Luka
18 Ndipo akaendelea kuwaambia mfano juu ya uhitaji wao wa kusali sikuzote bila kukata tamaa,+ 2 akisema: “Katika jiji fulani kulikuwako mwamuzi fulani ambaye hakuwa akimwogopa Mungu wala hakuwa na heshima kwa mwanadamu. 3 Lakini kulikuwako mjane katika jiji hilo naye akawa akimwendea,+ akisema, ‘Hakikisha kwamba nitapata haki kutoka kwa mshitaki wangu.’ 4 Basi, kwa muda fulani alikuwa hana nia, lakini baadaye akasema moyoni mwake, ‘Ijapokuwa mimi simwogopi Mungu wala simheshimu mwanadamu, 5 hakika, kwa sababu ya kuendelea kwa mjane huyu kunisumbua,+ nitahakikisha kwamba atapata haki, ili asiendelee kuja kunishambulia+ mpaka animalize.’ ” 6 Ndipo Bwana akasema: “Sikieni lile ambalo mwamuzi huyo, ijapokuwa si mwadilifu, alisema! 7 Basi, kwa hakika je, Mungu hatasababisha haki+ ifanywe kwa ajili ya watu wake waliochaguliwa ambao wanampaazia sauti mchana na usiku, hata ingawa ana ustahimilivu+ kwao? 8 Ninawaambia ninyi, Yeye atasababisha watendewe haki upesi.+ Hata hivyo, Mwana wa binadamu atakapofika, je, kwa kweli ataipata imani duniani?”
9 Lakini akawaambia mfano huu pia baadhi ya wale waliokuwa wakiamini kwamba walikuwa waadilifu+ na kuwaona wale wengine kama si kitu:+ 10 “Watu wawili walipanda kuingia hekaluni ili kusali, mmoja alikuwa Farisayo na yule mwingine alikuwa mkusanya-kodi. 11 Yule Farisayo akasimama+ na kuanza kusali+ mambo haya akisema moyoni, ‘Ee Mungu, ninakushukuru ya kuwa mimi si kama wale watu wengine, wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi, au hata kama mkusanya-kodi huyu.+ 12 Mimi hufunga mara mbili kwa juma, mimi hutoa sehemu ya kumi ya vitu vyote ninavyojipatia.’+ 13 Lakini yule mkusanya-kodi akiwa amesimama umbali fulani hakutaka hata kuinua macho yake kuelekea mbinguni, bali alikuwa akipiga-piga kifua chake,+ akisema, ‘Ee Mungu, unirehemu mimi mtenda-dhambi.’+ 14 Ninawaambia ninyi, Mtu huyu alishuka kwenda nyumbani kwake akiwa amethibitishwa kuwa mwadilifu+ zaidi kuliko yule mwingine; kwa sababu kila mtu anayejiinua atafedheheshwa, bali yule anayejinyenyekeza atainuliwa.”+
15 Sasa watu wakaanza kumletea pia watoto wao wachanga ili awaguse; lakini walipoona hilo wanafunzi wakaanza kuwakemea.+ 16 Hata hivyo, Yesu akawaita wale watoto, akisema: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu, wala msijaribu kuwazuia. Kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.+ 17 Kwa kweli ninawaambia ninyi, Mtu yeyote ambaye haupokei ufalme wa Mungu kama mtoto mchanga hataingia kamwe ndani yake.”+
18 Na mtawala fulani akamuuliza, akisema: “Mwalimu Mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”+ 19 Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniita mwema? Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.+ 20 Wewe unazijua amri,+ ‘Usifanye uzinzi,+ Usiue,+ Usiibe,+ Usitoe ushahidi wa uwongo,+ Mheshimu baba yako na mama yako.’ ”+ 21 Ndipo akasema: “Yote hayo nimeyashika tangu ujana wangu na kuendelea.”+ 22 Baada ya kusikia hilo, Yesu akamwambia: “Bado kuna jambo moja unalokosa: Uza vitu vyote ulivyo navyo uwagawie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 23 Aliposikia neno hilo, akahuzunika sana, kwa maana alikuwa tajiri sana.+
24 Yesu akamtazama na kusema: “Jinsi itakavyokuwa vigumu kwa wale walio na pesa kuingia katika ufalme wa Mungu!+ 25 Kwa kweli, ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano ya kushonea kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.”+ 26 Wale waliosikia hilo wakasema: “Ni nani anayeweza kuokolewa?” 27 Akasema: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.”+ 28 Lakini Petro akasema: “Tazama! Tumeacha vitu vyetu wenyewe na kukufuata wewe.”+ 29 Akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Hakuna yeyote ambaye ameacha nyumba au mke au ndugu au wazazi au watoto kwa ajili ya ufalme wa Mungu+ 30 ambaye hatapata mara nyingi zaidi katika kipindi hiki cha wakati, na katika mfumo wa mambo unaokuja uzima wa milele.”+
31 Ndipo akawachukua wale kumi na wawili kando na kuwaambia: “Tazameni! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na mambo yote yaliyoandikwa kupitia manabii+ juu ya Mwana wa binadamu yatatimia.+ 32 Kwa mfano, atatiwa mikononi mwa watu wa mataifa naye atadhihakiwa+ na kutendewa kwa dharau+ na kutemewa mate;+ 33 na baada ya kumpiga mijeledi+ watamuua,+ lakini katika siku ya tatu atafufuka.”+ 34 Hata hivyo, wao hawakupata maana ya lolote kati ya mambo hayo; lakini walikuwa wamefichwa maneno hayo, nao hawakujua mambo yaliyosemwa.+
35 Sasa alipokuwa akikaribia Yeriko mtu fulani aliye kipofu alikuwa ameketi kando ya barabara akiombaomba.+ 36 Kwa sababu aliusikia umati ukipita, akaanza kuuliza maana ya mambo hayo. 37 Wakamwambia: “Yesu Mnazareti anapitia hapa!”+ 38 Ndipo akapaaza sauti, akisema: “Yesu, Mwana wa Daudi, unirehemu!”+ 39 Na wale waliokuwa mbele wakaanza kumwambia kwa kusisitiza anyamaze, lakini ndivyo naye alivyozidi kupaaza sauti: “Mwana wa Daudi, unirehemu.”+ 40 Ndipo Yesu akasimama tuli na kuamuru mtu huyo aletwe kwake.+ Alipokaribia, Yesu akamuuliza: 41 “Unataka nikufanyie nini?”+ Akasema: “Bwana, acha nipate kuona tena.”+ 42 Kwa hiyo Yesu akamwambia: “Ona tena; imani yako imekuponya.”+ 43 Na mara moja akapata kuona tena,+ naye akaanza kumfuata, akimtukuza Mungu.+ Pia, watu wote, walipoona hilo, wakamsifu Mungu.