofisi ya tawi ya Ujerumani. Katika miaka ya 1930, mamia ya ndugu na dada walikuwa wakikamatwa kila mwaka kwa sababu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba katika nchi ya Marekani peke yake. Mnamo 1936, idadi hiyo ilifikia 1,149. Ili kushughulikia visa hivyo, Idara ya Sheria ilianzishwa pia nchini Marekani. Tangu mwaka wa 1933 hadi 1939, Mashahidi wa Yehova nchini Rumania walikuwa na kesi 530 mahakamani. Hata hivyo, walishinda katika rufani nyingi zilizokatwa katika Mahakama Kuu. Hali kama hizo zimetokea katika nchi nyingine nyingi.

      Nyakati nyingine matatizo hutokea kwa kuwa Wakristo hawawezi kujihusisha katika utendaji fulani kwa sababu kufanya hivyo kungevunja msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. (Isa. 2:2-4; Yoh. 17:14) Wapinzani hudai kwamba Mashahidi ni wachochezi, jambo ambalo wakati mwingine limesababisha kazi yao ipigwe marufuku. Hata hivyo, kadiri miaka inavyopita, serikali nyingi zimeona kwamba Mashahidi wa Yehova si tisho hata kidogo.g

      g Unaweza kupata habari zaidi kuhusu ushindi mbalimbali wa kisheria ambao Mashahidi wa Yehova wamepata katika nchi nyingi, katika sura ya 15 ya kitabu Ufalme wa Mungu Unatawala! na sura ya 30 ya kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.

      “Mimi Ni Farisayo” (Mdo. 23:1-10)

      16, 17. (a) Eleza kilichotokea Paulo alipokuwa akijitetea mbele ya Sanhedrini. (b) Alipopigwa, Paulo alionyeshaje unyenyekevu?

      16 Paulo alianza kujitetea mbele ya mahakama hiyo kwa kusema: “Wanaume, akina ndugu, nimetenda kwa dhamiri safi kabisa mbele za Mungu mpaka leo hii.” (Mdo. 23:1) Kabla hajasema zaidi, “kuhani mkuu Anania akawaagiza wale waliosimama kando yake wampige kofi mdomoni.” (Mdo. 23:2) Alimdharau sana! Tendo hilo lilionyesha chuki aliyokuwa nayo. Ni kana kwamba alisema Paulo ni mwongo hata kabla ya kumsikiliza! Si ajabu Paulo alisema: “Mungu atakupiga wewe, ewe ukuta uliopakwa chokaa. Je, unaketi kunihukumu kulingana na Sheria na wakati uleule unaivunja Sheria hiyo kwa kuamuru nipigwe?”​—Mdo. 23:3.

      17 Baadhi ya wale waliokuwa wamesimama hapo wakashangazwa—si na yule aliyempiga Paulo, bali na jibu la Paulo! Wakamuuliza: “Je, unamtukana kuhani mkuu wa Mungu?” Jibu la Paulo lilionyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu na pia anaiheshimu Sheria. Alisema: “Akina ndugu, sikujua yeye ni kuhani mkuu. Kwa maana imeandikwa, ‘Usiseme vibaya juu ya mtawala wa watu wako.’”d (Mdo. 23:4, 5; Kut. 22:28) Paulo akabadili njia yake. Akijua kwamba washiriki wa mahakama hiyo ni Mafarisayo na Masadukayo, akasema: “Wanaume, akina ndugu, mimi ni Farisayo, mwana wa Mafarisayo. Ninahukumiwa kwa sababu ya tumaini la ufufuo wa wafu.”​—Mdo. 23:6.

      Kasisi akiangalia kwa makini andiko katika Biblia yake huku ndugu akimhubiria.

      Kama Paulo alivyofanya, sisi hujaribu kuweka msingi mzuri wa mazungumzo tunapozungumza na watu wenye imani tofauti

      18. Kwa nini Paulo alijiita Farisayo, nasi tunaweza kufuata mfano wake jinsi gani?

      18 Kwa nini Paulo anajiita Farisayo? Kwa sababu alikuwa “mwana wa Mafarisayo” kutoka katika familia ya Kifarisayo. Kwa hiyo, machoni pa wengi alionwa kuwa Farisayo.e Hata hivyo, je, imani ya Paulo kuhusu ufufuo ilikuwa sawa na ya Mafarisayo? Mafarisayo waliamini nafsi haifi, na kwamba nafsi ya waadilifu huishi tena katika miili ya binadamu. Bila shaka, Paulo hakuamini hivyo bali aliamini ufufuo uliofundishwa na Yesu. (Yoh. 5:25-29) Hata hivyo, sawa na Mafarisayo, Paulo aliamini kwamba kuna tumaini la ufufuo. Kwa upande mwingine, Masadukayo hawakuamini kuna ufufuo. Tunaweza kufuata mfano wake tunapowahubiria Wakatoliki au Waprotestanti. Tunaweza kuwaambia sisi pia tunaamini kuna Mungu. Ingawa wanaamini Utatu, sisi tunamwamini Mungu anayetajwa katika Biblia. Hivyo, sote tunaamini kwamba kuna Mungu.

      19. Kwa nini kulikuwa na vurugu mahakamani?

      19 Maneno ya Paulo yalitokeza mgawanyiko. Simulizi hilo linasema: “Kukawa na vurugu, na baadhi ya waandishi wa chama cha Mafarisayo wakasimama na kuanza kubishana kwa ukali, wakisema: “Hatuoni kosa lolote katika mtu huyu, lakini ikiwa roho au malaika alizungumza naye—.’” (Mdo. 23:9) Wazo la kwamba huenda Paulo alikuwa ameongea na malaika, liliwachukiza sana Masadukayo ambao hawakuamini malaika! (Ona sanduku lenye kichwa “Masadukayo na Mafarisayo.”) Vurugu hizo zilikuwa kubwa sana hivi kwamba yule kiongozi akalazimika kumwokoa tena mtume huyo. (Mdo. 23:10) Hata hivyo, bado Paulo alikuwa hatarini. Ni nini kitakachompata mtume huyo? Tutaona katika sura inayofuata.

      MASADUKAYO NA MAFARISAYO

      Sanhedrini, baraza la kitaifa la usimamizi na mahakama kuu ya Wayahudi, ilifanyizwa na vikundi viwili vikuu—Masadukayo na Mafarisayo. Kulingana na mwanahistoria wa karne ya kwanza Flavio Yosefo, tofauti kubwa kati ya vikundi hivyo viwili ni kwamba Mafarisayo walitaka kuwatwika watu desturi nyingi, nao Masadukayo walishikilia mambo yaliyokuwa katika Sheria ya Musa tu. Vikundi vyote viwili vilimpinga Yesu.

      Inaonekana Masadukayo, ambao kwa ujumla hawakupenda mabadiliko, walikuwa na uhusiano wa karibu na makuhani. Pia, huenda Anasi na Kayafa waliotumikia wakiwa makuhani wakuu, walikuwa Masadukayo. (Mdo. 5:17) Hata hivyo, mwanahistoria Yosefo anasema kwamba mafundisho yao “hayakuvutia watu wowote isipokuwa matajiri.”

      Kwa upande mwingine, Mafarisayo, walikuwa na uvutano mkubwa kwa watu wa kawaida. Hata hivyo, maoni yao, ambayo yalitia ndani kushikilia sana utakaso wa kisherehe, yalifanya iwe vigumu kwa watu kushika Sheria. Tofauti na Masadukayo, Mafarisayo waliamini kwamba kila jambo linalompata mtu limeamuliwa mapema na kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mwili kufa, nayo huthawabishwa au huadhibiwa kulingana na mema au mabaya iliyotenda.

      a Ili kushughulikia mahitaji ya kiroho ya idadi kubwa ya Wakristo Wayahudi, lazima kulikuwa na makutaniko mengi yaliyokuwa yakikutana katika nyumba za watu binafsi.

      b Miaka michache baadaye, mtume Paulo aliandika barua yake kwa Waebrania, ambamo alithibitisha ubora wa agano jipya. Katika barua hiyo, alionyesha wazi kwamba kuanzishwa kwa agano jipya kuliondolea mbali agano la kale. Mbali na kutoa hoja zenye kusadikisha ambazo Wakristo Wayahudi wangeweza kutumia kuwajibu Wayahudi waliowapinga, hoja za Paulo ziliimarisha imani ya baadhi ya Wakristo waliokuwa wakishikilia kupita kiasi Sheria ya Musa.​—Ebr. 8:7-13.

      c Wasomi fulani wanadokeza kwamba watu hao walikuwa wameweka Nadhiri. (Hes. 6:1-21) Ni kweli kwamba Sheria ya Musa, iliyotumika kuweka nadhiri hizo, haikuwa ikitumika tena. Hata hivyo, huenda Paulo aliona kwamba hakuna ubaya kwa watu hao kutimiza nadhiri waliyoweka kwa Yehova. Kwa hiyo, haingekuwa vibaya kulipa gharama zao na kuandamana nao. Hatujui ni nadhiri ya aina gani iliyowekwa, hata hivyo, haielekei kwamba Paulo angeshiriki kutoa dhabihu ya mnyama (kama Wanadhiri walivyofanya), akiamini kwamba ingesafisha dhambi za mtu. Dhabihu kamilifu ya Kristo ilikuwa imeondolea mbali uwezo wa dhabihu hizo kusafisha dhambi. Vyovyote vile, tuna hakika kwamba Paulo hangekubali kufanya chochote ambacho kingechafua dhamiri yake.

      d Watu fulani wamesema kwamba inawezekana Paulo hakuwa akiona vizuri kwa hiyo hakumtambua kuhani mkuu. Au huenda alikuwa mbali na Yerusalemu kwa muda mrefu sana hivi kwamba hakumjua kuhani mkuu wa wakati huo. Au kwa sababu ya umati wa watu uliokuwapo labda Paulo hangeweza kuona ni nani aliyetoa amri apigwe.

      e Mwaka wa 49 W.K., mitume na wazee walipokuwa wakijadiliana ikiwa Watu wa Mataifa wanapaswa kushika Sheria ya Musa, baadhi ya Wakristo waliokuwako waliitwa “baadhi ya wale wa madhehebu ya Mafarisayo ambao sasa walikuwa waamini.” (Mdo. 15:5) Inaonekana kwa kiasi fulani waamini hao walikuwa bado wakihusianishwa na asili yao ya Kifarisayo.

  • “Jipe Moyo!”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 24

      “Jipe Moyo!”

      Paulo anusurika kifo na anajitetea mbele ya Feliksi

      Matendo 23:11–24:27

      1, 2. Kwa nini Paulo hashangazwi na mateso anayokabili jijini Yerusalemu?

      BAADA ya kuokolewa kutoka kwenye umati wenye hasira kali jijini Yerusalemu, Paulo awekwa kizuizini tena. Mateso anayokabili katika jiji la Yerusalemu hayamshangazi mtume huyo mwenye bidii. Aliambiwa atazamie ‘kufungwa gerezani na kupatwa na dhiki’ katika jiji hilo. (Mdo. 20:22, 23) Ijapokuwa Paulo hajui kitakachompata, anajua kwamba atateseka kwa ajili ya jina la Yesu.​—Mdo. 9:16.

      2 Hata manabii Wakristo walimwonya Paulo kwamba atafungwa na kutiwa “mikononi mwa watu wa mataifa.” (Mdo. 21:4, 10, 11) Siku chache zilizotangulia, umati wa Wayahudi ulijaribu kumuua, na muda mfupi baadaye, washiriki wa Sanhedrini karibu ‘wangemrarua-rarua’ walipokuwa wakibishana kwa sababu ya mambo aliyosema. Sasa mtume huyo ni mfungwa chini ya ulinzi wa askari jeshi Waroma, akikabili kesi na mashtaka mengi. (Mdo. 21:31; 23:10) Bila shaka, mtume Paulo anahitaji kutiwa moyo!

      3. Sisi hutiwa moyo jinsi gani kuendelea kuhubiri?

      3 Katika siku hizi za mwisho, tunajua kwamba “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:12) Mara kwa mara, sisi pia tunahitaji kutiwa moyo ili tuendelee katika kazi yetu ya kuhubiri. Tunathamini sana maneno yenye kutia moyo na yenye kufariji tunayopata kwa wakati unaofaa, kupitia machapisho na mikutano inayotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”! (Mt. 24:45) Yehova ametuhakikishia kwamba hakuna adui wa habari njema atakayefanikiwa. Hawawezi kuwaangamiza watumishi wake wakiwa kikundi wala kukomesha kazi yao ya kuhubiri. (Isa. 54:17; Yer. 1:19) Namna gani mtume Paulo? Je, alitiwa moyo kuendelea kutoa ushahidi kamili licha ya upinzani? Ikiwa ndivyo, alitiwa moyo jinsi gani, naye alifanya nini?

      ‘Hila Iliyofungwa kwa Kiapo’ Yazimwa (Mdo. 23:11-34)

      4, 5. Paulo alitiwa moyo jinsi gani, na kwa nini alitiwa moyo kwa wakati unaofaa?

      4 Mtume Paulo alitiwa moyo sana usiku uliofuata, baada ya kuokolewa kutoka kwa Sanhedrini. Masimulizi yaliyoongozwa na roho yanasema: “Bwana akasimama kando yake na kumwambia: ‘Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili kunihusu katika Yerusalemu, ndivyo utakavyotoa ushahidi huko Roma pia.’” (Mdo. 23:11) Maneno hayo ya Yesu yanayotia moyo yalimhakikishia Paulo kwamba atakombolewa. Alijua kwamba atafika Roma na kutoa ushahidi kumhusu Yesu.

      Mpwa wa Paulo akiongea na Klaudio Lisia.

      “Wanaume zaidi ya 40 kati yao walio tayari kumvizia.”—Matendo 23:21

      5 Paulo alitiwa moyo kwa wakati unaofaa. Siku iliyofuata, wanaume Wayahudi zaidi ya 40, “wakafanya hila na kujifunga kwa kiapo cha laana, wakisema hawatakula wala kunywa mpaka watakapomuua Paulo.” ‘Hila iliyofungwa kwa kiapo,’ ilionyesha jinsi Wayahudi hao walivyoazimia kabisa kumuua mtume huyo. Waliamini kwamba, ikiwa hawangefanikiwa katika hila yao, basi wangestahili kulaaniwa, au kupatwa na mabaya. (Mdo. 23:12-15) Wakiwa na kibali cha wakuu wa makuhani na wazee, walipanga Paulo arudishwe mbele ya mahakama ya Sanhedrini ili kujibu maswali zaidi, kana kwamba kuna mambo yanayomhusu ambayo wanataka kuhakikisha. Hata hivyo, lengo lao lilikuwa kumvizia Paulo akiwa njiani na kumuua.

      6. Njama ya kumuua Paulo ilifunuliwaje, na vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa mpwa wa Paulo?

      6 Hata hivyo, mpwa wa Paulo alipata habari kuhusu njama hiyo, naye akamjulisha Paulo. Kisha, Paulo akamwagiza kijana huyo amwambie Klaudio Lisia, kiongozi wa jeshi la Roma. (Mdo. 23:16-22) Bila shaka, Yehova anawapenda vijana ambao, kama mpwa huyo wa Paulo, hutanguliza kwa ujasiri hali njema ya watu wa Mungu na kufanya kwa uaminifu yote wawezayo ili kuendeleza kazi ya Ufalme.

      7, 8. Klaudio Lisia alifanya nini ili kuhakikisha usalama wa Paulo?

      7 Mara tu baada ya kuambiwa kuhusu njama iliyopangwa dhidi ya Paulo, Klaudio Lisia, aliyekuwa akisimamia askari 1,000, akaamuru kikosi cha askari 470—askari jeshi, wenye mikuki, na wapanda farasi—kiende Yerusalemu usiku huo na kumsindikiza Paulo mpaka Kaisaria. Akiwa huko alipaswa kufikishwa mbele ya Gavana Feliksi.a Jiji la Kaisaria lilikuwa kituo cha serikali ya Roma katika mkoa wa Yudea. Kulikuwa na Wayahudi wengi, lakini wakaaji wengi zaidi walikuwa Watu wa Mataifa. Mkoa huo ulikuwa tofauti kabisa na Yerusalemu, ambako watu wengi walionyesha chuki ya kidini na kusababisha ghasia. Kaisaria lilikuwa pia makao makuu ya majeshi ya Roma katika mkoa wa Yudea.

      8 Kupatana na sheria za Roma, Lisia alimtumia Feliksi barua kumweleza mashtaka yaliyotolewa. Lisia alitaja kwamba alipojua Paulo ni raia wa Roma, alimwokoa ili ‘asiuawe’ na Wayahudi. Lisia alisema kwamba hakumpata Paulo na hatia yoyote ya ‘kustahili kifo au kufungwa gerezani,’ lakini kwa sababu ya hila iliyopangwa dhidi ya Paulo, alimtuma kwa Feliksi ili awasikilize wanaomshtaki na kutoa hukumu.​—Mdo. 23:25-30.

      9. (a) Haki za Paulo akiwa raia wa Roma zilikiukwa jinsi gani? (b) Kwa nini huenda tukahitaji kutumia haki zetu tukiwa raia wa nchi?

      9 Je, mambo yote ambayo Lisia aliandika yalikuwa kweli? Hapana. Inaonekana alikuwa anajitafutia sifa. Ukweli ni kwamba hakumwokoa Paulo kwa kuwa alijua kwamba mtume huyo ni raia wa Roma. Isitoshe, Lisia hakutaja kwamba alikuwa ameamuru Paulo “afungwe kwa minyororo miwili” na baadaye alitoa amri Paulo “ahojiwe huku akipigwa mijeledi.” (Mdo. 21:30-34; 22:24-29) Lisia alikuwa amekiuka haki za Paulo akiwa raia wa Roma. Leo, Shetani hutumia wapinzani wa kidini kuchochea mateso, na huenda uhuru wetu wa ibada ukavurugwa. Hata hivyo, kama Paulo alivyofanya, watu wa Mungu wanaweza kutumia haki zao wakiwa raia wa nchi ili kutafuta ulinzi wa kisheria.

      “Nami Nafurahi Kujitetea Mbele Yako” (Mdo. 23:35–24:21)

      10. Paulo alishtakiwa mambo gani mazito?

      10 Akiwa Kaisaria, Paulo ‘aliwekwa chini ya ulinzi katika jumba la kifalme la Herode’ akingojea waliomshtaki wafike kutoka Yerusalemu. (Mdo. 23:35) Siku tano baadaye, wakafika—Kuhani Mkuu Anania, wakili anayeitwa Tertulo, na kikundi cha wazee. Tertulo alianza kwa kumsifu Feliksi kwa mambo aliyokuwa akiwafanyia Wayahudi, huenda ili apate kibali chake.b Kisha, akianza mashtaka yake, Tertulo alisema kwamba Paulo ni “msumbufu, akichochea uasi miongoni mwa Wayahudi wote katika dunia yote inayokaliwa, naye ni kiongozi wa madhehebu ya Wanazareti. Pia alijaribu kulichafua hekalu, basi tukamkamata.” Wale Wayahudi wengine “wakajiunga katika shambulio hilo, wakisisitiza kwamba mambo hayo ni ya kweli.” (Mdo. 24:5, 6, 9) Kuchochea uasi, kuongoza madhehebu hatari, na kulichafua hekalu—hayo yalikuwa mashtaka mazito ambayo yangeweza kufanya mtu ahukumiwe kifo.

      11, 12. Paulo alikanushaje mashtaka yaliyoletwa dhidi yake?

      11 Kisha, Paulo akaruhusiwa azungumze. Akasema hivi: “Nami nafurahi kujitetea mbele yako.” Kisha, akakanusha mashtaka hayo. Mtume huyo hakuwa amelichafua hekalu, wala kujaribu kuchochea uasi. Alisema kwamba hata hakuwa Yerusalemu kwa “miaka kadhaa” na kwamba alikuwa amefika kuleta “zawadi za rehema”​—michango kwa ajili ya Wakristo ambao walikuwa maskini kwa sababu ya njaa na mateso. Paulo alisisitiza kwamba kabla ya kuingia hekaluni, alikuwa ‘ametakaswa kisherehe’ naye aliazimia “kudumisha dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu.”​—Mdo. 24:10-13, 16-18.

      12 Paulo alikiri kwamba alikuwa akitoa utumishi mtakatifu kwa Mungu wa mababu zake “kulingana na njia wanayoiita madhehebu.” Hata hivyo, alisisitiza kwamba anaamini “mambo yote yaliyo katika Sheria na yaliyoandikwa katika Manabii.” Na kama washtaki wake, alikuwa na tumaini la “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” Kisha, Paulo akawataka washtaki wake watoe uthibitisho wa madai yao: “Uwaambie watu walio hapa waseme wenyewe kosa walilopata nilipokuwa nimesimama mbele ya Sanhedrini, isipokuwa jambo hili moja nililosema kwa sauti kubwa nilipokuwa nimesimama kati yao: ‘Mimi ninahukumiwa leo mbele yenu kwa sababu ya ufufuo wa wafu!’”​—Mdo. 24:14, 15, 20, 21.

      13-15. Ni kwa njia gani Paulo alituwekea mfano mzuri wa kutoa ushahidi kwa ujasiri tunaposhtakiwa?

      13 Paulo alituwekea mfano mzuri tunaoweza kufuata ikiwa tutashtakiwa kwa sababu ya ibada yetu na tukishtakiwa kuwa wachochezi, waasi, au washiriki wa “madhehebu hatari.” Paulo hakujaribu kujipendekeza mbele ya gavana, akimsifu kama alivyofanya Tertulo. Paulo alikuwa mtulivu na mwenye heshima. Kwa busara, alitoa ushahidi wenye kusadikisha na wa kweli. Paulo alitaja kwamba “Wayahudi fulani kutoka mkoa wa Asia” waliodai kwamba alichafua hekalu hawako, na kulingana na sheria wanapaswa kuwapo ili wathibitishe mashtaka yao.​—Mdo. 24:18, 19.

      14 Zaidi ya yote, Paulo hakuogopa kutoa ushahidi kuhusu imani yake. Kwa ujasiri mtume alitaja tena na tena imani yake katika ufufuo, suala ambalo lilisababisha vurugu alipokuwa mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 23:6-10) Alipokuwa akijitetea, Paulo alikazia tumaini la ufufuo. Kwa nini? Kwa sababu Paulo alikuwa akitoa ushahidi kumhusu Yesu na ufufuo wake—jambo ambalo wapinzani hao hawakukubali. (Mdo. 26:6-8, 22, 23) Vurugu zilizotokea zilitokana na suala la ufufuo, imani katika Yesu na ufufuo wake.

      15 Kama Paulo alivyofanya, tunaweza kutoa ushahidi kwa ujasiri, nasi tunaweza kutiwa moyo na maneno ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu. Lakini yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” Je, tunapaswa kuhangaikia tutakalosema? Hapana, kwa kuwa Yesu alitoa uhakikisho huu: “Watakapokuwa wakiwapeleka kuwashtaki, msihangaike kuhusu jambo mtakalosema; bali semeni jambo mtakalopewa saa hiyo, kwa maana si ninyi mnaosema, bali ni roho takatifu.”​—Marko 13:9-13.

      “Feliksi Akaogopa” (Mdo. 24:22-27)

      16, 17. (a) Feliksi alishughulikia jinsi gani kesi ya Paulo? (b) Huenda ni kwa nini Feliksi aliogopa, hata hivyo ni kwa nini aliendelea kukutana na Paulo?

      16 Hiyo haikuwa mara ya kwanza Gavana Feliksi kusikia kuhusu imani ya Kikristo. Masimulizi hayo yanasema: “Feliksi, akiwa anajua vizuri ukweli kuhusu Njia hii [jina lililotumiwa kufafanua Ukristo wa mapema], akaahirisha kesi yao kwa kusema: ‘Lisia kamanda wa jeshi atakapokuja, nitaamua mambo haya yanayowahusu.’ Naye akamwagiza ofisa wa jeshi kwamba mtu huyo awekwe chini ya kizuizi lakini apewe uhuru fulani, na watu wake waruhusiwe kumhudumia.”​—Mdo. 24:22, 23.

      17 Siku kadhaa baadaye, Feliksi na mke wake Myahudi, Drusila, waliwatuma watu wamwite Paulo ili ‘wamsikilize akizungumza kuhusu imani katika Kristo Yesu.’ (Mdo. 24:24) Hata hivyo, Paulo alipozungumzia “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja, Feliksi akaogopa,” huenda kwa sababu dhamiri yake ilimsumbua kwa kuwa alijua anaishi maisha mapotovu. Kwa hiyo akamruhusu Paulo aondoke na kumwambia: “Kwa sasa unaweza kwenda, lakini nitakapopata nafasi nitakuita tena.” Baada ya hapo Feliksi alikutana na Paulo mara nyingi, si kwa sababu alitaka kujua kweli, lakini kwa sababu alitumaini kwamba Paulo atampa rushwa.​—Mdo. 24:25, 26.

      18. Kwa nini Paulo alizungumza na Feliksi na mke wake kuhusu “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja”?

      18 Kwa nini Paulo alizungumza na Feliksi na mke wake kuhusu “uadilifu na kujizuia na hukumu itakayokuja”? Kumbuka, walitaka kujua “imani katika Kristo Yesu” inahusisha nini. Kwa kuwa Paulo alijua kwamba walikuwa wakiishi maisha mapotovu, walikuwa wakatili, na wasiotenda haki, aliwaonyesha wazi kinachohitajika ili kuwa wafuasi wa Yesu. Mambo ambayo Paulo alisema yalionyesha tofauti kubwa kati ya viwango vya Mungu vya uadilifu na mwenendo wa Feliksi na mke wake. Hayo yangewasaidia kuona kwamba wanadamu wote wanawajibika mbele ya Mungu kuhusu wanavyofikiri, kusema, na kutenda na kwamba jambo muhimu zaidi kuliko hukumu ambayo Paulo anakabili ni hukumu watakayokabili mbele za Mungu. Ndiyo sababu Feliksi ‘aliogopa’!

      19, 20. (a) Tunapohubiri, tunapaswa kushughulika jinsi gani na watu wanaoonekana kana kwamba wanapendezwa na kweli, lakini wana sababu za kibinafsi? (b) Tunajuaje kwamba Feliksi hakuwa rafiki ya Paulo?

      19 Tunapohubiri, huenda tukawapata watu walio kama Feliksi. Mwanzoni wanaweza kuonekana wanapendezwa na kweli, lakini labda wakawa na sababu za kibinafsi. Tunapaswa kuwa waangalifu tunaposhughulika nao. Hata hivyo, kama Paulo alivyofanya, tunaweza kutumia busara kuwaambia kuhusu viwango vya Mungu vya uadilifu. Huenda kweli ikagusa mioyo yao. Lakini, tukiona wazi kwamba hawana nia ya kuacha njia zao mbaya, tunawaacha na kutafuta wale wanaoitafuta sana kweli.

      20 Nia ya Feliksi inaonekana wazi kutokana na maneno haya: “Miaka miwili ilipokwisha, Porkio Festo alichukua nafasi ya Feliksi; na kwa sababu Feliksi alitamani kukubaliwa na Wayahudi, akamwacha Paulo akiwa amefungwa.” (Mdo. 24:27) Feliksi hakuwa rafiki wa kweli wa Paulo. Feliksi alijua kwamba wafuasi wa “Ile Njia” hawakuwa wachochezi wala wafanya mapinduzi. (Mdo. 19:23) Pia, alijua kwamba Paulo hakuwa amevunja sheria yoyote ya Roma. Hata hivyo, Feliksi alimtia mtume huyo kifungoni ili ‘akubaliwe na Wayahudi.’

      21. Ni nini kilichompata Paulo baada ya Porkio Festo kuwa gavana, na ni nini kilichoendelea kumwimarisha Paulo?

      21 Kama tunavyoona katika mstari wa mwisho wa Matendo sura ya 24, bado Paulo alikuwa gerezani Porkio Festo alipoanza kutawala baada ya Feliksi. Kukawa na mfululizo wa kesi, naye Paulo akapelekwa kutoka kwa ofisa mmoja hadi mwingine. Kwa kweli, mtume huyo mwenye ujasiri ‘alipelekwa mbele ya wafalme na magavana.’ (Luka 21:12) Kama tutakavyoona, baadaye alitoa ushahidi mbele ya mtawala mwenye nguvu zaidi wa siku zake. Wakati wote huo, imani ya Paulo haikuyumba kamwe. Bila shaka, aliendelea kuimarishwa na maneno ya Yesu: “Jipe moyo!”

      FELIKSI—GAVANA WA MKOA WA YUDEA

      Mwaka wa 52 hivi W.K., Klaudio, Maliki Mroma, alimchagua rafiki yake, Antonio Feliksi, kuwa gavana katika mkoa wa Yudea. Kama ndugu yake Pala, Feliksi alikuwa mtumwa wa familia ya maliki, aliyewekwa huru. Halikuwa jambo la kawaida kwa mtu ambaye awali alikuwa mtumwa kuwekwa kuwa gavana, na amiri jeshi.

      Felix.

      Kwa sababu ndugu yake alikuwa na ushawishi mkubwa kwa maliki, Feliksi “aliona kwamba angeweza kufanya uovu wowote bila kuadhibiwa,” asema Tasito, mwanahistoria Mroma. Akiwa gavana, Feliksi “alikuwa mkatili na mwenye tamaa sana, na ingawa alikuwa na mamlaka ya kifalme, alijiendesha kama mtumwa, bila ustaarabu.” Alipokuwa gavana, Feliksi alimwoa Drusila, binti ya Herode Agripa wa Kwanza, baada ya kumshawishi amuache mume wake. Feliksi alimtendea mtume Paulo kwa ufisadi na isivyo halali, akitaka Paulo ampe hongo.

      Utawala wa Feliksi ulikuwa na ufisadi mwingi sana na wenye kukandamiza hivi kwamba Maliki Nero alimuamuru arudi Roma mwaka wa 58 W.K. Kikundi kidogo cha Wayahudi kilimfuata Feliksi kwenda Roma ili kumshtaki kwa sababu ya utawala wake mbovu, hata hivyo, inasemekana kwamba ndugu yake, Pala, alimwokoa asiadhibiwe.

      a Ona sanduku lenye kichwa, “Feliksi—Gavana wa Mkoa wa Yudea.”

      b Tertulo alimshukuru Feliksi kwa “amani nyingi” aliyoileta katika taifa hilo. Hata hivyo, ukweli ni kwamba amani iliyokuwa Yudea Feliksi akiwa gavana, ilikuwa ndogo ukilinganisha na amani nyingi iliyokuwako wakati wa wale magavana wengine waliotangulia mpaka uasi dhidi ya Roma ulipotokea. Pia, hakusema kweli alipotaja kwamba Wayahudi walitoa “shukrani nyingi sana” kwa marekebisho ambayo Feliksi alikuwa amefanya. Ukweli ni kwamba Wayahudi wengi walimchukia Feliksi kwa sababu ya kuwakandamiza na kuwatendea kikatili walipoasi.​—Mdo. 24:2, 3.

  • “Ninakata Rufaa kwa Kaisari!”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 25

      “Ninakata Rufaa kwa Kaisari!”

      Paulo aweka kielelezo katika kuitetea habari njema

      Matendo 25:1–26:32

      1, 2. (a) Paulo anajikuta katika hali gani? (b) Rufaa ya Paulo kwa Kaisari inatokeza swali gani?

      PAULO bado yuko chini ya ulinzi mkali jijini Kaisaria. Miaka miwili mapema alipokuwa amerudi Yudea, siku chache tu baada ya kufika kwake Wayahudi walijaribu kumuua mara tatu hivi. (Mdo. 21:27-36; 23:10, 12-15, 27) Kufikia sasa, adui zake hawajafanikiwa, hata hivyo, hawakati tamaa. Paulo anapoona kwamba huenda akakabidhiwa mikononi mwao, anamwambia Festo, Gavana Mroma: “Ninakata rufaa kwa Kaisari!”​—Mdo. 25:11.

      2 Je, Yehova aliunga mkono uamuzi wa Paulo wa kukata rufaa kwa maliki wa Roma? Jibu la swali hilo ni muhimu kwetu leo, sisi tunaotoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu. Tunahitaji kujua ikiwa tunaweza kuiga mfano wa Paulo “katika kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”​—Flp. 1:7.

      “Nimesimama Mbele ya Kiti cha Hukumu” (Mdo. 25:1-12)

      3, 4. (a) Kwa nini Wayahudi wanaomba Paulo apelekwe Yerusalemu, naye anaepuka kifo jinsi gani? (b) Kama alivyomtegemeza Paulo, Yehova huwategemeza jinsi gani watumishi wake leo?

      3 Siku tatu baada ya kuteuliwa, Festo, gavana mpya wa Roma katika mkoa wa Yudea, anaenda Yerusalemu.a Akiwa huko, anawasikiliza wakuu wa makuhani na wakuu kati ya Wayahudi wakitoa mashtaka mazito dhidi ya Paulo. Wanajua kwamba gavana huyo mpya anataka sana kudumisha amani kati yake nao na Wayahudi wengine wote. Kwa hiyo wanamwomba Festo ampeleke Paulo Yerusalemu, na kumhukumu huko. Hata hivyo, adui hao walikuwa wamepanga njama ya kumuua Paulo akiwa njiani kutoka Kaisaria kwenda Yerusalemu. Festo akataa ombi lao na kusema: “Wale walio na mamlaka kati yenu washuke pamoja nami [mpaka Kaisaria] na kumshtaki, ikiwa kwa kweli mtu huyu amefanya kosa lolote.” (Mdo. 25:5) Hivyo, kwa mara nyingine tena, Paulo anaepuka kifo.

      4 Katika kesi zote za Paulo, Yehova alimtegemeza kupitia Bwana Yesu Kristo. Kumbuka kwamba katika maono, Yesu alimwambia mtume wake: “Jipe moyo!” (Mdo. 23:11) Leo, watumishi wa Mungu hukabili upinzani na vitisho. Yehova hatulindi kutokana na kila tatizo, lakini hutupatia hekima na nguvu za kuvumilia. Sikuzote tunaweza kutegemea “nguvu zinazopita zile za kawaida” ambazo Mungu wetu mwenye upendo hutoa.​—2 Kor. 4:7.

      5. Festo alishughulikiaje kesi ya Paulo?

      5 Siku kadhaa baadaye, Festo “akaketi kwenye kiti cha hukumu” jijini Kaisaria.b Paulo na wanaomshitaki walikuwa wamesimama mbele yake. Akijibu mashtaka yao yasiyo na msingi, Paulo akasema: “Sijatenda dhambi yoyote dhidi ya Sheria ya Wayahudi wala dhidi ya hekalu wala dhidi ya Kaisari.” Mtume huyo hakuwa na hatia na alistahili kuachiliwa huru. Festo atatoa uamuzi gani? Akitamani kukubaliwa na Wayahudi, anamuuliza Paulo: “Je, ungependa kupanda kwenda Yerusalemu ukahukumiwe huko mbele yangu kuhusu mambo haya?” (Mdo. 25:6-9) Pendekezo la kipumbavu sana. Ikiwa Paulo angerudishwa Yerusalemu, watu wanaomshtaki ndio ambao wangemhukumu, na bila shaka angeuawa. Katika kisa hiki, Festo alikuwa akihangaikia manufaa yake ya kisiasa badala ya kuzingatia haki. Pontio Pilato, gavana aliyemtangulia, alitenda vivyo hivyo katika kesi iliyomhusu Yesu. (Yoh. 19:12-16) Leo pia, huenda mahakimu wakatenda isivyo haki ili kuwapendeza wanasiasa. Kwa hiyo, tusishangae mahakama zinapotoa uamuzi usiopatana hata kidogo na ushahidi uliotolewa katika kesi zinazowahusu watu wa Mungu.

      6, 7. Kwa nini Paulo alikata rufaa kwa Kaisari, naye aliwawekea Wakristo wa kweli leo mfano gani?

      6 Tamaa ya Festo ya kuwapendeza Wayahudi ingeweza kufanya Paulo auawe. Kwa hiyo, Paulo akatumia haki yake akiwa raia wa Roma. Alimwambia Festo: “Mimi nimesimama mbele ya kiti cha hukumu cha Kaisari, ambapo ninapaswa kuhukumiwa. Sijawakosea Wayahudi, nawe pia umegundua jambo hilo. . . . Ninakata rufaa kwa Kaisari!” Baada ya rufaa kukatwa, lazima ingesikilizwa. Festo alikazia hilo kwa kusema: “Umekata rufaa kwa Kaisari; nawe utaenda kwa Kaisari.” (Mdo. 25:10-12) Paulo aliwawekea Wakristo wa kweli leo mfano wa kuiga. Wapinzani wanapojaribu kutunga “matatizo kwa kutumia sheria,” Mashahidi wa Yehova hutumia maandalizi ya kisheria yaliyopo ili kuitetea habari njema.c—Zab. 94:20.

      7 Hivyo, baada ya kufungwa kwa zaidi ya miaka miwili kwa sababu ya makosa ambayo hakuwa amefanya, Paulo alipewa nafasi ya kujitetea jijini Roma. Hata hivyo, kabla ya kuondoka, mtawala mwingine alitaka kumwona.

      Watu wakiwa mahakamani baada ya hukumu kutolewa. Ndugu, wanasheria wake, na Mashahidi wengine walio mahakamani wakiwa wamevunjika moyo. Watu wasio Mashahidi wana furaha na wanawapongeza wanasheria walioshinda kesi dhidi ya ndugu.

      Tunapohukumiwa isivyofaa, tunakata rufaa

      “Sikukosa Kutii” (Mdo. 25:13–26:23)

      8, 9. Kwa nini Mfalme Agripa alienda Kaisaria?

      8 Siku kadhaa baada ya Paulo kumwambia Festo kwamba anakata rufaa kwa Kaisari, Mfalme Agripa na dada yake, Bernike walifika kwa “ziara ya kumsalimia” gavana huyo mpya.d Katika siku za Waroma, ilikuwa kawaida kwa maofisa kuwatembelea magavana wapya. Kwa kumpongeza Festo, ni wazi kwamba Agripa alikuwa akijaribu kujenga urafiki wa kibinafsi na kisiasa kati yao kwa ajili ya wakati ujao.​—Mdo. 25:13.

      KUKATA RUFAA KWA AJILI YA IBADA YA KWELI LEO

      Nyakati nyingine, Mashahidi wa Yehova wamekata rufaa katika mahakama kuu wakitumaini vizuizi viondolewe ili waendelee kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Fikiria mifano miwili ifuatayo:

      Mnamo Machi 28, 1938, Mahakama Kuu ya Marekani ilibatilisha maamuzi ya mahakama ya jimbo na kuondolea hatia kikundi cha Mashahidi waliokuwa wamekamatwa kwa sababu ya kugawa vitabu na magazeti ya Biblia jijini Griffin, katika jimbo la Georgia, nchini Marekani. Rufaa hiyo ilikuwa ya kwanza kati ya nyingi zilizokatwa katika mahakama hiyo kuu kuhusu haki ya Mashahidi ya kuhubiri habari njema.g

      Kesi nyingine ilimhusu Shahidi mmoja nchini Ugiriki, Minos Kokkinakis. Katika kipindi cha miaka 48, alikamatwa zaidi ya mara 60 akishtakiwa kwa kosa la “kugeuza imani ya watu.” Alifikishwa mahakamani mara 18. Alifungwa gerezani kwa miaka mingi naye alipelekwa uhamishoni katika visiwa vya mbali katika Bahari ya Aegea. Mara ya mwisho aliposhtakiwa, mnamo mwaka wa 1986, mahakama kuu za Ugiriki zilimhukumia hatia Ndugu Kokkinakis. Kisha akatafuta msaada kupitia Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR). Mnamo Mei 25, 1993, Mahakama hiyo ilifikia uamuzi kwamba nchi ya Ugiriki imekiuka uhuru wa kuabudu wa Ndugu Kokkinakis.

      Mashahidi wa Yehova wamekata rufaa katika Mahakama Kuu ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu katika kesi mbalimbali, nao wamepata ushindi katika kesi nyingi. Hakuna tengenezo lingine lolote, la kidini au lingine lolote, ambalo limefanikiwa kiasi hicho katika kutetea haki za msingi za kibinadamu mbele za Mahakama hiyo.

      Je, wengine hunufaika kutokana na ushindi huo wa Mashahidi wa Yehova? Msomi Charles C. Haynes aliandika: “Sote tunapaswa kuwashukuru Mashahidi wa Yehova. Haidhuru ni mara ngapi wanatukanwa, wanafukuzwa mjini, au kupigwa, wao huendelea kupigania uhuru wao wa dini (na wetu pia). Na wanaposhinda, sote tunashinda.”

      g Ona simulizi la uamuzi wa Mahakama Kuu ya Marekani kuhusu uhuru wa kusema, katika gazeti la Amkeni! la Januari 8, 2003, ukurasa wa 3-11.

      9 Festo alimwambia mfalme kumhusu Paulo, naye Agripa akataka kumwona. Siku iliyofuata, watawala hao wawili wakaketi juu ya kiti cha hukumu. Hata hivyo, jambo la kuvutia zaidi lilikuwa maneno ya mfungwa aliyekuwa mbele yao wala si nguvu au fahari yao.​—Mdo. 25:22-27.

      10, 11. Paulo alimwonyesha Agripa heshima kwa njia gani, na Paulo alimwambia nini mfalme kuhusu maisha yake ya awali?

      10 Paulo alimshukuru kwa heshima Mfalme Agripa kwa kumpa nafasi ya kujitetea, akikiri kwamba mfalme ana ujuzi juu ya desturi zote na vilevile mabishano kati ya Wayahudi. Kisha, Paulo akasimulia maisha yake ya wakati uliopita: “Niliishi nikiwa Farisayo kulingana na madhehebu yetu yenye msimamo mkali zaidi katika ibada yetu.” (Mdo. 26:5) Akiwa Farisayo, Paulo alitazamia kuja kwa Masihi. Sasa akiwa Mkristo, alimtambulisha kwa ujasiri Yesu Kristo kuwa yule aliyekuwa akisubiriwa kwa muda mrefu. Paulo alishtakiwa kwa sababu ya jambo ambalo yeye na wale waliokuwa wakimshtaki waliamini, lile tumaini la ahadi ya Mungu kwa mababu zao. Maelezo ya Paulo yalimchochea Agripa atake kusikia zaidi.e

      11 Akikumbuka jinsi alivyokuwa akiwatendea Wakristo kwa ukatili hapo awali, Paulo alisema: “Mimi niliamini kwamba ninapaswa kufanya matendo mengi ili kulipinga jina la Yesu Mnazareti . . . kwa sababu nilikuwa nimewakasirikia sana [wafuasi wa Kristo], nilifikia hatua ya kuwatesa hata katika majiji yaliyo mbali.” (Mdo. 26:9-11) Paulo hakuwa akitia chumvi. Watu wengi walijua jinsi alivyokuwa amewatendea Wakristo kwa ujeuri. (Gal. 1:13, 23) Huenda Agripa alitaka kujua: ‘Ni nini kilichombadili mtu huyu?’

      12, 13. (a) Paulo alieleza jinsi gani kugeuzwa kwake? (b) Ni kwa njia gani Paulo alikuwa ‘akiipiga teke michokoo’?

      12 Maneno yafuatayo ya Paulo yanatoa jibu: “Nikiwa safarini kwenda Damasko pia nikiwa na mamlaka na maagizo kutoka kwa wakuu wa makuhani, katikati ya mchana niliona barabarani, ewe Mfalme, nuru kutoka mbinguni inayozidi mwangaza wa jua ikimulika kunizunguka mimi na wale waliokuwa wakisafiri pamoja nami. Sisi sote tulipoanguka chini, nikasikia sauti ikiniambia katika lugha ya Kiebrania: ‘Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa? Kuendelea kuipiga teke michokoo kunafanya iwe vigumu kwako.’ Lakini nikauliza: ‘Wewe ni nani Bwana?’ Naye Bwana akajibu: ‘Mimi ni Yesu, ambaye unamtesa.’”f—Mdo. 26:12-15.

      13 Kabla ya tukio hilo lisilo la kawaida, Paulo alikuwa ‘akiipiga teke michokoo.’ Kama vile mnyama wa kubeba mizigo angejiumiza kwa kupiga teke sehemu yenye ncha kali ya mchokoo, Paulo alijiumiza kiroho kwa kupinga mapenzi ya Mungu. Kwa kumtokea Paulo barabarani alipokuwa akielekea Damasko, Yesu aliyekuwa amefufuliwa alimchochea mtu huyo mnyoofu aliyetenda bila kujua, abadili maoni yake.​—Yoh. 16:1, 2.

      14, 15. Paulo alisema nini kuhusu mabadiliko aliyokuwa amefanya maishani?

      14 Bila shaka Paulo alifanya mabadiliko makubwa maishani. Alimwambia Agripa: “Mimi sikukosa kutii maono hayo kutoka mbinguni, lakini kwanza kwa wale walio huko Damasko kisha kwa wale walio Yerusalemu, na katika nchi yote ya Yudea, na pia kwa mataifa, nilikuwa nikipeleka ujumbe kwamba wanapaswa kutubu na kumgeukia Mungu kwa kufanya matendo yanayoonyesha toba.” (Mdo. 26:19, 20) Kwa miaka mingi, Paulo alikuwa akitimiza mgawo ambao Yesu Kristo alimpatia katika maono hayo aliyopata katikati ya mchana. Alipata matokeo gani? Waliokubali habari njema aliyohubiri Paulo, walitubu mwenendo wao mpotovu na usio mnyoofu, kisha wakamgeukia Mungu. Watu hao wakawa raia wazuri, wanaoheshimu sheria na mamlaka.

      15 Hata hivyo, matokeo hayo hayakuwa na maana yoyote kwa Wayahudi waliompinga Paulo. Paulo alisema hivi: “Hiyo ndiyo sababu Wayahudi walinikamata hekaluni na kujaribu kuniua. Hata hivyo, kwa sababu nimepata msaada kutoka kwa Mungu, mpaka leo hii ninaendelea kutoa ushahidi kwa wadogo na wakubwa pia.”​—Mdo. 26:21, 22.

      16. Tunaweza kumwigaje Paulo tunapozungumza na mahakimu na watawala kuhusu imani yetu?

      16 Tukiwa Wakristo wa kweli, tunapaswa ‘sikuzote kuwa tayari kuitetea’ imani yetu. (1 Pet. 3:15) Tunapozungumza na mahakimu na watawala kuhusu imani yetu, huenda ikafaa kuiga njia ambayo Paulo alitumia alipokuwa akizungumza na Agripa na Festo. Kwa kuwaeleza kwa heshima jinsi kweli za Biblia zimebadili maisha ya watu—yetu wenyewe na ya wale ambao wamekubali ujumbe wetu—huenda tukagusa mioyo ya watu hao wenye mamlaka.

      “Ungenishawishi Niwe Mkristo” (Mdo. 26:24-32)

      17. Baada ya kumsikiliza Paulo, Festo alisema nini, na ni mtazamo gani kama huo unaoonekana leo?

      17 Walipokuwa wakisikiliza ushahidi wenye kusadikisha wa Paulo, watawala hao wawili walichochewa sana. Ona jinsi mambo yalivyokuwa: “Paulo alipokuwa akijitetea kwa kusema mambo hayo, Festo akasema kwa sauti kubwa: ‘Unarukwa na akili, Paulo! Kusoma kwingi kunafanya urukwe na akili!’” (Mdo. 26:24) Huenda maneno ya Festo yanalingana sana na mtazamo unaoonekana leo. Machoni mwa wengi, wale wanaofundisha kweli za Biblia wamerukwa na akili. Wenye hekima ya ulimwengu huona vigumu kukubali fundisho la Biblia kuhusu ufufuo wa wafu.

      18. Paulo alimjibuje Festo, na hilo lilimfanya Agripa aseme nini?

      18 Hata hivyo, Paulo alimjibu gavana huyo: “Mimi sirukwi na akili, ewe Mtukufu Festo, bali ninasema maneno ya kweli na ya akili timamu. Kwa kweli, mfalme ninayezungumza naye kwa uhuru anajua vizuri mambo haya . . . Je, wewe, Mfalme Agripa, unawaamini Manabii? Ninajua unawaamini.” Agripa akamwambia Paulo: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Mdo. 26:25-28) Maneno hayo, yawe yalitoka moyoni au la, yanaonyesha kwamba ushahidi wa Paulo ulikuwa na matokeo makubwa kwa mfalme.

      19. Festo na Agripa walifikia mkataa gani kuhusu Paulo?

      19 Kisha Agripa na Festo wakasimama, kuonyesha kwamba mahojiano yamefikia mwisho. “Walipokuwa wakiondoka wakaanza kuambiana: ‘Mtu huyu hafanyi lolote linalostahili kifo au vifungo vya gereza.’ Kisha Agripa akamwambia Festo: ‘Mtu huyu angefunguliwa kama hangekuwa amekata rufaa kwa Kaisari.’” (Mdo. 26:31, 32) Walijua kwamba mtu aliyesimama mbele yao hakuwa na hatia. Huenda tangu wakati huo na kuendelea wangekuwa na maoni yanayofaa kuhusu Wakristo.

      20. Ushahidi ambao Paulo alitoa mbele ya watu wenye mamlaka ulikuwa na matokeo gani?

      20 Hakuna yeyote kati ya watawala hao wawili wenye nguvu aliyekubali habari njema ya Ufalme wa Mungu. Je, kulikuwa na manufaa yoyote kwa Paulo kujitetea mbele ya watu hao? Ndiyo. Kwa kuwa Paulo ‘alipelekwa mbele ya wafalme na magavana’ huko Yudea, habari njema iliwafikia maofisa Waroma ambao huenda hawangehubiriwa kamwe. (Luka 21:12, 13) Pia, mambo yaliyompata na uaminifu wake chini ya majaribu yaliwatia moyo ndugu na dada zake Wakristo.​—Flp. 1:12-14.

      21. Tunaweza kupata matokeo gani mazuri tukiendelea na kazi yetu ya Ufalme?

      21 Ndivyo ilivyo leo. Tukiendelea na kazi ya Ufalme licha ya majaribu na upinzani, tunaweza kupata matokeo mazuri. Huenda tukawahubiria maofisa ambao hawapatikani kwa urahisi. Kuvumilia kwetu kwa uaminifu kunaweza kuwatia moyo ndugu na dada zetu Wakristo na kuwachochea wawe na ujasiri zaidi katika kazi ya kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.

      PORKIO FESTO—GAVANA WA ROMA KATIKA MKOA WA YUDEA

      Habari kumhusu Porkio Festo, zinapatikana tu katika kitabu cha Matendo ya Mitume na maandishi ya Flavio Yosefo. Festo aliwekwa kuwa gavana wa Yudea baada ya Feliksi, mwaka wa 58 hivi W.K., na huenda alikufa akiwa gavana baada ya kutawala kwa miaka miwili au mitatu tu.

      Porkio Festo.

      Kwa ujumla, yaonekana Festo alikuwa gavana mwenye busara na uwezo, tofauti na Feliksi, gavana aliyemtangulia, na pia Albino, gavana aliyemfuata. Mwanzoni mwa utawala wa Festo, kulikuwa na wezi wengi Yudea. Yosefo alisema: “Festo . . . aliazimia kuwaadhibu wale waliosababisha usumbufu nchini. Hivyo, alikamata wezi wengi na wengi wao aliwaua.” Wakati wa utawala wake, Wayahudi walijenga ukuta ili kumzuia Mfalme Agripa asione kilichokuwa kikiendelea katika eneo la hekalu. Mwanzoni, Festo aliamuru ukuta huo ubomolewe. Hata hivyo, Wayahudi walipomwomba asiubomoe, aliwaruhusu wawasilishe ombi hilo kwa Nero, Maliki wa Roma.

      Inaonekana Festo alichukua hatua kali dhidi ya wahalifu na waasi. Hata hivyo, ili kuwafurahisha Wayahudi, alikuwa tayari kutotenda kwa haki—hasa aliposhughulika na mtume Paulo.

      MFALME HERODE AGRIPA WA PILI

      Agripa anayezungumziwa katika Matendo sura ya 25 ni Mfalme Herode Agripa wa Pili, mwana wa mjukuu wa Herode Mkuu na mwana wa Herode ambaye alikuwa ameshambulia kutaniko la Yerusalemu miaka 14 iliyopita. (Mdo. 12:1) Agripa alikuwa wa mwisho katika ukoo wa wana wa Herode.

      Mfalme Herode Agripa wa Pili.

      Baba yake alipokufa mwaka wa 44 W.K., Agripa alikuwa na umri wa miaka 17 naye alikuwa Roma, akisoma katika makao ya Maliki Mroma, Klaudio. Washauri wa maliki walimwona Agripa kuwa mchanga sana asiweze kumrithi baba yake; hivyo, gavana Mroma akachaguliwa badala yake. Hata hivyo, kulingana na Flavio Yosefo, Agripa akiwa bado Roma, aliendelea kuwasaidia Wayahudi na kutetea haki zao.

      Mwaka wa 50 W.K., Klaudio alimweka Agripa kuwa mtawala wa Chalcis na mwaka wa 53 W.K., akampa mamlaka juu ya Iturea, Trakoniti, na Abilene. Pia, Agripa alipewa wadhifa wa kusimamia hekalu la Yerusalemu, naye alikuwa na mamlaka ya kuwateua makuhani wakuu wa Wayahudi. Nero, aliyetawala baada ya Klaudio alipanua eneo la utawala wa Agripa likatia ndani sehemu za Galilaya na Perea. Alipokutana na Paulo, Agripa alikuwa Kaisaria pamoja na dada yake Bernike, aliyekuwa amemwacha mume wake, mfalme wa Kilikia.​—Mdo. 25:13.

      Mwaka wa 66 W.K., Agripa aliposhindwa kuzuia uasi wa Wayahudi dhidi ya Roma, aliamua kujiunga na Waroma kwa kuwa waasi hao walitaka kumshambulia. Baada ya kuzuia uasi wa Wayahudi, maliki mpya, Vaspasiani, alimshukuru Agripa kwa kumwongezea maeneo ya utawala.

      a Ona sanduku lenye kichwa “Porkio Festo—Gavana wa Roma Katika Mkoa wa Yudea.”

      b “Kiti cha hukumu” ni kiti kilichokuwa juu ya jukwaa lililoinuliwa. Kwa kuwa kiti hicho kilikuwa juu, basi ilionekana kana kwamba uamuzi wa hakimu unapaswa kuheshimiwa na hauwezi kupingwa. Pilato aliketi juu ya kiti hicho aliposikiliza kesi ya Yesu.

      c Ona sanduku lenye kichwa “Kukata Rufaa kwa Ajili ya Ibada ya Kweli Leo.”

      d Ona sanduku lenye kichwa “Mfalme Herode Agripa wa Pili.”

      e Akiwa Mkristo, Paulo aliamini kwamba Yesu ndiye Masihi. Wayahudi, waliomkataa Yesu, walimwona Paulo kuwa mwasi imani.​—Mdo. 21:21, 27, 28.

      f Kuhusu kusafiri kwa Paulo “katikati ya mchana,” msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Isipokuwa iwe kwamba msafiri alikuwa na jambo la dharura sana, alipumzika mchana wakati ambao joto lilikuwa kali sana. Hivyo, Paulo alifanya jitihada nyingi sana ili kuwatesa Wakristo.”

  • “Hakuna Hata Mmoja Wenu Atakayepotea”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 26

      “Hakuna Hata Mmoja Wenu Atakayepotea”

      Paulo avunjikiwa meli, aonyesha imani kubwa na upendo kwa watu

      Matendo 27:1–28:10

      1, 2. Paulo anaelekea wapi, na huenda anafikiria nini?

      “UTAENDA kwa Kaisari.” Bado mtume Paulo anakumbuka maneno hayo ya Gavana Festo. Paulo amekaa gerezani kwa miaka miwili, kwa hiyo safari ndefu ya kwenda Roma, angalau itampa nafasi ya kuona mazingira mapya. (Mdo. 25:12) Hata hivyo, Paulo anakumbuka mengi zaidi kuhusu safari zake nyingi za baharini mbali na upepo mwanana wenye kuburudisha na maji mengi ya bahari yanayofikia upeo wa macho. Kwa kuwa wakati huu anapelekwa kwa Kaisari, huenda anajiuliza maswali mengi.

      2 Paulo amekuwa katika “hatari baharini” mara nyingi, mara tatu ameokoka baada ya meli kuvunjika. Hata wakati fulani alikaa usiku na mchana baharini. (2 Kor. 11:25, 26) Isitoshe, safari hii ni tofauti kabisa na safari zake za umishonari alipokuwa huru. Wakati huu atasafiri akiwa mfungwa, tena anaenda mbali, kilomita zaidi ya 3,000, kutoka Kaisaria hadi Roma. Je, atafika salama? Hata ikiwa atafika salama, je, atahukumiwa kifo? Kumbuka kwamba anaenda kuhukumiwa na serikali kuu katika ulimwengu wa Shetani wakati huo.

      3. Paulo aliazimia kufanya nini, nasi tutazungumzia nini katika sura hii?

      3 Kutokana na habari ambazo umesoma kuhusu Paulo, unafikiri atakata tamaa na kujihurumia akifikiria mambo yatakayompata? Hapana! Anajua atakabili hali nyingi ngumu, ijapokuwa hajui ni hali gani hususa zitakazompata. Kwa nini apoteze shangwe ya huduma yake kwa sababu ya kuhangaikia mambo asiyoweza kubadili? (Mt. 6:27, 34) Paulo anajua mapenzi ya Yehova ni kwamba atumie kila nafasi anayopata kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, hata mbele ya watawala wa serikali. (Mdo. 9:15) Paulo aliazimia kutimiza mgawo wake, hata hali ziweje. Hilo ndilo linalopaswa kuwa azimio letu pia. Hivyo basi, acheni tuandamane na Paulo katika safari hiyo ya pekee tukifikiria jinsi tunavyoweza kufuata mfano mzuri aliotuwekea.

      “Pepo Zilizokuwa Zikivuma Kinyume Nasi” (Mdo. 27:1-7a)

      4. Paulo alianza safari yake katika meli ya aina gani, na ni nani waliosafiri pamoja naye?

      4 Paulo na wafungwa wengine walitiwa mikononi mwa ofisa Mroma anayeitwa Yulio. Ofisa huyo aliamua wapande meli ya kibiashara iliyokuwa imefika Kaisaria. Ilikuwa imetoka Adramitiamu, bandari iliyo upande wa magharibi wa pwani ya Asia Ndogo, ng’ambo ya jiji la Mitilene katika kisiwa cha Lesbos. Meli hiyo ingesafiri kuelekea kaskazini kisha kuelekea magharibi, ikitua sehemu mbalimbali ili kupakua na kupakia shehena. Meli hizo hazikukusudiwa kubeba abiria, hasa wafungwa. (Ona sanduku lenye kichwa “Safari za Baharini na Njia Zilizotumiwa na Wafanyabiashara.”) Jambo linalotia moyo ni kwamba Paulo hakuwa Mkristo pekee katikati ya kikundi hicho cha wahalifu. Waamini wengine wawili, Aristarko na Luka, walikuwa pamoja naye. Luka ndiye aliyeandika masimulizi hayo. Hatujui iwapo waandamani hao wawili walilipa nauli ili kusafiri au walikuwa watumishi wa Paulo.​—Mdo. 27:1, 2.

      SAFARI ZA BAHARINI NA NJIA ZILIZOTUMIWA NA WAFANYABIASHARA

      Katika ulimwengu wa kale, meli zilitumiwa kusafirisha mizigo si abiria. Watu waliotaka kusafiri walilazimika kutafuta meli ya wafanyabiashara inayoelekea katika eneo wanaloenda. Kisha, wangekubaliana nauli ya usafiri na kusubiri hadi meli itakapoondoka.

      Maelfu ya meli zilisafiri katika Bahari ya Mediterania zikisafirisha vyakula na bidhaa nyingine. Wengi waliosafiri katika meli hizo walilazimika kulala kwenye sitaha, labda katika vibanda walivyotengeneza kila jioni na kubomolewa kila asubuhi. Pia, walihitaji kujibebea vitu walivyohitaji kama vile chakula na vitu vya kulalia.

      Muda ambao safari ingechukua ulitegemea upepo. Kwa sababu ya hali mbaya ya hewa wakati wa majira ya baridi kali, meli hazikusafiri kuanzia katikati ya Novemba mpaka katikati ya Machi.

      Meli ya kale na sehemu zake kuu nne kuanzia kwenye tezi mpaka omo. 1. Makasia. 2. Tanga kuu. 3. Nanga. 4. Tanga la mbele.

      5. Paulo alifurahia ushirika gani alipokuwa Sidoni, nasi tunajifunza nini?

      5 Baada ya kukaa siku nzima baharini, wakiwa wamesafiri kilomita 110 hivi kuelekea upande wa kaskazini, meli hiyo ilitia nanga Sidoni, katika pwani ya Siria. Yaonekana Yulio hakumtendea Paulo kama alivyokuwa akiwatendea wafungwa, huenda ni kwa sababu Paulo alikuwa raia wa Roma naye hakuwa ameshtakiwa na kuthibitishwa kuwa na hatia. (Mdo. 22:27, 28; 26:31, 32) Yulio alimruhusu Paulo ashuke na kwenda kuwatembelea Wakristo wenzake. Lazima ndugu na dada hao waliliona kuwa pendeleo kubwa kumsaidia mtume huyo baada ya kufungwa kwa muda mrefu! Je, kuna pindi zozote unazoweza kuonyesha ukarimu kama huo kwa upendo nawe utiwe moyo pia?​—Mdo. 27:3.

      6-8. Safari ya Paulo kutoka Sidoni hadi Kinido ilikuwaje, na huenda alipata nafasi gani ya kuhubiri?

      6 Kisha, meli ikang’oa nanga kutoka Sidoni, na kusafiri kandokando ya pwani, ikapita Kilikia, karibu na Tarso, jiji la nyumbani kwa Paulo. Luka hataji vituo vingine, ijapokuwa anataja hali ya anga ambayo haikuwa shwari, anaposema ‘pepo zilikuwa zikivuma kinyume nasi.’ (Mdo. 27:4, 5) Haikosi Paulo alitumia kila nafasi ili kuhubiri habari njema. Bila shaka aliwahubiria wafungwa wenzake na wengine waliokuwa kwenye meli hiyo, kutia ndani mafundi wa mitambo na askari, na pia watu wengine wowote aliokutana nao meli ilipotia nanga katika bandari mbalimbali. Je, sisi hutumia kila nafasi tunayopata ili kuhubiri?

      7 Baada ya muda, meli hiyo ilifika Mira, bandari iliyo katika pwani ya kusini ya Asia Ndogo. Huko Paulo na wenzake walipanda meli nyingine, ambayo ingewafikisha Roma. (Mdo. 27:6) Siku hizo, Misri ilikuwa ghala ya Roma, na meli za nafaka kutoka Misri zilikuwa zikitia nanga Mira. Yulio alipata mojawapo ya meli hizo na kuwapandisha askari na wafungwa. Lazima meli hiyo ilikuwa kubwa zaidi kuliko ile ya kwanza. Ilikuwa na shehena kubwa ya ngano na abiria 276—mafundi wa mitambo, wafungwa, na huenda watu wengine waliokuwa wakielekea Roma. Bila shaka, katika meli hiyo, Paulo alipata eneo jipya la kuhubiri, naye hakusita kufanya hivyo.

      8 Kituo kilichofuata ni Kinido, kusini magharibi mwa Asia Ndogo. Kwa kawaida meli zingeweza kusafiri umbali huo kwa siku moja ikiwa hali ya hewa ni shwari. Hata hivyo, kama Luka anavyoripoti, “baada ya kusafiri polepole kwa siku kadhaa, tukafika kwa shida huko Kinido.” (Mdo. 27:7a) Bahari ilizidi kuchafuka. (Ona sanduku lenye kichwa “Pepo Hatari za Mediterania.”) Wazia hali ya watu waliokuwa katika meli hiyo huku wakikabili pepo zenye nguvu na bahari iliyochafuka.

      PEPO HATARI ZA MEDITERANIA

      Safari za meli za biashara katika Bahari ya Mediterania, inayoitwa pia Bahari Kuu, zilitegemea sana pepo na majira. Katika upande wa mashariki wa bahari hiyo, kwa kawaida pepo zilikuwa zikivuma kutoka magharibi kuelekea mashariki kuanzia Juni hadi Septemba. Kwa sababu hiyo, ilikuwa rahisi kusafiri kuelekea upande wa mashariki, kama ilivyokuwa wakati Paulo alipokuwa akirudi kutoka katika safari yake ya tatu ya umishonari. Yeye na wenzake walikuwa katika meli iliyotoka Mileto, ikapitia Rode, na kutia nanga Patara. Kisha meli hiyo ilisafiri moja kwa moja hadi Tiro, katika pwani ya Foinike. Luka anasema kwamba walipita kisiwa cha Kipro, kilichokuwa upande wao wa kushoto, ikimaanisha kwamba walikuwa wakisafiri kuelekea upande wa kusini wa Kipro.​—Mdo. 21:1-3.

      Namna gani safari za kuelekea magharibi? Meli zingeweza kuelekea upande wa magharibi zikifuata njia hiyohiyo iwapo pepo zingeruhusu. Lakini wakati mwingine haikuwezekana. Kitabu The International Standard Bible Encyclopedia kinasema hivi: “Wakati wa majira ya baridi kali, hali ya anga hubadilika badilika sana na vimbunga vikali huvuma kuelekea upande wa mashariki wa Mediterania, na kusababisha mvua nyingi au hata theluji.” Kulikuwa na hatari nyingi sana kwa sababu ya hali hizo.

      Katika majira yoyote, vyombo vilivyokuwa karibu na ufuo vingeweza kusafiri kuelekea kaskazini kandokando ya pwani ya Palestina na kuendelea na safari hadi Pamfilia. Mwishoni mwa safari hiyo, upepo mwanana kutoka nchi kavu na mikondo inayoelekea magharibi ilirahisisha safari za meli. Ndivyo ilivyokuwa katika sehemu ya kwanza ya safari ya Paulo kuelekea Roma akiwa mfungwa. Hata hivyo, nyakati nyingine pepo zingebadili mwelekeo na kuwa hatari. (Mdo. 27:4) Inawezekana kwamba meli ya nafaka inayotajwa sana katika masimulizi ya Luka ilisafiri kuelekea upande wa kaskazini kutoka Misri, kisha ikazunguka na kuingia bahari iliyokuwa salama kati ya Kipro na Asia Ndogo. Kutoka Mira, kapteni wa meli alikusudia kuendelea na safari kuelekea upande wa magharibi—azunguke chini ya Ugiriki, kisha apande kuelekea upande wa magharibi wa Italia. (Mdo. 27:5, 6) Hata hivyo, pepo na majira yalibadili kabisa safari hiyo!

      “Tukirushwarushwa kwa Nguvu na Dhoruba” (Mdo. 27:7b-26)

      9, 10. Ni hali gani ngumu zilizotokea karibu na Krete?

      9 Kapteni wa meli hiyo alipanga kuendelea na safari kuelekea upande wa magharibi kutoka Kinido, hata hivyo, Luka anasema “upepo ulituzuia kusonga mbele.” (Mdo. 27:7b) Meli ilipoanza kwenda mbali na nchi kavu, ilipoteza mkondo, kisha upepo mkali kutoka kaskazini magharibi ukaisukuma, huenda kwa kasi sana. Kama vile meli hiyo ilivyolindwa na kisiwa cha Kipro awali kutokana na pepo zilizokuwa zikivuma kinyume, ililindwa pia na kisiwa cha Krete. Baada ya meli hiyo kupita rasi ya Salmone upande wa mashariki wa Krete, kukawa na utulivu kiasi. Kwa nini? Kwa sababu meli hiyo ilikuwa upande wa kusini wa kisiwa hicho, na hivyo ililindwa kutokana na zile pepo kali. Wazia furaha ya muda waliokuwa nayo watu katika meli hiyo! Hata hivyo, maadamu meli bado ilikuwa baharini, mafundi wa mitambo hawangeweza kupuuza majira ya baridi kali yaliyokuwa yakikaribia. Walikuwa na wasiwasi.

      10 Luka anasema hivi kwa usahihi: “Tukasafiri kwa shida kandokando ya pwani [ya Krete], tukafika mahali panapoitwa Bandari Nzuri.” Hata hivyo, bado haikuwa rahisi kuendesha meli hiyo. Mwishowe, walitia nanga katika ghuba ndogo inayodhaniwa kuwa ilikuwa katika eneo la pwani, kabla tu ya kugeuka kuelekea kaskazini. Walikaa hapo muda gani? Luka anasema walikaa “muda mrefu,” hata hivyo, hawakuwa na wakati wa kupoteza, kwa sababu Septemba na Oktoba ni miezi hatari kusafiri.​—Mdo. 27:8, 9.

      11. Paulo aliwapa wenzake ushauri gani, hata hivyo waliamua kufanya nini?

      11 Huenda abiria fulani walimwomba Paulo ushauri kwa sababu alikuwa na uzoefu wa kusafiri katika Bahari ya Mediterania. Alipendekeza wasitishe safari, kwa kuwa ikiwa wangeendelea, wangepatwa na “madhara na hasara kubwa,” na huenda baadhi yao wangepoteza uhai. Hata hivyo, nahodha na mwenye meli walitaka kuendelea na safari, huenda kwa kuwa walitaka kufika haraka mahali salama zaidi. Walimsadikisha Yulio, na wengi wao wakakubaliana wajaribu kufika Feniki, bandari iliyokuwa mbali kidogo katika pwani hiyo. Huenda ilikuwa bandari kubwa na nzuri zaidi, mahali ambapo wangeweza kukaa wakati wa majira ya baridi kali. Kwa hiyo, upepo mwanana ulipoanza kupunga kutoka upande wa kaskazini, meli ikang’oa nanga.​—Mdo. 27:10-13.

      12. Baada ya kuondoka Krete, meli ilikumbwa na nini, nao mafundi wa mitambo walifanya nini ili kujaribu kuepuka msiba?

      12 Kisha mambo yakawa mabaya zaidi: kukazuka “upepo mkali” kutoka kaskazini mashariki. Kwa muda fulani, walifichwa na “kisiwa kidogo kinachoitwa Kauda,” kilomita 65 hivi kutoka Bandari Nzuri. Hata hivyo, bado meli hiyo ilikuwa hatarini, ingeweza kusukumwa upande wa kusini na kugonga ukingo wa bahari kwenye pwani ya Afrika. Wakihofia hali hiyo, mabaharia hao wakaivuta mashua ndogo iliyokuwa ikikokotwa na meli yao. Haikuwa rahisi kwa sababu inawezekana ilikuwa imejaa maji. Kisha wakajaribu kuikaza meli isivunjike, wakipitisha kamba au minyororo chini yake ili kushikilia mbao zake pamoja. Kisha wakashusha vifaa vya kuendeshea, tanga na kamba za mlingoti, na kung’ang’ana kuielekeza meli hiyo katika upepo huo hadi dhoruba ipite. Wazia jinsi tukio hilo lilivyokuwa lenye kuogopesha! Hata baada ya kufanya yote hayo, bado meli hiyo iliendelea ‘kurushwarushwa kwa nguvu na dhoruba.’ Siku ya tatu, wakatupa ayari majini, huenda ili kuiwezesha meli hiyo kuelea vizuri.​—Mdo. 27:14-19.

      13. Hali ilikuwaje katika meli ya Paulo wakati wa dhoruba?

      13 Wote walikuwa na hofu kubwa. Hata hivyo, Paulo na wenzake walijipa moyo. Bwana alikuwa amemhakikishia Paulo kwamba atatoa ushahidi Roma, na baadaye malaika akamthibitishia ahadi hiyo. (Mdo. 19:21; 23:11) Hata hivyo, dhoruba hiyo iliendelea kwa majuma mawili, usiku na mchana. Kwa sababu ya mvua iliyokuwa ikinyesha daima na mawingu mazito yaliyozuia nuru ya jua na nyota, kapteni wa meli hangeweza kuona mbali wala kujua wako wapi. Wasafiri hata hawakuweza kula chakula. Isitoshe, ni nani angeweza kula katika mazingira hayo ya baridi, mvua, kichefuchefu, na woga?

      14, 15. (a) Alipokuwa akizungumza na wasafiri wenzake, kwa nini Paulo aliwakumbusha ushauri wake wa awali? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na ujumbe wa tumaini ambao Paulo alitangaza?

      14 Paulo akasimama. Akawakumbusha ushauri aliowapa ijapokuwa hakuwa akiwalaumu na kusema, ‘Si niliwaambia.’ Hata hivyo, mambo yaliyowapata yalionyesha wazi kwamba hawapaswi kamwe kupuuza maneno yake. Kisha akasema: “Sasa ninawahimiza mjipe moyo, kwa maana hakuna hata mmoja wenu atakayepotea, meli tu ndiyo itakayopotea.” (Mdo. 27:21, 22) Lazima maneno hayo yaliwasisimua sana waliokuwa wakimsikiliza! Bila shaka Paulo pia alifurahi sana kwa kuwa Yehova alimpa ujumbe wenye tumaini wa kuwaambia wengine. Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova anajali uhai wa kila mtu. Kila mtu ni mwenye thamani machoni pake. Mtume Petro aliandika: “Yehova . . . hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9) Hivyo basi, tunapaswa kuwatangazia watu wengi iwezekanavyo ujumbe wa tumaini wa Yehova! Uhai wa watu uko hatarini.

      15 Inaelekea Paulo aliwahubiria wengi katika meli hiyo kuhusu “tumaini la ahadi iliyotolewa na Mungu.” (Mdo. 26:6; Kol. 1:5) Sasa, meli yao ikikaribia kuvunjika, Paulo angeweza kutoa msingi thabiti wa tumaini lililo karibu zaidi. Aliwaambia: “Usiku huu malaika wa Mungu ambaye mimi ni mali yake . . . , alisimama kando yangu akasema, ‘Usiogope, Paulo. Utasimama mbele ya Kaisari, na, tazama! Mungu amekupa wale wote wanaosafiri pamoja nawe.’” Kisha Paulo akawahimiza: “Basi jipeni moyo, kwa maana ninamwamini Mungu kwamba itakuwa kama nilivyoambiwa. Hata hivyo, ni lazima tutupwe kwenye ufuo wa kisiwa fulani.”​—Mdo. 27:23-26.

      “Wote Wakafika Salama Kwenye Nchi Kavu” (Mdo. 27:27-44)

      Paulo akisali katika meli ya mizigo iliyojaa watu. Baadhi ya abiria waliochoka wameinamisha vichwa vyao huku wengine wakiwaangalia. Kuna mikate juu ya baadhi ya masanduku.

      “Akamshukuru Mungu mbele yao wote.”—Matendo 27:35

      16, 17. (a) Paulo alitumia nafasi gani kutoa sala, na matokeo yalikuwa nini? (b) Mambo aliyotabiri Paulo yalitimiaje?

      16 Baada ya majuma mawili yenye kutia hofu, na baada ya meli kusukumwa na upepo kilomita 870 hivi, mabaharia hao walianza kuona ishara za mabadiliko, huenda hata walianza kusikia mawimbi yakigonga nchi kavu. Walishusha nanga kutoka kwenye tezi ili wasichukuliwe na mawimbi nao wakaanza kuielekeza meli nchi kavu endapo wangeweza kuifikisha pwani. Kisha, wakajaribu kuondoka melini lakini wakazuiwa na askari. Paulo akamwambia ofisa wa jeshi pamoja na askari hao: “Watu hawa wasipobaki katika meli, ninyi hamwezi kuokoka.” Sasa, meli ikiwa imara kiasi, Paulo aliwahimiza wale chakula, akiwahakikishia tena kwamba wataokoka. Kisha Paulo “akamshukuru Mungu mbele yao wote.” (Mdo. 27:31, 35) Kwa kutoa sala hiyo ya shukrani, Paulo aliwawekea mfano mzuri Luka, Aristarko, na Wakristo wa leo. Je, sala unazotoa mbele za wengine ni zenye kutia moyo na kuwafariji wengine?

      17 Baada ya Paulo kutoa sala, “wote wakajipa moyo, nao pia wakaanza kula.” (Mdo. 27:36) Kisha, wakaanza kupunguza uzito kwa kutupa baharini shehena ya ngano, na hivyo kuiwezesha meli kuelea zaidi inapokaribia pwani. Kulipopambazuka, wakakata nanga, wakafungua amari za makasia ya mtambo wa usukani, na kutweka tanga la mbele ili waweze kuiongoza meli hadi pwani. Omo ya meli ikakwama, huenda katika mchanga au matope, nayo tezi ikaanza kuvunjika kwa sababu ya mawimbi. Askari fulani walitaka kuwaua wafungwa ili yeyote kati yao asitoroke, lakini Yulio akaingilia kati na kuwazuia. Akawahimiza wote waogelee au kuelea juu ya mbao hadi nchi kavu. Aliyotabiri Paulo yakatimia—wote 276 wakaokoka. Ndiyo, “wote wakafika salama kwenye nchi kavu.” Hata hivyo, walikuwa wapi?​—Mdo. 27:44.

      “Fadhili Zinazopita za Kawaida” (Mdo. 28:1-10)

      18-20. Watu wa Malta walionyesha jinsi gani “fadhili zinazopita za kawaida,” na Mungu alifanya muujiza gani kupitia Paulo?

      18 Waokokaji hao walijikuta katika kisiwa cha Malta, upande wa kusini wa Sisili. (Ona sanduku lenye kichwa “Kisiwa cha Malta Kilikuwa Wapi?”) Watu wa kisiwa hicho wanaozungumza lugha ya kigeni walionyesha “fadhili zinazopita za kawaida.” (Mdo. 28:2) Waliwasha moto kwa ajili ya watu hao wasiowajua waliofika pwani wakiwa wamelowa na kutetemeka kwa sababu ya baridi. Moto huo uliwasaidia kujipasha joto. Hali hiyo pia ilitokeza muujiza.

      19 Paulo alijitolea kusaidia kazi. Alikusanya kuni kadhaa, na kuzitia motoni. Alipokuwa akifanya hivyo, nyoka mwenye sumu akatokea, akamuuma, na kujifunga mkononi mwake. Wenyeji hao wa Malta walidhani ni adhabu kutoka kwa Mungu.a

      20 Wenyeji waliomwona nyoka huyo akimuuma Paulo walifikiri “atavimba.” Kulingana na kitabu kimoja, neno la lugha ya awali linalotumiwa hapa ni “neno la kitiba.” Haishangazi kuona “Luka, daktari mpendwa” akitumia neno hilo katika masimulizi yake. (Mdo. 28:6; Kol. 4:14) Vyovyote vile, Paulo alimkung’uta nyoka huyo, naye hakupatwa na madhara yoyote.

      21. (a) Ni habari gani hususa, au sahihi, tunazopata katika masimulizi ya Luka? (b) Paulo alifanya miujiza gani, nayo ilikuwa na matokeo gani kwa wenyeji wa Malta?

      21 Publio, tajiri mwenye mashamba alikuwa akiishi katika eneo hilo. Huenda alikuwa mwakilishi mkuu wa Roma katika kisiwa cha Malta. Luka anamwita “mkuu wa kisiwa hicho,” akitumia jina la cheo linalopatikana katika vitabu viwili vya Kimalta. Aliwakaribisha Paulo na wenzake kwa siku tatu. Hata hivyo, baba ya Publio alikuwa mgonjwa. Kwa mara nyingine tena, Luka anafafanua hali yake kwa usahihi. Anataja ugonjwa hususa aliokuwa nao akisema kwamba “alikuwa amelala kitandani akiugua homa na ugonjwa wa kuhara damu.” Paulo alisali na kuweka mikono yake juu yake, naye akapona. Wakiwa wamevutiwa sana na muujiza huo, wenyeji wa kisiwa hicho wakaleta wagonjwa wengine waponywe, nao wakaleta zawadi kwa ajili ya mahitaji ya Paulo na wenzake.​—Mdo. 28:7-10.

      22. (a) Profesa mmoja amesema nini kuhusu masimulizi ya Luka ya safari ya kwenda Roma? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

      22 Habari kuhusu safari ya Paulo tuliyozungumzia kufikia sasa ni sahihi na kweli. Profesa mmoja alisema: “Masimulizi ya Luka . . . ni mojawapo ya masimulizi yaliyo wazi zaidi katika Biblia nzima. Mambo mbalimbali yanayotajwa kuhusu safari za baharini katika karne ya kwanza ni sahihi kabisa na hali zinazozungumziwa za upande wa mashariki wa Mediterania ni sahihi kabisa,” hivi kwamba lazima ziliandikwa kwa kutegemea daftari ya matukio ya kila siku ya mtu aliyekuwa katika safari hiyo. Yawezekana kwamba Luka alinakili mambo hayo alipokuwa akisafiri na mtume Paulo. Ikiwa alifanya hivyo, basi Luka alikuwa na mengi ya kuandika katika sehemu inayofuata ya safari hiyo. Paulo angepatwa na nini baada ya kufika Roma? Tutaona katika sura inayofuata.

      KISIWA CHA MALTA KILIKUWA WAPI?

      Visiwa mbalimbali vimedhaniwa kuwa “Malta,” ambako meli ya Paulo ilivunjikia. Watu fulani wanakisia kwamba ni kisiwa fulani karibu na Corfu, katika pwani ya magharibi ya Ugiriki. Makisio ya wengine yanategemea neno “Malta” linalotumiwa katika kitabu cha Matendo. Katika Kigiriki, neno hilo ni Me·liʹte. Kwa hiyo, wanafikiri kisiwa hicho ni Melite Illyrica, ambacho sasa kinaitwa Mljet, kilicho katika Bahari ya Adriatiki, karibu na pwani ya Kroatia.

      Ni kweli kwamba andiko la Matendo 27:27 linataja “Bahari ya Adria,” hata hivyo katika siku za Paulo, “Adria” ilitia ndani eneo kubwa zaidi kuliko Bahari ya Adriatiki ya leo. Ilitia ndani Bahari ya Ionia na bahari zilizo upande wa mashariki wa Sisili na upande wa magharibi wa Krete, hivyo ikitia ndani bahari iliyo karibu na eneo ambalo leo linaitwa Malta.

      Meli ambayo Paulo alipanda ililazimika kuelekea upande wa kusini kutoka Kinido kuelekea Krete. Kwa sababu ya pepo za dhoruba hiyo, haielekei kwamba meli hiyo iligeuka na kusafiri kuelekea kaskazini mpaka Mljet au kisiwa kingine karibu na Corfu. Kwa hiyo, uwezekano mkubwa ni kwamba kisiwa cha Malta kilikuwa upande wa magharibi. Ikiwa ndivyo, kisiwa cha Malta kingekuwa upande wa kusini wa Sisili, mahali ambapo huenda ndipo meli inayozungumziwa ilivunjikia.

      a Kwa kuwa wenyeji waliwajua nyoka hao, yaonekana kwamba nyoka hao walikuwako katika kisiwa cha Malta nyakati hizo. Leo, hawapatikani huko. Huenda sababu ikawa kwamba kadiri ambavyo miaka imepita, kumekuwa na mabadiliko ya mazingira. Au nyoka hao waliisha kwa sababu ya ongezeko la watu kwenye kisiwa hicho.

  • “Kutoa Ushahidi Kamili”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 27

      “Kutoa Ushahidi Kamili”

      Paulo afungwa Roma, aendelea kuhubiri

      Matendo 28:11-31

      1. Paulo na wenzake wana uhakika gani, na kwa nini?

      MELI yenye sanamu ya “Wana wa Zeu,” ambayo huenda ni meli kubwa ya nafaka, inasafiri kutoka kisiwani Malta katika Bahari ya Mediterania kwenda Italia. Ni mwaka wa 59 hivi W.K. Mtume Paulo—mfungwa aliye chini ya ulinzi wa askari—pamoja na Wakristo wenzake, Luka na Aristarko, wako katika meli hiyo. (Mdo. 27:2) Tofauti na mafundi wa mitambo wa meli hiyo, waeneza injili hao hawahitaji ulinzi wa ndugu pacha Castor na Pollux, wana wa Zeu, mungu wa Wagiriki. (Mdo. 28:11) Paulo na wenzake ni waabudu wa Yehova, aliyetabiri kwamba Paulo atatoa ushahidi kuhusu ile kweli jijini Roma na kwamba atasimama mbele ya Kaisari.​—Mdo. 23:11; 27:24.

      2, 3. Meli ya Paulo inaelekea wapi, na anategemezwa jinsi gani katika safari yake?

      2 Siku tatu baada ya kutia nanga Sirakusa, jiji lenye kupendeza la Sisili na maarufu kama Athene na Roma, meli yang’oa nanga na kuelekea Regiamu katika rasi ya Italia. Kisha, ikisukumwa na upepo wa kusi, meli hiyo yasafiri umbali wa kilomita 320 hadi bandari ya Italia inayoitwa Puteoli (karibu na mahali panapoitwa Naples leo), na kufika huko siku ya pili, haraka kuliko ilivyo kawaida.​—Mdo. 28:12, 13.

      3 Sasa, Paulo anaanza sehemu ya mwisho ya safari ya kuelekea Roma, ambapo atasimama mbele ya Maliki Nero. Katika safari yake yote, “Mungu wa faraja yote” amekuwa pamoja na Paulo. (2 Kor. 1:3) Kama tutakavyoona, Yehova hakumwacha kamwe; naye Paulo hakupunguza bidii yake akiwa mmishonari.

      “Paulo. . . Akamshukuru Mungu na Kujipa Moyo” (Mdo. 28:14, 15)

      4, 5. (a) Ni ukarimu gani ambao Paulo na wenzake walionyeshwa walipofika Puteoli, na kwa nini Paulo alipewa uhuru mwingi? (b) Hata wanapofungwa gerezani, Wakristo wanaweza kunufaikaje kutokana na mwenendo wao mzuri?

      4 Walipofika Puteoli, Paulo na wenzake ‘waliwakuta akina ndugu huko, wakawasihi wakae pamoja nao kwa siku saba.’ (Mdo. 28:14) Huo ni mfano mzuri sana wa ukarimu wa Kikristo! Bila shaka ndugu hao wakarimu walibarikiwa hata zaidi kwa kuwa Paulo na wenzake waliwatia moyo kiroho. Hata hivyo, mfungwa anayelindwa angewezaje kupata uhuru mwingi hivyo? Huenda kwa sababu walinzi hao Waroma walimwamini kabisa mtume huyo.

      5 Vivyo hivyo leo, watumishi wa Yehova, wanapokuwa katika magereza na kambi za mateso, mara nyingi hupewa uhuru zaidi na kuruhusiwa kufanya mambo ambayo wafungwa wengine hawawezi kwa sababu wakiwa Wakristo, ni wanyoofu na wenye kutegemeka. Kwa mfano, nchini Romania, mtu aliyehukumiwa kifungo cha miaka 75 kwa kosa la wizi, alianza kujifunza Neno la Mungu na kufanya mabadiliko makubwa maishani. Kwa sababu ya mabadiliko aliyokuwa amefanya, wenye mamlaka gerezani walimpa kazi ya kwenda mjini—akiwa peke yake—na kununua vitu vinavyohitajiwa gerezani! Zaidi ya yote, mwenendo wetu mzuri humtukuza Yehova.​—1 Pet. 2:12.

      6, 7. Akina ndugu wa Roma walionyeshaje ukarimu wa pekee?

      6 Kutoka Puteoli, yawezekana kwamba Paulo na wenzake walitembea kwa miguu kilomita 50 hivi hadi Kapua kwenye Njia ya Apio, inayoenda Roma. Ikiwa imetandazwa kwa mawe, njia hiyo maarufu ilikuwa na mandhari zenye kuvutia za nchi ya Italia, na mtu akiwa sehemu fulani katika njia hiyo, angeweza hata kuiona Bahari ya Mediterania. Pia, njia hiyo ilipitia Pontine Marshes, eneo lenye majimaji, kilomita 60 hivi kutoka Roma, ambapo Soko la Apio lilikuwa. Ndugu wa Roma “waliposikia habari zetu,” aandika Luka, baadhi yao walikuja mpaka Soko la Apio, na wengine wakasubiri mahali pa kupumzika panapoitwa Mikahawa Mitatu, umbali wa kilomita 50 hivi kutoka Roma. Walimpenda sana Paulo.​—Mdo. 28:15.

      7 Soko la Apio halikuwa mahali pa kustarehesha, hasa kwa wasafiri waliohitaji kupumzika baada ya safari ndefu yenye kuchosha. Horace, mshairi Mroma, anataja kwamba soko hilo lilikuwa “limesongamana na wenye mashua na wenye mikahawa wajeuri.” Aliandika kwamba “maji yalikuwa yenye kuchukiza.” Naye hata alikataa kula mahali hapo! Bila kujali yote hayo, akina ndugu kutoka Roma walimngoja Paulo na wenzake ili kuwasindikiza katika sehemu ya mwisho ya safari yao.

      8. Kwa nini Paulo alimshukuru Mungu “alipowaona” ndugu zake?

      8 “Alipowaona” ndugu zake, masimulizi yanasema, “Paulo . . . akamshukuru Mungu na kujipa moyo.” (Mdo. 28:15) Ndiyo, alipowaona tu ndugu hao wapendwa, ambao huenda mtume huyo aliwajua baadhi yao kibinafsi, alihisi kwamba amepata nguvu mpya na kufarijiwa. Kwa nini Paulo alimshukuru Mungu? Alijua kwamba upendo usio na ubinafsi ni sehemu ya tunda la roho. (Gal. 5:22) Leo pia, roho takatifu huwachochea Wakristo kujitoa kwa ajili ya wengine na kuwafariji wenye uhitaji.​—1 The. 5:11, 14.

      9. Tunaweza kuigaje roho iliyoonyeshwa na ndugu waliokuja kumpokea Paulo?

      9 Kwa mfano, roho takatifu huwachochea akina ndugu kuwaonyesha ukarimu waangalizi wa mzunguko, wamishonari, na watumishi wengine wa wakati wote, ambao wengi wao wamejinyima mengi ili kumtumikia Yehova kikamili zaidi. Jiulize: ‘Kuna lolote ninaloweza kufanya ili kutegemeza ziara ya mwangalizi wa mzunguko, labda kwa kumwonyesha ukarimu yeye na mke wake ikiwa ameoa? Ninaweza kupanga kuhubiri pamoja nao?’ Ukifanya hivyo utapata baraka nyingi. Kwa mfano, wazia shangwe ambayo ndugu wa Roma walipata walipokuwa wakimsikiliza Paulo na wenzake wakisimulia mambo mengi waliyojionea yenye kujenga imani.​—Mdo. 15:3, 4.

      “Yanasemwa Vibaya Kila Mahali” (Mdo. 28:16-22)

      10. Hali ya Paulo ilikuwaje huko Roma, na mtume huyo alifanya nini mara tu baada ya kufika huko?

      10 Mwishowe, kikundi hicho cha wasafiri kilipoingia Roma, “Paulo aliruhusiwa kukaa peke yake akiwa na mwanajeshi aliyemlinda.” (Mdo. 28:16) Kwa kawaida, wafungwa wa makosa madogo walizuiliwa kwa kufungwa kwa minyororo pamoja na askari walinzi. Hata hivyo, kwa kuwa Paulo alikuwa mtangazaji wa Ufalme, minyororo hiyo haikumfunga kinywa. Kwa hiyo, baada ya kupumzika kwa siku tatu, akawaita wakuu wa Wayahudi waliokuwa Roma ili ajitambulishe na kuwatolea ushahidi.

      11, 12. Alipokuwa akizungumza na Wayahudi wenzake, Paulo alijaribu jinsi gani kuondoa chuki yoyote ambayo huenda walikuwa nayo kumwelekea?

      11 Paulo akasema hivi: “Wanaume, akina ndugu, ingawa sikuwa nimefanya jambo lolote kinyume cha watu au desturi za mababu zetu, nilikabidhiwa nikiwa mfungwa kutoka Yerusalemu na kutiwa mikononi mwa Waroma. Na baada ya kufanya uchunguzi, walitaka kuniacha huru, kwa maana hawakuwa na sababu yoyote ya kuniua. Lakini Wayahudi walipopinga, nililazimika kukata rufaa kwa Kaisari, lakini si kwa sababu nilikuwa na shtaka lolote dhidi ya taifa langu.”​—Mdo. 28:17-19.

      12 Kwa kuwaita Wayahudi hao “ndugu,” Paulo alijaribu kujenga urafiki na kuondoa chuki yoyote ambayo huenda ilikuwa kati yao. (1 Kor. 9:20) Pia, aliwajulisha wazi kwamba hakuja kuwalaumu Wayahudi wenzake, bali ili kukata rufaa kwa Kaisari. Hata hivyo, Wayahudi hao walishangaa kusikia kwamba amekuja kukata rufaa. (Mdo. 28:21) Kwa nini Wayahudi wa Yudea hawakuwajulisha lolote? Kitabu kimoja kinasema: “Inaonekana kwamba meli ya Paulo ilikuwa miongoni mwa meli za kwanza kufika Italia baada ya majira ya baridi kali, nao wawakilishi wa wenye mamlaka miongoni mwa Wayahudi wa Yerusalemu hawakuwa wamefika, wala barua zozote kuhusu kesi hiyo hazikuwa zimewasili.”

      13, 14. Paulo alianzaje kuzungumzia Ufalme, na tunawezaje kuiga mfano wake?

      13 Kisha, Paulo akaanza kuzungumza kuhusu Ufalme. Alianza kwa kutaja jambo ambalo bila shaka liliamsha hamu ya Wayahudi waliokuwa wamekuja. Alisema: “Kwa sababu hii niliomba kuwaona na kuzungumza nanyi, kwa maana nimefungwa mnyororo huu kwa sababu ya tumaini la Israeli.” (Mdo. 28:20) Tumaini hilo lilitegemea Masihi na Ufalme wake uliokuwa ukitangazwa na kutaniko la Kikristo. Wazee hao Wayahudi wakamjibu: “Tunaona inafaa kusikia kutoka kwako maoni yako, kwa maana kwa kweli kuhusu madhehebu haya, tunajua yanasemwa vibaya kila mahali.”​—Mdo. 28:22.

      14 Tunapopata nafasi ya kutangaza habari njema, tunaweza kufuata mfano wa Paulo kwa kutumia maneno yanayoamsha hamu ya wasikilizaji wetu. Tunaweza kupata mapendekezo mazuri katika vitabu kama vile Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha. Je, unavitumia vizuri vitabu hivyo vya kujifunzia Biblia?

      “Kutoa Ushahidi Kamili”​—Mfano Tunaoweza Kufuata (Mdo. 28:23-29)

      15. Ni mambo gani manne yanayojitokeza wazi kuhusiana na njia ya Paulo ya kuhubiri?

      15 Siku iliyopangwa, Wayahudi wenyeji “wakaja wakiwa wengi hata zaidi,” mahali alipoishi Paulo. Naye akawafafanulia jambo hilo “kuanzia asubuhi mpaka jioni . . . na kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu, ili kuwashawishi kumhusu Yesu kwa kutumia Sheria ya Musa na pia Manabii.” (Mdo. 28:23) Mambo manne yanajitokeza wazi kuhusiana na njia ya Paulo ya kuhubiri. Kwanza, alikazia Ufalme wa Mungu. Pili, alijitahidi kuchochea mioyo ya wasikilizaji wake kwa kuwashawishi. Tatu, alijadiliana nao kwa kutumia Maandiko. Nne, alijitolea kwa nafsi yote, akiwahubiria “kuanzia asubuhi mpaka jioni.” Alituwekea mfano mzuri sana! Alipata matokeo gani? “Baadhi yao wakaanza kuamini,” lakini wengine hawakuamini. Mgawanyiko ukazuka, nao watu “wakaanza kuondoka,” asema Luka.​—Mdo. 28:24, 25a.

      16-18. Kwa nini kutoitikia kwa Wayahudi wa Roma hakukumshangaza Paulo, na tunapaswa kuhisije ujumbe wetu unapokataliwa?

      16 Hilo halikumshangaza Paulo, kwa kuwa lilipatana na unabii wa Biblia, isitoshe haikuwa mara ya kwanza kwake kujionea hilo. (Mdo. 13:42-47; 18:5, 6; 19:8, 9) Kwa hiyo, Paulo akawaambia wale waliokuwa wakiondoka: “Kwa kufaa roho takatifu ilisema kupitia Isaya nabii kwa mababu zenu, ikisema, ‘Nenda kwa watu hawa uwaambie: “Kwa kweli mtasikia lakini hamtaelewa kamwe, na kwa kweli mtatazama, lakini hamtaona kamwe. Kwa maana mioyo ya watu hawa imekuwa migumu.”’” (Mdo. 28:25b-27) Neno la lugha ya awali linalotafsiriwa “mgumu” hurejelea moyo “mnene” au “wenye mafuta mengi,” hivi kwamba ujumbe wa Ufalme haungeweza kupenya. (Mdo. 28:27) Ilikuwa hali yenye kusikitisha sana!

      17 Tofauti na Wayahudi hao, Paulo alisema kwamba, ‘mataifa wangesikiliza.’ (Mdo. 28:28; Zab. 67:2; Isa. 11:10) Bila shaka, mtume huyo angeweza kusema hivyo akiwa na uhakika, kwa sababu alijionea Watu wa Mataifa wakikubali ujumbe wa Ufalme!—Mdo. 13:48; 14:27.

      18 Kama Paulo, hatupaswi kuvunjika moyo watu wanapokataa habari njema. Tayari tunajua kwamba ni wachache watakaoipata barabara inayoongoza kwenye uzima. (Mt. 7:13, 14) Pia, watu wenye mwelekeo unaofaa wanapojiunga na ibada ya kweli, tunapaswa kufurahi na kuwakaribisha kwa moyo wote.​—Luka 15:7.

      “Akiwahubiria Ufalme wa Mungu” (Mdo. 28:30, 31)

      19. Ni kwa njia gani Paulo alitumia hali zake vizuri?

      19 Luka anamalizia masimulizi yake kwa jambo lenye kutia moyo sana. Anasema hivi: “[Paulo] akakaa huko kwa miaka miwili kamili katika nyumba yake ya kukodi, naye alikuwa akiwakaribisha kwa fadhili wale wote waliomtembelea, akiwahubiria Ufalme wa Mungu na kuwafundisha kumhusu Bwana Yesu Kristo kwa uhuru mwingi wa kusema, bila kizuizi.” (Mdo. 28:30, 31) Hicho ni kielelezo kizuri sana cha ukarimu, imani, na bidii!

      20, 21. Taja watu mbalimbali walionufaika na huduma ya Paulo katika jiji la Roma.

      20 Mmoja wa watu waliopokewa na Paulo kwa fadhili ni Onesimo, mtumwa aliyetoroka Kolosai. Paulo alimsaidia Onesimo kuwa Mkristo, naye Onesimo akawa “ndugu . . . mwaminifu na mpendwa” kwa Paulo. Paulo anamwita “mwanangu . . . ambaye nimekuwa baba yake.” (Kol. 4:9; Flm. 10-12) Bila shaka Onesimo alimtia moyo sana Paulo!a

      21 Wengine pia walinufaika na mfano mzuri wa Paulo. Aliwaandikia hivi Wafilipi: “Hali yangu kwa kweli imesaidia kuendeleza habari njema, hivi kwamba vifungo vyangu vya gereza kwa ajili ya Kristo vimejulikana wazi kati ya Walinzi wote wa Mfalme na watu wengine wote. Sasa akina ndugu wengi katika Bwana wamekuwa na uhakika kwa sababu ya vifungo vyangu vya gereza, nao wanaonyesha uhodari mwingi wa kulisema neno la Mungu bila woga.”​—Flp. 1:12-14.

      22. Paulo alitumia wakati wake jinsi gani alipokuwa mfungwa jijini Roma?

      22 Paulo alitumia wakati wake akiwa mfungwa jijini Roma kuandika barua muhimu ambazo sasa ni sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.b Barua hizo walizoandikiwa Wakristo wa karne ya kwanza, ziliwanufaisha sana. Sisi pia tunanufaika na barua za Paulo kwa sababu ushauri aliotoa ulioongozwa na roho unatufaa leo pia.​—2 Tim. 3:16, 17.

      BARUA TANO ALIZOANDIKA PAULO ALIPOFUNGWA ROMA MARA YA KWANZA

      Mtume Paulo aliandika barua tano mwaka wa 60-61 hivi W.K., alipofungwa jijini Roma mara ya kwanza. Katika barua yake kwa Filemoni, mwabudu mwenzake, Paulo anaeleza kwamba Onesimo, aliyekuwa mtumwa wa Filemoni lakini akatoroka, amekuwa Mkristo. Paulo alikuwa baba yake wa kiroho, naye alikuwa akimtuma mtumwa huyo ambaye ‘zamani hakufaa kitu’ arudi kwa bwana wake akiwa ndugu Mkristo.​—Flm. 10-12, 16.

      Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo anataja kwamba Onesimo alikuwa ‘anatoka kwao.’ (Kol. 4:9) Onesimo na Mkristo mwenzake Tikiko, walikuwa na pendeleo la kupeleka barua hizo mbili pamoja na barua ambayo Paulo aliwaandikia Waefeso.​—Efe. 6:21.

      Anapowaandikia Wafilipi, Paulo anataja ‘vifungo vyake vya gereza,’ kisha anataja hali ya ndugu aliyepeleka barua hiyo, Epafrodito. Wafilipi walikuwa wamemtuma Epafrodito akamsaidie Paulo. Lakini Epafrodito akawa mgonjwa karibu kufa. Pia, alikuwa amehuzunika sana kwa sababu Wafilipi ‘walisikia alikuwa mgonjwa.’ Kwa sababu hiyo, Paulo aliwaambia wawaheshimu sana “watu wa namna hiyo.”​—Flp. 1:7; 2:25-30.

      Barua kwa Waebrania iliandikwa kwa ajili ya Wakristo Waebrania waliokuwa Yudea. Ingawa barua yenyewe haitaji mwandikaji ni nani, uthibitisho unaonyesha kwamba Paulo ndiye aliyeiandika. Mtindo wa kuandika ni wake. Paulo anatuma salamu kutoka Italia, na anamtaja Timotheo, ambaye alikuwa pamoja naye Roma.​—Flp. 1:1; Kol. 1:1; Flm. 1; Ebr. 13:23, 24.

      23, 24. Kama Paulo, Wakristo wengi leo wamedumishaje shangwe yao na kuendelea kuhubiri ijapokuwa wamefungwa isivyo haki?

      23 Kufikia wakati ambapo alifunguliwa, ijapokuwa hautajwi katika kitabu cha Matendo, Paulo alikuwa amekaa gerezani miaka minne—miwili Kaisaria na miwili Roma.c (Mdo. 23:35; 24:27) Hata hivyo, hakupoteza shangwe, bali aliendelea kufanya yote aliyoweza katika utumishi wa Mungu. Vivyo hivyo pia, watumishi wengi wa Yehova leo, ijapokuwa wanatiwa gerezani isivyo haki kwa sababu ya imani yao, wao huendelea kuwa na shangwe na kuendelea kuhubiri. Fikiria mfano wa Adolfo, aliyefungwa huko Hispania kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. “Unatushangaza,” akasema ofisa mmoja. “Tumekuwa tukifanya maisha yako yawe magumu, na kadiri tunavyozidi ndivyo unavyozidi kutabasamu na kuzungumza nasi kwa fadhili.”

      24 Baada ya muda, Adolfo aliaminika kiasi cha kwamba mlango wa chumba chake cha gereza ulikuwa ukiachwa wazi. Askari walikuwa wakija kumuuliza maswali ya Biblia. Hata mlinzi mmoja alikuwa akiingia katika chumba cha Adolfo ili kuisoma Biblia, huku Adolfo akimlinda asikamatwe. Kwa hiyo, mfungwa akawa “akimlinda” mlinzi! Mfano mzuri wa Mashahidi kama hao na utuchochee kuonyesha “uhodari mwingi wa kulisema neno la Mungu bila woga,” hata chini ya hali ngumu.

      25, 26. Paulo alijionea utimizo wa unabii gani miaka isiyozidi 30 baadaye, na hali hiyo inalingana jinsi gani na siku zetu?

      25 Mtume wa Kristo aliye katika kifungo cha nyumbani “akiwahubiria Ufalme wa Mungu” wote wanaomtembelea—mwisho wenye kutia moyo sana wa kitabu cha Matendo! Katika sura ya kwanza, tulisoma kuhusu mgawo ambao Yesu aliwapa wafuasi wake aliposema: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Sasa, miaka isiyozidi 30 baadaye, tayari ujumbe wa Ufalme ulikuwa umehubiriwa “katika uumbaji wote chini ya mbingu.”d (Kol. 1:23) Huo ni ushahidi mkubwa wa nguvu za roho ya Mungu!—Zek. 4:6.

      26 Leo, roho hiyo imewawezesha ndugu za Kristo na waandamani wao, “kondoo wengine,” kuendelea “kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu” katika nchi zaidi ya 240! (Yoh. 10:16; Mdo. 28:23) Je, unashiriki kikamili katika kazi hiyo?

      MAISHA YA PAULO BAADA YA MWAKA WA 61 W.K.

      Inaonekana kwamba katika mwaka wa 61 hivi W.K., Paulo alifikishwa mbele ya Maliki Nero, ambaye yaelekea alikata kauli kwamba Paulo hana hatia. Hatujui mengi kuhusu shughuli za mtume huyo baada ya hapo. Ikiwa alifunga safari aliyopanga ya kwenda Uhispania, basi huenda alienda wakati huo. (Rom. 15:28) Paulo alisafiri “katika sehemu za mbali za [Magharibi],” akaandika Clement wa Roma mwaka wa 95 hivi W.K.

      Tunaposoma barua tatu za Paulo alizoandika wakati huo baada ya kufunguliwa—barua ya 1 na ya 2 ya Timotheo na Tito—ni wazi kwamba Paulo alienda Krete, Makedonia, Nikopoli, na Troa. (1 Tim. 1:3; 2 Tim. 4:13; Tito 1:5; 3:12) Huenda alikamatwa tena alipokuwa Nikopoli, Ugiriki. Vyovyote vile, mwaka wa 65 hivi W.K., alifungwa tena gerezani jijini Roma. Hata hivyo, wakati huo Nero hakumwonyesha rehema. Kulingana na Tasito, mwanahistoria Mroma, moto ulipoteketeza jiji hilo mwaka wa 64 W.K., Nero aliwalaumu Wakristo kwa uwongo kwamba walianzisha moto huo, naye akaanza kampeni kali ya kuwatesa.

      Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, Paulo, akitazamia kuuawa karibuni, aliwaomba Timotheo na Marko waje kwake upesi. Inapendeza kuona ujasiri wa Luka na Onesiforo, waliohatarisha uhai wao ili kumfariji Paulo. (2 Tim. 1:16, 17; 4:6-9, 11) Wakati huo, ikiwa mtu angekiri hadharani kuwa Mkristo, angekamatwa na hata kuuawa kikatili. Yaelekea kwamba Paulo aliuawa kwa sababu ya imani yake muda mfupi baada ya kuandika barua yake ya mwisho kwa Timotheo mwaka wa 65 hivi W.K. Inasemekana kwamba Nero mwenyewe aliuawa kikatili miaka mitatu hivi baada ya Paulo kuuawa.

      HABARI NJEMA “ILIHUBIRIWA KATIKA UUMBAJI WOTE”

      Mwaka wa 61 hivi W.K., mtume Paulo akiwa bado gerezani jijini Roma, aliandika kwamba “habari njema . . . ilihubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Alimaanisha nini?

      Inaonekana Paulo alikuwa akieleza kwa ujumla jinsi “habari njema” ilivyokuwa imeenea sana. Kwa mfano, Aleksanda Mkuu alikuwa ameingia Asia hadi mipaka ya India katika karne ya nne K.W.K. Kaisari Yulio alikuwa amevamia Uingereza mwaka wa 55 K.W.K., naye Klaudio alikuwa ameteka sehemu ya kusini ya kisiwa hicho na kukifanya kuwa sehemu ya Milki ya Roma katika mwaka wa 43 W.K. Eneo la Mashariki ya Mbali lilijulikana pia, kwa sababu hariri nzuri ilikuwa ikipatikana huko.

      Je, habari njema ilikuwa imehubiriwa Uingereza, China, na Mashariki ya Mbali? Haielekei. Paulo alipowaandikia Wakolosai, hakuwa ametimiza mradi wake alioweka mwaka wa 56 hivi W.K., lengo la kuhubiri Uhispania, ambako wakati huo lilikuwa “eneo ambalo halijaguswa.” (Rom. 15:20, 23, 24) Hata hivyo, kufikia mwaka wa 61 hivi W.K., ujumbe wa Ufalme ulikuwa umejulikana sana. Angalau ulikuwa umefika maeneo ya Wayahudi na wageuzwa imani waliobatizwa wakati wa Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., na pia katika nchi ambazo mitume wa Yesu walitembelea.​—Mdo. 2:1, 8-11, 41, 42.

      a Paulo alitaka Onesimo akae naye, lakini hilo lingevunja sheria za Roma na vilevile haki za Mkristo Filemoni, bwana mkubwa wa Onesimo. Kwa hiyo, Onesimo akarudi kwa Filemoni, akiwa na barua kutoka kwa Paulo iliyomhimiza Filemoni ampokee kwa fadhili, kama ndugu yake wa kiroho.​—Flm. 13-19.

      b Ona sanduku lenye kichwa “Barua Tano Alizoandika Paulo Alipofungwa Roma Mara ya Kwanza.”

      c Ona sanduku lenye kichwa “Maisha ya Paulo Baada ya Mwaka wa 61 W.K.”

      d Ona sanduku lenye kichwa “Habari Njema ‘Ilihubiriwa Katika Uumbaji Wote.’”

  • “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
    • SURA YA 28

      “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”

      Mashahidi wa Yehova wanaendeleza kazi iliyoanzishwa na wafuasi wa Yesu Kristo katika karne ya kwanza

      1. Kuna ulinganifu gani kati ya hali ya Wakristo wa karne ya kwanza na Mashahidi wa Yehova leo?

      WALITOA ushahidi kwa bidii. Mioyo yao iliwachochea kukubali msaada na mwongozo wa roho takatifu. Mateso hayakuwanyamazisha. Naye Mungu aliwabariki sana. Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza, kama vile ilivyo kwa Mashahidi wa Yehova leo.

      2, 3. Kwa nini kitabu cha Matendo ni cha pekee?

      2 Bila shaka, umetiwa moyo na masimulizi yenye kuimarisha imani na yenye kusisimua ya kitabu cha Biblia cha Matendo ya Mitume! Kitabu hicho ni cha pekee. Ndicho kitabu pekee kilichoongozwa na roho ya Mungu, ambacho kinaeleza historia ya Wakristo wa karne ya kwanza.

      3 Kitabu cha Matendo kinataja watu 95 kutoka nchi 32, majiji 54, na visiwa 9. Ni masimulizi yenye kusisimua kuhusu watu wa kawaida, wafuasi wa dini wenye majivuno, wanasiasa wenye kiburi, na watesaji wakatili. Lakini zaidi ya yote, kinasimulia kuhusu ndugu na dada zako wa karne ya kwanza, ambao licha ya hali ngumu ambazo ni kawaida maishani, waliendelea kuhubiri habari njema kwa bidii.

      4. Ni nini kinachofanya tuwe na uhusiano wa karibu pamoja na watu kama vile mtume Paulo, Tabitha, na Mashahidi wengine wengi waaminifu wa zamani?

      4 Miaka 2,000 hivi imepita tangu siku za mitume wenye bidii Petro na Paulo, daktari mpendwa Luka, Barnaba aliyekuwa mkarimu, Stefano mwenye ujasiri, Tabitha mwenye fadhili, Lidia mkaribishaji wageni, na Mashahidi wengine wengi waliokuwa waaminifu. Ingawa waliishi miaka mingi iliyopita, tunahisi tuna uhusiano wa karibu pamoja nao. Kwa nini? Kwa sababu sisi pia tuna mgawo wa kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Tuna pendeleo kubwa sana la kushiriki katika kazi hiyo!

      Paulo akiwa katika ubaraza wa ghorofa akitazama jiji la Roma huku yeye na mwanajeshi wakiwa wamefungwa mnyororo.

      “. . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Matendo 1:8

      5. Wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza walianza kuhubiri wapi?

      5 Hebu fikiria kazi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake. Aliwaambia: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kwanza, roho takatifu iliwawezesha wanafunzi kutoa ushahidi “katika Yerusalemu.” (Mdo. 1:1–8:3) Halafu, wakiongozwa na roho, wakatoa ushahidi “katika Yudea yote na Samaria.” (Mdo. 8:4–13:3) Kisha wakaanza kuhubiri “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”​—Mdo. 13:4–28:31.

      6, 7. Katika huduma yetu, tuna nini ambacho waamini wenzetu wa karne ya kwanza hawakuwa nacho?

      6 Waamini wenzako wa karne ya kwanza hawakuwa na Biblia nzima ili kuitumia katika kazi ya kuhubiri. Injili ya Mathayo haikuwa imeandikwa mpaka karibu mwaka wa 41 W.K. Baadhi ya barua za Paulo ziliandikwa kabla ya kitabu cha Matendo kukamilishwa, karibu mwaka wa 61 W.K. Lakini Wakristo wa karne ya kwanza hawakuwa na nakala za kibinafsi za Maandiko yote Matakatifu wala vitabu na magazeti ya kuwapatia watu wanaopendezwa. Kabla ya kuwa wanafunzi wa Yesu, Wakristo Wayahudi walikuwa wamesikia Maandiko ya Kiebrania yakisomwa katika sinagogi. (2 Kor. 3:14-16) Hata hivyo, wao pia walipaswa kujifunza kwa bidii, kwa kuwa huenda walihitaji kukariri maandiko.

      7 Leo, wengi wetu tuna nakala yetu wenyewe ya Biblia na vitabu vingi vinavyotegemea Biblia. Tunafanya wanafunzi kwa kuhubiri habari njema katika nchi 240 na katika lugha nyingi.

      Kutiwa Nguvu na Roho Takatifu

      8, 9. (a) Roho takatifu iliwawezesha wanafunzi wa Yesu kufanya nini? (b) Mtumwa mwaminifu anatokeza nini kwa msaada wa roho ya Mungu?

      8 Yesu alipowaamuru wanafunzi wake wawe mashahidi, aliwaambia: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu.” Wakiongozwa na roho ya Mungu, au nguvu zake za utendaji, hatimaye wafuasi wa Yesu wangekuwa mashahidi duniani pote. Kwa msaada wa roho takatifu, Petro na Paulo waliponya wagonjwa, wakawafukuza roho waovu, na hata kufufua wafu! Hata hivyo, nguvu walizopata kupitia roho takatifu zilikuwa na kusudi muhimu zaidi. Ziliwawezesha mitume na wale wanafunzi wengine kuwapa watu ujuzi sahihi ili wapate uzima wa milele.​—Yoh. 17:3.

      9 Katika siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wa Yesu walisema “katika lugha mbalimbali, kama roho ilivyowawezesha kusema.” Hivyo, wakatoa ushahidi kuhusu “mambo makuu ya Mungu.” (Mdo. 2:1-4, 11) Leo, hatuzungumzi kimuujiza katika lugha mbalimbali. Hata hivyo, chini ya mwelekezo wa roho ya Mungu, mtumwa mwaminifu anatoa vitabu na magazeti yanayotegemea Biblia katika lugha nyingi. Kwa mfano, mamilioni ya magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yanachapishwa kila mwezi, na pia katika tovuti yetu ya jw.org, kuna machapisho yanayotegemea Biblia na video katika lugha zaidi ya 1,000. Yote hayo yanatusaidia kutangaza “mambo makuu ya Mungu” kwa watu wa mataifa yote, makabila, na lugha.​—Ufu. 7:9.

      10. Tangu mwaka wa 1989, ni nini kimefanywa kuhusiana na kutafsiri Biblia?

      10 Tangu mwaka wa 1989, mtumwa mwaminifu ameongeza jitihada za kuhakikisha kwamba Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika lugha nyingi. Tayari Biblia hiyo imetafsiriwa katika lugha zaidi ya 200, na mamilioni ya nakala yamechapishwa—nyingine nyingi zikiwa njiani. Mungu tu, kupitia roho yake, ndiye amefanikisha jitihada hizo.

      11. Ni mambo gani yametimizwa kuhusiana na kutafsiriwa kwa machapisho ya Mashahidi wa Yehova?

      11 Kazi ya kutafsiri inafanywa na maelfu ya Wakristo wanaojitolea katika nchi na maeneo zaidi ya 150. Hilo halitushangazi kwa kuwa hakuna tengenezo lingine lolote duniani linaloongozwa na roho takatifu katika “kutoa ushahidi kamili” ulimwenguni pote kumhusu Yehova Mungu, Mfalme wake wa Kimasihi, na Ufalme uliosimamishwa mbinguni!—Mdo. 28:23.

      12. Ni nini kilichomsaidia Paulo na Wakristo wengine kutoa ushahidi?

      12 Paulo alipowahubiria Wayahudi na Watu wa Mataifa katika Antiokia ya Pisidia, “wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.” (Mdo. 13:48) Luka anapokamilisha kuandika kitabu cha Matendo, Paulo angali ‘akihubiri ufalme wa Mungu . . . kwa uhuru mwingi wa kusema, bila kizuizi.’ (Mdo. 28:31) Mtume huyo anahubiri wapi? Katika jiji la Roma—makao makuu ya serikali kuu ya ulimwengu! Iwe ni kupitia hotuba au njia nyingine, wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza walifanya kazi yao ya kutoa ushahidi kwa msaada na mwongozo wa roho takatifu.

      Uvumilivu Licha ya Mateso

      13. Kwa nini tunapaswa kusali tunapokabili mateso?

      13 Wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza walipoteswa, walimwomba Yehova awape ujasiri. Ikawaje? Walijazwa roho takatifu na kuwezeshwa kusema neno la Mungu kwa ujasiri. (Mdo. 4:18-31) Sisi pia husali ili tupate hekima na nguvu za kuendelea kutoa ushahidi licha ya mateso. (Yak. 1:2-8) Kwa kuwa tuna baraka za Mungu na msaada wa roho yake, tunaendelea kutangaza Ufalme. Hakuna chochote kinachoweza kuzuia kazi ya kutoa ushahidi—iwe ni upinzani mkali au mateso ya kikatili. Tunapoteswa, tunahitaji kumwomba Yehova atupatie roho takatifu, hekima, na ujasiri wa kutangaza habari njema.​—Luka 11:13.

      14, 15. (a) Mambo yalikuwaje baada ya “dhiki iliyotokea kwa sababu ya Stefano”? (b) Katika siku zetu, watu wengi katika eneo la Siberia walipataje kweli?

      14 Stefano alitoa ushahidi kwa ujasiri kabla ya kuuawa na adui zake. (Mdo. 6:5; 7:54-60) Kutaniko lilipoanza “kuteswa sana,” wanafunzi wote isipokuwa mitume walitawanyika kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria. Lakini hilo halikuzuia kazi ya kutoa ushahidi. Filipo alienda Samaria ‘kuwahubiria kumhusu Kristo,’ naye alipata matokeo mazuri. (Mdo. 8:1-8, 14, 15, 25) Isitoshe, tunaambiwa: “Wale waliokuwa wametawanyika kwa sababu ya dhiki iliyotokea kuhusiana na Stefano, wakaenda mpaka Foinike, Kipro, na Antiokia, lakini walitangaza lile neno kwa Wayahudi tu. Hata hivyo, wanaume fulani kati yao kutoka Kipro na Kirene walikuja Antiokia na kuanza kuongea na watu waliozungumza Kigiriki, wakitangaza habari njema ya Bwana Yesu.” (Mdo. 11:19, 20) Wakati huo, mateso yalichangia kuenezwa kwa ujumbe wa Ufalme.

      15 Katika siku zetu, jambo kama hilo lilitokea katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Hasa katika miaka ya 1950, maelfu ya Mashahidi wa Yehova walipelekwa uhamishoni Siberia. Kwa kuwa walipelekwa katika kambi mbalimbali, habari njema iliendelea kuenea katika eneo hilo kubwa. Bila shaka, Mashahidi wengi hivyo hawangeweza kamwe kupata pesa za kusafiri kilomita zaidi ya 10,000 ili kutangaza habari njema! Hata hivyo, serikali yenyewe iliwapeleka sehemu mbalimbali za nchi hiyo. Ndugu mmoja alisema: “Wenye mamlaka wenyewe waliwasaidia maelfu ya watu wanyoofu katika eneo la Siberia kujua kweli.”

      Baraka Nyingi za Yehova

      16, 17. Kitabu cha Matendo kinataja mambo gani yanayoonyesha kwamba Yehova anabariki kazi ya kutoa ushahidi?

      16 Bila shaka Yehova aliwabariki sana Wakristo wa karne ya kwanza. Paulo na wengine walipanda na kutilia maji, “lakini Mungu akaendelea kuikuza.” (1 Kor. 3:5, 6) Kitabu cha Matendo kina mifano mingi ya ukuzi huo unaopatikana kwa sababu ya baraka za Yehova katika kazi ya kutoa ushahidi. Kwa mfano, “Neno la Mungu likazidi kuenea, na idadi ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana huko Yerusalemu.” (Mdo. 6:7) Kadiri kazi ya kutoa ushahidi ilivyoenea, “kutaniko katika eneo lote la Yudea, Galilaya, na Samaria likaingia katika kipindi cha amani, huku likijengwa; nalo lilipokuwa likitembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu, likaendelea kuongezeka.”​—Mdo. 9:31.

      17 Katika Antiokia ya Siria, Wayahudi na watu waliozungumza Kigiriki walihubiriwa na mashahidi wenye ujasiri. Masimulizi yanasema: “Isitoshe, mkono wa Yehova ulikuwa pamoja nao, na idadi kubwa wakawa waamini na kumgeukia Bwana.” (Mdo. 11:21) Tunasoma hivi kuhusu maendeleo zaidi katika jiji hilo: “Neno la Yehova likazidi kukua na kuenea.” (Mdo. 12:24) Na kwa sababu ya bidii ya Paulo na wengine katika kazi ya kutoa ushahidi kwa Watu wa Mataifa, “kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi.”​—Mdo. 19:20.

      18, 19. (a) Tunajuaje kwamba “mkono wa Yehova” uko pamoja nasi? (b) Toa mfano unaoonyesha kwamba Yehova huwategemeza watu wake.

      18 Bila shaka, “mkono wa Yehova” uko pamoja nasi leo. Ndiyo sababu watu wengi sana wanakuwa wanaamini na kuonyesha wakfu wao kwa Mungu kwa kubatizwa. Isitoshe, msaada na baraka za Mungu zinatuwezesha kuvumilia upinzani—au hata mateso makali—na kuendelea kuitimiza huduma yetu kwa mafanikio, kama vile Paulo na Wakristo wengine wa karne ya kwanza walivyofanya. (Mdo. 14:19-21) Yehova Mungu atatusaidia sikuzote. “Mikono [yake] ya milele” inaendelea kutusaidia katika majaribu yetu yote. (Kum. 33:27) Na pia tusisahau kwamba kwa sababu ya jina lake kuu, Yehova hatawaacha kamwe watu wake.​—1 Sam. 12:22; Zab. 94:14.

      19 Kwa mfano: Maofisa wa Nazi walimpeleka Ndugu Harald Abt katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu kwa sababu ya kazi yake ya kutoa ushahidi. Mnamo Mei 1942, polisi wapelelezi walienda alipokuwa akikaa mke wake, Elsa, wakamchukua binti yao mdogo, na kumkamata Elsa. Alipelekwa katika kambi mbalimbali za mateso. Dada Abt alisema: “Muda niliokaa katika kambi za mateso za Ujerumani, ulinifundisha jambo fulani muhimu. Kwamba roho ya Yehova inaweza kukutia nguvu unapokuwa chini ya jaribu kali! Kabla ya kukamatwa nilikuwa nimesoma barua ya dada mmoja aliyeandika kwamba wakati wa majaribu makali, roho ya Yehova hutusaidia kuwa watulivu. Nilifikiri kwamba alikuwa akitia chumvi. Lakini mimi mwenyewe nilipokuwa nikijaribiwa, nilitambua ukweli wa mambo aliyosema. Kwa kweli, ndivyo inavyokuwa. Si rahisi kuwazia, ikiwa wewe binafsi hujapatwa na majaribu. Lakini kwangu, ndivyo ilivyokuwa.”

      Endelea Kutoa Ushahidi Kamili!

      20. Paulo alifanya nini alipokuwa katika kifungo cha nyumbani, na hilo linawezaje kuwatia moyo baadhi ya ndugu na dada zetu?

      20 Masimulizi ya kitabu cha Matendo yanamalizika Paulo ‘akihubiri Ufalme wa Mungu,’ kwa bidii. (Mdo. 28:31) Kwa sababu alikuwa katika kifungo cha nyumbani, hakuwa na uhuru wa kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba katika jiji la Roma. Hata hivyo, aliendelea kuwahubiria waliomtembelea. Leo, baadhi ya ndugu na dada zetu hawawezi kutoka nyumbani, labda ni wagonjwa kitandani, au wako katika makao ya kuwatunzia wazee, wagonjwa, au walemavu. Hata hivyo, upendo wao kwa Mungu na tamaa yao ya kutoa ushahidi bado ni yenye nguvu. Tunasali kwa ajili yao na tunaweza kumwomba Baba yetu wa mbinguni awasaidie wakutane na watu wanaotaka kujifunza kumhusu na kuhusu makusudi yake mazuri.

      21. Kwa nini tunapaswa kutoa ushahidi haraka?

      21 Wengi wetu tunaweza kushiriki katika utumishi wa nyumba kwa nyumba na katika njia nyingine za kufanya wanafunzi. Kwa hiyo, kila mmoja wetu na afanye kila awezalo ili tutimize wajibu wetu tukiwa watangazaji wa Ufalme, na kushiriki kutoa ushahidi “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” Lazima kazi hii ifanywe haraka, kwa sababu “ishara” ya kuwapo kwa Kristo inaonekana wazi. (Mt. 24:3-14) Hatuna wakati wa kupoteza. Tuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”​—1 Kor. 15:58.

      22. Tunapaswa kuazimia kufanya nini tunaipongojea siku ya Yehova?

      22 Tunapongojea “kuja kwa ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha,” na tuazimie kuendelea kutoa ushahidi kwa ujasiri na kwa uaminifu. (Yoe. 2:31) Bado tutapata watu wengi walio kama Waberoya ambao “walilikubali neno kwa hamu kubwa ya akili.” (Mdo. 17:10, 11) Kwa hiyo, na tuendelee kutoa ushahidi mpaka tutakapoambiwa: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu!” (Mt. 25:23) Tukitimiza sehemu yetu kwa bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi leo na kudumisha uaminifu wetu kwa Yehova, bila shaka, tutafurahi milele kwamba tulishiriki katika “kutoa ushahidi kamili” kuhusu Ufalme wa Mungu!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki